![]() |
Alipopata simu
za wadogo zake wakimtaka arudi nchini, akaamua kurudi kuja kuona linaloendelea.
Pam alimpokea uwanja wa ndege, moja kwa moja akampeleka nyumbani kwa baba yake.
Hakutaka hata kukaa, alichofanya Mill ni kumbeba na kumkimbiza hospitalini.
Kwani alikuta kuanzia miguuni mpaka magotini amebadilika rangi kama
ambaye damu imeacha kutembea chini. Mguu umeoza, na tumbo limeanza kujaa.
Akalipia chumba cha binafsi ili baba yake
alazwe hapo. Hakutoka huko hospitalini, mchana na usiku, alikuwa na baba yake.
Kamila na Mike wakipeleka vyakula. Na Pam kwenda kushinda naye huko kuanzia
asubuhi mpaka usiku akiwa amechukua likozo kama siku zote alivyomzoesha Mill. Akirudi
nchini wanajifungia, fungate. Ila safari hii ikawa wanashinda wote
hospitalini wakiuguza. Baada ya siku nne mbeleni, mzee akafariki.
~~~~~~~~~~~~~~
Aliporudi kwao
baada ya mwili wa baba yake kupelekwa chumba cha maiti, ambako marafiki zake
wote, majirani na ndugu walikuwa wakikusanyika hapo kwa msiba wa mzee Mgini,
akakuta hali ya fujo isiyo eleweka. Vijana wanataka mali ya mzee,
lakini wakijua mzee aliacha maagizo yote kwa Mill, ambaye ndiye mtoto
mkubwa. Yeye ndio agawe mali.
“Naombeni tumzike
baba kwanza.” Mill akawatuliza. Wakafanya taratibu za mazishi, mama Kenny akiwa
na wasiwasi sana, akijua wanae yeye wapo mwishoni kuzaliwa kwa
baba yao. Watapunjwa na kaka zao. Mbali na hiyo nyumba, na maduka ya vifaa vya magari
ambako hakutaka kabisa mama Kenny ajihusishe nako, hakujua mzazi
mwenzie ana mali gani nyingine maana aliishi naye kama hawara tu hata
ndoa hakutaka kufunga na kila wakati alimruhusu kuondoka atakaposhindwa.
~~~~~~~~~~~~~~
Yaani wametoka tu makaburini, na Pam alikuwepo, wakakuta wote wamekusanyika
sebuleni, wanamsubiria yeye. “Kwamba nyinyi hamuwezi kusubiri
hata kesho?!” “Tuweke tu sawa, bro ili tujue moja. Maana kuna fununu
zinasikika kuwa mama Kenny anataka tuondoke, huku Kenny mwenyewe anasema
hapa ni kwao wao kwa sababu mama yao ndio amekuwa mwanamke wa mwisho
kuwa na baba.” “Mzee alisema maagizo YOTE, wewe unayo. Akifa tu, tukusubiri
wewe, utupe hatima yetu.” Mill alichoka kabisa.
“Mill, acha sisi
tuwaache mmalizane kifamilia.” Mike akamuaga. “Nawashukuru aisee! Asante sana.
Nitawaona baada ya muda mfupi.” Ndugu zake wote wakashangaa.
“Sisi tulijua wewe ndio sasahivi utahamia hapa kama kiongozi! Nani sasa
atasimamia mali za baba?!” “Maana hapa hakuna mtu atamsikiliza mtu
mwingine ila wewe tu.” “Watu watatoana roho hapa bro, kama ukiondoka.”
Mill akawatizama na kumgeukia Mike.
“Acha niwatoe.”
“Hamna sababu. Au ulitaka tuondoke na Pam?” “Hapana. Huyu namtaka hapahapa nilipo.
Ndio mambo ya familia haya. Lazima awepo.” Mike na Kamila wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~
“Naombeni
mnisikilize kwa makini kwa sababu sitajirudia tena na tena. Na msiniingilie
ninapo zungumza. Subirieni mpaka mwisho ndipo muulize maswali.” Wote
kimya. Na mama Kenny na wanae pia walikuwepo.
“Najua baba
hakuwa amemuoa mama Kenny. Lakini kisheria, mama Kenny ndiye
MKEWE anayetambuliwa. Kwa sababu wameishi chini ya dari moja zaidi ya
miaka miwili. Na ndiye aliyekuwa na baba mpaka kifo.” Kidogo mama Kenny
akapumua kwa nguvu. Kama aliyepata aghueni.
“Ila ni kwa manyanyaso
sana bro, ndio maana sisi tulikupigia simu uje.” Mmoja wao akaongea kwa
jazba. “Alihama na chumba kabisa, msichana wake mwenyewe wa kazi anasema
alikuwa akimnyanyasa sana mzee, anasema ananuka.” “Yaani msichana
wa kazi ndiye aliyekuwa akimuhudumia baba kwa karibu, kuliko yeye,
mama Kenny. Baba alipozidiwa zaidi, hawezi hata kutoka kitandani, akaanza
ukorofi. Hataki kupikwe kama zamani, na akawa anafungia vyakula mpaka
aliposikia wewe unakuja, upo njiani ndio akajidai mwema. Muulize, abishe.
Tena yeye na mwanae Sheila.” “Unafiki tu kwa kaka Mill ili atuone sisi wabaya, atuchukie.
Kwani wewe kilichokuwa kikikushinda kuwa na baba usiku ni nini?”
“Haaah!” Wote wakahamaki kwa pamoja.
“Sio mama yenu
huyo alitusemea kwa baba kwamba hataki kutuona nyumba kubwa,
hatuna ustarabu labda iwe kufuata chakula tu? Tukaona isiwe shida,
tukaacha kuingia humu ndani labda mpaka tuitwe na baba au chakula!”
Mwingine akadakia. “Tena hata chakula chenyewe mlibadili utaratibu. Mlimwambia
msichana wa kazi awe anatuwekea kule nje jikoni kama mbwa vile! Ilimradi
tu, tusiingie ndani. Hatukulalamika. Mkaishia nyinyi wawili na mama yenu
kuishi humo ndani? Sasa tungerudi vipi wakati nyinyi na mama yenu
mlikuwa hamtutaki?” Wakaanza kubishana, Mill kimya.
“Acha tukwambie
ukweli bro.” Mill akamtizama huyo mmoja wa wadogo zake. “Yaliyokuwa yakiendelea
humo ndani sisi tulikuwa tukiambiwa na msichana wa kazi mpaka ikabidi tukutafute.
Hawa watatu, WALIMSUSA baba. Sheila ndio hakuwa akitaka kurudi kabisa nyumbani,
hataki kujihusisha kabisa na baba mpaka aliposikia umerudi nchini,
umemchukua baba na kumkimbiza hospitalini, ndio akaja hospitalini akijidai
alibanwa na shule kumbe alikuwa akikimbia hapa nyumbani. Nasikia alikuwa
akisema nyumba inanuka donda la baba.” “Muongo, Kenton.
Wananisingizia kaka Mill.” Sheila akaanza kulia.
Wote wakamdaka
kumchangia kwamba anajiliza mbele ya Mill ila ni kweli. “Na Kenny ndio
nasikia alikuwa hataki hata kuingia chumbani kwa baba. Wote hawa wakawa wanamlazimisha
msichana wa kazi kwenda ndani kwake, mpaka yule msichana wa kazi akaja kutoroka.
Huyo dada unayemuona hapo hana hata siku tano! Mgeni.” “Na wote tunahisi kilichomuua
baba kwa haraka ni NJAA.” Wakaanza kushambuliana kwa maneno. Hawamalizi.
“Twende Pam.
Tutarudi wakishamaliza.” Akamshika Pam mkono. Akasimama. Ikaanza kazi ya kumsihi
Mill abaki wao wananyamaza. “Sijalala tokea nimefika hapa nchini,
na muda wote nilipokuwa nikimuuguza baba hospitalini. Na huko nilikokuwepo
sikuwa mapumzikoni. Nilikuwa shuleni na ninafanya kazi. Akili na mwili vyote
vimechoka. Sitaki kelele.” “Tunanyamaza.” Wote wakajibu kwa pamoja.
~~~~~~~~~~~~~~
“Mirathi
aliyoacha baba kwangu, ipo na nitaituma kwenye kundi la familia.
Mpaka mwisho nazungumza naye, hakunipa maagizo mengine ya tofauti ya
mirathi kwamba anataka kubadilisha. Nilikuwa na baba mpaka dakika ya mwisho.
Japokuwa alikuwa na hali mbaya, lakini alikuwa na akili zake timamu.
Siku moja kabla ya kifo chake tulizungumza mengi, mpaka tukadhani
amepata nafuu, anapona. Muulizeni Pam. Alizungumza sana na Pam kama
ambaye hakuwa mgonjwa. Lakini hakugusia kabisa juu ya kubadili
mirathi ya kwanza.” Mill akaendelea wote wakisikiliza kwa makini.
“Sasa iwe alinyanyaswa
na mama Kenny au la, alikuwa mkewe na HAKUBADILI alichoniambia mwanzo, na mimi
NAFUATA kauli ya baba bila kufuatisha HISIA zetu.” Kimya
wakisikiliza kwa makini sana.
“Nyumba hii
tuliyopo sasahivi hapa, alinikabidhi na hati yake pia, alisema HAPA, nimkabidhi
yeye na watoto wake.” Hawakuamini.
“Nakuhakikishia
hayo si matakwa ya baba ya mwisho, bro.” “Hata kama. Mimi
nasimamia tulichozungumza naye siku ya kwanza nimekuja kumtambulisha Pam
kwa baba, akaniomba kikao. Na mama Kenny pamoja na Pam walikuwepo akinitaka
tukutane naye siku inayofuata. Baba alikuwa ameshaandika mirathi yake,
akaomba nimsaidie kuisimamia. Nilichomuomba mimi ni kunitoa
kwenye mirathi yake.” Wote hawakuamini.
“Kwamba wewe
bro, hutaki kitu kabisa!?” “Mimi nimeshachukua urithi wangu kwa
baba. Na yeye nilimwambia kabisa, sihitaji kitu tena kutoka kwake. Mzee
amenisomesha nje ya nchi kwa garama kubwa sana, bila kulalamika. Shule
sijaimaliza, lakini palipobakia namuamini Mungu atasaidia.” Wote kimya.
“Sasa basi. Kwa
kuwa undugu wenu na mama Kenny ulikuwa ukishikiliwa na baba, na
kwa sasa hayupo, baba ametaka kujengwe ukuta hapo, kutenganisha nyumba
ya mama Kenny pamoja na wanae, na hizo nyumba tatu za nje ambazo amesema
zitabakia kwenu kama alivyowagawa yeye mwenyewe.”
“Hamtatumia geti
moja na mama Kenny. Anataka yeye geti lake liangalie kwa ule upande mwingine,
nyinyi mbakiwe na geti hilo la sasa. Eneo la Goba, alinipa mimi
lakini litabaki la familia. Atakayetaka kuliendeleza, si kuuza,
anitafute akiwa na mipango inayoeleweka, nitamkatia sehemu yake.” Kimya.
“Maduka yake
yote matatu ya vifaa vya magari, alishauri myaendeleze ibakie kuwa ajira
yenu nyinyi, bila Kenny wala Sheila, kwa kuwa mlikataa shule.” Wote
kimya.
“Mnanielewa
Sheila, Kenny na mama Kenny?” “Kwamba wanangu hawana kitu kwenye yale maduka!?”
Akauliza kwa kulalamika. Wadogo zake wakataka kuanza kumchangia, Mill
akawakatisha.
“Nisikilize mama
Kenny. Narudia kufanya kile baba alichoniagiza. Kenny na Sheila kama
wakikazana, wanauhakika wakumaliza chuo na kupata ajira ya kuwaingizia kipato.”
“Wasipopata?” Akauliza tena mama Kenny. “Itakuwa bahati mbaya.” Mill akamjibu
bila wasiwasi na kuongeza swali kwa ukali kidogo.
“Hivi unajua
katika watoto wa baba wote, ni watoto wako tu ndio wamebahatika kupata
eneo au nyumba kubwa kuliko wote?” “Afadhali umelitambua hilo
bro! Tunashukuru.”
“Tafadhali kuwa muungwana
mama Kenny. Wengine wote wanabakia kwenye nyumba ndogo, wakijibana. Watoto wako
ni wawili tu, umebakishiwa jumba lote hili lenye vyumba kibao na wamesomeshwa!
Ulitaka baba afanye nini zaidi?!” “Naomba tusikosane Mill. Yalikuwa ni maswali
tu. Nimekuelewa na kukushukuru kusimamia haki. Maana ungeweza nipunja
na wala nisijue. Mungu akubariki.” Akajirudi kwa haraka. Mill akamtizama na
kuendelea.
“Swala la maduka
naomba niweke msisitizo nikimalizia wosia wa baba. Ameshauri myaendeleze
iwe ajira yenu nyinyi wote mkigawana majukumu kwa kuelewana mkisimamiwa na
Kenton ambaye baba amesema anaufahamu wa yale maduka, anajua mambo mengi kwa
kuwa alikuwa akifanya kazi chini yake kwa muda mrefu.” “Sio kwa kukukata
bro, au kukupinga. Lakini wote tunajua Kenton ni cha pombe
na hajiwezi kwa swala la wanawake. Akinywea pombe na kuhonga
pesa yote ya mtaji.” Hapo wote wakachangia Kenton akibisha.
“Msijidai watakatifu
mbele ya bro. Nani asiyekunywa kati yenu, na nani mwenye mwanamke mmoja
kama bro! Baba mwenyewe alisema ni yeye peke yake kwenye ukoo mzima,
amevunja rekodi. Mbona asiwataje nyinyi?” Kenton akawajia juu ila wote wakamkataa.
“Hapana bro!
Katika hilo tunaomba utusaidie. SIO Kenton.” “Ndipo ninapotaka kumalizia
wosia wa baba. Sio kwamba yeye ndio atasimamia peke yake, ila awasadie
kuwapa muongozi. Lakini baba alisema, mkishindwa, mniambie,
tuuze, mgawane pesa. Ndipo ninapokuja ushauri wangu mimi.”
“Jamani kuna uhalisia
wa maisha mbele yenu. Wakuwalipia umeme na maji hayupo. Hizo nyumba hapo
ni nzuri kama zilivyo kwa sababu baba alikuwa akizikarabati mara kwa
mara. Naungana na baba. Biashara hizo, mjitahidi kwa kila namna, mziendeleze.
Wekeni wawakilishi watatu kutoka kila nyumba, wawe karibu na Kenton, na muwe
mna vikao kila mwezi, kupeana muendelezo. Kila mmoja wenu awe na uhuru
wa kujua pesa inatumikaje. Na kusitolewe pesa benki bila makubaliano
yenu WOTE. Kuwe na zaidi ya watu watatu wa kuweka saini benki ili kutoa
pesa.”
“Hapo sawa bro.
Ila ikitokea kuna kuzidiwa, utarudi kutusaidia kuuza na kugawana?”
“Ndiyo. Lakini bado nasisitiza. Kuuza na kugawana pesa iwe jambo
la mwisho kabisa. Mimi nawajua nyinyi. Haitachukua muda mrefu, pesa
mtakayogawana yote itaishia kwa wanawake.” “Tutabadilika.
Sasahivi tunakua.” “Basi endelezeni yale maduka. Kuliko kuuza, ni bora mkishindwana
nyinyi wote, basi mgawane kwa nyumba. Kila nyumba iendeleze duka lake na
kujipanua zaidi. Sio mkipata faida mnahonga! Panueni biashara, ndio
urithi wenu wa MWISHO. Na wengi wenu mna mama zenu. Kueni kiakili, mtunze
na mama zenu. Swali kabla sijaondoka?”
Mama Kenny
akaonyoosha mkono. “Kuna pesa za mafao na salio benki. Hizo
zinakuaje?” “Samahanini nilisahau. Pesa ya benki na mafao yake yote, aliniambia
ameacha utaratibu nikachukue. Hapatakuwa na usiri. Nikishajua
salio zima. Nitaweka kwenye kundi la familia. Tutajenga ukuta kutenganisha
hizi nyumba. Zitakazo baki, baba ameomba niwagawie sawasawa.” “Hata
mimi?!” Mama Kenny akashangaa sana.
“Kwamba wewe
umefanyaje kwa mfano?!” Mmoja wao akauliza. “Mimi nilikuwa mke wa marehemu
jamani! Kwamba mafao yake nilitakiwa nipewe mimi.” Wakaanza kumcheka.
“Naombeni mnisikilize jamani! Baba amekufa hana furaha na maisha mnayoishi
nyinyi.” Akawaonyeshea wadogo zake.
“Amesema kwa
wazi kabisa. Maduka aliyowaachia, na mkipata hiyo pesa, acheni kuitumia
kwenye pombe na wanawake. Ndio msaada wenu wa mwisho kutoka kwake.
Ameomba MJIENDELEZE. Na naomba kuwakumbusha tena. Kuanzia kesho,
hizi nyumba zinatengwa ramsi. Japokuwa hapatakuwa na uzio, lakini umeme
na maji kila nyumba itajitegemea.”
“Hakuna
wakuwatunza tena kama watoto wadogo. Na mkumbuke inachukua muda kwa taratibu
zote kukamilika kupata mafao ya baba. Anzeni kuchangamka. Kwahiyo
mama Kenny, mafao ya mzee mtagawana na vijana wake.” Akaonekana
kutoridhika.
“Twende Pam.”
Wakasimama. “Nikitaka nianze ujenzi wa huo ukuta hata kesho?” “Tunza risiti,
pesa ikitoka nitakurudishia.” “Ndio mwanzo wa kutengeneza risiti za uongo.
Bro, hapo HAPANA. Sisi tunamjua mama Kenny.” Wakaanza kubishana. Mill
akawa kama anayefikiria.
“Mimi nikitafuta
fundi aanze huo ujenzi, nikaomba Kenny na watatu wenu kutoka kila nyumba
msimamie, itakuwa sawa?” Ukaanza ubishi mwingine tena. Hata hao wanne hawaaminiani.
Ila zaidi hawamtaki Kenny. Kenny akasema ni wivu tu. Wakabishana
hapo. Mill akahitimisha. “Mimi nitasimamia huo ujenzi wa ukuta. Mnashida
katika hilo?” “Labda mama Kenny na wanae. Sisi hatuna shida. Baba alishatuambia
maagizo yote atakuachia wewe na utaendeleza hii familia. Sisi
hatuna shida na wewe.” Wengine wote wakakubali kasoro mama Kenny na wanae
wakanyamaza.
“Jamani, usiku
mwema.” Akataka kuondoka akawa kama amekumbuka. “Kabla sijaondoka hapa, nataka
kujua kama kati yenu nyinyi kuna aliyeacha kitu humu ndani kwa mama Kenny.
Maana kuanzia leo, mtaingia humu ndani kwa kukaribishwa na mama
Kenny na wanae. Kama una kitu chako, chukua, mtoke hapa kabla sijaondoka.”
“Kwamba tunaanza
leoleo?!” “Chakula?!” Mwingine akauliza kwa kuhamaki. “Nyinyi si mmetaka
kugawana leo kila mmoja apewe chake? Sasa nishawapa. Mnachosubiria hapa
ni nini na nyinyi wote hampatani? Nataka kwenda kupumzika kabisa. Sio
nafika huko zinaanza simu za nirudi kuamua ugomvi. Tushamzika baba.
Wageni washaondoka. Waliobaki hapa ni ndugu wa karibu. Na wenyewe kesho
au kesho kutwa nitafanya utaratibu waondoke. Msiba ushaisha. Haya na
nyinyi naombeni muwapishe hapa.” Wakaanza kutoka mmoja baada ya mwingine
mpaka mwisho.
“Nakushukuru
sana Mill. Mungu atakulipa. Lakini jua wazi sikuwa nikimtesa baba yenu.”
“Mimi sio mtoto mdogo mama Kenny. Usiku mwema.” Akamjibu hivyo kwa ukali kidogo
na kuondoka na Pam wake.
~~~~~~~~~~~~~~
Mill aliondoka
nchini akijua maisha ndio yamembadilikia, lazima afanye kitu cha ziada.
Pam anamtaka na ndiye aliyeachiwa baraka zote za kusimama kama
mama Mgini. Baba yake alizungumza sana na Pam akimtambua kama mwanamke
wa kipekee katika ukoo wao kufikishwa alipofikishwa yeye na kina
Mgini. Ile ndoa ya kijijini kwao kina Pam, mzee Mgini aliitambua kama ni ndoa
KAMILIFU, kwani ya kanisani Mill alitaka wakafunge nchini Marekani ili watambulike
kiserikali kama mke na mume iwe rahisi kumsaidia kuishi huko kwa urahisi.
Hapo mzee Mgini
amekufa akijua ameshamuozesha kijana wake. Wanasema mahari huwa
haimalizwi lakini mzee Mgini yeye alimaliza kwa kina Pam, akimwambia babu
yake analipa yote ili ikumbukwe daima kuwa Pam ni Mgini na amefunga
milango ya mwingine kuja kumlipia mahari huyo Pam. Kwamba wasije pokea
mahari nyingine tena ya Pam, yeye ameshamaliza.
Akiwa mahututi
hospitalini akamsihi asije mbadilikia kijana wake. Alimsifia sana Mill kwa
Pam, akimuhakikishia Pam kuwa Mill amemaliza kwake, ni yeye tu kusimama
kama mke zaidi wanapokuwa mbalimbali. Akamuomba amsaidie Mill kusimama na
familia aliyoacha. Kwa hiyo Mill anaondoka nchini akiwa ameacha mke
kabisa wala si mchumba.
Mbali na jinsi
ya kumtoa Pam nchini, bado mzigo wa shule aliokuwa akimsaidia kubeba baba yake
ndio umeshakuwa wake. Na Mill alikuwa akilipa ada kama international
student, ada kubwa haswa.
Alihangaika
kutengeneza njia ya kumfanya awe raia, IKASHINDIKANA. Ikabakia njia
pekee ya kuoa mzawa wa Marekani ambaye angempa makaratasi/ kuja
kuwa raia baadaye. Akajaribu kwa udi na uvumba kumtafuta mmarekani
atakaye mlipa pesa ili amuoe kisheria, abadili status, lakini
napo AKASHINDWA. Malengo
makubwa, mazuri, lakini yakakumbana na UGUMU mkubwa sana.
~~~~~~~~~~~~~~
Safari ya mwisho
kurudi Tanzania, Mill hakuwa na furaha kabisa. Wazi alijua cha kwanza atapotea
nchini kwa kipindi chote anachoshugulikia kuwa raia huko nchini Marekani.
Hawezi kutoka mpaka mambo yake yakamilike. Hata hivyo itamlazimu kuongeza
juhudi ili kuhakikisha aharibu status yake ya kuwa mwanafunzi. Lazima
ahakikishe anayo pesa yakutosha. Mchezo wa kurudi nchini kwa Pam, mara kwa mara
lazima kupunguza.
Ikabidi awe
mkweli kwa Pam, ila hakumwambia kama itabidi kuoa huko, ili yeye awe
raia, kisha amkaribishe na yeye kiurahisi. Alimwambia itamchukua muda
kurudi tena, inabidi akapambane. Kutengeneza pesa, yakuweza kuishi huko, alipe
ada kama mwanafunzi wa Kimataifa kisha pesa ya kutosha kubadili uraia.
Pam akaelewa akimuhurumia.
Kuagana Kwa
Mara Ya Mwisho Kwa Pam & Mill.
Safari hii ni
kama walikwenda fungate kabisa. Walijitenga na kila mtu, wakaenda kujifungia
kwa majuma mawili mfululizo wakiliwazana, huku Mill hana raha! Anamuachia
nani Pam wake? Je, atafanikiwa kuja kurudi kumchukua? Maana tokea uhai wa baba
yake, walihangaika sana na baba yake kumtoa Pam nchini wakitumia benk
statement ya mzee Mgini, lakini mara zote alishindwa kupata Visa.
Leo anaondoka
bila tumaini, hajui anarudi lini! Na Pam naye alijua fika kazini analazimishia
tu, lakini hawamtaki. Sandra mwenyewe alikuwa akimtafutia sababu
kila wakati. Ikawa kuagana kwa uchungu, kila mmoja hajui hatima yake.
Baraka Za Ndoa
Na Wajibu Wake.
Ndoa ya Mina na Andy ikaendelea kuonyesha matunda
yakutamaniwa na wengi. Walishajaliwa mtoto huyo wa kiume ambaye ndio mjukuu
pekee wa kiume kwa familia ya Ruhinda. Wakati Ayan akiendelea kukua vizuri, baba
yake naye akapandishwa cheo kazini. Furaha ikazidi kuongezeka,
ila ubusy nao UKAZIDI kuongezeka.
Kila baraka unayopewa, inakuja na jukumu lake. Basi ndio ikawa Andy na hicho cheo. Ile tabia
yakurudi mchana nyumbani kwa chakula na penzi kwa Mina ikaanza kupungua kwa kasi
kubwa. Maana wakati mwingine akirudi nyumbani Mina naye anashugulika
na baraka nyingine, mtoto.
Alipokuwa akijitahidi kurudi nyumbani mida ya mchana
anamkuta Mina naye anakuwa na kazi za mtoto. Na yeye Andy anakuwa na majukumu
yanayomsubiria kazini, hawezi kukaa nyumbani muda mrefu. Matiti aliyozoea kuchezea atakavyo, yakageuka chakula chakutegemewa na mtoto.
Penzi la harakaharaka alilokuwa akipewa mchana arudipo nyumbani, likawa likishindikana,
Mina anakuwa na mtoto au kunakuwa na wageni wakumsaidia mtoto. Zaidi mama yake
au mama mkwe.
Uhalisia wa
maisha ukaanza kuchukua sura halisi.
VINGI vilivyokuwa vikiwaweka karibu kama wapenzi, vikaanza kukosa
nafasi. Kila arudipo nyumbani, habari ni ileile. Kama hataishia mikononi kwa
mama yake, basi mama mkwe au Mina anabembeleza mtoto.
Baada ya muda Andy AKAACHA kurudi nyumbani kwa chakula
cha mchana. Ikawa akitoka asubuhi ni mpaka jioni ndipo anaporudi. Ila
mawasiliano hapo katikati ya siku yalikuwepo.
Andy alimnunulia Mina gari nzuri tu. Undugu na ukaribu
na kina Ruhinda ukawa mkubwa. Mina kwenda na Ayan nyumbani kwa wakwe
zake bila Andy likawa jambo la kawaida sasa. Anaweza kuanzia kwa wakwe zake
Msasani. Atasalimia hapo akiwa na mtoto. Mzee Ruhinda acheze kidogo na mjuu,
ndipo aende Tegeta kwa mama yake na Ron.
Mina akawa wa viwango. Anarudi nyumbani kutembea na
mtoto, akiwa na usafiri safi pamoja na zawadi kemkem kwa mama yake. Mama yake
akiwa na safari zake, basi Mina atakwenda kumchukua na kumsindikiza. Waliokuwa
wakimsema Mina, wakafungwa midomo. Akaonekana amefanikiwa haswa, lakini majukumu
yakiwatenga wanandoa hao.
~~~~~~~~~~~~~~
Maisha bila Andy yakaendelea. Uzazi ulishaisha
muda mrefu tu, akabaki yeye tu na mtoto nyumbani bila Andy, na bila wakina mama
wakumsaidia. Maana mtoto ashachangamka. Kina mama/bibi za Ayan wote waajiriwa.
Na Andy lile pengo la kurudi mchana alishaziba na majukumu.
Upweke ukazidi kwa Mina. Wakati wengine wakiwapongeza
kwa maendeleo ya kiuchumi, zaidi kupandishwa cheo mumewe na kuhamishwa makao
makuu, kwa Mina ikawa tofauti. Akabaki na picha ile ya ndoa ya kabla
ya kuzaliwa Ayan, na Andy yule ambaye hakuwa na majukumu mazito.
Kupishana hapo nyumbani likawa jambo la kawaida. Andy
anaweza kurudi usiku tokea alipoondoka nyumbani alfajiri sana, Mina akiwa
amelala. Tabia yakuchelewa kurudi nyumbani kutokea kazini ikawa kawaida sana.
Zile siku za jumamosi na jumapili ambazo Andy alikuwa akizitumia
na familia, wakati mwingine hata hizo siku za jumamosi anakuwa anahitajika
kazini, tena kwa muda mrefu tu. Ila jumapili Andy akawa akijitahidi kuwepo na
familia. Kanisani, nyumbani kwa wazazi mpaka jioni. Wakirudi nyumbani wamechoka.
Majukumu ya mtoto, tayari inakuwa imeshakuwa usiku. Muda wao, hao wawili
kama wapenzi na wanandoa
ukawa haupo au ni mfupi sana, pale usiku mmoja anapoomba penzi,
basi.
~~~~~~~~~~~~~~
Mina ambaye amekuzwa kwenye kiasi, mali
ya kutoshea siku moja, ila yupo na watu anao wapenda, hayo mafanikio
makubwa akaanza kuona mzigo. Mpenda kupendwa. Mtaka mapenzi. Ashikwe. Anyonywe
hapa na pale. Abembelezwe
kama Omar alivyokuwa naye masaa mengi, akazidi kuteseka maana mwenzie
anashinda kazini siku nzima mpaka usiku. Akirudi nyumbani, akili imechoka,
anataka kupumzika tu. Wakati mwingine hata penzi anaona asamehe ili
alale muda mfupi kesho awahi tena kazini. Yeye anashinda nyumbani na mtoto,
hana awazalo ila familia tu.
~~~~~~~~~~~~~~
KILA MTU anaingia
kwenye ndoa na MATARAJIO yake, na BADO jamii inayowazunguka INAWAPA matarajio
yao.
Hutofautiana na si mara zote vinafanana.
Sasa mpaka
kutimia matarajio ya WOTE, kwenye ndoa ya wawili hao na uhalisia wa MAISHA Ya ndoa hiyo, ndipo TALAKA nyingi hutokea,
au kukiwa na rehema, basi, WAWILI hao hupitishwa
kwenye SHULE inayowapa mtazamo halisi wa ndoa YAO, WAO wawili. Na wala SI
ndoa kwa ujumla. Ndoa yao wao wawili, yenye msingi wao.
YAPI MAPITO ya hawa Love at First Sight?
Usikose
kuwafuatilia.
0 Comments:
Post a Comment