Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 23. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 23.

      

Kuna usemi unasema Timing is everything. Mina akabaki ametulia kiti cha mbele, kimya. “Niambie habari za mapumzikoni?” Pius akamchokoza. Mina akainama, kimya. “Maana uliondoka bila hata kuaga! Nikasikia tu Mina na familia yake wamekimbilia baharini! Nikasema hatuagani!”  Mina hakujibu. “Eti Mina?” “Hata mimi nilikuwa siijui hiyo safari, shem. Nilikuja kuchukuliwa mara baada ya mtihani wa mwisho, tukaondoka.” “Hata simu?” “Niliacha simu nyumbani. Sikuwa na simu wakati wote.” “Hapo sawa. Nikajua tunasahauliana.” “Hapana. Samahani.” Mina akaomba msamaha kwa upole. Pius akacheka kidogo.

It’s ok. Bora mmerudi salama.” Mina akanyamaza.

Alimfikisha nyumbani, hakuishia kwenye gari. Akamsaidia kutoa kiti cha mtoto kwenye gari yake na kukifunga kabisa kwenye gari ya Mina, ndipo akamchukua mtoto kutoka kwa Mina, akambemba, kupandisha ngazi mpaka juu kwenye apartment yao. Mina akafungua mlango, Pius akamwambia aingie yeye kwanza, ndipo wakaingia yeye akiwa amebeba mtoto.

“Najua umechoka shem. Naomba muweke tu hapo kwenye kochi ili nimuandalie chakula. Nakushukuru kwa msaada.” “Usijali. Wewe andaa tu, ngoja nikae naye kuliko kumuweka chini awe peke yake! Mkishatulia, ndio nitaondoka.” “Asante shem.” Mina akakimbilia jikoni. Alishapika mchana, alichofanya ni kumpashia moto tu.

“Njoo baba.” Pius akabaki akimwangalia Mina na mwanae. “Ukimaliza kula tu, sikusumbui tena. Nakuogesha, harakaharaka nakuacha ulale. Umesikia?” Mina akaendelea kumlisha mtoto wake huku akizungumza naye.

“Shem, nikuwekee chakula au utakwenda kula nyumbani?” “Nitakwenda kula nyumbani. Asante. Unahitaji lolote?” Pius akauliza kwa kujali. “Hapana shem. Nashukuru kwa pesa unayonipa. Nimefanya mengi kwa hiyo pesa! Umenifanya nitulie. Nakushukuru sana.” Mina akajibu kwa unyenyekevu sana. “Usijali. Na kama ukiwa na kitu kingine, niambie tuzungumze tujue chakufanya.” Akajibu kwa kujiamini. Pesa ipo, na mkewe anafanya kazi nzuri tu. Pesa haikuwa tatizo. “Usiwe na shida yeyote ile ukanyamaza. Nishirikishe.” Ile ikamgusa zaidi Mina. Pius akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina akaanza kulia asiweze kujizuia. Alilia. Akalia. Akalia. Alikuwa akimuogesha mtoto huku analia. Anamvalisha, huku analia. Akamuweka mtoto wake kitandani chumbani huku analia. Alipoingia chumbani alishindwa kulala. Alilia karibu usiku kucha, moyo ukimuuma vile jinsi Andy alivyombadilikia. Mkali, hana muda tena na yeye ila majukumu ya kazi tu. Hali ya upweke ikaongezeka moyoni, akabakia hana jinsi ila kusubiri akijua hapatakuwa na mwisho.

~~~~~~~~~~~~~~

Aliingia kwenye ndoa na Andy akijua ataanzisha familia ambayo ni ya baba na mama. Sio kama vile alivyokuzwa yeye na Ron. Akazidi kushuhudia historia ya mama yake ikijirudia kwake. Ni kama Ayan anakuwa bila baba yake. Tokea anamaliza mwaka mmoja, Andy akaanza ahadi zisizo isha. Ilianza taratibu na baraka za Mina. Kuchelewa kazini, Mina akawa anaelewa kwa kuwa angalau kulikuwa na MAWASILIANO kati yao.

Mambo yakaanza kubadilika. Ila hali ya ufamilia ikaisha. Hakuna tena kuzungumza au kupanga PAMOJA kama ilivyokuwa mwanzoni. Ikawa ni yeye akitoa muongozo wa nini anafanya. Yeye TU, bila maswala ya mkewe wala mtoto. Akamuacha Mina jijini na mtoto kama ambaye hajaolewa.

Ukali na ubabe akieleza nini anafanya tena kwa faida ya Mina ambaye hakuwa na makuu kama Lora. Mina hakuwahi kuhitaji makuu, yeye ndiye aliyempa makuu na kumuacha akihangaika kwenye maisha ambayo hata hakuwahi kufikiria.

Ukweli hata Mina alijua anachokifanya ni kitu kizuri kwa ajili ya familia. Lakini hapakuwa na MAWASILIANO kati yao, wao kama wanandoa. Hilo ndilo likawa TATIZO kubwa kati yao. Andy ambaye hakuwa akilala vizuri sababu ya kazi, akaishia kuwa mkali kwa Mina ambaye yeye alijua watalea wote mtoto hata kwa kupeana tu mawazo.

~~~~~~~~~~~~~~

Bila wao wenyewe kujua tatizo lao lilipo, Andy akidhani Mina analalamika bila yakuelewa uthamani wa kile anachokifanya kwa familia, na Mina akiumia akiona Andy amembadilikia, bila kujua kuna majira ya kila jambo. TATIZO ikawa ni MAWASILIANO kati yao.

Mipango MIZURI ilikuwa ikipangwa na kila mmoja wao ndani ya ndoa, na kila mmoja akipambana kivyake kuendesha hiyo mipango ndani ya familia bila kupambana kwa PAMOJA kama wanandoa. Siku zikaenda. Andy anafanikisha kivyake, na Mina hivyohivyo wasijue wanakumbatia BOMU hatari sana kwa ndoa yao.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina akaanza kumfikiria Andy, akajua hatakuja kubadilika kamwe. Ni mtu anayependa kazi, na yale maisha kwake ni sahihi. Akakumbuka maneno ya askofu wake juu ya Andy, kuwa Andy hapendi kitu kimuharibikie mkononi. Akajua yeye na mtoto ndio watalipa hiyo garama ya uaminifu na uchapakazi wa mumewe. Aliibeba hiyo kazi kama yake! Mchana na usiku bila kuchoka.

Akaanza kuvuta kumbukumbu ni wapi anguko la ndoa yao lilipoanzia. Akakumbuka alianza akiwa hata bado hajaamishwa hapo jijini Dar. Ayan akiwa na miezi kadhaa. Akawa busy kazini, simu hapokei kwa wakati. Akaanza vizuri kwa kumrudishia hizo simu na msamaha akitoa sababu za kueleweka tu. Pengine alikuwa mkutanoni au alikuwa akizungumza na simu ya kikazi wakati Mina akipiga. Hapo hapakuwa na shida, mkewe akawa akielewa na kumpa pole. Mina akaendelea kuvuta kumbukumbu ni kama akaanza kuacha kupokea simu zake nyingi na kutorudisha mpaka anaporudi nyumbani basi kuzitolea maelezo ni kwa nini hakuzijibu na kurudisha.

Akakumbuka jinsi na Dodoma napo kulivyoanza. Alianza kwa kumtaarifu safari ya Dodoma kama ni safari ya kikazi. Mina akazidi kuwaza. “Inawezekana tokea mwanzo Andy alijua atahamishiwa Dodoma ila alisita kuniambia. Na hajawahi kuzungumza na mimi juu ya safari zake zaidi ya kuniaga usiku mmoja kabla hajaondoka asubuhi yake!” Mina akakumbuka kwa uchungu sana. Akakumbuka hata hilo akawa kama amelichukulia sawa na kumtia moyo akijua ni kwa muda tu.

Mwanzoni alimrudishia majibu Mina kuwa huko anafanya vizuri mpaka akawatia tamaa wenye kampuni. Wakamwambia aanzishe tawi jingine na Iringa. Mina akakumbuka hapo ndipo ukorofi na ubabe ukazidi. Harudi nyumbani na kumpata kwa simu ni shida. Hajui uzima wake wala wa Ayan. Hata akipiga simu inakuwa kama anajambo la muhimu linalo msubiri huko kuliko kuzungumza naye kwenye simu.

Iringa nako akapata mwitikio mkubwa. Wenye kampuni wakamtuma tena akajaribu na Morogoro. Andy ambaye hakuwa na wegazi wa mke wala mtoto, ni yeye tu, huko Morogoro akafanikisha kwa kiwango cha juu sana. Mina na Ayan wakisubiria nyumbani wakati yeye akihangaika mkoa mmoja hadi mwingine.

Mina akakumbuka kuahirisha kwake kwa safari za kurudi nyumbani kwenda kuwaona. Kukaanza kwa kuomba msamaha akimwambia anaumia kutowaona. Akaja hatua yakutolea tu maelezo ya kawaida kama kitu tu cha kawaida kuwa hataweza kufika weekend hiyo na inayofuata. Ikaja sababu ya kukosa ndege na treni. Ndipo ukaja UBABE na UKALI sasa. Kuja nyumbani ni kwa shida, na mkali kwake japo anakuwa ni yeye mwenyewe ndiye aliyemuahidi atarudi kuwaona.

Haya, napo akifanikiwa kufika nyumbani nako ujenzi wa nyumba yao unakuwa unamchukulia nafasi, na kazi za huko alikotoka, zinahamia kwenye simu. Simu yake inakua busy akipigiwa na wafanyakazi walioko chini yake kuuliza hili na lile. Andy anakuwa nyumbani kama hayupo au kama aliyelazimishwa kutimiza jukumu fulani.

Maisha ya ndoa ni kama yaliwekwa pembeni kabisa. Akaonekana ni kama anatimiza jukumu zito sana la kulazimishwa. Akawa MGENI kwenye ndoa yake mwenyewe, hajui kinachoendelea anapokuwa hayupo na wala anapokuwa nyumbani hana muda wakutaka kujua yaliyompita. Mwingi wa majukumu ambayo ni kweli yalikuwa MUHIMU kwao wote wawili kama wanandoa, ILA hapakuwa na MAWASILIANO&MAKUBALIANO kama wanandoa na kuweza kujipanga na kukubaliana kupambana kwa kugawana.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina akaumia akikumbuka uzuri aliosema yule askofu ambao Andy anao, kwake umekuwa udhaifu na mwiba wa kumchoma yeye. Jukumu alilochagua Andy lisimfie au kumuharibikia ni kazi wala si yeye na mtoto! Akalia hapo asiwe nawakumbembeleza. Mina tokea mtoto alipenda kupendwa na mtu wa kumfuatisha ndio maana japo alikuwa mzuri sana, hakuwahi kutafuta mwanaume mwenye pesa ila KUMJALI, ndio maana alikuwa akilala na kila mwanaume anayeonyesha ana muda naye.

Hata kama ni konda wa daladala, hakuwa na shida kuhamia uswahilini ilimradi tu aonekane ana muda naye. Ila si pesa utakayomuhonga. Wewe muweke mkononi, mpapase, basi ameridhika. Hakuwa na shida. Sasa leo kujaziwa mipesa benki, gari zuri na kumfungia hapo gorofani, silo fungu lake hata kidogo. Sicho angechagua.

Bora vile alivyokuwa akikimbizana na Ron nyumbani kwao KULIKO hayo maisha hapo. Akajiambia angalau huyo Andy angekuwa akirudi nyumbani hizo siku mbili kama alivyoahidi na kumuonyesha anamtaka yeye. Kwamba ana muda naye! Lakini Andy alikuwa akirudi nyumbani na mipango mingi mno wala yeye hakuonekana ni kipaumbele!

Ukweli hata yeye Mina aliona jinsi mumewe anavyoingiza pesa. Ujenzi wa nyumba ya Kigamboni uliendelea kwa kasi tena kwa thamani za hali ya juu. Na yeye Mina alikuwa na pesa nyingi! Maisha kwake na mama yake yakabadilika kabisa.

          Kila alipokuwa akinunua kitu kizuri alimfikiria na mama yake. Mina na mama Ron wa miaka mitatu iliyopita, sio hawa. Waliosheka vizuri na vitu vya thamani. Kwa pesa ya Pius na ya ziada ya mumewe wakasaidiana na Ron, wakamaliza kujenga kwao. Tena ndani na nje. Alimshirikisha Pius juu ya tatizo la maji nyumbani kwao, akamsaidia mpaka mama yake akapata maji mpaka ndani.

Pius alimpa pesa akanunua matanki makubwa yakuhifadhia maji kwao. Usingekosa maji nyumbani kwa mama Ron. Mama yake akawa mwenye furaha KULIKO hata Mina mwenyewe, akifurahia mafanikio ya Andy, ASIJUE na pesa nyingine, tena NYINGI zinatoka kwa shemeji Pius.

Sasa hivi Andy yupo nje ya nchi kwa ahadi kuwa akirudi atatulia. Lakini Mina anamjua Andy wa baada ya ndoa. Hajui mahusiano ya mume na mke, ila mwadilifu wa kazi. Tena mwadilifu haswa, familia yake changa ndio iliyokuwa ikilipa garama. Mina ndio akawa muendesha familia hiyo. Uzima na ugonjwa wa huyo Ayan ilikuwa Mina bila Andy kupata muda wakujua maendeleo yao.

~~~~~~~~~~~~~~

Sio kuwa kina Ruhinda hawakuliona hilo. Zaidi baba yake lilimuogopesha sana. Mina alikuwa binti mdogo, tena mzuri SANA. Hakuna anakopita usigeuke. Hata kama hukumuona, basi cheka yake nzuri itakufanya utake kumuona mchekaji. Leo anamuona binti huyo anaachwa akizunguka tu hapo jijini, kwa uhuru wote!

Hamna mtu anayejua anaingia saa ngapi na kutoka saa ngapi! Akaangalia Mzee huyo, akashindwa kumwambia mwanae kwa kuogopa kumuudhi. Yeye Mina ndio alijua anaingia na kutoka saa ngapi hapo nyumbani. Nini afanye na mtoto huyo. Akawa ni kama binti ambaye hajaolewa. Akizunguka nyumba hii na ile kuomba msaada wa kushikiwa mtoto ili aende huku na kule.

Kilichokuwa kikiwatia moyo, ni ile hali yakumuona Mina anawakimbilia wao zaidi. Hatasita kumpigia simu mama Ruhinda na nyadhifa zake zote, atoke kazini aende akakae nyumbani kwake kwa masaa machache aende kwenye mtihani, au kwenda kumuacha kwa wakweze akisema anawahi kwenye mtihani, atarudi. Nidhamu kwa wakweze na kwenda kushinda huko hata siku nzima akalifanya jambo la kawaida kwake. Wakausoma moyo wake, wakamuona na yeye ni kama mtoto anayetafuta kwa kiu mahusiano. Mina sio mgomvi, mvumilivu na anapenda watu.

Ila kuachwa mwenyewe vile! Mpaka lini? Hilo likawa swali linalomtia wasiwasi sana mzee Ruhinda, lakini akajiambia anyamaze tu. Kila Andy alipokuwa akitoa UDHURU wakutokuwepo nyumbani kwake na akajua, alikuwa akishituka sana moyoni. “Unawezaje kuacha familia changa kama hiyo kwa muda mrefu hivi?” Akawa mtu wakujiuliza mzee Ruhinda na kubaki akitizama tu kwa macho.

~~~~~~~~~~~~~~

Swala kama Andy ni muhuni au ameanzisha mahusiano mengine ya kimapenzi huko nje, hakuna aliyewahi kumtilia mashaka. Hata kwa kumtizama tu, ungejua ni kijana mwadilifu. Anajiheshimu. Ila majukumu yake ya kazini, aliyaweka mbele, akijiambia na kuwaambia watu, itakuja kubadilika. Hakuna aliyeliona hilo, mpaka hapo Ayan ana miaka mitatu, baba yake anahangaika na majukumu ya kazi.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake Andy alipiga simu kutaka kumtaarifu Mina kuwa alifika salama, lakini Mina hakupokea. Ikaita na kuita, Mina akaona azime kabisa. Alipomkosa Mina akapiga simu kwa mama yake, mama Ruhinda. “Naona mambo yake na mtoto tu yatakuwa yamemtinga, lakini yupo salama. Jana nilirudi nyumbani, baba yenu akaniambia alipita hapo kuacha gari yako. Ilikuwa usiku, na hana usafiri wakumrudisha nyumbani yeye na mtoto. Lakini uzuri Pius naye alikuwa amepita pale nyumbani, ndio akawarudisha nyumbani kwenu. Nilimsikia baba yenu akimuuliza leo asubuhi kwa simu, nikamsikia Pius akisema aliwafikisha salama.” Andy akanyamaza. Akajua Mina bado amemkasirikia.

          “Basi nitawajaribisha tena baadaye.” “Vipi lakini huko? Unapaonaje?” Akauliza mama yake. “Mapokezi sio mabaya. Nashukuru.” “Afadhali.” Mama Ruhinda akaishia hivyo tu kama aliyejionya asiwe anaongea mengi na mtoto huyo asije akaharibu tena. Andy akaaga.

~~~~~~~~~~~~~~

Jioni Pius tena akapita kuwaona. Lakini alishazungumza na Mina asubuhi kuwajulia hali yeye na mtoto. Mchana tena alipiga, lakini ndipo Mina akawa amezima simu ili mumewe asimpate. Ndipo akapitia sasa kujua kulikoni.

“Kwema? Mbona hupatikaniki kwa simu?!” “Kwema. Nimekuwa na mambo mengi tu. Lakini tupo salama.” Mina akajibu wakati anamfungulia mlango shemeji yake. Macho mekunduu, na yamevimba. Pius akaingia kabisa na kukaa.

Mina akaenda kukaa pembeni yake, Pius akabaki akimwangalia. “Sijapika leo. Ni chakula cha mtoto tu, labda nikupe juisi au ungependelea soda?” Mina akavunja ukimya. “Na wine hatuna. Tokea mmalizie siku ile na mama, sikununua tena.” “Basi nitakuja nazo kesho. Usijali. Lakini kwa nini hujapika? Utakula nini?” “Nasikia kushiba leo. Sijisikii vizuri.” Mina akaongea kwa upole, macho chini.

“Unaumwa?” “Hapana. Nafikiri ni mawazo tu shem. Lakini nipo sawa. Usiwe na wasiwasi. Hata kutonipata kwa simu, nikutaka muda wakufikiria.” “Juu ya nini?” Mina akanyamaza. “Nilikwambia unaweza kuzungumza na mimi, chochote Mina.” Mina akanyamaza.

“Niambie unafikiria nini?” Pius akauliza kwa kubembeleza. Kaka hao walifanana, ungejua ni ndugu tu. Kasoro Pius hakukolea rangi kama wenzie, yeye alikuwa maji ya kunde, na alionekana ameshiba madaraka na pesa. Hapo alipokaa, harufu ya neema ilienea hapo sebuleni. Msafi kama ndio anakwenda kazini, kumbe ni jioni anatoka.

Akamsogelea Mina na kumshika mkono. “Mina?” Mina akamwangalia. “Nini kinakusumbua?” Shemeji akabembeleza. “Nafikiria maisha yangu shem. Mimi kama mimi na hatima ya mtoto wangu. Hiki anachopitia Ayan, kukuzwa na mama tu, hamna tofauti na kaka yangu Ron alivyokuzwa na mama peke yake, wakati baba alikuwepo.” “Lakini Andy atarudi baada ya miezi minne!” Mina akamwangalia Pius kama kumsuta.

Pius akacheka. “Haya, tuseme akijiweka sawa, atatulia nyumbani.” “Ambayo hiyo ni lini, shem?” Mina akauliza taratibu tu. Akajifuta machozi. “Andy anapenda kazi kuliko kitu chochote kile. Akirudi, kitakachobadilika ni jina tu la mahali atakapotakiwa kuwepo. Tena akionyesha ni muhimu sana, na hawezi kusubiri. Kwa hiyo yatakuwa ni yale yale.” Mina akaendelea taratibu kwa kuumia.

“Mimi nisingeweza kufanya anachofanya Andy. Unawezaje kuishi, tena sio kwa muda. Kuishi mbali na watu unaowapenda? Mbona hapa Dar kazi zipo tu shem? Au hata kwa nini asituchukue tukaishi naye huko? Ni nini chakusumbua familia kwa kiasi hiki! Ona mwanangu! Anakuwa bila baba! Wanaume anao waona ni babu yake, na nyinyi anko zake tu. Hana tofauti na sisi.” Mina akaendelea.

“Andy hajui uzima wangu wala ugonjwa. Kila kitu nilazima umuombe. Sio kama wewe hivyo unavyofanya kuniwekea pesa. Na pia hata hajiulizi ninaishije kwa matumizi yangu binafsi! Inamaana hapati hata muda wakunifikiria sababu ya majukumu! Maana ingekuwa mwanaume mwingine, angejiuliza. Hivi nilivyo, natunzwa na nani! Lakini hilo halipo kwa Andy sababu ya majukumu. Naishi hapa kama mtu niliyezalishwa tu na mwanaume, tena kama mume wa mtu ambaye anaishi na familia yake huko Dodoma. Sasa ndio najiuliza, hiyo itaendelea mpaka lini?” Pius akanyamaza kama aliyefungwa mdomo maana ilikuwa kweli.

Akaona abadili mazungumzo. “Unataka kula nini niende nikakuletee?” Mina akanyamaza. “Lazima kula Mina. Upo na mtoto. Naamini hivyo sivyo unavyotaka Ayan awe anakuona kila siku. Hutaki mtoto wako akue kwenye mazingira ya simanzi. Sikatai kuwa unatakiwa ufikirie, lakini nataka kukukumbusha upo na jukumu la mtoto pia. Anakutizama wewe zaidi na ndio mfano mkubwa wa maisha atakayokuwa nao. Ninauhakika unataka akue awe mtoto mwenye furaha, mtulivu na msikivu. Si ndiyo hivyo?” Mina akakubali.

“Basi, chakwanza nilazima wewe uchukue hatua na usimame kwenye nafasi yako kama mama. Na ukiweza, fanya yale ambayo unajua Andy alitakiwa kufanya kama baba kwake. Nimekuona ulikuwa ukifanya vizuri sana. Umetulia na mtoto. Sasa usipoteze dira. Kulia siku nzima na yeye akikuangalia, unamdhoofisha. Mtakuwa wote hamna furaha. Nashauri katika mazingira hayahaya uliyonayo sasa hivi. Hivi hivi ilivyo, tafuta jinsi yakuishi kwa furaha wewe na Ayan. Huku ukifikiria unachofikiria.” Pius akaendelea.

“Nimekwambia pesa isiwahi kuwa tatizo. Mimi nipo. Ukiwa na shida yeyote ile tafadhali usisite. Na nitajitahidi niwe nakuwekea pesa za matumizi ya hapa nyumbani, na kila mwisho wa mwezi nitakuwekea benki. Bado wazo la kuanza kazi unataka lisubiri?” “Nahofia kumuacha Ayan, shem. Huyu mtoto atakuzwa na watu baki  mpaka lini, wakati mimi na baba yake wote tukihangaikia pesa! Nimejaribu wasichana wa kazi, imeshindikana. Nahisi hapa tunapoishi pia panachangia kuwashawishi wanapokuwepo tu hapa nyumbani wakiwa hawana chakufanya. Wanaishia kumtesa tu mwanangu! Maadamu bado upo uwezo, acha nimsogeze angalau afikishe miaka 4 yakuanza shule ndipo na mimi nitafute kazi.” Mina akajieleza akiwa ametulia.

“Safi kabisa. Si umeona sasa? Kule kujua ni nini chakufanya kwa sasa tu, inatosha Mina. Tuliza mawazo katika hilo na tumia nafasi vizuri. Mjenge mtoto wako vizuri. Kwa furaha na mapenzi yote. Hakikisha hapo hapabadiliki, ndipo mengine yafuate. Si unaona ni sawa?” “Nashukuru kunisaidia shem. Naona nitafanya hivyo. Acha nitulie na mtoto.” Kidogo Mina akatulia. Hata usoni akaonekana amepata nafuu.

~~~~~~~~~~~~~~

“Basi subiri nikakuletee chakula.” “Asante.” Pius akatoka, Mina akaenda kuoga kabisa. Akavaa vizuri. Pius anarudi, akakutana na Mina wa tofauti. Mrembo na cheko. “Umependeza Mina! Mpaka natamani nikutoe!” Mina akacheka sana. “Nimeanza kufanyia kazi maneno yako.” “Safi sana. Usiwe unashinda ukilia. Ukijisikia kulia, ingia chumbani, nipigie simu ulie na mimi lakini sio mbele ya mtoto.” Ikamgusa sana Mina.  “Asante shem.” Akampa shemeji yake busu la shavuni lililomsisimua Pius vilivyo. Akamuachia chakula nakuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Mapenzi kwa binti huyo mdogo haswa, karibu kuweza kumzaa, mke wa mdogo wake, na yeye yalishamuanza muda mrefu sana. Pius alimpenda Mina, akawa akitaka kumuona kila wakati na kumsikia kwenye simu mara kwa mara. Akikaa naye karibu ikawa ndio burudani moyoni kwa Pius. Andy ndiye aliyemsaidia kumsogeza kwake zaidi. Ubusy wake Andy, na kwa kuwa na yeye ni kaka wafamilia, ndio ikawa zawadi yake. Anatumwa na kina Ruhinda kumtizama mke wa mdogo wake, lakini kumbe ndio ilikuwa furaha yake.

Alipoona Mina anaachwa huru na mumewe hapo jijini, na yeye wasiwasi ukamwingia kama baba yake. Na yeye akaamua kunyamaza kimya, lakini akachukua hatua yakujimilikisha Mina. Akamvuta karibu yake zaidi. Wivu ukaanza kwa Mina, utafikiri yeye ndio Andy! Anahofia walimwengu wasije kumteka. Mtoto akiumwa, au hata yeye mwenyewe Mina asilalamike kuumwa kidogo tu, Pius yupo. Tena yupo kwa hali na mali. Pesa yakutosha akawa akimpa Mina kiasi chakumshangaza hata Mina mwenyewe.

Akiwa na tatizo lolote lile, Pius akawa kimbilio la Mina. Akamsogeza mpaka nyumbani kwake, ili tu azoeane na Raza na awe huru kufika kwake. Lakini Mina akagundua Raza amembadilikia, hampendi kabisa. Dada huyo msomi, mwenye pesa akawa na mambo ya kulalamika kama mswahili ambaye hakwenda shule, anayeshinda kibarazani tu kuzungumza ya watu, siku nzima.

Chuki yake kwa Mina akashindwa kuificha. Na wala hakuweza kuwa mnafiki kwa Mina. Mina hakujua ni kwa nini, lakini hakuweka mazingira rafiki  nyumbani kwake, si kwa Mina tu hata mwanae pia.

Wakati mwingine Mina akifika nyumbani kwake na mwanae, anaweza kumuonyesha na yeye ndio anataka kutoka, na Mina aondoke. Tena kwa waziwazi. Na swala la kuacha mtoto wake kwake, alishalalamika kuwa msichana wa kazi aliye naye ni mmoja tu. Kumuacha Ayan pale ni kumuongezea majukumu msichana wake wa kazi, anaweza kukimbia kwa hofu ya kuongezewa majukumu.

Kwa hiyo Ayan alipokelewa hapo siku ambazo Raza mwenyewe anakubali kuwa atakuwepo naye pale, tena akiwa ameombwa na mama Ruhinda, au Pius akiwepo hapo nyumbani. Vinginevyo aliachwa kwa mzee Ruhinda. Msichana wa kazi anakaa naye ndipo mzee au mama Ruhinda anarudi kukaa naye kama mama Ron yupo na majukumu mengine.

Paulina yeye alijulikana. Hata watoto wake mwenyewe hakuwa na muda nao, labda Devi akisaidiana na wasichana wake wa kazi. Kwanza mvivu na hapendi majukumu ya nyumbani kabisa. Na wakati wote kwake kunakuwa na wasichana wawili wa kazi pamoja na kijana wa nje. Dada huyo msomi mwenye PHD, ukimtizama tu, utaona aibu yakumuomba akukalie na mtoto wako, labda umpe kalamu. Mpenda kazi, kama Andy. Majukumu ya ofisini ndio kipaumbele, nyumbani ni mumewe.

Paul naye mara chache. Tena akiachiwa mtoto hatakataa, ila baada ya nusu saa ukimpigia simu, utamsikia yupo na mtoto hospitalini. Alipata dharula, anamgonjwa huko. Anamtibu na Ayan akimsaidia hapohapo alipo. Hatamuacha mtoto popote, ila ujue atazunguka naye kila mahali mpaka mawodini kwa wagonjwa wake. Ndipo mzee Ruhinda akamkataa Paul kuwa hafai kuwa na mtoto. “Jamani, mkikwama kabisa msisite kuniambia.” Paul alikuwa akiwachokoza. “Wewe hapana bwana! Utamtia maradhi mjukuu wangu bure!” Mzee Ruhinda akawa akimkataa kabisa.

Swala la kupigiwa simu Pius na kusema yupo kwa Andy, wala si kwa Mina tu, likawa likisikika la kawada na la kujali japo si kwa Raza ambaye alishakiri kwa mumewe kuwa hao kina Ruhinda wana mtetemekea Mina. Akikohoa tu, kila mtu kwenye familia hiyo anamkimbilia. Akatoa mengi ya kukashifu akiona Mina ndio anatetemekewa kama mungu mtu! Akawa yeye anamkwepa Mina na mwanae.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati Andy Akipambana Na Maisha Ya Kazi, Ili Kuleta Maendeleo Kwenye Familia Aliyoiacha Katikati Ya Jiji La Dar, Kaka Yake Ameona Aingilie Kati KUMSAIDIA Kumtenga Mkewe Na Vishawishi.

Yale Yote Ya Andy Aliyoyaacha Kwenye Familia Yake, Amekusudia Kuyabeba Ili Kuziba Pengo la Andy, Ili Mina Asione Upungufu, Na Kushawishika Na Wanaume Wa Nje.

Ni Nini Kitaendelea?

Usikose Muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment