Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 58. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 58.

Sonia alimfikisha Raza na Katibu polisi. Akawashitaki ramsi. Wakawekwa ndani ndipo akatoka sasa kumpigia simu Mina. “Unanafasi tuzungumze?” “Nalisha timu yangu hapa. Nimeloa uji mwili mzima, Ayvin anakazi ya kutema tu hamezi, na kilio juu!” Sonia akacheka. “Mpaka nahisi tutarudishana kwenye kunyonya tu. Sioni dalili hapa.” “Basi atanyonya huyo mpaka kwa mkewe.” Mina alicheka sana.

“Unafikiri nakutania! Wewe muendekeze tu. Na ujue anakusoma na kukupima. Anataka kujua utaishia wapi. Ukimrudisha tu kwenye nyonyo, jua mchezo ni huohuo.” “Acha kunitisha bwana!” “Utakuja niambia. Watoto wanaakili kutuzidi sisi. Atatema hapo na kulia, utamuhurumia, kumbe mwenzio anakupima tu. Ukiyumba tu, basi ujue amekuweza. Wewe nenda naye taratibu bila ya kukata tamaa. Kidogo kidogo mpaka ajue hiyo nayo ni njia anayotakiwa kuishi kuanzia sasa. Usiache. Endelea hapohapo. Maana itakuja na kumuachisha diaper.”

“Mchezo utakuwa huohuo. Hataki poti anataka diaper tu. Sasa shule ataendaje na diaper?” “Na kweli! Acha nipambane naye hivyohivyo. Kwema?” “Wewe maliza kulisha wanao, tuzungumze kwa utulivu. Kwako kuna fujo bwana.” Mina akacheka. “Na usifikiri fujo hii ni ya wengi. Mtoto mmoja tu kama jeshi!” Sonia hana mbavu. “Nitakupigia dada yangu acha mimi nipambane naye.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya kama masaa mawili, akampigia. “Nipo na Andy. Nimekuweka kwenye spika.” Mina akamuwahi. “Au hutaki?” “Ni wewe tu. Kama umeridhia ni sawa. Ila nina ujumbe kutoka kwa Pius.” Mina akamuangalia mumewe.

“Ni ujumbe gani?” Andy akauliza. “Kwanza yeye ndiye aliyenifuata. Amekuja ofisini kwangu na ushahidi, kile anachokifanya Raza kwake, wewe Mina na mtoto. Akaniomba yeye ndio achukue hatua, sio kumtisha Raza, maana nikwambie tu ukweli Mina, Raza amefika mbali.” “Unamaanisha nini?” Ndipo sasa Sonia akamueleza Mina kuanzia mwanzo mpaka mwisho.

Andy alishituka sana ila si Mina. “Mimi siogopi dada. Hata aende kwa shetani mwenyewe, hakuna wakugusa wanangu. Nina uhakika na Yesu ninaye muomba. Hajawahi kuniangusha. Mimi uchawi wake siogopi kabisa.” Mina akazungumza kwa kujiamini.

“Nimefurahi kukusikia hivyo Mina, lakini yeye Pius ameingiwa hofu SANA. Kupita nitakavyokueleza. Ameomba nikwambie kwa sasa hata yeye hajiamini na Ayvin. Anagopa majitu aliyotupiwa yasije mdhuru mtoto wake. Amenituma nikwambie, anampenda sana mtoto wake, lakini hataonekana huko kwa muda mpaka aombewe na kuwekwa huru.” “Hapo atakuwa amefanya jambo la maana. Bila Mungu, ajue atatwanga maji kwenye kinu.” Andy kimya kwenye mshituko.

“Hata mimi kwa hilo nampongeza. Ila kwa hakika ameingiwa hofu na anajutia sana. Anajiuliza bila jibu, hajui amepatwa na nini kiasi cha kufanya aliyokuwa akiyafanya kama mwehu. Ameomba yeye ndio ashugulike na Raza. Yeye ndio amshitaki, wewe ukae pembeni. Ila ametoa ombi kwako.” “Ombi gani?”

“Huko kwa mganga inavyoonekana walikushindwa. Sasa anaomba hicho ulicho nacho umuombee na mwanae akipate ili wasije mdhuru.” “Dada, nakuhakikishia. Na hata yeye mwambie atakayeua hawa wanangu ni Mungu aliyewaumba wala si vinginevyo. Kama isingekuwa hivyo pengine huyo Raza angemuua mwanangu tokea yupo tumboni. Hawana uwezo wa kuua wanangu. Mwambie yeye ahangaike na huko kwake. Ila Ayvin anaulinzi wa kimungu. Hakuna silaha itainuka kinyume naye ikafanikiwa.” “Mina!” Sonia akashangazwa na imani yake.

“Hakika dada. Mimi namjua Mungu wa mama yangu. Ni hivyo tu ujana ulikuwa mwingi. Namjua kwa kumuona kwa mama. Na nikwambie wazi kabisa, nilipopata habari za Raza tu, za ushirikina, tokea nina Ayan, au alipojua nimezaa mtoto wa kiume wa kwanza mjuu kwa kina Ruhinda, nikaambiwa nijiandae na Raza, haraka sana nilijua Yesu ndio atakuwa msaada wangu. Ni ubinadamu tu, kwenye kuyumba. Lakini najua kwa hakika tumaini langu lisiloyumba na haliongopi ni YESU.”

“Mimi mwenyewe nilikuwa na madudu hayohayo, mama yangu alihangaika na mimi mpaka nikapona na kuwekwa huru. Najua nguvu ya msalaba. Najua ulinzi wa Kimungu. Kwa hiyo mwambie Pius, kwa hawa watoto wangu, aondoe wasiwasi. Ayvin ataishi na atayashuhudia makuu ya Mungu.” “Amina.” Sonia akaitika akicheka.

“Na swala lake la kutokuja umeelewa?” “Nimeelewa dada. Hamna shida. Yeye atakapokuwa tayari, mwambie siku zake ni zilezile na masharti ni yaleyale.” “Sawa. Kwa hiyo kuanzia leo, jua na yeye ni mteja wangu, nitafanya naye kazi mpaka mwisho.” “Sawa. Na ninakushukuru dada yangu. Wewe kweli ni wakuaminiwa.” Sonia akacheka na kuwaaga.

Historia Ya Raza.

Raza alizaliwa kwenye familia iliyokuwa imeshika dini sana. Yeye alikuwa mtoto wa nne kati ya familia ya watoto watano. Ilikuwa ni familia ya swala zote bila kuzembea tokea anaakili zake. Amekuzwa kwenye maadili ya dini. Watoto wakike walikuwa wawili tu. Ila yeye tokea mdogo hata baba yake alishamuona alikuwa mtoto mdadisi na mtaka zaidi.

Ndugu zake wote hawakusoma kama Raza. Tena si kwa wazazi kukosa uwezo, ni wenyewe hawakupenda kuendelea na shule. Kaka zake walioa mapema tu, wakajitupia kwenye biashara za baba yao hapo jijini. Maana mzee wao alifanikiwa sana kibiashara. Alikuwa na maduka matatu. Jumla na rejareja. Kariakoo na Msimbazi karibu na kwao. Kwa hiyo walipomaliza tu shule zile za awali, kidato cha nne ambaye ni kaka mkubwa, wadogo zake hata hawakumaliza kidato cha nne, wote wakajiunga na baba yao na wakawa wakifanya tu vizuri.

 Mdogo wake Raza ambaye anamfuata, wakike, na yeye alishika dini si kama Raza. Alipomaliza tu kidato cha nne, aliolewa na kuanzisha familia, akatulia kwenye ndoa yake. Ukiwatizama ndugu wa Raza na Raza mwenyewe, usingesema wanatoka nyumba moja na kulelewa na wazazi aina moja.

Usingemkuta Raza na hijabu nje na nyumbani kwao tokea zamani hata kabla hajabadili dini. Alificha kwenye mkoba na kuivaa akiwa anakaribia nyumbani kwao. Alifaulu shule nzuri, hakutaka kwenda kusoma shule za dini. Na baba yake alikuwa akimuunga mkono kwenye kila hatua ya elimu anayofikia. Na ndugu zake wengine walisema baba yao alikuwa mkali sana ila linapofika swala la Raza, analegeza kamba kabisa. Akawa kama mtoto wa baba haswa.

 Kwa asili Raza likuwa mpambanaji kwenye maisha kupita ndugu zake wote. Kitu kilichomtofautisha na wenzie. Wakati wote alitaka zaidi na kitu cha tofauti na anachojua wenzie wamefikia. Ilimsaidia kufanya vizuri kwenye kila kitu kwa sababu alijifunza kupambana.

Mambo yaliharibika siku alipokwenda kusema nyumbani kwao kuwa anaolewa na Pius Ruhinda, ndoa ya kanisani! Hakuna ndugu hata mmoja aliyetaka kumsikia tena. Hata mama yake mzazi hakufika kwenye harusi yake, na baba yake alimfukuza kabisa nyumbani kwao. Raza hakujali. Akabadili dini na kuolewa na Pius.

Hata baba yake alipofariki, kaka zake hawakumpokea tena. Mdogo wake alikuwa mtulivu mno. Mtu wa familia. Yeye aliolewa na mtu ambaye mshika dini kama kaka zake au baba yake. Naye ametulia kama yeye. Wakajaliwa watoto wao, kimya. Akabaki akijiangalizia maisha ya dada yake na kumuacha tu. Raza ni mtu ambaye akiamua jambo lake ni ngumu kumbadilisha.

Mama yake alikuja kurudi pichani miaka ya baadaye sana, hata Polla alikuwa ameshazaliwa. Ndio yakawa mahusiano napo si ya karibu sana, kwa sababu ya misimamo ya Raza. Mama yake akawa mtu wa kumwangalia tu na kunyamaza. Kwa hiyo Raza ndio akabakiwa na familia hiyo ya Ruhinda tu, na wanae. Na ndugu zake upande wa mama kidogo tena walimsogelea kwa kumuomba pesa wala si mahusiano ya undugu. Raza msomi, anakazi nzuri na mume asiyeuliza mshahara. Kwa hiyo alikuwa na pesa wakati wote.

~~~~~~~~~~~~~~

Polla hakurudi kusoma kama alivyomwambia baba yake. Akampigia tena simu mama yake, akamkosa na kuamua kumpigia simu bibi yake, yaani mama yake Raza, kumuulizia kama amemsikia mama yake.

“Mama yako sijamsikia leo, pengine ametingwa.” “Ametingwa na nini?” Polla akamfanya bibi yake atulie na kufiria maana alikuwa akimjibu tu. “We kwani mara ya mwisho kuzungumza naye ilikuwa saa ngapi?” “Asubuhi wakati naenda shule. Na aliniahidi leo atawahi kuja kusisaidia kujiandaa na mtihani asubuhi halafu nina mashindano kesho kutwa.”

“Na mimi aliniambia kama naweza nije. Ila jumamosi nina shuguli. Kuna mjukuu wa shoga yangu anachezwa, na nimeshalipia. Sare pia ninayo tayari. Nimemwambia hivyo naona akanikasirikia, sijamsikia tena.” “Labda kwa sababu kila siku unatoa sababu, bibi.” “Wala si sababu. Yeye ananiambia mambo yake kwa kunishitukiza wakati na mimi ninakuwa nishaweka mipango, nimeahidi watu. Siwezi kuwa kigeugeu.” Polla akanyamaza.

“Kwani baba yako amesemaje?” “Ameniambia amesafiri wakati mama hasafiri.” “Mama yako si mtu wa safari.” “Umeona bibi! Mimi ninazidi kuingiwa na wasiwasi. Nampigia auntie kumuulizia.” Huyo mtoto akakata simu kwa bibi yake akaendelea KUMSAKA mama yake. Uzazi mzuri.

~~~~~~~~~~~~~~

Aliwaza mpaka akashindwa ikabidi kuwapigia tena simu wazazi wake. Aliwaeleza kila kitu bila kificho, kwa hakika waliingiwa na hofu. “Utafanyaje Pius?” “Ili asije dhuru mtu mwingine, wao wawili hivi tunavyozungumza wameshapelekwa polisi. Lakini sijui nifanyaje na Polla! Hivi ndio nimegundua maisha ya yule mtoto ni mama yake kwenye kila kitu. Hapa tunapozungumza hajalala, na amekataa kuja hapo, anamsubiria mama yake. Anamtihani kesho asubuhi, na ana mashindano jumamosi.” “Na kweli Raza alituambia. Hivi tuliahidi kuhudhuria. Si unamjua Raza na hayo mashindano!” Mzee Ruhinda akazungumza kama aliye mawazoni.

“Subiri kwanza Pius. Swala la Ayvin ambalo wamesha tuma hayo majeshi?” Bibi mtu akauliza kwa wasiwasi. “Hata sijui mama! Nimevurugikiwa! Sonia, yule mwanasheria wa Mina ndiye na mimi namtumia. Nimeomba awasiliane na Mina, kwanza ajue hali ya mtoto, na pili amwambie Mina ukweli kwa kile kilichotokea ili Mina amuombee mtoto bila ya kuzembea. Inavyosemekana Mina anayo nguvu ya kimungu ambayo eti hata walivyokuwa wakimuita huku kwa mganga wake wanashindwa. Sasa mimi sijui hayo mambo mama. Ila kama wao wamemshindwa Mina, basi pengine anacho kitu cha tofauti.”

“Nataka hicho alichonacho Mina, kimsaidie na mwanangu mama. Nimeingiwa hofu kupita kiasi.” Wazazi wakabaki hawajui chakusema kwa hofu. “Ila kwa hakika mimi na wanangu tunatakiwa kufanyiwa kitu ili kutoa yote ambayo Raza ametuwekea.” “Kwa njia gani? Na wewe uende kwa mganga!?” “Huyo dada amenieleza kisa kinachofanana na hiki changu. Ila anasema wao hao waligeuzwa mpaka vichaa kabisa na wakasahauliana. Wakaja kuombewa. Sasa anasema atanipeleka kwao wakaniombee na mimi. Amenionya nisiende kwa mganga.” Wazazi hao wa RC damu, wakabaki kimya, ila hofu.

“Nakuja mama.” “Sasa unakimbia kwako?” Baba yake akamuwahi kabla hajakata simu. “Nataka kutoa kila kitu kwenye ile nyumba mpaka wafanyakazi wake Raza nawafukuza. Kusafishwe kabisa. Sitaki hata kijiko alichonunua Raza. Naanza upya.” Wazazi kimya.

“Maana kwa vitu tu vilivyotoka kwenye pochi yake, najiuliza ni vingapi vimeachwa huko nyumbani? Naogopa hata wazo la kufikiria kurudi pale.” “Pole sana Pius. Pole sana. Acha mimi nitoke nikamnunulie vitu Polla. Utanikuta ukija.”

Poliny Kwa Baba Yake.

Mara simu ya Poliny  ikawa inaingia. “Poliny  ananipigia. Acha nimpokee nimwambie na yeye aje ili nizungumze nao wote kwa pamoja.” Pius akawaaga wazazi wake na kupokea simu ya binti yake. “Mama yuko wapi? Maana Polla amenipigia simu analia mpaka ametapika baba. Anasema hampati mama kwa simu na kila anayempigia simu, anamjibu hajamsikia mama leo. Analia sana. Hivi nimemwambia dada amsaidie kuoga. Amejichafua, na bado analia. Wewe umezungumza na mama leo?” Mara simu ya mama yake Raza nayo ikawa inaingia kwenye simu yake. Ya Paul nayo ikawa inaingia, kisha Paulina. Akajua huyo mtoto alipigia kila mtu anayemjua mama yake.

“Inabidi kuzungumza Poliny. Nenda kamchukue Polla, uje naye kwa bibi, nitawaambia kila kitu. Lakini mama yenu yupo mzima kabisa.” “Wapi?” Kimya. “Dad? mama yuko wapi?” “Sio kwamba nimekwambia ukamchukue Polla nyumbani uje kwa bibi yako nitazungumza na nyinyi?” Akamuuliza kwa ukali kidogo. Poliny  alimjua baba yake. Yeye akakubali na kukata simu.

~~~~~~~~~~~~~~

Bado alikuwa mbali na nyumbani kwa wazazi wake. Akaendelea kukanyaga mafuta bila ya kujibu simu yeyote ila ikitaka azungumze na binti zake kwanza kabla ya maneno kuzagaa na kuwafikia.

Ilipoingia simu ya Sonia, akapokea. “Nimezungumza na Nyange, amekubali kuja usiku huu. Ni mtu mzuri sana. Anaelewa mnakopita. Jambo kama hilo huwa halazii damu. Amekubali. Nimempa namba yako, nikikata tu, atakupigia.” “Nakushukuru sana Sonia.” Alipokata tu, Nyange naye akampigia. Akamueleza kwa kifupi, Nyange akamwambia anatoka kwake kwenda kukutana nao huko nyumbani kwa wazazi wake. Akamshukuru na kuendelea kukanyaga mafuta kuwahi.

Usiku Wa Hekaheka.

Ikawa kama ameingia tu na binti zake. Anafika sebuleni na wenyewe ndio wanaingia hapo, Poliny anamsalimia babu yake, Polla ametulia kama aliyekuwa akilia. “Mama bado hajarudi?” Pius akamuuliza baba yake. “Nafikiri atakuwa anakaribia.” Pius akakaa. “Njoo Polla mtoto mzuri.” Akamsogelea baba yake. “Usilie mtoto mzuri.” Akamsaidia kufuta machozi. “Nilikwambia uache kila kitu nyumbani, mbona una huo mkoba tena?” “Begi langu la shule, lina madaftari yangu.” “Nitakununulia jingine. Hilo toa vitu ulitupe.” Polla akashangaa sana.

“Amenipa mama!” “Ndio nakwambia tutanunua jingine.” “Mimi nataka hilihili dad! Kwa nini ubadilishe? Kwanza lina ulinzi wangu.” Pius akawa hajaelewa. “Ulinzi gani?” “Ameniwekea mama.” Hapo akashituka akikumbuka madudu yaliyotoka kwenye pochi ya Raza.

“Ulinzi wa nini?” Mzee Ruhinda akashituka. “Sijui lakini mama ameniambia nikiwa na hili begi, na ulinzi wake, hakuna baya litanipata. Nitakuwa naelewa sana darasani na hata kwenye mazoezi nitakuwa nafanya vizuri. Nitakuwa nawashinda wote.” “Sio kweli Polla.” “Ni kweli. Na ndio maana nafanya vizuri. Mama yuko wapi?” Akalibeba begi lake vizuri na kusogea mbali kidogo na baba yake, Pius naye akamwangalia baba yake na Poliny aliyekuwa akijaribu kumpigia tena simu mama yake akiwa amesimama mbali kidogo na hapo.

“Ushawahi ona huo ulinzi wenyewe?” Babu yake akamuuliza. “Amenifungia kwenye zipu ya ndani, ile ndogo. Hamna haja ya kuitoa kila wakati. Naficha hata rafiki zangu hawaoni.” Akazungumza akiweka sawa hilo begi lake la shule huku akifuta machozi. “Umempata mama, Poliny?” “Sasa hivi hata simu yake haiiti.” Polla akaanza kulia tena. Poliny akarudi kupiga tena.

 “Naomba hilo begi.” Akasita kumpa baba yake. “Kwani alikwambia hata mimi nisishike?” “Mama aliniambia nisimuonyeshe mtu, lasivyo itakuwa haifanyi kazi.” “Sio kweli Polla.” “Ni kweli. Mbona nilikuwa sifikishi ule muda niliokuwa nikitakiwa kumaliza kila siku mazoezini. Kila siku nilikuwa nikijitahidi sifikii muda, nachelewa nakuwa namaliza kuogelea muda sio ule niliotaka. Ndio mama akaniambia atanisaidia. Akanisaidia, kuanzia wakati huo nikawa nakuwa wakwanza na hakuna mtu anaufikia muda wangu. Naogelea kwa haraka na muda mfupi kwa round zote.” Pius akaumia sana.

“Basi nipe nione.” Akakataa kabisa mpaka akahama kochi. “Ni nini tena? Mbona analia tena?” Poliny akasogea pale. Kabla hawajamjibu dada yake, bibi yao naye akaingia. Katika vitu alivyomnunulia ni pamoja na begi la shule.

“Haya, umeletewa begi jipya, hamishia hapa madaftari yako.” “Nalitunza mpaka mama anibadilishie. Mama yuko wapi?” “Mimi naweza kukuhamishia.” Akamkatalia baba yake kabisa.

Hasira zikampanda Pius, akampokonya kwa nguvu. Mtoto alilia huyo mpaka akatapika tena. Anataka begi lake. Pius akalichukua kama lilivyo akaenda tupa nje kabisa jalalani. Poliny akashangaa sana akiumia. “Kwa nini unafanya hivyo dad, na yeye amekwambia ni begi alilopewa na mama!?” “Hilo begi limebeba madudu matupu.” “Kuna madaftari yangu pia. Nataka begi langu.” Polla akazidi kulia kwa sauti na hasira ya ajabu.

“Mimi naenda kumchukulia ili atulie mpaka mama atakapokuja.” “Usithubutu Poliny. Nakuonya.” Hasira kwa mkewe na habari za hofu alizokuwa amebeba Pius, ilikuwa kama makaa ya moto ndani ya kifuu cha nazi. Alikuwa akilipuka na kushindwa kujizuia kwa binti wasio hatia. Yeye amewaka, Polla analia kwa uchungu. Anamuita mama yake. Poliny akabaki akimtizama baba yake kwa kuumia. Kisha akamsogelea mdogo wake akitaka kumtuliza, gafla akajirusha sakafuni.

Anatapatapa akigaragara. Nyumba ilikuwa ndogo. Mtoto anatambaa sakafuni kama joka. Ametoa macho kama anakata roho. Kina Ruhinda ni wakristo wasio na ugomvi na Mungu wala shetani. Mambo ya kiroho kwa undani hawayajui.

Nyumba ikataharuki hawajui chakufanya, ikabidi ampigie simu Nyange. “Kuna nini mbona kelele?” “Tafadhali tusaidie.” Hapo Pius anakimbilia jalalani kuokota begi amrudishie.

Poliny analia haswa kila anavyomuona mdogo wake vile. Mzee Ruhinda alishampigia simu Paul daktari wa familia, afike hapo kwa haraka kusaidia. Nyumba ikachangamka kwelikweli! Msichana wa kazi alishakimbia kujifungia chumbani kwake. Pius akawa anampa begi lakini ni kama Polla hana ufahamu tena.

~~~~~~~~~~~~~~

 Hawakuwa na chakufanya mpaka Paul mwenyewe alifika hapo akawa anaogopa kumshika! Wakabaki wote wanamkwepa maana anahangaika sakafuni, Pius kilio huku akisaidia kusogeza meza na viti ili binti yake asijiumize zaidi. Mara Paulina naye na mumewe wakafika hapo kwa haraka.

Hawajakaa sawa, mama yake Raza naye akawasili hapo na dereva akiwa na wasiwasi. Maana Raza hampati kwenye simu, na alipokwenda nyumbani kwao mlinzi alimkatalia kuingia ndani akisema nyumba imefungwa, haruhusiwi mtu kuingi na hakuna mtu ndani. Ndipo mama yake Raza akaamua kuwafuata kina mzee Ruhinda kuuliza kulikoni maana na Pius naye hakuwa akipokea simu zake! Ndio akakutana na hiyo hali ya mjukuu wake akijirusha sakafuni.

Ukweli aliogopesha. Hakuna aliyeweza msaidia huyo mtoto mpaka Nyange alipoingia hapo. Aliikuta ile hali pale mpaka akawahurumia.

Akamsogelea Polla. Akakemea kwa dakika chache tu, mara Polla akatulia kimya sakafuni na kuacha kugaragara akijipigiza sakafuni. Wote wakatulia wakimwangalia alipolala pale sakafuni. “Ndio amepona?” “Bado.” Nyange akajibu akimtizama. “Labda tumpe begi lake.” Nyange akawa hajaelewa. Ndipo Pius akamsimulia chanzo cha hilo begi na mkasa wa pochi ya mama yake huyo Polla.

“Anasema ni ulinzi wake.” “Ndio mambo nilikuwa nikigombana na mama hayo. Anataka kunipa mavitu ya ajabu, eti yanisaidie chuo, nikamwambia mimi nina akili zangu. Nitajitegemea. Nikishindwa nitaongeza juhudi kwenye kusoma lakini si mavitu ya ajabu.” Poliny akaongeza akilia sana.

Nyange akaomba apewe yeye hilo begi. Akalifungua na kumwaga vitu vyote chini, hakukuta kitu zaidi ya vitu vyake vya shule. “Amesema vipo zipu ya ndani mama yake anamfungia huko.” Mzee Ruhinda akasaidia. Ndipo Nyange akafungua zipu ya ndani. Akakuta kama hirizi imefungwa vizuri na kushiliwa na pini. Si rahisi kudondoka au kuonekana kwa urahisi. Akaitoa na kuogopesha wote.

“Naomba dada yake au bibi yake amuangalie mwilini kama kuna kitu amevaa.” Mama Ruhinda ameingiwa woga, hataki hata kusogea. Mama yake Raza yeye ndio ilikuwa mbaya zaidi, kama ameona mzimu! Hataki hata kusogea alipo Polla. Pius akaanza kumpapasa, ndipo Poliny naye akaanza kukagua sehemu zote alizokuwa akielekeza Nyange, hapakuwa na kitu.

“Sasa aina hizi za vitu vyote ni vya kuchoma. Na Sonia ameniambia kuna vingine vimewekwa kwenye mto unao lalia?” Akamuuliza Pius. Akiwa amejawa hofu, anachohitaji ni msaada wa haraka Pius ikabidi asimulie tena YOTE. Poliny akazidi kuogopa.

“Nilimuonya mimi Raza, na mambo yake ya kukimbilia kwa waganga. Nikamwambia, mume ushapata, mganga tena wa nini?! Kutwa yupo kwenye kuzindika kusikoisha. Haki nilimuonya mimi Raza. Na ndio maana mimi ananiona mbaya. Nilimwambia kwa kumpa mfano wangu wa waziwazi. Nimezaa mimi watoto watano, tena uswahili katikati ya watu, na mlango wa mganga siujui! Mbona wote wamekuwa hakuna mwenye shida! Basi mimi ndio kuniona mbaya! Simtakii mema! Yako wapi sasa? Ona jinsi anavyotesa watoto wasio hatia! Faida yake ipo wapi sasa?” Mama yake akaongeza akiwa na masikitiko. Wote wakamgeukia mama yake Raza aliyekuwa akizungumza pembeni kidogo na pale walipokuwa wamemzunguka Polla. Yeye hataki hata kusogea kwa hofu.

Pale Unapokula Mbivu Baada Ya Uvumilivu

Mapenzi ya kweli ni kuvumilia ukimya, pale  ambapo sauti zimekoma. Na wakati mwingine penzi la kweli huwa kama taa ya mwanga hafifu, pale moyo wa mwenzako anapokuwa gizani. Ndicho kilichowatokea wawili hao. Walipita mengi, lakini hatimaye wakajikuta wamesimama pamoja. Walishinda hapo kitandani. Kila mmoja akiwa na furaha ya aina yake. “Kwa hiyo huna shida ya kuishi Marekani?” “Nikiwa mkeo hata ukiniambia twende tukaishi Mlalo, milimani, sina shida.” Mill alifurahi sana. Ukweli hakuwa amepanga kuishi hapo nchini. Kwanza alikuwa akiishi kwa vibali tu, kama mgeni.

“Na hii kwa ajili ya kumuhangaikia Shema. Nimefurahi! Nimefurahi sana Mill. Sikutegemea kama ulikuwa ukifanya kitu kikubwa hivi!” Hapo tena akapongezwa kwa penzi la haja. Akapambwa sifa huyo Mill, akatamani atoe tarehe ya ndoa hapohapo kitandani ila akaona afanye taratibu, apange kitu cha kumfurahisha.

~~~~~~~~~~~~~~~

Alipohangaika na huo mwili wa Pam mpaka akatulia ndipo akatoka kwenda kuchukua maji. Akarudi na maji ya Pam. “Njaa inauma Mill!” Akarudi kwenda kupasha chakula walichobeba kutoka hotelini.

 “Nimefikiria.” Pam akakaa maana alirudi na sahani mbili. “Nianze kwa kukuuliza swali.” “Juu ya nini?” “Ni juu ya nani, sio nini.” Mill akakaa hapohapo kitandani na sahani yake, baada ya kupokelewa moja.

“Ulisema mama alirudi nyumbani kijijini sababu ya ugonjwa?” “Sio alirudi Mill. Alirudishwa na mumewe, sababu ya ugonjwa. Na alivyo mkatili yule mwanaume, akamrudisha na watoto wawili ambao hakuwahi kuhangaika matunzo.”

          Pam akaanza kupandisha hasira. “Sasa Eric akaona baba yake amefaidi, akaona amuige. Ni mshenzi sana. Na aisee jana ilikuwa mbaya! Ilikuwa mbaya sana.” “Jana uliponiambia ulikwenda kukutana naye kwa chakula cha mchana?” “Chakula chote kiliishia mwilini mwake na nikamuogesha na ile soda, kisha kummwagia maji juu.” Mill hakutegemea! Akashituka sana.

“Pam!” “Nilishaanza kumrushia ngumi, ndio wakanishika. Nilijaza watu pale! Nilimtukana Eric mpaka nikajisikia vizuri.” “Pam!” “Aisee ilikuwa mbaya. MBAYA mno. Hujawahi ona.”

“Basi mimi nilijua ulipata wakati mzuri!” “SANA, ambao sikujua kama ningekuja kuupata na yule mwanaume. Hivi unajua aliniacha jela nikiwa mjamzito, namlilia shida!” “Pole Pam.” “Mimi sawa, lakini Eric amemtupa mama kabisa! Mama aliyemuombea nafasi ya kuja mjini! Kwa kumsikia akiomba kwa kunyenyekea! Tena kwa shangazi!”

“Mwanzoni ni kama alimkatalia. Nikiwa nasikiliza mazungumzo yao, nikamsikia mama akimsihi shangazi au wifi yake, akamwambia kabisa, ‘ni hivi sina uwezo wa kupiga magoti, wifi, nisaidie japo Eric tu. Nitolee huku kijijini, asogee mjini, asome’. Akamuomba akimsihi kwa unyenyekevu. Akimwambia vile Eric alivyo na juhudi ya shule lakini kule kijijini hatafika mbali.” “Naomba usilie Pam. Tulia.”

“Hakika naumia Mill. Eric anakuja mjini, anaolewa, anamsahau mama! Anasema anajijenga yeye na mkewe, hawawezi msaidia mtu, huku anajua mama ni mlemavu hana msaada! Anasahau alivyotoka kwa kusaidiwa na yeye na watu! Anakua kama baba tu!”

“Kwani ilikuaje mpaka mkakutana tena jana? Naomba tulia unielezee.” Akajifuta machozi kabisa na kuendelea. “Yeye mwenyewe alinikuta natoka benki. Sikujua kama amehamia kwenye ile benki. Sikumuongelesha. Yeye mwenyewe akanianza kunisalimia tena kwa kunifuata. Nikaitika salamu na kuamua kumuacha. Maana aliniacha jela akiniambia hatanitoa, nijifunze. Nimetoka jela nikawa nahangaika na mwanangu huku nikimsaidia mama bila ya kumtafuta, huku nikijua anao uwezo ila hatanisaidia maana nasikia alikwenda kunawa eti mikono kwa mama kwamba hataki kunisikia tena mimi na mama eti kwa kuwa ananiendekeza, basi na yeye anaachana naye! Kweli Mill?”

“Haikuwa sawa Pam. Lakini jua mimi ndiye niliyemponza mama. Isingekuwa mama kuja kukusaidia Shema, asingeingia matatizoni.” “Nilikwambia hata mama mwenyewe anajua ni kisingizio tu. Eric si mtoaji tokea mwanzo. Aisee jana nilimsema! Nilitamani nipigane naye, nimg’ate mpaka nimtoe ngozi! Sema walinishika.” Mill akaanza kucheka.

“Angekupiga?” “Si na mimi ningekuwa nimempiga! Nilipanga nimwachie alama abaki nayo ya kudumu kila akiingalia awe anakumbuka alipotoka. Maana jana nilimkumbusha hatua kwa hatua. Mpaka nikamwambia nilikuwa natamani kuiona sura ya baba lakini kwa kuwa nishamuona yeye, inatosha. Hawana tofauti.” Mill akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha. Wakaendelea kula.

Uzazi Mzuri.

Hakuna anayetoa kumzidi Mungu. Haijalishi nafasi na kile ulichonacho, msaada ni mbegu. Huota kwa kadiri ya Mungu anavyojalia malipo yake. “Naona tumrudishe mama mjini kwenye maisha yake.” Pam akahisi kama hajamsikia vizuri. Akabaki amekodoa macho.

“Mama si anajua kusoma na kuandika?” “Anajua Mill! Ila sidhani kama…” “Kazi ya kupokea pale pesa na kuingiza kwenye kompyuta haiitaji shahada ya uhasibu. Mgonjwa anapoenda kulipia, akimtajia kiasi cha pesa cha kipimo chake, anamlipa, anaingiza kwenye system, risiti inajitoa yenyewe, anamkabidhi, kazi imeishia hapo.”

“Kwamba ndio mama afanye?!” “Unadhani itakuwa ngumu sana?” “Hapana Mill! Ataweza. Na nakuhidi nitamfundisha atakapokuwa anakwama au muda wangu wa chakula cha mchana nitakuwa nikiutumia naye.” “Sitamtoa nyumbani na kwenda kumuweka pale! Hapana Pam. Atapata muda wa kutosha tu pale wa kujifunza mpaka nitakapoona yupo tayari, ndipo watakapokuwa wakipokezana na yule msichana pale. Anabanwa, anakosa hata muda wa kula!” “Nimemuona. Ila si mlalamishi kabisa!”

“Ni rafiki wa karibu sana wa Fatma. Huwa nawafurahia utendaji kazi wao. Hutawasikia wakilalamika hata mara moja. Ndio maana mara nyingine huwa nawapa posho kama shukurani tu. Tulianza wachache sana, na wamejitoa bila kumlalamikia yeyote, hata Mbise anawasifia. Hutamkuta Fatma amekasirika hata mara moja.” Pam akaona haitoshi.

Akatoka kabisa kitandani na kupiga magoti chini ya kitanda, pembeni yake. “Nakushukuru Mill. Asante sana. Hujui unachofanya.” Na machozi juu! “Acha bwana Pam! Wewe unataka kunigombanisha na Mungu, aone namchukulia utukufu.” Ikabidi Pam acheke tu. “Kuna kipindi nilitaka arudi mjini moja kwa moja, ila akaniambia tuwe tu wakweli. Hali yangu mbaya, akija ndio itakuwa mbaya zaidi. Bora abakie kijijini hatashinda njaa. Maembe na matunda mengine yapo, halafu mjomba haachi wazazi wake na njaa. Watakachokula wazazi wake, na yeye atakula. Akaniambia ni bora nikipata cha ziada niwe na mtumia kuliko aje na yeye awe mzigo huku mjini.” “Haya simama hapo tujipange zaidi.” Akasimama.

“Unafikiri atahitaji msichana wa kazi?” Pam akabaki akifikiria maana kijijini hapakuwa na msichana wa kazi ila yupo jirani aliyekuwa akiwasaidia mambo muhimu. “Itabidi kumuuliza. Tutamuweka wapi sasa?” “Ninaposema aje huku, natamani arudie maisha yake. Yaani awe na kwake na mamlaka yake. Asijisikie anakula kwa shikamoo! Awe huru.” Pam akacheka akifikiria.

“Nafikiria akaishi kule ulikokuwa unataka kukimbilia.” Pam akacheka kama mazuri. “Usicheke bwana Pam!” “Mwenzio nataka unioe.” Mill akamtizama kwa kumsuta. “Sasa huko tusirudi tena bwana harusi wangu. Tuendelee na mipango. Huwezi jua naweza kukupa asante nyingine!” “Au unishukuru kabisa ndio…” “Hapana bwana, tulia! Wewe huchoki! Tokea asubuhi unashukuriwa tu, na hujamaliza jambo unataka kushukuriwa!” Mill alicheka hana mbavu. “Pam!” “Wewe endelea kutoa pointi za maana ili uzidi kunipandisha mzuka.”

“Maana pale nishalipia ya miezi 6. Na kuna kila kitu bado vichache sana. Halafu…” Pam mwenyewe akaanza kuhamasika. “Mama yangu anarudi mjini na ajira juu! Hakika Mungu ana mambo yake. Kuna kipindi, zamani lakini, alikuwa akizungumza na mimi tukiwa tumelala, hata kabla sijamzaa Shema. Akaniambia alikwenda mjini akiwa amejaa, akarudishwa mtupu na watoto. Aliiongea kwa uchungu. Akasema amepoteza nusu ya uhai wake akiwa mjini, na kurudishwa nusu. Nilimuhurumia na hapo ndipo niliposema nitakuja kumrudisha mjini nije niishi naye.” Akatulia akifikiria akawa kama kitu kimepita kichwani.

“Ulikuwa umepanga aje lini?” “Wewe zungumza naye umsikilize. Akikubali ijumaa wakati dereva akimshusha Shema hapa jioni, anakwenda kumfuata. Jumamosi mchana wanarudi.” Pam alifurahi huyo, hakuwa akiamini. “Asante Mill! Asante sana. Na mahari nimekusamehe!” “Acha uhuni Pam. Unataka kunitapeli wakati nimeambiwa sidaiwi!” Pam alicheka sana.

“Nilijua hujaelewa vizuri!” “Wewe nishukuru ili niendelee kufikiria vizuri.” “Naona kweli ukishukuriwa akili inatulia, na kutoa mambo mazuri.” “Sasa hii ni siku ya kwanza tu. Zikikamilika zile siku mbili nilizokuomba, nikushike bila muingiliano.” “Naona tutanunua dunia.” Mill alicheka sana na kutoka hapo kitandani akiwa amemaliza kula anarudisha sahani jikoni.

“Nimeshiba Pam.” “Urudi nikubembeleze ulale.” Akamsikia akicheka huko. “Ninavyopendwa Mill mimi!” “Na hapo bado hujatangaza ndoa! Ukitangaza je?” “Mama wewe utaolewa kanisani! Mbona ujumbe wangu nilishaupata! Na kufukuzwa juu!” “Sasa hivi unapendwa sana.”

“Twende basi kule ndani kwangu kuna sehemu nataka tukafanyie mapenzi.” “Mill!” “Utafurahia. Nakuhakikishia. Pazuri sana. Kwanza kule kuzuri Pam. Twende ukapaone. Patakuwa kwako pia. Twende.” “Mbona umeng’ang’ania hivyo?” “Kule kuna nafasi Pam. Nafanya mapenzi na wewe huku mazingira yananiunga mkono.” “Mbona hapa pazuri tu kama kule kwa Mike?” “Hilo daraja Mungu alishanivusha Pam.” Alicheka Pam, alicheka sana.

“Mill!” “Nakuwa mkweli. Mazingira haya ni wakati mwanafunzi. Sasa Mungu ashanibariki, kwa nini niishi kwa kujibana? Nimeinuliwa mwenzio!” Pam akamtizama. “Si kwa kujivuna tu, twende ukapaone na wewe, ili ujue ninachozungumzia?” “Kwa hiyo mimi ndio ngazi hii?” “Kwa kuchagua kwako Pam. Mimi nilikuwa nikihangaika ili tufaidi wote. Na haya nilikwambia tokea siku ya kwanza kabisa kuzungumza na wewe kwenye simu. Bisha.” “Kweli.” Pam akakumbuka kipindi hicho alikuwa akifanya kazi kwa Sandra.

“Sasa? Mwenzio nilijiona nipo juu na wewe. Ila naona mwenzangu unang’ang’ania vya chini. Mara uswahilini walipo mashoga zako. Haya, mara kwenye vijumba visivyo hata na madirisha! Tumehangaishana weee, umekuja kuishia kwenye kinyumba cha pembeni, hutaki kuingia ndani! Tena unakasirika kabisa kama si kuchagua maisha ya shida ni nini?” “Mbona hapa pazuri sana! Tokea nazaliwa mimi sijawahi ishi kama hapa.” “Ndio nakwambia, makubwa zaidi yapo hapo mlango wa pili tu, twende ukajionee jinsi unavyojipunja na kumtesa mmarekani wangu.” Pam alicheka, alicheka sana.

“Shema huyo!” “Kumbe! Si mtanzania tena. Sasa wewe unataka kutupunja bila sababu!” Pam alikuwa haamini akicheka. “Kuishi na watanzania kazi!” “Mmeanza kuninyanyasa Mill!” “Bwana wewe mbishi sana Pam! Jambo dogo unalifanya…” “Kuolewa mimi si jambo dogo.” “Nishakwambia nakuoa. Nipe huo mwili na kesho. Nikitoka hapa naandaa harusi. Tatizo ni nini mama? Kwa nini tuishi kama wakati ule mwanafunzi? Maana mimi siwezi kulala kule wakati wewe umelala hapa na mwanangu. Najiona kama mbinafsi!” “Basi Mill.” Pam akaona aende akajionee.

~~~~~~~~~~~~~~

Raza Alipanda Mbegu Ya Dhambi Kimykimya, Ikaota Mizizi Chini Ya Udongo Wa Siri; Mavuno Yake Ndio Hayo, Yanamtumbua Usiku Usio Na Mwanga.

Mwisho Wake Ni Upi?

Ya Pam Yanakwenda Zaidi Ya Alivyotarajia. Nao Mwisho Wao Ni Upi?

Love At First Sight.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment