Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 61. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 61.

Walimkuta Pam yupo busy, anapanga haridhiki. “Mbona dereva alishanipigia simu na kuniambia ameshafikisha vitu vyote nyumbani, kwamba umemaliza. Lakini wewe unaonekana hapa ni kama ndio unaanza!” “Nataka mama akija apafurahie.” “Bibi amenipa chakula nikuletee ule. Amesema cha bibi wa Lushoto ataleta mwenyewe asubuhi na mapema. Usihangaike mapishi wakati unamgeni.” Mpaka Pam akasimama wima na kumtizama Mill.

“Mimi mwenyewe ndio nasikia hapa sasahivi. Sijajua hata kama amekufungashia wewe chakula. Nilijua ni chake huyu.” “Amesema ataleta asubuhi ili aje amsalimie na bibi.” Shema akaongeza na kuzidi kumshangaza Mill. Maana ni kama aliwaomba wamuache Pam kabisa!

“Nisikilize Pam. Huyu mama ananipenda sana na ananijali. Ila kama unaona hutaki kuingiliwa, naweza wakataza.” “Hapana. Ila naona ni usumbufu usio na maana!” “Kwa jinsi ninavyomjua huyu mama kwake si usumbufu kabisa. Aisee wamejawa upendo hawa watu, kupita nitakavyokwambia. Ila siamini.” “Nini?” Pam akauliza.

“Nimetoka kuwaonya kabisa wakuache, na Shema huyu ni shahidi.” “Ila bibi alikutuma, dad. Amesema umwambie mama anamuhesabu kama binti yake. Umesahau?” “Sijasahahu ila nilitaka atulie kwanza. Tusimpe mambo mengi kwa wakati mmoja.” Pam akabaki akifikiria kwa muda kisha akamwambia Mill.

“Naomba mpigie simu nimshukuru.” Mill hakuamini. “Au unasemaje? Naona anajitoa kupita kiasi!” Hakutaka kuweka neno ila akampigia simu mama Colins. “Pam anataka kuzungumza na wewe.” Kisha akamkabidhi simu.

Upendo husitiri wingi wa dhambi. “Mama shikamoo.” “Hujambo Pam mwanangu?” “Sijambo. Nataka kushukuru kwa chakula. Asante.” “Karibu. Nimekupakulia cha kwako tu maana mjukuu ameniambia yeye ameshiba sanaaa!” “Huyu hana utani na chakula. Akikwambia ameshiba, jua ameshiba kweli. Asante. Ila naomba usihangaike kesho. Pumzika bwana! Mama mwenyewe Mungu akipenda ataingia hapa usiku usiku. Itabidi akute chakula, kwa hiyo atalala, kuja kuamka ni mchana. Usisumbuke.”

“Basi wewe pika cha usiku huu, cha mchana niachie mimi. Nitakileta na kuja kumsalimia na zawadi zake.” Pam akacheka asiamini. “Kweli?!” “Kabisa. Nimefurahi kweli, nataka na sisi tuwe miongoni mwa watu wa kwanza kumkaribisha mjini. Nimuonyeshe saluni zinazotutoa uzee.” Pam akaanza kucheka. “Hutaki uzee mama yangu?” “Hakuna mzee mjini. Nikishampeleka saluni, nikamuonyesha maduka yetu ya kututoa uzee. Apate vitu viwili vitatu ndio roho yangu itatulia. Sio aje huku akumbuke nyumbani kwa upweke kama wenyeji hatupo bwana!” Pam alifurahi sana.

“Yaani wewe ukiwepo kazini, yeye anakwama kama vile ndugu ni mmoja tu mjini! Shema amenionyesha picha zake, nishajua wapi pakumzungusha. Miili yetu inaendana kabisa. Wewe niruhusu kesho na mimi nije. Tufahamiane. Uniachie mimi.” “Nimefurahi mama, nimefurahi sana. Asante kumfikiria mama yangu. Najua na yeye atafurahi. Asante mama. Basi karibuni hiyo kesho. Nitakuelekeza wala hutapotea.” Mill aliposikia hivyo, akahema kwa nguvu.

~~~~~~~~~~~~~~

Katika mavumbi ya maanguko, chipukizi huota. Kutoka kwenye kilio, sauti ya matumaini huzaliwa. “Mama naona ujio wake wa mjini unaanza kwa baraka! Anaanza na wenyeji.” Akaongea akimrudishia Mill simu yake asijue jinsi alivyofurahi huyo Mill. “Nimesikia. Na utamfurahia huyo mama. Mtulivu sana kama binti yake Connie.” “Nimemsikia hata zungumza yake. Tulivu.” Akamuona anafikiria.

“Ni nini tena?” “Nina wazo. Tulaleni hap…” “Hapana Pam bwana! Si tumekubaliana tutarudi akifika? Wewe unataka nilalie kitanda cha mama mkwe!” Pam alicheka sana. “Kwanza hapa pako tayari. Twende tukapumzike. Wakiwa wanakaribia watatupigia simu, tutarudi na chakula. Mkishasalimiana ndio tunaondoka.” “Au mimi nibaki nitakuja baadaye au mtakuja huku na Shema mchana?” Mill akabaki akimtizama.

“Basi twende. Naona unataka kuanza kukasirika.” “Naona unanigeuka gafla wakati tuliweka mipango vizuri tu.” “Basi twende.” Wakatoka hapo kurudi kwao wakiacha hapo mazingira mazuri. Ila Mill hakutaka kabisa kumzungumzia Kamila. Akaona aache yatakuja jitengeneza yenyewe.

Hatimaye Mwangaza Mwishoni Mwa Giza Nene.

Njia ya mama Eric imekuwa ndefu, moyo ulishachoka, lakini hatimaye mbele kumeanza kutoa mwangaza. Mwangaza wa matumaini, wa neema, wa kufufuka kwa ndoto zilizozimia. Pam, Mill na Shema walirudi tena mchana baada ya kumuacha apumzike yeye na msichana aliyekuwa amekuja naye.

Akahakikisha mama yake ameoga vizuri na kuvaa mavazi mazuri kabla ya mama Colins kufika hapo na chakula. Ungejua Pam anayo furaha. Mill alikuwa akimwangalia tu anavyohangaika na mama yake. Mwishoe akaona aende akachungulie ofisini. Akawaacha.

Mida ya saa saba mama Colins na Connie wakawa wameingia hapo na vyakula kibao! “Nakushukuru mama. Asante sana. Naviweka mezani tuanzeni kula sasahivi.” Nyumba ikazidi kuchangamka. “Ila umepika vingi!” “Kamila huyo. Alikuwa akipika tokea asubuhi.” “Na Kamila anapika! Nilikuwa nikila vyakula alivyokuwa akimpikia Mill, alipokuwa akienda kwake! Aisee amejaliwa kupika. Nawashukuru sana.” Wakagundua amejitoa kwenye ukaribisho aliokuwa akifika kwa kina Mike hapo zamani. Kwamba alikuwepo kwa kina Mike kwa mgongo wa Mill sio yeye aliyekuwa akikarimiwa. Wakalibeba na kulinyamalizia. Zikaanza stori, mama Colins akizungumza na mama Eric na vicheko.

“Kesho kanisani. Nimekuletea nguo ya kanisani na viatu vyake. Mkoba na hereni. Connie nenda kalete. Naamini utapenda tu na nina uhakika vitakuenea. Shema alinionyesha picha zako, kama nimekosea basi kidogo sana.” Mama Eric akajisogeza kwenye kochi walilokuwa wamekaa na kumpa mkono kabisa akishukuru.

Bwana mama Colins alijifungasha! Vingine mpaka Shema ikabidi atoke. “Hizi nguo za ndani nilijua tu zitakufaa. Ila sidiria ndio sikujua size yako. Ila magauni ya kulalia haya ndio mazuri na joto la huku kwetu Dar. Na mafuta mazuri. Haya yatakufanya unukie wakati wote.” Akaendelea kumpa. Ikawa ni zaidi ya kuomba msamaha kwa Pam. Akabaki akingalia jinsi walivyowakarimu.

~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda Mill akarudi. Akawakuta bado Connie na mama yake wapo lakini ndio wanakaribia kuondoka. “Kesho jumapili mje nyumbani kwa chakula cha jioni.” Pam akamtizama Mill, Mill naye akabaki akimtizama. “Mje na mama. Apaone nyumbani kwa kina Mill, tujipange mambo ya harusi. Tujue tunavaa nini. Sisi wamama wa maharusi tunatakiwa tukitoka pale, tumependeza na tuvae kitu kinachofanana. Au unasemaje?” Yaani mama Colins alikuja hapo akiwa amejindaa kumfanya Pam ajisikie ni mmoja wa familia.

Mama Eric yeye hana moja, furaha tele. Akakubali kwa haraka na shukurani kubwa kuona amepokelewa vizuri. “Na mimi nilitaka nimuombe baba anilete kwa anko, kuna saa amesema alininunulia, ila aliicha ofisini. Amesema niwe navaa wakati wote, na app yake ataniwekea kwenye simu. Itakuwa rahisi kujua nilipo kila wakati hata kama nikiacha simu mahali, atajua nilipo. Na itakuwa ikimwambia afya yangu. Si na wewe alikwambia?” Akamuuliza baba yake.

“Aliniambia.” Akamjibu na kumtizama Pam. “Wewe kesho ukiamka ni kujiandaa, uje umchukue mama. Kanisani, mje kule nyumbani.” Pam akacheka kama anayesita bado akimwangalia Mill. “Eti Pam?” “Nashukuru mama. Asante kwa upendo wako.” Kisha akarudisha macho kwa Mill.

“Naomba tuzungumze na Pam hapo nje kwanza.” Mill akatoka, Pam akamfuata. “Nisikilize Pam, uamuzi ni wako. Kama hutaki kwenda, naweza kuzungumza nao na wakaelewa tu.” “Najiona sipo tayari!” “Jua haitakaa ukasikia upo tayari, ni mpaka uchukue hatua, Pam. Moyo wako umeumizwa na Kamila. Lakini Pam, hawa watu wana upendo sana. Nimekutanishwa nao na Kamila, lakini naona jinsi wanavyonichukulia, utafikiri na mimi ni mtoto wao. Wamenipokea na kunifungulia mikono yote. Wananifanya ni kama mimi ni kijana wao mkubwa na Kamila ambaye ni yatima wamefanya kama mtoto wao kabisa.”

“Hawa watu wanajua jinsi tulivyo kuumiza. Mimi nikiwa kiongozi wa wote. Kisha Mike, Kamila mwenyewe na rafiki zangu wote. Walinituma kibinafsi nikwambie wao kama wao wanaomba nafasi kwako. Na nakuhakikishia hutajuta. Wana upendo kama vile wamezidiwa nao, na hawana pakuupeleka wanatafuta pakuupeleka huo upendo wakati wana watoto wawili wazuri sana. Colins na Connie. Kisha huyo Kamila waliyemkumbatia, kama binti yao.”

“Colins huwa ananilalamikia kuwa baba yake anamlinda sana Kamila mpaka kwake yeye ambaye alimpeleka pale. Anasema bila yeye wala wasinge mfahamu Kamila, lakini mzee amekuwa mkali naye, hataki hata Colins amsogelee hovyohovyo. Ninachotaka kukwambia ni watu wazuri sana.” “Kamila ni mnafiki Mill. Na mimi siwezi watu wanafiki. Inaniwia vigumu sana hata kuwa naye sehemu moja nikamsikia anachozungumza maana najua atanidanganya tu ili wewe umuone mzuri. Kamila ni mnafiki kwangu Mill. Nyoka anayeweza kukuua hivihivi na..” “Unaanza kupandisha hasira Pam. Tafadhali tulia.”

“Nimeshazungumza na Kamila, nimemuomba akuache kabisa.” “Lakini sasa ndio nitakuwa nikimfuata kwao!” “Wewe pima na uamue ukijua nipo nyuma yako. Lakini jiulize tu, kipi bora kukaa mbali na Kamila na kukosa watu wazuri kama hawa, ambao pia wamempokea mama yako vizuri, au kuendelea kufanya kama alichokufanyia Kamila, halafu ukose upendo wa kina Komba, mama yako akose mtu mzuri kama mama Komba na Shema akose anko kama Colins.” “Mill!”

“Mimi nakwambia ukweli Pam. Hutakuwa na tofauti na Kamila. Yeye alikufungia milango ya kwake, na wewe umeshindwa kumfungulia milango yako. Halafu mbaya zaidi wewe umebeba hatima yetu sisi wote watatu. Mama yako, Shema na mimi. Na nikwambie ukweli tu, hata Shema anamkwepa Kamila.” “Haiwezekani Mill! Mbona huwa unakwenda naye?”

“Mwanao anakusikiliza na kukuangalia sana Pam. Tokea siku ile alivyogundua Kamila alikutenda ubaya, akiwa nao kina Komba, zaidi Kamila akiwepo, hata nikimwambia anisubirie nakwenda chooni, jua atanifuata na kunisubiria nje ya mlango.” “Haiwezekani!” “Nakwambia kweli. Anamkwepa Kamila mpaka Colins amejua ndio maana unamuona anahangaika na kumnunulia zawadi ili tu kumfanya awe karibu. Akishamsalimia Kamila, akimuongelesha tena, unamuona anakosa raha kabisa anazidi kunisogelea karibu kama ambaye anamuogopa. Huwezi muacha na Kamila sehemu moja akatulia. Anajawa wasiwasi, anabadilika mpaka anakuwa mwekundu.”

“Nafikiri Kamila alivyogundua, akawa anamuacha. Akimsalimia hatamuuliza kitu tena anaweza ondoka kabisa hapo kama mimi sipo ili kumfanya atulie. Haya, na ujue hawa watu siwezi wakaribisha nyumbani kwetu nikijua wewe upo na umeshindwa kuwapokea. Siwezi. Inamaana itaishia ni mimi kuwa nikienda tu kwao na si vinginevyo. Kwa hiyo jua umebeba hatima yetu sisi wote watatu.” Pam akabaki akifikiria.

“Lazima wewe uwe zaidi ya Kamila ili kulimaliza hili. Lakini si kwa kufanya kilekile alichokifanya yeye. Pengine atajifunza kutoka kwako. Kwamba utamsaidia abadilike.” Akatulia akionekana anauzito bado. “Chukua hatua ya mwanzoni. Taratibu ruhusu kuipokea kila siku itakavyokujia. Usifikirie mambo mengi kwa wakati mmoja. Utajichosha na hutakuwa na majibu yote.” “Sawa. Na samahani Mill. Kamila aliniumiza sana.” “Natambua na usifikiri sijazungumza naye. Nimezungumza naye tena kwa ukali kabisa. Hakufanya vizuri.” Wakatulia kidogo, akamuona anarudi ndani, Mill akamfuata.

“Mama Colins, ulitaka tuje nyumbani saa ngapi?” Alifurahi Mill, akamtizama mama Colins kwa shukurani maana alifanya jambo kubwa sana hakutegemea.

“Mkitoka tu kanisani, nyinyi mje. Sisi huwa tunakwendaga ile ibada ya kwanza kabisa. Kwa hiyo tunawahi kutoka. Tutakuwepo tu nyumbani.” Huyo mama akatoka hapo akiwa amejenga daraja ambalo pengine ingechukua muda mrefu sana kujengeka na neno samahani wala lisingefaa.

Wakati wanaagana, Mill akamkumbatia kwa nguvu zote mpaka mama Colins akacheka. Kisha akamnong’oneza sikioni kwa sauti ya chini. “Asante.” Mama Colins alicheka tu bila ya kujibu. Wakaondoka.

Baada Ya Dhoruba Za Ndoa Zilizosheheni Majonzi Na Majaribu.

Pius alifika kwake akiwa amechelewa. Maana simu ya Nyange ilimkuta amekaa mgahawani akila huku akisoma magazeti na kuangalia taarifa ya habari. Ule mgahawa ulikuwa tulivu, ulimfanya atulie na kupoteza mtiririko wa masaa.

Alifika kwake nyumba ilikuwa kimya mno, kuashiria kila mtu alishakwenda kulala. Akapandisha ngazi taratibu akijua wazi Raza hatakuwepo chumbani kwake. Akaingia chumbani kwa Polla kwa kunyata. Akamkuta amelala na toi lake. Akamuhurumia sana binti yake. Akakaa pale kwa muda akijua Raza amelala chumbani kwa Poliny.

Akatoka kwenda kuoga na kwenda chumbani kwa Poliny. Akamkuta Raza amepiga magoti sakafuni lakini ameegemeza kichwa kitandani, amelala hana habari, na bibilia imefunguliwa na kuachwa wazi hapo pembeni. Akavuta pumzi kwa nguvu na kumsogelea pale alipopiga magoti. Akatoa mashuka kitandani, akawa anamnyanyua. Akashituka sana.

“Nakusaidia kupanda kitandani.” “Nimepitiwa na usingizi.” “Panda ulale vizuri.” Hata hakuongeza neno. Akapanda. Akamsaidia kumfunika vizuri. “Asante akashukuru akijiweka sawa asiamini akihisi ni ndoto. “Pius!” Akabaki akijiuliza. “Unataka chandarua?” “Hamna mbu. Juzi alipita mtu wa famigation. Nitakuwa sawa. Nenda na wewe ukapumzike.” Pius akahema kwa nguvu na kuamua kutoka.

Akamuwahi alipofika mlangoni. “Pius?” Akageuka. “Nimeacha kuweka vitu vibaya kwenye chakula. Usiogope kula nyumbani ukajitesa kula nje. Chakula kipo salama. Unachokula wewe ndicho anachokula Polla, na mimi nakula hichohicho. Nimebadilika mume wangu.” Pius akabaki amesimama.

“Na kama hujala, nimekubakishia. Kipo mezani.” “Labda kesho asubuhi kabla sijaenda kazini. Sasahivi nimeshiba.” “Kwa hiyo asubuhi nikuandalie?” Pius akabaki kimya kwa sekunde kadhaa kama ambaye anashindana na nafsi lakini akasema, “Nitashukuru.” “Asante Pius. Asante sana.” Pius akatoka.

Raza alilala na kilio cha furaha. Akatamani kumwambia mtu, ila akatulia. Akakumbuka kumshukuru Mungu na kulala.

~~~~~~~~~~~~~~

Asubuhi akawahi kuamka mapema akiwa amejawa morali kwelikweli. Machozi yaliyomwagika yameotesha maua ya matumaini, na maumivu ya jana yamekuwa mbolea ya kesho yenye furaha. Raza mfanyakazi wa kuajiriwa, na yeye anatakiwa kazini kama Pius tu. Ila alijaliwa mkono mwepesi na mzuri sana jikoni. Alijua mumewe hukipenda chakula chake. Akamtayarishia kifungua kinywa cha nguvu na kurudi chumbani kujiandaa.

Akamkumta anamalizia kuvaa. “Kila kitu kipo mezani, tayari.” “Sasa wewe mwenyewe umekula?” “Nilikuwa nakula huku nikitayarisha. Sitaki kuchelewa.” “Polla?” “Na yeye anamalizia. Isa ameshafika kumchukua. Nilimsikia akimuhimiza akazane watoke.” Pius akaendelea kuvaa.

Raza akawahi bafuni, akashitukia Pius anafungua mlango. “Mchana una ratiba gani?” “Nakuwepo tu ofisini. Vipi?” “Nitakupitia twende tukale.” Raza alibaki amepigwa ganzi katikati ya shower, na sabuni mwilini, maji yakiendelea kutoka ameshikilia dodoki lenye sabuni. Baada ya kilio cha Raza kisichosikika, na maumivu ya moyo yaliyotafuna usiku, leo moyo wake unainuka polepole kama jua la mapema. Pius akatoka bila ya kujibiwa. Akala na kuondoka akiwahi foleni.

Ndoa Na Iheshimiwe Na Watu Wote

Akiwa ofisini kwake mida ya mchana akamsikia Pius akitaniana na sekretari wao hapo nje. Akajua amefika lakini akawa kama bado haamini! Pius! Tena amemfuata mpaka ndani ofisini na si kumuita atoke! ‘Kama ni usingizi saidia nisiamke Mungu wangu.’ Kweli baada ya dhiki, imekuja faraja kwa Raza. Na baada ya giza nene, jua limeanza kuangaza kwa nguvu za aina yake. Akachukua pochi yake na kutoka.

Bwana Raza alipendeza mno. “Umependeza.” Akamsifia mkewe wakiwa wanasubiria lifti. “Asante.” Ndilo aliloweza sema Raza, kwa hofu akijiwinda maneno.

“Unahamu ya kula nini?” Mumewe akamuuliza. “Chochote.” “Unauhakika?” “Kabisa. Nashukuru kuja kuni…” Akasita. Pius akamtizama. Akamuona amepoa. “Karibu.” Wakaondoka na gari ya Pius.

Raza akashangaa wanarudi kwenye mgahawa uleule aliomtoa mahirizi kwenye pochi. “Hapa siwezi kuingia Pius. Nasikia aibu! Hakika siwezi.” “Sasa utakimbia mpaka lini? Si bora unarudi na mimi niliyekuabisha siku ile?” Raza akashangaa kidogo na kumtizama. Maana alikuwa kama anayejilaumu tena

Mimi ndio natakiwa kuona aibu sio wewe. Nilikudhalilisha Raza. Haikuwa sawa kwako.” Bwana Raza alilia, hakuamini.

“Nilikuwa na hasira, nikashindwa kukusitiri. Yale yote nilitakwa kuyafanya sehemu ya ndani. Haikuwa sawa, na mimi nilikosea. Samahani.” Aisee hakuwa akiamini. Akamuacha akilia na yeye kama ambaye hakutegemea alichofanya, akabaki ametulia kwa muda mkewe akijaribu kutulia.

“Ila kama bado unaona haupo tayari, twende sehemu ingine. Hapa nimeshafanya mazoea. Nina sehemu maalumu nakaa wakati nakula. Na wahudumu wake wameanza kunijulia kama wewe.” Raza akacheka akijifuta machozi.

“Masharti mpaka mahotelini!” Pius akacheka tu. “Kwa hiyo hapa ndio wapinzani wangu?” “Hawafiki hata robo yako. Na wala si nakupamba! Kifungua kinywa cha leo ulichonitengenezea ni bora mara elfu kuliko walichokuwa wakinipa hapa kila siku. Twende ukale chakula chao ndio utaamini.” Raza akaanza kujisikia vizuri. “Au unataka twende kwingine?” “Naomba tutafute kwingine Pius. Najisikia aibu sana. Bado sijapata ujasiri.” Pius akaondoa gari hapo bila nyongeza.

Akamfikisha kwenye mgahawa mzuri sana. “Nashukuru kunielewa.” Akacheka tu na kwenda kumfungulia mlango. “Asante.” Wakaongozana mpaka ndani, wakatafuta mahali wakakaa. Kila mtu akaagiza kinywaji na chakula, wakatulia hawajui wazungumze nini.

“Hivi ujue mimi sijui kusoma bibilia?” Pius akaanzisha hilo na kumfanya Raza acheke. “Naona mwenzangu umekazana!” “Mimi mwenyewe ndio najifunza. Mambo mengine magumu nilikuwa hata sijui! Huwa namsubumbua kweli kaka Nyange.” Pius akacheka.

“Kama nini?” “Mambo ya Roho mtakatifu.” Raza akaanza kumuelezea mumewe angalau wakapata mazungumzo ya kuongea. Pius akabaki akimwangalia, akimsikiliza, kweli akagundua ni Raza wa tofauti. Akamuona taratibu anaanza kutulia, mpaka akatulia kabisa hata mikono na midomo vikaacha kutetemeka. Akamuhurumia na kuamini maneno ya Nyange kwamba kweli anamuogopa sana. Na yeye akawa anafanya kusudi kumuuliza maswali kumuonyesha hajui na anaamini anachokisema. Akaongeza ujasiri kumuelezea akiwa ametulia. Wakazungumza mpaka muda wao ulipoisha na kumrudisha ofisini kwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Mida ya jioni Raza huwahi kutoka na kufika nyumbani kabla ya mumewe ambaye mara nyingi hutoka na kupitia biashara zake. Siku hiyo nayo akajitahidi kuwahi kupika vizuri. Na hivi ashasifiwa anapika kuliko ile hoteli, basi ndio akazidisha.

Ila akashangaa siku hiyo Pius hajachelewa kurudi. “Polla yuko wapi? Au nishamchelewa?” “Nilikuwa namlazimisha atulie hapa, asaidie kupika, ndio akacheze game zake. Kamaliza kunisaidia mboga, kanikimbia. Atakuwa chumbani kwake anacheza game zake!” Pius akacheka.

“Acha nikacheze naye kidogo.” “Ujue atakushinda.” “Kwani mimi huwa nambishia? Poliny ndio mbishi. Mimi nilishasema sijui. Na nikamwambia asishindane na mimi, yeye anashinda kwenye game muda wote, siwezi mfikia.” Raza akacheka tu. “Nitarudi, acha nikakae naye kidogo. Ndio nije tule.” “Yeye ameshakula na kuoga huyo. Amebakisha kupiga mswaki, nije tuombe naye, awahi kulala. Kesho shule. Asije akakulaghai ukajisahau na wewe.” Pius akacheka akitoka. Maana walimjua Polla kwa game kama mtoto wa kiume! Na ukimchekea hapo, halali. Atakesha akicheza kama siku za ijumaa kuamkia jumamosi.

Akamsalimia baba yake wakati akiingia macho kwenye game. “Polla bwana! Hata huniangalii!” “Wataniua dad! Njoo ukae kiti cha pembeni.” Pius akavuta kiti na kukaa pembeni yake, Polla yupo busy anashindana na mwenzie mtandaoni, tena wa kiume huko upande wa pili. Pius akawa anamsikiliza. Mikono yote imeshikilia rimoti, busy akicheza hata hajali uwepo wa baba yake. Pius alipoona hivyo akaona bora aondoke tu, maana kila akiomba kucheza anaambiwa asubiri kidogo, hapewi.

“Sasa hapo usijisahau Polla. Mama yako amesema umebakiza mswaki na kusali.” “Sijisahau.” Anamjibu lakini macho yapo kwenye monitor. Screen ndogo tu iliyopo hapohapo chumbani kwake kwenye meza ya pembeni ya games zake. Akatoka na kumuacha. Huna utakachomwambia Polla na games. Na ukitaka kumfurahisha hata kwenye birthday zake, zawadi ziwe games. Hapo mtapatana.

~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi chumbani kwake kuoga. Wakati anatoka bafuni akamkuta Raza hapo chumbani akimsubiria. “Ungependa tuombe pamoja na Polla? Nimemwambia azime michezo yote, apige mswaki nitarudi niombe naye.” “Basi acha na mimi nije niwaunge mkono. Kwani mliacha kuomba na hawa vijana hapa?” “Naona tunavutana vutana. Nimebakiwa na Polla tu. Wao nafanya nao kila ijumaa. Hiyo nimewaambia nilazima.”

“Usichoke bwana Raza! Ulivyokuwa ukifanya ni vizuri sana.” “Kweli?!” “Kabisa. Jua una kondoo unaotakiwa utuhimize. Leo umenipata mimi. Kesho waambie wote hata Poliny, mwambie kuna ibada ya familia nyumbani, aje hata kwa masaa machache. Usichoke.” Raza alifurahi huyo!

“Au Poliny umwambie wewe?” “Hapana. Asikie kutoka kwako wewe mwenyewe.” “Mimi atanikatalia Pius. Unamjua Poliny kwangu. Lazima atanibishia tu na kunipa sababu akisema ana mitihani.” “Wewe mwambie kwa kumuhimiza. Atakaponipigia simu akilalamika, nitamwambia ni muhimu. Wewe mchungaji gani wa familia unashindwa na kondoo wachache hivi?” Raza alicheka sana. “Mchungaji mwenyewe sijui mambo mengi!” “Bora wewe unayejua machache. Nina uhakika Poliny yupo kama mimi tu. Wewe tupe kile kidogo unachokuwa unakielewa, tuwe tunakua pamoja.” Alimfanya Raza ajisikie vizuri sana.

Wakatoka hapo na kwenda chumbani kwa Polla. Akasoma naye neno lakini akitetemeka mbele ya Pius. Ila akajikaza. Kufafanua kwenyewe akawa anababaika, ila Pius akawa akimsikiliza kwa makini kitu kilichomtia moyo. Mwisho akampa nafasi Polla ya kuomba. Pius akashangaa mwanae anajua kuomba vizuri tu. Akaamini kweli huyo mtoto ni wa mama. Aliomba kwa uzoefu tena vizuri tu bila hata katekisimu. Akimuombea baba yake, Poliny, mama yake na ndugu wengine. Akamaliza ndipo wakamuacha amelala.

~~~~~~~~~~~~~~

Pius akapitiliza kwenda kula, Raza akarudi jikoni. “Kwani wewe ulishakula?” “Nilikuwa nikila na Polla hapa, ili atulie. Tulikula chakula nilichokubakizia jana. Hicho nimekupikia niliporudi.” “Asante.” Akamshukuru, Raza akacheka na kurudi jikoni maana alitoka alipokuwa akimjibu. Alishamuwashia taarifa ya habari akijua Pius anapenda sana habari. Akawa akila huku anaangalia BBC, Raza yupo jikoni akisafisha.

“Mbona shuguli haziishi huko jikoni Raza na wewe upumzike? Kwa nini usimuachie dada amalizie?!” “Aliondoka.” Pius akashituka sana, hakuwa hata na taarifa. “Lini tena?!” “Muda kidogo. Walimpa maneno ya vitisho juu yangu, akakimbia. Polla alirudi nyumbani hakumkuta. Akanipigia, ikabidi nirudi nyumbani, usiku wake nikamuuliza yule kijana akasema ameondoka kwa hofu. Kina Mamu na watoto wa shangazi walikuja hapa na kumpa maneno, akakimbia.” Pius akazidi kumuhurumia.

 “Daaah! Sikuwa nikijua kabisa! Sasa unafanyaje?” “Hivyohivyo. Nishazungumza na Polla. Akiwa anarudi nyumbani, anakuwa anaendelea na ratiba yake ileile na kumwambia asubiri asiogope. Na mimi najitahidi sichelewi kurudi ili asikae peke yake muda mrefu maana sitaki kijana awe naye ndani peke yao. Nakuwa nikimpigia mara kwa mara kuhakikisha yupo salama mpaka nikirudi mwenyewe.” Pius akabaki akifikiria na kuzidi kushangazwa.

~~~~~~~~~~~~~~

Kwa hakika yake hayakubadilika kabisa hapo ndani kiasi cha kuonyesha utofauti. Bado alikuta nguo zake safi na zimepangwa vilevile kila wakati. Chakula ni yeye tu alikuwa akikataa kula, ila hakuwahi kukosa chakula sehemu yake ambayo hupenda kukaa. Hakujua hata kama hakuna msichana wa kazi, kumbe Raza ndiye anayepambana kufanya yote hayo na yeye akiwa na majukumu ya kiofisi! Akabaki akitafakari.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipomaliza ya jikoni akawahi kuoga chumbani kwao ili ampishe Pius alale. Akaingia kuoga, Pius naye akarudi kusafisha meno. Wakati anatoka na taulo, akamkuta mumewe kwenye sinki hapo nje ya bafu hukohuko chumbani akisafisha meno. Bafu la chumbani kwao lilikuwa kubwa. Lina chumba cha choo, bafu na hilo sinki kubwa lililo na pande mbili. Wake na wa Raza ambako kuna mafuta yake baadhi na pafyume zake kama upande wa Pius tu. Mbele yake, yaani ukutani kulikuwa kuna kioo kikubwa.

Akasogea kusafisha na yeye meno Pius akimtizama kupitia kioo akiwa amesimama upande wake akiendelea kusugua meno. Kimya kila mtu akifanya lake. Pius akamaliza na kujikausha, akarudi chumbani. Raza naye akamaliza akajipaka mafuta yake ya usiku, akavaa nguo zake upande wa nguo, chumba cha pili ilipo closet, hukohuko chumbani kwao. Akatoka.

“Usiku mwema Pius.” Akawa akimuaga ili atoke. “Njoo kwanza. Nina zawadi yako.” Raza akacheka akisogea. “Asante.” “Sasa unashukuru hata hujajua ni nini!” “Kile kitendo tu cha kunifikiria. Nashukuru.” “Sasa ukiona zawadi yenyewe ndio utapiga goti kabisa. Kaa.” Raza alicheka sana. “Pius!” “Sasa wewe hujaona zawadi yenyewe unashukuru. Ukiona je?” “Haya tuone.” “Kaa, halafu nipe mgongo.” Tayari akajua ni nini amemnunulia. Akafurahi.

~~~~~~~~~~~~~~

Roho iliyovunjika sasa inapumua tena, ikiamini kuwa kila giza lina mwisho. Hatimaye, {Mama Eric, Kina Komba, Mill, Pam, Mina, Andy, Pius hata Raza,} wanatembea kwenye njia mpya wakiwa na tumaini mkononi, na imani moyoni, kuwa hata baada ya dhoruba, huchanua tena, na maisha huanza upya kwa mwangaza mpya.

Ni nini kitaendelea mbeleni?

Usipitwe.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment