Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 60. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 60.

Ni kweli kosa la leo, machungu ya baadaye. Na huwa ni kweli Mungu husamehe na hakumbuki dhambi zako endapo utatubu kwa kumaanisha. Lakini hutaepuka kulipa garama. Ndivyo ilivyokuwa kwa Raza. Kivuli cha matendo yake, vilianza kujitokeza kwa machungu. Haikuwa rahisi kama alivyodhania. Kutubu, kwa ahadi ya Mungu kuweka mbali dhambi zake na kuto kukumbuka kabisa. Ila haikuwa hivyo kwa wanao mzunguka. Hawakusahau.

Pius alibadilisha hicho chumba kikachukua sura yake wala si ya mke wake. Hofu aliyokuwa nayo Pius akaipata yeye. Akawa anaogopa kuwa na mumewe chumba kimoja au hata sehemu moja peke yao.

Poliny alipenda shule na kuizingatia. Kurudi kwake nyumbani ilikuwa ni kama hana mitihani, tena kwa muda mfupi. Kwa hiyo Raza alikuwa akibakiwa na Polla, na Polla mwenyewe akiwa nyumbani yupo kwenye monitor yake akicheza game muda wote mpaka mama yake amlazimishe kula au kusoma au kulala.

Akajikuta mpweke lakini akifanya kama alivyoambiwa na Nyange. Kila siku jioni anaita wote mpaka kijana wake wa nje, wanafanya maombi kwa pamoja.

Vikao vya nje akaacha kabisa. Ikawa kazini, nyumbani. Wakisha kula, anawaambia wasome bibilia ambayo alikuja pewa na huyohuyo Nyange. Raza hakuwa hata na bibilia. Na Nyange ndiye alikuwa akimuongoza jinsi ya kuisoma hiyo bibilia. Akiwa na swali, basi atamtafuta Nyange, atamuuliza mambo ya kiroho na kumsaidia.

Lakini mambo yake na Pius hayakurudi kuwa sawa. Tabia ya Pius kula nyumbani aliacha kabisa. Kila Raza alipokuwa akimkaribisha chakula, alimwambia yeye alishakula. Aliwahi kutoka asubuhi na kwenda kula hotelini. Mchana hivyohivyo na jioni alipitia kula mahotelini ndipo anarudi nyumbani. Hata maji ya nyumbani hakuwa akiweka mdomoni. Akijua mama yake yupo nyumbani, anakwenda kula kwao ndipo anarudi nyumbani.

Raza hakukata tamaa. Kila aliporudi alimwambia kuna chakula. Jibu lilibaki lilelile, ‘nilishakula’. Kama atawakuta wakiomba, atakaa hapo sebuleni akimtizama anavyofanya. Wazi alimuonyesha hamuamini. Akisema fungeni macho tuombe, basi yeye atabaki akimtizama mpaka amalize kisha kumuaga binti yake, anakwenda chumbani kwake.

Ilikuwa ikimuuma Raza, ila hana jinsi. Akiingia chumbani atakuta tv ya chumbani ikiendelea na taarifa za habari yeye akisoma kitabu. Pius alikuwa msomaji wa vitabu kama baba yake na ndugu zake wote na ndiko Poliny nako alipochukua kupenda vitabu. Walipenda sana kusoma.

~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa anaingia chumbani endapo atamkuta mumewe basi kimya kama hakuna aliyeingia hapo. Hatatoa macho kitabuni wala kutingishika kana kwamba hakuna aliyeingia hapo. Raza ataishia kuoga, kubadilisha nguo za kulalia na kutoka hapo chumbani kwenda kulala chumba cha Poliny ambaye hayupo hapo nyumbani bila ya kuulizwa la kheri wala la shari. Wawili hao wakageuka kama wazazi tu, tena wanao lazimika kuwa sehemu moja.

~~~~~~~~~~~~~~

Hayo maisha hapo nyumbani kwao yakaendelea. Hakuna kusemeshana isipokuwa ikilazimu. Tena zaidi yanayowahusu watoto. Pesa ya chakula akawa anatoa kama kawaida, ya ziada kwa Raza alishamwambia yeye ni mfanyakazi, analipwa mshahara, atumie pesa yake kwenye mambo yake.

“Sirudii kukupa pesa yangu kwa ajili ya kuja kuniangamiza mimi mwenyewe na watoto wangu, halafu ukiitumia kwa starehe zako na wanaume zako. Nakuwa nikihangaika kwa ajili ya wanaume zako! Hapana Raza. Tumia pesa zako. Matumizi ya humu ndani, mishahara ya wafanyakazi na magari yote itabaki juu yangu. Mambo yako binafsi, jigaramie. Na waambie mabwana zako huko nje, unanipumzisha, ni zamu yao na wao kukutunza.”

“Mimi nilikuwa nikikutunza, wao wanakufaidi. Sasa waambie maadamu wananufaika na huo mwili wako, wanawajibika kuutunza pia.” Raza alishindwa kunyanyua mguu. Ilikuwa kama amegongelewa misumari. “Si Chezo na yeye anakazi?” Kimya. “Nina uhakika hatashindwa kulipia chumba chenu mnachokuwa mkikutana kila siku mchana, na kukupa za matumizi yako binafsi kama anavyofanya kwa mke wake.” Akahitimisha na kurudisha macho kwenye kitabu. Raza akatoka kurudi kulala chumbani kwa Poliny maana Polla alishalala.

~~~~~~~~~~~~~~

Maisha hayo yakaendelea, Raza akipambana na maisha mapya ambayo hajawahi ishi kabla. Mapya halafu machungu. Maisha ya kukutana kwa Paulina na wakwe, wakipika, kupakua kisha kula pamoja ni kama yalikoma kwa namna fulani, tena kimyakimya. Kwa wakwe ni kama walisitisha ule mtindo wa kila siku za jumapili kukutana na kupika pamoja. Shoga yake Paulina aliyekuwa akimpa maneno, ni kama hakutaka afike tena nyumbani kwake wala asogelee binti zake. Kwa hakika walimkwepa kwa wazi kabisa.

Raza alikuwa akiwa peke yake chumbani basi hulia sana. Alikuwa akimlilia Mungu hajui tena chakufanya. Alishatubu na kubadili njia zake, lakini ikawa ngumu kupata tena watu. Alikuwa akipiga magoti mwenyewe chumbani kuomba, hawezi ila kulia tu. Atalia hapo mpaka wakati mwingine huamka asubuhi akiwa amelala sakafuni. Kufunga ndio halikuwa tatizo kabisa. Tokea binti mdogo kwao walikuwa wakifunga. Akawa akifunga akimsihi huyo Mungu amsaidie bila ya kuona mabadiliko yeyote kwa wanao mzunguka. Akawa akikwepa kama mwenye ukoma. Akabaki peke yake ila hakuacha kujitahidi. Hayo maisha ya upweke yakukwepa yakaendelea.

Machozi Ya Moyo Uliojirudi.

Akaona ajirudi kwa vitendo kwa wakwe zake. Muda wa chakula cha mchana, akajitahidi kutoka kazini na kumfuata Paulina na mama Ruhinda wanao fanya kazi ofisi moja, akiomba watoke wakale pamoja, wote walikataa kwa kisingizio cha kazi nyingi siku hiyo. Raza akaondoka.

Alifanya hivyo zaidi ya mara tatu na mara zote walitoa udhuru. Siku moja alikwenda kula mchana, akakutana nao wamekaa sehemu wanakula. Akaumia sana. Ila mama Ruhinda akamwambia avute kitu, ajiunge nao.

Akakaa nao, akaagiza na yeye chakula. Kwa hakika kilikuwa kipindi kigumu hapo mezani, haikuhitaji kuuliza. Watatu hao waliokuwa wakipika na kupakua pamoja, gafla wakajikuta hawana chakuzungumza na kila mmoja anajiwinda kivyake.

Kilichomuumiza Raza ni pale kila mmoja alipovuta sahani yake karibu wakihamisha vinywaji mbali na yeye. Akaiangalia ile hali pale, mwishoe akaaga nakuamua kuondoka hata akiwa hajamaliza chakula chake.

~~~~~~~~~~~~~~

Hakukata tamaa, akajishusha tena. Maana Polla alishakuwa na hamu na binti wa Paulina. Wamekua pamoja. Marafiki mbali ya undugu. Akawapigia simu kila mmoja kasoro wa Dodoma, kuwakaribisha kwake kwa chakula cha mchana siku ya jumapili baada ya kutoka kanisani. Kila mtu alitoa udhuru mpaka mumewe. Raza aliumia sana. Alikuwa njiani akitoka kazini.

Alilia. Alilia sana. Njia nzima alikuwa akilia nakushindwa kutulia. Alilia sana hata hakujua anarudi vipi nyumbani na kukutana na binti yake akiwa na hali ile. Alikuwa na uchungu, hana wakumwambia ukweli. Kwa mashoga zake, asingethubutu kuwaambia kisha wajue ya undani! Itakuwa ni kama kujivunguoa mwenyewe hadharani.

~~~~~~~~~~~~~~

Uzuri siku anaitwa na mumewe na pochi yake kutoa mahirizi, ilikuwa ni mgahawa wa kitalii, hakuna aliyempiga picha wala kusambaza mambo yake. Siku anawekwa jela, alitoka kazini akiaga anakwenda kukutana na mumewe kwa chakula cha mchana. Akaishia kupelekwa kwa mganga wake na kufungwa. Kabla hapaja pambazuka, kuzaa kukamuokoa, akatolewa jela.

Siku inayofuata ilikuwa ijumaa. Akapiga simu kuwataarifu ni mgonjwa hatafika kazini. Jumamosi na jumapili hakwenda kazini. Mpaka jumatatu anarudi kazini, amepoa, hakuna aliyejua kilichompata. Asingethubutu kushirikisha mashoga zake na kujidhalilisha. Akajificha nyuma ya tabasamu lenye machungu makali na aibu.

Kwa mama yake mzazi ndio alisha muonya tokea zamani. Na huo ndio ulikuwa ugomvi wao wa kuwaweka mbali zaidi, mbali na dini. Raza akimuona mama yake hamtakii mema, haoni sababu ya kuhangaika kwake. Mama yake akimwambia yeye amekaa katikati ya jiji. Amemkuza Raza na ndugu zake bila tunguli ya mnganga, mbona wamekua na kusoma, na mume hajawahi mpa talaka hata mara moja! Hilo likamuweka mbali na mama yake. Leo anarudije?!

~~~~~~~~~~~~~~

Raza akaendelea kulia pake yake hajui chakufanya. Ikawa kama bahati, Nyange akampigia akiwa kwake na mkewe. “Vipi mbona unalia?” “Sijui chakufanya tena kaka yangu. Nimejaribu kila njia, nimefika mwisho. Njia hii ni ngumu. Ngumu sana.” “Tulia niambie kinachoendelea.” Raza akawasimulia Nyange na mama Briana hapo anapopita, wakamuhurumia sana.

“Hata Polla binti yangu huyu mdogo wanamuogopa jamani! Shangazi yake amefanya bithday ya binti yake, isivyo kawaida watoto wengine darasani kwao wamealikwa ila hajamualika Polla! Kweli jamani!?” “Wanasoma darasa moja?” Nyange akauliza taratibu tu.

“Umri mmoja. Shule moja. Darasa moja. Yaani tokea wapo tumboni, kliniki tumekuwa tukiwapeleka pamoja. Hawa watoto hawajawahi kutengana. Leo wanamuadhibu mwanangu kwa makosa yangu! Kweli! Sasa Polla anahatia gani? Na amejua kama kulifanyika sherehe. Akanieleza na kuniomba nimpeleke kumnunulia zawadi. Nikafanya hivyo mpaka nikamsaidia kuifunga. Amempelekea shule, anasema alipokea lakini baadaye akakuta ameitupa kwenye trash bin ya hapohapo darasani. Niambie kaka, nini nifanye tena. Mbona kama nishatubu na ukasema huyu Mungu amenisamehe?” Raza alikuwa akizidi kulia.

“Nisikilize Raza. Ahadi za Mungu ni kweli na amina. Akisema amekusamehe, yeye kama Mungu amesamehe. Ila hutakwepa kuwajibika. Sasahivi upo kwenye kuvuna madhara ya ulichopanda. Wema wako wowote kwa sasa, utaonekana kama ndoto ya usiku. Nakuhakikishia haitakuwa rahisi hata kidogo.”

“Hawa watu ulikuwa kwenye majumba yao ukila na kunywa nao. Tena ukiwapikia. Wamejua vitu vibaya ulivyokuwa ukiweka kwenye vyakula vya kaka yao. Wakaona madhara kwa macho yao, walishuhudia kaka yao na mtoto uliyemzaa wewe mwenyewe wakijipigiza kwa kupandwa na madudu uliyopandikiza wewe. Haya, Polla alikuwa ameshikilia hirizi aliyokuwa akitembea nayo kwenye begi la shule na aliimiliki akiing’ang’ania kuwa ndio ulinzi wake.” “Lakini yeye hana hatia kaka Nyange! Mimi ndio nilimpa.”

“Usinione mbaya ila najiweka pembeni nakupa mtazamo wa kweli wa watu waliokuwa karibu na wewe. Wao wanachojua ni huyo mtoto anatembea na nguvu isiyo ya kawaida. Wanamuogopa. Tafadhali wape muda. Unanielewa Raza?” Akazidi kulia.

“Endelea kujionyesha na kuthibitisha umesamehewa na umekubalika na Mungu.” “Tena bila kuchoka wala kuzembea. Usitoe mwanya wa kukata tamaa.” Akaongeza mama Briana. “Unamsikia mama Briana?” “Nimemsikia kaka.” “Ewaah! Nilikwambia, juhudi ileile uliyoweka kwenye ushirikina, weka kwa Mungu ukijua huku kwa Mungu utalipwa. Ni lini, mimi na wewe hatujui. Ila, utavuna kwa wakati, usipozimia moyo. Na utukufu wa mwisho ni MKUU kuliko wa kwanza.”

“Ila jua kwa hakika sasahivi unapimwa. Na Mungu pamoja na wanadamu pia.” “Na hata shetani pia anampima.” Akaongeza mama Briana na kuendelea. “Yeye anakupima ili ajue jinsi atakavyojirudi kwako. Ukizembea tu, jua ndio unamfungulia mlango.” “Umesikia?” “Nasikia.” Akaitika akisikika ameanza kutulia.

“Ndio jua upo kwenye kipindi muhimu sana, tena cha thamani. Ndio umezaliwa upya, unajifunza kwa upya. Kila kitu kama mtoto mchanga. Kilio hicho ni kwa sababu kuna tabia upya zinajengwa ndani yako, mwili na akili pia havijazoea, kama mtoto mchanga kabisa aliyeletwa hapa duniani. Sio rahisi mdogo wangu!”

“Kumtegemea Mungu peke yake! Tena ambaye hakujibu kama amekusikia au la! Si rahisi. Kwa mganga ilikuwa rahisi kwa sababu yupo mtu mliyekuwa mkijibizana. Una mpa haja zako, anakuahidi atafanya. Unaondoka kwa furaha ukijua haja yako umejibiwa. Ila kwa Mungu ni tofauti. Ni imani tu. Na ndio maana imeandikwa, bila imani, hauwezi kumpendeza Mungu. Unatembea kwa kuamini yupo mwenye nguvu zaidi ya wote, amekusikia na atatenda kwa wakati.”

“Wote hao nao wanapitishwa kwenye wakati mpya kama wewe tu. Kuna kitu kipya kinajengwa katikati yenu. Mahusiano mapya yanajengwa. Ila uzuri sasahivi mjenzi wako ni Mungu ambaye unamuomba kwa siri wao hawajui. Sasa akimalizana nao. Na wewe ukiwa umesimama hapohapo ukimsubiria Mungu! Nakuhakikishia, safari hii ukiwapata, yaani Mungu akiwarudisha kwako. Hivyo ulivyo ukiwa na Yesu ndani yako, jua umewapata moja kwa moja na utaitwa heri. Na utakuja niambia hiyo thamani Mungu atakayokuwekea.”

“Cha msingi ni usiache kutenda wema. Usiache kuwasamehe huku ukielewa hofu yao kwako. Na ukumbuke, wao walivyo sasahivi, japokuwa wanakuona wewe ndio mbaya, hawana neema uliyo nayo wewe sasahivi.”

“Ishi nao ukiwatangazia msamaha bila wao kukuomba msamaha. Ishi nao ukitambua nguvu ya msamaha uliyopewa wewe. Watakujaribu sana. Lakini wakikuona umesimama, watajirudi tu. Na usiharakishe. Polepole.” Nyange alizungumza naye mpaka akatulia kabisa.

“Samahani mama Briana na kaka kwa kuwaharibia muda wenu. Hakika nashukuru kujitoa kwangu.” “Usijali Raza. Hata sisi tunaishi kwa neema tu. Si watakatifu. Kuna kukosea na Mungu anatusaidia kila iitwapo leo. Usichoke.” “Nimeelewa, nashukuru.” "Sasa hapa kwangu sina binti wadogo, lakini Sonia anaye binti nafikiri umri wa Polla. Jumapili hii tunakutana wote mpaka mama yake na baba yake. Wote watakuja hapa kwangu. Karibu na wewe ubadili mazingira. Utoke kidogo nyumbani.” “Nashukuru mama Briana. Nitakuja na Polla, na Poliny kama atakuwa hana mitihani.” “Mkaribishe na Pius.” “Mmmh!” Wakamsikia akiguna.

“Pius ameniambia weekend hii ana mambo yake yakufanya. Hana muda.” “Basi nyinyi njooni. Na usiache maombi Raza. Omba tu. Omba hata kwa Roho. Mruhusu yeye Roho wa Mungu akuombee yale ambayo hata hujui utamwambia nini Mungu. Au umeshapoteza kunena kwa Roho?” “Tokea kaka aniombee, sijaacha mama Briana. Ila wakati mwingine nakuwa nauchungu nashindwa kuomba.” Akaanza kulia tena.

“Basi hivyo ndivyo vipindi vyenyewe vya kuomba kwa Roho, wala usiache. Mruhusu yeye aombe. Itakusaidia sana na hata huo uchungu utapungua.” Akazungumza naye kwa upendo kama alivyo mama Briana, mpaka akatulia kabisa na kuagana.

Kwa Pius.

Kwenye mida ya saa mbili usiku Nyange akampigia simu Pius. “Unaweza kuzungumza?” “Karibu.” “Samahani kama nakuingilia Pius. Lakini kwa kuwa uliniruhusu, nitazungumza tu na wewe, au ile ruhusa iliisha?” “Hapana Nyange. Karibu tu.” Akamtania kidogo. Nyange maneno mengi mpaka Pius akajikuta akicheka.

Ndipo akaanza. “Lipo neno kwenye kitabu cha Mathayo 12:43-45. Nilishakugusia. Sijui kama unakumbuka au unataka nisome?” “Tafadhali soma tu.” Pius akamruhusu kwa heshima. Alishakutana na Nyange, amefanikiwa sana kwenye maswala ya biashara. Halafu akajitoa sana kwake. Heshima ilikuwepo.

Mstari wa 43 unaanza kwa kusema, ‘Pepo mchafu amtokapo mtu, hutangatanga katika sehemu zisizo na maji, akitafuta mahali pa kupumzika, lakini hapati.’ Mstari wa 44 unaendelea kusema. ‘Ndipo husema, Nitarudi kwenye nyumba yangu NILIKOTOKA. Naye anaporudi huikuta ile nyumba ikiwa tupu, imefagiliwa na kupangwa vizuri.’ Mstari wa 45 unaendelea kusema, ‘Kisha huenda na kuwaleta pepo wachafu wengine saba, WABAYA kuliko yeye mwenyewe, nao huingia na kukaa humo.’ Hapa ndipo pabaya maana unamalizia kwa kusema hivi, ‘Nayo hali ya mwisho ya yule mtu huwa ni MBAYA kuliko ile ya kwanza.’ Sijui umenisikiliza vizuri?” Nyange akauliza. Pius kimya.

“Nazungumza sana na mkeo, Pius. Sana. Mida ya chakula cha mchana ambayo anatakiwa kula, lakini utakuta anajisomea bibilia ambayo kwanza HAIJUI. Ukristo ni dini aliyojipa ukubwani kwa sababu yako, WEWE. Unanisikia Pius?” Kimya.

“Huyu binti aliacha dini aliyokuzwa nayo. Ambayo kwake nirahisi. Amefuata dini yako, ambayo anaishikilia kwa ajili yako, WEWE. Haelewi yale mambo ya kawaida kabisa yaliyomo humo kwenye bibilia au kwenye ukristo kwa ujumla wake, lakini ameyashikilia kwa ajili yako, WEWE.”

“Raza hakukuzwa kwenye ushirikina. Anakiri ni mambo ameanza ukubwani tena mtu alimshauri ili akufunge WEWE. Safari moja, ikaanzisha nyingine mpaka akakosona na mama yake. Mkeo hana ndugu wa karibu sababu ya kukana dini ya kwao, na kukufuata wewe, na wewe hili unalijua.”

“Mkeo amefundishwa ushirikina mpaka ukamkolea. Ni mapepo ndiyo yaliyokuwa yakimuendesha, na wewe ni shahidi kwa sababu ulikuwepo wakati nikihangaika kuyatoa. Nimekusomea neno. Yale mapepo kutoka siku ile, haimaanishi hayatarudi tena. Kila wakati yanarudi kuchungulia kwa mkeo yakitafuta kurudi. Yakifanikiwa kupata mwanya hata kidogo tu, umenisikia nikisoma. Yatakwenda kutafuta mengine mabaya zaidi ya yale ya mwanzo. Nakuhakikishia Pius, si hali yake tu yeye Raza itakuwa mbaya, na nyinyi wote mnaomzunguka hamtabaki salama.”

“Kama mwanzoni alifanya aliyoyafanya. Sasa fikiria kila moja likaongeze mengine saba, tena mabaya zaidi, niambie watakaposimama binti zako na kijana wako!” Kimya.

“Ni pabaya kuliko utakavyofikiria, kwa sababu mama ana nguvu kwa watoto zake mno. Na hujui mwisho wa yote yatamfanya nini huyo Raza. Kilio cha binti yako siku ile usiku uliweza kukinyamazisha kwa kumtoa mkeo jela. Niambie yakija kumuua, utaweza kuishi na kilio cha Polla kwa muda gani?” Kimya.

“Mbali na majini, mkeo ni mzuri Pius. Mzuri sana kama msichana ambaye hana mtoto hata mmoja. Na kufunga ndio kumemrudisha kuwa binti mdogo kabisa. Sasa mimi sijui maisha yaliwapitisha wapi mpaka mkafungua milango ya uaminifu. Lakini mwanamke kama Raza na wanaume wa hapa mjini, kushinda vishawishi ni kwa neema ya Mungu kwelikweli, tena hii aliyopokea mkeo sasahivi.” Kimya.

“Ushauri wangu, mimi kama kaka yenu. Nikiwa natambua kabisa ulipoumizwa na Raza. Na mimi pamoja na wewe tunajua na wewe upo na sehemu yako ya makosa, pambana kwa kadiri ya uwezo wako, MSAIDIE mkeo kusimama. Anajitahidi sana. Lakini na yeye ni mwanadamu, ATACHOKA. Umenisikia Pius?” Kimya.

“Mimi ni kaka yako, nakwambia ukweli. Ukishindwa wewe kumtuliza Raza, wapo wanaume hawana muda mwingine zaidi ya wake za watu. Watamtuliza kwa kuanzia kumfariji, maana sasahivi ni mpweke. Na kwa jinsi ninavyozungumza naye, ametengwa na kila mtu. Sasa wakifanikiwa kumsikiliza tu, ATAACHA maombi yake binafsi. Ibada za nyumbani zitakoma. Utamrudisha baa, kule alikokuwa na marafiki wanao muelewa. Hali yake haitakaa ikawa hata nusu na ya kwanza.” Kimya.

“Pius?” “Nakusikiliza kaka.” “Rudi kwa mkeo. Msaidie ASIMAME. Tafuta jinsi ya kumsamehe, na mwambie umemsamehe. Anakuogopa sana. Sana. Anaogopa hata jinsi unavyomtizama. Mkeo ana hofu mpaka ukizungumza naye kwenye simu unamsikia akitetemeka. Muulize mama Briana, juzi ilibidi kwenda kumfuata kazini na kuomba naye ndipo akatulia. Haamini kama majini yamemtoka. Haamini kama yupo salama, mpaka nikaomba naye tena na kumuhakikishia yupo salama.”

Mtetee kwa aliowaumiza. Msaidie malezi ya Polla aliyemuathiri mpaka kutengwa na ndugu.” “Polla ametengwa vipi?” “Wewe unajua kama mtoto wa Paulina alikuwa na birthday, Seacliff hoteli siku ya jumamosi iliyopita na alialika watoto wengi darasani kwao kasoro Polla?” Pius kimya akiwa ameanza kuumia. Alipenda watoto wake sana.

“Inamaana umekimbia nyumba Pius! Yale niliyokwambia uyafanye hujayafanya!” Nyange akamlaumu. “Binti yako alipojua amemnyima mualiko, alijitahidi zaidi. Akamuomba mama yake amsindikize akamnunulie zawadi. Lakini alipo mpelekea zawadi siku ya jumanne maana siku ya jumatatu ndipo alipokutana na hizo taarifa kwa marafiki, darasani kuwa walikuwa kwenye party ya mtoto wa dada yako, yule mtoto alitupa zawadi aliyopewa na Polla.” Pius alihisi mtu anamchoma mkuki moyoni kwa maumivu.

“Polla aliikuta kwenye trash can. Akaja kumwambia mama yake. Inamaana wewe hayo yote huna taarifa nayo Pius! Malezi ya karibu kwa binti yako bado unamuachia Raza peke yake!” “Acha nikwambie ukweli Nyange. Nimeshindwa kabisa kuwa sehemu moja na Raza. Nimeshindwa kula nyumbani. Hata maji yamenishinda. Nakula mahotelini au kwa mama. Ndio maana nachelewa kurudi nyumbani, nakuwahi kutoka asubuhi ili nikale mahali niwahi ofisini. Na hapo ndipo ninapomkosa Polla.”

“Tunaamka wote tukiwa na harakati za kuwahi, nikirudi nakuta amelala. Ila nimekusikia kaka. Nitabadilika.” “Msaidie na Raza. Hatua ndogondogo kwa vitu vidogovidogo mpaka utajikuta moyo unafunguka kabisa. Unaweza kuzungumza naye na ndipo na wewe upate nafasi ya kumuomba msamaha kuzaa na mke wa mdogo wako.” Nyange akapiga ikulu kabisa, tena makusudi kumkumbusha na yeye ni mkosaji pia. Pius akapoa.

“Sijui kama umenielewa?” Pius kimya. “Unayo nafasi kubwa sana ya kutengeneza Pius. Usikubali safari hii ikawa WEWE ndio unatumiwa kuharibu kwako. Ni hilo tu.” Kabla hajakata akamsikia kama mke wake anamuongelesha.

“Pius?” “Nipo kaka.” “Mama Briana anawakaribisha wewe na familia yako jumamosi hapa nyumbani. Kina Sonia pia watakuwepo na familia yake.” “Naomba nisitoe ahadi tafadhali. Ila nawashukuru sana. Asanteni kuwa na sisi na kutuvumilia. Usiku mwema.” Akaaga na kukata simu.

Safari ya Machungu na Tumaini

Maisha ni safari isiyo na ramani kamili. Barabara zake hupinda na kupotea, mara jua linawaka, mara mawingu yanatanda. Kuna siku za njaa, na siku za shibe. Siku za vicheko, na siku za machozi. Lakini ndani ya kila giza, kuna mwanga unaojificha. Ndani ya kila huzuni, kuna matumaini yanayoota kama jani jekundu katika jangwa. Huu ndio uhalisia wa maisha. Si rahisi, lakini si bure. Kwa SUBIRA na moyo thabiti, hata tufani kali hupita, na alfajiri mpya huangaza tena.

Siku ya pili yake jioni baada ya mapumziko waliyoyasubiria wawili hao kwa zaidi ya miaka 10, kwa machungu kila mmoja wao pande ingine ya dunia Mill alitoka na Shema kwenda kwa kina Komba, baada ya kumshusha Pam, Kinondoni alipokuwa amepanga.

Aliwaomba wote wawepo. Walifurahi sana kumuona Shema. Hakuwa kama wale watoto wa kwanza wa Kisha. Basi yeye akifika hapo salamu ya heshima na cheko akiwaita dokta Komba na mkewe bibi na babu kabisa. Colins na mchumba wa Connie anko. Connie na Kamila anti. Na Mill pale alishawazoea. Ungejua ni ndugu wa damu.

Ilikuwa ni siku ya ijumaa ambayo mama Eric ameenda kuchukuliwa Lushoto. Walimshusha Pam hapo  Kinondoni kuandaa nyumba maana dereva alitaka kwenda na kugeuza nao, asilale.

Pam alikuwa amejawa furaha sana. Akaanza maandalizi ya kutoa vitu vyake na mwanae ili mama yake akija akute mazingira ya kwake wala si ya Pam na mwanae. Mill akatuma dereva wa ofisi hapo Kinondoni ili amsaidie kuhamisha vitu vyake na mwanae. Akawa akifunga na kumpa dereva anaweka kwenye gari, huku akizungumza na mama yake kwenye simu aliyekuwa akija na msichana wa kazi kutokea hukohuko kijijini kwao. Furaha kwa wote.

~~~~~~~~~~~~~~

“Hatimae namuoa Pam jamani!” Kila mtu alicheka hapo mezani kwa jinsi Mill alivyoongea. “Hongera sana.” Kila mtu alimpongeza. “Lakini wazazi wangu mimi nataka kuoa kabla ya Colins.” “Haiwezekani Mill!” “Sasa wewe unataka kuoa kabla ya kaka yako!? Wewe vipi Colins?” “Yangu inakaribia!” “Sasa yangu mimi ishafika. Na sitaki kikao. Sitaki kuchangisha yeyote. Nataka nyinyi wazazi wangu. Marafiki zenu wa karibu na ndugu tu. Sio kitu kikubwa, lakini naomba tumuandalie Pam kitu kizuri.”

“Ndoto zake anataka kuvaa shela kabisa. Na iwe kanisani. Pesa ipo naomba msaada wa eneo, chakula, vinywaji na picha.” “Wasimamizi?” Hapo akapoa. “Mwanzo alikuwa atusimamie Mike na Kamila. Mambo yameharibika. Hata sijui nani atatusimami! Kwa ubaya wa Sandra aliomfanyia Pam, sidhani kama ni busara kumuomba Jerry watusimamie.”

“Tuanze taratibu Mill. Usihamie kwenye majonzi. Najua Mike alikuwa mtu wako wa karibu na najua hata yeye atafurahia ulichomtendea. Umesimamia haki yake. Umepambana mpaka umehakikisha aliyemuua amekamatwa.” “Aisee namshukuru Mungu. Nafikiri hatima ya shemeji yake, nikimaanisha hukumu yake itakuwa mwezi ujao.” Akaendelea mwanae akimsikiliza na yeye.

“Aisee tenda wema duniani. Hata ukifa wema wako unakufuata. Ni kama Mike ameendesha kesi yake mwenyewe! Wamekuja kugeukana wale ndugu! Yule jamaa niliyemuweka anisaidie upelelezi, anasema walikuwa wakishindana kumtafuta wakishitakiana. Ila wote walisema mke wa Luca ndiye aliyekuwa anahusika.”

“Walitoa ushahidi wa kutosha. Na alipoenda kumkamata anasema alimbana kidogo tu, akaishia kukiri mwenyewe kama aliye changanyikiwa kabisa. Ananiambia eti damu ya jamaa yangu ni kali.” “Kivipi?” Mama Colins akauliza.

“Anasema ni kama imemrudi yule mama. Yupo kama amepagawa. Anaomba aadhibiwe yeye ili wanae wapone. Anasema eti damu ya baba yake Luca na Mike inamlilia na kufuata mpaka wanae. Wanataka kuwaangamiza.” “Kwamba alimuua mpaka mkwewe?!” Mzee Komba akashangaa sana.

“Acha baba! Huu uchu wa kuvuna usikopanda, unafanya watu kufanya mambo ya ajabu sana! Yaani yeye alimuua yule mzee akidhania akifa atamuachia mumewe mali, akaja kuachiwa Mike badala ya Luca. Anavyosema akawa anafanya kusudi Mike na Kamila wasizae ili wasije na wao wakamuachia mtoto wao mali zikazidi kupotea. Mganga aliyemsaidia kumuu baba yake mkwe ndiye akampa na wazo la kumuua na Mike. Sijui ikawaje, vya mganga akaona vinachelewa kwa Mike mwenyewe lakini vilikuwa vikifanya kazi kwa watoto wao au mimba alizokuwa akibeba Kamila, ndio akamuwekea sumu kwenye kinywaji alichokunywa Mike siku walipoenda kwake kwa chakula. Ndio chanzo cha kifo chake.”

“Aisee poleni sana Kamila na Mill. Pole sana.” “Sasa umeishia kumpa nani pesa uliyoahidi zawadi kwa atakayemtaja muuaji?” Colins akauliza. “Aisee yule mpelelezi amenikataza kabisa. Amesema itakuwa ni kama nawazawadia kwa uovu wao. Hawa watu walijua kabisa ubaya aliokuwa akifanya huyu mama tokea mwanzo Mike mwenyewe akiwa hai. Japo wanakiri hawakujua mauaji ya baba yake mkwe, lakini mauaji ya watoto wa Mike waliyajua! Kwa nini hawakukomesha tokea mwanzo?” “Lakini kweli!”

“Na ujue vile Mungu anavyo waadhibu, aisee hakuna aliye na sawasawa tena. Ni kama wote waliojua na kushiriki kwa namna moja au nyingine hawajabaki sawa. Mali alizoacha Mike zote, nikisema zote, ni ZOTE baba. Zimepotea kabisa. Nyumba aliyokuwa akiishi Kamila na Mike, nikikuonyesha kwenye picha ilivyokuwa zamani na sasahivi, unaweza sema ni gofu la wapi sijui!”

“Hivi nimemuomba mazungumzo Luca, ili aniuzie pale. Wote wameshindwa kuishi pale. Wamekimbia. Na eti wameshindwa kupauza! Sasa mimi nitamwambia napanunua kwa kuendeleza kile alichotaka Mike mwenyewe. Kamila apate sehemu yake. Alimtoa Kamila kwenye nyumba za Yatima, hakutaka kumuacha Dar akimangamanga. Nitapanunua kwao. Napajenga kama Mike mwenyewe, namrudishia Kamila. Yeye na Colins watajua wanachotaka kukifanya na ile nyumba. Lakini ni nyumba ya Kamila, na ndio yalikuwa matakwa ya Mike tokea mwanzo.” “Nashukuru Mill.”

“Usijali Kamila. Kwanza Mike ananidai. Nikimaanisha kunidai, kifedha kabisa. Nakumbuka niliwasimulia. Kila nilipotaka kumrudishia pesa yake aliniambia nitajua siku atakapoihitaji.” “Na kweli!” “Basi ndio hivyo. Acha nilipe deni lake.” Wakatulia wakifikiria.

“Sina nia mbaya ya kukutoa kwa Mike. Lakini nina swali juu ya Pam. Umejaribu kututambulisha kwake?” Mill akatulia akifikiria jinsi ya kujibu. Mwanae akamwangalia. “Niseme anawafahamu na hana neno hata nikija na Shema. Ndio maana mnaona nipo hapa na Shema.” “Niongeze swali jingine nikiwa na maana yangu.” Mama Colins akaendelea kwa tahadhari.

“Unafikiri nikimwambia tumfanyie bridal shower atakubali?” Mill akatulia akionekana ni kama anasita kujibu. “Wewe usisite kujibu Mill. Tuambie ukweli. Nia ni kuwapa kitu kizuri na kumfurahisha.” “Usihangaike mama yangu. Naomba tumpe muda. Sijui kama mnanielewa?” “Kabisa.” Mama Colins akajibu.

“Ila jua nakushukuru sana mama yangu. Asante.” “Kwa hiyo ushauri wa kwamba Kamila aendelee kuwasimamia na Colins…” Kabla hajamaliza swali lake Mill akaanza kutingisha kichwa kabisa akikataa huku akicheka. Wote wakacheka.

“Tumeelewa.” “Nawashukuru kwa kunielewa. Naombeni tumchukulie taratibu. Naamini atafika tu. Nilimuumiza sana. Na watu nilio waacha nyuma nao wakamtendea ukatili mbaya sana. Kurudi kwa yeyote yule sasahivi yeye anachukulia wanarudi kwa ajili yangu MIMI, wala si yeye na mtoto wake.”

“Inavyoonekana hakubadili namba ya simu mpaka alipojifungua Shema na kuuza simu niliyokuwa nimemuachia ili kujikimu na maisha. Kina Mike walikuwepo, lakini hakuna hata mmoja wao aliyejaribu kumtafuta hata kumjulia hali!”

“Sandra ndiye huyo alimfunga jela akiwa mjamzito. Akamtoa kwa kumpokonya gari. Hakuna aliyeniambia kama alikuwa mjamzito na wala hakuna aliyemtafuta hata kumjulia hali! Leo wanarudi kwake kwa sababu ipi kama si mimi tu.” “Pana ukweli, lakini sisi ni wazazi Mill.” “Wazazi wangu mimi na wa Kamila.” Mill akakaa sawa.

“Kitendo cha Kamila kushindwa hata kumfungulia mlango na kumpa maji akiwa mjamzito wa Shema, katika nyumba ileile aliyokuwa akikaribishwa nikiwa naye, na asiwahi hata kumtafuta hata mara moja, kwake anaamini Kamila alimwambia kwa vitendo hamtambui yeye isipokuwa mimi. Na hamtaki kwenye maisha yake. Sasa kwa nini sasahivi! Ndio anarudi kwenye sababu ileile, wote waliopo upande wangu ni kwa ajili yangu mimi si yeye na watoto wake.” Kimya.

“Tafadhali naomba tumuache. Hata mimi namchukulia taratibu sana nikijua jinsi tulivyo muumiza. Haikuwa sawa.” “Haikuwa sawa Mill. Hata kidogo. Ila na sisi tungetaka mahusiano naye. Tunampenda sana Shema. Sana. Ikija tokea unapata naye muda mtulivu wa mazungumzo mengine, utuombee nafasi na sisi. Hata kama kama si undugu wakaribu, basi mwambie na sisi tunamtambua kama binti yetu.” “Lakini acha nimuoe kwanza.” Walicheka hapo, hakuna aliyeamini.

“Hutaki kitu kiharibike?” “Aisee hapana. Nimemsubiria Pam, acha nimfikishe kanisani. Nihakikishe wameshatufunga pingu za maisha, ndio tuanze ujenzi wa nje. Ila mama Kenny huyo amesema lazima twende kwake. Hasahau jinsi alivyo mkarimu. Huko nitampeleka na kuona watoto wa Mgini maana na yeye aliachiwa. Hao hajawasahau japo amesikia habari zao ni mbaya, lakini naona anasisitiza niwakusanye kwa haraka na kuonana nao. Kwa hiyo natembea kwa tahadhari sana.”

“Nafanya anachotaka. Jana jioni alitaka twende kwenye kaburi la baba. Alisafisha na kuweka vyungu vizuri sana vya maua. Na naona alifurahi jinsi nilivyopatengeneza.” “Aisee umetengeneza vizuri sana Mill. Sana.” “Nashukuru Colins. Yule mzee ndiye amenipa haya maisha aisee. Bila yeye nisingekuwa hivi. Nataka wajukuu na vitukuu wapate kumbukumbu yake.” Wakatulia kila mtu akiwaza lake.

“Kwa hiyo Colins?” “Wewe oa tu, nakupisha.” Wakaanza kucheka na kutaniana. Angalau pakachangamka. Mzee Komba akalipokea hilo kwa heshima. Mipango ya harusi ya Mill na Pam ikaanza na kukubaliana siku maalumu ya kufanya kikao kizuri na watu wao.

“Mill, nikimtafuta Pam nizungumze naye ni sawa?” Kamila akamuuliza kwa unyonge. “Utamwambia nini, Kamila!?” “Nimuombe msamaha?” “Narudia swali langu, utamwambia nini? Kumwambia ulikosea, atakuuliza hayo umejua lini? Mpaka niliporudi mimi nchini na kumtafuta yeye ndio unagundua kosa? Kwa nini usimtafute wakati ule iwe leo?” Yaani yeye Mill mwenyewe akaanza kupandisha hasira.

“Ulikuwa kwenye hali nzuri Kamila. Ukijua ni mjamzito, hana kazi, kwa nini hukumtafuta?” “Mimi sikujua maswala ya kufungwa kwake Mill. Na Mungu wangu ni shahidi. Hilo Jerry hakusema kabisa.” “Kama ungejua, ungefanyaje?” Kimya.

“Eti Kamila? Ungejua kama alifungwa, ungefanyaje?” Wote kimya. “Tulikosa Kamila. Tumemkosea sana Pam. Mbali ya kufungwa kwake ulijua wazi yupo na shida na nilimuacha na mtoto. Hukumtafuta hata kujua kama alijifungua salama! Ukanyamaza kimya. Sasahivi unarudije?”

“Tafadhali naomba muache. Kama nilivyokuomba mwanzo, hata pale kazini muache kabisa. Maana mimi namjua Pam. Akishajua unahusika na ile hospitali kwa Colins na familia yake kupamiliki pale na wewe upo, inaweza muwia vigumu kuendelea kufanya kazi pale. Tafadhali naomba tumpe muda. Si mtu mbaya, ila ana vidonda tulivyo msababishia. Anapona, ila taratibu. Tumpe muda, naamini atafunguka tu yeye mwenyewe na kukusogelea bila ya wewe kuomba msamaha na kumuumiza zaidi. Mwache aje aweze yeye mwenyewe kuwa na sisi wote hapa, lakini isiwe kwa haraka na kumlazimisha.” Shema kimya ila akisikiliza kwa makini sana.

“Tumekuelewa kaka. Na nilikuahidi kule kazini tutaweka mazingira matulivu ya yeye kufanya kazi, itabakia hivyohivyo. Sisi tupange harusi nzuri itakayo mfurahisha huku tukifikiria wasimamizi.” Angalau Colins akabadilisha ile hali maana Mill alishambadilikia hata Kamila. Wakapata mlo wa pamoja, na kuondoka kumfuata Pam Kinondoni.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya mawimbi makali na upepo wa majaribu, bahari hutulia na angani huonekana upinde wa mvua.

Maisha, licha ya machungu yake, hubeba ahadi ya mwanzo mpya.

Upi kwa Pius&Raza? Pam&Mill? Mina&Andy?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment