Alikaa Mina mpaka usiku, Andy hajarudi. Akaona afike
jikoni aangalie chakula. Akamkuta kijana wa Andy ameshasafisha. Jiko safi.
Akajua alimtuma yeye mwenyewe. Akamlisha mtoto, akampa maziwa na kumrudisha
chumbani. Mina naye akaona aende tu kulala.
Asubuhi akamkuta jikoni anapika. “Nilizungumza na
Kashinde. Nimemuomba kama anaweza kubadilisha muda wa kwenda kumchukua huyo
msichana. Akaja mapema kidogo labda hata kesho ili angalau tumuonyeshe
mazingira, tumuachie nyumba, ndio tuondoke.” “Nimegairi. Hakuna
safari tena, leo naanza kwenda kazini.” Mina akasimama pale nyuma yake kwani
hakuwa hata amemgeukia wakati akizungumza naye. Mwishoe Mina akaamua aondoke.
Andy alipika kifungua kinywa kwa wote, akajitayarisha.
Akatoka bila hata kuaga. Mina alipoangalia muda akajua ndio ameondoka moja kwa
moja. Akatoka. Mtoto wake hakuwa ameamka na wala yeye hakuwa ameletewa kifungua
kinywa chumbani. Hakujali.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Alirudi jioni kama saa kumi na nusu hivi. Akasalimia,
akamshika Ayan kidogo, Mina akamuona anaingia chumbani kwake kubadili nguo za
mazoezi, akatoka. Mina alishakuwa amepika. Mpaka Ayan anakwenda kulala usiku,
baba yake hakuwa amerudi kutoka mazoezini. Mina na yeye akaona akalale
tu.
Mungu Hutumia Yeyote.
Kesho yake akafanya hivyo hivyo. Kutengeneza kifungua
kinywa na kuondoka bila hata kuaga. Ilipofika saa saba mchana Kashinde
akawa amerudi na huyo msichana wa kazi. Alionekana ni dada mtu mzima. Tena
mkubwa hata kwa Mina. Lakini alionekana ni dada anayejielewa, anapenda watoto
na si mshangaaji.
Akamuuliza kama alishafanya kazi mahali. “Wakati
mdogo. Nilifanya Dar kwa mama mmoja kwa miaka 18, ndipo nikaondoka kwenda
kuolewa. Nina watoto watatu, wa mwisho ndio ameanza darasa la kwanza. Maisha
yamekuwa magumu ndio nimeona nitafute tena kazi ili ziwasaidie wanangu.”
Akajieleza vizuri tu.
“Oooh, kwa hiyo unaye mume? Au niulize watoto
umewaacha na nani?” “Wapo na mama, lakini mwanaume aliondoka. Akaniachia
watoto. Nilishajaribu kumfuata kuomba hata matumizi, lakini alinikatalia.
Nimebaki nikihudumia hao watoto peke yangu. Hivi ilikuwa nije tokea majuzi,
mtoto wangu mkubwa alikuwa mgonjwa, ndio nikamuomba Kashinde aniombee
mnisubiri.” “Anaendeleaje sasa hivi?” Mina akauliza kwa kujali. “Anaendelea
vizuri. Alimaliza na dawa.” “Afadhali. Kwa hiyo ndio umekuja moja kwa moja?”
“Kabisa dada. Ila mtoto wako mkimya! Au hajaweza kuongea?” Mina akacheka na
kumwangalia Ayan.
“Anaongea na kuelewa kila kitu. Ila ni mkimya sana.
Ukitaka akupende, umpe maziwa. Hapo mtaelewana. Anakunywa maziwa kabla
na baada ya kila mlo.” “Inamaana kuanzia asubuhi?” “Ewaa! Kabla hujampa uji wa
asubuhi lazima umkabidhi chupa yake ya maziwa ndipo baada ya nusu saa atakunywa
uji, na ukishamsaidia kumsafisha mdomo, mnaagana na chupa nyingine ya maziwa
mdomoni. Hapo mtaelewana.” Wakacheka. “Kama mtoto wa ng’ombe?” “Hapana,
yeye anasema kama mtoto wa Mina.” Wakacheka sana.
Mina akamuonyesha kila kitu na chumba chake.
Akamwambia baba yake Ayan anakwenda kazini, anatoka asubuhi anarudi jioni. “Ila
Andy ni msafi sana. Hivi unavyoiona hii nyumba ilivyo, ndivyo hivyo inatakiwa
iwe kuanzia asubuhi tunaamka mpaka usiku tunaenda kulala. Kusizagae hata
kandambili. Au asikute hata tone la maji limemwagika sehemu. Kila kitu anataka
kiwe sehemu yake, kila wakati.” Wakacheka. Akamueleza taratibu zote.
Mina akafurahia aina ya maswali aliyokuwa akimuuliza. Akajua kweli anajielewa.
~~~~~~~~~~~~~~
Maisha yakaanza. Judy akawa msaada kweli kwa Mina.
Anamjali yeye na mtoto wake. Andy bado akawa na hasira vilevile. Juma la
kwanza Judy akiwa ameanza kazi likaisha, akiwasoma wenye nyumba yake. Akaona kuna utofauti kati ya Mina
na Andy.
“Nikuulize kitu mama mwenye nyumba wangu?” Mina
akacheka. Andy alikuwa ameshatoka kwenda kazini. Siku ya ijumaa. “Niulize tu.”
Mina akamkubalia. “Mbona sijawaelewa wewe na baba Ayan! Kama mnapishana
vile! Hamlali chumba kimoja! Kosa gani kafanya umeshindwa kusamehe?
Maana mwanaume kama yule hapa kwenye hili jiji, watakuliza wenzako!” Mina akabaki akifikiria asijue ajibu nini.
“Sio lazima ukaniambia, lakini ninachotaka kukwambia, ukishikwa,
shikamana. Wapo wanawake kazi zao ni waume
za watu tu. Kama bado hujachelewa, funga hiyo mianya mdogo wangu. Usikubali ukajaribiwa bila sababu.” Ikabidi Mina
amwelezee kwa ufupi, Judy akabaki ameshangaa.
“Sasa umemwambia mwenzio?!” “Namwambia nini
wakati hata mimi mwenyewe bado sijaelewa?!” Judy akashangaa sana. “Wewe
mama Ayan kwani una miaka mingapi?!” “Kwa nini?” “Mimi naona kama wewe bado una
mambo ya kitoto, hujayajua maisha! Hasira
hiyo ikiendelea akakwambia sasa hivi naomba unipishe ninaye Judy wakunisaidia,
unafanyaje na mtoto usiyemjua baba yake?” “Sasa nifanyaje!?” “Wewe Mina!
Samahani mpaka nimekuita jina lako kwa mshituko bosi wangu!” Mina akacheka.
“Wewe usiwe na wasiwasi niambie tu.” “Mbona mimi umenieleza
hapa! Kinachokushinda kumueleza na yeye ni nini?” “Hawezi amini!”
“Hiyo itakuwa juu yake yeye. Ila angalau utakuwa umempa heshima yake.
Alikuwa mumeo, akakukuta mjamzito! Kweli mpaka leo umeshindwa
kumwambia! Kwanza naona mimi wala asingeniacha. Siku ile ile hata njiani
kwenda kwetu ningemwambia simama nikueleze. Na nikwambie kabisa, hasira
hizo ni zakuona unazaa na mwanaume wako.”
“Naogopa dada!” “Acha mimi nikuombee
Mina. Ninaye Mungu anayetenda mambo kwa namna ya ajabu sana.
Nilikwambia mume wangu aliniacha?” “Ndiyo.” “Nilimuomba Mungu anirudishie
yule mwanaume mpaka nikachoka. Lakini hakuna siku watoto wangu na mama
yangu wamelala njaa wala sijawahi kukosa pesa ya kuwatunza. Mungu ananijibu
kwa namna ya ajabu mpaka nashangaa. Huyo Kashinde hapo, ananipenda
anatamani kunioa hata leo!” Mina akacheka sana, akajua Andy alipatia.
“Sasa kwa nini hutaki akuoe?” “Mdogo kwangu, halafu
nahisi nimeingiwa hofu. Akinigeuka na yeye! Maana hapa nina
watoto watatu. Akinioa yeye, atataka watoto. Najiona umri umekwenda, na yeye
bado kijana. Nimemwambia atafute mtu mwingine, lakini naona amekazana
tu.” Mina akacheka sana.
“Muone hivyo hivyo Kashinde. Anamaneno huyo, hata mama
anamjua. Ila ananijali sana. Alikuwa akinitumia pesa za matumizi, na alikuwa
kila akija kule kijijini lazima aniletee zawadi. Watoto wangu wote wanamjua.”
“Sasa si muoane tu. Kashinde ametulia.” “Na ametulia kweli, pale
kijijini wanamjua. Ndio vijana wa mwanzoni kabisa pale kijijini kuokoka.
Na alinipenda tokea zamani, mimi nikaona mdogo kwangu kama miaka miwili hivi au
mmoja na miezi. Nikampuuza. Halafu nilikuwa nikiishi Dar yeye yuko huku!
Nikampata huyo tapeli, amenizalisha na kunikimbia. Na wala
usifikiri anaishi mbali. Yupo hapahapa Dodoma mjini.” Mina akabaki akicheka tu.
“Achana na mambo yangu na Kashinde, turudi kwako wewe
ambaye mambo yako yanaeleweka. Nataka tuombe kisha akirudi jioni muombe
akusikilize tu. Mwambie tu. Halafu mwache Mungu ashugulike naye. Fanya
kwa upande wako, uone vile Mungu alivyo wa ajabu. Huwa unakwenda
kanisani?” Hapo napo Mina akamwelezea kwa kifupi juu ya imani zao za dini.
“Kwa hiyo ndio maana unamuona kila jumapili anakwenda
na Ayan kanisani.” “Sasa wewe achana na maombi yakuombewa kama maiti. Anza kumuita huyo Mungu wa mama yako na Ron kaka
yako. Omba mwenyewe mdogo wangu. Ipo raha yake. Unamwambia Mungu kile unachokitaka
wewe na unachojisikia. Ambacho hakuna mtu anakijua isipokuwa wewe. Omba
kwa roho, achana na maombi hayo yaliyoandikwa na mtu mwingine. Roho
Mtakatifu atakusaidia kuomba, ndipo utasikia raha.” Judy akamueleza Mina, mpaka
akajisikia vizuri.
“Kwanza ulishawahi kumpa Yesu maisha yako Mina?”
“Ndiyo. Zamani. Mama alinipeleka. Nikaombewa na nikaokoka. Ila nimejichanganya
hapo katikati wala sitakudanganya.” “Mungu wetu ni warehema wala si kama
sisi wanadamu tunavyo hukumiana. Yeye mwenyewe anaita wenye
dhambi. Anasema atawapumzisha, na wala hatakumbuka dhambi zetu
tena endapo utaungama kwa nia. Omba toba pale ulipomfungulia
shetani mlango, uanze kukulia wokovu tena kwa upya. Soma bibilia na
ujifunze neno.” Akazungumza naye, mwisho akamuombea huyo bosi wake. Mina
akamwambia anajisikia vizuri.
Kwa Andy.
Andy alifanya kama kawaida. Alirudi nyumbani jioni.
Akazungumza kidogo na mtoto wake chumbani kwake, akatoka kwenda mazoezini. Kila
mtu alikwenda chumbani kwake, Mina akakaa chumbani kwake akimsubiria. Kwenye
saa tatu usiku akamsikia amerudi. Akajua lazima aoge kwanza na kula kidogo.
Akampa kama lisaa. Aliposikia mlango wa chumbani kwake unafungwa, akajua
ameingia chumbani kwake. Akasubiri kidogo akijua lazima asafishe meno.
Alijua huwa siku za jumamosi haendi kazini, kwa hiyo
ijumaa huchelewa kulala. Mara nyingine anakuwa tu chumbani kwake akijisomea
vitabu au kuangalia movie. Akaenda kumgongea. “Ni Mina?” “Ndiyo, mimi Mina.”
Akamkaribisha. Akamkuta amekaa kitandani. “Pole na kazi.” “Asante.” Akajibu
huku akimtizama.
“Naomba kuzungumza na wewe.” “Karibu.” “Naweza kukaa
hapo kwenye kochi?” “Karibu.” Akaenda kukaa. Akavuta pumzi kwa nguvu na
kuzishusha. Andy kimya akimtizama.
“Kuna kitu nataka kukwambia Andy. Najua kabisa hakileti
maana au hakieleweki, na ni ngumu kuaminika. Sitashangaa kwa kuwa
hata mimi bado nipo kwenye mshangao. Siamini! Lakini naona nawajibika
kwako. Kilitokea nikiwa bado ni mke wako. Unayo haki yakujua ni nini kilitokea.”
Akamuona Andy anakaa vizuri.
“Unakumbuka mawasiliano ya mwisho karibu unarudi
nyumbani?” Andy kimya. “Maneno yote niliyokuwa nikikwambia?” Andy kimya.
“Nakuhakikishia Andy, nilimaanisha. Sikukudanganya. Nilikuwa na hamu
na wewe mpaka nilikuwa nasikia kuchanganyikiwa! Nilikuwa nikikusubiria
kwa hamu uje uniguse,
lakini siku kama 8 hivi kabla ya kurudi kwako, nikaanza kutapika sana.
Yule msichana tuliyekuwa tukiishi naye,” “Mamu?” Andy akamuuliza.
“Ehe, Mamu. Akaniambia hiyo ni mimba. Sasa kwa
kuwa Mamu ni muongeaji sana, wakati mwingine nilikuwa nikimpuuza tu.
Lakini nikazidi kutapika mpaka siku ile niliyokwambia tunakwenda kwa Paulina,
jumamosi, nilikwenda nikitapika. Nakumbuka mpaka nikamwambia baba, mzee
Ruhinda. Wengine wakisikiliza. Nikamwambia baba, natapika kama mjamzito wakati hata mimba ya Ayan haikunisumbua! Baba
akaniuliza, umekwenda hospitalini? Mbele ya watu, mimi najibu, sikuwa hata na wazo
kama ni mimba. Nikamwambia nilifikiri ni ugonjwa, lakini nashangaa
natapika tu ila sina homa. Paul akadakia kuwa, lazima kwenda hospitalini ili
nikajue.” Mina akaendelea.
“Baba naye akanisisitiza nisizembee, nikamuone
daktari. Nikakubaliana nao nikiwaambia basi nitafanya hivyo ili Andy wangu akija, anikute mzima. Sasa nikawa nimemuomba
Paulina chakula ili nimlishe Ayan. Nikamwambia sijampikia Ayan muda
mrefu, na pale nyumbani nimekataa kusipikwe sababu ya harufu inanishinda
natapika. Nikamwambia...” “Hayo ni wewe ndio unamwambia Paulina?” Andy
akauliza.
“Nilikuwa nikizungumza na baba pale sebuleni kwa
Paulina, ila wote walikuwepo nafikiri waliweza kutusikia
mazungumzo yetu na baba, na ndio maana wengine wakaweza kuniuliza na kunishauri
kwenda hospitalini. Maana nilikuwa nimekaa sebuleni na baba, Paul, na Pius
wengine jikoni na watoto upande wa kulia chakula. Tena nilifika tu, kisha
nikatoka kwenda tena kutapika. Nikarudi moja kwa moja nikaenda kukaa mbele ya
baba nikawa nimeinama huku nikizungumza naye au nao.”
“Maana nilikuwa nimechoka Andy, sina jinsi
nikaeleza ukanielewa. Nilikuwa natapika, halafu sielewi na wala siamini
kama ni mimba kwa kuwa wewe ndio mtu wa mwisho kufanya naye mapenzi! Na
nilishapata siku zangu
kama mara tatu hivi tokea uondoke. Kwa hiyo wazo la mimba sikuwa nalo
kabisa.”
“Basi, wakati nimekaa pale ndio nikamuomba Paulina
chakula nimpe Ayan. Nikamwambia namuhurumia Ayan wangu kwa kuwa kwa siku
5 mfululizo nimekuwa nikimpa uji na maziwa tu, sababu ya mimi kutapika na
harufu zinanishinda sitaki nyumbani kupikwe kitu chochote.” “Subiri
kwanza Mina. Hayo unazungumza mbele ya kila mtu!?” “Ndiyo Andy! Mimi
sikujua kama ni mimba! Nikajua nimepatwa na tatizo baya. Halafu
kwa kuwa Mamu alishanitisha kuwa kwa kina Raza ni washirikina
sana na Raza hanipendi mimi na Ayan, Mamu aliniambia alishamsikia
akisema huyu Ayan hataishi. Nikwambie ukweli Andy, mpaka nikahisi Raza ameniloga.”
“Nini kilitokea?” Andy akataka aendelee.
“Basi. Nikawa sasa nasimama kufuata chakula jikoni
wakati kina Paulina wanamalizia kupika vitu vingine, ili nimlishe Ayan, maana
nilijua atakuwa anahamu tu na chakula. Ile nimeingia tu jikoni kwa Paulina,
hali ya kichefuchefu ikanipata. Nusu nitapikie pale jikoni! Nikakimbilia
bafuni. Nikatapika wee, ndio nikatoka nikakuta kila mtu ameduaa.”
“Lakini nikamkuta mama akinisubiri nje ya choo.
Akanipa pole, mimi nikamwambia mama ni tatizo lililonipata. Nikamwaambia
sina raha! Natapika kila wakati! Si ndio Paulina akasema anisindikize
hospitalini? Nikakubali kwa haraka na kushukuru kuwa ananisindikiza
hospitalini, nikiwa na uhakika baba yupo pale, Ayan wangu atakuwa salama. Maana
nilikuwa naogopa kumuacha na Mamu tu. Sababu ya maneno yake na ukaribu wake na Raza, nikawa najiambia asije Raza akamtuma amdhuru
mwanangu bure?”
“Ilifikia hapo!?” “Ni vile baba na mama hawataki
ugomvi, lakini kila mtu anajua kama Paulina na Raza hawampendi Ayan.
Hata Pius alikuwa akiniambia nisiwe nampeleka mtoto pale kwao labda yeye
awepo. Na kuna kipindi baba akaacha kusafiri akawaambia wote, yeye ndio
atakuwa akikaa na Ayan kama mimi ninadharula. Akasema hataki
kumuona Ayan kwenye nyumba ya mtu yeyote. Popote alipo, apigiwe simu, atarudi
kuwa na Ayan. Lakini sasa wewe unajua majukumu ya baba na mama, wakati mwingine
walikuwa inabidi wasafiri.”
“Nikawa namuomba Ron. Ron ndio akawa kimbilio
langu kubwa kama mzee Ruhinda na mama hawapo. Tena mzee Ruhinda alikuwa
akimchukua na kuwa naye ofisini kwake kabisa. Ayan alikuwa ananiambia anaingia
naye kwenye mikutano, anampa nafasi asalimie.” Andy akapoa, akijisuta yeye
baba mtu alishindwa vipi!
“Basi, ndio Paulina akanisindikiza hospitalini.
Baada ya vipimo ndio daktari akathibitisha ni mjamzito. Jamani Paulina alinipiga,
pale ndipo nilijua dada yako ananichukia Andy. Kuna muda alinisukuma
kwa nguvu mpaka nikaanguka sakafuni. Halafu mbele ya watu! Mara nyingine
akanisukuma nikajigonga hapa.” Mina akamuonyesha. Andy akamsogelea na
kuangalia. “Pole.” “Asante. Lakini nilikuwa na mshituko Andy, natetemeka
kwa hofu sijui ni nini kinanitokea!”
“Kwani wewe ulikuwa ukienda kusoma na wenzio?” “Na
mwanangu je? Nilikuja kushindwa. Sikuweza kwenda tena kwenye kusoma na
wenzangu sababu ya mtoto! Unamuacha mahali, unaomba kwa masaa machache tu.
Ilikuwa lazima niwe muungwana, niwahi kurudi kumchukua mtoto wangu.
Sikutaka baba alemewe halafu amchoke japo siku za jumamosi wakati
mwingine alikuwa akija kumchukua asubuhi ili nipate muda wakufanya mambo yangu
mwenyewe, lakini Andy, nilikuwa siwezi kutoka sababu ya ubusy wa shule na kazi za pale.”
“Na unamjua Ayan nikiwa naye, anataka nilale naye
kabisa. Aninuse mpaka aridhike yeye. Kwa hiyo ilikuwa ikitokea babu yake
anakuja kumchukua, nilikuwa nasafisha nyumba sasa, au kukimbilia saluni au
kufanya manunuzi. Marafiki walikuwa kwa simu tu. Lakini si kuonana.”
Andy akanyamza.
“Najua hutanielewa Andy, lakini Mungu wangu
atakuja kuyathibitisha haya siku moja. Sikukusaliti Andy. Ila sijui
kilichotokea kwenye huu ujauzito! Hata baba wa huyu mtoto mimi simjui,
Andy. Na Mungu wangu ni shahidi. Natamani ningekuwa na maelezo mengi yakueleweka,
lakini sina Andy. Ndio hivyo tu.” Andy akabaki akifikiria.
“Unauhakika hakuna hata kijana uliyewahi
kumfungulia mlango pale nyumbani?” “Najua hutaniamini Andy, kutokana na
historia yangu ya nyuma ya uchafu. Lakini akili yangu ilijaa Ayan
tu. Nilikuwa nikimuhurumia vile alivyokuwa akikataliwa na kunyanyaswa
kwenye majumba ya watu. Nikakusudia kila wakati, kuwa naye mimi mwenyewe
mpaka ilazimu sana. Sikuwa hata na wazo la mwanaume. Mbali na
ndugu zako kuingia pale ndani, labda na Ron, hakuna mwanaume mwingine
alikuwa akiingia.”
“Namaanisha
labda ulimkaribisha kwa wema tu, akakulevya hata kukuwekea
kidonge kwenye maji! Akakufanyia ubaya, akaondoka wewe usijue.” “Hapana Andy!
Mtu anifanye mapenzi, Ayan na Mamu wangekuwa wapi? Halafu wewe hujamjua
Mamu. Hawezi kunyamazia jambo. Angeshasema kama nilishawahi
kuingiza wanaume pale ndani.”
“Mbona amesema kuna siku ulikuwa ukimtuma
mbali akale chakula na hutaki arudi nyumbani?” Mina akashangaa sana.
“Andy wewe! Ndivyo alivyokwambia Mamu?” “Ndivyo alivyowaambia watu.” “Muongo.
Naomba fikiria na mimi bila hasira.” Mina akakaa sawa.
“Mamu alikuja kuishi na sisi, muda wakulingana
na ule ujauzito ulipogundulika. Nisikilize vizuri. Mimba inaanza kunisumbua,
ina mwezi mmoja, sawa sawa na siku alizokaa Mamu. Nikaanza kutapika
mwishoni nilipogundulika. Siku kama 5 kabla nikiwa naye nyumbani ndipo nikaanza
kutapika nikawa sitaki kupika kabisa. Ndio nikawa namtuma akanunue
chakula nje. Na sikutaka yeye ndio awe anapika kitu chochote mle ndani kuhofia
asije akaniwekea mambo ya ajabu ya uchawi.”
“Kwa hiyo nikawa sitaki apike kabisa. Na sikuwa
naweza harufu ya chakula chochote ndio maana nilikuwa nikimwambia akajinunulie
chakula chake na ale huko huko. Hiyo yakumwambia akanunue chakula ilianza
wakati nimeshaanza kutapika, yaani mimba ishakuwa na mwezi. Sasa huyo mwanaume
nilikuwa nikimuingiza hapo akanipa mimba ipi na tayari nilishakuwa
mjamzito?” Andy akaona ni kweli. Akabaki akifikiria.
“Halafu Andy, ukumbuke hapo na Ayan alikuwepo.
Kweli unafikiri Andy mimi naweza kulala na mwanaume mwingine pale ndani,
mwanangu akinisubiri sebuleni?” Hapo Andy na yeye akaona hapana.
“Kweli haieleweki!” “Sasa mimi nikadhani labda
ndio Raza ameniloga, ili nidhaniwe nina mimba. Yaani hata
huku kutapika na tumbo kuendelea kuwa kubwa nikawa nahisi ni uchawi tu,
humu ndani hakuna mtoto. Sasa mtoto alipoanza kucheza ndipo nikaanza kuamini
kidogo. Mwishoe nikaona ni heri nijiridhishe tu kuwa ni mtoto kweli aliyekuwepo
tumboni si mazingaombwe.”
“Ndipo nikaomba nionyeshwe kabisa kwenye ultrasound. Mpaka yule mtu aliyekuwa akinifanyia Ultrasound
alikuwa akinishangaa wakati akinifanyia hiyo ultrasound kwa maswali na kwamba anithibitishie kama huyu
mtoto tumboni ni kama watoto wengine ambao anawaonaga kwenye matumbo ya kina
mama wengine! Akanithibitishia huyu mtoto ni mtoto kabisa na ni mkamilifu,
ndipo nikaanza kumnunulia vitu sasa.” “Umejua jinsia?” Andy akauliza.
“Hilo ndilo sikutaka kujua.” “Kwa nini?” “Sijui Andy!
Labda ni vile kwenu au watu walionizunguka walivyokuwa na matatizo juu
ya jinsia! Nimemzaa Ayan, mtoto wa kiume, badala kuwa ni baraka,
wamegeuza kuwa tatizo! Nimeona hilo libaki kitendawili mpaka siku yakujifungua ndipo nitajua.” Andy kimya.
“Ni hivyo tu
Andy. Acha nikuache upumzike. Na pole, nimekwambia muda mbaya labda utashindwa
kulala, lakini nimeona nikwambie tu.” “Leo umejibu mambo mengi
sana. Kuna vitu niliambiwa, ndio leo kidogo vinajijibu.” “Sasa umejuaje
kama katika hili sijakudanganya?!” “Kumbuka nimeishi na wewe kama mke
wangu Mina. Nakufahamu sana. Na nimesoma saikolojia. Najua mtu
anapoongea uongo. Na nimefurahi umeniambia. Nilikuwa nikiteseka,
nakaribia kuchanganyikiwa.” “Pole Andy.” Andy akabaki akifikiria.
“Kuna kitu hakijakaa sawa Mina.
Tafadhali pata muda wa kufikiria.” “Itabidi. Nilikuwa naogopa kufikiria
sana kama alivyonishauri Pius ili nisijipe ugonjwa wa moyo.” “Sijaelewa.”
“Hapana, si kitu. Ni Pius tu alinitia moyo kuwa katika kipindi hiki niangalie
swala la mtoto tu, nisifikirie hayo mengine kama itakuaje hatima
ya mtoto au imekuaje.” Andy akashangaa sana.
“Hayo Pius alikwambia lini!?” “Uliponifukuza
kwako Andy.” Mina akajibu kwa wasiwasi kidogo. “Kwani uliendelea kuwasiliana na
Pius?!” “Ndiyo. Alinisaidia hata kunichukua na kunipeleka hospitalini. Unakumbuka
wewe ulinifukuza kwako, ukanirudisha kwa mama. Mama naye kesho yake
asubuhi akanifukuza kwake, tena baada ya kuniambia maneno machungu
kweli!”
“Nikawa sina pakwenda, natapika tu. Nikatafuta
hoteli, ndipo Pius akanitafuta tena. Nikamwambia nipo hotelini, hali yangu sio
nzuri. Wewe umeniacha na mama amenifukuza. Ndipo akaja pale
hotelini, kweli akanikuta sina hata nguvu, nina hali mbaya! Akanisaidia
na kunipeleka hospitalini. Pius amekuwa msaada sana kwangu na
Ayan. Alikuwa hachoki! Hata wengine walipokuwa wamenitenga,
alikuwa akinisaidia bila kuhesabu.” Mina akaendelea kumwaga sifa za shemeji
yake, Andy akimsikiliza tu kwa makini sana.
Mina akaendelea asijue anaibua mengi ndani ya
Andy. “Pius anajali Andy! Anajali sana. Katika ndugu zako wote,
angalau Pius ndio hata baba alikuwa akimwamini akimtuma atupe msaada,
atafanya kwa moyo na haraka.”
“Baada ya wewe kuniacha, ukanitoa kwako bila
hata pesa ukawa umeniandikisha kuwa nimekubali kuondoka kwako na kuanza
maisha yangu, nilijua kabisa ni njia ya kunibana ili nisipate kitu
Andy. Nilielewa. Ila nikaondoka nikijiambia Mungu atanisaidia tu.”
“Sasa kipindi hicho sina kitu na sina watu,
na hata wakati umenioa lakini upo busy na kazi, alinisaidia sana mimi na Ayan.
Katika uzima na maradhi, bila kuchoka. Alikuwa akisikia Ayan anaumwa
tu, au mimi, anaacha shuguli zake, anakuja kutusaidia. Mchana na usiku
huku akinitia moyo. Alihangaika na mimi bila kuchoka. Nakiri
kabisa, bila yeye, nisingekuwa hapa nilipo.” Andy kimya. Mina
akaaga na kuondoka, Andy kimya.
Andy Asaka Ukweli.
Kwa Paul.
Alikaa hapo akifikiria. Akaangalia muda wa alipo Paul
mdogo wake nchini India, akagundua kwao palisha pambazuka. Akampigia. Baada ya
salamu, Andy akaenda moja kwa moja kwenye swali. “Uliponiambia
niongeze umakini na nifungue macho, ulimaanisha nini?” “Mpaka leo bado hujatoka
hapo Andy!” Paul akashangaa sana. “Kwa maana
nyingine mambo ya familia yamekushinda kabisa Andy! Au nikuulize Andy,
wewe umejiapia hizo juhudi zako ni za kazini tu, mengine unaachana nayo?”
Paul akauliza kwa hasira na kushangaa sana mpaka Andy akawa anamsikia kwenye
sauti yake.
Kwa kuwa alikuwa amekasirika, na alishapandisha jazba
Andy akajua ataongea tu. “Wewe unamuacha mtoto
kama Mina yule, pale jijini, anatunzwa na wengine! Mimi mwenyewe
nilikuwa nikimtamani huyo mkeo ila tu kwa kuwa ni shemeji, nikaamua
kukaa naye mbali. Hata alipokuwa akilia shida, ilikuwa ni afadhali
nikamtoe mama kazini, niende naye nikamwangalie wakati mgonjwa ili nisije shawishika,
nikashindwa kujizuia. Wewe uliamini vipi watu kwa mwanamke kama Mina?”
Paul akamleta karibu.
“Yule mtoto ni mjamzito hata hajui!
Yaani anamwambia baba yake mkwe dalili zote za mimba, yeye mwenyewe HAJUI
kama ni mimba! Kila mtu akabaki ameduaa. Anajieleza hana habari! Lakini
mimi nikajiuliza pale na baadaye, hata mama nikamwambia. Huyu Mina kama
angekuwa amelala na mwanaume nje, angeficha. Ni kama na yeye ule
ujauzito alikuwa haujui!”
“Nikamwambia mama, atulie, asiende kasi.
Mama na baba ni watu wazima Andy. Ndio maana unaona linapokuja swala la Mina, wananyamaza
kimya kabisa. Jiulize kwa nini ni kwa Mina tu, sio Raza au tuseme Devi?” Kimya. Akaona ajijibu
mwenyewe. “Ni kwa kuwa wameishi
na hao wakwe zao wote watatu, wanawajua. Linapofika swala la Mina, baba anapoa
kabisa. Ameusoma moyo wa mkeo au aliyekuwa mkeo, wameshamjua.” Paul akaendelea.
“Siku ile Paulina aliporudi nakusema amemfungia
Mina kwa kuwa amemkuta ni mjamzito, na vile baba anavyompenda Paulina na
kumuunga mkono katika kila kitu, lakini siku ile baba hakuongea
neno hata moja! Akasimama na kuondoka kabisa. Unafikiri ni kwa nini?” Kimya.
“Mkeo yule muwazi Andy! Anasomeka kama kitabu cha kiswahili kwa wazawa na
akiongea jambo hafichi. Kama hujamjua, basi wenzako wote wanajua.
Hata mama alishasema. Mina sio muongo na wala si mnafiki. Hajui
kuficha jambo lolote. Natamani ungekuwepo siku akielezea jinsi anavyojisikia!
Ungejua hata yeye hajui kitu. Tena anamweleza baba! Yaani baba yake
mkwe, sisi tukimsikiliza.” Paul
akaendelea kwa jazba.
“Wenzako wote pale wana watoto wa kike. Hilo
moja. Unajua wazi Raza na Paulina hilo linawakera kuona Mina amefika tu
na kuzaa mtoto wa kiume ambaye baba anamtambua kama Ruhinda wake, MRITHI!
Mama alimlaumu sana baba, akamwambia anaanzisha chuki kati yao. Lakini
baba akasema, hata asiposema, ni kweli. Ayan ndiye atabaki akibeba jina
la Ruhinda miaka 50 ijayo ambapo wengi wetu hatutakuwepo. Hilo ni
jingine.” Paul akaendelea.
“Wewe unajua kabisa Paulina ndiye kipenzi
cha baba. Paulina hajui upendo mkubwa wa mtu mwingine isipokuwa wa baba.
Leo unamuacha Mina anaingilia mapenzi yake! Baba amehamisha
kujali kwa Paulina, anampenda Mina na mtoto wake! Baba, namaanisha
mzee Ruhinda vile alivyo, niwakuacha mikutano nje ya nchi sababu yakukaa
na Ayan! Hajawahi kumfanyia hivyo hata mtoto wake wa kumzaa mwenyewe,
leo anakaa ofisini kwake na kuzunguka na Ayan! Anampiga picha Ayan amekaa
kwenye kiti chake ofisini na kuitundika nyumbani kwake, sebuleni!”
“Fikiria Andy. Baba ndio anakwenda
kuchapisha picha studio! Tena kwa mjukuu mmoja tu, aliyekuja juzi tu
hapa wakati baba alishakuwa na wajukuu wengine wanne! Mzee Ruhinda anatangaza
hataki kumuona Ayan kwenye nyumba ya mtu mwingine yeyote isipokuwa pale
kwake Msasani! Anayemtaka Ayan, amfuate pale kwake! Hayo anawaambia watu, na
yeye wakati mwingine anatoka kazini siku za kazi, anakuja kukaa naye pale
nyumbani kwako ili mkeo aende shule! Kweli Andy?”
“Wewe unafikiri watu wengine, au wazazi wa
watoto wengine, zaidi mama zao, vile unavyowajua wale wanawake wawili
walivyo wakorofi, watakuwa na mahusiano gani na mkeo unayemuacha
peke yake mchana na usiku?” Andy kimya.
“Sijui bwana Andy! Labda kwa kuwa mimi
sijaoa sijui mambo ya ndoa, lakini acha nikwambie ukweli Andy, umecheza
sana chini ya kiwango. Ni kama uliyemtupa mbuzi wako aliyenona, katikati ya
simba. Unanunua alumasi, unakwenda kumvalisha nguruwe! Halafu
unamkabidhi huyo nguruwe mwenye alumasi kwa mwenye bucha! Unafikiri
watamfanyaje huyo nguruwe kama si kumchinja na kuficha hiyo alumasi?” Paul akazungumza naye kwa mafumbo, lakini Andy akawa
ameelewa.
“Yaani wewe Andy, Paulina! Yaani Lina ndio
anakupa muongozo WAKUMUACHA Mina, mwanamke ambaye hajawahi hata kumkubali
kwenye ile familia! Yeye ndio unakubali akusaidie kumuacha mkeo! Kweli
Andy?! Hata kama ni kuamini watu, Paulina! Yeye mwenyewe ndoa yake unaijua.
Ni vile tu amepata mwanaume muungwana. Tokea lini yeye akawa anajua
mambo ya ndoa? Kutwa yupo ofisini na safarini. Nyumba yake chafu. Tukienda
kwake mama yake anatangulia kwenda kumsaidia kusafisha kwanza ili wageni
ndio twende na kuweza hata kukaa, na hilo kila mtu analijua. Hajiwezi
kwenye mambo ya nyumbani isipokuwa kazini tu. Leo ndio na wewe unamsikiliza!
Au na wewe upo kama yeye! KAZI kwanza mambo ya familia baadaye?” Paul hakumuacha.
“Kuna kipindi mimi mpaka nikajiuliza ni kwa
nini ulioa kama haupo tayari kutulia na familia, Andy?! Amebaki
Pius anayejua ku balance mambo yake mengi na mazito, anazungukia nyumba zenu
pia wakati nyinyi akili zenu mmeweka sehemu moja tu! Akiitwa Paulina shuleni
kwa watoto wake, anampigia simu baba, baba anamtupa Pius. Mtu mkubwa na mzito mwenye madaraka mazito kuliko sisi
wote! Eti ndio akaweke sawa mambo ya watoto wa Paulina shuleni, eti yeye
Paulina anavikao vya muhimu!”
“Na mkeo naye akiumwa, au mtoto wako,
Pius huyohuyo ndio aache majukumu yake, akahangaike na
mkeo na mtoto wako kuwakimbiza hospitalini, kuwapa dawa na ahakikishe kuna
chakula kwenye majumba yenu! Nyinyi mnahangaika na viofisi vinavyowalipa mshahara kama
marupurupu ya Pius tu! Sasa wewe jiulize Pius anawezaje, halafu wewe na
Paulina mnashindwa vipi!”
“Ushamsikia Raza akimlalamikia mumewe
au anahangaika na familia yake? Maneno yote yale ya Raza na gubu lake, likifika swala la Pius anafunga
mdomo kabisa, kwa jinsi Pius alivyoweza kuweka sawa nyumba yake! Watoto
wa Pius wenyewe umeona jinsi wanavyompenda baba yao kuliko mama yao!
Siku zote hutawasikia wakimlalamikia baba yao ila mama yao.”
“Mwanao mwenyewe ana mahusiano mazuri
na Pius kuliko hata wewe baba mtu! Ndio ujue unakosea pakubwa sana Andy.
Haya ninayokwambia hapa, si mama wala baba wanaweza kukwambia, ila mimi
nakwambia, fungua MACHO, kama bado kujachelewa. Maana unaweza
kukuta sasa hivi kuna amani usione mengi, kwa kuwa TATIZO lao, Mina,
ameondoka. Amewapisha kwenye maisha yao. Sasa wewe si mtu mzima? Kaa
chini na utafakari kwa makini sana. Jiulize na kuhesabu nani ANAYE NUFAIKA sasa hivi na kushindwa kwako kumtunza msichana kama
Mina? Kushindwa kwako wewe, ujue kuna anayenufaika sasa hivi.
Nani na kivipi? Akili kichwani kaka. Kwa heri. ” Paul akakata simu, akamuacha Andy usingizi umepaa.
~~~~~~~~~~~~~~
Kushindwa kwake Andy, kuna anayenufaika. Nani na kivipi? Swali ameachiwa na
mdogo wake. Dr. Ruhinda.
Inaendelea….
0 Comments:
Post a Comment