Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 51. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 51.

“Mbona haamki?!” Pius akauliza akionekana ameshapaniki. Ikabidi wampime tena pressure huku kila mtu hapo akionekana ameshaingiwa hofu. “Pressure yake ipo zivuri tu. Vidonda vinaendelea vizuri, itakuwa ni uchovu wa madawa.” Akazungumza daktari yeye akionekana ametulia.

 Pius hakuridhika. “Mmemzidishia madawa nini?” “Hata kidogo. Alikuwa kwenye dozi sahihi kabisa. Huu ni uchovu tu. Yupo sawa.” Daktari akaendelea kumuhakikishia baba mtu huku akiendelea kumuamsha. “Sasa kama mlihakikisha kila kitu kipo kwa kipimo sahihi, mbona haamki na mlisema ataamka!?” “Naomba tulia bwana, Pius! Unataka kuzidisha wasiwasi hapa, umchanganye daktari, ashindwe hata kufikiria jinsi ya kumsaidia mtoto.” Mina akamwambia kwa ukali kidogo.

“Ni sawa nikimtoa hapo kitandani?” “Kabisa.” Akamtoa kitandani na kwenda kukaa naye kwenye kochi. Akaanza kumuombea kimya kimya huku akimnyoosha vizuri taratibu. Mwishoe akafungua macho. “Muone! Ulalaji gani huo bwana! Unataka kumtia mama wasiwasi!” Akaanza kucheka kichovu.

“Mchekaji huyo! Mpaka kule theater walikuwa wakicheka anavyocheka na madawa ya usingizi.” “Ndivyo alivyo. Mwanangu hana neno. Nawashukuru sanaaa. Tena sana. Kazi yenu njema, na Mungu awabariki kunirudishia mtoto anayecheka hivi na si kilio.” Angalau Mina akabadili ile hali ya wasiwasi na lawama aliyoanzisha Pius.

 “Nigeuzie na mimi, Mina.” Bibi yake akaomba akimsogelea. “Haya, msalimie bibi, na Ruhinda mwenyewe, babu.” Akawa na kazi ya kucheka ila wazi alionekana amejawa usingizi. “Naomba nimshike kidogo.” Mzee Ruhinda akasogea kabisa karibu ili kumpokea. Mina akampa.

Akawa anamwangalia. “Haya meno mawili anayatangaza kweli! Sijui kwa kuwa yanampendeza!” “Nakwambia dada yake alikuwa akimwambia ataibwa!” Bibi yake akacheka. “Umezaa mtoto mzuri sana Mina. Vijana wako wote hawana neno na mtu. Hata Ayan alikuwa mtoto mtulivu sana.” “Asante mama. Namshukuru Mungu.” “Ayan ndio alikuwa si mlizi kabisa.” Babu mtu akaongeza. “Huyo adui yake njaa na hayo mamumivu.” Mina akaongeza akimwangalia.

“Basi tukupishe anyonye kabla hajaanza kulia. Sitaki alie wakati bado ana vidonda.” Pius akatoa wazo lakini hata Mina hakumwangalia kama ambaye hakumsikia. Ila mzee Ruhinda akamkabidhi mtoto. “Acha haya mazungumzo na daktari tukayamalizie nje wakati mtoto anakula.” Wakajua ndio anatoka. Mkewe akamfuata nyuma, Pius na daktari wakatoka. Mina akaanza kunyonyesha akiwasikiliza huko nje zaidi maswali anayojibu huyo daktari. Ila akajua wanaruhusiwa.

~~~~~~~~~~~~~~

Mtoto alinyonya mpaka Mina akaishiwa na yeye Ayvin akamaliza na kuanza kucheka. “Wagonjwa huwa hawali hivi Ayvin wewe! Mpaka ukomboleze sahani ndio unamaliza!” Mama Ruhinda akaingia. “Ayvin mchekaji! Sasa hapo amefurahia nini?” “Kushiba! Anapenda kula huyu, naona amemzidi kaka yake. Angalau Ayan alikuwa anakubakisha na maziwa. Huyu! Haachi mpaka amalize yote ndio anatulia.” “Maziwa yote?” “Yote mama. Na ni kama anajua. Anafanya kusubiria umbadilishie.” Wakacheka.

Akasikia mzee Ruhinda anaagana na Pius kuwa anakwenda kulipia. Kisha akaingia ndani. “Nipe na mimi nimshike!” “Ruhinda kwa wajukuu! Wewe si umetoka kumshika hapa sasahivi!” “Bora hawa hawanipi pressure kama baba zao.” Akamchukua kutoka kwa mkewe na kurudi naye kukaa.

Mina Na Mapinduzi.

Mina akaona azungumze nao. “Najua kuna sehemu Andy aliwachosha. Lakini wazazi wangu, Andy ananipenda. Alishanieleza ilivyokuwa, binafsi nimeamua kumsamehe mume wangu na kuendelea na ndoa yangu. Mimi napenda ndoa yangu, sitaki iishie njiani.” “Umefanya vizuri Mina. Hakuna ndoa isiyo na matatizo, ni kuvumiliana tu.” Mzee Ruhinda akaafiki. “Na urahisi unakuja pale nyie wawili mnapoamua kuendelea. Mimi nakupongeza Mina. Usiondoke na kwenda kulea watoto peke yako.” “Lakini lazima kufanya mabadiliko mama.” Mina akaongeza na kufikiria kidogo.

Kisha akaendelea. “Jamani, Andy ni mwanadamu kama sisi tu. Nia anayo, lakini bila sisi sote kumsaidia, huyu mtoto wa Pius anaweza geuka kuwa tatizo wakati Ayvin ni baraka. Najua nyinyi mnafanya kwa nafasi yenu wazazi wangu, na hakika nawashukuru. Najua mnamajukumu mengi, ila mpo na sisi kila mahali katika kila hali. Lakini na mimi lazima nifanye kitu. Lazima kumuonyesha Andy, ya kale yamepita kabisa.”

“Huu mtindo wa ndugu zake kumsema hovyo mbele za watu na kwangu! Tena kwa kurudiarudia kila wakati, sidhani kama ni sawa.” “Si sawa Mina.” “Eti mama jamani! Mtu mzima amekiri kosa. Ameomba msamaha, jambo haliishi!” Mina akaanza kulia. “Usilie Mina.” “Sipendi jinsi wanavyo mdhalilisha mume wangu! Si sawa mama.  Si sawa kabisa. Na Pius haonekani kubadilika.” “Mina, binti yangu, nimezungumza sana na Pius. Sana.” “Nashukuru baba, lakini nafikiri na mimi lazima nifanye kitu ili kukomesha hii hali.” “Tulia uniambie vile unavyofikiria kufanya.” Mama Ruhinda akamtuliza.

 “Pius anataka kuniharibia kwangu, wakati kwake ameshapajenga msingi imara, kiasi ya kwamba, anauhakika Raza hawezi muacha hata akifanya nini. Huo ni msingi alioweka kwenye ndoa yake. Sisi huko bado hatujafika. Ndoa yetu inashikiliwa na mapenzi tu. Ndio maana nirahisi kuyumba, ila tunarudiana sababu ya mapenzi. Lazima na mimi nijenge kwangu mama. Na siwezi jenga kwangu kama endapo Pius akiwa katikati yetu. Lazima nimuhakikishie mimi ni mke wa Andy. Japokuwa nimezaa naye, lakini kwangu ni kwa Andy.”

Atakuja kuwalalamikia kwa mengi, lakini naomba mnisaidie tu mjue nia ni nzuri. Sitaruhusu mawasiliano kati yangu na yeye.” “Hapo atachanganyikiwa.” Mama yake akawaza kwa sauti. “Siwezi mama. Lasivyo Andy ataishia kuumia tu.” “Utafanyaje juu ya mtoto wake?” “Nitahakikisha anarudisha HESHIMA kwa Andy. Na atambue kama mtoto wake anatunzwa nyumbani kwetu, chini ya Andy. Chochote anachotaka kwa Ayvin, apitie kwa Andy sio mimi moja kwa moja. Au unasemaje baba?” Mzee Ruhinda akatulia akifikiria.

“Labda kumjulia mtoto hali tu.” “Hapana mama Pius. Mimi nahisi Mina yupo sahihi, kuvunja hili daraja kati yao kwa muda, mpaka mahusiano ya ushemeji yarudi. Inaweza ikawa ngumu mwanzoni, lakini nafikiri hii itakuwa njia pekee yakuponya familia nzima ya Ruhinda.” “Asante baba.” Mama Ruhinda hapo akanyamaza. Pius kipenzi chake.

“Nakuahidi ni kwa muda tu mama. Na wewe nakuruhusu uwe kati yetu. Andy anashugulikia uhamisho turudi huku Dar. Ila popote tulipo, milango yetu ipo wazi kwa yeyote anayetaka kuona mtoto. Hata Pius akitaka kuja kumchukua mtoto na kukaa naye kidogo, ruksa. Na hili nitazungumza na Andy, ila si kwa kupitia mimi. Hata kama itakuwa wewe mama, kisha mnaweka mipango na Andy, muda anaotaka kuja kuona mtoto wake, au hata kumchukua.” “Kuwepo na utaratibu na taarifa maalumu sio mambo yaende kienyeji enyeji.” “Asante baba. Na haya naomba na wewe mama uzungumze naye, maana mimi sitazungumza tena na Pius. Ameniumiza sana. Na namuona ni mbinafsi kupita kiasi.”

“Naomba usimchukie, tafadhali Mina. Na yeye yupo katikati, hajui chakufanya na hili.” “Hapana mama. Anafanya makusudi na sitamruhusu hata kidogo. Mtu huyuhuyu asifiwe KOTE kuwa anahekima, aje ashindwe kumuheshimu mume wangu! Anamtusi mbele ya watu na kwangu bila kujali! Tena si mara moja! Kwa kurudiarudia bila huruma! Hapana mama. Lazima katika hilo ajifunze kwa garama yeyote ile. Tena nashauri umshauri iwe kwa haraka, lasivyo yeye ndio ataishia kuwa muhanga wala sitakubali iwe Andy au Ayvin.” Wakajua amekasirika. Pius akaingia, Mina akaingia bafuni. Hakutaka hata kuwepo hapo.

~~~~~~~~~~~~~~

“Kwema?” Akauliza Pius alipomuona Mina ameondoka kwa hasira. “Umeshakamilisha huko?” “Kila kitu kipo tayari.” Mina aliposikia tu hivyo, hapohapo akampigia simu Andy. “Nimekuamsha?” “Hapana. Nipo njiani narudi huko.” “Mbona hata hujapumzika muda mrefu?” “Nipo sawa. Nitapumzika mkitoka hospitalini. Na kabla hujauliza, nimekuta Ayan amelala. Dada yake aliniambia ndio amerudi kulala tena wakati naingia, sikutaka kumuamsha.” “Afadhali. Naona na sisi tumeruhusiwa.”

 “Basi nisubiri nakuja.” “Asante Andy.” “Acha kushukuru kama nakusaidia bwana!” “Hapana. Nashukuru kuacha mambo yako na kuwa na sisi huku!” “Ni wajibu wangu. Najua unaweza ukadhania sijui au nilikupuuza Mina, lakini natambua ni wajibu wangu, nilikosea tu, au nilipitiliza.” “Nakusubiri Andy.” Wakaagana na kutoka.

Mina Ambadilikia Vibaya Sana Pius.

“Tunaweza kuongozana wote. Gari yangu nimeweka mpaka kiti chake huyu.” “Mimi namsubiria Andy. Nyinyi mnaweza kutangulia tu.” Mina akajibu na kumsogelea mtoto. “Acha nimbadilishe baba. Mkiondoka naye awe msafi.” “Nipe mimi nguo zake nikusaidie kuvaa wakati ukila tena.” Bibi yake akamuwahi, Pius akabaki amekunja uso.

“Kwamba hutaondoka hapa mpaka Andy aje?” Kimya, Mina hakumjibu. “Akipata simu zake za kikazi zitakazomlazimu kushugulikia kwanza! Inamaana sisi wote tutabaki hapa tukimsubiria yeye?!” Mina hakumjibu.

“Nafikiri alichosema, ni YEYE atamsubiria mumewe. Mtoto huyu anaandaliwa. Akiwa tayari upo huru kutangulia naye na bibi yake, yeye atafuata na mumewe.” “Huyu mtoto kula yake ni kunyonya kutoka kwa mama yake tu baba! Akichelewa sababu ya kumsubiria mtu ambaye hana uhakika…” “Huyo mtu asiye na uhakika ni mume WANGU, na ndiye atakayekuwa akimlea Ayvin. Itakusaidia kama utalielewa hilo kwa haraka, Pius. Acha dharau za kijinga.” Alishituka Pius, wote hawakutegemea. Mina alizungumza kwa jazba na hasira kali. Wote kimya.

Pius aliondoka bila ya kuongeza neno. Pakazuka ukimya hapo, kila mmoja akageuka kuwa bubu. Mpaka Andy alipoingia. Wala hakuchelewa. Walipishana na Pius kama dakika nne tu hivi.

Mwenye Mke.

Mina akasimama na kumsogelea. “Vipi?” “Sisi tupo tayari.” “Naona na Ayvin ameshapendeza!” “Hapo ni rafiki wa kila mtu, ameshiba.” “Na ni mchekaji huyo!” Bibi yake akaongeza. “Ukikaa naye huyu, kama una pressure hata ya uzee inapona.” Ruhinda akafanya wacheke. Andy akamsogelea pale alipokuwa ameshikwa na baba yake.

“Baba hii damu ni yako, haina ubishi, lakini safari hii Mina amekupokonya kidogo.” “Karangi kidogo kamenigomea. Utajua ni mtoto wa Mina. Lakini mpaka viganja nilivyowarithisha nyinyi wote na yeye amechukua.” “Ruhinda! Unakazi ya kumwangalia humalizi!” “Kwa sababu mwenyewe amechangamka. Anataka kushika miwani yangu.” “Na pia anaonekana yeye anamwili si kama kina Ruhinda wangu, wakavu! Unanyonyesha mpaka mgongo unauma, lakini watoto wamekaukiana, utafikiri wamekosa lishe! Utajua wanakua kwa kurefuka tu!” Mama Ruhinda akalalamika.

“Mama wewe ulinyonyesha kwa muda gani?” “Mimi vilinishinda sio kama wewe hivyo. Kazi na hao! Sikuweza. Mapema sana niliwachanganyia na maziwa mengine. Kunyonyesha nikiwa nao na maziwa ya chupa nilipokuwa nakuwa kazini. Kujibu swali lako, niliendelea kunyonyesha nafikiri mpaka miezi 8 hivi. Paul ndiye alinyonya nafikiri mpaka miaka miwili, baba yake akanikataza akasema atakuwa mjinga.” Wakacheka.

“Alikuwa akimfuata mama yake mpaka chooni bwana! Nikajua ataharibika.” “Ila Paul mpaka leo yupo karibu na wewe mama.” “Na hata asiponiona, lazima atanipigia kila siku. Tofauti yake na Pius yeye ni anione. Nikiwa nchini, na nipo Dar, na yeye yupo hapa, atanifuata hata kazini mchana, anisalimie hata kwa dakika. Na hata nikiwa nje ya nchi, lazima kila siku anisikie.” “Na hao ndio waliobahatika kuwa karibu na wewe. Mimi mlinitupa mbali na nyinyi.” Andy akaongea akisikika na uchungu.

Hatukukutupa Andy. Na hili nilishakwambia. Ulionyesha ukaribu sana na alta. Kutumika kanisani hata siku za katikati za juma. Ulipenda kuwa kanisani mpaka yule askofu aliniomba kama ungeenda kwenye shule yao ukue karibu yao ujue kama upadri ndio ulikuwa wito wako au la. Nilikuuliza, ukakubali.” “Nilikuwa mtoto baba! Na mimi ningependa kukua nyumbani kama wengine. Lakini si kuwekwa mbali na familia kwa miaka yote! Japokuwa naweza nikaonekana mimi ni baba mbaya, lakini siwezi mfanyia hivyo mtoto wangu.” Wazazi hao kimya.

“Mimi nipo tayari Andy.” Mina akazungumza naye kwa upendo. “Mtoto utampakata?” “Anaondoka na bibi yake pamoja na Pius. Ana kiti chake cha gari. Sisi tutangulie nimuwahi Ayan.” Andy akawa kama hajaridhika.

“Huyu mtoto ananyonya tu, Mina. Halafu ametulia hivyo sababu pengine bado anadawa za kupunguza maumivu na ameshiba. Sidhani kama ni sawa ukimuacha hivyo tukiwa hatujui hapo njiani mpaka nyumbani tutakutana na nini. Foleni, na mengine yanayoweza kutuzuia barabarani tukachelewa kukutana. Ayan ni mkubwa, atavumilia kwa muda, ukifika tutampakata huyu, aendelee kukunusa mpaka achoke.” Mina akacheka.

“Au ameacha kukunusa?” “Yupo hivyohivyo mwanao. Tena ndio vinazidi. Akiweka chupa yake mdomoni, akininusa ndio anasikia raha mpaka usingizi. Na hapo hataki hata dada yake amguse mpaka alale kabisa ndio amtoe hapo, amuweke kitandani kwake.” “Mina, mpaka leo?!” “Mpaka leo mama, na urefu wake wote ule. Yupo hivyohivyo.” “Ndio maana asipokuona analia.” Babu yake akaongeza na kuendelea. “Hakuwa hivyo Ayan!” “Naona anavyozidi kukua ndio anazidi kuelewa.” “Nitawafuata kwa nyuma. Usiwe na wasiwasi. Sawa?” Andy akamwambia mkewe. Mina akakubali bila shida.

~~~~~~~~~~~~~~

Mara Pius akaingia. “Naomba kuwa muungwana kwenye maamuzi yako Andy. Unavyomshauri Mina, kumbuka na wewe ni baba. Hivyo unavyo mpelekesha kwa faida yako ili tu kunikomoa, ujue unamuadhibu malaika wa Mungu asiye na hatia. Huyu mtoto bado ananyonya na anamtegemea mama yake. Huna kiti chake kwenye gari yako. Mimi nilikinunua hata kabla hajafika hapa Dar, ili aweze kusafirishwa kwa usalama. Wewe sijakuona na kiti hata cha mtoto wako mwenyewe!” Akaendelea kwa jazba.

“Leo unataka tu kumchukua mtoto wangu, kwa usalama upi? Kama…” “Tafadhali nyamaza Pius.” Mama yake akamuwahi. “Hapana mama. Huyu Andy anatakiwa kuambiwa mama! Hasira zisizoisha, zitakuja kumdhuru mtu asiye na hatia. Chochote kikitokea hapo barabarani, atamlaumu nani? Au ataishia kusema tu ‘samahani’ halafu basi!” “Jamani, mimi nitasubiria kwenye gari. Mina, nitaarifu mkiwa mnaondoka.” “Hata kama unanidhara…” Andy hakumjibu, akatoka na kufunga mlango kabisa.

“Umepatwa nini Pius wewe?!” Mina akamchukua mtoto wake na pochi akawa anatoka. “Acha tukupokee mizigo mingine mama.” “Mimi nipo sawa tu baba. Asante.” Akatoka na kuwaacha hapo ndani.

Upande Wa Pili

Kesho yake siku ya jumamosi ambayo hafanyi kazi, na yeye akataka kwenda kuona anakocheza Shema. Dereva akawachukua wote na kutoka nao mpaka kwenye kituo wanachofanyia mazoezi. Wakati wanashushwa, na Mill naye akawa anashushwa na mrembo yuleyule aliyemuona naye jana kule ofisini. Bwana Mill alikuwa amependeza ki weekend! Msafi halafu amejipangilia juu mpaka chini.

Mrembo akaondoka bila hata kuwasalimia, Mill akawasogelea. Akamsalimia Pam na kumgeukia mwanae. “Leo uliniambia huji baba!” “Nimepata muda kidogo, nikaona nije hata kwa huo muda mfupi tu. Nikuone mwanzoni japo nitawahi kutoka. Umekula vizuri lakini?” “Nilikula na nina maji ya kunywa.” “Nenda, usichelewe.” Mtoto mwenyewe kama baba yake na anavyojua kumvalisha vizuri! Ungependa kumuangalia. Akamuaga mama yake na kukimbilia kwa wenzie.

“Samahani nilikuja bila kuuliza kama ni sawa.” Mill akamgeukia kama ambaye hakuwa na habari naye. “Hamna tatizo kabisa.” Mapigo ya moyo ya Pam yakaanza kwenda kasi vile tu alivyo mtizama. “Kuna sehemu nzuri tu ya kukaa. Kuna kivuli. Twende nikuonyeshe ili ukija siku nyingine ujue pakukaa.” Akamfuata nyuma kimyakimya mpaka wakafika. Wakakaa. Ni kwenye ngazi tu ila wanawaona wanavyo cheza.

“Shema anapendeka kirahisi! Na hapa napo ameshatengeneza marafiki. Na kocha wake naye anamsifia sana.” “Ameniambia anapafurahia.” Pam akajibu taratibu na kutulia. Akapotea kabisa mawazoni wala asijue kama mpira umeanza. Akamsikia Mill akishangilia na wazazi wengine ndipo akarudisha mawazo hapo. Shema alijaliwa kipaji. Alijua kucheza mpira wa miguu na aliupenda.

Mpira ukaendelea mpaka muda wa mapumziko. Shema na timu yake wakaingia sehemu, wakiongozwa na kocha wao. Mill akamgeukia akamkuta ameinama kama anawaza kitu. Akamwangalia akawa kama anataka kumuuliza kitu, akasita. Pam akamtizama akakuta akimwangalia. “Umemuona Shema lakini?” “Nimemuona.” “Kweli au ulikuwa ukiwaza yako? Mwanangu mpira anaujua kwelikweli!” Pam akacheka vile alivyozungumza kishabiki.

“Najua nilikushukuru kwa kazi. Lakini ninaanza kutafuta sehemu nyingine ya kuishi. Naona kwa muda anao lala huyu, ni mdogo kwa sababu tunapoishi na shuleni kwao ni mbali. Nikisogea maeneo ya kule Kinondoni nilipokuwa nikiishi zamani, itapunguza safari zake za asubuhi na jioni.” “Na mashoga zako wale uliokuwa hutaki kuwaacha?” Akamuuliza kama kwa kumsuta. Pam akainama bila ya kumjibu. Bwana Pam huyu ni mpole!

“Eti Pam? Huogopi tena kuwapoteza?” “Shema ndio wa kudumu. Wengine wanakuja na kupita. Sitaki yeye ndio aendelee kulipa garama ya hofu yangu ya kesho.” Mill akamtizama, na kunyamaza. Hakuongeza neno mpaka Pam akaumia. Maana alitegemea pengine angekaribishwa tena kwake au kumwambia angemsaidia kutafuta pakuishi, lakini hakuongeza. Akanyamaza tu.

Waliporudi kina Shema kucheza tena, karibu na mwisho simu ya Mill ikaanza kuita. Akapokea na kusikika kwa mbali sauti ya kike. “Nashukuru. Nakuja sasahivi, hata wenyewe wanamalizia.” Akarudisha simu mfukoni. Kisha akaitoa tena kama aliyekumbuka kitu. Akamuona anampiga picha kadhaa mwanae. Akamuga. “Jioni njema.” “Asante na wewe.” Akasimama.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati anaondoka hapo, BILA kutarajia Pam akajikuta anasimama na kumuita. Mill akageuka. Akamkimbilia. Akawa ametulia akimwangalia. “Nilikwenda kupima UKIMWI.” Mill akabaki akimtizama kama ambaye HAKUTEGEMEA hilo! Midomo ikaanza kutetemeka na mikono ikitoa jasho.

“Hiyo ni mara ya kwanza. Nilirudi tena kama majuma mawili yamepita, kupima tena. Majibu yote ninayo hapa kwenye pochi. Sijaathirika.” Mill akabaki akimtizama. Pam akajihisi amefanya KITUKO.

Hata yeye alifanya bila kupanga wala kufikiria. Pengine wivu! Au kummiss Mill! Au kuona ameshachezea shilingi chooni! Akabaki ameinama. Alipoona hakuna jibu, akamwangalia akakuta na yeye ametulia tu, akaondoka kurudi walipokuwa wamekaa. Mill na yeye akaondoka zake bila ya kujibu.

~~~~~~~~~~~~~~

Pam alijisikia vibaya, na kujuta kwa alichokifanya. Akajihisi kujidhalilisha mpaka MWISHO. Alirudi kukaa pale akiwa amepoa, mpaka mwanae anamaliza kucheza akamkuta amepoa. “Baba ameniambia aliondoka. Amenitumia picha nilizokuwa na cheza na video zake.” Shema akawa akimwambia mama yake wakielekea garini macho kwenye simu akiangalia video alizotumiwa vile alivyokuwa akicheza. Akajua kumbe alishawasiliana na mwanae. Pam akatulia hapo garini kimya mpaka waliposhushwa nyumbani.

Jumatatu.

Jumatatu kazini kama kawaida. Alipoona Mill hamfuatilizi tena, akili akahamisha kazini akijua ameshakosa la mapenzi, aendelee na yake. Maana hapo kazini  bado hakuwa amemtambulisha kama ni mzazi mwenzie. Alimchukulia kama mfanyazi wa kawaida kabisa tena hata hakuwa akimfuata kuzungumzia lolote juu ya Shema. Na ikitokea kama wanakutana mapokezi, inakuwa salamu tu. Hakuzungumzia tena maswala yale ya kupima kwake UKWIMWI, hata kwa ujumbe! Pam akaona amuache kabisa.

Juma la pili likaisha hata hakupishana naye popote japo ofisi si kubwa. Hakurudi tena mpirani. Juma la tatu akiwa tena mapokezi anatoka siku hiyo ya ijumaa, akamuona yule mrembo akiingia ofisini kwa Mill. Akajua amemfuata tena, wakafunge juma pamoja.

Usafiri ulipokuja, akaondoka kwenda benki moyo ukimuuma. Lakini  angalau alishaanza kuzoea chakufanya hapo kazini na kufahamiana na watu wa benki. Akawa mwepesi kwenye kazi zake. Akawa wa kuaminiwa na mapesa mengi tu. Naye anafanya bila shida.

~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa anarudi kutoka benki, Fatma mrembo wa mapokezi akamwambia bosi amemuita ofisini kwake mara atakaporudi tu. Mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi. Akarudisha karatasi ofisini na kwenda moja kwa moja. Akagonga, akamsikia akimkaribisha.

“Vipi kazi?” “Naendelea vizuri.” Akajibu kwa kifupi ila akamuona kama anawasiwasi. “Karibu ukae.” Akakaa kama mtoto wa shule ya msingi mbele ya meza ya mwalimu mkuu! Akajiweka sawa mpaka akatulia, Mill akimsubiria. Alipomuona ametulia ndipo akaanza.

“Ulifanikiwa kupata sehemu nyingine yakuhamia na mtoto?” “Nimeambiwa kuna sehemu mbili. Kesho ndio nataka nikapaone mara dereva atakapokuja kumchukua Shema.” “Ni wapi?” “Mmmh!” Akafikiria kidogo. “Au ni siri hamtaki mimi nijue?” Akajua anaamisha na Mgaya.

“Sipo tena na Mgaya, Mill! Nilishamalizana naye! Sema nafikiria. Maana sehemu ya kwanza, ni Kinondoni, ila Makaburini. Mwenye nyumba anataka pesa kubwa, ndio nasita. Sehemu ya pili ni Mwananyamala karibu na hospitali. Kidogo hapo sio bei mbaya. Lakini nitakwenda kupaona ndio nifanye maamuzi mazuri.” “Kama ukipenda sehemu moja wapo, ungependa kuhamia lini?” “Haraka iwezekanavyo. Sina sababu ya kuendelea kuishi kule huku mwanangu anahangaika na foleni.” Akamuona kama anayefikiria kidogo.

“Nenda kaangalie chaguzi zako zote mbili. Kisha uje upaangalie na kwangu. Palinganishe na hizo sehemu zako kisha fanya maamuzi.” Pam akabakia akifikiria hajui kama ndio habari njema au la. Maana alisema akiwekana sawa na huyo mwanamke, ndio atawakaribisha kwake. Inamaana ukaribisho huo ni kama hana chake tena kwa mazazi mwenzie. Akapotelea mawazoni hapo mbele ya Mill.

“Au kwangu umeshapasusa?” Akanyanyua kichwa na kumtizama. “Hapana. Ila mara ya mwisho kwako ni kama kulionekana pana ugumu. Sitaki kukuingilia Mill. Hapa ulipotufikisha na Shema, tunaweza ishi popote, na pazuri bila kuingilia maisha yako.” “Hapana. Nilipo sasahivi ni pazuri ndio maana nina wakaribisha. Kama utapenda na ukaona panawafaa, karibuni.” “Sawa.” Akajibu na kusimama. Kisha akakumbuka ni bosi wake. Akarudi kukaa kwa haraka. “Mimi nimeshamaliza.” Ndio akasimama.

“Halafu unajua kuna sehemu ya kula hapahapa? Huwa na mimi wakati mwingine huwa nakwenda kula huko. Wanavyakula vizuri.” “Nimesikia.” Akajibu tu hivyo, nakuondoka akiwaza.

~~~~~~~~~~~~~~

“Siwezi ishi nyumba ndogo nikijua nyumba kubwa Mill anaishi na mwanamke mwingine. Waje wazae na kuanzisha familia, mimi nipo hapo kama wegazi!” Akawaza Pam siku nzima mpaka kwake. Mwishoe akaajiambia anayo shida, lakini kwa Mill HAPANA.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake akashangaa dereva anamaagizo ya kumshusha mtoto mpirani kisha kumzungusha na yeye kwenye kusaka nyumba. Hilo akalifurahia wala hakujivunga.

Wakatoka na mwanae na kumshusha mpirani. Akazunguka kwenye hizo nyumba mbili, akaishia kupenda ya Kinondoni Makaburini. Ilikuwa ni kinyumba kidogo cha uwani kinajitegemea na kigeti kidogo cha kutumia wao japo imeunganishwa ndani ya ukuta mkubwa, ambao mbele kuna geti kubwa la kuingilia magari. Na yenyewe ipo ndani ya huo uzio. Vyumba viwili sebule na jiko.

Akaadhimia kuhamia hapo. Akazungumza na mwenye nyumba, wakakubaliana alipe kodi ya miezi sita kwanza, wakaandikishiana mkataba. Pam akapachangamkia. Pesa ya mwanae ipo, akalipa bila ya kuchelewa. Akakabidhiwa funguo, moyo ukatulia.

~~~~~~~~~~~~~~

Ndipo akarudi garini. “Ameniambia baada ya kumchukua mtoto, niwapeleke na kwake mkaangalie.” “Naona huko hatutakwenda. Hapa nimepapenda. Kwanza karibu na barabarani. Rahisi kufika kazini. Patatutosha tu.” Wakaenda kumchukua mtoto, njiani akamtumia ujumbe.

‘Mill, nashukuru kwa kutukaribisha kwako. Lakini naona nimeshapata pakutufaa mimi na Shema. Tutahamia Kinondoni. Nikishapaweka sawa, tutakukaribisha na wewe upafahamu anapoishi mwanao. Jioni njema.’ Mill alipopata huo ujumbe, HAKUTEGEMEA.

Ilikuwa kama kibao cha usoni. Alijua Pam angekimbilia kwake. Na yeye hiyo siku IKAHARIBIKA kabisa. Akashindwa hata kujibu ujumbe, Pam yeye akajua yupo na mwanamke wake. Akajituliza.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipofika tu kwake mwanae akataka kwenda kuonyesha wenzie huko mtaani picha na video alizochukuliwa na baba yake akicheza mpira. “Sasa sio uchelewe kurudi Shema. Unakumbuka baba yako amekukataza kuzurula usiku.” “Sikai sana mama! Naenda tu kuwasalimia.” “Na ulikumbuke hilo unapoona mpira, na wenzio wakicheza. Nikikufuata huko!” “Hata kama nacheza ni kidogo tu.” “Basi hakuna kwenda.” “Kidogo tu mama! Sasa unataka nikudanganye kuwa sichezi halafu nicheze kwa sirisiri!” Pam akamtizama asimmalize.

“Mimi sitaki kukudanganya mama yangu mzuri mzuri.” Akaanza kumlaghai mama yake. “Huchoki Shema mwanangu wewe! Siku nzima ulikuwa mpirani!” “Nataka niwe nao kidogo tu, halafu narudi. Nikichelewa wewe usikasirike, nifuate kwa amani kabisa, halafu tunarudi wote nakusimulia stori.” “Shema!” “Mimi mtoto mzuri mama!” Akampooza mama yake kwa maneno mazuri mpaka Pam akalainika, akamruhusu.

~~~~~~~~~~~~~~

Akaona aende ndani akazungumze na mwenye nyuma. Akamkuta na mkewe, “Kwema mama Shema?” “Kwema. Nimekuja kuwaaga. Nahama.” Wakashituka. “Mbona bila notice! Si unavunja mkataba?” “Haiwezekani!” Jazba ikawapanda. Pam akawatuliza. “Wala msijali. Nawalipa miezi iliyobakia ya mkataba wangu, na ndio hapa natoa na notice.  Si sawa?” Pesa ipo na kodi ya hapo haikuwa kubwa, hata hakutetemeka. Walishajua baba Shema anayo pesa. Jeuri.

“Kesho nikirudisha funguo, tutamalizana kabisa. Nawashukuru kwa kufanyika familia kwangu na Shema.” Hawakutegemea. Akajishusha japokuwa alijua walishaanza kumsema. Wivu. Lakini hakusita kutoa shukurani zake. “Kuna kipindi mlifanyika ndugu niliowahitaji. Mkawa wazazi hata kwa Shema. Asanteni sana.” Akashukuru na kuondoka akiwa amewafunga midomo kabisa. Walitegemea aondoke kwa jeuri, lakini ndio akawa amejishusha hivyo.

Kutingishiana Viberiti.

Alipoingia tu ndani kwake, akaanza kufungasha. Hakuwa na vitu vingi na hakutaka kubeba hivyo vitu vya ndani kwake. Kwanza vilishakuwa vya zamani karibu umri wa mwanae! Kisha anakohamia maji yanatoka mpaka bafuni. Sio yakuoga kwa ndoo. Vikorokoro vingi akakusudia kuviacha.

Nyingi zilikuwa nguo zake na mwanae. Akajikuta amepotelea mawazoni. Amekaa kwenye kiti. Muda unazidi kwenda, hana habari. Mara akasikia sauti ya Mill akisalimia nje! Pam alishituka mpaka akafa ganzi. Hakika hakutegemea kumsikia tena hapo mtaani kwao. “Yupo ndani, muda tu.” Akamsikia akiambiwa na mama Batuli.

Akagonga mara moja na kuingia. Akamkuta Pam amekaa ameshikilia nguo. “Mzima!? Mbona umenyong’onyea?” “Mzima tu. Nikupokee?” “Nitaweka tu hapa. Ni nguo za Shema, safi.” Pam akashangaa. Maana hizo nguo huletwa jumapili na dereva zikiwa zimefuliwa.  Huzichukua siku za jumamosi anapomrudisha mazoezini. Pam huzikusanya za juma zima, zinakwenda kufuliwa kwenye mashine huko kwa baba yake ili tu kumpunguzia kazi Pam. Ila akashangaa yeye ndio amezileta.

“Sikuzitegemea leo! Maana amezichukua le,..” Akaona anaanza kuongea sana kwa kubabaika na haina maana tena. “Nashukuru.” “Karibu.” Akakaa. “Hongera kwa kupata sehemu nzuri. Nimeambiwa ni pazuri.” “Nashukuru.” Pam akabaki ameinama akifikiria baada ya kumjibu.

“Unampango wa kuhama saa ngapi?” “Sina vitu vingi. Kuna kaka yangu hapo mbele, gengeni, nimempa vitu karibu vyote vya humu ndani. Atakuja kuvichukua kwenye saa nne. Nikimaliza kusafisha, ndio tutaondoka.” “Sasa mtakwenda kuishi vipi kule bila vitu?” “Nitaanza chumba cha Shema kwanza. Kikikamilika ndio vingine nitanunua taratibu. Hivi vya hapa vimechoka, siwezi kuhamisha hapa. Ni vya miaka mingi sana.” Mill akaanza kuangaza macho.

“Na kweli hakuna chakubeba hapa.” Akaafikiana naye. “Kesho anaweza kulala kwangu. Chumba chake kipo tayari kabisa na anakipenda.” “Ameniambia. Na kunionyesha picha zake mpaka kitanda. Ila sitaki akuingilie. Mpaka kesho jioni nitakuwa nimekamilisha chumba chake. Kuna mahali nitakwenda kuchukua kila kitu. Nilipita jana. Nikachagua vitu vyake, nimewaambia nitakwenda kuvibeba kesho mchana.” Mill akamwangalia na kutulia.

“Kesho ni birthday yake Shema. Huwa unafanya nini?” Pam ndio akakumbuka. “Sina nifanyalo Mill.” “Kwamba hata keki hukati!?” “Kwanza huwa hata sikumbuki! Ndio kama hivi wewe unanikumbusha. Sina utamaduni huo. Yeye mwenyewe kwanza hata hajui kama kuna kitu anatakiwa kufanyiwa. Sijawahi mfanyia chochote.” Mill akafikiria.

“Ni sawa kabla hamjaondoka nikamletea keki na vinywaji akala na wenzie?” “Atafurahi sana. Tena itakuwa njia nzuri ya kuwaaga.” “Kwanza yuko wapi?” Pam akababaika. “Usiniambie umemuacha kwenda kucheza tena, usiku huu, Pam!” “Amenibembeleza, akisema anaenda kuonyesha wenzie picha na video ulizomtumia. Ila nakwenda kumfuata.” “Giza limeshaingia! Si sawa Pam! Na hili nilikuomba maalumu. Asiwe nje mpaka giza limkute huko!” “Samahani.” Pam akasimama.

“Wewe endelea tu. Acha mimi nimfuate.” “Utajuaje sasa alipo?” “Nime pin simu yake. Ni rahisi kumfuatilia.” Akasimama. Pam akamuwahi akijua amekasirika. Kila akija hapo anakutana na kitu asichopenda. Akaona ajishushe. “Samahani Mill. Niliona aagane na wenzie.” Akatilisha huruma. Mill akamwangalia akitoa macho kwenye simu akitaka kujua mwanae alipo kupitia simu yake aliyounganisha na yake. “Usijali. Acha nimfuate. Nitarudi naye muda si mrefu.” Akatoka akimfutilia kwenye simu.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda akamsikia akiongea huko nje kama anayemsimulia baba yake kitu kutokana na mechi ya siku hiyo. Amechangamka kwelikweli wakiingia. “Sasa hapo usikae Shema. Pitiliza kuoga.” “Hata nisile kwanza?!” Akamuuliza baba yake. “Hapana Shema. Unanuka jasho na umejaa michanga.” Akaanza kucheka huku akivua nguo hapohapo mbele yao, Mill akashangaa sana. Pam akamuona anavyoshangaa.

Akaenda kumuwekea maji bafuni akamuita kwenda kuoga. Akaondoka hapo na taulo kafunga kiunoni. “Pam! Hivi huyu Shema hajui kama ameshakuwa mkubwa!?” Pam akaanza kucheka. “Anavua nguo mbele yako, hana hata wasiwasi?!” “Wala hana wazo la pili! Nakwambia akili yake ni ya kitoto, ni huo urefu tu.” Mill akatingisha kichwa kwa masikitiko. “Huyu kweli anahitaji chumba chake aisee.” Baba yake akaafiki.

“Kesho nitakuja mapema. Nitaleta hiyo keki, vyakula kidogo na vinywaji. Tukimaliza nitawasaidia kuhama.” “Nashukuru Mill, asante.” Aliporudi mwanae, akamuaga na kumwambia mipango ya kesho yake. Akafurahi huyo!

“Nitaenda kuita rafiki zangu wote. Nitawaambia wakija ndio tunakula pamoja halafu tunaagana nao.” Akaweka mipango hapo akifurahia, Mill akashangaa vile alivyo mtoto mrahisi. Wala hakulalamika kuhama na kuacha rafiki zake. Yeye chochote anachoambiwa anakubali tu. Akaaga. “Naomba tuzungumze kidogo hapo nje, Mill.” “Bila shaka.” Wakatoka.

“Niliambiwa mlinunua chakula kabla hamjarudi nyumbani!” “Alishakula huyu, ila najua atataka kula tena. Nitampikia kabla hajalala, hawezi kulala bila kula tena.” Wakatoka mpaka nje.

~~~~~~~~~~~~~~

Mill akamgeukia aliporidhika wapo peke yao. Pam akaanza kutetemeka kidogo. Mill si mzazi mwenzie tu, ni bosi wake pia. “Ni nini?” “Nilipopenda kile chumba na kuona wengi wanakihitaji, nilifanya maamuzi ya haraka bila kukushirikisha. Nimetumia pesa ya kwenye akaunti ya Shema.” Mill akabaki akimwangalia. Pam akameza mate. “Ila nakuahidi nitairudishia taratibu kila nikilipwa mshahara.” “Hiyo ndio ilikuwa kazi ya hiyo pesa, Pam. Ikusaidie kumlea Shema kwenye mazingira mazuri.”

“Kwanza nakupongeza kwa kuchukua hatua ngumu uliyokuwa ukisita kufanya. Najua pengine unaacha maisha ya kueleweka na watu wako kwa sasa, sababu ya Shema. Katika hilo nakushukuru. Ila nimeshangaa kwa nini hujakupa na kwangu nafasi hata kupaangalia! Ni sehemu nzuri ambayo ungeishi bila garama, na ni karibu na shuleni kwa kina Shema. Asingesumbuka na foleni na ungetunza pesa yako.” Pam hakumjibu. Akanyamaza.

“Labda nikuulize ni kwa nini?” “Nilifikiria Mill. Nataka mazingira ya kudumu na ya kueleweka kwa Shema. Najua nakwenda kupanga. Lakini kwa yale mazingira na kwa jinsi mwenye nyumba alivyo, nahisi patakuwa ni nyumbani kwa kudumu kwa Shema kama hapa palivyofanyika. Sio leo yupo kwako, kesho ikitokea havijafaa na mwanamke huyu, ukianza na mwengine inamlazimu kujitenga na kwako mpaka kieleweke na mwanamke mpya. Hivyo naona si sawa kwa Shema, Mill.” Mill aliishiwa nguvu, akabaki kama amepigwa shoti ya umeme. Hakutegemea kama Pam angechukulia hivyo. Nia ilikuwa ni kumrusha tu roho.

“Najua naweza nisifikie viwango vya wanawake zako, na kumkuta Mgaya siku ile kulikupa picha mbaya. Lakini Mill, Shema ni mwanangu na ni kila kitu changu. Katika kila jambo ni yeye KWANZA ndio wengine. Isingekuwa Shema, ungekuta pengine nilishaolewa. Lakini kwangu hakuna mwanadamu anakuja KABLA ya Shema. Na hata Mgaya siku ile ndio ilikuwa mara yake ya kwanza kufika ndani kwangu ninapoishi na Shema. Kwanza nilishajua hajampokea mwanangu. Nilishajua moyoni hawezi kuwa mume, kwa hiyo sikutaka kumsogeza sehemu pekee ambayo kwa Shema ndio nyumbani na kila kitu chake.”

“Nilipo mimi, ni Shema KWANZA hata kama patanigarimu mimi. Kwa hiyo hata kama sehemu inasikika ni nzuri na ingenisaidia mimi, ni bora nifanye kazi kwa bidii, nimpatie mwanangu sehemu yenye uhakika. Sio kubabaisha.” “Kwangu sio pakubabaisha Pam!” “Lakini WANAWAKE zako ndio wanatangulia kabla ya mwanangu Mill! Hilo HAPANA kwakweli. Nina shida, sikatai, lakini linapofika swala la mwanangu, tena akiwa na UHITAJI, SIWEZI nikampa mtu mwingine kipaumbele.”

“Na mimi nampa Shema kipaumbele.” “Mimi sijui kwa upande wako Mill. Siwezi kukusemea. Ila najua nilikutafuta nikikuomba pakuishi mimi na mtoto. Hapa mazingira yamenibadilikia si kama zamani. Wivu kwa majirani umeongezeka. Maneno na lawama kwamba nina roho mbaya, nimeshindwa kumpatia kazi ya udereva baba Batuli.” Ndio Mill akakumbuka.

“Aaahh! Aisee nimesahau kabisa.” “Imekua mbaya sana. Yule mama anashindwa hata kuzungumza na mimi! Undugu wote umeisha kabisa. Maneno machungu.” “Samahani Pam. Sikukusudia kukuharibia na hapa. Nilisahau kabisa maswala ya udereva wa yule baba. Kwa nini hukunikumbusha?” “Tuliacha kuzungumza kabisa Mill! Na wewe ukawa ukinisaidia mwanangu, kweli ningeanza na matatizo ya majirani pia?” Mill akatulia.

Pakuishi kwenyewe ulinikatalia!” “Sikukukatalia Pam! Nilikuomba usubiri kidogo na nilikupa sababu.” “Nilikuelewa, na mimi ndio maana nakupa sababu ya kutokaa kwenye mazingira YASIYO na UHAKIKA kwa Shema. Sitaki mwanangu ayumbishwe. Leo yupo hapa, kesho kule, hakuna sababu yakumfanyia hivyo. Kwanza SITAKI kufanya hivyo. Lazima mmoja wetu alipe garama kwa ajili yake. Mimi nimejitolea Mill. Na usifikiri nakulaumu! Nakushukuru sana. Ila siwezi kukuacha ulipe garama zote peke yako. Unafanya vyakutosha. Acha mambo mengine nikusaidie.” Mill alipoa huyo! Hakutegemea.

Pam alimng’ata na kumpuliza kwa heshima tu bila ugomvi. “Naomba nikuombe jambo moja tu. Ila sina nia ya kukukwaza.” Mill akarudisha macho kwake maana alipotelea mawazoni akiangalia pembeni. “Hapa mtaani nimeshaingia doa. Maneno yanayoendelea ni ULIACHA kuonekana hapa sababu ya kunifumania na Mgaya. Najua kwako umeshaweka vizuri, upo tayari kumtambulisha au kumsogeza Shema kwa Brenda.” Mill hakutegemea. Hakujua hata kama anamjua. Mill akashangaa sana.

“Niliambiwa jina lake na Fatma.” Mill hakujibu. “Nakuomba sana. Nakusihi. Kesho usije ukaja naye hapa.” Mill akashituka. “Mnaweza kumchukua mkasherehekea naye sehemu nyingine, lakini HAPA, naomba nitunzie heshima yangu.” “Unawezaje kufikiria hivyo Pam?!” “Lisingekuwa jambo baya, maana najua hata mpirani kwa Shema umeanza kuingia naye, lakini hapa, nimeshaharibu Mill. Acha niondoke na heshima ndogo niliyobakia nayo.”

“Mpirani kwa Shema aliingia na kukaa, lakini hata Shema hakukutana naye! Kabla ya mpira kuisha na Shema kutoka nilimuomba aende kunisubiria kwenye gari! Huyo anayekupa habari zangu, hakupi kamili!” “Sitaki kukuudhi Mill. Ni ombi tu. Naomba usije na Brenda hapa. Ni hilo tu. Usiku mwema.” Akasubiria kidogo, nakuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~ 

Inaendelea….


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment