Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 10 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 10

Ukapita mwezi mwingine, katika chunguza yake kimyakimya, akagundua Jelini ni mfanya biashara. Akapeleleza mpaka akajua sehemu zilipo biashara zake. Siku ya jumatatu mida ya jioni akapita hapo kazini. Jelini akacheka alipomuona. “Ndio unapendeza hivyo ukitoka kazini?” Akacheka tu akijiangalia. “Tena naona unapendeza kuliko kanisani!” “Nashukuru. Lakini huwa najitahidi kubadili mavazi siku za jumapili, maana ofisini inanilazimu kuwa hivi. Vipi lakini siku yako?” Akamsalimia kwa kifupi tu, na hapo akawa muungwana, ulikuwa muda ndio biashara inachanganya dukani kwao, wateja wengi na wao wametoka kazini, wamepitia kufanya manunuzi. Ezra akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Zikapita kama siku mbili hivi, mida ya mchana akamfuata tena Jelini. “Kwani wewe unakaa maeneo haya!” Ikabidi amuulize. “Sio mbali na hapa. Ni kama tu njiani nikiwa nakwenda kwangu. Nimetoka kukutana na mtu sehemu. Tukapata chakula cha pamoja, nikaona nikuchukulie na wewe.” Jelini akakunja uso. “Mimi huwa sipokei vitu vya watu hovyo, Ezra! Sipendi kuhongwa.” Kama kawaida yake, akaongea bila kuchuja fikra zake.

Ezra akacheka taratibu akimtizama. “Ni chakula tu, Jelini! Hakuna hongo hapa. Kama bado hujala basi nimekupunguzia haso yakutafuta mlo wa leo. Ila kama umeshakula, unaweza mpa yeyote hata wafanyakazi wako.” Jelini akajishauri, akamtizama akifikiria, kisha akakataa kabisa.

Na hapo Ezra akawa muungwana. “Tafadhali usinielewe vibaya.” “Hata kidogo. Uwe na amani kabisa. Nilileta nikidhani ni kitu kidogo tu, sikufikiria inaweza kubeba sura ya hongo!” Jelini akafikiria kama ajitetee akaona haina maana. “Uwe na mchana mwema.” Akamuaga na kuondoka zake. Hakumuona tena Ezra ila akaanza kumfikiria. Ezra hakuwa mweusi ila maji ya kunde. Mrefu wa kiasi. Kijana anayevutia tu. Ila hakufanana na Colins kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hawakuacha kwenda kanisani, ila wakagundua hata Jelini anamkwepa. Akiona anawasogelea kwa salamu, basi atajifanya anasimu inayompasa kwenda kuzungumza pembeni ya hapo. Naye Ezra hata katika hilo akawa muugwana, alipoona anafanya hivyo mara tatu akaacha kabisa hata kuwasogelea kwa salamu. Jema hakupenda.

“Ezra ni kijana mzuri.” Akaanzisha mazungumzo wakiwa wote wanakula. Jumapili hiyo walipanga kwenda kula pamoja. “Nimejaribu kufuatilia habari zake, anaonekana ametulia.” Mpaka James akapaliwa na juisi aliyokuwa akinywa. “Hapo unakaribia kuharibu Jema!” “Ni kwa uzuri!” “Hapana. Utaniua kwa pressure bure, nikuache na JJ. Kwamba unamfuatilia zaidi ya kukutana naye pale kanisani!?” Mama Jema hana mbavu.

“Ni kwa wema tu! Namuona kama ni kijana aliyetulia. Mstaarabu na…” Alipomuona mumewe anaweka kila kitu mezani, kisu na uma, anamkodolea macho akaona afupishe. “Kwamba ni mtumishi wa Mungu.” Mpaka Jelini akacheka. “Sifa zote hizo zake yeye tu Ezra!?” “James naye!” “Hapo hapana aisee! Hivyo mimi ishaanza kunisumbua. Na sipendi.” “Basi yaishe.” Wakaona kama hajaridhika.

“Kwamba umemchunguza ukapata sifa zote hizo!” Mama Jema na Jelini wakazidi kucheka. “Leo ukuwadi utakutokea puani.” “Mara ya pili! Mpaka najuta mama yangu. Niliongelea kwa uzuri tu!” “Sasa hapo ndipo panaponitia wasiwasi. Huo uzuri wake umepitiliza!” “Lakini hawezi kukufikia wewe mume wangu. Wewe viwango vingine kabisa!” James akamtizama kwa kumsuta, Jelini anacheka mpaka machozi.

“Kweli James. Au wewe mama unasemaje?” “We! Ishia hapohapo. Ujichanganye mwenyewe, unataka unikosanishe na baba JJ, mimi! Wewe endelea tu.” Mama Jema akajitoa. “Mama naye! Jelini mwaya nisaidie. Wewe unamuonaje Ezra?” “Binafsi sijapata muda wa kumchunguza. Kwa hiyo simjui.” “Ewaaa! Sasa eti jamani, mke wangu mimi, eti ameshapata mpaka muda wa kumchunguza huyo Ezra! Ni sawa kweli? Au ndio kuporwa tonge mdomoni mchana kweupe hivihivi!” “Huibiwi bwana James! Mimi ni kama dada yake tu!” “Hakika huo undugu uishie hapohapo, tafadhali Jema mke wangu.” “Sawa.” James akabaki akimwangalia. Jelini na mama yake wakicheka huku wanamwangalia Jema alivyopoa.

“Unataka nikuongezee kinywaji mpenzi wangu?” Wakazidi kumcheka. “Eti baba JJ wangu?” “Hamu ya kunywa imeisha.” “James naye!” Akampooza hapo akimpamba kwa mengi mpaka akapoa. Wakaendelea na mengine, wakaachana na habari za Ezra.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kila walipokuwa wakienda siku ya jumapili hawakuwa wakimuona tena Ezra, kama na yeye akawa akiwakwepa. Jema naye akaacha kabisa kumtaja.

 Colins.

Huku kwa Colins alianza maisha na Love akifanya kila anachoagizwa bila shida. Furaha ya Love ikatimilika. Anaishi kwenye jumba la ndoto yake ambalo hata hakutolea jasho, kisha akampata na Colins tena akiwa amemshinda Jelini akisaidiwa na mpambe Kemi. Mtumishi alikuwa akiendelea kwenda kumshugulikia Colins. Akajawa furaha ndani ya jumba hilo la kifahari akitumikiwa na wafanyakazi kwa kupitia nafasi ya Colins aliyopewa huko kwenye makapuni ya wazazi wao. Pesa yote anayolipwa Colins ikawa yake akiipangia majukumu na kuitumia apendavyo. Colins hana shida anafanya na kufuata kila anachomwambia.

Miezi mitatu ikawa mizuri. Mambo swafi. Mwezi wa nne, akaanza kusuasua. Akaanza kuonyesha uzubaifu. Love akamwambia huyo mtumishi wa Kemi. Akaenda nyumbani kwao. “Mbona anakuwa kama anazubaa zaidi!?” Akalalamika kwa mtumishi. “Nikuzidi kuomba tu.” Na hapo akapata muda na Colins huko chumbani, akamuacha amelala.

Mpaka mwezi wa nne unaisha, Colins akawa hana afanyalo. Akikaa mahali, amepoa kama hayupo! Love akajaribu kumlazimisha kwenda kazini. Akiwa anakwenda kazini na yeye, anamlazimisha kwenda. Akamtafutia dereva, ilimradi tu kumtoa hapo ndani. Wakawa wanatoka wote asubuhi.

Juma la kwanza la mwezi wa tano likawezekana. Juma la pili wakati Love amefika kazini, dereva akampigia kumwambia tokea amefika hapo nyumbani, alikuwa akimbembeleza Colins aingie garini, lakini ameshindwa. “Mwache tu, usiwe na wasiwasi. Nikuchoka. Jana alikuwa na siku ndefu. Hata kesho usiwe na wasiwasi, nitampeleka kazini mimi mwenyewe.” Huo ukawa mwisho wa kwenda kazini kwa Colins. Hilo likamkera sana Love na kumpandisha hasira kali sana dhidi yake. Akawa kama anampa adhabu ya kutokwenda kazini, nakutomjali kabisa ili ajirudi, lakini wapi. 

Ikawa yeye ndio muenda kazini. Akamuombea likizo kuwa wanasafiri kwenda mapumzikoni kwa majuma matatu, ilimradi tu kupunguza maswali ya kutoonekana kwake kazini. Akakusudia ndani ya muda huo, basi amtafutie suluhu. Akamtafuta tena yule mtumishi, akawa hapatikaniki tena.

Tamu Yageuka Shubiri.

Akaamua sasa kumtafuta Kemi. Akamueleza yote juu ya Colins, tofauti na alivyotarajia, Kemi akamjia juu. “Ndoa zina mambo yake. Lazima ujifunze kuvumilia. Uling’ang’ania mwenyewe, nimekufanikishia kukuingizia mwanaume ndani, kazi kwako. Huu mtindo tena wakupigiana simu na kuelezana ya undani, tutachoshana. Maana na mimi nina yangu, mengi tu. Lakini hunioni nikikupigia simu na kulalamikia yangu.” Simu ikakatwa na kumuacha Love haamini!

Nani Kama Mama!

Akaamua kumtafuta mama yake. Wakakutana muda wa chakula cha mchana wote wakiwa kazini. Wakatafuta hoteli nzuri ya hadhi yao, wakakaa hapo. Akazungumza naye kwa marefu na mapana juu ya Colins. “Hebu niambie mama yangu, nafanyaje? Na pale mimi nishafika, sitaki kutoka kwenye lile jumba. Kila mtu anajua naishi pale. Nishakaribisha rafiki zangu karibia wote na watu wa kazini kwa tafrija nzuri sana, imebaki gumnzo na nimejipatia heshima kwa watu. Kweli gafla nitoke tu na nishatangaza utajiri kwa kiasi kile!” “Sasa hapo ndio shuguli! Bora mngekuwa mmeona. Akitoka yeye, na wewe ujue utatoka tu pale. Maana ile nyumba ni nusu kwa nusu. Ukisema tu wewe umeshindwa, ujue unaondoka. Bora uburuzane naye hivyohivyo mpaka uone mwisho wake.” Ushauri wa mama Simba kwa mwanae ukaendelea.

“Mshahara wake si bado unaweza kuufikia?” “Hilo nimehakikisha namdhibiti tokea mwanzo.” “Bora. Sasa hapo wewe ndio akili kichwani. Jiweke sawa, na mimi nitaenda kuzungumza na baba yako. Ila maisha yako yasikwame Love. Una ndoto kubwa sana, usikubali akakukwamisha. Maana hata mama yake anakajiasili cha uvivu. Si unakumbuka wakati ule namuhimiza turudi wote shule, yeye akakataa akijificha kwenye kulea watoto?” “Nakumbuka.”

“Kile kilikuwa kisingizio tu! Ni uvivu tu na roho ya kukataa kuthubutu makubwa. Kaambukiza kijana wake, kapewa majukumu makubwa, ndio anajidai utahira, sasa wewe usikwame nao. Japokuwa mama yake alikuwa rafiki yangu sana, lakini lilipofika swala la maendeleo, nilipomuona anataka nikwame naye, mimi nikarudi shule. Mpaka leo yeye nesi vilevile, ona mimi nilipo! Sasa wewe asikuzubaishe.” “Hathubutu.” Wakajipanga na mama yake. Wakawekana sawa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baba yake alibanwa sana na mambo ya kitengo kipya alichokabidhiwa cha mambo ya moyo huko kwenye hospitali kuu ya taifa ya Muhimbili. Ikawa safari pia nje ya nchi zimeongezeka. Mara nyingi hakuwepo nchini kwa hiyo mambo ya kliniki zao akawa amemuachia mzee Simba na kijana wake Colins. Kazi yake ikawa ni kuulizia kwa mzee Simba tu. Kila akiulizia, anapewa sifa njema za Colins, mzee anaendelea na yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku moja ya jumamosi mama Colins akajifungasha mpaka Kigamboni kumuona kijana wake na Love. Kilicho cha ajabu, hakupokelewa kama alivyozoea. Alimtuma msichana wa kazi akawaite huko chumbani. Msichana wa kazi aliporudisha majibu kuwa wanakuja, alikaa hapo sebuleni zaidi ya lisaa ndipo akatoka Love na uso wa kusumbuliwa. “Kumbe bado mlikuwa mmelala?” “Ndiyo. Yaani hapa hata Colins bado hajaamka. Jana kachelewa na kazi, tumelala usiku sana.” Mama Colins alivyoona huo upokelewaji, tena hapo Love anazungumza akiwa amesimama hata hajakaa, akaaga na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Juma jingine likapita kimya hata Colins asipige simu kumwambia mama yake alipata habari kuwa alifika nyumbani kwao! Mama Colins akaanza kupatwa wasiwasi. Mama huyu hana majukumu mazito tokea zamani ila wanae. Ajue walipo na wanachofanya, ndio na hiyo kazi yake ya uuguzi. Basi. Sasa ule ukimya ukamfanya amfuate kazini. Hapo kazini akaambiwa hayupo. Lakini jinsi alivyojibiwa, hakupenda. Ni kama waliokuwa wamepewa maagizo kuwa akiuliziwa Colins, apigiwe Love. Mama Colins hakufanya hivyo.

Akaamua kumfuata tena kwake. Akamkuta msichana wa kazi. Akamwambia Colins ametoka. “Amekwenda wapi!?” Ikabidi aulize. “Dada amesema umpigie yeye.” Mama Colins akaingiwa na wasiwasi. Akabaki akifikiria, tena mlangoni. “Mida gani mizuri naweza kumkuta?” Akaogopa kumwambia. “Mimi nataka kumsalimia tu.” “Ila usimwambie dada?” “Usiwe na wasiwasi. Mimi siwezi kukuchongea.” “Shem huwa anaondokaga hapa asubuhi. Wakati mwingine anarudishwa na Issa usiku. Issa anasema anakuwa anamkuta mbali kabisa ya hapa. Anakuwa kama kuna kitu anatafuta, halafu hajui jinsi ya kurudi nyumbani.” Mama Colins akawa hajaelewa kabisa.

Ila huyo binti akapata simu. Wazi alionekana anaongea na mtu mwenye mamlaka kwake. Ila baada ya hiyo simu, akamjibu kwa kifupi mama Colins kuwa, mpigie simu dada mwenyewe ndio anamaelezo yote.” Kisha akaingia ndani, akafunga mlango kwa ndani na kumuacha mama Colins amesimama nje ya mlango.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake akafika hapo kama kwenye mida ya saa tatu asubuhi. Aligonga getini, mpaka akachoka. Akataka kukata tamaa, lakini roho ikazidi kumtuma asichoke. Akaanza tena kugonga. Mwishoe akatoka mlinzi. “Wote hawapo mama yangu.” “Na msichana wa kazi?” “Naye pia hayupo.” “Nilimkuta hapa jana tu!” “Kaondolewa leo asubuhi. Hapa nyumba haina mtu, nipo mimi tu.” Mama Colins akabaki haelewi. Mlinzi akafunga geti. Akaachwa tena nje ya geti, amesimama.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akampigia simu mumewe. “Kuna kitu kinaendelea, na hakipo sawa.” Akamuelezea kwa jinsi ilivyokuwa kuanzia siku alipoenda na Love kumuonyesha kana kwamba anawasumbua. “Hayo ananiambia akiwa amesimama, na nilimsubiria zaidi ya lisaa, sikumuona Colins.” Akamueleza pia alikwenda ofisini kwake hakumkuta kijana wao, na jinsi alivyojibiwa, kisha kurudi tena hapo mpaka safari hiyo kukutana na mlinzi

“Kwani wewe mara ya mwisho kuzungumza na Colins ilikuwa lini?” “Mara ya mwisho kumpigia, niliporudi tu juma lililopita, nikampigia, alipokea Love, akasema Colins ametoka, amesahau simu. Lakini wapo sawa kabisa. Akazungumzia swala la kazi ya Colins na vile anavyofurahia na kushukuru kwa hiyo nafasi, basi.” “Mmmh!” Bado huyo mama akawa na wasiwasi.

“Acha wasiwasi bwana! Kama mpaka sasa Simba hajalalamika, ujue kila kitu kipo sawa.” “Hapana baba CJ. Hawa watu wanamsikiliza sana Love. Inawezekana wanajibu na kuongozwa na kile wanachotumwa na Love. Huyu binti anayo nguvu na mamlaka ya ajabu sana. Na ni kama amenibadilikia kabisa. Tafadhali nenda kwao, na hakikisha unakutana na Colins.” “Basi bora niweke mazingira yakutoka mapema, nimtafute. Nitaanzia kazini.” “Kazini hayupo. Nimekwambia nimetoka huko. Tafadhali nenda kwao na wasiliana na Love. Na ujue nasubiria majibu. Mimi sili wala kulala mpaka nipate taarifa za mwanangu.” “Acha kulia sasa. Mbona nakwenda na nitamwambia Colins akupigie mzungumze? Tulia bwana mama CJ!” “Siwezi kutulia. Roho yangu haina amani. Wewe kanitafutie mwanangu.” Mzee akajua mama hataki utani. Lazima achangamke.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Colins yupo wapi? Usipitwe.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment