Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 57. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 57.

Kwa hakika mapenzi yamerudi kwa hatua za aina yake. Kama jua la asubuhi baada ya mawingu, likichoma baridi ya majonzi ya kale ndivyo ilivyokuwa kwa wawili hao. Mill alibaki akimtizama Pam akimalizia kujiweka sawa mbele ya kioo akiwa amesimama nyuma yake, kabla ya kutoka kwa kifungua kinywa. Tamaa ikampanda kila alipomtizama juu mpaka chini. Ni Pam kwa hakika.

Pam akimtizama kupitia kioo. “Unawaza nini? Bado upo na mambo ya Shema tu?” “Bado siamini Pam! Siamini kama tupo wote.” Pam akacheka na kugeuka. “Nikuulize kitu Mill?” “Kabla hujanitoa kwenye hii hali, acha nikukumbatie kidogo. Nishaamka kwenye asubuhi mbaya, bora wewe ulikuwa ukiamka huna pesa, una mtoto anayekupenda. Suluhu ilikuwa ni kufanya kazi kwa bidii, ukijinyima muda wa kupumzika, kutengeneza pesa, mnakula na kulala na Shema kwa furaha.” Pam akakunja uso.

“Mimi nilikuwa na kila kitu. Juhudi zilikuwa zikilipa, ila silali na sina jinsi ya kufanya. Pesa ipo, mke ndani yupo na watoto wa jinsia zote, lakini hakuna amani. Aisee usiombe kuishi na mwanamke mwenye kelele Pam! Halafu mlalamishi! Huwezi kufikiria, huwezi kutulia, halafu yupo na wewe kila mahali. Nyumbani na ofisini. Huna pakuhemea.” “Pole Mill!”

“Aisee acha mama. Kila mtu anawasifia, lakini ndani kunawaka moto, na hakuna dalili ya kuzimika. Hakika nakupenda na nakuhitaji Pam. Ni kama Mungu alinipitisha kuonja lile fukuto, ili nithamini nilichokiacha huku nyumbani.”

“Mwanamke alinitesa yule! Halafu juhudi zangu zote akaishia kutapanya na mwanaume asiye na mbele wala nyuma! Pesa yangu yote! Mali zangu zote! Kweli?” “Unaanza kuharibu mudi Mill. Mpaka uso umebadilika wakati muda mfupi tu ulikuwa na furaha.” Pam akamsogelea. “Huko umeshatoka. Tupo hapa sasahivi. Naomba tulia.”

“Wewe mwenyewe ulisema tulichonacho hakiwezi kutafutwa, ila mali inatafutwa. Tulia. Fikiria kwa upya. Anza tena. Tena sio kuanza Mill. Hapa nchini kwenyewe nimeona unatengeneza pesa nzuri sana.” Mill akakumbuka yeye ndiye muweka pesa benki.

“Unatengeneza pesa nzuri tu. Na ukiamua kwa jinsi ulivyo na akili nzuri, unaweza fanya kitu kingine zaidi na ukaingiza pesa ziadi.” “Pesa unayoiona hapa, haifiki hata robo ya pesa niliyokuwa nikitengeneza kwa siku kule.” “Mill!” “Acha Pam! Acha mama. Nilitengeneza pesa kule, na ilikuwa ya uhakika. Juhudi zangu zote na pesa aliyowekeza baba yangu ni kama imepotea bure tu!” Pam akawa hajamuelewa.

“Twende tukale, kisha unielezee vizuri.” Wakatoka wawili hao kwenda kula sehemu nzuri ya hadhi ya Mill. Bwana Pam alipendeza, ile ya kupania. Mill alikaa mbele yake. Wakaendelea kula.

“Acha kuniangalia hivyo bwana!” Mill alicheka. Akacheka sana. “Mimi nimekuangaliaje?” “Nimekuona mpaka umepotea! Sasa umefika wapi?” “Kukuvua chupi.” Pam alicheka mpaka akapaliwa. “Na gauni?” “Hilo nishalirarua zamani sana, lilishanipotezea muda.” Pam akazidi kucheka asiamini.

“Yaani tumetulia hapa najua unafurahia chakula!” “Na ndivyo ilivyokuwa mpaka yule muhudumu alivyokuja na juisi hapa, akapotelea hapo kifuani!” “Ndio maana ukakohoa!” Pam akacheka sana.

“Maana nilimuona haondoi macho hapo.” “Alipoondoka?” “Ndio nikajiambia acha niangalie kwa makini kilichomvutia mwizi yule. Ziwa mama! Nikajikuta nakuvua gauni, nakutoa sidiria.” “Hapahapa!?” “Kama hakuna mtu vile. Juu ya hiihii meza.” “Vyakula?” “Nilishavisukuma vyote kwa mkono, ukabakia wewe tu mezani.” Pam alikuwa akicheka haamini.

“Naomba toa mawazo huko, tuzungumze bwana Mill!” “Nimekwambia nipe siku mbili. Nikishakushika hizo siku mbili angalau akili itaanza kufanya kazi. Tena kadiri nilivyokuwa nikikusimulia hapa, hali ishakuwa mbaya. Tumuite muhudumu, tuondoke hapa.” Naye Pam hali ilishabadilika, anataka kweli akatolewe hilo gauni. Wakafungashiwa vyakula na kutoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Kula njiani wakati nakuendesha.” “Ndio maana nakupenda.” Pam hana mbavu. Mill anakula huku Pam akiendesha kurudi nyumbani. Akala mpaka akamaliza wakiwa ndio wanaingia getini. “Naomba ukaribie kwangu.” Pam akashituka na kumgeukia. “Uliniahidi nini Mill?!” “Acha kukasirika Pam. Ni kwa sasahivi tu! Sio kwamba nakuhamisha. Mbona mimi nimelala kwako?” “Hapana Mill. Hutaishi na mimi unyumba. Mwishoe tutajisahau. Tuishie hivihivi, Shema akituangalia, na yeye aje aishi hivihivi kama wadogo zako. Umeniahidi utaishi maisha ya mfano kwa ajili ya Shema.”

“Pam umepaniki tu mpenzi wangu.” “Hapan…” “Subiri kwanza Pam. Nilipokwambia nataka kuanza upya na wewe, na hili likiwemo. Kupafahamu kwangu! Kuna ubaya gani? Au unafikiri na mimi napenda haya maisha kwamba nataka kumkuza Shema kwenye makuzi ya nyumbani kwetu?” Akatulia.

“Siwezi. Naanza kwa heshima na sitaacha kukuoa kanisani. Nilikuahidi na nitatekeleza. Tafadhali tulia.” Pam akapoa. “Nakupenda Pam.” “Samahani Mill. Samahani.” “Najua kuna sehemu unajiambia kuhamia hapa ndio umefunga milango yote ya tumaini la ndoa.” “Na ndio maana jana nilikuwa nikisita Mill. Sisi tunakuwa watu wakuanza, hatufiki mwisho. Mwenzangu Kisha ulimuoa akawa akijulikana kisheria. Mimi nimebakia..” Pam akakwama kwa uchungu.

“Kisha sio mwenzio. Na sikumuoa kwa mapenzi. Nilimuoa kwa ajili yako Pam. Kisha alikuwa njia ya kumaliza safari niliyoanza mimi na wewe, ila nikakwama kwake. Sasahivi sina sababu ya kutokukuoa wewe. Wewe hushangai kwa nini sikumfikisha yeye kanisani?” Pam kimya akiegesha gari.

“Pam?” “Mimi sijui Mill?” “Kwa sababu kanisani ni sehemu yetu mimi na wewe. Nilijiambia hakuna mwanamke ataingia kanisani na mimi na kupeana kiapo kama si wewe. Nitakuoa Pam. Uwe unaishi hapa, au kwingineko, ukikubali tu, nitakuoa. Ila sikutaka tukurupuke tujikute tu tunakimbilia kanisani!” “Kwa nini?” Pam akamuuliza na kumshangaza Mill.

“Kwamba wewe unataka ndoa hata kesho?” “Nataka ndoa ya kanisani na wewe tokea miaka 10 iliyopita Mill. Sijabadilika. Mimi hivyo vyakuanza upya sitaki. Nataka tuendelee. Utanitoa huko kwenye starehe nikiwa mkeo, sio kama Pam wa wakati ule. Nishakuwa mama Shema. Nataka tuendelee. Tutaanza mpaka lini? Maana tusipoangalia, huu mchezo wa kupeana penzi tutauzoea, mtoto mwingine atakuja, itakuja sababu ingine tena, ndoa ishindikane, nibakiwe na kazi ya kuzaa tu, wengine ndio wanajulikana ni wake zako. Hivyo mimi sitaki.”

“Na mimi nataka kukuoa Pam.” “Lini?” Pam akawahi. “Maana safari hii sitaki mambo yakusema unataka…” “Ndio jambo nilitaka kukwambia Pam. Kule nilifanikiwa sana. Kwa nini tusiondoke wote watatu. Tukafunge ndoa kule ili…” “Hapana Mill.”

“Nisikilize Pam.” “Hapana. Huo mchezo sifanyi tena.” Pam akashuka garini kabisa, akachukua pochi yake na kwenda kwake, kwenye nyumba ndogo.

Mill akashuka na vyakula akamfuata. Hakutegemea kumkuta anafungasha. “Pam!” “Hakika hapana Mill. Huu mchezo sifanyi tena. Kama unanipenda kweli na unania ya kunioa, utakuja nitafuta. Sipotezi tena muda.” “Tafadhali nisikilize.” “Tulishindwa safari ile, safari hii kitakachowezekana ni kipi? Ubalozi wa Marekani washaninyima mimi Visa mara tatu! Kweli unataka tuanze upya kabisa! Hapana Mill.”

“Tafadhali naomba tuzungumze Pam. Nisikilize acha kufungasha.” Pam akaendelea. “Safari hii unakwenda ubalozini ukiwa na mimi pamoja na Shema. Mimi nakuombea wewe nikiwa kama raia wa kule! Hawatakunyima.” “Basi mimi SITAKI.” Mill akabaki amesimama.

“Sitaki. Na hapana Mill.” “Hutaki kwenda Marekani au hutaki k…” “Hutanianzishia mambo yasiyo na uhakika. Kwamba hatima yetu inategemeana na tutakayemkuta siku hiyo pale ubalozini! Huo mchezo sifanyi. Tumkute hana mudi nzuri, aninyime mimi na mwanangu hiyo Visa kwa sababu zake tu!” “Kwanza ukumbuke Shema yupo chini ya miaka 18, na yeye ameshakuwa raia kule.” Pam akasimama wima.

“Usikasirike. Na usipaniki.” “Umefanya nini Mill?” “Nilipowarudisha wale watoto wa Kisha kule, nikamuanzishia process za uraia. Unakumbuka kuna siku nilikuja kumchukua nikakwambia kuna sehemu anahitajika?” Pam akabaki akimtizama.

“Huyu mtoto anakipaji kikubwa Pam. Kuna nchi wanaweza kukitambua na kukikuza kwa kiwango cha juu sana. Ndio maana umeona nimemuweka kwenye timu kubwa na uangalizi mzu…” “Umefanyaje Mill?” “Alipata nafasi ubalozini. Wakamchukua alama za vidole, tukapeleka na picha zake. Nikawaachia. Wameshatuma hata hati yake ya kusafiria kama raia wa Marekani. Yeye kwake haikuchukua process ndefu. Kwa sababu mimi baba yake ni raia.” Pam akahisi hajaelewa.

Akakaa kitandani. “Kwa hiyo mimi na Shema kisheria ni raia wa Marekani.” Mill akamalizia akicheka kama mazuri. “Unanitania Mill?” “Najua umekasirika. Ila sikutanii.” Pam akabaki akimtizama. “Labda ungetaka kujua kwa nini sijakwambia?” Pam akabaki akimtizama. “Eti Pam?” Kimya.

“Ni kwa sababu kwanza tulikuwa hatupo kwenye maelewano. Halafu nilimuahidi Shema kumpeleka nilipokuwa nikiishi. Kumuombea Visa, ingekuwa ngumu kuliko kumfanya awe raia. Halafu Pam, si kitu kibaya. Hata tukiamua mimi na wewe tubakie hapahapa nchini, wewe unatudhamini.” Pam akabaki akimtizama.

“Niambie mtanzania wangu?” “Ujue Mill umenikosea wewe?” “Kumfanya Shema kuwa mmarekani ndio nimekukosea Pam? Hivi unajua faida zake lakini?” Pam akabaki kimya. “Huyu mtoto anauwezo wa kusoma shule zenye kiwango cha kwanza hapa ulimwenguni. Hao unaowaona kwenye luninga wakicheza mpira ligi za kimataifa ndio atakuwa akitazamwa Shema Mgini.” “Shema Shelukindo Mgini. Au umembadili jina?” “Sithubutu. Acha nikuletee passport zetu.” Mill akatoka kwa haraka, Pam asiamini.

Kwa upande fulani hakuamini kwa furaha. Yake yalikuwa magumu sana. Mara tatu, aliomba uraia akiwa na vithibitisho vyote na kunyimwa. Leo mwanae amekuwa raia! Akabaki kama amepigwa butwaa.

Mill akarudi na passport mbili. Zote zinafanana. Akamkabidhi. Pam akazifungua akakutana kweli na ya mwanae. Shema Shelukindo Mgini.  “Hiyo hati ya rangi hiyo, mama si mchezo.” Akaanza kujisifia. “Huyo mtoto inamaana anaweza ingia nchi yeyote ulimwenguni hapa bila zile shida kama zako za kuomba VISA.” “Haiwezekani Mill!” “Wewe kwa nini unafikiri nilichangamkia kwa haraka? Passport ya Marekani ina nguvu mama. Unaingia utakapo, wanakuwa wakikugongea tu VISA ukifika uwanja wa ndege wa hiyo nchi, basi. Mwanangu huyo hatakaa akapata shida kama ile yako ya kuombaomba VISA. Yaani huyo sasahivi nikimwambia twende zetu, London. Tunakata ticket, bila swali, mpaka uwanja wa ndege wa Heathrow, hukohuko London, pale ndipo watatugongea muhuri na kutukaribisha kwa heshima zote.”

“Hakika sikuwahi hata kufikiria kama unawe..” “Ninapokwambia nakupenda, jua NAKUPENDA na Shema ni mzaliwa wangu wa kwanza. Nawafikiria kupita unavyofikiria wewe japo sikuwa nikijua ni jinsi gani nitakupata tena. Ila hivi ndivyo nilivyokuwa nikitaka kukwambia.” Pam akamtizama maana macho yalirudi kwenye hati ya kusafiria mwanae.

“Pesa unayopeleka benki kila siku, sio pesa ile Pam. Kule nina uwezo wa kutengeneza mara dufu ya hizi. Kile kitu nimeanzisha kwa sababu yako na Shema. Ni nafasi niliyopewa na kina Komba, nikaikubali nikijua itanisaidia wakati tukiwekana sawa na wewe na niwe karibu na Shema. Sitaki akue bila baba. Ila ukikubali kwenda kuishi kule na mimi, au sisi Marekani!” “Mmeshaanza kunibagua?” Mill akacheka sana.

“Nisikilize mama. Twende tukatengeneze dola mpenzi wangu. Pesa ya maana isiyo na maswali wala kubabaishana.” “Kwamba pesa unayotengeneza hapa si kitu?” “Hiyo unayopeleka benki?” “Mbona nyingi hivi?” “Pam! Hiyo pesa ya kubadilishia mboga, mama! Wewe unafikiri ni kwa nini Kisha alikuwa akining’ang’ania japo hanipendi?” “Pesa?” “Pesa haswa. Hapa nilipajenga kama mchezo mpaka Mike alikuwa akinishangaa. Twende zetu tukatengeneza pesa ya ukweli Pam. Wewe unanidhamu ya kazi na unajituma. Twende zetu.”

“Ulaya!” Pam akawa ashahamasika. “Sio Ulaya, Pam! Nilishakwambia.” Akaanza kumcheka. “Wewe cheka utakavyo. Iwe Ulaya iwe Marekani, japokuwa nataka sana kwenda huko, lakini hutanitoa hapa bila ndoa ya kanisani. Hakika HAPANA.” “Wenzio wakisikia Marekani wanarukaruka, hawafikirii mara mbili!” “Hapana Mill. Acha mengine yaongezeke. Mimi nataka ndoa kwanza.”

“Hudhani kama wazo langu zuri? Tukifungia kule itakuwa rahisi kupa…” “Hapana Mill.” “Safari hii hawatakunyima Pam. Itakuwa rahisi. Mwanao mwenyewe ni raia, mimi baba yake raia, watakunyima vipi?” “Mill, ndoa ya kanisani KWANZA, mengine baadaye. Hutanitoa hapa mimi na Shema, mimi nikiwa kama hawara. Acha waninyime huo uraia wao, kwani huku nimefukuzwa?” Mill akatulia akifikiria.

“Nenda kafikirie kule kwako. Hapa uondoke kabisa.” “Pam! Na ile mipango yetu?” “Unishikeshike hapa, kumbe mwenzangu una yako? Wewe kama mnywaji sana wa maziwa, nunua ng’ombe.” Bwana Mill alicheka. “Nilishakununua Pam.” “Miaka yote ile! Ng’ombe uliyemuacha alishakufa. Unaanza upya.” “Pam!?” “Sasa ulimaliza safari uliyoanzisha na baba yako? Kama kweli ulimuacha huyo ng’ombe, nani alikuwa akimlisha?” Kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Haya toka humu ndani, kaendelee kufikiria kwako. Huna lako humu ndani.” Akamuona anatoa simu, anapiga. “Kapigie simu zako huko kwako, sio hapa.” Akamtizama na kuweka kwenye spika kabisa. “Baba Shema?” “Shikamoo mama.” Pam akashituka aliposikia sauti ya mama yake. “Mnaendeleaje huko? Shema na mama yake?” “Wote wazima mama yangu. Nilikuwa na swali.” Pam akakaa.

“Karibu.” “Najua safari yangu na Pam tulifika katikati, ndoa ya kanisani nilitaka ikafanyike nilipokuwa nikiishi. Sasa safari hii nikitaka tumalizie kufunga ndoa ya kanisani, natakiwa kufanya nini?” Pam hakuamini. “Ni kwenda kumuona mchungaji. Kwanza inabidi mtubu, mrudishwe kundini. Mlianza maisha ya ndoa kabla ya ndoa yenyewe. Mmezaa kabla…” Pam akaanza kucheka kwa sauti ya chini akijua siyo anayotaka kuyasikia Mill. Mama Eric akaendelea, Mill akiwa ametulia akimwangalia Pam jinsi anavyomcheka huku akimsikiliza mkwewe.

“Hapo mkweo anakuita wewe mdhambi.” Pam akamnong’oneza kwa sauti ya chini sana, Mill akaanza kucheka taratibu huku akisikiliza dhambi zake huko kwenye simu. Akaweka mute kwenye simu. “Naona mama mkwe anaorodha ya dhambi zangu ZOTE! Na utaratibu wa kutubu mrefu!” Mill akamwambia Pam na kufanya wacheke kwa pamoja. Mama Eric bado alikuwa akiendelea.

“Kwa hiyo ndio hivyo baba.” Mill akagutuka na kutoa mute. “Nashukuru sana mama yangu. Hayo nitayatendea kazi. Na kwa upande wa hapo nyumbani? Natakiwa kuanzia wapi?” “Ukimaanisha nini?” “Swala la mahari?” Mill akajibu. “Huko tulishapita Mill mwanangu. Umesahau jinsi marehemu baba yako alivyosihi tusije pokea mahari ya mwingine maana ameshamchukua Pam na kumfanya ni Mgini? Au umesahau?” “Hapana mama. Ila kwa sababu niliishia katikati, nilidhania natakiwa kuanza upya.” “Si kwa huku nyumbani. Si eti baba?” Akamsikia akimuliza babu yake Pam.

“Ni vile na sisi ni wakristo. Ila kimila huyo Pam ni mkewe kabisa. Ile harusi alifanyiwa siku ile, ndio ilikuwa imekamilisha kila kitu huku nyumbani.” Mill na Pam walifurahi hao. “Nashukuru sana wazee wangu. Acha nianze utaratibu wa kumalizia kanisani. Nitawajulisha hivi karibuni.” Wakamshuru huyo baba Shema kama mungu vile.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka Mill anakata simu, Pam hana nguo hata moja. Acha Mill arushe simu mbali na kuvua kwa haraka. “Ningekuvua Pam wangu.” “Nimekusaidia kwa hatua uliyochukua. Nakushukuru Mill.” “Nakupenda Pam. Na sikuwa nimekusudia eti tuendelee kuishi hivi! Hapana. Lazima nikuoe ili niweze pia kurudi kwa wadogo zangu kwa heshima. Nimeshindwa kabisa kuwatafuta. Nimejiona kama msaliti wa baba. Aliniacha kuwa kiongozi, nimeharibu.” “Anza kutengeneza hapa kitandani, halafu tujipange huko nje.” Mill alicheka sana na kuanza penzi.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa haraka sana Sonia akapata neno la maarifa baada ya kugundua hofu ya Pius. “Usikubali akuingie akilini Pius. Kama kweli yeye anao uwezo wa kukufanikisha, kwa nini asijifanyie yeye huo uchawi ndio akashika nyadhifa zako hizo anazokwambia amekufanikisha?” Akamfanya Pius atoe macho kwa Raza na kumgeukia yeye.

“Kwa nini aloge ili wewe ufanikiwe hivyo na si yeye ambaye pia amesoma!? Si angeloga yeye ndio ayapate hayo yote anayokwambia amekufanyia ili wewe ndio uwe ukimuomba pesa?” “Lakini kweli!” “Ona anapoishi huyo mganga wake! Kama kweli wananguvu hiyo si hata yeye angekuwa na maisha mazuri?” Kidogo Pius akaanza kutulia.

“Huo ni uongo na usikubali. Upo ulipo kwa akili zako na kufanikiwa kwasababu umefuata kanuni za kawaida tu alizoweka Mungu. Amebariki kazi ya mikono yako wala si kwa uchawi wake. Shetani HANA zawadi kwa mwanadamu zaidi ya uharibifu tu. Anachoweza ni kuharibu si kubariki. Asikuogopeshe.”

“Na sikwambii ufanye nini na mkeo. Ila jua mimi nitaendelea. Sitishwi na uchawi mimi. Nitamuwajibisha mkeo bila hofu pamoja na mganga wake. Umesikia Raza?”

“Hivi mumeo ameniwahi tu. Ilikuwa nikutafute leo, nikupe onyo bila kujua umbali ambao umeshakwenda. Maana mawasiliano niliyokuwa nayo si ya undani hivi kama ya mumeo. Ni malalamiko yako na vitisho ulivyotuma kwa ndugu wa Mina, basi. Nikijua ni vitisho tu, nikataka na wewe upewe onyo kisheria. Ila kwa hapa ulipofika, kukupa onyo ni kutotimiza wajibu wangu, na mimi naishi kwa neno langu.”

“Hili nilimwambia mumeo. Hata akiamua kukusamehe kwa udanganyifu wowote utakaochagua wewe kumdanganya ili akuhurumie, akaamua yaishe, sio kwangu. Kwa msaada wake au la, wewe nitakuwajibisha. Hutauwa mtoto wa Mina kwa uonevu. Na kuwasaidia tu wewe na mganga wako, jua Mina anaomba sana. Na mama yake haachi kumuombea mwanae mchana na usiku tena kwa kufunga na kuomba. Hata muhangaike vipi, hamuwezi kumpata Mina. Ana ulinzi wa kimungu na hii nimesikia kutoka kwa Mina mwenyewe na kutoka kwenye jumbe za ndugu zao. Yule mama ni muombaji, hamuwezi pata binti yake. Haya, wachukueni nawafuata kituo cha polisi, kesi yao inaanza ramsi leo.”

Akamgeukia Zilo. “Twende.” Raza na Katibu wakatiwa pingu, wakaingizwa ndani ya gari ya wale askari kanzu, wakaondoka. Akafuata Sonia na Zilo, Pius naye ikabidi ajikusanye awafuate akiwa anahofu ya kupita kiasi. “Mpaka watoto wangu!?” Aliendelea kujiuliza bila jibu.

~~~~~~~~~~~~~~

Hofu ya kurudi kwake ikamuingia. Hajui analalaje pale kwenye kitanda alichokuwa akilalia na Raza, alichogundua alikuwa akilalia hirizi. Hofu akihisi nyumba nzima imejaa majini. Akampigia simu mama yake. “Kwema?” “Naomba tuhamie hapo kwako kwa muda.” “Wewe na nani, na kwa nini?” “Mimi na Polla! Sababu nitakuja kukueleza nikifika, ila kama unakubali, namtuma dereva amlete hapo, ila hatakuwa na nguo mama. Naomba nenda ukamnunulie nguo aina zote unazojua atahitaji kuanzia usiku huu mpaka kesho akiamka. Nataka awe hata na begi la shule jipya. Sitaki atumie alilokuwa nalo.”

“Ni nini kinaendelea Pius? Raza yuko wapi?” Pius akajikuta machozi yakimtoka. Alilia, mpaka akaegesha gari pembeni na kuzidi kulia. Alilia sana mama yake akimsikiliza huku akiingiwa hofu.

“Tafadhali tulia ili tuweze kuzungumza Pius. Unamtia hofu mama yako.” Akasikia sauti ya baba yake. Akajaribu kutulia na kuondoa tena gari. “Pius? Raza yuko wapi na kwa nini muhamie hapa na mtoto?” “Acha kwanza nimtume dereva amlete Polla hapo. Kisha nitawapigia.” Akaagana na baba yake na kumtafuta dereva wa Polla.

Upandacho Ndicho Uvunacho.

Alishaacha gari nyumbani kwani siku yake ya kazi huisha huyo mtoto anaporudishwa nyumbani. Akamuomba arudi akamchukue na kumpeleka kwa bibi yake. “Utamkuta yupo tayari.” Kisha akakata simu na kumpigia simu binti yake.

“Ungependa kwenda kulala kwa bibi?” Polla hujua ratiba yake na jinsi inavyosimamiwa, haijawahi badilika. “Kesho shule dad na nina mtihani! Hapa nilikuwa sijalala, namsubiria mama. Hajarudi nyumbani mpaka sasahivi, na simpati kwa simu. Nina wasiwasi, siwezi kulala bila ya kuzungumza naye.” Ndipo akili ikamjia Pius, huyo ni kiziwanda kweli wa Raza, alimdekeza kupita kiasi.

Raza na ukorofi wake wote lakini kwa huyo mtoto hajiwezi. Na huyo mtoto anazungumza na mama yake kuliko mtu mwingine yeyote. Wakati mwingine Raza huenda kukaa naye chumbani usiku mpaka apitiwe na usingizi. Na huyo mtoto humwambia mama yake kila kitu. Ndiye msiri wake.

 “Sijamsikia mama, dad! Nashindwa kulala.” “Simu yake itakuwa imeishiwa tu na chaji. Yupo safarini.” “Amekwenda wapi!?” “Safari ya kikazi.” Polla akashangaa sana. “Mama hana safari za kikazi. Kwanza hawezi kusafiri bila ya kuniambia mimi.” Ni kweli. Pius aliropoka tu. Raza hanaga safari za kikazi. Pius ndio huwa anasafiri, si Raza.

“Beba madaftari yako tu. Utakuta bibi amekununulia vitu vingine, na mimi nitakuja kwa bibi. Umesikia?” “Leo!?” Akamuuliza kwa kushangaa sana. “Dereva anakuja kukuchukua muda si mrefu. Nitakwambia kila kitu tukikutana kwa bibi.” “Mwambie bibi nitalala kwake siku nyingine. Leo nalala nyumbani, namsubiria mama.” “Polla, mama yako hatarudi nyumbani leo.” “Kwa nini na yupo wapi? Mbona mimi hajaniambia! Mama hawezi niacha nikalala bila kuzungumza na mimi hata kama anachelewa kurudi nyumbani, lazima anazungumza na mimi. Haijawahi tokea akaacha kuzungumza na mimi.”

“Kwanza hata hajanipigia kuniuliza maswala ya shule na kuniandaa kwa mtihani kesho. Halafu kesho kutwa ni mashindano. Amesema nitakuwa naye kuanzia asubuhi kwenye mazoezi kabla ya mashindano jioni, ambayo ameshawaambia kila mtu awepo kwenye mashindano. Na bibi na babu walisema watakuja, kwa kuwa hawatasafiri. Hata Poliny alimkubalia mama kuja kwenye mashindano yangu. Kwanza leo aliniambia atanijia na swimming suits mpya. Za mazoezi na za siku hiyo ya mashindano. Kuna mahali yeye ndio ananinunulia.”

“Mimi nitakununulia kesho.” “Kwa nini sio mama?! Wewe hujui. Kwanza hujawahi hata mara moja kuninunulia swimming suits zangu! Hujui zinapouzwa, na hujui aina ninazopenda. Mama yeye anajua. Na huwa kwenye mazoezi yote ya siku ya jumamosi au wakati mwingine ijumaa jioni anakwenda na mimi, sio dereva.” Pius akajua kwa Polla kazi atakua nayo. Maisha yake yamezungukwa sana na mama yake.

“Mimi namsubiria mama. Kwaheri.” “Usikate simu Polla.” “Mimi leo siendi kulala  kwa bibi, kwanza silali. Namsubiria mama. Mpaka aje, tupange mipango ya kesho. Ndio nalala. Kwanza nasoma. Kesho asubuhi nina mtihani. Mama ananisaidia kupitia maswali kabla sijalala. Namalizia kusoma, akija akiniuliza maswali, akaridhika, ndio nalala.”

“Mimi nitakusaidia.” “Namtaka mama. Mama ndiye anayejua kuniandaa kwenye kila mtihani wangu. Sio mkali kwangu kama wewe na Poliny. Nyinyi mnataka nielewe harakaharaka, ila mama yeye ananichukulia taratibu. Nyinyi mnanipanikisha. Mama ananifanya natulia, naweza kufikiria.” Pius akakwama.

“Mama akikupigia, mkumbushe mtihani wangu wa kesho. Mwambie namsubiria. Silali mpaka aje.” “Nisikilize Polla. Mama yako hatarudi leo. Lazima ujifunze kusoma peke yako. Unaweza. Acha uoga.” “Umeanza kunigombesha dad! Na ndio unazidi kunitia hofu.”

“Sijagomba Polla. Ila nakwambia unaweza.” “Kwani kuna tatizo gani kumsubiria mama?! Mbona kila siku namsubiria yeye?” “Nimekwambia mama yako amesafiri.” “Mimi nina uhakika mama hajasafiri. Mimi najua anarudi. Asubuhi alinisaidia kujitayarisha kwenda shule. Akaniaga. Na aliniahidi atarudi na vitu vyangu vyote na atanisaidia kujiandaa na mtihani wangu. Angekuwa anasafiri, angeniambia mimi. Pengine amechelewa tu. Ila atakuja. Mama hanidanganyi. Na kama kuna dharula, angeniambia. Mimi najua na nina uhakika.” Pius akakwama.

Ukweli Raza aliwekeza kwenye mambo ya nyumbani. Japokuwa Pius alipenda sana binti zake na walijua, lakini yeye Raza ndiye aliyekuwa mtekelezaji wa kila kitu na alikuwa na hao watoto bila kuzembea. Uzima wao na ugonjwa wao, baba yao anapokuwa safarini, ni Raza. Wakilazwa mahospitalini walikuwa na mama yao mchana na usiku.

Kwa ukweli, yeye ndio alikuwa karibu na watoto wake. Ratiba ya huyo mtoto aliiweza. Kila mashindano ya huyo mtoto yeye ndio alikuwa mstari wa kwanza kuhamasisha watu wa familia, popote anapokwenda kushindana, wahudhurie. Pius angeweza kukosa sababu ya safari za kikazi, lakini si Raza.

Na Polla ameanza kuogelea tokea mtoto mdogo sana, akiwa na mama yake. Raza alijua walimu wake wote waliokuwa wakimfundisha kuogelea, na kuulizia njia za kumsaidia kuwa mzuri majini. Huyo Polla huwa siku za weekend anapelekwa na mama yake viwanjani kukimbia angalau kwa masaa mawili. Raza alisimamia mambo ya watoto wake bila kuchoka wala kuzembea. Ilimradi kuwafanya bora hata kama si wakiume.

Huyo Polla akiwa majini, unaweza sema samaki. Hakuna aliyewahi mpita kwenye kuogelea. Akiingia uwanjani kukimbia, utatamani kumwambia ashindane mbio za riadha, lakini ilibidi kukimbia ili kumsaidia pumzi majini. Yote hayo ni juhudi za Raza, kuwekeza kwake tokea mdogo.

Ni hivyo tu Poliny anakichwa kama cha baba yake. Lakini hata yeye anajua jinsi mama yao anavyohangaika nao tokea wadogo. Tena peke yake bila kulalamika kwa sababu baba yao alikuwa mtu wa kusafiri safiri sana. Raza akakwepa kabisa safari za kikazi hata kama zina pesa, ilimradi tu aweze kuwepo nyumbani na binti zake.

Alijaliwa roho ya umama, na kuishilia hiyo familia kwa mikono yake yote miwili bila kutaka chochote kiingilie. Mambo ya nyumbani kama mama, alikuwa makini mno kiasi ya kwamba hata Pius mwenyewe hapo mwanzoni alipokuwa akisikia alimloga ili amuoe, aliona hajapoteza. Raza ni mke kwa yeyote aliyehitaji wife material. Hapajaonekana tatizo kwake mpaka ya sirini yalipowekwa mwangani au pale Mina alipoingia pichani ndio akawekwa mwangani.

Hata Pius alipokuwa akishindwa mambo ya unyumba, Raza hakuonyesha tatizo kitu kilichomsaidia Puis na kutomtoa ujasiri kama mwanamme. Wakati mwingine alipokuwa akishindwa, basi Raza alikuwa akimtuliza na kumwambia pengine amechoka sana, wajaribu tena kesho yake. Tena kwa upendo tu, kitu kilichokuwa kikimuacha Pius salama. Na anapofanikisha penzi kitandani, basi huyo Raza huwa anamsifia mumewe! Utafikiri mchepuko kapewa penzi la mume wa mtu! Atampamba hapo weee, nakumfanya Pius ajisikie vizuri, asijue kumbe Raza ndiye ameshika makali. “Namalizia kusoma dad, baadaye.” Simu ikakatwa.

~~~~~~~~~~~~~~~

Pius akabaki amesimama njia panda, moyo unavutwa pande zote mbili. Hatua ni nzito kama kufunga jiwe shingoni. Akili ikabaki ikipima faida na hasara, moyo ukilia maumivu.

Njia ya kulia ni salama, lakini baridi; ya kushoto ni hatari, lakini ipo historia NZITO.

 Kilio cha nafsi kinagongana na sauti ya UHALISIA.

Raza ni mke wa miaka kibao! Si hawara. Amezaa watoto, na amepanda vilivyo. Huyo Polla ni mavuno ya Raza aliyewekeza kwa jasho lake, bila kuzembea. Hawezi kuepuka HILO. Polyin yupo chuo kikuu kwa juhudi za mama yake, hata kwenye sherehe ya mahafali yake alikiri wazi mbele za watu kuwa mama yake alihangaika kumtafutia walimu wa ziada kuhakikisha masomo yanayomsumbua anafanya vizuri, ndio maana amefaulu vizuri sana kumaliza kidato cha 6.

Gari alinunuliwa na baba yake, lakini mwalimu alikuwa Raza mwenyewe mpaka Polyin aliyekuwa muoga barabarani akaweza kuendesha vizuri.

Japokuwa hupishana, lakini mama ni mama. Akisikia baba yake amemfunga jela!?

“Nifanye nini, nipoteze nini?” Pius akabaki akijiuliza.

“Maamuzi ni kivuli cha hatima, nami natega sikio kwa sauti ya ndani.” Akabaki akiwaza barabarani, hajui chakufanya tena

Anamlinda Ayvin au Polla na dada yake?

Pam analilia ndoa ya kanisani.

INAENDELEA…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment