Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 47. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 47.

Maji yamezidi unga, bado Mina alikuwa njia panda asubuhi hiyo ya saa nne akiwa bado yupo chumba cha daktari, ameshindwa kufanya maamuzi ya huyo mtoto, kufanyiwa upasuaji. Akakumbuka fujo aliyoacha nyuma, hakuona atakayempa ushauri wa haraka bila kufikiwa baba wa mtoto mwenyewe. “Hata nikimpigia mzee Ruhinda, ataishia kuzungumza na Pius mwenyewe kwanza ndipo anirudie.”

Akaendelea kuwaza. Andy na mtoto wa Pius!” Akazidi kusita kila alipokumbuka jinsi walivyoachana na mumewe, na vile Andy walipofika na kaka yake. “Hata yeye atataka kumshirikisha Pius kwanza kabla hajafanya maamuzi ya mtoto wa Pius mwenyewe asije laumiwa baadaye. Kwanza hata sijui kama bado anatutaka mimi na mtoto wa Pius!” Akawa anaendelea kuwaza hapohapo mbele ya daktari akiwa bado anahofu ya ajabu. “Bora niokoe muda.” Daktari akamuona anachukua simu na kupiga. Ikaita kama mara tatu hivi, upande wa pili akaitika.

“Mimi Mina.” Akajitambulisha. Kimya asijue mshituko uliompata. “Pius?” “Nimekutafuta Mina! Mpaka nimechanganyikiwa. Nipo kama mwehu! Mpaka leo asubuhi pia nilikuwa nahangaika kukutafuta! Upo mzima?” Akauliza kisha akaongeza. “Ulifanikiwa kujifungua salama?” Ayvin anaumwa, ndio maana nimekupigia.” “Ni nini tena?” Mina akaanza kilio.

“Usilie niambie.” “Mtoto alikuwa mzima kabisa. Akaanza kulia sana, halali. Nimemleta hapa hospitalini tokea asubuhi ndio hatimae daktari amesema ana henia, wanataka kumfanyia upasuji. Ndio nikasema nikwambie kabla hawajaanza kumkatakata.” “Sasa hivi anaendeleaje?” “Analia kila wakati mpaka amepata homa! Hanyonyi vizuri tokea juzi. Analia tu. Yaani sasahivi ndio amepitiwa na usingizi. Amelala, tupo hapa chumba cha daktari.” “Naomba kuzungumza na daktari.” Mina akampa simu daktari.

Pius akazungumza naye kwa kifupi ila akajua walipo. “Anataka kuzungumza na wewe.” Daktari akamrudishia simu. “Nashukuru kwa hatua uliyochukua, lakini tafadhali hapo wasimguse kabisa mwanangu.” “Sasa nitafanyaje?!” “Kodi gari. Sogea mpaka Mtwara. Nakutumia tiketi ya ndege, yako na ya watoto.” “Mimi nina msichana wa kazi anayenisaidia watoto. Siwezi muacha. Kwanza bado mdogo, mama yake amenikabidhi.” “Basi na yeye namkatia ticketi. Lakini Mina, lazima muondoke sasahivi ili muwahi ndege, huyo mtoto atibiwe LEO. Yaani wewe ukiwa safarini, mimi nafanya taratibu za madaktari huku ili mkifika tu, moja kwa moja twende hospitalini. Usiogope, kila kitu kitakuwa sawa.” “Asante Pius.” Akamalizia taratibu za hapo hospitalini huku akiwa amepiga simu kwa mama mwenye nyumba wake amsaidie kuandaa safari.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mina anafika kwake, wapo tayari, wanamsubiria kuondoka. Akawachukua mpaka Mtwara. Akamlipa huyo mama mwenye nyumba wake, pesa yakutosha haswa, kama shukurani kubwa kwa mengi aliyomfanyia kwa upendo. Maana na hapo napo alijitolea kumuendesha mpaka Mtwara kumuwahisha uwanja wa ndege.

Hawakuwa wamechelewa sana. Wakaondoka na ndege ya mwisho kutoka Mtwara kurudi Dar. Yaani safari ya Lindi mpaka Mtwara ikawa ndefu kuliko ndege ya kuwatoa Mtwara mpaka Dar iliyochukua lisaa na dakika kumi tu, wakati ya Lindi mpaka Mtwara ilikuwa lisaa na dakika 45.

Jijini Dar.

Alitoka uwanja wa ndege na wanae pamoja na msichana wa kazi akakuta wanasubiriwa! Mpaka akatamani arudi ndani. Uzuri mtoto alikuwa akilia. Pius akamuwahi na kumpokea mwanae, akaondoka naye kabisa hapo akisikika akimbembeleza. “Pole Ayvin. Pole sana.” Akashika kazi ya kubembeleza, Mina akamshika mkono Ayan na kumsogeza karibu yake hajui pakuanzia na hao alio watoroka.

Pole na kuuguza, mama.” Alikuwa mzee Ruhinda. “Shikamooni.” Akasalimia. “Marahaba Mina mwanangu. Pole kwa kila kitu. Kujifungua na kulea mwenyewe.” Alikuwa mama Ruhinda. “Asante. Ila Ayvin ndio anaumwa, mama. Analala kidogo, anaamka na kilio. Hivi hapo homa imerudi. Tulipokuwa hospitalini Pius aliwaambia wamuongezee dawa ya maumivu, naona inaisha mwilini. Hali vizuri.” “Atapona tu. Hivi anasubiriwa huko hospitalini.” “Asanteni na samahanini kwa kuwa…” Akasita na kunyamaza. Akamsogeza Ayan karibu kama kujibaraguza tu akimwangalia mwanae.

“Ayan njoo unisalimie.” Alikuwa Andy. Moyo wa Mina ukapasuka kama kulikoanguka chuma sakafuni. Mwanae akawa kama anasita. Akazidi kujisogeza kwa mama yake. Mina akamwangalia. “Nenda kamsalimie dad.” Ndio akaenda baada ya mama yake kumuhimiza.

“Wote mna afya nzuri. Hongera kulea, Mina. Kumbe mwenyewe unayaweza bila msaada!” Akacheka kwa aibu. “Na umependeza kweli! Uzazi umekupenda.” “Naombeni tuondoke jamani. Huyu anahoma kali, inamaana ana maumivu makali.” Pius alirudi na mtoto aliyekuwa akiendelea kulia.

Sababu ya mtoto kulia na ile hali pale akawa kama amechanganyikiwa pale. Akajikuta anamfuata mtoto anayelia na kupanda kwenye gari, Ayan hayupo, Ayvin analia, baba yake ndio anaendesha na mtoto mkubwa wa Pius, Poliny, yupo pembeni. Akajua wamepatana na baba yake.

“Simuoni Ayan!” Mina akazungumza akimbembeleza mtoto. “Atakuwa na Andy.” “Tafadhali naomba mpigie, nihakikishe Pius. Sina amani.” Pius akampigia Andy. “Mina anataka kuzungumza na wewe.” Akampa simu. “Samahani Andy, unaye Ayan?” “Ninaye hapa na dada yake.” “Nashukuru. Naomba mwambie dada ampe maziwa yake. Yapo kwenye thermos. Atakuwa na njaa. Alilala njia nzima kutoka nyumbani mpaka hapa. Halafu akifika nyumbani amtengenezee chakula. Asimuache hivyo mpaka nyumbani. Atateseka na njaa.” “Sawa. Nitahakikisha. Nakushukuru Mina. Anaonekana na afya nzuri!” “Asante. Tutaongea zaidi baadaye.” Akamrudishia simu Pius.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mina, una roho ya umama wewe! Unamtoto anayelia maumivu na bado unamkumbuka kaka yake!” “Ayan ni mkimya sana. Unaweza msahau chakula, na akanyamaza tu. Lakini huyu! Mpaka majirani watajua kama humo ndani kuna njaa! Atalia kama kuna hatari ya kifo, mpaka majirani wanamjua. Ukishasikia tu, ‘Mina, humo ndani kwako hapaliwi leo?’ Ujue ni Ayvin ashasikika mpaka nje. Na kama ukitoka ukamuacha amelala, kokote uliko ukishapata simu ukasikia, ‘kwako kuna njaa,’ ujue ni yeye ameamka, akajisikia tumbo lipo tupu.”

Binti wa Pius akacheka sana akimwangalia baba yake. “Sasa unacheka nini wewe?” Baba yake akamuuliza kama anayejua anachocheka. “Mimi najua alikorithi huyu Ayvin. Pale ndani mpaka wasichana wa kazi wanajua. Chakula kiwe kinamsubiria dad, sio yeye akisubirie. Hapo hapatakuwa na amani. Muone dad mkimya hivyohivyo. Ila asiumwe na njaa. Bwana nyumba inakua ndogo, na hakuna mtakalozungumza mpaka aone chakula mbele yake.”

“Basi ndio huyu. Kunakuwa kama kuna kipimo huko tumboni kwake. Kikipungua tu, amani inapotea. Na nimchekaji huyo! Mpaka nje mtamsikia akicheka. Ila njaa ikianza tu, basi. Hana urafiki.” “Sasa kwa nini msubirie mpaka apatwe njaa? Kwa nini asiwe anakuta chakula kila wakati?” “Bado ananyonya, na amekataa chupa kabisa. Nilijaribu kuwa namkamulia, nikamuanzishia na chupa. Akishatia mdomoni, akakutana na plastiki anatema, anaanza kulia. Na hatatulia mpaka umpe nyonyo.” “Kwamba bado ananyonya tu mpaka leo!?” Dada yake akashangaa.

“Mimi nanyonyeshaga wanangu miezi sita bila kuwapa kitu chochote ila maziwa yangu tu. Akishafikisha miezi sita kamili ndio naanza kumuongezea vyakula laini taratibu. Miezi nane anakula kabisa.” “Unajuhudi Mina, huchoki?” “Ndio umama, halafu naona kama wanakua vizuri kama Ayan. Hakuwa mtoto mgonjwa mgonjwa ndio maana huyu aliniogopesha alivyoanza kuumwa. Alikuwa mzima kabisa, hana ugonjwa hata wa mafua!” Wakawa wanaongea hapo nyuma, Mina na mtoto mkubwa wa Pius. Poliny.

Hospitalini

Wakafika hospitalini wakakuta kweli wanasubiriwa. Mpaka Paul mtoto wa mwisho wa Ruhinda alikuwepo hapo hospitalini akimsubiria. “Pole sana Mina.” “Asante.” Akaishia kumjibu tu hivyo asijue pole hiyo ni ya nini kwa Paul aliyekuwa hayupo nchini wakati hekaheka za kaka zake zikiendelea. “Kwamba shule ndio imeisha au?” Akajiuliza ila alikuwa na mengi kichwani, akaangalia yake.

Baada ya muda mfupi kina Ruhinda wengine na mume wa Paulina naye akawa ameshafika hapo. Wamejaa, Mina hajui kama wamemjalia yeye au huyo mtoto aliyeondoka na mimba yake. Asijue ni mengi ya uzushi, yanaendelea. Kila mtu alitaka kushuhudia, na kuthibitisha kama kweli mtoto ni wa Pius!

 Akaanzishiwa vipimo vya harakaharaka na kumpa dawa ya kutuliza maumivu, akalala. Pius alikuwa amembeba muda wote akimwangalia kama aliyeokota lulu!

Kwenye majira ya saa mbili, akawa anaingizwa chumba cha upasuaji. “Naomba hata dakika moja tu, niombe naye kabla hamjamuingiza huko.” Mina akawahi na kushangaza kila mtu. Ikabidi wote watulie. Akainama kwenye kitanda cha mtoto wake aliyekuwa amelala. Akaanza kuomba ila kimyakimya. Akaomba kisha akamaliza. Aliposema Amina kwa sauti ya kusikika kidogo, na wengine wote mpaka mzee Ruhinda akasema Amen. “Afadhali umekumbuka kuomba Mina. Wote naona tumechanganyikiwa.” Akaongeza mama Ruhinda wakimwangalia Ayvin. Ndipo akaingizwa chumba cha upasuaji.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamsogelea Pius. “Nisaidie tena simu, nizungumze na Andy.” Akamnong’oneza ila wote wakasikia. Pius akapiga na Andy akapokea bila kuchelewa, akamkabidhi simu. “Nimemchelewa kaka mkubwa?” “Naona alikuwa akiogeshwa. Hivi nilikuwa nasubiri amalize, nimuage, nije huko.” “Naomba kuzungumza naye. Niwekee video.” Akasogea pembeni.

Akamsikia akitembea kama anayewafuata. “Mama anataka kuzungumza na wewe.” Akampa na kumuona. “Umekula vizuri?” Akamuuliza kwa upendo. Akakubali. “Maziwa?” Akanyamaza. Akamuuliza tena, akamuona na yeye anamwangalia dada yake. “Nipe dada nizungumze naye.” Akampa. “Mbona kaka hana maziwa?” “Tulikutana na foleni njiani, amemaliza yote, naona alikuwa na njaa.” “Sasa kwa nini usimuombee hapo maziwa? Hawezi kulala vizuri.” Kila mtu akawa anasikiliza japo alikuwa pembeni.

“Hapa ugenini dada, sijapazoea.” “Naomba kuzungumza na baba yake.” “Nimesikia Mina. Naenda kuangalia kama kuna maziwa, lasivyo itabidi nikanunue.” “Maziwa yapo. Mwambie dada ampe. Yapo kwenye friji. Tukiwa tunarudi tutanunua mengine.” Akageuka, alikuwa mama Ruhinda. “Asante mama na samahani kwa kuwaharibia bajeti. Lakini Ayan bila maziwa, hapapambazuki vizuri.” “Bado mpenzi wa maziwa tu?” “Naona ndio vinazidi!” Akamjibu mzee Ruhinda na kurudi kwa Andy.

“Andy?” “Nimesikia. Wakati wanampa haya, nitaenda kutafuta mengine ili na kina mama wasiishiwe na kesho akute mengine.” “Nakushukuru. Basi naomba nimuage kabla hujaondoka.” Akamrudishia simu.

“Watakupa maziwa. Sawa?” “Unarudi saa ngapi?” Wakamsikia akimuuliza mama yake. “Ayvin akipata tu nafuu, narudi naye. Usiwe na wasiwasi. Sikuachi. Sawa?” Akakubali. “Haya, funga macho tuombe. Leo si unaomba wewe?” “Nimuombee na Ayvin?” “Utafanya vizuri.” Wote wakatulia. Akaomba kwa kifupi akimuombea mdogo wake mpaka msichana wao wa kazi. Akamaliza.

“Asante Ayan na nitamwambia Ayvin kwamba umemuombea.” “Atapona haraka?” “Kwa maombi hayo! Lazima atapona tu. Kunywa maziwa, ulale.” “Lakini utarudi kunichukua na mimi tuwe wote na Ayvin.” “Sikuachi Ayan. Mtoto akipata tu nafuu, nakuja kukufuata. Usiogope. Sawa?” Akakubali lakini wazi akionyesha mashaka, lakini ikabidi amuage tu, na kukata. Kila mtu akakutana na Mina wa tofauti.

~~~~~~~~~~~~~~

Akamrudishia simu Pius. “Asante.” “Karibu. Upo sawa? Hata chakula wewe mwenyewe umekula?” Akakumbuka jali ya Pius. “Nimeshindwa! Nina hofu tokea jana hata maji hayapiti kooni. Acha nipate muda nimuombee mwanangu.” “Subiri kwanza Mina! Wewe unanyonyesha halafu huli!?” “Hanyonyi! Ndio kitu kinanitia wasiwasi hata dokta kule nilimwambia. Ayvin ni mlaji haswa, na mchekaji akiwa ameshiba. Kitendo cha kukataa kula halafu analia tu, siwezi kufikiria. Halafu mwanangu hajawahi ugua hata mafua! Leo wanaenda kumkatakata!” Pius akakwama.

Usiangalie kwa njia hiyo, mama.” Akamsikia mzee Ruhinda, akageuka. “Huko alipo jua wanamsaidia kurudia hali yake. Kisu ndio njia ya kumfanya arudi kwenye hali yake. Na nakuhakikishia yupo kwenye mikono salama sana. Na watamuwekea maji ya kumpa nguvu. Atapona kwa haraka sana. Usiogope.” “Asante baba. Acha tu nimuombee japo kidogo labda na mimi nitatulia. Sijui kwa nini, nimeingiwa na hofu kweli!” “Ni roho ya umama hiyo. Pole sana, Mina mwanangu. Atapona tu.” “Asante mama.” Akaenda kutafuta sehemu ya peke yake, pembeni kabisa, akaanza kuomba kimyakimya bila hata kutoa maneno, akiwa amejiinamia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda daktari aliyekuwa akimfanyia upasuaji akatoka. Wote wakamsogelea. “Kila kitu kimekwenda salama?” Pius akawa wa kwanza kuuliza. “Safi kabisa na…” “Subiri kwanza. Ngoja nimuite mama yake akusikie. Maana ana wasiwasi sana.” “Lakini niliwaambia msiwe na wasiwasi ni procedure ya muda mfupi na sahihi.” “Hayo hawezi sadiki mpaka kwa vitendo. Acha tu aitwe.” Mzee Ruhinda akaingilia. Pius akaenda kumuita pale alipokuwa amejiinamia.

Akasogea. Akawaelezea kwa kifupi. “Na kama tulivyozungumza, ili asirudie maumivu kwa mara ya pili, tumemfanyia na tohara kabisa.” “Ni Pius huyo anayetaka mambo yote, kwa wakati mmoja, wakati mtoto mgonjwa! Sasa si atakuwa na maumivu makali?” “Hata kidogo. Kila kitu kimeenda sawa. Tumemuweka kwenye usingizi kwa muda, ili asijitoneshe.” “Sasa yuko wapi?” “Wanamalizia, wamtoe.” Hapo Mina akavurugwa.

“Kina nani tena wanammalizia wakati wewe ndio tumekuamini naye? Hao wanao mmalizia wakiharibu!?” Wakajua ni hali ya umama na kutoelewa. “Ni utaratibu wa kawaida Mina! Huyu kazi yake imeshaisha. Lazima apishe wataalamu wengine wafanye huduma nyingine kwa Ayvin.” Paul daktari wa familia akajaribu kumuelewesha. “Kwanza hapo palipobakia hakuna kuharibika tena. Yupo kwenye mikono salama.” Akazungumza na tabasamu kubwa tu kumfariji, haikusaidia.

Mina mashozi mpaka kifuani. “Mimi sijazungumza na mtu mwingine akanielewesha na kumuelewa mtoto wangu kama wewe. Hawajamshika mtoto wangu kwa upendo kama wewe kabla hawajamuingiza humo ndani. Wamekutana naye tu humo ndani, hawamjui na hawaelewi ni nini kinaendelea. Wataanza…” “Nakuomba, rudi tu ndani. Tafadhali dokta Patel. Labda ukitoka naye, utatuliza hii hali.” Mzee Ruhinda akamsihi kwa heshima sana. Huyo daktari wa kichotara akakubali kwa heshima ya hao kina Ruhinda, akarudi japokuwa ni kweli kazi yake ilishaisha.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda kweli wakatoka naye akiwa anasukumwa na manesi, amelala. “Alivyo hivyo, isikutishe. Daktari wa watoto ameshauri aongezewe dawa ya usingizi ili atulie. Lakini tulishamuamsha ndani baada ya kumaliza kila kitu. Na nimchekaji sana.” “Hapo nimekuamini. Ayvin ni mchekaji kwa kila mtu. Na inamaana maumivu yamepungua.” Mina akadakia akionekana amefurahia.

“Asante sanaaa. Nashukuru.” “Nitapita baadaye kuwaona. Ila daktari wa watoto atakuja kuzungumza na wewe. Lakini watamuweka kwa uangalizi angalau mpaka kesho ndipo tutawaruhusu.” Akaondoka na wao wakarudishwa chumba cha kupumzika upande wa watoto.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walipomuweka tu kitandani wote wakamzunguka akiwa amelala. “Ruhinda una damu kali! Damu yako haipotei kabisa! Japokuwa huyu ana rangi tofauti, lakini hajifichi kabisa kama ni Ruhinda!” Akaongea mama Ruhinda wote wakimtizama hapo kitandani kama wapo  kwenye kivutio cha wanyama! Kila mtu yupo kuthibitisha maneno yaliyozagaa juu ya Mina aliyeondoka na huo ujauzito.

Raza aliwahakikishia kuwa alikimbia baada ya kuona atakamatwa uongo, mtoto si wa Pius. Na shutuma nyingine nyingi tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mzee Ruhinda wazi alikuwa na furaha sana. “Na anaonekana na afya nzuri kweli!” “Mlaji huyo! Na hana neno na yeyote labda awe na njaa, hapo haelewani na yeyote mpaka mimi nimshike. Mchekaji haswa. Yaani huwa akipitiliza usingizi, mimi na Ayan tunaenda msubiria pembeni ya kitanda aamke aanze kucheka. Na akifungua tu macho, akituona mimi na Ayan, anaanza kucheka haswa. Analeta furaha huyu, mpaka raha.” Mina akamsifia mwanae.

“Ni kama tu baba yake. Pius alikuwa hivyohivyo, mtoto asiye na shida.” “Sasa nani aliyekuwa na shida?” Paulina akauliza na kufanya waanze kucheka. “Kuna waliokuwa wakitaka kuwa mikononi wakati wote. Hawawekeki chini.” “Labda Paul.” “Mimi nilishaambiwa nilikuwa mtoto ninayependa kujitegemea.” Paul akajiwahi. “Huyo ni Andy. Alijua kujitegemea mapema sana.” Mzee Ruhinda akarekebisha kwa haraka sana na kufanya wacheke tena.

“Inamaana waliobaki hapo ni Paulina na Paul.” Mumewe Paulina akaongeza. “Sasa mwenye ufahamu atambue. Ambaye hapendi kuwekwa chini mpaka leo ni nani, na ambaye yupo na mama mpaka kesho, basi ndiye huyohuyo.” “Paul unanitafuta wewe!” “Kwani mimi nimemtaja mtu jina?” Vile ambavyo wazazi wao hawakukanusha tena wakajua ni yeye Paulina. Wakazidi kucheka.

Andy Kwa Mkewe.

Wakati wakiendelea kuzungumza Andy akaingia. Moyo wa Mina ukajawa furaha, wote wakamuona anamsogelea mumewe. Angalau Andy akajisikia umuhimu. Wote wakawageukia. “Poleni.” “Asante. Naona kila kitu kimeenda sawa. Wamempa dawa ya usingizi ili alale asijitoneshe.” “Pole kuuguza na kulea.” Akaendelea kuzungumza na mkewe taratibu wakiwa pembeni.

“Hatukuwa na matatizo mpaka majuzi alipoanza kulia mfululizo na hataki kula. Vinginevyo wote ni watoto warahisi kulea.” “Acha nimuone. Amefungua hata macho?” Akasogea, wakampisha kama kumpa nafasi wasiamini kwa hatua kubwa anayotaka kuchukua! Hata Mina alifurahi kumuona anataka kumuona Ayvin.

“Hapana. Wamempa dawa ya usingizi ili apumzike. Hata hivyo anaonekana alilia sana. Mpaka homa!” Baba yake akajibu macho kwa mwanae. “Aisee mmefanana! Hajachukua rangi kali ya baba, aliyotupa sisi wote kasoro wewe Pius.” Pius akacheka wote wakimwangalia huyo mtoto. “Na naona yeye atakuwa  na mwili sio kama miili yenu hiyo mikavu mtafikiri hamlishwi!” “Watoto wanabadilika mama! Anaweza kuja kurudi kwetu tu.” Paul akadakia.

“Na anakula huyu! Mkianza kulishana mpaka mgongo unauma. Na haachii mpaka amalize maziwa yote.” “Ndivyo wakina Ruhinda walivyo. Sasa mimi huo mchezo kama wako nilikuwa sifanyi. Kwanza sikuwa na maziwa mengi hivyo yakuwatosha. Miezi mitatu tu, ziwa peke yake. Matenity leave yakiisha, nikiwa narudi kazini, week moja kabla nilikuwa nawaanzishia maziwa ya chupa.”

“Hivyo niliweza kwa Ayan wangu, hakuwa na neno. Huyu, hataki kabisa. Akishajua umemuwekea plastiki mdomoni, ndio hasira zinaongezeka. Atalia hapo kama amekatwa!” “Basi atakuwa kama baba.” “Wewe mbona umenikazania mabaya yote ni mimi?” “Muulize bibi. Dad anasahani yake, kijiko, uma na kisu maalumu vya kulia. Visibadilishwe.” “Na sehemu anayokaa wakati akila, iwe hiyohiyo.” Mama Ruhinda akaongeza. “Na ni kwenye kila nyumba, iwe hivyohivyo mpaka tushamzoea Pius. Kila nyumba anaachiwa kiti chake kama baba!”

“Basi kazi itakuwepo!” Mina akaongeza. “Wala si kazi. Ni mambo ya kawaida tu. Na yeye atafika hatua ataelewa anatakiwa kutumia chupa. Au kula vyakula vingine. Taratibu si kumuharakisha. Atazoea tu.” Pius akaongeza wote macho kwa mtoto.

“Umemuacha Ayan amelala?” “Anawasiwasi huyo! Sijui kama atalala kwa haraka.” “Alipewa maziwa?” “Alipewa, lakini nayo ikawa kama hana raha nayo! Kila wakati anauliza kama utarudi kwenda kumchukua.” Mina akatulia na kurudisha macho kwa Ayvin. Wakatulia.

~~~~~~~~~~~~~~

“Nimekuletea chakula ule. Msichana wako ameniambia hujala tokea majuzi.” “Asante kunifikiria Andy. Yaani sasahivi ndio nasikia njaa baada ya kumuona Ayvin ametulia.” Wote wakajisuta, walikuwa naye huyo mama mtoto hakuna aliyekuwa akimfikiria chakula mawazo yao yote kwa mtoto japo alishasema alishindwa kuweka chochote mdomoni.

 “Basi, kaa ule. Nimekuletea na nguo za kubadili ukioga. Msichana wako amenipa.” “Nahisi wewe umetumwa na Mungu wangu. Asante Andy, mume wangu.” Andy alitamani kurukaruka kwa furaha. Pius wivu. Wengine kimya.

“Naona acha nioge kwanza, maana tokea asubuhi nilipotoka nyumbani sijatulia, na taskii yenyewe niliyokuwa nimepanda asubuhi mpaka nilishindwa kuweka pochi chini, ilikuwa chafu! Nilibaki nimepakata mtoto na pochi zangu.” “Pole.” Andy akaonekana kujali kweli.

“Itabidi uwe na gari yako. Ninunue haraka iwezekanavyo.” Hapo AKAMTIBUA Andy. “Umnunulie wewe kama nani?!” Chumba kizima kikataharuki jinsi alivyouliza. “Mimi kama Pius na baba yake Ayvin ambaye hilo jina nilishaomba lisiitwe hivyo aitwe Pius Junior Ruhinda. Lakini wewe…” “Nisikilize Pius. Mina ni mke wangu na anayo gari ambayo mimi nilishamnunulia.” “Mwanangu ataishi kwa uwezo wangu sio kwa uwezo wako Andy. Hawezi kuendesha gari ya miaka ambayo hata mtoto wangu hakuwa amezaliwa! Kwa nini haswa?” “Mmeanza! Nyinyi wawili mmeanza.” “Hayakuhusu Paulina.” Wote wawili wakamchangia kwa pamoja. Wazazi wao kimya. Mina akabaki ameduaa.

Kuliko Ungua Mpini.

Ilimuia ngumu kwa Pam kupata usingizi lakini mwishoe akalala mpaka pakapambazuka kabisa. Kimya. Mill hata hakuwagongea. Pam alioga akajitengeneza vizuri mpaka saa nne, kimya. Mwanae bado akawa anakoroma tu. Ikabidi ajitulize akijua fika Mill ameamka. Shuguli zake hufanya asubuhi na mapema.

Kwenye saa tano hivi ndipo Shema akaamka. Akaoga na kuvaa ndipo yeye akaenda kumgongea baba yake. Na kweli alimkuta alishavaa. “Njaa inauma baba!” “Nilikuwa nikiwasubiria nyinyi. Kama mama yako yupo tayari mwambie tutoke tukale.” Shema akatoka kwa haraka wakati baba yake akimalizia kufunga kompyuta zake.

Pam akaenda kumgongea na kuingia. “Nilijua bado umelala!” Akajizungumzisha. “Mimi nilazima niamke mapema. Hapa nimeshaenda mazoezini, nishafanya na kazi zangu, sasahivi nipo huru kwa siku nzima.” Ndipo akamgeukia. “Umependeza Pam.” “Asante. Na wewe unaonekana msafi!” Akasimama. Ukweli alivutia, halafu akawa ananukia vizuri. Ila akawa kama amebadilika kidogo si kama alivyokuwa jana yake.

Shema akarudi. “Nimeshabadili viatu, mama.” “Basi twendeni.” Wakazunguka hiyo siku sehemu ambazo alijua wazi zimemgarimu mno. Ukweli akawa ametulia kwa Pam tofauti kabisa na jana yake. Mazungumzo mengi yalikuwa kati yake na mwanae. Mpaka siku ikaisha. Walirudi hotelini usiku wakiwa wamechoka.

~~~~~~~~~~~~~~

“Nashauri tuwahi kulala ili kesho tuwahi kuamka kwa safari ya mbugani.” Hayo anawaambia wakiwa kwenye lifti. Akawasindikiza mpaka mlangoni, hata ndani hakuingia, walipoingia tu ndani na yeye akaingia chumbani kwake kwa mlango wa nje wala sio ule wa ndani unao ingiliana nao. Pam akajua amembadilikia.

Kimya. Akaoga yeye na mwanae na kulala. Kimya mpaka tena kesho yake. Pam alitegesha alamu ya kumuamsha,  akajitayarisha yeye ndipo akamuamsha na mwanae, alipomaliza ndipo akamtuma akamgongee baba yake. Akakuta yupo tayari mpaka na masanduku. Wakatoka na kupata gari ya kuwapeleka mbugani. Ilikuwa bado mapema tu. Wakawa na muda mzuri huko mbugani ndipo safari ya kurudi Dar siku inayofuata ikaanza.

Safari yakurudi Dar.

Safari hii kurudi Dar haikuwa imejaa furaha kama walivyokuwa wakielekea Arusha. Walisimama kila walipotaka kula na kujisaidia, vinginevyo aliendelea kukanyaga mafuta mpaka nyumbani kwao. “Kesho nitamtuma dereva aje amfuate huyu, akakate nywele. Zimeanza kutisha.” “Sawa.” Akawasaidia mizigo mpaka ndani na kuondoka bila ya kukaa wala kuzungumzia swala la kuhama. Pam naye akaona atulie.

~~~~~~~~~~~~~~

Juma likaisha, kimya. Hakuna kuulizwa lolote juu ya kuhama wala kazi. Na akawa akimtuma tu dereva kumchukua Shema na kumrudisha mpaka shule ikafunguliwa. Hakumuona wala kumsikia Mill. Ila alijua anazungumza na mwanae.

Safari hii dereva ndiye aliyekuwa akimfuata Shema kumpeleka shule, na kumrudisha. Mwezi ukaisha, KIMYA. Yeye hajamtafuta, na Mill hajamtafuta. Ila Shema alikuwa akimwambia kama huwa baba yake anamfuata shuleni mida ya chakula cha mchana na kula naye kisha anaondoka.

Pam akabaki njia panda. Hakuna mawasiliano kati yao, ila anatunza mtoto wake vizuri tu. Na pale kwake hakuonekana tena tokea alipowashusha siku alipowarudisha toka safari. Wasiwasi ukamzidi Pam. Ila akajikaza.

~~~~~~~~~~~~~~

Miezi 3 ikapita, hajamuona wala kuwasiliana. Akazidi kummiss ila hajui anajirudije. Alipoona muda aliombiwa wa kumpumzisha mkono umeisha akaanza kutafuta kazi. Alihangaika Pam mpaka akachoka, kazi hapati.

Usiku huo akaamua kumtumia ujumbe. ‘Samahani kukusumbua Mill. Nakujulia hali na pia kuulizia ile nafasi ya kazi kama bado ipo? Mkono ulishapona na ninaweza fanya kazi.’ Akatuma huo ujumbe. Akaona umefika. Ila hata haukusomwa.

Kesho yake kwenye majira ya saa nne asubuhi akapata majibu. ‘Huku kwema kabisa. Nilipoona kimya, nikajua huhitaji tena. Nikatafuta mtu wa kuijaza ile nafasi. Nilikuwa na uhitaji ambao sikuweza kuendelea kusubiri zaidi.’ Pam alipoa, mpaka akasikia baridi mwili mzima. Akarudia ujumbe tena na tena ukawa umeishia hapo. Mwanae alikuwa shuleni.

Akafikiria kwa haraka, akamrudishia mwingine. ‘Nina shida sana na kazi Mill. Ikitokea unasikia nafasi popote au kwako kukifunguka tena nafasi utakayodhania naweza fanya, tafadhali nikumbuke.’ Mill akasoma akajua inamaana ametafuta kwingi amekwama na amefika mwisho. Pam si wakujishusha. Ni jeuri. Na alimjua. Akamjibu kwa kifupi tu. ‘Sawa.’ Ukaishia hapo.

~~~~~~~~~~~~~~

Mwezi mwingine tena ukaisha kimya. Minong’ono uswahilini ikazidi, kuwa ameachwa. Wakasahau yote, ikawa sasa eti alipokutwa Mgaya chumbani kwake, eti ni kufumaniwa. Baba Shema hamtaki tena, anatunza tu mwanae. Pale alipokuwa akiishi pakaanza kuwa pachungu. Kina mama Pili wanamsema mpaka kwa majirani kwamba walimuonya, lakini amefanya kichwa ngumu mpaka akaachwa. Pam akanyong’onyea haswa.

Muda huohuo na  Shema naye akawa anafunga shule kwa mapumziko mafupi. Akarudi na bahasha. “Baba amesema usome, ukiafikiana nayo, nimjibu.” Akafurahia akijua ni kazi. Akafungua kwa haraka akagundua ni kuhusu huyo Shema. Amemtafutia kikundi cha mpira wa miguu anataka ajiunge. Alipoa Pam, asiamini. Safari hii akaamua kujishusha.

Akamtumia ujumbe. ‘Nafikiri hii timu ya mpira itamsaidia na kumuongezea ujuzi zaidi. Nashukuru kumfikiria. Na muda na wakati wowote anapohitajika kwenda, nitajitahidi awe tayari.’ Baada ya muda majibu yakarudi kwa kifupi. ‘Sawa.’ Pam akazidi kuumia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Aliyoyakimbia Ndio Anakutana Nayo Siku Ya Kwanza Mtoto Akiwa Mgonjwa Hata Hajafungua Macho Baada Ya Upasuaji.

Ila HISIA Kwa Mumewe Bado Zipo Wala Si Za Kulazimisha, Na Andy Bado ANAMPENDA sana na anaonekana KUMUHITAJI mkewe.

 Ila Bado Pius Yupo Kwenye Picha, HAKWEPEKI Tena, Maana Na Ayvin naye Yupo.

 Mill&Pam Bado Wanahangaika Kurudi Mwanzo.

Wivu, Kujihami, Hofu Ya Kuumizana TENA, Jeuri, Kila Mmoja Ameshika Pakali Japo Penzi Lipo, Lakini Uharibifu Ulishatokea. Ni Kama Washapoteza Dira.

Ni nini Kitaendelea kwa wote Love At First time?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment