![]() |
Mtoto huyo wa Mina na Andy, ungempenda. Hajui
kukataa watu na pia hakuwa mlizi. Ilimradi umpe maziwa, basi atazunguka
na chupa yake, akiwa na usingizi ukimuweka kitandani kwake bila shida, atalala.
Hilo likawa na faida na hasara kwa huyo mtoto na sehemu
wanayoishi, katikati ya jiji kwenye mengi.
Wasichana wa kazi wakawa wakimpuuza sana. Mina
akitoka tu kwenda chuo, akiwaachia mtoto, na wao wanaondoka. Wanampa
huyo mtoto maziwa, wanamuweka kitandani kwake, na wao wanaondoka na kumfungia
ndani. Wakawa wakimpuuza
huyo mtoto hawamjali. Afya yake ikazidi kudhorota Mina asijue
sababu, maana akirudi anamkuta mtoto msafi na msichana wa kazi yupo.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku moja darasa la mchana la Mina liliahirishwa.
Akaingia vipindi vya asubuhi tu na kuamua kurudi nyumbani. Alifika
akakuta nyumba imefungwa. Kwa kuwa alikuwa na funguo ya akiba, akafungua.
Alimkuta mtoto wake anaongea kitandani. Msichana wa kazi hayupo.
Akamtoa na kumsafisha. Hapakuwa hata na chakula
kilichopikwa. Akapika na kumlisha mwanae. Akamuogesha kabisa, bado msichana wa
kazi akawa hajarudi. Akiwa amemlaza mtoto wake kitandani kwake yeye akijisomea,
akasikia mlango unafunguliwa. Akaangalia saa. Akaona ni muda karibu na ule
aliomwambia yule msichana atarudi siku hiyo. Akaumia sana.
Basi hata ajali, hakujali kwa kuwa hakujua kama Mina
yupo ndani. Akaanza kuzungumza na simu yake bila hata kuingia na kumtizama
mtoto. Akamsikia yupo jikoni, ndipo akahisi ameshituka baada ya kukuta chakula.
Pakatulia.
Mina akajua ameshajua kama yupo ndani. Akatoka. “Hivi ndivyo unavyofanya kila siku
ninapokuachia mtoto wangu?” Mina akamuuliza taratibu tu. Akajaribu kujitetea
uongo wa wazi kabisa, jioni ileile Mina akamuondoa.
Baraka &
Jukumu Lake.
Na hivi kila baraka huja na majukumu yake. Kuitunza hiyo baraka ili idumu, basi ndicho kilichowapata wanandoa hao. Ila kwa swala la mtoto ikawa Mina ndio anahangaika mwenyewe. Baraka ya uchumi, Andy ambaye akili alishazamisha
kazini, ili ya nyumbani yasiharibike, pesa isipungue ila kuendelea kuongezeka.
Kwa hiyo yeye yake yakawa yakimuendea vizuri huko
kazini. Hana kipingamizi. Akabakiwa na maisha yake, na kazi tu.
Anadamka asubuhi, anawahi kazini mpaka usiku anaporudi nyumbani. Yanayoendelea
hapa katikati nje ya ulimwengu wa
kazi, hayakumuhusu moja kwa moja japo ni familia yake.
Shuguli ikabakia kwa mkewe. Shida za wasichana wa kazi kwa malezi ya mtoto wao, na
shule inayo endelea. Mina akaendelea kupambana kwa juhudi zote
ili chochote kisikwame. Msichana wa kazi akisumbua, mama Ron na
mama Ruhinda ndio wanahusika na Ayan ili shule ya Mina isisimame
na asilemewe. Na yeye akaweka juhudi na uaminifu. Mwaka wa kwanza wa
Mina ukaisha, Ayan akiwa na miaka miwili tayari.
Jamii inayo wazunguka ikizidi kuona mafanikio
kwao. Kwa upande wa kina Mina, kuona Mina ametulia kwenye ndoa yenye pesa
na mume mwenye juhudi ya kazi, anamtoto na amerudi shule. Huo ukawa muujiza
kwa mama Ron ambao hata malaika angeshuka kutoka mbinguni na kumwambia huko
mbinguni hakuna Mungu, asingeamini. Na kwa upande wa kina Andy, ni kweli
alifanya vizuri. Akafanania na kina Ruhinda kabisa. Na akawa ameleta faraja ya
huyo mjukuu. Watizamaji jamii wakazidi kushangulia ndoa hiyo. Maisha
yakaendelea
~~~~~~~~~~~~~~
Utendaji kazi wa Andy ukawa mzuri SANA. Andy muaminifu
na mchapa kazi haswa. Sifa yake ni kama baba mlezi wake alivyosema. Hataki
jambo limuharibikie
mkononi. Jambo alilotabiri yule
baba mlezi, ikawa tofauti. Si Mina, uaminifu akaweka kwenye KAZI.
Usingemkuta Andy akizembea kazini. Alichapa kazi vilevile kama alivyokuwa mseja.
Hajui Mina anaendeleaje kibinafsi wala maswala ya
mtoto hayakuingilia kazi yake kabisa. Alipomuona Mina ameshikilia
ya familia, yeye akazidi kuzama kazini na kuwa mfano mzuri sana mpaka akachaguliwa
kwenda kujaribisha kufungua tawi Dodoma ili akifikia idadi kadhaa ya wateja
fulani, kampuni ifungue huko tawi jingine. Na yeye ndio akaahidiwa
ikifanya vizuri, atapewa Zone/kanda ya kati.
Baraka Zikazidi Kumiminika.
Mina anafanya vizuri CHUONI, Andy naye anafanya
vizuri sana KAZINI na mshahara
kuongezeka, huku mtoto wao akizidi kukua. Akiwa yupo mwaka wa pili
chuoni, mumewe akaanza safari za Dodoma huko kuliko ongezeka baraka. Wanao wazunguka wakaendelea kufurahia
mafanikio yao, wasijue kinachoendelea ndani ya hiyo ndoa.
Walishaanza kuishi kama WAPANGAJI waaminifu. Walianza
kwa ahadi nzuri tu. “Usijali Mina. Nikifanikiwa huko, utasahau shida
zote. Tutakuwa tunazungumzia mshahara wa mamilioni mengi mnoo.” “Naomba usinisahau
Andy!” “Ni kwa muda tu.” Shida ya Mina ni watu kama alivyozoea kwa mama yake,
maisha ya umoja si mapesa.
Lakini Andy yeye amelelewa kwenye mafanikio
makubwa. Halafu Lora alishamuingia akilini, alitaka kuhakikisha
alichomwambia Lora hakitimii kwake. Ayan anakua na kukutana na baba aliyefanikiwa
SANa kwenye maisha si kama alivyosema
Lora.
Akaongeza juhudi kazini. Safari za Dodoma zikaanza
huku akijitahidi kuwepo nyumbani siku za weekend. Mina akabakiwa na jukumu zito la mtoto asiye
na msichana wa kazi na shule hiyo ya mwaka wa mwisho.
~~~~~~~~~~~~~~
Andy akawa na pesa nyingi sababu ya marupurupu mengi
anayokuwa akilipwa kazini zikiwepo hizo safari, malazi ya kila
siku huko aliko Dodoma, maana bado alikuwa ni mwajiriwa wa Dar. Kwa hiyo huko
Dodoma ikawa ni kama anatumwa na kampuni, kikazi. Lazima kugharamiwa. Na
mengine mengi. Kwa hiyo kweli PESA ilikuwepo. Akaona aendeleze nyumba yake ya
Kigamboni.
Hiyo nayo ikaongezeka kuwa BARAKA ingine, iliyohitaji muda
wake PIA. Kusimamia ujenzi. Siku za jumamosi anaporudi Dar kwa familia, karibu
siku nzima yupo kwenye ujenzi wa nyumba yao, Kigamboni. Akirudi amechoka.
Wakati mwingine Mina anaporudi na mtoto nyumbani wanamkuta amelala kwenye
kochi, hoi.
Akiwa macho napo simu haziishi. Atapigiwa
simu na wafanyakazi wa Dodoma kwenye hilo tawi jipya alilofungua. Wakiuliza
maswali na yeye kufuatilia kwa karibu sana kujua mambo yanavyoenda huko, ili KUSIHARIBIKE
kitu. Huko Dodoma kukawa kukipewa kipaumbele cha hali ya juu. Iwe kwa
uwepo wake au kwa simu awapo nyumbani. Halafu napo bado huku
wakishindana na wajenzi wa nyumba yao huko Kigamboni, wakitaka hili na lile.
Mina akianzisha mazungumzo, akitaka kuzungumzia
jambo na mumewe, simu itaingilia. Pakawa na fujo ya namna yake, ya maendeleo. Hakuna utulivu wakifamilia. Andy
akaweka kipaumbele kwenye mambo yake na yao kama huo ujenzi wa
nyumba YAO, kazi ambayo inasadia familia kiuchumi maana Mina
hakuwa na kazi, yeye ndio breadwinner.
Ikawa hekaheka
ya maendeleo katikati yao akitaka
jambo katika HAYO lisiharibike, Mina akimwangalia tu.
Akiwa Dar kwa familia, hajulikani kama yupo nyumbani
au bado yupo Dodoma kazini. Yupo nyumbani kimwili lakini mawazo na muda wake
wote vipo Dodoma kwa simu kama si Kigamboni.
~~~~~~~~~~~~~~
Wazungu wanausemi wa wapenzi wakiwa
kwenye hali hiyo, ku grow apart. Ikawa dhahiri sasa, wapenzi hao wakawa wapangaji wenye
jukumu la kuwalazimu kuishi nyumba moja wawapo mji mmoja. Na Andy naye
ikawa kama anayejitahidi tu kuwepo nyumbani, lakini sio kwa
wakati huo. Ikawa kama lipo jambo la
msingi na muhimu
sana, pengine angemaliza kwanza, ndio angetulia. Ikawa anakimbizana nayo. Busy kuanzia asubuhi mpaka usiku. Jumapili wakitoka kanisani, wanaenda
kujumuika na wenzao kwa wazazi mpaka jioni. Usiku au jumatatu asubuhi anarudi
Dodoma.
Mina akajaribu kuzungumza naye, nalo HILO halikufanikiwa
kufikia mwisho, kwani simu ya kikazi ikaingia ambayo ilimlazimu Andy
kutoka kwenda kuzungumza nao akitoa maelekezo.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku hiyo ya birthday ya mzee Ruhinda, watoto wote
walikuwepo na Andy akamuahidi Mina atarudi ili awe naye kwenye sherehe. Mina
akaenda saluni, akatengenezwa vizuri. Akampigia simu Andy. “Naondoka na ndege ya mwisho ya huku.” “Utawahi?” Mina
akauliza kwa wasiwasi. “Nimekwambia nitawahi Mina! Au
unafikiri na mimi nafurahia haya maisha?” Andy akiwa amechoka, hajala
siku nzima, halali vizuri, mambo mengi, akaanza kumfoka. Mina
akanyamaza.
“Au wewe ndivyo ulivyokuwa ukifikiria kwamba
nafurahia hivi?” Kimya. “Mimi nahangaika kwa ajili yetu wote! Nilipokwambia
nakuja huku kikazi ulifikiri nipo huku kustarehe? Nina nyumba
ambayo najenga ambayo inabidi kazi hii hii ndio nijitahidi nilipwe ili
iweze kukamilika. Shule yako pia inahitajika pesa. Bado
wewe mwenyewe na mtoto mnahitaji pesa. Hapo usisahau gharama za
hapo nyumbani ili maisha yenu ya kila siku yaende vizuri. Chakula, maji, umeme,
kodi na mambo mengine yote ni MIMI. Ulitaka nifanye nini?” “Mimi
sikutaka unihesabie jinsi ninavyokugharimu Andy na wala
sikukupigia ili nikuudhi. Lakini
kumbuka hii ni week ya pili haupo nyumbani!” Mina
akaongea taratibu tu.
“Ndio nakuuliza unafikiri mimi nafurahia
haya maisha?” “Mimi naona tuagane Andy. Huko unakokwenda, unataka kuniumiza
bila sababu. Hii ni birthday ya baba yako. Uje, usije ni juu yako.” “Kwa nini nikuumize
sasa!? Mimi nimezungumzia uhalisia tu.” “Kazi njema Andy.” Mina akakata simu.
~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment