Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 26. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 26.

Hali ilipozidi kuwa mbaya na kushindwa kutulia ndipo ikabidi amtafute mama yake. “Nina umwa mama, naomba uje tukae wote kwa muda.” Mama yake akasafirishwa mpaka mjini. Pam akaenda kumpokea. Hakuamini. “Una mimba ya kuzaa!” Pam kwa mara ya kwanza akalia. Alilia sana. Na mama yake alimjua ni jasiri kuliko Eric.

Akamchukua na kumrudisha nyumbani. Uzuri Mill alimletea mama yake vifaa mbalimbali vya kutumia. Haikuwa shida tena kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Anaweza kujisaidia mwenyewe kwa vitu mbalimbali. Na ni mpishi mzuri sana.

Pam akamsimulia juu ya Mill. Hata mama Eric hakuamini. “Haiwezekani Pam! Mill!?” Ikabidi na yeye amfungulie Instagram, amuonyeshe mama yake ndipo akaamini. “Alinifungia simu zangu. Nikajua amepatwa na tatizo pengine simu ikapotea. Sikujua kama ndio amenifungia kunikwepa! Kumbe yupo mzima, na anawasiliana na watu wengine kama kawaida. Ni mimi tu. Silali mama! Nina pressure haishuki.” Akamuelezea mama yake kila kitu.

Ikabidi sasa mama Eric yeye kujikaza ili awe msaada hapo. Wakaanza kulala pamoja. Usiku walalapo, na kumshika kama kumfariji, angalau Pam akaanza kulala na kutulia. Kazi hana, anatumia akiba.

Mama yake akamwambia akiwa hapo nyumbani waanze kupika chapati na maandazi waanze kuuza. “Mama!” “Nilikuwa nikifanya hivyo wakati nyinyi wadogo. Si haba. Unapata pesa.” Wazo likamjia Pam, kwenda kutafuta na kwenye mabaa wanayouza kifungua kiywa. Akajua wanywa supu na mtori watapenda. Akazunguka sehemu kadhaa, akabahatika kwenye  baa moja. Wao wakataka chapati tu.

Mama Eric akaanza kazi ya kupika hizo chapati, kisha Pam anapeleka au wao wenyewe wanakuja kufuata. Wakati mwingine walitaka zaidi. Ikasaidia pesa ya chakula. Maisha na mama yake hapo jijini yakaendelea.

Siku Nazo Hazigandi.

Kufikisha miezi nane na siku chache, mwili wa Pam ukalemewa na kushindwa kuendelea kubeba huyo mtoto mwenye mwili mkubwa kama baba yake. Akajifungua salama tu ila kwa kuchanika haswa. Mtoto alikuwa mkubwa sana na Pam alikuwa akisikia njaa hata baada ya kula. Basi alikuwa na kazi ya kula kama mchwa! Akampa jina la babu yake. Shemaghembe ila yeye akamfupisha na kumuita Shema.

Baada ya siku mbili tu, mtoto aliyekuwa amezaliwa kabla ya siku kutimia akaonekana hana tatizo, Pam na mwanae wakaruhusiwa kurudi nyumbani, mama yake akashika kazi ya ulezi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Ukawa mchana, ukawa usiku. Mtoto anakua kama uyoga! Alifanana na Mill mpaka macho yao na masikio madogo yaliyojikunja kidogo kwa juu. Ilikuwa kama kopi yake kuanzia utosi mpaka unyayo kasoro tu rangi ilikuwa ya mama yake. Pam alikuwa akimwangalia mwanae na kupotelea mawazoni asiamini kama kuna wanaume matapeli kwa kiasi kikubwa kama hivyo Mill, au ni yeye tu na ukoo wao!

Pam hakuwa amesoma shule ndefu sana. Elimu ya kidato cha nne, tena kijijini na pia alifeli. Kazi gani aombe! Akazunguka mpaka akajikuta anaomba kazi kwenye Depot ndogo tu ya familia moja wanayouza maziwa wanayoingiza kutoka kwenye kiwanda cha maziwa huko Tanga.

Wanauza maziwa ya kupima na ya paketi. Mtindi na fresh. Akaanza hapo kazi. Ni maeneo ya Ch’angombe unashukia Veta. Sio mbali na kituoni. Anafanya kazi jumatatu mpaka jumamosi mchana. Saa moja na nusu anatakiwa kufika kazini. Mbili kamili wanafungua milango, anafanya mpaka saa nane, anapokelewa na msichana mwingine. Kijana aliyekuwa hapo ni mmoja wa ndugu wa mwenye hiyo depot, alikuwa hapo muda mwingi. Kama kuwasimamia na kusaidia kuuza kama wakizidiwa. Zaidi mida ya asubuhi na jioni watu wanapotoka makazini.

Angalau akaanza kuingiza pesa. Japokuwa haikuwa nyingi, lakini ilikuwa nafuu kuliko kukosa kabisa. Mama yake akawa anabakia na mtoto nyumbani. Akitoka kazini wanasaidiana na mama yake kupika hivyo vitafunywa. Watu wa kwenye baa wanakuja kuchukua au Pam anawapelekea asubuhi akiwa anaenda kazini. Na karibu na kazini napo pia palikuwa na kimgahawa. Nako akapata tenda. Angalau maisha yakawa yanaenda.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka mtoto ana miaka mitatu, hakuwahi kumsikia wala kukutana na Mill au Mike hata kwa bahati mbaya barabarani. “Kweli Dar kubwa!” Alikuwa akijisemea Pam. Pam alijidharau kupita kiasi. Ule ujasiri wa zamani uliisha kabisa. Alijawa hasira na uchungu wa kusalitiwa. Usingemkuta akicheka kwa furaha.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati maisha yanaendelea, wakisaidiana na mama yake, babu akaugua, ikabidi mama Eric arudi kijijini ila ikabidi ondoke na Shema kwa muda ili mama yake afanye kazi.

Lakini Pam akashindwa. “Siwezi kulala bila mwanangu, mama.” “Utafanyaje kazi na mtoto utamuachia nani?” Hilo likawa swali la msingi. Ikabidi aanze kutafuta shule ya chekechea karibu na pale. Akahangaika lakini mitaa hiyo bei kubwa. Hata hivyo kodi ilishaanza kumlemea.

Akahama hapo na kupata chumba mitaa ya Tandika. Basi moja tu mpaka kazini kwake na si mbali kama alikokuwa akiishi mwanzo. Lakini nyumba ikawa tofauti na alikotoka! Kwanza ilikuwa uswahilini haswa. Wapangaji walikuwa familia tatu na yeye angekuwa wanne. Na chumba alichopata ni cha uwani wanakopikia wote.

Watu wakianza kupika nje, ndani mnasikia kila kitu au ukiwa ndani wa nje wanasikia japo kukawa kama na ukuta uliozunguka chumba chake na sebule ukafunga huo uzio. Kwamba mlango wa kuingilia chumbani kwake na sebule upo ndani. Unaingia hapo uwani kwa kigeti kidogo kizuri tu, ndipo utakutana na kwa Pam, au unaingilia mlango wa mbele kwa mwenye nyumba. Madirisha yake mawili yapo nje kabisa wanakopita watu huko mtaani, halafu dirisha moja lipo uwani. Taarabu ikipigwa kwa jirani, unazima redio yako, wote mnasikiliza mpaka atosheke ndio na wewe uwashe yako.

Lakini alichokifurahia Pam, waliishi hapo kama ndugu wakipatana sana. Aliona jinsi wanavyolea watoto wao, akajua kwa hakika hapo patamfaa. Kila mtoto wa hapo ndani ni wa kila mzazi. Japokuwa walikuwa na hali za chini kiuchumi, lakini walisaidiana sana. Kama binadamu wengine kulikuwa na kupishana ila na walijua kupatana. Na kwenye ugonjwa wote walibebana na kuuguzana. Hilo akamshukuru Mungu kwa yeye aliyekuwa hana mtu hapo mjini.

Akaenda kijijini kumchukua mwanae, akamuanzisha shule ya chekechea karibu na anakoishi. Basi muda ukifika wakutoka, yeye mwenyewe kama amechelewa, anamuomba mama yeyote hapo anaenda kumchukua mwanae, wanakaa naye mpaka mwenyewe anarudi. Angalau hapo uswahili na huo umoja wao, ukamfaa sana Pam na mwanae. Kazi ikawa inafanyika na mwanae anaendelea kukua.

Muendelezo Wa Mill Kutokea

( MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 30.)

Sasa aliporudi nchini na watoto wawili, maisha ya ugaibuni yakiwa yamemshinda. Uraia aliokuwa akiuhangaikia, aliupata na mafanikio ya hali ya juu. Ukweli Mill alifanikiwa kipesa, kasoro ndoa tu. Malengo mazuri aliyokuwa nayo, ikakosekana njia sahihi ya kuyafikia. Mpaka Kisha alipofanikisha kumpa uraia wa nchini Marekani kwa kupitia ndoa.

Biashara ya nyumba ya kulelea wazee alifungua mjini Maryland zaidi ya tatu. Kisha akawa anaajiri watu kwenda kusaidia wazee aliokuwa akipata, majumbani kwao. Kwa hiyo akawa anaingiza pesa kotekote, tena si kwa kubabaisha kwa kuwa alikuwa akilipwa na serikali upande wa afya kwa wazee hao.

Ndani ya muda mfupi sana, alinunua si nyumba, ila hekali la hali ya juu hukohuko mjini Maryland. Aina ya magari aliyokuwa akiendesha yeye na mkewe, hata wa kazi wa huko walijua weusi hao, WAMEFANIKIWA.

Uzuri alijenga mpaka nyumbani. Alinunua kiwanja, alipoona hakitoshi, akamuhamisha jirani yake hapo na kumlipa zaidi ili anunue na kiwanja chake. Napo akapata kiwanja kikubwa sana, eneo alilopenda yeye, akajenga nyumba muundo uleule kama wa nyumba aliyokuwa akiishi mjini Maryland nchini Marekani. Alichimba kisima cha maji na kuingiza pump za mamilion ya pesa kuvuta maji. Nyumbani kwa Mill hapo Dar hapakuwa na mgao.

Na kwa sababu ya shida ya umeme, akaleta mtaalamu kutoka nchini Marekani. Akaangalia mazingira na nchi nzima. Akaingiza mitambo yake mwenyewe, kimyakimya, nyumba ikawekwa Solar Power. Yaani wakati nyinyi mnaungua na jua. Mnalalamikia jua kali nje, ndio furaha ya Mill. Nyumba yake inatengeneza umeme, kwa jua hilohilo.

Ukifika kwa Mill unaweza sema ni kama hapo kwake kupo mbingu nyingine. Kijani kibichi kuanzia getini mpaka nyuma. Maji yapo masaa 24, mashine zinamwagilia asubuhi na usiku. Umeme wa kumwaga. Na asivyopenda matatizo, akafunga generetor za umeme za nguvu. Hutakatikiwa umeme nyumbani kwa Mill. Akafunga central A/c. Yaani kiyoyozi kinapuliza baridi masaa yote, nyumba nzima.

Akiwa nchini Marekani alikuwa akiagiza thamani nzuri sana za ndani kwake huku Tanzania. Yaani anarudi kuishi na wanae nchini Tanzania, hawaoni utofauti na maisha ya kwao, kasoro tu lugha na mazingira wakitoka kwao.

Maisha ya Mill Nchini Tz.

Kama alivyokuwa amekusudia kumtafuta aliyemuaa Mike. Hakuacha. Kifo cha Mike kilikuwa kikimuuma sana. Maisha yakazidi kukosa furaha bila Mike mtu wake wa karibu sana.

Alitafuta watu wake wa karibu waliokuwa wakimfahamu Mike, pamoja na ndugu zake. “Najua Mike amefariki. Kwenu ni muda mrefu, lakini kwangu na Kamila kwa sababu hatukumzika, tutafanya misa, na tutakusanyika sehemu kama kumuenzi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Akatafuta kabisa sehemu ya kukodi kwa sababu ni kama mali ya Mike ilirudi kwa ndugu. Hakuacha mtoto wala Kamila hakuwa mke, kwa hiyo ndugu walipopokonya kila kitu, hapakuwa na nyumba yakufanyia hiyo kumbukumbu yake, ndio Mill akakodi ukumbi. Pakapambwa vizuri lakini kimsiba.

Akatengeneza picha za Mike, na video zake. Wakachanganya na clips mbalimbali alizokuwepo yeye na watu wake wakaribu kwenye matukio tofauti tofauti. Zikawa zikirushwa hapo ukumbini. Kwengine ni yeye mwenyewe Mike akiongea. Ukawa wakati wa furaha na majonzi wakilia.

Kamila na Colins pamoja na familia yake pia walikuwepo. Marafiki wa tokea sekondari waliokuwa wakisoma pamoja nao pia walikuwepo. Jerry alikuwepo bila Sandra.  Na hao ndugu wa Mike wenyewe ambao walishapoteza mali zote pia na wenyewe walihudhuria kwa wingi tu. Kukawa na kula na kunywa kwa kusaza.

Karibu ya mwisho Mill akatoa TANGAZO lililochanganya wengi. “Mike amekufa lakini bado anaishi moyoni kwangu.” Akaendelea. “Kifo chake kilikuwa cha mateso MAKALI sababu alipewa sumu. Mwili wake kwa ndani uliharibika sana, hakuweza hata kusubirishwa sababu ya kuharibiwa na sumu.”

“Moyo wangu unaniuma, kila nikifikiria mateso aliyopitia kabla ya kifo chake, mtu kama Mike. Mike! Kiumbe kisicho na hatia na mtu, hakika nataka haki itendeke. Nyinyi wote nilio waita hapa ni watu wakaribu na Mike. Na wengine mlikuwa naye siku ya mwisho ya uhai wake.” Akatulia.

“Sasa basi, yeyote atakayeniletea fununu za kweli. Namaanisha taarifa yenye ushahidi juu ya aliyempa sumu Mike. Nitamlipa pesa.” Alipotaja hayo mamilioni ya pesa atakayotoa kwa atakaye muweka muuwaji mwangani, wote walishangaa mpaka Kamila. Hakutegemea kama Mill alikuwa na utayari huo.

Akazua gumzo hapo ndani. “Acha niweke sawa. Hiyo pesa haitakuwa na maswali. Nitakukabidhi bila shida. Ila na mimi nitataka ushahidi, na uwe tayari kwenda mpaka mahakamani kushuhudia hili.” Hapo pakatulia kidogo. Watu WANAFIKI! Wanaweza semana nyuma ya mgongo, lakini si uso kwa uso. Mill akawagundua. Akaona aweke msisitizo. “Namaanisha hivi, iwe na kwa msaada wenu au la, NITAMPATA aliyemuua Mike. Na nitahakikisha ANALIPA. Na Mungu anisaidie.” Akataja namba ya simu yake na nyingine.

Nimeshafungua kesi.” Watu wakashangaa sana. “Kabisa. Sitatulia mpaka nimpate aliyemuua Mike. Namba ya pili niliyotoa ni ya mpelelezi niliyempata na kukubali kufanya kazi na mimi kwenye hili swala. Vipimo vya hospitalini ameshavichukua. Amehakikisha kweli kilichomuua ni sumu aliyonyweshwa. Ameshaanza upelelezi wake. TUTAMKAMATA tu. Asanteni.” Akawashukuru kwa kuhudhuria hapo, na kuruhusu wanaotaka kuondoka wawe huru, wanao pendelea kubaki kula na kunywa, ruksa.

~~~~~~~~~~~~~~

Colins na yeye siku hiyo akapata bahati ya kukutana na Mike. Video alizokuwa ametengeneza Mill, utafikiri Mike mwenyewe yupo hai hapo! Alionyesha nyakati tofauti tofauti za furaha walizokuwa pamoja, nchi mbalimbali akipewo hata huyo mrembo Kamila, yeye Mill, watoto na Kisha. Nyingine wao tu wawili. Mike na Mill. Walionekana ni watu waliokuwa wameshibana sana. Na hata kwenye hizo picha tu Mike alionekana ni mtu aliyekuwa akipenda amani.

~~~~~~~~~~~~~~

Wao walikuwa watu wa mwisho kuondoka hapo. Kamila akapata nafasi ya kumshukuru Mill na kumuomba azungumze naye pembeni. “Ni nini?” “Unakumbuka nilikwambia nitamtafuta yule binti mkubwa wa dada yao kina Luca?” “Ulisema upo naye karibu. Kwema? Maana leo hajatokea!” “Amesafiri kikazi. Lakini Mill, kuna mambo mimi ameniambia jana, tena nilikuwa na mama, ikabidi kuweka spika, na kumuomba mama asikilize.” “Amesema nini?!”

“Ameniambia mke wa Luca ndio mbaya wangu, nisikae nae karibu au nijiepushe naye sana. Niache kabisa kula chochote anachonipa.” “Kwa nini?! Yeye ndiye amemuua Mike!?” “Na mimi nilimuuliza. Akasema alicho na uhakika nacho ni kuua watoto wangu.” Mill akashituka sana.

“Anasema yeye ndiye anayempandikizia hasira mumewe kwamba yeye ndio mtoto wa kiume wa kwanza, kwa nini Mike ndio achukue MALI za baba yao. Nasikia akawa analalamika sana na kusema mwishoe Mike naye atazaa mtoto wa kiume, atamrithisha mali hizohizo, mwisho kabisa mali zote za Luca zitapotelea mikononi kwa Mike na wanae.”

“Zulfa nasema anauhakika kwa asilimia zote, kwa sababu aliyekwenda naye kwa mganga kunifunga kizazi amemwambia.” “Kamila!?” “Mama Colins ni shahidi yangu. Na ninahisi kabisa atakayekuwa amemsindikiza ni mama yake Zulfa mwenyewe, ndio maana Zulfa ameshindwa kumtaja mama yake. Maana yule wifi pia hakuwa amefurahia Mike kusimamia mali ZAO. Anasema anauhakika na akaniambia mganga alimpa dawa, anipe. Kuwa kila mimba nitakayokuwa nikishika mtoto anakufa. Sasa mimi sijui Mill.” Roho ilimuuma sana Mill.

“Una jinsi ya kumuuliza kama ndiye aliyempa Mike sumu?” “Mbona nilimuuliza! Akasema katika hilo hana uhakika, lakini akaniambia mimi nitumie tu akili. Mara ya mwisho sisi tulikuwa nyumbani kwake mama Luca aliyetayarisha chakula, na Mike kuugua mpaka kifo. Akaniambia, mtu anayeweza kuua watoto wa Mike ili wasije kurithi, anashindwa vipi kumuua Mike mwenyewe ambaye amerithi?” “Kamila?!”

“Nakwambia hivyohivyo na mama Colins ni shahidi yangu. Anasema yeye anahisi amesubiria kuona Mike anakufa kwa njia zake nyingine, ila akawa hafi. Anasema anahisi atakuwa pengine pia amejaribu kumuua kwa uchawi akashindwa, ndio akaona bora ammalize kabisa kwa sumu. Tena akasema hivi, huoni walivyoishiwa kwa haraka?” “Unamaanisha nini?”

“Si nilikwambia walinipokonya kila kitu mpaka gari?” “Nakumbuka.” “Sasa Zulfa anasema wameishiwa mpaka wanapikia na kuni hapa katikati ya jiji. Anasema gari walilonipokonya na kumpa mtoto wao yule mkubwa wakiume, unaambiwa nusura limuue. Zulfa anasema eti alishawaambia babu yao, yaani baba yao kina Luca, amekasirika wao kuchukua mali, ndio maana amewapokonya kwa haraka. Unaambiwa ni kama wamepatwa na laana! Ile nyumba waliyonipokonya mimi, Zera anasema imekua kama gofu, mpaka imeoza, hapafai. Mpaka geti hamna.” Mill alishabadilika sura.

“Unafikiri Luca anahusika?” “Na hilo nilimuuliza. Ila yeye anavyomjua mjomba wake alisema anauhakika hausiki. Anasema yeye ni hasira tu, lakini si mtu mwenye roho ya kuua. Na mimi nahisi ni kweli. Maana Luca alidhania eti mimi ndio nimemuua Mike. Akataka kuniwajibisha kama hivyo wewe unavyotaka kufanya.” “Na mimi aliniambia hivyohivyo. Kwa hiyo ni kweli. Hausiki. Lakini Kamila, kama ni mkewe, hakika nitamkamata tu na atalipa kwa yote. Kumnyima Mike watoto na kumuua yeye mwenyewe. Nitapeleleza tu, na nitahakikisha na yeye anapewa kipaumbele kwenye upelelezi wa kipolisi. Usilie, wewe nenda kapumzike. Nitakujulisha.” Kamila alikuwa akilizwa na mengi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Siri ya kuwa Pam alifika kwake na alikuwa mjamzito, hakumwambia hata Mike. Alilificha hilo, asiseme. Hapo anajilaumu kwa mengi, lakini hawezi kusema tena. Alishahisi pengine Mungu anamlipiza KISASI kwa alichomfanyia Pam, kwamba Mungu ndiye aliyekuwa akimuulia kila kiumbe aliyebeba yeye.

Akamfanya Mungu ni mdogo, eti kumuadhibu kwa kosa la kuficha kama Pam anamtoto aliyejua wazi atakuwa ni wa Mill. Akahukumiwa kumficha Mill aliyekuwa nao yeye na Mike katika shida na raha bila kuwachoka. Mpaka sasa hata Mike hayupo bado anamjali. Akajisikia kuhukumiwa lakini hapakuwa na jinsi ya kujirudi. Akanyamazia tu akijua kwa hakika hawezi kuja kumpata Pam. Kwanza miaka mingi ilishapita. Akajua kwa wakati huo Pam atakuwa na maisha yake, hana habari naye.

~~~~~~~~~~~~~~~~

“Umefikia wapi kumtafuta Pam?”  Akaona aulize tu. Mill akijua ana nia njema kumbe analake, anataka kuepusha kikombe. “Aisee sijampata! Nilikwenda alipokuwa akiishi zamani. Hawajui hata namzungumzia nani! Nimekuta wapangaji wengine kabisa na wenyewe hawana hata mwaka hapo.” “Kwao?” “Huko Lushoto!?” “Namaanisha hapa Dar.” Kamila akaendelea kudodosa.

“Ni kama nilichangia kuharibika kwa mahusiano yake na mke wa mjomba wake kabisa. Alikasirika sana kitendo cha sisi kwenda kulipa mahari kijijini aliko mama yake Pam, wakati anasema ni kama Pam nilimtoa kwake na malalamishi mengi. Nimeshindwa kwenda.” “Jerry anasemaje?” “Anasema hana taarifa zake zozote. Alikutana naye mara moja tu kama alivyosema,  tena zamani sana. Mbali ya salamu anasema hawakuzungumza na hajamuona tena. Ila bado sijakata tamaa.” Akaongea Mill akifikiria. Hapo akamtia hofu Kamila. Alijua angekata tamaa, ila bado anania ya kumsaka! Akaona aondoke.

Cha Mtu Mavi!

Mina aliuguza huo mguu akiwa na msichana wa kazi akimsaidia. Aliletewa na mama Ruhinda. Akawa kitandani tu akimtuma hiki na kile. Pius akakosa sababu ya kufika hapo mara kwa mara, uhuru wa kuwa hapo kwa Mina, hakuna tena sababu ya huyo msichana wa kazi, na mama Ruhinda kupita hapo mara kwa mara.

Siku ya tano yake akamkumbuka sana Andy. Akatamani kama angekuwepo pale. Akalia kuanzia anaamka asubuhi mpaka mchana, akaamua kumpigia kwa video akiwa amejilaza na mtoto wake kitandani.

 Haikuita hata mara mbili Andy akaipokea kwa haraka. Mpaka akamuona Andy anafuta machozi wakati anawaangalia. Mina akamuhurumia. Alishindwa hata kuzungumza. “Andy!” Mina akaita kwa upendo. Andy akabaki akifuta machozi. “Niliumia mguu mwenzio!” Mina akaongea kwa kulalamika.

Andy akafuta tena machozi. “Pole. Nini tena?” “Niliutengua kwa bahati mbaya.” Akamuona anafunga macho. “Lakini sasa hivi naendelea vizuri.” “Sasa nani anakusaidia wewe na mtoto?” Andy akauliza kwa kuumia sana. “Mama Ruhinda alinitafutia msichana wa kazi. Sasa hivi ndio naishi naye hapa.” “Pole Mina. Pole sana mpenzi wangu.” “Asante, unamuona Ayan?” “Mbona na yeye amelala au mgonjwa?” “Mzima kabisa. Atakuwa amesinzia tu. Babu yake alipita asubuhi, amemnywesha uji vizuri tu, ndipo akaenda kazini.” Andy akanyamaza kidogo.

“Kwa heri. Nilitaka kukusalimia tu.” “Nashukuru Mina. Nilikuwa na wakati mbaya, hivi nilikuwa nataka kurudi nyumbani.” Mina akawa hajamuelewa. “Shule imeisha mapema?” “Hapana Mina! Nimeona siwezi kuendelea na haya maisha. Vitu vyote vinakosa maana bila wewe, Mina. Niamini kuwa nahangaika kwa ajili yetu wote. Sasa itanisaidia nini nipate yote haya halafu nakukosa wewe?” Mina akanyamaza.

“Na ninakusikiliza sasa hivi. Ukitaka nirudi, narudi mama. Nimetoka kuangalia tiketi, nimeona naweza kupata ya kurudi huko hata kesho kutwa. Lakini ukiniambia utakuwa na mimi kwa muda huu uliobaki, nitamaliza.” “Umebadilika Andy! Hata naona sikuelewi tena.”

Nitajirekebisha. Nakuahidi. Tutarudia maisha yetu yale ya mwanzo kabisa mpenzi wangu. Sawa?” “Kwa hiyo nikusubiri kwa hamu, safari hii hudanganyi?” “Tafadhali Mina. Usinikatie tamaa mpenzi.” Mina akajifuta machozi.

“Niambie kama bado unanipenda Mina.” “Nakupenda Andy na ndio maana nimetulia kwako tu.” “Nakushukuru kwa hilo. Umekua mke ambaye sikutarajia! Umenivumilia hata pale niliposhindwa kuwa mume mzuri. Umeshika nafasi ya baba ambayo nilipelea sana. Nakushukuru Mina wangu.” Andy akampamba mkewe, mpaka Mina akajisikia vizuri na kujipongeza kushinda nafsi na kumsubiria mumewe.

“Ninahamu na wewe Andy! Nataka unikumbatie tena na kunibusu.” Andy akacheka kwa furaha. “Na mimi ninahamu ya kukukumbatia, kunyonya hiyo midomo yako huku nikifanya mapenzi na wewe.” Mina akacheka sana. “Mtoto anakusikia Andy!” “Acha hizo bwana! Si amelala?” Mina akamuhamishia mtoto kamera. “Amelala bwana! Ila ujue ni kweli. Nilikuwa nataka kurudi.” “Maliza tu Andy. Lasivyo gharama yote tuliyolipa mimi na Ayan itakuwa bure kabisa.” “Unauhakika Mina?” “Ndiyo Andy, nitasubiri. Si bado siku..” “40 mama. 40 tu.” Andy akamalizia. “Basi hizo nitasubiria Andy. Mungu akusaidie urudi salama.” Andy alifurahi sana. Wakazungumza kidogo wakaagana wote wakiwa wametulia. Shida ya Mina ni kumsikia Andy bado anampenda na kumuhitaji. Sasa ashamsikia, Mina roho kwatu. Dhambi zote ameshasamehe.

~~~~~~~~~~~~~~

Nyumbani kwa Mina kukawa na msichana wa kazi, anaitwa Mamu, ambaye anafahamiana kwa karibu sana na mpaka ndugu wa Raza, mke wa Pius. Alitakiwa awe mfanyakazi wa mama Ruhinda, Raza alimtafutia, lakini mama Ruhinda akampa Mina. Alimuita Pius shemeji, na alimfahamu kwa kumuona Pius ukweni.

Kwa hiyo uhuru wakufika pale ukapungua, ikawa kwa simu ndio mara nyingi lakini napo mambo yakabadilika kwa kuwa Andy akarudi pichani kwa NGUVU. Simu kwa mkewe asubuhi akiamka, mchana akila, na usiku akienda kulala. Na lazima awaone. Azungumze na mkewe na mtoto, ndipo wanaagana. Kwa hiyo Mina akawa amerudisha mapenzi kwa mumewe. Pius akipiga simu habari anazopewa ni za Uswiz, alipo Andy. Atamsimulia hili na lile juu ya Andy wake. Hata Pius akajua Mina amerudisha furaha.

Akiwa na shida yeyote ile hapigi tena simu kwa mtu mwingine, ni Andy, mumewe ambaye sasahivi ana muda naye, na simu zake hazisubiri. Anapokea kwa wakati na anamsikiliza mkewe. Andy atambembeleza hapo na kumshauri kwa hili na lile. Mina akapunguza mawasiliano na Pius. Akipiga simu, Mina anaweza asipokee, anamrudishia tu ujumbe. ‘Nitakupigia shem.’ Hapo anaweza kumrudishia hiyo simu siku hiyo au hata kesho yake.

Hilo likaanza kumnyima raha Pius. Akaanza kumkumbuka Mina aliyeonja penzi kwa usiku moja tu. Kila akikaa, anakumbuka jinsi alivyomfaidi mtoto huyo mdogooo, mke wa mdogo wake, lakini Mina mwenyewe hana taarifa hata. Akawa ameshapona, anaendelea na maisha kama kawaida.

Mawasiliano na Andy yakawa ni ya kila mara. Mina akawa akimsubiria kwa hamu mumewe, akiahidiwa hili na lile atakachofanyiwa siku ya kurudi kwake. Siku nazo zikawa zikienda bila shida. Mina anamsubiria mumewe kwa hamu, hana jingine analofanya wala kuwaza. Yeye mawazo yapo kwa Andy.

Yasirini Yaja Mwangani.

Siku moja asubuhi Mina aliamshwa na kichefuchefu kikali, akashangaa sana. Hata alipokuwa mjamzito, hakuwa akitapika. Akakaa. Ghafla kitu kikapanda, akakimbilia chooni. Mina alitapika mpaka akamuamsha Mamu, msichana wake wa kazi. “Dada! Upo salama?” “Hata sijui ni nini!?” Mina akatoka bafuni na kwenda kupika uji wa mtoto wake.

Huko jikoni akapatwa tena na kichefu chefu. Akarudi bafuni kutapika. Kuanzia hapo, Mina akawa na kazi ya kutapika hana anachoweka mdomoni kikapita na harufu nayo ikawa shida. Hataki tena yule msichana wa kazi apike chochote pale ndani. Akawa anampa pesa ya kwenda kununua chips. Tena akale huko huko asije nazo ndani. Mwanae ni uji tu. Hapo Andy alikuwa amebakisha siku kama 8 tu arudi nchini.

Lakini akashangaa hana homa, wala haumwi na kichwa ila kutapika kama mgonjwa haswa. Akajiambia ni hali tu, itaisha. Hata hakwenda hospitalini. Akaendelea na hayo maisha ya shida yakushindwa kula chochote ila kutapika tu.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya siku chache jumamosi ambayo jumatatu yake mumewe alikuwa akirudi, ilikuwa wakutane nyumbani kwa Paulina, aliwakaribisha kina Ruhinda wote kwa chakula cha usiku. Ilikuwa lazima Mina naye ahudhurie na Ayan ambaye babu yake alishapiga simu kuzungumza naye na kumwambia Mina anamsubiria kumuona jioni nyumbani kwa Paulina.

Mina akajiandaa bila hata kupaka pafyumu, na mtoto pamoja na msichana wa kazi, wakatoka mpaka nyumbani kwa Paulina Kinondoni B, karibu kabisa na makaburini. Msichana wa Mina akataka kumbemba mtoto, Mina akamwambia anataka yeye abebe begi la mtoto, yeye atamshika tu mkono atembee, asibebwe.

“Eti kaka mkubwa! Unataka kubembwa.” Ayan akamwangalia mama yake na chupa ya maziwa mdomoni, akacheka tu. “Tembea bwana!” Mina akamlazimisha atembee. Wakaingia ndani. Ule mchanganyiko wa harufu za vyakula pale, Mina akawa amechafukwa haswa. Akawasalimia na kuwaambia atarudi baada ya muda mfupi sana. akakimbilia nje, bila kutaka kuwatia hofu.

“Hapo mwenzenu anaenda kutapika tena, huyo!” Msichana wake wa kazi akaongea kwa kusengenya. Wote wakamgeukia. Mama Ruhinda akamtizama kwa mshangao. Kama anayemuuliza ‘huna hofu!’ Nyumba ilijaa watu wa maana watupu! Kina Ruhinda na watoto wake. Wote wasafi, halafu wakubwa kuliko huyo msichana aliyeongea kama umbea.

“Kwani anaumwa?” Akauliza Paulina. “Ile itakuwa mimba tu! Japo mwenyewe anakataa. Kabla ya kuja huku pia katapika wee, ndio tukaja. Kila siku asubuhi anatapika. Nyumbani hakupikwi, hataki harufu. Ananipa pesa nikale chips, tena gengeni. Nisirudi nazo hapo nyumbani. Hataki harufu. Ana kazi yakumnywesha mtoto wake uji na maziwa kila saa, hataki kupikwe. Mimi nishazaa, najua tapika ya mimba.” Mamu akaongeza bila kumumunya maneno. Pakazuka ukimya wa ghafla.

~~~~~~~~~~~~~~

Maji Yashamwagika…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment