Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 32. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 32.

Huku kwa Mina nako alikokuwa akiendelea kulea muujiza wake aliorudishiwa. AYAN. Alipomuona anasuasua kumalizia uji, akaona amsaidie tu kumalizia. Akamnywesha mpaka akamaliza. “Umeshiba?” Akamuuliza mwanae wakati akimfuta mdomo. “Naomba maziwa kidogo.” “Hivi unapata maziwa yakutosha hapa?” Andy akaingilia mazungumzo ya Mina na mwanae kwa kuuliza swali.

“Yapo mengi. Wananiletea kutokana na ninavyohitaji. Tena wakati mwingine akikosa wateja, ananipunguzia bei ili nichukue mengi. Kwa hiyo nagandisha kwenye friji, nakuwa nampashia tu huyu. Kwa hiyo maziwa yapo.” Mina akamuwekea mtoto wake maziwa, akachukua ile chupa na kwenda kujilaza kitandani kwa mama yake.

“Njoo mama.” Ayan akamuita mama yake. Mina akaenda, akajilaza kwenye mto ili mwanae aweze kumnusa huku anakunywa hayo maziwa. Na kweli akamsogelea mama yake akaanza kumnusa huku anavuta maziwa yake. Andy na Mina wakacheka. “Ujue umekuwa mkubwa wewe Ayan!” Ayan akacheka na chupa mdomoni. Akatulia.

~~~~~~~~~~~~~~

“Ile nyumba ni kubwa kama ile tuliyokuwa tukijenga Kigamboni.” “Hivi ulimaliza? Maana nakumbuka ilibaki kidogo tu kuisha.” “Ni kama imeisha. Bado kidogo sana. Nilihamisha nguvu kwenye hii ya Dodoma. Kuna vitu sikuvipenda nilipo inunua. Nikabomoa na kurekebisha. Ilivyo sasa hivi ni afadhali kwa kuwa haikuwa ramani yangu, sio mbaya.” “Hongera Andy, unajitahidi sana.” Andy akatulia kidogo.

Kisha akaendelea. “Nilichotaka kusema ni hivi, pale unaweza kabisa kupata sehemu ya kuishi.” Mina akawa kama amepigwa na butwaa. “Hata kama tutakuwa na msichana wa kazi, bado utapata nafasi yako tulivu bila shida.” Mina kimya akishindwa ajibu nini.

 “Kama unahofia uhuru wako, pia hakuna atakayekubana, ila nisingependa kumuona mwenzio pale. Hilo sitaruhusu. Ila kama ni wewe tu, haitakuwa na shida.” Andy akaweka msisitizo kwa jazba kidogo baada ya kuona Mina hajibu, akijua anamkatalia.

“Au unaweza kupaacha hapa ikawa ni sehemu yenu yakukutania. Ukitaka, unaweza kuishi kule na sisi, na ukawa ukirudi hapa.” Mina akaumia sana. “Sina maisha mengine ninayoishi zaidi ya haya Andy. Hivi unavyoniona ninaishi hapa na Ayan ndio hivyo hivyo. Hakuna mwanaume anayeingia hapa mchana wala usiku. Ni wewe tu ndiye mwanaume pekee unayeingia hapa nakulala. Na sikudanganyi. Hakuna anayepajua hapa isipokuwa wewe na Ayan. Hata Ron pia hajui nilipo.” “Basi kama kinachokuweka hapa ni unafuu wa maisha, twende ukaishi na sisi Dodoma.” Mina akatulia tena.

“Au mpaka ushauriane na mwenzio?” Andy akaanza tena. “Hakuna mwenzangu Andy! Nipo kama hivi. Lakini nafikiria sasa hivi nipo peke yangu. Baada ya muda nitajifungua, itakuaje na mtoto?” “Mimi na wewe tulikuwa na mipango ya miaka na miaka. Nilikupigia simu siku ile jumamosi asubuhi, tulikuwa na mipango ya kwenda mapumzikoni mara nitakaporudi nchini. Ilifanikiwa?” Mina kimya.

“Sidhani kama sisi mipango ya baadaye imetusaidia sana. Kinachowezekana sasa hivi, naona tukifanye tu. Baadaye itakuja na itajijibu.” “Sawa.” Mina akakubali akijua Andy anakaribia kupandisha hasira. “Kwa hiyo umekubali kuhamia Dodoma na sisi?” “Ndiyo, lakini nafikiri nitawafuata baadaye.” “Mpaka uage kwanza?!” Andy akauliza kwa hasira.

“Sina mtu ninayewasiliana naye isipokuwa wewe Andy! Ila nina kliniki siku ya jumatano ijayo. Kuna jinsi najisikia, nataka nikienda kliniki nimuulize daktari.” “Nani amekwambia Dodoma hakuna madaktari na huwezi kuanza kliniki huko?” Andy akauliza tena.

“Unakumbuka ulinifukuza kwako nikiwa natapika sana? Sasa huyu daktari nilianza naye muda mrefu, naona kama ananipatia Andy! Ananisaidia sana. Nilikonda kupita kiasi, wakasema sio vizuri mimba inakuwa, halafu mimi napunguza uzito na si kuongezeka. Ndio akanipa dawa na ushauri ambao nimeona unanisaidia. Nataka niende angalau nizungumze naye na nimwambie hivi ninavyojisikia. Wanipime, anishauri dawa na ndipo nimwambie kuwa ninahama, halafu nimuombe kama anaweza kunihamishia kwa daktari mwingine mzuri kama yeye huko Dodoma.” Kimya.

“Umenielewa Andy?” Mina akauliza taratibu. “Sasa kama unaumwa sasa hivi, kwa nini tusiende kwa daktari tukajua kama kuna tatizo au la! Kuliko kusubiri mpaka jumatano ijayo!?” “Nahisi pia inaweza ikawa sio tatizo kubwa labda mabadiliko tu ya mwili.” “Wewe acha daktari akatuambie huko huko.” “Na kliniki?” Andy akasimama kwa hasira. “Mbona kama unaweka vipingamizi tu!?” Akagomba, Ayan akashituka. Akatoa shingo kwa mama yake akamwangalia baba yake. 

“Naomba ukae Andy, usikasirike.” “Naona kama huoni ushauri wangu ni wa maana! Huoni kama upo umuhimu wa wazo langu! Unang’ang’ania daktari mmoja tu! Kwani ndiye huyo huyo aliyekuzalisha Ayan? Mbona Ayan alizaliwa vizuri tu na daktari hakuwa huyo? Au kuna kitu kingine ambacho mimi sikifahamu?” “Unataka tuondoke hapa lini?” Mina akaona ayafanye yaishe.

“Hata leo.” Mina akashangaa. “Usiku huu!” “Ndio maana nimekuuliza unataka kumuaga nani?” “Naomba ukae Andy. Najua unahasira, na mimi sikulaumu. Lakini naomba utulie tuzungumze.” Andy akabaki amesimama kwa muda, kisha akarudi kukaa.

“Kwa kuwa nitakuwa Dodoma kwa muda. Pengine mpaka muda wa kujifungua ukifika ndipo nitakapo rudi huku kuja kujifungua, na pengine nitakaa kidogo mpaka mtoto aelewe muda wake wa kulala. Ili usiku asijekuwa usumbufu kwa wengine. Kwa hiyo nilazima hapa niache mazingira mazuri yakueleweka.” Mina akaendelea.

“Naomba tufanye hivi. Nipe siku ya kesho ya kumuweka sawa huyu mama, nimwambie nitakuwa nikirudi hapa, asije akaingiwa tamaa, akapakodisha kwa mtu mwingine ili ajipatie pesa. Halafu nimtafute na daktari wangu. Nizungumze naye kuwa nitaondoka, lakini karibu na kujifungua nitarudi kwake. Kisha niwafuate Dodoma baada ya kuweka mambo yangu sawa. Na sitachelewa.”

“Na kingine, naomba usiwe unasafiri usiku Andy! Humo barabarani unakutana na madereva wengine usiku wamelewa au kuchoka. Wanaweza kukusababishia ajali. Kama unafanya safari zakuendesha mwenyewe, naomba iwe mchana Andy. Ni sawa?” Kimya. Mina akajua anataka kufikiria. Akaona anyamaze.

“Mama! Njoo nikwambie.” Ayan akamuita taratibu, Andy akimsikia. Mina akamgeukia. “Mwambie dad wewe unataka kukaa na mimi tu. Tubaki wote, asinichukue.” Mina akamuhurumia.  “Hata hivyo mimi nataka niwe na wewe Ayan. Ila lazima nitibiwe mwanangu, halafu nitakufuata.” “Kwa nini usitibiwe hapa na mimi? Mimi nitakuwa nakupa maji ya kunywa.” Mina akamuhurumia sana Ayan mpaka akaanza kulia. Akajua anaogopa labda baba yake atakwenda kumuacha kwa ndugu.

“Naomba twende hospitalini sasa hivi Mina. Najua hospitali nzuri tu hapa. Twende ukapimwe kila kitu kwanza, tujue unatatizo gani.” Mina hakubisha. “Nashukuru Andy. Asante.” “Karibu.” Akajibu ila safari hii akisikika ametulia sio kwa hasira tena. “Unaenda na mimi, mama?” “Nakwenda kuvaa, nakuja sasa hivi Ayan. Nisubiri.” “Nakusubiria mama. Usiniache. Twende wote.” “Mama anakuja Ayan. Njoo nikubadilishe uvae nguo nzito kidogo. Kuna baridi nje.” Ayan akashuka kitandani kwenda kwa baba yake, na Mina akaenda kujiandaa.

~~~~~~~~~~~~~~

Walifika hospitalini, wakaingia wote kwa daktari. Kwa kuwa alikuwa daktari mgeni, ikabidi Mina ajieleze na aina ya dawa alizopewa atumie na vile anavyojisikia kwa wakati ule. Akaandikiwa vipimo, wakatoka. Alipokuwa anakwenda kutolewa damu, akafanya makusudi kumpa Andy simu yake amshikie. Haikuwa na namba ya siri, kwa hiyo alijua Andy ataweza kuingia popote na kujiridhisha kuwa hana mwanaume mwingine.

Akaondoka nakumuacha Andy na Ayan wakimsubiria. Bila kupoteza muda Andy akaanza kupekuwa simu ya Mina. Akaingia kulia na kushoto. Juu chini, akakuta namba za watu wote na wengine anao wafahamu hata yeye, lakini akakuta jumbe zake tu. Hilo likamtuliza kidogo.

Huwezi ukaishi na Mina kama mpenzi ukamkinahi huyoo mtoto! Hapendi ugomvi, amejawa upendo na kujali kwa aina yake. Andy alishakuwa na hamu naye, ila wivu wa mume mwenzie ndio ulikuwa ukimsumbua akidhani mwenzie anafaidi kuliko yeye. Akaona ambane mpaka arudi naye Dodoma.

“Pole.” Mina alitoka amejishikilia damu isitoke sehemu aliyotolewa damu. “Pole mama.” Ayan naye akaiga na kusimama akimfuata mama yake. “Asante. Wamenitoa damu nyingi!” Mina akakaa na mwanae akamuegemea. “Ndio vizuri tujue tatizo ni nini.” Ayan akambusu mama yake kama kumkumbushia na yeye yupo. Mina akamwangalia na kumshika vizuri.

“Nimekuta namba ya daktari wako humu kwenye simu yako, nimejaribu kuwapigia, inaonekana hata kesho anakuwa na kliniki sehemu nyingine. Tunaweza kwenda huko ukazungumze naye kabla hatujaondoka.” “Sawa.” Mina akakubali bila swali lakini akacheka moyoni akajua Andy amepekua simu yake vilivyo. 

Vipimo vilionyesha hana ugonjwa wowote. Akashauriwa apate muda wa mapumziko tu na anywe maji yakutosha. Andy akalipia hapo, wakaondoka kurudi nyumbani kwa Mina. Njiani Mina akaona ashukuru. “Nashukuru Andy. Asante. Angalau sasa hivi nitakuwa sina hofu ya ugonjwa.” “Karibu. Naomba jaribu kuwasiliana na mwenye nyumba wako. Bado nimapema. Kama bado hajalala, ukazungumze naye.” Mina akabaki akijifikiria.

Andy akamgeukia. Akajua ataanza kugomba tena. “Kwani kesho unataka tuondoke saa ngapi?” Ikabidi tu aulize. “Mapema tu. Tukitoka kwenda kukutana na huyo daktari wako, haturudi tena hapa, tunaelekea Dodoma, ili nisiwe naendesha usiku.” Mina akacheka na kuinama, maana Andy aliongea akimnukuu yeye.

“Au kuna mtu mwingine nilazima umuage?” “Hapana. Naomba simu nimpigie huyo mama.” Andy akamtolea simu yake mfukoni, maana alibaki nayo tokea alipomuachia kule hospitalini, akamkabidhi. Mina akazungumza na huyo mama, akamkaribisha nyumbani kwake.

Andy alimshusha nyumba ya mbele, akaingia kwenda kuzungumza na huyo mama. Alikuwa muungwana, wala hakuhitaji maelezo mengi akawa amemuelewa kabisa. Hapakuwa na shida. Ila Mina alimwambia atakuwa akirudi mara kwa mara mpaka muda wa kujifungua ufike. Wakakubaliana na akamruhusu aondoke na funguo zake ila akamuomba amuachie moja ili kukitokea chochote cha hatari humo ndani kwake akiwa hayupo, basi aweze kuingia na kusaidia. Hilo halikuwa na tatizo, akamuahidi kumpa kabla  hajaondoka.

Andy arudi na Mina Dodoma.

Mina aliweka kila kitu sawa ndipo safari ya kuelekea Dodoma ikaanza. Alishangaa vile Andy alivyomtaka abebe vitu vyake vyote hasa nguo. Kila Mina alipomwambia labda abakishe hata baadhi ya vitu, zaidi vya mtoto mchanga ambavyo alikuwa amemnunulia tayari akijiandaa ili akijifungua asipate shida, lakini alikuwa akilazimishia kwa ukali kuwa abebe vyote, kila kitu, kwa nini anakataa anakuwa ni mtu ambaye kama hana uhakika na maamuzi yake. Kama anayekwenda kujaribisha ili vikishindikana akimbie. Baada ya ubishi wa muda, Mina akaona akusanye kila kitu kasoro vifaa. Wakajaza hilo gari. Vitu vya Mina na wanae, ndipo wakondoka.

Hata safari ya kwenda kumuona daktari wake wa kliniki nayo ikaonekana ni tatizo. Andy akawa mkali kuwa ni kama Mina anataka kwenda kuonana naye tu. Hana tatizo lolote lile. Akitaka ampigie simu amuage wakiwa njiani. Sio lazima kwenda kuiona sura yake huyo daktari. “Wapo mamilioni ya wakina mama hapa duniani. Wanazaa bila shida yeyote ile na hawazalishwi na huyo daktari wako.” “Basi Andy. Naona hiyo siku ya kujifungua ikifika nitajua chakufanya.” Mina akaona yaishe. Andy hakumjibu akaendelea kukanyaga mafuta wakiondoka mkoani Iringa.

Andy alikuwa akiendesha mwendo wa kawaida tu. Mwangalifu barabarani mpaka abiria wake wakalala. Mina aliomba wasimame mara mbili tu njiani ili ajisaidie. Baada ya kama masaa manne na nusu wakawa wameshawasili Dodoma. Mina akakaa sawa. “Hapa ndio Dodoma, Andy?” “Tumeianza kama dakika 10 zilizopita.” Macho yakawa nje akiangalia jiji kuu la Tanzania. Hakuwahi kufika.

Andy akaendesha mpaka nyumbani kwake. Mina akashangaa nyumba inafanana kama ya wazazi wake. “Ulichukua ramani ya kwa wazazi?” “Kidogo. Napenda pale nje kwao palivyo. Hata huko nyuma utapaona, panafanana kasoro hii sio gorofa.” “Ila pazuri Andy. Hongera.” “Asante.” Andy akamshusha Ayan.

“Nisubirini nichukue baadhi ya mizigo tufungue mlango.” “Unaishi peke yako?” “Yupo kijana anaishi nje, aliniahidi ataniletea msichana wa kazi nikiwa tayari. Ila nahisi ni mkewe, ila anaogopa kuniambia!” Mina akacheka wakawa wanamfuata kwa nyuma.

Ndani palikuwa pasafi sana. Hakushangaa, Andy ni msafi na anapenda kila kitu kikae sehemu yake. Mina na mwanae wakakaa hapo sebuleni kama wageni. Andy akaanza kuingiza mizigo. Wakamuona anaingiza ndani kabisa. Akafanya hivyo mizigo yote mpaka akamaliza. “Njooni huku niwaonyeshe vyumba vyenu.” Wakaanza cha Ayan. Kikawa kweli cha mtoto wa kiume kama kile alichokuwa amekitengeneza kule cha Kigamboni.  Wakamuacha Ayan chumbani kwake akiangalia na kupanga michezo yake, aliyokuja nayo na aliyoikuta hapo.

Ndipo akampeleka Mina kwenye chumba chake. Hapakuwa mbali na hapo kwa Ayan. Kilikuwa kikubwa na kitanda kizuri tu kama palipokuwa pameandaliwa maalumu au kama kuna mtu anaishi hapo. “Nani alikuwa anatumia hiki chumba?” “Hakuna! Kwani vipi?” “Kimekaa kama vile kilikuwa kikitumiwa na mtu!” “Sijawahi kuingiza mwanamke humu ndani Mina, kama huo ndio wasiwasi wako.” Mina hakujibu, akaelekea upande mwingine wa hicho chumba.

“Muulize huyo kijana hapo nje kama ameshawahi ona msichana anaingia humu ndani. Hata mara moja. Na Mungu wangu ni shahidi.” “Nashukuru kunikaribisha hapa Andy. Asante.” Mina akafungua masanduku yake nakuanza kutoa vitu vyake akiweka kitandani.

“Unataka nikusaidie ili upumzike?” “Hapana, nipo tu sawa.” Andy akabaki amesimama. “Sasa unafikiri huyo msichana tumuagize lini? Maana nilimwambia huyu kijana tutazungumza tukirudi. Na nimeona ameshasogea mlangoni. Aliniambia huyo msichana ni mzuri sana, hatasumbua. Na nikiangalia, na ushauri wa jana wa daktari, ni kweli unahitaji kupumzika. Tutahitaji msaada.”  Kutokana na alivyoongea, Mina akajua ujio wa Andy Iringa, ilikuwa ni kwenda kuwachukua aje aishi nao. Haikuwa matembezi. “Mimi nakusikiliza wewe Andy.” “Basi nitamwambia akamlete tu.” “Asante. Nashukuru Andy.” “Karibu.” Akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Maisha yakaanza hapo ndani, Mina asijue sasa kama amekwenda hapo kulea au ndio kulelewa! Andy akawa busy akiwasaidia yeye na mtoto. Anaamka asubuhi, anapika. Mina kabla hajatoka kitandani na yeye anapelekewa uji kama ujauzito wa Ayan. Akimaliza akitaka kutoka, anakuta Ayan alishaogeshwa, msafi na ameshalishwa.

Akitaka kufanya chochote, anakataliwa. “Mimi nipo likizo. Nikianza kazi utafanya tu. Sasa hivi pumzika.” Mina akakumbuka alipokuwa Uswiz alimwambia akirudi atarudia yale maisha ya mwanzoni. Andy akawa anajituma mpaka Mina akawa anamuonea huruma. Maisha yakaendelea mpaka Mina akaanza kunenepa kwa kula na kulala tu.

Moyo Uliojeruhiwa!

“Nimebakisha siku kama tano likizo iishe. Nafikiria kumpeleka Ayan mahali nilipaona wakati fulani nikiwa nafanya kazi hapa Dodoma. Pazuri sana. Naamini Ayan atafurahia.” “Sawa.” Mina akaafiki. “Kwa hiyo na wewe utaongozana na sisi?” Andy akauliza. “Yule msichana wa kazi anakuja jumamosi hii. Labda wewe uende na mtoto, mimi nibaki nimsubirie ili awepo hapa nyumbani mtu wa kumpokea na kumuelekeza mambo ya humu ndani.” Mina akajibu vizuri tu akidhani ni wazo ambalo lingefurahiwa, lakini ALIJUTA.

Andy akageuka akawa kama simba mpaka Mina akajiuliza hiyo safari ilikuwa yake au ni ya mtoto! Andy alikuwa akigomba akiingia na kutoka bila kutulia. “Sijajua natakiwa kufanya nini hapa duniani! Najiona ni kama nimefanya kila kitu na bado haionekaniki kama nimefanya! Nimejishusha na kufanya ambayo ninauhakika mwengine asingeweza, lakini ni kama bado naonekana sina ninachokifanya!” Akaelekea jikoni, Mina akasikia vyombo vinavunja. Na glasi zinapigizwa chini.

Akamchukua mtoto wake akaenda kumfungia chumbani. “Hata kama ni dharau au hunioni mimi ni bora kuliko wanaume wengine, lakini sio lazima kunifanyia hivyo kwa waziwazi. Unanivunjia heshima kwa kiasi kikubwa sana. Umekubali kubeba mtoto wa mwanaume mwingine ndani ya ndoa yetu!”

Nimekubali tuishi pamoja tulee mtoto, napo unaona shida kuongozana na mimi! Nina ubaya gani unaoshindwa kuvumilia kwa siku chache tu kuonekana na mimi hadharani?” Andy alitoka hapo akaendelea kugomba.

Alipoondoka tena kwa mara nyingine, Mina akakimbilia chumbani kwake akaanza kuhema. Hakuwahi kuonana na Andy huyo simba. Andy ni mkimya, hakujua kama ni mkali wa kiasi kile. Mlango ukafunguliwa. “Na ninajua tokea mwanzo nakuomba uje uishi na mimi hapa Dodoma ulikuwa unatafuta sababu ya kuondoka humu ndani ili ukawe huru huko. Sasa leo umeipata, ondoka tu.” Akafunga mlango na kuondoka.

Mina alijua haitakuwa rahisi kuendelea kumuona na tumbo kubwa akizunguka mle ndani na mtoto asiye wake. Akajua ni mengi yanaendelea ndani mwake, asijue chakufanya. Bado ana hasira na ni ngumu kukubaliana na hali ya kuwa yeye amebeba mimba si yake. Mina akabaki ametulia chumbani kwake. Akasikia gari likitoka. Akajua ni yeye.

Kwa Pam&Mill

Alipoingia tu ndani baada ya majibizano na Mill nje, Shema akamuwahi. “Naomba kufungua mifuko mama. Ameniambia ameninunulia viatu. Halafu kuna chakula kinanukia hicho!” Akambembeleza mama yake. “Hiyo nyama choma inanukia mpaka huku nje, mama Shema! Tuonje.” Akacheka na kuingia ndani chumbani kwake na mwanae. Akakuta ameleta kuku mzima wakuchoma, na nyama ya mbuzi nyingi haswa. Chips, ndizi za kukaanga na fanta pineaple nne. Akawapakulia wenzie, akawapelekea akarudi ndani. “Haya kula halafu ujaribishe.” Wakakaa na mama yake wakala.

Kuja kufungua hiyo mizigo, Pam mwenyewe akapoa. Alimnunulia Shema viatu vizuri na japokuwa Pam wa safari hii amechoka ila alijua ni vya bei. Alinunua 5 pairs. Vyakuchezea mpira viwili, kanisani kimoja na shule viwili. Akamnunulia jezi zakuchezea mpira tano. Nzuri sana. T-sheti na chupi zakutosha na singilendi. Mfuko mwingine alimnunulia mwanae deodorant, mpaka akamshangaza Pam. “Kamsikia mwanangu ananuka kwapa nini!” Akacheka moyoni ila kwa shukurani. Maana asingeweza nunua vyote hivyo. Akaweka na lotion nzuri, inanukia karibu na yeye. Hapo Pam akapotelea mawazoni mwanae akijaribu.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku ya jumamosi hiyo alikuwa akifanya kazi nusu siku. Akatoka kwenda kazini akamuacha Shema amelala. Kwenye majira ya saa tano akamuona amemsimamia kaunta kama mteja. Alipohakikisha amemuona, akasogea pembeni kabisa. Akahudumia wateja, walikuwa wengi akashindwa kutoka.

Akamuona anaenda ofisini kwa bosi wake. Akakaa huko mpaka saa 6 mchana alipokuwa anamaliza na kutoka. Akaenda kutoa epron yake na nyavu kichwani akabakiwa na kitambaa alichokuwa amefunga. Akaenda kumuaga bosi wake, Mill akiwepo hapo. Akamchangamkia kwelikweli. Lakini Pam hakutaka unafiki, akaondoka zake.

Mill akamkimbilia. “Pam! Pam! Simama basi.” Hakusimama. Akamkimbilia mpaka akamfikia na kwenda kusimama mbele yake. Ndio akasimama. “Mmeamka salama?” “Unanipotezea muda. Ongea shida yako.” Mill akatingisha kichwa kwa masikitiko. “Naondoka.” “Sawa Pam. Leo nimemuahidi Shema nitakuja kumchukua, twende tukacheze mpira. Ni sawa?” “Isizidi saa 12 kamili jioni. Lasivyo utanisikia kwenye vyombo vya habari.” “Pam!” “Hakika sikutanii.” “Kesho huyu mtoto haendi shule. Nataka kumpeleka kwa kinyozi, kisha..” “12 kamili awe amerudi. Usiniletee mchezo. Kama hutaki basi.” Akabaki akimwangalia.

“Wewe unahangaika nini na mwanangu mmoja tu, wakati unao watoto kibao na bado utazaa! Fujo zote hizi kwa Shema ni nini lakini?” “Ndiye mtoto peke yake ninaye fanana naye hivi.” “Umekutana na tapeli mwenzio nini? Akakubambikizia watoto wa tapeli mwenzenu!” Akamkejeli lakini Mill akaendelea.

“Halafu Shema ndio mzaliwa wangu wa kwanza. Lazima niwekeze kwake.” Pam akampita na kuendelea na safari yake.

“Viatu vimemuenea vizuri?” Hapo akasimama. “Nakushukuru sana. Sana. Asante kwa kila kitu ulichomnunulia. Shema anakua kama uyoga! Miguu na yenyewe inakua kwa haraka, halafu mpira ndio kila kitu kwake. Nimepitia kipindi kigumu hapo katikati. Nimejikuta nimeshindwa kumnunulia viatu kwa haraka. Ila ni uhitaji aliokuwa nao kwa muda mrefu sana, ila sema amejaliwa si mtoto mlalamishi. Ukimwambia asubiri, atasubiri bila kukughasi. Kwa hiyo umeleta kwa wakati muafaka. Nakushukuru sana.” Alizungumza kwa kutulia na unyenyekevu kama sio yeye, mpaka Mill akabaki amepigwa na butwaa.

“Na nashukuru kwa pesa pia. Jumatatu nitaenda kumalizia michango yote ninayodaiwa huko shuleni kwao.” “Si tumesema anahama shule? Zile pesa ni zako wewe na mahitaji yako binafsi!” “Lazima nimalizie deni, na awepo darasani wakati ukihangaikia uhamisho.” “Uhamisho si wakuhangaikia, Pam. Wanataka pesa tu. Na pesa ipo.” “Upande mmoja wa nafsi yangu una wasiwasi sana, lakini upande mwingine naogopa nisije mnyima mwanangu nafasi nzuri. Lakini ingekuwa vinginevyo, asingehama.” Akawa kama anayefikiria.

“Niambie wasiwasi wako.” “Jana nimezidi kufikiria hilo swala. Shema hajasoma hizo shule zenu za lugha zenu hizo. English anaiona kwenye somo tu. Naona kama mtamchanganya huko! Anafanya vizuri sana shuleni. Leo anakwenda kuanza upya wakati yupo darasa la nne! Hakika sina amani. Au kwa nini  asianze huko sekondari?”

“Hapana Pam. Mimi nipo nita…” “Sasa hivi ukiwa umesimama hapa ndio upo. Wazimu wako ukikupanda, na tamaa zako zikikuwaka, utaondoka hapa, umuache mwanangu njia panda. Huko sitaweza mlipia, na huku hawezi kurudi. Asiee HAPANA. Nimekumbuka.” Hapo hasira zikarudi.

“Pam! Tafadhali nisikilize.” “Hatahama shule ambayo mimi sina uwezo wa kumlipia. Atasoma shule ya uwezo wangu, sio uwezo wako wewe tapeli. Acha kutaka kumchanganya mwanangu. Kwanza ni katikati ya muhula. Unataka kumchanganya tu.” “Mimi sitaondoka tena nchini. Na sidanga..” “Usinitanie kabisa! Wewe maneno yako ni kama upepo. Hayana maana kabisa. Acha kunipotezea muda.” Mill akaumia sana.

Akaondoka kurudi kituoni. “Acha nikupe lifti mpaka nyumbani.” “Sina shida.” “Sasa si tunakwenda nyumba moja?!” “Kwa sababu tofautitofauti. Wewe achana na mimi. Utamkuta Shema yupo tayari. Kwanza alilala na viatu, nimemvua alivyopitiwa na usingizi. Nikimaanisha anakusubiria. Sasa usimtapeli mwanangu kama ulivyozoea kutapeli wengine.”

“Pam, nimekosa mama. Nisamehe.” “Acha kunifanya mimi mtoto mdogo. Umekosa kwani ilikuwa bahati mbaya? Wewe ni TAPELI tu Mill. Na mama Kenny anasema akikuona atakushauri. Ukapige magoti kanisani, uombewe. Walikuwa wakikuheshimu sana pale. Kenny alikuwa anakufuatilia mtandaoni, anasema alikuwa haamini kama ni wewe! Wote wakaniambia upo kama baba yako. Huna huruma. Roho zenu za kinyama. Hamjui kumfikiria mtu yeyote linapofika swala lenu. Ni nyinyi tu. Kwanza sikuamini kama UMENITELEKEZA!

“Maana nilihangaika na tumbo langu! Shema ni mkubwa, ananilemea. Lakini nilikuwa sijali wala sijikumbuki mimi, nakuhurumia wewe, kwa vile nilivyokuamini! Sikujua kama wewe ni tapeli katili wa kiasi hicho! Nimefungwa jela, sina hata wazo kama nimewekwa rumande, hofu yamgu kwako! Najiambia masikini Mill atakua yupo matatizoni, baba hana, mama hana. Hakuna atakayeona uzito wa kumtafuta huko, kujua kinachoendelea.”

“Yaani Sandra anakuja kunipokonya gari kule rumande, mimi nashukuru Mungu. Maana yeye ndio kama aliyenikumbusha kama ni mjamzito. Akili ilikuwa haipo kabisa, nipo jela, ila akili ipo kwako tu, muda wote nakuhurumia. Wala pia sikuwa nikijua kwa nini Sandra amenifunga! Sijifikirii mimi, hofu ipo kwako muda wote!”

“Sasa aliponiambia nimpe gari ndio atanitoa rumande na kufuta kesi, lasivyo nitazalia jela, ndio nikagutuka sasa, kumbe mimi mjamzito! Na ndipo akili ikanijia kumbe hapa shida ni wivu tu, kunirudisha chini! Aliniambia nikimpa gari ndio atanitoa, sikutaka mengi, shida nitoke, nihamasishe watu wakutafute huko, wajue kulikoni! Usaidiwe!”

“Nimetoka tu, bila kupumzika akili ipo kwako nakuhurumia. Nina njaa, jua kali, natafuta mtu anayeelewa mambo ya huko, basi usaidiwe. Simu yako, hapatikaniki si mchana si usiku. Na mimi nilivyokuwa mjinga, eti nakupigia kila saa! Sasa vile NILIVYOKUAMINI na yale maneno yako yaliyokuwa yamejaa hekima, nisijue kama wewe ni TAPELI tu, ushamalizana na mimi, umehamia kwa fala mwingine kama mimi, eti mimi nikazidi kuchanganyikiwa, najihakikishia upo matatizoni kabisa.”

“Zunguka! Zunguka! Zunguka na wewe. Kunywa hata maji naona najichelewesha, nawahi kukuokoa. Hangaika! Hangaika na wewe, ndio nikasema japokuwa mama Kenny, hataki undugu na nyinyi, labda yeye atanifungulia mlango maana wote uliowafundisha kunikimbia, bwana walinitenda! Huko sitakwenda.”

“Basi, ndio nikafika kwa mama Kenny. Namuelezea wasiwasi wangu juu yako kwamba kuna kitu hakipo sawa, upo matatizoni, naomba msaada utafutwe, mama Kenny akanihurumia sana yule mama. Akaniambia, Pam binti yangu, umetapeliwa. Mimi tena hee! SIAMINI!”

“Akashika kazi ya kunisimulia. Akaniambia yeye amekuza wanae pale ndani, akiona binti wadogo kama mimi, wakifika pale na matumbo yao kwa baba yenu. Akasema yaani vilevile kama mimi. Na mzee Mgini alikuwa akiwaambia, kama wanauhakika ni wake, wakishusha mzigo, wawalete pale. Alikuwa akiwaambia hakatai damu yake. Anasema nyumba ile ilijaa vilio vya wanawake, wa idadi ya wale watoto.”

“Akaniambia mimi si wa kwanza na wala nisidhani nitakua wa mwisho. Alisema na babu yenu ni wale waliokuwa wameshika pesa nyingi kipindi cha nyuma wengine hawana pesa. Pesa ilikuwepo mfukoni kwake, basi akaniambia alikuwa malaya kama baba yenu na wale ndugu zako pale. Ndio akasema ilibidi yeye kufunga na kuomba, na kupeleka wanae wakaombewe kabisa, kuwatenga na roho za KWENU. Kwani bado nilikuwa namuamini! Mill anidanganye mimi! HAIWEZEKANI. Wanamsingizia Mill.”

“Kumbe Kenny ananiangalia tu, anajua siamini. Ndio akanisaidia. Akaniambia wewe ni mzima. Huna tatizo. Na una mwanamke ana mimba ila yake ipo Instagram. Akaniambia yupo huko anapost kila siku maendeleo ya mtoto na bwana wewe upo. Mimi bado siamini. Mill si muongo jamani! Ndio kuonyeshwa picha sasa.”

“Nikidhania mimi nimebeba malaika, kumbe Marekani kuna uliyembebesha mungu mtu! Bwana mwanamke alikuwa amependeza na tumbo lake! Tena analipiga picha tuputupu, uchi halijafunikwa hata na nguo, na wewe bwana unaonekana upo tu! Kwengine umelishika tumbo kabisa! Mimi tena hee!”

“Mama Kenny akaniambia ila wewe umejiongeza. Pengine ulitaka kumuonyesha baba yako wewe ni watofauti, ili uendelee kuchota mapesa yake. Ukamtapeli utaoa. Ndio kumpeleka baba yako mpaka mlimali, kwenda kulipa mahari. Akasema umeona mchezo mtamu, ndio umeendelea kujiongeza utapeli wako wa kudanganya kama kuna ndoa. Ndio picha zenu sasa za harusi na yule mwanamke wako, nikaonyeshwa. Baba ulipendeza wewe! Suti ya nguvu, nyeusi imekukaa kitajiri kwelikweli! Na mashoga zako wakike na wakiume walikuwepo!”

“Basi mimi pale ndio akili ikanijia. Ndio maana na wenyewe wananifukuza makwao, na siwapati kwenye simu! Kenny akanicheka, hana mbavu. Akaniambia sio kwamba siwapati kwenye simu, ni kwamba umenifungia simu zangu. Nikawa kama mjinga zaidi, SIELEWI. Mama Kenny akasema, nyinyi kina Mgini mkiondoka kwa mwanamke, mnakua mmemalizana kabisa. Ashaona kwa wengi.”

“Ndio Kenny akanisaidia kunihakikishia. Akachukua namba ileile niliyokuwa nayo nikiwasiliana na wewe, sikupati. Akaniambia nikupigie na kukutumia ujumbe palepale. Nikawaonyesha kuwa sikupati na jumbe zangu zote tiki moja. Kenny hana mbavu. Akasema niangalie sasa simu yake.”

“Akakutumia ujumbe, ‘vipi bro, upo mzima na familia huko?’ Palepale zikatokea tiki mbili. Gafla zikageuka za rangi ya bluu. Akaniambia ushapokea na umesoma. Mimi tena hee! Bwana ulivyokuwa wewe! Palepale ukamjibu, ‘huku kwema kabisa. Vipi na nyinyi?’ Pale ndipo nikajirudisha kwenye kochi. Na kuhema.”

“Mama Kenny akaniambia, nikatulie, nijilelee tu mtoto wangu. Habari yangu ilishakwisha muda mrefu sana. Ile mahari waliyolipwa bibi na babu, ndio zawadi yangu. Yule mama akanikarimu chakula, na maji, kisha kunitakia safari njema kwenye maisha. Ndio hofu sasa!”

“Tumbo kubwa zaidi ya urefu wangu na umri wake. Hospitalini wananiambia mtoto yupo kama wa miezi tisa huko tumboni. Nazaaje? Sina kazi, sina familia, Mill aliyenitelekeza, alishanitoa muda mrefu sana huko kwenye familia, na kila anayenifahamu. Mama yangu alizaa, akapooza. Akaachwa. Uzuri wake yeye, alikuwa na pakurudia. Mimi narudi kwa nani!? Hofu, silali.”

Pressure. Ndugu hawanitaki, sina pakwenda wala wakunisaidia. Ndio nikamuomba mama yangu aje mjini haraka, nipo matatuzoni. Mama yangu yule mlemavu, akaomba aletwe huku mjini vilevile. Nakwenda kituoni kumpokea, ndio anakutana na tumbo lisilo na baba. Baba yupo Instagram na tumbo JINGINE. Nikamueleza ukweli wote na kumuonyesha na picha zenu sasa.”

“Nikamwambia kwa mara ya kwanza maishani, naogopa. Silali kwa hofu, nisije kufa wakati wa kujifungua, mwanangu akatupwa tu kama mzigo au nikapatwa matatizo, nitafanyaje nipo peke yangu! Basi, siku ya kwanza mama amefika hapa jijini, na kulala na mimi, akaniwekea mkono usiku, kama kunikumbatia nilale ndio nikaweza kufunga macho, na kunywa dawa, nikaweza kulala.”

“Ule ukweli ukawa unaniingia taratibu. Kila nafsi ikitaka kukutetea, basi na mimi nikawa follower wa Kisha Mgini huko Istagram. Bwana mlikuwa mnawapambe nyinyi! Mashabiki kibao mpaka wa hukohuko kweni wana LIKE na ku comment kwenye kila post za Kisha Mgini. Starehe zenu na kina Mike na Kamila nchi tofauti tofauti! Mpo wenyewe na Kisha! Mimi ninakazi ya kufuatilia tu ili kujikumbusha, na kukubali ukweli kwamba, wewe upo MZIMAA, ila mimi ni gazeti ushamaliza kulisoma, umetupa kama uchafu! Nikabakia kujiangalizia tu maisha yako na mwanamke wako mtandaoni! Kumbe nazidi kujimaliza mwenyewe, pressure haishuki.”

“Mwishoe yangu yakanishinda, mwili ukalemewa, Shema nikazaa kabla ya siku zake. Mrembo Kisha yeye akawa anazidi kushamiri na tumbo lake, na bwana wewe, upo nyuma yake kila wakati! Picha za mtoto wenu huko tumboni nazo zikawa zinatumwa na Kisha kila mkitoka kliniki! Mimi tena hee! Kumbe kuna wanaume wanapelekaga wanawake zao kliniki! Kama kwenye movie! Halafu na yeye mtoto wa kiume! Mapenzi mazito! Hakika siamini kama na YULE, naye ulimuacha!” Mill alikuwa amebadilika sura, kama aliyekuwa amelemewa na mzigo hapo aliposimama. Kuushusha hawezi! Kukaa hawezi! Na Pam naye alionekana lazima amuweke sawa hapohapo kwenye jua kali.

“Sasa nisikilize Mill. Baba yako aliwakusanya pale kama anayevundika maembe, akaacha watoto wake hawana mbele wala nyuma. Wanakazi ya kupigana mchana na usiku, nasikia wameuza mpaka madirisha kwenye zile nyumba alizowaachia.” Mill akashituka sana.

“Sasa wewe ukaona usirithi mali, urithi umalaya. Sasa Shema hatakuwa moja ya watoto unaofikiria kuwakusanya halafu uje uwaache kama alivyowafanyia baba yenu. Nitakuwa makini sana na wewe. Sasa nikuone unakosea hata stepu moja. Hakika utaniona mchungu, kuliko shubiri. Sikutanii juu ya Shema.”

“Na leo, saa 12 isipomkuta pale ndani, jua ndio mwisho wa kumchukua, na nisije kukuona tena pale. Kama unafikiri nakutania, au ni Pam yule wa wakati ule wakumlaghai, basi nisimuone Shema saa 12 jioni. Huwezi kufuata mashariti yangu, muache.” Pam akaondoka kabisa, Mill akabaki miguu imekufa ganzi. Bado amelemewa.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni Nini Kitaendelea Kwenye Mioyo Hiyo Iliyojeruhiwa Kwa Wapenzi Hao Wa Love At First Sight?

Inaendelea


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment