Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 18. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 18.

“Subiri kwanza Mina.” Akamkimbilia. “Mwenzio mjamzito Andy!” “Haiwezekani!” Andy akaanza kucheka kwa furaha. “Andy!” Mina akashangaa asimuelewe na malengo waliyokuwa nayo juu yake. Akamnyanyua na kumrushia kitandani. Akaanza kumbusu tumboni, Mina akasikia nguo ya ndani ikishushwa, akaanza kucheka taratibu akijua mchezo unaofuata sio wakitoto.

Andy alifurahia Mina alijua kwa ufanywaji wake mapenzi siku hiyo, mpaka akashangaa. Andy alichangamkia mapenzi tena na tena akimpongeza Mina kwa maneno na vitendo, alipomaliza, akarudi tumboni. Akambusu tena na tena.

Akakumbuka kisa cha Omar jinsi alivyotafuta mtoto na huyo Mina, leo bila kutoa jasho ila starehe tu, Mina anambebea mtoto! Hakuamini. “Nimefurahi Mina! Nimefurahi sana. Na kuhusu shule, vyote vitaenda tu, wala usiogope.” Wakaweka mipango hapo kitandani Mina akicheka na kuanza kufurahia mimba sasa.

~~~~~~~~~~~~~~

Mambo yakabadilika, Andy ndio akawa anaamka kuandaa kifungua kinywa akimtaka Mina apumzike tu. Atapewa penzi zito asubuhi hiyo. Watakwenda kuoga, Mina atarudi kitandani. Andy anamwandalia kifungua kinywa kizuri akidai ni chake na mtoto, atampelekea kitandani yeye anawahi kazini. Kazi ya Mina ikawa kula kulala. Akaanza kupanuka na kuzidi kuiva.

Hana anapokwenda, analelewa kama mgonjwa. Akitoka hapo yupo na Andy. Kliniki, kanisani na sokoni. Akipata kitu kizuri, basi atamnunulia na mama yake na kutaka ampelekee kabla hawajarudi nyumbani. Basi watapita kwa mama yake, watacheka kidogo, yeye na mumewe wanarudi nyumbani.

Maisha yakawa ya amani na furaha. Akili na macho ya Andy vyote vipo kwa Mina kitu alichokuwa akikifurahia sana Mina. Wakitembea mkono wa Mina upo kwapani kwa Andy. Mina akajawa deko lakupitiliza. Hajaongea, Andy ametenda. Penzi zito likanoga.

Kina Ruhinda.

Mmoja wa mfanyakazi mwenzake Andy alikuwa akibatiza mtoto kwenye kanisa lile lile ambalo walikuwa wakienda kina Ruhinda. Na wao wakaalikwa kuhudhuria. Andy akaona kwa kuwa na wao ni wa RC basi na wao waanzie kanisani kabla ya tafrija.  Mina alikuwa amependeza na kigauni chake na tumbo la mimba ya miezi 8 akiwa amejazia haswa.

Cheko, mkono kwapani kwa Andy wakisogelea jengo hilo kubwa ambalo ndio kanisa ambalo kina Ruhinda huudhuria wakati wote. Na wao wakawa wapo kwenye ibada hiyo wakiwa na wao wamehudhuria moja ya ubatizo wa mjukuu wa rafiki yao.

Kwa kuwa haikuwa ni misa wanayokwenda kina Ruhinda, Andy hakuwa na wasiwasi wa kukutana nao. Lakini ikawa sivyo. Wakiwa wanasogelea jengo la kanisa, ana kwa ana na familia hiyo ya Ruhinda. Tena wote. Wakaduaa. Mina akajirudisha nyuma ya Andy taratibu kama anayejificha. Pakabaki kushangaana. Andy bila kupoteza muda. “Shikamooni.” Wazazi wakaitika.

“Hongereni Andy na Mina.” Akaongeza mama Ruhinda. Mina hakujibu, ila Andy akaitika kwa mshangao kidogo. “Asante! Japo sijui ni kwa nini!” Bila kusubiri jibu Andy akaendelea. “Anyway niwatakie misa njema.” Akamvuta Mina.

“Karibuni nyumbani Mina.” Mina na Andy wakamgeukia mama Ruhinda kisha Mina akamtizama Andy. “Asante. Lakini tupo hapa kwa ajili ya ubatizo wa mtoto wa rafiki yangu. Kwa hiyo tuna mipango tayari.” “Hata wakati mwingine Andy mwanangu. Karibuni nyumbani. Milango ipo wazi. Umesikia Mina mama? Karibu sana.” “Asante.” Mina akajibu kwa kifupi tu. Andy akakunja uso kidogo kama mwenye swali, lakini akashindwa kuliuliza, akaona waondoke tu. Ndugu zake wengine kimya wakishangaa. Hata baba yake hakuongea kitu zaidi ya kuitika salamu. Wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wanatoka, mama Ruhinda akawawahi tena. “Andy!” Mina na Andy wakasimama na kugeuka. “Tuna chakula chakumshukuru Mungu kwa ajili ya kaka yako kutimiza miaka 45, jumapili ijayo. Naomba na nyinyi mfike nyumbani.” Akaongea mama Ruhinda kwa kujihami. “Asante.” Akajibu jibu la jumla Andy nakutaka kuondoka na mkewe.

“Mina mama, utakuja? Najua tulianza vibaya na ninaomba unisamehe. Najua sikufanya vizuri na ndio maana nilikuja kukuona shuleni kukuomba msamaha.” “Mimi nimesamehe mama. Yameisha.” “Asante Mina mwanangu. Basi nawaombea kila la kheri na nina amini nitawaona nyumbani wewe na Andy.” Mina akamwangalia Andy, Andy naye akabaki akimwangalia. “Naamini tutakuja mama.” Mina akajibu huku akicheka kidogo akimtizama Andy. Andy kimya. “Basi nitawasubiri.” Akajibu mama Ruhinda na tabasamu na kuondoka.

Kwa Kina Ruhinda Tena.

Jumapili inayofuata Mina na Andy walikwenda kanisani kwao Mwenge, sio pale walipokuwa wakienda kina Ruhinda. Kisha wakaenda nyumbani kwa kina Ruhinda. Walikuta watu wengi na kumeandaliwa vizuri tu. Marafiki wakaribu wa hao kina Ruhinda hapo ndio waliokuwepo hapo. Vikajaa vicheko. Alipoingia tu Mina na Andy, mama Ruhinda akamuwahi.

Akamfuata na kumshika mkono kabisa. Akamtambulisha kwa kila mtu akijivuna. Andy kimya akiwatizama. Mina alijawa cheko, Andy akimwangalia tu. Pongezi zikaendelea kwa Andy kwa mke mzuri na mtoto wanaye mtarajia siku za karibuni. Gafla Mina akawa ndio jina hapo kwenye hiyo tafrija. Upendo alioonyeshwa, na kujaliwa, yeye Mina akasahau ubaya wote.

“Ungependa tufanye babyshower?” Mama Ruhinda akauliza kwa kujihami ila kwa upendo sana kwa Mina. Mina akamwangalia Andy, akakuta akimtizama. Walikuwa wamebaki ndugu tu hapo, watoto wakisinzia. “Kama mtaona sawa, tunaweza kuifanya hapahapa ili kupata zawadi za mtoto.” “Tulishanunua kila kitu cha mtoto. Andy ameshafunga hata kitanda kabisa. Chumba chake kipo tayari.” Mina akaongea kwa upole na cheko akimwangalia Andy.

“Hata diaper na baby wipes tu!” Mama Ruhinda akaweka msisitizo. “Tena mama, tunaweza kuwaambia watu iwe ni zawadi ya diapers na baby wipes tu. Mnaweza mkapata nyingi wala msinunue mpaka mtoto anafika mwaka.” Akadakia Paulina kwa mama yake kama kuweka msisitizo. “Kwani umebakiza muda gani ujifungue?” Akauliza Raza naye akionekana akiwa amehamasika. Mina akamwangalia tena Andy huku akicheka kama ambaye ameshalemewa.

“Kwani mmeshajua hata mtoto mwenyewe ni jinsia gani?” Akadakia Devi mme wa Paulina. Wao walikuwa wamekaa sehemu ya sebuleni, wanawake na hiyo mipango sehemu yakulia chakula. Andy kimya akiwa amekaa sehemu ambayo wanaonana na Mina vizuri tu. Pakazuka ukimya. Wakisubiri jibu.

“Andy?” Mina akamuita taratibu kama akimtaka yeye ndio ajibu. “Tunategemea mtoto wa kiume baada ya majuma matatu kuanzia sasa, anaitwa Ayan. Kama ilivyo maana ya jina lake, ni zawadi yetu kutoka kwa Mungu. Naomba kwa sasa Mina akapumzike. Amekuwa na siku ndefu sana. Asanteni kutukaribisha.” Andy akasimama.

Mina akajua ndio wanaondoka. “Asanteni kwa kila kitu. Nitakwenda kuzungumza na Andy, kisha nitawajulisha.” Mina akaongezea huku akisimama. Andy akamsogelea. “Pochi na viatu vipo wapi?” Andy akamuuliza huku akimsaidia kusimama na kumuweka nguo vizuri kama mtoto mdogo! “Viatu nilivua pale nje kabisa na pochi...” Mina akajaribu kukumbuka. Mama Ruhinda akasimama haraka kwenda kumtafutia.

“Hongereni sana Andy na Mina. Mungu akujalie Mina ujifungue salama. Utuletee huyo Ruhinda hapa. Na sisi tunamsubiria kwa hamu.” Akaongeza mzee Ruhinda. “Asante baba.” Akaitika Mina na cheko la heshima kidogo. Ndio kila mmoja akatoa tena pongezi kwa mjukuu huyo wa KWANZA wa kiume kwenye familia hiyo, maana ni kama palizuka ukimya kwa ndugu wa Andy baada ya kujua ni mtoto wa kiume.

“Kama mtaafikiana na mwenzio juu ya hiyo babyshower anayotaka kuwafanyia mama yenu hapa, itakuwa njia nzuri pia ya mama yako kushirikiana na mama hapa, wakafahamiana zaidi. Na huyo mzee mwenzangu akakaribishwa ramsi nyumbani. Azaliwe akijua mji wake.” Akaongeza mzee Ruhinda kwa furaha ya waziwazi baada yakujua mjukuu ni wa kiume, kila mtu akamuona alivyobadilika ghafla. Maana alikuwa kimya muda wote, gafla akawa amechangamka!

Mina akamwangalia Andy, Andy akaanza kutafuta pochi ya mkewe. “Basi nitazungumza na Andy, akikubali nitamwambia na mama, halafu Andy atawajulisha. Asanteni.” Mina akajibu kwa heshima, mumewe akaipata pochi pembeni ya kochi alilokuwa amekalia yeye mwenyewe muda wote. “Twende Mina. Usiku mwema.” Andy akaaga akimshika mkewe mkono kwamba waondoke. “Na nyinyi.” Wakatoka mpaka mlangoni mama na baba Ruhinda wakisindikiza.

“Nishike mgongoni wakati nakuvalisha viatu.” Wakamsikia Andy akimwambia mkewe. “Mguu wa kushoto umevimba zaidi Andy! Kiatu hakiwezi kuenea sasa hivi. Acha nikanyagie tu.” “Ulikumbuka kunywa maji leo?” Wakamsikia Andy akiuliza taratibu kwa kumjali mkewe. “Nilikunywa. Lakini sidhani kama yalitosha.” “Itabidi kesho turudi kwa daktari.” “Mpaka kesho nitakuwa sawa Andy. Usiwe na wasiwasi. Nikifika nyumbani nitainyoosha. Asubuhi utaona. Itakuwa imerudi kuwa sawa.” Wakabaki wakiwasikiliza.

Andy amebeba pochi ya Mina, anamvalisha viatu mlango. “Kazana maji Mina mwanangu. Na hivyo ulivyosema ndio muhimu. Usiining’inize sana.” “Nitajitahidi mama. Usiku mwema.” Mina akaitika na kuaga tena, wakaondoka.

Babyshower ya Mina.

Kina Ruhinda wakachangamkia hiyo babyshower mpaka wakawashangaza Andy na Mina! Ikawa tena kama sherehe kubwa! Walikuwa wanaume na wanawake! Andy na Mina kimya wakijiangalizia hekaheka. Mzee Ruhinda alitangaza wazi kuwa Mungu amempa mrithi wa kwanza, kitu ambacho hata Andy mwenyewe hakufurahia. Akaona si sawa kwa kaka yake ambaye alikuwa na watoto wa kike watupu. Lakini Pius hakuonekana kujali sana. Na yeye alikuwepo hapo akifanikisha.

Mama Ron, Ron na ndugu wa karibu pamoja na marafiki wa mama Ron baadhi nao walikuwepo hapo kwenye hiyo sherehe.  Mama Ron akijivuna haswa! Mina aliyekuwa gumzo kwa jamii, ameolewa pazuri!

Ila hakuwa na imani nao sana. Alimwambia Mina ale kabisa nyumbani ashibe,  na akifika pale na kinywaji chake kwenye chupa. Akamuonya kwenye sherehe nzima asije kula wala kunywa isipokuwa kitu alichofika nacho hapo. Naye Mina akafuata kama mama yake. Jambo la furaha likageuka, kujihami.

Andy alikuwa mtulivu na makini katika kila analolizungumza na kusikia, akimwangalia Mina wakati wote. Marafiki wa karibu ndio waliokuwepo hapo na pakapambwa vizuri. Ni kweli kulifana na walipata zawadi zaidi ya walivyotegemea. Zawadi nyingi waliacha hapo, Mina na Andy walisema hawana nafasi yakuweka na vingi walishanunua. Basi, shuguli ilipoisha Andy akamchukulia taksii mama yake Mina, wakarudi nyumbani na Ron, wao wakarudi kwao. Mina alikuwa amechoka.

Mungu Humpa Amtakaye, Na Hakuna Wakumuuliza Kwa Nini.

Katika wote ambao pengine wangestaili kushika mimba hiyo ya mtoto wa kiume pengine angekuwa Raza, kama si Paulina. Raza alimtafuta huyo mtoto wa kiume kwa garama kubwa mno mpaka akasalimu amri. Alitaka sana kumzalia Pius mtoto wa kiume, ambaye ni kijana wa kwanza wa Ruhinda. Yeye na mumewe walimsaka mtoto wa kiume kwa wazi kabisa bila kuficha, wakiomba msaada mpaka wa kitaalumu, wakiwa tayari kutumia pesa aina yeyote ile ili tu Raza azae mtoto wa kiume.

Raza amesoma na anakazi nzuri tu. Mumewe ndio hivyo. Wakati akitafuta huyo mtoto wa kiume ndio alikuwa ameingia kuwa miongoni mwa watu watatu wa msaidizi wa Gavana wa pesa wa Tanzania. Pesa ilikuwepo ya kumpeleka Raza kwa daktari yeyote yule, popote kule duniani kusaidia kupata mtoto huyo wa kiume, lakini akaishia mtoto wa pili tena ndio na kizazi kikatolewa kabisa akiwa anaponea kifo. Habari ya mtoto wa kiume ikaishia hapo, hawakuzungumzia tena. Pius akaridhika na watoto wake wawili wakike.

Ikawa hivyohivyo kwa Paulina, msomi wa kike wa Ruhinda. Yeye alishapanga kuingia leba ni mara mbili tu. Akapanga mtoto wa kwanza wa kiume, na wa pili wakike, BASI. Na mimba zake hazikuwa za kushika hovyohovyo. Yeye na mumewe walishapanga muda. Wakati wakiwa tayari kwa mtoto wa kwanza, walikwenda kwa daktari. Wakazungumza naye ili kupata ushauri wa kushika mimba ya mtoto wa kiume. Walifuata mashariti yote lakini akaishia wakike.

Wapili naye hawakukata tamaa wakijua ndio wa mwisho. Safari hii wakaongozwa na daktari kabisa. Devi mumewe akiwa mstari wa mbele, LAKINI akaishia mtoto wa kike na yeye akapatwa na matatizo ya uzazi. Hata walipotaka kujaribu mtoto wa tatu, ikashindikana. Wakaishia hapo. Na wao wawili, wakike.

Mzee Ruhinda akapenda wajukuu zake hao wakike, ila moyoni akijua ndio jina litakufa endapo hao watoto wawili waliobaki, Andy na Paul wasipopata hao watoto wa kiume. Sasa alipokuja Mina ambaye kwanza walimdharau. Hakutoka kwenye hali kama zao, halafu kubeba mtoto wa kiume! Akainua FURAHA ya ajabu kwa Ruhinda mwenyewe, na mkewe pia.

Mina ambaye kwanza hata hakuwa akijua umuhimu wa huyo mtoto wa kiume. Mumewe wala hakuwahi kuzungumzia anataka mtoto gani! Kwanza hata hawakuwa wakizungumzia kuanzisha familia ila tu kufurahia mapenzi. Eti leo anabarikiwa mtoto wa kiume bila hangaika yeyote! Japokuwa Raza na Paulina hawakusema, lakini mioyoni walijiambia Mungu ana upendeleo.

~~~~~~~~~~~~~~

Zilikuwa zimebaki siku kama 7 Mina kujifungua huyo mtoto aliyekuwa akisubiriwa kwa hamu na baba yake lakini pia na bibi na babu yake. Siku hiyo akiwa amelala na mumewe akaanza kulalamika. “Nasikia maumivu Andy! Kiuno, tumbo na vichomi. Unafikiri ni sababu ya kukaa sana wakati wa kusuka?” Andy akakaa na kuwasha taa. “Pole. Kudhani kama ndio uchungu?” Mina akafikiria. “Bado week nzima, ndio maana nimesuka hizi nywele ili nikae nazo muda mrefu.” “Basi subiri nikupe dawa ya maumivu, halafu nikubembeleze ulale. Maumivu yakiendelea hivyo mpaka asubuhi, nakupeleka hospitalini.” Mina akakubali.

Andy akawa na kazi ya kumsugua kiuno na kumpapasa kuzunguka tumbo zima. Mina analala kama dakika 20, Andy akisinzia, anamsikia akilia. “Inauma Andy! Naomba nimpigie simu mama nimuulize.” “Sasa hivi ni saa 9 usiku, Mina! Mama amelala. Heri twende tu hospitalini.” Wakakubaliana hivyo.

Akamletea nguo hapohapo kitandani, akamvalisha. Ile Mina anasimama tu kutoka kitandani, chupa ikapasuka. Wakaangaliana, ndio wakajua ni kweli ulikuwa uchungu. Uzuri hawakuwa mbali na hospitalini. Akambemba mpaka kwenye gari, njiani akampigia simu Ron na mama yake. Wakakubaliana watawafuata hospitalini.

Akaendesha mpaka hospitalini, akambemba Mina mpaka mapokezi, wakampokea na kumkimbiza leba akiwa na Andy. “Usiniache Andy!” “Siwezi. Nipo na wewe. Usilie na wala usiogope. Sawa?” “Sawa, ila vinauma!” “Najua mpenzi wangu. Pole.” Mina akawa anasukumwa kwenye kigari akipelekwa leba, Andy amemshika mkono.

~~~~~~~~~~~~~~

Bado mapenzi yalikuwa mazito yakutokea uchumba, ndoa, na fungate yao haikuwahi isha. Wawili hao wakajuliana na kupendana haswa. Kwa hakika Andy akapata alichokuwa akitamani maishani na kuzidi. Mina akawa mke wa zaidi ya ndoto zake. Akianza kumpa penzi, basi mtoto wa mapadri atabaki akimfikiria mpaka kazini nakumfanya arudi tena mchana.

Usingekuta wakipishana kwa neno. Kwa haiba Mina alijua kuishi na watu. Hakuwa na makuu na kujishusha kwake haikuwa tatizo. Halafu hakuwa mgomvi kabisa. Akampatia vilivyo Andy. Akajifunza kwa haraka sana kuishi naye. Usafi na akamjulia ukimya wake. Nini anapenda na wapi asivuke mipaka. Kwa ufupi akampatia vilivyo. Ndio ikaja baraka ya mimba, tena mtoto wa kiume, mali hadimu kwenye familia ya Ruhinda, tena hata hakutarajia! Mungu awape nini!

~~~~~~~~~~~~~~

 Wakaingizwa chumba chakujifungulia, Andy akapewa kiti pembeni ya Mina, akawa amemshika mkono akitetemeka huku amefunga miguu. Kila nesi akimuongelesha, alibaki amefunga macho akilia tu, mpaka nesi akaishiwa maneno. Uzuri alikuwa hospitali ya wenye pesa zao. Amelipiwa kuzaa first class, chumba kizima peke yake anasubiriwa na wauguzi wakutosha na daktari yupo tayari kuitwa muda wowote atakao hitajika ili kuja kusaidia. Ilimradi tu jambo lisiharibike kwa mjukuu huyo wa kwanza wa kiume kwa kina Ruhinda. Kwa hiyo hata wauguzi wanazungumza naye kitajiri sio kukaripa.

          Alikuwa akizaa kwa kawaida na hakutaka sindano za kupunguza maumivu wakati wa kujifungua, “Epidural”. Alishaogopeshwa na watu kuwa aina hizo za sindano zina madhara makubwa. Anaweza kupooza endapo atatumia sindano hiyo. Kwa hiyo akawa akiyapata maumivu yote kama yalivyo.

~~~~~~~~~~~~~~

Ikabidi mumewe asaidie maana wauguzi wote waliishiwa lugha ya kuzungumza naye. Mina anatetemeka haijulikani kama ni baridi au hofu, na muda wa kusukuma ulishafika. “Unasikia baridi?” “Nahisi hofu ya ajabu na maumivu makali sana, Andy.” “Niangalie Mina.” Alikuwa akilia sana, anatetemeka mpaka midomo inacheza. Kamasi na machozi vimejaa uso mzima. Kumbe akili ilimrudisha siku mimba ilivyotoka na kusafishwa akiwa Iringa kwa Omar bila ganzi, tena akiwa na kipigo kikali.

          Andy akasimama na kumbusu mara kadhaa, huku akimsafisha uso, wauguzi wakijiangalizia tu mpaka akaanza kutulia. “Najua unaumia, lakini naomba usiogope, jipe moyo ukijua unafanya jambo lakijasiri. Maisha ya Ayan yanakutegemea wewe sasa hivi. Fuata unachoambia na hawa manesi. Fungua miguu, ili akusaidie. Sawa?” “Sawa.” Akapewa denda la mwisho, mpaka akafungua miguu.

“Mtoto anatoka!” Akapiga kelele aliyekuwa anataka kumpima tena njia na kuishia kukutana na kichwa cha Ayan. “Akifunga tu miguu, ataua mtoto wake.” Akaongeza kwa paniki. Wala Andy hakupaniki. Akambusu mkewe na kumwambia. “Usiwe na wasiwasi Mina, karibu sana unamaliza upumzike. Naomba utulie.” “Sawa Andy.” Mina akatulia na kuanza kufuata maelezo, Andy akimbusu na kumfuta machozi.

Akaanza kufuata maelekezo jasho likimtoka na mashozi kama anayenyeshewa mvua. Baada ya hangaika ya muda akisukuma, yule nesi akamwambia asukume kwa nguvu kwa mara ya mwisho, ila iwe ya nguvu sana. Mina akaminya mkono wa Andy  kwa nguvu huku ameng’ata meno. Akasukuma Mina kwa uchungu, maumivu makali, mpaka akafanikiwa kumtoa Ayan.

Huyo mtoto ametoka tu, Mina na Andy wakasikia analia hapo hapo. “Hili dume linaonekana akili yake itakuwa juu sana.” Mmoja akaongea akicheka sababu ya huyo mtoto kulia kwa haraka.

“Hongereni sana na pole mama.” Mina akawekewa mtoto kifuani huku akitokwa na machozi na kucheka. “Ayan!” Mina akamgusa. Na Andy akambusu akiwa vilevile bado hata hajasafishwa vizuri. “Ayan!” Andy naye akamuita taratibu huku haamini kama ni mtoto wake. Ungejua wawili hao wamebarikiwa hiyo zawadi ya Ayan. Walijawa furaha macho kwa mtoto hawaamini kama ni wao.

~~~~~~~~~~~~~~

Simu ya Andy ikaanza kuita mfululizo. “Mama huyo! Ngoja nipokee.” Andy akasogea pembeni wakati Mina akiendelea kusafishwa na kushonwa. “Mina amejifungua salama. Yeye na Ayan wote wapo salama.” Mina akamsikia mama yake akifurahia. Akacheka. “Tupo tu hapa nje tunawasubiria.” Wakaagana na kukata.

Alirudishwa chumbani akalazwa na mtoto wake. Wote hawakuwa na tatizo. “Pole mama yangu mzazi. Pole sana na hongera.” Mama yake Mina akawa akimbembeleza Mina lakini akijivunia. “Nimeshonwa pakubwa mama! Inauma. Mtoto alikuwa mrefu na mkubwa sana.” “Nimezungumza nao pale ndani, wanakuja kukuchoma sindano ya maumivu ili upumzike. Pole.” Andy akaingilia. “Kweli huyu mtoto ni mkubwa sana, lazima kuchanika. Pole mama.” “Asante. Ila nimefurahi!”  Wakacheka.

~~~~~~~~~~~~~~

Andy hakuwa anamuweka mtoto chini. Kila mama yake Mina alipombadili na kutaka alale, Andy alimnyanyua. “Naona Kiongozi umeokota alumasi!” Ron akamtania. Bado ilikuwa alfajiri tu, hakuwa hata amerudi nyumbani kujiandaa kwenda kazini. Mina alipitiwa na usingizi baada ya sindano.

“Daah! Siamini kama ni wangu, aisee! Nilikuwa nikimsubiri kwa hamu! Chumba chake nilianza kukiandaa naona akiwa hata hajatimiza miezi minne!” Wakacheka. “Watoto watamu! Hisia yake ya upendo ni ya tofauti!” “Huwa hakuna anayeelewa hilo Andy mwanangu, mpaka upate wako.” Ron akacheka. “Mimi sasa hivi hapo nakuelewa mama. Ni hisia za ajabu na kipekee mno.” Muda wote huo wanazungumza, Andy macho kwa mtoto wake.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina aliamka aliposikia tu mtoto wake ananung’unika. “Dume hilo! Hakuna kulala! Uzazi ndio umeanza.” “Nilikuwa nimepitiwa na usingizi mzito! Unafikiri ni njaa?” Mina akauliza wakati akikaa kwa shida. “Nakwambia kama ulifikiri mimba ilikuwa kazi, basi ujue ndio umeanza.” Wakacheka.

Mama yake akamchukua mtoto kutoka kwa Andy, akamuwekea Mina. “Toka Ron.” “Naona umeanza kupona, na ujeuri umeanza upya!” Ron akasimama akijua dada yake anataka kunyonyesha. “Sasa Kiongozi?” “Nisaidie kwa leo. Nenda kaangalie mambo yasiharibike pale ofisini. Mimi..” Andy na Ron wakawa wanatoka huku wakiongea.

“Andy!” Mina akaita. “Nakuja sasa hivi, nampa maagizo Ron.” “Naomba usisahau kumwambia mama yako tafadhali. Amekuwa akiniulizia hali yangu na mtoto kila siku!” “Halafu kweli! Nitawapigia. Asante kunikumbusha.” Ndipo akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

 

 

 

 

 

 

Ilipofika saa nne asubuhi chumba cha Mina kilikuwa kimejaa maua, kadi na baluni nzuri za rangi ya bluu. Kina Ruhinda walijaa humo kumpongeza Andy na Mina. Ila mama Ruhinda yeye tokea afike asubuhi, hakutoka. Alikuwa na kazi yakuagiza tu. Mzee Ruhinda, Pius, Paul, Raza, Dave na Paulina ni kama walifika wakati mmoja alfajiri na mapema kabla ya kwenda maofisini kwao.

Mzee Ruhinda alijawa furaha, ungejua bila kuuliza. Alikaa hapo kwa muda ila ikabidi kuondoka baada ya kuchukua picha zakutosha, akasema anakwenda mkutanoni, ukiisha tu, anarudi tena.

Ikawa hivyohivyo kwa wengine muda wa ofisini ulipofika wakaondoka kwa ahadi ya kuja kurudi baadaye. Ilikuwa siku ya kazi. Wote hao wananyadhifa za juu kwenye maofisi yao. Lazima kuwepo ofisini siku ya kazi inapoanza. Ila Paulina baada ya kama masaa mawili akarudi tena akawa hapo na mama yake, pamoja na wengine.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina alijazwa sifa, akikohoa tu, kila mtu anauliza kama yupo sawa. Dume la nguvu, mjukuu wa kwanza wa kiume, Mina amewaletea bila shida! Mzuri, amekomaa na anaonekana ni Ruhinda kwelikweli.

Muda wa asubuhi wakati wanaume hao wakina Ruhinda wakiwa wamejaa kwenye hicho chumba, walikuwa wakitaniana kuwa wao wanadamu kali sana. Mtoto amewafanana haswa. Wanaume hao wote walikuwa warefu, walionyooka wima. Weusi waliokolea, kasoro Pius kidogo alichukua rangi kidogo ya mama yake. Akatoka kama maji ya kunde. Halafu wasafi kwa kuwatizama hata ngozi. Huna muda ukawakuta ni wachafu, yaani usafi wa mwili wao na mavazi ni kama asili. Na wote walichukua mwili wa baba yao, sio mkubwa. Hata Paulina mwili ulikuwa kama baba yake.

Kila mmoja alibashiri chake juu ya Ayan. Mama Ruhinda alikuwa akicheka mpaka ungejua mama huyo amefurahi. Mama Ron hakuwa akiamini kama Mina amemketisha na WAKUU!

~~~~~~~~~~~~~~

Maana Pius, kaka mkubwa wa familia hiyo, ndio huyo miongoni mwa watu watatu wa msaidizi wa Gavana wa pesa wa Tanzania. Na ametumika kwenye hiyo ofisi kwa miaka mingi sana mpaka akaizoea kama kiganja cha mkono wake. Kwa kumuangalia tu, ungejua anayo pesa na utisho wa mamlaka.

Mzee Ruhinda mwenyewe alikuwa mkuu wa boardies za pesa za wakurugenzi za taasisi zaidi ya 6 hapo nchini. Kwa umri huo, bado alikuwa akiongoza! Kijana mdogo, wa Ruhinda, Paul, ndio huyo dokta wa hospitali ya Taifa ya Muhimbili na hospitali ya Hindu mandal. Kijana mdogo tu, lakini jina zuri pia.

Paulina ndio huyo naye yupo ngazi ya juu sana kwenye board ya Auditing nchini, kama kazi aliyoifanya mama yake kwa miaka mingi sana. Paulina alipoingia hapo akafanya vizuri akiongozwa na mama yake.

~~~~~~~~~~~~~~

Kwa hiyo hicho chumba kilijaa neema ya madaraka tupu na Mina ambaye hakuwa kitu, Mungu akampa cha tofauti na wao wote. Kuzaa mtoto wa kiume wa kwanza kati yao. Uthamani wake ukapandishwa hakuna aliyekumbuka hata shule yake kichwani.

Pesa kila mtu hapo anayo, kasoro mtoto wa kiume. Mina akaiunuliwa gafla. Akaleta sababu ya kina Ruhinda hao, mida hiyo ya asubuhi, kukutana kabla ya majukumu yao mazito ya kazi. Vilijaa vicheko, kila mmoja akizungumza lake mpaka walipotawanyika kuwahi maofisini.

~~~~~~~~~~~~~~

“Baada ya hapa mmepanga nini?” Mama Ruhinda akauliza kwa upole. Andy alikuwa na yeye ametoka. Mina akacheka lile swali. “Vipi?” “Andy! Yaani wakati nipo mjamzito, nilimuomba nikijifungua, nikakae kwa mama mpaka angalau mtoto achangamke. Akakubali vizuri tu. Hapa mlipomuona anazungumza na mimi, alikuwa akiniambia anakwenda kuchukua likizo yake kazini, tukiruhusiwa, arudi na sisi nyumbani.” Wakacheka.

“Kumbe safari sio ya Tegeta tena?!” Mama Ron akauliza akishangaa. “Amebadili mawazo, anasema hawezi kulala nyumbani wakati sisi tupo Tegeta, labda tuhame naye!” Wakazidi kucheka. “Tokea mtoto ameletwa hapa, hataki awekwe chini. Ukimchukua tu kutoka kwake pengine umbadilishe, anasubiria kama sekunde hivi, ukimaliza tu, anamchukua mwanae, anakaa naye pale, anabaki akimwangalia, mnamuona anacheka taratibu.” “Na mabusu hayaishi!”  Akaongeza Paulina kwa mama yake Mina. Wakacheka. “Kumbe na wewe umemuona?” Mama Ruhinda akauliza. “Nilikuwa namwangalia tu.” Wakacheka.

“Kwa hiyo hapa naona safari ni yakurudi tu nyumbani. Itabidi mama ndio awe anakuja nyumbani kunisaidia.” “Nilishajaza fomu zangu za likizo. Nikawaambia Mina akijifungua tu, naanza likizo. Kwa hiyo wala usijali. Nitakuwa nakuja asubuhi, jioni Ron akitoka kazini ananipitia, tunarudi nyumbani.” “Asante mama.” Mina akafurahi.

“Basi naona mimi niwe mpole tu. Nilitaka niombe angalau siku hizi za mwanzoni tukakae wote pale nyumbani ili tukusaidie mtoto mpaka upone kabisa, lakini naona heri nimuache tu Andy afurahie mwanae.” Akamalizia mama Ruhinda.

“Lakini asante mama. Nashukuru kwa moyo wa utayari wa kutaka kutusaidia.” “Karibu Mina mwanangu. Sasa muda huu wakati huyu kaka amelala, na wewe lala. Kina Ruhinda usiwaone wembamba hivyo, wanakula hao! Utanikumbuka.” Wakacheka.

“Sikutanii Mina mwanangu. Mimi nilikuwa nikinyonyesha, mpaka napitiwa na usingizi bado wamo tu. Ndio baba yao akawa anasema tuwaanzishie na maziwa mengine. Lakini nikawa nakazana hivyo hivyo. Nilikuwa nakonda kama kijiti kwa kunyonyesha. Labda kwa Paulina kidogo.” Akamwangalia Paulina. “Wanao walaji mpaka sasa hivi mama.” Paulina akaongeza, wakacheka. “Lala Mina. Angalau upumzike. Kazi yakuzaa sio ndogo.” Mama yake akaweka msisitizo. Mina akacheka na kulala.

 ~~~~~~~~~~~~~~

Nyumbani kwa Andy kukawa kituo cha kina Ruhinda. Walikuwa wakipokezana na kupishana hapo mchana kutwa, usiku ndipo walibaki Andy na Mina wakilea wenyewe. Ila saa 12 alfajiri, mama Ron anakuwa ameshawasili hapo nyumbani. Atawasaidia kazi hapo na mtoto, huku akimtaka Mina ajilaze mgongo, apone uzazi. Mina akawa wakudekezwa na kulelewa.

~~~~~~~~~~~~~~

Bado Ndoa Ya Mina Ipo Fungate, Haijaanza Kupitishwa MOTONI Kama Nyingine.

Mungu Ameweka Mkono Wake Hapo, Kila Kitu Kinakwenda Kirahisiii!

Nini Kitaendelea Kwao!

Mill&Pam Je?

Inaendelea…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment