Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 53. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 53.

“Hiki alichokifanya Mina, kinaweza onekana ni kibaya sana,..” “Sio kinaweza onekana! Ni hatari Ruhinda! HATARI SANA. Tusipoangalia hawa wawili wataishia jela!” “Najua mama, unampenda sana Pius, lakini pengine hii itakuwa njia nzuri sana ya kutuliza hii fujo. Na mnajua mimi nitasimama na mke wangu.” “Andy amenipokonya maneno. Mimi nataka kusema, pengine hii njia itasaidia. Mina hajakosea. Watoto hawa wametushinda mama! Hata ukikataa.” Mzee Ruhinda akaendelea.

Mzee Ruhinda akakaa sawa. “Niambieni tu, katikati ya fujo yote hii, moto mkali unaowaka na moshi wake kuenea kwa kila anayetufahamu, au hata wasio tufahamu, eti leo Paulina anaona ni sawa kwenda kuongeza mafuta katikati yake! Kweli?” “Kulikuwa na ulazima gani Paulina!?” “Wala usipoteze muda kumuuliza huyo, mama. Paulina ni mfitini. Hawezi kuona watu wanapatana au sehemu kuna amani, roho yake ikatulia.” Paul akaongeza.

“Au Pius. Niambie ni mara ngapi nimezungumza na wewe juu ya hili jambo?” Mzee Ruhinda akaendelea. “Ukijua kabisa, tokea mwanzo wa hili jambo ni hatari kwa kila mtu. Huyu binti amejirudia rudia kwa kukusihi sana. Tokea mwanzo alisema wazi kabisa, wema wako kwake, ndio ulizidi ubaya uliomtendea, ndio maana ameacha kama ilivyo. Haya, ukaona watu ni wajinga, ukaenda kuanzisha fujo huko. Na usiseme ni Andy, maana wewe ndio baba wa mtoto, ulitakiwa kujifanya mjinga katika kila jambo, ili tu hiki anachokifanya Mina, wewe ndio uwe umekifanya! Kutengeneza mazingira mazuri kwa mtoto wenu!”

“Lakini hebu fikiria FUJO ulizokuwa ukiendesha, hata katikati ya mtoto aliyekuwa mgonjwa! Mama yake, hata sisi wenyewe tukikusihi utulie, lakini wapi! Leo mtoto mdogo huyu anawaita wote HAMNA ADABU kwa wazazi wenu! Kweli?!”

“Nyinyi watu wazima mnakosa uelewa kwa jambo kama hili mpaka kushitakiwa?!” “Baba naomba niseme jambo moja tu kabla sijaondoka hapa. Maana lasivyo tutachelewa ndege.” Andy akaingilia.

“Jamani! Zaidi mama. Kuweni makini sana kuanzia hapa. Huu upendo aliowatangazia Mina, msije mkauharibu. Zaidi kwenu nyinyi wazazi.” “Unamaanisha nini?” Mama yake akauliza.

“Ukumbuke hiki alichokifanya Mina, ndicho Paulina na mimi ndicho tulichomfanyia YEYE. Sidhani kama mlishakaa naye na kuonyesha ni jambo baya tulilomfanyia, japo amekuwa akilirudiarudia sana mbele yetu.” “Na mimi nimegundua amekuwa akirudiarudia sana.” “Sawasawa Paul. Na hakuna kati yenu aliye zungumzia hilo hata mara moja.” Wote kimya.

“Sasa kwa kuwa hamkuonyesha kuwa ni kitu kibaya kilimpata yeye au tulimfanyia sisi tokea mwanzo, nashauri msije muhukumu yeye kwa hili. Maana kwa ninavyomjua Mina, akishahisi mnamuhukumu kwa kitendo kilekile mlichombariki nacho Paulina na mimi, jueni mmempoteza. Na mkimpoteza Mina, mmepoteza wajukuu wawili. Na mjue fika, historia itajirudia.” Wote wakamtizama.

Nimekusudia kujenga kwangu. Kwa nguvu zote nilizowekeza kazini, nitarudisha kwangu, alipo Mina na watoto wangu tena bila kuzembea. Sasa basi, atakapokuwa amesimamia Mina, mjue na MIMI nitasimamia hapohapo. Japo najua kwa upande wangu hamtajali kwa kuwa mmeshazoea kuishi bila mimi. Ila nimeona niliweke hili wazi. Nitasimama na Mina.” Akaweka kituo akiwatizama. Kimya.

Akaendelea. “Baba na mama, naomba niwaage. Nikamsaidie Mina ili tutoke hapa kwa utulivu.” “Naona na mimi nitawasindikiza ili nikaagane na wajukuu huko uwanja wa ndege.” “Nashukuru baba.” Andy akaondoka.

“Na Pius, nakuonya. Najua siku hizi hunisikilizi, …” “Nakusikiliza baba!” “Basi usimpige tena Paulina. Umenisikia?” Kimya. “Naondoka hapa, huku nyuma usije mpiga.” “Na mimi naomba niongozane na nyinyi ili nikamuage mwanangu.” “Tafadhali zungumza nao kwanza. Usitibue mambo zaidi. Umesikia Pius?” Kimya.

“Hakika mtaishia jela. Umesikia Paulina?” Kimya. “Kama hii video kama hivi ilivyo, endapo ikifika mbele ya jaji yeyote yule, halafu ikajulikana uliyafanya haya ukijua unamfanyia mama mjamzito, HAKUNA wakili atakutoa kwenye hii kesi.” Kimya. Mzee Ruhinda akasimama.

“Kinachokushinda kujishusha kwa Andy ni nini Pius, wewe?!” “Sasa mimi nimefanyaje mama?!” “Hivi unajua kwa lugha rahisi ni umempoteza Mina na mtoto wako?” “Mimi na Mina…” “Bro! Hakika upo kwenye denial. Unapingana na UKWELI wa waziwazi kabisa! Wewe unafikiri Mina atakuja kutengana tena na Andy?!” Paul akauliza kwa kushangaa sana.

“Jamani, hawa wawili wamekusudia. Na kama mnadhania nawatania, jueni historia INAJIRUDIA. Mlipomkataa Mina wakati ule, Andy alimtoa hapa nchini, akaenda kumuoa nje ya nchi bila nyinyi. Sasa kaka, ukiendeleza hiyo tabia, jua mtoto wako, baba atakayemfahamu ni Andy.” “Haiwezekani!” Pius akakanusha kwa kujiamini. Paul akamtizama na kuamua kusimama.

“Jamani usiku mwema. Acha na mimi nikaangalie yangu. Kama Mina alivyosema, watoto wa Ruhinda, mmeshindikana. Ila mjue MTAVUNA tu.” Paul akaondoka.

“Kabla sijaondoka hapa, Paulina na mume wako naomba muondoke. Sitaki niwaache hapa msababishe matatizo mengine humu ndani.” Wakaondoka, ndipo mzee Ruhinda naye akapandisha chumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Akamgeukia mwanae kipenzi. “Hutaondoka hapa kwenda uwanja wa ndege, bila ya kuomba ruhusa kwa Andy.” “Mama!” “Hakika Pius. Usitake kunifanya nitembee humo barabarani nimechanganyikiwa, kwa kufungwa kwako jela. Tafadhali Pius. Na kama unaona haupo tayari kuzungumza naye, basi subiri hizo siku zako za kwenda kumuona mtoto zikifika ndipo uende. Usitoe mguu hapa kutufuata nyuma bila kuzungumza na Andy kwanza.”

“Nilipokuwa nikimlelea mwanae mbona haku…” “Sikuwahi kukudharau wala kukudhalilisha wakati ukisaidia familia yangu, ila kukushukuru kila wakati Pius. Na nafsi yako nishahidi hata kama unakataa sasahivi mbele ya watu.” Kumbe Andy alikuwa akipita kutoka chumba kimoja kwenda kingine, akawasikia.

Hatimaye Bubu Kasema.

Akashuka mpaka ngazi ya mwisho akawa akiwaona pale alipokaa mama yake na Pius. “Nilikuwa nikizungumza na wewe Pius kuliko mtu mwingine yeyote kwenye hii familia au hata Mina mwenyewe. Nilipokuwa nikishindwa kuja nyumbani nilikuwa nikikupa sababu ni kwa nini nimeshindwa, tena kwa heshima! Ukawa ukinitia moyo na kusema utazungumza na mke wangu. Nikakuamini naye, kwa vile ulivyo JIFANYA kusimama katikati yangu na yeye.”

“Leo unanibadilikia mbele ya mke wangu, kujipa umaarufu ambao hukuwa nao! Unanitusi juu ya malezi kwa mwanangu huku ukijua kilichokuwa kikiendelea kwenye ajira yangu na wewe kunitia moyo ukiniambia mwanzo ni mgumu, nipambane tu!” Ndio wote wakajua kumbe Pius alikuwa akiwasiliana na mdogo wake!

Sikuwahi kukuvunjia heshima Pius. Nilikusikiliza, nikiheshimu mawazo yako nikitambua kufanikiwa kwako kwenye ajira. Halafu unakuja kunigeuka kinyama hivi, kana kwamba hukujua kilichokuwa kikiendelea!”

“Wewe ndio mtu wa kwanza kukwambia juu ya kupewa kwangu ile fulsa ya kwenda kusoma nje ya nchi. Nilikushirikisha WEWE hata kabla ya mke wangu. Unakumbuka ushauri wako kwangu?” Mina alishituka sana huko alikokuwa akisikiliza. Kwamba Pius alijua mumewe amepata nafasi ya kwenda masomoni na kumtia moyo aende! Akazidi kujilaumu akijiona mjinga kuangukia mikononi kwa Pius kiurahisi vile.

“Unanitia moyo nipambane bila kuchoka ili viongozi wangu waniamini, kumbe ni janja ya kunitenga na familia yangu, ili ujinufaishe wewe na kujipatia sifa kwa wazazi kisha kuja kunigeuka VIBAYA kwa kiasi hiki! Unanitangaza ubaya ili Mina anichukie, akuone wewe ni wa maana kuliko mimi!”

“Unajirudia rudia sana juu ya kulea mtoto wangu. Kama kweli ulifanya kwa wema, kwa nini leo KUniSIMANGIA wema wako? Wazi unaonekana ulifanya kwa HILA! Hakuna mtu humu ndani anamkumbushia mwenzie jambo jema alilofanya kwa mwenzie, wewe umekuwa wa kwanza Pius. Au useme ni mimi tu, wengine kuwafanyii hivyo!”

“Lakini pia, hukuwa mtu pekee uliyetusaidia mimi na Mina kukaa na mtoto wetu. Hata kama wazazi wanakutetea kuwa ulifanya kwa wema na kujituma, mbona wengine wasirudi kutunyanyasa kama wewe? Nimezungumza na Ron ambaye nilimuumiza zaidi kwa sababu nilimuacha dada yake vibaya sana. Na yeye alikaa na Ayan akitusaidia na wakati mwingine kumlazimu kuwa naye mpaka ofisini kwake. Akiwa na hasira na mimi nimezungumza naye. Lakini hata mara moja hajawi kunitukania au kuninyanyasia kunisaidia mwanangu. Wewe imekua kero, wimbo na FIMBO ya kutuchapia mimi na mke wangu! Wema huo UNAOSIFIWA na wazazi kuwa umenifanyia, ni wema gani huo unao UMIZA ndoa yangu kwa kiasi hiki ambacho umekusudia kutuangamiza kabisa?”

Wema huu unautangaza na kujivuna nao kila mahali, mbele ya kila mtu, kwa kujirudiarudia! Kweli?! Kwa kumsaidia Mina kipindi hicho ndio unaona una haki ya kuongoza familia yako na yangu, bila kufikiria, na mimi mwenyewe nikiwepo? Kwamba wewe unataka kuwa baba mwenye nyumba yako na yangu! Uwe kiongozi wa Mina na Raza! Watoto wako na wangu! Halafu mimi niwe wapi, na niwe nani, nikifanya nini!? Watu wote tukufuate wewe kama kiongozi mpaka wa ndoa ZETU kwa sababu unazo pesa na umeweza kumsaidia Mina? Kweli Pius?”

Umemng’ang’ania mke wangu bila aibu wala nidhamu, ukijigamba unampenda. MKE WANGU! WA NDOA TAKATIFU! Kweli Pius? Nidhamu ya wapi hiyo? Ni hizo pesa au kwa sababu unaona mama yupo upande wako ndio unaona una nguvu ya kufanya chochote kwenye hii familia?” “Mimi sijasema nipo upande wa Piu.” Hapo akamtibua zaidi Andy.

“Acha kunifanya mimi ni mjinga wakupitiliza mama. Ni mara ngapi umemkemea Pius ki ukweli kwa anayofanya kama si umechukua makosa yake ukanipa mimi, ukisema mimi ndiye NIMEMSABABISHA kukosea?” Akamuuliza kwa ukali kabisa.

“Andy ume…” “Hapana mama. Pius ANABAKA mke wangu, UNANILAUMU mimi! Au umesahau maneno yako tulipokuwa Dodoma nyumbani kwangu?” Mama Ruhinda akashindwa kujibu.

“Kwa nini Paul asilale na Mina na yeye alikiri wazi Mina anatamanisha lakini ilikuwa bora akutafute wewe uende naye kwangu kumsaidia Mina, au kumchukua mtoto akakae naye kwingine asije jiingiza vishawishini. Kilichomshinda huyo mwanao mpendwa mtukufu, ni nini mpaka kuingia CHUMBANI KWANGU, KUVUA NGUO na KULALA NA MKE WANGU, tena kwenye KITANDA CHA NDOA YANGU takatifu!?”

“Halafu bila huruma wala kunifikiria, eti wewe mama uliyetuzaa sisi wote, eti unakuja KUNIKEMEA mimi kuwa KOSA ni LANGU, NIMEMSABABISHA alale na mke wangu! Kweli?!” Mzee Ruhinda akatoka chumbani.

“Andy! Tafadhali naomba utulie.” “HAPANA baba. Mmenidhalilisha vyakutosha. Kwamba huyu Pius yeye hakosei, na akikosea basi amekoseshwa! AMELALA na mke wangu, kwenye kitanda changu cha ndoa! NDOA TAKATIFU, niliyohangaikia mimi mpaka Nairobi, mkiwa mmemkataa Mina, nikahangaika mpaka nimemfikisha Mina kanisani. Pius ANABAKA mke wangu, nyinyi hamuoni hilo ni kosa, mnakuja KUNISEMA nyumbani kwangu! Mbele ya mke wangu na mtoto, MKIMSIFIA yeye! Mnashindwa kuwa wanafiki kwangu hata katika JANGA zito kama hili lililonipata jamani! Hakika nilinyamaza kimya, nikishangaa na kujiuliza, ni katika lipi mtakuja simama na mimi?! Na pia nilinyamaza kwa kuwa sikujua upande aliopo Mina kwa wakati ule.”

“Ningejua kama japokuwa ulimrubuni mke wangu kwa mengi ikiwepo mapesa mengi ili kumgeuza moyo lakini bado Mina ananitaka mimi, kwa HAKIKA siku ile pale nyumbani, nyinyi watatu, msingeondoka na mke wangu. Mlinifunga macho na mdomo. Mkafanikiwa kuweka hukumu moyoni mwangu, MSINISAIDIE mke wangu ABAKI na mimi mumewe, mkabakia kunitupia mimi lawama, kisha kuondoka na mke wangu na mtoto wangu, halafu nyinyi mnaojiona mnabusara, na wajuaji, pia mlishindwa kumtuliza Mina, mkidhania Mina anatulizwa na mali.”

“Mkaja kumuweka hapa kwenu, kwenye nyumba hii nzuri ya thamani ambayo milango ni miwili tu inayotumika na kijana wenu huyu mtukufu mwenye mapesa mengi akiwa mtaa wa pili tu hapo, na bado mlishindwa kumtuliza Mina. Halafu eti mlivyo wa ajabu, Mina ameondoka mikononi kwenu, bado mkanitupia mimi LAWAMA kwa kuondoka kwake!”

“Sikusema kitu, nikakubali yote kwa sababu nayajua mahusiano yenu na yangu. Shida yangu ilikuwa Mina na mtoto wangu mliokuwa mkiwaharibu akili mkiwaambia mimi sifai, ili na wao wanitizame kwa jicho lenu. Lakini baba, mama na Pius, Mungu ameniangalia huzuni yangu na upweke wangu. Amenipa mke anayenipenda, na kunijali mimi kama Andy na jumla yangu yote. KAMWE Mina hataniangalia kwa jicho lenu, japokuwa Pius unahangaika sana kumpandikizia Mina CHUKI dhidi yangu.”

“Kwa Mina na kijana wangu UMEKOSA. Subiria mke wa Paul, mjinga mkubwa wewe. Malaya usiye na maadili wala aibu kwa jamii. Mchafu wa kupitiliza ila unashindwa kwa sababu mkeo amekufunga.” “Mama, unamsikia Andy?” “Wewe ni malaya Pius. Mchafu. Na leo ndio nimejua SI kwa sababu wewe ni mwadilifu ndio maana hulali huko nje, ni kwa sababu huna huo uwezo kama sisi wengine ambao nguvu tunazo ila tunathamini viapo vyetu vya ndoa.”

“Mkeo amejisahau kukufunga kwa Mina akijua huwezi fanya uchafu wako kwa shemeji yako, akidhani unatambua hata miiko ya jamii, ndipo ukapata mwanya. Kumbe wewe ni mnyama zaidi ya mnyama wa porini. HUNA maadili wala miiko! Huna adabu Pius na wewe ni MCHAFU wakupitiliza. Na nafikiri Raza alikujua tokea mwanzo, kuwa wewe ni kunguru usiyefugiga ndipo akatumia njia ya kukulogwa.”

“Sasa NAKUONYA Pius. Mbele ya wazazi wako, wanao kusifia. Mimi sitakuloga kama mkeo. ILA ukijichanganya tu, mimi mwenyewe naenda KUKUSHITAKI kwa kumbaka mke wangu.” Wote wakashituka.

“Si wewe mtakatifu sana, wazazi wanakuona mfalme wa hii familia, wanakubembeleza kama yai, ukikosa, umekoseshwa? Kokote unataka utawale kwa kiburi, hata hospitalini kwa mtoto aliye mgonjwa, ukijua mama yake hajala wala kupumzika, unatuendesha wote, ukikazana uonekane wewe ndio wewe! Sasa endeleza kiburi chako, uone nitakachokufanya. Na kama unafikiri nakutania, au nakutisha tu, NIKUSIKIE UNAMSOGELEA MKE WANGU hata kwa ujumbe wa salamu, ndipo utanijua mimi ni nani.”

“Undugu na mimi kwenu si ni mzigo? Mnanitusi mpaka nyumbani kwangu, mbele ya mke wangu na mtoto, mnaniona sifai, na mnanichafua kwa familia yangu? Sasa jichanganye kama hujawaacha wazazi wako na kilio huku mtaani, wakati wewe upo JELA.”

“Msogelee Mina kwa kisingizio cha mtoto asiye na hatia. Nitakutia ADABU uliyoshindwa kufundishwa hapa nyumbani.” Mina akatoka na kumfuata taratibu mpaka alipokuwa amesimama, akasimama nyuma yake.

“Maana nilikuja kwa wazazi kwa heshima, nikitoa malalamiko yangu juu ya hili lakini WAMENIPUUZA, na kunipa mimi kosa lako. Sasa utaona jinsi sheria itakavyo kushugulikia. Kule ambako hakuna kina Ruhinda, ila haki tu. Tuone na wao watasema nini juu ya ubakaji wako, kwa mke wangu. Wewe si unayo pesa na nikiburi? Sasa tutakuona jeuri yako na pesa vitakapo kufikisha.” Alipoweka tu kituo, akamgusa kwa upendo.

“Mama na Ron wameshafika kutuchukua kutupeleka uwanja wa ndege, nimewaambia wasiingie.” Andy akamgeukia mkewe. “Usikasirike Andy!” Wakamsikia akimbembeleza mumewe kwa upendo na sauti ya yake ya kitoto. Andy akajaribu kutulia.

“Twende nyumbani kwetu. Halafu kuna kitu kizuri, nitakwambia.” Jinsi alivyoongea mpaka Andy akacheka kidogo. Utafikiri anaye mdanganyishia mtoto mdogo! “Nini?” “Ni siri Andy! Twende tusichelewe.” “Samahani Mina.” “Pius anatakiwa kuambiwa. Sio mtu mzuri. Hata mimi nimemuona ananinyanyasia kwa misaada yake aliyokuwa akinipa. Twende kwetu, Andy. Tutakuwa sawa, usikasirike. Mimi na Ayan tunakupenda wewe na tunataka uwe na sisi hapa. Twende tusichelewe.”

“Sikujua kama uliomba usafiri kwa Ron. Mimi nilitaka kuwasindikiza.” Mzee Ruhinda akaingilia. “Sikujua taarifa za kuwashitaki watoto wenu mtazichukuliaje baba. Ndio nikamuomba msaada Ron mwenye gari kubwa. Ila sio sababu ya kutotusindikiza kama bado unanafasi. Nakupandishia wajukuu zako WOTE kwenye gari. Tena Ayvin ameamka. Anakazi ya kucheka tu hapo chumbani, ameshiba. Unakaa nao nyuma. Mimi au Andy tunakuendesha, halafu kina Ron watatufuata kwa nyuma, si ndio Andy?” “Ndio tutoke sasahivi. Tunaanza kuchelewa.”

“Ila wewe hapo Pius hakuna kuja. Subiria siku zako za kumuona mtoto zifike ndio uje. Wewe hapo mkorofi. Sisi hatutaki fujo na matusi mbele ya mama na Ron. Haya mambo mabaya, tunayaacha hapahapa ndani, nyumbani kwenu. Usitufuate nyuma.” Mina akaweka msisitizo. Pius na mama yake walibaki kama mabubu. Mzee Ruhinda peke yake ndiye aliyefanikiwa kuwasindikiza hiyo familia ya Andy.

Pande Ya Pili

Baada ya kuweka ombi lake kwa Mill kutotaka Brenda asifike kwake, na msimamo wa kutohamia nyumbani kwake, akamuacha Mill amesimama nje kama sanamu, hata kuondoka anashindwa. Akarudi ndani na kukuta hali ya tofauti. Kina mama Pili wakampokea kwa kuchangamka. 

“Nasikia shoga unahama! Tuachie basi hata ukumbusho!” “Chumba chote kama kitakavyobakia nimemuahidi kumuachia kaka Mgoshi.” “Kweli shoga unatuacha hivihivi!” “Hali yangu kama mlivyokuwa mkisema. Mlalahoi, ila maringo ya baba Shema. Nawaachia nini?” Akawafanyia kusudi kuwaambia alijua wanamsema vibaya.

“Wanakupa maneno ya kutuchonganisha mama Shema. Sie tumetoka mbali!” “Kwa kuwasikia mimi mwenyewe! Lakini mie sitaki kesi. Nataka kusema sina kitu chamaana chakuwapa. Hata kaka Mgoshi mwenywe anakuja kuchambua, atakachoona kitamfaa, ndio atachukua, vingine vyote atanisaidia kutupa.” “Basi akishamaliza yeye kuchagua, ndio naomba na sisi tupite.” “Hamna neno.” Akaingia chumbani kwake.

“Hamna chakula mama!” Akaongea kama hajala cha jioni hiyo! “Nakutengenezea tambi sasahivi. Subiri kidogo tu.” Akamchemshia tambi, akamuwekea na sukari akampa na chai. Akala, akajitupa kitandani ndio ikawa kwa heri. Akaanza kukoroma, Pam akaendelea kufungasha. Akiwaza.

                                     Siku ya Kuhama Pam na Mwanae na      

Kwa MARA YA KWANZA Birthday Ya Shema.

Kesho yake kwenye majira ya saa tatu na nusu asubuhi akaanza kuja dereva na vitu. Vinywaji vingi tu. Sahani, na baadhi ya vyakula. “Ameniambia uniambie ni wapi pakuweka.” “Mimi sikujua kama anataka mambo makubwa hivi! Nilijua analeta keki tu, akakate na wenzie wale, tuondoke. Hii ni shuguli kabisa, halafu mimi sina hata meza yakuwekea!” Gari kwa nyuma ilijaa vitu, Pam mwenyewe akachoka.

Akampigia Mill. “Nashukuru kwa vitu,…” “Lakini nimezidisha?” Akamalizia kwa swali akicheka. “Sikujua kama ndio unataka kitu kikubwa hivi!” “Hivi unajua tokea asubuhi nilikuwa huko kwenu kuzungumza na Mwenyekiti wa mtaa wenu?” “Mill!” “Mtoto wa peke yake huyo, halafu ndio birthday yake ya kwanza! Siwezi nikafanya jambo dogo. Nishaomba kibali hapo kwenye uwanja, wanapochezea mpira yeye na wenzie. Nimepata meza. Wanakuja kuweka hapo, na vyakula vingine vinakuja muda si mrefu. Hutakuwa na kazi kubwa ila kusimamia tu.”

“Bibi yake wa hapa, ndiye anayenisaidia kuandaa. Mama Colins. Wanakuja na familia yake. Ila sikujua kama Kamila anakaribishwa ua la. Nimemuomba nizungumze na wewe kwanza. Au tatizo ni Brenda tu?” Akachomekea kusudi. “Kwa ukubwa huu, hata yeye akija, watu hawatajua. Wakaribishe tu wote.” Akazidi kumchanganya kwa kumuonyesha hajali tena. Mill akazidi kupoa.

“Sikukusudia kuja na Brenda tokea mwanzo, Pam! Nisingefanya hivyo kwa kukushitukiza. Nakuheshimu sana.” “Nashukuru.” Wakatulia.

“Nakuja muda si mrefu, nimekaribia.” “Basi utanikuta nikikusubiria pale uwanjani.” “Ujue kuna mechi. Nimemwambia mwanao anayependa kunionea, leo nakuja na timu yangu na refa wa kueleweka. Sitaki anipangie watu wake.” “Ndio maana anahangaika!” “Nimemwambia atafute timu yake, hata akitaka kukodi mcheza ligi za Ulaya, leo lazima nimfunge.” Pam alikuwa akicheka hana mbavu.

Masikini mwanangu! Ndio maana anahangaika!” “Akome uonezi. Tunakuja. Na usiwe na wasiwasi nimejipanga kila kitu. Njoo kuwa mtizamaji na kusaidia kupanga.” “Sawa. Nashukuru Mill. Asante kwa yote.” “Ni mwanangu pia Pam! Najua naweza kuwa nilikuumiza juu ya kuhama kwenu, samahani. Nia ilikuwa njema. Najali, najali kupita utakavyo fikiria.” “Hamna neno Mill. Na najua kama unamjali Shema. Naona, na nakushukuru sana. Karibuni.” Mill akaishiwa maneno, akaona amuage tu.

~~~~~~~~~~~~~~

 Kufika saa sita, pakawa pamechangamka kwelikweli. Wakubwa kwa wadogo wakawa wapo uwanjani. Walivuta watu hapo uswahilini kupita kiasi. Maana Mill alikuja na watu na wadhifa zao ila wote wamevaa jezi. Mpaka mzee Komba alikuwepo, daktari mzima na jezi ya kucheza mpira! Colins na shemeji yake, mchumba wa Connie nao walikuwa kwenye jezi. Alihakikisha anatafuta kweli timu ya kutoshea. Na Shema naye akatafuta watoto wa Kitaa, wanao ucheza mpira tokea wanaanza kutembea.

~~~~~~~~~~~~~~

“Sasa msione ni watoto wadogo, bwana watoto wanacheza hao! Hapa tukazeni msuli.” Mill akawa anahamasisha timu yake wakati na Shema naye akihamasisha wenzie hapo uwanjani. Maji ya kunywa yalikuwa ni mengi na soda kibao. Mashabiki kibao. Hao waliokuwa wakicheza kwenye timu ya Mill walikuja na wake zao au wapenzi na marafiki zao na viti maalumu vya kukaa mpirani, wao wakajiwekea miavuli.

Refa akapuliza kipenga, mpira ukaanza. Walicheza hapo kama wanagombania kombe la dunia. Wazee hao waliokuwa hawajashika mpira miaka zaidi ya umri wa hao watoto, walikimbizwa mpaka wakachoka. Wake zao walikuwa wakicheka mpaka machozi.

Shema na timu yake walikuwa uwanja wa nyumbani, wakapata washangiliaji wengi sana. Alikuwa na furaha huyo mtoto mpaka baba yake aliona pesa liyomwaga hapo inastahili. Lakini waliwafunga hao wazee 3-1.

Akakata keki wakimuimbia wote. Akamlisha mama yake kwanza, kisha baba yake na hao kina Komba kama ndugu upande wa baba. Pam akashangaa anawaita bibi na babu kwa ukaribu kabisa! Akajua alishapelekwa huko. Akajituliza.

Wakati wakinywa na kula, Kamila akamsogelea Pam. “Nashukuru kuniruhusu kuja.” Pam akamwangalia, akashindwa chakumjibu kwa muda ila akasema tu, “Karibu.” Kisha akaondoka kabisa hapo alipofuatwa na Kamila na kwenda upande mwingine kabisa kama aliyekuwa akijitenga.

Mill aliona maana macho yake wakati wote yalikuwa kwa Pam mpaka Colins akaanza kumcheka. “Nini wewe?” “Mzee hupepesi macho!?” Ndio Mill akajishitukia. “Hamna bwana!” Akajibaraguza kidogo ila akajikuta macho yanarudi kwake hata katikati ya wenzie na mazungumzo ya kuchekesha, basi yeye alibakia macho kwa Pam muda wote ndio maana aliweza ona kilichoendelea kati ya Pam na Kamila.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipomuona ameondoka pale alipofuatwa na Kamila, akamfuata. “Vipi?” “Kuna mtu amefika nyumbani, nataka nikamkabidhi vitu ninavyobakiza ili kubakie kutupu, nisafishe, tukimaliza hapa tuondoke kukiwa mapema, niwahi kwenye duka lile lenye vifaa vya Shema.” “Pam, nakuulizia WEWE. Upo sawa?” Akainama na kushindwa kuzungumza.

“Usiwe na wasiwasi, hapa tunamalizia muda si mrefu. Nina watu wa kukusaidia kuhama. Tutawahi tu. Naomba usiondoke na kuacha wageni hapa. Shema hawezi tulia akiona unaondoka. Na yeye ataondoka na kupoteza maana nzima ya watu wote hawa walioacha shuguli zao na kuja kusherehekea siku yake ya kuzaliwa.” Pam akatulia.

Mara Shema akawasogelea, shida ilikuwa mama yake. “Unaona lakini nakunywa maji?” Mill akacheka. “Na umalize hiyo chupa, sio ukazane na soda tu.” Mama yake akamuwekea msisitizo. “Sasa mbona na wewe huli, mama!?” “Nishamaliza chakula changu.” Mill akawa akiwaangalia. “Nikuongezee kingine ili baadaye usisikie njaa?” “Nimeshiba Shema mwanangu. Asante. Wewe nenda kafurahie na wenzio.” “Na wewe utanisubiria?” Mill akamwangalia Pam kama kumkumbusha alichomwambia. “Siondoki mpaka mwisho, tushukuru wageni kwanza, wakishaondoka, ndio na sisi tunakuwa wa mwisho kuondoka.” Akafurahi huyo, na ndio akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Haikuchukua muda mrefu. Watu wa hapo mtaani mpaka mtaa wa jirani waliitana. Wakashambulia vyakula vyote na maji pamoja na vinywaji mpaka wakamaliza. Walioleta vyakula wakakusanya vitu vyao, na hizo sahani za disposable walizolia watu vyakula, wakakusanya takataka zote ndipo wakaondoka wakiacha hapo pasafi.

Kila familia walio alikwa na Mill ni kama ilikuja na cooler box zao. Wakamwaga barafu maana vinywaji viliisha. Wakakunja viti vyao na miamvuli. Wakarudisha kwenye magari yao.

Hao marafiki wa karibu wa Mill, wakajikusanya tena pembeni peke yao, wakamuimbia tena huyo Shema akicheka kweli! Kwanza alikuwa amewafunga. Anajisifia hapo, akiwaambia hawajui mpira. Vikajaa vicheko hapo. Wakampa zawadi zake, watu wa mtaani wakiangalia kwa pembeni maana walijitenga kufanya chao cha tofauti. Kisha na wao wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Akabakia Mill na magari mengine mawili. Wakarudi kwa Pam. Gari moja wakapakia vitu vyote vya Pam na mwanae. Jingine akawaambia wawafuate nyuma. Pam akaaga wapangaji wenzie, wakatoka ili waondoke na gari la Mill.

~~~~~~~~~~~~~~

Akamuona anaingia mlango wa nyuma. “Kwa nini hukai mbele!?” “Hapa panatosha. Asante.” Mill akabaki akimwangalia. “Naheshimu mali na vitu vya watu Mill! Natambua nafasi yangu. Unataka nijizoeze kwenye viti vya watu, akija kuwepo mwenyewe, itabidi tena uniambie mimi nikae nyuma, kumpisha mmiliki? Si bora nikae hukuhuku nitakapobakia kuruhusiwa kukaa.” Mill akajua Brenda ameshakuwa tatizo litakalosumbua.

Akanyamaza na kuondoa gari maana Shema alishakaa sawa kusikiliza akimwangalia kwa makini. Akaona asije muharibia siku yake, akatulia. Gari ya pili ikaanza kuwafuata mpaka kwenye hilo duka. Shema alishasinzia garini. Mill akaacha gari ikiwaka, akamfuata Pam. “Nashauri ununue na vitu vya chumbani kwako.” “Taratibu. Hivyo vingine nitanunua wakati mwingine.” “Leo lipo gari hapo nje na vitu vipo humo ndani dukani. Naomba tumalize Pam.” Akajua yeye ndio atalipia. Akaanza kuchagua vitu na yeye akimsaidia mpaka wakamaliza.

Mill alihangaika siku hiyo mpaka Pam akamuonea huruma. Kuanzia kupandisha mpaka kushusha kwenye hiyo nyumba wanayo hamia, na kuingiza ndani akimsaidia kupanga kila kitu. Madereva waliondoka baada ya kulipwa, akabaki yeye akisaidiana na Pam. Hapakuwa na tv wala friji. Mill aliliona hilo. Akaendelea kumsaidia kufunga vitanda, kuweka makabati na kumuhamishia Shema vitu vyake chumbani kwake.

“Yaani huyu, kuanzia leo, anaanza kulala chumbani kwake na awe anafunga mlango akiwa anavua nguo.” Pam alicheka tu. “Mfundishe bwana Pam! Ujue ameshakuwa mkubwa!” “Taratibu, ataelewa. Mazingira yatamsaidia. Mpe muda. Muone anavyo koroma pale chini! Hapo hajui hata alipo! Akiamka hapo, njaa.” “Basi acha nitoke nikanunue chakula, niwaletee, ndio nirudi kwangu nikaoge. Nimeloa jasho mpaka najionea kinyaa!” “Pole na asante. Naona leo ningecheza ngoma za kisambaa hapa mimi mwenyewe na hivi vitu, mpaka kupambazuke. Nisingemaliza leo.” “Karibu.” Akatoka.

Akaenda kuwaletea chakula. “Si mtakuwa sawa?” “Kabisa. Wewe nenda kapumzike tu. Hata mimi naoga, akiamka huyu akaoga, akala na kulala, na mimi nitalala. Mengine nitamalizia kesho.” “Basi nitawaona kesho. Usipatwe tamaa yakuendelea. Pumzika kweli, kesho nitakuja kukusaidia, tumalizie.” Akaaga na kuondoka.

Siku ya Pili Ugenini.

Siku ya jumapili kwenye mida ya saa nne, Mill akawa ameshawasili. “Nimekuamsha?” “Usijali. Karibu ndani. Jana nilisahau kukupa funguo zako.” “Wewe usiyeniamini hata na kiti cha gari, leo unataka kunipa funguo za nyumba!” Pam akajua maneno ya jana bado anayo moyoni. Akanyamaza. “Eti Pam?” “Njoo upumzike ndani kwangu. Hatuna makochi.” Akabaki amesimama.

“Njoo ndani. Shema bado amelala.” Akatangulia ndani. Bado alikuwa na nguo za kulalia ila alijifunika khanga juu. Akamsikia akimfuata. “Jinyooshe hapo kitandani wakati naandaa kifungua kinywa.” “Kama ni kwa ajili yangu mimi nilishaamka muda mrefu sana. Hapa nasubiria cha mchana.” “Basi jinyooshe hapo kitandani wakati unamsubiria Shema aamke.”

“Hivi vitu vimependezea chumba! Sema unakosa taarifa za habari Pam! Mmekosana wapi na tv?” “Nitanunua. Pale palikuwa padogo sana, hapakuwa na nafasi.”

~~~~~~~~~~~~~~

“Naomba nikuombe kitu Pam. Ila usinichukie.” Pam akakunja uso. “Mike amefariki, ni kama ameniachia Kamila. Tafadhali naomba umsamehe.” “Hata nikisema nimemsamehe au sijamsamehe, mimi ni nani kwamba kuna huo ulazima? Ni mtu wako wewe! Mimi alinifukuza kwake. Sijarudi tena huko. Kuniona ni kama hivyo kukiwa na jambo la Shema, ambaye ni mtu pekee anayetuunganisha mimi na wewe. Na ni matukio machache sana tunaweza jikuta tupo sehemu moja, na yeye kutaka kuwepo ili kukufurahisha wewe.”

“Haya, birthday ya Shema ni mpaka mwakani tena. Muhula wa mwisho wa shule Mungu akisaidia Shema akafaulu tena, zawadi wanapewa mwishoni mwa mwaka. Na Mungu akisaidia kama atakuwepo kwa ajili yako, kama hivi jana, sitambughudhi, sitamuingilia. Tatizo lipo wapi?”

Natamani Shema awe nao karibu.” Mill akaongeza kwa tahadhari. “Kwa nini, wakati alimkataa! Anafanya yote hayo na kujidai ukaribu kwa ajili yako WEWE. Mimi si mkeo! Na wala si Brenda useme kwamba kwenye mambo yenu mengine tutakutana. Kukutana, tena ikilazimu, kwa kutaka kukufurahisha WEWE ni mara mbili kwa mwaka! AKIJIDAI anataka kuhudhuria ya mwanangu! Sasa mimi kwake nina faida gani?” Mill akapoa kidogo.

“Kwangu wewe unafaida Pam! Na yeye ni kama mdogo niliyeachiwa na Mike. Sina ndugu wengi na wewe unajua. Amefanyika kama shangazi yake Shema.” “Kama yeye ni kama shangazi yake Shema, kwangu ni nani? Au kuna ulazima gani wa haya mazungumzo Mill, kama si kutaka kuniumiza tu?” “Sio nia yangu.”

“Ndio NIA yako. Kwamba yeye unaona ni wa muhimu sana, na kile alichonifanyia ni SAWA!” Akawa ameshabadilika. “Kama kweli yeye alikuwa muungwana na anashida na mimi si angenitafuta muda wote! Alijua ni mjamzito. Alijua sina kazi. Nilifukuzwa, na mke mwenzie alinifunga jela nikiwa mjamzito. Namba yangu ya simu alikuwa nayo na sikubadili mimi mpaka nilipokuja uza simu, tena ni miaka ambayo hali ilikuwa mbaya haswa. Nina mtoto, sina kodi. Yeye alikuwa na hali nzuri. Alishindwa nini hata kunitafuta na kunijulia hali, leo ANAKUONA wewe ndio anajirudisha kwangu!?”

“Hivi unajua mateso niliyopata nikiwa mjamzito, nafungwa jela na wewe sijui upo wapi? Nahangaika, yeye akijua kila kitu, ANAFICHA ukweli kwa sababu zake binafsi? Kweli hata Mike ashindwe kumwambia, leo uje hapa uanze KUMTETEA?” Mill akasimama.

“Samahani Pam. Samahani mpenzi wangu. Sikukusudia kukuumiza. Samahani. Tafadhali naomba yaishe. Basi.” “Mimi sio mpenzi wako Mill! Tafadhali usije sahau kuwa UMENIKATAA, na upo na mwanamke mwingine. Na nafikiri ndio maana unajichanganya. Huo undugu unaotaka uwepo, ni kati yake na Brenda wifi yake, sio mimi.”

“Subiri kwanza Pam, aliyemkataa mwenzie ni nani kati yetu!? Sema ukweli mpenzi wa Mungu.” “Hatukuwa wote Milimani nikakueleza kwa mapana mahali nilipo na Mgaya na nikakuomba unipe muda?” Mill akakunja ndita.

“Lakini Arusha…” “Kwamba gafla wewe ulisahau mazungumzo yote yale kwa siku moja tu!? Nikiwa nilikwambia nilitambulishwa na Mgaya mpaka kwao. Tulikuwa kwenye hatua mpaka kukaribia ndoa, mimi ndio nilikuwa nikisita sababu ya Shema! Na nikakwambia kabisa, ni kama nilishajua tokea zamani, ni nini natakiwa kufanya. Wewe mwenyewe ukaniambia unaomba nichukue hatua kwa haraka. Tumekubaliana vizuri, unanigeuka KIKATILI kabisa bila kunifikiria!” “Pam!” Akataka kumshika, akakwepa.

“Wewe niambie ni kwamba ulisahau ua ulikusudia tu kurudi kwenye maisha yangu na kuendelea kunitesa?” “Nilijua umenikataa Pam! Nilikuuliza…” “Wewe unaniuliza maswali ya KUNIDHALILISHA halafu nimeshindwa kukujibu, badala unifikirie, unaniadhibu! Hukuwahi kunipenda Mill.” Shema akaingia. Wote kimya.

“Baba hakupendi! Kwa nini?!” Hilo ndilo aliingia nalo. Wote wakabaki kimya. “Amefanya nini?!” Akamgeukia baba yake. “Ni kutoelewana kidogo tu!” “Ndio maana humpendi?” Pam akatoka kwenda bafuni. Mill akabaki hajui amjibu nini!

“Ungemuuliza akuelezee, kama hujaelewa, kuliko kumchukia!” Shema akamlaumu kwa wazi kabisa. “Sijamchukia mama yako, Shema! Haya yalikuwa mazungumzo tu. Tunawekana sawa.” “Mama yangu hajafurahia. Ukimuona hivyo ujue hajafurahia kabisa. Ungemuuliza tu, angekuelezea. Mimi mama yangu ananipenda. Hataki nikasirike wala nilie. Ananipenda. Halafu ananijali. Na mimi nampenda. Huwa ndio maana simbishii. Akiniambia jambo, hata kama sitaki, nambembeleza mpaka anakubali. Ananiruhusu, na kwenda kucheza mpira bila kumkasirisha.”

“Nikijisahau kurudi, akikasirika, namuomba msamaha. Nambembeleza mpaka ananisamehe. Halafu nikirudi nyumbani namfanyia kitu kizuri, anakuwa hakasiriki tena. Mama yangu sio mtu mbaya. Usimchukie.” “Shema, simchukuii mama yako hata kidogo. Nikinyume na hivyo unavyodhania.” Akamwangalia kwa kutoridhika, akatoka kumfuata mama yake bafuni.

~~~~~~~~~~~~~~

Akamsikia akimrubuni mama yake. “Nikupikie chai?” Akaanza akiwa amesimama nje ya mlango wa bafuni. Akamsikia Pam akicheka. “Mikate yako nakupakia mimi blueband, halafu nakupa kabisa mkononi. Nakutengenezea chai ya kisambaa kama ya bibi. Inakua inanukia mtaa mzima! Watu wote wanaanza kusema yeye Shema anampenda SANA mama yake.”

“Unanidanganya tu hapo. Ukiweka sufuria tu jikoni unaanza kuniambia, ‘niangalizie, narudi sasahivi’, sikuoni tena!” “Lakini si huwa narudi kuangalia?” “Chai inapikwa kwa masaa mangapi kama si unakua unanianzishiaga kazi, halafu unaniachia mwenyewe?” “Leo siendi mpirani mpaka chai iive. Unakunywa, naosha vyombo kabisa. Leo mimi ndio nakutunza.” Pam akacheka akiguna.

“Uanze kwa kutandika kitanda chako huko ulikolala, ndio utakuwa umeanza kunitunza.” “Haya. Halafu niokote nguo zote au nyingine unamalizia wewe wakati mimi…” “Hakuna Shema. Tulia ndani. Wewe safisha chumba chako bwana. Tulizungumza nini?” “Basi mama. Nasafisha chumba changu. Patakuwa pasafi kama kwako.” “Hapo ndio utakuwa unanipenda sana na unanitunza.” “Haya.” Pakatulia.

~~~~~~~~~~~~~~

Mill akabaki akiwaza mpaka Pam akarudi chumbani. “Maji yanatoka mengi au ni ya kujipaka tu?” “Yanatosha.” Pam akajibu akijipaka lotion. Akatulia ila akahamisha macho kwenye simu ili kumpa uhuru wa kuvaa. Akafanya yake mpaka akamaliza. Akamuona anatoka. Akamfuata kwa haraka.

“Utoke huko, ukaoge.” Akatoka. “Njaa inauma mama! Nikianguka bafuni je?” “Shema!” “Kweli. Nimezidiwa.” “Wewe hutaki kuoga bwana!” Akaanza kucheka. “Nikila ndio naweza kuoga.” “Sasa ile chai uliyoniahidi iko wapi?” Mama yake akamuuliza, akaanza kucheka kisha akamwambia. “Sasa wewe anza kuweka sufuria jikoni, nakuja.” “Huna lolote. Nenda kaoge.”

“Tunaweza kwenda kula wote mahali.” Mill akajipenyeza kwa kujikomba. “Mimi nitabakia hapa. Nenda na Shema” Pam akajibu bila ya kumuangalia. “Mimi nataka kubakia na mama yangu.” Shema akawahi kwa haraka akikataa. Mill akajua pashatibuka. “Nenda kaoge Shema. Ukitoka utakuta chai tayari.” Shema akaondoka na kuacha wazazi wake hapo hata hawaangaliani.

~~~~~~~~~~~~~~

Love At First Sight!

Inaendelea.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment