Juma zima
hakumsikia wala kumuona Mill. Siku ya jumamosi jioni Pam akapokea mgeni
anayemuulizia mama Shema. Alikuwa akipika chapati. “Unataka nini?” Akamuuliza
kwa jeuri akijua wazi ametumwa na Mill. “Nina mizigo yenu hapa.”
Akatulia akifikiria kama apokee au la! Wote kimya. Walimjua Pam alivyo jeuri.
Na hataki kuingiliwa. Wote kimya wakisubiria kujua uamuzi wake.
“Nani
amekutuma?” Akimjua mtumaji kabisa, ila akauliza. “Baba Shema na ameomba usome
barua yake.” Akanyamaza. “Niweke wapi?” Akauliza kwa makini kama aliyeonywa.
“Shema, mpokee uweke ndani.” “Bora shoga, nilijua ungekataa!” Ndio kila
mtu akaanza kuongea lake.
Akaweka mpaka
akamliza. “Amesema funguo za gari nikuachie hapa. Halafu uniambie
asubuhi nije niwafuate saa ngapi.” Alishituka Pam, hakutegemea. Akamgeukia
vizuri. “Amesema nini?!” “Ni usafiri kwa ajili yako na mtoto.” Pam akafikiria.
“Mrudishie gari yake. Mwambie sina shida.” Bwana walishangaa pale, mpaka
mletaji mwenyewe. “Haya, potea.” Akamuwekea msisitizo. Akaondoka.
Ujumbe Mzito
Kwa Pam.
Alipoingia ndani
akakuta amenunua vyakula vya humo ndani kibao! Akaoga wakati analala,
akafungua hiyo bahasha yenye barua. Akakuta kadi ya benki, imeandikwa jina la
mwanae. Akaanza kusoma.
‘Pam mke wangu!’ Hapo akafyonza kabisa. “Huyu ananitania huyu.” Akawaza moyoni akiwa
amejawa hasira. ‘Najua nimekuumiza na huwezi kuniamini kwa chochote. Lakini
Shema ni mtu wa mwisho kabisa nataka kumuumiza. Nimekosa sana, na
nakusudia nisirudie kosa mpenzi. Katika jitihada za kukuleta kule
nilipokuwa, nchini Marekani, ndio nikajikuta nimeangukia kwa Kisha.
Mimba zote alizoshika, ni kama alinitega tu. Ulichokiona huko Insta,
alikulenga WEWE moja kwa moja kwa sababu mwanzoni kabisa alinitongoza,
tukiwa chuoni, nilimkataa na kumwambia nina mke nyumbani, anaitwa Pam.’
‘Nilipokwama jinsi ya kukuleta kule, ikabidi
kumrudia yeye na kumuomba kama anaweza kunisaidia ndoa ya kumlipa
ili mimi nipate uraia wa Marekani kupitia yeye, kisha nikutafutie na
wewe Green card. Tuweze kuishi pamoja.’
‘Ikabidi kufunga ndoa yakueleweka na
picha nzuri kabisa ili kuaminisha
Uhamiaji kuwa ilikuwa ndoa ya kweli. Hakika nilifilisika Pam.
Alikuwa akinidai pesa mchana na usiku. Nilikuwa nikifanya kazi bila kupumzika.
Kila nilipokuwa nikitaka kukata tamaa, nilikuwa nakukumbuka wewe mpenzi.
Ilibidi nijitoe ili tuje kuwa pamoja.
Kwa hakika tulifanikiwa upande wa
harusi hiyo ya maigizo. Na Mungu ni shahidi, hata pale ulipotuona kwenye
harusi, nilikuwa nikimlipa Kisha.’
‘Najua unaweza usiniamini tena,
lakini Pam, nilifika sehemu nilikwama kabisa. Njia zote za kukuleta
kule tuwe pamoja zilifunga, akabakia Kisha TU. Na najua nilitakiwa kukwambia,
ila tokea mwanzo kwa kuwa ilikuwa ni biashara, nikaona nisikutie wasiwasi wa
wivu wa bure juu yake. Nikiamini baada ya muda, nitaachana naye,
sisi tuendelee na yetu.’
‘Ili kuaminika, kwa sababu hii
njia hata wao wamarekani wanajua wageni wengi hutumia kudanganya
ili kujipatia uraia, ilibidi niwe makini, sisi tuanzie mbali. Sio
kukurupuka tu kwenye ndoa na kugundulika kirahisi. Angalau kuonekane kulikuwa
na mahusiano kabla ya hiyo ndoa. Kukusanya USHAHIDI wa kutosha
ili wakija kutuita kwenye usahili tusionekane ni matapeli na kuingia
matatizoni.”
“Ilibidi kumuhamishia Kisha pale nilipokuwa
nikiishi ili tuonekane tuliishi pamoja, au kulikuwa na mahusiano ya
kweli kabla ya hiyo ndoa. Tupeleke ushahidi wa kutumia address
moja na bills zenye majina yetu sisi wote wawili hata tunapotokea kwenye
mahojiano baada ya ndoa, tuonekane tuna HISTORIA ya muda mrefu, ya
kweli, sio kudanganya. LAKINI Pam, hakika nilikoma, nitakuja
kukusimulia, siku utakapo nifungulia moyo wako tena.’
‘Turudi kwenye swala la Kisha. Tukafanikiwa
kwenye hatua ya kwanza. Mambo mengi yakaanza kuchukua picha yetu sisi
kama wapenzi. Majina yetu wote mawili yalifanikiwa kuingia kwenye systems za
nchini, tukionekana tunaishi pamoja kama wapenzi. Ndipo sasa
nikaanza taratibu za kufunga ndoa, ili sasa ijulikane kama ni mke wangu, ndio
niombe rasmi au nianze hatua ya kubadili uraia wangu.’
‘Nikiwa nimeshampanga Kisha, nimelipia
ukumbi na garama zote za harusi ambazo ni kubwa sana, halafu nilibeba peke
yangu. Ilibidi kumuomba Mike na Kamila na wao wahudhurie ili ionekane kama ni
ndoa ya kweli kabisa. Yaani ionekane mpaka nimeleta ndugu kutoka nyumbani kuhudhuria
harusi hiyo. Nilifanya taratibu za wazi kabisa, kuwaalika wao kwa kuwaandikia
kabisa barua ya mwaliko wa harusi yetu. Yote hayo ni ili kuaminisha
Uhamiaji kuwa si ndoa ya uongo.”
‘Pia nilishaalika jamaa
niliokuwa nikiwafahamu wa kutokea kulekule nchini Marekani, kuhudhuria hiyo
harusi, ilimradi tu kupata USHAHIDI wa kutosha wa picha kuwaridhisha wamarekani
waone ni ndoa ya kweli. Na ukumbuke hapo na yeye nilikuwa nimemlipa pesa nyingi
sana.’
‘Alinimaliza yule
mwanamke, sina jinsi nikakwambia ukaelewa. Madai ya kila siku yasiyoisha.
Nilifika sehemu sikuwa na pesa kabisa kwa ajili yake. Na akijua wewe upo
na tupo kwenye mahusiano si ya uchumba, nilimwambia wewe ni mke uliye na
baraka za marehemu baba yangu, maana alikuachia na wewe watoto wake.’ Hapo Pam akaanza kupoa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akakumbuka siku
za mwisho za uhai wa mzee Mgini, akiwa hospitalini alimwambia mzigo wa familia
yake anamuachia Mill ambaye ndio yeye. Akamsihi amsaidie Mill
kusogeza ndugu zake sehemu watakayoweza kujitegemea. Hasira na uchungu
vilimfanya asahau, akabakia kumtukania baba yake na ndugu zake. Akapoa
kabisa. Akarudi kusoma.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
‘Usiku wa kuamkia asubuhi ya kufunga
hiyo ndoa ya maigizo ambayo tayari ilishakuwa imenigharimu
kiasi cha kunifilisi, Kisha akanibadilikia. Nilirudi nyumbani jioni hiyo
tayari kwa ndoa ya kesho yake, maana sikuwa nikiishi hapo na yeye, japo ilikuwa
ni kwangu. Aliniambia hatakwenda huko kwenye kufunga ndoa mpaka nilale
naye. Yaani nifanye naye mapenzi. Na aliniambia nikikataa, hataendelea na mchakato mzima na
kunitisha kunishitaki kwenye vyombo vya usalama vya Marekani.
Kwamba nilimlipa pesa ili anisaidie makaratasi. Hilo ni kosa
kubwa sana kwa huku, Pam. Nisingebaki salama.’
‘Halafu ningerudije nyumbani, sina
kitu! Na baba hayupo! Na hapo tulikuwa tumeshaalika watu kuhudhuria harusi
hiyo kama nilivyokwambia awali. Mike na Kamila walikuwa wameshatua
nchini, wapo hotelini tayari kwa harusi siku inayofuata. Nyumbani kwa kina
Kisha nao walikuwa miongoni mwa hao wageni waalikwa, na wenyewe walishakuwa wakiitizamia
siku hiyo kwa hamu, wakijua binti yao anaolewa ndoa ya kweli. Kwamba
mabadiliko yeyote yale, ingebidi wajue ukweli na mimi kuangamia
vibaya zaidi, na bado wageni wengine waalikwa waliokuwa tayari kwa shuguli
nzima.”
“Sikuwa na jinsi mpenzi. Nilikuwa na
hali mbaya, nikajikuta nimekwama, nisingekuwa na maelezo ya kueleweka ya kwa
nini naahirisha harusi iliyokwisha nigarimu kwa kiasi hicho, halafu
pengine kuja kuishia tena jela nikiwa sijapata kitu! Akiwa ananiita mimi
ni mbinafsi, kwamba ananisaidia lakini mimi nakataa
kumsaidia, huko kulala naye, ilinibidi kulala naye tu.”
‘Kesho yake akafanya vizuri sana huko
mahakamani, ndoa ikafungwa, kisha kwenye sherehe hiyo ya harusi, mpaka kwenye
hiyo honeymoon ya maigizo ambayo hakuomba tena penzi. Huko
alitulia kabisa ila kutoa ushirikiano mzuri sana wa picha mpaka
nikafanikiwa kukusanya ushahidi mzuri sana.’
‘Nikiwa na hukumu ya kukusaliti, baada
tu ya hiyo fungate ya maigizo na kupata picha zangu, niliondoka
kabisa pale tulipokuwa tukiishi naye, nikaenda kujifungia kwenye sehemu
ninayofanya kazi. Kuishi kwa shida, nakula vyakula vya wagonjwa, nikimtunza
yeye kwa gharama kubwa sana.’
‘Sikurudi kwake mpaka baada ya mwezi.
Siku niliyozungumza na wewe kwa mara ya mwisho, nikakwambia ninarudi
nyumbani. Nimechoka sana. Lakini nikioga na kupumzika kidogo, nitataka
kusikia sauti yako. Lakini ndiyo siku iliyobadili maisha yangu mpaka leo.’
‘Nilifika nyumbani nikakuta Kisha akinisubiria
na mama yake. Ukumbuke hata kwao ilikuwa ni siri. Walijua ni ndoa ya kweli.
Aliyekuwa akijua ukweli ni Mike, Kamila pamoja na yeye mwenyewe Kisha.’
‘Kisha akiwa na mama yake, eti
akaniambia ni mjamzito. Siku ile tulipolala pamoja kwamba ameshika
mimba! Nilikuwa nahali mbaya Pam! Mungu anajua. Niliingiwa na hofu,
sikuwa na lugha ya kukwambia ukaelewa. Nikaamua kujificha na JANGA
langu.’
‘Ulichoona huko Istagram, sio
wewe pekee uliamini. Hata wale wamarekani tulifanikiwa vizuri
sana kuwaaminisha. Hatukupata shida kabisa siku tumeitwa kwenye usahili.
Kwanza ukumbuke tayari nilikuwa na ushahidi wa wazi kabisa wa ndoa yetu,
iliyopo mitandaoni na tayari Kisha alikuwa mjamzito.”
“Nilipewa Green card ya miaka
miwili. Kwamba baada ya miaka miwili, kama bado tupo PAMOJA na hatujaachana,
ndipo ningepewa ya miaka 10 ambapo sasa hapo, ndani ya muda huo ningeweza kubadili,
kutoka kwenye Green Card na kuweza kupata uraia. Na kwa NJIA ya ndoa, hiyo
niliyotumia mimi, ni rahisi sana. Nikimaanisha ni njia ya haraka endapo
ukifanikiwa kuitumia vizuri na kufanikiwa kuwaaminisha. Ilimradi tu, wasijue
kama mmedanganya.’
‘Sitakudanganya mpenzi. Kiuchumi
nilifanikiwa sana. SANA. Nilijijenga sana kule. Na huku nyumbani pia namshukuru
Mungu niliwekeza, na nikaweka vyanzo vya pesa vinavyonisaidia
mpaka sasa. Lakini Pam, Mungu aliniadhibu kuliko hivyo unavyoniadhibu
wewe. Nililipa kwa machozi.’
‘Nilijikuta nimekwama kwenye
ndoa ya vitisho kila siku. Hapakuwa na amani hata siku moja. Chochote
ulichokiona huko mtandaoni alikokuwa akipost Kisha ulikuwa umekusudiwa
wewe mpenzi, na Uhamiaji wa Marekani. Kwa upande wako,
alikufanyia makusudi ilimradi tu kuniumiza mimi na kuhakikisha sirudi
tena kwako. Na Uhamiaji ili kuendelea kurekebisha mpaka kupata uraia.’
‘Ili nisikuchoshe, ndoa ile Mungu unayemshangaa
namuombaje, ndiye aliyenisaidia mama. Ilibidi kumgeukia nikiwa nimekata
tamaa, nikimuomba anitoe. Nikiwa na hofu ya kurudia kosa la baba,
siwezi kimbia watoto wangu, nisijue kumbe huku yupo tayari
Shema, watu wakinishauri niondoke kwa yule mwanamke, lakini nilishindwa
kuondoka na kuachana naye tukiwa tayari na watoto wawili. Nilikwama
kabisa. Ndipo nikajisalimisha kwa Mungu.’
‘Nilikuwa nikifunga ila sijui niombe
nini. Maana nina watoto, na ndoa ya hila. Mungu mwenye rehema
akaishia kunitoa kwenye ile ndoa kupitia JELA alikokuwa amenishitaki
Kisha kwa kosa baya sana. Pengine nisingetoka mpaka leo.’ Pam akashituka sana.
‘Nilikaa huko rumande kwa muda mpaka
mwanasheria alipoweza msoma Kisha na kugundua shida ni zile mali, na hataki
hata watoto. Nilipo mkubalia kumpa mali zote na kuchukua watoto, ndipo akafuta
kesi, na mimi kutoka kifungoni, nikiwa nimepoteza kila kitu huko
nchini Marekani. Kasoro uwekezaji niliokuwa nikifanya kwa siri mtandaoni,
asijue. Nilimuachia mali yote ndipo nikafanikiwa kupata talaka
yangu, nakuondoka na watoto wangu.’
‘Ndivyo ilivyokuwa. Huna adhabu
utakayonipa ambayo Kisha hajanipa Pam. Alikuwa akinitusi mpaka
watoto wangu wanashindwa kuniheshimu kabisa.’ Pam akajisikia vibaya. ‘Hawa watoto hawawezi kuzungumza na mimi
kama hivyo Shema anavyozungumza na mimi, kwa jinsi wanavyonidharau kwa
aina ya maisha mabaya niliyokuwa nikiishi na Kisha, mama yao.’
‘Kwa hiyo kama ni adhabu mpenzi,
Mungu wako amekusaidia kukulipia. Nimelipa kwa machungu ambayo
hutawahi hata kufikiria kama niliweza pitia. Sijawahi kulala usingizi
ule tuliokuwa tukilala mimi na wewe kwa miaka yote 10, miezi
miwili na siku 5 mpaka sasa.’
‘Sitakuficha Pam, nina watoto wenye tabia
mbaya sana. SANA. Lakini Shema ni mwanangu. Nitamficha wapi?
Kilichotokea juzi, najua ni kosa langu lakushindwa kulea, lakini
niliwaacha kwa dakika chache nikiwa naandaa popcorn wale pale sebuleni
alipokuwa Mia na Shema. Miles alikuwa chumbani. Kumbe huku nyuma Mia alienda
kuchukua kitabu cha hesabu cha Miles, ili amuonyeshe Shema vitu
wanavyofundishwa huko shuleni.’
‘Mia alichukua bila kumuomba Miles,
akampa Shema. Sasa wakati Shema anasoma ndio Miles akamkuta, mimi nikiwa
jikoni. Mia ni muongeaji kama mama yake na mwepesi sana kudanganya.
Kwa haraka sana akadanganya kwamba yeye alimuona Shema ameingia chumbani
kwa Miles na kuchukua kitabu chake. Miles akampokonya na kumpiga na game
controller.’
‘Nakuapia kwa Mungu, Pam,
nilichomwambia Shema nikiwa sijui stori nzima, ila kuambiwa na Miles ameiba
kitabu chake, nilimwambia, ‘siku nyingine ni vizuri aombe’. Sasa wakati
nakwenda kuchukua sanduku la huduma ya kwanza nimsaidie kabla sijampeleka
hospitalini, huku nyuma ndio akaondoka.’
‘Nisamehe mpenzi kama kuna jinsi
nilitakiwa kufanya, nikakosea. Nampenda Shema, na sina sababu ya kurudi
kwako kama si kiapo tulichoapiana na wewe mpaka kifo. Nakutambua
wewe kama mke wangu, na HAITABADILIKA. Shema ni damu yangu, siwezi mnyanyasa.
Tafadhali nihurumie mpenzi. Na kama bado moyo wako haupo tayari
na mimi, naelewa kabisa. Ila naomba Shema asome kama tulivyokubaliana.’
‘Naomba tuendelee kama tulivyokubaliana.
Hiyo ni kadi, inayo pesa yote atakayohitajika shuleni. Ameshapata nafasi, tena
wamekubali kumpokea bila mtihani. Ila wamesema watampa muda. Wakiona anapata
shida, ndipo watazungumza na sisi jinsi ya kumsaidia ili aendelee
vizuri. Usafiri upo tayari. Kwa upande wangu nimekamilisha. Utakapokuwa
tayari kwenda benki, nenda na hiyo kadi na vitambulisho vyako,
watakuongeza wewe kama msimamizi. Wanazo taarifa zako zote kasoro vitambulisho.’
‘Nakupenda Pam! Nakupenda sana
mpenzi wangu. Sina sababu ya kurudi kwako kama si kukusudia kufanya bora
kuliko baba yangu. Na nikikutambua wewe kama mke wangu. Naamini
utanielewa, na kukubali kuweka tofauti zetu pembeni, ili tusimuathiri Shema.
Pale watamuendeleza kipaji chake cha mpira, atakua bora sana. Ni hilo tu mama.’ Pam akahema kwa nguvu. Zilikuwa barua zilizoandikwa kwa mkono. Mbele na
nyuma. Akabaki akifikiria na kupitiwa na usingizi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Lilipita juma
jingine tena, kimya. Pam akaanza sasa kuhaha rohoni. Mill hamuoni
wala yule kijana aliyetumwa hizo barua na vyakula. Akaanza kupooza
rohoni. Mtoto ameachiwa, alichokitaka kimekua. Mill hajarudisha
sura yake. Akapotea akiwa amehakikisha amejua kilichokuwa kikiendelea
huko ugaibuni. Pam ubinadamu ukamrudia.
Andy na familia yake kwa Kina Ruhinda tena.
Ilikuwa mida ya saa 10 jioni wakati taksii ikiwaingiza
Andy na familia yake, Msasani nyumbani kwa wazazi wake. Alishawapigia simu na
kuuliza kama wapo nyumbani. Baba yake akamwambia wote wapo. Hakusema kama
anakwenda na Mina. Walishafika hotelini, wakaacha mizigo yao yote ndipo
alipoambiwa wote wanamsubiri yeye, ndipo wakatoka. Walishushwa karibu na
mlango, Andy akawafungulia mlango, Mina na mwanae wakapita na kusimama pembeni
kama wanao msubiria yeye ndio aingie ndani kwanza.
Akapita Andy, wakashangaa Mina na mwanae nao wanaingia.
Pakazuka ukimya wa namna yake. Alikuwa Paulina na mume wake. Pius na wazazi
wao. Raza hakuwepo.
“Njoo ukae hapa Mina.” Andy akavunja ukimya.
“Shikamooni.” Mina akasalimia na kwenda kukaa na tumbo lake. “Marahaba Mina,
mama. Unaendeleaje?” “Naendelea vizuri kabisa.” “Uliacha kutapika?” Mzee
Ruhinda akaendeleza mazungumzo na Mina. “Kwa asilimia kubwa, baba. Sasa hivi ni
mara chache sana. Si ndio Andy?” Mina akamrushia swali Andy, akajisikia vizuri.
“Mpaka ale kitu ambacho hakipendi. Au kupikwe samaki.”
Kila mtu akajua wamerudi kuishi pamoja. “Basi ndio vitu vya kuepuka
hivyo. Mwenye hamu na samaki akamlie hotelini.” Akaongeza mzee Ruhinda, Mina
akacheka taratibu. Andy alipita na kwenda kumfungia Ayan chumbani na chupa ya
maziwa. Akamwashia tv na kumwambia asitoke mpaka aende akamchukue. Ayan
akakubali.
Andy akatoka. Akakaa pembeni ya Mina. “Nashukuru kwa kukubali
kufika hapa.” Andy akaanza. “Baba na mama, Pius ALIMLEVYA mke wangu, akambaka. Na ndiye aliyempa mimba.”
“Mina sio mke wako, Andy. Usisahau hilo.” Pius akadakia akiwa AMETULIA
kabisa. Watu wote wakawa wameduaa. Wakashangaa sana.
“Pius!” Mama yake akashituka na mshangao kama aanguke.
“Hapana mama. Anaongea hapa yeye kama nani? Kilichotokea ni kati yangu
mimi na Mina. Hayamuhusu.” “Lakini kipindi hicho alikuwa ni mke
wa mwenzio, Pius!” Mzee Ruhinda akaongeza kwa kuumia sana, asiamini kama Pius
kijana anayemuamini SANA, anaweza fanya hivyo.
“Na mimi nililewa baba. Nikajikuta nimefanya
hivyo. Nikashindwa kusema kwa haraka sababu ya mshituko. Na ndio maana
mimi sijamtelekeza Mina. Muulizeni. Andy alimfukuza, mimi
nikaenda kumchukua na kumpeleka hospitalini akatibiwa. Namtunza
Mina mpaka leo. Na nilikuwa natafuta wakati mwafaka wa kukiri kwake na kumuomba
msamaha, ndipo nije kwenu niwaambie nyinyi. Nilifanya kosa, na nikakubali kuwajibika.
Mimi sijamtupa Mina!” “Si nilikwambia Andy?” Mina akaongea kwa
kulalamika kinyonge na tumbo lake.
Andy akasimama na kumpiga ngumi kaka yake pale
alipokuwa amekaa. “Ulijua wazi Mina hanywi pombe, kwa nini ulienda
kununua champagne yenye kileo na kumnywesha mpenzi wangu kama hukukusudia
KUMBAKA?” Andy akamshindilia ngumi nyingine kaka yake. Pius akasimama, zikaanza
kupigwa. Ndugu hao, kaka wasomi na nyadhifa za juu
kwenye jamii, wakaanza kupigana hapo kama mabondia mbele ya wazazi wao,
kila mtu akishangaa.
Walipoona wanazidi kuharibu pale na kuumizana, ikabidi
Devi asimame na baba yake asimame wasaidiane kuwaamulia, maana walikuwa
wakirushiana ngumi za haswa. Walitenganishwa lakini wakarudiana tena. Mina
akasimama. “Sasa kama mnaendelea kupigana, mimi naenda kumchukua mtoto wangu, naondoka.
Nyinyi endeleeni kupigana mpaka muuane au kumuua mama na baba kwa
pressure.” Wakaachina.
“Subiri kwanza Mina.” “Naomba usiongee na mimi
Pius. Umenikosea sana. Umenitendea ubaya, ukaacha ninadhalilika!
Umesababisha nikaachika.” “Come on Mina!
Ndoa yenyewe kila mtu alijua ilishaisha.” Andy akamrushia ngumi, Pius
akaikwepa huku akicheka.
“Nakushangaa hasira za nini Andy! Mina si
mkeo na mapenzi yote yalishaisha kabisa tokea zamani sana, kila mtu
aliliona hilo. Ulimtelekeza hapa mjini, na hukuwa ukijali! Mimi
ndio nilikuwa nikimtunza yeye na mtoto wako wakati ulikuwa
hapahapa nchini!” “Sijawahi kuacha kumpenda Mina. Na wewe ulitumia udhaifu wangu kuzaa na mke wangu. Hukuwa umelewa Pius.
Ulifanya makusudi. Sababu ya tamaa zako kwa Mina. Ulishindwaje
kujizuia Pius!?” Andy akauliza kwa kuumia lakini Pius hakumjibu. Akamgeukia
Mina.
“Mina, nilikusudia kabla mtoto hajazaliwa
tulizungumzie hilo ila ukaniblock kila
mahali, nikashindwa kukupata kwa simu. Nilikufuata mpaka Iringa
kujaribu kufuatilia sehemu ulizokuwa ukiniambia ulipata sehemu ya kuishi pia sikufanikiwa.
Hangaika yote hiyo ni kukiri kosa na kuomba msamaha.” “Sio kwangu kwanza Pius. Anza
kwa Andy, akikusamehe Andy...” “Mina!? Huyu Andy si alikutelekeza
wewe aka..” “Kilichokuwa kikiendelea kati yangu na Andy, hakikuwa kikikuhusu
Pius. Acha kuhalalisha kosa lako kwa kumdhalilisha hapa Andy.
Unazidi kuharibu.” Pakawa kama watu wamepigwa na butwaa tena.
“Kaa chini Pius, maana naona wewe unataka kuharibu na usiwahi
hata kuwa na mahusiano na huyu mtoto.” “No way Mina! Mimi namtunza mtoto wangu na wewe kwa ukaribu sana. Nimekutunza
Mina, hata kabla hujabeba mtoto wangu.” “Mimi mpaka nakuhisi
vibaya Pius! Nahisi ule msaada wako ilikuwa ni njia ya kunivutia.
Ulipoona sijaelekea kwenye mapenzi bado nakuheshimu kama shemeji ndipo ukanibaka.”
“Ninachotaka usije kuwahi kusahau Mina, ni kuwa, mimi nakupenda sana na ninakujali.” Andy akaruka kutaka kumfikia kaka yake, Pius naye
akakimbia upande wa pili.
“Pius, umechanganyikiwa wewe!?” Paulina
akashangaa sana. “Wala sijachanganyikiwa. Mlitaka nidanganye ndipo
mjisikie vizuri? Naongea ukweli wangu. Nampenda sana Mina.” “Baba,
unamsikia lakini Pius!?” Andy akamsemelea kana kwamba mzee Ruhinda hakusikia.
“Umepatwa na nini Pius!?” Baba yake akamuuliza kwa kumshangaa sana.
“Juu ya kumpenda
Mina au kumpa mimba?” Akauliza Pius bila wasiwasi, wote wakabaki
wameshangaa. “Mbona lakini mnashangaa kama nimefanya jambo la ajabu sana!? Sasa
hivi Mina si mke wa Andy, kilicho cha ajabu ni kipi? Wote mnanijua mimi
sio muhuni. Miaka yote nimekuwa na Raza tu, hamshangai kwa nini iwe kwa
Mina? Ni kwa kuwa nampenda.” Pius akaongea bila wasiwasi.
“Ujue Pius una wazimu wewe!?” Paulina akamshangaa kaka
yake. “Wazimu ni mimi nimependa au wewe unayepita kwenye majumba ya watu
na kuharibu? Aliyesaidia kuvunja ndoa ya Andy na Mina ni nani
kama sio wewe? Unaingilia mambo ya watu hata huyajui, lakini unataka
wewe ndio uwe kimbelembele!” Pius akaendelea kwa ukali kabisa.
“Mina alikuja siku ile akawa muwazi kabisa.
Hana hata taarifa kama ni mjamzito! Mtu mwenye akili timamu si angetulia,
na kumsaidia? Umempiga na kumvunjia ndoa yake. Sasa hivi
ndio unaniita mimi wazimu! Mnafiki
mkubwa wewe Paulina. Mbaya kuliko shetani. Umejua Andy hana
uwezo wa kuwa mume, ndipo hapo na wewe ukaweza kuingia na kuharibu.”
“Sikuvunja ndoa ya Andy mimi.” Paulina akaruka.
“Paulina wewe!” Andy akashangaa sana. “Mimi nilikushauri
chakufanya, sikukulazimisha umuache mkeo, Andy! Yalikushinda wewe
mwenyewe, tokea mwanzo.” Pius akaanza kucheka. “Mmeona sasa? Mnarudi kulekule
mliko nishangaa mimi. Mimi mkweli na sikutaka kuzunguka. Wewe
Andy ndoa ilishakushinda muda tu, sababu ya kushindwa kubalance mambo. Ukalemea
upande mmoja kama ambaye hukuwa na mke wala watoto! Paulina alikusaidia tu kuhitimisha
kihalali. Lakini ubaya wa Paulina, kila mtu anaujua. Muulize mama yake
huyo hapo.” “Msiniingize kwenye mambo yenu.” Mama Ruhinda akakataa
kabisa, tena kwa haraka bado akionekana na mshituko.
“Unakataa tu mama. Lakini wote tunamjua Paulina ni mbeya
na mchonganishi. Alianza kwenye ndoa yangu mimi. Akawa anamsema Raza
vibaya, nikamkanya na vibao vya usoni. Akaja kunisemea hapa kwa baba
akiwa analia. Na wewe ulikuwepo. Najua mnakumbuka. Akavumilia akashindwa,
akahamia kwa Raza kunishitakia mimi. Raza alipoona unataka kumtoa kwenye
pesa zangu, maana mimi nilimwambia Raza, akiendelea kukusikiliza wewe
Paulina, anaondoka pale kwangu bila kitu. Raza akaanza kukukwepa.
Ndipo ukajirudi. Bisha kama ni uongo?” “Uongo.” Pius akamkazia macho.
“Sasa kwa kuwa najua huwezi kunyamaza, hata hili
utamwambia Raza. Nakutuma nenda kamwambie kama ilivyo. Ila ONGEZA hivi,
chochote kitakachompata Mina na mtoto wangu, ajue ndicho kitakachoipata
ndoa yake. Aombe na akaloge kwa waganga zake, wote hawa,
Mina na mwanangu waishi ili na yeye ndoa yake iishi.” Pius
aliongea bila wasiwasi na kushangaza kila mtu mpaka hata Mina mwenyewe kwamba haogopi hata kwa mkewe!
Akamsogelea Mina. “Nataka mahusiano yangu na
wewe yasiharibike, Mina. Na nipo tayari kumlea mtoto wangu. Na
ninataka anitambue mimi kama baba yake. Niambie unataka nifanye nini.”
“Cha kwanza Pius na Andy kama mnataka kuzungumza kaeni chini wote mtulie. Kama hamtaki
mimi naondoka zangu na wanangu. Mnakuwa kama watoto bwana!” Wote wakakaa.
“Weka msisitizo kwa Andy. Yeye ndio anataka fujo.”
Pius aliongea huku akicheka tu. “Tafadhali acha dhihaka kwa mwenzio Pius!”
“Kwani mimi nimefanya nini baba!?” “Mbona halipo lakuchekesha hapa?!” Mzee Ruhinda akauliza kwa ukali, Pius
akanyamaza. “Hiyo ni dharau ya hali ya juu Pius! Umenifedhehesha
sana mimi kama baba yako na mtu niliyekuamini na Mina.” “Naomba baba
usijilaumu. Haya ni makosa yangu mimi mwenyewe.” “Nitaacha vipi kujilaumu wakati na mimi
nilihusika kuwa nikikutuma kwenda kumsaidia Mina!” “Haya ni makosa
yangu baba. Ni mimi.” Hapo Pius akatulia, kidogo akaonekana anazingatia.
Pakatulia kila mtu akiwaza lake kama walio kwenye mshituko mkali
sana.
“Naomba tumsikilize na Mina. Karibu mama.” Mzee
Ruhinda akavunja ukimya. “Asante baba. Mimi nilitaka kumwambia Pius, ajue sijamshitaki
polisi ni kwa sababu ya wema wake kwangu. Japo hata huo wema naanza kuutilia
mashaka, lakini...” “Naomba kosa moja lisikufanye...” “Tafadhali nyamaza
Pius. Kwa hakika umeharibu na kuniumiza sana.” “Sawa baba.” Pius
akanyamaza.
“Endelea mama.” Mzee Ruhinda akataka Mina aendelee. “Andy ameniacha sababu yake! Hata kama
kulikuwa na mapungufu kwa Andy, lakini bado alikuwa mume wangu na
nilikuwa nampenda Andy wangu. Alishakiri makosa yake na kuamua tuanze
upya.” Mina akajifuta machozi.
“Na niwaambie kweli tu, mwezi mmoja
kabla ya kurudi kwa Andy, alishakuwa tayari kuacha kila kitu, ili aje awe na
mimi na Ayan. Alishakubali kurudi atafute kazi ingine ili awe na mimi. Ndio
nikamtia moyo, nikamwambia nimesamehe yote, tukakubaliana tuanze upya.
Lakini Pius umenipokonya ndoa, wakati wewe bado upo kwenye ndoa yako!” Mina akaendelea taratibu tu akilia.
“Amemfedhehesha Andy vibaya sana.
Kila mtu aliyejua mimi nimeshika mimba nje ya ndoa atakuwa amemuona Andy ni hovyo.
Ameoa mke wa ajabu!” “Unakwenda mbali
Mina.” “Sio mbali Pius. Hata hapa pia, umemsema
vibaya Andy wakati ni baba wa mtoto wangu. Sitakusamehe kwa hilo. Ukitaka amani
na mimi na uwe na mahusiano na huyu mtoto, muombe msamaha Andy, tena
wakumaanisha.” Pakazuka ukimya, Pius akainama.
“Cha pili Pius, umesababisha nilifukuzwa
nyumbani. Mama anajua mimi ni mtoto mbaya, nimemsaliti Andy, akanifukuza.
Sina mawasiliano na mama pamoja na Ron. Sasa, Andy akishakusamehe,
mkaweka mambo sawa na Andy, nataka uende na kwa mama na Ron. Uwaeleze ukweli usafishe
jina langu kwa mama. Wengine sijali. Ila mama yangu, Ron na Andy. Ukishapatana
na hao, ndipo unitafute sasa tuzungumze maswala ya mtoto. Mimi nimemaliza.” Pakazuka ukimya lakini Mina alimfurahisha sana Andy,
hapakuwa na mfano. Alimrejeshea heshima aliyokuwa amepoteza hapo kwao.
“Umesikia Pius?” “Nafikiria baba.” Pius akajibu. “Basi
twende zetu Andy. Ukimaliza kufikiria utamtafuta Andy.” Mina akasimama. “Subiri
kwanza Mina.” Mina akamwangalia. “Nitajuaje kama nikienda hawatanifunga?”
“Hutajua mpaka utakapofika pale. Mimi sina hayo
majibu Pius.” Pius akabaki akimwangalia.
“Huna haraka. Na sikulazimishi kwa lolote. Siku
utakayokuwa tayari kufanya hayo, fanya. Ukiona ni ujinga, pia ni sawa.
Endelea kunyamaza kama ulivyofanya mpaka tukakufuata hapa na kutukejeli
mimi na Andy.” “Sijakukejeli Mina!”
“Usinifanye mimi mtoto mdogo Pius.
Huwezi kumcheka Andy mbele yangu, tena kwa kitendo cha kinyama ulichonifanyia
mimi nikiwa mkewe, halafu utegemee mimi niwe sawa! Kivipi? Kwa lipi
lakunifanya umcheke Andy, halafu kuwe sawa! Wewe ni mbaya na unadharau mbaya sana.
Labda ni kwa vile ulivyoyajua mahusiano yetu kwa undani kati yangu mimi na
Andy, ndio ukaona sisi ni watu wakutudharau tu. Au labda ni mimi ndiye unanidharau.”
“Sikudharau Mina!” Pius akajitetea tena
kwa kumbembeleza Mina. Akionyesha wazi hataki kukosana hata
kidogo na Mina, lakini si mtu mwingine.
“Ni dharau na uonevu wa hali ya juu Pius. Mwenzio Andy
kabla yakunigusa, alikwenda
nyumbani. Akazungumza na mama pamoja na Ron. Akafanya taratibu zote, ndipo
akanioa. Andy aliniheshimu, hakunigusa mpaka ndoa. Pius wewe umenidharau
mimi na mama yangu. Sasa sijui kwa kuwa umetuona hatuna hali kama zenu! Sijui!”
“Usiseme hivyo Mina! Nilikosea.” Mina akakunja uso wa mshangao.
“Tuwe wawazi tu. Hivi mimi ningekuwa ni kama
Paulina huyu dada yako. Mzee Ruhinda na mama Ruhinda ni wazazi
wangu, mimi. Nikalelewa kwa hali kama hii ya Paulina. Nina wazazi
wote wenye uwezo na wanafahamika kwa nyadhifa za juu hapa nchini, kama
kina Ruhinda. Ungenifanyia ulichonifanyia kweli Pius?” Kimya. Kila mtu
akabaki kimya.
“Twende Andy.” Andy akasimama na kwenda kumchukua
mtoto wake. “Lakini katika yote Mina, naomba uamini nakupenda. Najua lilifanyika kosa tokea mwanzo sababu ya pombe na
kwa kuwa nakupenda SANA. Lakini sio dharau kwako wala kwa mama
yako. Na mimi si muhuni. Kila mtu ni shahidi yangu. Wananijua.” “Pius wewe
mwanangu umerukwa na akili!” “Nampenda Mina, mama. Si heri nimwambie
tu ukweli, ajue.” Kila mtu akabaki amemkodolea macho Pius kama wameona muujiza
wa fimbo
kugeuka nyoka.
Mina akatoka bila hata kujibu. Andy akarudi na mtoto
wake, akakuta Mina alishaondoka pale. Wakaondoka. Lakini Andy alijisikia vizuri
sana kwa heshima aliyopewa na Mina. Ni kama alimtetea na kutaka Pius asimpuuze
hata kidogo.
~~~~~~~~~~~~~~
Mahusino yapi yatapona, yepi yataharibika?
Na mahusiano hayo yatakuje
na watoto wa wanaume wawili, tena NDUGU waliokwisha umizana? Halafu
wote WANAMPENDA mwanamke mmoja?
Pius anamtaka mwanae na Mina.
Andy anamtaka mkewe.
0 Comments:
Post a Comment