Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 37. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 37.

Jumapili usiku akiwa ameshaingia chumbani na mwanae walale maana hapo ni wao tu ndio walikuwa wakidamka. Na Pam peke yake ndiye aliyekuwa akifanya kazi ya kuajiriwa, wengine wote haswa wakina mama, walikuwa wakina mama wa nyumbani, waume zao ndio waliokuwa wakitoka kwenda kusaka vibarua mtaani.

Akasikia Mill akisalimia nje. Alifurahia moyoni, hakuamini. “Washaingia kulala.” Akasikia akiambiwa na mama Pili aliyekuwa akimalizia usafi hapo uwani na yeye aingie nyumba kubwa anakoishi na familia yake, alale. Aliposikia mlango wao ukigongwa Shema akamwangalia mama yake wakiwa wamelala pamoja. “Kamfungulie.” Akashuka na kumfungulia baba yake.

Akamsalimia na kumkaribisha ndani. “Unaendeleaje?” “Vizuri.” “Pole sana Shema. Pole sana. Naomba kuona ulipoumia.” Akamwangalia mama yake huku akisita. “Naona tu.” Mill akamsihi kwa upendo. “Ila mimi sio mwizi. Alinipa Mia. Sikujichukulia tu. Kwanza hata chumbani kwake sikuingia. Watoto wako wamedanganya. Wamesema uongo.” Mill akaumia na kumuhurumia.

“Najua wewe si muongo wala si mwizi, Shema. Ilibidi baadaye kumbana Mia, akaniambia ukweli. Lakini pia sikukutilia mashaka. Nilizungumza vile sio kukushutumu au kukuhisi vibaya, ni kuweka tu utaratibu wa pale. Na pia kama niliongea vibaya, naomba unisamehe.” Mpaka Pam akajisikia vibaya.

Mill mtu mzima na uwezo wake, anajishusha mpaka huruma! Shema akarudi kitandani kwa mama yake. Akalala. Mill akabaki ameinama pale alipokuwa amekaa, Pam akatoka kitandani na kwenda kukaa mbele ya kitanda.

Akamwangalia. “Anaendeleaje?” “Wamemtoa nyuzi. Kumebaki hapo palipovilia damu, ila kidonda kimepona.” “Samahani sana Pam. Tafadhali nisamehe. Lakini jua siwezi kuacha mtu yeyote yule akamnyanyasa Shema. Sithubutu! Na yeye ni mwanangu na ninampenda. Na nimezungumza nao sana.”

“Lakini naomba huko usimrudishe. Tafadhali sana. Huyu mtoto yupo sawa kabisa hapa. Usione unawajibika kumuweka kwenye hayo mazingira yenu ya hali ya juu, ya kitajiri. Mwanangu yupo sawa. Mmemtia hofu, anaogopa kabisa kuwasogelea! Hapana Mill.” “Naelewa. Lakini swala la shule? Maana nilitaka nije kumchukua kesho nimpeleke shule. Angalau aendelee na wenzake. Hawajafika mbali. Mihula yao ya shule si kama shule za hapa. Wao ni kama wanaanza. Nimezungumza nao, hajachelewa.” “Sawa.” Mill hakuamini.

“Kwamba upo tayari anaanze kesho?” Akauliza kwa kutaka uhakika. “Si ndivyo unavyotaka?” Ikabidi Pam na yeye aulize. “Kabisa. Kila kitu kipo tayari kasoro yeye na sare zake. Tena akifika wakimjaribisha, wanaweza kumpa siku hiyohiyo.” “Unataka saa ngapi awe tayari? Naweza hata kumsogeza.” “Hapana. Nitamfuata. Saa 12 kamili asubuhi awe tayari.” “Sawa.” Mill akatulia kidogo akawa kama anasita kusema kitu.

Pam akamgundua. “Umefanya nini tena?” “Sio kitu kibaya.” “Sasa mbona unasita kusema?” “Katika majina ya Shema nimeongeza na langu.” Pam akapigwa na butwaa. “Na usikasirike. Kama hutaki, tusigombane, nitalitoa. Ila nimemuandikisha kwa jina la Shema Shelukindo Mgini.” “Kwamba la ukoo wetu ndio liwe la katikati lako ndio liwe la mwisho?!” “Ndiyo.” Akamuona kama anayetaka kulipuka, akawa kama amejionya. Akatulia.

“Ila kama unaona ni sawa mtoto wangu MIMI, aitwe jina la BABU yako WEWE, sio langu, mimi sitabisha. Nitaenda kulifuta kesho. Nimuache aitwe vile unavyotaka wewe.” “Hakika unanijaribu kupita uwezo wangu!” “Basi Pam. Basi. Kesho nitaenda kufuta langu.” Akajilalamisha makusudi.

“Na uhakikishe anaitwa majina yote matatu. Sio Shelukindo lifupishwe liwe ‘S’ aishie kuitwa Shema S Mgini!” “Sithubitu.” Alifurahi huyo na kuondoka haraka bila ya kuongeza jingine, asije haribu. Ila akashangaa vile Pam alivyo tulia siku ile. Akajua amesoma barua zake.

Kutoka Uswaz Mpaka Internatinal School.

Alifika hapo saa 12 kamili asubuhi. Pam alishamwandaa mwanae. Alikuwa msafi na alishatolewa pop. Baba yake akamchukua, Pam akawahi daladala na chapati zake kuelekea kazini.

Aliweka juhudi na mwanae, mpaka Pam alikuwa akimuhurumia. Alfajiri anakuwa amewasili hapo na kumrudisha jioni kwa wakati. Akafanya hivyo kama mwezi mzima.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Jioni moja wakati amemrudisha mtoto, Pam akatoka na kumfuata garini na kumuuliza. “Kwani yule dereva aliishia wapi?” “Alinimbia ulimfukuza. Nikajua hutaki mtu mwingine amchukue Shema.” “Wewe tuma dereva ili uwe huru na kazi zako.” Akamuona anafikiria.

“Ingenisaidia. Lakini, huu muda ninaokuwa naye njiani, nahisi unamsaidia sana Shema. Kumbuka ametoka kwenye masomo karibu yote ni kiswahili, lakini sasahivi masomo yote ni English. Sasa alipogundua na mimi nilisoma kiswahili na najua English, kuna maswali ananiuliza tukiwa njiani. Nahisi anakuwa akiyaandika kila akikwama, ambayo ni yale madogo madogo nafikiri hawezi muuliza mwalimu, akamuelewa. Sijui kama unanielewa?” Pam akawa bado anataka kujua zaidi. Akaendelea.

“Namuhisi anaakili sana, halafu ni msomaji. Hata jinsi anavyouliza, utagundua ni mtu mwenye uelewa wa juu. Au anaufahamu na anachokizungumzia. Kwa hiyo kila akiwa anasoma, akikutana na kitu kikamtatiza, nahisi anaandika. Nikiwa naye njiani anaomba nimtafarisie. Au kumuelezea zaidi.”

“Kwa mfano mdogo tu, upande wa hesabu anajua kigao kidogo cha shirika. Hesabu ni zilezile, lakini sasahivi anakutana na hesabu anazozijua, lakini wanamwambia kwa lugha nyingine kwamba atafute low denominator. Basi ndio ananiuliza kama ni vilevile au ni tofauti.”

 “Aaah! Masikini mwanangu! Ndio maana amepoa, michezo amepunguza! Kutwa yupo ndani anaandika, wenzie wapo mlangoni wanamsubiria hamalizi! Utawaonea huruma! Nikimuuliza, ananiambia anamalizia. Wakati mwingine usiku anaomba tusizime taa, ili asome, analala ameshika kitabu! Sijamuona akisoma hivi tangu anaanza shule, mdogo. Amezaliwa na ile akili akifundishwa darasani, ujue ndio kimekaa. Harudii kusoma tena. Sasa kumuona anajisomea mpaka muda wa mpira hamna, nikahisi amepata kibako yake. Kumbe ni lugha!”

“Ila kwa jinsi ninavyomuona na hiyo juhudi, anahitaji muda mfupi sana, atakaa sawa tu. Lugha ndio kwa sasa ni kikwazo. Hajaweza pia kuzungumza na wenzie. Walimu wake wameniambia bado hajaweza pata rafiki. Maana pale ni watoto wa mabalozi, na wafanyakazi wa kigeni waliopo hapa nchini kwa shuguli maalumu. Na waafrica wachache ambao ni kweli hawajui kiswahili. Amejikuta amekwama peke yake.”

Masikini mwanangu!” “Hapana Pam. Namuona hajakata tamaa. Na mimi sitaki kumuonyesha ni tatizo. Nimewasisitiza walimu wake wamchukulie taratibu sana ili asipaniki na kukata tamaa. Kwa upande mmoja bila marafiki itamsaidia kupunguza destruction, atajiangalia mwenyewe na kufanya mambo kwa haraka na vizuri.”

“Wanasema muda mwingi kwa kuwa yupo peke yake, anakuwa anasoma. Na wanasema kwa kuwa anapenda kusoma na anatabia nzuri, walimu wengi wanajisogeza kwake kumsaidia. Akishaweza kuweka lugha kwenye anachokifahamu, atawakimbiza wale watoto wakizungu pale, mpaka watamjua Mgini kwa kumtamka kama wazawa wa hapa.” “Unavyojisifia! Ndio maana umeweka jina lako mwisho na kutoa la babu yangu. Mbaya wewe!” Mill akacheka sana.

“Acha nimsaidie kidogo. Nabanwa kwenye majukumu yangu mengine, na dereva angenisaidia sana tu, lakini nimeona ni mtoto mwenye muelekeo, halafu ananihitaji si kama wale ndugu zake, acha nimtie moyo. Nikishamuona amekaa sawa, ndio nitamtafutia dereva. Ila acha sasahivi niwe naye mwenyewe. Apate smooth transition.”

“Naomba uelewe nakushukuru Mill. Kutoka kwenye moyo wangu, pokea shukurani zangu. Asante kwa kuwekeza kwa mwanangu, nakushukuru sana. Asante.” “Pam, ni mtoto wangu pia!” “Mtoto wa kukutana naye barabarani ndio umuhangaikie hivi! Sisi tulikuwa watoto wa ndani ya ndoa na pia tuliachwa, sembuse Shema wangu huyu! ASANTE.” “Shema si mtoto wa barabarani. Huyu mtoto amezaliwa ndani ya penzi zito la agano lenye baraka za wazazi wetu.” Pam akaondoka kabisa hapo dirishani alipokuwa amesimama kwenye gari lake. Akaingia ndani bila ya kujibu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mill akakazana na huyo mtoto, yeye mwenyewe bila kuweka mtu. Ndani ya miezi mitatu kweli matokea yakaanza kuonekana. Akaanza kuburuza watu darasani kiasi cha kushangaza wote. Yale masomo waliyokuwa wakifeli wengine, yeye anaweza pata asilimia 100 au akifeli ni 98, halafu anayemfuata anaweza akapata hata asilimia 45 au chini zaidi. Akaanza kuwa gumzo hapo shuleni.

Kila mwalimu akamjua. Na kwakuwa hakulelewa mazingira ya watoto wa wakishua/kitajiri ya kulemazwa, akawa na adabu za kitanzania kabisa hapo shuleni, halafu kwa wote. Akazidi kuwavutia walimu wake ila wanafunzi wenzie kumuona mjinga au mshamba.

Mtoto aliyelelewa kwenye nyumba ya kupanga uswahilini, mama watatu, wote wapo naye na watoto wa mtaani wakiishi kijamaa, basi pale shuleni akajulikana kwa kujali watu wote bila kubagua.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku ya mwisho kabla ya kufunga shule, walipanga kutambua watoto waliofanya vizuri na kuwapa zawadi. Sasa kabla ya hiyo siku kufika, jioni moja ambayo anamshusha Shema, Pam alifanya kama mazoea, lazima amfuate Mill garini aulizie maendeleo ya mwanae. Maana huwa hashuki garini, akimshusha tu, anaondoka.

Mara nyingi Pam husubiria kabisa nje. Akiona tu gari, anasimama karibu. Mwanae atasalimia na kuingia ndani kuwahi chakula, yeye anabaki kuuliza kwa kifupi. “Nimepewa barua maalumu ya mualiko pale shuleni kwao hawa. Katika watoto wanaofanya vizuri shuleni kwao, na yeye yupo. Watawatambua mbele ya shule nzima na wazazi. Wametuambia tunaweza kualika watu wa karibu. Ni muhimu Pam. Na ni kitu kikubwa. Naomba ujitahidi uwepo.”

 “Na mimi ameniletea hiyo barua. Lakini kumbuka nimeajiriwa. Ikitokea yule mama ananipa ruhusa, nitakuja. Kesho nikifika tu, nitamuomba ruhusa. Sasa inategemea na kichwa chake vile alivyoamka. Hatabiriki. Ila nikishindwa, tafadhali nichukulie video na picha nyingi nimuone.” “Tafadhali naomba uhudhurie Pam.” “Nitajitahidi. Sina chaguzi Mill! Hii kazi ndio inategemewa mpaka na mama yangu mzazi kule kijijini! Hana msaada mwingine ila mimi tu. Siwezi ipuuza au kukosea. Nikikwama mimi, jua na wao kule kijijini wamekwama.” “Naelewa.” Akafikiria na kuona aulize.

“Mbona kama Eric ana kazi nzuri sana?” “Mmmh! Hafikiki. Na mkewe alishakuwa muwazi kabisa kuwa na wao wana majukumu mazito. Wanasomesha watoto wao kwenye shule za garama na kujijenga. Ni kama mkewe ndiye anayeshikilia pesa yote. Mbaya zaidi, niliposhika hii mimba ya Shema na mama kuja huku kunisaidia, aisee ni kama nilimponza. Eti amemsusa mama, kwamba ananiendekeza. Alitakiwa kuniacha, nijifunze peke yangu. Ila mama ananiambia nisijali. Amepata tu sababu. Hakuwa mtoaji tokea amepata mke. Kwa hiyo Eric si wakumtegemea kabisa. Nisipomtumia mama pesa, ujue ndio amekwama.”

“Ndio na bibi na babu?!” “Mjomba anajitahidi kwakweli. Na mkewe ni msaidiaji japo mlalamishi sana. Japokuwa nilikuwa nikiishi kwao, nilipokuwa nikienda kijijini, shangazi alikuwa haachi kunipa vitu nipeleke kwa wakwe zake. Hana roho mbaya, ni ubinadamu wa kawaida tu. Ila sasa sitaki mama akae pale aombe wazazi wake mpaka pesa ya sabuni yake yakuogea! Au akiugua ndio tena ategemee wazazi ambao kwanza ni wazee, pili na wenyewe wanamtegemea mjomba! Naona sio sawa.”

“Unajitahidi Pam! Unajitahidi sana.” “Hivyohivyo, sio nyingi ila tunasogea.” “Binafsi najivunia Pam wangu.” Pam akacheka kinyonge na kuondoka hapo garini. Ila angalau waliweza zungumza. Angalau hilo likamfariji Mill!

Maji Yamezidi Unga kwa Mill na watoto wa Marekani.

Ila ukweli furaha ya Mill ilikuwa ni pale anapokuwa na Shema. Mengine yote ilikuwa vurugu. Watoto aliokuja nao nchini alijikaza mpaka maji yakafika shingoni. Hawabadiliki na jeuri inazidi. Hawana shukurani na yeye hata kidogo. Walimdharau kama walivyoona mama yao akifanya. Wakaibua maswali mengi sana kwa Mill. Kadiri akiwalinganisha na Shema mtoto aliyekutana naye muda mfupi, ni kama usiku na mchana.

Kadiri alivyokuwa akiwaangalia na kuwatafakari, mahesabu yakaanza kutolipa. Kwa kuwa hapo hospitalini kwa kina Komba aliweka mashine za kisasa. Nzuri sana zilizokuwa zikimuingizia pesa nzuri, maana zilikuwa chache nchini kwa hiyo watu walitoka sehemu mbalimbali kufuata vipimo kwenye kitengo chake. Akawa na ofisi yake nzuri tu na wafanyakazi baadhi chini yake. Basi hapo akaweka kituo akifanya na mambo yake ya stocks mtandaoni. Kuuza na kununua hisa, kitega uchumi alichojifunza na kufanya kwa miaka mingi sana na ndiko alikojilundikizia pesa.

Alijua ni mida gani aingie sokoni auze na kununua hisa. Wakati gani hisa/stocks ziko vibaya, ashikilie asiuze, au kipindi gani anunue nyingi. Amefanya hivyo kwa miaka mingi tokea tu alipofika nchini Marekani mpaka akawa mtaalamu. Haishi sehemu bila kuwa hewani. Mtandao kwake ni masaa 24.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Colins akamtembelea upande zilizopo kazi zake hapohapo hospitalini. “Mbona kama haupo sawa?” “Kuna kitu nataka kufanya, lakini nahisi ni hofu tu. Nimejaribu kukipuuzia muda mrefu, naona kinazidi kunipigia kelele. Siwezi kulala, siwezi kufikiria.” Colins akakaa vizuri.

“Unataka kukizungumzia?” Akafikiria, akawa kama anasita. “Hivi ndivyo vipindi namkumbuka sana Mike. Ndio alikuwa kama jalala langu. Namtupia kila kitu. Huzuni zote na furaha zote alijua kuzibeba! Hakika wamenikatili aisee! Kumtoa Mike duniani!” “Pole sana  Mill. Lakini na mimi nipo.” “Sitaki kukuchosha na maisha yangu! Nahisi nimejivuruga sana.” “Unamzungumzia Pam?” “Nianze mimi mwenyewe.” Akajiweka sawa.

“Nisikilize tu nikwambie kitu.” Akamsimulia mkasa wa mara ya kwanza kulala na Kisha. “Yaani Colins, ilikuwa ni kama nilazima NILALE naye usiku ule na si vinginevyo. Na zikawa siku kamili zimetimia za mtu kujua kama alishika mimba, akanivaa akiwa na mama yake kuwa ameshika hiyo mimba. Kumbuka huyu mtu hatukuwa hata tukitumia chumba kimoja na haikuwahi kubadilika.”

“Miles akazaliwa siku zikiwa hazijatimia tokea nilale na mama yake na kushika hiyo mimba. Tena nakuja kupata taarifa za kujifungua kwake masaa machache baadaye.” “Haiwezekani!” “Kabisa. Na ukumbuke wanawake wa kule wanavyokuwa kwenye swala la kujifungua.” “Lazima uwepo.” “Ewahh! Sasa sikiliza juu ya Mia.”

“Hapakuwahi kuwa na amani aisee pale kwetu. Ila tukawa tukilea mtoto nyumba moja, vyumba tofauti tofauti. Akaanza kuwa mwema mpaka nikashangaa! Ubishi akaacha kabisa, hataki nikasirike. Akafanya kama majuma mawili mpaka kufikia siku ya Anniversary yetu. Akaomba tusafiri sisi tu na mtoto. Sasa kwa kuwa kulikuwa na amani, na bado sijapata uraia, tupo kwenye ndoa ya maigizo, namtegemea  yeye baada ya hiyo miaka miwili nirudi naye Uhamiaji anitetee kama bado mimi ni mumewe, ndio nipewe sasa Green Card ya miaka 10, alipo nibembeleza, nikajiambia sio wazo baya. Tutapata hata picha za ushahidi. Nikakubali, sikutaka kumtibua.”

“Tulipofika huko akawa mwema, mke kwelikweli. Na mimi si muhuni Colins. Sijui kuwa na wanawake hovyo na hapo ukumbuke bado moyoni nilikuwa na Pam. Ila nikalala naye tena kwa mara ya pili.” “Subiri kwanza Mill.”

“Kwamba sio kwamba mlikuwa mkifanya mapenzi mara kwa mara?” “Nakwambia ni mara ya kwanza aliponigomea kwenda kufunga hiyo ndoa na siku hiyo. Kwa sababu ilikuwa ni ndoa ya MKATABA kabisa. Namlipa kama mfanyakazi. Sasa siku inayofuata baada ya kulala naye kwa hiyo mara ya pili, yaani sasahivi ndio natulia, nafikiria na kugundua ni kama alinitafutia sababu kabisa.”

“Aliamka kama mbogo, tena hukohuko tulikokuwa mapumzikoni. Tulirudi nyumbani hatusemeshani kabisa. Na ndani ya majuma manne akasema tena ameshika mimba ya Mia. Hakika sikuamini. Ila sasa kukataa siwezi. Maana na safari hii alifanya kama mwanzo ila zaidi. Aliniambia taarifa za huo ujauzito wa Mia, akiwa na mama yake pamoja na anti zake. Niliwakuta wakisherehekea hapo tulipokuwa tukiishi, ndio wakaniambia wanasherehekea ameshika mimba.”

“Akaanza kliniki ambazo nyingi hanikaribishi.” “Mmmh!” “Umeona hapo? Wanawake wa kule kwenda kliniki ni lazima uwepo, usipokuwepo ni kosa la talaka kabisa.” “Najua!” “Basi yeye akawa ananiambia nisiache kazi kwa ajili hiyo. Mpaka wakati mwingine nilikuwa nikimlazimisha na mimi kuwepo kwenye hizo kliniki ambazo anafanyiwa ultrasound ili angalau na mimi nione mtoto. Napo ikawa kama kuna kukwepwa fulani hivi mpaka nikaona nimuache tu. Ila hapo katikati akaanza kusema kuna complication, daktari anamwambia hadhani kama mtoto atatimiza miezi tisa. Kufupisha habari, naye Mia akazaliwa kwa staili hiyohiyo kama kaka yake. Amepatwa uchungu, sikuambiwa, nimekuja ambiwa ashajifungua. Nikanyamaza kwa sababu nilijua hata hivyo haikuwa ndoa, tupo kimkataba.”

“Sasa kadiri ninavyomuangalia Shema na hawa, nazidi kuwa na wasiwasi Colins! Hawa watoto ni wangu kweli!?” “Mbona rahisi sana. Wapime!” “Naogopa jibu ambalo nishalihisi ndilo.” “Huna chakupoteza. Ukijua ukweli utapata uhuru wa kuchagua kama kuwatunza ukijua si wako, au kuwarudisha kwa wazazi wao.” Mill akatulia akifikiria mwishoe akaona liwalo na liwe.

Maamuzi Magumu.

Kujua Mbivu & Mbichi.

Akatoka muda huohuo kurudi kwake. Akachukua miswaki ya hao watoto na baadhi ya nywele walizoacha kwenye vyanuo vyao, na kurudi navyo hapo hospitalini. Wakasaidiana na Colins, wakamuachia mtu wa maabara  afanye vipimo. Maana hata damu hazikuwa zikifanana na hao watoto wawili, Mia na Miles. Ilikuwa ni vipimo vinatakavyochukua majuma matatu mpaka mwezi. Akabaki akisubiria kwa hamu ili ajue moja. Ila hakumshirikisha hata Pam juu ya wasiwasi wake juu ya hao watoto japo na yeye aliongeza wasiwasi pale aliposema ametapeliwaAkalinyamazia hilo. Ikabakia siri yake yeye na Colins akisubiria hayo majibu.

Siku Ya Zawadi, Yazua Janga kwa Pam

Siku hiyo ilianza kama kawaida tu. “Naomba usikose mama. Nataka uwepo wakati napewa zawadi, ndio nitafurahi.” “Acha nikaombe ruhusa kwanza. Nitaona. Ila nitajitahidi.” Mill akaja kumchukua mwanae, wakaondoka. Kama kawaida naye Pam akachukua daladala, akaelekea kazini. Jambo la kwanza akamuomba bosi wake ruhusa, akamkatalia. “Yaani uache kazi hapa sababu mwanao anaenda pewa zawadi! Ujinga gani huo? Kama hutaki kazi, basi.” Akakwama.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Huku kwa Mill yeye kumbe alilifanya jambo kuwa zito. Alishaalika familia ya Komba wote akisisitiza ni muhimu kwake kwa ajili ya Pam atambue jinsi wao walivyo wamuhimu kwake. Kwamba Dokta Komba aliacha shuguli zake muhimu, akaenda kuhudhuria. Colins na Kamila pia walitoka kazini wakaenda huko shuleni kwa watoto wa Mill. Mama Colins yeye ndio hata kazini hakwenda, na wote walimnunulia zawadi huyo Shema.

Muda wa saa nne na nusu, shuguli ikaanza. Wazazi wote na wageni wao pamoja na wanafunzi wakakusanyika ukumbini. Mkuu wa shule akaeleza dhumuni kubwa la kuwa hapo. Akaweka uzito haswa. Mpaka kila mtu akaona umuhimu wa kuwa pale.

Wakaanza kutaja madarasa ya juu mpaka darasa la nne la kina Shema. Wanafunzi wenyewe waliokuwa wakipewa zawadi ni wachache sana kulinganisha na idadi ya wanafunzi wote wa hiyo shule. Ila Mill akamuona mwanae amekuwa mwekundu, macho yapo mlangoni, kuingilia hapo ukumbini.

Mtu wa kwanza kutajwa kwenye hilo darasa la nne akawa yeye Shema Shelukindo Mgini. Baba yake akaona hasimami, macho yapo nje. Watu wakapiga makofi mpaka wakaacha, Shema hasimami. Akaitwa tena. Hakusimama. Alikuwa amekaa katikati ya Colins na baba yake, ndugu zake upande mwingine wa baba yao, wapo kwenye simu zao wanachezea game wala hawana habari na walipo na kinachoondelea.

Mill akamwangalia. “Pengine mama yako amekosa ruhusa. Nenda nitamchukulia video, ataona.” Akabaki ameinama. Jina lake likaitwa tena. Mill akasihi, akasimama na kwenda kupokea. Hajafika katikati ya ukumbi kurudi alipokuwa amekaa, akaitwa tena kwa soma jingine kwamba amefaulu kwa kiwango cha juu sana. Akarudi akapokea tena zawadi. Kabla hajafika tena katikati, akasikia tena jina lake. Watu wakaanza kushangilia sasa mpaka kusimama. Maana walikuwa wakieleza uzito wa somo, kiwango alichofika mpokea zawadi, ndipo anatajwa jina.

Mara Shema akaangua kilio. Watu wakashangaa. Ikabidi Mill aende kumchukua maana alibaki amesimama katikati ya ukumbi. Hataki kurudi kuchukua zawadi, hawezi kurudi tena kukaa. Analia kwa kwikwi kabisa. Mill akaenda kumkumbatia na kurudi naye pale mbele ya walimu.

Samahanini. Alitaka mama yake awepo, ila ametingwa kwenye kazi. Nakwenda kumpigia simu nijue alipofikia. Kama mnaweza, naomba zawadi zake ziwekwe mwisho. Wakakubali kuahirisha kwa muda. Ndipo akatoka na mwanae sasa kwenda kumtafuta Pam.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Namba ya Pam hana, mwanae analia kwelikweli. Ikabidi amtulize amuombe namba ya mama yake, akampigia. Colins naye akatoka na wengine wakafuata kwenye familia ya Komba. “Vipi?” “Hawezi kupokea zawadi bila mama yake.” Baada ya muda akapokea kukiwa na kelele kama yupo kwenye pikipiki.

“Tafadhali naomba niambie upo njiani, Pam. Shema ameshindwa kupokea zawadi bila wewe.” “Nilikataliwa ruhusa, hivi nimelazimishia. Nimechukua pikipiki nakuja.” “Naomba uzungumze naye, atulie.” “Nipe.” Mtoto alikuwa akilia huyo, akashindwa hata kuzungumza na mama yake, ila akamrudishia simu baba yake.

“Huyo hawezi kutulia mpaka anione. Na hapa naweza kuongea na unanisikia sababu nipo kwenye foleni tumesimama, ikiruhusiwa sitaweza. Ila nipo njiani nakuja.” Akakata. “Mama yako anakuja, Shema. Naomba turudi ndani.” Wakarudi akiwa analia taratibu.

Ikabidi watoe nusu saa ya vinywaji na vitu vidogo vya kujitafuna, wakisema itaendelea baada ya muda. Wanafunzi wengine wakiwepo kina Mill wakatoka nje ya ukumbi, wengine wakabaki ndani wakizungumza na wazazi wao hapo ndani wakiulizana kulikoni kwa huyo mwanafunzi bora! Wakabaki hapo nje kimya wakimsubiria Pam.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya kama dakika 10 hivi Mill akamuona Pam katikati ya watu akiwatafuta, kama aliyekuwa akikimbia. Nywele kama amemwagiwa mchanga! Chafu. Yeye mwenyewe kama aliyeanguka! Amefunika mkono. Mill akamuita akimfuata.

“Vipi, kwema? Mbona upo hivyo?” “Mimi nipo sawa. Yuko wapi?” “Mwanao amegoma kupokea zawadi zote. Na bado analia.” “Yuko wapi?” Mill akaongoza njia mpaka akamuona mwanae. Akamsogelea Shema. “Pole nimechelewa. Nionyeshe zawadi.” “Anazo baba.” “Nyamaza, usilie. Nimekuja tupokee hizo zawadi. Pole.” Akaendelea kumbembeleza mwanae taratibu asijue hata waliopo pembeni yao, maana watu walikuwa wengi. Yeye akili akaweka kwa mwanae tu, kumtuliza. Mill akamkabidhi mama yake hizo zawadi alizokuwa amepewa na kuondoka kumuwahi mkuu wa shule kumtaarifu kwamba mama Shema amefika.

Kwa Mara Nyingine Tena, Pam Akutana Na Kamila

Wakaitwa tena watu wote ndani. Watu kuangalia huyo mama aliyekuwa akisubiriwa! Ni mchafu huwezi sema alikuwa kwenye kazi ya maana! “Mbona kama una mamumivu mama?” Wakamsikia akimuuliza mama yake. “Nipo sawa. Usiwe na wasiwasi. Jua najivunia sana wewe baba mzazi. Nimefurahi mimi! Leo nitacheza mdumange mpaka kuchwe.” Mill na wengine wak awa wanawasikiliza wakiingia ndani. Wakamsikia Shema akicheka huyo, kama siye yeye aliyekuwa akilia.

“Unanichezea mimi mdumange?” “Nakwambia mpaka kuchwe. Na zawadi zote hizi!” “Nyingine bado mama! Ninazo nyingi.” “Basi twende. Tukusanye zote. Halafu..” “Unaweka kitandani kwanza, halafu ucheze sana?” Akamuuliza mama yake akicheka. Wakawa wanazungumza wao wawili wakiingia ndani.

“Mambo Pam?” Kamila akamsalimia. Pam akageuka na kukunja uso. “Umezungumza na mimi?!” Jinsi alivyomuuliza, kidogo ikasikika sio vizuri, akafanya wote wawaangalie. “Nimekusalimia.” Kamila akajibu na tabasamu. “Unanisalimia mimi?! LEO ndio unanijua?” Akafanya kabisa kusimama, wote wakasimama.

“Huna haja ya kuwa mnafiki Kamila. Mimi si kitu hata kwa huyo Mill kama UNAFANYA kwa ajili yake.” “Pam!” Mill akamtuliza, kina Komba wote wakasimama. “Nilikufuata kwako Kamila. Nikiwa na tumbo la Shema, NIMETOKA jela. Njaa inaniuma, nina kiu, UKAKATAA hata nisifunguliwe geti! Mlinzi wako akakwambia kabisa, ‘Mama, huyu mama ni mjamzito, amekaukiwa kabisa, labda umfungulie angalau umpe hata maji ya kunywa, anaweza kuanguka.’ Unakumbuka jibu lako?” Kimya.

“Kwa taarifa yako nilikuwa nikisikiliza mazungumzo yako na yule mlinzi wako, ulimjibu kwa kumfoka kabisa maana alikuomba kwa mara ya pili unifungulie, baada ya mara ya kwanza pia kumkatalia. Ukamwambia aniambie NIONDOKE, haupo.” Wote wakashangaa. “Nikamrudia tena yule mlinzi, nikamwambia shida yangu ni kumuulizia tu Mill. Nina wasiwasi, sijamsikia, akuulize kama unajua kama Mill yupo salama? Unakumbuka Kamila?” Jabza ikawa imeshampanda Pam, Kamila kimya.

“Kwa mara ingine tena, ulimfoka yule mlinzi. Ukamwambia NIONDOKE pale, aniambie hampo, wakati nikikusikia ndani! Ulishindwa hata kunipa maji ya kunywa, mlinzi wako akikusihi unisaidie, nimekaukia na nina mimba! Ukabaki gorofani kwenu pale, ukitoa amri nifukuzwe. Eti leo unaniulizaje?” Kimya.

“Acha unafiki Kamila. Na wala usijisumbue. Mimi ni Pam yuleyule uliyenifukuza kwako, sijabadilika. Sikuwa na maana siku ile, na LEO sina maana. Nimekuja hapa kwa ajili ya mwanangu, sitakubugudhi, na wewe usinibughudhi. Mungu wako atashugulika na wewe, wala si mimi. Twenda Shema mwanangu.”

“Kwamba Kamila wewe ulijua kama Pam ni mjamzito, ulishindwa kuniambia!?” “Sikutaka kuingia katikati yenu Mill!” Pam akaondoka na mwanae, akawaacha. “Kwamba hata usinigusie, halafu ukanipa nafasi ya kuchagua?! Kweli Kamila? Miaka yote hiyo tupo pamoja!” Kimya. “Mike alijua swala la ujauzito wa Pam?” “Sikumwambia.” Mill alishangaa, akashindwa kuelewa, ila akagundua watu wanazidi kuwapita kuingia ndani. “Nashauri haya mambo tuzungumze baadaye Mill. Tumalize hili la Shema kwanza.” Mzee Komba akashauri, wakaingia ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Shuguli ikaanza tena. Mkuu wa shule akaomba radhi na kueleza UMUHIMU wa kusubiri, ndipo wakaelewa. Walisema ni kwa mara ya kwanza kupata mwanafunzi kama Shema. Kutoka chini sana, na kuweka juhudi ya namna ile. Alieleza jinsi alivyofunga mwaka kwa kupata alama zote 100 mpaka kushangaza waalimu wote. Watu walipiga makofi mpaka kusimama kabisa.

Baba yake akamkumbatia na kumbusu kichwani, Pam asiamini! Walishangilia ukumbi mzima kasoro ndugu zake hao wawili. Miles na Mia, walibaki wameinamia simu zao kama hawapo hapo.

Ndipo sasa akaitwa kuanza kupokea zawadi. Ilibidi tu asimame palepale. Maana kila somo alipata 100. Utii na nidhamu kwa walimu, YEYE, Shema Shelukindo Mgini. Usafi. YEYE. Utulivu mpaka darasani, YEYE. Mtoto alipewa zawadi huyo, mpaka akalemewa. Akakimbia akiwa amebeba, anacheka, mpaka kwa mama yake. Akamkabidhi zote akicheka na kurudi tena mbele.

Akakabidhiwa vitu vyake na kupewa mkono. Ndipo sasa ikatangazwa zawadi KUBWA. Akapewa schoolarship, asilimia 100. Kwamba huyo Shema atasoma hapo bure kwa miaka yote mpaka amalize grade 7. Na wakatangaza kumrusha darasa moja maana walishampa mitihani ya kidato cha tano, akafaulu vizuri tu. Pam alishangaa! Kwamba mwanae akiwa na umri wa miaka 9, anakwenda 10 anakwenda darasa la sita! Alifurahi sana.

Akatoka hapo na kumkimbilia baba yake, akampa vyeti vyote. Maana kila zawadi aliyokuwa akipewa, alipewa na cheti/certificate yake. “Asante baba.” Hakika Mill alifurahi sana. Akaitwa aongee, akawa anacheka. Alivyo mzuri wakaanza kumpigia makofi, akaenda.

“Mimi nililelewa na bibi na mama yangu yule pale. Mama alipokuwa akienda kazini, ananiacha na bibi yangu, na bibi yangu hawezi kutembea, ni mlemavu, kwahiyo nikawa nashinda naye tu ndani, ananifundisha hesabu na kusoma. Halafu mama na yeye akawa ananifundisha kusoma pia. Nikaanza kusoma tokea mdogo sana.”

“Bibi alipoondoka, mama alipokuwa akienda kazini, akawa akiniacha kwa rafiki yake ana shule ya chekechea na mimi nikawa nasoma nao. Ila nikawa tayari najua kila kitu anachowafundisha wale watoto. Akamuomba mama anipeleke shule nikiwa mdogo. Walimu wakanipokea, nikaweza kuanza shule nikiwa na umri wa miaka minne tu nikaanza la kwanza.” Watu wakampigia makofi.

“Baba yangu alipokuja, akanihamishia kwenye hii shule. Mwanzoni nikawa naogopa. Lugha sijui. Lakini baba akawa ananifundisha vitu vile ambavyo sijui jinsi ya kuuliza kwa english hapa shule, wakanielewa. Nikawa kila nikisoma, naandika maswali yangu, nikipata tu muda na baba, namuuliza ananielewesha.”

“Baba yangu amenisadia SANA. Isingekuwa yeye najua nisingeweza hii shule. Kuna vitu nisingeweza elewa kwa haraka bila yeye. Kila siku za shule alfajiri ananifuata kwa mama, na ananirudisha yeye mwenyewe jioni. Bila kuchoka. Na njiani anazungumza na mimi, na kunielekeza mambo mengi. Yeye ndiye aliyenitoa hofu akiniamini nitaweza, huku akiniongoza taratibu, mpaka nimeweza kuweka mengi niliyokuwa nikiyajua kwa lugha ya kiswahili na kujifunza hapa kwa upya kwa lugha hii ya kingereza na kuelewa kwa haraka. Yote hayo ni baba yangu.”

“Na mama aliniambia inamgarimu SANA pesa na muda wake ambao kwake ni muhimu sana. Anaacha mambo yake muhimu, anakua akiniendesha yeye mwenyewe, wala sio dereva ili anisaidie njiani pia. Tangia naanza hii shule mpaka leo asubuhi, baba hajaacha kuniendesha kuhakikisha nawahi shuleni na narudi nyumbani salama. ASANTE baba.” Watu wakapiga sana makofi mpaka kusimama huku wakimwangalia Mill. Kwamba ni makofi yake.

“Halafu hapa nimekutana na walimu wazuri sana. Kila mwalimu yupo tayari kunisaidia ndio nikawa nawatumia. Halafu wakawa wananitia moyo, hata wanafunzi wengine walipokuwa wakinicheka siwezi lugha, wao wakawa wananitia moyo. Nawashukuru…” Akawataja walimu wake wote na kuondoka kurudi kwa mama yake. Watu wakapiga sana makofi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati mkuu wa shule anafunga kwa neno la mwisho, Shema akamwangalia mama yake. “Mama, mtandio umeloa damu!” Akajikuta anaongea kwa sauti ya wasiwasi. “Usiwe na wasiwasi.” Mill akawa anasikia. Ikabidi kuamwangalia. “Ni nini Pam!? Mbona mpaka jasho linakutoka jingi kama upo kwenye maumivu makali?” “Nipo sawa tu.” Akajifuta na mkono mwingine wazi akionekana na maumivu.

Shuguli ikaisha, watu wakawa wanatoka. Wale watoto wa Mill walikuwa kama hakuna kilichotokea kwa kaka yao au hawakujua walipo. Walipoambiwa wasimame walisimama na kuendelea na simu zao. Wakisimama, macho wanahamisha kwenye simu, kimya.

Walipotoka dereva wa wale watoto alikuwa ameshafika. Mill akawagutusha, wanae wakaondoka hapo na kupanda kwenye gari na kuondoka bila kumsemesha mtu wala kumpa hongera kaka yao au hata kumtambua kama yupo, ni kama hakuwepo pale.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Pam akajiangalizia, akaamua kumuaga Mill anayemfahamu na kumshukuru kwa yote. “Hakika Mungu akubariki Mill. Asante kwa yote unayomfanyia Shema. Nashukuru sana.” Kina Komba walikuwa pembeni, wakijingalizia yote. Mill katikati ya hiyo familia iliyochanganyika. Watoto wa wanawake wawili tofauti tofauti, na huyo Pam. “Usihesabu Pam! Shema ni mtoto wangu.” “Hata hivyo. Nakushukuru. Asante. Yote haya yamewezekana sababu yako. Muda na pesa. Shema hajakosea. Wewe ndio umemfanya afike hapa na kuweza yote haya. Nakushukuru.” Mill akajisikia vizuri. Angalau mwanamke huyu wa ndoa ya kimila, alijawa shukurani, si kama Kisha, mke wa ndoa ya mahamani, na wanae.

“Karibu Pam.” “Basi acha leo mimi nimrudishe Shema nyumbani, ili na wewe angalau leo ukafanye shuguli zako. Mchana mwema.” Bila kugeuka nyuma, akaanza kuondoka na mwanae wakitoka nje ya geti wakatafute usafiri. Kina Komba walishatoa pongezi zao, Pam akiwa pembeni tu anamsubiria mwanae, kimya. Walipomaliza ndio akaondoka naye.

Ila Mill alibaki akiwaangalia vile wanavyoondoka pale wao tu wakitembea kwa miguu, Pam yupo hovyo, mchafu, amejawa vumbi halafu kama yupo na maumivu, wakati wengine wote magari ya maana na ya kifahari yakiwasubiria! Akashindwa.

Akawakimbilia Pam na mwanae bila hata kusema kitu kwa hao wageni wake kina Komba. “Acha niwasogeze Pam.” “Usijali. Sisi tutakuwa sawa. Na wewe pata muda leo, ufanye mambo yako kwa utulivu.” “Upo na maumivu Pam. Ni nini? Na usiniambie si kitu, maana naona kabisa damu.” “Ni nini mama!?” “Wakati nakuja huku, tulipata ajali na pikipiki. Nitakuwa sawa. Usiwe na wasiwasi. Twende.” “Kwa nini unakataa nisiwapeleke?!” “Unayofanya kwa huyu, yanatosha, Mill! Achana na mimi. Baadaye.” Akamgeukia Shema. “Twende.” Wakataka kuondoka.

Mill akamuwahi tena. “Pam, kuna hospitali niliyompeleka na Shema, wale ulio waona pale ni wamiliki, na watu wangu wa karibu sana. Na nimewekeza baadhi ya mashine zangu pale. Ukienda pale, watakuangalia kwa haraka. Tafadhali usirudi na mtoto nyumbani ukiwa na maumivu, ukaugua mkiwa peke yenu. Mimi sina majukumu mazito ya kushindwa kutoa muda wangu sasahivi. Tafadhali twende.” “Mkono unauma! Unauma sana.” Akajikuta anajisalimisha. “Basi twende hospitalini.” Safari ya hospitalini kwa kina Komba ikaanza.

Pam na Ajali.

Kwa hakika Pam alikuwa ameumia haswa. Kumbe mkono ulipasuka, akafunga na shati la mwenye pikipiki na ndio kujifunika mtandio. Alizuia kuvuja kwa damu kwa kufunga hilo shati, hasemi, ameng’ata meno mpaka shuguli ilipoisha. Mbaya ilikuwa ni mkono wa kulia.

“Mill, ni mbaya aisee!” Colins akamfuata baada ya kutoka chumba alichokuwepo Pam akiangaliwa na daktari. “Naombeni mumsadie, asiondoke hivyo alivyo.” “Lakini unajua inabidi aingizwe chumba cha upasuaji kabisa? Amepasuka kuzunguka mkono mzima! Nyama za ndani kukaribia mfupa mkubwa zinaonekana kabisa! Na amepoteza damu nyingi.” “Mimi aina yangu ya damu ni O, kama atahitajika damu, nitampa yangu.” Ikabidi akimbizwe theater, chumba cha upasuaji.

Alishonwa na kurudishwa kwenye chumba cha kupumzikia. Alimkuta Mill na Shema wakimsubiria. “Vipi?” “Nashukuru, asante.” “Najua Pam! Ila nataka kujua unaendeleaje maumivu?” “Nahisi wamenipa dawa inayonifanya nisikie nafuu kubwa.” “Pumzika basi.” “Hapana Mill. Inatosha. Acha sisi tuondoke.” “Unaweza kupumzika hapa kwa leo, nitamchukua Shema.” Alishituka Pam kama anaombwa roho.

Hapana Mill! Nisaidie kuturudisha nyumbani, tutakuwa sawa tu.” Hapo anazungumza ana madawa ya usingizi kibao. Akapitiwa usingizi hata kabla hajajibiwa. Mill akabaki njia panda. Huyo mrudishwa nyumbani na mtoto, yupo hoi. Shema akabaki akimwangalia mama yake kwa wasiwasi.

Colins akaingia. “Vipi?” “Anasema maumivu yamepungua ila naona analemewa na usingizi.” “Nashauri umuache apumzike hapa kwa leo.” “Ndivyo ninavyotamani, lakini mwenyewe hataki. Anataka nimrudishe nyumbani.” “Atafanyaje na mtoto?! Huo mkono hataweza kuutumia kwa muda mrefu aisee! Vinginevyo atajikuta anajitonesha kila wakati. Ameshonwa karibu sana na kiwiko!” Mill akabaki akifikiria.

“Najua shida yake ni Shema.” Akawaza kwa sauti na kumgeukia Shema. “Kwa leo twende ukalale nyumbani uta…” Mtoto alishituka huyo mpaka Colins akashangaa. Akasimama pale alipokuwa amekaaa akaanza kusogelea kitanda cha mama yake.

“Shema! Na mimi nitakuwepo, nitakupa chumba chako.” “Watoto WAKO hawanipendi. Yule wa kiume, Miles, amewaambia darasani kwao mimi ni mwizi, nilikuja kwenu, nikaingia chumbani kwake nikamuibia. Rafiki zake wote hawaniiti Shema, wamenipa jina la mwizi. Wakiniona popote wananiita mwizi na kunicheka. Na yule mtoto wako wakike, mdogo, Mia, amewaambia rafiki zake nilikuja kwenu nikawa sijui kutumia vyoo vyenu, nikajinyea, rafiki zake wananiita pop face. Hata wakinikuta sehemu na rafiki zake wananiita pop face.”

“Wakati mwingine Miles na rafiki zake wananizomea bwaloni, siwezi kula naenda kukaa chooni. Sitaki kwenda kwenu, nabaki na mama.” Akaanza kulia. Nusura Mill kutokwa na machozi. Mpaka Colins alibadilika rangi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Mill Anafanyaje na aina hiyo ya watoto tofautitafauti.

Je, watoto wa Kisha ni Wake?

Usikose Kujua majibu ya DNA, na HATUA atakayochukua baada ya hapo.

Aidha wawe wake au la, atafanyaje kukuza watoto hao wa aina mbili TOFAUTI, pamoja?

Pam anamtaka, lakini Pam alishakataa kuwa mama Kenny. Na Pam hajui kinachoendelea kwa mwanae akiwa shuleni.

Je, Shema atamshirikisha mama yake juu ya mateso ya ndugu zake wanapokuwa shuleni? Pam atafanyaje?

Nini Kitaendelea kwa Love at first sight kwa Pam&Mill?

Inaendelea…..


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment