Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 59. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 59.

 “Sasa kama upo tayari ni vya kwenda kuchoma vyote.” Nyange akaweka msisitizo. “Aisee huko nyumbani sitarudi.” “Na huo ndio mpango wa shetani. Kuchinja, kuharibu na kuangamiza kabisa. Atakukimbiza kwenye vitu vizuri ulivyopewa na Mungu. Usikubali. Yeye ndio anatakiwa kukimbia.” Nyange akaanza kuomba.

Pius naye akapandwa mashetani akaanza kupiga yowe na kujitupa kama Polla. Poliny analia sana kwa hofu. Nyange akaendelea kukemea, ya Polla tena yakapanda, yanadai vitu. Nyange akayakatalia na kuwaambia watoke kimyakimya, na yawaache wote huru. Akiwa peke yake, maana hapo ndio hali ilikuwa mbaya zaidi. Mama Ruhinda analia akihisi Pius anaweza kufa, kila mtu akazidi kukaa mbali. Bora Polla alikuwa mtoto na baba yake alijikaza akitoa vitu asijuimize. Safari hii ni wote wawili. Hakuna aliyetaka kuwa karibu nao ila Nyange ndio alionyesha ujasiri.

Akayakemea, wala haikuchukua muda, Pius na binti yake wakaachwa huru. Pius anarudiwa na akili zake, yupo sakafuni. Haelewi alifikaje pale. Nyange akamsaidia kusimama. Akamueleza kilichotokea. “Na Polla?” “Yupo huru. Lakini lazima kuzungumza naye ili akubali kuachilia hivi vitu na tuchome moto.” Ndipo wakakaa sasa.

Pius akaeleza mwanzo kuanzia pale alipowasilimulia mwanzoni kwenye pochi, mpaka kwa mganga walipoachana ila kwa sitara ili wanae wasiumie zaidi na hakuzungumzia juu ya mahusiano ya mkewe ya nje. Poliny ni kama alijua tu mambo ya mama yake. Hakushituka.

“Sasa, sasahivi mama yuko wapi?” Poliny akauliza swali lililomfanya Pius asite. “Maana nimemtafuta kweli huyo Raza mpaka nikaingiwa wasiwasi. Nimekwenda kwanu, nimeambiwa wote hampo. Mpo hapa na hakuna mtu kuingia ndani. Ndio nikasema nije nijue kulikoni.” Mama yake akaongeza.

“Raza amepelekwa jela.” Hapo ndipo wakashituka. “Ameshitakiwa kwa kosa la kukusudia kutaka kuua. Hawezi toka.” Bwana watoto wa Raza walilia. Wote wawili kama msiba. Polla anamtaka mama yake au apelekwe na yeye huko polisi akakae na mama yake. Poliny amepiga magoti wamsamehe mama yake. Atolewe. Huyo Polla ya uchawi alishaelewa. Hataki tena hata begi. Ila anamtaka mama yake. Watoto walilia hao. Hawasikii la mtu. Hapo ndipo Pius alipoelewa madhara ya kilichotokea kwa mkewe. Ila afanye nini? Raza ameshitakiwa. Kila mtu kimya.

Mama Ni Mama Tu.

Wanasema mtoto wa mwenzio mtamu akiwa amelala. Wakamuona Poliny anapiga simu, lakini bado analia sana. Hawakujua anampigia nani. Ikawa imepokelewa huko.

Wakamuona anapiga magoti. “Nimepiga magoti, naomba msamehe mama yangu. Nakuahidi hatarudia tena.” Mtoto alilia huyo kwenye simu kama amechinjwa na si Poliny wanao mjua wao.

Huyo mtoto alikuwa mbishi kwa mama yake kutwa wanabishana kwa hili na lile. Hata Pius hakutegemea alie hivyo baada ya kusikia yaliyompata mama yake. Kesi zake na mama yake ilikuwa ni kila leo kwa Pius. Na mara nyingi alizira kurudi nyumbani na kubakia hosteli sababu ya kugombana na mama yake.

Lakini usiku huo, ungejua alibebwa na tumbo la Raza miezi 9. Yale mapenzi kwa mama yake yalikuwa dhahiri hataki baya limpate mama yake. “Tusaidie mimi na Polla. Msamehe mama, anti Mina.” Pius aliposikia hivyo akashituka sana. Akataka kumpokonya simu, baba yake akamkataza. “Mwache.” “Tutazidi kuingia matatizoni baba!” “Yeye ndiye aliyempigia anti yake. Sio wewe. Mwache.” Poliny akazidi kulia.

“Tumeombewa wote. Tumepona. Na mama ataombewa, atapona. Msamehe mama yangu. Usimfunge, hatamdhuru tena Ayvin. Msamehe mama yetu, anti Mina. Polla hataweza kufanya kitu, bila mama. Shule itamshinda kabisa. Leo ameshindwa kulala na kusoma sababu mama hajarudi nyumbani, na kesho anamtihani. Msamehe mama.” Mtoto alilia huyo akisaidiwa na mdogo wake kama msibani. Nyumba yote simanzi.

“Naomba kuzungumza na baba yako Poliny.” Poliny akampa simu baba yake. Pius akapokea na kuweka spika wote wasikie. “Mina, nipo na wazazi, Paul, Paulina, Davi na mama yake Raza pamoja na Nyange aliyekuja kutuombea. Nimeweka spika. Nakuapia na Mungu wangu ni shahidi na hawa watanitetea, huyu mtoto amekupigia simu, mimi sijamtuma. Tafadhali mwambie Andy asije kasirika.” “Nipo hapa Pius. Aisee poleni sana.” Kwa kuchanganyikiwa na paniki  akawa hajaelewa, hiyo ‘pole’ ya Andy ikawashangaza wengine. Hawakutegemea.

“Naahidi hawatasumbua tena. Nitazungumza nao.” “Hapana Pius. Hao watoto ni wadogo sana. Hutaweza kuwakuza bila mama yao. Mina hana hofu na hayo mambo ya kichawi. Na tumezungumza kwa kina baada ya kupewa taarifa za kufungwa kwa Raza.” Pius akaendelea kusikiliza.

“Hivi tulipanga kumtafuta Sonia asubuhi nakumwambia tunafuta hiyo kesi. Raza ni mama Ruhinda. Kumfunga yeye ni kujidhalilisha sisi wote akiwepo mama aliyehangaika kujijenga sana hapo nchini na anaaminiwa na kuheshimiwa na wanawake wakubwa sana hapa nchini. Itakuwa tunamdhalilisha mama zaidi na kutesa watoto wake wasio hatia. Si sawa. Sisi tupo tayari kumaliza hayo mambo kifamilia si mahakamani. Kwanza Mina mwenyewe anaona hakuna kesi hapo, kwa sababu anasema hata huyo mganga asingeweza muua Ayvin. Anaona hamna kesi.” Mpaka Pius akalia. Bwana alilia Pius. Mpaka baba yake akachukua simu. Mama Ruhinda mwenyewe hakuamini.

“Nakushukuru sana Andy. Asante. Kibinafsi nakushukuruni sana. Mwambie Mina natoa shukurani zangu toka moyoni, asante.” “Hapana baba, tumefika mbali sana. Nafikiri ni wakati wa kuweka kikomo kwenye haya mambo. Lasivyo hapatakuwa na mwisho.” “Ni kweli Andy. Kweli kabisa. Ila nawaahidi mimi mwenyewe nitazungumza na Raza, naahidi hatarudia tena.” Mzee Ruhinda akaendelea.

“Raza anamtoto anayemtegemea sana. Ndio tumekuja kugundua leo, kumbe maisha ya huyu mtoto yanamtegemea mama yake kwa asilimia 100! Sidhani kama kweli atakuwa tayari kurudia kosa na kuacha binti yake alelewe bila yeye. Asanteni sana.” “Hamna shida baba. Nyinyi muwe na usiku mwema. Kesho tutawasiliana na Sonia. Tumalize hayo mambo. Sasahivi imeshakuwa usiku, naona tusimsumbue.”

“Sonia si wakulala sasahivi. Hivi anasubiri nimpe maendeleo ya hapa baada ya maombi. Naweza kumwambia awapigie sasahivi. Akisikia kutoka kwenu, anaweza mtoa Raza.” Nyange akaingilia mazungumza yao. “Sio mpaka asubuhi!” Mzee Ruhinda akauliza kwa kushangaa. “Sonia ataweza wasaidia. Au niseme nilazima atatoa msaada. Huyu mtoto hawezi kulala na kilio hivi.” Polla bado alikuwa akilia.

“Eti Andy?” “Hamna shida baba. Sisi tulishakubali haya mambo yaishe ila tulidhani hatakuwa na uwezo wa kufanya chochote usiku huu.” “Huyo Sonia anafahamika pale polisi kama ni moja ya ofisi yake. Baba yake na bibi pamoja na babu yake waliacha jina zuri sana hapa nchini.” Nyange akaendelea.

“Na bibi yake yupo nyuma yake kwenye kila hatua ya maisha yake. Hakuna sehemu akienda na jina lake hilo la Tambo, milango isifunguliwe. Hana cha usiku wala mchana. Anaweza fanya mambo mpaka akawashangaza. Kichwa kizuri cha sheria kama baba yake.” “Na kweli baba yake alikuwa jaji mzuri sana.” “Basi ndio Sonia. Akili kama baba yake. Mwenyewe jaji Mkuu huwa anasema ni mwanasheria mmoja tu hapa nchini, anaweza mfunga.” “Sonia?” Mzee Ruhinda akauliza na kufanya angalau wacheke.

Nyange kwa asili ni mtundu na maneno mengi. “Anasema ni binti yake tu, ndiye anayemshinda kwa hoja na si mwingine. Kwa hiyo Andy, ni wewe tu.” “Kama nilivyotangulia kusema, sisi hatuna shida.  Akitupigia, tutazungumza naye.” “Basi acha nikazungumze na Sonia.” Nyange akatoka. Andy akaaga. Nakukata.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda Nyange akarudi. “Anawapigia kina Mina. Ila ameniambia niwaambie mjue na yule mganga wake ataachiwa, maana hatakuwa na kesi ya kumshikilia.” Pius akabaki ameinama. “Na akiachiliwa yule, inamaana yupo huru kuendelea kuharibu familia nyingine.” Wote kimya.

“Naomba muombe Sonia amwachie kwa onyo. Kama kumtisha tu, ili Raza arudi kwa watoto wake. Tafadhali Nyange. Najua ni hatari. Lakini kwa kushikiliwa yeye, na kuwekwa ndani itakuwa ameingiwa hofu.” Mzee Ruhinda akatoa ombi. “Au yeye anaweza akamshikilia hata kwa muda kidogo ndipo akamuachia.” Nyange mwenyewe akatoa wazo na kutoka kwenda kuzungumza tena na Sonia.

Alikaa huko nje kwa muda wa kutosha tu. Poliny akaenda kumkumbatia mdogo wake akimbembeleza, yeye mwenyewe akilia taratibu. Akarudi. “Sasa naona kila kitu kimekaa sawa. Nimemwambia Sonia mimi ndio nitaenda kumchukua Raza, familia yake ikiwa kwenye gari ya mumewe ili njiani tukiwa tunakwenda kwake nipate muda naye, tuzungumze kabla hatujafika kwake na kufanya maombi.”

Pius nusu apige goti akishukuru jinsi Nyange alivyojitoa kwao. Ilibidi Poliny aache gari hapo, aongozane na baba yake pamoja na Polla, kituo cha polisi kumtoa mama yao. Bado alikuwa akilia. Nyange aliomba mama yake Raza, awaache kwa usiku huo, wasiongozane. Wote wakaelewa. Akaondoka na dereva aliyemleta, maana mama huyo hakuwa akiendesha usiku. Na wao safari ya kuelekea kituo cha polisi, ikaanza.

~~~~~~~~~~~~~~

Walifika kwenye kituo cha polisi ambako bado Raza alikuwa hapo akisubiria kupambazuke, apelekwe jela. Alishangaa sana kukutana na Nyange. “Mimi naitwa Nyange. Nimeongozana na familia yako.” Raza akabaki na mshangao. “Nitakuchukua kukurudisha nyumbani. Tutakuwa na wewe njiani, ili tunzungumze kabla hujakutana na binti zako.” Akakubali akiwa amepoa sana ila hailewi kinacho endelea.

Wakaondoka. “Nimetoka kuomba na familia yako.” Nyange akaanza. “Unajua madhara ya vitu unavyofunga kwenye begi ya Polla, binti anayekuangalia wewe kama mfano wa kuigwa?” Nyange akaendelea kuzungumza naye taratibu tu. Kimya. “Una binti wazuri sana Raza. Lakini njia unazoendea, unawadhuru binti zako wewe mwenyewe. Kinga au msaada unaotafuta kwa nia nzuri kwa binti zako, matokeo yake ni ya muda tu, na huishia kuwadhuru wao wenyewe, hata wewe. Shetani hana zawadi ya bure Raza, mimi ni shahidi wa haya. Mwisho wake ni fedheha.” Nyange akamsimulia historia yake.

“Dhambi yangu mimi, iliangamiza familia nzima. Mwanya mdogo niliomfungulia shetani, alitumia kudhuru familia yangu. Kwa wakati ule sikuona madhara yake, lakini niliharibu familia vibaya sana. Shemeji niliyekuwa nikiiba naye penzi la kwa siri, alifika umbali mbaya sana. Kwanza kwa mshituko wa kujua wizi niliokuwa nikifanya na mdogo wake, mke wangu alipoteza mtoto niliyekuwa nikimsubiria kwa hamu sana.”

“Haikuishia hapo, yule shemeji alianza kuloga ili kunimiliki sasa, baada ya kuona dada yake amenisamehe na tunaendelea. Ukweli alifanikiwa kunipata, ila kwa garama kubwa sana. Hivi analipa mpaka leo. Ninachotaka kukwambia, ni kwamba, unaweza ukawa na sababu nzuri sana za kueleweka kufanya unachofanya, na shetani akakufanikishia kwa muda, lakini mwisho wake ni kama huu.”

“Binti yako alikuwa amefungwa na nguvu za giza, nisingewahi angeweza hata kufa! Mumeo mwenyewe ulimfunga, alikuwa amefungwa na nguvu za giza. Jiangalie wewe mwenyewe ulipokuwa! Ni fedheha Raza. Umesumbua familia yako bure! Niambie umepata faida gani?” “Wala havina faida ila mateso tu.” Nyange hakutegemea.

“Nimepata muda pale mahabusu, nikawa nikihesabu faida, ni mateso kaka yangu, wala sitakudanganya. Nihivyo sijui chakufanya tena.” “Ulipofika si mbali. Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa mwanae wa pekee Yesu kristo. Kwa kila amuaminie, asipotee bali awe na uzima wa milele. Yesu anaita wote wasumbukao na mizigo, kwa ahadi yakupata pumziko. Ameahidi kusamehe dhambi zetu zote na ahadi ya kutokukumbuka kabisa.” Nyange alizungumza naye taratibu kwa upendo huku akielekea nyumbani kwao.

Mpaka wanafika kwake, yaani Raza mwenyewe ndiye anayetoa mauchawi akimuomba Nyange amsaidie kuyachoma na amuombee. Pius na watoto wake walibaki na hofu wakiangalia vitu anavyokusanya Raza na kuviweka hapo sebuleni. Nyange alikuwa ametulia tu akisubiria amalize.

Alizunguka kwenye hiyo nyumba, kila kona akitoa mauchawi aliyokuwa ameficha. Jumba hilo lilikuwa limewekwa hirizi na nyingine amechimbia nje. Pius alikuwa haamini. Mzee Ruhinda akafika hapo na mkewe wakakuta ndio Raza anakusanya vitu.

“Raza!” Pius akashangaa sana wakati akimwaga vya nje hapo sebuleni. “Nimekosa Pius. Na nakubali kudhalilika mbele ya wanangu na wakwe zangu ili uone nimekusudia kuacha maisha mabaya. Si ningenyamazia tu dawa nyingine?” “Tafadhali muache amalize kutoa kila kitu. Hiki anachokifanya ni muhimu sana kwenye hatua ya kukombolewa. Mwache tu.” Raza akakusanya kila kitu, Nyange akachoma moto ndipo akaanza kumuombea sasa Raza. Ilikuwa shuguli mpaka watoto wake wenyewe walikimbia. Mpaka Polla aliyekuwa akimtaka mama yake alikimbia.

Akabaki Pius na wazazi wake wakitetemeka wakati Nyange akiomba. Hayo majini yalidai hiki na kile ili yaondoke, lakini Nyange aliwakatalia na kuwaamuru yaondoke na kumuacha Raza huru. Mwishoe karibu panapambazuka, ndipo yakatoka na Raza kuwekwa huru. Akawaita wote sasa kama familia. Akazungumza nao sana. Kisha akawaombea baraka na kutoka na Pius kuzungumza naye.

Kwa Pius.

Akamueleza makosa aliyomfanyia mama Briana, mkewe. “Ninapokwambia naishi nikiwa na deni mbele za Mungu na mke wangu, jua ni deni ambalo Mungu akiniita popote akitaka nikatumike kama hivi, nashindwa kukataa. Mungu alinisamehe na kuniponya nikiwa na hali mbaya mno. Mke wangu alinisamehe kabisa pamoja na watoto.”

“Baraka alizokuja kunirejeshea Mungu, ni zaidi ya mwanzo nilizopoteza kwa upumbavu wangu. Najua ni ngumu. Lakini Pius, Raza ni mke wa ndoa takatifu. Hizi ndio zile katika shida na raha zenyewe tulizo apiana. Tafuta jinsi ya kusamehe, ili kuweka hii familia pamoja. Hii nyumba haina madudu tena. Ila haimaanishi hayawezi kurudi! Yakifunguliwa mlango kwa namna yeyote ile, yanarudi.”

“Tena bibilia inasema hali ya mtu yule inakuwa mbaya kuliko mwanzo. Maana yanakwenda kuitana zaidi. Ishi maisha matakatifu wewe na mkeo. Nyumba yenu muigeuze nyumba ya sala. Akazungumza na Pius akionekana kabisa upo ugumu mpaka usoni. “Raza tena!” Akaendelea kujiuliza huku akimsikiliza Nyange. Lakini Nyange alizungumza naye tu akielewa ugumu anaopambana nao moyoni. Mwishoe akaaga na kuondoka.

Maisha Yashachukua Sura Mpya.

Kurudi ndani, akamkuta Polla amelala mapajani kwa mama yake. “Naweza kumuomba mama nikakae kwake kwa muda Pius.” Akaongea kwa kunyenyekea kama anayemsihi amsamehe. “Hivi unajua aliyesaidia kutoka kwako ni huyo mtoto hapo?” “Na kweli Raza! Mwanao huyo amelia, akikutafuta kuanzia muda aliojua unatakiwa kurudi nyumbani mpaka sasa. Amekutafuta kwa kila anayejua anakufahamu, kwa kilio na kutapika usiku kuchwa.” Mama Ruhinda akaongeza na kumfanya alie sana.

“Sasa unapoaga sasahivi ili akiamka aanze kulia tena?!” Pius akamuuliza kwa ukali kidogo. “Kilio chake huyo ndio kimemfanya dada yake ampigie simu auntie yake usiku na kulia kwa machozi akimsihi akusamehe, urudi nyumbani kwa ajili ya mdogo wake na akikiri atazungumza na wewe USIRUDIE tena. Tafadhali tulia Raza, ulee binti zako.”

“Hicho unachohangaikia mbona ni kama umepata! Kwa nini unafundisha watoto njia mbaya? Umejaliwa na Mungu watoto wenye akili nzuri na uwezo mzuri sana darasani na wana vipaji vizuri tu. Kweli unafundisha watoto kuwa hawana uwezo wa kufanya mambo au kufikiria mpaka hirizi!? Kweli Raza binti yangu?” Mzee Ruhinda akamuuliza kwa kuumia.

“Yaani unaondoa ujasiri kwa binti yako, unataka aishi kwa kutegemea vimikoba vilivyotengenezwa na mwanadamu ambaye yeye mwenyewe hana hata nusu ya ulicho nacho!” “Mimi mwenyewe alinitisha eti nikimuacha, nitaharibikiwa! Kwamba sijafika hapa nilipo kwa akili zangu, ila kwa nguvu zake yeye  na huyo mganga wake.” “Haiwezekani!” Mama Ruhinda akashangaa sana. “Si huyo hapo abishe. Tena kwa kunihakikishia eti nikimfunga yeye, nitajuta.”

“Wewe Raza hukumkuta Pius na kazi yake na nyumba hii alishakuwa anakaribia kumaliza? Sijawahi peleka mtoto wangu kwa mganga wala sisi wenyewe hatuamini kwenye hayo mambo, mbona wanangu wote wana maisha mazuri tu? Kwa nini unataka kumdanganya mwenzio?” Mama Ruhinda akawa mkali kabisa.

“Ilikuwa njia ya kumfanya asinifunge mama, nirudi kwa wanangu. Nimekosa jamani, na naahidi kubadilika.” “Aisee acha kabisa Raza. Unamtia majini mwanangu asie na hatia! Unamtesa bila sababu wakati wewe ukiendelea na maisha yako huko nje! Muda mfupi uliopita sisi tulijua tutampoteza kabisa huyu kwa jinsi alivyokuwa akitupwa na madudu uliyokuwa umemuwekea! Anajipigiza kila mahali, kwa sababu ya ubinafsi wako tu! Unataka mpaka kuua mtoto wa mwenzio!” “Tena kwa kutekeleza mauuaji kwa kiumbe kisicho hatia! Kweli Raza?!” Mzee Ruhinda akaongeza kwa mkewe.

“Huyo Pius kama mpaka leo angekuwa akisubiria kurithi kutoka kwangu hata wewe mwenyewe usingekuwa na maisha uliyo nayo! Sikuwajenga vijana wangu wakue wakisubiria kurithi mali zangu, ila kujitegemea. Si huyo Pius na wenzie wamehangaika wenyewe kwa akili zao mpaka wamefanikiwa tena kunipita hata mimi baba yao! Kwa nini wewe unahangaika kufikiria kurithisha binti zako mali za baba yao ambaye yupo hai, badala ya kuwafundisha kupambana wawe mbali kumzidi baba yao? Unalinda mali hizi chake tu wakati binti zako wana akili nzuri sana! Wafundishe, waamini kwamba wanaweza fanya makubwa kuliko wewe na baba yao ili wasikae wakisubiria mali za baba yao!”

“Acha fikra potovu Raza. Acha fikra za mauuji kwa kulinda mali ambazo hata hujui Pius mwenyewe atakufa lini au hata akifa kama bado atakuwa nazo!” “Au na yeye ulipanga kumuua?” Mama Ruhinda akamuuliza akiwa wazi anaonyesha hasira. “Hapana wazazi wangu. Nampenda Pius. Nimefanya…” “Acha uongo. Utaniudhi zaidi Raza. Kama kweli ungekuwa ukinipenda ungenifanyia yote haya?! Unanilaza kwenye majini na kunifanya niwe dhaifu? Unaniulia kijana wangu kwa sababu zako binafsi tu! Unamahusiano ya kudumu huko nje na unarudi kwangu ukiniangalia vile ninavyohangaika bila hata huruma! Tafadhali kama umekusudia kubadilika, na uongo uache.” “Nisamehe Pius. Nabadilika.” Raza alizidi kulia.

“Na usisahau kupiga simu kwa Mina, umuombe radhi kwa kumaanisha. Umenisikia Raza?” “Nimesikia baba.” “Muombe radhi. Muahidi kwa kumthibitishia kwamba hutarudia tena. Kisha umshukuru yeye na mume wake. Walishapanga kufuta kesi hata kabla ya mwanao kukuombea msamaha. Kisha pata muda wa kuzungumza na binti zako. Futa kabisa hayo mafundisho machafu uliyopanda kichwani mwao. Zaidi kwa Polla. Umeharibu kichwa cha binti yako, hajiamini yeye kama yeye mpaka wewe, na hizo hirizi zako.” “Nitafanya hivyo baba yangu.”

“Aisee hapana Raza. Hakika badilika. Na isiwahi jirudia tena akilini mwako kumtesa tena Pius na wajukuu zangu. Iwe MWISHO. Sitakubali na jua nitakuwa makini sana na wewe. Umesikia Raza?” “Ndio mama. Nakuahidi ninaacha. Sitarudia tena hayo maisha.” Raza alikuwa anakaribia kupiga magoti akiwa bado na mwanae.

“Msaidie huyo akalale. Tutawaambia shule huo mtihani atafanya kesho. Leo hawezi kwenda shule. Amelia sana na kujipigiza. Inabidi kumuangalia.” “Nashukuru.” Raza hakuamini kama ameruhusiwa kubaki pale.

~~~~~~~~~~~~~~

Akachukua binti zake akilia. Akamsaidia Polla mpaka juu chumbani. Akamwambia wakati akioga, na yeye anakwenda kuoga kisha kurudi kukaa naye mpaka alale. Akakubali. Raza akaenda kuoga chumbani kwao akiwa amemuacha mumewe na wazazi wake hapo sebuleni.

“Unajisikiaje?” “Vizuri mama. Najisikia mwepesi kweli!” Hizo zikawa habari zilizomtuliza mama Ruhinda. “Nawashukuru baba na mama. Niliwahitaji leo.” “Kapumzike Pius. Tutazungumza baadaye mkiamka.” Wakaondoka.

Pius akabaki ametulia hapo sebuleni hataki kurudi kulala kwenye kitanda chao. Kumbukumbu ya vitu walivyochoma na vile yale mapepo yalivyokuwa yakipiga kelele kwa kila mmoja aliyeshuhudia yakimtoka, na yeye kuambiwa hali yake ilikuwa hivyohivyo, japokuwa aliambiwa aliombewa na yametoka hata hapo nyumbani kwake, lakini bado alikuwa na hofu.

Hapohapo akamtumia ujumbe mmoja wa wafanyakazi wake anayemtuma mara kwa mara na ni mwepesi, anayajua maisha yao. Akamuagiza maduka yakifunguliwa, aletewe godoro jipya, ukubwa kama lililopo hapo chumbani kwake, mashuka na mito mipya.

~~~~~~~~~~~~~~

Raza akatoka kuoga, akaenda kulala chumbani kwa Polla. Na Poliny naye akawafuata. Wakalala watatu hapo kitandani. Raza amelala chali binti zake wamemlalia kila mmoja ubavuni akawakumbatia. Pius yeye akapitiwa na usingizi kwenye kochi vilevile na nguo zake na viatu mpaka msichana wa kazi alipozidisha shuguli jikoni asubuhi hiyo ndipo akaamka.

Hakumkuta Raza chumbani, akaenda kumuangalia chumbani kwa Polla, akawakuta wote wamelala na mama yao. Akaangalia kwa muda, akafunga mlango taratibu akarudi chumbani kwao.

Akaingia kuoga na kutoka. Raza alikuwa ametoa matandiko yote kitandani. Akamuita kijana wao wa kazi hapo ndani. Akamwambia atoe matandiko yote kabatini na hayo aliyotoa Raza, mito na godoro. “Weka jalalani na choma moto.” Akahisi hajamsikia bosi wake vizuri.

“Si kuna mafuta ya taa stoo?” “Ndiyo.” “Mwagia. Hakikisha vinateketea isibakie hata kitambaa kinachozagaa.” Kijana akaelewa. Kazi ya kutoa hapo ikaanza. Aliporidhika hakuna kilichobakia hata foronya, kimebaki kitanda tu, akatulia akiangalia kile kitanda. Kilikuwa kizuri sana cha ngozi. Thamani ya juu mno, tena alinunua huyohuyo Raza.

Akaona haitoshi. Akamuita tena atoe na hicho kitanda. “Na hiki choma moto.” “Nakiomba mimi bosi wangu.” “Unanisikia?” “Sawa.” “Tena kaongeze mafuta ya taa, choma mpaka kiteketee kabisa.” Kazi ya kukitoa ikaanza tena safari hii akimsaidia mpaka jalalani na kuanza kukibomoa akitupa vipande jalalani. Kisha akamuacha akimwagia mafuta ya taa. Ndipo akaridhika na kurudi sasa chumbani kwake.

Akajitupa kwenye kochi la hapohapo chumbani. Alilala Pius, alikuja kuamka mchana wa saa saba, hata kazini hakwenda. Ila alishatuma ujumbe kwa wenzie kuwataarifu anadharula ya kifamilia, siku hiyo hatafika ofisini. Pius mwadilifu wa kazi. Hakosi kazini hovyo, wakamuelewa.

~~~~~~~~~~~~~~

Raza ndiye aliyemtoa usingizini wakati akiingia. “Sikukusudia kukuamsha.” Akamtizama akigeuka. “Vipi Polla?” “Anaendelea vizuri. Nilikuwa namsaidia kusoma kwa mtihani kesho. Ila nataka kwenda naye kumtafutia nguo za kuogelea. Wanamashindano jumamosi.” “Wakati unamuandaa na mitihani ya shule, hakikisha unamtoa ujinga uliomuingizia kwamba hawezi fanya kitu bila madudu yak…” Akajirudi.

“Mfundishe kuwa anao uwezo wa kufanya vizuri bila manjia ya ajabuajabu kama babu yake alivyokwambia jana.” “Nimeshazungumza nao. Na nimewaleza njia nilizokuwa nikitumia si sahihi kwanza wala hazikuwa na uwezo wa kuwasaidia. Ni imani mbaya tu.” Hakumjibu.

“Poliny amesema nikuage. Amerudi chuo. Anamtihani jioni.” Hapo akatoka kochini alipokuwa amelala na kuanza kusaka simu yake. Akaipata ili ampigie simu binti yake. “Sitarudia tena Pius. Na hata mambo mabaya ya nje naachana nayo kabisa. Hutamsikia tena Chezo, wala mtu mwingine. Siweki tena namba ya siri kwenye simu yangu. Muda na wakati wowote chukua angalia. Utathibitisha nimebadilika.” “Kwani mwanzoni ulikuwa ukiacha jumbe zako na Chezo? Si ulikuwa unaweka dissapiring, wewe? Hivi unajua ni pesa kiasi gani nimetumia kufufu hizo jumbe?”

“Nimekosa Pius. Sitarudia tena.” “Unasema hivyo kwa sababu umekamatwa, lakini si kwa sababu umekusudia kuacha umalaya wako. Acha kunifanya mimi mjinga. Hata jana mlikuwa na miahadi ya kukutana! Inamaana mida ile kama nisingekuita mimi, ungekuwa naye hotelini, mkifanya yenu, halafu mimi huku unanifanya hanisi, joka la kibisa. Mkatili usiye hata na chembe ya huruma.” Akazidi kuwaka kwa uchungu.

“Ulikuwa na mimi humu ndani ukinisanifu tu usiku, halafu wewe unaenda kukatwa kiu zako huko, mchana kutwa. Halafu sasahivi unasema nini?!” Hasira zilikuwa zimempanda Pius, anamtizama kwa jicho baya, Raza kimya akishindwa hata kumtizama mumewe.

 Akamtizama kwa sekunde kadhaa na kurudisha macho kwenye simu. Akampigia binti yake na kutoka hapo chumbani kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~

 “Ulipata muda wa kupumzika kweli wewe?” Akamsikia akimuuliza binti yake. “Inatosha dad. Nataka nijisomee tena kidogo kabla ya mtihani.” “Umekula sasa?” “Nitakuwa sawa, usiwe na wasiwasi.” “Kula lazima. Kula ndio usome.” Akamsikia ametulia kabisa wakatia akizungumza na binti yake. Alimjua jinsi anavyompenda Poliny. Akaenda kwa Polla.

~~~~~~~~~~~~~~

Akamkuta ametulia chumbani kwake, anasoma. “Vipi kichwa?” “Mama amenipa dawa. Njoo ukae hapa na mimi.” Pius akacheka na kwenda kukaa pembeni yake, kitandani. “Niambie unasoma nini.” “Ila sio uanze kunifundisha au kuniuliza maswali. Wewe na Poliny wakali.” Pius akaanza kucheka tena.

“Kwanza mama ashanisaidia.” “Polla kwa wasiwasi!” “Wewe hapo hukawii kuanza kunigombesha. Unataka niwe kama Poliny, kuelewa kwa harakaharaka.” “Kwa kuwa akili zako muda wote zipo kwenye game zako hizo ndio maana nataka urudishe akili kwenye masomo.” “Mbona mama yeye ananichukulia taratibu mpaka naelewa?” “Basi namuachia mama yako. Ila wakati anaenda kukununulia nguo za kuogelea na mimi nakuja, ili nipaone.” Alifurahi huyo Polla. Akaanza stori kwa baba yake akimtajia rangi anazotaka. Wakabaki hapo wakizungumza akafurahia akiona ametulia. Yeye shida yake mama yake awepo.

~~~~~~~~~~~~~

Je, Maisha Ya Pius&Raza Yatakuaje Baada Ya Wanandoa Hawa Kufikishana Umbali Huo Wa Kuumizana Na Majanga Waliyofanyiana Wote Wawili Huku Wakiwa Na Watoto Wanao Wategemea Na Kuwaangalia Kwa Karibu, LAKINI WOTE WAMESHAOMBEWA NAKUTOLEWA MAPEPO?

LAKINI Bado Mioyo yao imebeba kumbukumbu mbaya na majeraha bado ni mabichi kabisa, japo AHADI YA MUNGU IMESIMAMA PALEPALE. Waebrania 8:12, Yer 31:34b{Mungu amesamehe kwa ahadi ya kutokukumbuka dhambi zao daima.}

Ni Nini Kitaendelea Kwa Love At First Time?

Mina&Andy! {Wakiwa na mtoto wa Pius?}

Mill&Pam! {Kwenye Mwanzo Mpya wa Maisha, Mill akiwa na familia mpya yenye Kamila ambaye Pam bado hajamalizana naye? Na Familia waliyoachiwa wawili hao na marehemu Mzee Mgini? Maisha Marekani au Tanzania? Safari hii watafanikiwa Ndoa Takatifu?}

Inaendelea….


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment