Bado Mill
hakujua chakumwambia Pam mpaka aelewe. Kwanza hata hakuwa amejua kama alioa
huko nchini Marekani. Ilibaki ni siri kubwa sana kati yake na kina Mike.
Moja kwa moja akajua akimwambia yote hayo juu ya Kisha, Pam atajua fika
ndio sababu alikataa ndoa ya kanisani nchini Tanzania.
“Nitamwambia
nini Pam!” Ndio likawa swali lililokosa jibu. “Kwamba
niliombwa penzi kwa nguvu!” Yaani hata yeye Mill akaona itasikika ni sababu
ya kijinga sana. Akabaki akijiuliza bila jibu.
Hata Pam
alipokuwa akimpigia simu alishindwa kabisa kupokea. Mwishoe
akaamua kumblock kabisa kila mahali. Na huo ndio ukawa MWISHO wa kuwasiliana
na PAM.
Aliyafanya hayo
yote akiwa na paniki, hukumu, akasahau historia nzima ya Pam,
vile baba yao alivyowatelekeza wao na mama yao. Na alimuapisha mara
kadhaa asije kuwa kama baba yake, na Mill akaapa kwa mbingu na nchi,
haitakaa ikatokea. Lakini yote hayo yakafunikwa kwenye ubongo wa
Mill, akijua wazi, kwa vile Pam alivyo mzuri, atamtafuta kidogo tu, atachoka
na kuamua kuendelea na maisha yake. Akahakikisha Pam hampati hata kwa
barua pepe. AKAFUNGA hata akaunti ya barua pepe aliyowahi kumuandikia Pam.
Ikawa hakuna jinsi ya kumfikia kabisa.
Kupenda Kubaya!
Asijue
na huku kwa Pam nako aliacha msala mwingine. Kazi ya kumsaka Mill ikaanza.
Wasiwasi ukamjaa akijua pengine yupo matatizoni. Labda ajali mbaya au
ugonjwa umempata mupenzi. Wakumuuliza ni nani! Jerry hajazungumzia naye
tena swala la Mill. Na Jerry alikuwa akimkwepa. Hakutaka aingie katikati
yake na Sandra ambaye wazi alionyesha kumchukia Pam. Sifa zote alizokuwa
akimpa Pam, zikageuka kuwa lawama, sababu maalumu hana.
Wivu kama yeye ndio Lona!
Mwezi
wa kwanza ukapita na wapili nao ukayoyoma bila ya kumsikia Mill.
Pam akawa kama amechanganyikiwa. Si kwamba alizitaka pesa za
Mill, HAPANA. Yeye wasiwasi wake uzima wa Mill tu! Japo kumsikia
ajue yupo mzima. Alikuwa akimpigia simu zaidi ya kawaida. Asubuhi,
mchana, jioni, na usiku. Tena hata usiku wa manane akishituka kutoka
usingizini, basi atampigia Mill.
Za Mwizi
zimefika 40.
Arobaini
zake kwa kina Lona zikawa zimetimia. Akiwa kwenye ile hali ya kuchanganyikiwa
wakajua huo ndio wakati muafaka, wa kumlipiza kisasi. Wakamtega na malipo
hewa. Wakamsainisha kumpa malipo apeleke benki. Wakamshanganyia
hundi na pesa taslimu. Akiwa na mawazo yaliyosambaa, bila ya
kuhesabu, akaweka saini kuwa amepokea pesa kiasi ambacho SICHO. Yeye hana
habari anakimbilia kwenda benki, ilimradi tu atoke hapo ofisini, apate uhuru
huko njiani amtafute Mill kwa simu.
Kuja
kurudi, Sandra anapitia mahesabu yake na ile slip ya benki aliyorudisha,
akagundua upungufu wa pesa. Kumuuliza Pam yule aliyekuwa akimsifia
zamani kabla ya Mill, kuwa ni mwaminifu sana, haibi hata
shilingi, Pam hajui hata anachozungumzia.
Huwezi muibia mwizi. Ndio Sandra. Pesa hiyo
aliyoipata kwa wizi alikuwa akiilinda kama anavyomlinda Jerry na
roho yake. Ikaonekana ni kama
ameiba pesa pale ofisini.
Akifa Nyani, Miti Yote Huteleza.
Ndilo
lililompata Pam. Sandra hakutaka maneno mengi, akampeleka polisi bila ya
kufikiria mara mbili. Na yeye akapata nafasi ya kumlipiza Pam.
Alishafika sehemu akawa ameshakuwa kero kwake. Ilikuwa ukifika hapo
ofisini kwake, unaweza sema Pam ndiye mmiliki. Alijawa neema huyo Pam!
Na alivyo mzuri, Mill alimthaminisha haswa!
Alikuwa na aina
ya marashi, akiwa ofisini kwake hata ukiingia mapokezi mtajua kama Pam
yupo. Ilitulia vizuri mno. Mwanaume mwenyewe aliyekuwa naye, huwezi
mfananisha na Jerry wala Mike. Mill alijaliwa mvuto wa kuanzia sura
mpaka mwili, halafu aliujualia mwili wake. Ukiwakuta na Pam, unaweza
sema walichaguana. Hawana picha wakapiga usitake kutulia na kuiangalia
tena na tena. Kila kitu cha Pam kililia mafanikio. Hicho kilimkera
sana Sandra.
~~~~~~~~~~~~~~
Alipofikishwa
kituo cha polisi, kama wahalifu wote wanaofikishwa hapo kwa kosa hilo la wizi,
usemi wao ni mmoja, “Sijaiba.” Yakawa maneno hayohayo kutoka kwinywani kwa Pam.
Hakuna jipya, akasekwa lupango. Sandra anataka pesa yake.
Japokuwa wote
wanajua mdeni hafungwi, lakini Sandra alitaka tu kumkomoa.
Akasema anaweka fundisho kwa wafanyakazi wake wote, mtu mwingine asije
rudia mfanyia hivyo.
~~~~~~~~~~~~~~
Pam alikuwa
hajui chakufanya, hana msaada. Nyumbani
kwa shangazi na mjomba alishaondoka. Leo hawezi kurudi kuomba msaada wa
swala wizi. Akajua na kwa kaka yake pia asingeweza msaidia hata
kidogo. Kwanza mkewe ndiye mshika pesa yote. Leo anamwambia watoe mamilioni ya
pesa kumlipia yeye atoke jela! Akajua hizo ni ndoto za alinacha.
Akatulia akifikiria chakufanya.
~~~~~~~~~~~~~~
Miezi mitatu
ikapita akiwa jela, nyumbani kwao hawajui kinachoendelea na yeye hakutaka
kusema. Mawazo yapo kwa Mill, hata hajiangalii hali yake. Wakati mwezi wa tatu
unakaribia kuisha, kesi yake haitajwi wala hana anayemtembelea
huko rumande, Sandra akaenda kumuona.
Akamwambia
atafuta kesi ya uwizi endapo atamlipa pesa yake. “Naitoa wapi hiyo pesa
mimi!?” “Uza gari.” Pam akacheka. “Kumbe ndio maana umenifunga! Yaani
wewe unaumwa na gari ambalo halina hata nusu ya thamani ya gari unayoendesha!”
“Sina muda wa kujitetea Pam. Unanipa pesa yangu au la! Jiangalie ulivyo
na ulipo. Unataka uje uzalie jela!” Ndio akili ikamrudia Pam na
kuanza kujifikiria. “Hayakuhusu.” Akamjibu hivyo Sandra kwa jeuri, akamcheka na
kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~
Japokuwa
alijaliwa katumbo kadogo sana kalichobebwa na hips pana na tako la duara
lililokuwa likionekana kwenye kila kitu anachotupia hapo mwilini mwake, mwezi
huo kwenda wa 7 tumbo lilishaonyesha kabisa, kubwa haswa kama anayekaribia
kujifungua, ila ni yeye tu hakuwa akitilia maanani. Ukabaki
mtihani, nani wa kumsaidia angalau kumtoa jela!
Tumbo likazidi
kukua, ndipo akasalimu amri. Akampigia simu mjomba wake. Akamueleza akimtaka
msaada.
Baada ya siku
mbili alifika hapo na mkewe. “Nisikilize Pam. Tushakusaidia vyakutosha. Ni wewe mwenyewe ndio umechezea
maisha yako. Sikukuonya mimi utulie? Ona ulipo? Upo jela na tumbo lisilo
na baba.” Gafla Pam aliyekuwa akijitunza na shangazi yake kujua, tena
wakati mwingine kumtolea mfano hata kwa wanae kuwa ametulia, eti
leo gafla akaonekana malaya!
“Sasa sisi hatuna
msaada wa kukusaidia. Maisha magumu. Pesa yenyewe hakuna. Kama unataka
uza vitu vyako.” Ushauri uleule aliokuwa ametoa Sandra. Akaona hamna
jinsi. Walipoondoka tu hao, akampigia simu Sandra. Akamwambia amekubali ampe
hilo gari, afute kesi.
Bila aibu,
Sandra akakubali. Alimfuata huko lupango na waraka kabisa. Akamsainisha
kuwa analipa deni kwa hilo gari. Pam kwa uchungu mkubwa, akasaini ndipo akamtoa
jela. Akachukua funguo za gari. Nataka na kadi yake. “Nitakupa.” “Usinitanie
Pam. Zikipita siku tatu sijapata kadi ya gari, nakurudisha jela.” Pam
akakubali bila shida. “Na pale ofisini kwangu nisikuone tena. Kibarua
ndio kimeisha hivyo. Sitaki wizi.” Pam akachukua pochi yake na kurudi
kwake.
~~~~~~~~~~~~~~
Uzuri alilipia
hapo kodi ya mwaka mzima. Alikuta hapajaguswa. Kwa haraka ili asije ishiwa
tena, akalipia tena hapo kodi ya mwaka maana ilikuwa imebakia miezi miwili kodi
iishe. Akajiambia atajifungulia hapohapo. Japokuwa ilikuwa ni chumba kimoja tu
na sebule, lakini alipapenda. Wapangaji wenzie walikuwa wastaarabu.
Hakuna fujo na mambo ya ajabuajabu.
Alilala siku moja
tu kutoa uchovu, kazi ya kuanza kumsaka tena Mill ikaanza. Piga
simu kama mwanzo bila mafanikio. Siku inayofuata akaenda kuanza kliniki.
Sababu ya watu kuwa wengi, alikaa huko karibia siku nzima. Sababu ya wasiwasi,
hofu alikuwa amekaukwa mdomo, amechoka, Pam akarudia
maisha ya daladala, ila safari hii na ujauzito.
Kwa kina
Kamila.
Alitoka mida ya
saa nane mchana akiwa na kadi yake ya kliniki, hata hajala, akapanda
daladala mpaka alipokuwa akiishi Mill, nyumbani kwa Mike na Kamila.
Alifika getini akiwa anatokwa jasho karibia aanguke. Mapigo ya
moyo yalikuwa yakienda kasi kama aliyekuwa akikimbia kumbe ni kutembea
tu juani.
Hata hivyo mimba
ilishakuwa kubwa. Halafu aliambiwa mtoto wake ni mrefu. Mkubwa zaidi ya miezi
yake. Hakushangaa. Mill ni mkubwa sana kama baba yake. Akajua mwanae amechukua
mwili wa kwao. Akafika kwenye kibanda cha mlinzi, bila kukaribishwa, akakaa
chini kabisa mlangoni akijipepea.
“Pole mama.
Karibu.” Mlinzi aliyemkuta akawa mstaarabu kweli. “Ndio nishakuwa mama!”
Akawaza Pam akiwa anajipepea amepakata tumbo lake. Urembo wote uliisha,
ukabakia uzuri wa asili.
“Namuulizia
Mill. Anaishi kijumba cha pembeni humo ndani.” “Mmmh! Simfahamu. Na mimi mgeni.
Lakini mke wa mwenye nyumba yupo. Acha nimuulizie.” Pam akashukuru Mungu.
Akajua Kamila alivyokuwa akimpenda na kumkarimu, basi
atamkaribisha hata ndani, aombe chakula. Maana alikuwa na njaa kali, na kiu.
Akamsikia mlinzi
akipiga simu ya mezani. Ukasikika mlio kwa sauti ya juu tu maana ni simu ya
mezani hapo getini. “Kuna mgeni hapa getini. Amesema anamuulizia..” Akamgeukia Pam. “Mwambie naitwa Pam, namuulizia Mill na naomba
kuzungumza naye.” Kwa tumaini kubwa sana, akamwambia akisimama
kabisa maana alijua jibu ni afunguliwe geti aingie ndani, kama zamani
alivyokuwa akitetemekewa alipokuwa na Mill.
Lakini Pam
HAKUAMINI masikio yake aliposikia, “Mwambie hatupo.” Mlinzi mwenyewe alishindwa kumgeukia Pam. “Anahali mbaya
dada! Ungemuona tu. Amekaukiwa, halafu ni mjamzito yule wa tumbo kubwa kabisa!
Jasho linamtoka kama amenyeshewa mvua. Anaweza anguka kabisa.” Mlinzi akamsihi. Safari hii kwa sauti ya chini akiwa amempa mgongo
kabisa Pam, na ameinamia simu kama asisikie.
“Mwambie hapa Mill hayupo, hajarudi
nchini. Ataondoka tu.” Simu ikakatwa Pam asiamini. Huyo
Kamila ndiye aliyekuwa akiwaletea chakula hapo alipokuwa akiishi na Mill, kama
wapo fungate! Alikuwa akiwaletea kuanzia cha asubuhi mpaka cha usiku,
akionyesha kuwajali na kumpenda sana Pam MBELE ya Mill! Leo
anaambiwa anahali mbaya, kweli ameshindwa hata kumfungulia mlango
kwenye nyumba aliyokuwa akimbembelezea akiwa na Mill! Pam HAKUTEGEMEA.
Ikabidi aondoke tu maana hata mlinzi alishindwa kurudisha jibu. Akaanza
kutembea taratibu kurudi barabarani.
Kwa Mama Kenny.
“Ni nini
kinaendelea?!” Akazidi kuchanganyikiwa. Kila alivyokumbuka mapenzi
ya Mill kwake, kwamba amemuacha hivihivi, ilikuwa haiingii
akilini kabisa. Wema wa Kamila alipokuwa akienda kwake, leo amgeuke hivihivi!
“HAPANA.” Akahisi jambo baya limepata Mill, ameogopa kumwambia.
Akamtetea Kamila moyoni mwake.
Akajiambia hata
kama waliamua kumuacha mama Kenny, lakini ni lazima watakuwa wanajua habari za
Mill, aliyeachwa hapo kama msimamizi wa familia. Akaonelea aende kwa
mama Kenny akajue ukweli.
Akachukua
daladala ingine, na kuunganisha mpaka kwa mama Kenny. Akazunguka hiyo nyumba
mpaka akakutana na hilo geti jipya lililokuwa limetenganisha nyumba yake
na vijana wa Mgini.
Hapo akagonga,
msichana wa kazi akaenda kumfungulia. Ilishafika saa 12 jioni. “Nimemkuta mama
Kenny?” “Yupo. Na yeye amerudi muda si mrefu. Karibu ndani.” Akaongozana naye
akijivuta mpaka sebuleni. Akakaa, msichana wa kazi akaenda kumuita mama Kenny.
Hakuamini kama ni Pam. “Nimekufananisha au ni Pam mwenyewe?” “Ni mimi, shikamoo.”
“Mbona umechoka hivyo!?” “Maisha tu mama yangu.” Akamuita msichana wa kazi na
kumuagiza juisi. “Naomba na maji tafadhali. Nimekaukiwa!” Mama Kenny
akakaa.
“Kwema? Mbona
umejiachia hivyo?!” “Mill yuko wapi?” Mama Kenny akatulia kidogo. “Sijui kama
mzima au mgonjwa! Sijui kama yupo hai au amekufa! Sijui
chochote na kwenye simu simpati kabisa.” Mama Kenny akaguna.
“Acha nikwambie ukweli Pam, binti yangu. Kwa
asilimia 100, mimi nilijua ni Mill peke yake atakuwa tofauti na babu
yake pamoja na baba yake. Lakini kumbe sivyo! Kwa hakika hawa watu wana laana
inayofuatilia kizazi hadi kizazi. Mill alikuwa mfano wa kuigwa hata Kenny
alikuwa anatamani awe kama yeye.”
“Nilipoona mambo
ni yaleyale, sikudanganyi Pam. Nilimpeleka mwanangu kanisani kuombewa.
Atokwe na laana ya kwao. Si bure!”
Akazidi kumchanganya Pam. “Kwani Mill amefanyaje?!” “Hakuna aliyeamini
jinsi alivyokuwa amekuleta hapa, nikafikiria amechagua fungu la tofauti,
atatulia! Tukashangaa yupo na mwanamke mwingine huko na yeye ni mjamzito!”
Pam akahisi hajamsikia vizuri.
“Unamzungumzia
Mill!?” “Huyuhuyo. Kaanza na wewe. Kila nikiuliza mbona ndoa ya kanisani kimya
ni ile tu ya kimila, baba yake akawa anamtetea hapa, eti anataka
akakuolee hukohuko Marekani. Kavuta weee. Alipoona tu baba yake kaondoka,
kachukua mwanamke mwingine.” “Haiwezekani mama Kenny!” “Wala si
siri. Mimi namfuatilia mwanamke wake. Anajiita Kisha Mgini. Mwanamke
wake mjamzito hata tumbo si kubwa, lakini limejaa huko Instagram!
Linapigwa picha kila siku, zinatumwa. Ngoja nikuonyeshe.” Kenny akadakia na
kumsogelea kabisa.
“Kwamba Mill
AMEOA huko?!” Bado hakuwa akiamini. “Pam binti yangu, umetapeliwa kama
sisi wote. Mchezo aliokuwa akifanya baba yake, ndio huohuo
anafanya na yeye. Sema naona yeye amekuja kivingine. Tapeli mstaarabu.
Maana baba yake hajawahi oa yeyote, wala kulipia mtu mahari. Ila Mill naona amejiongeza.
Kwako alilipa mahari na ile ndoa yenu ya kimila, mwenzio kamuolea mahamani!
Mbona picha atakuonyesha Kenny!” Kenny akafungua simu yake. Akamuonyesha picha
zote.
Kamila na Mike
walikuwepo huko mahakamani akifunga ndoa. Ndio akajua ni kwa nini Kamila
alishindwa hata kuzungumza naye. Pam akajiegemeza kwenye
kochi kabisa haamini. “Mill!” “Ni WASHENZI hao kina Mgini! Hujapata ona.
Wanajua kuzaa kama panya! Si uliona watoto wa Mgini hapa? Kafa,
kaacha wanae wana mangamanga! Hawana mbele wala nyuma. Malaya
kama baba yao. Hivi kama hilo tumbo ni lake, ukimtoa tu huyo
mtoto, kimbiza kanisani. Lasivyo jua umezalia watoto wa wenzio tatizo.”
Pam akabaki kimya.
Mwenzie, Kisha Mgini, alikuwa na tumbo, ila amependeza haswa! Kila mwezi
alipiga picha na kuposti, lakini tumbo wazi kabisa akiwa amelishika kwa kuvutia
haswa. Pozi tofauti tofauti. Akaangalia picha zote na kumrudishia Kenny simu
yake. “Nashukuru. Angalau nimejua ukweli. Sasahivi nitatulia niangalie
yangu. Nilikuwa na wasiwasi sana. Maana aliniacha na mipango
mingi! Sikudhania kama…” Pam akasita na kupotelea mawazoni asiamini.
“Halafu wewe si
umesema ulikuwa humpati kwenye simu?” Kenny akamtoa Pam mawazoni. Akamtizama. “Amezifungia
namba zako zote, ndio maana humpati. Lakini bro yupo, na anajibu
jumbe kama kawaida. Acha nikuonyeshe.” Pam kimya akijiangalizia.
Kenny akamtumia
ujumbe kwa kupitia namba ileile ambayo Pam yeye hampati, ila kwa simu
yake yeye Kenny. ‘Unaendeleaje huko Marekani, bro?’ Hapohapo
akamjibu. ‘Mzima. Kwema huko?’ ‘Kwema. Nilikuwa nikikusalimia tu.’ ‘Nashukuru.
Nisalimie mama na Sheila.’ Akawa akimuonyesha Pam
majibizano yao. Pam hoi haamini kama Mill yupo na ni mzima.
“Kuna chakula
mezani.” “Naomba nile mama Kenny. Nina njaa. Sijala. Mpaka nasikia kizunguzungu.”
Akakaribishwa mezani. Akala mpaka wenyeji wake wakabaki wakimwangalia yeye.
Akamaliza na kushukuru. “Unayo nauli sasa?” “Ninayo. Na hivi nimeshiba,
nikifika nikulala.” Akaondoka zake hapo.
~~~~~~~~~~~~~~
Haikuwa hivyo.
Pam alihangaika kitandani, usinginzi hauji. Alikuwa na mshituko
nakushindwa kuamini kama kweli ndio ametapeliwa na Mill. “Hakika
ndege mjanja nimenaswa kijinga sana.” Akajilaumu Pam, asiamini jinsi
alivyokuwa akijitunza, ameishia kutapeliwa.
“Lakini hapana!” Hilo ndilo likabakia kichwani kwa Pam kila akimfikiria Mill na jinsi
alivyomuonyesha mapenzi! “Hakika HAPANA.” Akashindwa kuamini kabisa.
Hakukaa sana,
ule mshituko na kutoweza kulala kukaibua pressure kali sana. Kila wakati
mapigo ya moyo yanakwenda kasi. Mikono inatetemeka kama aliyejawa hofu ya ajabu
sana.
Huku Kwa Mina.
Uhusiano wa karibu sana kati ya Mina na Pius
ukaendelea. Pius aliweza kupiga simu muda na wakati wowote, tena kwa stori tu
zakawaida. Shemeji akanogewa na Mina. Asipomsikia, siku haiendi.
Kwenda kumuona na kukaa na Mina wacheke kwa muda wakutosha tu, likawa jambo
la kawaida. Hata katikati ya siku, ungemkuta Pius nyumbani kwa mdogo wake
akicheka na shemejie, ambaye alikuwa tu kwake, na yeye anamajukumu mazito
tu ya kiofisi.
Wakaanzisha taratibu zao wao ndani ya
familia hiyo hiyo. Kama movie day,
yaani siku yakuangalia sinema pamoja au siku ya kwenda kula ice cream nje ya
nyumba na mengineyo. Siku hizo walizojiwekea wao wawili, Mina na shemejie, Pius
atatoka kazini na kuja hapo nyumbani kama ni siku ya kuangalia sinema. Atakaa
kwenye makochi hayo kwenye kijumba hicho kidogo kama punje ndogo ya jumba
lake, akiwa na Mina pamoja na Ayan, wakitizama movie. Mtoto akilala, atalazwa chumbani kwake. Hapo atabaki Mina na
shemejie.
Atamvuta miguu amuegemee. Basi Mina atakuwa
amekaa, miguu imepakatwa na shemeji. Movie na stori vinaendelea. Ataminyaminya hiyo miguu ya Mina hapo
huku akiipapasa taratibu macho kwenye luninga, mpaka muda uishe, ndipo
ataondoka. Hata Mina hakujua anaagaje huko kwa mkewe Raza. Lakini yeye alimpata
Pius muda na wakati wowote aliotaka na kumfurahia.
~~~~~~~~~~~~~~
Tofauti ya
Andy na Pius ikawa jinsi ya kujali tu. Andy alibadilika. Akimshika ujue anataka
penzi si kama Pius, alimshika kwa kumbembeleza bila kuomba penzi. Andy hakuwa mchoyo
wa pesa kabisa, ila mpaka uombe. Na ukiomba, haulizi, atatuma kiasi kile
kile ulichoomba bila hata kuongeza shilingi. Kwa hiyo maisha yao ikawa ni mpaka
Mina amuombe ndipo atatuma bila hivyo Andy hakuwa akikumbuka kutuma pesa.
Ikawa tofauti kubwa sana kati yake na Pius.
Pius akaingia kwenye maisha ya Mina akawa kinyume
kabisa na mdogo wake. Akawa ameshamsoma Mina ameshajua nini anataka.
Pius akawa kile anacholilia Mina. Kumjali yeye kama Mina. Alimpapasa
na kumbembeleza tena bila hata kutaka penzi kitu ambacho hakikua shida
kwa Pius. Ni asili yake, Pius mtoto wa mama, amekua na yeye kwa kubembelezwa
akakutana na Raza hapendi mapenzi ya kushikwa shikwa. Kwanza anaona kero.
Sasa Pius mtoto wa mama anayependa kupendana.
Hata ukimkuta amekaa na mama yake, ataanza kumminya mabegani akimtaka apumzike
aondoe stress za hiyo siku. Haya,
kabla hujalia shida kama ni mtu wake, anakusaidia. Kwa sili tu alijaliwa
kujali. Sio mchoyo.
Sasa wakakutana na Mina, mtoto wa mwisho
kwao, mtafuta kupendwa. Akafurahia
mikono ya Pius ambaye anataka wa kumbembeleza ila hana. Raza
ambaye yeye bora apewe pesa na Pius, na Andy aliyetingwa na
majukumu WAKAWASAIDIA kuwaweka karibu. Yao yakaanza kuwanogea.
Ikawa Pius na Mina kama waliokusudiwa. Upendo mwingi ndani ya
mioyo yao, wenza wamewaacha wapo busy na yao.
Wakati Raza akitapanya pesa ya mumewe na kutingwa
na majukumu yake binafsi na ya kiofisi, HAJALI ya mumewe, mumewe akapata nafasi na Mina. Simu za Raza kwa mumewe ni kuomba
pesa. Alipenda pesa kama benki. Na Pius alimjua. Ili
kumtuliza ni kumpa kila pesa anayoomba tena wakati mwingine alimpa kabla, ili asimkere.
Kwa kumuangalia Raza, ungejua anayo pesa.
Mashoga zake wa mjini walikuwa hadhi yake. Kula starehe kwenda mbele.
Kukutana kwenye sehemu za starehe na mashoga zake yakawa maisha ya Raza karibu
kila siku. Alitapanya bila kujipunja. Na kwa kuwa watoto wao, wao
hawakuwa wadogo, halafu wa mwisho alikuwa na ratiba za kisomi, za hadhi ya wazazi wao, alikuwa na dereva
maalumu kuhakikisha anafuata ratiba za binti huyo bila kukosea.
Kumtoa nyumbani na kumpeleka shule. Kisha kumfuata
shule na kumpeleka kwenye mafunzo ya kuogelea kama ni siku ya kuogelea.
Maana alikuwa akiogelea sana. Au kupelekwa kucheza tennis. Kama ni siku ya mchezo huo, na baada ya hapo
kurudishwa nyumbani akiwa anasubiriwa na mwalimu maalumu wakumsaidia kusoma na
kufanya kazi za shule.
Hivyohivyo kwa
dada yake. Alikuwa mwaka wa kwanza chuoni kikuu cha Dar-es salaam. Anao usafiri
wake. Anachagua pakulala. Kazi za chuo zikiwa nyingi, basi atalala
chuoni au akigombana na mama yake, basi hatakuwepo nyumbani. Kwa ufupi
Raza na Pius hawakuwa na watoto wadogo kama Ayan.
Kwa hiyo kila mmoja maisha yake yakaendelea vizuri
bila kukanyagana hapo jijini. Andy akaendelea na yake, Raza
naye yake yakaendelea bila kubugudhiwa na mumewe. Hata akirudi kutoka
kwenye starehe zake na mashoga zake, hakuna wakumuuliza kwani na mumewe
naye anakuwa kwa Mina ndio pengine na yeye anakuwa amerudi hapo nyumbani
kwao. Wamepishana kidogo tu.
Kwa kina Ruhinda kukawa kuna utulivu. Mina ametulia
nyumbani kwake na mtoto wake. Hakuna hekaheka ya kukaa na Ayan. Mzee
Ruhinda na mkewe wakarudi kazini wakiwa na akili iliyotulia, wakiwa na amani.
Na Mina naye alibaki kufika nyumbani kutembea tu. Mwanae msafi, yeye mwenyewe
ametulia. Hana huzuni wala kulalamika juu ya mumewe. Maisha yakaendelea kwa utulivu
wa aina yake, kwa kila mtu. Kumbe Pius ndiye aliyekuwa AMETULIZA hiyo ghasia.
~~~~~~~~~~~~~~
Mwezi ulishapita, Mina hapokei simu za mumewe kabisa.
Kwanza alishatoa Whatsapp kabisa
ambayo aligundua ndio njia rahisi ya mumewe kumpigia. Ikawa huwezi kumpata Mina
kwa njia hiyo. Andy akawa anahangaika kupiga mchana na usiku akidhani anaweza
kumpata, lakini wapi.
Ila ujumbe wa mwisho aliomtumia kabla hajatoa Whatsapp
ndio alijua anamfanyia makusudi. ‘Nilisikia ulifika
salama. Na sisi hatujambo, tunaendelea vizuri. Nakutakia kila la kheri kwa hilo
unalo lihangaikia.’ Mina akatuma huo ujumbe. Basi, kuanzia hapo
ikawa kimya, na wala hakusubiri majibu, akatoa Whatsapp kabisa.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku zilikwenda, Mina akiwa amejawa furaha
tele, hana wasiwasi. Maisha yake na shemeji yake yakaendelea kama kawaida. Mara
nyingine Pius alifika hapo mchana, na kujilaza kwenye makochi kama yupo
kwake tu. Ataweza kukaa hapo akizungumza na Mina hata masaa mawili ndipo
anarudi kazini. Swala lakuitiwa chakula cha mchana nyumbani kwa Andy likawa la kawaida
sana.
Mina akiivisha, Pius anajua, kwa kuwa mara
nyingi wanakuwa wote kwenye simu. Mina anapika na kufanya ya nyumbani, Pius
ofisini akifanya yake. Basi akiivisha tu, anajua. Utasikia akimwambia Mina, “Nakuja na mimi kula.” Basi Mina atacheka hapo,
shemeji anakuja kula. Watacheka na kufurahi ndipo anarudi kazini.
Na Pius naye hakuwa akimpa pesa ndogo. Ukimuona
Mina, ungejua pesa ipo. Pesa ya kutoka kwa mumewe kwa matumizi yote ya pale
nyumbani bado alikuwa akipokea kutoka kwa Andy na bado Pius sasa asiyejua
kutuma pesa ndogo ndogo!
Zawadi zake
kwa Mina si za mchezo na wakati wote zakushitukiza. Utoaji wake pia Mina
aliupenda. Alikuwa akicheka Mina, kama amepewa ulimwengu. Akajazwa
dhahabu za kiutuuzima. Nguo sasa! Pius alikuwa mwanaume anayependa kuvaa sana
kama asili ya kina Ruhinda. Kwa hiyo zawadi ya nguo kwa Mina, ilikuwa
kawaida. Wala hakuhitaji kutoka nje ya nchi ili arudi na zawadi. Akiwa hapo
hapo Dar, alikuwa akitokea kwa Mina na zawadi kemkem.
~~~~~~~~~~~~~~
Mwezi wa pili ukaisha. Bado Mina akawa HAJAWASILIANA na
mumewe. Hapokei simu zake kabisa. Andy naye akazira. Kila akiulizia hali
ya Mina na mtoto, anaambiwa ni wazima kabisa na wanaendelea vizuri. Akaona amuache
kwa muda labda atajirudi kwa kuwa na hamu naye, kwani alimjua mkewe.
Mwingi wa upendo kwake, asijue kaka yake amejaa nyumbani kwake, Mina hana
muda wa kuwaza kingine isipokuwa upendo wa Pius.
Maisha yakaendelea kwa Pius na Mina kwa nafasi yote.
Andy akiendelea kuzira nje ya nchi, Raza busy na pilikapilika za jiji. Pesa ya mumewe ipo, kilichobaki
matumizi na mipango tu.
~~~~~~~~~~~~~~
Wakati Andy Anasema
Cha Nini, Pius Anakililia. Na Wakati Raza keshakinahiwa, Akipambana Na Starehe Za Jiji, Mina Amempata Pius Kilaini,
Na Baraka Za Wazazi Juu!
Analiwazwa
na kubembelezwa huku akipewa matunzo ya hali ya juu.
Ni Nini
Kitaendelea Kwa Wawili Hao Walioachwa Huru Kabisa Mbele Ya Macho Ya Kila Mtu?
Pam Naye Aliyeachiwa
Tumbo,
Mill Akilea Tumbo Jingine Huko Ugaibuni, tena na ndoa juu!?
Usikose Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment