Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 10. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 10.

Ron alirudi kwao akiwa amechelewa. “Umenitia wasiwasi bwana! Kwa nini hukuniambia kama utachelewa?” “Nilikuwa na kikao na kiongozi wangu, sikujua kama kitachukua muda mrefu.” Mama yake akaingiwa na wasiwasi. “Kwema!?” “Kwema. Umekula?” Akamuuliza mama yake huku akikaa. “Hivi unajua sasa hivi ni saa nne? Tushakula muda mrefu sana.” “Mina yuko wapi?” “Amelala ndani. Kuna nini tena!?” Ron akatulia kidogo kama anayefikiria.

“Ameshaharibu nini tena huko kazini kwako? Maana nilikuonya Ron! Usimfikishe kazini kwako, atakuharibia lakini hukutaka kunis..” “Mama! Mama! Hajafanya kitu kibaya bwana! Nimekwambia ametulia. Kwanza huwezi amini.” Ron akacheka kidogo nakutingisha kichwa.

Akaangalia mlango wa chumbani kwa mama yake, ambako analala na Mina. “Nini?!” “Huwezi amini leo amekwenda IFM kwenda kuulizia chuo.” “Huyo Mina?!” Mama yake akashangaa sana. “Mimi mwenyewe sikuamini.” “Labda mwanangu kakua jamani! Mungu wangu mkubwa!” Mama yake akaangalia juu kabisa kama anayemshukuru mungu.

“Lakini kuna jingine.” Akapunguza kabisa sauti. “Wewe umemjua aliyemfuata siku ya jumamosi?” “Amekataa kabisa kunitajia jina. Lakini si unamjua Mina alivyo msiri kwenye hayo mambo yake? Mpaka yamuharibikie ndio atarudi analia hapa, na majina atataja. Lakini si kabla.” Mama yake aliongea kwa sauti ya chini, ya kunong’ona na yeye kama Ron.

“Wewe umemjua?” “Unamkumbuka yule bosi wangu alikuja hapa kunichukua tukaenda kuangalia mpira?” “Subiri kwanza Ron. Yule kijana!?” “Anaitwa Andrew Ruhinda, ila watu wamezoea kumuita Andy.” Mama yake akabaki ameduaa. “Ndiye aliyenichelewesha. Anaonekana ana nia na Mina, mama. Hivi ameomba kuja kukuona ili ajitambulishe kwako rasmi.” Mama yake akabaki bado ametoa macho.

“Mama?” “Umesema ndiye aliyekuwa naye jumamosi?” Mama yao akataka uhakika kwanza. Maana alimjua binti yake. “Amesema alianza naye hospitalini.” “Basi kweli ameamua. Ujue Mina alikuwa anawasiwasi hatamtafuta tena, kwa kuwa alimwambia ukweli wote juu yake!” “Ameniambia!”

“Mimi mpaka nikamlaumu Mina. Nikamwambia ameharakisha sana.” “Mimi huwa sielewi mama. Sijui ni bahati Mungu amemjalia Mina au sijui! Hivi unajua amemuacha mwanamke mzuri tu sababu ya Mina!?” “Ameniambia Mina! Nahisi ni bahati. Maana mimi nilijua wanachanganywa na huo muonekano wake wa nje, lakini kama na wewe unasema huyo mwanamke alikuwa mzuri, basi ni bahati.” “Mzuri sana tu ila yeye anaonekana wa kileo zaidi na amesoma si kama Mina!” Wakabaki kimya kwa muda.

“Sasa unasemaje?” Mama yake akavunja ukimya. “Kuhusu nini?” “Kumkaribisha huyo kijana hapa nyumbani! Mimi binafsi sidhani kama ni sawa Ron.” “Kwa nini?” “Wewe unamjua Mina. Akiharibu huko si atakuharibia na wewe?” Mama yao akasita. “Mina anaonekana amebadilika mama. Hata pale kazini nimesikia walikuwa wakimtongoza anakataa. Naomba tumpe nafasi nyingine. Tena uzuri safari hii analeta mwanaume nyumbani! Huoni kama itakuwa nafuu? Itakusaidia au itatusaidia kujua kinachoendelea kwenye maisha yake na kumshauri.” “Mmmh!” Mama yake akaguna.

“Lakini ameonyesha mabadiliko makubwa kwa kweli. Ametulia na shule.” “Hilo ndilo linanipa moyo mama. Pengine amekuwa sasa.” “Labda.” Wakanyamaza kwa muda. “Amesema anakuja jumapili hii asubuhi, halafu twende naye kanisani na kurudi hapa nyumbani.” Mama yake akacheka kama aliyeridhika.

“Anaonekana amempenda Mina! Mungu amsaidie mwanangu jamani. Atulie na huyu.” “Hilo ndilo la msingi. Maana amesema yeye hajali ya nyuma, labda kuanzia hapa. Kwa maana nyingine inategemea na Mina mwenyewe. Ameniomba nimuache Mina awe huru, hata akija kazini, aingie ofisini kwake, nisimkataze.” “Kwamba anataka hata kazini wamtambue?” “Ndivyo alivyosema. Hana chakuficha kwa yeyote. Anasema anamtaka Mina amfahamu bila kificho.”

“Mmmh! Labda hatimaye Mungu amenisikia jamani! Nilimlilia Mungu na huyu mtoto! Mchana na usiku bila kuchoka.” “Nakumbuka mama. Mara tuambiwe alishachukuliwa nafsi yake ndio maana hasikii!” Wakaanza kucheka. Wakazungumza wakikumbushana shida walizopata na Mina mpaka kufika hapo, kila mtu akaenda kulala.

Mina alikuwa amelala, hana habari. Mama yake akamwangalia. Kisha akamfunika vizuri, na yeye akajilaza pembeni yake asiamini na usiku huo yupo hapo.

Kipendacho Roho.

Jumapili asubuhi ya saa tatu kamili Andy alikuwa akiegesha gari mbele ya nyumba ya kina Mina. Mama yake akamwangalia Mina wakiwa chumbani. Akamuona anacheka na kuchungulia dirishani. “Amefika mama!” Mama yake akacheka. “Nenda sasa kampokee.” Mina akatoka mbio.

“Karibu.” Wakamsikia ameshafika nje. “Naamini nimefika muda sahihi.” “Mama anamalizia kujiandaa, anatoka sasa hivi. Umependeza Andy!” Andy akacheka. “Na unanukia vizuri.” “Njoo kwenye gari nikupe zawadi yako.” Akamvuta mkono.

“Umeniletea nini?” “Pafyumu. Nimekuona unapenda harufu nzuri.” Akacheka. Akafungua mlango akamtolea kimkoba. “Angalia kama utapenda.” “Asante.” Mina akaanza kuifungua kuitoa kwenye boksi. “Nzuri hata kwa kuitizama kwa macho! Chupa nzuri. Inaonekana imekugharimu sana!” Akasifia. “Pulizia uone kama utapenda harufu.” Akajipuliza. Akaipenda. “Asante. Nimependa. Naenda kumpulizia na mama. Twende.” Na yeye akamshika mkono wakawa wanangia ndani.

“Mama! Andy amekuja.” Ron akatoka akamsalimia Andy kwa kumshika mkono. Mina akaingia chumbani kwa mama yake akamwacha Andy na Ron. “Ameniletea pafyumu.” “Naipata hiyo harufu.” “Jipulize na wewe mama yangu, unukie.” “Siku nyingine bwana! Ameleta leo tu, halafu aone wote tunanukia kama tulikuwa na...” Mina akampulizia mama yake kila mahali. “Mina!” “Na wewe unukie mama yangu.” Wakaanza kucheka.

Baada ya muda wakatoka chumbani. “Karibu Andy mwanangu.” Andy akasimama kusalimia. “Asante mama. Nashukuru kwa kunikaribisha.” Akampa mkono na kumsalimia. “Na mimi nimeshukuru kwa hiyo heshima yakutaka kufika nyumbani. Karibu.” Wakakaa. “Najua ibada inaanza saa nne na nusu. Lakini niliomba kuwahi kidogo ili nizungumze na wewe pamoja na Ron kabla hatujaenda kanisani.” “Karibu.” Mama yao akakaa vizuri.

Andy akaanza kusugua mikono kama anayetafuta pakuanzia. Mina alikuwa amekaa tu pembeni ametulia. “Labda niseme tu kwa kifupi, ili nisikuchoshe kwa habari ndefu mama yangu.” “Hata kidogo. Labda kama unataka tukutayarishie kifungua kinywa ule wakati unaongea.” “Asante mama yangu. Lakini nilimwambia Mina msisumbuke na kifungua kinywa kwa leo. Huwa nina mtindo wa kuamka mapema sana. Nikishafanya mazoezi nakuwa na njaa, siwezi kuvumilia. Inabidi nile tu. Kwa hiyo hapa nilishapata kifungua kinywa, labda nyinyi. Naweza kusubiri.” “Hapa hakuna mfanya mazoezi baba. Lakini tunakula mapemaa.” Wote wakacheka.

“Hapa tulishakula, tunasubiri cha mchana tu. Wewe endelea.” “Asante.” Andy akatulia tena kidogo kama mwenye hofu. Pakazuka ukimya. “Labda niseme, au labda nianzie tulivyokubaliana na na..”  Akasita na kucheka kwa hofu. Wote walikuwa kimya wakimtizama mpaka akawa anashindwa kuzungumza. “Sikujua kama itakuwa ngumu hivi!” Andy akaongea huku akisugua mikono na kucheka kama kujituliza. Wote wakacheka na kunyamaza tena.

“Labda nianzie mwanzo, lakini nitafupisha ili nisiwachoshe.” Akaanza tena. “Mara ya kwanza kumuona Mina hapa nyumbani, nilivutiwa naye sana. Nikadhani ni hisia tu. Nikajaribu kujituliza kwa hili na lile. Wakati huo tayari kulikuwa na shindikizo la Lora, kutoka kwa wazazi. Nikajaribu kupuuza juu ya Mina, nikaona nifanye hatua ya mbele zaidi kwa Lora, ili angalau kumtoa Mina mawazoni. Ron na Mina wanamfahamu Lora. Ni binti aliyekuzwa kwenye mazingira yanayofanana na kwetu, hata wazazi wetu walifikiri ndiye angekuwa mke sahihi kwangu.”

“Lakini kila nilipokuwa nikijitahidi kwa Lora, haikuwa kama ninavyojisikia kwa Mina. Nikaona sijitendei haki mimi mwenyewe na Lora pia. Ikabidi kumwambia Lora kabla hatujafika mbali. Sikudanganya, japo alikasirika sana. Nilimwambia kuna mtu nampenda sana. Na ninahofia kwa kadiri ninavyopoteza muda, naweza kumpoteza. Kufupisha stori, baada yakuona Lora ameshatoka kwenye picha, ndipo nikamwambia Mina. Baada ya mazungumzo ya muda mrefu na Mina, akihofia kudanganywa, tukakubaliana tupeane muda wakuchunguzana ili tuje kufikia muafaka. Yeye achunguze kama mimi nitakuja kumfaa kama mume, na yeye kama mke. Hatukupeana muda, ila nilimwambia atakapoona yupo tayari aniambie na mimi hivyo hivyo.”

“Tumekubaliana kwa kipindi hicho kusiwe na mtu katikati yetu. Ni mimi na yeye tu, mpaka tuone hatutafaana. Tutaambizana, na ndipo kila mtu ataendelea na maisha yake. Sasa kwa makubaliano hayo ndipo nikaomba angalau na mimi mnitambue kama nipo na Mina. Sina kificho kokote na kwa yeyote. Na nia yangu ni kutaka kuoa. Nampenda Mina. Na naomba Mungu atusaidie, kusitokee chochote chakututenganisha. Tuweze kurekebisha tofauti zetu ili tuweze kuwa pamoja. Ni hivyo tu mama yangu.” Andy aliongea kwa heshima.

“Labda niulize Andy.” “Karibu mama.” Mama yao akakaa vizuri. “Kama nimekusikia vizuri, Lora alikuwa chaguo la wazazi. Umesema mnaendana. Kwa haraka haraka, wewe umetuona sisi. Maisha yetu. Unamfahamu Mina kwa kiasi. Najua wazi ipo tofauti kubwa sana kielimu na kiuchumi. Hata maadili, nikikuangalia, unaonekana umekuzwa kwa namna yakisomi.” Mama Ron akaendelea.

“Swali la kwanza, wazazi wako wanajua juu ya muafaka wako na Lora? Swali la pili, wanajua juu ya Mina? Namaanisha wanajua vizuri juu ya Mina?” Mama Ron akauliza vizuri.

“Nilipomalizana na Lora, niliwaambia. Huwa tunakutana kwa chakula cha mchana kila siku ya jumapili baada ya misa, nyumbani kwa wazazi, Msasani. Jumatano nilihitimisha na Lora, jumamosi tukakubaliana na Mina, jumapili nilipofika nyumbani nikawaambia hitimisho langu na Lora. Na makubaliano yangu na Mina, japo sikuwa nimekwenda kwa undani kama hivi nilivyojieleza kwako. Lakini Mina atakapokuwa tayari, nitampeleka kumtambulisha.” Pakazuka ukimya.

Andy akawaangalia kwa zamu. Akamsogelea Mina na kumshika mkono. “Labda niseme hivi, kama nilivyowaambia wazazi wangu.” Wote wakamwangalia. “Mimi ndiye muoji. Najua ninataka mke wa namna gani. Mimi ndiye nitakayeishi na mke wangu mpaka kifo. Nafikiri nina haki zote zakuchagua mke mwenye vigezo vyangu mimi. Hata kama kwa wengine itakuwa ngumu, lakini mimi muoaji niwe nimeridhika naye.” Andy akaendelea.

“Sikuwa na wanawake wengi kabla. Nilisoma shule ya bweni ya mapadri. Ila nilipata msichana wakati nipo chuoni. Nikaja kuwa na Lora, niko na Mina. Nimesoma saikolojia. Nina uwezo wakumsoma mtu na kumuelewa hata kama anazungumza kingine, nina uwezo wa kuujua ukweli.”

“Kwa uwazi alionao Mina. Vile alivyoniamini na kujifungua kwangu bila kunificha chochote!  Vile ninavyojisikia nikiwa na Mina, ndivyo ninavyotaka iwe hivyo kwa maisha yangu yote. Najua mnaweza kusema ni mapema sana kusema hivyo, lakini Mina ana vigezo vingi vya mwanamke ninayemtaka kwenye maisha yangu. Nampenda Mina.” Andy akawa kama amemaliza. Ron akamgeukia mama yao.

Akajua ndio anasikilizwa yeye. “Mimi binafsi nirudie tena kukushukuru kwa heshima uliyompa Mina. Asante. Na ninaahidi kuwaombea. Ili iwe kama Mungu alivyokusudia. Hivi unavyotuona hapa ndio familia imekamilika. Tunaishi sisi tu. Unakaribishwa muda na wakati wowote ule.” Andy akaachia mkono wa Mina akasimama. Akamsogelea mama yao akampa mkono. “Asante mama yangu. Nashukuru sana. Angalau itaturahisishia mimi na Mina.” “Nitawaombea.” Mama Ron akaongeza.

~~~~~~~~~~~~~~

Kijana huyo aliyekuzwa na malezi ya kipadri, kwa mara ya kwanza mapenzi yakamfikisha kanisa ya Kiluteri. Hapakuwa na maji mlangoni ya kuweka ishara ya msalaba kama alivyozoea na kupiga magoti. Akawa mpole akifuatisha anachofanya Mina mpaka mwisho.

Baada ya ibada, akasahau yupo na familia hiyo inayoendeshwa na mwalimu wa shule ya sekondari. Aliyepambana kufikisha wanae hapo walipo. Hapakuwa na muda wakuwafundisha kula kwa kisu na uma, ila kuhakikisha chakula kipo mezani, kila wakati. Basi.

Akawapeleka kwenye hoteli inayolingana na kina Ruhinda. Yenye napkins za vitambaa safi vyeupe, kwenye meza zilizopagwa vizuri visu, umma na vijiko. Tena vijiko vya size tofauti tofauti. Kwa supu, chakula na dessert kama wangechagua dessert ya kutumia kijiko. Wakabaki wakiangaliana.

~~~~~~~~~~~~~~

Mama Ron mwenyewe alihamia Dar kikazi. Alizaliwa kijijini, akakulia kijijini. Akaja mjini akiwa binti tu. Maisha yakachanganya na ubusy. Waliomzunguka na mwanaume aliyempata walikuwa watu wa kawaida sana. Kula kwa mkono, suna! Hapakuwa na maswala ya kula na kisu pamoja na uma. Kwenye sherehe alizokuwa akihudhuria yeye ni kula pilau kwa mkono, wakijitahidi ukumbini basi kijiko. Leo wameketishwa kwenye visu na uma! Wakabaki hawajui chakufanya na hivyo vifaa hapo mezani.

~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka muhudumu anamaliza kutaja aina ya vinywaji walivyo navyo, wote wamechanganyikiwa. Wakaishia kuagiza soda aina ya Sprite. Nazo hizo soda zikaletwa na glasi za namna yeke na ice cubes/barafu kwenye birauli za aina yake.

Kila mmoja alipokabidhiwa menu ya vyakula, ikawa msala mwingine. Hakuna kati yao aliyeelewa hata kimoja wapo. Kila kitu kimeandikwa kwa lugha ya kigeni. Andy alishachagua chakula chake, akaendeleza mazungumzo akiwa ametulia anasubiri muhudumu arudi amwambie anachotaka.

“Andy!” Mina akaita kwa upole, Andy akamgeukia. “Mimi mwenzio sielewi hapa. Sioni hata wali na maharage!” Andy alicheka sana. “Mina!” “Kweli bwana! Hata chips hamna!” Mina akalalamika huku akiendelea kusoma. “Naona Mina na mimi hatutofautiani baba.” Akaongeza mama Ron. “Nimesoma mpaka nimechanganyikiwa. Huku huwa hatuji baba!” Akaongea mama Ron kinyenyekevu lakini wakacheka.

“Labda niulize, mnataka kula nini? Naweza kumuita muhudumu akaja, mkamwambia mnachotaka kula.” “Kwani wewe unataka kuagiza nini? Nionyeshe hapo kwenye menu.” Andy akamfungulia Menu yake akamuonyesha.

“Namba 17.” Mina akaanza kusoma. Akamwangalia usoni. Andy akaanza kucheka. “Sasa ndio nini hivi!?” “Nimetaka tu kiazi kikubwa kimoja kilichookwa, watakiweka cheese, watamwagia vipande vidogo vya beacons, nitaomba na sour cream juu yake. Wataleta na mchanganyiko wa mboga mboga, ni aina ya kama kachumbari lakini yenyewe ni kama inasukari sio chumvi, inaitwa slow, na kipande cha nyama ya ng’ombe ya kuchoma, lakini upande wa mguu. Nitaomba medium rare, kwamba nyama wasiikaushe sana.” Wote wakabaki wametoa macho.

“Kumbe ndio maana hatuelewi! Vyote hivyo!” Andy akazidi kucheka. “Mavyakula mengi hivyo!” “Wewe unataka kula nini?” “Chips kuku.” Mina akajibu haraka sana. “Hivyo tu!?” Akauliza Andy kama anayeona anajipunja. “Kwani huwa wanakula na nini?” Andy akazidi kucheka. “Hutaki hata starter?” Mina akabaki ametoa macho. “Naona mimi niwe kama Mina tu. Hizo starter tuache.” Wakazidi kucheka. Ukaanza utani, mpaka chakula kikaja.

“Lakini hata mimi sifahamu vitu vyote. Wakati mwingine unawaita, wanakuelekeza.” Wakamuona yeye Andy anatumia kisu na uma. Anakula bila shida. Wakapoa. Hapakuwa na kunawishwa mikono. “Twende mama.” Mina akamtoa mama yake pale.

“Kuzaa kuna kuona mengi!” Walipofika chooni wakaanza kucheka. “Sasa pale tutakulaje?” “Ndio maana nimekuleta huku unawe, twende ukale kwa kutumia mkono mama yangu.” “Aibu gani hii!” Wakazidi kucheka.

Walirudi mezani Ron alikuwa akila kwa mkono hana hata habari. Kuku, chips vilikwenda mdomoni kwa kutumia mkono bila shida.  Wala wazo la pili halikuwepo kutoka kwa Ron. Walikula wakizungumza ndipo akawarudisha nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati huku ya Mina yakimuendea sawa, jumapili ya Pam ilikuwa ikimuendea kombo. Mpaka siku hiyo hakuwa amesikia chochote kutoka kwa Mill. Akakata tamaa akijua kama Jerry hajasahau kumpa, basi Mill hakuitaka. “Hata hivyo hakuniomba. Sijui kwa nini nimejidhalilisha kwa kiasi hiki!” Akaanza kujilaunu akiwa amekata tamaa.

~~~~~~~~~~~~~~

Usiku wakati akilala, akiwahi sababu ya kazi siku inayofuata, ujumbe kwa WhatsApp ukaingia. ‘Nashukuru kwa namba Pam wangu. Ila nilipewa bila masharti. Sasa sijui mida hiini ni mibaya?’ Nusura aruke. Akajibu kwa haraka. ‘Ni sawa tu. Hakuna masharti.’ Akamuona amesoma na kujibu hapohapo. ‘Kwamba hata nikitaka kuisikia sauti yako sasahivi ni ruksa?’ Pam akacheka na kujibu. ‘Hakuna masharti.’ Akamjibu, ‘Nashukuru’. Kisha akaona anampigia.

“Mzima Pam?” “Mimi mzima lakini nilikuwa na wasiwasi na wewe! Uliondoka umeloa na ulikuwa na safari ndefu! Hujaugua?” “Nashukuru kujali. Lakini huwa nina mtindo wa kusafiri na nguo za ziada. Nilibadilisha kwenye ndege. Nilikuwa sawa tu. Niambie hali yako.” “Naendelea vizuri.” “Kama ingekuwa vibaya, ungeniambia?” Akamsikia akicheka taratibu.

“Eti Pam?” “Naendelea vizuri.” “Vizuri hii ni ya wote. Sasa nipe yangu ya peke yangu. Ya ukweli.” “Nipo sawa Mill. Asante kunijali mimi kama Pam.” Mill akacheka kama anayefikiria. “Ni nini?” “Hata nikikwambia sasahivi, haitaleta maana. Ushazoea kusikia ukiambiwa na wengi. Nina uhakika unaambiwa kila siku.” “Wengi wananidanganya.” Ikawa kama analalamika.

 “Katika hao wengi na mimi unahisi nitakuwa mmoja wao?” “Sijui Mill! Mimi sikufahamu.” “Ila kwa muda mfupi niliokuwa na wewe, umeshaniweka kwenye kundi lao?” “Nisinge kupa mawasiliano yangu.” Hapo akaridhika.

“Nashukuru kama unaniamini, na nakuahidi sitakudanganya. Sawa?” “Nakusikiliza.” “Basi naomba vitendo ndio viongee. Ila jua nimefurahi sana kukusikia.” “Kwa nini sasa wakati hata hunijui?” “Naomba ulitunze hilo swali nitakuja kukujibu endapo Mungu atajalia kuonana. Ila jua nimefurahi kukusia. SANA. Na nimefurahi kupata namba yako.” “Ila hiyo namba niliomba upewe tokea jana!” Akajua alikuwa akisubiria simu yake tokea hiyo jana.

“Pole.” “Sio kwamba nalaumu!” Mill akacheka. “Silaumu bwana!” “Hamna shida, ila na mimi nimepewa sasahivi, na kukupigia. Nisingeweza subiri. Muda mwingi simu ya Jerry inakuwa mikononi kwa Sandra. Mawasiliano yeyote yanayokuhusu wewe inabidi kutumia barua pepe, tena ya zamani sana, enzi ya tokea tupo shuleni na Jerry, ambayo Sandra haifahamu. Kwa hiyo hata utumaji wake lazima uwe nje ya alipo Sandra.”

“Kwa jinsi alivyonieleza Jerry ilimbidi aage kwenda kunyoa nywele na huko ndiko alitafuta Café akanitumia email yenye namba yako. Anasema alikuwa na Sandra tokea jana, asingeweza ku risk. Umeelewa sasa?” “Mimi nilijua hujataka au na wewe Sandra wako huko amekubana.” Mill alicheka sana.

“Usicheke bwana!” “Huku hakuna Pam mwingine! Upo peke yako.” “Mmmh!” “Kwamba huamini?” “Mimi sijui bwana! Sasa kwa nini?” “Kwani wewe hujamsikia Lona? Mie choka mbaya.” Alishituka Pam! Maana ndio maneno aliyokuwa akiyasema ofisini, akimkashifu Mill. Akajua Jerry amemwambia.

“Eti Pam? Maana hata wewe sikujua kama utanitafuta tena.” “Amepatwa wivu tu. Hamaanishi. Mimi namfahamu Lona na nishamzoea. Tafadhali asikuumize.” Akamsikia akicheka. Kisha akaongeza.

“Hata kidogo. Na mimi nilimuelewa. Ila sababu ya kutokuwa na Pam mwingine huku au huko ni utapeli mwingi. Ukiacha mwanamke huko nyumbani jua utakuwa na kazi ya kumtunza ila wanafaidi wengine. Huku nako hakuna mapenzi ya kweli kama hivyo Mike na Kamila. Usanii mwingi. Na mimi sasahivi sina muda. Nina malengo ambayo nataka yatimie mapema.”

“Bado nasoma. Nilimaliza shahada ya pili huku, nikagundua kuna kitu kingine nikisoma kinaweza nisaidia zaidi. Shahada ya pili nilisoma bila kufikiria. Nilitaka tu niwe huku. Lakini sasahivi nina malengo. Nasomea ujuzi. Na baba ndiye anayenisaidia kwa asilimia 60. Hiyo iliyobaki lazima nipambane mwenyewe.”

“Kwa hiyo nina shule ngumu na nina kazi ninayofanya usiku na wakati mwingine nikipata nafasi naomba kufanya kazi masaa ya mchana. Nipo busy mno. Kwa hiyo sina muda wa Pam mwingine. Pam wangu mmoja tu.” Pam akacheka sana.

“Piga simu muda wowote utakao ila jua kuna muda naweza shindwa kupokea. Zaidi ninapokuwa na mgonjwa au mtu namuhudumia. Nitakutumia ratiba yangu vizuri ili uwe unajua nilipo na ninachofanya wakati wote. Sio ratiba ngumu maana haibadiliki. Na najitahidi isibadilike angalau kwa muhula mzima wa shule ili isiathiri shule yangu. Umeelewa?” Akawa ameibua swali kwa Pam.

“Kwamba wewe ni daktari huko?” “Hapana. Nipo nafanya kazi kwenye nyumba ya wazee huku nikisomea unesi.” Pam akashangaa sana. “Nina shahada ya uongozi, inayoendana na mambo ya uhasibu. Nikafanya ya pili hukuhuku nikazama kwenye mambo ya uhasibu zaidi lakini naona pesa yake haiwezi nitunzia Pam wangu na watoto wetu.” Pam hakuamini.

“Hiki ninachofanya usiku, nina malengo nacho. Naiba ujuzi. Ila sasa, ukifungua sehemu kama hii kwa kiwango hikihili, lazima uwe na RN, ambaye lazima utamlipa mshahara mkubwa. Sasa kwa nini mimi mwenyewe nisiwe huyo Registered Nurse na mmiliki?” “Unaakili!” Akacheka.

“Itanisaidia kusimamia biashara yangu kwa urahisi. Nitaajiri watu wenye elimu ya chini yangu ambao nitawalipa pesa ya kawaida. Na pia itanisaidia kupata kibali cha kuanzisha kampuni yangu kwa haraka. Sasa malengo kama hayo hayahitaji watu kama kina Lona wa huku. Sitatulia.” Pam alicheka sana.

“Wewe unamsema Lona wakati hunijui mimi!” “Sasahivi nakufahamu kwa asilimia kubwa sana Pam. Nyingine najua tutaendelea kufahamiana taratibu. Ila kwa nilipo, na ninapokwenda, najua wewe ndio utaniwezea. Au utapawezea.” “Sijui Mill. Wewe upo mbali, mimi nipo huku! Ndio inakuaje?” “Naandaa mazingira Pam wangu. Tutakuwa pamoja tu. Usiwe na wasiwasi. Nipe muda mama. Na usinikatie tamaa. Hilo ndilo ombi langu kwako. Umenielewa?” “Nakuelewa Mill.”

“Ewaaah! Mipango inaweza sikika mizuri, lakini kufikia inaweza kutugarimu mno. Hapa nilipo penyewe si rahisi. Lakini nimejiwekea malengo ambayo hayawezi timia bila mimi mwenyewe kuyasimamia. Ndio maana unaona na wewe nimekushirikisha mapema. Ujue mwisho tokea mwanzo, unisaidie kutembea. Ilitufikie mwisho mzuri.” Akazidi kumgusa Pam.

“Sitaki tuishie kuwa ombaomba. Au watoto wetu wahangaike. Nataka uzee wetu uwe wa heshima, sio wakudharauliwa hata watoto wanaogopa kuwasiliana na sisi wanaogopa tutaomba pesa! Hapana.” Pam akacheka ila furaha!

~~~~~~~~~~~~~~

Hajawahi pata mwanaume anayemuonyesha mwisho mzuri hivyo mpaka uzee! Wote aliokwisha kutana nao, mwisho wao ni kitandani wakishamvua nguo. Leo Mill anazungumzia mpaka watoto! Mipango yao ya pamoja mpaka uzeeni! Wala hakuhitaji kutongoza. Mke alishajipatia. Hapo anamuuzia sera za maisha yao wala si yake huko ugaibuni! Akaupata moyo wa Pam kwa asilimia ZOTE.

~~~~~~~~~~~~~~

“Uko Pam?” “Nipo.” “Basi nisikuchoshe. Nikuache upumzike.” “Hunichoshi. Ila sema najua na wewe unahitaji kupumzika. Tutazungumza wakati mwingine.” “Unaendaje kazini?” “Nawahi daladala. Asubuhi si shida nikiwahi kutoka nyumbani. Jioni ndio kuna sumbua kidogo. Lakini nimeshazoea.” Mill akafikiria kidogo.

“Ningemtuma dereva wa Mike akuletee gari yangu. Maana inakaa tu pale kwake. Lakini najua Sandra anaifahamu. Anaipenda sana. Ameniambia anakusanya pesa nimletee kama hiyo.” Pam akapigwa na butwaa.

“Au hapatakuwa na shida?” “Mmmh! Usijisumbue. Mimi nitakuwa sawa tu.” “Wewe kupata usafiri ni muhimu kwangu wala si usumbufu. Usalama wako ni muhimu sana Pam. Hiyo gari inakaa tu hapo mpaka mimi nirudi nchini. Haina matumizi. Ingekufaa.” “Siwezi kuendesha gari nzuri zaidi ya Sandra. Huwa hapendi kupitwa na yeyeote pale kati yetu. Tunamchukulia kwa tahadhari sana. Aje aone naendesha gari anayoitamani na hana uwezo nayo! Italeta shida sana. Halafu mimi mwenyewe naishi kwa watu. Wakiniona na gari ya thamani hivyo!”

“Sikujua kama unaishi kwa watu!” “Sio kwa watu baki. Ni kaka yake mama. Mjomba na familia yake. Alitusaidia mimi na kaka. Kaka alipooa akaondoka, ndio nimebaki mimi na binti zake. Napo nahisi muda wangu wa kukaa hapo umeshaisha, natakiwa kuondoka ila navuta tu.” “Kwa nini hutafuti kwako?” Akanyamaza.

“Pam?” “Nina majukumu mengi. Kaka kabla hajaoa ndiye aliyekuwa akimsaidia mama. Sasahivi ameoa, mkewe hataki kabisa. Anasema hawawezi kusaidia tena mtu. Na wao wanajijenga. Na ubaya au uzuri, kaka alimuoa yeye akiwa amejenga. Kwa hiyo ni kama kaka amehamia kwake, hana usemi sana. Yeye ndio anaongoza mambo ya familia.”

“Kwa hiyo kila pesa ninayopata najibana kumsaidia na mama anayetunzwa huko kwa bibi na babu.” Kidogo akaibua maswali kwa Mill. “Naona nikianza kupanga, hapa mjini ambapo maisha ni magumu, nitamaliza kidogo ninachoingiza hapo ninapofanya kazi kwa Sandra na Jerry! Na ndio imekuwa kisingizio changu wakati wote kwa shangazi anapotaka nihame, nipishe chumba kwa binti zake.”

“Sasa nikianza kuonekana na gari hapa kwa shangazi, itazua maswali. Atalalamika akisema nakataa kuhama kwake ili nijitajirishe wakati naendelea kuwabana hapa. Zaidi binti zake ninao tumia nao chumba. Sijui kama unanielewa?” “Nahisi nimekuelewa kwa sehemu. Pole.” Akamsikia akicheka.

“Sio mbaya kwa kiasi hicho. Nipo sawa ila na mimi nina malengo yangu. Sitaki kutoka hapa kwa shangazi kwa haraka kabla sijajiandaa vizuri. Nitakuwa sawa tu juu ya usafiri. Usiwe na wasiwasi.” “Basi jua nina wasiwasi. Acha nifikirie nijue chakufanya. Ila nina swali juu ya mama.” Akamsikia amenyamaza.

 Pam aliona historia yake ni ya aibu asije kudharaulika na Mill ambaye ni mgeni kwake. Au asije akaiga na kumfanyia na yeye. Akaamua ayafiche moyoni na kumshangaza Mill. Mill asijue ni makubwa na mapana yaliyomfanya Pam kuchukia wanaume na kuwaona kama  nyoka. Aliwachukia wanaume kupita kiasi yaani huyo Mill alimgusa kwa tofauti ndio sababu aliweza hata kuzungumza naye.

~~~~~~~~~~~~~~

Ipi nayo historia ya Pam?

Inaendelea…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment