Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 43. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 43.

Siku moja kabla ya safari. Mida ya saa nne dereva akawa ameshawasili. Shema alikuwa anakuja kuchukuliwa na baba yake mida ya mchana. Alikuwa anamuacha hapo akimsubiria baba yake. Dereva akagonga na kuingia ndani.

“Nimeambiwa nikukabidhi na hii bahasha. Nitakuwa hapo nje nikisubiria. Utakapokuwa tayari, utanikuta hapo nje.” Pam akapokea. Alipotoka tu akafungua akijua ni pesa. “Sasa pesa yote hii ya nini!” Akashangaa. Mara mama Batuli akagonga.

“Tunaweza kuzungumza?” “Karibu japo natoka.” “Sitakuweka.” Akaingia na kukaa kabisa. “Kaa nikwambie kitu.” Pam akakaa akiwa amekunja uso. “Hili tulikuwa tukiliongea na mama Pili. Nikasema nitakwambia.” Pam kimya akimsikiliza.

“Pam wewe ni mdogo na ni mzuri mdogo wangu. Ila umeshazalishwa na baba Shema. Matunzo unayoyapata sasahivi, ni kwa sababu hana anayemshika mkono. Akija pata mwanamke mwenye roho mbaya, hata kama nia ya kumtunza mwanae ipo, mwanamke akamkoleza vizuri, mengi unaweza usiyaone kwa wingi huu.”

Ukishikwa mdogo wangu, shikamana. Makosa yanaweza tokea, lakini kama mwenzio amejirudi, samehe. Najua mpo kwenye mahusiano na Mgaya. Wewe unataka ukaanze upya? Baba Shema lishakuwa jini likujuwalo. Halikuli likakwisha. Endeleza hapohapo.” Kimya.

 “Watu wa baya Pam wewe! Eza pata mwanamke akampeleka kwa wataalamu, wakamfunga akili huyo, asikae akakukumbuka tena. Lakini ukikaa mwenyewe jikoni, unayo jeuri ya kupakua utakavyo! Ni hilo tu. Akili kumkichwa. Mjini hapa!” Alizungumza na lafudhi yake laini ya pwani. Akaondoka bila ya kujibiwa, ila akamuacha ametulia akifikiria.

~~~~~~~~~~~~~~

Alishampa Mill maneno machungu kwa hasira. Mill ameyatunza moyoni na yeye ni kama hataki tena. Anajirudije kwa Mill anayeondoka nchini!? Akawaza na kuamua kuyaacha tu. Akaondoka kwenda kufanya manunuzi, kijana akimsaidia kama aliyeambiwa ahakikishe asinyanyue kitu.

Alinunua vyakula vya kutosha ili huyo mtoto wa Mill asiende shinda njaa huko kwao kama mwenyewe Mill alivyosema. Akanunua zawadi mpaka kwa babu yake! Pesa si ipo! Yale mahitaji ya muhimu aliyojua kwao wanahitaji lakini hakuwa na uwezo, safari hiyo alifanya. Kuja kumaliza, gari nyuma imejaa. Anapangaje kwenye masanduku kusafirisha kwa basi! Akawa amekwama.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wanarudi ilishakuwa jioni kama ya saa 10 hivi. Foleni na manunuzi mengi wakajikuta wanafika Tandika mida hiyo. Akakuta gari ya Mill imeegeshwa pembeni kidogo ya nyumba. Akajua yupo hapo anamsubiria. Akashuka garini, akaenda kwenye gari yake.

“Shema yuko wapi?” “Tumerudi hapa, nimekuta kundi la watoto wakimsubiria. Ameingia ndani kubadili nguo, ameondoka muda si mrefu.” “Yaani Shema na mpira jamani! Hachoki!” “Na wanampenda kweli wenzie! Wakimuona ndio kama siku imeanza.” Akacheka na kutulia.

“Nashukuru kwa msaada wa pesa.” “Umepata kila kitu?” “Naona nimezidisha pia. Walikuwa na mahitaji huko nyumbani, ila uwezo ndio sikuwa nao. Nikawa nawaambia wanipe muda. Leo nimejibana mpaka nimewapatia kila mmoja mahitaji yake. Nashukuru, ila ujue naenda kuwaambia ni zawadi kutoka kwako.” “Haina maana Pam!” “Kwangu inamaana Mill! Unanijali mimi na Shema. Asante.” Mill akamwangalia kama hajamuelewa sawasawa. Kama aliyejirudi vile!

Pam akashindwa azungumze nini tena, ila kuaga. “Acha nikuache ukaendelee na shuguli zako.” Akabadili mazungumzo akiaga. “Nina wazo. Ila kuwa huru kukataa kama vitaingiliana na mipango yenu.” “Mill! Sina mpango na Mgaya! Na siendeshi maisha yangu kwa kupitia yeye! Ni uhusiano wa kawaida tu. Lakini si kama napanga naye mambo!” “Ingekuwa mimi nisingechukulia kawaida. Mtu anayekufaa kipindi cha ugonjwa! Uliyemchagua kuwa karibu yako kipindi cha uhitaji wako na yeye akatoa muda wake kwa ajili yako! Sidhani kama ni mahusiano ya kawaida.” Wivu tu.

“Lakini tuyaache hayo. Hayanihusu tena.” “Unamaanisha nini!?” “Mimi mbaya! Nina laana ya kwetu! Nipo kama baba yangu! Nataka kukufanya mama Kenny! Nakuona mjinga! Kweli kuna unalotaka kulisikia tena kutoka kwangu?” Pam akashindwa hata kumtizama, akainama hapo dirishani alipokuwa amekaa Mill.

“Huyu dereva ni mzuri sana. Mtu mzima na ametulia. Naweza kumuomba awasindikize mpaka nyumbani Lushoto, kisha kurudi kuja kuwachukua. Itasaidia kuwa na safari tulivu. Unaonaje?” “Nitashukuru.” Alijibu akiwa bado ameinama.

“Basi kesho mida ya saa moja asubuhi nitamwambia awe ameshafika, asaidie kumalizia kupandisha mizigo kwenye gari, muondoke.” “Asante. Nashukuru.” Akabaki ameinama. Mill anaona tu kichwa. Wakatulia kidogo, akaona aage. “Usiku mwema. Na mkisafiri muwe nasafari njema.” “Na nyinyi. Mwambie Shema anipigie mkiwa njiani. Na nitakuwa nikiwasiliana na dereva pia kumkumbusha awe makini huko barabarani.” “Sawa. Asante.” Pam akaondoka bila hata kumwangalia.

Barua Kwa Mill.

Maneno anayo rudiarudia Mill aliyomwambia akajua yamemuumiza sana. Na kadiri alivyokuwa akiyarudia kwake akayasikia machungu hata masikioni kwake yeye mwenyewe. Kumtafuta kwa simu, aibu. Alishamkatalia namba. Sasahivi amempa mtoto wake simu, anawasiliana na mtoto wake, hana tena shida na kumtafuta. Na maneno ya mama Batuli akajua yanaweza kuja tokea. Akamwandikia barua ili dereva akirudi aje ampe.

‘Mill, ni mengi yametokea katikati yetu. Nasikitika umerudi umekutana na Pam aliyejeruhiwa nafsi. Imejaa uchungu na kusalitiwa. Lakini sio sababu ya kukurushia maneno mabaya. Nimekosa, naomba unisamehe. Nisamehe kukufananisha na baba yako pamoja na babu yako.’

‘Huna laana, ila mimi nahisi ndiye mwenye laana kama mama yangu. Imekuwa ngumu kwetu kubahatika kama wanawake wengine. Tafadhali naomba nisamehe. Sitarudia kusema hivyo. Naamini Mungu atakusaidia kama unavyoomba kuja kuwa mume mzuri, kwani nimekuona jinsi ulivyo baba mzuri kwa Shema. Nashukuru. Asante.’

‘Swala la Mgaya nalo pia naomba unisamehe kwa mazingira uliyoyakuta siku ile. Nilishazungumza naye, na nimemuweka sawa. Ameelewa. Kwa hiyo ile hali haitajirudia tena. Tafadhali naomba unisamehe. Kwangu si dangulo. Na mimi namuheshimu sana Shema. Sijawahi fanya lolote la kumfedhehesha mwanangu.’

‘Naomba msamaha kwa yote niliyokuumiza. Nakuahidi kubadili maneno yangu ili yasiendelee kukuumiza. Samahani na asante kwa yote unayotufanyia mimi na Shema. Asante. Nakutakia kila la kheri kwenye maisha yako. Pam.’

Akaifunga vizuri na kuiweka. Mama Pili akaingia kumsaidia kufungasha, kisha akaja mama Batuli. Vicheko na mengi yakaendelea mpaka wakamaliza. Pam amekaa tu anawaelekeza. Akawashukuru kila mmoja akaenda kulala.

Safari ya Lushoto.

 Saa moja kamili dereva akawagongea. “Na baba Shema yupo nje. Na yeye amesema amekuja kuwaaga.” Shema alivyosikia tu hivyo, akatoka kwa haraka. Alipendeza huyo! Maana baba yake alimpeleka tena kwenda kunyoa. Mama yake alimuamsha siku hiyo alfajiri. Akaoga na kumpa track suite nyeusi alinunuliwa na baba yake na sneakers nyeusi zenye nyekundu kidogo. Akapendeza, ungejua ni mtoto wa Mill.

Pam akamkabidhi yule dereva vitu vyote kisha akatoka na kufunga mlango wake. Akakuta shoga zake wameshaamka wametoka kumuaga. “Utafikiri mwali! Umependeza sana mama Shema.” “Najitahidi kumtia moyo mama yangu. Akiniona, afurahi.” Wakataniana hapo kisha kuagana nao, ndipo wakatoka wakimsindikiza. Na wenyewe wakashangaa kumuona baba Shema hapo nje.

“Sasa huyu Shema anapanda gari gani?” Wakawa wanaulizana wakitamania maisha hayo mapya ya wenzao. “Anasalimia tu.” Mill akashuka garini alipowaona. Yeye Pam alivaa gauni zuri, ila refu juu mpaka chini. Japokuwa mwili uliisha, lakini lilimkaa mpaka mate yakamtoka Mill. Nywele alishasukwa rasta ndogondogo na mama Pili. Siku hiyo hakufunga kitambaa. Na hivi alisikia Mill yupo nje, akaziachia kusudi kumrusha roho. Akaweka na hereni na lipstick nyekundu. Bwana Pam alipendeza! Ungejua kuna neema.

“Umependeza sana Pam!” Mill kama kawaida yake, hajiwezi kwa huyo mrembo. Na kwa asili alipenda vitu nadhifu. Sasa siku hiyo Pam akajiweka sawa mpaka akakubali. Yaani tangia wanakutana baada ya kurudi nchini, siku hiyo ndio anamsifia mbele ya wenzie.

“Asante. Lakini usingedamka mapema hivi! Ungepumzika tu.” “Naona bora hivi nikishawaona mmepanda kwenye gari, nitaridhika. Umembembea huyu masweta yakumtosha?” “Nimebeba, na nishampa dereva amuwekee moja kwenye gari. Atakua sawa.” “Mnakwenda nyumbani, hakuna haraka. Tafadhali msisitize huyu, asije pata tamaa ya kuwahi kufika ili ageuze kwa haraka.” “Nimesikia. Na nitakuwa makini. Mbona tutafika tu salama, wala usiwe na wasiwasi.” Akajibu huyo dereva.

Akaenda kumtoa Shema garini. “Usiache kunipigia. Kila baada ya masaa…” “Mawili.” Akamalizia Shema akicheka. “Kumbe maagizo yote anayo!” Mama yake akasikia. “Nakumbuka kila kitu. Asante baba. Na wewe usafiri salama. Ningekuwepo ningekusindikiza.” Mill akacheka. “Tutapanga safari nyingine, tutakwenda wote. Na wewe ukapaone huko.” Akafurahi Shema. Baba yake akamkumbatia kwa muda na kumsindikiza garini.

“Funga mkanda wakati nakuona. Na huo mkanda usitoke hapo mpaka gari iwe imesimama, unashuka.” Pam akashangaa kuna mito na blangeti kabisa. “Hivi vyote ni vya humuhumu?” “Nimewanunulia ili mpate pakujiegemezea, mlale mkichoka.” “Nashukuru kujali Mill. Asante.” Shoga zake wakamuaga wakishangaa kwa kuchungulia mpaka ndani ya gari.

Akamsogelea Mill. “Hii ni barua yako.” Mill akamwangalia machoni na kuipokea akimuuliza. “Ndio talaka yangu rasmi?” “Utaisoma na nina maanisha kila neno.” “Sawa.” Akaiweka mfukoni. Kisha akampa mkono wala si kumkumbatia. Kiroho kikamuuma kidogo Pam, ila akampa na yeye mkono. “Muwe na safari nje, na mapumziko mema. Gari itakuwepo tu nyumbani. Ukihitaji kurudi, mpigie, atakuja kuwafuata.” “Nitafanya hivyo. Asante.” Pam na mwanae wakaondoka. Safari hii kwa heshima si kama safari nyingine.

~~~~~~~~~~~~~~

Picha ya Pam vile walivyoagana ikawa ikimsumbua. Ukweli Mill alimpenda sana Pam. Akakumbuka ile barua. Alipofika tu kwake hata ndani hakuingia. Akaanza kuisoma garini. Akarudia tena na tena. Hakupata dawa ya kile, kinachomsumbua rohoni.

“Inamaana hawa wawili wapo na mahusiano halisi!” Wivu ukazidi kumsumbua. Mgaya na Pam! Akazidi kuumia kwa wivu. Akabaki akiwaza garini. Shema akampigia. “Umefika salama nyumbani?” Akajisikia kufarijika, mwanae kumjali. “Nimefika salama. Na nyinyi?” “Tupo salama. Nataka kulala, ndio mama ameniambia nikupigie kwanza kabla sijalala, nijue kama umefika salama.” Akacheka aliposema ukweli.

“Haya nashukuru. Wewe lala. Utanipigia ukiamka. Na mwambie mama asante kwa kujali.” Angalau Pam akafurahia hilo ila kujiuliza kama alisoma barua yake. Wawili hao wakageuka wa miaka ya 90. Kwa wote kushindwa kujishusha. Pam aliombwa simu akakataa, baadaye akajuta, ila kushindwa kumpa tena. Mill naye alinyimwa mara moja, jeuri hataki kubabaishwa. Ila Pam anamtaka.

~~~~~~~~~~~~~~

Pam na mwanae wakafikishwa kijijini salama. Dereva aliposhusha vitu vyao vyote, yeye akageuza kurudi Dar. Huku nyuma Mill anawaza kurudi Marekani, kukaa muda wote huo, akisubiria majibu ya DNA, kisha tarehe ya mahakama! “Nitarudi Pam akiwa ameshaolewa, mwanangu alelewe na Mgaya.” Akaendelea kuwaza akikusanya vitu vya hao watoto akiwa hana uhakika kama atarudi nao au la. Kisheria walikuwa wake wakiwa wameandikishana mpaka mahakamani.

Lakini Mwanasheria alimpa moyo kwamba huo mkataba utakuwa void kwa sababu aliingia akijua watoto ni wake. Pam alishakataa kuwa mama Kenny. Inamaana hataki kuja kuwa mama wa hao watoto. Akazidi kuwaza Mill huku akijiandaa na safari.

Pam hakuwa akijua hapo anapopita Mill. Kubambikiziwa watoto wasio wake, na hata hao watoto hawakuwa wakijua linalowasubiria mbeleni au kwa nini wanarudi Marekani. Walijua ni kutembea tu. Jeuri, wanaishi na Mill akiwatetemekea, wasijue kama Mill amefika mwisho.

Kwa Mina.

Kitumbua Kishaingia Mchanga.

Mina akajua kwa hakika kitumbua kimeshaingia mchanga. Taratibu bila kutoa sauti, akarudi juu kwenye chumba alichokaribishwa. Akaingia bafuni akihema. Akaanza kufikiria kwa haraka. “Hapa hapatakalika tena.” Akawaza Mina. “Si sawa kwa Raza wala watoto wake. Itakua mimi nachukua nafasi yao hapa.” Mina akaendelea kuwaza akajisikia uchungu sana na kuanza kulia. Alilia sana akijutia maisha machafu aliyoishi zamani.

“Hakuna atakayeniamini tena, na utabiri wa wengi umetimia. Kweli nishachanganya wanaume na ndoa imeshindikana!” Akalia Mina akijilaumu sana. Mwishoe akasikia mlango wa chumbani unagongwa taratibu kama mtu anayetaka kujaribisha kama yupo macho au amelala asimsumbue.

~~~~~~~~~~~~~~

Akaosha uso kwa haraka na kutoka. Akafungua mlango. “Nilijua umelala! Nimekuletea chakula.” “Nilikuwa chooni mama. Ingia tu.” “Hili jicho ni lakuangaliwa tena na daktari wa macho. Sijalipenda linavyoendelea.” “Na linauma pia.” Mama Ruhinda akaliangalia tena. “Sio zuri kwakweli.” Akamfuta na tissue.

“Kula ulale. Tutazungumza. Kama twende kwa daktari leo au kesho.” “Lakini mama, naona mimi niondoke tu hapa.” Mama Ruhinda akashituka sana. “Kwa nini, na uende wapi!?”

“Sikuwa nimefikiria vizuri. Si sawa kwa Raza na watoto wake. Hapa ni nyumbani kwao. Kwa mimi kuwepo hapa ni kama nitawanyima uhuru. Mimi ninapo sehemu ya kuishi pamoja na watoto wangu, kwa muda mpaka wote tutakapojua chakufanya. Tafadhali mama yangu. Acha mimi niondoke ili kuleta amani. Ndoa yangu imeharibika, sitaki na ya Pius iharibike.”

“Nisikilize Mina, najua kuna uliyosikia, umeumia. Lakini ndoa ya huyo Pius ipo hivyohivyo tokea zamani. Inabadilika vijimambo tu. Wewe sie utahayesababisha lolote, na Raza si muondokaji kwa Pius. Hata iweje, ile ndoa si yakuvunjika. Atatulia tu.” Mama Ruhinda akamtuliza.

“Raza anapenda kuhamisha maneno na kila mtu anamjua, ndio maana hata mumewe hakutaka kumsikiliza.” “Lakini mama, kwa asilimia fulani alichozungumza Raza, hakukosea. Yupo sahihi.” Mama Ruhinda akashituka zaidi. Akidhani mtoto si wa Pius.

“Unamaanisha nini!?” “Kabla sijaolewa na Andy, ilibidi kumwambia historia yangu ya nyuma. Sikuwa nimetulia mama yangu. Nilikuwa mtoto mbaya, ndio maana nikashindwa hata kusoma. Lakini mama, nilitulia kabisa. Nikabadilika na tokea niwe na Andy, sijawahi kuwa na mahusiano na mwanaume yeyote yule, na Mungu wangu ni shahidi.” Akamuona mama Ruhinda amehema kwa nguvu.

“Ni maisha ya zamani mama yangu.” “Nisikilize Mina. Naomba utulie. Kama ni maisha ya zamani, na mumeo alijua na bado akakuamini kiasi cha kukuacha hapa mjini, inamaana alijiridhisha na tabia zako za sasa. Naomba utulie hapa. Kwanza hapa utakuwa na uangalizi mzuri, na wanao wapo kwenye mji wao. Ninachotaka kukwambia ni kuwa, haitakuwa rahisi hata kidogo. Na ninajua kwa sehemu unamfahamu Raza. Si ndio?” “Kwa kumsikia tu.” “Basi kama ulikuwa ukiomba, omba haswa. Huwa hajui kutania, na huwa hakubali hata iweje Pius akawa na mwanamke mwingine.” Mina akawa ameelewa kwa kiasi ila akataka uhakika.

“Nitakuja kukwambia habari za Raza na huyo Pius, acha niende nikamwangalie Ruhinda nijue anahali gani. Lakini usiondoke hapa hata iweje. Tulia tuli, jiuguze, uhudumiwe vizuri. Ruhinda si mnafiki. Akikupenda, amekupenda. Yeye ameruhusu uwe hapa, ujue atasimama na wewe kwa kuwa anakupenda. Tulia kabisa, na uwe na msimamo.” Mina akanyamaza akiwa hajaridhika kabisa moyoni. Bado akaona kuwepo pale si SAWA.

~~~~~~~~~~~~~~

Akakumbuka jinsi Poliny alivyomfukuza baba yake. Na alijua huyo binti si kipenzi cha Pius tu, hata babu yake alimpenda sana. Alikuwa binti aliyetulia, haiba nzuri na hapo kwa babu yake alipapenda sana. Akakumbuka maisha aliyowakuta nayo hapo kabla hajaolewa. Kupika pamoja japo wote wanao wafanyakazi. Lakini mlo wa jumapili walifanya kama kijidesturi chao wao wanawake kupikia waume zao na familia, siku hiyo! Umoja waliokuwa nao. Utulivu wa aina yake! Akajua utabiri wa watu utazidi kutimia kuwa huwa akiingia mahali, lazima avuruge.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati kila mmoja anataka kwenda kulala, ili waimalize hiyo siku ndefu, mama Ruhinda akaingia chumbani kwa Mina kumuangalia. Hakumkuta vizuri. Kichwa bado kilikuwa kikimuuma japo alishampa dawa ya maumivu. Akaamua kumpima pressure, akaikuta ipo juu sana. Akaingiwa na wasiwasi, akajaribu kumtuliza kwa hili na lile baada ya kumpa dawa ya usingizi, akamuomba alale kabisa na kesho yake ndipo waende hospitalini kwa ajili ya hiyo pressure na jicho. Akamuacha ili alale.

Lakini alishindwa kulala usiku huo kwa mawazo. Alimwangalia mwanae jinsi alivyolala pale kitandani na yule wa tumboni, akabaki akiwaza.

Akakumbuka ushauri mgumu aliopewa na mama yake siku aliporudishwa na Andy akiwa ni mjauzito. Asisumbue watu, akaanze kambi yake na wanae wa baba tofautitofauti! Akaona huo ndio wakati mwafaka wa kuutendea kazi.

Maamuzi Magumu.

Alikaa akiwaza mpaka kama kwenye saa tano usiku bila ya kupata usingizi ila kukubaliana na wazo lake. Nyumba ilishatulia. Wazee hao hulala mapema, kwa hiyo walishalala. Akaenda getini na kuomba mlinzi amtafutie taksii na kumwambia isubiri hapohapo nje, wasiingie ndani, wasije kuamsha watu. Akaanza kutoa vitu vyake na mwanae taratibu tena kwa kunyata akitumia mlango wa jikoni. Jumba hilo ni la gorofa, vyumba vya kulala vipo juu. Mlinzi akamsaidia kupandisha kila kitu garini. Akambeba na mwanae, Mina akaondoka hapo bila wenye nyumba kujua.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kila mtu Maji yamemfika shingoni. Itakuaje?

-          Mill atafanikiwa kushinda kesi na kumrudishia Kisha watoto wake?

-          Mgaya yupo pichani, ameshakuwa kizuizi kati yao. Watafanyaje?

-          Kwa Mina na wanae? Huku ametahadharishwa juu ya Raza kuwa ajipange haswa, hakubali mwanamke mwingine kwa Pius. Ki vipi!? Japo Pius anaonekana kummudu, Ila kwa aliyoyasikia, Raza si wakuchezea.

-          Je, Kwa Pius anayemtaka huyo mtoto? Aje asikie Mina ameondoka na mwanae hajulikani alipo!

-          Kwa Andy je?

Usikose Muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment