Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 35. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 35.

Lakini kwa hakika akajua ameharibu vibaya sana hata kwa Mina. Mina anamsifia Pius kama Paul mdogo wake! Akajifananisha na Pius kaka yake, akajiona amempita mbali sana. Yeye mtoto mmoja tu alimshindwa akawa wakuhama nyumba moja hadi nyingine! Akawa amemtelekeza kama yeye alivyotelekezwa na wazazi wake Nairobi! Akajichukia Andy, na kujilaumu sana.

Kwa Mina.

Akatoka hapo na kwenda chumbani kwa Mina. Akamkuta amelala. “Mina!” Mina akaamka. “Vipi?” “Nakuomba ufikirie na ukumbuke.” “Juu ya nini!?” Mina akakaa kwa shida kidogo. “Uliniambia hukuwahi kwenda nyumbani kwa rafiki zako wala kuwakaribisha pale nyumbani hata siku moja. Una uhakika? Naomba ufikirie kwanza kabla hujajibu.” “Katika hilo sihitaji kukumbuka Andy. Nina uhakika.”

“Okay. Je, kukutana nao sehemu wakakupa kinywaji chochote, hata maji?” Mina akafikiria. “Labda kula nao palepale chuoni. Na tunakuwa wengi Andy! Sio kwamba nakuwa peke yangu. Kikundi.” “Kwa hiyo hukuwa karibu na kijana yeyote yule?” Mina akafikiria.

“Kama wawili hivi, lakini tulikuwa nao palepale chuoni hata kukutana nao kwenye kundi la kujisomea nilikuja kushindwa hata kabla wewe hujaondoka nchini. Nilikuwa nikikosa muda Andy! Mara nyingi walikuwa wao wanakutana siku za weekend na usiku mara mbili kwa juma.” “Na hukuwahi kufika huko?” “Hapana. Nilitaka, lakini nilishindwa.” Mina akajibu kwa uhakika.

“Kwa hiyo unao uhakika hapakuwahi kuwa na mazingira mkawa nao hao rafiki wawili?” “Nina uhakika Andy.” Andy akatulia kidogo.

“Kwani vipi?” “Wewe sio mlevi Mina. Hunywi kabisa. Haiitaji mtu kutumia nguvu nyingi kukulevya na kukufanyia mambo mabaya na akakuacha ukiwa umelewa. Na hata pombe ikikuishia usikumbuke.” Mina akaanza kufikiria. “Sijawahi..” Gafla akamuona amesita. Halafu kama aliyeshituka SANA, kisha akajibaraguza.

“Sijawahi kudhania hivyo.” Andy akajua amebadilisha alichotaka kusema. “Sasa hivi, hapo, umenidanganya.” “Bee!” Mina akajidai kama hajaelewa.

“Mina?” “Juu ya nini?” “Hicho ulichokumbuka na kutaka kunificha sasa hivi. Nani aliwahi kukupa pombe hata kwa kuonja?” “Mimi?” Mina akauliza na kusimama. “Nakwenda chooni.” Akaelekea chooni. Andy akamuona kama ameingiwa na hofu kubwa. Mina akawa kama amefunguliwa macho kwa haraka sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati analala alimuomba Mungu amfunulie ajue ni kwa jinsi gani ameshika hiyo mimba. Andy amemsaidia kumvuta kumbukumbu. Akakumbuka ni Pius pekee ndiye kwa mara ya kwanza alikunywa akiwa naye na kulewa sana. Kesho yake hakukumbuka na hakumwambia kilichotokea.

Mina akaanza kulia sana huku amefunga mdomo ametoa macho asijue alikuwa akila na kunywa na baba mtoto wake! Akakumbuka jinsi Pius alivyokuwa akimfuatilia kwa karibu hata kutaka kujua jinsia ya mtoto! Mahela aliyokuwa akimtumia! Upendo wa kumjali na kutaka kujua mtoto anaendeleaje kila wakati! Mina akaumia sana. Anamwambia nini Andy? KIPI na KUACHA kipi? Ameshalala na Pius! Akaona heri asimtaje. Akaosha uso, akatoka akiwa ametulia asijue hata macho yanaonekana.

Mambo Hadharani.

Alimkuta Andy ametulia kimya ameinama. Akanyanyua uso alipomsogelea. “Ni lini na wapi ulipokunywa pombe na Pius?” Mina alishituka akakaribia kukaa chini. Kimya. “Mlikuwa na mahusiano naye?” “Ya kama shemeji mpaka uliponifukuza kwako, na mama naye akanifukuza ndipo nikaenda hotelini, akanipigia kunijulia hali. Akanikuta natapika sana, ndipo akanipeleka hospitalini. Akakaa na mimi mpaka dripu niliyowekewa ikaisha, akanirudisha hotelini. Akanihudumia, nikapata nafuu ndipo nikamuaga kuwa lazima nikaanze maisha yakujitegemea kwa ajili yangu na mtoto.” Mina akaenda kukaa pembeni ya Andy pale pale kitandani.

“Tuliagana lakini akiwa ameniambia muda na wakati wowote hata nikitaka mtu wa kuzungumza naye nimpigie. Au ushauri. Nikitaka kitu, nimuombe yeye. Hapo alishakuwa na akaunti yangu ya benki.” “Aliipata wakati gani?” “Wakati bado mimi ni mke wako. Alisema atakuwa akiniwekea hapo pesa za matumizi yangu na Ayan ikitokea kama wewe umetingwa, hujatutumia pesa.”

“Maana kuna siku alinipigia simu kutaka kunijulia hali, wewe ukiwa huku. Akaniuliza mbona nimekuwa kimya. Nikamwambia sina pesa ya simu kwa wakati huo, nakusubiria wewe, unitumie pesa za matumizi ya week, niliishiwa mapema, nilinunua vitu vya mtoto ambavyo havikuwa kwenye bajeti ya pesa uliyokuwa umenitumia. Halafu kuna wakati mwingine alitaka anisaidie kukaa na mtoto, nikafanye shopping ya nyumbani. Nikamwambia asije kesho yake maana bado hujatuma pesa, sina hela. Ndipo akaniomba namba ya akaunti kuwa na yeye atakuwa akiweka pesa humo ili nisiwe napata shida.” 

“Kwa hiyo akawa akikuwekea pesa hata kipindi tupo wote?!” “Kwa kweli katika hilo sitadanganya Andy. Pius alikuwa hataki anisikie napata shida wakati wowote ule. Alijitoa kwangu kwa namna ya ajabu sana. Na alikuwa akiweka pesa nzuri sana. Mambo mengi ya pale nyumbani kwa mama niliyafanya kwa pesa aliyokuwa akiniwekea Pius. Sikuwahi kuishiwa wala kukopa tena, kuanzia wakati ule mpaka uliponifukuza kwako. Kwa asilimia 100, nilikuwa nikitunzwa na Pius hata kule uliponikuta nikiishi, Iringa.” Andy akainama. Akatulia. Mina naye akatulia.

“Na ni lini alikupa pombe?” Andy akauliza akionyesha wazi kuishiwa nguvu. Macho yalishakuwa mekundu haswa. “Unakumbuka tulikuwa hatuwasiliani kabisa wakati ulipoenda Uswiz?” Andy akabaki kimya akimtizama. “Kipindi kile Pius ndio akawa karibu sana na sisi. Zaidi. Akinisaidia mambo yote ya pale nyumbani na mtoto. Sasa nilipopata matokeo yangu kuwa nimefaulu, mtu wa kwanza kumfikiria ilikuwa wewe. Nikijiambia wewe ndio ulikuwa mtu sahihi wakufurahia mafanikio yangu. Ndio maana nikakupigia kukwambia.” Mina akaendelea.

“Nilipomaliza kuzungumza na wewe, bila maelewano sikukwambia hata kama nilitegua mguu. Hata hivyo nilijua usingejali, Andy. Maana hata ulipokuwa upo huku Tanzania nilikuwa nikiumwa huna hata habari! Hujali. Anyway, nikawa nimekaa tu kwenye kochi, mguu unauma, siwezi hata kutembea. Ikabidi kumwambia yeye kuwa nina maumivu ya mguu, siwezi hata kukanyaga. Hapo hapo akaja na kunipeleka hospitalini. Nikawa nimemwambia pia kuwa nimefaulu akasema lazima tusherehekee.” Mina akatulia kidogo.

“Hospitalini wakanifanyia vipimo, mguu ukawa haujavunjika. Ni kuteguka tu. Ukawa pia umeshajaa, umevimba na unauma sana. Wakaniandikia dawa kali za maumivu pia. Pius akanichukua tena mimi na Ayan, tukaenda kununua dawa na chakula. Akasema lazima tusherehekee. Akanunua na champagne na wine.” Mina akajifuta machozi, tayari Andy akawa yupo kwenye mahesabu makali.

Muda huo mpaka Mina kugundulika mjamzito. “Tulifika nyumbani. Akanisaidia kumuogesha Ayan baada ya kumlisha, akamuweka kitandani wakati na mimi nilishakula na kuoga, nikajilaza kitandani. Alipomalizana na mtoto akagonga kule chumbani, akaniambia nisilale lazima tusherehekee. Nikamwambia nilidhani itakuwa wakati mwingine kwa kuwa amechoka. Kunipeleka hospitalini, kukaa na mimi mpaka matibabu, kununua dawa, kuturudisha nyumbani na kuanza kumuhudumia Ayan, nikajua atakuwa amechoka.” Mina akajifuta tena machozi kama ambaye na yeye alishamjua moja kwa moja.

“Basi, akaniambia hiyo siku ndio ya habari njema, lazima tusherehekee. Champagne ikawa kali. Akasema nisiogope. Ninywe tu. Nakumbuka akaniambia tugonge, halafu ninywe yote bila kufikiria ule uchungu. Nikafanya hivyo. Nikaona nimeweza, halafu sio chungu kama nilivyodhania. Akaniambia sasa tunywe ile wine. Ni tamu. Na kweli ilikuwa tamu kama juisi. Kumbukumbu nafikiri zinaniishia kwenye glasi ya tatu. Vile alivyokuwa akiniambia ninywe kama maji, nisisikilizie.”

“Kesho yake nakumbuka niliamka kichwa kizito sana. Lakini msafi vile vile kama nilivyotoka bafuni jana yake na mguu ule ulioteguka ukawa upo vizuri tu, juu ya mto. Akaja asubuhi na mapema. Nikamuuliza jana kulitokea nini, mbona sikumbuki chochote, akacheka. Nikahisi niliharibu kwa kuwa sikuwahi kunywa pombe, ile ilikuwa mara yangu ya kwanza. Nikaingiwa hofu, nikajiambia labda nililewa sana, nikajisahau. Akaniambia nisiwe na wasiwasi, uzuri nilikuwa na yeye. Hakunipa maelezo marefu na mimi nikawa nimeingiwa hofu ya pengine nilitamka jambo baya au nilimsimulia mambo mabaya au hata kufanya jambo baya! Nikaona iishe hivyo tu, nimuulize zaidi.” Mina akajifuta tena machozi.

“Ndio akawa amempigia simu mama kumwambia nimeumia mguu, nahitaji msaada. Ndio mama akaniletea Mamu. Lakini sasa kuanzia hapo wote wakawa kama wamepeana zamu kuja pale kuniangalia hakuwa tena peke yake. Wakati mwingine akija akawa anamkuta baba na wengineo. Na wewe ukawa kama umetengeneza. Unajali. Ukarudisha simu za mara kwa mara, tena ukitaka kuniona! Ikawa sasa nakosa muda wakumtafuta tena.”

“Hata alikuwa akinipigia nakuwa labda nipo na wewe kwenye simu. Ndipo nikagundulika na ujauzito. Mkanifukuza, yeye akarudi kwenye picha tena, ndio akaanza kunitunza sasa kwa asilimia zote, mpaka leo.” Pakazuka ukimya. Wote wakawa wamemjua baba wa mtoto. Andy akabaki ameinama. Mina analia. Akajipandisha kwenye kitanda, akajilaza. Akamuona Andy anatoa simu. Ulikuwa usiku sana.

Kwa wazazi.

Akampigia simu baba yake. “Kwema!? Mbona usiku sana!?” “Samahani baba. Kesho utakuwepo nyumbani wewe na mama?” Andy akauliza. “Hata kama nikutoka, ni hapahapa mjini. Ninauhakika hata mama yako hatasafiri. Ulitaka nini?” “Nina mazungumzo na wewe, mama, Paulina na Pius.” “Saa ngapi?” Baba yake akauliza. “Nategemea kuwa hapo mida ya jioni.” “Basi nitawauliza wenzako. Ila hata kama wao watashindwa, mimi na mama yako tutakuwepo. Karibu sana.” “Ni muhimu wawepo baba.” “Basi nitazungumza nao.” Andy akakata.

~~~~~~~~~~~~~~

 “Unataka kufanya nini Andy?!” “Lazima kuzungumza na Pius mbele ya wazazi wajue alichokifanya.” Mina akanyamaza. “Au wewe ulikuwa ukifikiria nini?” “Hata sioni maana Andy!  Kwa sasa haileti maana tena. Heri ningekuwa mkeo! Sasa hivi unaongea juu yangu, wewe kama nani? Halafu ni ndugu yako. Huwezi kumshitaki popote. Hata mimi sitamshitaki popote. Namuacha tu.” Andy hakuridhika.

“Lakini lazima ajue, ninajua.” “Halafu kitatokea nini Andy? Itasaidia nini? Pius hakuwahi kuniacha hata mara moja! Ni ukiri tu wa alilonifanyia. Lakini kila nikimfikiria sasa hivi, ni kama mtu aliyekuwa akiniandaa kuja kumsamehe au akiniambia anawajibika na alichokifanya kwa maneno na vitendo. Wakati watu wote mmenitupa,  yeye alibaki na mimi.”

Ulinifukuza nyumbani ukanirudisha kwa mama na kuniacha nikiwa mgonjwa, bila hata shilingi! Mama akijua umeniacha bila hata pesa, naye akanitukana sana na kunifukuza bila hata kujali wapi nakwenda. Pius alinitafuta na kuhakikisha natibiwa. Silali nje, na silali na njaa.” Mina akaendelea.

Wewe na mama yangu mzazi hamkujua nilipo wala ninaendeleaje, lakini sio Pius. Yule mtu amehangaika na mimi mpaka natamani kama ingekuwa vinginevyo sio kufanya mapenzi na mimi bila ufahamu wangu, tena nikiwa mke wako. Halafu pia asiniambie, aache naaibika! Natamani ingekuwa ni mtu mwingine sio Pius. Sisemi kuwa wema wake unazidi ubaya alionitendea, lakini hakunikimbia kama nyinyi. Na angeweza Andy. Nani angejua?” Andy alipandwa na hasira, akashindwa hata kuzungumza.

Nipende, nisipende, na yeye atakuwa kama wewe. Tumezaa naye.” “Naomba usiseme hivyo Mina! Mimi nilikuwa mume wako.” “Wewe nishahidi Andy, ulifika sehemu ukawa mume tuliyekuwa tumeandikishana tu kanisani, yeye ndio ananitunza. Na nafikiri ndio maana haikukusumbua kunifukuza kwako mikono mitupu na usijali nilipo wala ninaendeleaje, kwa kule ulipokuwa umefika na mimi Andy. Mapenzi yaliisha kabisa, nikabaki kama mfanyakazi wako tu, nikikutumikia.”

“Ukinituma huku na kule. Mara kwenda kuwalipa mafundi, kununua hiki na kufanya kile. Na ukanifukuza bila hata marupurupu wakati nilikutumikia bila kuiba! Haikukusumbua Andy. Lakini sio Pius.”

“Pius alihakikisha siishiwi nilipokuwa mkeo na pia uliponiacha. Alikuwa ananiwekea pesa benki mara kwa mara. Hivi ninavyokwambia Andy, nina mamilioni ya pesa, amekuwa akinipa Pius. Sina uhitaji na chochote jinsi anavyoweka pesa. Na ni vile nimeamua mimi nisimtafute tena, lakini Pius alikuwa hawezi kulala bila hata kujua nimeshindaje au asubuhi kujua kama niliamka salama. Jana nimeangalia salio benki, japokuwa hatuwasiliani, lakini Pius ameweka tena pesa. Sasa, sasa hivi naelewa ni kwa nini anahangaika hivyo.”

“Wewe nishahidi Andy. Watu WANAWAPA mimba wanawake, wanakimbia nakuja kudai watoto baadaye sana. Au hata kukataa watoto wao! Alishindwa vipi Pius? Huyu dada hapa, Judy, amekimbiwa na mume aliyezaa naye watoto watatu, lakini Pius amebaki kulea mimba ambayo ni yeye peke yake ndiye anayejua ni YAKE, wakati hata mimi mwenyewe sijui!” Andy akasimama na kuondoka pale kwa hasira.

~~~~~~~~~~~~~~

Asubuhi Mina akaamshwa na sinia la chakula. Akakaa. “Andy!” “Amka ule. Nataka twende Dar.” “Kufanya nini?” Mina akauliza. “Lazima tuwekane sawa Mina. Pius ametumia udhaifu wangu kuvunja ndoa yangu. Lazima wazazi wajue.” “Mimi sitaki kesi Andy!” “Kwa hiyo wewe unataka yaishe hivi hivi!? Na yanaishaje?”

“Niliamua muda mrefu sana. Tokea mama amenifukuza na yeye nyumbani kwake, kuwa hii mimba nitazaa na mtoto nitalea. Japo sikuwa namjua baba yake, niliamua nitalea tu. Ni WANGU. Sina uwezo wakumfukuza. Jana usiku ndio nimemjua baba yake, sitaki kukurupuka, sitaki kesi mbele ya familia yako. Haitanisaidia mimi wala mtoto wangu.” Mina akatoka pale kitandani kwenda kuosha uso.

“Mbona kama wewe hizi habari hazijakushitua Mina!?” Akashitukia Andy amemsimamia hapo maliwatoni. “Habari zipi zinishitue? Hii mimba nilikuwa nayo tokea miezi 6 na siku kadhaa iliyopita? Pius nilikuwa naye karibu, akinitunza kama mume kwa takribani miaka mitatu sasa. Hajawahi kuniacha, atakachokwenda kusema ni ‘samahani’. Akijitahidi, atadanganya labda na yeye siku ile ALILEWA, shetani akampitia. Ataomba msamaha wa dhati. Atabaki kuwa kaka kwako na baba wa mtoto wangu ambaye anamtunza. Sasa natakiwa kufanya nini mimi!?” Kimya.  Mina akainamia sinki na kuendelea kuosha uso.

Akatoka kurudi chumbani. Andy anamfuata nyuma. “Basi nisindikize mimi kuzungumza na wazazi.” “Na kwenda kwenu mimi kama nani, Andy? Mimi si mkeo! Mimi sio Ruhinda tena. Au umesahau mara ya mwisho nilipokwenda kwenu dada yako alivyonitukana?” “Nilimkataza na nilizungumza naye tena mbele ya familia yote ya Ruhinda. Nikamuonya kuwa asithubutu hata kukugusa tena au kukuongelesha vibaya. Na nilimwambia sitamsamehe, mpaka akuombe msamaha.” Mina akakaa kwenye kochi, Andy akamsogezea chakula.

“Na kwa taarifa yako tu Mina, mimi sikukutafuta kwa kuwa nilijua unaishi na mwanaume aliyekupa mimba. Sikutaka kujiumiza zaidi. Nilijua umeshindwa kunisamehe, japo nilipokuwa Uswiz nilijieleza na kukuomba msamaha sana. Mwanzoni ulionyesha ni kama hutaweza kunisamehe. Mwishoni nakaribia kurudi ndipo ukanirudia vizuri sana. Nikawa na nguvu hata yakumaliza mafunzo. Narudi, naambiwa ni mjamzito! Moja kwa moja nikajua ndio sababu hukuwa ukitaka kuzungumza na mimi kwa kuwa ulishaanza mahusiano mengine.”

“Mimi ni binadamu Mina, nilikosea jinsi ya kukuacha bila kujali utaishije. Lakini naomba na wewe unifikirie, kama mimi ningekuwa mchoyo wa kiasi hicho, ningekuwa nikikupa kadi zangu karibu zote za benki na namba za siri? Wewe mwenyewe ndio ulikuwa ukisema unaogopa kuchukua bila kuniomba. Au umesahau hilo?” Mina akanyamaza.

“Mina?” “Sasa kwa nini ulinifukuza nikiwa mgonjwa na bila kunijali? Mambo ya zamani nilishasamehe Andy, na nilikwambia nimesamehe na wewe ukaniahidi ukirudi nitaona mabadiliko. Hiyo sitazungumzia. Yameisha. Lakini kwa nini uliniacha kikatili vile?” “Hasira Mina. Ni hasira kutaka uende huko kwa huyo mwanaume hivyo hivyo ukateseke mpaka unikumbuke.” Mina akacheka kwa kushangaa.

“Andy wewe!?” “Nakwambia ukweli kile kilichokuwa kikiendelea kwenye moyo uliokuwa umeumia na kujua umenisaliti! Hata wewe ungekuwa mimi ungeumia Mina. MIMBA!” Mina akanyamaza akaendelea kula. “Ila nimefurahi kama unakumbuka kukuomba kwangu msamaha. Nashukuru. Nilijua bado unahasira na mambo ya nyuma!” “Ulivyokuwa umenibembeleza vile!” Wakacheka.

“Nilisamehe Andy. Na nikwambie ukweli tu, nimekusifu kitendo chakuweza kumudu kunichukua na kuishi na mimi nikiwa na mimba isiyo yako! Nakushukuru. Najua ni ngumu.” Akamuona Andy anatoka huku akicheka. Mina akaendelea kula.

Akamuona anarudi na kabrasha. Akakaa pembeni yake. “Unakumbuka hii?” Akamkabidhi Mina. Akaanza kusoma. “Si ndio talaka yangu uliyoniambia niweke saini!?” “Basi sikuipeleka popote. Ilibaki hapahapa.” Mina akamwangalia na kuendelea kula. “Kisheria wewe bado ni mke wangu Mina. Hata ofisini bado unajulikana kama wewe ni mke wangu. Haya makaratasi yanabaki hivi hivi mpaka ningeyapeleka kwa mwanasheria, yakafanyiwa kazi. Tukiamua mimi na wewe tunaweza kuyachana tu, tukaendelea kama kawaida. Na ahadi zangu za Uswiz zile nilizokuahidi, zitabaki vile vile.” Mina kimya  kwa muda akifikiria.

“Mina?” “Ulitaka twende Dar saa ngapi?” “Tuondoke dakika 45 kuanzia sasa. Halafu tunaweza rudi hata kesho.” “Ila sitamuacha Ayan.” “Mina! Siku moja tu!” “Hapana Andy, huyo sitamuachia mtu. Judy mwenyewe nilishamuona anamshangaa vile anavyokunywa maziwa mengi. Acha tu nikiwa na uhai, niwe naye mpaka atakapoweza kujitetea. Ayan ni mpole sana.” Mina akafikiria kidogo.

“Mimi nitajilipia nauli yangu na Ayan. Na nitalipia chumba cha hotelini. Wewe jilipie nauli yako. Lakini sitamuacha Ayan. Naenda naye.” Andy akatoka. Mina akala kwa haraka, akaanza kujitayarisha kwa safari.

~~~~~~~~~~~~~~

Familia ya Ruhinda Na janga la ndugu wa tumbo moja wote kuzaa na mwanammke mmoja!

Nini Kitaendelea kwa ndugu hao?

Mill na Pam Nao?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment