Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 9. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 9.

Taskii ya kumpeleka uwanja wa ndege ilikuwa ikipambana na foleni kumuwahisha asichelewe ndege yake, huku mawazo yakiwa kwa Pam. Akajipongeza kwa kitendo alichoamua, kubakia naye. Kwanza utabiri wake umekuwa wa kweli. Angebakia pale peke yake bila msaada! “Bora nilibaki naye. Giza lingemkuta peke yake. Na wanavyomuwinda! Wangejinufaisha kwa Pam wangu.” Akawaza wakati dereva akiendelea kukanyaga mafuta yeye hana habari hata na alipo au anapopelekwa.

Akili na mawazo yako kwa Pam. Akajikuta akimshukuru Mungu angalau amepata naye muda japo kwa muda mfupi, lakini angalau wameanzia sehemu. Alitamani kumuomba namba, ila akaonelea amuache tu mpaka mwenyewe aje amuombe. Alikusudia ajitofautishe na wanaume wote kwake. Asijiuze kwa mali na asikimbilie kuomba namba tena mara baada tu ya kumsaidia! Akaona juhudi zake zisiwe bure kwa kukimbilia kuomba namba, itakuwa kama kujilipa.

~~~~~~~~~~~~~

Na Pam naye huku akabaki amejishika shingoni alipopokea busu la Mill. Mawazo yakirudia kila neno alilozungumza Mill. Akavuta pumzi akimfikiria Mill. Ukweli alishavutiwa naye. Macho yake! Jinsi alivyokuwa akijisikia akimwangalia! Halafu Mill ana mwili mzuri wa kiume wa kuvutia. Kwa asili ni mtu mkubwa kwa maumbile. Mrefu halafu mpana. Akaonekana ni mtu wa mazoezi. “Sasa na yeye kwa nini hata asiombe namba!” Akajilalamisha mawazoni mpaka analala usiku mawazo kwa Mill.

Alikuwa na wakati mgumu akitamani kujua kama alipata ndege! Kama alifanikiwa kuondoka! “Aliondokaje amelowa vile!” Hayo yakawa maswali yaliyomsumbua Pam usiku kuchwa, lakini hakuwa na wakumuuliza.

~~~~~~~~~~~~~~

Jerry ndiye rafiki mkuu wa Mill lakini pia ni mume wa Sandra, mmiliki wa hiyo ofisi, na yeye Jerry anasimamia sheria za pale. Ishajulikana Mill ni wa Lona. Leo anavunjaje mwiko kwa kumuulizia Mill wa Lona!

Alifika ofisini siku inayofuata akaendelea na kazi kama kawaida, lakini rohoni hana amani kabisa, mpaka akajishangaa.

Alishinda hiyo siku mawazo yapo kwa Mill mpaka anatoka jioni, kimya. Ila Lona kwa kujibaraguza akawa anamsema vibaya Mill. Kwamba ni mwanaume suruali tu, hana kitu. Kajaa shombo. Ikawa akimsema makusudi mbele ya Pam mwenyewe ilimradi tu kumuonyesha Mill aliyemkataa mbele ya watu wote, akisema anamtaka Pam, si kitu. Pam alinyamaza tu kimya akamuacha aendelee kubwatuka siku nzima mpaka jioni wanatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake mida ya jioni karibu wanatoka, Jerry akampigia simu ya mezani akimuita ofisini kwake. Akaenda. Akamkabidhi kabrasha. “Ndani kuna ujumbe wako. Sasa akili kichwani.” Akapokea akiwa hajaelewa vizuri. Ilikuwa kama barua ndani ya bahasha. Akafungua palepale mbele yake, akakimbilia kusoma jina chini ya ujumbe, akakuta imeandikwa ‘MM’ moyo ukajawa furaha, akajua ni Mill tu. Ilikuwa ni email/barua pepe imeandikwa kwa Jerry kutoka kwa millm@hotmail.com.

“Asante Jerry.” Jinsi alivyoshukuru akijua ameshajua mtumaji, Jerry akajua Mill ashajishindia Pam. Ila akashangaa sana. Asijue mwenzie alibaki mvuani kuweka msingi. Na huyo Pam hajawahi tongozwa na mwanaume anayejitangaza hana pesa hata mara moja. Mill ndio mwanamme wa kwanza.

Kwake akawa amekuwa watofauti, akamuona yeye mkweli kuliko wanao mtongoza na kujigamba wanayo pesa nyingi wakijinadi ni nini watampa.

“Lakini si unaelewa ni lazima kwa hapa uwe makini?” “Najua bosi wangu.” Akamshangaza vile anavyokubali. “Kwamba hata huo ujumbe mimi sijakupa!” “Najua. Na nakuahidi sitakutaja popote. Na sitamwambia mtu. Nilikuwa na wasiwasi kutaka kujua kama alifika salama, lakini nikashindwa kukuuliza. Nashukuru na nakuahidi nitakuwa makini.” Jerry hakuamini. Pam!

Kwamba kirahisi hivyo yupo tayari na Mill aliyemwambia hana kitu na ofisi nzima ilisikia kejeli za Lona siku nzima iliyopita na siku hiyo akimtusi Mill kwa waziwazi! “Kweli kila shetani na mbuyu wake!” Akajiwazia Jerry wakati Pam akitoka hapo ofisini akiwa na hilo kabrasha lenye ujumbe kutoka kwa Mill.

Akaenda nalo chooni. Akaanza kusoma.

‘Pam, namshukuru Mungu tumefika salama. Na namshukuru Mungu na wewe ulifika salama. Nilipofika Doha, nilihakikisha yule mzee alikufikisha salama kwa kuzungumza naye. Nilimuomba namba yake ya simu kabla sijamkodi akurudishe nyumbani. Na yeye akawa muungwana, alipokea simu yangu na kunihakikishia alikushusha nje ya geti la nyumbani kwenu. Hiyo imenituliza na kunipa amani kwamba upo salama. Nakutakia kila la kheri. Ufanikiwe katika kila jambo.’ Ikaishia hapo asiamini kama aliweza muomba namba mwenye taksii, ila si yeye!

Akabaki akiwaza hapo chooni. Mwishoe akatoka akiwa ameweka ile barua kwenye sidiria kabisa, isije anguka.

“Mbona hata asiniombe namba yangu!” Gafla mchoyo wa namba huyo, akajilalamisha. Pam asiyethubutu kutoa namba yake kwa mtu, mkali, asiyetaka na namba yake ya simu, gafla anaumia kutoombwa namba ya simu! “Wanaume hawa! Huwezi jua. Ukute huko ana mtu wake, hataki mawasiliano ya huku.” Huo ukawa ukweli alioupokea, na kuamini. Ila akajikuta kawivu kanaanza tena.

~~~~~~~~~~~~~~

Juma hilo likaisha, kukawa kimya hajasikia kutoka kwa Mill ila angalau Lona akapata mwanaume mwingine aliyekuwa akisifiwa hapo! Pam akajua anamfanyia makusudi kama kushindana. Ukweli Pam alikuwa mzuri wakuvutia. Kwa hiyo wateja wao wengi walimkimbilia yeye, ndio wakazidisha mtindo wakuwahi. Na hata huko wanapokuwa na hao wanaume, bado walibakia kumuulizia Pam wakiwataka haohao kina Lona wawasaidie kwa Pam. Wakawa wakiishia kumponda Pam, wakimchafua kwa hao wanaume kwa hili na lile ilimradi tu wabakie nao hao wanaume.

Pam alikuwa akijua, lakini hakuwa akijali. Ni Mill peke yake ndiye aliyeonyesha msimamo wa waziwazi kuwa yeye hatachua mrembo yeyote pale ila Pam.

Majigambo ya Lona yakaendelea ya muda tu pale ofisini kuwa amepata mwanaume mwenye pesa. Pam kimya.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku ya jumamosi ambayo ni nusu siku Pam alikuwa akienda yeye benki kuweka hundi walizolipwa kama kampuni kisha kuondoka moja kwa moja nyumbani. Akaenda ofisini kwa Jerry akamkuta anamuandalia. “Nimewahi sana nini?” “Nimemfanyia kusudi Lona. Alitaka yeye ndio aende ili asirudi tena ofisini. Nikamwambia leo ni zamu yako na hata hivyo sija andaa. Ndio akaondoka.” Pam akakaa.

“Katika hizi hundi, katikati kuna ujumbe wako.” Akamuona anafikiria. “Vipi? Hutaki, nirudishe majibu?” “Hapana, nafikiria jinsi ya kuwasiliana naye!” Jerry akacheka sana. “Pammmm!” “Sio kwa nia mbaya!” Jerry akazidi kucheka.

“Pam huyu ndio wakuomba mawasiliano ya mtu, kweli?!” “Amekua mtu mzuri!” Jerry hana mbavu. “Mill huyo?” “Acha bwana Jerry! Mkeo ataingia sasahivi.” “Nitakavyokubadilikia! Kama sikujui.” Akacheka akisimama. Walimjua Sandra. Mkali kama pilipili. Aliwaweza wote hapo.

“Kwa hiyo upo sawa nikimpa namba yako?” Akamchokoza. Pam akacheka akitingisha kichwa kukubali. “Sawa mama. Mjumbe mimi sina neno! Ila chonde mama! Ukikamatwa, hakika sikujui.” “Nipo makini. Usihofu.” Akatoka akiwa na shauku akitaka kujua safari hii Mill amemwambia nini!

Alipopanda tu kwenye gari ya kazini, dereva alivyoondoa gari akafungua bahasha. Kukawa na ujumbe mfupi sana. ‘Pam, upo mawazoni mwangu.’ Ukaishia hapo. Akatamani angeandika zaidi. Akabaki akiwaza nakutamani Jerry ampe namba yake kwa haraka, asihau.

~~~~~~~~~~~~~~

Macho kwenye simu hata alipokuwa saluni. Muda wote akitizamia ujumbe kutoka  kwa Mill. Akawa mtumwa wa hiyo simu mpaka akajichukia! Watu husubiri namba yake ya simu wakiisaka kwa udi na uvumba! Leo yeye ndio amegeuka wa kusubiria simu ya mwanaume! Akazidi kujishangaa kilichompata! Masaa yakazidi kuwa marefu zaidi ya Mungu alivyoyaumba. Usiku ukazidi kuwa mzito kwa kutosikia kutoka kwa Mill. Akaanza kujidharau kumpa namba bila kuombwa.

Kila Mtu Hupenda Kupendwa.

Wakiwa wanapitiwa na usingizi ujumbe ukaingia na kumfanya Mina kuchukua simu yake na kusoma. ‘Upo Mina wangu?’ Akafurahi mpaka akajikuta akicheka. Alishajutia kitendo chakumwambia achukue muda afikirie kabla hawajaendelea kwenye mapenzi. Akajua baada ya pale alifikiria na kujiona mjinga kumkataa Lora kumtaka yeye mchafu. Sasa jinsi alivyoandika huo ujumbe! Mina akafarijika sana na kujibu kwa haraka.

 ‘Ndio nilikuwa napitiwa na usingizi. Umekuwa na jumapili nzuri?’ Mina akauliza. ‘Ilitaka kuisha vibaya, lakini nipo sawa. Nilienda kukimbia baharini, ndio narudi. Angalau akili imetulia.’ ‘Itabidi siku nyingine ukimbie na mimi akili itulie.’ ‘Ninaweza kukupigia?’ Mina akamwangalia mama yake. Akamkuta mama yake akimtizama, wakacheka kwa pamoja. “Anataka kunipigia.” “Nenda kazungumze naye.” “Nitamuamsha Ron!” “Kakae sebuleni upunguze sauti.” Mina akatoka huku akicheka.

‘Sasa hivi unaweza kunipigia.’ Akamtumia huo ujumbe, Andy akapiga. “Kwa nini akili ilikuwa haijatulia?” Mina akaanza. “Mambo ya familia tu. Lakini nimefurahi kusikia sauti yako.” “Kweli!?” “Kweli, si ndio maana nimetaka tuzungumze!” Mina akacheka. “Kuna kitu nilikutana nacho jana. Nikafikiri kitakufaa.” “Nini?” “Najua upo unasoma. Lakini hivi unajua kitu hicho hicho unachosomea pale, unaweza kukisomea kwenye chuo kama IFM na ukapata cheti kizuri zaidi? Ukapata certificate in Computing and Information technology.” “Najua Andy.” Mina akaongea taratibu.

“Sasa kwa nini usihamie hapo? Sidhani kama utaanzia mwanzo kabisa. Wanahamishia masomo yako na mitihani uliokwisha fanya.” “Najua Andy, lakini ada yake ni kubwa. Nishauliza. Na nilishachukua mpaka fomu zao.” “Basi tukutane kesho mchana tuzipitie pamoja.” Hilo likamfurahisha Mina. Wakazungumza kidogo, wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake alipomaliza tu darasa la mwisho, wakati anatoka, akamkuta Andy anamsubiria nje. Akacheka. “Nimefurahi kukuona.” Andy akacheka. “Na mimi nimefurahi kukuona. Umependeza.” Mina akakunja uso huku akijiangalia. “Sema asante bwana!” “Haya, asante.” “Sasa twende tukale, halafu tukakutane na mtu pale IFM, atatusaidia.” Wakatoka hapo.

Akapelekwa kula sehemu nzuri, ya hadhi ya kina Andy. Tatizo akawa hajui kutumia kisu na uma. Hilo nalo ikawa tofauti nyingine. Familia hiyo ya Ruhinda hawali kwa mkono. Anampelekaje kwao!

Akamuona amekosa raha. “Tumia tu uma.” Mina akamwangalia. Andy hakuwa akishika chakula hata paja la kuku kwa mkono. Ni uma na kisu kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Hata wali alikula na uma. “Siwezi Andy! Nashindwa.” “Unataka kulaje?” Andy akamuuliza kwa upole. “Huwa nakula kwa mkono.” Andy akabaki kama anayefikiria. “Hata hivyo mimi nimeshiba.” Mina akasogeza sahani pembeni. “Hujala hata kidogo!” “Nitaenda kula kwa mama Ron.” Andy akacheka.

“Nenda ukanawe mikono ‘bathroom’ ndipo uje ule.” “Kwani hapa hawanawishi watu mikono!?” “Hapana Mina.” Mina akaanza kuishiwa nguvu. “Nenda.” Mina akaenda maliwatoni kunawa mikono na kurudi kula. Mara nyingi alitumia mikono, Andy akimwangalia. Lakini akala mpaka akamaliza chakula chote kwa kutumia tu mikono yake.

IFM

Walifika IFM wakakutana na Dean of students, ambaye alikuwa rafiki wa Andy. Akamuhoji Mina maswali mawili matatu, kiurafiki tu. Alipoelewa mengi kutoka kwa Mina, ndipo akamshauri Andy, asubirie aanze na wengine muhula unaofuata kwa kuwa ni kama aliyoyasoma Mina, ni ya chini sana. Hayaendani na ya pale. Wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

“Kwa hiyo ni kama pale napoteza muda tu?” “Hapana Mina! Naomba usivunjike moyo. Maliza pale kwa bidiii zote, halafu baada ya miezi mitatu tu, unakuja hapa. Tena kwa kuwa utakuwa na certificate ya pale, huku utakuja kufanya diploma.” “Ndio miaka mingapi!?” Akauliza kwa hofu kidogo. “Kwani wewe ulitaka kusoma mpaka lini ndio iwe mwisho?” “Sijui Andy! Wewe unanishaurije?” Hilo likamfurahisha Andy. “Wewe bado mdogo Mina. Huna sababu yakutojiendeleza. Kama ukipata nafasi, itumie.” Mina akanyamaza.

“Au unaonaje?” “Nitajitahidi Andy. Japo naona kama hayo mambo unayotaka nikasomee sio kama hichi ninachofanya. Naona yatazidi kuwa magumu!” “Naomba usiogope. Usiweke hofu kwanza ila jipe muda. Hakuna haraka. Fikiria, halafu amua. Ila nakuahidi kama ukichagua chochote kile, mimi nitakusaidia. Hata kutafuta mwalimu wa ziada. Ni sawa?” “Sawa.” Wakakubaliana. Mchana huo badala ya Andy kuwepo kazini, alikuwa akihangaika na Mina. Alimrudisha mpaka karibu na kwao ndipo akarudi kazini.

Andy kwa Ron.

Aliporudi, akamuita Ron ofisini kwake. “Niambie kiongozi.” “Naomba leo baada ya kazi tupate muda wa mazungumzo.” Ron akashangaa kidogo. “Kwema!?” “Kwema kabisa. Ni mambo nje ya kazi.” “Oooh! Hamna shida. Nilifikiri ndio kazi imeisha!” Wakacheka kidogo na kukubaliana baada ya kazi, watoke pamoja.

Mara nyingi Ron ndio anakuwa wa mwisho akimalizia kufunga kazi za wote ndipo anamtumia Andy, nakuondoka. Andy alibaki ofisini kwake akimsubiria. Alipoona tu ripoti imeingia, akajua amemaliza. Akasikia simu yake ya mezani inaita. “Mimi nipo tayari. Ukimaliza utanikuta hapo nje.” Alikuwa Ron. “Okay.” Akajibu na kukata.

Baada ya muda akatoka na kumkuta Ron anazungumza na dada yake. Akamuona anacheka, “Acha uchokozi Mina!” Akamsikia akisema hivyo na kukata.

“Ungependa kula wapi?” “Kiongozi leo unataka ukanipe dinner?” Andy akacheka. “Mazungumzo yasindikizwe na chakula.”  Wakaongozana mpaka Surrender Pub. Wakaagiza nyama choma. Wakajikuta wote hawanywi pombe. Wakaagiza na maji ya kunywa wakaanza mazungumzo ya kawaida tu. Ila Ron akawa na hamu yakujua anachotaka kuambiwa na kiongozi wake. Alimuona amejawa na wasiwasi! Akashindwa kumuelewa ni nini hicho kizito anachotaka kusema. “Kwema lakini?” Ikabidi Ron ammrudishe kwenye lengo la kukutana hapo. Maana wao si marafiki, nini chakuwaweka pamoja!

“Nilisomea Nairobi tokea shule ya msingi mpaka sekondari. Ila chuo kikuu ndio nilisomea chuo kikuu cha Kampala, Uganda.” Ron akatulia akitaka kujua mwisho wa yale mazungumzo ni nini! Akabaki akimwangalia na kumuongezea wasiwasi Andy. “Kuna kipindi mpaka mimi mwenyewe nilifikiria kuwa padri.” Ron akacheka kidogo. “Kabisa. Maana shule niliyosoma ilikuwa ni ya mapadri na wakawa watu wa karibu yangu sana.” “Ungefaa Kiongozi.” Andy akacheka. “Nafikiri haukuwa wito wangu.” Wakacheka tena. “Nilipofika chuoni, nikapata msichana.” “Uliacha wito, Kiongozi?” Wakataniana kidogo, akaendelea.

“Lakini nafikiri haukuwa mpango wa Mungu. Tuliachana. Anyways, akaja Lora.” “Kiongozi leo unatafuta kitubio nini?” Wakacheka sana kisha akaendelea. “Sasa Lora ni binti ambaye tumekuwa tukifahamiana. Ni mdogo kwangu karibu kidogo kulingana na mdogo wangu wa kiume ambaye ni daktari pale Muhimbili. Sasa tukirudi kwa Lora, ni kama wazazi wetu wote walitamani tuoane.” “Lakini Kiongozi sio wazo baya!” Ron akaongea kwa utani.

“Wazo sio baya, lakini nafikiri hatukukusudiwa.” Ron akatulia kidogo. “Mbali na kile kilichokuwa kikionekana kwa nje, hatukufika mbali. Tulikuwa tumechukua muda wa kusomana tu, lakini week iliyopita, tukakaa chini na kutafakari, wote tukakubaliana kuacha tu.” “Kwamba mmevunja mahusiano!?” “Yeah! Kwanza hatukuwa tumefika mbali kwa ukweli. Ila pia kulikuwa na sababu nyingine iliyonifanya nisivute zaidi.” Ron akawa ametulia anamsikiliza.

Chakula kikaletwa. Kama kawaida yake, akaomba kisu na uma, Ron akanawa mikono, nakuanza kula na mkono kabisa kama dada yake. Aliokota ndizi na nyama kwa mkono. Akala kachumbari pia kwa mkono, bila hata wazo la pili, Andy akimtizama.

“Ehe!” Ron akataka aendelee huku akila kwa furaha zote bila kuona kuna alichopungukiwa, mambo ya kutumia kisu na uma.

 “Japokuwa mahusiano yangu na Lora hayakuwa ya muda mrefu, lakini niliyasitisha mapema kwa kuwa nilijihakikishia kabisa, kuwa hawezi kuwa mke wangu.” “Naona Kiongozi unataka kuoa si kuchezea.” Ron akatania.

“Nashukuru kama hilo umelielewa. Lengo nataka mke. Si msichana tu wakuonekana naye mbele za watu na kuburudishana tu. Hapana. Sijui kama unanielewa?” “Naona kama nakupata!” Ron akaafiki nakuendelea kula. “Basi ndio maana ilibidi kukatisha mahusiano yangu na Lora, sababu ya kile ninachojisikia kwa Mina.” Ron akashituka mpaka akapaliwa na maji aliyokuwa anakunywa. Akaanza kukohoa. Alikohoa kama dakika hivi mpaka macho yakawa mekundu.

“Pole sana.” “Subiri kwanza Andy!” Hapo jina la Kiongozi likaisha. Ron akanywa tena maji. “Umesema Mina, Mina dada yangu mimi!? Au sijakusikia vizuri?” “Namzungumzia Mina, ndiyo.” Ron akabaki akimtizama. “Najua utakuwa huamini lakini nampenda sana Mina. Kile ninachojisikia kwa Mina, sijasikia kwa mwanamke mwingine yeyote na...” “Subiri kwanza Andy. Wewe unaongea kitu ambacho hukijui. Humjui Mina hata kidogo!” “Kwa sasa namfahamu kwa asilimia 90. Nilimpenda nikiwa namfahamu kwa asilimia kama 7 hivi, lakini sasa hivi nina mfahamu kwa asilimia 90.” Ron akakunja uso.

“Andy! Wewe ni mtu unayejiheshimu sana. Na mimi nakuheshimu, tafadhali naomba kabla hujafika mbali katika hili na tukashindwa kufanya kazi mimi na wewe, naomba hicho unachokifikiria kinakuvutia kwa Mina, acha kabisa. Tafadhali sana.” “Labda kuwe kuna cha tofauti na kile alichoniambia Mina mwenyewe.” Ron akatulia kidogo akimtizama ila mwishoe akaona aulize tu.

 “Inamaana umeshazungumza na Mina mwenyewe!?” “Ndiyo.” Ron akamkazia macho. “Wewe ndiye uliyetoka naye siku ya jumamosi!?” “Kwa kuwa nilitaka kumuhakikishia nataka kutulia na yeye tu. Na kwa kuwa alishaniona na Lora, nilitaka ahakikishe yupo na mtu ambaye yupo salama. Na nilitaka kumuhakikishia mimi sina mpango wakumchezea. Kwa hiyo nilitaka awe na mimi hospitalini wakati naangalia afya yangu kwanza. Ahakikishe naanza na yeye nikiwa mzima kabisa, ndipo nikamchukua mpaka nyumbani kwangu. Tukapata muda wa mazungumzo. Mrefu tu.” Ron alibaki ameduaa.

“Na kwa kuwa saikolojia ni moja ya somo nililosoma na kulifanyia kazi kidogo wakati nikiishi na mapadri kule Nairobi, nina uhakika hajanidanganya. Ameniambia ukweli.” Ron akajivuta vizuri. “Labda niulize, upande upi wa Mina unaoujua wewe?” “Wote, na ndio maana nimekwambia namfahamu kwa asilimia 90.” Ron akawa kama hajamuelewa.

“Subiri kwanza Andy, kwa hiyo wewe unajua kuwa Mina aliishi na...” “Omar, aliyemtoa kwa wafanyakazi wake? Wakaishi Iringa, akampiga mpaka akamtoa mimba?” Akamalizia na swali lililomfanya Ron abaki ametoa macho.

“Nafahamu Ron. Ameniambia.” Ron akaishiwa maneno. Akarudi nyuma na kujiegemeza kwenye kiti. “Tumekubaliana tupeane muda wa kuchunguzana. Na yeye aangalie kama mimi nitamfaa kuwa mume wake.” Ron akabaki akimtizama.

 “Kwa hiyo ndipo tulipofikia hapo, nilitaka na wewe ujue. Na ninafanya hivyo makusudi kwa heshima ya Mina mwenyewe, na yenu. Sitaki kujificha naye. Nataka hata wewe ujue, ili niwe huru na Mina.” Ron akashindwa ajibu nini! Andy akaelewa yupo kwenye mshituko, lakini akaendelea tu akitaka ujumbe wake ufike siku hiyo.

“Kwa sasa nimemuomba anisubiri. Anipe muda wakumfahamu vizuri yeye kama Mina. Na mimi anifahamu. Akiona sitamfaa, aniambie, na mimi nitamwambia, ndipo atafute mtu mwingine. Ameniahidi kuwa hatakubali mtu mwingine mpaka ahitimishe na mimi.” Andy akajieleza vizuri tu.

“Hivi unajua kama Mina aliishia kidato cha nne, yaani kwa mara ya kwanza ndio amekubali kusoma? Ndio anarudi shule sasa hivi! Unalijua hilo?” Ron akauliza. “Najua, ameniambia. Na ninajua hapendi hesabu.” “Sio hesabu tu. Mina hapendi SHULE. Ndio maana alivyokubali tu kusoma, nilihakikisha hasubiri na hakuna kinachomzuia asisome.” Ron akaweka msisitizo.

“Nafahamu Ron. Na ninakuahidi sitamfanya asisome. Leo nimetoka naye IFM. Niliona kwa haraka masomo ya certificate pale. Nikazungumza naye kutaka kujua kama angependa kusoma pale kwenye chuo ambacho angalau kinaeleweka. Akakubali lakini akasema tatizo ni pesa. Sasa kwa kuwa yule Dean wa pale nafahamiana naye, nikaenda naye leo. Akamuhoji maswali, akatushauri tusubiri aje aanze mwanzo kabisa. Kwa hiyo nimezungumza na Mina. Nimemtia moyo amalize hiki anachokisoma sasa hivi, halafu aende pale akasomee mambo ya IT.” Ron akatoa macho. “Mina asome IT!?” “Amekubali. Na nimemuahidi nitamsaidia kama akikutana na ugumu wowote ule.” “Amesemaje?!” Ron akauliza kama ambaye haamini. “Anaonekana ameridhia.” “Mina!?” “Ndiyo.” Ron akakunja uso.

“Anajua kama anatakiwa akae darasani si pungufu ya mwaka lakini au hilo hujamwambia!?” “Ron, Mina amebadilika. Tafadhali naomba na nyinyi mumpe nafasi.” “Huelewi Andy! Huelewi na ninahofia unataka kujiingiza kwenye kitu ambacho kitakuja kutukosanisha sana sisi na kutufanya tushindwe kufanya kazi.” Ron akajisogeza vizuri kwa Andy.

“Mama yetu hana mwanaume, isipokuwa mimi. Kazi niliyonayo, imempunguzia mama majukumu mengi sana. Naomba Mungu mchana na usiku, mama naye akinisaidia kuomba ili kusiharibike jambo pale kazini, ndio maana unaniona nahangaika na kujituma sana, Andy.” “Nafahamu Ron.” “Basi naomba punguza kasi kaka. Mina bado mdogo mno. Akili zake zipo kama vile ulivyomuona siku ya kwanza ulipokuja nyumbani. Ni mtoto. Ila wanaume wakimtizama kwa nje kwa haraka, wanachanganyikiwa. Mina ni mtoto ambaye bado anahitaji kuongozwa.” Ron akawa kama anamsihi.

“Nimekaa na Lora, nimekaa na Mina. Nimekuwa na mahusiano ya kimapenzi pia. Ya muda tu. Najua ni nini naongelea Ron, na ninajua ni nini nakifanya.” Ron akajua Andy ameshaamua. “Tafadhali mpeni Mina nafasi na mumuonyeshe mnamwamini.” “Kwani hayo unayotuambia ni mageni kaka? Mina ashaaminiwa pale nyumbani zaidi ya nitakavyokwambia! Hizo nafasi unazosema apewe, amepewa mpaka mama amemaliza.” Ron akajiweka sawa ili kujaribu kumshawishi Andy, pengine atamuelewa aachane na Mina, mdogo wake.

“Alianza kwa ukali kwa Mina. Mpaka kumchapa. Nikisema kuchapwa, Mina amechapwa yule mtoto, hakuna jinsi. Lakini kama unavyomjua Mina, akili zake za kitoto, akawa akichapwa, analia halafu anataka mama huyo huyo eti ndio ambembeleze.” Andy akacheka. “Sikutanii. Ikabidi mama abadili adhabu. Akidhani atajifunza. Labda kumnyima hiki au kile anachokipenda. Lakini Mina hajui kununa. Mama napo hapo akashindwa. Akaona ni kama haelewi. Akajirudi kuwa rafiki. Tunahangaika na Mina, naona tokea yupo darasa la saba.” “Ameniambia.” Ron akashindwa kumuelewa.

“Kama ni lile umbile lake, Andy, Kiongozi wangu, mbona Lora ni mzuri tu kaka?” “Sio umbile Ron, nampenda Mina.” “Daah! Kwa maana nyingine ni kwamba umeamua?” “Nakutaarifu ili ujue simuibi dada yako. Nia yangu ipo dhahiri, labda abadilike baada ya hapa lakini si kwa alivyoishi zamani.” Ron akabaki kimya akimtizama.

“Na atasoma. Naomba tumchukulie hatua kwa hatu kama ulivyofanya naye. Na mimi nitamchukulia kwa utaratibu kabisa. Sitamuwekea pressure yeyote ile ila kumtia moyo. Na hata akimaliza hii na kukataa kuendelea, pia nitamuacha na kuheshimu maamuzi yake.” Ron kimya.

“Ron?” “Daah! Mimi sina chakusema tena Andy. Naona umefikia maamuzi. Na ninavyokujua kwa kukuona pale kazini, wewe si mtu wa kubadilika. Ila naomba unihakikishie Andy, na hili nitakukumbusha.” “Nini?” “Yatakapokushinda kwa Mina, tafadhali usilete kwenye kazi yangu. Usije ukanichukia mimi kwa kuumizwa na Mina.” “Haitakaa ikatokea.” “Basi ni hilo tu kaka. Maana mahusiano yako na Mina yanaweza yakaharibika, ila mimi hata iweje, Mina ni mdogo wangu. Katika lolote, nitakuwa upande wake.” “Hilo nalielewa. Na ninakuahidi sitaingiza mambo yangu na Mina, pale kazini.” “Basi ni hilo tu.” Ron akaonekana ni kama ameridhia. Akaendelea kula.

“Naomba nikaribie nyumbani. Angalau mama anifahamu, ili nisiwe naishia njiani na Mina. Sidhani kama ni jambo la heshima.” Ron akanyanyua macho akabaki akimtizama. “Sijasema nakuja kutoa mahari Ron! Nataka mama anifahamu, ili Mina anapotoka, mjue yupo kwangu. Na utakapomuona Mina pale ofisini, awe huru hata kuja ofisini kwangu na kunisalimia.” “Unataka na kazini wamtambue kama mtu wako!?” Ron akashituka sana.

“Mambo yakienda vizuri nitamuoa Mina. Sina chakuficha kwa yeyote. Kwa nini iwe tatizo watu kumtambua kama nipo naye kwenye mahusiano?” “Hivi Andy umefikiria vizuri lakini?” “Mimi si mkurupukaji Ron. Nafikiri kwa sehemu utakuwa umelifahamu hilo.” Ron akabaki akimtizama.

“Nataka Mina akisema ‘Ndiyo’ kwangu, awe anajua anaolewa na mtu wa namna gani. Anifahamu katika kila eneo la maisha yangu.” Ron akainamia sahani yake akaendelea kula. “Kwa hiyo siku gani ni nzuri kuja kumuona mama?” Andy akaendelea. Ron akamtizama. “Daah! Umekazana Andy!” Andy akacheka.

“Ikishafika saa 12 kamili jioni, mama anakuwa ameshamaliza shuguli zake zote, yupo nyumbani. Siku za jumamosi mara nyingi anakuwepo nyumbani. Ana biashara ya chapati. Kwa hiyo anazipika. Jioni ndio mimi nakwenda kumsambazia. Yeye anakuwepo tu nyumbani anapumzika. Na jumapili inategemea. Tukitoka kanisani, huwa mara nyingi tunasimama sehemu kula, ndipo tunarudi nyumbani. Siku hiyo hafanyi kazi kabisa.” “Basi mpaka hapo naona jumapili ndio niongozane na nyinyi.” Ron akabaki akimtizama.

“Nije asubuhi, twende wote kanisani, tukale, ndipo turudi nyumbani. Ni sawa?” “Nitamwandaa.” “Nashukuru kwa kunielewa Ron. Utaturahisishia sana mimi na Mina.” Ron akavuta pumzi kwa nguvu. “Sijui niseme na mimi nashukuru kwa heshima uliyotupa! Maana ungeweza kupotea naye baada yakujua ni binti mrahisi tu.” “Hapana Ron. Nafikiri nyinyi bado mna Mina yuleyule wazamani. Mina niliyekutana naye mimi si mrahisi kama unavyodhania. Hana malengo mazito, lakini anao msimamo katika kidogo alicho nacho. Hata pale kazini wamemjaribu jaribu, lakini amewakataa.” “Kina nani!?” Andy akacheka.

“Acha kupaniki bwana! Mimi mwenyewe nilisikia tu fununu. Nilimuuliza jumamosi, akakiri ni kweli na aliwakataa. Kwa hiyo mpe credit Mina wangu bwana! Amebadilika. Sio mrahisi hivyo.” “Daah! Itachukua muda, lakini hata sisi tunamuona. Tokea arudi, jumamosi ndio ametoka kwa mara ya kwanza. Mama alishindwa kufanya kazi kwa wasiwasi.” “Aliniambia.”

“Sasa ndio ujue jinsi hali ilivyo mbaya! Mimi mwenyewe nilishindwa kutoka ikabidi nikae na mama. Alikuwa akilia anasema hadhani kama atakuja kumuona tena.” “Hii jumamosi!?” Andy akashangaa sana. “Ndiyo! Hii jumamosi! Mina ni mpoteaji sana. Na kama unavyomuona. Akirudi mtajua yupo. Sio mbishi wala mvivu. Atafanya kila kitu utakachomwambia. Atasaidia kila mtakachomtuma. Atawachangamsha, gafla anapotea. Anarudi anakaa kidogo, anapotea tena. Kwa hiyo mama anakuwa na wasiwasi sana. Na hakuna mwanaume hata mmoja aliyekuja pale nyumbani kama hivi unavyotaka kufanya wewe. Wote wanamchukua juu kwa juu. Hawajulikani majumbani kwao na sisi tunakuwa hata hatuwajui. Kwa hiyo akiondoka, mnakuwa hata hamjui mumtafutie wapi!” Andy akanyamaza. Wakamalizia chakula.

“Nitakuja nyumbani jumapili asubuhi.” Ron akamtizama kama asiyeamini. “Nitakuja.” “Sawa Kiongozi.” Wakaagana, akamshusha Ron kituo cha daladala pale pale Palm Beach, yeye Andy akarudi kwake. Akiwa na utulivu kuwa angalau amefanikiwa kumuweka sawa kaka mtu, akajua mama yao hatakuwa na shida.

Ikabaki kwao sasa, kwa kina Ruhinda. Anampelekaje Mina huko kwao! Ndio ukabaki mtihani mgumu kwa Andy. Ukweli Mina na familia yake, walikuwa hawaendani kabisa na kwao. Akatamani ingekuwa tofauti, lakini hawezi badilisha chochote. Moyo na akili vinamtaka Mina. Anafanyaje?!

~~~~~~~~~~~~~~

Inaendelea…

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment