Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 28. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 28.

Maisha Mapya baada ya Talaka na kufukuzwa nyumbani.

Mina alikuwa amechoka, hana hata akili yakufikiria. Alichofanya ni kutafuta nyumba ya kulala wageni yenye choo humo humo ndani, akaingia humo na kuanza kutapika. Asingethubutu kwenda kwa ndugu yeyote, kuogopa kumfedhehesha mama yake zaidi. Alijua jina baya alilonalo kwa ndugu.

Kwanza akajua watafurahi ameachika na utabiri wao umetimia kuwa Mina, hatawahi kutulia kwa mwanaume mmoja. Akaona atulie tu hapo hotelini. Akaendelea kutapika na kurudi kitandani. Akakuta Pius amemtumia pesa nyingi, na ujumbe kuwa ahadi yake ipo pale pale. Akiwa na shida yeyote amtafute. Akaanza kulia.

Pius!

Akalia hapo asiamini kama bado Pius anaweza kuendelea kumjali, tena baada yakumpuuza takribani mwezi sasa! Akajisikia vibaya kuona alimtupa Pius na kumpuuza vibaya vile! Aliacha kupokea simu zake kabisa ila kuwa akimtumia ujumbe kuwa yupo kwenye simu na Andy. Baada ya muda akajua ujumbe umemfikia, kwani aliacha kumpigia simu za mara kwa mara. Ikawa jumbe moja moja akimuulizia kama yeye na mtoto wapo salama. Napo akawa akimjibu kama anayemsumbua tu. Mina akajisikia vibaya sana. Akajuta.

Akaamua kumrudishia ujumbe, ‘Asante na samahani.’ Akamwandikia hivyo tu akautuma ule ujumbe. Akaona simu yake inaita. Pius! Mina akapokea. “Asante kwa pesa.” “Ulipata dawa ya kuzuia kutapika?” “Hapana. Bado natapika sana.” “Uko wapi?” Mina akaanza kulia tena. Akalia hapo, Pius akimtuliza. “Lazima kwenda hospitalini. Huwezi kuendelea kutapika hivyo. Nakuja kukuchukua.” Akamuelekeza alipo.

Baada ya dakika 45, Pius akawa ameshawasili. Ilibidi kumsubiria atapike tena ndipo watoke. Alimshika mbavu wakati akitapika, angalau Mina akapata nafuu mbavuni. Kwani zilikuwa zikimuuma sana kila alipokuwa akitapika. Akamfuta vizuri na kumrudishia nywele zake vizuri.

“Pole sana Mina.” “Asante.” Akashukuru kutoka moyoni asiamini kama Pius yuko naye tena. Alikuwa na kizunguzungu, mpaka kuona giza kwa kutapika siku nyingi bila ya kula. Wakatoka moja kwa moja mpaka hospitalini, Pius akiwa amembeba mpaka garini. Alimpeleka kwenye hospitali nzuri tu. Mina akapata huduma ya kwanza tena kwa haraka. Wakamchoma sindano yakuzuia kutapika na kumuwekea dripu ya maji kwa kuwa alikuwa amekaukiwa haswa.

Sindano aliyochomwa ilimpa usingizi pia mbali ya kumsaidia kuzuia kutapika. Alilala mpaka Pius alipomuamsha kuwa wameruhusiwa. Akaandikiwa na dawa. Pius akanunua hapo hapo hospitalini, akamrudisha hotelini. Akasogeza gari karibu kabisa ya mlango. “Naweza kukubeba Mina.” Mina akaanza kulia tena, lakini akakataa nakumwambia safari hiyo anaweza kutembea.

“Nikuletee chakula gani, kabla hujarudi tena kulala?” Pius akauliza kwa upendo. “Leo naomba nisile kabisa. Harufu ya chakula inanitesa sana. Labda nipumzike tu.” Wakarudi ndani kwenye chumba alichokodi.

Alikwenda chooni kujisaidia, asiamini hajatapika. Akapanda kitandani bila hata kubadili nguo. Pius akamsogelea, akamfunika vizuri na kukaa hapohapo kitandani akaanza kumsugua mbavuni taratibu. Akamuona anasinzia. “Asante.” Akaongea wakati anapotelea usingizini. Akakaa hapo mpaka alipohakikisha amelala kabisa. Ndipo akaondoka. Alichukua funguo moja, moja akamuachia na kufunga kwa nje.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina alilala mpaka akasikia Pius akimuamsha tena. Tayari ilikuwa asubuhi ya siku inayofuata. “Nilikuwa nimechoka!” Mina akalalamika. “Nenda kaoge, uje ule.” Bila swali, akaenda kuoga, na kusafisha kinywa, akarudi. “Nimekuletea mtori. Kuna limao hapo. Jaribu uone kama utaweza kula.” Mina akajifuta machozi wakati akikaa. Akajimiminia mtori. Akala mtori wote uliokuwa kwenye bakuli akabakisha mwingine. Akamwambia Pius atakula tena mchana.

“Kunywa na hizo dawa, ndipo urudi kulala. Nitakuona baadaye.” “Asante.” Akashukuru. Alikuwa amemletea na chupa za maji. Akasubiri mpaka akanywa dawa, ndipo akaondoka. Akarudi kulala.

~~~~~~~~~~~~~~

Alilala mpaka kama kwenye saa saba mchana, akaamka sasa akiwa na nguvu. Akapata nafasi sasa na kuwaza maisha yake na nini kinamtokea. Aliwaza Mina, bila kupata majibu yakueleweka. Akaumia kuona amefukuzwa nyumbani kwao. Akamkumbuka Ayan. Mina akaanza kulia. Alilia Mina bila kunyamaza mpaka akapitiwa na usingizi.

Pius alirudi mida ya jioni. Akamkuta amejilaza tu kitandani. “Umeshindaje?” Mina akakaa. “Sijatapika tena. Nilikula kile chakula chote na nimeweza kulala. Uchovu umeisha. Njoo ukae hapa.” Akamtaka Pius akae kitandani. Pius akakaa.

Ahadi Mpya kati ya Mina na Shemeji{Pius}

Mina akakaa kimya kwa muda, kisha akaanza. “Naomba nikushukuru kwa kuwa na mimi muda wote. Zaidi kipindi nilichohitaji faraja na msaada. Umekuwa faraja na msaada ambao sikutegemea. Maisha yangu yamebadilika ghafla bila kutarajia na sina majibu. Lakini najua ni mjamzito, baada ya miezi nane nitakuwa na mtoto. Lazima maisha yaendelee. Wapi, kivipi, nafanya nini, hayo yote nimejiambia yatajijibu taratibu kadiri siku zinavyo kwenda. Lakini naona nilazima nichangamke.” Mina akaendelea akiwa ametulia.

“Nashukuru sana kwa kujali na kuja kunipeleka hospitali. Angalau sasa hivi naweza hata kufanya kitu au kufikiria. Asante sana.” “Karibu.” Pius akaitika. “Kesho nitatoka hapa, nikatafute sehemu ya kuishi mimi na mtoto, kama Mungu atanijalia nikija kujifungua salama. Nikishatulia, ndipo nitafute kazi sasa yakuja kumsaidia mtoto au yakututunza mimi na mtoto.”

“Unafikiria kuishi maeneo yapi?” “Sijawahi hata kulifikiria hilo! Ndio inabidi kuanza sasa. Nitakapopapata ndio hapo hapo.” “Unataka nikusaidie kutafuta.” “Hapana shem. Nitakutegemea mpaka lini? Mwisho tutajikuta wote tunakwama kwenye moja. Umeacha kazi na familia yako ili uwe na mimi hapa, kuniuguza. Najua hii haitaendelea daima. Acha na mimi nihangaike mpaka niweze. Naamini nitapata sehemu nzuri tu yakuishi na kazi. Maisha yataendelea tu.” Pius akabaki kama anayefikiria.

“Nina ombi moja na la mwisho kwako.” Pius akamtizama. “Najua nimeondolewa kwenye maisha ya mtoto wangu na unajua mazingira yanayo mzunguka. Tafadhali shem, kila utakapoweza naomba ukamtizame. Ayan ni mtoto mrahisi sana, kwa hiyo ni rahisi pia kumsahau.” “Nitajitahidi Mina.” “Asante.” Mina akawa kama amemaliza, akajifuta machozi.

“Na mimi nikuombe kitu.” “Karibu.” Mina akajiweka sawa. “Usikate mawasiliano na mimi. Kwa lolote na chochote, naomba tuwasiliane kama zamani. Hata ukibadili namba, naomba na mimi niwe wa kwanza kujua.” Mina akainama. Akakumbuka alivyokuwa akimpuuza siku chache zilizopita. Akabaki ameinama akimfikiria kaka huyo. ‘Ni upendo wa namna gani huu!’ Mina akajiuliza.

Pius sio mchovu mchovu. Ni mtu mwenye nyadhifa ya juu sana na familia yake. Kaka mzuri wa kupata mwanamke yeyote yule anayemtaka mbali na Raza. Lakini bado amemng’ang’ania! Mina akashindwa kumuelewa.

“Kingine.” Mina akanyanyua uso kumuangalia. “Pesa isiwahi kuwa tatizo. Nitajitahidi kuwa nikiweka pesa kila wakati. Ni rahisi na salama. Hapatakuwa na maswali.” “Labda kwako, lakini si kwangu. Najua nimewashangaza wengi shem, lakini naomba uniamini shemeji yangu, sija.....” Mina akasita kisha akaendelea.

“Najua ni ngumu kueleweka kwa sasa. Na sitaaminika. Ila nakuomba, kwa imani tu. Niamini shem. Sina mahusiano ya nje ya ndoa yangu. Vile ulivyokuwa ukinikuta nipo nyumbani kwangu wakati wote, ndivyo ilivyokuwa. Hakuna kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia. Hata marafiki walinishinda sababu ya Ayan. Ilikuwa lazima niwepo alipo kwa kuwa niliona ni kama kwenye nyumba za wengi hatakiwi. Ndio maana nilikuwa nikijitahidi sana kupunguza safari za mbali na mtoto wangu, ili niweze kuwa naye. Na nilikuwa nikitoka, endapo ikinilazimu tu. Tafadhali naomba uniamini.” “Naomba nikushauri kitu Mina.” Mina akakubali.

“Narudia tena. Kitendo cha wewe wakati wote kujua ni nini chakufanya, ni hatua ya kwanza na kubwa ya msingi. Kama nimekuelewa, utamtunza mtoto. Si ndiyo? Au utakuja kumtoa?” Mina akashituka sana. “Hapana shemeji! Sitathubutu na Mungu anisaidie. Nitahangaika naye hivyo hivyo. Ila sitaua kiumbe kisicho na hatia!” “Na mimi sitakuacha uhangaike naye.” Mina alikuwa hamuelewi Pius. “Anawezaje!” Akajiuliza bila jibu.

Nitakusaidia kwa kadiri niwezavyo, labda usiniambie. Kwa hiyo kama nilivyokuwa nikisema, weka akili na mawazo yako kwenye hilo. Jiangalie kwa makini sana afya yako. Hilo liwe la kwanza na la muhimu. Utulivu ili usianze magonjwa ya moyo. Tafuta faraja katika hilo, ukijua baada ya muda utakuwa na mtoto wako. Acha kwa sasa kuhangaika kuaminisha watu kwa hili linalokupata. Haimuhusu tena mtu. Halafu limeshatokea, huna chakufanya. Watu huamini kile watakacho. Achana na watu kabisa kujieleza ili wakuamini. Kutafuta ni nini chakujitetea, iwe sio kipaumbele, na usifanye hivyo. Sawa?” Mina akatingisha kichwa kukubali.

“Halafu tunza ujauzito wako vizuri. Hakikisha unakula vizuri na kulala vizuri. Achana na mawazo yakuhangaika kutafuta kazi kwa sasa mpaka ujifungue na mtoto akue kidogo. Mimi nitakuwa nikikuwekea pesa kila mwisho wa mwezi. Hesabu ndio mshahara wako, kazi ni kulea huyo mtoto tu.” Mina akajifuta machozi.

“Na ili usipoteze ujuzi. Fanya kama ulivyokuwa ukifanya nyumbani. Sijui kama uliondoka na laptop yako.” “Ninayo.” “Basi endelea kufanya mazoezi. Ukiona upo tayari anza kutengenezea watu website. Na mimi nikipata kazi au mtu anataka afanyiwe kazi zake nitamtuma kwako. Tengeneza hizo logo, website, kadi za harusi na mialiko mbali mbali. Tena unaweza hata kununua mashine ukawa ukifanyia tu nyumbani, unawatumia ili tu usiboreke.” Mina akalifurahia sana hilo wazo.

“Tafuta mashine ya kuprint, ndogo na nzuri, ya kisasa, utakayoweza kuiweka ndani. Niambie bei yake. Nitakununulia. Na mimi nikiiona kabla yako, nitainunua. Au nikipata mtu anayesafiri nitamwagiza.” Kidogo Mina akatulia. Akaanza kuona mambo yatafanyika tu.

“Nakusihi utulie kabisa Mina.” Wivu wa kuishi mbali na Mina ukaanza kumsumbua Pius. Akaingiwa na wasiwasi wakuwa naye mbali, akaanzisha mahusiano mengine.

“Tulia, weka mawazo yako kwako na kwa mtoto, basi.” Mina akamuelewa. “Nitatulia. Nakuahidi nitatulia. Siwezi kujichanganya tena kwa sasa. Nitatulia shem.” “Basi. Tuwasiliane tu. Swali lolote lile, tuwasiliane. Ukikwama popote pale, nitafute, tutashauriana.” “Asante. Na nitafanya hivyo. Ila usiponisikia kwa muda, ujue ni kwa kuwa nimepumzika pengine nahitaji muda wakujiweka sawa. Nikitulia kabisa, nitakutafuta.”

“Hiyo naichukua kama ahadi ambayo hutaivunja Mina. Nitakusubiri. Naomba usichukue muda mrefu kunitafuta.” Mina akamsogelea. Akambusu shavuni na kumkumbatia. Alilia Mina. Akalia huku amemkumbatia shemeji yake. Pius akawa akimbembeleza tu. “Kila kitu kitakuwa sawa, na utashangaa.” Akambusu tena shavuni na kukaa pembeni. Akaona aende akaoshe uso, akarudi.

“Kesho nitatoka mapema sana kuanza kutafuta pakuishi. Kwa hiyo huna haja yakuja.” “Basi na mimi nitakwenda kuweka pesa ili ikusaidie upate nyumba nzuri na vifaa vyakuanzia maisha.” Mina hakuamini kinachomtokea. Alijua atapata shida,  lakini akajikuta mambo ni mazuri ni kama maisha mengine yalikuwa yakimsubiria NJE ya ndoa yake. Wakaagana, Pius akatoka.

Mina na Makazi Mapya.

Ujasiri ukaongezeka kwa Mina. Anaanza maisha na pesa! Mungu ampe nini! Ilikuwa bado ni mapema tu pale Pius alipomuacha. Akaanza kupigia simu watu aliosoma nao, waliomfahamu akiwa Mina mke wa Andy Ruhinda. Akaanza kuulizia kama wamesikia sehemu kunakodishwa nyumba ndogo. Iwe chumba kimoja, au viwili. Iwe inajitegemea.  Mina alihangaika usiku huo kwa simu, akitaka kujua hata kama kuna mtu anafahamu dalali, lakini mpaka saa tano usiku, hakuwa amepata jibu la kueleweka. Akabaki akiwaza.

Na kote alipokuwa akiwapigia, alijaribu kuulizia kodi walizokuwa wanalipa wao na familia zao. Akagundua maisha ya Dar ni magumu. Wengi wakamshauri labda akakae nje kidogo ya mji ndio itakuwa nafuu. Akabaki akiwaza. Akajiambia ahadi za shemeji, zitabaki kuwa ahadi mpaka ziwe zikitimia. Chochote chaweza kutokea, akabadili mawazo. Akaona wazo la marafiki zake ni jema. Heri akaanze maisha mbali na jiji la Dar.

“Nisije kutapanya pesa ndogo niliyonayo, nikitegemea ahadi.” Akawaza Mina. “Wapi niende?” Swali likafuata. Mina mtoto wa jiji la Dar kama si kwa mama yake basi kwa wanaume. Hakuwahi kuwaza anakula nini wala analala wapi. Mama yake na hao wanaume waliokuwa wakimtorosha kwao ndio waliokuwa wakihangaika naye. Akaja na Andy ndio akamuhamishia kwenye apartment wala asijue analipa kiasi gani.

Sasa yupo mtaani na mimba asiyojua ameipataje! Ameachika, nyumbani amefukuzwa. Lakini maisha lazima yaendelee. Hajui maisha mengine isopokuwa hapo jijini Dar na... Mina akakaa. “Iringa!” Akaongea kwa sauti. Akakumbuka alishaishi Iringa na Omar. Akapapenda japo alikuwa akifungiwa ndani. Alipenda hali yake ya hewa, moyo ukajawa furaha. Akaona huko kutamfaa. Akapanga mipango yake akakubaliana nayo ndipo akalala.

~~~~~~~~~~~~~~

Aliamka asubuhi na mapema kabisa. Akapiga simu mapokezi kuomba aitiwe usafiri. Ilipokuja, akapandisha mizigo yake yote, safari ya kutafuta kituo cha mabasi yaendayo mikoani ikaanza. Akafurahia maamuzi yake, akakumbuka shemeji yake alimwambia kitendo chakujua nini chakufanya wakati wote ndio njia ya mafanikio, hata kama si sahihi, ni heri ajaribu akosee, kuliko kubaki njia panda hajui chakufanya.

Alifika kituo cha mabasi, akapata tiketi yake, wakampandishia mizigo yake yote, mabegi ambayo alikuwa ameshayaandika jina lake na namba ili yasipotee au kuibiwa hata moja. Akamuonyesha kondakta ambaye angekuwepo kwenye hilo basi. Andy alimnunulia masanduku mazuri sana. Akajiambia ndio kiinua mgongo chake alichotoka nacho kwa Andy. Akajicheka. Akataka kufikiria hilo, akakumbuka alivyohusiwa na Pius. Atafute faraja, asiwaze vitu vitakavyomnyima raha. Akatoa mawazo huko. Akapanda basi na kutulia kwenye kiti na kumtumia ujumbe Pius akimtaarifu maamuzi yake kuwa anahamia mjini Iringa.

~~~~~~~~~~~~~~

Hakuwa amekumbuka swala la baridi ya mkoa huo wa Iringa. Basi lilifika mida ya jioni, Mina anatetemeka baridi. Akachukua tena taksii mpaka hotelini na kwenda kujifungia. Kwa hofu ya kuishiwa na hakuwa akitapika, alichukua hoteli ya kawaida sana, tena mtaani kwani hakujua atakuwa hapo kwa muda gani.

Kesho yake akaenda mapokezi kuzungumza na muhudumu wa hapo. Akamueleza uhitaji wake wa sehemu ya kuishi. Akamwambia shemeji yake yupo anamalizia nyumba ndogo ya chumba kimoja cha nje, alimsikia akitaka kukifanyia biashara. “Naomba namba yake ya simu.” “Lakini bado hakijaisha vizuri. Nafikiri amekwama pesa.” Yule kijana, muhudumu akamtahadharisha. “Wewe nipe namba yake.” Yule kijana akamtajia, hapo hapo Mina akapiga.

Huyo mama akapokea, akamwambia ni kweli anayo sehemu. Alianza kujenga. Lakini ameishiwa pesa. “Nimeshafunika juu na inayo madirisha na mlango tayari. Mpaka umeme upo, sema sijavuta maji na choo cha ndani hakijakamilika.” “Naweza kuja kupaona?” “Nipo nyumbani. Karibu. Kama unachukua taksii mwambie akulete mtaa wa Gangilonga. Aje mpaka mwisho kabisa. Mwambie jiweni kwenye nyumba za Kotazi. Nyumba yangu ipo mwisho kabisa. Juu, upande wa kushoto kama unatokea mjini, na ina nyumba ndogo nje, lakini nyuma.” Wakakubaliana, Mina akarudi ndani akajiandaa na kutoka. Akachukua taksii aliyoipata hapo nje tu ya hiyo hoteli.

Yule kijana muhudumu wa pale akamsaidia kumuelewesha dereva taksii, kwa kuwa yeye anapafahamu na ni mwenyeji. Kwa urahisi sana yule dereva akawa ameelewa. Wakaondoka mpaka kwenye hiyo nyumba. Akamkuta huyo mama. Akachukua funguo na kwenda kumuonyesha.

“Mpaka kigeti cha nje nilishaweka.” “Mbona hii ipo tayari kabisa!” Mina akashangaa.   Mina akaingia upande wa choo. Akashangaa. “Hii ni kazi ya siku moja au mbili tu mama yangu. Wewe kama unaye fundi mpigie. Tuandikishane mkataba, mimi nikupe hela, animalizie, kesho au kesho kutwa nihamie.” “Kama pesa ipo, mume wangu ndio mjenzi. Atatengeneza kwa haraka tu.” Hilo likamfurahisha Mina.

Wakaingia ndani ya nyumba ya huyo mama, wakaandikishana kuwa amemkabidhi pesa kwa ajili ya ujenzi hapo, utakapoisha yeye Mina ndiye atakayehamia na pesa aliyompa ndio itakuwa kodi. Wakawekeana saini, Mina akamrushia pesa hapo hapo bila tatizo, akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya siku tatu, Mina akahamia hapo akiwa amesaidiwa na kijana wa huyo mama ambaye alikuwa na gari. Akaenda naye kununua kitanda cha kawaida tu, godoro, meza, kabati na vyombo. Kila alipokuwa akikumbuka kitu, alimuomba waongozane kwenye manunuzi. Mpaka anamaliza week, nyumba ya Mina ikawa inavitu vichache, vyakawaida sana, lakini panakalika. Ndipo akapumzika. Kwa mara ya kwanza akawa na kwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku kumi na nne tokea apelekwe na Pius kwa daktari, Mina akaishiwa zile dawa za kuzuia kutapika. Na zenyewe alikuwa akila kama pipi. Kila akisikia kichefu chefu anameza. Akaishiwa. Siku ya tatu yake, kazi ya kutapika ikarudi vile vile. Akawa hawezi kulala wala kufikiria. Nikutapika tu. Yule mama pale akajua, akamfariji kuwa baada ya miezi mitatu, atakuwa tu sawa. Akawa na kazi ya kuhesabu siku akisubiri hiyo miezi mitatu ya mwanzo wa ujauzito iishe, apumzike kutapika.

Kwa Andy.

Huku kwa Andy yeye, siku aliyomrudisha Mina kwao, alitoka hapo akiwa amejawa na hasira, na aibu juu. Akikumbuka jinsi alivyoonywa na mama yake asimuoe Mina, akakimbia naye mpaka Kenya na kwenda kumuoa huko! Alikuwa akiendesha huku akifikiria hili na lile, roho ikimuuma sana. Akakumbuka hili na lile nakuzidi kuumia. “Yaani mimi nahangaika huko, Mina anafanya umalaya, tena bila kinga!” Andy akazidi kukasirika huku maneno aliyojazwa na dada yake yakijirudia kichwani.

Akaendesha mpaka kwa dada yake ambako yupo mtoto wake. Akafika hapo ilikuwa inakaribia saa nne usiku. Kila mtu amelala kasoro Paulina. Akamwambia Ayan alishakwenda kulala. Akaomba mchukue hivyo hivyo. Paulina akamuamsha na msichana wa kazi, Andy akashukuru na kuondoka nao wote wawili.

Alirudi nyumbani asiamini kama Mina hayupo pale. Lakini akajifariji angalau yeye na mtoto wake watalala pazuri bila kelele ya kutapika. Alishamsikia Mina akitapika, akajua uwepo wake pale ndio ungemkera zaidi. Heri alivyomtoa usiku uleule.

Akaenda kumlaza mtoto wake chumbani, akamkuta yule msichana kwenye makochi. Akashindwa kuelewa. “Kwani wewe ulikuwa ukilala wapi?” “Hapa kwenye makochi japo dada aliniruhusu niwe nalala chumbani kwa mtoto. Alisema hamna neno, lakini mimi napenda kuangalia tv. Nikiamka hata usiku au asubuhi, nawasha, mwenyewe naangalia. Hapa nilikuwa nasubiri patulie, nirudi kulala hapa kwenye makochi. Na..” Andy akaondoka kama ambaye ametosheka na hayo maelezo. Mamu alikuwa muongeaji haswa.

Andy akatoa mizigo yake yote kwenye gari akawa anapandisha juu. Yule msichana ametulia kimya akimtizama tu. Hakumsaidia hata kwa kujisogeza. Andy akaingia chumbani kwake na kufunga mlango. Mamu akajua ndio amekwenda kulala, akawasha tv mida hiyo kwenye nyumba hiyo ya vyumba viwili tena ndogo tu.

Andy akaenda kuoga, akatoka wakati anavaa nguo za kulalia, akagundua hiyo tv kweli imewashwa usiku huo. Akanyamaza. Akasema labda itazimwa, atoe nguo kwenye masanduku aliyotoka nayo safari apange kabatini mpaka Mamu alale.

Andy akakutana na zawadi nyingi alizokuwa amemletea Mina. Akaumia sana. Akaanza kazi ya kuzirudisha ndani ya begi. Zote za Mina akaweka kwenye hilo begi na kusukumia uvunguni mwa kitanda. Alitumia pesa nyingi sana kwa ajili ya zawadi za Mina. Ilikuwa ni kama kumshukuru na kumpa pole ya upweke.

Mpaka saa saba usiku tv ilikuwa inatoa tu sauti. Akatoka, akamkuta Mamu ametulia kimya anaangalia kama ndio pamepambazuka. “Siwezi kulala na kelele za tv.” “Naweza kupunguza sauti.” Mamu akamjibu bila hata shaka. Akachukua rimoti, akapunguza Andy akimwangalia. “Hiyo sauti  hapo pia itakukera!? Maana ni kama nimebakisha tano tu! Au nayo unataka nipunguze?!” Mamu akamuuliza Andy yaani kama anayemuingilia kwenye maisha yake, Andy akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Asubuhi Andy akaamshwa na sauti ya mtoto wake anaongea kitandani. Akajua amemka. Akawa anasubiria kuona kama Mamu atamtoa hapo. Ayan akaongea hapo weee akiendesha magari yake hapo kitandani, kisha akabadilika akaanza kumuita mama yake. Andy akaona atoke tu. Akamkuta Mamu amelala kwenye kochi, kavua shati, amejifunika kanga, hana habari utafikiri ndio usiku wa giza nene!

Akapitiliza chumbani kwa Ayan akamkuta amesimama. Akajua njaa ndio inayomfanya asimame mpaka atake kuruka kitandani. Tayari ilikuwa saa nne asubuhi. Kitanda chake kilizungushiwa mbao za urembo kama kulinda asianguke. Akamtoa kitandani kwake.

Akaelekea jikoni. Akafungua friji. Akakuta uji. Akajua ni wa siku zilizopita. Ulifanana na mapishi ya Mina. Akajua ni Mina ndiye aliyepika, ulipobaki akauhifadhi humo. Ayan alionekana na njaa, hawezi kusubiri. Akampashia moto huo uji, akamwambia akae kwenye meza, akaanza kumlisha mpaka akamaliza. Lakini Ayan akawa akimwangalia kama hamuelewi vizuri au anayemfananisha. Andy akajua.

~~~~~~~~~~~~~~

Hawakuwa wameonana kwa muda wa miezi 4 na hata alipokuwepo hapo hawakuwa karibu kihivyo. Hata kipindi cha mwisho alipokuwa naye, wakati Mina anafanya mitihani, Mina alikuwa akimlisha mtoto wake na kumfanyia kila kitu ndipo anamuacha na baba yake anakimbilia kufanya mitihani akimaliza anarudi haraka nyumbani.

Wakajikuta wote ni wakimya. Ayan anakuwa kimya, na baba yake anakuwa na shuguli zake. Kama hayupo kwenye simu basi ana mambo yake kwenye kompyuta. Ayan akiona baba yake yupo busy, anaelekea chumbani kwake kuchezea magari mpaka amuite au mama yake arudi kutoka shule. Kwa hiyo hawakuwa karibu kihivyo.

~~~~~~~~~~~~~~

Ayan akabaki kimya hapo mezani akila, akimtizama kama anayemfikiria. Alipomaliza tu uji, akamuomba baba yake maziwa. Ndivyo alivyozoea huyo mtoto. Kila chakula, lazima amalizie na maziwa. Hapakuwa na maziwa. “Hamna maziwa.” Ayan akamtizama baba yake kwa muda, akamuona anashuka kwenye kiti. Akaelekea kwenye friji. Andy akasimama. “Huko kwenye friji pia hamna, Ayan. Twende tukanunue.” Andy akamsafisha, wakatoka hapo. Mamu amelala hata hajageuka!

Wanarudi, ilishakuwa saa sita mchana. Mamu bado amelala. Ikabidi amuamshe. “Kwani sasa hivi saa ngapi?” Akamuuliza Andy. Andy hakumjibu, akaendelea na shuguli zake. Kumuogesha Ayan huku akifikiria pengine Mamu ataanza kupika chakula cha mchana. Na yeye akaoga wakati Ayan amekaa chumbani kwake, akichezea magari yake.

Andy akatoka, Mamu amekaa kochini. Akamdaka. “Nilikuwa nakusubiria unipe pesa ya chakula, nikale.” Andy akabaki akimtizama. “Mwenzio dada alikuwa akinipa hela nikale huko huko kwa kuwa humu ndani alibadilisha utaratibu, akaacha kupika. Akawa hataki kupikwe tena. Kwa hiyo nikawa naenda kula chips.” “Kwani wewe kazi yako humu ndani ni nini?” Andy akamuuliza.

“Si kazi za ndani! Lakini dada alikuwa akipika mwenyewe, na mwanae ana muhudumia mwenyewe. Nikajua ndio utaratibu wake. Kila nyumba ina utaratibu wake, inategemea na huyo tajiri. Sasa dada wa hapa yeye nili..” “Subiri kwanza. Unaongea sana unanifanya nashindwa kufikiria.” “Mbona nilikuwa nakujibu tu! Labda kama hupendi...”

“Nimekuomba unyamaze kidogo tu. Haya, kwa kifupi sana, nani amekuleta hapa. Taja tu jina bila maelezo.” “Unamjua yule Raza?” “Kwa hiyo umeletwa hapa na Raza?” Andy akauliza akitaka kufupisha habari.

“Hapana! Yaani Raza, ni kama ndiye ninayefahamiana naye mimi. Ndio akaniambia kuna mama anataka mfanyakazi, kwa kuwa mfanyakazi wake ame..” Andy akafunga macho. “Nani amekuleta hapa?” “Si ndio nakujibu sasa?!” “Tafadhali nipe tu jina.” “Ndio hivyo! Raza akanipeleka kwa mama yake mkwe, ndio mama yake mkwe akasema hapa pana uhitaji kuliko yeye, ndio akanileta hapa. Tena wakati huo mkeo alikuwa kavunjika mguu. Hana ile hali yake..” “Wazazi wako au ndugu zako wako hapa karibu?” “Unamjua mama yake wa kufikia Raza?” Andy akaondoka.

Akatoka kabisa pale akaenda kumpigia simu mama yake. “Shikamoo mama.” “Marahaba. Vipi safari?” “Ilikuwa nzuri tu. Naomba nikushukuru kwa msaada mliokuwa mkimpa Mina zaidi kumlea Ayan.” “Mkeo alikuwa akihangaika naye huyo Ayan yeye mwenyewe, Andy. Msaada ni kidogo tu.” Andy akatulia kidogo kama tena anachanganywa.

Ila akaendelea. “Nilikuta msichana wa kazi hapa. Lakini nafikiri hapa ni padogo sana na mimi nipo mwenyewe. Sidhani kama ni sawa kuishi hapa na msichana kama huyu. Si sawa.” “Umewaza vizuri. Unaweza kumleta tu hapa, nitamrudisha kwa Raza.” “Asante.” Andy akaaga na kurudi ndani.

“Una mizigo yeyote hapa?” “Kijibegi tu hapo chumbani kwa mwanao.” “Ulishakaa humu ndani siku ngapi?” Akaanza kuwaza. “Mmmh!” Akaguna Mamu. “Wala si muda sana. Ni kipindi kileee...” “Umeshamaliza mwezi?” Andy akauliza tena akitaka kufupisha habari. “Nahisi. Kwani vipi?” “Nataka kukulipa, nakurudisha kwa mama. Kwa sasa hivi mimi sihitaji msaada wowote humu ndani.” “Sawa.” Mamu akanyanyuka bila shida akaenda kuchukua kibegi chake.

“Sasa unanirudisha na njaa!? Maana sijala.” “Naamini kwa mama kutakuwa na chakula.” Andy akamuita Ayan, akamwambia wanakwenda kwa babu. Wakatoka. “Si ungenipitisha hapo nikanunue hata chips yai! Au unaona nitakuchelewesha?” Mamu akamuuliza. Andy kimya. Akafungua gari. Akamfunga mtoto wake mkanda, akamwambia apande. Hakumjibu mpaka walipofika kwa wazazi wake ndipo akamwambia ashuke.

Hakumkuta mama yake mida hiyo ya mchana. Akampigia simu kumwambia amemuacha hapo, na kama kuna malipo yeyote yale, amalizane naye, yeye atamrudishia. Hakutaka hata kuzungumza na Mamu tena. Akaondoka na mwanae baada yakumchukulia maziwa hapo. Uzuri wa Ayan awe na maziwa mdomoni. Hutamsikia akiongea. Andy akaenda kununua vitu vya kupika hapo ndani na mahitaji mengine. Alikuwa na likizo ya siku 15, akaona azitumie na mtoto wake wakati akijipanga upya. Maisha yakaanza.

~~~~~~~~~~~~~~

Mwezi wa kwanza ukawa wa hasira sana akimlaumu Mina kumuharibia mipango yake. Kumpotezea muda. Kujilaumu kwa nini aliamini yeye ndio ataweza kumtuliza Mina, mwanamke aliyezoea kuwa na wanaume zaidi ya mmoja kwa wakati mmoja. Akamlaumu wee huku maisha yakiendelea mpaka likizo ilipoisha. Ukweli mambo ya kazini kwake bado hayakuwa yamekaa sawa kama alivyokuwa amemuhidi Mina, kuwa akirudi atatulia sehemu moja na familia.

~~~~~~~~~~~~~~

Ikabidi kurudi kuzungumza na wazazi wake, akawaomba Ayan akae hapo kwa muda mfupi tu, wakati anakwenda Dodoma kuweka mambo sawa. Wazazi wakakubali kwa makubaliano ya kumuongeza msichana wao wa kazi mshahara ili angalau Ayan aangaliwe na msichana wa kazi wakati Andy yupo Dodoma.

Mwezi wa kwanza ukaisha, na wa pili pia. Andy anakuja kila weekend. Anamchukua mtoto wake, anakwenda kukaa nae kwao, jumatatu anamrudisha tena kwa wazazi wake, anarudi zake Dodoma.

Wazazi wakaona siku zinazidi kwenda, hachukui mtoto wake. Hawakumuuliza mbona makubaliano yalikuwa ya mwezi tu. Kimya, wakijiangalizia. Mzee Ruhinda na mkewe ni watu wazima wenye majukumu mazito. Hawashindi nyumbani. Na swala la kusafiri ni kitu cha kawaida sana kwao.

Katikati ya mwezi wa pili wa kuishi hapo, wazee hao wakawa na safari wote wawili. Kwa kuwa afya ya Ayan ilishaanza kuyumba, kwa kukosa matunzo, wakamshauri Andy mtoto ahamie kwa dada yake, wakati anajiweka sawa. Paulina naye akamwambia hamna shida kabisa, msichana wake anapenda watoto, Ayan ahamie hapo.

Ayan akahamia kwa shangazi yake. Mara akakae na baba yake siku za weekend, endapo weekend hiyo atarudi jijini kama hatazidiwa na kazi, jumatatu anarudishwa tena kwa Paulina. Mara apelekwe kwa mzee Ruhinda akakae na msichana wao wa kazi, msichana wa Paulina akiwa anaumwa au Paulina akisema anampa msichana wake mapumziko. Ikawa FUJO tu, huyo mtoto hajulikani ataamkia nyumba ipi.

~~~~~~~~~~~~~~

Andy akaanza kumkumbuka Mina. “Aliwezaje kusoma na huyu mtoto!” Akajiuliza Andy. “Hata huo uhuni alifanya saa ngapi na kumlea huyu mtoto muda gani!” Hapo Andy akajiuliza na kumpongeza Mina. Ayan aliyekuwa na mama yake sio huyu! Alikuwa amekonda haswa. Ungejua wazi HANA matunzo.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo Pius alipita kwa waazazi wake kuangalia nyumba, akamkuta Ayan na msichana wa kazi. Kwanza akashangaa. Ayan alikuwa amebadilika, amekonda, ametulia peke yake kwenye kochi. Msichana wa kazi naye na shuguli zake. Pius akaumia sana. Akamkumbuka Mina na kile alichomuomba rasmi. Akampigia simu Andy kumtaarifu atamchukua Ayan kwenda kuishi naye kwa muda mpaka wazazi warudi hapo. Andy akamshukuru na kumruhusu.

Raza ni mkali haswa. Hataki ujinga kwa mtoto wala mkubwa. Ukizingatia ni Ayan, mtoto wa kiume ambaye yeye hakujaliwa, chuki yake ikawa waziwazi. Pius akawa anajitahidi kumuhudumia yeye mwenyewe kwa kadiri anavyoweza. Napo akashindwa. Nyumba mwanamke! Raza akazidi kumlalamikia kuwa lazima Ayan aondoke pale, kabla msichana wao hajaondoka  kwa kulemewa na malezi ya ziada ya huyo mtoto ambaye hakuwa kwenye makubaliano naye tokea mwanzo. Raza akasema watoto wake yeye, au wao ndio wataishia kulipa gharama ya umalaya wa Mina. Raza akaweka mguu chini, hamtaki huyo mtoto hapo kwake. Pius akasalimu amri.

Kwa shingo upande akijua uvivu wa Paulina, maana hata watoto wake yeye mwenyewe wanalelewa na mumewe Devi, ikabidi kumrudisha tena kwake. Ayan akawa mtoto wa kumangamanga. Leo yupo Msasani kwa babu na bibi yake akilelewa na mfanyakazi, kesho Kinondoni kwa shangazi yake, kidogo anarudishwa Mikocheni kwa Raza, Pius akijua atawahi kurudi nyumbani anaenda anampitia popote alipo Ayan, anakwenda naye kwake. Dad wake akifanikiwa kurudi jijini Dar, anamfuata huyo mtoto alipo. Anakaa naye siku mbili, anahamishwa nyumba nyingine, dad anarudi kazini Dodoma. Maisha yanaendelea.

~~~~~~~~~~~~~~

“Mwenzio mama alikuwa akimchapaga Ayan. Usimuone mdogo hivyo, mama anasema anachapika sana.” Mtoto mdogo wa Raza akamwambia babu yake alipomkuta amekaa na Ayan. Babu yake akanyamaza akishangaa moyoni vile huyo Ayan alivyo mkimya, unawezaje kumchapa! “Halafu kama hivyo unavyompa maziwa hivyo, mama alikuwa anasema dada amchanganyie na maji. Asinywe maziwa peke yake, ni gharama.” Akaongeza huyo mtoto.

 “Babu! Si na wewe unajua maziwa ni gharama sana? Hata mama mwenyewe hanywi chai ya maziwa vizuri sababu ya ugumu wa pesa.” Mzee Ruhinda akajua hayo ni maneno ya mama yake sio yule mtoto. Mzee Ruhinda akamtuma maji ya kunywa ili kumtoa kwenye hayo mazungumzo.

Mzee Ruhinda akaumia sana lakini asijue atamsaidiaje huyo mtoto. Baba yake haonekaniki kuwa na dalili ya kutulia na mwanae. Ayan afya yake inazidi kubadilika na yeye majukumu yake yanazidi kumsonga. Yeye na mkewe wakajiambia labda kwa kumpeleka Andy shule za bweni huko Nairobi kumemuathiri. Haoni shida kumuacha mtoto wake kwa watu. Wakashangaa hata hiyo afya yake haimshitui! Ila wakaamua kunyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~

Tembo Wakigombana, Manyasi Ndio Huumia.

Inaendelea…..


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment