Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 39. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 39.

Mama Ron aliendelea kulia na kuzua hali ya simanzi hapo ndani. Mwishoe Ron akawa kama amefikiria kitu, akaona aulize. “Inamaana Andy amekubaliana na hilo!?” “Labda nizungumze kidogo.” Wakamgeukia mzee Ruhinda. “Hii habari imetushitua wote. Nikimaanisha wote tupo kwenye mshituko mkubwa, hata Andy na Mina wapo kwenye mshituko hivyo hivyo. Kwa haraka sana, inachanganya na hakuna mwenye jibu ya itakuaje. Nikuombe mama Ron na Ron, tuungane pamoja ili kumsaidia zaidi Mina ambaye ndio najua ni muhanga mkubwa katika hili.” Akaendelea mzee huyo msomi aliyezoea kuzungumza mbele wakubwa na viongozi wenye nyadhifa mbali mbali.

“Nimezungumza sana na Andy, nikimsihi amsaidie Mina. Najua inauma sana, lakini imeshatokea. Mtoto anakaribia kuzaliwa. Hakuchagua azaliwe kwa njia hii. Ni mtoto kama wengine wote tuliopewa na Mungu. Tafadhali mama, tuungane ili kutengeneza mazingira matulivu ili mpaka huyo mtoto atakapozaliwa, akute amani. Ukiniuliza kivipi! Hata mimi sina majibu yote.” Akaendelea mzee Ruhinda.

“Binafsi mimi kama baba yake Andy na Pius, nimekusudia kukabiliana kila siku na changamoto yake katika hili. Nikihakikisha zaidi Mina anakuwa kwenye mazingira matulivu mpaka atakapojifungua. Mimi mwenyewe Mungu akinipa uzima, nataka hiyo siku ya kujifungua Mina, niwepo na siku chache baada ya hapo ili tu Mina asijisikie kuchanganyikiwa na kuona ameachwa kwenye wakati mgumu. Na nilikuwa nikizungumza naye jana, muda na wakati wowote akijisikia kuchanganywa na chochote au yeyote, anipigie mimi mwenyewe simu.” Akaendelea.

“Nilitaka aje ajifungulie pale  nyumbani. Akae na mtoto mpaka muda fulani. Ili pia kumpa nafasi Andy, lakini mumewe amekataa kabisa. Anataka mke wake ajifungue yeye akiwepo na yeye amtunze mkewe. Ndio hapo sasa na sisi tukaomba chumba hapo kwao kwa kipindi hicho. Mimi na mama yao hapa, tumewaambia tutakuwa nao kipindi hicho.” Mzee Ruhinda akajisogeza mbele ya kochi.

          “Mina aliniambia alifukuzwa hapa nyumbani.” Mzee Ruhinda akaongeza. “Nipo hapa kukuomba mama, tumsaidie Mina katika kipindi hiki kigumu kwanza cha ujauzito wake na hata malezi ya huyo mtoto. Ninaukakika itakuwa ngumu zaidi kama wakijikuta wapo peke yao bila wazazi kuliingilia kati. Tafadhali mama, msamehe Mina.”

          “Nilikuwa naye siku akiwa anatapika kabla hajapelekwa hospitalini akathibitishiwa ni mjamzito. Ungejua hakuwa akijua! Yeye mwenyewe alikuwa akiniambia jinsi anavyojisikia. Akaniambia, ‘baba, inakuwa kama nina mimba wakati hata mimba ya Ayan sikutapika kabisa!’ Ndio maana haikuchukua nguvu nyingi kuamini kuwa Mina hakuwa akijua kama alijamiiana na Pius.” Mama Ron aliendelea kulia akijuta.

“Nipo hapa kwa ajili ya Mina, wala si Pius. Nataka kukuomba umsamehe Mina. Wala hakukosa. Yeye ni muhanga katika hili.” “Mimi nilimfukuza nikijua amemsaliti Andy! Nilichukia sana. Nitampigia simu nizungumze naye.” Akakubali mama Ron huku akiendelea kutokwa machozi.

“Nataka kulipa pesa kwa..” “Naomba usizungumze lolote Pius. Unafikiri pesa yako itasaidia nini sasa hivi?” Akauliza mama Ron kwa ukali akilia. “Samahani mama Mina au mama Ron kama Mina mwenyewe anavyokuita.” Akaingilia mama Ruhinda. “Najua umekasirika, lakini mama, hiyo pesa unastahili. Hata kama sio leo, lakini ipokee tena ukitaka mwambie akuongezee. Nitahakikisha anaileta yote. Kichwa chake kibaya! Usikatae pesa mama. Umehangaika kulea peke yako! Unastahili hiyo pesa. Hata ukitaka gari, nitahakikisha ananunua hata mawili.” Mzee Ruhinda akamgeukia mkewe kwa mshituko. Mkewe akafyonza kwa hasira na kuongeza. 

“Ndiyo Ruhinda! Na wala mama Mina hakukosea. Ameingia kwenye ndoa ya mwenzie, amesababisha sintofahamu ya hali ya juu! Ameingiza familia aibu ya hali ya juu! Wala samahani yake haisaidii.” “Sasa hapo mama, husaidii!” Akaongea mzee Ruhinda taratibu.“Kusaidia nini? Yeye ndio kaka wa familia. Kaka mkubwa tuliyetegemea hata sisi tusipokuwepo,  asimamie ndugu zake, mambo yaende vizuri! Ona alipotufikisha sasa hivi! Atakuwa mtawala wa nani!?”

“Wala hujaharibu familia ya Andy tu, umeharibu familia nzima ya Ruhinda. Ya sasa na ijayo. Kizazi hata kizazi kinachofuata cha kina Ayan na ndugu zake hili litasemwa na kushangaza watu. Ukae kabisa ukilijua hilo wewe Pius.” Mama Ruhinda akaendelea kuwaka.

“Ndoto zetu zote umeziua kwa..” “Tafadhali punguza hasira mama Pius. Tulia kidogo.” Mzee Ruhinda akajaribu kumtuliza mkewe. Ikabidi Ron na mama yake wapoe maana ni kama mama Ruhinda akanunua yeye ugomvi na kuwa mkali zaidi. “Toa hizo hela ulizoleta hapa. Haraka.” Akagomba mama Ruhinda. “Nimekuja na hundi.”

“Nione umeandika kiasi gani. Maana kama ni pesa ya kishenzi naku..” “Mama Pius, taratibu mama! Tafadhali tutafute amani.” “Amani inatoka wapi katika hili? Niambie amani yake inatokea wapi hapa na wewe Ruhinda! Nipe hiyo hundi acha kuniangalia.” Pius akampa mama yake. Akaisoma. Wakamuona ametoa macho. Akaichana na kumtupia.

Usinitanie Pius wewe! Hii ndio pesa yakumpa huyu mama baada ya ujinga wote huo! Unataka nikuvulie nguo hapa? Ushabeba mimba wewe ukajua...” “Subiri kwanza mama. Sijakataa! Naomba usiende mbali mama yangu. Wewe niambie pesa unayoona inafaa. Mimi mbona nitaandika tu.” “Haya niandikie hundi nauweke saini mimi mwenyewe nitaweka kiwango.” Mama Ruhinda akaamuru.  

“Nashauri undike ukiwa umetulia mama Pius, maana bado Pius anamajukumu ya huyo mtoto na familia yake.” “Hayo hakuwa akiyajua wakati anafanya ujinga wake? Afilisiwe ndipo ajue uchungu wa watu wanavyojisikia. Na nitaandika mabilioni humu ndani.” “Naomba tulia mama. Tulia mke wangu.” Mzee Ruhinda akazidi kumtuliza, mama huyo akawa anawaka kweli kweli. Maneno yakaendelea kumtoka kwa hasira.

“Jamani kosa moja lisifanye mkafuta kila kitu juu yangu. Wote mnanijua mimi sio muhuni jamani! Mama, mimi nimekuwa mtoto wako unayejisifia kwa kila mtu, kila wakati. Tafadhali naomba ukumbuke hilo mama yangu. Miaka yote tangia kijana mama, unakumbuka kusikia nimekuwa na mambo ya wanawake? Nimeingia kwenye ndoa yangu, mmeshawahi kusikia natembea nje ya ndoa? Na matatizo yote yale ya Raza, lakini mbona nimetulia! Ikathibitika, tena kutoka kwa ndugu zake wenyewe kuwa Raza aliniloga ili nimuoe, lakini sikuwahi kumuacha Raza wala sikubadilika kwenye ndoa yangu. Nikatulia kabisa.” Pius akaendelea kwa unyenyekevu.

“Katika hili nimekiri kosa, naomba na nyinyi mnisaidie kama hivi baba. Nielekezeni kitu cha kufanya, mimi mbona nitafanya tu, ili kusaidia hii hali niliyosababisha!” Pius akaendelea kuzungumza huku amepiga magoti.

“Najua sitatatua tatizo. Nimeharibu. Basi angalau ndugu zangu, wanangu na vizazi vijavyo, vijue nimewajibika. Sikukimbia. Nilikosa, na nimekubali kosa. Naomba hilo msilisahau jamani!”

“Mbona ningeweza tu kunyamaza na mtu asijue! Lakini nimekubali kubeba fedheha mama yangu. Kumbukeni na mimi nina familia. Mabinti wanao karibiana na Mina. Nakubali kosa, ndio maana nimejifikiria, nimeona niombe msamaha. Na niwajibike.” Pius akawafunga wote mdomo wakatulia.

“Nimekosa wazazi wangu. Naomba mnisaidie katika hili jamani! Nampenda sana Mina, nyinyi wote ni mashahidi. Na ninataka mtoto wangu azaliwe kwenye mazingira mazuri. Katika hili sitabadilika wala sitayumba. Nimekosa, lakini mtoto ni wangu na ninataka hata yeye ajue hivyo. Ndio maana nipo hapa kupokea ushauri wowote ule, ila tu usiwe wakunitenga na mwanangu. Katika hilo naomba mnielewe jamani, sitakubali. Ndio mtoto wangu wa pekee wa kiume!” Ron na mama yake wakashangaa.

          “Sasa hapo Pius unaanza kuharibu.” “Hapana baba. Moja ya sifa yakuwa kiongozi bora ni kuwajibika. Nimewajibika na njia aliyopatikana huyo mtoto. Lakini mtoto mwenyewe ni zawadi yangu jamani! Naomba muelewe. Mnakumbuka nilivyokuwa nikitafuta mtoto wa kiume? Nimemkosa kwa Raza, Mungu amenipa kwa kupitia Mina.” Mama Ron hoi!

“Wote tunaamini Mungu ni muweza. Wangapi wanatoka nje ya ndoa hata kubaka watoto wao wakuwazaa? Mimi si wa kwanza. Wangapi wanashika mimba? Wote tunakubali watoto wanatoka kwa Mungu. Sasa iweje mimi nizuiliwe kupokea baraka kutoka kwa Mungu! Raza alihangaika sana kushika mimba mpaka akatolewa kizazi! Wewe mama nishahidi ulinisaidia mpaka kuomba. Mbona sikufanikiwa!”

“Mtoto aliyekuwepo kwa Mina, ni wangu na ninamtaka mtoto wangu. Mungu amenijibu kwa njia hii, naamini tukishirikiana, wote tutamfurahia huyo mtoto. Tafadhali naomba na mimi mnisaidie niwe na mwanangu.”  Pius akahitimisha. Wote wakakwama.

“Jamani naona yaishe tu. Mama Ruhinda, tafadhali yaishe.” Ikabidi mama Ron mwenyewe amalize kesi. Maana washitaki wake walianza kesi na kuiendeleza wao wenyewe mpaka yeye akapoa. “Nimemsikiliza Pius, na nimeishi naye, ameongea kweli. Na yeye ni binadamu. Kupo kukosea. Halafu hata iweje, bado atakuwa baba wa mtoto wa Mina. Naona tufuate ushauri wa mzee Ruhinda. Tuwe msaada. Hawa ni watoto wetu wote. Aibu hii ni yetu wote.”

“Halafu hata kwa kitendo cha yeye kukiri kosa, nacho nichakumpongeza Pius. Ni kweli angeweza kunyamaza. Wangapi wanatelekeza wanawake wanao wabaka? Ni wengi tu, tena wengine wanawakana kabisa wakati walikuwa kwenye mahusiano! Kwa hiyo hata kwa hili pia tumpongeze Pius.” Kwa hekaheka aliyoianzisha mama Ruhinda, na maelezo ya Pius, mpaka IKAMTULIZA mama Ron mwenyewe. Bila kutarajia akajikuta akimtetea Pius, muhalifu.

“Jamani naona yaishe. Yaishe kabisa. Mimi nitamtafuta Mina nitazungumza naye. Kuwe na amani. Wala hamna haja ya pesa. Tusameheane tu. Tuendelee kuanzia hapa tukimfikiria Mina na watoto. Tafadhali mama Ruhinda.” Na yeye akaungana na mzee Ruhinda kumtuliza mpaka akatulia.

“Lakini lazima huyu Pius aache faini. Kutokufanya hivyo ni kama kumdhalilisha Mina. Mina ni binti aliyemkuta amelelewa na alikuwa na ndoa yake. Sio malaya tu. Kimila na utataribu hawezi akaachwa hivi hivi. Hakika mimi sitakubali. Unanisikia Pius?” “Sawa mama. Sijakataa!” “Sasa nisikilize Pius.” Mama Ruhinda akashika usukani.

“Si Andy amekukatalia usimtunze mkewe?” Mama Ruhinda akauliza. “Labda kwa kuwa bado anahasira.” Akajibu Pius. “Tafadhali Pius, fuata kila kitu anachokwambia Andy.” Ron na mama yake wakaletewa ugomvi hapo kwao. Wanazozana wenyewe kwa wenyewe, wao wakiwatizama.

“Sawa baba. Mbona sijatuma tena pesa!” “Sasa kwa kuwa mzigo umepungua kwa Mina, jua hii hundi ya mama yake nitaandika pesa ya kueleweka mpaka ikuume.” “Sawa mama.” “Ndio ukome kuchezea watoto wa watu. Huna adabu wewe!” “Sawa mama yangu, wewe andika pesa yeyote ile unayo itaka. Nakubali yote kwa garama yeyote ile, bora nimpate mtoto wangu.” Kufunga na kufungua mama Mina akafutwa machozi kitajiri.

~~~~~~~~~~~~~~

Waliondoka hao kina Ruhinda na kuwaacha Ron na mama yake wamepigwa na butwaa. Wakatulia kimya kwa muda. “Mbona Mungu amenipa kizaizai!” Ron akabaki kimya. “Mina imekuwa ni shuguli! Tokea anazaliwa huyu mtoto mpaka sasa, ni heka heka jamani!” Mama Ron akabaki hajui afanye nini.

“Nashauri zungumza na Andy na yeye umsikie.” “Naona hata aibu Ron. Nilimfukuza Mina vibaya sana. Matusi niliyomtukana wakati alikuwa akijinyima kwaajili yangu! Ona alivyopabadilisha hapa nyumbani! Nikamtupa wakati akinihitaji hata nisimtafute! Yeye mtu baki akaenda kumchukua, mimi nilimtoa mgonjwa na kumzira!” “Ndio umepata nafasi yakutengeneza. Halafu uzuri umemkosea Mina. Hajui kukasirika. Atasamehe tu. Lakini nashauri uanze na Andy.” Ron akashauri.

Mama Ron kwa Andy!

Mama Ron akampigia Andy. Akamueleza kila kitu kuhusu Pius, nakutaka kumsikia yeye anasemaje. “Sijui mama yangu! Hata sielewi ndio itakuaje, lakini ninachomshukuru Mungu, mke wangu amenitanguliza mimi katika kila jambo, angalau hilo linanipa moyo na kunifariji. Mengine nitafanya kama alivyoshauri baba. Kila siku tutaipokea kwa kadiri itakavyokuja.” “Huo ni uamuzi wa busara. Najua hakuna aliyejiandaa kwa hili. Mimi nawaombea kila la kheri.” “Asante.” Wakatulia kwa muda. Akajua anataka kuomba kuzungumza na Mina.

Na yeye akatulia kabisa. Mwishoe akajikaza. “Mina yupo karibu nizungumze naye?” Mina alikuwa amekaa pembeni ya mumewe, akasimama na kuondoka kabisa pale. “Amekwenda chumbani.” Hakutaka kudanganya. Mama Ron akaona aage bila ya kuongeza neno.

~~~~~~~~~~~~~~

Andy akamfuata Mina chumbani, akamkuta akilia. “Mama alinifukuza wakati namuhitaji, Andy! Mtu ambaye ndio alikuwa kimbilio langu alinifukuza bila hata kunisaidia! Kama ningekufa, inamaana mpaka sasa hivi angekuwa hajui na wala hajali!” “Kutojali nina uhakika anajali. Hujamuona mama yako Mina. Amebadilika kabisa. Hayupo sawa, hata afya yake haipo sawa. Nafikiri na yeye alipatwa na hali kama yangu. Hakujua jinsi ya kufanya. Njoo hapa nikwambie kitu.” Akaenda kukaa pembeni yake.

“Kuwa na moyo mkubwa zaidi ya hicho unachojisikia. Kama ulivyofanya kwangu. Japokuwa nilikuwa nimekukosea, lakini uliweza kunitafuta, ukazungumza na mimi, ukapambana na Paulina, hukujali maneno yake makali, ukakaza moyo mpaka ukampata Ayan. Sasa kumbuka ni mara ngapi mama amekuwa akikutafuta kila unapokuwa unamtoroka.” Mina akalia sana. 

“Japokuwa unakuwa umemtoroka na kumuumiza, lakini bado amekuwa akikutafuta. Naomba safari hii iwe zamu yako.” “Andy!” “Fanya tu. Ni ngumu lakini jitahidi. Si na wewe ni mama? Na pengine tutajaliwa mtoto wa kike, au ndio hutazaa tena? Unaishia na huyo tu?” “Nataka kama ni kuzaa tena iwe na wewe, Andy. Nitakuzalia watoto wote unao wataka. Ila nilijua tutazaa mtoto wa pili wa kike. Unajua nilishamfikiria na jina lake?” Andy akacheka tayari alishaanza kumvua nguo ya ndani mkewe.

Akaanza kupitisha mikono huku akimnyonya midomo yake. “Huchoshi Mina!” Mina akacheka taratibu huku akijiweka sawa hapo kitandani na kumalizia kutoa nguo ya juu. “Nataka nifurahie, sitaki vitu vya juu juu.” Andy akachangamka huku anavua nguo zote. “Jina la mtoto?” Akauliza Andy huku anarukia kitandani.

“Ayana.” Andy akafurahia sana. “Mbona kama namtaka huyo Ayana kwa haraka?” “Tutaunganisha Andy, wala usijali. Niombee nijifungue salama.” Andy alishakimbilia matiti yake na kuyanyonya taratibu asimuumize. Akamsikia Mina akifurahia, akajua haumii. Yakaanza mapenzi mpaka wakaridhika, wakatulia hapo kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~

“Nina mambo mengi sana sasa hivi Andy. Akili haijatulia. Pius anaonekana anamuhitaji huyu mtoto, sijui itakuaje, sijui nitafanyaje!” Andy akabaki kimya. “Si sasa tu, hata baadaye. Nafikiria wanangu Andy! Wanaitanaje, wanawaitaje nyinyi! Malezo gani mazuri yatakayowatosha ili wasije rudia kosa! Hayo yote nayawaza.”

“Maswala ya mama, naomba niyaache kiporo kwa muda mpaka nitakapotulia. Najiona nipo sehemu ambayo mimi mwenyewe  sijielewi! Siwezi kuongeza mtu mwingine, tena ambaye nitamwangalia, nikumbuke amenikatia tamaa, haniamini! Natakiwa niwe naye kwa namna fulani ili kumthibitishia hili na lile.” Mina akavuta shuka na kujifunika, akakaa sawa.

“Unajua Andy, mama bado hajaamini au haamini kama nimebadilika?” Andy kimya. “Mama haamini kama naweza kutulia na wewe tu. Hanipi heshima kama anayompa Ron. Kwa upande fulani namuelewa, lakini najihisi kama nastahili kuaminika kwa maisha niliyoishi takribani miaka minne sasa! Nimemuonyesha mama kwa vitendo na maneno kuwa nimebadilika. Lakini tokea hili jambo halijatokea, au tokea hajanifukuza nyumbani, bado mama amekuwa na wasiwasi na mimi sana. Tena ilikuwa heri wewe Andy, mpaka nilikushangaa.” Andy akamwangalia vizuri.

“Kitendo chakuniacha peke yangu kwenye lile jiji, tena ukiwa huna wasiwasi kama nitakusaliti! Nilikipenda Andy na nikajisikia vizuri japo nilikuwa nakuwa na hamu na wewe. Hukuwahi kunitilia mashaka hata mara moja, Andy! Mpaka nilikuwa nikikushangaa wewe ni kiumbe wa namna gani!”

“Hukuwahi kuwa na wasiwasi na nani nazungumza naye kwenye simu hata nikiwa na wewe au nani nakuwa nikichat naye! Uliniamini mpaka ukaniongezea ujasiri. Lakini sio mama, Andy. Alikuwa akiniona natuma tu ujumbe, anaanza kukasirika na kuniambia nisije nikaanza tena. Na atataka nimuonyeshe simu yangu!” “Haiwezekani Mina!” Andy akashangaa.

“Kweli Andy! Kunakipindi mpaka tukagombana kabisa. Hatukuzungumza kama mwezi, nikawa hata simpeleki mtoto nyumbani, ukaribu na mzee Ruhinda na mama yako ndipo ukaongezeka. Nikaona wao wananiamini kuliko mama.” “Ilikuaje?” “Nilikuwa pale nyumbani kwa mama. Nikapigiwa simu na mmoja wa wale vijana wawili niliokuwa nimekwambia nilikuwa nao karibu lakini hatukupata nafasi yakuwa peke yetu hata kusoma.”

“Sasa nikapokea simu nikiwa ndani. Nikaanza kucheka naye sana. Nikamuona kama mama amekasirika, nikafikiri ni kama napiga kelele, yaani naongea kwa sauti. Nikaamua kutoka, kwenda kuzungumza naye nje. Tukazungumza kwa muda mrefu tu. Nikarudi ndani. Acha mama aanze kunitukana. Sasa mimi nikamwambia mbona anakasirika na kuongea maneno mengi mbele ya mtoto wangu wakati sijakosa!” “Yeye alikuwa anasemaje?” Andy akauliza.

“Anajua ni mwanaume wangu! Kwamba nimeanza mahusiano wakati wewe upo huku! Nikamwambia mama, nampenda Andy. Nimeamua kutulia na Andy. Siwezi kumsaliti hata iweje. Unajua aliniambia yeye ananijua siwezi kuishi bila kushikwa shikwa, na wewe upo mbali, nilazima nikutafutie msaidizi.” “Mina! HAIWEZEKANI!” “Kweli Andy!”

“Na ni maneno yanayofanana na hayohayo alinitukana nayo wakati ananifukuza kwake, uliponiacha. Nahisi nimemuumiza sana mama kiasi ya kwamba, hakuna jinsi ananiamini tena. Mahusiano yetu nahisi yaliisha muda mrefu, hajui tena aishije na mimi. Hata siku ya harusi yetu tulipokuwa naye kule Nairobi. Ile siku yetu ya harusi, mama aliongea jamani!” “Anaongea nini!?” Andy akauliza.

“Sijui ndio ulikuwa ni wosia au la! Aliniharibia ile asubuhi, nikashindwa hata kula kile chakula uliniletea na kadi yenye maneno mazuri kuwa unanipenda sana. Unakumbuka?” “Nakumbuka.” “Basi hata sikufaidi yale maneno wala kile chakula. Nilikuwa nina hali mbaya, Andy! Kama nipo msibani, wakati ilikuwa siku yangu ya harusi.” “Pole Mina. Sikuwa najua!”

“Acha tu. Nilikuwa nimeumia, mpaka nikatamani kama na yeye asingekuwepo kama kina Ruhinda! Alichukua furaha yangu yote. Hakika alivuka mipaka. Alianza usiku uliopita vizuri tu kama wosia, nikamuhakikishia tena kwa machozi kuwa nimebadilika, sitakusaliti. Akaona haijatosha, ndio asubuhi yake akaanza sasa kunikumbusha uchafu wangu wote!” “Haiwezekani Mina!” “Ilikuwa mbaya Andy, mpaka ikabidi nimuite Ron. Akamtuliza, akaniambia nijaribu kutulia, tukakaa naye mpaka muda wa kuja kanisani ulipofika.” Andy akaumia sana.

“Ndio maana haikumuia vigumu kunifukuza Andy. Mama hakutaka hata kuniuliza baba wa mtoto! Hakutaka kujua kama uliniacha hata na shilingi! Hakutaka kujua ninakwenda wapi! Na hakutaka kunitafuta kujua nilipo! Na nikwambie kabisa, ujue, kuwa mbali na  kwake au yeye, ilikuwa nafuu.” “Kwa nini!?” “Nilishamtia aibu sana kwa ndugu zake. Kitendo cha mimi kujulikana nimeachika na ninazunguka na tumbo lisilo lako, ndicho kinamkondesha mama. Ninaukakika na hilo kwa asilimia 100 Andy, lakini sio mimi kuwa matatizoni.” “Unajuaje Mina?” “Kwa kuwa aliniambia Andy!” Andy akashangaa sana na kuumia.

“Haiwezekani Mina!” “Hakika aliniambia Andy. Aliniambia nishamuaibisha kwa wazazi wake na ndugu zake vyakutosha. Kwenye ukoo wao mimi ndio tatizo na gumzo. Ikitokea nashindwana na wewe, sura yangu nisiirudishe kwa ndugu zake, wala nisiwaambie. Niendelee na maisha yangu kwa kuwa kila walilowahi kutabiri ndugu zake juu yangu, huwa linatimia. Akaseme safari hii nikisababisha likitimia, yeye hataficha sura yake kwa kuwa ameishiwa na sehemu yakuficha uso wake. Iwe zamu yangu.” Andy akanyamaza kabisa lakini akiwa ameumia sana.

“Kwa hiyo nakuomba Andy, kwa mara ya kwanza, niache nitatue matatizo yangu mimi mwenyewe kwanza bila mama. Acha hili la Pius na huyu mtoto nilijue hatima yake, ndipo aje arudi kwenye maisha yangu. Lakini sio sasa hivi nikiwa au kukiwa kwenye hii hali ya sitofahamu na yeye akaja kujisikia anawajibika kwenye kutafuta suluhu! HAPANA.”

“Acha nihangaike na wanangu kama alivyoniambia yeye mwenyewe. Niweke mambo yangu sawa, ajue aibu yangu ni yangu haimuhusu yeye wala ndugu zake. Na nitajitahidi kuweka mbali hii aibu yangu. Pakitulia, ndipo nimtafute sasa.” “Sawa. Naona tufanye hivyo. Nitazungumza na Ron pia kuwa kwa sasa wakuache kwanza. Unahitaji kutulia.” Mina akalifurahia hilo kuona wamekubaliana na Andy.

Better Late Than Never.

Japokuwa ni kama alishachelewa kwa mkewe, maji yalishamwagika, alishaacha mwanya, Pius akaingia katikati yao, lakini ahadi ya kwenda mapumzikoni hao wawili Andy akahakikisha anaitimiza tu. Lakini Mina alihakikisha Ayan anaongozana nao. Waliondoka Dodoma siku ya jumamosi asubuhi, kuelekea Zanzibar. Huko ni kweli Mina alipata fungate ya pili. Palikuwa na utulivu wa namna yake. Wao watatu kama familia wakijiwekea msingi na malengo yao.

Nia Ipo Ila Uhalisia Ni Halisi.

Ni kama Andy alikuwa akikwepa kabisa mazungumzo juu ya mtoto aliyekuwepo tumboni kwa mkewe, wa Pius. Na Mina naye akaona asianzishe mambo yatakayowaondoa kwenye ile furaha aliyokuwepo nayo Andy na mwanae. Akabaki akimfikiria mtoto wake na nafasi yake kwenye hiyo familia.

Alikuwa akiwatizama Andy na Ayan jinsi wanavyocheza kwa furaha. Na kwa muda aliowachukua kutoka Iringa, ukweli Andy alijirudi haswa. Mina akamuona hata amekuwa bora kwa Ayan. Mambo mengi alimuiga Mina vile anavyomfanyia Ayan, ukaribu kati ya Ayan na baba yake ukaongezeka. Ungejua kama ni mtoto wake anayempenda sana. Wakawa wao wawili wakicheza hili na lile na Andy akizungumza naye Ayan, kumfanya tu achangamke na kumuonyesha yeye yupo na anamjali.

Mina akawaangalia wakiwa wanachezea maji yeye amejilaza kwenye kiti na tumbo lake mtoto akicheza kimya kimya. Amejishikilia tumbo. “Huyu mtoto akija kuitwa tu Pius Junior, ndio atatengwa kabisa kwenye hii familia. Atabakia na mimi peke yangu, Andy hataweza kuwa naye karibu.” Mina akawaza hapo kitini huku akimsikia Ayan akiongea kwa sauti huku akicheka sana na mtoto wake tumboni naye akawa anacheza.

Akatamani hiyo mimba ingekuwa ni mtoto wa Andy ili awe anamshika kama alivyokuwa akifanya kwenye ujauzito wa Ayan. Lakini Andy ni kama alijionya au hakutaka kuchezea hilo tumbo kabisa. Akakumbuka jinsi Pius alivyokuwa akimshika kwenye huo ujauzito. Kwa upendo akimpapasa na kumbusu. Kumbukumbu zikaendelea kumjia na hapo akaelewa kuwa ilikuwa upendo wa kibaba kwa mtoto wake. Pius alijua ni mtoto wake tokea zamani. Shika ile ya tumbo, alimaanisha si kutaka tu kumshika Mina. “Alikuwa akimshika mtoto wake.” Mina akawaza.

Akakumbuka mapenzi aliyoyafanya na Pius. Akavuta pumzi kwa nguvu. Hata yeye alimfurahia. Kwa hakika Pius alimjali sana. Kwa sehemu akaanza kuelewa mengi.

          Swali kubwa likawa, mapenzi hayo ya tokea mwanzo yalikuwa kama shemeji kwa kuwa Pius ni mtu anayejali sana, au kama alivyomwambia kuwa anampenda sana! Kumpenda huko ni ili amzalie mtoto, au yalikuwa mapenzi ya dhati kwake! Mina akaendelea kumuwaza Pius huku akimpapasa mtoto wake. Kila alipotafuta sababu yakumchukia Pius, akajikuta wema wake unazidi.

Siku alizokuwa naye hospitalini akimuuguza yeye au Ayan. Jinsi alivyomtunza! Akakumbuka ombi la Pius akimuomba amfikirie juu ya jina. Akatamani ingekuwa mtu mwingine, lakini ni “Pius!” Mina akawaza. “Huyu mtoto wake anastahili kupewa jina lake Pius.”

Mina akaendelea kuwaza akitamani moyo wa Andy ndio ungekuwa wa Pius. Alijua ingekuwa rahisi. Pius ALIJAWA upendo wa hali ya juu na alijaliwa kujali pasipo unafiki. Akamkumbuka jinsi alivyokuwa akimpenda Ayan kama mtoto wake wa kumzaa, na Ayan aliyajua mapenzi ya Pius. Alikuwa akibebwa tu na Pius, atatulia mikononi au kifuani kama kwa baba yake na si anko.

Sio kwamba Andy hakuwa akijua nyakati huyo mtoto akicheza, zaidi macho yake yanapokuwa yako kwa Mina. Alishajua kabisa ni wakati gani huwa anacheza, kwani aligundua Mina huwa anatulia kimya kabisa akimsikilizia mwanae. Mara kadhaa Andy alimuona Mina anatulia kabisa, hata katikati ya mlo au mazungumzo, anajishika tumbo na kutulia kabisa. Ndipo akajua ni kipindi mtoto wake anapocheza huko tumboni, akajikuta na yeye ndio muda anamfikiria huyo mtoto, na itakuje! Lakini hakuwahi hata kugusa hilo tumbo. Alinyamaza kimya, na wakati mwingine kuondoka kabisa hapo.

Ayvin Pius Junior Ruhinda.” Wazo likamjia Mina. Akacheka maana moyoni lilikubalika. “Ayvin Ruhinda. Hili ndilo litajulikana kwa watu, halafu hilo la Ayvin Pius Junior Ruhinda itakuwa kwenye cheti.” Akakubaliana na hilo, akaendelea kumpapasa mwanae. “Wewe utaitwa Ayvin, kama Ayan kaka yako.” Mina akampapasa mwanae taratibu.

Akamuombea, akamtabiria mema mengi si kama kwa Ayan. Mina huyu alimjua Mungu kwa karibu si kama alivyokuwa mjamzito wa Ayan. Mimba hii ni ya Pius mume wa Raza. Mina alimuogopa sana Raza. Hofu ya kudhuriwa yeye na mwanae ikamfanya awe karibu na Mungu zaidi. Hakuacha kuomba kila wakati akimuombea mwanae ulinzi pia.

~~~~~~~~~~~~~~

“Unasinzia?” Andy akamtoa katikati ya maombi akiwa amefunga macho. “Hapana, nilikuwa nikizungumza na Mungu wangu pamoja na Ayvin.” Andy akatulia kidogo, akakaa kwenye kiti cha pembeni macho kwa Ayan. “Nimempa jina la Ayvin ili asitofautiane na ndugu zake.” Mina akajieleza taratibu, Andy hakujibu. Mina na yeye akaona anyamaze lakini akiumia asijue itakuaje. Ni kama Andy alishindwa kabisa kuwa karibu na huyo mtoto japo alimtaka Mina.

~~~~~~~~~~~~~~

Je, itakuaje?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment