Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 66. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 66.

 Andy aligundua jinsi kaka yake alivyoumia kukataliwa na Ayvin, mtoto aliyejihesabu ni zawadi kutoka kwa Mungu. Akahamia kwenye kochi walilokuwa wamekaa, akamchukua Ayvin kisha akaanza kumzungumzisha taratibu palepale akitaka amsalimie Pius kwa kumpa mkono. Akagoma na kujificha tena kwa Andy, hataki hata kumwangalia.

“Una funguo?” Akamuuliza Pius. Pius akatoa mfukoni. Zichezeshe huku ukimuongelesha. Anapenda michezo kupita kiasi, sasahivi atakufuata.” “Na Ayan aje hapo. Akimuona Ayan yupo karibu na Pius na yeye ataanza kujisogeza, kama baba alivyofanya mwanzo kabisa wakabaki kuwa marafiki.” Mina akaongeza wazo jingine. Wakamuita Ayan.

“Nenda kapokee zawadi kutoka kwa anko na umwambie asante.” Ndio Ayan akasogea kwa Pius, akambeba na kumkalisha kwenye mguu wake mmoja. Kisha akampa pole kwa magumu aliyopitia kipindi cha nyuma. Akamuomba msamaha kabisa. Ikamgusa mpaka Andy.

“Najua una akili Ayan. Lakini uliletwa kwenye maisha yetu sisi wote tukiwa hatujakuandalia mazingira mazuri. Tulikukosea. Ila jua tunakupenda sana. Na kuanzia sasahivi utaona mabadiliko. Hata anti Raza naye ataacha kukuchapa. Atakuwa anti mzuri kwako. Umenisikia?” Akatingisha kichwa kukubali. “Umenisamehe na mimi pamoja na anti Raza?” Akakubali bila shida. “Basi nashukuru na nakuahidi, kuanzia sasahivi, hata dad na mummy wako wasipokuwepo, wote tutakuangalia kwa upendo. Usiogope tena.” Wakamuona anaanza kutulia.

Ndipo akaanza kumuuliza maswali mengine ya shule na kama ametengeneza marafiki. Akataka amtajie majina yao, mpaka Ayan akatulia kabisa akionyesha hofu imeisha maana Pius alimuuliza maswali ya shule yaliyoanza kumfanya acheke huku akimsifia kwa hili na lile. Ayvin akawa anawatizama tu huku amepakatwa na Andy.

Pius alipotengeneza na Ayan akamwambia amsomee kile kitabu alichomletea. Akaanza kusoma taratibu mpaka akamshangaza Pius. “Huyu mtoto si mdogo sana kujua kusoma kwa kiasi hichi!?” Wakacheka.

Akaendelea kusoma, alipofika katikati Pius akaanza kumuita na Ayvin akimwambia aende akasikilize hadithi, kaka yake akisoma. “Hapo ndipo uchezeshe hizo funguo. Ndio atawasogelea na kuanza yeye kutaka kusoma na fujo zote. Hapo anatamani apewe yeye hicho kitabu cha mwenzie. Anakuogopa tu, lakini angeshamsogelea, akivute, aanze kusoma huku anamwangalia kaka yake.” “Sasa mwenzie anasomaje?” “Amejifunza kulala naye hapo sakafuni, wanaweka kitabu chini anasoma na yeye pia anasoma kwa kelele. Na kwa kuwa hawezi kutulia sehemu moja, mwishoe anamuachia kitabu chake anaenda kufanya fujo kwingine.” Wakacheka.

Na kweli baada ya muda akaanza kuchangamka akawasogelea. Mpaka Raza anarudi na watoto wake, amechangamka, ila alipoa tena walipoingia mpaka Polla cha utundu na yeye akaanza fujo zake hapo ndio pakachangamka zaidi. Yeye na Polla ndio fujo wakifanya kila kitu, na Polla akamjualia zaidi anataka acheze naye kama umri mmoja!

~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa hakika ipo nguvu ya msamaha. Jambo ambalo lilikuwa gumu wakajikuta wapo wote hapo kwa furaha zote kama familia moja. Vilijaa vicheko, Raza akamfuata Mina jikoni. Nikusaidie nini au na wewe unaniogopa nitakuwekea dawa?” “Mimi mwenzio uchawi siogopi Raza.” “Kweli Mina!?” “Wala si kwa kujisingizia.” Mina akaendelea.

“Acha nikwambie. Upande wa baba walikuwa washirikina sana. Na walimtisha sana mama wakimwambia watamkomesha kwa kuwa ametuchukua kutoka kwao basi hata yeye ni kama atatukosa. Nafikiri kuna ukweli aliuelewaga juu ya nguvu ya mwamini na ulinzi wa kiMungu kwa wana wake, hapo mama yangu hakuwahi kutoka. Hata mimi nilipokuwa nikimsumbua, aling’ang’ana tu na maombi, basi. Nafikiri na mimi hicho kitu kiliniingia. Siogopi ushirikina kabisa na wala si kwa kujidai. Ila si mjinga kwamba siamini kama naweza kujaribiwa! Ila naamini kwenye ushindi wa kiMungu. Wewe karibu fanya utakacho.”

“Naomba nisaidie ili kutoa kitu kitakachojaza tumbo la Pius aweze kulala vizuri.” Stori kwa wawili hao zikaanza. Kuongea na kucheka. Kwa hakika Mina akawa faraja kwa Raza asijue tu. Jinsi alivyomchukulia! Alivyozungumza naye, hakumuonyesha kumuhukumu kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~

 Wakajikuta wamenogewa hapo, wamesahau mabaya yote wala hawayazungumzii. “Umebadilika Raza! Mpaka neno unajua!” “Nilipata kaka wa kiroho, na mkewe mtulivu mno. Tena hakika Mungu alibadili mabaya yangu kwa wema. Sonia aliyekuwa anifunge ndiye aliyenitambulisha kwa kaka Nyange na mkewe. Aisee, ni watu wazuri! Nilihamia kanisani kwao. Wanasimama na mimi kwa kila hatua. Pazuri sana.”

“Nakwenda kanisani mpaka nasikia raha! Polla naye ameanza Sunday school. Poliny naye na Pius wameniunga mkono.” “Haiwezekani Raza! Pius ameacha kwenda kwa wakatoliki!?” “Mimi mwenyewe sikuamini. Kina Ruhinda na dhehebu lao, utafikiri walichanjiwa! Lakini hivyo vichwa viwili vigumu, vimejiunga na mimi. Siamini!”

“Mama Ruhinda atachanganyikiwa.” “Sidhani Mina. Wananiogopa na kunikimbia kwa wazi kabisa. Watakuwa wamefurahi nimeondoka kwenye maisha yao. Paulina hamtaki hata Polla nyumbani kwake!” “Pole Raza. Acha sasa kulia bwana!” “Naumia Mina, naumia sana. Wanamtenda ubaya malaika wa Mungu huyu hana hatia jamani!”

“Nisikilize Raza, hawa watu umewatisha sana. Wape muda. Na wewe unamjua Paulina shoga yako. Ni bendera fuata upepo. Sasa kwa kuwa sasahivi Pius yupo upande wako, yule mama hajiwezi bila Pius, watarudi tu wenyewe.” “Na wewe usinitupe Mina. Tukue wote kiroho. Ukija Dar kuwa upande wangu.” Mina alicheka sana.

“Mimi mwenzio tokea mwanzo sinaga upande.” “Sio kihivyo na wewe Mina! Tuwe mashoga. Kwanza familia zetu zenyewe zishajichanganya watoto sijui baba zao wako huku na kule! Si bora sisi tuwe pamoja halafu nakuwa nakuja kwako na wewe uje kwangu? Wakikuona wewe wanayekupenda sasahivi upo upande wangu ndio watajirudi na kuniheshimu kama zamani.”

“Hilo halina tatizo. Lakini Raza, hata tufanyaje, bado wewe ndio bimkubwa. Akitoka mama Ruhinda ni wewe.” “Mmmh! Sio kama zamani Mina. Sasahivi wewe unapendwa. Wewe ndio umeshika ukoo wa Ruhinda.” “Acha mawazo hayo ya kukunyima raha, Raza. Mwenzio mimi nakuheshimu sana.”

“Hivi nikikwambia na mimi natamani mtoto wa kike kama wewe utaamini?” “Mmmh!” “Ndio ujue Mungu naye anayake! Hampi mtu kila kitu. Nimeomba mtoto wa kike mpaka kwa kufunga na kuomba, lakini naona nimepewa dume jingine. Wala vilio vyetu havijapishana.” Akamtuliza kwa maneno mengi weee, mpaka Raza akatulia.

“Wewe tushikamane. Na tukirudi Dar na mimi nitakuwa nikija kanisani kwenu. Hivi vya wakatoliki vimenishinda bwana! Anaishiga kwenda Andy na wanae. Nikienda nao, naishia kukaa mwanzo mwisho na Ayvin anaongeza utundu.” “Sasa huko kanisani kwetu kuna madarasa ya mpaka umri wa Ayvin.” “Pangetufaa sana tu. Ila kwa Andy kumtoa Roma yeye na wanae, ni hatua kwa hatua. Kila jumapili anaandaa wanae yeye mwenyewe na anatoka hapa bila kuchelewa. Itachukua muda sana au inaweza hata isitokee. Ila jua mimi mshirika wako.” Raza alifurahi huyo!

“Na ule utaratibu wa kukutana kila jumapili ulikufa Mina. Hawanikaribishi tena kwao. Wananiogopa.” “Ndio tutakuwa tukikutana kwako, wewe bimkubwa, mama Ruhinda. Tunapika na kula pamoja. Wakiona kuna amani, watajirudi tu.” Bwana Raza alifurahi huyo! Huna jinsi yakumtoa kwenye ukweli wa kwamba Mungu hubadilisha mabaya kuwa mema, akaamini tena.

~~~~~~~~~~~~~~

Kwa hakika walipata wakati mzuri. Watoto wao walikuwa wakibaki hapo wao wakawa wakienda hotelini na kurudi hapo wanashinda  mpaka usiku. Hata Poliny mpenda shule akatulia. Akaonekana kufurahia hayo madhari ya amani. Akamgeuza sasa Andy kuzungumza naye mambo anayoyapenda ya msingi. Uchumi wa dunia na mengine anayoyafurahia huyo Poliny. Kama si nywele, ungemtizama ungesema ni Pius kwa muonekano na haiba.

Walikaa hapo mpaka siku ya jumapili ndipo walipoondoka, wakiwa na Judy, kama msichana wa kazi. Judy alipanda mbegu moyoni kwa Mina, akashindwa kumsahau. Japokuwa alirudi kwao, kwa mama yake na watoto wake, lakini bado Mina alikuwa na deni moyoni mwake huku mjini. Akitaka kumsaidia kama yeye alivyomsaidia mpaka akapatana na Andy.

Judy ndiye aliyemtia moyo na kumuombea ili kwenda kuzungumza na Andy akiwa mjamzito, hajui baba wa mtoto, Andy akimalizwa na hasira za wivu.

Ikawa msaada haswa kwa Raza aliyekuwa na majukumu ya kazini na nyumbani. Sasa ikawa Raza amepata mengi kwa wakati mmoja. Dada mtu mzima, mcha Mungu, na yeye anawatoto kama Polla. Kwa kumwangalia tu Raza alimpenda. Alionekana anauelewa wa mambo si mshamba wa kuanza kumfundisha kila kitu cha kisasa na ametulia.

 Waliondoka kwa ahadi ya jumamosi inayofuata wao kina Raza kuwa wenyeji wao kwelikweli. Kwamba Raza na familia yake watatangulia nyumbani kwa kina Mina huko Kigamboni wakiwasubiria.

Raza alimwambia Mina wao watatangulia kwenye nyumba yao. Atasaidia usafi na kuandaa chakula kabisa kwamba wao wakiwa wanafika hiyo siku wanahamia jijini, wanapokelewa kwenye mazingira mazuri. Yakaanza mahusiano mapya kati yao. Ikawa furaha ya namna yake angalau Raza akaanza kurejeshewa watu tena, Mina! Moyo ukapoa kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~

Ila kabla ya kuondoka, akaomba kuzungumza na Mina na Andy. Pius akakunja uso. “Naomba wewe Pius nisubiri hapa ndani na watoto.” Wakamfuata Raza nje. Andy na Mina wakamgeukia. “Ni ombi. Na hili hata Pius hajui kama ninalo moyoni. Ila nilianza kumuomba Mungu kwanza. Na sina nia ya kuwaudhi.” Andy na Mina wakawa na shauku yakutaka kujua.

“Msikasirike wala kunisemea kwa Pius.” “Ni nini?” Raza akavuta pumzi kwa nguvu sana na kuzishusha akionekana na wasiwasi. “Ni nini Raza? Wewe sema tu.” Mina akamtia moyo. “Jamani, huyu mtoto kwa Pius ni muujiza ambao sina jinsi nikawaambia mkaelewa. Pius amefurahi SANA. Yaani tukifika hotelini anakuwa na kazi ya kuangalia video zake unazokuwa ukimtumia wewe Andy, anacheka sana. Kama mmegundua hizi siku mbili hapa, Pius amebadilika sana. Pius si wakukaa sakafuni au wakukaa popote bila viatu!” “Nimemuona aisee!” Andy akaafiki akicheka.

“Mimi kwa mara ya kwanza ndio namuona Pius anakuwa sehemu mbali ya kitandani bila viatu  mguuni kwake, na kukaa sakafuni kabisa! Hakika sijawahi muona Pius sakafuni na akicheza magari kwa kukimbizana akitambaa.” Wakacheka.

“Huyu mtoto, amenipa Pius mwingine kabisa! Hata anaweza kutoa utani kabisa, mkacheka! Pius amebadilika jamani! Naombeni mumsaidie.” “Nini?” Andy akauliza. “Najua naomba jambo gumu na ni kama nataka kuwavuruga. Sio nia yangu. Lakini Paulina aliniambia mlimkatalia Pius asiweke jina lake kwa Ayvin.” Hapo wote wakapoa.

“Inaweza isiwe kama vile alivyotaka yeye moja kwa moja. Lakini naombeni angalau aitwe kama mnavyotaka nyinyi, ila angalau muongeze jina lake Pius, iwe Ayvin Pius Ruhinda. Tuache maswala ya Junior kwa sababu tayari yupo Ayan, ila angalau na jina lake liwepo tu. Ni hilo tu jamani. Na samahanini kama nitakuwa nimewaingilia. Na hata mkikataa tena, itaishia hapahapa, sitatoka na kuanzisha tena habari ambayo ilishazikwa.” Mina alinyamaza kabisa, hakutaka kumuingilia Andy na kumtibua. Kimya.

“Acheni tuwahi kuondoka. Tusichelewe.” Raza akawa muungwana kama kuwapa nafasi ya kufikiria. Akaondoka kabisa hapo na kuwaacha. “Sio lazima Andy. Kama alivyosema Raza mwenyewe, nafikiri hata Pius ameshakubaliana na hilo. Tuache tu ibakie kama ilivyo.” “Sawa.” Likawa jibu la jumla. Na Mina naye akaona aache asije anzisha jingine la kuvunja amani.

Baraka Za Moyo Ulionyenyekea

Siku ya jumatatu akiwa ofisini kwake, Andy akampigia simu. “Ulishatengeneza cheti cha kuzaliwa cha Ayvin?” “Bado. Kwa nini unauliza, au unataka ukitengeneze wewe?” “Hapana. Ila nimefikiria, nimeona wazo la Raza si baya.” Pius akawa hajaelewa.

“Ni nini?” “Ayvin ameshalijua jina lake. Si sawa kuanza kumuita jina jingine. Lakini Raza aliomba angalau tuweke jina lako katikati. Aitwe Ayvin Pius Ruhinda.” “Nitashukuru Andy. Nitashukuru sana. Na nakuahidi katika hilo sitafanya fujo kuja kumuita vinginevyo mpaka atakapokuwa mkubwa akijielewa, ndipo atalitambua hilo jina la Pius katikati. Na hata hivyo Andy, hakika nakushukuru kuniruhusu niwe kwenye maisha yake. Unaweza usijue hili, lakini aisee huyo mtoto nilimtafuta, Andy. Mnoo.”

“Na ukweli, nakwambia na Mungu nishahidi, sidanganyi, sikutaka huyo mtoto atokee kwa mwanamke mwingine ila Raza ili kupunguza fujo. Mimi sipendi mabadiliko aina yoyote yale kwenye maisha yangu, nafikiri ndio maana siwezi mahusiano ya nje. Nilijua hata nikipata mtoto wa kiume nje, anaweza akaja na fujo zake, akatuharibia amani pale nyumbani. Ndio maana aliposhindwa Raza, nikarizika na kutulia kabisa.” Andy aliweza kusikia kweli inayotoka kwenye moyo wa kaka yake. Akatulia kabisa akimsikiliza.

“Kwa Mina nilifanya kosa, Andy. Lakini sikuwa na nia yakuzaa naye. Nakwambia hili kwa sababu umempokea mtoto wangu kiasi ambacho nahisi mimi nilikuja kushindwa kwa Ayan. Ni kama nilikuja kulegeza kamba baadaye.”

“Lakini wewe Andy, unampenda huyo mtoto na yeye anakupenda aisee. Nimemuona akiwa mikononi mwako. Sina budi ila kukushukuru kwa kumwambia ukweli. Sikukusudia kuzaa na Mina. Nilikosa, na ninajua hata ukinisamehe bado nitabeba hiyo shutuma hata nikiondoka hapa duniani, vizazi na vizazi watazungumzia hili KOSA langu.”

“Ila kwa sasa nakushukuru kwa jinsi ulivyolibeba na kumfanya huyo mtoto kuwa baraka kwenye familia nzima ya Ruhinda. Najua umenisamehe, lakini jua ni deni unanidai mpaka kifo.” Andy akacheka akisikika ametulia.

“Yameisha Pius. Kwa swala la jina?” “Aisee hilo sitalazia damu. Nahisi mpaka mnakuja jumamosi, nitakuwa nimeshakamilisha. Nitawaletea na hati yake ya kusafiria endapo kutakuwa na safari itakayohitajika hati ya kusafiria.” “Ujue hata Ayan hana hati ya kusafiria?” “Basi acha nitashugulikia zote mbili.” Pius alifurahi, hapakuwa na mfano.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipokata tu simu, hapohapo akampigia simu Raza. “Mbona unafuraha hivyo, katikati ya siku ya kazi!?” Pius akazidi kucheka na kumuuliza. “Bosi wako kanuna nini leo?” “Tupo busy sana. Vipi lakini?” “Nashukuru kwa ombi uliloweka kwa Andy. Amenipigia na kuniambia amekubali.” “Muone anavyocheka!” “Wewe hujafurahi? Tulimuhangaikia sana huyu mtoto Raza. Mungu amempitisha kwingine na bado ametusogezea karibu. Tunasababu ya kufurahi.” Alipomjumuisha hivyo hata Raza mwenyewe akajisikia kuridhika.

“Mapenzi Yanayopitia Dhoruba Kutafuta Utulivu”

Muda wa mama yake kutoka kazini ufikapo, hurudishwa  na dereva wa hapo ofisini. Inakuwa ni jioni ya saa 10. Hutoka kama wengine lakini Pam na Mill wao huchelewa kidogo kutoka, wanatoka saa 10:30 jioni. Yaani wanakuwa wamwisho kama wafunga hicho kitengo, japo sio kwamba wanakuwa wakwanza kufika.

Basi isivyo kawaida muda wa mama yake ukawa wake siku hiyo. Mama yake akashangaa anaingia ofisini kwake na pochi yake. “Kwema!?” Kabla Pam hajamjibu mama yake, akafika hapo dirishani kwa nje ya ofisi waliyopo wao ndani kama mteja.  Pam akatulia akijua ni mteja, amekwenda kulipia japo muda wa kufunga ulikuwa umefika.

Msafi kwa muonekano. Hakuwa amevaa kiofisi, ila nadhifu haswa. Alionekana ni mtu mzima ila aliyegoma kuzeeka. Harufu ya marashi ya kiume, tulivu iliweza penya mpaka ndani walipokuwepo.

“Nimepita kukujulia hali.” Pam akakunja uso akidhani anamuongelesha yeye na yeye hakuwa akimfahamu. “Mbona kama nimeambiwa mgonjwa wako ametolewa tokea asubuhi!?” Mama Eric akamuuliza kwa mshangao akionekana yeye anamfahamu. “Pengine hukuwa umenisikia.” “Umesema umepita…” Ikawa kama mama Eric hajaelewa tena vizuri, japo alionekana kukumbuka alichosema, akasita kumalizia.

“Nilisema hivi, nimepita kukujulia hali.” Akaweka msisitizo na kumchanganya sasa Mama Eric kiasi chakumgeukia Pam akidhania anazungumza na Pam japo alikuwa akimuangalia yeye wala si Pam. Pam akapandisha mabega kumkatalia mama yake,  kama anayesema si mimi au simfahamu! Kisha wote wawili wakamgeukia tena. Wakamkuta ametulia na tabasamu.

“Mimi!?” Akauliza mama Eric kwa mshangao akijishika kabisa. “Ndio wewe mwenyeji wangu hapa.” Jinsi alivyojibu! Mama Eric akawa kama ameshamuelewa, akaona ampunguzie shuguli mapemaa! “Ujue mimi ni mama mtu mzima sana? Huyu ni mwanangu wa mwisho. Ana kaka yake mkubwa kabisa.  Naitwa mama Eric.” “Na jina lako kabla ya Eric?” Aliposikia hivyo, Pam akavuta kiti na kukaa kusikiliza vizuri.

“Wewe! Hivi unavyoniona mimi, ni BIBI wa wajukuu watatu! Tena wakubwa kabisa.” “Mimi ninao wawili, sema kijana wangu huyu wa mwisho amegoma kuoa. Ila kaka yake anao watoto wawili. Jina lako kabla ya Eric walikuwa wakikuita nani?” Akazidi kumchanganya mama Eric. Pam akajiweka sawa kujua kulikoni. Umbea tu!

“Ujue hapa ninapokaa, mtu wa hapo nje hanioni kwa huku chini.” Akajivuta nyuma kabisa ili amuone vizuri na kigari chake cha umeme, cha walemavu, alimpa Mill, kina kiti kizuri tu. “Hivi unavyoniona mimi, ni mlemavu wa zaidi ya miaka 20.” Wakashangaa anacheka. “Hapo nimekwambia mambo mawili tu! Kukujulia hali, na kukuomba kujua jina lako, basi. Lakini ndio unanifukuza kwa nguvu hivyo! Hivi unajua si mambo yote yanafikiwa kwa miguu?” Bwana Pam alishangaa mpaka akaachama mdomo.

“Unakumbuka siku ya pili kupita hapa nilijitambulisha jina langu?” Mama Eric kimya akabaki amekodoa macho. “Mwenzio aliitika, tena akafungua dirisha kabisa mpaka akanipa mkono na kujitambulisha kwangu kwa jina la Stella. Lakini sikufanikiwa kulipata jina lako.” “Sasa wewe kwa nini usiridhike naye binti mdogo yule na…” Akaanza kucheka akitingisha kichwa.

“Mimi sitakuita mama Eric.” “Anaitwa Dorothy Shelukindo, na Shelukindo ni jina la babu.” Pam akadakia yeye. Mama yake akamshangaa sana Pam mpaka kumgeukia. “Mimi naitwa Pam, kiziwanda wake.” “Basi umechukua uzuri wote wa mama yako.” Pam akamwangalia mama yake akicheka kama ambaye haamini kinachompata mama yake. Akawa kama amekumbuka kitu.

Akamgeukia tena. “Lakini ujue mama atakuwa hakumbuki jina lako!” “Joel kama kwenye bibilia. Ila marafiki zangu wa karibu wamezoea kuniita Jo. Ila mimi ni kama nabii Joel kabisa au Yoeli kwa kiswahili.” “Naona umekusudia tusikusahau kabisa!” Pam akaongeza akicheka.

“Mbea wewe!” Mama yake akamwambia Pam akimshangaa. “Maana hii sio mara yangu ya kwanza, Pam. Nilishajitambulisha hapahapa!” “Basi mimi sitakusahau. Nabii Joel.” “Ewaah!” “Mimi natangulia kwenye gari mama. Tutakusubiri usiwe na wasiwasi.” “Ujue Pam acha ushabiki wewe!” Pam hana mbavu. Akaondoka na pochi yake kama kuwapa nafasi.

Wakabaki wao wawili. “Mimi si kama kina Stella, binti wadogo hao ambao maisha hayajawapitisha kwingi.” Akamuona na tabasamu tu usoni akimwangalia. “Umenisikia?” “Juu ya Stella?” “Ndiyo. Na ni binti ambaye bado hajaolewa.” Akacheka sana akimtizama.

“Dorothy unajihami! Mbona mimi sijasema mengi, ila kuja kukusalimia tu?” “Na yeye ndiye aliyeniambia kama mgonjwa wako aliruhusiwa. Akawa akilalamika hapa kwamba umeondoka bila ya kumuaga, hamjaachiana mawasiliano. Na wala hatakuwa amefika mbali. Ameondoka sasahivi na yule binti wa kule ndani ofisini. Ni marafiki sana na Fatma. Wote ni binti wadogo ambao hawajaolewa.” Akazidi kucheka akimtizama vile anavyojieleza kwa kujihami.

“Naweza hata kumpigia kumwambia kama upo hapa, akarudi sasahivi bila ya kuchelewa.” “Kwa hiyo unataka kuniunganisha na Stella?” “Sio mimi ni yeye mwenyewe! Unakumbuka ni yeye ndiye aliyekupeleka mpaka alipo mgonjwa wako? Na mara zote ni yeye ndiye mliyekuwa mkizungumza naye hapa! Naweza kukupa namba yake ya simu.” “Nipe yako.” “Yangu mimi!?” Mama alishangaa huyo! Kama ameombwa roho. “Ndiyo.” “Mmmh!” Akaguna kama anayemvuruga kabisa.

“Tutapata muda uniambie ni kwa nini mpaka leo unatumia jina la mzee.” “Ni…” “Hapana bwana Dorothy! Si leo, na si hapa.” Akamkatiza kwa haraka na kuongeza. “Hayo tutayazungumza tukiwa na chakula huku kinywaji kikitusindikiza. Siku gani ni nzuri kwako?” Akabaki amemkodolea macho.

“Dorothy?” Kimya, akionekana amevurugikiwa haswa. Hamuelewi. “Nipe basi simu yako nijipigie.” “Mimi ni mlemavu kabisa, Jo. Kuanzia kiunoni kwenda chini nimlemavu kabisa. Nilipooza nikiwa najifungua watoto mapacha. Wao walifariki, mimi nikapooza. Nilikuwa ni wakutokwa haja zote, sijijui mpaka nikaja kufanyiwa operation.”

Tena hapo ilikuwa ni baada ya miaka mingi sana baadaye ndipo kaka akaja kunichukua kijijini na kunileta huku mjini kujaribisha tu kama nitapona. Sikuweza kurudi kutembea lakini angalau nikarudisha uhisi huku chini. Ikawa hata mtu akinigusa chini nahisi kama nimeshikwa. Nikarudisha uwezo wa kujua ni wakati gani natakiwa kwenda chooni. Lakini sikuwahi, kurudi kuweza kutembea. Mimi ni MLEMAVU kabisa.”

Pole kwa kupoteza watoto na matatizo kipindi unajifungua. Pole sana Dorothy.” Ilimgusa huyo mama, hakutegemea. Ila akajikaza. “Mzazi mwenzie Pam ndiye anayeniwezesha kusogea sehemu moja kwenda nyingine kiurahisi. Lakini mimi nilikuwa ni mtu wa kusota aridhini kabisa. Na kama si kifo kuchukua watoto wangu wawili, sasahivi ningekuwa ni mama wa watoto wanne! Kwa hiyo Jo, mimi si binti mdogo kama kina Stella!”

“Hilo jina la Dorothy lenyewe nahisi hata watu walishalisahau! Yaani baada ya miaka mingi sanaa, ndio leo nalisikia hilo jina mtu akilitamka. Ni kama lilishasahaulika na Pam amenishangaza hata kulitamka kwa haraka hivyo. Hakuna mtu ananiita tena hivyo! Mimi ni mama Eric!” Akawa akimuelezea kwa makini akiweka msisitizo ili aelewe anachozungumza, akihisi Jo hamuelewi kabisa.

“Naelewa maisha yanaweza kukupa sura fulani hivi! Ukawepo hapo kwa muda mrefu mpaka ukafanania na vile maisha yalivyokubatiza. Naelewa. Lakini pole sana kwa kupoteza watoto na kupatwa na matatizo.” “Nimekwisha poa na kuzoea. Asante!” Akaitika lakini bado akiwa na mshangao usoni, kama ambaye bado hajampata vizuri.

“Mimi na mke wangu hatukutaka watoto wengi kwa makusudi. Tulitaka wawili tu, tukapata wakiume wawili tukiwa bado vijana, ikatosha. Wa mwisho nahisi ni mkubwa kwa Pam. Tulizaa mapema sana. Tulipomaliza tu chuo mwaka wa kwanza, tukaoana, tukapata mtoto wa kwanza. Shahada zetu za pili, tulisoma tukiwa na watoto wetu wote wawili. Mark tulimzaa karibu sana na kaka yake Matthew. Mengi tutazungumza tutakapokutana tena. Niambie ni lini, unanafasi.” Akazidi kumshangaza vile alivyomng’ang’ania!

“Eti Dorothy?” “Sijui Jo! Yaani leo ndio nimemwambia Pam kama ni mjamzito.” “Hakuwa akijua?” “Hapana! Na imemshitua sana. Na sidhani hata kama mzazi mwenzie anajua. Hayupo sawa. Kumuona amenisimamia hapa na pochi yake, mida hii, najua kuna jambo halijakaa sawa lakini najua hataniambia ila kutaka kuwa karibu na mimi kama ulivyomuona hapa. Ndivyo alivyo. Sasa sijui hata itakuaje! Siwezi toa ahadi za uongo.”

“Huoni ukinipa namba itasaidia mawasiliano?” “Wewe unamke Jo! Mawasiliano na mtu kama mimi ni ya nini?” “Betty alifariki muda mrefu sana, akaniachia hao vijana wawili. Mimi si malaya, Dorothy. Namuheshimu sana mke wangu. Kabla na baada ya kifo chake. Naishi nikimuwakilisha na yeye pia.” “Pole kwa kumpoteza mwenzio.” “Asante. Kwa hiyo namba yako ya simu?” Ikabidi tu amtajie maana alionekana ni jambo alilokusudia.

“Nashukuru. Akaandika vitu kadhaa kisha akamtumia ujumbe wenye jina tu, ‘Jo’. “Nimekutumia ujumbe. Naomba utunze namba yangu. Na niambie rahisi ni nini? Nisubirie mpaka utakaponitafuta au ni sawa nikikupigia mimi?” “Hata sijui ndio inakuje Jo! Acha niwe mkweli kwako ili kukupunguzie usumbufu na uelewe usipoteze muda kwangu.”

“Mimi hayo maisha sijawahi ishi kabisa. Ndio maana ulimuona Stella yeye alikuchangamkia kwa vizuri hata akijua ni jambo gani sahihi lakuzungumza na wewe, na nini akuombe kwa wepesi! Nafikiri ndio maana yeye alishangaa kidogo ilipotokea kuna uzito wa kumpa namba yako. Alitegemea pengine leo ndio ungempa.” Jo akacheka tu.

“Tafadhali naomba unielewe na uniamini. Mimi sio kama hao warembo wadogo kina Stella wenye uelewa wa mambo hayo yenu ya kisasa.”

“Jeraha la Moyo kwa Jina la Mapenzi”

Hakuwa akidanganya. Aliolewaga binti mdogo akiwa hata hajamaliza chuo cha ufugaji hukohuko mkoani Tanga. Alikutana na baba Eric akiwa chuoni hapo, yeye kama mmoja wa walimu hapo chuoni. Akamganda binti wa watu akiwa bado mdogo tu. Amemaliza kidato cha nne miaka hiyo na kujiunga chuoni hapo.

Alipopata yeye nafasi nyingine ya kikazi mkoani Ruvuma, ndipo akaona asizidiwe mahesabu huku nyuma. Maana huyo Dorothy alikuwa Dorothy kwelikweli kama Pam anavyo mchanganya Mill. Akaenda kwa kina Dorothy, akamdai kwa magoti kwa ahadi yakuja  kumuendeleza baadaye. Mzee Shelukindo alipoona huo upendo, akakubali. Akamlipia mahari ndoa ya harakaharaka ikafungwa, Dorothy akiwa binti wa miaka 19 kwenda 20.

Akaenda kumfungia huko Ruvuma, kazi ya kuzaa na kulea ikaanza huku akimtumia kwa manyanyaso makali sana. Hakutaka kukaribisha mazungumzo ya kuja kurudi tena chuoni. Alikuwa mbabe kwa mkewe, yeye akawa baba mwenye nyumba haswa anayewaweka mjini. Naye mama Eric bado alikuwa mdogo. Malezi ya kijijini, baba mzee wa kanisa, na yeye alikuwa binti mwadilifu muimba kwaya kanisani huko kwao milimani, Lushoto. Maadili mazuri. Binti aliyekuzwa kwenye kusubiri mpaka ndoa. Naye hakuwa akisumbua nyumbani. Binti mtulivu asiye na makuu kama kaka yake. Hakuwahi kuwa hata na mwanaume.”

Aliagwa kwao kwamba, maisha ya ndoa ni kuvumilia. Basi, ndicho alichokwenda kufanya huko Ruvuma pale huyo mwanaume alipombadilikia. Akatulia akivumilia YOTE huku akiongeza kipato kwa kufanya vijishuguli vidogovidogo ili angalau kuweza lisha wanae. Maana baba Eric ugomvi wake ulikuwa ukizidi pale anapoombwa pesa hata ya chumvi. Hapo atawaka nyumba haitakalika. Basi mama Eric ndipo alipoanza kupika chapati na kuuza pamoja na maandazi ili kupunguza ukali kwa mumewe. Lakini haikuwahi saidia. Alikuwa mbahili hata kwa wanae. Haombeki pesa, na hajui kuzungumza naye kabisa.

Alimbadilikia kama mchana na usiku. Akimtesa mpaka aliposhika mimba ya hao mapacha na kupatwa na hayo matatizo. Akarudishwa kijijini na watoto wawili, na ulemavu juu, bila cheti chochote zaidi ya kile alichotoka nacho kwao, cha kidato cha nne.

Na hakuwaga romatic kabisa. Si mwanzo kabla ya ndoa, na ndio ikawa mbaya zaidi alipoingia naye kwenye ndoa. Hakuwa akijua kubembeleza. Ila aliweza mtongoza na kuzungumza naye mpaka akakubali ndoa, kwa ahadi ya kumpeka mjini. Ambako ndio huko Ruvuma alikoenda muonyesha rangi zote.

Mtu wa kuamrisha wakati wote. Na alikuwa akimshika ujue ni anataka kuingia. Na akimaliza yeye ujue ndio mchezo mzima umekamilika. Tendo la ndoa ilikuwa ni anapotaka yeye, na mwisho wake ni pale anaporidhika yeye. Na hakuwa mlevi wa pombe ila ngono. Alikuwa akimtumia binti wa watu atakavyo yeye, na  kwa muda wake. Akiwa amejifungua au akiwa kwenye siku zake, ujue wanawake wa nje watamsaidia kumtuliza huyo baba Eric na haikuwa kwa kificho wala aibu. Anaingia na kutoka kwake atakavyo huku akimkumbusha Dorothy nyumba ni yake anafanya atakavyo.

Mbaya zaidi, ili kumdidimiza kihisia na kumfanya mateka wake ili hata asifikirie kumsaliti. Kama wafanyavyo wanaume wengine, akamtafutia kasoro alizokuwa akimkumbusha anazo yeye kama mwanamke, tena mara kwa mara mapaka Dorothy akaamini ni kweli. Kwa sababu kwanza yeye ndio alikuwa mwanamme wake wa kwanza. Alimuamini kile alichomwambia. Basi Dorothy akapoteza kabisa thamani ya uzuri wake, akajiona kama anayeishi kwa kusaidiwa na kuvumiliwa tu na mumewe. Akamuingiza donda la moyo, likajitibu asijue anatembea na kovu asilojua hata lilipona lini.

Huyo Dorothy hakuwa akijua hata kama wanawake huwa wanapigaga mabao. Na kwa maadili ya kwao, mambo ya chumbani, mapenzi, si mambo ya kuzungumza hovyo.

Sasa hayo anayotaka kuanzisha Jo ni maisha ambayo hata hakuwahi yawaza, kwanza hayajui maana hata tamthilia hakuwa akiangalia. Huko kijijini kwa wazazi wake walikuja kuletewa luninga na kaka yake, baadaye sana, wakina Pam washakuwa wakubwa kabisa wapo mjini. Na ikiwashwa ni taarifa ya habari na mambo ya dini. Leo Jo anataka kumvuruga tu.

~~~~~~~~~~~~~~

“Basi nitaanza kwa ujumbe, nikisubiria upate nafasi tutoke. Tafadhali weka mazingira tutoke. Nakuahidi wakati mzuri.” Kwa hakika alishindwa nini chakujibu ila kuondoka. “Naomba nikuage. Nimpeleke Pam kupumzika.” “Twende nikusogeze garini.” Napo hapo alishangaa kwa sekunde kadhaa akiwa amemtolea macho kabisa. Kwamba inawezekanaje!

“Nisaidie nini?” “Sina chakubeba zaidi ya pochi, nayo naweka hapa kwenye kigari changu.” “Basi funga twende.” Walishakuwa wamemaliza kazi. Hata kompyuta walishafunga tokea Stella anaondoka hapo na pesa yote kupeleka kwa Mbise, bosi wake Pam, muhasibu wa hiyo kampuni.

Akafunga dirisha mbele ya Jo, akawa haoni tena ndani. Walikuwa wametenganishwa na kioo kikubwa chenye upenyo wa kuweza kupenyeza pesa na kupokea risiti, mbele ya dirisha. Akachukua vitu vyake, akawasha kigari chake akageuza kigari chake kuelekea mlangoni.

Alipomsikia anafungua mlango kwa ndani, akamsaidia kusukuma mlango ili apite na kigari chake kisha akamsaidia kurudishia mlango. “Lazima nifunge kwa funguo.” “Lete mimi nifunge.” Akachukua funguo mikononi mwake akaanza kufunga milango mpaka kigeti cha nje akimuelekeza. “Asante. Lakini ujue huwa nafungaga mwenyewe wakati wote. Stella huwa anawahi kutoka kupeleka pesa na kumuwahi Fatma rafiki yake, huwa wanaondoka pamoja. Kwa hiyo naweza kufunga mwenyewe.” “Nimekusaidia si kwa sababu nilihisi huwezi.” Mama Eric akaanza kuondoka akawa anamfuata nyuma.

“Lakini nimeona unakitu hapa. Naweza kukutoa.” Mama Eric akaanza kujipangusa. Jo akamuacha tu. Akajifuta uso mzima mpaka akaridhika. “Bado hakijatoka.” “Wapi?” “Mikono yangu nimisafi.” Kisha akamsogelea na kuinama pale alipokuwa amekaa, akaanza kumfuta pembeni ya mdomo. Mwanzo mama Eric alishituka, ila akaendelea kumpangusa taratibu kama ambaye hana haraka.

“Naona kimegandia.” “Pam huyo! Itakuwa mtindi wake huo, umegandia! Acha nikajisafishe uso tu. Asante.” Akataka kujitoa maana naye huyo Jo alikuwa akimsugua taratibu, bila haraka na kidole gumba. “Nakaribia kumaliza.” Akaendelea kumfuta ikabidi atulie maana alikuwa amemuinamia hapo karibu kabisa na uso! Taratibu mpaka akamaliza yeye na kuridhika.

“Naona sasa uko sawa.” Ndio akawa anamtoa alikokuwa amepotelea. Alianzisha jambo jipya kwa huyo mama! Halikuwahi hata kuwepo maishani. Hisia za ajabu za kujaliwa kwa kipekee kabisa. “Asante.” “Karibu.” Hiyo karibu yenyewe anavyomjibu! Mpaka akashindwa kumtizama. Akageukia pembeni. Na kuondoa kigari chake. Wakaongozana mpaka kwenye gari wakitembea kimyakimya akimfuata kwa pembeni ila kwa nyuma.

“Ile pale ndio gari yenyewe.” “Nani anapandisha gari yako?” “Dereva hutoka kunisaidia.” “Mpaka kupanda garini?” “Napanda mwenyewe. Nasogeza gari mpaka karibu kabisa na gari, napanda, yeye anakuja kutoa hiki kigari na kuweka nyuma.” “Ni sawa nikusubirie mpaka upande, ndio niondoke?” Na hapo akawa hajui ajibu nini.

“Dorothy, sitaki kukunyima raha. Ila ningependa kukusubiria mpaka unaondoka. Pam akashuka garini na kumfungulia mama yake mlango, hawakuwa wamesimama mbali. Bali alishindwa kujibu. “Twende.” Jo akaongeza mwendo mpaka garini. “Acha nikusaidie mlango Pam.” Pam akaondoka kabisa hapo na kurudi upande wa pili wa gari. Akaingia na kujituliza kimya, kiti cha nyuma.

Akasukuma kigari chake mpaka garini, Jo akiwa ameshikilia mlango. “Nipe pochi yako.” “Huwa nairushia ndani kisha nadandia.” “Mimi nimesimama hapa, huna haja ya kuirusha. Nipe.” Pam akabaki kujisikilizia ila hawaangalii. Akampokea, na kujisogeza pembeni ili kumpisha. Akamuona jinsi anavyopanda garini kama mzoefu lakini hakupenda.  Dereva akachukua kigari kwa haraka na kwenda kukiweka nyuma.

“Funga mkanda kabisa, ndipo nikupe pochi yako.” Akajifunga mkanda akiwa amemsimamia hapohapo pembeni ya mlango, aliporidhika amekaa sawa ndipo akamkabidhi pochi yake. “Mfike nyumbani salama na uwe na mapumziko mema.” “Asante na wewe.” Mama Eric akaitika ila kwa utulivu. Pam akamuona jinsi anavyomjali mama yake na kumchukulia kwa upendo. Akashangazwa sana, asiamini mtu kama Jo anaweza toa muda wake kwa mtu kama mama yake! Na yeye kikamchanganya.

“Pam, salimia familia. Na nimefurahi kukufahamu. Naamini kuna siku nitabahatika kumuona na Eric.” “Na mimi nimefurahi kukufahamu nabii Joel.” Akacheka na kufunga mlango. Kwa hakika alionekana na ustaarabu usio wa hapo nchini kabisa japo aliongea kiswahili fasaha sana. Akapunga mkono. Dereva akaondoa gari.

~~~~~~~~~~~~~

Pam akamgeukia mama yake maana alimuona amebadilika kabisa, amepoa na macho yapo nje ya gari. Akamuacha maana na yeye alikuwa na yake. Mama yake naye alimuacha hakumuuliza lolote kwani alimuona hayupo sawa tokea anamfuata na pochi yake kuashiria anaondoka naye. Huwa anamjua  Pam ni mkorofi. Na huwa anazungumza jambo lake anapotaka yeye. Kwa hiyo wote wakabaki kiti cha nyuma, kimya. Kila mmoja akiwaza lake, dereva akiendelea kukanyaga mafuta. Kimya tu hapo garini.

~~~~~~~~~~~~~

Walipokuwa wakikaribia madukani akamwambia dereva wapitie dukani anunue mtindi. Dereva akatii bila shida, na hivi mama bosi kasema, akamsogeza mpaka karibu ya duka. Akanunua na baadhi ya vitu, safari ya kwa mama yake ikaendelea akiwa na chakula chake.

Kufika akaingia moja kwa moja chumbani kwa mama yake. Akatoa nguo zote. Akajifunga kitenge. Mama yake kimya akiendelea na yake na msichana wake anayemsaidia kazi. Akimpa maagizo nini cha kupika jioni hiyo huku akimwangalia Pam akijua wazi hayupo sawa.

Akamuona anatoa ugali wake wa muhogo alionunua mchana alipokwenda kula na Mill. Kuku wa makange. Pilipili nyingiii na limao lakutosha. Kulikuwa na mboga za majani. Akaomba atolewe mtindi wake alionunua. Maana dada alishaweka kwenye friji. Akakaa chini kabisa sakafuni. Ungemuona anavyokula, ungesema ni mbeba magunia kule Kariakoo sokoni, siku hiyo alifanya kazi siku nzima, hajala. Na ugali wenyewe haukuwa kidogo. Bwana Pam alikula huku feni ikimpepea.

Alipomaliza akatangaza. “Nakwenda kulala. Mtu asiniamshe.” Mama yake alimsikia, hakumjibu. Akarudi kitandani kwa mama yake, akauchapa usingizi. Alilala asijue alipo na hana habari na yanayoendelea ulimwenguni.

Kwa Mill.

Huku nyuma saa 10:26 Mill akatoka kwa kujiwinda akimfuata warudi nyumbani, hakumkuta ofisini wala hapakuwa na pochi yake. Akapaniki. Akampigia simu ikawa inaita ila haipokelewi. Akatoka kumuuliza mlinzi. Akamwambia Pam alisharudishwa nyumbani. Akapata moyo akatoka hapo kurudi nyumbani.

Shema huwa akitoka shule anapitishwa mpirani. Wanafanya mazoezi. Mpaka kuja kufika nyumbani inakuwa karibia muda wa wazazi wake kufika hapo au huwa anawakuta walishafika. Akajikuta wamefika hapo yeye na mwanae karibia muda mmoja. “Mama yuko wapi?” Shema akamuuliza wakati akitoa viatu vyake mlangoni. “Yeye alitangulia kurudi.” Akajibu hivyo na kumuuliza habari za shule ila kama kutimiza wajibu huku akitaka kukimbilia ndani kumuangalia Pam. Akashukuru Mungu na jibu la mwanae halikuwa refu ila tu, ‘nzuri.’

Hakuongeza, akakimbilia ndani akiwa na wasiwasi na hofu akijua kweli ile sawa ya Pam haikuwa sawasawa. Na ndio maana aliondoka bila ya kumuaga asijue kwamba wala Pam hayupo hapo.

Shema akaanzia jikoni akimsikia baba yake akipandisha ngazi kwa kukimbia. “Humu ndani hamna chakula na mimi njaa inaniuma siwezi hata kusogea!” Akapaza sauti baba yake asikie, lakini hakupata jibu. Si kwamba baba yake hakusikia, lakini binafsi alikuwa na yake yakiendelea, hawezi shugulika na njaa ya kijana wake kabla hajamuona mama mtu.

~~~~~~~~~~~~~

Maswala ya chakula ni Pam. Alimjua Shema kwa njaa zake. Kila akitoka mazoezini lazima akute kitu chakula. Sasa Pam hupitia vitu vidogovidogo vya kujitafuta. Akifika Shema anapata glasi ya maziwa na hivyo vitu kama ni sambusa na bajia au kababu au eggchop. Kisha ndio ukaja utaratibu mpya wa kusongewa ugali usiku. Ukawashinda yeye na baba yake, wakawa wakinunua chakula wakati Pam akifaidi ugali peke yake.

Mill alisahau kupitia dukani/bekary wanayopitaga na Pam kila siku jioni watokapo kazini ili kununua vitafunwa hivyo na pia huwasaidia kwa kifungua kinywa asubuhi. Ni utaratibu wa Pam wala si wake. Na wakati wote hubaki garini wakati Pam akishuka kununua.

~~~~~~~~~~~~~

Kufika chumbani kitanda kisafi kama alivyotandika yeye mwenyewe Mill alipokuwa wamwisho kutoka hapo kitandani. Maana Pam huwahi kutoka kuandaa kifungua kinywa kwa wote. Basi wakawa wamejiwekea utaratibu anayekuwa wamwisho kutoka kitandani basi ndio anatandika kitanda. Mara nyingi anakuwa Mill ndio mtandikaji.

“Mama!” Akasikia sauti ya Shema chini ashapaniki. “Kunywa maziwa.” “Hivihivi!?” Shema akamuuliza baba yake kwa kushangaa sana. “Mbona mama hanijibu sasa?” “Hayupo.” “Yuko wapi?” Shema na baba yake wakawa wanajibishana. Shema yupo chini, baba yake juu akihaha hajui Pam alipo.

~~~~~~~~~~~~~

Mambo Yanaendelea kusonga.

Usipitwe na muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment