Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 56. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 56.

Ni kweli mapenzi ya kweli yakingoja, hulipa zaidi ya dhahabu. Kwa Mill alikuwa akimsubiria Pam kama mti ukiamini mvua itarudi tu. Kulikuwa kuna kukata tamaa kila mazingira yalipokuwa yakionyesha viashiria vyote vya hapana, na kwa Pam ndio kabisaa. Kitendo cha Brenda kuingia kwenye picha na Mill kuonyesha kumpuuza, alishajua wamemalizana, kumbe kwa Mill kila hatua yake ilikuwa kama mchezo wa karata, akitupia ndoano yake baharini akiamini anaweza mrudisha Pam kwa haraka kumbe alizidi kuweka daraja. Wote wakabakia kama samaki wakitapatapa nchi kavu.

Mpaka Mill alipoamua kuweka kikomo na kujishusha ndipo alipoweza kunasa samaki wake kwa utulivu. Ilikuwa usiku mwingi tu pale walinzi walipokuwa wakimfungulia geti nyumbani kwake. Akavuta gari mpaka kwenye hiyo nyumba ndogo. Akaanza mwenyewe kuwashushia vitu hata kabla hawajaamka. Aliacha gari ikiwaka.

Akiwa anamalizia ndio Pam akashituka. “Tumefika?” “Karibuni sanaaa.” “Hiyo sanaaa yako iishie hapohapo Mill. Mimi nina usingizi.” Mill alicheka sana.

“Hakuna kukukaribisha nyumbani?” “Hapana. Leo tulale, kesho ndio tutakaribishana. Mwenzio nimechoka. Wewe umeshalala.” Akatoka garini na kukutana na nyumba hizo! Akatulia.

“Hapa sijui nianzie wapi? Kote hapa unaishi peke yako?” “Ndio na nyinyi.” “Mill! Hii nyumba umeijenga kwa muda gani?!” “Sio muda mrefu, ila niamini nikikwambia imechukua pesa yakutosha. Nyingi MNO. Hapa hutasikia shida ya umeme wala maji. Matatizo yenu yale ya mgao si hapa. Nilihakikisha katika hilo eneo Mike anasimamia kwa makini. Wakati jua likiwachoma huko nje, mimi natengeneza umeme hapa. Utawasha taa hapa, masaa 24, hakuna wakukuuliza. Hata ukitaka kufua kila baada ya lisaa! Huna atakaye kubugudhi. Mashine zinafanya kazi utakavyo. Nimechimba kisima cha maji, hata ukiamka usiku wa saa ngapi, maji yanatoka ndani. Jumatatu mpaka jumatatu. Moto na baridi, kila bomba. Ushindwe wewe tu.”

“Mmmh! Na hii ulioyosema ndogo, mbona hivyo!?” “Hiyo ni vyumba viwili tu, lakini nilihakikisha ina kila kitu ndani. Kila chumba kina jitegemea na choo chake pamoja na bafu, closet na sehemu ndogo ya sebule yenye tv. Ila kuna choo cha wageni, hakina bafu. Jiko, sebule kubwa ya wote na sehemu ya kulia. Twende ukaone.” “Na kwenyewe kuna maji  na umeme kama huko kwako?” Mill akaanza kucheka.

“Maana unaweza jipendelea, halafu wapangaji wako tukawa tukiishi kwa shida huku.” “Mfumo wa umeme kote ni sawa. Nakwambia nimeingiza vifaa vya solor power kutoka nje ya nchi. Sikutaka kutapeliwa. Twende ukaone.” Wakaingia ndani na Shema aliyekuwa na usingizi hajali alipo ilimradi alishajihakikishia mama yake yupo.

~~~~~~~~~~~~~~

Pam alifikiri Mill angelala kwake, ila alichofanya ni kuhakikisha mwanae amelala chumbani kwake. Kila kitu kilikuwa kipo sehemu yake. Alichofanya Pam  ni kutoa mashuka yaliyokuwepo kabatini na kutandika vitanda, ndio mwanae akalala. Palikuwa pazuri, pakuvutia mno. Zaidi hata ya hoteli ya kitalii.

Wakati anamalizia kujipanga alale, Mill akamwambia yupo mlangoni, amfungulie. “Ni nini Mill usiku huu, kwa nini hutulii kwako?!” “Nimekuleta hapa karibu na mimi ili nikufaidi. Unafikiri utakuwa hapa halafu mimi nilale kule! Hata kidogo.” Akajikaribisha mpaka chumbani kwa Pam, akajirusha kitandani na PJ zake. Pam akamfuata.

“Njoo kwanza nikulambe mwili mzima, ninyonye nitakapo ndio nitaweza kulala.” Pam alifurahi huyo, hata hakujivunga, akakimbilia kitandani. “Muone! Si ulikuwa unajidai hunitaki wewe?” “Nilivyokuwa na hamu na mapenzi yako! Acha Mill! Unanifanya nifurahie nilivyo. Hakuna kiungo mwilini mwangu hukithamini! Unajua kunishika.” Mill akamsogelea na kuanza kumvua nguo taratibu huku akimbusu kila anaposogeza nguo. Akaanza kumsisimua. “Endelea nakusikiliza.” Maneno yakaanza kuwa mazito, hayatoki. Walikesha hapo.

Mpaka kwenye majira ya saa kumi ndipo Pam akazima kabisa kama mshumaa. Mill akategesha saa ili imsaidie kumuamsha, kisha amuamshe na Shema. Na kumtumia ujumbe dereva afike hapo kwake kumchukua Shema kumpeleka shule. Akambadilishia na muda.

Siku ya Kwanza nyumbani kwa Mill

Bado ilikuwa kama ndoto kwa Mill, haamini kama yupo nao hapo. Aliamka pembeni mwa Pam! Kwa dakika kadhaa alibaki akimwangalia kama sungura na ndizi mbivu mtini. Akili ikataka kumrudisha kwenye asubuhi alizokuwa akimka kwenye nyumba aliyokuwa akiishi na Kisha pamoja na wanae, akagoma kujiharibia siku yake. “Mungu amenitoa huko.” Akavuta pumzi kwa nguvu na kutoka kitandani kwenda kumuamsha Shema, mama yake akiwa amelala hana habari.

Walisumbuana na Shema, maana alishazoea kuandaliwa na mama yake. Hajui jinsi nyingine ila vile anavyoandaliwa na mama yake. Mpaka Mill anafanikiwa kumpandisha ndani ya gari, hawazungumzi.

~~~~~~~~~~~~~~

Kwenye majira ya saa tatu na nusu ndio Pam anaamka kwa kukurupuka. Akakimbilia chumbani kwa Shema, hakumkuta ndipo akaangalia muda. Akatulia. Akaingia kuoga na kujisafi haswa, Mill hakuwepo. Akajua yupo kwake.

Wakati anatandika kitanda akagundua Mill aliacha ujumbe juu ya mto aliokuwa amelalia hapo. ‘Ukiamka, nipigie.’ Akampigia. “Nakuja twende tukapate kifungua kinywa kizuru ndipo tuanze fungate ya pili kabla ya kubwa ninayo kuandalia.” Pam akacheka na kuanza kubadili sasa ili apendeze.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda akaingia. “Naanza upya na wewe. Nahisi niliruka hatua moja. Nataka kuanza kukutoa kama wasichana wengine. Date. Tunaanza upya. Nakutoa kwa chakula, movie na mambo mengine mengi ndio tufikie pale tulipoachia.” Hatimaye kungojangoja kwa Pam kunazaa tunda zuri lenye ladha tamu isiyofifia. Alifurahi huyo mpaka usoni akaonyesha.

Mill alimvuta kupata kiss isiyo haraka. Pam akatulia akisikilizia ladha yake. Ni Mill. Akimuweka mikononi, hajiwezi. Alikuwa akisikia raha! Hajui afanyaje, maana alikuwa akimnyonya ulimi na midomo kwa huba! Kama amvue chupi, lakini akamuachia. “Nakupenda Pam, na hakika utajua nakupenda.” “Na mimi nakupenda Mill.” Akampa kiss ya juu ya mdomo. “Halafu umependeza sana.” Akamsifia akimkiss tena juu ya midomo, Pam akajua hapo njaa inamuuma, hakuna penzi mpaka ale. “Na wewe umependeza. Nisubiri nimalizie tutoke.”

Mill akamfuata chumbani. “Nashukuru kunisaidia Shema.” “Ahaaaa! Hakika naomba badilika jinsi unavyomkuza aisee!” Pam akakunja uso na kugeuka. “Atakuja kukwambia. Ameondoka amekasirika, na ameniambia eti yeye kesho anataka aandaliwe na mama yake.” Pam akaanza kucheka.

“Kwa nini?!” “Eti yule baba mtu mzima, anataka kwanza eti yeye wakati akioga, akute nguo zake kitandani! Safi, zimenyooshwa, zinamsubiria yeye mpaka boksa!” “Sasa, kumbe!?” Pam akashangaa. “Kwani yeye hana mikono! Yaani eti nimemkuta ametoka kuoga amesimama chumbani, ananiuliza, ‘mbona hakuna nguo kitandani!’ Namuelekeza zilipo, ananiambia, ‘Mama anahakikisha kila kitu kipo kitandani. Nikitoka kuoga, nikuvaa tu.’ Nikamwambia sasa nishamuonyesha, achukue avae, akaanza kulalamika. Eti yeye mama yake huwa hamfanyii hivyo.” Pam akazidi kucheka.

“Tena anasema, ‘mama yangu.’ Yaani kama mimi simfahamu huyo mama yake. Haya, hapo tukasumbuana, tukamaliza. Tukaja kwenye chai. Nimemuwekea mezani, namwambia mbona hali, anasema sijampoozeshea!” Pam alicheka mpaka machozi. “Nikafikiri sijamsikia vizuri. Nikamuuliza. Akasema yeye mama yake anampoozeshea kwanza, ndio anampa. Yeye hawezi kunywa, anaogopa kuungua! Nikampa kikombe cha pili. Maana hapo alikuwa kashanikera. Ananiambia, mama yake hataki ajipoozeshee. Namuuliza kwa nini, anasema ndio mwanzo wa kujiunguza, ampe huyo mama yake majonzi. Halafu eti, anaweza jichafua, ikaanza kazi ya kutafuta shati jingine!” Pam alikuwa akicheka mpaka akakaa.

“Namwambia mimi namuamini kuwa ni mkubwa, hatajiunguza. Eti ananiuliza na akijiunguza nitamwambia nini mama yake. Aisee aligoma kunywa chai. Akasema ni bora aende shule bila kula, asije akampa mama yake majonzi. Namwambia mimi nitamuelekeza, akakataa. Halafu ananiuliza sasa nitamwambia nini mama yake, akijua amekwenda shule bila kula! Maana mama yake anamwambia akiwa na njaa, hawezi kujifunza vizuri. Haya nikapoozesha nikampa, akala.”

“Namwambia aharakishe dereva ashafika, ananiambia yeye mama yake huwa anawahi kumuamsha, ili apate muda wa kutosha wa kula, na hajawahi chelewa shule. Nikanyamaza maana alishanikera. Ananitishia mama, wakati mwenzie yatima. Haya, tukaja kwenye kuvaa viatu. Bwana yule mtoto hajui kufunga kamba za viatu kabisa! Nikaanza kumgomea. Namwambia aende hivyohivyo. Akaniambia kuna hatari ya kukanyaga zile kamba na kuanguka. Eti sasa mimi nitamwambia nini mama yake akiumia!” Pam alikuwa akicheka mpaka machozi.

“Ukamfunga?” “Nifanyaje? Nikamfunga huku namwambia akirudi lazima ajifunze. Ndio akaniambia yeye kesho anataka kuandaliwa na mama yake. Na mimi nikamwambia hakuna tena kuandaliwa na mtu. Nitakuwa namsimamia ajiandae mwenyewe, yeye mkubwa. Ndio kaondoka amenuna. Sasa akirudi hapa, na wewe usianze kumbembeleza. Mwambie kuanzia leo mimi nitakuwa nikimuandaa. Lazima akue.” “Acha kumpania bwana! Taratibu, hatua kwa hatua. Hutaki wewe ndio akufanye adui. Tufanye kwamba mimi na wewe tunasimama sehemu moja. Hata kama na mimi namwandaa, nianze kumfundisha kujitegemea ili msitengeneze uadui.”

Adhabu yeyote kutoka kwangu, ataichukulia kwa upendo. Lakini ikitokea kwako mtatengeneza uadui. Wewe niambie vile unavyotaka, halafu mimi nitaanza kumnyoosha taratibu. Tusimfanyie mabadiliko mengi, kwa wakati mmoja.”

Tumemuhamisha kule kwenye ule mtaa ambao ndio amekulia kule. Wale watoto wa pale mtaani wamemzoea na yeye anawapenda kama moja ya familia. Najua itakuja kumuumiza tu akitulia na kujua hawezi rudi tena kule. Halafu tumehamia huku kwako ambako tena mnakwaruzana! Tukimfanyia mabadiliko mengi kwa wakati mmoja, tutamuumiza na wewe atakuona adui wakati najua unakusudia mazuri kwake.” Hapo Mill akatulia akijua ni kweli.

“Nakushukuru kunifikiria Pam. Kweli sitaki mwanzo mbaya na yeye. Asijeona mimi ni tatizo. Ila lazima tutekeleze bila kuzembea. Ndio mzaliwa wangu wa kwanza huyo! Sitaki akue kizembe.” “Atabadilika tu wala usijali. Si mkorofi hivyo, ila hajui maisha mengine ila hayo tumeishi naye. Na wakati mwingine nilikuwa nikifanya kuokoa muda au kuepusha garama za hospitali kwa ajali zisizo lazima au ninazoweza epuka, lakini si kumdekeza.”

Kifuniko Kinapopasuka, Kweli Yabaki Wazi

          Ndiyo yaliyokuwa yamempata Pius. Ilikuwa kama anaondolewa ukungu machoni nakuona yote ya mkewe kwa wazi kabisa bila kificho. Alikuwa kwenye hali ambayo hawezi mueleza mtu akaelewa. Ila kwa kuwa hakuwa amekula tokea jana yake usiku, na Pius ni kama huyo mwanae Ayvin, hawajiwezi kwa njaa. Alipofika tu hapo mgahawani akaagiza chakula kizuri tu akabaki akiwaza akiwa anasubiria chakula, mpaka kikaletwa. Akamuona Sonia na watu watatu wanakaa meza ya pembeni yake wala si mbali na yeye. Na wao wakaagiza chakula. Hawakusemeshana. Ila yeye Sonia na hao askari kanzu waliendelea kuzungumza yao kama wanao fahamiana kwa karibu tu.

Chakula chake kikaletwa, akaanza kula taratibu tu akiangalia muda. Bila ya kuchelewa, Raza akawasili akionekana na hali mbaya mpaka usoni. Pius akamtizama wakati akivuta kiti akikaa mbele yake.

Akamwangalia alipokaa huku akiendelea kutafuna. Raza akameza mate na kuanza. “Kuhusu swala la Chezo…” Pius akamtizama na kumuwahi. “Najua umejiandaa kwa UONGO mwingi tu. Ushajipanga na kujua nini chakuniambia. Usipoteze muda na usiniudhi zaidi. Nyamaza kabisa, mimi ndiye niliyekuita hapa.” Raza akatulia.

Pius akaendelea kula. Kimya. Raza akitetemeka mpaka tumbo lake lilikuwa likisikika likiunguruma kama mvuvi kwenye mtumbwi, katikati ya bahari, dhoruba ikipiga chombo chake, hajui anatoka vipi.

Baada ya muda akamwangalia. “Bila maneno mengi, nataka unijibu, ni umbali gani kutoka hapa, mpaka kwa Katibu, mganga wako.” Mwisho wa uwongo ni kilio cha moyo, kwani ukweli unaibuka kama jua kuteketeza giza la udanganyifu. Raza alitamani ardhi ipasuke aingie humo ndani. Akabaki ameganda, kama sanamu. Maana lilikuwa swali la moja kwa moja, hakuna kuzunguka.

“Nakuuliza Raza, kutoka hapa, mida hii, mpaka kwa mganga wako, itachukua muda gani? Na uongo si muda wake. Zaidi sasahivi. Hutafurahia endapo utanidanganya kwa lolote lile, maana tunakwenda wote sasahivi.” “Inategemea.” Ndilo aliloweza kujibu Raza. Pius akabaki akimtizama huku akitafuna. Kimya.

“RAZA?” Akamuita kwa ukali mpaka Raza akashituka na watu kuwageukia. Na hapo ndipo alipoiona hasira ya mumewe. Chuki iliweza kuchomoza kutoka kwenye vipande vya moyo uliovunjika, kama mchanga mkali unaotoka kwenye glasi iliyopondeka. Hapo Raza aliogopa zaidi. “Inategemeana na foleni.” Akajibu kwa haraka. Pius akaendelea kula mpaka akamaliza, Raza amekaa mbele yake akishindwa hata kujisogeza hapo kitini.

Kifo Cha Kivuli Kibaya

Alikula na kunywa kinywaji chake mpaka akamaliza. “Mwaga kila kitu kilichopo kwenye pochi yako, hapo mezani.” Raza akabaki akitetemeka, pochi bado ipo kwapani amening’iniza begani. “Namaanisha sasahivi. Na utoe vitu vyote mpaka kwenye zipu za pembeni ya hiyo pochi. Weka hapo mezani.” Akaanza kutoa simu. “Unanichelewesha Raza. Nimekwambia mwaga na kung’uta. Au unataka nimuite mtu akusaidie?” Kwa hakika Raza alishindwa. Ndipo akaamini kweli kuna anavyoweka humo ndani na kutembea navyo kama ulinzi.

“Nipe hiyo pochi.” Raza akabaki ameshikilia pochi yake. Pochi yenyewe ilionekana ya thamani SANA. Nzuri, classic. “Raza? Sitajirudia tena. Nipe hiyo pochi. Maana sitaondoa gari yangu hapa kuongozana na wewe ukiwa unazungukwa na madudu uliyopewa na mganga wako.” Akabaki akimtizama Pius akitetemeka. Pius akasimama na kuivuta kwa nguvu, kisha akamwaga mezani.

Yaliyotoka humo, usingedhania kama yanatoka kwa mrembo kama Raza. Maana hapo kwenyewe Raza alikuwa amependeza! Nadhifu! Anavutia kwelikweli. Hapakuwa na ubishi kama ni mke wa Pius Ruhinda. Yeye mwenyewe ni msomi anafanya kazi ya maana, mshahara mzuri. Halafu alijiweka kisomi haswa. Amejipangilia juu mpaka chini. Gari aliyeegesha hapo nje, ilitangaza utajiri usio kificho. Kwa kumwangalia tu, usingedhania vilivyopo mezani ni vyake. Pius mwenyewe alishituka mpaka akaruka pembeni akibaki akikodolea macho kwa hofu.

Sonia akasimama. “Naomba kijana wangu achuchukue picha na video, nataka ushahidi wakueleweka.” Raza akageuka asielewe. Walishavuta macho na masikio ya watu hapo kwenye huo mgahawa wa maana haswa. Kijana wa Sonia akapiga picha na kuchukua video mpaka akaridhika, Raza akiwa amekaa vilevile.

“Naona kwa hapa, kwangu inatosha. Anaweza tu rudisha kwenye pochi.” “Rudisha madudu yako.” Mumewe akamuamuru akiwa amesimama pembeni kabisa akiogopa hata kusogea. “Na akimaliza naomba mimi nitunze hiyo pochi kama ushahidi mbali na hizo picha.” Sonia akaongeza na kumshangaza Pius.

“Kwamba ukae nayo hayo madudu!?” “Oooh yeah! Itanisaidia ushahidi huko polisi.” “Huogopi!?” Sonia akacheka. “Hakuna silaha itainuka kinyume nami ikafanikiwa, Pius. Mimi nalindwa eti.” Sonia akajibu kwa kujiamini, Pius amesimama pembeni kwa hofu. “Na kama anashindwa, naweza kumsaidia kukusanya.” Sonia akaongeza. Raza akakusanya kwa haraka na kurudisha ndani ya pochi yake.

“Huwezi chukua pochi yangu.” “Usinitanie Raza. Mpe hiyo pochi.” “Sasa yeye inamuhusu nini?” “Nitakwambia tutakapotoka nje. Lakini hutashikilia tena hiyo pochi.” Sonia akamjibu. “Na wala simu. Vyote vitabakia ndani ya hiyo pochi.” Akaongeza Pius hapo kwa Sonia.

Mmoja wa wale askari kanzu akachukua pochi kwa Raza na kumtaka asimame. Wakatoka hapo kwenye eneo la watu la bishara huku Pius akiomba radhi kwa wateja wengine kwa kuwabugudhi.

~~~~~~~~~~~~~~

“Sasa, utaongoza njia mpaka kwa mganga wako. Na nakuonya Raza, usifanye mchezo wowote huko barabara. Hakikisha hupotei njia. Wote hao wanamajukumu yao, hakuna mwenye muda wa kupoteza. Fanya ili kufupisha hii safari. Na mkifika mimi ndio nitazungumza na mganga wako si wewe.” Hakujibu.

Wakamuingiza kwenye gari yao wake askari kanzu, safari ikaanza. Wao wapo mbele, Pius kwenye gari yake, na Sonia akiwa na kijana wake kwenye gari ingine wanafuata nyuma.

Mganga wa Raza alikuwa akiishi mbali na jiji. Mkadini, panapakana na Chalinze na Bagamoyo. Mpaka Pius akashangaa. Walikaza mwendo wakifuatana hayo magari matatu bila kuruhusu gari yeyote katikati yao. Waliacha lami na kuanza kufuata barabara ya vumbi. “Mbali kote hivi, huyu alikuwa akija muda gani!?” Pius akajiuliza akiendelea kufuata nyuma ya gari iliyombeba mkewe, mpaka kwa huyo mganga. Ilishakuwa saa kumi jioni.

Walipofika Pius hakuamini. Kijumba chenyewe kimechoka! “Unauhakika ni hapa?” Kabla Raza hajajibu Katibu mwenyewe akatoka. “Kwema Raza?” Akamuuliza kwa kumtambua kabisa, Pius akamuwahi kabla hajajibu.

Machozi ya Mwisho ya Shetani

“Mpaka mawasiliano yako ya mwisho na Raza ya jana usiku, akikulalamikia juu ya dawa zako kutofanya kazi kwangu, maana nimempokea mtoto wangu, na naonekana kumkubali si kama ulivyomuahidi. Na akikuuliza njia gani nyingine atumie maana kwa mara ya kwanza nimekataa kula chakula alichoniwekea ambacho kilikuwa na dawa ulizompa WEWE, na mengineyo ambayo najua unayajua nazungumzia nini, sitaki kujirudia na kupoteza muda, mawasiliano yenu NINAYO.” Katibu alishituka sana.

“Sasa nakuonya kama nilivyomuonya mteja wako hapa, usinidanganye na kunipotezea muda. NATAKA upindue yale YOTE uliyoyafanya kwangu, tokea mwanzo wako na Raza na..” “Kwamba unataka kuanzia tokea hujamuoa?! Maana hapo itakugarimu sana.” Pius akazidi kushituka.

“Kwamba huyu ameanza kunileta hapa KWAKO kabla sijamuoa!?” Hapo Katibu akajua ameshamwaga mchele kwenye kuku wengi. Alidhania Pius anajua yote, kumbe ya nyuma yeye hakuwa akiyafahamu ndio anatoa siri.

“Wewe Katibu? Inamaana huyu ananifanyia haya mambo tokea sijamuoa?” “Wala si tokea zamani, ni kipindi hicho nilipokuwa tukitafuta mtoto wa kiume, ndio nikaelekezwa kwake kuwa atanisaidia kupata mtoto wa kiume. Ndio…” “Unaanza kudanganya Raza, na nitakuumiza hapahapa. Nilikwambia nini?” Pius akamuuliza kwa ukali.

“Hapa nazungumza na yeye, kwa nini wewe unaingilia? Hicho unachozungumza sasahivi najua ni sababu uliyotengeneza ukiwa njiani tukija hapa maana hukuwa ukijua kama nakuleta hapa mpaka tulipokutana pale mgahawani. Sasa nakuonya Raza. Nyamaza.” “Aisee kweli! Kumbe wewe unamjua mkeo. Maana Katibu amesema kwa wazi kabisa ni tokea hujamuoa, yeye ashatengeneza uongo unaofanana na kweli!” “Na kwa taarifa yako, nilishajua kama ulinifanyia mauchawi yako ili nikuoe. Nilinyamaza, sikukuuliza kwa kuwa kwa wakati huo sikuona ubaya kwako. Kwangu ulijionyesha ni mwanamke wa kawaida tu. Nikajiambia japokuwa ulinifanyia mambo yako, sina nilichopoteza. Nilitaka mke, nikakupata wewe!”

“Sasa badala utulie ukiwa ni mke wangu. Sina ubaya na wewe Raza. Nakutunza bila hata kukuuliza pesa yako. Nakupa unachokitaka na bad…” “Unajuaje kama na hayo yote unayomfanyia ni moja ya uchawi wake ili umpe anachotaka?” Mmoja wa askari kanzu akamfanya Pius azidi kuogopa.

“Wala sijamfanyia hivyo. Amekuwa akinipa kwa ridhaa yake.” Raza akakanusha. “Tutajuaje kama ni kweli kwa mtu uliyemloga mpaka akakuoa? Kama umeweza kumfanya akuoe kwa sababu zako, utashindwa vipi kuhakikisha hizo sababu zinatimia?” Mwingine tena kamuuliza. Pius alishajisogeza mbali kidogo ya Raza kama aliyeingiwa hofu naye.

“Mimi napenda jinsi Pius anavyoendesha haya mambo. Tafadhali usipotee kwenye Lengo Pius. Rudisha akili kwa Katibu.” Sonia akaweka msisitizo. Yupo kikazi. Anachotaka ni ushahidi. Na kijana wake aliendelea kuwachukua video bila kuwafanya wakajua.

Pius akajaribu kutulia, nakuendelea. “Sitajali unarudia umbali gani. Nataka kuanzia ananileta hapa kwako unifanyie anachokitaka mpaka jana usiku. Yote uliyoyafanya, nataka tuingie wote humo ndani, uyapindue. Na ndipo uje kwenye swala la kijana yangu. Hayo majini mliyoyatuma kwake, yakamuharibu sijui kumuangamiza, uyaite mbele yangu, yarudi na kumuacha mwanangu huru. Unanielewa Katibu?”

“Sasa yote hayo unayotaka nikufanyie ni lazima kuwe na damu. Siwaoni hapa hata na jogoo!” Mpaka hapo Sonia akawa amepata UKIRI wa Katibu. “Maana kwenye kila jambo ninalofanya lazima agano la damu. Na Raza anajua kabisa. Iweje leo aje mikono mitupu? Makubaliano yetu ni afike hapa siku ya jumamosi na kila nilichomuagiza.” Sonia akatoa zile karatasi za jumbe za Raza.

“Ulimuagiza lini?” “Jana. Na akaahidi ataleta kila kitu siku ya jumamosi bila kukosekana kitu. Sasa kwa kuwa tunaanzia mbali, na ni kama tunatengua kila kitu, lazima kutuliza mizimu. Hivyo nilivyomuagiza hapo lazima kuongeza na mbuzi, tena beberu.” Sonia akarudisha macho kwenye mawasiliano yao. Akasoma na kumuonyesha Pius na yeye akasoma na kutingisha kichwa kwa masikitiko.

“Yote hii ni pesa yangu unachukua na kutumia kunifanyia mimi mwenyewe uchawi! Yaani unatumia pesa yangu kwa kuniangamiza mimi na kijana wangu!” Pius akaongea kwa uchungu sana akilalamika. Raza kimya.

“Huwezi pokea pesa, taslimu?” “Beberu ni lazima ili mizimu inywe damu kuituliza. Ukishafanya nao agano, huwezi badilisha hivihivi.” “Naomba tuzungumze hapo pembeni, Pius.” Sonia akamgusa Pius.

~~~~~~~~~~~~~~

Akajivuta pembeni kabisa na Pius. Akaridhika hawatasikika. “Nisikilize Pius. Sijui unapotaka kuelekea, lakini agano la damu ni halisi. Utakapotoa tu hivyo vitu ili wafanye kafara, yakubatilisha hayo mambo yao, jua wazi umejiingiza kwenye mkataba nao, hutatoka. Huwezi jua na Raza naye alianzia wapi mpaka kujikuta anaendelea naye. Sijui kama unanielewa?”

“Hawa watu wamefanya mambo mengi sana kwangu, Sonia! Na umeona ahadi aliyompa Raza. Kwamba wameshatuma mashambulizi kwa kijana wangu. Wanasubiri tu kukutana, aletewe hivyo vitu wahitimishe.” “Naelewa. Ila nataka na wewe uelewe hivi, kamwe hutamshinda shetani kwa kutumia nguvu zake. Huwezi na hakuna aliyeweza mshinda shetani kwa nguvu za giza maana ni zake.”

“Ninapokwambia Mungu ni muweza, nina uhakika naye kwa KUMTHIBITISHA mimi mwenyewe kwa kuona si kusimuliwa. Hayo yote uliyofanyiwa wewe na kijana wako, anaweza kukurejeshea tena maradufu, halafu bila DENI.” Sonia akaendelea.

“Yule binti niliyekwambia alimloga dada yake na shemeji yake, alianza kwa kusaidiwa hivyohivyo na mganga, lakini na yeye alimuendesha haswa. Akamlazimisha kuja kulala naye.” Pius akashituka na kumgeukia Raza kwa sekunde kadhaa.

“Na dada mwenyewe ni mzuri haswa, msomi anayejielewa. Lakini mganga akawa akimtaka kimapenzi huku akimtisha. Yakaendelea hayo mpaka akaja kumpa mimba.” Pius akazidi kuingiwa hofu.

“Shetani hana zawadi ya bure Pius. Ila Yesu ninayekwambia atakupa uzima. Atakuweka huru na kukurejeshea uliyopeteza bila kukudai ila kukutaka tu mahusiano naye tena bila kukulazimisha! Achana na haya. Yatakurudia na kukutesa sana.” “Sasa tutafanyaje? Natamani walipe kwa waliyonifanyia.”

“Sasa wewe endelea na msimamo huuhuu. Nenda naye hivyohivyo kama unataka akufanyie. Mwambie upo tayari kumlipa pesa yeyote ile, na tutawatuma wale askari wakalete huyo beberu. Atakubali kwa haraka na kukutajia pesa anayotaka yeye. Lakini wewe mwambie hutalipia hiyo pesa mpaka ujue anakuagua kwenye lipi. Kwa kuwa anajua unayo pesa, na Raza anaonekana alikuwa akimlipa bila shida, atataja kwa haraka. Akishataja ndipo tutamuweka chini ya ulinzi. Tunaondoka naye hapa ili asirudie kudhuru wengine.” Hapo Pius akakubali. Wakarudi.

~~~~~~~~~~~~~~

“Sasa Sonia amekubali kutuma vijana wake wakaniletee huyo beberu. Vingine umekubali iwe kwa pesa. Si ndivyo?” “Kabisa. Ila ujue itakuwa garama maana tunaanzia tokea mwanzo.” “Hamna shida. Ilimradi tu mimi na kijana wangu tupone.” Pius alionekana ametulia kabisa na anataka kufanyiwa na yeye.

“Kiasi gani?” Akamtajia mamilioni ya pesa akijua anayo tu, maana alimjua huyo Pius hata kabla hajafika hapo. Yeye mwenyewe tu na gari yake alitangaza utajiri. “Yote hiyo! Kwani unaniagua nini na nini?” Akaanza kumtajia kishawishi. “Tokea hamjaona, alitaka umpende yeye tu. Hapo kuna maagano yake. Kukurudishia fikra zako, hapo kuna maagano yake.” Pius akakumbuka dawa alizojuwa amewekewa chini ya mto anao lalia kila siku usiku. Akahisi pengine ndio kazi yake. Akazidi kuogopa.

Kukurudishia nguvu zako za kiume, ili urudi kuwa kama zamani. Sio mpaka Raza akufungue. Hapo napo kuna agano lake.” Pius akamtizama Raza, akainama. Akaendelea kumtajia mwanzo mpaka hapo kwa Ayvin akitaka kiwe kifo cha usingizini. Pius alikuwa akitetemeka baridi kama yupo kwenye friza.

“Na usifikiri hilo la mtoto kwa sababu hakuna kilichotokea ndio udhanie hakuna kilichofanyika! Nishatuma jeshi, tulikuwa tumalizie akija hiyo jumamosi. Kwa hiyo hapo nataka pesa kutuliza mizimu na kurudisha jeshi zima. Tena ujue hivyo nakupunguzia. Na Raza anajua bei zangu. Sifanyagi kwa pesa hizo. Nafanya kwa bei hii kwa kuwa nabadilisha alichokianzisha mkeo ndio maana unaona sianzii mbali na kuna punguzo la bei.” Akaongea mengi akijisifia asijue anamfunga Raza na kujifunga mwenyewe.

Mpaka hapo Raza hakujua kwa hakika kinachoendelea kati ya Sonia na Pius. Alijua ni kweli mumewe anataka kuaguliwa, afute aliyoanzisha. Alikuwa amenyamaza muda mwingi akishindwa hata kumtizama mumewe.

“Mimi naona nimetosheka Pius. Nipo sawa kabisa.” Sonia akafanya wamuangalie. “Unauhakika?” “Kabisa. Au unasemaje Zilo.” “Aisee nimewapata wote, tena vizuri kabisa. Kila mmoja na UKIRI wake. Hapa hutapata shida. Sasa tunaweza kwenda tu, ukaanze kazi.” Ndipo wote wakamgeukia huyo Zilo aliyekuwa akichukua video. Moja kwa moja Raza akajua amejifunga.

“Sasa mnaweza kuwachukua. Wote wawili.” Raza alishituka, asiamini kama mumewe anataka akafungwe. “Kwamba Pius unataka kunipeleka polisi kwa kuilinda familia yetu?!” Pius akashangaa sana.

Umechanganyikiwa Raza au na wewe haya madudu ya mganga wako yanakufanya hujielewi! Kwa haya uliyofanya mpaka sasa, unalinda familia ipi?!” “Mina amekuloga Pius. Ona ulipo, na vile anavyotufanyia kutusambaratisha. Muulize Katibu mambo anayoyaona kwa Mina, kila akiita jina lake!” “Sina muda huo.” “Kwa kuwa amefanikiwa kukufunga Pius! Mina ni mshirikina sana ndio maana unaona napambana naye.” “Unazungumza ni nini Raza wewe!? Kwani Mina amekuja kwenye maisha yetu lini na wewe umeanza kunifanyia haya mambo lini?” Kabla hajajibu akaendelea.

“Kwani Mina alikuwepo wakati ukitaka nikuoe?” Kabla hajajibu akaongeza. “Kwani Mina alikuwepo wakati unakuja hapa kunifunga nguvu za kiume?” “Hiyo ni kwa nia nzuri tu ulipokuwa ukienda huko kwenye safari zako za kikazi ili kukunusuru Pius. Watu wanatembea na vijidudu vya UKIMWI, kazi yao kusambaza.” “Kwa hiyo wewe kufanya umalaya ni ruksa, ila si mimi?” Hapo Raza akakwama.

“Unataka kuja kuwa mama wa namna gani kwa binti zangu wewe?” “Mimi napenda wanangu Pius. Na wewe ni shahidi.” “Kwa hiyo hizi ndio njia ulizokuwa ukiwafundisha wanangu muda wote?” “Sijawahi leta wanangu kwa mganga hata mara moja.” “Raza!?” Katibu akamuita kwa kumsuta.

“Sasa kuwazindika ndio…” Pius alishituka sana. “Kwamba hata watoto wangu umewafanyia haya mambo, Raza!?” “Ni kwa nia nzuri ili mtu asiwadhuru! Huoni walivyotulia, hawana hata mambo ya wanaume? Na darasani wanafanya vizuri.” “Naombeni mumtoe hapa haraka sana  kabla sijamjeruhi vibaya sana. Mimi nilikuwa nikifanya vizuri mpaka kwenye shahada zangu zote, mbona mama yangu hajawahi nipeleka kwa mganga?” “Nakuonya Pius, usiende kinyume na mimi. Utajuta.” Raza akamtisha. “Na kweli!” Katibu akaongeza kitisho. “Haya mambo hayaendi hivihivi! Unajidhuru zaidi, wewe mwenyewe.”

“Mtanifanya nini? Mtaniloga zaidi?” Pius akauliza kwa kuwadhihaki. “Upo chini ya maagano makali sana. Unaudhi mizimu na hawatakuacha hivihivi. Hakika utajuta.” Katibu akaongeza kama akimsihi kwa kitisho. Mkewe akaongeza kwa Katibu. “Wewe unafikiri umefika hapo ulipo hivihivi? Kwa kipi mno? Mimi ndiye niliyekuwa nikikusaidia ufike hapo. Bila mimi hata biashara zako zisingekuwa hivyo. Sasa usije fikiria umefika hapo hunihitaji mimi! Utarudi kuwa chini kabisa. Muulize Katibu jinsi anavyokusaidia. Maana wewe umeshikilia upande mmoja tu, wa huyo Mina, hujui upande mwingine.” Pius alibaki akimwangalia mkewe kama ameona msukule.

“Nafasi ZOTE huko ofisini ulizokuwa ukishika ni juhudi yangu na Katibu. Kila mafanikio uliyo nayo usifikiri ni hilo jina lako la Ruhinda, ni mimi kuhangaika sana mpaka watu wanaona nyota yako. Lasivyo ungeishia vilevile kawaida. Na jua wazi, wewe si kitu bila MIMI. Sasa wewe kubali Mina akupotoshe uone yatakayo kutokea.”

~~~~~~~~~~~~~~

Nguvu ya mke aliyeishi naye kwa muda mrefu.

Alimjulia mumewe, alijua wapi pakumpata. Akatumia uzoefu wake kwake mpaka akafanikiwa kumuweka mumewe njia panda, kiasi cha kuona kila upande una kiza.

Kumuweka jela, ataharibikiwa, kumuacha uraiani hatari kwa wanae na wanao mzunguka.
Akaweza kupofusha fikra nzuri zilizoweza kutoa ushahidi mgumu mpaka Sonia akamsifia, lakini kwa sekunde chache Raza akafanikiwa kumuwekea hofu isiyosemeka.
Akamfanya kuanza kufikiria kila hatua kuanzia hapo.

Kwa mara ya kwanza akaanza kutilia shaka juhudi zilizomfikisha hapo alipo na mafanikio yake yote anayosifiwa nayo.

Mapigo ya moyo ya Pius yalikuwa yakipigana na akili, gafla akabaki mwenye hofu mbele ya Raza na Mganga wake.
Kwa muda mfupi Raza kuzungumza naye, akimjua mumewe, kwa yale apendayo, KAZI YAKE na MAFANIKIO yake yote zikiwepo biashara zake, alifanikiwa kumfikisha kwenye bahari yenye mafuriko, anatapatapa akitafuta kisiwa ambacho kweli hakipo.

Ni kweli mafanikio yake yote yameshiliwa na Raza?

Akimuweka jela na KUHARIBIKIWA kikazi na kibiashara je?

“Kweli nianze moja!?” Pius akabaki akijiuliza akiwa njia panda amejawa hofu.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment