Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 45. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 45.

Alipofika nchini Marekani tu, baada ya mapumziko ya siku mbili akakutana na mwanasheria wake. “Nina wazo ambalo naomba tujaribu. Mtafute mwanasheria wa Kisha. Muombe kikao na sisi, ila mwambie lazima Kisha awepo. Mimi nitazungumza na Kisha. Kwa sehemu fulani najua udhaifu wake, tunaweza kuutumia.”

“Kisha bila kumtisha hawezi kutulia na kukusikiliza.” “Wewe usiwe na wasiwasi kwa sababu katika hili nina uhakika alikuwa akijua analofanya. Sio bahati mbaya. Sitaki kukaa sana huku. Natakiwa nyumbani kwa haraka. Vinginevyo tukifuata taratibu za kawaida, nitajikuta nakaa huku muda mrefu.” “Basi nashauri angalau ufanye vipimo hata vya huku. Vyenye uhakika kabla hujazungumza naye.” Akafikiria, akaona hana la kupoteza.

Safari hii alikwenda na hao watoto hospitalini kabisa. Wakafanyiwa vipimo. Aliambiwa itachukua majuma matatu. Akatulia lakini akiendelea kuwasiliana na Shema kwa shida kwa sababu ya network huko kijijini kwa kina Pam. Akajitahidi mwanzoni na hivi mida inatofautiana, Tanzania walikuwa mbele kwa masaa nane! Mwishoe mawasiliano yakakata kabisa. Pam akajua ndio ameshakutana na wakimarekani tena, habari yake imeisha. Akapoa akijutia hili na lile.

Mill Apoteza Yote Aliyohangaikia Nchini Marekani.

Baada ya majuma matatu kwenda la nne majibu yakatoka kama ya Tanzania. Watoto hao wawili hawakuwa wa Mill. “Sasa mtafute mwanasheria wake. Mwambie ni muhimu tukutane kabla sijawafungulia mashitaka.” Mwanasheria wa Mill akafanya hivyo. Kisha kusikia kuna mashitaka, akakubali kukutana kwa haraka sana, hakujua anataka kumshitaki kwa lipi tena. Maana wawili hao walishindana kwa kushitakiana.

Mwanzoni ilikuwa ni Kisha akimtishia kwamba atamsema kwa Uhamiaji kuwa alimlipa pesa ili ampe uraia, lakini baadaye Mill akafikiria na kumgeuzia na yeye kibao kuwa atamshitaki kwa kumuomba RUSHWA ampe uraia. Na ushahidi ni pesa alizokuwa akimpa na kupokea. Katika hilo Kisha akatulia.

Mill&Kisha

Siku wanakutana Mill alihakikisha anakuja na wale watoto na mizigo yao yote ili ikitokea tu Kisha anakubali amkabidhi watoto wake hapohapo. Ila chakushangaza wakati wanajipanga kumtisha, Kisha alizungumza bila shida kuwa, “Itakuwa ni watoto wa Trey tu. Maana tulikuwa na mahusiano ya muda mrefu sana, kabla hajanitapeli na kukimbia.” Mill akaumia sana. “Kwamba wakati upo na mimi pia ulikuwa na Trey!?” “Hatukuwahi kuachana!” Alijibu Kisha bila wasiwasi maana ni kweli ilikuwa ni ndoa ya mkataba.

Mill hakutaka mengi. Akamkabidhi kila kitu cha hao watoto. “Ila huwezi kurudi kinyumenyume na kudai mali ulizokuwa umeniachia. Maana tulikabidhiana kwa mkataba. Wewe mwenyewe uling’ang’ania watoto. Sikukulazimisha. Na hata hivyo ni kama tuliuza kila kitu.” “Kwamba na ile nyumba pia umeuza, Kisha!?” “Wewe ulitegemea niendeshe nyumba kama ile kwa pesa gani!?” Mill hakutaka kumjibu. Kwa asilimia fulani alitegemea, hakuwa na uwezo wa kiakili ya kumiliki mali zote hizo. Alijua tu ni shindikizo kutoka kwa Trey. Na alijua wazi, nia ya Trey ni badaye kuja kumtapeli kama hivyo. Wakafanya makubaliano na kuandikishana tena.

Akaondoka hapo akiwa kama ametua MZIGO. Ila hangaika yote nchini Marekani ikawa imeishia kwa Kisha. Mali karibia asilimia 80 alizokuwa amehangaikia nchini Marekani na kulipa garama kubwa sana mpaka mahusiano yake na watu wake wa karibu akiwemo Pam, viliishia kupotelea kwa Kisha. Na watoto walio mgharimu pia wakaishia kwa Kisha. Aliondoka hapo akijua ndio amebakiwa na Shema tu.

Mtakuja.

Akarudi nchini na kuanza kuweka nyumba yake kama mseja sasa. Alihakikisha vile vitu vya wale watoto vyote, haachi hata karatasi yao. Akasafisha na kupaka rangi ya nyumba nzima, maana vyumbani mwao aliwapakia rangi zile walizotaka wao, wale watoto. Ilimradi tu kuwapa mazingira mazuri watulie, lakini hakuna walichothamini. Kukabadilishwa mpaka mashuka, vikabaki vyumba vilivyo safi ila vitupu kabisa ndipo akatulia.

Alifanya shuguli zake. Akaweka mambo yake sawa ofisini ndipo akajiandaa na safari ya Mlalo, Lushoto, alipo Pam na kijana wake. Akajifungasha kweli. Vyakula na zawadi za wakwe alizowanunulia pia kutoka nchini Marekani, pamoja na vitu vya Shema. Mapigo ya ukweli na nguo za michezo. Safari hii hakumsahau Pam. Ila yeye na mwanae aliwabea vitu baadhi vingine akaacha kwake.

Mapenzi!

Aliondoka mida ya mchana tu. Hakuwa na haraka na wala hakuwataarifu kama atakwenda. Alishamuuliza yule dereva aliyewapeleka. Akamkumbusha njia vizuri. Akaenda moja kwa moja mpaka alipofika kijijini kwao ndipo akaulizia nyumbani kwa mzee Shelukindo. Ilikuwa rahisi maana alishafika huko alipokwenda kulipa mahari na kufanyiwa hiyo harusi ya kimila.

Ilikuwa majira ya saa mbili usiku wakati Mill akibisha hodi hapo kwao. Walikwisha kula mapema tu, wakabaki wakizungumza sebuleni, Pam amepakata kichwa cha mwanae anasinzia. Babu yake Pam ndiye aliyekwenda kufungua.

Kwanza hakuamini. “Ni mimi Mill, mume wa Pam.” Alishituka Pam, hakutegemea! Mwili mzima ulikufa ganzi. Akabaki kama ametolewa kwenye barafu. Shema akashituka usingizini na kukimbilia mlangoni. “Baba!” “Sasa wewe utamuangusha babu yako, vipi wewe!” Bibi yake akamwambia Shema aliyempita babu yake hapo mlangoni. Na yeye alimuita babu kama mama yake.

Akakaribishwa ndani, Pam akabaki amekaa vilevile amekufa ganzi. Hata hakusogea wala kuzungumza. Yeye na mwanae walikuwa wamekaa tu chini kwenye mkeka.

Pakachangamka hapo. Maana taarifa za kurudi kwake nchini na kuwa anawatunza hao, zilitangulia hata kabla mwenyewe hajafika. Ikawa kama ameingia mungu mtu! Akasalimia wote kwa kuwapa mkono, kisha akaenda pale alipokaa Pam. Alimjua anavyokuwa. Mbaya wa kuagana na kumpokea. Hapo tayari machozi yalikuwa yakimtoka.

Akaenda kumbusu pale apendako Pam, kusudi tu. Chini ya shavu, kwenye shingo. Ili kupafikia hapo, basi uso wake huenea vizuri kwa Pam na kumsikia hapo shingoni. Sasa akimbusu ndio hummaliza kabisa. Akamuona machozi yakimtoka. “Nimerudi mama.” “Nilijua umetusahau!” Pam akalalamika akilia. “Nawezaje?! Network ilikuwa ikisumbua. Hatupatani na Shema. Mwishoe nikaona namchosha tu. Kwanza mida haikuwa ikiendana! Nikahisi usumbufu tu. Nampotezea muda wake. Pole.” Akamfuta kabisa machozi hapo mbele ya wakweze. Akajisikia vizuri huyo! Alijua keshaachwa.

“Pole na wewe kwa safari. Umekula?” “Nilinunua nyama choma nyingi, na ndizi za kukaanga anazopenda Shema na za kuchoma. Vipo kwenye gari. Ukiniongezea nyanya na tango, hapo utanikamilishia.” “Kuoga kwanza au kula kwanza?” “Kabla ya kushusha mizigo ndipo nile kisha kuoga, halafu  kulala, naomba kuzungumza na wazazi kwanza.” Pakatulia kabisa kumpa nafasi yakumsikiliza.

“Niombe radhi wazazi wangu kwa kilichotokea kati yangu na Pam. Nakumbuka kuanza vizuri nikisindikizwa na baba yangu mzazi. Lakini katika juhudi za kumleta Pam kule nchini Marekani, ndipo mambo yalipo haribika.” Akawasimulia kwa kifupi jinsi ilivyokuwa. “Na kwa hakika sikujua kama nilimuacha Pam akiwa mjamzito.” Hapo napo akajieleza. “Nilikosea tangia mwanzo, nimekosa, naomba mnisamehe wazazi wangu. Najua hata nikitoa sababu nzuri za namna gani, hazitabadilisha nilichokifanya kwa Pam na kuwafedhehesha hata nyinyi wazazi wangu.” Hapo akajinyenyekeza karibu apige goti.

“Mnisamehe. Najua nilimtelekeza vibaya sana. Tafadhali wazazi wangu, mnisamehe.” Wazee wenyewe hawakuwa hata na neno. Babu yake Pam ndio kabisa. Kwake ilikuwa kama MUUJIZA. Binti yake alitelekezwa akiwa ameolewa ndoa kama hiyo ya mjukuu wake na kanisani kabisa. Akarudishwa hapo na watoto wawili, mume hajawahi kurudi tena! Sembuse huyo mjukuu! Amemzalisha na ameshajua anamtunza mtoto wake kwa garama kubwa hivyo! Mzee Shelukindo akasamehe kabisa na kumshukuru kwa yote anayoyafanya. Mill akasimama kabisa na kuwapa mkono  hao wazee kila mmoja kisha kuendelea.

“Kipekee nikushuru mama kusimama na Pam tokea ni mjamzito. Najua ilikuwa fedheha kubwa lakini ulimbeba yeye na mtoto kwa kadiri ya uwezo wako, bila kumtelekeza! Leo Shema anao msingi mzuri wa kielimu ni kwa sababu ya msingi ulioweka wewe, kwake tokea mdogo kabisa! Na anakutambua kuwa wewe ndio chanzo cha kufanya kwake vizuri shuleni japo imekugarimu kusimama na hawa wawili. Umepoteza heshima kwa wengine kwa sababu ya kusimama kwenye nafasi yangu! Nakushukuru na hakika nitakuenzi mama yangu, daima. Asante sana. Tena sana.” “Karibu sana. Na tunashukuru kwa kurudi. Maana ungeweza potea na wala tusijue ulipo. Karibu tena. Na ujisikie upo nyumbani.” Akasimama na kumpa tena mkono.

“Maadamu mmenisamehe na kunikaribisha tena, sasa naweza shusha mizigo yangu, nikaribie rasmi.” Pakachangamka hapo. Maana zawadi zilizokuwa zimeletwa, nyumba ilijaa uhai. Kila mtu alijazwa zawadi zaidi mama Eric, kama kumshukuru na kumuomba msamaha. Vyakula pia ni kama alijazilizia tena palipokuwa kumepungua pale Pam alileta. Pakajaa shamrashamra kila mtu akihangaika pakuweka. Nyumba yenyewe haikuwa imechoka. Kawaida ya kijijini. Ya bati na vyumba vinne, alijenga mjomba wake Pam. Na hivi huwa anakujaga likizo na mkewe na watoto, walipaweka aghueni pakijijini.

“Hii hali ya hewa huku, mnaweza nifukuza.” “Kweli baba! Na vumbi hili!” Akauliza mama Eric kwa heshima. “Kabisa mama. Joto ni adui yangu mkubwa na wa kwanza. Ila ukiniweka sehemu kama hii, naweza hata kufikiria jambo, likafanyika.” Shema alishakula, lakini hapo akaanza kula tena. Nyama ya kuchoma tena! Alianza upya. Wakaendelea kula wakati Pam akimwandalia chumba.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya yote akapelekwa bafuni, ni nje tu. Akaoga bila shida Pam akimsubiria nje. “Angalia usije anguka humo ndani!” “Maji mazuri hayo! Nayafurahia.” “Ningekuwekea ndoo mbili?” Mill akacheka na kujibu, “inatosha kwa leo.”

Baada ya yote akamsaidia kurudi chumbani kwake, akataka kutoka. “Mbona unanikimbia tena!?” “Nakupisha uvae.” Mill akamwangalia kwa kumsuta. Pam akarudi na kukaa ila akawa hamwangalii.

“Vipi Shema huku kijijini? Ashapata wenyeji?” “Mmmh! Hana ugeni wowote huyo! Washamzoea. Huwa namleta huku mara kwa mara. Na ugonjwa wake huo wa mpira, hajaacha. Anakusanya watoto, kuna uwanja kule mbele karibu na shule, basi huko ndiko anakoshinda.”

“Na huku pia!?” “Hutamuweza Shema. Na hivi sasahivi ana ile mipira yake uliyo mnunulia, asubuhi wanakuja kumuulizia. Au wale wakubwa wakitoka shule, pia wanataka kucheza naye. Siku za jumamosi ndio hutamuona hapa mpaka umfuate na umgombeshe, ndio atarudi kula kama anakimbizwa. Akitoka hapo hutamuona tena mpaka jioni! Maji ya kunywa ni ya kumpelekea hukohuko!” Mill akawa anacheka.

“Pakulala?” “Nalala naye. Hajiwezi. Usingizi bila kuniona hapo kitandani, halali.” “Itabidi aanze kujifunza kulala peke yake Pam! Huyu mtoto ni mkubwa sana.” “Halafu nitapata wapi hicho chumba chakumuweka peke yake?” “Maisha lazima yatabadilika. Hamtabakia hivyo wakati wote. Tutazungumza zaidi.” “Nashukuru kwa kuzungumza na wazee. Na asante kwa zawadi zote. Zote. Kuanzia zangu, Shema, mama, bibi na babu. Babu amefurahia mashati huyo! Saa ndio hataki hata kutoa mkononi.” Mill akacheka akifikiria.

“Na asante pia kwa kuja.” “Karibu.” Akamuona ni kama ana kitu ila hawezi kukisema. “Kuna nini?” “Tutazungumza vizuri kesho. Si tunaweza toka kidogo? Si lazima sehemu maalumu! Hata huko milimani kwenye hayo maji. Nasikia huku kunasifika kwa mitiririko ya maji. Ndio twende huko.” “Sawa.” Shema akaingia na vitu alivyoletewa na baba yake. Akachangamka hapo, maneno mengi, Pam akimwangalia tu alivyochangamka.

“Kesho tunakwenda kucheza wote baba.” “Shema na mpira! Husubiri hata apumzike?” “Aliniambia lazima atachukua likizo, halafu tutapata muda. Sasa huku yupo mbali na nyumbani. Hana kazi. Tukacheze tu. Sasahivi nina viatu vipya na ameniletea mipira mingine miwili.” “Naona ungemalizia vile viatu vyeusi huku kwenye udongo mwekundu, vingine uache  mpaka tukirudi mjini.” “Sasa mtoto wako mwenyewe huyo miguu inakua mchana na usiku. Mpaka arudi mjini vitakuwa havimtoshi tena.” Shema kusikia hivyo, akafurahia sana. Miguu hiyo ilishazoea viatu chakavu, leo kubadilisha viatu atakavyo!

~~~~~~~~~~~~~~

Asubuhi Pam, mama yake na bibi yake waliamka kuandaa kifungua kinywa cha nguvu kama chakula cha mchana. Kilikuwa kikinukia, ungejua kwao kuna neema. Wakaandaa meza akaenda kumuangalia Mill.

“Kumbe ulishaamka!” “Nipo mtandaoni nasoma habari za uchumi. Napitia kujua leo soko la dunia likoje. Stock ipo na thamani gani na mengine mengi.” “Maji yakuoga yapo tayari.” “Acha nikacheze kwanza huo mpira, kulipa deni, ndio nije kuoga. Ila nitataka kusafisha kinywa na uso.” “Una vitu vizuri! Chumba kizima kinanukia!” “Ni vilevile ulivyoniacha navyo. Sijabadilisha.” “Nimeona na mimi umenikumbushia enzi! Umeniletea kama vya mwanzoni. Nashukuru.” “Pam kwa shukurani! Ulishashukuru jana, zaidi ya nitakavyokumbuka! Unafurahia mapumziko yako lakini?’

“Sana. Nikiwa hivi, huku na mama! Nadeka.” Mill akacheka. “Hajui umeshakua, na una mtoto anayekuzidi mpaka urefu?” “Naona mimi na Shema wote tunadekezwa. Njoo uoshe uso upate kifungua kinywa.” “Mbona simsikii Shema?” “Huyo mpaka saa nne kwenda saa tano. Analala kama aliyekufa. Sasahivi si muda wake. Na namuacha makusudi ili huo mwili upumzike, maana najua akimka tu, mpira.” “Njoo nione mkono.” Mill bado alikuwa amejilaza na kujifunika ndani ya chandarua.

Akakifunga vizuri, Pam akasogea. “Naona nje kumepona kabisa. Labda huko ndani kama alivyoniambia dokta. Nje kunaweza funga, lakini ndani kukachelewa. Ndio nachukulia taratibu.” “Kaa hapa tuone.” Akimuonyeshea pembeni ya kitanda. Akakaa taratibu.

Mill akajinyanyua kutoka kwenye mto na kumvuta mkono. Jinsi alivyomshika akimpapasa ili kutizama huo mkono, mwili mzima wa Pam ulikuwa ukisisimkwa mpaka akahisi anamfanyia makusudi! Alimpapasa kama alivyokuwa akimfanyia kitandani. Pam akashindwa kuvumilia, akasimama kwa haraka.

“Si unaona unavyoendelea vizuri?” Mill akacheka taratibu kama kwa masikitiko akitoka kitandani. Jamaa alikuwa amesimama wima mpaka Pam akabaki ameduaa. Akaona bora atoke. Mill kawakwa tamaa kwa kumshika tu, na yeye kabadilika hisia kwa kushikwa tu mkono! “Acha nikuandalie maji.” Akawa kama anakimbia hapo chumbani.

Mungu Asiyechunguzika & Asiyetaka Msaada Anapofanya Yake

Muda wake wa kujifungua ulipofika, hakujua. Maana alianza maumivu ya kawaida tu jioni akiwa na mwanae nje, ndani ya geti. Ayan anazunguka na baiskeli, yeye amekaa akimwangalia. Vile mwanae alivyokuwa akifurahia, akaona asimkatili, akapuuzia yale maumivu. Ni kama yakaisha, asiwe na habari ni uchungu. Yakawa ni maumivu ya kuja na kuondoka.

Usiku wa saa sita wamelala, ndio vikazidi. Ikabidi ampigie simu mama mwenye nyumba wake. Naye kwa kuwa alishajua ni mjamzito wa kujifungua wakati wowote na yupo peke yake na watoto tu, akiwepo Ayan na huyo msichana wa kazi naye mdogo tu, hakuchelewa.

Kufika, hali ya Mina ni mbaya, mtoto anachungulia kabisa. “Mina, kichwa cha mwanao nakiona kabisa! Kwa nini umechelewa?” “Sikujua kama ni uchungu anti! Nisaidie nijifungue tu hapahapa nisije ua mwanagu.” Ni mama mtu mzima anafahamiana na watu. Hapohapo akampigia simu nesi anayemfahamu. Akawa akimuelekeza chakufanya na yeye akakimbilia hapo. Wakamsadia Mina.

Yule mtoto aliyekuwa akisubiriwa na wakunga WAMAANA. Walioandaliwa kwa pesa nyingi, baba yake akitaka uzembe wowote usitokee siku ya KUZALIWA kwake, akazaliwa nyumbani. Tena akizalishwa na mama mfanyabiashara tu, hana elimu yeyote ya unesi na kuja kumaliziwa na nesi wa kawaida tu.

 Ila wakashangaa Mina hataki kwenda hospitalini. “Kwani mimi na mtoto ni wagonjwa?” “Hapana Mina! Ila unatakiwa kwenda kuangaliwa! Kuandikishwa tarehe na jina la mtoto!” Hicho ndio alikuwa akikwepa, wao wasijue. “Nitakwenda lakini sio leo, anti. Acha nipumzike.” Wakamsaidia usafi na uji wa mzazi. Na kwa kuwa aling’ang’ania kutokwenda, wakaona wamuache tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kumbe Mina akili kichwani. Alijua akienda tu hospitalini kwa haraka, na kumuandikisha huyo mtoto, kina Ruhinda wanao fahamiana na kila mtu, kila sehemu, wanaweza pata taarifa kwa urahisi, wakampata, na yeye hakuwa tayari kurudi Dar. Maisha na wanae yakaendelea bila shida.

Hakuna Marefu Yasiyokuwa Na Ncha.

Watoto wake wakaendelea kukua na yeye ametulia. Mina akang’aa kwa uzazi usio na stress. Anafanya anachotaka na wanae, hana shida pesa si ipo! Akaendelea hivyo mpaka Ayvin alipofikisha miezi karibia 6 ndipo akambadilikia vibaya sana.

Akaanza kulia mfululizo. Siku na hiyo alilia usiku mpaka panapambazuka! Mina hajalala anabembeleza tu. Asubuhi akawa ameshikwa homa ndipo ikabidi kumpeleka hospitalini. Baada ya vipimo vya muda akagundulika ana henia, anatakiwa kufanyiwa UPASUAJI ili kumtibu.

Hofu ikamuingia Mina kupita kiasi. Mtoto wa Pius aliyekuwa akimpigania na fujo zote zile! Hajawahi kumuona hata mara moja! Iweje MAKOSA yatokee chumba cha upasuaji, mtoto afe hajamuona baba yake wala Pius mwenyewe hajamuona mwanae! Akabaki amekwama. Anafanya nini kwenye hiyo hali! Akabaki akiwaza mbele ya daktari aliyekuwa akimpa maelekezo na mtoto bado akiwa analia, anatakiwa kutoa maamuzi ili mtoto atibiwe.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni Nini Afanye Mina Katikati Ya Hali Hiyo?

Katika Wote Aliowaacha Nyuma, Nani Ampigie Simu Kwanza Kueleza Ugonjwa wa Ayvin?

Au Afanye Maamuzi Magumu Kumuingiza Mtoto Chumba Cha Upasujia, Tena Huko Hospitali Ya Wilaya, Halafu Mengine Yaje Yajijibu Baadaye?

Inaendelea....


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment