“Sasa kama uliambiwa vitamuumiza mtoto tumbo,
kwa nini unakula Mina, wakati mtoto anakutegemea wewe tu?” Pius
akaingilia. Mina akamwangalia maana walikuwa wakizungumza wao wawili. “Tafadhali
jikaze umalize. Zaidi kipindi hiki mgonjwa. Hutataka akiwa na
vidonda hivi, halafu aanze tena na
maumivu ya tumbo! Tafadhali Mina. Na kama navuka mipaka hata kwako Andy, naomba mnisamehe. Utakuja
kula hizo nyama, mpaka uchoke. Vumilia tu umsogeze.” Hakuna
aliyeingilia.
“Basi wakati nyinyi bado mpo, acha mimi nikaoge,
nibadili nguo. Nikila nitakuja kulala hapa na Mina, maana Pius hatalala
hapa na mke wangu.” Andy akasimama kabisa. “Tafadhali baba, usiondeke
kabla sijarudi.” “Sawa.” “Sasa wewe unahisi ni nini kitatokea nikibaki hapa
na Mina?” Andy hakumjibu. Akamgeukia mkewe. “Ice cream si sawa?” “Hayo ni maziwa tu. Mletee na yeye ajipongeze.”
Mina akacheka aliposema hivyo mama Ruhinda.
“Asante mama yangu. Lakini si umeelewa sababu yangu ya
kutokuja nyumbani? Mimi sitaki nikuudhi mama.” “Sana tu. Tena naona unahekima
kuliko wote hawa. Ila nakusihi Mina, usiondoke tena mama. Wajukuu
watamu mama! Najua mazingira ya hapa si
mazuri,`lakini naomba tutafute jinsi yakufanya muishi hapa na sisi.”
“Binafsi nikuombe radhi Mina. Kucheka
kule kiukweli sikuwa nikikucheka wewe wala bro, hapa.” “Ulikuwa
ukimcheka nani?” Paulina akauliza kwa haraka. “Nikisema ndio mtakasirika
kabisa, bora ninyamaze tu. Na Paulina acha uchochezi.” “Wote tunajua
uliyekuwa ukimcheka ni mama na mkwe aliyekuwa ameletewa.”
Paul akamtizama mama yake.
“Ushabiki tu! Haya uliyekuwa ukinicheka ni
mimi, lakini aliyeumia ni Mina. Umepata faida gani? Maana mimi nilishamuomba
msamaha. Mimi na Mina hatuna tatizo. Si ndiyo Mina mwanangu?” Mina
akacheka. “Mimi na wewe tushapita kwingi mama yangu, mpaka nimesahau
ubaya wote kama ulikuwepo! Naona nakuamini wewe kuliko
hata mama yangu mzazi.” “Andy, nenda nizungumze na Mina.” “Baba usiondoke
bila mimi kurudi.” “Usiwe na wasiwasi.” Akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~
“Mina, mtafute mama yako. Anawasiwasi sana.” “Si
kwa mazingira haya anayoyaweka Pius. Mimi namjua mama yangu. Hawezi.
Andy ataelewa ninacho zungumzia. Mama yangu hii fujo ni kumchanganya, kisha kunichanganya
na mimi mwenyewe na kushindwa kufikiria kabisa.”
“Mama amehangaika sana na mimi. Sana,
kuliko nitakavyo kwambia. Nishamfedhehesha kupita kiasi. Tokea anaachwa
na baba mpaka nakaribia kuolewa na Andy, mimi nilikuwa ni mzigo mzito
sana kwa mama yangu.” “Kama unalijua hilo, ndio iwe sababu ya kumtafuta ili ajue unaendelea salama.” “Siendelei
salama, mama yangu. Na yeye si mjinga, sina jinsi ya kumdanganya.”
“Picha ya mama baada ya yote, kwangu mimi,
ilikuwa si niishie hivi hata kidogo. Kuolewa na Andy ilikuwa ni muujiza
kwake, muujiza mkubwa sana. Kisha kumpata Ayan, ndio mama aliweza
kurudisha sura kwa ndugu zake, akazungumza jambo kwa kujiamini.
Siku nimeachwa na Andy. Amenirudisha nyumbani akimwambia mama ananiacha
kwa ujauzito ambao si wake, mama hakujisumbua hata kuniuliza
ilikuaje.”
“Alifanya kama Paulina huyu. Moja kwa moja akajua nimerudia
tabia mbaya, asubuhi na mapema nikiwa natapika na yeye akanifukuza kwake.”
“Mina!” “Hakika mama. Alinifukuza kwa maneno machungu mno.
Kumbuka hapo nilikuwa nimeachwa sina pesa, na mtoto niliyekuwa
nikihangaika naye nimenyang’anywa. Natapika sina hata nguvu, ila
masanduku aliyonifungasha nayo Andy. Na alisema nisiache kwake hata mswaki!”
“Niliondoka pale siwezi hata kuangalia sababu
ya kutokula, natapika mfululizo na siwezi kunywa hata maji! Nahisi isingekuwa
Pius, ningefia kwenye ile nyumba ya kulala wageni peke yangu.”
Wakamwangalia Pius.
“Alinipigia simu, hata kuzungumza nilikuwa siwezi.
Akaja kunichukua, na kunibeba mpaka hospitalini ndio nikapoteza fahamu, nikaja
kuzinduka nina dripu. Ndio maana hata wakati mwingine nikitaka kumchukia
sana, najirudi.” “Mimi sio mtu mbaya. Sema sitaki mwanangu akue kinyonge.” “Tafuta amani Pius.” “Sawa mama, lakini sitatafuta
amani wakiwa wanataka kumkandamiza mwanangu. Hapana.”
“Sasa nani atakaye mkandamiza mwanao? Kwanza ni
hivyo hujakutana naye Ayvin mwenyewe. Hakandamiziki. Amejawa amani
na mleta furaha kwa kila anaye mzunguka. Nilikuwa nikimfikiria Andy kwa
vile alivyokuwa, nikimlinganisha na Ayan anavyoishi naye huyo. Na ukimya
wake wote, ilikuwa akimka yeye kabla ya Ayvin anasononeka. Kila wakati
anaenda kumchungulia ili aamke achangamshe nyumba. Sasa wewe utapokonya
hiyo nafasi ya Andy na kuweka uadui kati yao, hata asimfurahie
mtoto mzuri kama huyu.”
“Hiyo siyo nia yangu.” “Tafadhali baba,
nisaidie kumuuliza Pius, NIA yake yeye haswa
ni nini? Na anafikiria nini kwa maisha ya Ayvin sasahivi?” “Wala sio lazima
baba aniulize. Nia yangu kwa mwanangu ni nzuri, na nataka
mwanangu ajue mimi ni baba yake na ninampenda.”
“Wewe baba unaona kwa sasahivi huyo mtoto anahitaji
kweli gari, kama si kutaka kumuharibia mazingira ya kuishi
huyo mtoto anayetaka ajue anampenda?” “Na kabla hujajibu kwa haraka Pius,
tafadhali fikiria haya maswali maana ni muhimu sana.” “Sitaki mtoto
wangu akue kwa shida wakati mimi nina pesa! Hapana jamani.”
“Wewe unavyofikiria, huyo mtoto wako atakuja kukumbuka
aina ya gari unayomnunulia sasahivi au mazingira yaliyomkuza ndio
yatamfanya aje awe mtu mzuri ambaye wala hutahitaji kuwekeza mapesa
kwake kama sisi tulivyofanya kwenu?” “Asante mama. Na muulize…” “Kwa nini unatuma
watu wazungumze na mimi wakati tunaweza zungumza sisi wenyewe?”
Pius akamuuliza kwa kulalamika.
“Kwa sababu mimi sikukujua kama upo hivyo Pius!”
“Nipoje?” “Mbinafsi.” “Mina!” “Hakika tena. Wewe ni mbinafsi
Pius. Unajifikiria wewe mwenyewe tu. Vile unavyotaka mambo yawe,
unataka yabakie hivyo ilivyo bila kumfikiria yeyote yule hata huyo mtoto
unayesema unataka aishi kitajiri kulingana na pesa yako. Humfikirii
yeye. Hunifikirii mimi, wala hutaki kumuelewa Andy!” “Andy
ndio ameshindwa kukubaliana na….” “Tafadhali jipe muda wa kufikiria
Pius.” Mzee Ruhinda akamkatisha, Mina akaendelea.
“Jamani, Andy si mkamilifu na mimi si mkamilifu.
Lakini ni mume wangu. Tupo na ndoa takatifu na tumekubaliana
kuendelea mpaka kifo. Hilo ni agano aliniomba Andy kabla ya ndoa.
Haamini kwenye talaka kabisa. Haamini kwenye kuachana.
Yakatokea yakutokea akapata ushabiki
mpaka akaandika talaka, lakini Andy alishindwa kabisa kuendelea
na ile talaka.” “Haiwezekani Mina!” “Kweli mama. Alikuja nirudishia yale
makaratasi vilevile. Kisheria nilibaki kuwa mkewe, japo alinirudisha
nyumbani.”
“Lakini hata kabla ya kuniambia yote hayo. Akijua mimi
ni mjamzito, mimba hajui ni ya nani, alikuja kule Iringa na kunichukua.
Tena kwa kulazimishia kabisa akitaka niondoke naye, nikaishi naye
Dodoma, mpaka mimi nikawa namshangaa! Tumbo kubwa kabisa, sijampa hata maelezo
juu ya ujauzito wenyewe, maana na mimi mwenyewe nilikuwa sijui.”
“Alinirudisha kwenye maisha yake na mtoto wetu,
akiniachia niendeshe nyumba yake ile ya Dodoma vile nitakavyo. Na
hapo bado alikuwa hajui mimba ni ya nani ila yupo tayari kuendelea
vile ilivyo. Ila nafikiri ni kwakuwa alipata muda wa peke yake wa kufikiria
na kuamua. Sasa wewe Pius, unataka kila kitu kiendelee kwa haraka,
kwa muda wako wewe, na vile unavyotaka WEWE! Umezaa na mkewe.
Huonyeshi hata kama ni ajali imepata familia nzima, zaidi yeye mwenyewe
Andy. Unataka mambo yaendelee kama kawaida! Kweli jamani!?”
“Ingekuwa ni Paul au Andy amezaa na Raza, kweli
Pius ungesema tu sawa, yaishe?” Kimya. “Ni ngumu jamani, tafadhalini
naombeni mumuelewe Andy wangu. Ni ngumu. Na mbaya zaidi Pius amekusudia
kuharibu kabisa na si kutengeneza. Naombeni wengine zaidi wazazi,
mumchukulie Andy taratibu. Anajitahidi kwa kadiri ya uwezo
wake.” “Sisi tunamuelewa, Mina binti yangu. Ndio maana unatuona tupo hapa.”
Mzee Ruhinda akaingilia.
“Na hivi ninavyozungumza na Pius, ndivyo
ninavyozungumza na Andy ila nafikiri yeye Andy amekua msikivu zaidi kuliko
Pius.” “Baba!” “Ni kweli Pius. Nilichozungumza na wewe leo, ndivyo nilivyozungumza
na Andy. Amefika mjini, kimya. Wote tulimkuta pale uwanja wa ndege ametulia
kabisa akisubiria familia yake. Aliyemuanza mwenzie pale uwanjani
ni nani kama sio wewe Pius?” “Na kweli! Na Andy alinyamaza kabisa. Hakukujibu.
Umepatwa na nini Pius?” Mama yake akaingilia na kumuuliza kwa ukali.
Mina hakujua kilichoendelea hapo uwanjani kabla hajafika.
“Na usifikiri nilizungumza na huyu mtoto wako kwa
kifupi! Nilimueleza kabisa. Andy anaomba AMANI, ili aipate
familia yake. Na alisema wazi kabisa, mazingira ya utulivu
atakayoyakuta Mina, yatamfanya atulie na watoto kuliko
kwenda kuishi maisha ya kimasikini.” Mina akaumia sana. “Sikukwambia
hivyo Pius?” Kimya. “Nilimwambia. Tena nikamuongezea mazungumzo niliyozungumza
na Andy kabla ya hapo, kuwa mdogo wake anasema alikuwa akihangaika
japo alikosea jinsi ya kufikia lengo, akaishia Mina kulipa garama,
lakini alitaka afike sehemu Mina na watoto wake waishi vizuri.”
“Andy anasema alikuwa halali,
akihangaika kuwafurahisha mabosi wake, wamkabidhi cheo alicho
nacho, akiamini atakuja kutulia na mkewe. Andy alilia kwangu
akisema amekuja vipata VYOTE, lakini hana Mina, hana
kijana wake. Kulikuwa na nafasi ya kurudi Dar, alisema alishindwa kurudi
na kuja kuishi kwenye ile nyumba waliyojenga na Mina, sababu ya hukumu.
Ameamua kubaki Dodoma. Akawa analalamika kabisa anasema anauhakika huko
mkewe na mtoto wake walipo, hawaishi kama wanavyostahili, na yeye
ndio anajilaumu.”
“Yote hayo nilikwambia Pius, na nikakusihi, hayahaya
anayokuomba Mina. Huyu mtoto anakuwa kama anarudia maneno yangu kwa Pius. Mpe
muda Andy, msaidie akae sawa na familia yake, ili Ayvin aje aishi
vizuri.” “Kwani inawawia vigumu vipi kumuita mwanangu jina langu?” Walishangaa
hapo, hata mama yake hakuamini. Mina akaona hawafiki popote, akapasha
chakula akaendelea kula.
“Ni jina tu jamani! Kwani mnaona ugumu gani?” Mzee
Ruhinda alinyamaza kabisa akajisogeza kwenye kiti, akakaa vizuri. Wakajua amemaliza.
“Wewe umeamua kuvuruga hii familia Pius.” “Kwani mimi nimefanya fujo
gani hapa? Kinacho washinda kumuita mwanangu jina lake ni nini?” “Huyu
Pius anafikiria mtoto analelewa na pesa tu. Kwamba akitoa pesa nyingi, ndio
mwanae atakua vizuri.” “Kwani kuna ubaya gani wa pesa kwenye
maisha yake?!”
“Mtoe basi hapo mpeleke benki akakulie
zilipo pesa zako. Pesa si muhimu? Mpeleke akalelewe benki kwenye mamilioni
yako. Wamnyonyeshe huko, wamuuguze, halafu wewe uwe unaenda kumuangalia
tu kama salio.” “Umekasirika Mina. Na mimi sitaki kukuudhi.” “Najua
lengo lako ni kuharibu Pius. Wewe si mjinga wa kiasi hiki chakutufanya sisi WOTE, tujirudierudie
na kushindwa kuelewa.”
Paul.
“Hapo naungana mkono na Mina.” Paul akaingilia.
“Kabla hajarudi Andy, acha mimi niseme vile nilivyowaangalia
nyinyi.” Paul akaendelea. “Utanisamehe bro, ila hii ni kutaka kuwasaidia
mama na baba, wakuache kabisa. Maana kile wanachotamani kukiona
kwako kinatokea, wewe umekusudia kwa makusudi kabisa, kutowapa.
Na kama Mina unaacha kumtafuta mama yako mpaka mambo hapa yakae vizuri, jua unamuadhibu
mama yako bure.”
“Mama anapokwambia mtafute mama yako, ni kwa ile hali
tuliyomkuta nayo. Niliporudi nchini, japokuwa nasikia mama yako ni kama hakutaka
kabisa familia yetu tena baada ya wewe kuondoka, lakini mama akaniomba nimsindikize
angalau akamjulie hali. Tulimkuta ni kama mgonjwa. Ila kwa sababu mimi ni daktari, nilijua ni msongo wa mawazo.
Mama alizungumza naye sana, mimi nikiwasikiliza. Mama yako yupo tayari
kukupokea vile ulivyo na hii familia yetu.”
“Ana majuto makubwa sana. Alituelezea hatua kwa hatua
na mpaka ni kwa nini wewe umekosa imani naye, yeye kama MAMA. Alitueleza
vile ilivyokuwa hata siku ya harusi yenu. Alivyokufanya siku uliporudishwa. Alijilaumu
kushindwa kusimama nawewe kama mama, ila hakutuambia kama alikufukuza.
Alijionyesha na majuto makubwa sana. Na hajui chakufanya. Alikuwa
akimwambia mama, ingekuwa si kuharibu kwake, ungekimbilia kwake. Yaani
nyumbani. Lakini yeye amekuondolea mazingira ya pale kwake kama ni
nyumbani kwenu na wewe. Hilo anajutia Mina. Nakushauri, pata muda
fikiria na ujirudi kwa mama yako.” Paul akaendelea.
“Mimi nimezungumza sana na Andy. Msamaha
niliokuomba wewe Mina, ndio nilimuomba Andy. Sikukusudia kuwacheka.
Nilikuwa nikimcheka mama, na utaratibu wa pale nyumbani. Kabla
mama hujakasirika, acha nimwambie ukweli Mina, maana na yeye sasahivi ni
mama na anafamilia, ndipo nitakuja kuwaambia juu ya Pius. Ili wote mtulie.”
“Kila mzazi anakuwa na ndoto juu ya watoto
wake. Mimi najua nimefikia ndoto za wazazi wangu isipokuwa kwenye
maswala ya kuoa tu.” “Sasa kwa nini huoi na wewe kama si …” “Mama,
utanitoa kwenye pointi!” “Mwache amalize. Tushajua huyu si muoji, basi.” Baba
yake akataka aendelee. Paul akacheka na kuendelea.
“Wewe Mina, vile ulivyokuja kwetu, na vile wazazi walivyokuwa
wametulea sisi, hawakutarajia kabisa Andy alete msichana wa namna
yako! Samahani Mina. Na si kwa kukudharau, ila ni kule tulikokuzwa,
mazingira yetu ambayo najua unayajua, na aina ya watu
wanao tuzunguka. Haijawahi pita akilini kwa wazazi kwa kijana wao kuja
kukutana na msichana ambaye hakuwa amesoma kabisa. Si kiuwezo.
Hapana. Elimu na aina hiyo ya ustaarabu. Si hata na wewe mwenyewe
ulisema mwanzoni kabisa, tuna ustaarabu wetu?” Mina akanyamaza.
“Ninachokwambia ni hivi, tatizo haukuwa
wewe kama Mina. Tatizo ni yale malengo yao kwetu.
Siku ile ulikutana na mama aliyeshitushwa tu. Ila si kwamba tulikudharau.
Na mimi nilikuwa nikicheka japo nilikosea, kwamba wamepambanishwa!
Wanasema mapenzi ni maua, huota popote.
Huwezi mpangia mtu ampende nani. Yaliyobaki wewe unayajua na kina mama
wakajifunza kwa machungu, pale walipomlazimishia Andy aende kwa mwanamke
waliyefikiri anafaa. Wenyewe walishindwa.”
“Kama alivyokwambia Raza, si uliona mwenyewe baadaye
jinsi walivyokufungulia mikono na kukumbatia?” Mina akacheka
taratibu. “Mzee Ruhinda si wa kuahirisha safari zake eti alee
mtoto!” “Hata wake wakuwazaa alikuwa hafanyi hivyo.” “Sasa hapo mama
Pius unazidisha.” “Kweli baba. Kwani uadui wa Paulina na Mina
ulianzia wapi kama si wivu.”
“Paul jiangalie wewe!” “Acha kunitisha, utanifanya
nini? Huo ndio ukweli. Chuki yako kwa Mina hata kutaka kumtoa
Mina kwenye familia ukimshawishi mumewe amuache, ukikimbilia
hospitalini kumpima mimba, huku wakweze wametulia kimya ilikuwa
ni kuthibitisha ubaya wake, ATOKE, akupishe kwa baba. Bisha.”
“Wewe ni mnafiki.” “Sina ninachonufaika
hapa ila kuwaweka huru kwa ukweli ili kila mtu ajue moja, hivi vikao
vyenu visivyoisha, na kumpandisha pressure baba, kuishe. Mtamuua mzee bure!” “Pole
baba, kumbe unaumwa!?” “Uzee tu Mina binti yangu.” “Hauna uzee wowote wa
kuanzwa na pressure sasahivi wakati upo
na afya nzuri. Ni msongo wa mawazo. Na usipo angalia, hawa wanao wawili hawa, watakuua baba.” Akimaanisha
Paulina na Pius.
“Paul jiangalie wewe!” “Paul kuwa na kiasi.” “Hapana
bro. Wewe umekusudia kuharibu na ni kwa MAKUSUDI.” Paul akawa
mkali kabisa.
“Baba, Pius anampenda SANA Mina.” “Kwani hilo
ni siri?” “Hapana Pius, nasikia umesema hilo. Lakini
ambacho baba hajui na ni ukweli ambao hata ukipinga,
utabakia ukweli, shida yako ni hawa wawili WATENGANE, abakie Mina
BILA Andy, wewe uendelee naye.” “HAIWEZEKANI!” Mama Ruhinda akahamaki kama aliyefunguliwa macho
gafla, mzee akamtizama Pius.
“Baba, acha kunitizama
hivyo! Paul amechanganyikiwa.” “Si ubishe? Wewe jiulize baba. Atakayenufaika
na kuvunjika kwa ndoa ya Andy na Mina, mbali na Paulina ambaye yeye ni mchonganishi tu na wivu, ni
nani kama si PIUS?” Paulina akamrushia funguo za gari mdogo wake, akakwepa.
“Tafadhali tulia Paulina. Maana ni kweli wewe ndiye uliyehangaikia
karatasi za talaka za ndoa yao hao mpaka kumlazimisha Andy asaini.
Na usinijibu maana unajua ni kweli.” “Asante baba. Sasa nia ya
kijana wako huyu, kama alivyosema Mina, maana wote tunamjua Pius si mjinga. Wakati wote, Pius ni mleta AMANI. Kukiwa na tatizo
kama mzee hayupo au hata mzee akiwepo, ataitwa kuongeza nguvu ya amani.
Pius hana tatizo la kuelewa. Wote mnamjua. Hafanyi
jambo kwa hasara na ndio maana amefanikiwa sana kila alipoamua
kuwekeza muda wake.”
“Sio kama hata mmoja wetu hapa. Anajua kufikiria
mbele. Anajua kuweka faida ya kila jambo na hasara zake,
ndipo anachukua hatua kwenye kila jambo kwenye maisha yake. Na ndio siri
kubwa ya mafanio yake kutuzidi sisi sote. Na najua baba anajua maana
nilishamsikia akilisema hili.”
“Sasa basi, nina uhakika kabisa. Hata kabla
hajapanda kitandani na kulala na Mina, alishapiga mahesabu
yote haya. Akaona siku mpaka za leo. Akimjua Andy ni mtu
wa uchungu mwingi. Aina ya familia yetu na atakachokifanya.
Nina UHAKIKA ameshajua mpaka kesho ya leo,
ndipo akalala na Mina.”
“Pius hajakurupuka jamani! Na hili nilimwambia
Andy. Yeye mwenyewe Andy alifungua mlango wa kumfanya mpaka Pius ampende
hivi Mina, kiasi hata chakuwa tayari kumchukua Mina kama mkewe.
Bisha, bro.” “Sina muda wa kubishana na wewe.” “Si umeona baba? Pius anampenda
Mina ile yakupitiliza. Na kwa mara ya kwanza, hawezi jisaidia
ndio maana yupo tayari kubeba yote ili tu, ampate Mina. Yaani
Andy akijichanganya tu na kumuacha huyu mtoto, ndio furaha
ya Pius. ALEE mtoto wake na Mina tu. Andy asiwepo kwenye
picha.”
“Umechanganyikiwa Paul?” “Kwani uongo bro? Sijui ya
nyuma, yakukubali kujidhalilisha mpaka mitandaoni, wewe na nyadhifa
zako, lakini kwa LEO tu. Nakuona unafanya MAKUSUDI kabisa, KUHARIBU. Kuanzia
uwanja wa ndege, ulikusudia kumuharibu Andy akili ili akija
mkewe, amkute AMETIBUKA. Kusudi tu. Hapa kwenyewe unahangaika, kuwatibua
bila sababu.”
“Unapenda sana kuongea Paul.” “Kwa sababu unajua ni kweli.
Huyo mtoto wako unajua wazi hana rikodi yeyote ile serikali wala
hospitalini. Umeletewa mpaka mikononi mwako na ukweli UNAuJUA. Kinachokushinda
kufanya hiki unachokitaka hapa kihalali, kisheria ni nini,
UNAKAZANA kupoteza amani kwa mama ambaye unajua ananyonyesha,
hajala, alikuwa akiuguza mtoto aliyekuwa akilia muda
wote?” Kimya macho kwa mwanae.
Ila Paul akawa amemfungua macho kila mtu zaidi Mina. “Najua unajua bro. Ila unafanya KUSUDI
tu.” “Na kweli! Maana kama shida ni jina la mtoto, si
angeenda kumuandikisha jina analotaka yeye. Akatengeneza vyeti
vya kuzaliwa hata vitambulisho anavyotaka yeye, kwa majina
anayotaka yeye, na kuleta akisema ndio majina ya mtoto!” “Umeona baba? Sasa
wewe unafikiri haya yeye Pius hajui kama si kwamba anafanya tu kusudi KUWAVURUGA
hawa wawili?” Mina aliumia sana, ila aliendelea kula.
“Na mkewe?” Paulina akauliza. “Kwani Pius anashida
na Raza? Raza ndiye anayeshikilia ile ndoa. Na Pius anajua wazi, Raza hawezi
muacha hata akimwambia anaoa mke wa pili. Atapiga kelele na uchawi,
lakini si muondokaji.” “Na bora umejiingiza kwa Yesu na kuwa muombaji,
Mina mwanangu.” Mama Ruhinda akazungumza hivyo tu.
“Mimi natoka. Namrudisha Poliny chuo. Kukitokea
chochote, tafadhali unijulishe Mina. Nitarudi hapa asubuhi na mapema.” Hakuna
aliyemjibu Pius. Akainama kumbusu mwanae akamwangalia Mina. “Jaribu kupata muda
wa kupumzika, kipindi hiki mtoto akiwa amelala. Huwezi jua akiamka atakuaje?
Sawa?” “Sawa.” “Na acha mawazo ya kutaka kuondoka. Nakuahidi kila kitu
kitakuwa sawa. Tulia ulee watoto kwenye mazingira yakueleweka. Kila kitu
kitakuwa sawa.”
Akamgeukia Paul. “Acha kueneza sumu na kumjaza
Mina ujinga. Namtegemea kulea huyu mtoto. Kama huwezi
kuleta amani hapa, ondoka. Nisikuone karibu ya mtoto wangu.
Umenielewa Paul?” Hapo akawa mkali kabisa. “Kama wewe una hekima sana
kwenye mambo, mbona hatukuoni ukaanzisha familia na kuiongoza
kwa hiyo hekima yako? Umejawa maneno maneno tu ya uchonganishi!
Nani amekukaribisha hapa?” “Paul ni mmoja wa hii familia Pius. Acha
kumkaripia.” “Hapana mama. Anachotaka ni kuchonganisha si kuleta amani.”
“Unataka yeye alete amani wakati wewe ndio unaharibu?” Mama yake akamjia
juu.
“Leta amani hapa uone kama kuna atakaye haribu.”
“Naomba Paul, aondoke mama.” Paul akaanza kucheka. “Ukimfukuza Paul ujue
umenifukuza na mimi.” “Mama?!” “Unafikiri nilimuokota huyu? Acha
kujifanya umechanganyikiwa.” Pius akaondoka kwa hasira.
“Na Pius.” Akasikia akiwa ameshatoka. Akarudi. “Zingatia
mawasiliano kwa Mina. Kama mumewe alivyoomba, ukitaka kitu kwa
Mina, wasiliana naye. Ukishindwa, mwambie mama yako.” “Sikukubaliana
na hilo baba. Na sioni sababu. Yaani mimi kutaka kujua hali ya mwanangu
ni mpaka nimuulize mama ua yeye, wakati mama yake ndio yupo karibu?!
Hapana baba!”
“Mnamwadhibu mwanangu bila sababu! Mwambie Andy
nimekataa. Sitafanya hivyo. Hata mahakamani nitaenda.
Acheni kunifanya mimi ndio mbaya wakati aliondoka kwake, nikamlelea
mtoto wake mchana na usiku yeye akishindwa hata kupiga simu! Leo eti
gafla nimuamini kwamba atakuwa na mawasiliano juu ya mtoto wangu
wakati wakwakwe alimshindwa! HAPANA baba. Mwambie nikitaka hali
ya mwanangu nitamtafuta mama yake. Akitaka awe na Mina kila
wakati ili awe analinda mazungumzo yetu. Msinichezee akili.”
Akaondoka kwa hasira.
Huko Upande Wa
Pili.
Shema akarudi
tena shule. Safari hii ratiba ikawa shule na mpirani. Akawa anaondoka asubuhi
kurudi usiku. Ameshakula, ni kuoga na kulala. Upweke ukaongezeka kwa
Pam. Maisha yakaendelea, kimya, hamsikii Mill kwa la kheri wala kwa
salamu! Na yeye akatulia.
Nafasi Ingine
Baada ya mwezi
tena kupita kwenye majira ya saa nne asubuhi akapata ujumbe kutoka kwa Mill. ‘Sijui kama naruhusiwa
mawasiliano kwa mida gani, lakini ni maswala ya kazi. Kama bado unatafuta kazi,
wasiliana na namba hii.’ Akamrushia namba. ‘Asante.
Nashukuru Mill. Muda gani mzuri wa kumpigia?’ ‘Anatafuta kujaza hiyo nafasi kwa
haraka. Nashauri usivute.’ ‘Asante. Nampigia sasahivi.’ Hakumjibu.
~~~~~~~~~~~~~~
Akapiga bila ya
kuchelewa. Akapokea sauti ya kiume. Akajitambulisha na kumwambia amepewa namba
yake na Mr. Mgini. Kwake akamtambulisha kikazi, sio kwa jina la Mill. Akaonekana
kuelewa kwa haraka na kama aliyekuwa kitarajia simu yake. Akamuhoji maswali ya
msingi tu na kumuuliza yupo tayari kuanza kazi lini. Pam akasema baada ya siku
mbili. Akitaka kujiandaa maana ni kazi ya kiofisi.
Ilifanana kama
aliyokuwa ameambiwa na Mill mwanzoni. Na ni kama kazi aliyokuwa akifanya
kwa Sandra, ila si mikopo. Kushugulika na maswala ya benki, akimsaidia
muhasibu. Alifurahi Pam, hakuamini.
~~~~~~~~~~~~~~
Akaenda kujisafi
haswa, kusudi ili kumrudisha Pam wa viwango. Na hivi alishaletewa na
Mill mapigo ya ukweli! Hakutaka kujikosea. Alitengeneza nywele vizuri na
kuongezea kununua baadhi ya nguo za kiofisi. Pam alishafanya ofisi za warembo,
alijua wapi pakupata nguo zakueleweka za kiofisi. Na hivi bado Mill alikuwa
akiweka pesa benki, hakujipunja. Uzuri viatu vya maana Mill
alishamletea, alijua lazima enzi zitarudi tu.
Akaona awe muungwana. Siku kabla yakuanza kazi
akamtumia ujumbe. ‘Nashukuru, ile kazi nilipata. Naianza kesho. Asante.’
‘Karibu. Na kama utahitaji usafiri, unaweza kumtumia dereva wa Shema.
Vinginevyo kila la kheri.’ Alifurahia Pam, mpaka
akajikuta akirukaruka kwa shangwe na kumjibu. ‘Nitashukuru. Akija kumchukua
Shema, na mimi nitaomba lifti.’ Hakujibiwa. Akasubiria
majibu mpaka akachoka na kunyong’onyea. Hakujibiwa.
Light, at the
end of tunel.
Hakumwambia mtu
kama anaanza kazi maana mahusiano ni kama yalishaharibika na wapangaji
wenzie. Mama Batuli alishakuwa akimtangaza ana roho mbaya, alishindwa kumuombea
kazi mumewe kwa baba Shema, ndio maana na yeye Mungu amemnyima. Ushoga
ukaisha kabisa hapo ndani, wakasahau mazuri yote waliyokwisha fanyiana.
Akawa amebakia peke yake tu. Akajiapia mshahara wa kwanza, anahama
hapo. Ila hakumwambia mtu.
~~~~~~~~~~~~~~
Hatimaye nuru
ingine tena ikaangaza. Alitoka hapo alfajiri na mwanae. Bwana alipendeza kama
aliyekuwa amepania! Kuanzia juu mpaka chini, kiatu cha juu. Na mguu wake
ukapendeza maana alivaa gauni fupi mpaka kwenye magoti. Dereva alifika na
maelezo kuwa amfikishe Shema shule kwanza kisha ampeleke na yeye kazini. Akajua
Mill alishashugulikia hilo. Ila wasiwasi wa kuwahi kazini ndio
ukamuingia.
Walipofika kituo
cha Sayansi, akamuomba amshushe achukue daladala ya kazini kwake. Hakumbishia
sana japo alimwambia wasingechelewa. Pam akalazimishia akiwa na hofu
ya kutoharibu kazi mpya.
Daladala
ilimshusha nje ya geti la hospitalini, akajitambulisha getini na kuulizia
zilipo ofisi zao. Akaonyweshwa. Akatembea mpaka huko. Ikawa imetimia saa mbili
kamili na yeye yupo mapokezi.
Lilikuwa eneo
dogo lakini safi sana. Ofisi nadhifu mno tofauti kabisa na kwa Sandra. Mambo
yaliendeshwa kitaalamu. Akaitiwa huyo muhasibu. Akiwa anasubiria hapo mapokezi,
akatokea mwanaume amevaa shati jeupe na tai. Alionekana na neema.
Akamtambulisha kwa mrembo pale mapokezi, Fatma, kuwa na yeye atakua mfanyakazi
wa hapo, ndipo akamkaribisha ofisini.
Akampa
utambulisho na kumzungusha sehemu ya biashara. Akahisi ni kama kile
alichoambiwa na Mill anamiliki hapo nchini lakini bado hakuwa ameonana na Mill
mwenyewe, akajiambia atulie, pengine vinafanana. Akampeleka sehemu
wanazo fanyia vipimo, wanapopokea pesa au malipo na kuandikiwa risiti maana
kote huko alitakiwa yeye ndio awe anapita kukusanya malipo na kopi za risiti.
Kumpelekea muhasibu. Kufunga mahesabu, kisha anapewa yeye kupeleka benki.
Haikuwa ngumu.
“Ningekupeleka
kwa bosi, lakini leo yupo busy kidogo.” Hilo halikuwa tatizo kwa Pam,
shida ilikuwa kazi wala si bosi wao. Akaanza kuelekezwa chakufanya.
Hapakuwa na kitu kigumu alichoona kingemshinda. Mida ya mchana walizoea
huyo muhasibu na wengine wawili kutoka kwenda kula kwenye mgahawa wa hapohapo
hospitalini. Lakini Pam alipokaribishwa, akakataa kiuungwana.
Jioni wakati
anatoka akakutana na dereva wa Shema nje akimsubiria. “Anakaribia kumaliza
mazoezi. Nakufuata wewe, kisha namfuata na yeye, nawarudisha nyumbani.”
Alishukuru Pam, maana hakujua angerudije nyumbani na foleni hizo. Wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~
Kesho yake
akafanya vilevile, alishukia kituo cha Sayansi na kuchukua daladala ya
kumpeleka kazini. Alimkuta Mill amesimama mapokezi. Amevaa kiofisi. Bwana Mill alipendeza,
mpaka Pam akababaika. Alikuwa kwenye simu hapo mapokezi. Akasimama kusubiria
mpaka alipomaliza kuzungumza, ilisikika ni simu ya kikazi maana alikuwa
akizungumza kwenye simu ya mezani, akionekana amepewa na huyo mrembo wa hapo
mapokezi, Fatma.
Kama apige
goti kumsalimia. “Vipi umeonaje siku ya kwanza?” “Bado najifunza na kuelewa
kazi yenyewe.” Akamuona ni Pam aliyenyong’onyea na amepungua mwili si
kama alivyoachana naye wakitokea Arusha. Akagundua hapo hajamsifia kama amependeza.
Kabla hajaongeza kingine, muhasibu, ambaye ndio Pam anafanya kazi naye,
alijitambulisha kwake kwa jina moja tu, Mbise, akatoka akionekana anamazungumzo
naye. Akamwambia waelekee ofisini kwake. Ndio akajua ni kweli. Yeye ndiye anayemiliki
hapo.
Akapoa na
kuelekea ofisini kwao. Maana Mill aliondoka bila hata kuaga, na hapo
aliheshimika kama mmiliki wala si bosi tu. Alishaona hapo mambo yanaendeshwa kitaalamu
wala si kiswahili. Sekretari mwenyewe, huyo Fatma, alikuwa msafi haswa
na amependeza. Anazungumza lugha zote mbili, kiswahili fasaha na kingereza bila
kona ndefu.
Akaenda kutulia
ofisini kwao akifanya kazi. Siku hiyo mida ya saa tano wakatoka kwenda benki kutambulishwa
kama mmoja wa wafanyakazi wa hapo ili akifika wawe wanamsaidia kwa
haraka asiwe anasimama kwenye foleni. Na hapo walipelekwa na gari ya ofisi.
Nzuri sana. Safi. Akajua ni mambo ya Mill tu, kupenda vizuri.
~~~~~~~~~~~~~~
Akaendelea na
kazi mpaka siku ya tano ambayo ni ijumaa wakati anakwenda benki akakutana na
Mill akitoka na mrembo wa nguvu! Pam mwenyewe alimkubali.
Msichana alikuwa mzuri, halafu alijijulia. Yeye hakuwa mweupe kama Pam, maji ya
kunde inayokwenda rangi nzuri nyeusi. Ila umbile kama la Pam! Na alijua vile
Mill anavyopenda wanawake wenye maumbile ya kibantu! Wenye minofu
sehemu zao. Akajua wazi ndiye huyo mwanamke wake. Wote walijikuta mapokezi.
Pam akitaka
Fatma amuitie dereva, na Mill naye alikuwa akiaga kwa Fatma huyohuyo
akimalizia maelezo akisema siku hiyo hatarudi, ndio amemaliza. Ilikuwa
saa tano asubuhi. Pam akajiweka pembeni AKIUMIA. “Inamaana anakwenda
kupumzika na mwanamke wake!” Pam akawaza AKISONONEKA. “Ila nao wamezidisha. Mapema hivi!” Akajilalamisha moyoni ila
akakumbuka mapenzi ya Mill. Mkiwa naye kitandani, huwezi jua kama masaa
yanakwenda. Akaenda kukaa kwenye makochi akisubiria gari, akapotelea mawazoni.
Alisikia kiitwa
kuwa dereva amefika. Wala Mill na mrembo wake hawakuwepo pale. Kwamba
walishaondoka, hata hakumsemesha wala kumtambulisha kwa huyo msichana! “Ameshindwa
hata kusema mimi ni mzazi mwenzie!” Pam AKAUMIA sana. Siku ikawa imeshamuendea vibaya.
~~~~~~~~~~~~~~
Inaendelea…
0 Comments:
Post a Comment