Wakati anapata usingizi usiku wa saa nne baada
yakufanya kazi zake kwenye kompyuta yake, akasikia hodi mlangoni. Mina
akashituka. Alikuwa akilala kinyumba cha nje tu. Kila ilipokuwa ikifika saa
kumi na mbili jioni alikuwa akifunga milango yote mpaka kigeti cha hapo
nje mbele ya mlango wa kuingilia. Akachungulia dirishani. Akamuona Andy
amembeba mtoto, wanatetemeka baridi.
“Ayan!” Akaanza kufungua mlango wa ndani kwa haraka.
“Poleni.” Akatoka ili afungue geti dogo. Ayan akamwangalia. “Pole baba. Pole
sana.” Mina akamwambia mwanae. Akafungua geti, akataka kumpokea, Andy
akamkatalia. “Labda ukae naye. Usimbebe.” “Basi niwekee hapo kitandani
nimfunike na mablangeti.” Andy akamuweka kitandani. Mina akamuona anatoka.
Kumbe alikwenda kushusha mizigo kwenye taksii.
Akashusha masanduku makubwa mawili na dogo kidogo.
Akafunga mlango. Mina hakujua kama anabaki au anaondoka. Akaona anyamaze. “Huyu
ameingia baridi. Nimembandikia maji ya moto aoge, kisha nimpe maziwa.” “Naona na
chakula pia. Hatujala.” “Sawa.” Mina alikuwa akichemsha maji kwa mashine. Kwa
haraka yakachemka. Akamuogesha mtoto haraka, akampa maziwa wakati anapasha
chakula moto.
Hakuwa hata na meza. “Unataka kuoga kwanza au kula
kwanza?” “Utakuwa na nafasi ya mimi kulala usiku huu?” Mina hakuwa na vitanda
viwili wala kochi. Akafikiria kwa haraka. “Hiki kitanda ni kikubwa Andy.
Tulaleni wote kwa usiku huu, kesho tujipange upya. Kuna baridi sana huko nje,
na ni usiku sana sasa. Jikaze tu tubanane.” “Asante.” Andy akashukuru na
kusogea sehemu ya kuchemshia maji.
Mina anatayarisha chakula, Andy anajitayarishia maji
ya kuoga. Akamuona amekuwa mwenyeji. Akajiwekea maji. Akamuomba taulo. Akampa
safi kabisa. Akaelekea bafuni na begi lake. Baada ya muda akatoka, Mina
akimlisha Ayan. “Anasinzia huyu!” “Tumekuwa na siku ndefu. Anahaki ya kuchoka.”
Akajibu akisogea pale.
“Chakula kipo hapo.” Akajiwekea, akaanza kula, huku
Mina akimlisha Ayan. “Jikaze ule Ayan. Ukishiba utalala vizuri.” Mina
akaendelea kumbembeleza, mwishoe akaona ni heri ampe tu maziwa mengine.
Akamuwekea chupa nyingine ya maziwa mdomoni, akamfunika. “Nitakuja Ayan. Lala.”
Akamuona amefunga macho huku anakunywa hayo maziwa.
“Pole. Naona umeshika sahani. Sina meza, ila
nitanunua.” “Nipo sawa tu. Nimeshamaliza. Asante.” “Basi nikupokee, na wewe
ulale.” Andy akamkabidhi sahani, akarudi bafuni kusafisha meno, akarudi na
kupanda kitandani. Akakuta Mina amemuwekea blangeti jingine.
“Nimefurahi Andy! Asante.” Mina akamuwahi na
sauti yake ya kitoto, kabla hajalala. Andy hakujibu, lakini akajua amemsikia.
Akaweka mambo sawa, akazima taa, akapanda kitandani na wageni wake, wakalala.
~~~~~~~~~~~~~~
Asubuhi baada ya kupata kifungua kinywa Andy
akamwambia Mina aandike kila kitu anachohitaji hapo, pamoja na kitanda cha
Ayan, akanunue. “Nitajitahidi kuwahi kuvileta mapema. Nina ondoka na ndege ya
mchana.” Akajua ndio anaambiwa asimuhesabu hata kwa chakula cha mchana.
Kwa kuwa Mina anajua aina ya maisha yao watatu, akajua
ni nini mtoto wake atahitaji. Akamwandikia kila kitu, akamkabidhi. Andy
akatoka. Alirudi kwenye saa tano na kila kitu alichotumwa na Mina, akamsaidia
kuweka sawa pale ndani. Akapanga vitu vya mtoto hapo hapo ndani. Akakaa.
“Ukiwa na shida
yeyote, naomba unitaarifu Mina. Nitarudi kwa haraka tu nikusaidie.”
“Asante Andy. Nashukuru sana. Naamini tutakuwa sawa. Si eti Ayan?” Ayan
akakubali. Andy akamuita amsogelee pale alipokuwa amekaa. Akamsogelea.
Akamkumbatia na kumbusu. “Usimsumbue mama, Ayan. Chochote anachokwambia,
usikilize. Sawa?” “Sawa.” Ayan akakubali. Andy akambusu tena kijana wake,
akabaki kama anayefikiria, mwishoe akasimama.
“Hii pesa itakusaidia kwa matumizi ya hapa. Dawa zake
zakumpaka huko kwenye mapele zipo kwenye sanduku lake pale, nilishampaka
asubuhi.” “Sawa.” Akamkabidhi Mina ile pesa, akashukuru. Nakuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~
Maisha ya Mina yakarudi kuwa na furaha haswa.
Hiyo siku alijawa furaha kama amekabidhiwa ulimwengu. Yupo na mtoto
wake! Hakuwa akiamini. Walishinda wakicheza magari, huku akimwangalia
anavyopanga vitofali vyake wakicheka. Kwa asili Ayan alikuwa mtulivu sana, ila
mama yake alijua jinsi yakumfanya acheke. Mpaka nyumba kubwa walijua Mina ana
mgeni. Kwake kulijaa vicheko na fujo ndogo ndogo.
Usiku Andy akapiga simu, Mina akampa mtoto simu. Andy
akashangaa Ayan ndio anapokea. Akamsalimia, na kuzungumza naye kidogo. “Dad
amesema alifika salama.” Ayan akamwambia mama yake. Akajua ndio ujumbe wake
yeye.
~~~~~~~~~~~~~~
Maisha yakaendelea. Baada ya siku 7, Andy akarudi na
gari yake kubwa. Alifika hapo asubuhi kama kwenye saa mbili. Mina na mtoto wake
walikuwa wamelala. Hakuwa amemwambia kama atafika, kama kumfumania vile!
Lakini uzuri Mina alijituliza kulea mwanae. Akaamka kwenda kumfungulia.
Akamkaribisha ndani. “Ayan bado amelala.” Akaongea kwa kunong’ona. Andy
akamsogelea pale kitandani. Akabaki akimwangalia vile alivyo lala. Akamfunika
tena vizuri. Mina akaanza kujitayarisha.
Anatoka bafuni kuoga, akamkuta Andy amelala kwenye
kiti. “Andy!” Akamuita taratibu. “Panda kitandani ulale kidogo.” Bila hata kubisha,
Andy na nguo zake akapanda kitandani. Akamfunika mablangeti mawili, hata dakika
haikupita akamsikia akihema kama aliyelala.
Hakujua kama ndio aliendesha usiku kuchwa ndio anafika
au alikuwa hotelini. Akaanza kuandaa kifungua kinywa. Saa nne na nusu mtoto
akaamka. Akamlisha, mpaka akamaliza na kumuogesha, Andy amelala. Akapika
chakula cha mchana, akamlisha mtoto, Andy bado amelala. Wakaamua na wao wapate
usingizi wa mchana. Ayan akalala kitandani kwake. Wapi Mina alale! Akabaki
akifikiria, mwishoe akaamua ajilaze pembeni kabisa hapo hapo kitandani. Wote
wakalala.
Baada ya masaa mawili akaamka na kumkuta Andy
akimwangalia. Mina akaona aibu. “Nilikuwa nakoroma?” Andy akacheka. “Pole.
Nalala vibaya siku hizi!” “Hujakoroma bwana! Acha hujihami.” Mina
akacheka na kujiweka sawa. “Unakula vizuri?” “Hivyo hivyo.” Mina akajibu pakawa
kimya.
“Unafikiri utaweza kuendelea kuishi na Ayan kwa
muda gani? Nikimaanisha kabla hujajifungua.” Mina akashituka sana.
“Nilipata ile nafasi ya kazi Dodoma. Sasa hivi ninauhakika wa kutulia Dodoma
tu. Nilinunua na nyumba kabisa. Muda huu nilipokuwa nimemuacha
hapa Ayan, nilikuwa nikimalizia kununua vifaa vya ndani. Nimeridhika
kuwa imekamilika. Niliulizia shule pale, naona wanazo nzuri tu. Ndio maana
nauliza ili nijipange. Sitataka Ayan akaishi kwa mtu mwingine
tena. Kama sio wewe, ni mimi.” Mina akabaki kimya kwa muda.
“Ukinipa mimi, nitatafuta mfanyakazi wakutusaidia
kazi, na nitamuanzisha shule. Ni kweli anauelewa mzuri tu. Anafaa aanze
shule.” Mina akajifuta machozi. “Natamani ingekuwa
hapa Iringa Andy!” “Kwanza ni kwa nini ulichagua kuishi huku? Mbali sana
na nyumbani!” “Mama alinifukuza pia. Halafu
sikuwa na pesa yakutosha. Nilijua pale Dar nisingepaweza. Nyumba
zakupanga ni gharama Andy, sikuwa najua!” Andy akacheka kidogo kama
anayefikiria. Mina akajifuta machozi.
“Kweli! Si unajua pale kwa mama tulianza kuishi nikiwa
mdogo sana? Kwa hiyo nilikuwa sijui maswala ya kodi. Nilipoanza kutafuta sehemu
ya kuishi ndipo heshima ya lile jiji ikaongezeka. Nikajua sitapaweza.”
“Hapa unalipa kiasi gani?” Andy akauliza. Akamtajia.
“Lakini kwa kuwa ni kama nilipamalizia ujenzi, sidaiwi
kwa muda mrefu. Nafikiri hata miezi 7 ijayo. Nitapiga naye mahesabu, maana kila
nikinunua kitu, tunaandikishana.” Kimya. “Ndio maana nasema ingekuwa
Dodoma ni karibu na hapa, ningekuomba mimi hiyo nafasi ya kazi
hapo nyumbani kwenu.” Andy akamwangalia.
“Ningeweza Andy! Kumbuka mimi nawafahamu.
Hutahitaji kunielekeza chochote. Najua nini unapenda, nini hupendi.
Kwenye chakula hivyo hivyo. Na bado Ayan angepata nafasi ya kuwa karibu na sisi
wote. Lakini ni Dodoma!” Mina akafikiria kidogo.
“Nikuombe kitu Andy?” “Nini?” “Namuona kama sasa hivi
anakula vizuri. Ameanza kuchangamka na madonda yamekauka. Naomba
niachie kwa muda mpaka kodi ya hapa iishe. Nitajaribu kuangalia sehemu ya
kuishi Dodoma. Nikipata sehemu nafuu, nitahamia huko. Ili tuwe
karibu.” Andy akafikiria.
“Tukichukulia miezi 7 tu ijayo kama ndio kodi yako
inaisha hapa, inamaana ndani ya huo muda utakuwa umejifungua. Utakuwa na
mtoto mdogo Mina. Utawezaje na watoto wawili wote wanakulilia wewe peke yako?”
“Mimi ni mama yao Andy. Sihitaji kufundishwa nimpende yupi kwanza
aje yupi. Sihitaji kukumbushwa Ayan anahitaji kula au kuoga. Nitajipanga
vizuri tu, naomba usiwe na wasiwasi juu ya hilo na uwe na hakika
katika hilo Andy. Ayan hatateseka sababu ya mdogo wake.” Andy
akanyamaza.
“Naomba usiwe hata na shaka juu ya hilo Andy. Nakuhakikishia.
Hakuna atakayemtunza Ayan vizuri kama mimi.
Nimeishi na watu, nimeona. Na ubaya au uzuri Ayan ni mpole au mrahisi
sana kuishi naye, kiasi ya kwamba nirahisi kumsahau au kumpuuza.
Lakini hicho hakiwezi kutokea akiwa na mimi, Andy.” “Najua Mina. Hilo
sina wasiwasi nalo. Ila wewe mwenyewe. Hutalemewa?” “Hata
kidogo.” Mina akakaa kabisa ili kumshawishi.
“Naamini nitaweza Andy. Labda kwa siku zile
nikiwa nakaribia kujifungua na baada. Ili nipone vizuri. Hapo nitakuomba msaada.
Lakini wakati mwingine, naomba uwe na amani. Na nitajitahidi
kutafuta makazi karibu na wewe ili uwe na uwezo wa kuja
kumtembelea wakati wowote.” Andy akanyamaza.
“Andy?” “Nafikiria Mina!” Akamuona anafunga macho kama anayesikilizia
maumivu, Mina akaelewa. “Sikukusudia kukuharibia taratibu ya maisha Andy.
Sikukusudia kukufedhehesha.” Akamuona anafuta machozi. Mina akajisikia
vibaya sana. “Nilikuwa nahangaika Mina. Nilihangaika
sana ili siku kama hii itukute pamoja, wote tupumzike. Naona juhudi
zangu zimegonga mwamba!” Mina akaanza kulia na yeye. Alilia sana
Mina.
Mpaka akatoka pale kitandani na kwenda maliwatoni. Kwa
mara ya kwanza akatamani kama angekuwa na maelezo ya kumpa Andy,
siku hiyo amueleze lakini hakuwa nayo. Ni mjamzito asiyejua
ilikuwaje. Na alijua hakuna ambaye angemuamini. Ni Mina! Akaendelea
kulia. Akasikia mlango unafunguliwa na kufungwa. Akajua anakwenda kukimbia
kama kawaida yake mpaka atulie. Mina akatoka, akawa amekaa akifikiria.
Ayan aliamka, akahamia kulala kitandani kwa mama yake. Akawa amemlalia huku
anakunywa maziwa.
Andy akarudi anatokwa jasho kama amelowa mvua.
Akajitayarishia maji, akaenda kuoga, akatoka. “Kuna kitu cha kula?” Mina
akasimama kumuwekea kwenye sahani. Akampangia vizuri kwenye stuli aliyonunua
mara baada ya Ayan kuhamia hapo, akamkaribisha na kurudi kukaa mbele, kitandani
alipokuwa amemuacha Ayan.
Ayan akajirudisha kwa mama yake, akamlalia. “Umeshiba
au unataka uji?” “Nataka uji.” Ayan akajibu. “Sema naomba bwana Ayan,
vipi wewe!” Andy akaingilia. “Njoo basi ukae hapa na dad ule, au unataka
nikulishe?” Akamuona Ayan anacheka. Akajua anamuogopa baba yake. “Njoo
nikwambie mama.” Mina akacheka. Akaweka uji kwenye bakuli akarudi pale
alipokuwa amejilaza Ayan.
“Nini?” Mina akamuuliza mwanae huku akicheka. “Mikono imechoka.”
Ayan akamnong’oneza mama yake masikioni Mina akacheka sana. “Ayan wewe!
Kunywa maziwa tu ndio mikono huwa haichoki, kingine chochote
mikono inachoka! Aibu zako.” Ayan akacheka.
“Njoo ukae hapa ule Ayan. Mama amepika, sisi tunakula.
Njoo ukae hapa.” Ayan akamwangalia mama yake, akarudisha macho kwa baba yake.
Wakamuona anatoka kitandani taratibu kama anayesubiria mama yake amuokoe.
“Njoo ukae hapa.” Baba yake akamuwekea msisitizo. Akaenda kukaa, Mina
akampoozeshea uji akampa kwenye bakuli. “Usijimwagie.” Akamwambia kwa upendo
akitamani amlishe tu. Akaanza kunywa taratibu huku akimwangalia mama yake.
Pakawa kimya.
~~~~~~~~~~~~~~
“Nimepata wazo Andy, naamini itaturahisishia.”
Andy akamwangalia. “Kwa sasa si upo likizo ya kuhama?” Andy kimya akimsikiliza.
“Na kama nimekuelewa vizuri ni kama ulishahama. Basi kwa siku hizo zilizobaki
za likizo, unaweza kumchukua Ayan, mimi nianze kuhangaikia makazi huko
huko Dodoma. Ikitokea napata kabla hujaanza kazi, nitahamia. Ikitokea
nakosa, umrudishe Ayan hapa ili uweze kutulia kazini. Au unaonaje?” Andy akanyamaza.
“Nataka kukaa na mama.” Ayan akawafanya wote
wamgeukie. Alikuwa ametulia, hawakujua kama anasikiliza. Kwa mara ya kwanza
huyo mtoto akaongea juu ya aishi wapi. “Ni kwa muda tu Ayan. Na mimi
nikiweka mambo sawa kama dad, tutakuwa wote.” “Au tuwe wote
wakati ukiweka mambo sawa, mama.” Akaongeza Ayan na kushangaza sana wazazi
wake, wote wakanyamaza. Andy akala mpaka akamaliza.
Hatimaye!
Kesho yake
asubuhi akiwa anampimia mteja maziwa, akahisi mtu mwingine ameongezeka kaunta.
Ilikuwa mida ya saa tano. Huwa mida hiyo wanakuwa hawana wateja wengi.
Alipomuangalia, akakuta Mill amesimama pembeni kabisa. Pam alishituka
mpaka akamwaga maziwa ndoo nzima. Bosi wake akaona kupitia dirisha la ofisini
kwake. Ilikuwa mbaya sana.
Alimfoka Pam kama mtoto mdogo na kumwambia atamkata mshahara, mwezi huo asitegemee
kitu, kama hataki aondoke. Alimsema mbele yao, asijue Pam alikuwa kwenye
mshituko hawezi hata kumsikia. Alibaki akiyaangalia yale maziwa pale
sakafuni bila ya kusogea wala kupepesa macho. “Samahani.” Mill akasema hivyo na
kuondoka kabisa hapo.
Pam alikuwa
amefunga nywele na kuvaa kofia ya wavu kwa afya, ili nywele zisiingie kwenye
maziwa, na apron nyeupe. Akaanza kusafisha hapo, bosi wake akiendelea kufoka
huku akimuhudumia mteja aliyekuwa pale. Kisha akaondoka hapo kurudi ofisini
kwake huku akiendelea kuongea.
Pam akabaki
amesimama kaunta akisubiria wateja ila mwili mzima ukitetemeka. Baada ya kama
lisaa, akamuona Mill upande mwingine anaenda ofisini kwa bosi wake. Hata
hakuendelea kumuangalia tena, na hakujua ameenda kuzungumza nini ila alihisi.
Baada ya kama
dakika 10 akatoka bosi wake, yaani mama Chali, akiwa na tabasamu kubwa. “Kumbe
unamgeni hujaniambia! Nenda kazungumze naye, nitakushikia mimi
mwenyewe.” Akajua amepewa tu hela na Mill. “Hamna haja. Mambo ya nyumbani nitamaliza
nyumbani. Naomba niendelee na kazi mpaka muda wangu wa kwenda kula.” Vile
alivyomjibu bila tabasamu, akaondoka.
Baada ya muda
akamuona Mill anatoka bila ya kurudi pale kaunta alipo. Akatulia kimya.
Akaendelea na kazi mpaka muda wake wa chakula ulipofika, mtu wa kumpokea akaja,
akatoka mpaka hapo mgahawani wanapokula.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Akatafuta sehemu
akakaa. Isah akamfuata. “Nikupe nini dada yangu? Mtori bado upo.”
“Usimuendekeze huyo, mpe chakula.” Pam akaanza kucheka. “Hamu yakula haijarudi
dada Tuma! Nihurumie.” “Basi utazidi kunyongea. Ugonjwa hauishi!”
“Nikiendelea kula mtori na limao jingi jua ndio napata nguvu, kesho
nakuletea chapati tani yako.” “Mmmh!” Akamsikia Tuma akiguna. “Nakuletea dada
Pam, wala usijali.” Pam akacheka na kutulia.
Akashangaa Mill anakaa
mezani kwake. Alishituka ila akajikaza. “Ulikuwa ukiumwa nini?” Pam hakumjibu
wala kumwangalia, kama hayupo. “Shema anaendeleaje na mkono?” Ikawa kama
anazungumza na upepo.
“Najua umenichukia.
Na najua umefanya kazi nzuri sana kumlea Shema, lakini tafadhali ongeza
umakini Pam.” Pam akamwangalia amekunja sura huyo! “Unamuacha mtoto anacheza
mpira barabarani! Akigongwa?” “Acha kunifundisha jinsi ya kulea
mtoto wangu.” “Naomba kukurekebisha. Ni mtoto WETU. Na katika hili naomba
tuweke tofauti zetu pembeni, lizingatie tafadhali. Kosa dogo tu,
tunaweza kumpoteza, halafu tukaishia kuambiwa ‘samahani, ilikuwa bahati
mbaya’. Ambayo haitasaidia.” Pam akasimama na kuondoka hapo kabisa.
“Pam!” Mill
akamfuata. “Naomba unisikilize. Nimekuja kuzungumza na wewe.”
Wala hakugeuka. Akarudi kazini kwake
na kufunga mlango kwa nyuma na kupitiliza nyuma kabisa na kukaa huko kwa sababu
muda wake wa kula ulikuwa haujaisha. Akatulia huko.
Baada ya muda
kidogo akasikia sauti ya Isah akimuilizia. Akamfuata. “Nimekuletea chakula. Na
mumeo amesema nikuletee na sambusa pamoja na Fanta pineapple. Amesema ujikaze
ule.” “Mume wangu!?” Akashangaa Pam. “Yule uliyekuwa umekaa naye pale. Alirudi
akajitambulisha na kuomba uletewe ulichokuwa umeagiza. Ila uongezewe na hivi.”
Pam akabaki
amesimama akiangalia kile chakula, akitamani kama akimwage kwa hasira lakini Fanta
Pineapple huwa inamchanganya hawezi kujizuia. Na alijua Mill
alimfanyia makusudi akijua hiyo soda ni udhaifu wake. Halafu harufu
ya sambusa ikaanza kumuita. “Achana naye.” “Ashalipia kabisa. Acha nikuwekee
hapa niwahi kumsaidia Tuma.” Akaweka na kuondoka akamuacha amekodolea macho
hivyo vitu.
Bosi wake
akamfuata tena, ila akashangaa anajichekesha wakati si kawaida yake.
Mkali kwao kwelikweli. Akiwepo hapo, hata maji hayanywewi. Na alishamgombesha
mbele ya watu mpaka wateja! Pam akajifanya kama hajamuona. Si ni muda wake wa
chakula! Akatulia tu.
“Sambusa
zinanukia vizuri! Naomba moja ya kuonja.” “Chukua tu.” Akachukua na kuvuta kiti
kabisa, akashangaa anakaa. “Kumbe una mume! Mbona hatuambizani!” Akamuuliza kishoga
wakati wala si marafiki! Pam alimtizama tu na kurudisha macho kwenye
chakula chake.
Ni siku
iliyopita tu, alitoka kumuomba ampe nusu ya mshahara wake amlipie mwanae
michango ya shule, ni darasa la nne, lazima alipe ndipo aweze kufanya mitihani,
na kumnunulia viatu, akamkatalia akimwambia amezidi. Leo anataka
habari zake za nini! Alipomuona amemtizama vile, akanyanyuka na kuondoka. Jeuri
ya Pam si ya kufundishwa. Na hivi alishatendwa, alijawa chuki
usingemkuta akicheka kama zamani.
Akataka kususia
chakula, ila akashindwa. Akala chote na kusukumia na soda ndipo akarudi kazini.
~~~~~~~~~~~~~~
Mill alishajua
mida anayotoka. Akarudi tena hapo saa nane kamili. Kwenye saa 8:15
mchana akamuona Pam na mtoto wake wanatoka. Ila Shema amevaa sare za shule.
Akashindwa kuelewa mida hiyo ni kwa nini atokee kazini kwa mama yake na nguo za
shule! Akawakimbilia mpaka akawafikia. Pam alipogeuka akamuona ni yeye,
akaendelea na safari. “Twende Shema.” Akamshika mwanae mkono akawa kama
anamvuta.
“Badala ya
kupanda daladala naweza kuwapeleka nyumbani.” Pam wala hakumjibu. Akaendelea
kumvuta mtoto, haelewi. “Kwani huyu ni nani?” Kimya. “Mama?” “Twende,
acha maswali mengi.” Wakafika kituoni, basi likaja, wakapanda na kuondoka.
Walifika wanakoishi, akasalimia wapangaji wenzie hapo, wakaingia ndani kwake.
~~~~~~~~~~~~~~
Mwanae aliingia
tu ndani akaanza kubadili nguo akawa anataka kutoka. “Kwani ni lazima na leo
uende Shema mwanangu wewe? Si utulie tu ndani? Hilo gozi limekuwa chafu
halifai! Tulia kidogo.” “Yaani nikae tu hapa ndani, nisikilize taarabu?”
Hapo akakwama.
“Sasa sio upotee
kabisa mpaka giza likukute hukohuko. Nikitoka kukutafuta tena! Kesho hutoki.”
“Siendi mbali mama. Napiga danadana tu hapo nje.” “Shema!” “Basi nitakuwa
narudi kukuangalia kila wakati. Siendi mbali.” “Sasa ole wako ujisahau huko na
mpira, usirudi kama ulivyoahidi.” Akawa anamsaidia kuvua nguo.
~~~~~~~~~~~~~~
Mara akasikia
sauti ya Mill akisalimia nje. Hakika hakuamini. “Mimi naitwa Mill, mume
wake Pam, mama yake Shema. Sijui nimemkuta?” Pam alishangaa mpaka akakaa
kitandani. Mwanae akamwangalia kama hajaelewa. Ukiwa chumbani kwao kila
kinacho zungumzwa uwani, na kila anayepita nje mtaani na kutukana basi wanasikia
yeye na mwanae.
“Umesema wewe mume wa mama Shema!?”
“Ndiyo. Mume wa Pam.” Wote wakatoka kumuangalia, tena kwa kuitana, Mill
akiwaangalia. “Mama Batuli njoo muone mume wa mama Shema!” “Kwani mama
Shema ana mume na wewe, kama si uongo huo?” “Huyu hapa.” Wakazidi
kutoka, Mill amebaki amesimama hata hajakaribishwa.
“Lakini sura si
ngeni! Unafanana sana na Shema!” “Kasoro rangi ya mama yake. Shema mweupee.”
Shema akamwangalia mama yake. “Ila sura ya Shema na urefu ule, ni wewe
mtupu!” Kila mmoja akasema lake, Mill amesimama tu juani. “Na kama ungekataa
mimba, ungeumbuka.” Wakacheka kama mazuri.
Mmoja akauliza
swali. “Mbona hatujawahi kukuona miaka yote wamehamia hapa?!” “Nilikuwa
nje ya nchi. Nikapatwa na matatizo yaliyonifanya kushindwa kurudi
huku nyumbani. Sijui wapo?” “Wameingia ndani na mwanae muda si mrefu. Walikuwa
hapa wakisalimia. Umembahatisha.” Wakamuonyesha chumba.
Akaenda kugonga.
Kimya. Akagonga tena, Shema akaenda kufungua akiwa ameshika mpira wake mkononi.
“Shikamoo.” Akasalimia. “Marahaba. Unaendeleaje?” “Vizuri.” Ila safari hii
jinsi alivyomsalimia na kumuangalia, ilikuwa tofauti kabisa.
“Unaenda
kucheza?” “Mama ameniruhusu.” Mill akacheka kama kuweka hali ya utulivu
kati yao. “Unakwenda wapi? Nataka na mimi nije tucheze wote.” Hapo akampata.
Akaanza kutabasamu. “Na mimi nilikuwa nikicheza sana mpira nilipokuwa na umri
kama wako mpaka sekondari.” “Kumbe unajua!” “Ni wakati huo nikiwa kijana!
Sijacheza miaka mingi sana. Acha nizungumze na mama yako, halafu nitatoka tucheze
kidogo.” “Basi nitakuwa hapo nje.” Shema akatoka amechangamka kwelikweli. Mpira
tena! Akawa amempata kirahisi.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Hata hakumwangalia wakati akiingia.
Akavua viatu na kwenda kukaa. Ni chumba kilichokuwa na kochi kubwa moja,
kitanda kikubwa kimoja. Kisha kukawekwa kabati kubwa la nguo na vyombo kiasi.
Kwa ufupi sebule, chumba, sehemu ya kulia chakula, na jiko dogo la mafuta, vyote
vilikuwa sehemu moja.
“Pam mpenzi! Nimerudi
mama, japo kwa kuchelewa.” Kimya. “Unakumbuka nilikwambia ninakwenda
kuandaa mazingira, mimi nipate uraia wa kule, kisha nikuombee wewe Green
Card?” Kimya. “Nilikwama njia zote, nikaishia kuoa. Uraia
umekuja na watoto wawili! Ile ndoa niliihitimisha kwa shida sana. Ila nilifanikiwa
kutoka, nimerudi hapa nchini na watoto wawili.”
“Naona umejiongeza
kutoka kwa baba yako na babu yako. Wao walikuwa wakizaa hovyo,
naona wewe umeamua kuboresha. Unaoa na kuacha huku ukitapeli
wengine. Na kwa umri huo, ukiendelea hivyo au ukakazana kidogo tu, ukija
kufika umri wa baba yako, utakuwa umemfikia, kama si kumpita idadi ya
watoto.” “Pam, umekasirika.”
“Hapana. Ila kitakachoniudhi,
na ukaniona mbaya, si utapeli ulionifanyia mimi ila kumuingiza
Shema kwenye maisha machafu mliyokuwa mkiishi kwenu. Shema hatakuwa muhanga
wa laana na maisha uliyochagua kuishi wewe. Hutamfanya mwanangu
kama moja ya nazi unazokusanya shambani na kuweka kwenye
kapu moja na wanao ulioanza kukusanya kila kona ya dunia kama
baba yako.” “Pam!”
“Kwa chochote
utakachofanya, usimuhusishe Shema na maisha yako. Hakika nakuonya.
Huyu mtoto nimemuombea kama alivyonishauri mama Kenny.” Mill akashangaa
sana. “Nimemtenga na roho chafu za kwenu, kama mama Kenny
alivyowaombea watoto wake. Sitaki Shema aje awe kama wewe, au
baba yako. Hakika sitaki. Na nakuomba na wewe uliheshimu hilo.”
“Wewe una nguvu,
na pesa unayo. Endelea kuoa na kuzaa huko, kusanya watoto kila kona kama baba
yako, lakini si Shema. Huyu mtoto ni mzuri sana. Uliza hapo nje.
Kila mtu anampenda hapa mtaani. Anapenda shule. Si kama wale
ndugu zako. Mtulivu. Anaheshima kwa kila mtu. Mwanangu si mwizi.
Hajui ugomvi na mtu. Sasa wewe unataka umtoee kwenye haya maisha anayoona
wanaume hapo nje wametulia na wake zao. Unataka kumuingiza kwenye
maisha yako ya useja?” Mill ALIUMIA sana.
“Japokuwa sina
uwezo, lakini hii nyumba nimeipenda na nimechagua kuishi hapa na
Shema. Aone wanaume ambao pengine hawajasoma au hawana makazi
kama hayo yenu, lakini wametulia na wake zao na watoto wao
majumbani kwao. Si matajiri hao. Lakini Shema mwanangu anakitu
cha kujifunza kwao. Japokuwa yeye hajajaliwa familia kama hizi,
ila ANAJIFUNZA kuwa, kuna wanaume WAAMINIFU. Kwenye shida na raha,
WAPO na wake zao na watoto.”
“Sasa unataka
umtoe hapa, ukamuingize kwenye maisha yako hayo na ndugu zako,
yasiyo na maana ila uharibifu tu? HAPANA.” “Nisikilize Pam. Najua nimekuumiza.
Ila Shema ni mtoto wangu, na umezaa na mimi. Kama Mungu
aliniona sifai mimi kuwa baba yake, angekupa na mwanaume mwingine.
Ila amenipa mimi. Na KUKUKUMBUSHA kama ni wangu, amempa kila kitu changu.
Sina mtoto ninayefanana naye kama Shema.”
“Na mimi
nilirudi nikiwa nakutafuta wewe.” “Ili unifanye mimi mama Kenny?” “Pam, nimekosa.
Najua sasahivi hata nikisema hutanielewa. Ila jua nimerudi
kukutafuta WEWE kama Pam, sio kama mama Kenny. Sijawahi kukuona hivyo na
wala sina mpango wa kukufanya hivyo. Imetokea nina watoto nikiwa
nimeshapata baraka zote za wazazi wetu na Mungu, tukafanyiwa harusi ya kimila
kule kwenu baada ya mahari, kitu ambacho baba hakufanya kwa mama
Kenny. Mimi nimefanya kwako.” “Basi sitaki.”
“Nahisi umeshachelewa.
Wazee wako walishapokea mahari yangu na tumeombewa baraka zote na
marehemu baba yangu na kwenu walinikabidhi wewe rasmi.” “N…” “Hapana
Pam. Usiongee tena, umekasirika. Utazungumza jambo ambalo utakuja juta.
Nisikilize msimamo wangu, kwa sababu kuanzia sasa nitasimamia
hapo.” Akanyamaza.
“Shema ni mwanangu.
Sitamtelekeza eti kwa kuogopa nitaharibu. Nakusudia nisiharibu
kwake ila kumtengenezea na kumsaidia pale nilipoharibu mimi, basi
yeye asiharibu. Shema ni mzaliwa wangu wa KWANZA, nitawekeza
kwake nikijua ni kiongozi wa wadogo zake.”
“Na kwa taarifa
yako tu. Damu ya Shema ni Mgini kwa asilimia 100. Nikiwa nimekata tamaa
ya kukupata maana kila nilikokwenda walinipa habari zako mbaya,
lakini damu ya mwanangu ILINITAFUTA mpaka akanipata. Bila Shema, nisingekuwa
hapa leo. Na SITAMUACHA. Na kwenda kucheza naye mpira kidogo, ndipo
nitaondoka.” Akasimama nakutoka. Akakuta watu wanasikiliza madirishani. Akashangaa
sana asielewe ndio maisha ya uswahilini, kila habari ni ya wote!
Wakaanza kukimbia alipotoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Akaenda akamkuta
Shema anacheza na wenzie. Akabaki amesimama tu pembeni akimwangalia. Alipomuona
baba yake akamfuata. “Unataka kucheza?” “Endelea na wenzio. Nitakuja
kukuchukua, twende tukacheze uwanjani.” “Kwenye uwanja kabisa!?” “Unaogopa
nitakufunga?” Akacheka sana.
“Hapana, ila
sema mimi sina viatu. Alivyoninunulia mama vyakuchezea, vilipasuka.
Akaenda kunishonea mara mbili, vikafaa ila mara ya tatu nilivyopasuka
wakati naumia huu mkono, alipovirudisha tena kwa fundi amemwambia havifai
tena. Amesema nitumie vya shule mpaka atakapo ninunulia vingine. Lakini nahofia
kuchezea mpira visije haribika nikakosa vyakuvaa shuleni, maana najua hawezi
ninunulia viatu vingine kwa haraka. Kwa hiyo nikiwa nacheza tu hapa,
nacheza bila viatu. Huko uwanjani si watataka viatu?” Mill akaumia
sana.
“Nione miguu
yako.” Akacheka na kumuonyesha miguu hiyo isiyo na viatu. “Mimi nina miguu
mikubwa sana.” “Kweli una miguu mikubwa kama yangu! Viatu ulivyokuwa umetoka
navyo ndani vipo wapi?” “Nimemuomba mama yake Abuu anishikie wakati tunacheza.”
“Basi utaenda kuniletea niviangalie.”
“Nikuulize swali
jingine?” “Juu ya nini?” “Mbona na leo hukwenda shule?” “Nilikwenda
shule kama kawaida lakini wakaja kunitoa tena darasani. Mama alipata
hela kidogo. Akaona asisubirie mpaka apate zote, leo niende tu na hiyo hela
ndogo ili nisome na wenzangu tukijiandaa na mitihani ya darasa la nne. Lakini wamekataa.
Wanasema ana deni kubwa, huwa halipagi hata michango mingine
midogomidogo, angalau alipe nusu. Ndio nasubiria.” Mill akazidi kuumia.
“Sasa ukirudi
shule unafanyaje kufikia wenzio darasani?” Akamuona anacheka. “Hutafeli?”
“Siwezi. Muulize mama. Darasani najitahidi. Alikuwa akinilipia tution.
Nikawa nafundishwa. Yule mwalimu akamwambia mama naelewa, yeye ataendelea
kunifundisha tu bila kufuata silabasi. Nimekuja kugundua nimemaliza
hesabu zote za darasa letu mpaka za mbele.” Akaendelea Mili akimsikiliza kwa
makini.
“Mimi nilianza
shule nikiwa mdogo sana kiumri, ila mrefu tu. Halafu nikawa najua mambo
mengi. Mwanzoni kabisa bibi alipokuwa akinilea, akawa ananifundisha
kusoma na kuhesabu. Bibi yangu mimi ni mlemavu. Kwa hiyo mama alipokuwa akienda
kazini, anatuacha ndani tu. Ndio nikaanza kuongea na uelewa wa kusoma na
kuhesabu.” Mill akawa akimsikiliza mwanae huku akipata majibu ya maswali mengi
sana aliyokuwa hajui hata ayaulizaje.
“Sasa baadaye
nilipobakia na mama tu, ndio akawa akiniacha kwa mwalimu wakati anaenda kazini.
Akawa ananifundisha na watoto wakubwa. Ndio akaniombea shuleni
nianze na miaka 5. Ila wao wakawa hawaamini kama nina miaka mitano. Wakanipa
hesabu nikaweza. Ndio nikaanza darasa la kwanza . Huwezi amini sasahivi
nipo darasa la nne, nasoma na watoto wakubwa kwa umri ila mimi mrefu.” Mill
akacheka.
“Kweli tena! Na nawasaidia
darasa la tano hesabu.” Mill akacheka kwa furaha. Maana watoto aliotoka nao
huko Marekani, ni mzigo. “Kweli! Muulize mama.” “Nakuamini Shema. Sema nimefurahi
sana. Hongera. Kaniletee viatu nione.” Akaenda kuleta. Mill akatafuta kuona
namba ya kiatu, akashindwa. Maana kilionekana kilitumiwa zaidi ya
uwezo wake. Vilishonwa tena na tena.”
Mwishoe akamtuka
kalamu na karatasi. Akamchora mguu, na kuondoka akiwa amemwachia maagizo.
“Mwambie mama asipike, nitaleta chakula cha usiku.” Pam alivyosikia hivyo, akafyonza
rohoni na kupika. “Anataka kunifanya mimi mjinga kila siku!
Asiporudi, anilazie mtoto njaa!” Shema akashangaa mama yake anaendelea
kupika. Akamuacha tu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Aliwafuata Pam
na mwanae tokea kazini mpaka hapo kwao. Alipoona ni uswahilini akahofia wahuni
wasije ng’oa vioo vya gari yake ya thamani. Akaamua kutafuta sehemu
salama. Akaacha gari hapo na kutembea kurudi mpaka hapo kwa Pam. Ndio maana
ilikuwa rahisi kuwafuata mpaka nyumbani.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwenye majira ya
saa 12:45 jioni akarudi tena kama aliyekuwa akikimbia. Alikuwa na mifuko huyo,
Shema alisharudi nyumbani, akaoga, akawa anasubiria msosi alioahidiwa na
baba yake. Alipomuona anaingia na mifuko kwenye mlango wa hapo uwani akasimama
kwa haraka. Akampokea baadhi ya mifuko na mkono mmoja. Pam akawa kama hajamuona!
Yeye na mwanae wakahangaika
kubebelezea mizigo mpaka akamaliza. Akamsogelea pale alipokuwa akipika na
wenzie. Wote kimya. “Naomba tuzungumze hapo nje.” Kimya. “Pam? Au unataka
nizungumze mambo yote hapahapa?”
Ikabidi Pam akubali. “Naomba niangalizie.” Akamwambia mwenzie, na
kuongoza njia akitaka kuingia ndani. “Naomba iwe nje, tafadhali.” Akamsikia,
akabadili njia kutoka.
“Ni sawa
tukizungumzia ndani ya gari?” “Sitaki.” Mill akamwangalia kwa muda na
kumuomba wasogee mbali kidogo na watu. “Nilimwambia Shema akwambie usipike!”
“Mimi si mjinga kama ulivyonifikiria. Na wala si toi lako la kubonyeza
kila unapojisikia. Tafadhali usinipotezee muda.” Mill alimtizama, akajua
kweli amembadilikia.
“Vitu viwili.
Nimeleta baadhi ya matumizi ya Shema. Tafadhali angalia na unijulishe
kinachopungua.” Akaona amenyamaza, akajua kweli amelemewa. “Pili,
nakushukuru kunibebea mzigo wa malezi mpaka hapa. Umefanya vizuri Pam.
Inaweza isilete maana kwa sababu ni mimi nazungumza, lakini
kutoka ndani ya moyo wangu, nakupongeza. Shema ni mtoto mzuri sana.
Japokuwa sijakaa naye muda mrefu, lakini kwa muda mfupi niliozungumza naye, ni
mtoto mzuri sana na anakipaji ambacho nahisi kikiendelezwa
vizuri, atafika mbali.” Akamuona ametulia.
“Nakuja na pendekezo
la pili sasa, kwa kusema hivyo, naomba nimuhamishe shule. Nimpeleke
kwenye shule itakayomuendeleza zaidi.” “Wewe unataka kumchanganya mtoto,
Mill. Unataka kumpeleka kwenye mashule yenu hayo yanayozungumza lugha
zenu, wakati huku alipo anafanya vizuri sana. Shema anaakili ya mtoto
kama wa darasa la saba!” “Kama wanalitambua hilo mbona hawampeleki huko
darasa la 7, wana kazi ya kumfukuza tu shule?”
“Nilipungukiwa
pesa kidogo. Na jumatatu nikipokea mshahara wangu nakwenda kumalizia. Kwanza
wala si pesa nyingi. Mwache atulie pale alipopazoea.” “Hapana Pam. Mimi nipo
na nina uwezo. Tafadhali acha nimsaidie mwanangu kukuza kile
Mungu amemuwekea ndani yake, kutokana na pesa yangu si mazoea.
Na najua wewe ukiafikiana na hili, na yeye atakubali tu.”
“Hiyo shule ni
shule gani?” “Ni nzuri sana. Ndiko wanakosoma hao watoto wangu wengine.” “Sasa nakuonya
wewe na hao watoto wako, msije ninyanyasia mwanangu kwa sababu mnamuona hajaendelea
kama nyinyi. Nikikuhisi tu, na nikisikia wanao wanamnyanyasa
mwanangu huko kwenye mazingira unayotaka kumpeleka wakati hapa ametulia,
utaniona mbaya zaidi ya mwanzo. Nitamchukua mwanangu na nisiione
sura yako hapa.” Mill akacheka kwa masikitiko.
“Cheka udhani
nakutania. Pam uliyekutana naye safari hii ni mama Shema, uliza hapa
mtaani kama kuna anayegusa mwanangu hata kwa bahati mbaya.” “Sawa.
Nitakuwa makini.” “Hakika katika hilo Mungu akusaidie. Hutampelekesha
mwanangu utakavyo kwa madai unamsaidia. Kwanza mwenyewe alivyo vile wala
hataki msaada. Halafu anafikaje huko shuleni wakati sisi tunakaa huku au
kutaka kuongeza shuguli zisizo na sababu?” “Ndio linakuja ombi la msingi. Na
naomba ulifikirie kabla hujakataa.” Pam akabaki akimtizama. Mill akameza
mate.
“Uhamie…” “Uishie
hapohapo na usije rudia tena. Nimekwambia mimi si mjinga kama
unavyofikiria. Usinifanye mimi toi lako.” “Sivyo…” “Nakuonya. Hakika nakuonya.
Mara ya kwanza ulikuja na maneno yako yaliyojaa hekima, nikakuamini,
kumbe ni tapeli, mstaarabu.” “Pam!” Mill alikuwa anashindwa hata
kujitetea.
“Ulinitoa
katikati ya maisha yangu. Nikiwa nimezungukwa na ndugu, jamaa na marafiki.
Nikiwa nasita, na kukupa madhara yake mpaka kazini kwangu, ukanishawishi
kwa maneno ya ulaghai, mpaka ukanitoa katikati ya ulinzi wa watu,
ukanitenga na kunitelekeza kikatili bila huruma, ukaenda kuzaa huko na
mjinga mwingine kama mimi na yeye ukamuacha kama mimi tu.”
“Nimepata shida
kufika hapa nilipo. Kwako panaweza kuonekana duni, lakini pale ndani
tunaishi kama ndugu. Shema akiwa na shida pale, mimi sipo, atasaidiwa
kama mimi nipo. Kwa ugonjwa na uzima, tunasaidiana kwa uwezo wetu, ndio
maana umeweza kumkuta Shema yupo vile. Mtaani kote yule mtoto anasifiwa
na kupendwa mpaka na watoto wadogo.”
“Mwanzoni ulinitapeli
mimi, ikawa sawa. Sasahivi unataka unitoe hapa nikiwa na mtoto, ukanitende unyama
kama ulionitenda mwanzo! Acha kunifanya mimi mjinga. Hapa sitoki.
Ongea jingine kama huna, nenda zako katafute watoto kwengine. Nguvu ya
kuzaa unayo. Maneno ya utapeli unayo, nenda katafute malaya
wengine, sio mimi.” Pam akataka kuondoka.
“Sijamaliza
Pam!” “Nahisi mimi nimeshamaliza.” “Naomba namba yako ya simu ili tuwe
tunawasiliana kwa mambo ya msingi.” Pam akarudi pale aliposimama.
“Unaomba nini?!” “Namba ya simu.” “Hukuwa na namba yangu ya simu wewe?” Mill
akanyamaza na kukumbuka jinsi alivyomblock kila mahali ili asije hata
kosea akapokea.
Alipomuona
amenyamaza, akaanza kuondoka. “Wewe hujanijua vizuri wewe.” Akamsikia akiongea
huku akiwa anarudi ndani.
“Pam! Pam!”
“Unanipotezea muda.” “Basi nimnunulie yeye simu. Awe…” “Usithubutu.
Unataka kumgeuza mwanangu kama yale makuku ya kizungu yakufugwa ndani?
Awe mjinga kama matoto yenu hayo mnayoyafungia kwenye mageti!
Unafikiri mimi ndio masikini sana, sina uwezo wa kumnunulia simu?
Usimuone mtaani anacheza yule, ukafikiri mimi sijui mamichezo yenu hayo
ya kwenye simu yanayo pumbaza akili! Akifika umri wa simu, nitajua,
halafu mimi, ndio nitampa simu. Usitake kunichanganya
sasahivi.” Mill akakwama. Alidhania Kisha ni mkorofi, sasa akakutana na mbogo,
aliyejeruhiwa. Moyo umejaa uchungu, hawezi jisaidia. Mill
akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Inaendelea….
0 Comments:
Post a Comment