Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 29. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 29.

Baada ya kumsaka Pam kwa juhudi zote bila ya mafanikio, akiwa hana uhakika kama anamtafuta mke wa mtu au la, akaona wazo la kurudi kwa shangazi yake kumuulizia sio baya. Lakini alijuta.

Kwa Shangazi.

Alikutana na sifa mbaya za Pam zilizomchanganya Mill. “Umalaya umemponza.” Akaongeza shangazi mtu. “Wewe ulivyonikimbia hapa na kwenda kulipa mahari kwao huko Milimalini, akajihakikishia wewe keshakukamata, ubaya au uzuri kwake wewe si haupo hapa nchini, huko alikohamia chumba akakigeuza dangulo. Unaambiwa pakawa kama chumba cha kulala wageni sema ni wakiume.”

“Anawaingiza na kuwatoa atakavyo, mpaka akashika mimba. Anambambikizia nani tumbo hilo, na mwanaume si mmoja! Walivyoona hivyo akaanza kukimbia mmoja baada ya mwingine kama laana ya mama yake vile! Nasikia akaachwa anahangaika peke yake! Kama sijakosea ashazaa wawototo wawili kama si watatu na mabwana tofautitofauti. Mwili ule anautembeza kila mahali! Hata kama ni mzuri wa namna gani, wanaume wanachoka!” Mill aliondoka hapo amepandwa hasira asijue ni nini.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~

“Pam!” Hakuwa akiamini. Akahisi hasira za kumuacha ndizo zimemfanya awe malaya. Basi akazira kabisa, kana kwamba yeye ametokea nyumba ya watawa wakati na yeye alikuwa na mwanamke na watoto wawili juu! Akasusa na kuacha kumtafuta Pam huku roho ikimuuma, halafu wakati mwingine kujipongeza kumuacha, kwamba amejiepushia.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati upelelezi ukiendelea watu wakitajana hata kwa kusingiziana ilimradi tu kuipata hiyo pesa, ila kukwama kwenye ushahidi. Maisha ya Mill na hao watoto wa kimarekani yakaendelea kwa SHIDA sana. Mali zipo lakini ulezi mgumu kwelikweli. Watoto wajeuri hawamsikilizi hata kidogo!

Akawatafutia shule inayoendana na huko kwao Marekani. Angalau akawa anapata muda wa mambo mengine mbali na wao. Wanatoka asubuhi kwenda shule, wanarudi jioni, kila mmoja chumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Kuna mambo alifikiria kufanya hospitalini kwa Komba. Mill ni nesi. Anaakili na ufahamu ya mahospitali ya huko ulimwengu wa kwanza. Kuna vifaa vya upimaji alitaka aingize nchini, ikiwepo cha Sonography. Tatizo akawa tayari ni raia wa nchini Marekani, si Mtanzania tena.

Akazungumza na Colins. Akamsaidia kumuombea kibali cha kufanya kazi hospitalini kwao. Ndipo sasa akaingiza vifaa vya kisasa vya hospitali nchini, kupitia Colins na kupewa sehemu maalumu, akaweka mashine zake hapo hospitalini kwao. Mzee Komba akawa akijisifu sana kupata kijana mwingine mwenye akili na anayesaidiana na Colins. Kwamba wana nyanyuana. Wawili hao wakashikana kwelikweli. Undugu ukanoga.

Ukienda kutibiwa hospitali kuu ya Muhimbili, ukikutana na mzee Komba, ukataka kipimo, atakuelekeza hospitalini kwa mwanae. Na hapo ndipo utakutana na vifaa vya kisasa vya Mill. Na kama endapo utafika hospitalini kwa kina Colins, ukiandikiwa vipimo, basi vingine vitafanyika upande huo wa Mill.

Ukifuata vipimo tu hapo kwenye upande wa Mill, basi utakutanishwa kwa kuelekezwa upande wa pili, hapohapo kwa madaktari hospitali anayosimamia Colins. Ikawa neema kwa wote. Mill anaingiza pesa na Colins hivyohivyo

Damu Nzito Kuliko Maji.

Siku hiyo Mill alikuwa ofisini kwa Colins, wakawa wakizungumza. Akawa amekaa mbele ya meza ya Colins wanaangaliana wakizungumza. Akamuona Colins anacheka. “Nini?” “Ushawahi sikia duniani wawili wawili?” Colins akamuuliza akicheka, Mill asimuelewe. “Kuna siku nilikuwa pale mapokezi nikakutana na mtoto. Mkubwa tu. Bwana Mill, unafanana naye,  mpaka nikabaki nimemkodolea macho!”

“Yaani nimekuangalia sasahivi hapa ulivyotulia, ndio nimekumbuka. Unaona hayo macho yako yalivyo? Hivyo ulivyotulia sasahivi.” Colins akaendelea, akicheka. “Yaani hivyohivyo, halafu si unajua masikio yako madogo fulani hivi, halafu kama yamejikunja kwa juu? Bwana hivyohivyo!” Moyo wa Mill ukapasuka paa! Kama kumeangushwa chuma sakafuni. Ila akajikaza.

“Walikuwa wakinitania masikio yangu wakati nipo shule ya msingi. Mpaka wengine walikuwa wakiniita masikio.” Colins akacheka sana. “Basi huyo mtoto yupo hivyohiyo, kasoro tu yeye ni mweupeee! Nikasema kama ungekuwa umekana mimba enzi hizo za ujanani, ungeumbuka.” “Kwamba ni kijana mkubwa wa kiasi hicho?” “Oooh yeah! Mkubwa kama miaka 12 hivi.” Akapiga mahesabu kwa harakaharaka, akajua hawezi kuwa wake. Miaka 12 iliyopita hakuwa ameanzana na Pam. Akahema.

“Alikuwa mgonjwa?” Lakini akajikuta tu anauliza akitaka kujua zaidi. “Kilichonifanya nimwangalie ni aliyekuja naye, ni kijana tu alikuwa akimwambi mpira usio na kiasi, utamuua. Sasa na dogo mwenyewe akawa na maumivu akawa anamwambia aache kumuongelesha. Wakazidi kubishana pale mapokezi wakisubiria zamu yao ifike, wahudumiwe. Nahisi ameumiza mkono, dogo akawa analalamika maumivu ndio nikawaambia wamsaidie kwanza akamuone daktari. Sijawafuatilia tena, nikaondoka zangu. Ila mmefanana aisee! Sana.” Mill akacheka na kunyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Kile kitu kikazidi kumsumbua nafsini mwake, japo kwa umri ashajiridhisha si wake. Wazo kwamba wao ni wakubwa kimaumbile, lilishaondoka. “Hawezi kuwa wangu.” Akajifariji. Lakini usiku huo akashindwa hata kulala kila akiwaza jinsi alivyomuacha Pam! Moyo unapasuka kwa mshituko.

Asubuhi yake wakati anasaidia wanae waende shule akaanza kuwaangalia kwa makini kama hata wamerithi chochote kutoka kwake. Hakuna hata ukucha! Wote wanafanana na mama yao. Akafikiria na kuamua kupuuza.

Zikapita siku mbili nyingine, lakini hana amani kabisa anamfikiria huyo mtoto tu. Akaonelea aanze kumtafuta tena Pam. Safari hii akaamua kwenda kazini kwa kaka yake.

Kwa Eric.

Watoto wake walipotoka tu, akashika safari mpaka kwenye benki aliyokuwa akifanya kazi kaka yake Pam. Napo alihama benki muda mrefu zaidi ya miaka 9. Akaulizia alipohamia ilikuwa benki nyingine ila amepanda cheo. Anafanya makao makuu.

Akaenda, akaomba kumuona. Baada ya muda mfupi akamuona anatoka kwenye lifti. Hali yake nzuri tu. Alishituka sana kumuona Mill.

“Umekuja kudai mahari yako nini?” Kabla hajajibu akaendelea. “Nilijua tu mambo yatakufikia huko uliko. Lakini sikulaumu. Pam amebadilika sana. Sisi wote tulijua atatulia na wewe! Lakini wapi! Shangazi aliniambia habari zake, mpaka nilitokwa na machozi na kumuomba radhi kwa niaba yake na mama. Anasema kumbe nilipomuacha pale kwa shangazi akaanza umalaya akibadili wanaume mchana na usiku. Chakusikitisha alikuwa akifanya uchafu wake mbele ya watoto wa shangazi aisee!”

“Na nasikia usiku alikuwa akizungumza na wanaume zake, palepale chumbani wengine hawawezi kulala! Yaani shangazi anasema alivyosikia tu anachumbiwa, akajua sababu ya kukimbilia kulipiwa mahari huko kwa mama, ni kuficha aibu ya uchafu wake huku mjini. Anasema alijua tu angeachika. Sasa ndio yakampata ya kumpata mpaka ukamuacha.” Mill akakunja uso, akawa hajaelewa.

Eric akaendelea kwa jazba. “Halafu sasa nasikia hata mimba yenyewe haijulikani baba kwa sababu alikuwa na wanaume kibao! Wanaume wote walimkimbia baada ya kushika mimba. Shangazi anasema akamkamata mume wa mtu kutaka kumbambikizia, nasikia jamaa alikataa kabisa, hataki kusingiziwa mtoto peke yake wakati walikuwa wengi. Ndio kasusiwa mtoto, analea mwenyewe.”

“Mbaya zaidi, nasikia alipoona maisha magumu, ana tumbo lisilo na baba, akaanza uwizi pale nilipokuwa nimemtafutia kazi kwa Sandra. Sandra akachoka, akamfunga.” Mill ALISHITUKA sana. “Unamaanisha kumfunga jela!?” “Kumbe! Wewe unacheza na Sandra? Yule hana mchezo na pesa yake. Na nilimwambia kabisa Pam. Hajasoma, ila kazi niliyokuwa nimemtafutia ni muujiza ambao hautakaa ukatokea tena. Awe mwanangalifu, makini na anyenyekee. Akaanza tamaa mpaka wakamfunga.”

“Sasa eti yupo jela ndio ananipigia simu nikamsadie! Mke wangu akaniambia hatakaa akajifunza. Amejiingiza mwenyewe, ajitoe mwenyewe. Sikumtafuta tena. Ila nilikuja kumtafuta Sandra kumuomba radhi, maana mimi ndiye niliyemuombea nafasi ya kazi pale. Akasema alilipa pesa yote aliyokuwa akimuibia, kwa gari alilokuwa nalo Pam.” Mill akasikia kutetemeka miguu.

“Bwana Pam sijui aliingiwa na nini aisee! Na nilimsihi sana kabla sijamleta mjini. Babu akazungumza naye kwa mifano kabisa. Amekuja mjini, ameanza tamaa zisizo na sababu, ona alipo sasahivi.” “Unajua anako ishi?” Mill akauliza akiwa amevurugikiwa kabisa.

“Mimi!? Aisee hapana. Nilienda kunawa mikono mbele ya bibi na babu. Tena mama yake anayemuendekeza alikuwepo. Nikawaambia nimefanya kwa sehemu yangu, yeye mwenyewe ameshindwa. Sitaki tena kuja kumuona kwangu wala kumsikia. Na mke wangu ndio hataki hata kumsikia. Tuna binti waliopevuka, hataki Pam afike pale aanze kuwachanganya. Wakajifunza njia zake. Kwa hiyo kama unadai mahari yako, andika maumivu. Wazee ndio wamezeeka kabisa. Nina uhakika hata pesa ulizotoa walishasahau. Na mimi sin…” “Eric, sikuja kudai pesa. Uwe na siku njema.” Mill akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Alifika kwenye gari, akashindwa hata kuondoa gari. Akahisi kuna kitu hakijakaa sawa. Yeye ndio alikuwa mwanamme wa KWANZA kulala na Pam. Akakumbuka damu alizomwaga siku anamtoa bikra. Maana  ni Mill yeye mwenyewe ndiye aliyefua shuka pale kwenye damu, ndipo akayapeleka yote nyumbani kwa Mike kufuliwa na mashine.

“Hapana. Kwa swala la umalaya,…” Akataka kumkania lakini akasita. “Pengine alibadilika nilivyoondoka.” Akili ikamrudisha kwenye shutuma za simu. “Inavyoonekana hizo simu alizokuwa akizungumza usiku akiwa kwa shangazi yake, ni kabla sijamchumbia. Pam alikuwa na maringo sana. Hakuwa na mwanamme wakuzungumza naye usiku isipokuwa mimi! Ni nini kinaendelea?” Akazidi kuwaza bila jibu.

Ila kitendo cha Sandra kumpokonya gari, kilimuuma sana. “Sio hawa waliniambia Pam ni mwaminifu sana hawezi iba hata pesa ambayo Sandra mwenyewe hakuwa akijua kama ipo?” Akajiuliza na kushangazwa sana. Akaamua kumsaka Jerry.

Kwa Jerry.

Simu ikaita, Jerry akapokea kwa haraka sana. “Kwema kaka?” “Samahani naomba kukuchukulia muda wako wakati wa kazi. Kuna kitu kinanisumbua kidogo.” “Bila shaka.” Jerry akajibu.

“Ni kwa nini mlimfunga Pam?” Pakazuka ukimya hapo mpaka akahisi simu imekatika. “Jerry?” “Kulitokea wizi hapa, ikaonekana yeye ndiye amechukua hiyo pesa.” “Unamaanisha Pam yuleyule mliyekuwa mkimsifia ni mwaminifu sana, hata Sandra anaamani pesa yake ikiwa mikononi mwake?!” “Na mimi nilimkumbusha hilo Sandra, ila akaniambia watu wanabadilika.”

“Kweli Jerry ukakubali afungwe jela kwa kosa ambalo hamkuthibitisha?” “Yeye Sandra alisema alikuwa na uhakika. Sasa mimi ningefanyaje!?” “Hata ungeniambia mimi nilipe hilo deni.” Mill akalaumu na kumshangaza sana Jerry na kumpandisha hasira juu.

“Mill! Unazungumza nini kaka!? Unaongea nini wewe?! Si wewe ulioa kimyakimya, ukaniweka mimi mbali? Tena mimi niliyekuwa nikikusaidia kipindi kile na Pam? Ukamuacha yule binti bila huruma na kwenda kuoa huko! Kama vile mimi ni ADUI yako, ukamkaribisha tu Mike na Kamila kama vile hunijui au nidharau ukaona mimi sina pesa kama nyinyi!”

“Nakuja kugundua mtandaoni! Nikamuuliza Mike, Mike akaniambia umeamua iwe siri. Hata Pam hajui na nisiseme. Ulitaka mimi nifanye nini na wakati kwanza ulishaoa huko, bila kutaka mimi kujua, ukiniona ni mtu baki tu, sina maana?” Jerry alimbadilikia vibaya sana.

“Kwanza lazima utambue hili, ni WEWE ndiye uliyemuingiza yule binti matatizoni Mill. Maana hiki kitu kimekuwa kikiniumiza sana na Mike nilimwambia waziwazi.” Ikawa kama Jerry amefunguliwa funguo.

“Ulimkuta yule binti ametulia sana hapa kazini. Alikuwa akiheshimiwa na kila mtu. Ukaanza kumfutilia. Nikakupa madhara yake. Na hata Sandra alikwambia wazi kabisa. Alikuwahi Lona, huwezi kuendelea na Pam. Ni SHERIA na walisainishana hapa. Nikakwambia waziwazi, achana na Pam.”

“Ukatuthibitishia unampenda na utamuoa. Ukaja ukatangaza hapa, ukamtia matatizoni akawa CHUKI na MSALITI kwenye hii ofisi. Akabakiwa akiwindwa na kila mtu ili kulipizwa kisasi, halafu wewe ukamtelekeza huku. Halafu usivyo na huruma hata simu zake ukamfungia, ukaendeleza starehe zako huko Marekani, mkisaidiana na rafiki yako kipenzi Mike.”

“Sasa kabla hujamlaumu mke wangu kwa makosa YAKO, jua hivi, ALISHINDWA kumfukuza kazi kwa heshima yako na Mike, mpaka ulipotokea huo wizi.”

“Pam ambaye isingekuwa WEWE, hata kungeibiwa mamilioni ya pesa, na kamera zikamuonyesha anachukua, watu wote wangemtetea. Lakini wewe ulikuja, ukamtia dosari yule binti, alitolewa hapa na pingu na wote wakimshitaki kwa polisi waliokuwa wameletwa na Sandra. Wakajitolea hata kutoa ushahidi mahakamani, ilimradi tu KUMTOA hapa ofisini, wakimuhesabu ni msaliti wanaogopa asije akaendelea kuwaibia mabwana zao.”

“Nakushauri ushauri wa mwisho, kabla hujamtafuta aliyemuua Mike, nashauri angalia kwenye kioo, umtafute aliyeua au kuangamiza maisha ya Pam, binti aliyekuwa AMETULIA na kuendesha maisha yake hapa mjini bila TAMAA, akiwa anazungukwa na vishawishi. Ukimpata ndiye yeye umlaumi, akisindikizwa kwenye maangamizi yake na rafiki yake kipenzi Mike. Lakini sio mimi mliyekuwa mkinitenga na kuniona sifai hata kuwa karibu na nyinyi kwenye safari zenu za mapumziko.” Simu ikakatwa.

Mill alibaki kama amepigwa na shoti ya umeme. Mwili wote umekufa gazi. Nyayo zinatoa jasho wakati gari ameweka baridi mpaka mwisho.

Kwenye Vita Ya Tembo….

Siku moja ya alhamis Andy alikuwa amefika hapo nyumbani kwao kumchukua Ayan. Wakati akiegesha gari, akaona na gari ya Paul inaingia getini. Akamsubiri. “Vipi?” “Nimeleta dawa za mama.” Paul akajibu. “Na mimi ameniambia hajisikii vizuri ndio maana nimekuja leo. Vipi na wewe kazi.” Paul akatulia kidogo kama anayefikiria akamwangalia Andy tena kisha akatulia kidogo.

“Kwema?” Ikabidi Andy aulize. “Mimi mambo si mabaya. Nitakwenda India mwezi ujao. Kwa ajili ya mambo ya moyo.” “Mama aliniambia. Hongera.” “Asante. Lakini Andy, kuna jambo nataka kukwambia.” Andy akatulia. “Ongeza umakini kaka.” Andy akatulia.

“Najua upo makini, sana tu. Lakini nashauri, uongeze umakini. Ni hilo tu.” “Kwa upande gani?” Andy akauliza. “Wewe ni mtu mzima Andy. Fungua macho, ona. Najua wazazi wanaogopa kukwambia. Lakini kaka, ongeza umakini.” Paul akaingia ndani na kumuacha kaka yake hapo nje akitafakari.

~~~~~~~~~~~~~~

Maneno ya Paul mdogo wake yakaanza kumsumbua, lakini hajui anamaanisha nini! Akafikiri labda ni swala la kumuacha mtoto kwenye mikono ya watu. Akabaki akitafakari. Hata yeye hakujua kama mambo ya kazini yangechukua muda mrefu kwa kiasi kile ili kuweza kutulia na kujua kwa hakika makazi yatakuwa Dodoma au Morogoro au Iringa. Alitamani kulijua hilo kwa hakika ili atulie na mtoto wake nyumbani, lakini ikawa ni mvurugano. Anaambiwa azunguke kwenye maofisi yao, afundishe kile alichojifunza yeye huko Uswiz. Ikawa na yeye hata hajui juma hilo litamkuta mkoa gani!

Hiyo kazi ikawa imeshamgharimu NDOA, sasa MTOTO. Na yeye mwenyewe akawa wakuhangaika tu! Wakamuahidi akiweka mambo sawa, ndipo atapewa sasa kitengo maalumu. Lakini ikawa shida. Akiwa Dar, angalau aliweza kuwa na Ayan. Anampeleka kwao asubuhi na kwenda kumchukua jioni akitoka kazini.

~~~~~~~~~~~~~~

Miezi minne ikawa imeshapita tokea aachane na Mina. Mina akawa anakaribia kumaliza mimba ya miezi 5 kwa wakati huo. Alisharudisha nguvu na afya yake baada ya kuacha kutapika. Angalau akawa anaweza hata kukaa siku nzima hajatapika. Akawa ameshajua ni vitu gani vinamfanya atapike. Akawa mtu wakujiwinda kweli ili asitapike.

Mama Ni Mama Tu.

Siku moja Andy akiwa Dodoma akapata ujumbe kutoka kwa Mina. ‘Sina nia ya kukukera Andy, naulizia hali ya mwanangu. Na ninajua anakaribia kutimiza miaka minne sasa. Tafadhali Andy, naomba niruhusu kumuona mwanangu. Hata hiyo siku ya birthday yake tu. Nimletee zawadi, nimsalimie kidogo, niondoke.’ Andy hakutegemea. Alikuwa kati kati ya kikao, akabaki ameduwaa. Hakujua hata birthday ya Ayan inakaribia. “Nimekosa ngapi!?” Akajiuliza Andy.

Akaadhimia kutomjibu Mina mpaka awe ameweka mipango mizuri ya hiyo birthday. Hapo hapo akatoka na kwenda kumpigia simu mama yake. Birthday ya Ayan yakutimiza miaka minne ni alhamisi hii. Naomba tumfanyie sherehe.” Ilikuwa jumatatu asubuhi. “Mbona babu yake ameshaanza maandalizi! Amewaambia watu wote. Na keki nimeshaenda kuweka oda.” “Nashukuru mama.” Andy akajisikia vibaya sana, lakini angalau akashukuru Mina amemkumbusha, hajaingia aibu.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Mina akaona amesoma ujumbe, lakini hamna majibu. Akanyamaza. Alisubiri siku nzima ili ajue kama anarudi Dar kumuona mtoto wake au la. Akasubiri mpaka usiku. Kwenye saa nne hivi, ujumbe kutoka kwa Andy ukaingia. ‘Itafanyika sherehe yake siku ya jumamosi, Msasani kwa wazazi. Mida ya jioni. Unaweza kuwepo.’ Mina hakuamini.  Akakaa na kuanza kulia.

‘Asante Andy. Ni sawa mimi nikamuona siku ya alhamisi yenyewe ya birthday yake? Kwa muda mfupi tu. Popote alipo, nitamfuata. Angalau nimsalimie na nimpe zawadi yake.’ Kimya. Andy akajua Mina anataka kumuharibia utaratibu. Alhamis hawezi kuwepo Dar, alitaka kwenda ijumaa, ili akae mpaka jumatatu. Na hakutaka Mina ajue kama UTABIRI wake umetimia, kuwa hawezi kuja kutulia, kazi inamlemea.

‘Itatoa utulivu kwenye sherehe ya Ayan akiwa na familia, Andy. Fikiria kwa sasa, mimi niwe katikati ya ndugu zake Ayan, sidhani kama ni sawa. Tutaharibu sherehe muhimu ya mtoto. Bora kuwapa nafasi bila mimi kuwepo kuwakera.’ Hapo Mina alikuwa sahihi hata Andy akaafiki. Lakini atafanyaje na yeye yupo Dodoma! Andy akabaki akifikiria. Mina akajua ndio amekataa. Akaweka simu pembeni, akalala na kumuacha kabisa kama kumpa nafasi yakufikiria.

Asubuhi alipoamka, akakuta ujumbe kutoka kwa Andy. ‘Unaweza kufika siku hiyo ya jumamosi asubuhi pale Msasani. Utamkuta Ayan. Mkapata muda kabla ya sherehe jioni.’ Mina naye akaona ni sawa. Akajua Andy hataki kabisa afike nyumbani kwake kule kwenye apartment. Lakini akaona ni haki yake. ‘Nitafanya hivyo. Nashukuru.’ Akarudisha majibu.

~~~~~~~~~~~~~~

          Mina aliondoka Iringa siku ya alhamisi. Akarudi kwenye hoteli ile ile aliyotumia alipofukuzwa kwao. Kesho yake siku ya ijumaa akaiita siku ya kujisafi. Alikwenda kuoshwa miguu na kupakwa rangi. Akabandika kucha nzuri sana, zikamkaa vizuri. Akasukwa vizuri. Hata yeye Mina alijua amependeza. Aliporudi hotelini ndipo akamtafuta shem Pius.

Mina na Pius tena.

Pius alitoka kazini moja kwa moja kwa Mina, hotelini. Alifurahi sana kumuona Mina. “Umekonda lakini ukapendeza. Mtoto anaendeleaje?” “Si nilishakwambia anacheza?” Mina akauliza akicheka. “Uliniahidi tukionana, akicheza utaniruhusu nimshike.” Mina akacheka sana.

“Sawa. Mbona na mifuko sasa?” Mina akauliza. “Zawadi zako na mtoto.” “Asante sana P. Mungu akubariki.” Jina la shemeji walishaliua. “Nilikuwa na hamu ya kukuona Mina!” Mina akacheka kama anayefikiria. “Lakini nikushukuru kwa kutunza ahadi yako yakunitafuta na kutunza mawasiliano kati yetu.” “Na mimi nikushukuru kwa ahadi ya kunitunza vizuri. Nashukuru P. Naishi vizuri, na daktari wa wakina mama uliyenitafutia ni mzuri. Ananisaidia sana mimi na mtoto. Nakushukuru. Asante.” Pius na Mina wakakaa kitandani wakiongea.

Wawili hao ni kuonana tu, lakini walikuwa wakiwasiliana sana. Asubuhi, mchana na jioni. Kila siku. Vikajaa vicheko hapo, kama marafiki wa muda mrefu kukutana. “Umekula?” “Nilikula nikiwa nimechelewa, bado nimeshiba. Wewe unanjaa?” “Nitakwenda kula nyumbani.” “Sawa.” Wakaendeleza mazungumzo.

Katikati ya mazungumzo Mina akashituka kidogo. “Nini?” “Anacheza P!” Mina akamshika mkono na kumvutia tumboni. “Atakuwa mcheza mpira nini! Mbona fujo!” Mina akacheka sana. “Si nilikwambia, akianza kama unasinzia nilazima uamke!” Pius akaanza kumpapasa tumbo taratibu na kwa makini. Akambusu tumboni mara kadhaa. Akashangaa Pius anafurahia sana.

Mina akamuona amepotelea mawazoni akiendelea kumpapasa taratibu. “Utanifanya nilale bwana P! Acha kunibembeleza.” “Basi nenda kaoge kabisa, upande kitandani nikubembeleze mpaka ulale.” Mina akacheka. “Kweli?” “Kweli, nitakusubiri.” Akasimama kwa haraka kuelekea bafuni.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Pius alikuwa akimtunza kwa kumtumia mapesa haswa. Na ni yeye Pius ndiye aliyemuomba waache kuitana shemeji. Ndoa ilishakufa. Na talaka alishapewa! Akamwambia wasiitane shemeji. Mahusiano mengi yakawa yakubembelezana kwenye simu. Mpaka akamvutia Mina na kumbadili hisia kabisa. Kwa kuwasikiliza kwenye simu, wazi ungejua mambo yameshabadilika. Zipo hisia zingine kabisa katikati yao, japo hawakuwa wameambiana kwa simu.

Timing…

Wanasema timing is everything.  Ndicho alichokuwa akifanikiwa nacho Pius. Alijua kusoma majira na nyakati ya kila kitu mpaka kuweza kupata kila kitu anachokitaka, nakufanikiwa pande zote. Alijua kusoma watu na mazingira. Andy akiwa amemuacha Mina, tena kikatitili kama hawara tu, yeye Pius ndio akaingia ndani ya picha. Akaziba pengo la Andy kwa upande wa matunzo na kujali kwa kila namna. Kisha akaziba pengo la mama Ron kwa haraka sana, kwa kumjali sana Mina huku akimfariji na kumtafutia matibabu mazuri.

Kwa hasira, WOTE wakamkosa Mina, wakiwa wamemzira, lakini Pius aliyebeba siri ya dhambi ndani yake, akajishindia Mina kiulaini na kujihalalishia juu! Talaka kapewa. Mina si mke wa mtu tena, halafu amembebea mtoto wake! Pius akajihalalishia Mina. Na hivi alishaonja asali, akakusudia kujenga mzinga kwa garama yeyote ile.

~~~~~~~~~~~~~~~~

 Akaoga harakahara, akatoka na nguo yakulalia. Nzuri tu. Pius akimtizama. Akajua usiku huo hata akiomba penzi, atapewa tu.

“Bado hutaki kujua jinsia ya mtoto?” Pius akauliza taratibu tu. “Naona haina maana. Kwangu mtoto ni mtoto tu. Sina uchaguzi. Atakayekuja ndio huyo huyo.” “Ngoja mimi nimuulize mwenyewe.” Akaenda pale aliposimama Mina, akamvutia kitandani. “Si naruhusiwa kuuliza?” Pius akauliza taratibu. Mina akacheka akitingisha kichwa kukubali akiwa amejilaza hapo kitandani, amejiegemeza kwenye mto.

Pius akaanza kumpapasa tumboni huku akiongea na huyo mtoto. Juu ya tumbo, chini. Juu karibu na matiti kabisa, chini kabisa. Mina ambaye mwili huo haukuwa umeshikwa na mwanaume akiwa na fahamu yake karibia mwaka, akalegea kabisa hapo kitandani.

Pius akajua ameridhia. Akaenda kumbusu midomoni. Akashangaaa Mina anamkumbatia kwa nguvu zote. Pius akachangamka, kama aliyeokota lulu. Yakaanza mapenzi. Pius alimtoa nguo zote na kuzitupa mbali kama hazitakiwi tena. Akatoa zake kwa haraka. Mapenzi yakaendelea hapo Mina akimkumbatia kwa hisia zote.

Pius mwenyewe hakuamini kama Mina na tumbo lile angempa ya ukweli kiasi kile. Mina alijitoa hapo kitandani akilipa fadhila. Alijitahidi kumfurahisha Pius, Pius akabaki akilia kama mtoto. Mina alihakikisha anamfurahisha na kumshukuru kwa maneno mbali na hivyo vitendo. “Hii ni kwa kunitunza mimi na mtoto.” Akajituma tena na tena, ndipo sasa Pius akarudisha kumfurahisha. Ilichezwa mechi hapo, kama wanao gombania kombe la dunia! Kila mtu akatoa ujuzi wake kwa kujinafasi mpaka wakaridhika. Alirudi kuoga tena, akambembeleza mpaka akalala ndipo akaondoka akiwa amemuacha amelala.

~~~~~~~~~~~~~~

Jumamosi asubuhi sana, Pius akarudi tena hapo hotelini. Ikaanza romance ya nguvu iliyoambatana na mapenzi jingine tena. Wakaendelea hapo, Pius akishindwa kutosheka mpaka kwenye mida ya saa tatu asubuhi, ndipo Mina akamwambia anataka alale kidogo kabla ya kuondoka kwenda kumuona mtoto wake.

Akamshukuru, akaondoka akiwa na tumaini na penzi la kudumu la Mina. Kwani safari hii alimpa penzi kwa akili yake timamu, na alimuonyesha ni WAKE, hawezi kumnyima. Pius akafurahia juhudi za kumtunza, zimemlipa. Ataendelea kumfaidi Mina bila shida wala kipingamizi. Akamuacha amelala akijua watajipanga zaidi baadaye.

~~~~~~~~~~~~~~

Huwa Mara nyingi, Maisha ya wazazi huendelea baada ya Talaka, wanabakia watoto kuwa wahanga, wakilipa gharama ya maamuzi ya wazazi wao.

Huachwa kwenye majumba makubwa na ya kifahari, lakini wakiteseka.

Ndicho kinachompata Ayan. Baba yake anaendelea kukimbizana na ndoto zake, mama yake anafarijiwa na Pius, yeye ameachwa akimangamanga kwenye majumba ya watu akiteswa.

Inaendelea….


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment