Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 8. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 8.

Baada ya ukimya wa kutosha kupita hamsikii akisema chochote, Mina akajua akufukuzae, hakwambii toka! Akaona ajitoe mwenyewe. “Naomba nikushukuru kwa chakula.” Andy akacheka. “Ulishashukuru. Au ndio unaniaga?” “Naona nirudi tu nyumbani. Tutawasiliaana Mungu akipenda.” “Hatujamaliza mazungumzo bwana!” Akacheka kidogo kiiungwana kama kujirudisha pale japo wazi alionekana alikuwa mbali sana na pale.

“Naamini kwa sasa unanifahamu kwa asilimia 100, Andy. Hakuna nilichobakiza. Kuanzia wazazi, mimi mwenyewe, zamani na sasa. Unanijua.” “Sijui baadaye.” Mina akamwangalia na kuinama kama anayefikiria.

 “Eti Mina?” “Mimi mwenyewe sijui baadaye yangu Andy. Ila naomba nikuombe kitu.” “Karibu.” Andy akajiweka sawa. “Leo ndio umenifahamu kwa undani sana. Na wewe unaonekana sio mtu mbambaishaji au tapeli. Hiyo naongea kutokana na ulivyoniambia juu ya Lora na sifa zako nilizozisikia pale ofisini.” Andy akacheka akijua jinsi maneno yanavyojua kuzagaa pale ofisini kwao! Akajua hapo Mina amejazwa maneno juu ya kila mtu.

Mina akaendelea. “Naomba kwa leo tuishie hapa, ili wote tupate muda wakufikiria. Tusipeane ahadi yeyote. Hata kuniambia utanipigia simu, tuache kabisa, muda uje ujibu kila kitu.” Andy akatulia kwa muda. Kila akitaka kumruhusu aondoke, moyo unakataa. Hisia anazozipata kwa huyo Mina! Hajiwezi! Gafla akaanza kumuelewa Omar. “Ngumu kuishi bila huyu kiumbe aisee!” Akawaza na kumwangalia, akakuta akimsubiria.

“Labda nikuulize swali moja la mwisho.” Andy akaanza. “Wewe binafsi, upo na malengo gani ya baadaye?” “Nisikudanganye Andy, ili unione wa maana. Binafsi maisha yangu ndio kama yanaanza. Natembea kwa hatua ndogo ndogo sana, tena kwa tahadhari, nikijua mama na Ron wananiangalia kwa makini, na mimi ninajiona ninawajibika kwao. Sijui mshahara wa Ron, lakini anamsaidia mama kunisomesha. Hiki ninachosomea sasa hivi, hata sikujua kama ningesomea. Nimekuja kukutana nacho muda mfupi uliopita. Nikiwa na maana hii, sina uelewa na mambo mengi kiasi chakuweka mipango ya kusikika yamaana.”

 “Hata hapa nilipokaa sasa hivi, sijui ni kwa nini nipo hapa sasa hivi. Nahisi ni kama nilivyokwambia. Pale hospitalini, moyoni kwangu ulisikika ukiwa halisi sana kitu ambacho sikuwahi kukisikia kwa matapeli wote niliokuwa nao.” Mina akaendelea taratibu.

“Nikikwambia nilikusubiria, niamini nilikusubiri. Nilijiambia mimi ni mchemshaji, na nimeishi na matapeli. Lakini wewe nikakutetea nafsini mwangu, nikasema upo ukweli niliousikia tokea rohoni, ile siku nikiumwa. Nikawa najiambia lazima utarudi tu. Hata kwa kuchelewa, nikajihakikishia utarudi kuja kuniona tena. Nilikusubiria mpaka jumatano natoka pale hospitalini.”

“Lakini Ron alikuwa ameniambia wewe ni bosi wake sio rafiki. Nikakumbuka hiyo hali yako ilivyo. Na pale uliponikuta nimelazwa, nikajifariji kuwa labda nilikuwa sahihi, hukudanganya ila mazingira yalikushinda kurudi. Nikatamani hata kukusikia ukiniambia sababu yakutokurudi! Ukanionyesha ni kama hukumbuki kabisa! Nikazidi kujidharau nakujiona ni mjinga ambaye nimeshindwa kujifunza kutokana na makosa! Nakuwa naamini watu hovyohovyo tu! Sasa kuja kumuona na Lora naye, ndio ikabidi niwe mpole kabisa.”

“Daah! Kumbe afadhali ningerudi hata kwa kuchelewa!” Mina akacheka na kuinama. “Nimeharibu.” “Ninachotaka kusema, ni maisha yangu ndio yanaanza. Nasikitika kuwa yanaanza nikiwa nimeshakuwa mkubwa. Lakini ndio yanaanza. Sijui kesho itakuaje Andy. Kama nilivyokusimulia, mimi sio mtu wakusubiriwa. Au kuacha mipango yako kwa ajili yangu. Nashauri..” “Umesema leo tusiwekeane ahadi. Tujipe muda. Sasa mbona unataka kuniamulia tena!?” Mina akanyamaza.

“Mimi ndiye niliyeomba nafasi yakuwa muamuzi wa hili. Unakumbuka?” “Nakumbuka.” Mina akajibu taratibu tu.

“Naomba nikuulize tena.” Mina akamwangalia. “Kwa hivi ulivyonifahamu. Nikaharibu kwako kwa kutoa ahadi ambayo sikutimiza. Ingekuwa sijaharibu hivyo, tukakutana kwenye mazingira mazuri, au nikarudi siku ile hospitalini, unafikiri kama ningeomba mahusiano na wewe, ungekubali?” Andy akauliza kama anayeogopa tena kumpoteza!

“Niambie ukweli wako kutoka moyoni Mina. Unafikiri ningefaa kuwa mwanaume wako ambaye ungekuwa na mimi tu mpaka kifo?” Mina akawa hamuelewi! Na yote aliyo mwambia! Akatulia akitafakari, mwenzie akajua ndio anamkataa.

“Ndio niliharibu kwa kiasi hicho!?” Akauliza kinyonge. “Kwamba siwezi kusamehewa tena?!” Yeye ndio akawa mbembelezaji tena! “Hapana Andy! Ni mimi mwenyewe nakosa ujasiri!” “Tafadhali naomba unijibu tu. Hii inamaana kubwa sana kwangu. Nataka kujua.” “Nikujibu hivi hivi kwa yote niliyokusimulia juu yangu!?” Mina akauliza kwa kumshangaa zaidi ila kuvutiwa naye. Kwamba ni kama anampenda alivyo!

“Vyooote. Wewe kama Mina na jumla yako yote. Nataka kujua. Je, ningefaa?” “Kwanza naomba nikuhakikishie kuwa nimebadilika Andy.” “Sawa.” Andy akakubali bila tatizo. “Na ninakuhakikishia sitarudia ile tabia yakuwa na wanaume hovyo. Au kuwa na wewe na wanaume wengine, au kufanya ngono hovyo. Nimebadilika.” Andy akacheka taratibu na kuongeza. “Sawa Mina. Mimi bado nataka jibu langu. Unafikiri ningekufaa?” “Ndiyo Andy.” Mina akajibu taratibu na kwa unyenyekevu.

Akamuona Andy anafunga macho na kuvuta pumzi kwa nguvu. Akajirudisha nyuma kwenye kochi. Akajiegemeza kichwa, akiangalia dari kwa muda. Kila hesabu aliyokuwa akipiga hapo kichwani mwake, jibu ni Mina. Upendo ukawa na nguvu kuliko yote. Nafsi inamtaka Mina.

Baada ya muda akamwangalia. “Nilikwambia kuwa nakupenda, si ndiyo?” Mina akabaki akimwangalia. “Unakumbuka?” “Uliniambia kabla sijakwambia historia yangu! Au kabla hujanifahamu!” Mina akajibu taratibu. Andy akaenda kupiga magoti mbele yake. “Nilitaka kukubusu wakati ule, ukasema nisubiri kwanza mpaka unieleze wewe ni nani. Umenieleza na umeniambia, umeniambia ukweli. Si ndiyo?” Mina akatingisha kichwa kukubali.

“Naomba nisikie sauti yako Mina!” Akamvuta mikono yake yote akaishika vizuri akibembeleza. “Sijadanganya na hakuna nilichokuficha Andy.” “Sawa. Naomba tujipe muda wa pamoja. Sio tukiwa mbali, halafu tuone itakwendaje.” Mina akanyamaza.

“Umenielewa lakini?” “Hapana Andy! Ndio inakuaje?” “Tuwe pamoja, wakati wewe ukinifahamu mimi na kuangalia kama nafaa kuwa mume wako, na mimi hivyo hivyo. Itakapofika wakati tukaona ni sawa tunaweza kuishi pamoja, tufanye taratibu, tufunge ndoa. Unafikiri ni wazo zuri.” Mina akabaki amemkodolea macho kama hamuamini! Anawezaje!? Hata Mina akashindwa kumuelewa.

 “Lakini haitakuwa yakujificha. Mama ameshaingiwa na hofu kwa maisha uliyoishi nyuma, pamoja na Ron. Halafu Ron yupo chini yangu, sitataka kuharibu mahusiano yangu na Ron. Ni mtu ninayemtegemea sana pale kazini.” “Utafanyaje Andy na yeye anajua unaye Lora? Ron hawezi kukubali.” Hofu ikamuingia.

“Nitazungumza naye, nimweleze ukweli na nia yangu. Unafikiri ataelewa?” Ikawa kama kengele tena. Andy anafanya kweli, anaendelea! Akaona kama mambo yanakwenda kwa kasi sana. “Mina?” “Sijui Andy! Sijui! Au labda tusubiri kwanza.” “Tunasubiri nini?” Andy akauliza akijua ameingiwa hofu. Mara Mina akasimama ghafla kama aliyekumbuka kitu. Akamuacha Andy amepiga magoti pale.

“Ni nini tena?!” “Sijui Andy, kama nimeingiwa na hofu ya mahusiano! Unajua Omar aliniambia ananijua na ananipenda kama nilivyo! Akasema atanichukua, atanipenda, halafu akaishia kunipiga kila wakati! Akawa haniamini tena.” Andy akasimama.

“Mina!” “Hapana Andy. Hii historia inajirudia. Naomba pata muda wakufikiria zaidi. Unampendaje mtu mwenye historia ngumu kama yangu!? Hapana Andy! Mimi nimepita hapo unapotaka tupite sasahivi. Sio rahisi Andy. Nilimuona Omar. Alikuwa kama amechanganyikiwa! Haniamini na yeyote, kwa chochote. Kila wakati alikuwa akiota anaibiwa. Hapana.” Mina akajirudisha nyuma kabisa. Andy alikuwa amemsogelea. Akampisha pembeni, akarudi pale alipokuwa ameacha pochi yake. Akaichukua.

“Mimi sio Omar, Mina!” “Basi naomba tujipe muda. Tafadhali pata muda wakufikiria bila mimi nyuma yako au bila kuona unawajibika kunijulia hali au la. Tafadhali Andy. Jipe muda wakutafakari mbali na hisia.” Mina akataka kuondoka.

“Subiri kwanza Mina!” Mina akageuka. “Nimeelewa. Nitafanya hivyo. Na wewe naomba unipe muda.” Mina akawa hajaelewa. “Njoo.” Akasogea, Andy akamshika tena mikono yote miwili.

“Unamaanisha nini?” “Wewe umesema nipate muda nifikirie kabla yakuchukua hatua nyingine. Si ndivyo?” “Mimi ndivyo ninavyofikiria.” “Wazo zuri. Lakini naomba na wewe unisubiri mimi. Namaanisha mimi tu, usije kumfungulia mtu mwingine mlango kabla hujahitimisha na mimi.” Andy akajiweka sawa.

“Hapa leo tumeweka msingi. Naomba tusidharau mwanzo wetu. Mimi kwangu nahesabu umeniamini na kuniheshimu kwa kunieleza ukweli wote. Sichukulii kuwa ni maongezi tu. Na imeniongezea kukuamini.” “Kweli Andy!?” “Kabisa Mina. Ungeweza kufunika mambo hayo ya nyuma, ukaja kwangu na Mina huyu. Na mbona tungeendelea tu! Lakini kwa kuniambia ukweli bila kunificha, naona tunaanza msingi mzuri.” Kidogo Mina akatulia.

“Nachukua muda kama ulivyonishauri, na wewe naomba unisubiri mimi.” “Sitakubali mwanaume mwingine Andy. Kwanza hata sikuwa na mpango huo.” “Nashukuru. Naomba tujipe muda. Wewe hunifahamu kabisa. Pata muda na wewe wakunisoma ili ujue utakuwa ukiishi na mtu wa namna gani.” Mina akatingisha kichwa kukubali. Akamuona Andy anavuta pumzi kama aliyepata aghueni.

“Bado unataka kuondoka?” “Ndiyo. Naomba nikupe muda.” Andy akacheka. “Mimi naelewa ninachozungumzia Andy. Pata muda wakufikiria.” “Sawa. Lakini naomba nikusogeze mpaka karibu na nyumbani.” Mina akacheka. “Nitashukuru.”  Akachukua funguo za gari, akavaa viatu, wakatoka wakiwa wametulia kila mtu akiwaza lake. Njiani Mina alitulia kimya, Andy naye kimya. Wakaendesha mpaka Tegeta karibu na njia ya kwendea kwao.

“Naomba nikuchukulie usafiri wa kukufikisha nyumbani.” Mina akacheka kama anayefikiria. “Ron anapikipiki anaifanyia biashara. Huwa tukifika hapa, tunamuita huyo kijana, anakuja kutuchukua na kutufikisha nyumbani.” Akamuona anatoa walet na kumtolea pesa. “Basi hii itakusaidia kulipia.” Akamkabidhi.

Nimefurahi umeitikia wito na kuniahidi kunipa muda.” Mina akajua ndio anamkumbushia. “Nitakusubiria Andy. Nakuahidi sitafanya chochote bila kukwambia.” “Na ninaomba Mungu chochote kisitokee.” Mina akacheka taratibu kama ambaye na yeye anafikiria.

“Si hakuna chochote kitakachotokea?” “Ndiyo Andy. Nitakusubiria wewe.” “Hapo sawa.” Wakacheka kidogo, wakabaki wametulia pale ndani ya gari kwa muda. Ila ile hali ya utulivu pale, kila mtu aliipenda. Wakajisahau. Mwishoe Mina akacheka na kumuaga. “Asante Andy.” “Karibu.” Akashuka garini.

~~~~~~~~~~~~~~

Alirudi nyumbani akamkuta mama yake yupo jikoni. “Nimerudi mama.” Mama yake akageuka. “Mbona umejawa cheko?” “Nimefurahi.” “Haya, niambie kila kitu.” Mina akaanza kujiuliza aseme nini na nini aache! “Tumepeana muda, mama. Nimemwambia apate muda wakufikiria. Tuchunguzane, ndipo tutajua baada ya hapo.” Mama yake akageuka vizuri.

“Safari hii nikijana wakueleweka, mama. Anajiheshimu na ananiheshimu. Anathamini maisha yangu na anachukua mambo kwa heshima.” Akamuona mama yake yupo kimya. Akaumia sana.

“Anaonekana ananipenda mama! Na si kwamba anataka kunichezea. Anaonekana anataka kunioa.” Mina akazidi kuumia baada ya kuona vile mama yake anavyomwangalia. “Nimebadilika mama. Safari hii nafanya tofauti na ndio maana sikufichi kitu. Naomba nipe nafasi nyingine.” Mina aliendelea kumbembeleza mama yake.

“Mina mwanangu, hakuna mwanaume aliyekamilika, akakuona wewe, asikutamani. Hilo nalirudia tokea upo shuleni.” Mama yake akaanza.

“Umetoka hapa hata miezi mitatu haijaisha, tayari mtu anasema anakupenda na anataka kukuoa! Mtu huyo wa kukwambia leo anataka kukuoa wakati hakufahamu, anatokea wapi kama sio anataka kuyagusa anayoyaona kwa nje! Utajifunza lini Mina, mwanangu wewe?” Mina akazidi kuumia.

“Unataka nini kitokee kwenye maisha yako ili ujifunze!? Unakumbuka lililokupata kwa Omar?” Mina akashindwa hata kumjibu. “Unataka tena?” “Safari hii ni tofauti mama!” “Tofauti yake ni nini? Niambie.” “Kwa kuwa nitakuwa na wewe katika kila hatua. Sitakuficha chochote katika kila hatua ili unishauri.” Hapo akamfunga mdomo mama yake. Akanyamaza na kugeuka akaendelea na alichokuwa akifanya, Mina akaondoka.

Kwa Kina Andy.

          Siku ya jumapili baada ya kutoka kanisani wakiwa wanakula vikiwa vimejaa vicheko, mama yake akaanza kumuulizia Lora. Hasira ikapanda ndani ya Andy, akaweka kisu na uma chini kwa nguvu. Kila mtu akamgeukia. “Naomba niweke hili sawa.” Akaanza Andy. “Nilichukua ushauri wako mama. Na wengine ambao mnaotaka Lora awe mke wangu. Nikajaribu mahusiano lakini imeshindikana.” “Umeanza lini na umeshindwa lini?”  Akauliza mama yake. “Tafadhali naomba nimalize mama. Kwa kuwa unataka Lora awe mke wangu mimi, si ndivyo?” “Ndiyo lakini pia ujue mahusiano sio rahisi hivyo. Kuna kuvumilia, na watu wanatofautiana na...” “Mama!” Andy akamuita.

“Mimi naona umuache amalizie mama.” Akashauri dada yake. “Thank you.” Akashukuru Andy. “Narudia tena. Nilichukua hatua kama ulivyotamani mama, niwe na Mina.” Akashituka, akaangalia kila mtu. “Mina ni nani?” “Nilitaka kusema Lora. Mimi na Lora, imeshindikana. Na haitawezekana. Kama unataka awe mkwe wako, Paul huyo hapo. Muunganishe na Paul.” “Haa! Hapana!” Paul akakataa kabisa.

“Kwa nini unakataa sasa?” “Ninaye mpenzi wangu. Halafu Lora mkubwa kwangu na anajidai anajua kila kitu.”  Paul akaropoka. “Haaa! Kwa hiyo wewe ulitaka mimi ndio nimuoe!?” “Mama ndiye anayetaka umuoe. Mimi ushanisikia nikisema umuoe Lora? Hata mara moja. Kwa kuwa namjua Lora vizuri sana.” Paul akajitetea.

“Ana nini na wewe? Kama sio kutaka kumkatisha tamaa mwenzio?” “Kila mtu atajionea mwenyewe. Lakini mimi sina mpango na Lora. Ila ujue tu, Lora anadharau. Na ndio maana unamuona mpaka leo na uzuri wake ule, hana hata boyfriend.” Akaongeza Paul.

“Si watu wanamuogopa sababu ya elimu na kazi yake?” “Kwani wasomi wangapi hapa duniani wameolewa? Kwani Lora ndio amesoma peke yake?” Akauliza Paul. “Hata mimi nimesoma jamani, msinisahau.” Akaongeza Paulina. “Haya! Mfano ulio hai huo hapo. Kama hata Andy ameshindwa, basi ujue wazi Lora sio muolewaji yule.” “Kwa nini na wewe?” Mama yake akauliza tena kwa hasira.

“Utanichukia bure mama yangu. Ila ujue mimi na Lora ni kama tumekuwa pamoja tu. Japokuwa amenipita mwaka mmoja, kumbuka nimesoma naye darasa moja. Na tumekuwa naye karibu hapa mjini. Mimi ananidharau kwa kuwa udaktari wangu nimesomea Tanzania.” Andy akashituka na kumwangalia.

“Unajishuku tu.” Mama yao akatetea. “Najishuku nini wakati nina kazi na nina tibu watu!? Lakini si kwa Lora. Aliniambia hata akiwa kwenye hali ya kufa, nisimguse. Sina hadhi yakumtibu kwa kuwa nilisomea udaktari wangu chini ya mwembe.” Pakazuka ukimya. “Sasa mimi nikajua kwa kuwa Andy mwenzangu amesomea nje ya Tanzania ambako Lora anapaita chini ya mwembe, labda mwenzangu atakubaliwa! Lakini Andy huyo naye amenyanyua mikono.” “Kila mtu anamadhaifu yake. Inatakiwa mjifunze kuishi na watu.” Mama yake akaongeza akizidi kutetea. Kila mtu akainamia sahani yake. Hakuna aliyetaka kujibu tena.

“Kwanza Mina ni nani?” Baada ya muda mama yake akauliza kama aliyekumbuka. Kimya. Andy akaendelea kula. “Wewe Andy?” Andy akavuta pumzi kwa nguvu nakuweka chini kila kitu, uma na kisu. Wote wakamgeukia. “Mina ni msichana ambaye tumepeana muda wa kuchunguzana ili tuone kama tunaweza kuwa kwenye mahusiano.” Kimya. Akainama na kuchukua vitu vyake. Kisu na uma, akaanza kula tena. “Sasa kama kulikuwa na Mina, uliwezaje kumchunguza Lora nakufikia mwafaka kuwa hafai?” “Mama, mimi sio mtoto mdogo.” “Mapenzi huwa hayana mtu mzima. Na unaweza kufanya maamuzi mabaya sababu ya hisia tu.” Andy akamgeukia shemeji yake.

“Mbona unaniangalia kama unanilaumu!? Sijaongea chochote na yeyote. Kwa hiyo kama kuna mwingine ulimwambia, ujue ndiye aliyesema.” “Unaongea nini na wewe?” Paulina akamuuliza mumewe aliyejishuku. “Sitaki Andy afikiri mimi ndiye nimemwambia mama juu ya Mina.” Andy akaishiwa nguvu kabisa, wote wakamgeukia mume wa Paulina, Devi.

“Kwa hiyo wewe unamfahamu Mina?”  Akauliza Paulina, mkewe. “Kwa hiyo nyinyi mpo hapa, mnatusanifu tu tunavyomuongelea Lora, kumbe mna Mina nyuma ya pazia?” Akauliza mama yao kwa ukali. “Mimi Mina simfahamu jamani. Na wala sina habari naye.” Akajihami Devi. “Wewe leo utayaongea yote!” Mkewe akamtisha. Andy kimya. “Wewe Andy?” Mama yake akamuita kwa ukali. Andy akamwangalia. “Mina ni nani?” “Narudia tena, Mina ni binti ambaye tupo kwenye kufahamiana. Nitakapokuwa na chakusema zaidi, nitawajulisha.”

 “Kwa hiyo umeona umjulishe shemeji yako, sisi..” “Nyinyi msubiri mpaka nitakapokuwa na chakuwaambia.” Akamalizia Andy huku akimtizama shemeji yake. “Sijasema kitu.” Akanong’ona shemeji yake. “Leo utayasema yote. Wala usihangaike hapo.” Paulina akamwambia mumewe.

“Wasiwasi wangu ni kuwa, huyu Mina sijui, ndiye aliyekufanya ushindwe kupata muda wakutosha na Lora.” Akaanza tena mama yake. “Jamani, tutaonana tena jumapili ijayo.” Andy akasimama na sahani yake. “Unanidharau mimi wewe Andy?”  Andy akasimama. “Labda nizungumze na mimi kidogo, kama nitakuwa nimemuelewa Andy na wewe mama.” Akaanza mzee Ruhinda. Andy akageuka. Na wengine wote wakatulia kumsikiliza.

“Kama nilisikiliza vizuri tokea mwanzo kabisa, na kukuelewa mama, ulitaka Andy ampe nafasi Lora. Amchunguze, aone kama wataweza kuja kuona. Au sikuwa nimeelewa?” Akamuuliza mkewe kwa tahadhari sana.

“Ndiyo. Maana Lora ni mwanamke wakuendana na Andy na hii familia. Ataleta mwanamke gani humu ndani atakayefanana na Lora?” Andy akashangaa sana. “Subiri kwanza Andy. Mimi ndiye ninayezungumza.” Mzee Ruhinda, baba aliyesoma na kuongoza wazee wasomi mjini akataka aweke sawa hilo swala.

“Sasa kama nimemuelewa sawasawa na Andy, ndio amerudisha majibu baada yakuchukua hatua ya kile ulichomshauri. Kuwa, Lora hatamfaa yeye kama mkewe.” “Asante baba.” “Ruhinda!” “Subirini kwanza niongee mimi, ni zamu yangu.” Ruhinda akamkatisha mkewe na Andy.

“Inavyoonekana Lora anaweza akafaa sana kuwa mtoto mzuri wa humu ndani. Akawa rafiki wa kila mtu. Maana nimeona na Paulina amemfurahia sana Lora. Lakini kwa kuwa Pius ameshaoa. Na ninaona ndoa yake imetulia. Hana mpango wa kumuacha mkewe, Lora hawezi kuwa mkwe humu ndani kwa kuwa waliobaki hawa wawili, Andy na Paul, wote wawili, wameshindwa kuwa na Lora.” “Hiyo ni dharau unayoifanya kwangu Ruhinda. Tena mbele ya watoto!”  Akaanza mama Ruhinda.

“Jamani! Mimi naeleza wanachosema wanao. Nasaidia kukuelewesha tu!” “Mimi unaniona ni mjinga sana, sielewi?” Ugomvi akatupiwa baba yao.

“Hujawahi kuyaheshimu wawazo yangu na hutakaa kuniheshimu mimi kama mkeo na mama wa watoto wako, utafikiri hawa watoto umewaokota barabarani!” Akabadilika mama Ruhinda. “Naomba uniambie nilipokosea! Au kwenye tatizo ni wapi hapa!? Maana naona unataka kwenda kinyume na wewe mwenyewe. Sikumbuki ulipomwambia Andy kuwa nilazima amuoe Lora! Nakumbuka ushawishi tu! Na yeye amekurudishia majibu kwa wazi kabisa. Sasa kwa nini unakasirika mama, na muoaji ni Andy?” Akajieleza Ruhinda taratibu tu.

“Wewe hushauriki kama watoto wako. Unanidharau kwa kila kitu ndio maana unashindwa hata kufikiria. Wewe umesikia kuna Mina sijui! Sasa huyo Lora alifikiriwa saa ngapi mpaka akaonekana hafai, Mina ndiye anayefaaa?” “Habari za Mina, huna mke wangu. Andy ameomba umpe muda, kukiwa na chakusema, atasema. Sasa kwa nini unawasiwasi wa Mina, ambaye hata hujajua kama na yeye ataolewa? Kwa nini unatengeneza hali ya wasiwasi wakat...” “Mimi kama mama ndiye ninayejua kinachomfaa mtoto wangu.” Mama Ruhinda hakutaka kushindwa.

“Ninaposema Lora anafaa ni katika kila kitu. Huyu Andy aliyesoma shule za mapadri atapata wapi mwanamke mzuri kama Lora!? Unakumbuka yule mwanamke aliyemletaga hapa wakati ule yupo chuoni? Haeleweki kama ni mwanaume au mwanamke! Sauti ipo kama imekauka!” “Lakini si ndiye aliyekuwa amemchagua mwenyewe?” Akauliza Ruhinda.

“Kwa kuwa wewe umekusudia kwenye maisha yako uwe kinyume na mimi, hata jambo la msingi hutaona. Unanidharau na kunipinga hata kwa jambo ambalo ni la msingi kabisa.” “Labda mama ungetulia kwanza na kumpa nafas...” “Unamtetea baba yako kwa kila kitu!” Paulina na yeye akageuziwa kibao.

“Nilitaka kusema huyo Mina, mama. Sio baba. Unaweza kukuta unamkataa mtu mzuri kwa Andy bila kumfahamu.” “Naona tuache mambo ya Mina kwanza ili hapa ndani apite Lora. Sitaki mpenzi wangu aje hapa, muanze kumlinganisha na Lora.” Kila mtu akamgeukia Andy.

“Unaona sasa!? Wewe Ruhinda uliyekuwa ukitetea ujinga? Huyo Mina ameshakuwa ni mpenzi!” “Ninachotaka kusema mama, Lora na Mina ni watu wawili tofauti. Na kwangu Lora sio kipimo cha mke, ila ni kipimo chako wewe. Kama alivyosema baba, yeyote nitakayemchagua, ni wangu mimi. Nataka mke atakayenifanya mimi niwe na furaha, sio yeyote yule humu ndani. Anaweza akakosa vigezo kwenu, lakini akawa anavigezo vyote vya kuishi na mimi. Nataka niliweke hilo wazi na wote mliheshimu.” “Mimi naliona hilo ndilo la msingi.” Akaongeza baba yao.

“Ruhinda unatafuta matatizo wewe leo!” “Nimefanya nini mimi!? Au ni mimi mwenyewe ndiye niliyekuwa nikimsikiliza Andy? Naona eti ni kama ameongea jambo la msingi sana! Au wewe Pius unasemaje? Maana naona wewe huwa ukiongea mama yako huwa anakusikiliza na kukuelewa bila shida.” Pius akanyamaza. “Huo ni unafiki Pius. Unajua nipo sahihi ndio maana unashindwa kuongea ili usimuudhi mama.” Andy akakasirika kabisa.

          “Mimi nashauri Mina apewe nafasi. Akaribishwe nyumbani kama Lora tu na..” “Subiri kwanza Paulina. Simleti Mina hapa ili mumpitishe. Au mumchunguze. Naomba niliweke hilo wazi kwenu nyinyi wote. Mimi ndiye muoji.” “Kabisa.” Akaongeza baba yao. “Asante baba. Na mimi ndiye nina vigezo vya mwanamke nitakayeishi naye. Nyinyi wote hapa hamna vigezo vya mwanamke ninayetaka kumuoa.” “Pana ukweli hapo japo ni mchungu!” Akaongeza Paul. Mama yao akanyanyuka kwa hasira na kuondoka.

Kwa kina Mina.

Mina aliendelea na shuguli zake kama kawaida bila hata kuzungumza na mama yake tena. Akawa ametulia, mpole hata ule utani ukaisha. Siku ya jumapili kama kawaida, Ron aliita taksii hapo nyumbani, wote wakaenda kwenye kanisa wanaloabudu kila jumapili. Usharika wa Mbezi. Mina alikuwa ametulia kweli kumbe mawazo kwa Andy akijutia kumpa muda wa kumfikiria.

Usiku wakati wamelala na mama yake, akaanza. “Nina wasiwasi mama!” Mama yake akamgeukia. “Nini?” “Hajanitafuta tena! Unafikiri nitakuwa nimemtisha?” Mama yake akamuhurumia.

“Kwa nini ufikiri ulimtisha?” “Ni mtu wa maana mama! Na anaonekana nia ni kunioa kweli. Aliniambia alinipenda mara tu aliponiona. Nikaogopa yale ya Omar yasije kujirudia. Akawa ananipenda kwa muonekano tu. Lakini mama, alikuwa na msichana wake mzuri huyo! Tena msomi, mimi mwenyewe nawajua. Walikuwa wakipendezana.” Mina akaendelea.

“Sasa anasema tokea aliponiona mimi akanipenda. Na alivyojisikia kwangu sio kama kwa yule dada, ikabidi amwambie ukweli kuwa anampenda mtu mwingine. Wameachana. Sasa nilipoona amefika umbali huo zaidi ya muonekano, ikabidi niwe mkweli kwake. Nikamwambia asimuache msichana wake kwa ajili yangu. Nikapaniki mama, ikabidi nimwelezee historia yangu yote.” Mama yake akakaa haraka kwa mshituko.

“Mina!” “Ningefanyaje mama? Huyo msichana aliyekuwa naye ni mzuri mno. Halafu nilisikia ana kazi nzuri sana. Nikaogopa tusije tukaanzana, akaja kunijua, akaanza kunichukia kwa kumuacha mwanamke kama huyo kwa ajili yangu. Sitaki tena mambo ya nusu nusu mama! Nishacheza vyakutosha. Sasa hivi nataka nikiwa na mtu, nitulie moja kwa moja.” “Umemwambia kila kitu!?” “Kila kitu mama, sijabakisha.”  Mama yake akabaki ametoa macho.

 “Nisingemwambia?” “Nafikiri ungesubiri kidogo, Mina, mwanangu! Angalau afahamu huo moyo wako, ndipo umwambie kidogo kidogo. Tena sio yote! Mengine ungeyaacha tu yabakie nyuma. Kwa wakati mmoja! Utakuwa umemtisha sana.” Yaani mpaka mama yake aliishiwa nguvu.

Akahisi labda hajaelewa vizuri. “Unauhakika ni yoooote!” “Jamani mama!” “Nauliza tu Mina, mwanangu mzuri. Yote kama yalivyo au ulitafuta hekima kidogo?” “Sasa hekima gani?” “Labda kuacha vijipande vingine.” “Kama vipi?” Akamuuliza mama yake.

“Labda kama mahusiano waliyokuwa nayo Mozee, Afidhi na Omar.” “Ningesemaje?” “Ungemwacha Afidhi, ukapunguza. Ukamtaja tu Omar na Mozee!” Mina akanyamaza. “Kwani na yale ya shuleni ulimwambia? Utakuwa hujamwambia. Si eti Mina, mama?” “Nilimwambia mama.” Mama yake akatoa macho.

“Ni vibaya sana?” “Uuuu! Mina, mwanangu wewe ni muwazi sana! Wenzako vingine wanamezea!” “Sasa akija kusikia kwa wengine?” “Angalau anakuwa ameshakujua mwanangu! Mbali na mambo mengine, wewe ni mtu mzuri Mina! Unaweza kuishi na watu ukiamua. Una upendo, huna majibishano na mtu!” “Nimetoa na zile tabia chafu mama. Leo sijafanya kitu chochote na yeye.” Mama yake akacheka.

“Najua umebadilika. Nakuombea Mina! Nakuombea sana mwanangu. Sitaki watu wakuchezee.” Mina akatulia. “Wakikuona tu hivyo, wanataka kukugusa.” “Sasa hivi nimebadilika mama.” “Basi, kuwa mvumilivu. Kama ni wako, atarudi. Kama sio wako, Mungu atakuletea wakufanana na wewe.” Hilo likamfanya Mina kutulia.

~~~~~~~~~~~~~~

Inaendelea….


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment