“Na naomba uzingatie.
Kuanzia kesho, anza kutafuta dada zako kwa zamu, kuwajulia hali. Una dada
wazuri sana na bado wadogo, wanazagaa mtaani wakiwa hawana uangalizi maalumu,
na wewe ukiwepo hapa mjini, ukimuangalia Nanaa tu, wakati Nanaa amezungukwa na
watu kibao.” Hapo akajua akijitetea ataharibu. Kimya.
“Pili, katika
kumtafuta Vai, kwa upande wake, usigusie chochote juu ya mazungumzo yake na
Joshua, ila kuonyesha unamjali. Inamaana ujirudi kwake.” “Jema!” “Hakika James.
Ukizungumza naye, mpe sababu ya wasiwasi wako siku ile, mwambie ni kwakuwa
hukutaka…” Akasita.
“Hapana. Ukisema ni
kwa kuwa unamjali. Atajua unamdanganya maana ulimfukuza kwako na kumuacha aende
na huyo Bale unaye muona mbaya, ila kwa Nanaa ndio ulitaka uwekewe ulinzi
asifikiwe na Bale, yeye ambaye ni bora kuliko kina Vai.” “Jema
umeniamualia mama.” “Kwani ni uongo?” “Nakulinda mke wangu. Wewe na mtoto.”
“Basi endelea kunilinda mimi na JJ kwa kurekebisha.” “Kwani
nimekataa? Si ndio nasikiliza maelekezo!” “Tengeneza na Vai kwanza. Ndio wewe mwenyewe
uwakaribishe nyumbani.” “Au labda tuwe wote.” “Hapana James. Wadogo zako
wanakuhitaji wewe. Na naomba uwe mwema kwao kama unavyokuwa mwema kwa Nanaa.”
Akazidi kumkaba, James hawezi kujitetea.
“Wadogo zako
wamepitia ujana kama Nanaa tu. Viola amezaa kabla ya ndoa kama Nanaa tu.”
Akataka kusema lakini Nanaa aliolewa, lakini akaona usiku huo ameamuliwa yeye,
bora awe bigger person. Apokee dozi yake, paishe. “Wewe umezaliwa na
dada warembo kwenye ulimwengu huu wa wanaume waliojawa uchu, halafu
ukajitenga nao, ukamkazania Nanaa tu, ulitegemea nini? Nanaa ameishia hapo
sababu hata Geb mwenyewe aliona yupo mwanaume mwenye msimamo kwenye maisha ya
Nanaa, unamlinda na kumjali, ndio maana na yeye akaongeza umakini kwa Nanaa.
Sasa unafikiri kwa Vai na Viola ingekuwa hivyohivyo?” Kimya.
“Ndio maana mama Jema
anakua mkali kwa mtu anayetuonea. Wakati wote anasema wanaume wakiona binti
yupo yupo tu, hamna baba au mwanaume wa kumlinda, ndio na wao wanawachezea.
Sasa wewe ukaweka ulinzi upande mmoja, ukajisahau kwa dada zako. Ndio ujirudi.”
“Sawa.” James akatoka hapo na mwanae kimya kimya. Usiku huo ukaisha kwa
kujihami haswa, hakutaka hata kuomba penzi, akawa mpole. Mume mwema.
Kulikoungua Mpini.
Sasa huko kanisani,
akatokea kijana, mtanashati, jina Ezra, akaonekana anayo aghueni ya maisha,
akawa anamtaka Jelini. Alipowasalimia siku hiyo ya jumapili, alikuwa
akifahamiana na Jema zaidi, akamsoma Jelini kwa haraka, akajua ni wa kumuendea
taratibu sana tena kwa tahadhari. Akajaribu kuwakaribisha waungane kwa chakula
cha mchana siku hiyo kwenye hoteli aliyosema wanapika vyakula vizuri sana. Kumbe
James alishamsoma, kwa haraka sana akakataa mpaka Jema akashangaa. “Tuna ratiba
ingine.” Ezra akawa muungwana. “Basi wakati mwingine.” Akaondoka. Jema
akamtizama James, James akachukua mwanae na kwenda kumfunga kwenye gari,
wengine wakafuata nyuma. Jelini hata hana mpango.
Wakati wanakula Jema
akaanza. “Ezra ni kijana mzuri! Mcha Mungu na ametulia.” “Na mimi nimemuona. Ni
wale vijana wanaonekana wanajielewa.” Mama Jema akaongeza bila kufikiria mbali,
au asijue kinachoendelea, wakila. “Muonekano unaweza ukadanganya.” Akadakia
James na kuongeza. “Maana mtu anaweza akajionyesha kwa nje ni mzuri, kumbe
anamakando mengi.” “Kwa jinsi nilivyomuona kwa pale kanisani, anaonekana ni mtu
mzuri.” Jema naye akaongeza. “Kanisani kila mtu ni mtu mzuri, mtakatifu.
Maana pale kila mtu anavaa sura ya kitauwa.” Mumewe alivyojibu hivyo, Jema
akaona anyamaze. Wakala na kutawanyika.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Njiani wakiwa
wanarudi kwao Jema akaanza. “Mbona kama nakuhisi unampinga sana Ezra?” “Mimi
sijampinga, ila nimeongea ukweli.” Jema akacheka kwa masikitiko. “Nini sasa?”
“Nisikilize James, najua Colins amefanyika kama ndugu, unaona kutoa baraka zako
kwa mtu mwingine ili awe na Jelini, unaona ni kama usaliti. Lakini wote
tunajua, maisha ya Colins yanaendelea kama kawaida. Hatakaa akarudiana tena na
Jelini. Kwa nini tusimpe nafasi na Ezra naye tukaona. Pengine anaweza akageuka
akawa mtu mzuri kwa Jelini.” “Hilo huwezi jua.” “Basi niombe tumpe nafasi.”
“Kwani wewe Jelini amekwambia anatafuta kuwa na mahusiano?!” Hapo akawa mkali
kidogo. “Hajasema, ila sio mbaya akaanza kufikiria mwanaume mwingine ili maisha
yaendelee.” Akanyamaza.
James kwa Vai.
Kabla jumapili hiyo
haijaisha, akampigia simu Vai. Alimshusha Jema na mtoto nyumbani, akaenda
kwenye biashara zake, akiwa anarudi usiku nyumbani ndipo akampigia. Vai akiwa
na Bale na wenyewe ndio walikuwa wamefika tu nyumbani baada ya jumapili ndefu,
aliingia ndani na kujitupa kwenye kochi. Alipoona simu ya kaka yake alishituka
mpaka akakaa.
Akamuonyesha Bale.
“Usiogope. Pokea.” “Naogopa Bale!” “Alishakugombesha mpaka akatosheka.
Unafikiri sasahivi atakwambia nini kingine? Na uzuri alikufukuzia kwangu. Huna
chakuficha. Usiogope, pokea tu.” Bale akamtia moyo.
Kabla haijakatika,
Vai akapokea. “Halo.” Akaanza kwa upole. “Hujambo?” James akasikika. “Tunaendelea
vizuri. Shikamoo kaka.” James akajua inamaana ni yeye na Bale. Vai
hapapendi nyumbani kwa mama yake. Kwanza mama yao huwa hashindi nyumbani.
Anatoka asubuhi nakurudi usiku mwingi. Ni kama hapo kwa mama yake anaishi
Viola, na mtoto wake tu. Mahali baba yake Nanaa alimjengea mama yao nyumba ilikuwa
mbali kidogo na makazi ya watu. Kutembea parefu kufikia usafiri. Ni mara chache
sana Vai anakwenda huko. Kwa hiyo akajua moja kwa moja anamzungumzia Bale.
“Vai?”
“Nipo kaka.”
James akaona ajishushe. “Nisiongee mengi, nikaharibu
zaidi. Naomba radhi kwa jinsi nilivyokupokea ukiwa na mgeni wako.” Vai
hakutegemea. Alilia sana. “Sikufanya vizuri, nisamehe
dada yangu. Nilipaniki nikashindwa kufikiria. Niliongea maneno mabaya. Si sawa
kwako. Naomba radhi.” Vai alikuwa akilia sana. Hakika hakutegemea. Akasimama
kuelekea chumbani ili akazungumze vizuri na kaka yake.
“Nashukuru
kaka. Na samahani kwa kumleta Bale kwako. Ila yeye binafsi amekuelewa kaka. Na
aliniambia ilimuongezea heshima kwako. Unalinda familia yako wakati yeye
aliangamiza yake. Ila kaka, binafsi imeniumiza sana. Nilifikiria na mimi
ungenichukulia kama vile Nanaa!” Hapo akakumbuka maneno ya Jema.
“Nakumbuka
jinsi ulivyohangaika naye kuhakikisha mchumba wake na wakwe zake wanapokelewa
nyumbani, japo mama alikusumbua sana. Nakumbuka uliweza kuwaleta mpaka nyumbani
Moshi. Moyoni mwangu na mimi niliamini kwa asilimia zote ungenichukulia japo
inaweza isiwe kama Nanaa, lakini angalau hata kunifungulia mlango kaka
yangu! Lakini ulinifukuza kikatili sana.” James akaumia sana.
“Inawezekana
Bale asiwe kama mume wa Nanaa. Lakini Bale anajua amekosa kaka. Anajutia kosa.
Ametubu. Ananijali sana. Ananitunza na kunifanya nitulie shuleni. Ananiongoza
vizuri. Najua ubaya aliotenda zamani, kwa kunisimulia yeye mwenyewe mwanzoni tu
tulipokutana. Alijitambulisha kwangu kwa historia yake mbaya, bila
kunificha. Lakini kaka, Bale amebadilika.”
“Leo
tumetoka kanisani, hajapumzika, tumeenda mpaka kwa mama, kumuangalia Nelson.
Viola alikuwa hajui chakufanya. Bale alituchukua wote na Viola akiwa na mtoto
wake. Akatusindikiza hospitalini.” James akaumia sana na kujilaumu.
“Nelson
anaumwa nini tena!? Mbona mama hajaniambia!?” “Wewe
unamjua mama. Hana muda na yeyote isipokuwa biashara zake. Viola anasema hii ni
siku ya tatu mtoto anapandisha joto, anaharisha na kutapika pia. Wote wawili
yeye na Nelson wameshindwa kwenda shule ijumaa. Mama hashindi nyumbani,
alipompigia simu, amemwambia ampe dawa ya kushusha homa na kuzuia kuharisha,
mpaka Bale alipoona ni lazima tumpeleke mtoto hospitalini. Si sawa kwa mtoto
kama huyo kuendelea kuharisha kwa zaidi ya siku tatu. Tumemkuta mtoto
amedhoofu, na Viola hana hela kabisa, mama amemkatalia kumpa, amemwambia
ampigie simu baba yake Nelson, amdai na kumtisha atampeleka polisi.” “Na wakati wote tunajua alishagoma kumtunza mtoto wake!”
James akashangaa sana.
“Wewe
unamjua mama linapofika kwenye swala la kutoa pesa yake. Alikuwa tu akimtoa
barabarani.” “Sasa hospitalini wamesema ni nini?” “Wamempima, amekutwa na
Amoeba. Bale akaomba angalau awekewe maji, maana alikuwa amedhoofu sana kwa kuharisha na kutapika. Tumekaa hapo hospitalini wakimuwekea
maji na kumpa glucose mpaka amepata nafuu. Bale mwenyewe amelipia na
kuhakikisha anawarudisha nyumbani wakiwa na dawa na matumizi kwakuwa Viola
alikuwa ameishiwa kabisa.”
“Ninachotaka
kusema, Bale wa zamani sikubahatika kumfahamu, kaka yangu. Na nasikitika
alikuumiza na wewe pia. Lakini huyu Bale wa sasa, sijawahi pata mtu akatujali
kama yeye. Ameweka heshima katikati yangu na Viola, sio kama wanaume wengine
walikuwa wakitufanya tujione tunashindana. Ananijali mimi na Viola ambaye yupo
kama ametelekezwa na kila mtu, akihangaika na malezi ya mtoto peke yake.
Bale anajali kaka, na makosa yake ya zamani, yamempa hofu ya Mungu.” Akajikuta machozi
yakimtoka tena.
“Ananiheshimu,
hanichezei au kunitumia vibaya kama wanaume wengine. Ananifikiria bila kuchoka.
Ananitunza mpaka apate baraka zenu. Sijawahi pata mimi mwanaume kama Bale, kaka.
Ndio maana nikapata ujasiri na mimi kumtambulisha kwako kama Nanaa. Najua na
mimi nimekua mtoto mbaya. Nimekua na maisha machafu, lakini nimebadilika. Bale
ananiongoza katika njia sahihi. Akili imetulia. Nafikiria mambo mazuri sio
mabaya kama zamani. Ni hilo tu kaka yangu.” Vai akapata jukwaa kutoa dukuduku lake
“Nafikiri
na mimi nilitakiwa kumpa nafasi. Nitazungumza naye, nimuombe radhi na
kumshukuru kumsaidia Viola na Nelson pia.” “Nashukuru kaka. JJ na wifi
wanaendeleaje?”
Vai akawa muungwana kubadili mazungumzo. Mtu mzima ameomba msamaha, akaona
asibakie kwenye hilo. Hawakuzungumza muda mrefu, wakakata simu.
Nyumbani.
Jema akamuona mumewe
amerudi amepoa kweli. Akaona amuache kwanza. Wakiwa chumbani peke yao akaanza
yeye mwenyewe. “Nashukuru kuzungumza na mimi jana. Kweli nimezembea kwa kina
Viola. Wamekua ni mabinti waliozungukwa na watu, lakini wapo peke yao kabisa, wakiteseka.”
James akazungumza kwa majuto kidogo.
“Nimezungumza na Vai,
nimeumia sana. Kumbe Bale ndio anawasaidia wote wawili na mtoto wa Viola!”
“Hujachelewa James.” “Naona na wenyewe hawana shida. Wapo tayari na mimi muda
wowote. Nimezungumza na Viola naye baada ya kujua mtoto wake ni mgonjwa. Hakuwa
na mengi ila shukurani tu, kwa msaada wa Vai na Bale. Anasema alikwama, akajua
atampoteza mtoto wake.” “Kwa nini hakututafuta sisi?” “Nilitamani kumuuliza
hivyo, ila nikajisuta. Nimemwambia asiache kunitafuta kwa lolote, hata kama
analiona halina muhimu. Mimi ni kaka yake. Nahusika na Nelson kama vile yeye.
Hakutegemea. Alilia sana.”
“Imeniuma sana Jema. Sana.
Nimejilaumu sana kuona Mungu amenibariki mali zote hizi, halafu dada zangu
wanateseka na kusaidiwa na mtu baki tu! Tena ambaye mimi nilimuona hafai,
kumbe ndiye anafanya vizuri kuliko hata mimi! Ni kweli lazima kusimama kwenye
nafasi yangu kwa ndugu zangu na kufanya mabadiliko ya makusudi. Nashukuru kwa
kunifungua macho jana.” “Na Bale?” Jema akaona pasipoe. Kimya kidogo.
“Utanisamehe James.
Usione kama nakuwekea pressure.” “Hapana. Ni sawa. Nimepanga kumuomba
nipate naye muda wa chakula cha mchana kwenye mapumziko ya kazini. Nizungumze
naye ana kwa ana. Sikutaka kuzungumza naye kwa simu. Naona anastahili heshima
anayowapa dada zangu.” Jema alifurahi huyo, James akaona anavamiwa. Akapewa
dozi ya kiutuuzima, akabaki akihema na kucheka. Akajua Jema amefurahi.
“Nashauri aina hii ya
pongezi iwe ya mara kwa mara. Niwe nabakwa hovyohovyo tu.” Jema alicheka mpaka
machozi. “James, umebakwa?” “Hakika huku ni kubakwa. Ila mimi sina neno.
Na hivi jana nilinyimwa! Wewe ukijisikia kunibaka, ruksa.” Jema akambusu na
kuelekea bafuni akicheka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akiwa ofisini
akapokea ujumbe, ‘Kama utakuwa na nafasi leo, tafadhali
tukutane kwa chakula cha mchana. James.’ Bale alibaki akiitizama simu
yake, asijue chakufanya. Akautuma ule ujumbe kama ulivyo kwa Joshua. Hapo hapo
akajibu. ‘Milango imefunguliwa, ni wewe kupata ujasiri
wa kuingia. Usiogope.’ Joshua akajibu, eti Bale akapata ujasiri kusoma
hayo majibu ya Joshua. Hapo hapo akamjibu Joshua. ‘Asante.’
‘Anytime.’ Joshua akajibu kwa haraka kama
aliyekuwa na simu mkononi. Kisha akamjibu James muda na mahali anapoona
pangefaa kwa kukutania.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walipokutana, James
akawa muungwana. Hakutaka mengi, ila kuomba radhi. “Binafsi nakuelewa James, nilikosa
sana. Na najua wazi neno samahani, au nimebadilika halitoshi ila
muda kuthibitisha najutia nilichotenda. Nilijawa na haraka ya maisha. Nikaona
taratibu za baba zinachelewesha. Alibaki akiomba bila kuona mafanikio ambayo
kwa sasa najua kwa hakika mimi na mama tulikosa kuona majibu ya Mungu kwa
sababu tulipima mafanikio kwa namna yetu.”
“Tumekosa wakati wa
Mungu na familia iliyokuwa imebarikiwa kwa namna ya ajabu sana. Kwa
wakati ule ungeniambia haya, nisingeamini mpaka nilipoishi kwenye uhalisia.
Kuwa na kila kitu bila Mungu. Ni kweli ni kama kukimbiza upepo tu. Havina raha!
Nilikuwa na pesa nyingi sana, bila utulivu. Ilifika kipindi, nilitamani maisha
ya nyumbani na sikujua jinsi ya kujirudi. Mungu alihakikisha ananipa kila
nilichodhani ni muhimu, ilimradi tu nimtambue YEYE na nguvu zake
anapokuwa kwenye maisha ya mtu. Nimeharibu sana, na siwezi kurekebisha nyuma.
Tafadhali nipe muda na nafasi. Naomba Mungu anijalie niwe kile alichokusudia
kwangu mpaka kunileta hapa duniani.” James kimya akisikiliza.
“Na kingine James, nampenda
sana Vai. Sina nia naye mbaya, kumtumia sababu ya uzuri wake tu. Vai kama
Vaileth mbali na muonekano wake, yeye ni mtu mzuri sana. Mpaka nahisi
watu wengi wamemkosa au wanamkosa yule mtu wake wa ndani wakibakiwa kuhangaika
na mtu wa nje tu, uzuri wake.” James kimya akimsikiliza maana na yeye ndio kwa
mara nyingine tena ni kama anatambulishwa huyo dada yake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Tokea wanakua, wapo
nyumbani kwao, alikerwa na tabia za hao dada zake, mama yao akiwakingia kifua
hata kwa makosa ya waziwazi. Alipoona wamejiunga wote wakimtesa Nanaa, ndipo
akawekeza nguvu za makusudi kwa Nanaa, na kuwaacha hao mabinti mkononi kwa mama
yao. Hakujihusisha nao mpaka walipotaka tena kujaribu maisha.
Bila shida James
aliwaleta mjini. Akaishi nao mmoja baada ya mwingine. Wakawa ni kama usiku na
mchana kuwalingalisha na Nanaa. Wakawa wavivu wakupitiliza. Yeye ndio
anawatumikia hapo nyumbani kwake japo ndiye aliyekuwa akifanya kazi, wao wakishinda
tu nyumbani, tofauti na Nanaa aliyekuwa yeye ndio akimtumikia na kumshukuru
kumtunza. Nanaa alimtunza kaka yake akihakikisha akirudi nyumbani baada ya kazi
ni mapumziko tu, kinyume na hao wawili. Vai na Viola.
Akaja kumpa Nanaa
nafasi kama aliyompa Viola. Kuishi kwa kina Magesa. Viola akaishia kumuingilia Danny
chumbani akiwa uchi, alipodhani mkewe hayupo. Likatokea la kutokea, kumbe Danny
wa wakati ule akiwa chini ya ulinzi wa maombi ya kina mama G, alikuwa
mwaminifu sana kwa Grace, mpaka alipotoka nje ya ulinzi wa Mungu, na
kukuta shetani alikuwa akimsubiria kwa hamu zote. Shetani akiwa hana
zawadi ya bure, alimpokea kwa mikono miwili, akampa
mrembo aliyekuja kumuachia ubachela, kuua watoto na gonjwa
analoishi nalo mpaka sasa.
James aliomba radhi kwa
kina Magesa na kumtoa Viola hapo kwao, moja kwa moja kituo cha mabasi
kumrudisha kwao Moshi. Kuanzia wakati huo, akanawa mikono kwa hao dada zake.
Akawaacha mikononi kwa mama yao. Akahamisha akili na juhudi kwa Nanaa. Akampa
nafasi kama yao. Nanaa wa wakati ule alikuwa yatima, hana kimbilio ila
kila nafasi aliyokuwa akipewa kuitumia kwa makini. Akaishia kusoma mpaka
shahada ya kwanza. Na nyumba ileile aliyotia aibu Viola, mabinti hao
wanaofanana karibia sawa tu kasoro tabia, Nanaa akatoka na mume. Geb. Nanaa
akawa fahari ya James. Kuonyesha juhudi zake si bure, ila dada zake wakibakia
kumfedhehesha na mengine mengi. Ndio James kuwaacha kabisa mpaka wakati Jema
alipotaka warudi shule. Napo ni kama alisaidia kidogo tu. Alipohakikisha wamerudi
shuleni, akaachana nao.
Visa na mikasa ya hao mabinti Viola, Vai na Nanaa, vinapatikana
kwenye Simulizi
ya ….Ni Wangu!
https://www.naomisimulizi.com/2022/11/utambulisho-wa-simulizi-ya-ni-wangu.html
ITAKUPELEKA KWENYE VIDEO YouTube
https://www.naomisimulizi.com/2022/11/ni-wangu-sehemu-ya-1.html
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Vai ameleta maana
nzima ya maisha kwangu.” Bale aliendelea. “Mungu alimleta kwangu kunikamilisha.
Nilikuwa nikimwambia Joshua, kila upungufu nilio nao mimi, ukamilifu wake upo
kwa Vai.” James akamwangalia akihisi anasikiliza habari za mtu mwingine, si
Vai, mdogo wake. Vai! James akaona aendelee kusikiliza tu akiamini kuwa kweli
watu hubadilika!
“Ninaishi na Vai,”
“Kwa nini unaishi naye na amelipiwa chuo aishi hosteli?” James akauliza
kiiungwana tu akimkatisha. Lakini hata Bale aliweza kugundua hapakuwa na ukali
kwenye swali lake, ni kama anayetaka kufahamu zaidi. Ikamtuliza kueleza ukweli.
“Cha kwanza, siishi
naye kama mke, kwa sababu siwezi kufanya hivyo bila baraka zenu au mpaka
ndoa. Mazingira ya chuo huwa yanamfanya hatulii. Kuna aina ya ushindani
ulitokea hapo katikati baina yake na waliokuwa rafiki zake. Kukatokea uadui na lawama,
inamuwia ngumu Vai kuishi pale na kutuliza mawazo chuoni. Sasa kwa kuwa nina
usafiri, naona ni bora aishi kwangu, atulie ili shule iishe. Asichanganywe.”
“Kwangu kuna utulivu.
Hawazi swala lolote hata chakula, kwa kuwa mimi mwenyewe nampikia, nahakikisha
anakua na chakula wakati wote, mawazo yake ni shule tu. Akishasoma na wenzie na
madarasa yakiisha, nampitia kurudi naye nyumbani. Asubuhi nahakikisha yupo
chuoni kwa wakati. Kukiwa na mtihani, na wenzie wakakataa kusoma naye mchana,
hapo inamlazimu kulala hosteli. Anajitahidi kwakweli. Anafanya vizuri na Mungu
amempa kibali huko hata kwa walimu wake na matron. Nipo naye nyumbani ili
kumfanya atulie ila si kwa nia mbaya.” “Nashukuru Bale.” Bale akavuta
pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu.
“Na naomba pia
nikushukuru kwa ajili ya Viola. Alihitaji msaada.” “Karibu. Ila naomba baraka
zako James. Nampenda Vai, nataka kumuoa.” “Bale! Kabla hajamaliza chuo!?”
“Hatutaanzisha familia, mpaka amalize chuo. Hilo nakuahidi James. Sitaki
kumtenda Mungu dhambi, na siwezi kuendelea kuishi naye kwa jinsi
ninavyoishi naye hivi. Tafadhali naomba baraka zako, nimuoe, awe mke wangu
kihalali.” “Labda nikuulize, Joshua anajua hili?” “Ndiyo.” James akachoka
kabisa.
“Kwamba yeye anaona
sawa mfunge ndoa sasahivi?!” “Kipindi Vai yupo likizo baada ya kumaliza huu
mwaka. Mwaka wapili anasoma akiwa mke wangu. Na yeye Joshua amesema nilazima
nihakikishe anamaliza chuo kwa muda wazazi wake au nyinyi mmelipia bila
kuzembea. Na ameahidi na yeye kulisimamia hilo.” James akabaki hoi. Inamaana
hapo anazungumza na Bale, alishapata baraka kutoka kwa Joshua na Geb!
“Tafadhali James.
Namtunza Vai vizuri, nipe baraka zako awe mke wangu, hicho kipengele
tukimalize, tuendelee na mengine.” “Aisee nipe muda Bale. Nifikirie. Kisha
nizungumze na Joshua pamoja na Geb, ndipo nikazungumze na mzee. Nimsikie na
yeye.” “Nitasubiri bila kukubugudhi James. Utakapokuwa tayari, nijulishe tu,
tuanze taratibu za mahari. Joshua ameniahidi atasimamia, nioe kwa heshima.”
James hakuamini. Akacheka akitingisha kichwa.
“Nini?” “Aisee Joshua
nimemnyanyulia mikono! Yupo na mimi kana kwamba hajui chochote kinachoendelea
kabisa!” “Yeye mwenyewe aliniambia hajui jinsi ya kufanya, amemuachia Mungu
atende mwenyewe. Ila ukweli anatuombea sana mimi na Vai. Anatubeba magotini
bila kuchoka.” “Aisee huyo Mungu wake naona anatenda kwa ajabu! Acha
mimi niwahi kazini. Tutazungumza zaidi.” James akamalizia chakula na kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Sasa imekua
akizungumza Bale popote, ni Joshua. Na Joshua akizungumza popote, lazima
umsikilize kwa jinsi alivyoheshimishwa na Mungu. Sasa Bale naye amekua Kumu.
Akamtumia ujumbe Joshua kumwambia kilichoendelea kati yake na James mpaka
kutaka kumuoa Vai. ‘Amesema atafikiria na kuzungumza na
wewe.’ Joshua akacheka mwenyewe. ‘Wewe ni
Mungu, na badala yako SITAKI mwingine. Umepigana vita yote, unaniletea
tu mateka!’ Akamwambia hivyo Mungu wake akicheka, na kumjibu Bale. ‘Acha Simba wa Kabila ya Yuda angurume mpaka pakae sawa.
Hajawahi kuongopa, na hataanzia kwako.’ Bale akacheka aliposoma hivyo.
Akajua kwa hakika mwaka huo ataoa, na yeye apate starehe ya mwanamke.
Kwa Jelini
Jumapili inayofuata
baada ya ibada, Ezra aliwasalimia na kucheza kidogo tu JJ akaondoka bila kutaka
mengi maana na yeye alishaanza kumuogopa James. Wakarudi nyumbani kama kawaida,
Jema akamwambia mumewe anataka kumkaribisha Ezra kwa chakula cha mchana jumapili
inayofuata. “Taratibu Jema bwana! Mbona hivyo!?” “Hivi unajua ni miezi mingapi
tokea Colins aondoke?” “Miezi 6, na siku 15 tu! Tayari tunafanya mapinduzi!”
Jema akabaki ametoa macho. “Kwamba wewe mwenzangu unahesabu!” “Sasa si
kama umri wa JJ tu. Unawezaje kusahau!?” Akaondoka kabisa hapo nyumbani kwenda
kwenye biashara zake.
Lakini akajua
itamuwia vigumu sana kukaribisha mtu mwingine kwenye maisha yao mbali na
Colins. Hata huyo kijana aliyeshika nafasi ya Colins, hakuacha kumlalamikia, na
hakuthubutu hata kumkaribisha hapo nyumbani. Jema akajua anapata naye shida kwa
sababu si Colins.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mungu Wa Wakati Ameanza Kutenda Yake.
Mwisho Wa Yote Ni Nini?
Inaendelea.
0 Comments:
Post a Comment