Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 42. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 42.

Walipigana hao kaka wawili mbele ya wazazi wao kama mabondia ulingoni, mwishoe mzee Ruhinda akawaamulia kwa kuwachapa makofi kila mmoja kama watoto wadogo ndipo wakatulia, na ndipo wakafanikiwa kwenda kulala bila maelewano.

Asubuhi.

Mzee Ruhinda aliwakatalia kabisa Andy na Pius wasiongozane nao hospitalini, wabaki. Na mama yao akawaonyesha tena ile picha aliyompiga Mina usiku uliopita kama kuwakumbusha madhara waliyomuachia Mina. Wakatulia. Walifika hapo hospitalini, jicho la Mina lilikuwa limevimba haswa mpaka wakashangaa. Hakuwa akiweza kufungua tena. Lilijaa mpaka shavu lilivimba.

“Mungu wangu!”  Akasikika mama Ruhinda. Ikabidi mzee Ruhinda kuzungumza na daktari, akamwambia asubuhi hiyo Mina ameamka pressure ipo nzuri kabisa ni hilo jicho tu, nalo alimwambia walipe muda litakuja kurudia hali yake. Daktari akawatia moyo.

“Naomba niwaombe kitu wazazi wangu.” Mina akaanza taratibu wakiwa wanasubiria kuruhusiwa. “Karibu Mina, mama.” “Kwa sasa kama mnavyoona, hali sio nzuri. Naomba kama itawezekana, nije niishi kwenu kwa muda mpaka hii hali itakapotulia.” Akaona wanaangaliana.

“Lakini kama haitakuwa sawa, nitakwenda kuishi kwangu mpaka nitakapojifungua.” “Hapana. Naona mawazo yako yamekuwa kama ya mama yako hapa. Alifikiria hivyo hivyo.” Angalau Mina akalifurahia hilo. “Lakini lazima nikazungumze na Andy. Nitaondoka na Ayan.” Hapo wakapoa. Wakaona wamuachie yeye mwenyewe.

~~~~~~~~~~~~~~

Walifika nyumbani kwa Andy wakamkuta na Pius yupo. Mina akashangaa, akajua lazima atakuwa ameambiwa na wazazi wake awepo hapo. Lakini hakuwa hata na hali ya kulifikiria hilo. Akaingia na kwenda kukaa moja kwa moja. Wote wakashituka sana kumuona vile. Alivimba uso, zaidi upande ule wa jicho lililoumia. Usingeweza kumtambua Mina vile alivyo. Alitisha sura na kuogopesha kumtizama.

          “Pole sana Mina.” Andy akamsogelea akataka kumshika, Mina akasogea kama kumkwepa. Wote wakaona. “Sikukusudia kukuumiza Mina! Samahani sana.” “Ulitafuta njia yakumlipa kisasi. Acha uongo.” “Tafadhali Pius, nyamaza.” “Sitaki amdanganye Mina, baba. Andy ni hatari. Amebeba chuki kwa Mina, anaweza kumdhuru yeye na mtoto wangu. Mwangalieni alivyo Mina sasa hivi. Halafu niambieni ni kwa jinsi gani mwanangu atapona kwenye mikono yake huyu! Kuweni wakweli na mniambie. Andy amejawa chuki, hawezi kujisaidia.” “Nakuonya Pius wewe!” “Utanipiga tena?” Pius akamuuliza Andy.

Mina akasimama kuelekea chumbani kwa mtoto wake. “Mina!” “Naona niondoke kwa muda Andy.” Andy naye akasimama na kumfuata nyuma. “Mbona nimekuomba msamaha!” Mina akasimama na kumgeukia wakiwa wamefika koridoni karibu na kuingia chumbani. Watu wa sebuleni hawawaoni lakini wanaweza kusikia.

“Mina?” “Sio hivyo tu Andy. Hii hali ni ngumu, mimi nakuelewa na wala sikulaumu. Nimeishi na wewe nimeona jinsi inavyokuwia ngumu Andy. Najua nia unayo, lakini uhalisia nao unakuvuta nyuma.” “Nakupenda Mina!” “Hilo nalijua. Najua unanipenda sana, mimi kama Mina. Lakini mambo yamebadilika Andy, tuwe tu wakweli. Sio kama zamani. Unaogopa hata kunikumbatia kama zamani ulivyokuwa ukitaka nilale mikononi mwako kipindi chote hata nilipokuwa mjamzito wa Ayan.” Mina akaendelea taratibu.

“Sasa sijui tatizo ni Ayvin au mimi kwa ujumla wake! Sijui..” “Nakup...” “Naomba nisubiri nimalize Andy. Umekuwa ukirusha ngumi na maneno makali kila wakati. Umejawa hasira huwezi, kujisaidia. Na huniamini tena Andy!” “Nakuamini.” Andy akajitetea.

Hapana Andy. Tafadhali naomba nisikilize. Ugomvi wa jana umetokana na kile alichokifanya Pius, kwa kuwa wewe umeshindwa kabisa. Na umekataa hata kujaribu!” “Hunitendei haki Mina! Nimemkuta Pius akikushika.” Mina akashangaa.

“Kuwa mkweli Andy na tafadhali fikiria kabla hujajibu. Kama kweli mimi nilikuwa na nia mbaya, ningekuomba kweli unisindikize kliniki ili tuwe pamoja? Fikiria tu Andy. Nilikuomba kabisa nikitaka tuwe wote, lakini ulikataa mwenyewe ukaniambia upo na kazi nyingi kazini, na muda ni mbaya!” Mina akaendelea tu taratibu. “Na ndio kisingizio chake kila siku, KAZI.” Pius akadakia, wakajua wanasikilizwa. “Pius nyamaza.” Baba yao akasikika na sauti ya kuonya.

“Nakuomba pata muda wakufikiria Andy. Hii kitu sio rahisi kama tulivyodhani. Ayvin atakuwa kwenye maisha yangu daima. Sina jinsi yakumkimbia au kumuacha. Hawezi kulelewa na Pius, kwa hiyo nilazima awe kwangu. Pata muda wakufikiria kwa kina, bila mimi kuwepo na kuamsha hasira kila ukiniona na tumbo langu. Usifanye haraka na sitalaumu kwa maamuzi yeyote utakayoyachukua. Utanijulisha, na ninakuahidi, sitakudai hata shilingi moja.” “Unanifanyia hivyo kwa kuwa unajua unaye Pius!” Andy akalalamika kwa kuumia.

“Husemi kweli Andy! Mara ya kwanza ulinifukuza kwako kwa kunitaliki nikiwa mgonjwa bila hata pesa ya kwenda kumuona daktari! Mbona nilikutafuta kwa ajili ya mwanangu tu na wala si mali? Unafikiri sikuwa nikijua kuwa nilikuwa na haki yakudai mali kwa kuwa nilikuwa mke wako halali kwa miaka takribani minne! Lakini nilijiambia Mungu hataniacha. Kama anavyosema Pius, mimi sijui kwa nini Mungu ameruhusu mimba ya Ayvin itungwe. Sijui! Ila ninachojua mimi ni mama yake, na ninawajibika kwake kama kwa Ayan.” Mina akaendelea.

“Nitaondoka na Ayan pia.” “Mina!” Andy akashangaa. Huwezi kumlea Ayan, Andy! Wewe ni shahidi. Huna huo muda. Hujawahi kuwa nao, na sidhani hata kama unao mpango wa kutenga muda kwa ajili ya mambo ya familia, Andy. Unakuwa kama unalazimishia tu! Nafikiri hata jana ulikuja hospitalini kwenye kliniki yangu si kwa ajili yangu, ila kufumania. Ukijua Pius yupo.” “Sio kweli Mina!” Andy akabisha.

“Mimi sitaki kubishana na wewe Andy. Nakuheshimu mume wangu. Lakini utagundua ninachosema ni kweli. Na ndio maana ulipofika pale ulikuja ukiwa umejawa na hasira. Na kwa haraka sana bila hata salamu, ukatafuta kosa. Ukanilaumu mimi kwanza na kuanza kurusha ngumi bila kujali aliyekuwepo mbele yako ni nani.” “Hapana Mina! Labda umetafasiri vibaya!” Akajaribu kujitetea Andy.

“Sasa ile hasira uliyokuja nayo na kuanza kumpiga Pius, ilikuwa ni ya nini Andy?” “Alikuwa amekushika Mina! Kweli ulitaka mimi nifurahie tu?” “Wewe ulifikiri ni nini kinaendelea pale mbele ya watu, tena hadharani kama si tayari moyo wako umeshachafuka juu yangu mimi na mtoto niliyebeba! Au niambie ukweli tu Andy, utakuwa na amani uje utukute mimi na Pius tu peke yetu tumekaa tu sehemu hivi?” Kimya.

“Najua ni ngumu na ndio maana kwa heshima yako Andy, na kwa kuwa nakupenda, nimeomba nikakae kwa wazazi kwa muda hata mpaka nitakapojifungua.” “Mina!” “Sina jinsi Andy! Mtakuja kuniua, niache watoto wangu bure! Acha kila mmoja wetu ajipange kwa upya. Ukija kunitafuta uwe umeamua kweli kuishi na Ayvin kama vile Ayan.” Wakamsikia Pius akicheka.

“Pius wewe, ujue unanitafuta Pius!” “Mimi nimefanya nini mama yangu!?” “Unachocheka hapo nini?!” “Mina anamtaka Andy awe baba kwa PJ wakati alishindwa kuwa baba hata kwa Ayan mwanae!” “Pius unakokwenda huko wewe utaharibu kabisa!” “Basi Mina, mama. Nimeongea tu nikikuhurumia wewe. Usitegemee kitu ambacho wazi unajua hutaweza kukipata. Sitaki uje uumie.” Pius akajaribu kumtahadharisha kwa upendo.

“Kwa hiyo yeye Pius ndiye anayeruhusiwa kuwa karibu na wewe?” “Hapana Andy. Na yeye lazima apate muda wakujifikiria ni jinsi gani ataishi na mimi akijua mimi ni mke wako, kama utaamua uwe na mimi. Lazima jukumu la kuandaa mazingira mazuri kwa mtoto wake liwe kwa Pius mwenyewe. Hawezi akaendelea kukukejeli wewe na kukujibu vile atakavyoweza na kupigana na wewe huku mtoto wake anakutizama wewe kama baba! Hilo haliwezekani.”

“Kama anataka mahusiano na mtoto, nilazima ajifunze kuwa baba, na garama pekee ninayotaka ailipe kwa Ayvin, iwe kukuheshimu na kukukubali wewe kwa namna yeyote ile ulivyo. Unaweza ukabaki kwenye maisha ya Ayvin kama baba atakayekuwa akikuona kila siku, KAMA narudia tena KAMA TUTAKUWA WOTE. Tusipokuwa wote kwenye ndoa, basi mimi na Pius, tukisaidiwa na wazazi, tutajipanga upya.” Pakazuka ukimya mkubwa sana.

“Yaani Mina, mama, hapo nakupongeza. Umeamua vizuri sana. Na naona wote umewagusa pabaya.” “Wala si pabaya mama.” Pius akabisha. “Mbona umepoa kama kweli ni rahisi kumuheshimu Andy na kukubali masharti yote Mina anayokupa?” “Kwa kuwa Andy mwenyewe hajui hata kuwa baba kwa mwanae, mama! Atawezaje kuwa mfano wa kuigwa kwa mwanangu?” “Ndio sasa umeambiwa utamkosa mtoto.” “Mimi na Mina hatujawahi kushindwana.” Mina akarudi pale sebuleni.

Hutafika kuonana na mimi, kama baba na mama hawapo nyumbani Pius. Ili kumfanya Andy arudishe imani na wewe. Kuanzia leo, tafadhali anza kufikiria jinsi ya kumuheshimu Andy. Vile alivyo, ukijua ndiye atakayempa mwanao sehemu ya kuishi kama nitakuwa naye. Na wakati nyinyi wote mnajifikiria na kujipanga upya, jua ili kuniona mimi ni mpaka uzungumze na baba pamoja au na mama kwanza. Wakiwepo nyumbani, ndipo uje. Lasivyo itakuwa ni kutoniheshimu, na hapo utaniudhi. Nitaondoka na watoto wote, niende nikawawekee nyinyi wote restrain order msiwe karibu na wanangu kwa kuwa mtawadhuru kama mlivyonifanyia mimi jana.”

“Na ushahidi wa picha jinsi nilivyoumia kumbe kuna mtu alijiiba na kunipiga picha pale hospitalini, nesi aliyenisaidia asubuhi hii ameniambia, nasikia upo mtandaoni. Kila mtu ameona jinsi mlivyokuwa mkipigana, wakati mimi na mtoto tukiwa katikati yenu, wala hamkujali hilo. Mkaniumiza. Sitapata shida kuwawekea nyinyi wote wawili restrain order.” Wote wakashituka wasiamini kama Mina anayajua hayo yote. Wakapoa haswa.

“Niliwapa dhamana, nikiwaheshimu lakini naona mmeshindwa. Mmeishia kunidhuru na kubishana kusiko isha. Sasa ili wote muwe na mahusiano na watoto wenu, naomba nikaishi kwa wazazi kwa muda wakati nikijipanga na wote tukifikiria chakufanya sasa na baada ya mtoto kuzaliwa.”

Majibu yangu kutoka kwa Andy na wewe Pius nitayapata kwa vile mtakavyofanya kuanzia sasa. Nawaahidi, sitafanya chochote bila kuwataarifu. Kama nikiwa naondoka kwa wazazi na kwenda kuanza maisha yangu, nitatafuta ushauri wa kisheria, wote mtawasiliana na huyo mwanasheria.” Pakawa kimya zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakamuona mzee Ruhinda akicheka taratibu. Mina akasimama na kuelekea chumbani, akampita Andy pale alipokuwa amesimama. “Niliwaambia mimi! Tulieni ili mpange mambo kama watu wazima! Mmeona mambo yenu ya kitoto jinsi yalipowafikisha? Mmejiharibia sifa bila sababu!” “Mimi ninayo sababu baba. Pius amempa mimba mke wangu.” “Sasa kwa fujo mnazozifanya hizo, imebadilisha nini?”  Akauliza mama Ruhinda.

Umeharibu sana Andy. Tena nilikwambia unayo nafasi nzuri yakuongoza haya mambo utakavyo, kwa sababu Mina alikuamini wewe. Ona ulipomfikisha huyu binti! Wote mmekuwa kama watoto wadogo! Wote mnakosa nafasi ya kuwa na watoto wenu!” “Ni kwa muda tu baba, naamini akipona atatulia.” “Nafikiri katika vitu ambavyo unatakiwa ujifunze Andy, kwa kipindi hichi ni juu ya mahusiano.” Akaanza mama Ruhinda.

“Acha nikwambie ukweli tu, pengine itakusaidia. Umeshindwa vikubwa mno. Tupo hapa sasa hivi, katika hili sababu yako WEWE Andy.” “Unampendelea Pius, mama. Kwa nini hum..” “Nisikilize kwanza Andy, kisha uwamue lolote utakalo. Useme nampendelea Pius au la, sitajali tena. Mimi ni mama yako, na nina jukumu la kukufundisha. Umekosea kwa Mina mara ya kwanza, ukapewa nafasi ya pili, UKAHARIBU kwa kumsikiliza Paulina, lakini napo ukifikiria kwa makini ni kwa kuwa HUJUI mahusiano Andy.” Mama Ruhinda akaendelea.

“Ukapewa dhamana nyingine na Mina, akakutanguliza huyu binti katika hili. Mbele ya kila mtu, Mina akakutangaza wewe ndio utakuwa kiongozi wa haya yote. Nishamsikia baba yako akizungumza na wewe kwenye simu, akikwambia ukitulia utaweza kuongoza hili jambo vizuri sana. Lakini hebu angalia hapa tulipo, jinsi ulivyoshindwa vibaya na kudhalilisha kila mtu mwenye jina la Ruhinda! Wote tupo kama uchi huko mtandaoni.”

“Usingekuwa kumtelekeza Mina, wala huyu mwenzio tamaa isingemwingia.” Mama Ruhinda akawa mkali kabisa. “Wewe unaacha mkeo analishwa, anauguzwa na kutunzwa na mwanaume mwingine! Eti wewe unazunguka kila mahali sababu ya kazi! Ulitegemea nini Andy? Tena ushukuru Mina alitulia, angekuwa malaya huyo, angekuua kwa maradhi kwa kubadili wanaume! Sasa badala utulie na kujirudi, unapigana kila mahali, na sijui kama hiyo kazi bado utakuwa nayo endapo viongozi wako wataona hiyo video.” Andy kimya.

“Huko unakojificha Andy, lazima utoke na ukubali kuwajibika kwa kuwa uliamua mwenyewe kuanzisha familia. Wote sisi tunazo kazi, lakini mbona bado tunakumbuka majumbani kwetu? Pius huyo ni shahidi. Ana kazi kubwa sana, lakini ameweza kumudu FAMILIA MBILI! Yake na yako.” “Na bado nyumbani amekuwa tegemezi.” Mzee Ruhinda akaongeza.

“Haya, umemsikia baba yako! Hutamuita Pius, au kumtuma popote na chochote, akashindwa. Japokuwa wote mnasema nampendelea Pius, haya, umemsikia na baba yako? Ndiye mtoto anayepita nyumbani kutuona mara kwa mara na kutujulia hali kwa simu kila siku. Anajua habari zote za nyumbani. Sasa jiulize yeye anawezaje, tena bila kuchoka au kubadilika, na kazi nzito aliyo nayo! Na bado anazo biashara zake, halafu wewe mwenye kazi moja tu, huna hata biashara, mke mmoja, mtoto mmoja tu, unashindweje!?” Siku hiyo mama Ruhinda akawa amekusudia, bila kumuogopa tena.

“Na kama  alivyokwambia mkeo, mtafute baada ya kujifikiria. Ukishindwa, SEMA. Tena sema haraka uache kupotezea watu muda!   Wewe sio wakwanza kushindwa na mambo ya familia na wala hutakuwa wa mwisho. Sema mapema watu wajue moja. Twende Ruhinda tukajiandae, turudi kwetu.” Mama Ruhinda akasimama na kwenda kwenye chumba walicholala usiku huo, Mzee Ruhinda naye akafuata. Pakawa kimya.

Kuruka Moto, Kakanyaga Majivu.

Mina aliondoka kwake na Judy pia ili akamsaidie kazi nyumbani kwa wakweze.  Walifika mida ya jioni. Hata hawakujua Pius aliondokaje pale Dodoma, lakini mzee Ruhinda alimkataza kuongozana nao. Wakaondoka yeye, mkewe, Mina, Ayan na Judy. Moja kwa moja mama Ruhinda akampeleka Mina chumbani.

“Judy atalala na mwenzie.” “Nashukuru mama, labda nilale na Ayan chumba hiki. Asiwe peke yake.” “Sawa kabisa. Ila ujue vyumba vipo vingi tu, ukitaka tunaweza kumtayarishia chumba chake.” “Nashukuru mama yangu. Lakini acha nilale naye tu.” “Basi pumzika, chakula kikiwa tayari nitakuletea.” Mama Ruhinda akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati anapitiwa na usingizi baada ya kumeza dawa ya maumivu akasikia kilio sebuleni kama mtu aliyefiwa. Mina akashituka sana, akatoka chumbani. Kadiri alipokuwa akishuka ngazi kutoka chumbani kuelekea sebuleni, akagundua ni sauti ya Raza. Mina akasimama kusikiliza.

 “Nafikiri pata muda na Pius, atakueleza vizuri.” “Pius ananidharau baba! Tangia anikatie simu jana, hapokei simu zangu. Hajarudi nyumbani na wala hajanipigia mpaka sasa!” “Ni kweli tulikuwa naye Dodoma, nafikiri leo atakuwa nyumbani.” Mzee Ruhinda akajaribu kumtuliza kwa kuzungumza naye taratibu.

“Kwa hiyo nyinyi wazazi mpo na mume wangu, na baba wa watoto ambao hawana hatia kuzaliwa wakike, mnamuuza mtoto wenu kwa mwanamke mwingine!?” “Najua upo kwenye mshituko Raza, lakini angalia usivuke mipaka.” Akazungumza mama Ruhinda kwa kumtahadharisha.

“Najua hamnipendi na mnanilaumu kwa kumzalia Pius watoto wa kike, lakini mkumbuke mwenye uwezo wa kutoa mtoto wa kiume ni mwanaume wala si mwanamke. Nyinyi mmesoma, mnawezaje kunilaumu mimi na si mtoto wenu!” Raza akaendelea kulalamika huku akilia.

Mama Ruhinda akachukua simu na kumpigia Pius. “Uko wapi?” “Njiani naelekea nyumbani.” Pius akajibu. “Pitia hapa nyumbani haraka.” “Kuna nini tena!?” Pius akauliza. “Wewe husikii sauti ya mkeo bwana! Hebu njoo hapa.” Mina akabaki akitetemeka amesimama kwenye ngazi za kushukia.

 Namjua Mina ndani na nje. Nimepata leo habari zake zote kutoka kwa mtoto wa mama yake mkubwa! Mina ni malaya na...” “Raza! Raza!” Mzee Ruhinda akamuita haraka. “Tafadhali sana.” “Mimi nawaambia ukweli ili mumjue Mina. Mina ni...” “Najua upo kwenye mshituko, kuwa mwangalifu sana, haswa kwenye kipindi hiki.” “Mina ndivyo alivyo hivyo. Yupo kama na jini fulani lakuvuta watu upande wake, Pius na Andy sio wakwanza.” Mara Pius akaingia kama aliyekuwa akipita hapo nje nyumbani kwao, hakuwa mbali. Bado mkewe alikuwa akiongea.

“Huyu Mina alishatembea na mtu na rafiki yake kipenzi. Akatembea na bosi wao pia. Mina ni malaya asiyeweza kujisaidia.” “Unaongea nini hapa kwa wazazi wangu Raza!? Umechanganyikiwa wewe!?” Pius akashituka sana kusikia maneno anayoongea mkewe wakati akiingia ndani.

“Nakuokoa Pius, usifikiri wewe ndio mwanaume wa kwanza kwa Mina.” “Hujui ni nini unaongea hata kidogo. Nyamaza na usimame haraka kabla HUJAJUTA, vibaya sana!” “Kwa nini nijute wakati mimi naongea tu?” “Unanijua jinsi ninavyochukia maneno ya uzushi. Na nilikuonya usifike kwa wazazi wangu na maneno ya uzushi.” “Huu sio uzushi Pius, ni ukweli kabisa kutoka kwa ndugu yake Mina, wa damu! Mina alichowafanyia wewe na Andy sio kigeni. Ni mchezo..” “SIMAMA Raza!” Pius akaamrisha.

“Pius!” “Kabla hujaniudhi zaidi, kwanza funga mdomo wako, na utoke hapa ndani kimyakimya.” Mina akamsikia Pius ambaye hajawahi kumsikia kabla. Anaunguruma kama simba. Akabaki amesimama kwenye ngazi, miguu ikitetemeka. Raza akabaki amekaa kochini akilia.

“RAZA!” Pius akaita kwa ukali mpaka Mina akakaa kwenye ngazi. Raza akasimama kwa haraka. “Mimi ni mkeo Pius na nina haki.” “Haki yako unaipoteza kwa kuja hapa na kumwaga sumu. Hujui chochote kinachoendelea, unazunguka kutafuta habari za Mina na kuja hapa na kuanza kuongea kama mwehu!” “Nitajua vipi wakati wewe na wazazi wako mnanificha? Ulishindwa vipi kuniambia ukweli?” “Jana uliponitumia ile video na kunipigia simu, nilikwambia nini?” Raza kimya.

“Nakuuliza wewe? Nilikwambia nini?” “Sasa kwa nini mpaka leo hujanitafuta na jana hukulala nyumbani!?” “Wewe mara ya mwisho kuzungumza na mimi nilikwambia nini? Mbona unakataa kujibu?” Kimya. “Sikukwambia nipo Dodoma, nipo kwenye wakati mgumu sana, ila nikirudi nyumbani tutazungumza? Sikukwambia hivyo wewe?” “Kwa hiyo ni sawa mimi kujua mambo mtandaoni?”

 “Na kama wewe na wazazi wako mnanilaumu mimi kuzaa watoto wa kike, nawashauri mjifikirie kwa upya. Kosa ni lako. Na kama unafikiri mtoto aliyembemba Mina ni wako, unajidanganya. Unaambiwa Mina hana uwezo wa kukaa na mwanaume mmoja. Kama alikudanganya kipindi mumewe amemtelekeza, ukadhani upo naye wewe tu, basi ujue mlikuwa wanaume wengi tu.” Mina alisikia sauti kubwa kama mtu amechapwa kofi. Alishituka mpaka akajishika tumbo.

Raza alilia kama amepasuliwa. “Toka Raza.” Unanifukuza mimi mkeo, unamuacha malaya huyo ndani!” “Nitakuumiza Raza, toka.” “Na nyinyi wazazi mpo hapa mnaacha nadhalilika mimi sababu ya malaya huyo! Mnadhani atawaletea mtoto wa kiume mwingine! Kama amewaambia ana mimba ya mtoto wa kiume ili mumpende, basi mjue Mina ni tapeli. Na kwa kuwa mmekubali nifukuzwe hapa, basi mjue na watoto wangu hawatakaa wakakanyaga hapa.” “Ona unavyo jidhalilisha! Nani amekwambia watoto wangu huwa wanakuja hapa kwa sababu wewe unafika hapa?” Pius akaenda kumvuta na kumtoa nje, Raza akilia. Pakatulia kimya. Wakasikia magari nje yanaondoka. Mzee Ruhinda na mkewe wakabakia hapo kama wamepigwa ganzi.

~~~~~~~~~~~~~~

Kila Mahali Moto & Sintofahamu Ya Hali Ya Juu.

Baba Wa Watoto Wote Wamekuja Juu Wanamtaka Mina Aliyebeba Suluhu Ya Watoto Wao.

Ndio Raza Na Andy Wanakumbuka Shuka, Kushakuchwa.

Maji Yashamwagika.

Ayvin YUPO Mzima Wa Afya Njema, Tumboni Kwa Mama Yake Na ANAKUJA. Ready Or Not, Ayvin Muda Wake Utakapowadia Atakuja Tu Kwenye Ulimwengu Huohuo Wa Wazazi Wake Na Wanao Wazunguka.

Kuna Garama Ya Kulipa Ambayo Pesa Na Elimu Yao Vinashindwa Kuwasaidia.

Nini Kitaendelea?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment