Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 22 - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 22

Alipokaribia mitihani ikabidi Mina kutafuta muda wa mazungumzo rasmi na Andy. Alimtumia ujumbe kuwa anaomba atafute muda usio na mwingiliano, ampigie kwa kuwa ana kitu cha muhimu sana anataka kuzungumza naye. Usiku kabisa Andy akampigia. Akajua ndio muda aliopata. Mina akajiweka sawa ili kuzungumza naye bila hasira. “Nina mitihani ambayo sitaki chochote kiingilie Andy. Na nimechoka kumuhangaisha mtoto. Juzi nimetoka kumchukua kwa Raza, sijafurahia jinsi alivyoniangalia na kunijibu. Nimebakisha kidogo tu nimalize. Tafadhali naomba chukua likizo hata ya siku 10 tu, nifanye mitihani.” “Sawa.” Mpaka Mina akashangaa. Hakutegemea jibu la kukubaliwa kwa haraka kiasi hicho.

Weekend hii nitakuja, tutapanga vizuri.” Mpaka Mina akakosa jibu. “Mina?” “Kama nitakuona Andy! Maana huwa unakuja na kuishia kwenye ujenzi Kigamboni.” “Si nimetoka kukwambia kuwa nitakuona weekend hii? Unataka nini kutoka kwangu Mina?” “Ungeniuliza mapema hilo swali, ningefurahi sana Andy. Ila pia kwa kuwa umeuliza acha tu nikwambie.” Andy kimya.

“Upo Andy?” “Nakusikiliza maana sijui tena chakufanya!” Andy akajibu. “Mimi nakutaka wewe Andy. Ukiniambia nichague, ni heri kuwa na wewe kuliko hili gari na hiyo nyumba ya Kigamboni. Vyote vinakosa maana kama vikiwepo hapa, halafu wewe haupo Andy.” “Lakini ni kwa muda tu Mina!”

“Ulianza na Dodoma tu Andy! Sasa hivi umekabidhiwa Morogoro na Iringa.” “Bado sijakabidhiwa. Nashika kwa muda tu. Mambo yatapungua, nitarudi nyumbani na tutakuwa wote.” “Sawa Andy! Naomba usije ukanogewa na kunisahau kabisa. Jua nipo nyumbani, nakusubiri.” “Nitakuona weekend hii, kwa hakika.”  Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~

Weekend hiyo Andy alirudi nyumbani, hakugusa chochote, akawepo tu nyumbani na Mina pamoja na Ayan. Mina akakatwa kiu zake zote. Andy alimtendea haki vilivyo. Mina alijawa cheko kila wakati. “Nakupenda Andy.” Mina akarudia tena na tena kila aliposhikwa na kukumbatiwa na Andy. “Nakupenda Mina. Nakuahidi mambo yatabadilika.” “Kweli Andy?” “Kabisa. Na nitakuja kukaa na mtoto siku tatu kabla yakuanza mitihani yako.” Hapo napo Mina akatoa penzi zito la shukurani. Jumatatu Andy akaondoka na kurudi Dodoma.

~~~~~~~~~~~~~~

Andy akawa mwaminifu katika hilo. Siku 5 kabla ya mitihani ya Mina, akarudi nyumbani. Akawa baba kweli kweli na kumshangaza Mina. Akitoka lazima awe na mtoto wake. Kumlisha na kumfanyia yote bila hata kuombwa na mkewe! Mina akapata muda wakutosha wa kujiandaa na mitihani.

Kukawa na amani na utulivu kwenye kila nyumba na ofisi aliyokuwa akitembezwa huyo mtoto. Mina naye akatulia. Akakazana akifanya mitihani yake vizuri na kwa amani hata mama yake hakuamini kama ni Mina yule waliyekuwa wakimlazimisha kusoma, sasa amegeuka ndiye mwenye njaa haswa na shule!

Mama Ron akaona Mungu amemjibu kwa wakati mmoja. Ron amepandishwa cheo, Mina ametulia nyumbani kwenye ndoa yake na anasoma! Hakuna jinsi ungemwambia mama Ron Mungu hajibu maombi akaamini. Imani yake kwa Mungu ikaongezeka maana hata yeye maisha yalimbadilikia. Ron na Mina walikuwa wakimtunza sana huyo mama yao aliyekuwa ametengwa na ndugu na kuachwa na mume.

Baraka Nyingine Tena.

Wakati Mina anafurahia uwepo wa mumewe nyumbani, familia imetulia, aibu ya kuombaomba kushikiwa mtoto imetulia, asijue likizo hiyo aliyochukua mumewe ilikuwa na jambo nyuma yake.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina alitoka kwenye mtihani wa mwisho akiwa na furaha zote. Akakuta Andy na mtoto wanamsubiria nje ya chuo. Akacheka. “Vipi mtihani?” “Mgumu Andy!” Akalalamika wakati anakaa sawa garini. “Pole na hongera kumaliza.” “Asante. Nashukuru kuja kuwa hapa na sisi. Najua una mambo mengi. Lakini kwa hili, nakushukuru.” Andy akacheka huku akiondoa gari.

“Nataka nikakupongeze.” Mina akacheka. “Nataka twende tukajifungie Bagamoyo. Siku 4 tu. Sisi watatu tu.” Mina akafurahia sana hilo asiamini. Wakati wanarudi nyumbani kujiandaa, njiani akampigia simu mama yake kumuaga na kumpa habari za mitihani. Kisha akamtaarifu na mama Ruhinda kuwa hatakuwepo weekend hiyo, atakuwa mapumzikoni na mumewe pamoja na Ayan. Kisha akazima simu kabisa.

Hakutaka muingiliano na yeyote yule! Andy wake yupo! Hataki kelele na mtu ila kumsikia tu Andy na mwanae. Ungemuona Mina, ungedhani amepewa ulimwengu kumbe Andy amempa muda wake. Dhambi zote akasamehe. Akasahau yote na wote, akili yote kwa mumewe.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mina, Ayan na Andy walifika Bagamoyo wakiwa wamejawa vicheko. Hata Andy alijua Mina anayo furaha. Akafanya na yeye ajisikie vizuri. Hoteli tu waliyoshukia, ungejua pesa ipo. Waliagiza chakula chumbani, Mina akiwa anamuogesha mtoto wao baada yakujimwagia maziwa. Andy akampokea wakati wanatoka bafuni. Akamchokoza Ayan wakati mama yake anamwandalia nguo.

“Utafanya nini baada ya hapa?” Andy akamuuliza. “Nimemuhangaisha sana mwanangu Andy. Nataka nitulie nyumbani. Tupendane kwanza hata kwa mwezi. Ndio nitajua wapi pakutafuta kazi na mimi nianze kuingiza pesa, angalau nikupunguzie majukumu labda utapata muda wakutulia nyumbani na sisi.” Mina akaongea kwa upole.

“Siku ile nilikuwa nimechoka Mina!  Si wewe wala Ayan ni mzigo kwangu. Nyinyi ni jukumu ninaloyafanya kwa furaha kabisa. Ila ile kazi kule nafanya kwenye mazingira magumu sana! Natumia muda na nguvu nyingi kuelekeza hiyo timu mpya ya wafanyakazi, na wateja pia.” Mina akanyamaza. Hakumjibu. Andy akajua ile siku aliumia .

~~~~~~~~~~~~~~

Akafikiria na kugundua ni kama Mina aliacha kabisa kumuomba pesa zake yeye binafsi za matumizi. Akabaki akifikiria nakuvuta kumbukumbu zaidi. Kila pesa aliyoomba baada ya yale mazungumzo, haikuwa kwa ajili yake tena. Lakini Mina hakuonekana kama mwenye shida! Alizidi kupendeza, tena sana. Hata akimwangalia akagundua ana hali nzuri ya kitajiri. Kila kitu chake kilikuwa cha hali ya juu mno. Sio vya bei ya kawaida. Andy akamwangalia tena. Hata hapo alikuwa nadhafu, amejaa dhahabu kila mahali!

Akataka kutafuta muda wakumuuliza anakidhi vipi tena mahitaji yake binafsi, mbona haombi tena pesa, akaona asianzishe jambo jingine, wakati LAKE, lililomfanya awalete hapo, Mina akidhani ni mapumziko ya yaliyojawa upendo na kujirudi, kumbe anayo ajenda yake, bado hajazungumza naye. Akaona hilo la ukidhiji wake wa mahitaji, alinyamazie tu. Kumbe kaka yake anamwaga mapesa kwenye akaunti ya Mina, wala si kumrushia kwenye simu! Hapo Mina anapesa kama ameajiriwa kwenye kampuni kubwa na kulipwa mshahara wa hali ya juu sana.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina akamvalisha mtoto wake kimya kimya, akamlisha kisha akamuweka kitandani na chupa ya maziwa. Mtoto huyo wa Mina, alikuwa akinywa maziwa, kila wakati, kama maji ya kunywa. Na hajali. Yawe moto, vuguvugu au yawe baridi, atakunywa tu. Na ni mara chache sana ukimsikia akilia.

Mina akarudi kukaa karibu na chakula. “Vipi na wewe huko? Ipo hata dalili yakurudi huku Dar au ndio umehamia huko moja kwa moja?” Mina akauliza kwa wasiwasi. “Sasa hivi nataka tuishi wote Mina. Popote nitakapokuwepo, nataka na nyinyi muwepo.” Hilo Mina akalifurahia.

“Itakuwa afadhali Andy! Hivi tunavyoishi sidhani kama ni sawa.” “Utakuwa tayari kuhama hapa Dar?” “Unafikiri hawatakurudisha tena Dar?” “Sidhani. Labda niache kazi nitafute kwengine.” Mina kimya.

“Naomba niambie Mina.” “Sijui Andy! Lakini naona tumeachana muda mrefu sana. Umekuwa ukifanya mipango yako bila hata kunishirikisha! Sasa hivi umefika mbali! Ukiniomba ushauri leo, nashindwa hata naanzia wapi!” Mina akalalamika.

“Tulianza vizuri Andy, ni nini kilitokea tena!?” “Maisha tu Mina. Majukumu.” “Mmmh!” Mina akaguna nakuanza kula. “Mbona unaguna?” “Nahisi tofauti Andy! Tulipoteza lengo. Tukaweka vitu vingine mbele, tukasahauliana. Ulifika hatua yakunihesabia Andy! Wakati mimi sijawahi kukuomba gari wala haya maisha. Wewe mwenyewe ulifanya, nikashangaa ukageuka nakuanza kulalamika!” “Sikukusudia mpenzi wangu. Siku ile nilikuwa nimechoka, nahisi nikakumalizia wewe hasira. Naomba unisamehe.” “Nimekusamehe Andy.” Akakubali hapohapo bila kubembelezwa.

“Naamini hatupo mbali sana Mina. Unafikiri tunaweza kuendelea? Au umeshanichukia kabisa?” “Mimi nakupenda Andy. Naamini tunaweza kurekebisha.” “Hapo umenipa moyo.” Mina akacheka. “Sasa je, utakuwa tayari tukaishi Dodoma?” “Ndio itakuwa maisha yetu yote!?” Mina akauliza akifikiria familia yake. “Tutaangalia watakachotulipa na upepo. Tukiona hapatufai, hapa Dar tuna nyumba Kigamboni. Umesoma na mimi nimesoma, hatuwezi kushindwa kupata kazi, lakini tusije kuishi tena mbali mbali.” Mina alifurahi huyo! Hakuamini.

“Tutaongozana popote Andy. Na mimi nataka tuwe pamoja. Sio hivi tunaishi mbalimbali halafu bila sababu! Sioni kama ni sawa. Hata watu watakuwa wakitushangaa! Ingekuwa mimi nimefungwa na kazi huku siwezi kuwa na wewe huko, hapo sawa. Lakini kutuacha tu nyumbani halafu wewe unakua pengine! Mimi hivyo sipendi Andy. Nataka kuwa na wewe.” Andy akacheka akimfikiria Mina na anachotaka kumwambia.

~~~~~~~~~~~~~~

“Njoo kwanza Mina wangu.” “Ukitulia unakuwa mtu mzuri Andy!” Andy akacheka akitafuta njia ya kuzungumza naye ili kumuweka sawa. “Nakuwa nimechoka! Njoo hapa.” Mina akahamia mapajani kwake kwa upendo. “Sasa nikwambie kitu?” “Nakusikiliza.” “Nakuomba nipe miezi 4 mingine. Niende safari ya kikazi, ni masomo mafupu.” Mina akaishiwa nguvu, silo alilotegemea.

“Minne tu. Nikirudi baada ya hapo, tunahamia Dodoma. Tunaanza kuishi wote.” Mina akasimama. “Usiondoke Mina. Njoo tuzungumze.” “Labda niulize Andy, hapa unaniaga au unaomba tushauriane?” “Nimechaguliwa na ofisi kwenda kuongeza ujuzi kwa miezi minne tu, nchini Uswiz. Nita..” Mina akaondoka kuelekea bafuni.

“Mina?” Andy akamuita. “Tupo hapa kunitaarifu Andy. Umeshanitaarifu. Sitaki ugomvi na maneno. Naomba tumalize hizo siku zilizobaki hapa hotelini kwa usalama. Na mimi nimechoka kweli sababu ya mitihani. Tupumzike, tukitoka hapa, maisha yakaendelee vile ulivyochagua wewe Andy.” “Mbona unafanya mambo kuwa magumu Mina!? Hizi nafasi watu wanazililia!” “Andy, mwenzio nimechoka. Naomba nikaoge nilale.” Mina akaelekea bafuni. Hata hakumalizia kula.

Akaoga, nakutoka kwenda kulala kitandani. Akajifunika, kimya. “Acha hasira Mina.” Kimya. “Mina?” “Naomba kulala Andy. Naomba tutumie hizi pesa ulizolipia hapa hotelini vizuri. Unafikiri tunaweza?” “Kwa nini tusimalize hili?” “Kwani unataka kunisikia nikisema nini Andy? Mbona kama nimekuachia uendeshe hii familia vile unavyopenda wewe? Mimi sijakataa chochote. Tuendelee hivyo hivyo unavyofikiri ni sawa. Mimi sina chakuongeza tena. Lakini kama unataka nisilale, nitakaa.” Akatoka kabisa kwenye shuka. “Basi bwana!” Andy na yeye akaelekea bafuni, Mina akarudi kulala.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakakaa hapo hizo siku 4 lakini kimya kimya. Mina mchache wa maneno. Anajibu kila swali analoulizwa vizuri tu. Bila kiburi wala kinyongo. Anakula vizuri. Anaweza kutoka na mtoto kwenda kucheza, wakati mwingine Andy anawafuata, wakati mwingine Andy anabaki chumbani kupiga simu zake. Wakati mwingine Mina akisikia simu yake inaita tu, anamchukua mtoto wake, anatoka hapo chumbani anakwenda naye upande wa baharini kucheza mpira mpaka Andy awafuate.

Siku zikaisha, wakaondoka hapo hotelini kimya kimya. Hawakugusana hata kwa mapenzi. Walipofika Tegeta, Mina akaona Andy anaelekea nyumbani kwao. Hakumuuliza. “Nataka kwenda kumuaga mama.” Hakumjibu. Tena safari hii akakaa kiti cha nyuma na mtoto wake.

Kwa Mama Ron!

Walifika kwao wakamkuta mama yake na Ron. Mama yake Mina aliposikia Andy anakwenda masomoni, tena Ulaya! Akafurahia SANA. “Yaani ndoa yenu imekuja na baraka baba! Hongereni sana. Umeanza Dodoma, wakakuongeza na hiyo mikoa miwili mingine, sasa hivi ndio wanaona ukaongeze ujuzi! Mungu mkubwa.” Mina akamuona mama yake amefurahia sana. Ila Ron alinyamaza kimya hata hakuchangia kitu.

“Naomba muendelee kumsaidia Mina kwa miezi hii 4 tu. Nikirudi sitawaacha tena. Nahangaika mama kwa ajili ya familia yangu!” “Na Mungu atakusaidia baba. Sisi tupo, wala usiwe na wasiwasi. Kwanza mwanao huyo hana shida baba. Mpole kama wewe.” Andy akacheka.

“Kweli kabisa! Yeye umpe maziwa yake, hataongea wala kulia. Kimya.” Mama Ron akatoa sifa nyingi wee. Akimpamba mkwewe na mjukuu wake. Mina kimya akisikiliza. Mwishoe wakaaga na kuondoka.

Kwa Ruhinda.

Wakaelekea mpaka kwa Ruhinda. Akamkuta baba na mama yake. Akawaambia vile vile kama kule kwa kina Mina. Ila hapo pakazuka ukimya mkubwa tofauti na kwa mama Ron. Ikawa kama wazazi wake hawajui waseme nini, mwishoe mzee Ruhinda akauliza. “Unaondoka lini?” “Kesho usiku.” Pakazuka ukimya mwingine. Mpaka Mina akashangaa asiamini kama safari ndio ipo tayari kwamba mpaka na tiketi! Akaumia sana. Lakini kama aliyejionya, akanyamaza.

“Nilazima niende, lasivyo muda wote niliohangaika Dodoma, Morogoro na Iringa utakuwa bure. Ni miezi minne tu yakumalizia ili nipewe zone nzima ya kanda ya kati. Najua baada ya hapo nitatulia na familia.” Ikabidi Andy ajitetee sababu ya ukimya, alipoona wote kimya.

“Huyu mume wangu hana neno. Hapa ni nyumbani. Mkeo naye kama unavyomjua, hana makuu. Ni hivyo tu wakati huu na mimi nina safari mbili tatu hivi. Nikirudi, nitatulia nao.” Akajibu mama Ruhinda akiwa amempakata Ayan. Lakini ni kama na yeye alijitoa, akiaga kuwa atakuwa busy na safari za kikazi. Mzee Ruhinda kimya kwa muda kama anayefikiria.

“Ruhinda?” Mkewe akamshitua. “Kuhusu hawa wawili usiwe na wasiwasi. Nilimuona vile Mina anavyojituma na mambo ya familia. Amehangaika hapa na mtoto naona mpaka amemaliza hiyo miaka miwili akiwa peke yake. Sidhani kama atashindwa hiyo miezi minne tena. Na kama tulivyokwambia Mina, muda na wakati wowote unapokuwa na shida, tupigie.” “Asante baba.” Mina akajibu, macho ameelekezea chini akijikaza asilie. Wakaaga na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Walipofika nyumbani, Andy akamlaza mtoto. Akamkuta Mina anakunja nguo chumbani. “Kuna kitu unataka nikusaidie kuandaa kabla ya hiyo safari?” Mina akauliza. “Naona kila kitu kipo tayari. Nilishaandaa kipindi upo kwenye mitihani. Asante.” Mina akanyamaza. “Nitarudi Mina. Na usifikiri ndio nafurahia kuwaacha! Na mimi natamani tubaki wote.” “Sawa Andy. Mungu akusaidie.” Akajibu tu hivyo Mina.

~~~~~~~~~~~~~~

Akaingia kuoga, akamuacha Andy anasoma vitu na kuweka kwenye kibegi kidogo. Akatoka, Andy naye akaingia kuoga, kisha akawahi kitandani. “Naomba uniage vizuri Mina.” Andy aliingia ndani ya shuka alilokuwa amejifunika Mina. Bila kinyongo, Mina akachangamkia penzi. Akamzungusha Andy hapo kitandani mpaka akamuona ameridhika. Akaenda kuoga tena, akarudi kitandani.

Andy naye akatoka akaelekea bafuni akarudi akidhani Mina amelala, akajilaza pembeni yake. Akasikia anamvuta mkono, akaubusu na kuuvuta karibu yake, akaukumbatia kwa upendo. “Asante Mina.” Andy akashukuru asiamini, lakini Mina hakujibu.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake akaamka akakuta Andy alishaandaa kifungua kinywa, mtoto msafi. Hapakuwa na maongezi mengi. Baada ya chakula cha mchana akamuomba Mina kama anaweza yeye na mtoto wakamsindikiza uwanja wa ndege. Mina akakubali. Muda ulipofika, akamtaarisha mtoto wake vizuri, wakaondoka. Njiani Andy akawa akimuaga Mina.

“Nitakuwa nikiwapigia simu mara kwa mara.” Mina akabaki ametulia tu. “Nitakuwa nikikutumia pesa za matumizi kama kawaida. Sitasahau. Halafu hii gari yangu unaweza kwenda kuiacha nyumbani kwa wazazi kwa ajili ya usalama.” “Nitafanya hivyo nikitoka tu uwanja wa ndege.” Akaafiki Mina bila ubishi.

“Nakupenda Mina. Nakupenda sana mpenzi wangu. Nahangaika, lakini tukija kupumzika, tutapumzika pazuri. Tafadhali nipe hiyo miezi minne ya mwisho. Nivumilie mpenzi wangu. Sijapoteza dira, ila inanilazimu kuchukua au kufanya maamuzi magumu ili tu wewe na watoto mje muishi vizuri zaidi. Tafadhali niage na kicheko angalau niondoke vizuri.” Mina alikuwa ameshamfikisha uwanja wa ndege, Andy ametoa mabegi yake amerudi kusimama dirishani, Mina hakutaka hata kushuka. Kimya.

Akarudi upande wa nyuma kwa mtoto wake, akambusu na kumuaga. Kisha akarudi tena pale kwa Mina dirishani, akamkuta anafuta machozi. “Nakupenda Mina. Nakupenda sana mpenzi wangu.” “Asante Andy, uwe na maisha mema huko.” Mina akaaga na kuondoka.

Maisha Mapya bila Andy Nchini.

Alitoka uwanja wa ndege akaelekea Msasani.  Wakati anaingia getini, Pius naye akawa anaingia nyuma yake. Pius mtoto wa mama. Lazima amuone mama yake kila siku kama yupo hapo jijini, na mawasiliano ya simu ni ya mara kwa mara. Na kwa asili Pius alikuwa mtu wa kujali, mapenzi kwa mama yake yalikuwa dhahiri. Huwezi kumsema Pius mbele ya mama Ruhinda, hapo nikutaka umuudhi huyo mama. Alimpenda huyo mtoto mkubwa kuliko hata kiziwanda Paul. Hakuna kukosana kwa wawili hao. Na jambo alilojua litamuuzi mama yake, hatalizungumza Pius, hata iweje.

Mina akaenda kuegesha gari sehemu ya kuegeshea magari lakini mwisho kabisa kwa kuwa alijua litakaa hapo kwa muda mrefu. Akashuka na kuzunguka nyuma. Wakati anamfungua mtoto wake, Pius akamsogelea. “Vipi Mina?” “Safi shem. Pole na kazi.” “Asante. Acha nikusaidie.” Pius akasogea pale mlangoni. “Nashukuru. Ila nataka kutoa na hicho kiti.” Akamsaidia kufungua kiti kizima cha mtoto, akamtoa mtoto na kiti chake. “Anasinzia huyu.” Pius aliongea wakati anamkabidhi mtoto. “Asante. Sitakaa sana. Naingia kumsalimia baba, naona gari yake ipo hapa nje, niondoke niwahi nyumbani ale ndio alale.” “Mtarudije nyumbani?” Pius akauliza kwa kujali kama kawaida yake. “Hata sijui shem! Nahisi nitachukua taksi hapo nje. Acha nisalimie ndani kwanza mengine nitajua baadaye.” Mina akataka kuondoka.

“Mina.” Mina akasimama. “Mimi nitawarudisha nyumbani.” Mina akainama nakuanza kulia. Giza lilishaanza kuingia. “Kila kitu kitakuwa sawa. Usiwe na wasiwasi. Nimekuahidi mimi nitakuwa na wewe, wakati wote. Unakumbuka?” Mina akatingisha kichwa kukubali.

“Basi naomba tuwe tunazungumza. Chochote kile, usisite kuniambia. Hata ukitaka mtu wa kuzungumza naye, nipigie simu. Sawa?” Mina akatingisha kichwa kukubali. “Basi naomba unyamze. Tukamsalimie mzee, twende.” Akajifuta machozi. 

Walimkuta mzee Ruhinda anasoma kitabu kama kawaida yake akiwa peke yake, anasoma. Ni msomaji sana. Wakamsalimia. “Vipi mwenzako ameondoka salama?” “Nilimshusha uwanja wa ndege. Ameomba niache hapa gari yake mpaka atakapo rudi. Funguo hizi.” Mina akaweka mezani. “Hamna shida. Sasa mtarudije nyumbani?” “Nitawarudisha mara moja.” Akadakia Pius. “Afadhali ili asihangaike na mtoto.” Mzee Ruhinda akalifurahia hilo.

“Acha niwahi baba, Ayan anasinzia.” “Naona na chakula humu bado, dada ndio anapika. Na mama yenu leo atachelewa.” “Nitarudi jumamosi mcheze mpira na Ayan.” Akaongeza Mina akimchungulia Ayan kule alipojiegemeza na chupa yake ya maziwa. “Ewaah! Hayo ndio maneno. Naona leo hataki hata kushuka!” “Si unamjua huyu na maziwa? Hapo nimemfunga mdomo.” Mina na Pius wakaondoka.

                              ~~~~~~~~~~~~~~

Inaendelea…

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment