Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 41. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 41.

Siri ya mtoto, ajuaye Mama, na DNA siku hizi. Kumbe ukimya wa Mill ulikuwa na mengi. Majibu yalitoka kama alivyodhania. Watoto wote hawakuwa wake. Lakini aliondoka nchini Marekani akiwa amekabidhiwa kisheria kuwa ni wake kihalali, kwamba Kisha hawezi KUWACHUKUA. Alipopata tu majibu akamtafuta mwanasheria wake. Akamueleza ilivyo.

“Nitafanyaje na watoto nimekabidhiwa na mahakama?” “Wewe ulitaka nini?” Mwanasheria wake akamuuliza. “Si sawa hawa watoto kulelewa na mtu baki! Wanahaki ya kulelewa na wazazi wao!” “Basi hiyo ni rahisi sana. Cha kwanza, Kisha alikudanganya. Na wakati ukidai hao watoto ulijua ni wako. Huo mkataba mpaka hapo ni haramu. Si halali. Nitafungua kesi. Ila itabidi urudi nao huku, vifanyike vipimo upya, kisha kumshitaki Kisha.” Mill akafikiria.

“Nafikiri tufanye hatua kwa hatua. Nisingependa tena kesi. Vipimo vya huko vitakapo kamilika, ndipo tumtafute Kisha tuone anasema nini. Akianza ukorofi wake, ndipo nitamshitaki kwa hakika maana alijua kabisa alichokuwa akikifanya. Na kinachoniuma zaidi ni kutumia watoto kujinufaisha. Ni ukatili wa namna gani huo?! Ni mwanadamu gani eti anakubali watoto wake walelewe na mtu mwingine, tena kwenye Bara jingine kabisa!” “Kwake wewe si mtu baki, Mr Mgini. Unaweza usiwe umewazaa lakini wakawa ni watoto uliolea. Na najua anajua jinsi unavyo wapenda. Nina uhakika kwa jinsi ulivyo wahangaikia hao watoto na kupoteza kila kitu kwa ajili yao, kama wangekua ni watoto wa kawaida, nina uhakika usingewarudisha.” Mill akabaki kimya maana ni kweli.

Huyo mwanasheria ametembea naye kwa muda mrefu sana kwenye hiyo ndoa yake. Anawafahamu hao wote watano ndani na nje. Mill, Kisha, Trey, Miles na Mia. Hawawezi hata kujificha kwake. Wakazungumza mengi, Mill ikamlazimu kuondoka nchini kwa haraka.

~~~~~~~~~~~~~~

Huku kwa Pam yeye hana habari, anajua bado Mill amezira. Ila mkono ulikuwa ukiendelea vizuri. Siku anapata ajali akienda shuleni kwa mwanae alicha mazingira ya kazi akijua anaweza fukuzwa maana ni kama alilazimishia baada ya kukataliwa.

Sasa alipopata ajali, alipokwenda kupeleka vipimo vya hospitalini na kumuonyesha bosi wake kumuaminisha kama kweli ameumia na ameambiwa hataweza tumia huo mkono kwa miezi mitatu, hawezi kunyanyua vitu vizito, wala bosi wake hakutaka kupoteza muda. Akamwambia ataangalia akipona kama kutakuwa na nafasi yake, maana siku hiyohiyo anatafuta mtu wa kuziba pengo. Pam akaondoka hapo akijua hiyo kazi nayo imeisha.

Kwa hiyo alikuwepo tu nyumbani na akajua ni mpaka apone kabisa ndipo itambidi kuanza kutafuta kazi kwingine. Akaonelea kipindi hicho ndio muda muafaka na yeye kurudi kusalimia kijijini kwao, kabla hajarudi mjini kutafuta tena kazi. Hata hivyo Shema alikuwa amefunga shule. Ilikuwa ni kawaida yake kwenda kumuona mama yake.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo mchana wakati dereva alipoleta matumizi akamuomba mama Shema wazungumze. Wakatoka nje kabisa kwenye gari. “Nimetumwa na bro. Anauliza kama anaweza kuja jioni? Ni muhimu, ila kama kuna wageni wako wengine, anaomba muda ambao hautakuwa na muingiliano. Na ameahidi hatakuchukulia muda mrefu.” Pam akashangaa sana moyoni mwake ila akamjibu amwambie yeye atakuwepo.

Mjumbe hauwawi akarudisha jibu, lakini Pam akaelewa kwamba ndio hataki amkute pale Mgaya. “Kwamba anadhania kwangu ni dangulo!” Akajilalamisha lakini akimsubiria kwa hamu haswa.

~~~~~~~~~~~~~~

Jioni Mill akawasili hapo anapoegeshaga gari akiwa anajishauri kama aingie au atume mtu, akamuona Shema dirishani kwake. Akashusha kioo. Akamsalimia baba yake na kupanda garini. Alikuwa mchafu, jasho linamtoka haswa. Mill akacheka. “Hivi unakumbuka kunywa maji lakini?” “Nakunywa. Wakati mwingine mama anamtuma mtu aniite, nirudi nyumbani halafu ananipa maji.” “Kwa hiyo wewe mpira ni kuanzia asubuhi mpaka jioni?” “Hivi nilikuwa katikati ya mechi mama akanilazimisha kurudi.” Mill akabaki akicheka akimtizama.

“Naenda kwa mama.” “Mwambie nipo hapa nje, naomba atoke tuzungumze.” Shema akashuka garini kwa haraka kuingia ndani kumuita mama yake. Pam akashangaa kwamba amegoma kuingia ndani! Lakini akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Akasimama dirishani. Akashusha kioo maana bado gari ilikuwa ikiwaka ili apate upepo. Akashusha kioo pale aliposimama. “Unaendeleaje?” “Vizuri tu. Na wewe pamoja na watoto?” “Sisi wazima. Kama hutajali, naomba upande kwenye gari, nina mazungumzo ya msingi kidogo na sitakuchukulia muda mrefu.” Akaguna na kupanda.

“Hivi unajua hapa kwangu si dangulo, Mill? Useme kwamba huwa naingiza wanaume unaohofia utakutana nao!” “Nishakutana na mmoja, inatosha. Hata hivyo sikutegemea tofauti Pam. Wewe bado ni mdogo na ni mzuri tu. Tokea mwanzo nakuacha nilijifariji kuwa ungeumia kuwa nimepotea, lakini nilijua ungeendelea na maisha kama hivi. Nasikitika njia zangu nilizochukua zimekuwa ndefu na si sahihi, lakini sikuwa na nia ya kukuumiza. Naomba unisamehe ila nashukuru Mungu ameweza kukurudishia niliyokupokonya.” Akaendelea.

Mwanaume unayemuamini kuliko mimi, na marafiki wa kweli si wadanganyifu kama mimi.” Pam alishikwa na kitu, akashindwa kujibu. Alinyamaza kimya.

“Hii ni bahasha. Ndani kuna nyaraka za muhimu SANA. Tafadhali zitunze. Mimi naondoka tena nchini.” Pam alishituka, hakutegemea. “Natarajia kurudi nitakapokamilisha mambo yanayonipeleka huko. Ila miezi miwili ikipita sijarudi, tafadhali fungua na usome kwa makini. Humo ndani kuna maelekezo ambayo nina uhakika kwa akili yako, hutachanganyikiwa. Nimejitahidi kuweka maelezo kwa lugha nyepesi sana. Sijui kama umenielewa?” Pam alibaki kama amepigwa na ganzi.

“Tafadhali naomba uulize swali ili nisikuache njia panda. Maswala ya mtoto na shule, vipo sawa. Ada ni kama ulivyosikia. Italipwa mpaka amalize pale. Na ninavyomuona Shema, wataendelea kumlipia tu mpaka amalize grades zote pale. Na pia kama hatabadilika, nina uhakika watamsomesha na chuo.”

“Gari iliyokuwa ikiwaletea matumizi, ni yenu. Kadi za gari zipo humo ndani. Upo huru kumuacha yuleyule akawa dereva au ukatafuta dereva mwingine. Lakini kuanzia kesho utaletewa gari. Najua kuhama ulikataa. Lakini usafiri nafikiri ni muhimu. Au nakosea?” “Nashukuru japo na sisi tutaenda kijijini.” “Ulipanga kwenda lini na utataka kukaa huko kwa muda gani?” Akatulia.

“Kama ni mambo ambayo labda haupo tayari kunishirikisha, labda niseme si kwa kutaka kukuingilia. Nilikuwa na ushauri. Sijui naruhusiwa?” “Huniingilii Mill! Nilikuwa nikijaribu kufikiria!”

“Ile kazi nilifukuzwa. Nimeambiwa ameshapata mtu wa kuziba nafasi yangu.” “Pole.” “Yote maisha tu. Najua nitapata ingine ila nataka kufuatisha ushauri wa yule daktari. Kuupa muda mkono, upone kabisa. Naona nitaenda kuusubiria kwa mama wakati nikisubiria na shule ya Shema kufungua. Kwa hiyo nitakuwa huko muda wote mpaka labda siku chache kabla ya shule yake kufunguliwa. Sasa nitafanyaje na hilo gari?”

“Unataka kuondoka lini?” “Kesho kutwa ili kesho ninunue vitu muhimu.” “Basi mtumie huyohuyo dereva. Kesho akuzungushe ufanye manunuzi yako. Aje kesho kutwa tena kuwapeleka kituo cha mabasi. Mkirudi, mnamtaarifu atakuja kuwapokea. Gari nitamwambia aache nyumbani kwangu mpaka mtakapo rudi. Au unaonaje?” “Sawa. Nashukuru.” “Karibu.” Wakatulia kidogo. Akaendelea.

“Naondoka, lakini sitaki kupoteza mawasiliano na Shema. Nimekuja na simu ili tuwasiliane kipindi ambacho sipo ili tusikuingilie na simu yako.” Pam akamwangalia, akaona anyamaze tu. “Nikirudi nitaichukua. Lakini kama msimamo wako ni uleule, hutaki awe na simu, basi nisaidie hata namba ya simu ya bibi yake, niwasiliane naye kwa kupitia bibi yake, mama Eric.” “Wewe mpe tu. Ila kama utarudi, tafadhali uichukue. Sitaki awe na simu sasahivi.” “Sawa.” Akatoa simu na kumkabidhi.

Pam akashangaa sana. “Kwamba ndio unampa Shema hii simu mpya na ya ghali hivi!?” “Wewe ulitegemea ningempa simu gani!?” “Hata iliyotumika!” “Na nani?” Hapo akakwama. “Kwamba mwanangu ndio yeye atumie vitu walivyochoka watu wengine! Sasa anafaida gani ya kuwa na baba!” “Mmmh!” Pam akaendelea kushangaa. “Nimemnunulia na kijipochi chake chakufunga mkononi akiwa anacheza ili isimkere na asipoteze kwa kuiacha chini.” Akamuonyesha jinsi ya kuifunga. Ilikuwa na mikanda mizuri sana ya kufunga juu kabisa ya mkono. Pam akabaki akishangaa.

“Binafsi sina la nyongeza. Mengi nimejieleza humo kwenye hiyo bahasha niliyo kukabidhi. Ila nina ombi Pam. Tafadhali nisikilize na ulizingatie.” Pam akamwangalia.

“Shema ni mtoto wangu wa kwanza. Nimekosa maisha yake ya nyuma, lakini nimekusudia ya mbeleni nisikose. Kwa garama yeyote ile, sitamtelekeza. Na nakushukuru sana kwa nafasi unayonipa kuwa naye, japo siridhiki. Haya maisha mnayoishi hapa, ni WEWE umechagua. Na pengine mimi nimechangia kwa asilimia kubwa sana. Lakini nakusihi Pam, mwanangu asiendelee kuishi maisha ya kimasikini, wakati mimi ninayo pesa.”

“Chakula kisiwe cha kuhesabu. Kama utakuwa umeangalia akaunti yake, utagundua inayo pesa nyingi tu. Na hata kama utaamua kuolewa na huyo Mgaya, naomba mtoto wangu asiishi kwa uwezo wako na mumeo, ila uwezo WANGU.” “Mill, umekuza jambo la dokta Mgaya…” “Sio dokta.” Akakanusha kwa jazba. Wivu tu.

“Sawa. Lakini ndivyo anavyofahamika hapa. Lakini..” “Ndivyo alivyojitambulisha na kwangu, mbele yako na hukukanusha. Nimemkuta akikuhudumia ndani ya chumba chako, kitandani, wala si eneo analofanyia yeye kazi, kuashiria ni kweli mpo na mahusiano. Hilo si tatizo, ila tatizo ni mtoto WANGU.”

“Mimi sina mambo ya wanawake. Sina wasiwasi akiwa kwangu. Najua umeniambia nina laana. Nimerithi kutoka kwa baba yangu, lakini Pam, nimekusudia kubadilika hata kabla hujaja kwenye maisha yangu. Chumba tulicho lala mimi na wewe, pale kwa Mike, hapakuwahi kuingia mwanamke, hata daktari, isipokuwa wewe.” Pam akaangalia pembeni.

“Nimekusudia kubadilika. Japo njia yangu imekuwa na vikwazo na sijabahatika, lakini sikati tamaa. Naamini siku moja na mimi naweza kupata atakayenipokea kama nilivyo. Ila kwa sasa ukweli najitahidi. Nikiwa na Shema, najitahidi kuzungumza naye na kumuelewesha nilikopita na kukosea. Mfano mzuri wa kuiga. Nafanya kwa maneno na vitendo. Naomba na wewe jitahidi.”

Kutaneni sehemu ingine. Mambo yenu yatakapokuwa yamekamilika, na yeye mpeleke kwa wazazi kama ulivyonipeleka mimi, na Shema ajue hilo. Ajifunze. Mkioana ndio angalau amuone ndani lakini si kabla. Maana na mimi ananiona nipo. Naingia palepale mnakoishi na mwanangu, ambapo Mgaya naye anaingia na kuwa huru mpaka kitandani! Tunakuwa tunamchanganya! Hata kama unataka ajifunze kwa kina baba Pili unao waamini kuliko mimi, halafu anaona maisha mengine tunayoishi, sidhani kama utafanikiwa sana. Ni hilo tu. Na samahani kama nimevuka mipaka.” Yaani mpaka hapo yeye Pam ndio malaya! Akanyamaza hakujibu. Alikabwa na kitu kooni, alishindwa kuzungumza kabisa.

Kwanza swala la Mill kuondoka tena nchini lilisha mchanganya. Leo anaaga kama anaacha wosia! Akabaki ametulia kitini akifikiria. Na yeye Mill akatulia kabisa. Akawa kama amekumbuka kitu. “Wewe unaondoka lini?” “Tunaondoka siku mbili kuanzia sasa.” “Kwamba unaondoka na watoto kabisa?!” “Ndiyo.” Pam akatulia akijua ndio kwa heri, kuja kuonana ni majaliwa.

“Unampango wa kuja kurudi tena Tanzania, Mill?” Akauliza kwa wasiwasi. “Namuomba Mungu anisaidie nije nirudi salama. Naogopa nisije nikasema kitu ikawa kama mara ya mwisho nilipokuaga. Ila jua nia ya kurudi ipo. Sitaki Shema akue bila mimi. Hata kama hatutakuwa tukiishi nyumba moja, ila angalau ajue nipo na namjali. Mengine ni matokeo tu.” Pam akatulia.

“Kama hakuna jingine, basi nisikuchukulie muda wako zaidi. Ni hayo tu, nilitaka kuzungumza na wewe. Unafikiri Shema atakuwa tayari nitoke naye kidogo au ndio mpira umechanganya? Nataka nimuage.” “Akijua unasafiri anaweza kukubali kuacha mpira ili muagane. Acha nimuite. Nimemlazimisha atulie kidogo, ale na kunywa maji ndio arudi mpirani.” “Basi nitashukuru. Ila na pia akionekana ni lazima sana kurudi kucheza, usimlazimishe. Naweza tenga muda kesho jioni nikaja kumuaga kabla hamjaondoka. Si ni sawa?

“Mill, hapa kwangu hakuna wanaume wanao ingia. Tafadhali naomba uelewe. Siku ile ulimkuta humo ndani kwa sababu nilikuwa na kizunguzungu. Nakiri mazingira pengine yanaweza yakawa hayakueleweka, lakini si kwamba ni kawaida yake kuingia mle ndani. Siwezi fanya hivyo na Shema yupo! Mimi si malaya, Mill! Na wala si mjinga.” “Sijasema hivyo, ila nakutahadharisha tu. Mapenzi yanaweza kukolea, ukaona kila kitu kipo sawa na kina wezekana. Na pia tafadhali usimuamini kupita kiasi. Shema bado mdogo na anakuhitaji.”

“Kwamba unachoniambia hapa niwe nafanya ngono na kinga?!” “Mimi nakusihi kuwa tu makini, ndio hilo tu. Sitaki kukuudhi, hilo ni ombi. Maana unaweza nikataa mimi ukidhania mimi ni mchafu sana kama baba yangu au babu yangu kama ulivyosema, ukadhania huko kwa Mgaya ni salama kwa sababu yeye yupo karibu yako. Ndio naomba kuwa makini.” Pam akashuka bila ya kujibu.

Mara akaona kikundi cha watoto wanaingia ndani kwao wakimuita Shema. Akajua kumtoa hapo ni kumsumbua. Akampigia honi Pam, akageuka. Akamfanyia ishara ya kumuita. Akarudi. “Naona umuache tu. Nitamfuata kesho kumuaga.” “Sawa.” Pam akaondoka.

Kwa Mina.

Mina alipoteza fahamu kwa muda wa kutosha. Baada ya muda akasikia kwa mbali kelele, kisha akapotea tena. Akasikia akiitwa tena na tena, lakini safari hii hapakuwa na kelele. Kulitulia. “Mina! Mina!” Huku wakimtingisha. “Pius!” “Mimi ni dokta Kwayu! Unajisikiaje?” Mina akatulia kidogo. “Unaweza kufungua macho yote?” Akajitahidi akafungua.

“Kichwa kinauma sana.” “Unakumbuka una watoto wangapi?” Mina akafikiria. “Wawili. Ayan na Ayvin.” Akajibu taratibu. “Naomba ufikirie vizuri.” Mina akanyamaza. Wakamuona analia.

“Naomba usilie Mina. Pole.” “Hayakuhusu Pius.” “Yananihusu, Mina ni..” “Naomba utoke. Hapa hakuna mtoto wako.” Mina akasikia tena Andy na Pius wakibishana. “Naombeni wote msubiri hapo nje. Tafadhali sana.” Daktari akataka watoke. Wakaendelea.

“Kwanza wewe ndiye uliyempiga!” Akasikia sauti ya Pius akimshutumu Andy. “Pius nakutahadharisha wewe!” “Utanifanya nini? Roho yako ni mbaya Andy. Na ukisababisha chochote kitokee kwa mtoto wangu nita..” “Utanifanya nini?” Akauliza Andy kwa jeuri. Mina akafungua macho. Lakini likafunguka moja. Akawatizama. Wote walikuwa wameumia.

“Muongo mkubwa wewe Pius. Upo hapa kwa ajili ya mke wangu wala si mtoto peke yake.” “Ndiyo. Nipo hapa kwa ajili ya Mina na mtoto wangu. Nani amekwambia ninapinga hilo!? Wewe vipi Andy!?” Wakaanza tena hapo hapo chumbani. Mina akagundua humo ndani ya chumba yupo na nesi pamoja na daktari. Akajitahidi, akakaa.

“Naomba utulie Mina.” “Acha kumgusa mke wangu.” Andy akamsukuma Pius aliyemuwahi Mina. “Naomba mimi niondoke niwapishe jamani! Hivi sitaweza.” Mina akaanza kulia. “Naombeni mtulie, ili tujue hali yake! Huyu ni mama mjamzito. Mmempiga mpaka mmemuumiza jicho. Sijui ni kwa kiasi gani mmemdhuru! Ameanguka mpaka sakafuni!” “Andy ndiye aliyempiga.” Akadakia Pius.

“Sawa. Lakini naomba nafasi nimuangalie. Maana hata huyo mtoto huko tumboni hatujui ameathirika kwa namna gani!” “Hakika Andy nitaku...” “Acha kunitisha Pius. Ilikuwa bahati mbaya! Nilitaka nikupige wewe.”

“Hivi wewe, unamtaka huyu mtoto kwa kiasi gani?” Akauliza nesi, mama mtumzima kidogo. “SANA.” Akajibu Pius. “Basi anza kutoka wewe ili mkeo ahudumi..” “Sio mke wake. Ni mke wangu MIMI.” “Haya, na wewe uliyempiga mkeo mbele ya umati, ndio uanze kutoka, ili daktari aangalie madhara uliyosababisha kwa mkeo.” Nesi akaongea kwa msisitizo. “Siwezi kumuacha tena Pius na mke wangu. Yeye ndio atoke kwanza.” “Na mimi siwezi kukuacha wewe na Mina humu ndani. Umebeba chuki sana kwa Mina, hutashindwa kumdhuru mtoto wangu. Sikuamini!” Pius naye akagoma kutoka. Wakaanza tena.

Mina akasimama. Akavuta pochi yake iliyokuwa mkononi kwa Andy. Akataka kutoka, wote wakaanza kumfuata. “Sitaki mtu anifuate. Tafadhali sana Pius na Andy. SITAKI. Nyinyi wote si salama kwangu wala mtoto wangu. Narudia, naomba wote MSINIFUATE.”

“Ila, kila mmoja kwa wakati wake, kuanzia sasa hivi, lazima afikirie kwanza jinsi atakavyoweza kuishi na mimi pamoja na Ayvin. Ukishapata jibu ndipo unitafute.” “Mimi nakufuata Mina kwa sababu najua jinsi yakuishi na..” “Nisikilize Pius. Tafadhali nisikilize.” Mina akamtuliza, jicho likimuuma haswa.

“Wewe si unanipenda?” “Sana Mina.” “Hamuwezi kunifanyia hivyo mbele yangu! Huko ni kunidhalilisha.” “Naomba Andy utulie. Tafadhali sana.” Mina akawa mkali na yeye. “Basi kama unanipenda kwa kiasi hicho, na kumpenda Ayvin kweli, tafadhali pata muda wakujifikiria. Fikiria mazingira atakayokulia Ayvin, kama nilivyokwambia mwanzoni kabisa tulipofika tu hapa.” “Nimef..” “Unakaribia kuniudhi Pius!” Mina akamtahadharisha.

“Nakusikiliza Mina.” “Hivi mnavyofanya ndivyo unavyotaka mtoto aje akute haya mazingira?” “Namshangaa sana Pius.” “Tafadhali sana Andy, nyamaza. Nilikupa dhamana yakuendesha familia yetu, naona umeshindwa. Umejawa na hasira, mpaka umeniumiza. Hasira zako zimeisha sasa? Maana ni kama ulikuwa ukitafuta jinsi ya kuniadhibu, leo umepata.” “Ilikuwa bahati mbaya Mina! Pius..” “Naomba nyamaza na ujiangalie nafsi YAKO kabla hujamnyooshea kidole mwingine. Nyinyi wote wawili. Mmekuwa kama watoto bwana! Mtakuja kuniulia watoto wangu bure! Nipambane na nyinyi, na nguvu ya nje pia!” “Mimi nakulinda Mina.” “Wewe unamlinda kwa lipi Pius? Acha unafiki ili wewe ndio uonekane mzuri!” Wakaanza tena. Mina akaondoka katikati ya malumbano yao.

Alichofanya Mina, alitoka tu hapo na kukimbilia ofisi ya jirani akajificha chini ya meza, akatulia. Akasikia wanatoka wakikimbia kulia na kushoto huku bado wakigombana. Akajua lazima watakimbilia nje ya hospitali ili kumuwahi. Palipotulia, kama baada ya dakika 20 hivi, ndipo akatoka chini ya meza mwenye ofisi akimshangaa.

~~~~~~~~~~~~~~

“Naomba niitie dokta Kwayu. Alitakiwa kuniona muda mfupi uliopita, mwambie Mina Ruhinda.” Mina akakaa, yule mtu akapiga simu, kweli dokta akarudi akiwa na mshangao. “Najua unafahamiana na Pius, tafadhali nitibu bila kumwambia kwa sasa ili angalau nipumzike kwa leo. Sijisikii vizuri.” “Naona na jicho limezidi kuwa jekundu.” Akaanza kumpima pressure, haikuwa mbaya. Hilo likamfurahisha Mina.

“Wanakutafuta sana.” “Nisaidie sehemu ya kupumzika tu kwa leo, mpaka baba mkwe wangu aje. Hapa hakuna kitakachofanyika kama hawa wawili watakuwa pamoja. Na ninajisikia kuchoka.” Yule daktari aliposikia mzee Ruhinda mwenyewe atafika hapo, akaona jambo la msingi kujulikana yeye ndiye aliyetoa msaada. Akaandika kuwa alazwe, ili kuangaliwa zaidi. Na kweli vipimo vikaanza.

Kwa Raza.

Rafiki wa Raza, akaona video ya Pius na Andy wakipigana, Mina akitajwa. Na yeye akamtumia Raza shoga yake. Raza akaangalia, hakuelewa vizuri lakini akawa ameingiwa hofu. Akamtumia hiyo video Paulina wifi yake anayejua hawezi kujizuia kwenye mambo ya watu. Alipoona ameifungua tu, akampigia lakini Paulina cha umbea hakupokea.

Kumbe Paulina ameshituka sana, haraka akampigia simu baba yake. “Wanao wanauana Dodoma.” Mzee Ruhinda akawa hajaelewa, hapo hapo Paulina na yeye akamtumia hiyo video baba yake, mama yao alikuwa karibu, akampokonya simu mumewe aone yeye maana alikuwa akiwasikiliza Paulina na baba yake.

Paulina akawapigia wote wawili baada ya kukadiria muda. Akajua baba yake ameshaona. “Sasa kwa kifupi mzee Ruhinda, vijana wako wapo mtandaoni. Wanampigania Mina, na yeye mwenyewe Mina, wamempiga, ameanguka na amezimia. Video hiyo niliyokutumia nimetumiwa na Raza. Ananipigia mpaka sasa hivi, sijapokea.” “Mungu wangu!” Akasikika mama Ruhinda.

“We Ruhinda si nilikwambia mimi?” “Pius aliniahidi hatafanya fujo. Ningejuaje kama wataishia kupigana huko!? Mimi nilikuwa na shuguli zangu leo, sikuwa tayari kwenda Dodoma!” Mzee Ruhinda akajibu lakini akiwa ameishiwa nguvu kama anayetafakari chakufanya kwa haraka.

“Sasa ndio uende. Maana mwishowe watauana kweli.” “Wewe mama mpe baba hiyo video ajionee mwenyewe. Wote wanatema damu. Aibu tupu hii jamani! Na sijui Raza mtamwambia nini!” “Hilo sio la sasa hivi, inabidi kumtafuta kwanza Mina.”  Akajibu Mzee Ruhinda.

“Sasa mama wewe mtafute Pius. Akikusikia wewe, atatulia.” “Mimi nashauri tuongozane tu mama Pius.” “Ujue huyu Pius anatafuta matatizo jamani! Ni nini anakuwa kama amechanganyikiwa!” “Wewe mama nenda huko huko, hii ni aibu ya mwaka.” Paulina akasisitiza.

“Mungu wangu Raza ananipigia na mimi! Namwambia nini mimi huyu mtoto!” Mara video kama aliyowatumia Paulina ikaingia kutoka kwa Raza, safari hii kwenye simu ya mama Ruhinda. “Amenitumia na mimi!” “Amechanganyikiwa, anataka majibu.” “Naona twende wote Dodoma.” Mama Ruhinda akasikika kama aliyekwisha ingiwa hofu. “Sio kwa kukimbia sasa! Wewe pokea simu. Mwambie unaelekea Dodoma, ukirudi mtazungumza. Acha nitafute tiketi za kuondoka leo.” Mzee Ruhinda akajitoa kwenye conference call kati yake, Paulina na mkewe.

Kwa Mina.

Mina alilala mpaka jioni, ndipo akaamka. Akaamua kumpigia simu mama Ruhinda. Alipomkosa, akampigia simu mzee Ruhinda. Tunakutafuta mama, tunakaribia kuchanganyikiwa.” “Poleni baba. Lakini hali sio nzuri. Nilirudi hospitalini, kichwa kinauma na jicho nalo lilivilia damu, limeanza kujaa.” “Hapa ndio tumefika Dodoma. Tumekuja kukuona. Kwahiyo...” “Tafadhali usiwaambie kina Andy, baba. Nakuomba sana. Wanafanya fujo zisizoisha. Wameniumiza mimi, lakini nashukuru Mungu vipimo kwa mtoto anaonekana yupo salama. Naomba nipumzike kwa leo tu, kesho ndipo nitajua chakufanya.” Mina akabembeleza.

“Kwa hiyo hutaki wajue hata ulipo?” Mzee Ruhinda akauliza. “Tafadhali nisaidie baba yangu, angalau nipumzike kwa leo tu.” “Basi kwa kuwa watu wote wanawasiwasi, nitawaambia upo hospitalini, na umeomba muda. Ukiwa tayari utawatafuta.” “Sidhani kama wataelewa baba!” Mina akatilia mashaka na kuanza kulia. “Mama yao amezungumza nao sana. Naona wameelewa, wametulia. Tutazungumza zaidi nikifika hapo. Hatutakawia.” “Nashukuru baba.” Mina akamuelekeza alipolazwa, wakaelewa na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati mzee Ruhinda akizungumza na Mina, mama Ruhinda alikuwa akigombesha wanae hao wakiume. Raza naye alikuwa ameshapaniki hakuna anayepokea simu yake, hakuna anayempa majibu yakueleweka. Akamtumia na mumewe hiyo video kisha akampigia. “Sasa hivi sipo kwenye wakati wakuzungumza wala kubishana na wewe Raza. Tutazungumza baadaye.” Hapo Pius alikuwa kwenye kumtafuta Mina.

“Umeangalia hiyo video niliyokutumia lakini?” “Nilishatumiwa na watu zaidi ya wawili, wewe sio wa kwanza. Naomba nikuage.” “Hivi unajua ni kwa kiasi gani umenivua nguo hapa mjini wewe Pius! Kumbe wewe ndio..” “Nisikilize Raza. Nimekwambia sina muda sasa hivi wakugombana na wewe. Nipo kwenye wakati mgumu kuliko AIBU yako. Naomba nikuage kwa sasa, tutazungumza utakaponiona nyumbani.” “Yaani unasafiri bila..” Pius akamkatia simu, ndipo Raza akampigia tena mama yake mkwe.

~~~~~~~~~~~~~~

Raza akapiga simu tena na tena safari hii akiwa na megi. Kutukanwa na mumewe, kukatiwa simu bila maelezo ya kueleweka, kumdhalilisha, na kufichwa na wakwe pia. Alipiga mpaka mama Ruhinda ikabidi apokee.

“Mimi ndio nimekuwa mtu wakupata habari nzito kama hizo mitandaoni kweli! Kwa ubaya gani huo ambao mmeshindwa kuniambia nyinyi kama wazazi wangu! Mnajua jambo kubwa hivyo mnanificha! Mina anazaa na mume wangu nyinyi mnanyamaza!” “Ni vile upo kwenye mshituko Raza mwanangu na unahasira. Lakini..” “Halafu Pius ananikatia simu, ananiambia hana muda wakunisikiliza! Paulina naye hataki kupokea simu zangu! Lakini hata mfanye nini, hata kama mnanichukia mimi, mkumbuke mimi ni mke halali wa Pius. Tena wa kanisani kabisa. Nimezaa naye watoto wawili. Ten...” Raza aliendelea kuongea, mama Ruhinda akisikiliza.

Mwishoe akaweka mute’ kwenye simu yake ili asiwasikie wao, wakati yeye akiendelea kuongea bila kunyamaza huku akilia kwa uchungu sana.

~~~~~~~~~~~~~~

 Mama Ruhinda akaweka simu pembeni Raza akiendelea, akamgeukia mumewe. “Huyo alikuwa nani?” “Mina. Yupo hospitalini ameomba nisiwaambie Andy na Pius.” “Afadhali, wajinga kabisa!” Mama Ruhinda akawa ameshachoka na kuchukia kabisa.

“Nimemuomba Mina niwaambie ila wasiende, wamuache atulie kwanza.” “Wewe ungewaacha wahangaike usiku kucha mpaka kesho au hata siku tatu baadaye. Hawana akili kabisa! Huyu Pius mkewe bado anaongea hapa kwenye simu. Analia na kulaumu kila mtu! Pius kamkatia simu na haonekaniki kujali.” “Sasa kabla hajaaribu na huko nyumbani kwake, ni heri kumtuliza Pius, ili aweze kuzungumza na mkewe.” Mama Ruhinda akarudi kwenye simu akakuta bado Raza anahesabu jinsi anavyopuuzwa kwenye hiyo familia. Mama Ruhinda akashindwa hata kupenyeza neno. Akabaki kimya na kuendelea kumsikiliza. 

~~~~~~~~~~~~~~

Mzee Ruhinda akawapigia vijana wake. “Sasa naomba mnisikilize kwa makini.” Akaanza baada yakuwapata wote kwenye simu na kuwaunganisha. “Mina ametutafuta mimi na mama yenu.” “Yuko wapi!?” Andy akauliza wa kwanza. “Naomba unisikilize Andy. Inaonekana huyu binti umemjeruhi sana. Ameomba muda wa kujitibu na kupumzika, atawatafuta.” “Lini?”  Akadakia Pius na kuendelea. “Na mtoto wangu je, baba? Yupo salama? Maana Andy alimpiga vibaya sana, akaanguka vibaya sana. Hajadhurika?” “Kama hayo uliyajua Pius, kwa nini kwenda kuanza kupigana mbele yake akiwa mjamzito?” Mzee Ruhinda akauliza.

“Ni Andy huyo baba! Sio..” “Acha kujitetea Pius. Nilimkuta huyu Pius ameshika tumbo la mke wangu! Ulitaka nikufanye nini?” “Mimi nilikuwa nashika mtoto wangu sio Mina! Roho yako mbaya wewe Andy.” “Wewe unamtaka Mina sio...” “Mimi nakujua Andy wewe, roho yako mbaya huwezi...” Wakaanza tena kubishana hapo kwenye simu baba yao akiwasikiliza.

“Sasa hayo ndiyo yanayomfanya Mina ajione hayupo salama akiwa na nyinyi.” Mzee Ruhinda akawakatisha. Wakatulia.

“Pius, naomba mtafute mkeo mzungumze na urudi nyumbani.” “Siwezi kurudi nyumbani bila ya  kumuona Mina, baba. Hapo Raza atanisamehe. Shida yote hiyo itakuwa bure kabisa! Nawezaje kwenda kulala nikiwa sijui hali ya mwanangu?” “Sasa Mina hataki kukuona.” “Mimi niambie alipo, najua Mina atataka kuniona mimi. Tatizo ni Andy.” “Pius jiangalie wewe!” Andy akamuonya.

“Kumbe nani aliyempiga Mina? Ulitukuta tumetulia, ukaanza fujo. Kama wewe unahasira sana, mwache Mina uone kama sijamtunza vizuri kuliko wewe.” “Pius! Tafadhali tafuta amani.” “Anataka kumuua mtoto wangu kwa makusudi baba! Sitamruhusu.” “Nitawatafuta kuwataarifu hali ya Mina.” “Baba!” Mzee Ruhinda akakata simu na kumgeukia mkewe.

~~~~~~~~~~~~~~

“Naomba umuage Raza, tuzungumze.” “Sasa nitamuagaje wakati bado anaongea na kulia?” “Wewe muage, mwambie utampigia baadaye. Usisubiri jibu. Hawezi kumaliza leo, yupo kwenye mshituko huyo.” “Na kweli.” Mama Ruhinda akajaribu kuaga zaidi ya mara mbili akashindwa, ikabidi aseme tu, “Nitakupigia baadaye.” Kisha akakata wakiwa garini wanapelekwa hospitalini alipo Mina.

~~~~~~~~~~~~~~

Walimkuta Mina amelala, upande mmoja mweusi kama mkaa kabisa na Mina ni mweupe haswa kwa hiyo palitisha. Na kweli palianza kujaa. Mama Ruhinda akashika mdomo. “Mungu wangu, watakuja kumuua huyu mtoto!” Akanong’ona mama Ruhinda akiwa na mshangao. “Tumuamshe au tumuache?” “Subiri kwanza Ruhinda.” Mama Ruhinda akampiga picha akiwa vilevile amelala. Ndipo wakamuamsha.

Alipofungua macho lile jicho lilikuwa kama limevilia damu kwa ndani hata mboni ya jicho ni nyekundu. Mama Ruhinda akaweka mikono kichwani. “Mungu wangu Ruhinda!” “Naomba tulia. Utaongeza hofu.” Ruhinda akamtuliza mkewe na kumgeukia Mina. “Vipi mama?” “Kichwa ndio kinauma, lakini wamenipa dawa za usingizi ndio zinanilevya. Na pressure inaanza kupanda sasahivi. Maana mwanzo waliponipima ilikuwa nzuri, sasahivi wameangalia tena, inapanda.”

“Pole Mina mwanangu. Au ni mawazo?” “Nahisi nimeingiwa hofu, mama. Hali sio nzuri.” “Pole sana. Naamini tutapata ufumbuzi. Jaribu kulala. Sisi tutatoka kwenda kukununulia chakula, kisha tutarudi.” “Asante. Naomba msije kuwaambia kina Andy, ili angalau leo nipumzike. Hata mama na Ron msiwaambie kitu chochote. Tafadhali wazazi wangu. Tuache tu kwanza.” Hilo wakashukuru Mungu maana walijua mama yake akiongezeka hapo, akimuona hivyo alivyo, inaweza kuwa mbaya zaidi.

 “Sawa kabisa. Naona umewaza kama mtu mzima kabisa. Tunashukuru Mina. Ili patulie kwanza. Patatulia tu. Tupo na wewe.” Wakamfariji ndipo wakamuacha, akarudi kulala.

Walichofanya nikumletea chakula usiku huo, wakahakikisha amekula vizuri. “Naomba mpitie nyumbani mkahakikishe Ayan anapewa maziwa yakutosha, baba. Na kesho asubuhi kabla hamjarudi hapa awe amepewa chakula na mumuache akiwa na maziwa. Naamini kesho nitatoka tu, nitakuwa naye.” “Usiwe na wasiwasi. Pumzika tu. Tumemwambia Andy atutayarishie chumba. Tumeamua kulala hapohapo nyumbani kwake.” “Nashukuru mama yangu.” Ndipo wakaagana na kuondoka kuelekea nyumbani kwa Andy.

~~~~~~~~~~~~~~

Usiku Mina yeye alilala kama nusu mfu kwa madawa ya usingizi, lakini nyumbani kwake na Andy walilala panakaribia kupambazuka kwa kikao kirefu sana mpaka mama Ruhinda akapandisha pressure. Pius hakujali swala jingine lolote hata ndoa yake isipokuwa huyo mtoto aliyekuwepo tumboni kwa Mina. Utafikiri alishakaa kwenye ndoa kwa miaka mingi bila mtoto ndio Mina amempatia mtoto!

Andy naye hataki ukaribu wake Pius na mkewe. Ndipo ugomvi ukaanza upyaa. Wakaanza kupigana tena mbele ya wazazi wao.

~~~~~~~~~~~~~~

Pius Kaonjeshwa Asali, Anataka Kujenga Mzinga Kama Kina Afidhi, Mozee Na Omar. Na Andy Naye Ndio Ameshituka kukiwa kushakuchwa, Anakaba Mpaka Kona.

Inaendelea…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment