Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 34. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 34.

Andy akawa amefunguliwa macho kwa asilimia kubwa sana. Akaanza kuunganisha mambo na matukio. Maneno na vitendo. Akajidharau na kuona hata wao wameshamuhesabu kama mjinga. Akajifikiria. Akaona vile wanavyomtizama hata pale nyumbani kwao si kwa mafanikio ila kama kijana aliyeshindwa.

Nani amempa mimba Mina? Akarudi hapo akakumbuka maneno ya Paul. Akawa kama amepata jibu alilokuwa akilikataa nafsini kwake na kupingana nalo akiomba Mungu isiwe hivyo. Akatetea kwa hili na lile.

Mtoto Wa Ujanani Aibua Maswali Kwa Baba Yake.

Alimkuta Shema anamsubiria. Ameshavaa, amependeza. Msafi. Amevaa nguo mpyaa zote alizomnunulia. “Nilijua huji tena!” Akamwambia alipompokea. “Nilipitia kazini kwa mama yako ndio nimekuja hapa. Naona upo tayari, twende.” Wakatoka kila mtu hapo mtaani akimsifia Shema alivyopendeza na vitu vyake vipya. Basi Shema yeye hana moja, anacheka tu.

Moja kwa moja kwa kinyozi. Wale vinyozi ambao Shema hajawahi hata hisi anaweza ingia huko. Wakamchonga mtoto wa Mill, akaanza kufanania na pesa za baba yake. Alishaongea na Colins amsaidie kumtafutia daktari atakayeangalia huo mkono tena. Gozi lilikuwa chafu sana, alitaka abadilishwe.

Akafika hospitalini. Akakuta Colins na Kamila wanawasubiria. Shema akasalimia kwa heshima huyo! Lakini wakabaki wanamshangaa huyo mtoto. “Aisee umefanana na na huyu mtoto! Kama ni mimba ulikuwa uliikataa, hapa ungeumbuka!” Mill akacheka akikumbuka maneno ya kule uswahilini kwa kina Pam.

“Hafanani kabisa na Mia wala Miles! Utafikiri si watoto wa baba mmoja!” Collins akaongeza akiendelea kushangaa bila hila asijue anazidi kugongelea msumari kwenye wazo aliloanzisha Pam kichwani kwa Mill mpaka moyoni kwake.

Mill akamwangalia mwanae akacheka akifikiria mengi. “Sasa huyu sina muda naye mrefu. Hili gozi chafu sana aisee. Nimeambiwa muda uliobakia ni majuma mawili tu atolewe, nataka kujua kama anaweza kutolewa hili akawekewa jingine, na pili nataka kumuanzishia faili lake hapa la afya yake. Afanyiwe annual checkup, iwepo rikodi ya aina yake ya damu. Kama kuna kilichopungua huko mwilini mwake, nijue, ili kiongezwe. Nataka na physical checkup maana ni mcheza mpira wa miguu. Afanyiwe kila kitu, ila kwa haraka tafadhali.” Colins akamsaidia akafanyiwa huduma kwa haraka huku Mill akiangalia saa asije pitisha muda.

Mpaka kuja kumalizana na mambo ya hospitalini. X-ray na kufungwa tena, muda ukawa umeshaenda. Akampeleka tu kula, akaanza kupambana na foleni kurudi Tandika kwa Pam lakini akiwa ameibua maswali mengi sana.

Shema alikuwa na aina ya damu, ‘O’ kama baba yake kabisa. Majibu ya DNA yalikuwa hayajatoka, japo aliomba vipimo vyote ili viwekwe kwenye faili lake la hospitalini. Hakutilia mashaka kabisa kama Shema ni mwanae. Bila DNA, huyo mtoto alifanana sana na baba yake.

“Hawa watoto wengine mbona kama hatufanani na hata damu yao ni ‘B’!” Akajiuliza na kujirudi. “Pengine Kisha ni ‘B’! Lakini ndio wasifanane na mimi hata urefu jamani! Unaweza kuta Pam yupo sahihi. Japo aliongea kwa hasira. Isije kuwa nilibambikiziwa!” Akaendelea kuwaza akikimbizana na foleni.

“Ukute ndio maana damu zetu zimeshindwa kuendana kabisa na hawa watoto!” Akaendelea kuwaza ugumu anao pambana nao akiwa anawalea hapo.

Mwishoe akaamua kuacha kufikiria hilo akihofia matokeo. “Huku kufungwa na kuwaacha na Kisha pamoja na Trey ndio kumewaharibu tu. Na pengine Kisha ana damu kali, watoto wamechukua kwake.” Akajifariji na kutulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alifika pale saa 12 kasoro. Akamkuta Pam amejilaza ndani. Mwanae akaenda kumuamsha. “Ona nilivyopendeza!” Pam akacheka na kukaa. “Umekua msafi! Umependeza kila mahali!” “Asante mama.” “Basi naomba ukacheze na miguu, Shema mwanangu! Mkono huo msafi, utunze ili tupunguze kukunana usiku. Walikuosha kabla hawajakufunga tena?” “Wamenisugua vizuri na kunikausha. Wakanipaka kama mafuta, wameniambia itanisaidia kupunguza kuwasha. Ndio wakanifunga tena.”

“Wamesema unaonekana umeunga, ila daktari ameonelea amalize muda wake.” Mill akaingilia kwa kujihami. “Nakushukuru. Asante sana. Amekua msafi! Na nywele pia amependeza. Asante.” Akagundua likifika swala la mwanae, anatulia na anajawa shukurani.

Watoto wakawa wamejaa mlangoni, wanamuita Shema atoke. “Sasa sio upotee, nianze kazi ya kukutafuta!” “Siendi mbali. Leo nataka nisijichafue, ili kanisani wanione msafi.” “Na ulikumbuke hilo, unapokwenda huko nje, halafu ukaona mpira. Sio ushawishike.” “Siwezi. Na hata nikicheza…” “Nilijua tu.” “Sijichafui mama! Nacheza kwa miguu kama ulivyoniambia.” Mill akacheka akimwangalia mwanae.

“Basi badili nguo vaa..” “Nataka wanione na nguo mpya, mama!” “Wewe unataka ukazitie madoa, mimi nishike kazi ya kufua tu!” “Naenda kuwaonyesha, halafu narudi kubadili za kuchezea.” “Naomba ukumbuke Shema! Maana wewe ukiona mpira tu, akili inapotea kabisa.” “Sipotei mama. Nitarudi.” Akatoka.

“Nimewaletea zawadi ya pipi.” Akamsikia akiwaambia wenzie. “Na mimi Shema?” Kila mmoja akawa anamuuliza huyo Shema. “Nimemuomba baba aninunulie mfuko mkubwa, nikamwambia nina marafiki wengi. Wote mtapata.” Wakamsikia akiongea huko nje.

“Basi kuja kurudi humu ndani tena ni usiku au mpaka nikamtafute! Atapita kila nyumba kwenda kugawa hizo pipi, kisha mpira. Shema bwana!” “Lakini Pam, huyu mtoto umemlea vizuri aisee! Kila unapokwenda naye, mpaka raha! Kila mtu anamsifia! Halafu nafikiri ana damu ya kupendwa tu.” Pam akanyamaza akiwa amekaa tu kitandani.

Mill&Pam Mkakati wa Shema.

“Ulikuwa umelala?” Akamuuliza kwa kujali. “Nimetoka kupika chapati za biashara, nikaona nipumzike.” “Hazijabaki na mimi nichukue?” Pam akabaki akimwangalia. “Wewe mfanyabiashara gani unachagua wateja?!” “Wa uzunguni nyinyi mnakula vya uswahilini vinavyopikwa na mkaa?” “Hakika nataka chapati. Kama unazo za ziada nipe na mimi.” Pam akacheka taratibu na kunyamaza.

“Huwa unamuuzia nani?” “Pale kwenye ule mgahawa karibu na kazini. Na kwenye lile eneo linalopakana na pale ninapofanya kazi, wanalouza matairi na kutengeneza magari. Wale wanaume wote pale wanategemea vitafunwa kutoka kwangu. Nawatengenezea chapati na maandazi. Ila mgahawani wanachukua chapati. Leo kama hivi nikipika ni chache za hapahapa mtaani. Si haba! Zinasaidia. Na ni wazo la mama. Alinikuta sina kazi, halafu tumbo kubwa, siwezi ajiriwa.”

“Akanifundisha hiyo biashara. Tukawa tunapika naye, napeleka kwenye
mahoteli mpaka nikajifungua. Akanisaidia kukaa na mtoto, nikaanza kazi. Yeye anakaa na mtoto na kupika. Nikitoka kazini tunamalizia. Nasambaza jioni au asubuhi. Tunapata pesa. Shema alipofikisha miaka minne nafikiri, ndio akaondoka kurudi kumsaidia na bibi kijijini, babu alikuwa mgonjwa.”

“Ndio nikaona nalemewa. Kazini na malezi ya mtoto.  Nikampa mama Batuli hoteli moja, na mama Pili hoteli ingine. Mimi nikabakiwa na za huko upande wa kazini. Jumapili nikiwa siendi kazini, napumzika mpaka jioni ndio naanza kupika vya kupeleka kazini siku za jumatatu. Kwa hiyo napika jumapili, jumatano na ijumaa wakati mwingine jumamosi. Inategemea. Si haba! Inanisaidia kutusogeza.” “Hongera Pam. Na pole kwa matatizo.” Hakumjibu akatoka kitandani.

“Kabla sijaondoka, nimefikiria. Nakusihi Pam, kubali mtoto wangu akapate elimu bora, si bora elimu. Tafadhali Pam. Na kukuhakikishia kwamba nimekusudia,  maana umesema huamini chochote nitakachokwambia.” “Hata kidogo.” Akaweka msisitizo. “Sawa. Na mimi nakubaliana na wewe. Hata mimi nisingeamini tena. Ila kumbuka ulisema hatasoma shule ambayo huna uwezo wa kumlipia wewe.”

“Huko kwenye mashule yenu ya kizungu, sitaweza mimi.” “Basi, mimi nitafanya hivi, jumatatu, nakwenda huko shuleni. Watanipa jumla ya pesa yote watakayokuwa wakitaka kwa mwaka. Nitakuletea kule ofisini. Ukitoka, tunakwenda wote benki. Naiweka pesa hiyo kwa miaka yote mitatu iliyobaki kumaliza darasa la saba. Ya kumalizia mwaka huu nalipa kabisa.” Hapo Pam akakaa.

“Na hiyo akaunti inakua ya jina lake, lakini wewe unaisimamia. Unaonaje wazo langu.” “Usafiri wa kumtoa huku kwetu uswahilini kumpeleka shule? Na kuhama hapa, HAKUPO kwenye mjadala.”

“Nimekuelewa. Ila jua utamtesa mtoto.” “Atafanyaje na yeye kajaliwa baba wa namna yako? Ingekuwa chaguzi yangu na si ujinga wangu tokea siku ya kwanza na kuku..” “Naomba huko usirudi Pam. Ukipandisha hasira, hutaki tena kunisikiliza. Hatua kwa hatua. Kwa swala la kwanza la shule, si mpaka hapo umekubali?” “Hapo sawa. Nakuuliza usafiri wa kueleweka. Maana wewe una mwanzo, mwisho huna. Tutaanza vizuri hapa, kisha uje uniache na mwanangu ana nguo za shule, hajui jinsi ya kufika huko shuleni kwenyewe, halafu wewe hupatikaniki, upo Ulaya huko!” “Ni Marekani.” “Unanitania Mill!?” Akaanza kucheka.

“Nilikuwa naweka sawa hoja yako. Ulaya na Marekani ni tofauti kabisa. Kwanza ukiangalia hata kwenye ramani ni mbalimbali sana.” “Kweli huu ndio muda wakutaka kunifundisha mimi jografia ya ulimwengu, kweli?” Mill akacheka. “Basi mama Shema. Maana siku hizi nasikia unaitwa mama Shema, sio Pam tena.” “Pam ulimuua muda mrefu sana. Naomba ongea maswala ya msingi.” “Sawa mama. Turudi kwenye swala la usafiri.”

Akajiweka sawa. “Gari ya mara ya mwisho uliyokuwa nayo uliipenda au unataka aina nyingine?” Pam akabaki akimtizama. “Nina maana yangu kukuuliza Pam!” “Unachokifanya hapa, ni kutaka kunitibua.” “Basi. Kazi ya kuanzia leo mpaka kesho natafuta dereva wake Shema. Jumatatu, nakuletea gari. Tutakuwa tunaliacha pale CCM. Wameniambia watu hulaza magari yao usiku, malipo kidogo. Asubuhi huyo dereva anawahi, anakwenda kuchukua gari, anampeleka Shema shule. Anaacha gari shuleni. Anarudi kwenda kumchukua jioni akitoka shule. Alipo Shema, ndio hilo gari litakuwepo.” “Haaa!” Wakasikia nje wakihamaki. Wote wakaangalia dirishani. Wakajua wanawasikiliza.

Wakatulia kidogo. “Unaonaje hilo wazo langu?” Akauliza kwa sauti ya chini. “Hapo sawa.” “Yess!” Akashangilia kwa sauti ya chini. “Basi jumatatu nakuja kumchukua Shema tunakwenda naye ….” “Umeanza!” “Nisikilize. Acha kuondoka.”

“Nikimuombea nafasi ya darasa la nne, akiwa mtoto wa umri wake, miaka 9, lazima watataka kumpima. Kujua kweli anastahili hilo darasa au arudishwe kuwa darasa moja la watoto wa mri wake. Maana yule mdogo wake ni kama mwaka wanalingana lakini kwa kuwa yeye alikwenda kawaida kama watoto wengine yupo 3rd grade. Kama darasa la tatu anakotakiwa kuwepo Shema.” Pam akamtizama kama ammeze.

Nimeshakosea Pam, mpenzi wangu. Nitafanyaje? Siwezi kukimbia, siwezi telekeza damu yangu.” “Kama baba yako!” “Sawa mama! Ila naona bora mimi kuliko wengine hawajali watoto wanao zaa nje. Kwa hiyo jumatatu nije kumchukua?” “Saa ngapi? Maana mimi nakwenda kazini alfajiri. Saa moja natakiwa niwe nishafika maeneo ya kule. Nisambaze chapati ndio kazini. Na yule ni wakumsaidia kuoga lasivyo anajilowesha gozi.” “Nikikuomba uwe naye ili nikija kumchukua na wewe nikuone, si ni sawa?” “Acha kunipaka mafuta kwa mgongo wa chupa!” Mill akacheka.

“Wewe nenda naye, nitakuja kumchukua niende naye shule kwenye mida kama ya saa nne. Saa nane wakati unatoka kazini, nakuja kukuchukua twende benki.” “Sitakaa nikikusubiria popote. Kamwe sirudii huo ujinga. Niambie ni benki gani unataka tukutane. Tumalizane, tuachane palepale kila mtu ashike lake. Usitake kunifanya mimi mtoto mdogo.” “Kwamba unachofikiria, ni kwamba nina tiketi tayari ya kuondoka hapa nchini, na jumatatu naweza kuondoka nikakuacha ukinisubiria?” “Unataka nikujibu hilo swali, kweli?” “Hapana.” Mill akakataa kwa haraka. Pam akasimama.

“Pam!” Akamgeukia. “Nikikuomba ukatengeneze nywele, nitakukera?” Pam akamtizama na kuendelea na shuguli zake palepale ndani. “Leo upo tu nyumbani na kesho. Pesa sasahivi unayo. Kwa nini usiende ukatengeneza nywele kama zamani?” “Pam wa zamani alikuwa akifanya kazi ofisini. Huyu sasahivi ni mama Shema, anauza maziwa. Lazima kufunga nywele. Ni sheria ya kiafya. Bila hivyo unapigwa fine. Huko unakokwenda sasahivi ndio unakaribia kunikera. Kwanza ondoka. Tushamalizana mambo ya mtoto, huna jingine. Nenda unipishe nifanye mambo yangu.” “Nilikubebea chakula tulichokula mchana. Mambo yako matupu humo.” “Asante.” Kwa shukurani tu, alijaliwa.

“Ombi la mwisho.” “Wewe unataka kuharibu!” “Jambo zuri.” “Nini?” “Kesho naomba nije nimchukue Shema…” “Ishia hapohapo. Naona unataka kufanya mazoea sasa.” “Ni jambo la kheri. Nataka akakutane na ndugu zake.” Hapo Pam akageuka.

“Unasema nini?!” “Nampeleka nyumbani Pam. Kwao.” “Nilikuonya Mill wewe!” “Basi Pam.” “Nilipo mimi ndipo nyumbani kwa Shema.” “Sawa, sawa. Acha nitengeneze. Nataka afahamiane na wadogo zake.” “Yaani ukiongea hivyo unazidi kunikera.”

“Basi na wenzie. Kumbuka kuanzia jumatatu au niseme jumanne, hawa watu wote watakuwa wakisoma shule moja. Kweli unataka wakakutane shuleni kama watu baki?” Akatulia kidogo akifikiria. “Nakuahidi hatachelewa. Nakuja kumchukua tukitoka kanisani halafu…” “Na wewe unasali?! Makubwa! Unamuomba Mungu gani?” Mill akaamua asijibu, aendelee.

“Tunakwenda kula chakula cha mchana, halafu nyumbani, jioni namrudisha. Na tutacheza mpira pale kwangu. Nina uwanja mkubwa tu. Leo hatukucheza sababu muda ulionipa ni mfupi.” “Na kesho arudi muda kama wa leo. Sasa umcheleweshe.” “Si umeona leo nimekuwa mwaminifu, nimemrudisha kwa wakati?” “Ulikumbuke hilo kesho. Maana ukichelewa, sitakumbuka kuwahi kwa leo.” Akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha kama aliyetua mzigo.

“Nina ombi jingine, ila hilo nalitunza mpaka jumatatu. Nahisi nikilileta sasahivi, naweza nikaharibu.” “Sasa kwa nini ulilete hilo ombi kama unajua kabisa ni la kukera?” “Ni lazima tutafikia tu muafaka. Nishakuona wewe kwenye mambo ya msingi tunaelewana.” “Haya, jioni njema. Naona muda wako wa kukaa hapa umeisha.” Mill akacheka na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Alipotoka tu, majirani zake wote mlangoni. “Mimi ndio nimewahi, mama Batuli!” “Sasa kwani baba Pili alishaendesha wapi gari, kama si tamaa tu?” Pam akawa hajaelewa. “Nakuomba muombee baba Batuli hiyo kazi ya kumuendesha Shema. Tafadhali shoga.” Pam akabaki amepigwa na butwaa hapo mlangoni.

“Mimi niliwahi tokea baba Shema yupo ndani!” “Sasa acha niwaambie. Huyu mwanaume hayupo na mambo ya juujuu. Kama kweli kuna anayetaka hiyo kazi, ataitisha leseni ya kuendesha. Ataipeleka ikakaguliwe, na atataka huyo mtu amuendeshe yeye kwanza. Ndivyo alivyo Mill. Hafanyi mambo ya kienyeji.” “Mimi leseni ninayo mama Shema.” Akadakia baba Batuli mwenyewe.

“Na nina uzoefu wakuendesha mabosi wa Wizara ya Afya. Sema walinipunguza kazi.” “Na wewe baba Pili?” “Naona hapo mimi nitakwama. Leseni ilishapotea zaidi ya miaka 10. Naona hiyo riziki ni ya baba Batuli.” “Basi mimi nitazungumza naye akija kesho. Ila hakikisha unayo kweli leseni. Atataka kuiona na kuifuatilia kujua ulikuwa ukiendesha vipi! Ulishapata ajali au la.” “Mama Shema!” “Hakika sikudanganyi. Hana njia za mikato. Utamsikia mwenyewe.”

“Ila bwana dume lile unalo!” Akasifia mama Batuli. Pam akamwangalia hakutaka kuongeza neno. “Ngoja mimi nikamtafute Shema. Maana najua kuja kurudi hapa ni usiku!” “Na hivi ana viatu vipya!” Mama Pili akamfanya Pam acheke. “Mwanangu kipofu kaona mwezi! Utafikiri apae!” “Kaniambia alilala navyo jana usiku.” “Wewe acha tu!” “Naomba mimi vile vya zamani, mama Pam. Mwanao navaliana naye kabisa.” Baba Pili akaomba.

“Wala usijali. Acha nikamuwahi kabla hajajichafua huko alipo. Baba yake msafi sana. Hapo kambadilisha gozi sababu kaliona chafu. Sasa mtoto mwenyewe anacheza mpira wa miguu na mikono! Jasho litamtoka.” Wote wakacheka, Pam akatoka.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~

Pam aliwahi ibada mapema, kwenye majira ya saa tano anarudi akitembea na mwanae, akaona gari ya Mill akajua anawasubiria. Shema akakimbilia mpaka dirishani. Mill alipomuona, akashuka garini. Akamsalimia Pam na mwanae. “Mimi naomba hata ndani nisiingie. Kuna mahali tunakutana kwa chakula cha mchana. Wengine wameshatangulia, wananisubiria mimi na Shema tu.” “Nirudishie mwanangu kama ulivyomchukua. Sio arudi hapa mnyonge.” “Pam!” “Kumbe! Maana unaweza kwenda kumkutanisha na watu wa hali za juu, ukamfedhehesha. Sasa arudi hapa amenyongea, jua ndio mwisho wa kwenda kumnyanyasa mwanangu.” Mill akaona asiongeze.

“Ushapata dereva?” “Bado. Kwanini?” “Baba Batuli alikuwa…” “Hapana Pam. Mimi mambo ya ujamaa, halafu uje uniletee matatizo, hapana kwakweli.” “Alikuwa dereva anaendesha magari ya Wizara ya Afya.” “Una uhakika?” Pam akanyamaza.

“Pam? Maana ujue itabidi aniletee uthibitisho. Na nitataka kuona leseni.” “Nimemwambia, amekubali.” “Sawa. Nitazungumza naye nikirudi. Panda kwenye gari Shema, twende.” Shema akapanda kwa haraka. “Umependeza sana Shema. Halafu msafi!” Akamsikia akimsifia mwanae. Ila alimjua Mill anapenda vitu vizuri.

“Humu ndani kuna baridi sana.” Pam akamsikia mwanae. Akadakia. “Sasa sio arudi anakohoa huyo!” “Napunguza mama. Wewe hutaki kuongozana na sisi?” Ikawa kama amemfukuza Pam, akaanza kuondoka. Mill akaanza kucheka. “Umependeza Pam, mke wa ujana wangu.” Hata hakugeuka, akaingia ndani. Akaondoa gari.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwenye majira ya saa 10 hivi, amejilaza akipepewa na feni. Joto haswa ndani, anasubiria papoe nje, akaanze kupika chapati, akaona Shema anaingia na nundu kubwa pembeni ya jicho. Na hivi ni mtoto mweupe, ule uvimbe ulikuwa mwekundu haswa.

Pam alishituka, nusura roho imtoke. “Njoo hapa. Umefanyaje?” Shema akaanza kulia. “Mtoto wake wakiume amenipiga na game.” Pam aliumia sana. “Kwa nini?!” “Anasema nimemuibia kitabu chake. Na baba yake ameamini.” “Yuko wapi huyo baba yake?!” “Sijui! Mimi nimeondoka kwao, nikarudi nyumbani.” “Kwamba umekuja hapa bila yeye?!” Shema akazidi kulia. “Na hapa juu pamechanika. Twende dispensari.” Akatoka na mwanae amemshika mkono akimtuliza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Huku nyuma Mill akafika kama aliyekuwa akikimbia. Akakutana na majirani wamekaa pale uwani. Baba Pili akamuwahi. “Mimi nashauri kwa leo, ukae mbali. Mtaa mzima huu wanamjua mama Shema. Hakuna anayegusa mwanae. Ashapigana na kijana mmoja pale baoni, sababu ya kumgusa mwanae. Ngumi zilizopigwa pale, mpaka leo wanasimulia.”

“Mama Shema alimpiga yule kijana, kama kapigwa na bondika. Waulize pale baoni watakukusimulia. Huyo Shema haguswi.” “Wala hatukanwi.” Akadakia mama Pili. “Ukimtukana tu mwanae, akisikia, anakufuata mpaka kwako na hutamtuliza kwa maneno.” “Ilitokea ajali tu!” Mill akawa anajitetea.

“Basi sivyo alivyosema mwanao. Kasema mtoto wako kampiga na game kwa makusudi akimsingizia WIZI. Na wewe ukaamini kama kaiba.” “Na Shema si mwizi, wote tunamjua. Akiokota hela, haweki mfukoni mpaka wenzie wanamcheka.” Mwingine akadakia. “Hata uangushe pesa hapa, akiokota yeye jua utaipata pesa yako.” Akaongeza baba Batuli.

“Sio kwamba niliamini! Ila nilikuwa najaribu kuwapatanisha.” “Sasa hapa uondoke, lasivyo usiku huu utakuishia vibaya.” “Wameenda wapi?” “Kuna dispensari moja ipo kule mbele ya CCM. Kuna daktari pale anampenda sana mama Shema. Atakuwa ndio kaenda hukohuko.” Mill akaondoka kama akimbie.

“Sasa na wewe mambo ya kupendwa yanamuhusu vipi?” “Ndio ajue tena hayupo peke yake.” Wote wakacheka. Mill akasikia ila akanyamaza na kuongeza mwendo atoke hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Akaendesha akitafuta hiyo dispensary mpaka akapapata. Akajiandaa kuingia akijipanga, mpaka akapata ujasiri. Palikuwa pametulia mlango umefungwa kwa nje. Akajua siku hiyo huwa hapafunguliwi, inamaana kama kweli wapo ndani, huyo daktari yupo hapo kwa ajili ya Pam.

Akagonga mpaka mlango ukafunguliwa. Alikuwa Pam. Roho ikampasuka paa! Alikuwa mwekundu kama apasuke. “Wewe ndio wa kumuita mwanangu mwizi?!” Likawa swali la kwanza. “Umenikuta nikiishi uswahilini ukadhania nimekuza jambazi!” “Nisikilize Pam.” “Kati yako na Shema, nitamsikiliza Shema, kwa sababu yeye si muongo. Umeniumiza Mill, kuliko ulivyowahi kuniumiza. Hivi ninavyozungumza na wewe, nisiwahi kukuona tena.” “Pam!” Pam akatoka nje kabisa.

“Nina faida gani na mtoto anaye vaa viatu vipya halafu mmempasua kichwa? Nina faida gani na mtoto anayevaa nguo mpya huku ananyanyasika?” Pam alikuwa anaongea mpaka anatetemeka. “Nimemfikisha hapo alipo, sitashindwa kumuendeleza zaidi. Uliniacha nikiwa na mimba yake huyu, si amefika hapo alipo? Hakika nisikuone Mill. Leo mwisho wako. Hutakaa ukamnyanyasa mwanangu.”

“Nikija kukuona kesho au kesho kutwa, itakua mbaya! Hutaamini na utajuta hata kunifahamu. Nimempiga picha ushahidi wa kile ulichomfanya wewe na watoto wako. Huyu daktari ni shahidi wa kumtibu leo. Wewe si unapesa, utataka kunichukulia hatua, sasa NIANZE uone jinsi nitakavyo kumaliza. Hutakaa ukamuona huyu mtoto mpaka aje kuwa mtu mzima, na tena pengine aje akutafute mwenyewe.”

“Siwezi kufanya hivyo. Naheshimu kila unachokisema juu yake. Na samahani sana, Pam. Nia yangu ilikuwa nzuri. Nahisi nimefanya haraka.” “Naomba uondoke, kabla hujaniumiza zaidi. Na ukumbuke, USIRUDI tena. Si pale tunapoishi tu, hata kazini kwangu nisikuone Mill. Nitazungumza na yule mama na nitamuonyesha picha kwa kile ulichomfanya mwanangu.” “Nakusihi Pam, usifike huko. Tafadhali mpenzi.” “Basi usitufuate nyuma tena. Kazae kwingine. Shema SAHAU.” Akaingia ndani na kumuacha amesimama nje.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Inaendelea…

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment