Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 54. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 54.

“Nilitaka tukishapata chakula tukamalizie kununua vitu vya humu ndani.” Pam akanyamaza. “Pam?” “Havina haraka, vinaweza subiri.” “Sasa mtakaa wapi hapa? Hata hiyo chai mtakunywa mmesimama?!” Ndio akakumbuka na kuanza kuangaza macho. Hapakuwa hata na stuli. Akatulia.

Ila kwa kuwa alikuwa amekasirika akamjibu, “Sisi tutakuwa sawa.” Akaendelea kusaka sufuria. Akagundua hata jiko hana. Mill amesimama anaangalia. Akageuka. “Naomba nikalie na Shema mara moja naenda kutafuta jiko.” “Sasa kwa nini tusiongozane wote tukaenda kula na kufanya manunuzi mengine?” Akaondoka kurudi chumbani bila ya kumjibu. Akamfuata.

Unanichukia bure mimi, malaika wa Mungu. Shida yangu ilikuwa kupendwa tu. Lakini sasahivi lawama zote ni mimi! Lakini mkubwa jalala, nakubali makosa. Naomba weka hasira zote pembeni, tufanye mambo ya msingi.” “Nataka kubadili nguo.” “Nakuahidi sitakuangalia.” “Mill! Toka bwana!” “Hakuna pakwenda kukaa!” “Huna lolote, wewe unataka kuchungulia tu. Toka bwana!” Akaanza kucheka.

“Hakika kungekuwa na makochi, ningetoka.” “Basi nenda chumbani kwa Shema.” “Pam amekosa imani na mimi! Mbona mwanzo umevaa hapa kila kitu na nilikuwepo?” “Ulikuwa kwenye simu, na nikajua mawazo yamezama huko. Hapa sasahivi umenisimamia na unajua kabisa nabadili nguo, macho yatashindwa kujizuia.” “Nitayakataza.” “Hapana. Ondoka. Wewe unataka kuchungulia wanawake wangapi kwa wakati mmoja? Toka.” Hapo akatoka kimyakimya. 

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda akarudi na vyakula. “Muwe na siku njema.” Akatilisha huruma mpaka kumshangaza Pam. Ile jeuri wanayowekeana ni kama ilipungua. “Wewe umeshakula?” “Mimi kula wimawima siwezi. Acha niwaache tu.” Pam hakumjibu, kweli akaondoka. Akala na mwanae, wakajikuta wamelala kitandani kwake mpaka jioni, aliporudi.

Pam akatoka kitandani na kwenda kumfungulia. “Nimewaletea tv na meza ya kulia chakula.” Pam hakuamini. “Pole Mill! Mimi nilijua umekwenda kupumzika!” “Acha waingize ndani na kukupangia kabisa. Hii tv naiweka chumbani kwako mpaka utakapoenda kuchagua makochi unayopenda. Sikutaka kukuchagulia kitu ambacho hutapenda.” “Nakushukuru sana.” Wakawawekea kila kitu. Hakukaa, maana hapo alikuwa akitokwa na jasho haswa. Hata hivyo Pam alijua anajikaza tu. Mill hapendi joto kabisa.

Akaaga bila maneno mengi. “Dereva atakuja kumchukua huyu asubuhi. Muwe na usiku mwema.” “Na wewe.” Akaondoka. Hakumsikia tena siku hiyo hata kwa ujumbe wa usiku mwema. Akajua yupo na Brenda akaona ajinyamazie tu.

Jumatatu Baada ya Kuhama.

Kama kawaida akaamka kumsaidia mwanae kujiandaa, alipokuja kuchukuliwa, na yeye akaondoka kwenda kazini. Siku ikaanza kama kawaida. Upande walipo wao sio wa wagonjwa. Kumetulia. Kila mtu na kazi yake. Hakuwa amemuona Mill tangia amefika. Ila ni kawaida. Mill huwa ofisini kwake muda wote ni mpaka awe anatoka au akuite ofisini kwake ndio kumuona. Sasa aliyemkuta hapo huyo muhasibu ndiye aliyekuwa akizungumza na Mill mara kwa mara na kumpa maagiza Pam, kwa hiyo hawakuwa na sababu ya kuonana hapo kazini. Kwanza ni kama hawakuwa wakifahamiana wanapokuwa hapo kazini.

~~~~~~~~~~~~~~

Muda wake wa kwenda benki ulipofika, akatoka. Alipofika huko akamtumia ujumbe Mbise, muhasibu wa hapo kazini, ambaye ndio kama bosi wake. ‘Nitarudi baada ya muda wa chakula, kuna mtu nakutana naye kwa chakula cha mchana, ila sitachelewa.’ ‘Leo naona mambo yako si mabaya.’ Akamtania kwa sababu hakuwahi kutoka kwenda kula, hula hapohapo. ‘Acha hizo.’ Akamalizia hivyo, akaendelea na yake.

~~~~~~~~~~~~~~

Sasa huku nyuma ikawa hekaheka. Pam harudi. Kumbe yeye Mill anamfuatilia. Anajua anatoka muda gani na anao rudi. Akaanza kuangalia saa, Pam harudi. Uzalendo ukamshinda. Akamfuata Mbise. “Umemtuma wapi Pam?” “Benki tu.” Akaangalia saa hapohapo mbele yake. “Benki mpaka sasa?!” Mbise akakumbuka. “Aaah! Nimekumbuka. Aliniambia atapitia kula kabisa.” Akaangalia muda unakaribia wa chakula cha mchana. Akatoka.

Baada ya dakika tano akarudi ofisini kwa Mbise. “Amesharudi?” “Bado.” Akaangalia tena saa yake ya mkononi, hapohapo mbele yake, akatoka. Akaenda kukaa ofisini kwake kama dakika 10 nyingine, akarudi tena. “Amesharudi?” “Hapana Kiongozi.” “Kwani huko benki ulimtambulisha kwa watu wa namna gani? Isije kuwa ni wahuniwahuni wakaanza mambo yao ya ajabuajabu!” Wivu.

“Ni walewale wa siku zote. Tunaheshimiana sana. Labda atarudi baada ya muda wa chakula. Maana huu ndio muda wenyewe wa chakula.” Akaangalia tena saa, na kuondoka. Mbise akaangaliana na mfanyakazi mwingine.

“Kwema!?” “Naona Pam ana bahati mbaya! Siku ya kwanza kutoka ndio anahitajika kweli!” “Labda umpigie umshitue.” “Kama yupo na mtu wake je? Mimi niingilie, si nitaonekana hovyo!” Kama aliyekuwa mlangoni, akarudi. “Mtu wake! Mtu gani?! Maana Pam ni mama watoto wangu!” Ndio kila mtu akashangaa mpaka Fatma aliyekuwa mapokezi alisikia. Wote wakatega sikio vizuri.

“Kwa hiyo kama kuna linalo endelea, ningependa kufahamu. Unanisikia Mbise?” Akamjia juu Mbise. “Maana wewe ndio upo naye ofisi moja. Na ndiye uliyekwenda kumtambulisha huko. Isijekuwa umemtambulisha kwa watu walio anzisha jambo la tofauti kwake badala ya maswala ya kazi tu.” Mzee akang’aka. “Kwakweli sifahamu Kiongozi. Kwanza hajawahi toka kwa chakula cha mchana, yaani leo ndio kwa mara ya kwanza ametoka!” “Ndio amekuaga anakutana na mtu muda huu?” Hapo Mbise akaona atakuwa amezua janga.

“Pengine sikuwa nimemuelewa vizuri. Ila nina uhakika alisema leo atakula kabisa hukohuko ndipo arudi.” “Alikwambia kwa njia ya simu au ujumbe?” Mbise akajua amekamatwa. Kabla hajajibu akaongeza. “Naomba kuona huo ujumbe.” “Labda akirudi nitakujulisha Mkuu.” “Screen short mazungumzo yenu juu ya kuchelewa kwake, unitumie sasahivi.” Akatoka amepaniki kwelikweli.

~~~~~~~~~~~~~~

Wasijue huwa ana udhaifu wa miguu ya Pam na ile rangi yake. Sasa huwa anajua muda wa Pam kufika kazini. Hufungua pazia za ofisini kwake kusudi ili kumuona anapopita akiingia hapo kazini na muda anaotoka hapo ofisini. Sasa siku hiyo Pam alivaa gauni jeusi, fupi mpaka katikati ya magoti, halafu likamshika. Ni la kiofisi na alimnunuliaga yeye mwenyewe Mill, zamani akifanya kazi kwa Sandra. Lina zipu nyekundu moja mgongoni, ndefu kuanzia juu mpaka chini kabisa kama ndilo linalounganisha hilo gauni.

Akitembea kiungo cha mguu, gotini mpaka chini vinaonekana. Mill huupenda SANA mguu wa Pam. Hata kwenye romance ilikuwa lazima aushike kwa kupapasa, humpa mzuka zaidi na hapo atafanya naye mapenzi kwa kufurahi mwanzo mwisho. Mguu wa Pam!

~~~~~~~~~~~~~~

Sasa kile kigauni na ile rangi, Pam aliwaka haswa halafu kilimkamata vizuri, umbile lake ambalo ndio udhaifu zaidi wa Mill, ikawa bayana mpaka kina Mbise walipiga miluzi alipoingia asubuhi hiyo. Na kwa sababu hutembea kutoka kituoni mpaka ofisini na nyumbani mpaka kwenye daladala basi huvaa viatu vya chini, ila akifika ofisini hubadili na kuvaa vya juu.

Sasa siku hiyo akavalia kiatu cha juu chekundu kama hiyo zipu huko mgongoni. Bwana Pam alipendeza! Napo pia Mill alimchungulia alipokuwa akienda benki. Hapo alikuwa amepandwa na mzuka, hawezi kukaa chini.

Halafu mbaya zaidi, huyu Pam alishaacha kujali maswala yake na Brenda. Akamuonyesha hajali tena na kwake hataki tena kuhamia. “Ukute alishaniona mimi si kitu, kashamkubali jamaa mwingine huko, anaona kuhamia kwangu atakosa uhuru na mtu wake!” Akazidi kuwaza Mill akili zikienda kasi.

Akakumbuka vile Pam alivyomwambia hata Brenda anaweza tu kuja kwenye shuguli ya mtoto wao. “Yaani anikatalie, halafu baadaye akubali aje! Hapana, ipo namna. Huyu Pam ananitega tu. Alitaka Shema anione mimi na Brenda, mwanamke mwingine, halafu ili yeye akija sasa kumtambulisha mtu wake, iwe sawa!” Mill akazidi kuvurugwa mawazoni.

~~~~~~~~~~~~~~

Ikabidi Mbise apige picha ule ujumbe na kumtumia bosi wake kitu ambacho si kawaida na ndio wamejua yule mtoto anayekuja pale, akizunguka na Mill, ule weupe ni wa Pam. Maana hakuwa mgeni hapo. Mill alishamzungusha Shema kila mahali. Wanamfahamu Shema. Mbali na hapo, picha zake zimejaa ofisini kwa baba yake kama raisi wa nchi. Ofisi nzima kimya, wakiingiza taarifa za Pam, mama watoto wa bosi wao.

“Sasa na Brenda naye vipi?!” Fatma maneno mengi, sekretari wa ofisi, akawafuata na kuwauliza kimbea. “Hapo ndipo kitendawili!” “Sasa mbona Pam naye hata kutukonyeza!” “Kama hujamgundua Pam ni msiri sana.” “Lakini si kwa jambo zito hivyo bwana! Hata kujishaua kama na yeye mama bosi!” “Sasa leo hapa, pashawaka, Fatma. Utakutwa humu ndani, utamtibua zaidi.” Vile Fatma anarudi mapokezi, Mill naye anarudi kwa Mbise akiwa amemchanganya zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~

“Kwamba Pam anakutana na mtu kwa chakula cha mchana! Kwamba ndio wamefika mbali hivyo! Ukute inabidi kukutana mchana na kufanya mambo yao, kwa sababu nishapajua walipohamia, na nilishamkataza asilete mtu alipo Shema. Mwanaume gani tena huyu, au ukute wamerudiana na Mgaya nini!” Ndipo kiti kikazidi kuwa cha moto na kumfuata tena Mbise.

~~~~~~~~~~~~~~

“Amerudi?” “Au labda nimpigie simu, nimwambie arudi.” Akamuona kama amesita. Halafu tena kama aliyeogopa! Mbise hakuelewa. Maana alifanya ikawa kama kosa, gafla akanywea kusikia apigiwe! Akaweka msisitizo. “Naweza mwambia arudi sasahivi.” “Hapana! Hapana! Huu ni muda wake wa chakula.” “Basi akirudi nitamwambia kama ulikuwa ukimtafuta.” Akamuona ameshituka tena.

“Hamna haja!” Akaondoka akiwa ametulia kabisa. Wakaangaliana na wenzie. “Ni nini kinaendelea!?” Wakanong’ona. Na wao wakaona watoke, wakatete vizuri huko kwenye mgahawa wa hospitali.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakaanza kucheka. “Ni kile kigauni tu, kampagawisha.” “Lakini hajamuona!” “Sasa wewe uwe na mali kama ile, usichunge? Atakua ashazoea hatoki, anayetoka ni yeye tu. Sasa leo mwenzie katoka, ndio wivu.” Wakaanza kucheka. “Sasa mtoto mtamu vile, anahangaika na makapi kina Brenda wa nini?” “Kwani na wewe Mbise unamuona Brenda ni makapi!? Bosi wa viwango!” “Huwezi mfananisha na Pam bwana!” Wakaanza kumchambua Brenda na Pam, wanacheka mbavu hawana.

Kuliko Ungua Mpini, Likabaki Shoka

Andy waliondoka na familia yake jijini wakiwa kitu kimoja na mipango ya KUANZA upya. Kulijawa na tumaini kwa wawili hao! Kitu kipya kikajengeka. Tena safari hii wakiwa makini wakijua hakuna kitu cha kudumu, wakati wowote walichonacho wanaweza poteza. Kukawepo na heshima na umakinifu ukajengeka kwa wote wawili.

~~~~~~~~~~~~~~

Haikuwa hivyo kwa Pius. Moyo wake ulikuwa umejuruhiwa vibaya sana na Raza mkewe. Kitendo cha kumfunga yeye nguvu za kiume halafu yeye ana mahusiano nje! Halafu mbaya zaidi kuhalalisha alichokifanya hadharani mpaka ndugu kujua na kuaibishwa kwa kiasi kile!

Alinyanyuka pale alipokuwa wameachwa wamekaa na mama yake. Akatoka kimyakimya na kwenda kuegesha gari Shoppers plazza. Akabaki garini akiwaza anayofanyiwa na mkewe. Na nini afanye. Alijua akimuuliza, asingekubali. Akabaki garini muda ukienda mpaka kwenye majira ya saa nne na nusu usiku binti yake alipomtumia ujumbe wakumtakia usiku mwema na kuwa anampenda sana. Akajua ndio anataka kulala. Akamjibu na kurudi nyumbani.

Isivyo kawaida, chakula alichokuta pale nyumbani kilimshinda kabisa kula. Alikaa mezani akikiangalia akishindwa hata kuweka mdomoni. Raza alikuwa sebuleni kwenye luninga akimsubiria ale. Huwa ni lazima chakula cha usiku awe anakula nyumbani na Raza alishazoea hivyo. Lakini siku hiyo alishindwa kabisa. Hakumsemesha sana Raza, akaenda kuoga na kulala.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake alitoka nyumbani akawahi ofisini kama kuripoti tu. Kisha akatafuta mawasiliano ya Raza. Akaomba kupakuliwa ya miezi sita nyuma. Jumbe na simu zake. Akapata na kwenda kukaa nayo sehemu na kuanza kusoma jumbe kuanzia za asubuhi hiyo kurudi nyuma.

Jasho lilikuwa likimtoka Pius kadiri alivyokuwa akisoma zile jumbe. Zilizomuuma zaidi ni zile za vitisho kwa kijana wake, na mipango aliyokuwa akifanya kwa siri juu ya huyo mtoto. Ni kweli Raza alikusudia kumuangamiza Ayvin. Bado Sonia alionekana hakuwa amemtafuta. Akajua Mina hakukosea.

Akarudi kwa upende wa mahusino ya siri aliyokuwa nayo. Walionekana ni wapenzi wa muda mrefu na walichofanya ni kubadili tu muda. Kutoka kukutana jioni mara tu baada ya kazi mpaka usiku, wafanyakazi hao waajiriwa, walikuwa wakikutana muda wa chakula cha mchana. Pius alikuwa akitetemeka mpaka baridi.

~~~~~~~~~~~~~~

Akafikiria chakufanya, akamtumia ujumbe Raza. ‘Leo badala ya kukutana na Chezo mida yenu ya mchana, tafadhali naomba tukutane.’ Raza alipopata huo ujumbe kutoka kwa mumewe, alikaribia kurusha simu. Alishituka, hakutegemea. Kisha akaongeza ujumbe wa pili. ‘Nitakutumia sehemu utakayo nifuata. Na Raza, nakuonya. Kutofika kwako kwa wakati, sehemu nitakayokwambia, kwa sababu yeyote ile utakayochagua wewe kuja nidanganya nayo baadaye, hutapenda matokeo yake. Itakuwa ni kunikaidi vibaya sana, maana ikiwa ni miahadi yako na Chezo huwa huchelewi. Sasa kwangu USITHUBUTU kufanya kinyume.’ Raza alikuwa na hali mbaya, alishindwa hata kujibu.

Kwa Sonia.

Wakati akisubiria muda wa mkewe kupata mapumziko ya chakula cha mchana akaamua kumtafuta Sonia ili azungumze naye. Sonia akawa muungwana kumsikiliza kwa upande wake. Akamkaribisha ofisini kwake. Alifika bila ya kuchelewa. Kwa Sonia alikiri kosa la kusababisha karaha kwa Mina ila hakukiri kosa la ubakaji wala hakuweka mazingira ya kutaka kuzungumzia hilo.

“Ukiniuliza kwa nini, sitakuwa na jibu zuri. Ila nakiri sikuweka mazingira mazuri tokea Mina anarudi na mtoto. Nilimpokea nikiwa na paniki huku na furaha ya kumuona mtoto ambaye kwanza sikujua kama alizaliwa au la. Kisha kuletwa akiwa mgonjwa. Wasiwasi wangu mpaka sasa ni kule kujiona ni kama nipo ndotoni, nahisi naweza kuamka na kujiona nilikuwa nikiota. Ndio kutapatapa kwangu.”

“Ila naahidi kubadilika. Nimefanya kosa, ila nakuahidi kuanzia sasa, nitakuwa makini kwa kila nitakachofanya ili kumfanya Mina na mtoto wangu watulie. Mimi mwenyewe nitaweka ulinzi kwao, nikitambua uwepo wa Andy.” “Hili ndilo nataka kulisikia.” Sonia akaonekana kuridhika.

“Sasa basi, NAANZA na Raza. Nimeona jumbe zake mbaya sana. Nimeweza pata mawasiliano yake yote mpaka na ya huyo mganga wake.” Sonia akashituka sana. “Kwamba ameshaanza kufanyia kazi!” “Kabisa. Hivi ninapozungumza na wewe, ninazo jumbe zake au mawasiliano yake ya mpaka jana usiku. Ameshamtumia mganga wake mpaka picha ya kijana wangu.” “Haiwezekani! Huyu aliyerudi na Mina juzi tu!?” “Nina mtoto mmoja tu wa kiume ambaye nimezaa na Mina. Kwa hiyo kujibu swali lako ni huyohuyo.”

“Tena simu yake ya mwisho kwa huyo mganga wake, japo sijui alizungumza naye nini ni usiku wa kuamkia leo. Jana niliwahi kulala kabla yake, na kwa mara ya kwanza sikula nyumbani. Pengine hilo lilimshitua.”

“Kwani yeye alishakutana na Ayvin? Namaanisha alipata wapi picha ya kumtumia mganga wapi au ndio kutoka kwa dada yako?” “Nina uhakika ni hivyo. Na yeye amepokea onyo lako, mbele yangu na wazazi. Sidhani kama atakuja rudia tena.” “Au wote wana njama ya kumuua kijana wako?” “Paulina yeye ni mchonganishi tu. Furaha yake ni hii hali iliopo sasa. Lakini si kuua kama Raza. Raza amefika mbali sana.”

“Turudi nyuma taratibu. Yeye aliyachukuliaje mahusiano yako na Mina? Nikimaanisha tokea mwanzo, hayohayo ya kishemeji! Maana Mina amekiri kwangu hapakuwa na mahusiano ya kimapenzi kati yenu. Ila ni jambo lililotokea katikati ya ulevi. Ila amekiri mlikuwa karibu sana, hata mida mwingine mlijikuta usiku peke yenu, na likawa jambo la kawaida hata kwenye familia yenu, watu wakijua ulikuwa ukiwasaidia familia ya mdogo wako!”

“Ni kweli hapakuwa na mahusiano mengine ila hayohayo yakatuweka karibu kwa muda mwingi.” “Hilo ndilo likaibua maswali kwangu. Mkeo alichukuliaje hilo? Kurudi kwako usiku, ukisema unatokea kwa Mina! Nikahisi pengine hilo ndilo lililo ibua chuki kwake tokea mwanzo. Lakini katika upelelezi wangi, ndipo nikaja kugundua kuwa na yeye anayo mahusiano yaliyokuwa yakimuweka nje mpaka usiku mwingi, kiasi cha kumfanya mke wa huyo jamaa, niliyetajiwa kwa jina la Chezo.” “Sawasawa.” Pius akaafiki.

“Alikuwa akilalamika kuwa mkeo, yaani Raza, anamchelewesha mumewe nyumbani.” Ndipo akagundua kuwa yeye ndiye aliyemwambia Mina habari za mahusiano ya nje ya Raza. “Cha kwanza, sikuwa nikikaa usiku mwingi hivyo kwa Mina. Nilikuwa nikijitahidi kurudi nyumbani muda mzuri tu, maana chakula cha usiku mara zote inakuwa ni lazima nile nyumbani, na Raza ndiye aliyekuwa akindaa mara anapotoka kazini.”

“Huwa akitoka kazini lazima arudi nyumbani. Tuna binti bado anaishi nyumbani. Lazima kuzungumza naye na kuangalia kazi zake za shule. Na yeye lazima kusimamia chakula cha usiku. Ndipo anatoka sasa kwa starehe. Na mara nyingi ilijulikana anakuwa na hao rafiki zake. Ni kama wana kikundi chao. Basi hukutana sehemu, au niseme club kwa kula na kunywa. Huna muda ukampigia akashindwa kupokea.”

“Nawafahamu hao watu niliodhania anakuwa nao muda wote akiwa kwenye starehe na mimi wananifahamu, wote ni watu na kazi za maana tu. Wamejitengenezea kundi lao. Sikuona tatizo maana mimi sinywi pombe ile ya kukaa baa. Ni wine tu. Raza ni mnywaji. Sikutaka kumfunga kwa starehe ambayo alichagua mwenyewe na sikuona madhara yake.”

“Sikuwa nikiyajua hayo mahusiano hata kuyahisi kwa sababu hakuna cha ajabu kutoka kwa Raza kilichobadilika na kuibua maswali kwangu. Kama ni kuchelewa kurudi nyumbani lilikuwa jambo la kawaida. Na hakuwa akichelewa sana, sababu ya kazi siku inayofuata. Hatazidisha saa tano usiku. Sasa kwa mtu aliyetoka nyumbani tuseme saa moja usiku au 12:30 jioni. Akafanya majukumu yake kama mama. Anaporudi nyumbani saa 4 usiku au tano, sio jambo la kuibua maswali. Au tuseme binafsi sikujali kwa sababu na mimi swala la kusafiri nje ya nchi kikazi ni kawaida sana. Sipo nyumbani, na yeye akajitengenezea marafiki zake, sikuona ajabu.”

“Ila ni kama akabadili ratiba. Si siku zote anakuwa club na hao marafiki zake. Akitoka kazini akirudi nyumbani, hatatoka tena labda siku za ijumaa, ndipo atafanya hivyo na atarudi usiku mwingi tu kwa sababu siku inayofuata jumamosi haendi kazini. Sasa kwa mtu ambaye hatoki siku za katikati ya juma, mpaka ijumaa na anakuwa na watu unao wafahamu, binafsi sikuona tatizo. Ni maisha aliyochagua, nikamuacha.”

“Kumbe walichofanya baada ya mke wa Chezo kugundua, na kumsemelea kwa Paulina akimtisha atakuja kumsemea kwa mzee wangu, walibadilisha tu sehemu wanayokutania na MUDA. Ndio maana kumbe siku hizi Raza anawahi nyumbani na Chezo hivyohivyo. Wote waliogundua hayo mahusiano yao ndio wanadhania wameachana, kumbe la. Hawakuwahi kuachana.”

“Jinsi yao ya kuwasiliana ni Whatsapp na wameweka Disappearing messages. Kwamba hata wakisahau kufuta jumbe zao, basi system inawasaidia kufuta. Huwezi kukuta jumbe zao hata kwa bahati mbaya. Mimi mwenyewe imenibidi KULIPIA pesa nyingi tu ili kuweza kufufuliwa jumbe zao.” Sonia akachoka kabisa.

“Utafanyaje Pius, na huyu ni mkeo?” “Mke anayenifunga mimi, akinitesa halafu yeye anastarehe na wanaume wengine! Anafurahia kuteseka kwangu, tena akiniona! Ananifanyia kusudi tu! Halafu anataka kuua kijana wangu asiye na hatia! Kweli Sonia?” “MmmH! Nionyeshe kile ulichonacho Pius. Maana mimi nilichonacho ni vitisho tu. Sikujua kama atafanya kweli!” Ndipo wakalinganisha alichonacho Sonia na yale aliyoyakamata Pius juu ya mkewe kwa mtoto wake, yaani Ayvin na mengineyo. Mpaka Sonia akaingiwa hofu.

“Pius!” “Ni hatari sana. Mpaka najiuliza huyu ni kiumbe gani mwenye roho ya kikatili hivi!” “Bado narudia swali langu, Pius. Utafanyaje? Maana mimi nilitaka kumtafuta ili kumtisha tu. Lakini hivi ilivyo, si kutishana tena! Mkeo ameshafika mbali na maangamizi yake yameshaanza.”

~~~~~~~~~~~~~~

Kama swali la Sonia, Je kwa Yote aliyofanya, nini Pius atafanya kwa Raza.

Ni Umbali gani Raza amekwenda kumuangamiza Ayvin?

Pam&Mill nao? Pam yuko wapi mchana huo? Ni kweli ameamua kuendelea na yake? 

Nani anakutana na Pam mchana huo?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment