Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 16. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 16.

Mill ndio alikuwa kijana wakwanza kutoka kwa mzee Mgini. Ujana mwingi, hakuwahi kuutaka uzee hata siku moja. Uvaaji wake na alivyo, ungesema ni kaka yao mkubwa. Alilipenda jiji na starehe zake kama zilivyo. Hakuwahi kutongoza msichana ilimradi awe msichana. Alisimamia vigezo vyake. Ni bora asilale na huyo msichana kama kwanza si mweupe, halafu asi
we amebeba maumbile aliyoyataka yeye.

Swala la kuzaa kila kona yeye kwake ilikuwa fahari. “Huwezi jua atakayekuja kukusitiri baadaye. Hivi vitoto viwili mnazaa kwenye ndoa, mnanyang’any’ana na magonjwa, kifo, na shetani. Ukipata mmoja jambazi mwingine mchoyo, ujue ndio basi tena. Au kakigongwa kamoja na gari kakafa ndio umebakiwa na jambazi au mchoyo. Sambaza mbegu.” Ndio ulikuwa usemi wake baa na kwa kila mtu aliyemfahamu.

Kwa Kina Mgini.

Pam akapelekwa nyumbani kwa Mgini. Mill hakumdanganya. Mzee alijijenga huyo! Jumba lilikuwa kama hekalu mpaka akashangaa ni kwa nini Mill akajibane kwenye kijumba kidogo vile hapo kwa Mike. Kulizungushwa uwa mkubwa na pia kulikuwa kama na nyumba nyingine ndogo kama tatu, nazo nzuri haswa ndani ya ua hiyohiyo.

Ilikuwa mida ya jioni. Giza halikuwa limeingia sawasawa. Alipendeza Pam. Alivaa moja ya gauni alilokuwa ameletewa na Mill. Refu mpaka chini ila limemshika vizuri kwa heshima.

Wakakaribishwa ndani sebuleni. Akashangazwa na kundi la vijana kama wapo uwanjani wanasubiria mpira. Akaanza kutetemeka. Ila akashangaa Mill anaanza kucheka kwa masikitiko. “Mashabiki nyinyi!” “Ni baba huyo! Kasema unaleta mchumba. Wote lazima tukae hapa. Tuone jinsi wewe ulivyo na akili sio sisi mafala.” “Hajasema tu hivyo. Kasema tuje tuige mfano.” “Kasisitiza lazima tuwepo na umesema hutaki ulevi.” “Hayo nimemwambia yeye ninayemletea mkwe.” Mill akawajibu wadogo zake waliokuwa wakishindania kumjibu kaka yao.

Pam akababaika, hajui baba ni yupi! Wote wasafi, halafu wapo kama vijana! Nyumba safi halafu na sebule yenyewe kubwa, kila kitu hapo ni cha thamani. “Shikamoo baba.” Aliyeitika akajua ndio mwenyewe. Halafu asilimia kubwa wote walikuwa na mwili mkubwa kama baba yao. Yaani warefu halafu wapana kama huyo Mill.

“Karibu mama. Hapa ni nyumbani. Na hawa wote si wageni na wala sijaona muondokaji hapa ila Mill tu. Wamejaa hapa, wanabadilisha miaka tu, hakuna anayetaka kutafuta kwake.” Wote wakacheka.

Pam akasogea kumsalimia na kumpa mkono. “Mbali na baba, anayempa mkono ni mama Kenny tu. Hakuna kuanza habari zenu za kihuni kwa mwanamke wangu.” “Sasa tutafahamianaje naye kwa karibu kama unamficha?” “Unataka kumfahamu kwa karibu ili iweje?” Mill akamuuliza kwa ukali kidogo.

“Sawa bro. Lakini sisi wote hapa tupo kwa ajili ya kukutana na shemeji.” “Sijawaita. Nimemleta kwa baba tu. Haya. Mshamuona, ondokeni bila ya…” “Mzuri aisee! Huyu kweli haaribu ukoo wa mzee.” “Hana mdogo wake wa kike?” Mwingine akadakia. “Mimi hata dada yake sina neno, bora awe amefanana naye hivyohivyo.” Pam akazidi kuona aibu, tena alikuwa amesimama na Mill katikati ya sebule.

“Kama kafanana na upande wa mama yake, hata mama yake mdogo mimi sina shida, naoa.” “Kama kachukua upande wa baba, mimi hata shangazi yake!” Mwingine tena akadakia. “Haya, ondokeni. Naona muda wenu wa kukaa hapa umeisha.” Wote wakasimama wakicheka mpaka baba yao.

“Bro anataka kuoa peke yake!” “Nyinyi si waoaji.” “Pam anipe mdogo wake halafu muone kama mimi sitaoa. Tena naoa kabla yako.” “Haya ondokeni.” Mzee akaweka msisitizo, wakaondoka wakilalamika.

“Karibu ukae mama. Mama mwenye nyumba atakuja muda si mrefu na yeye umsalimie.” “Asante baba.” Ndipo wakakaa. “Unaendeleaje? Mill aliniambia ulikuwa mgonjwa.” Pam akauliza kwa kujali. “Ni yale maradhi ya kunyimana raha. Usile hiki, usinywe kile, kama vile wanakukomoa!” “Unafuata mashariti lakini baba?” “Hata kidogo.” Wakasikia sauti ya mwanamke ikijibu.

“Baba!” “Hivi nilitaka kukutafuta ili uzungumze naye. Hanywi chai isiyo na sukari. Vyakula vyote alivyokatazwa, baba yako anakula. Bia zake ni vilevile. Hapo umemkuta sababu alijua ni wewe unakuja.” “Ndio umepata jukwaa, mama Kenny?” Akaingia huyo mama hapo sebuleni.

“Basi vile vyote alivyokatazwa hospitalini, ndivyo anavyovifanya. Na hapo ukitoa tu mguu wako, jua yupo nyuma yako. Anaenda baa. Akikuomba chakula anachokitaka yeye, ukampikia alichoshauriwa hospitalini, anakwambia ataenda kula baa. Hali nyumbani, anakwenda kula huko wasikojua anamshariti. Ukimwambia apime sukari kabla hajala, anakwambia ili iweje?” “Mnakaribia kunikera, ili niondoke humu ndani.” Akajibu mzee Mgini.

“Kwa nini unafanya hivyo baba?” Akalalamika Mill. “Nisikilize Mill. Huu ugonjwa hauna tiba. Kweli wewe unataka nife kifo cha mateso? Yaani nijinyime sasahivi kama ndio nitaishi milele?” “Lakini unaweza kuishi na huu ugonjwa kwa muda mrefu baba, bila matatizo!” “Hivi unajua tokea waniambie nina kisukari ni watu wangapi nishazika ambao walikuwa hawaumwi hata kidogo?” “Basi ndio usemi wake huo?” Mama Kenny akadaikia.

“Wote tutakufa. Hakuna atakayeishi hapa duniani milele. Mimi nimekataa kuishi kwa kujinyima. Nikijinyima kwa hili halafu nikatoka hapa nikagongwa na gari, nikafa kwa hiyo ajali je? Dawa unazonisisitiza kunywa kila wakati mpaka siwezi kupumua, nameza. Shida ni nini?” “Haziwezi kufanya kazi kama hufuati mashariti, baba! Kweli unataka uondoke uache vijana wako hawana muelekeo kama hivi?!”

“Unamuona kuna hata mmoja wao hapo mwenye muelekeo wa maisha? Yaani mimi nishindwe kufurahia maisha kwa ajili ya wajinga hao? Ni wewe, Kenny na Sheila ndio naona mna malengo ya baadaye, na ndio maana mnaona sizembei. Wengine wote ni kama hivyo. Kweli eti nyinyi mnataka nikae hapa kama mfungwa kwa ajili ya wapuuzi hao? Anayetaka kunitumia sasahivi, anitumie. Nikiondoka shauri yao. Pam mama, wazazi wako wapi?”

Pam akagutuka maana mzee alishaanza kugomba nyumba nzima. “Mama anaishi na wazazi wake huko Mlalo, Lushoto.” “Huko milimani haswa! Lakini tutaenda tu. Lazima akirudi Mill safari ingine, twende tukaone wazazi. Nijitambulishe na kulipa mahari kabisa. Wasije niwahi wahuni wengine wa hapa mjini, wakalipia vijana wao. Mill keshawahi, tunaenda kumalizana kabisa. Au unasemaje?” Pam akacheka kwa wasiwasi akimwangalia Mill aliyekuwa amenyamaza baada ya swala la ugonjwa.

“Eti Mill? Huyu si umesema unaoa kabisa?” “Kama utakuwa hai baba! Unamipango mingi wakati hutaki kuhakikisha inakukuta ukiwa hai!” “Kuwa na imani wewe!” “Imani bila matendo itasaidai nini baba? Tafadhali fuata mashariti.” “Sawa.” “Mmmh!” Mama Kenny akaguna.

“Naona muda wako wakukaa hapa sebuleni umekuishia, mama Kenny. Unataka kunikera tu bila sababu!” “Unamdanganya tu Mill. Akiondoka hapo, unarudia mambo yako kama kawaida. Usimdanganye.” “Sasa, safari hii namuahidi mimi mwenyewe. Acha kumtia wasiwasi usio na sababu! Umesikia Mill?” Mill akamwangalia akionyesha hana imani kabisa.

“Ukirudi tunakwenda wote Mlalo, kujitokeza na kutoa mahari kabisa.” “Naomba badili maisha baba! Taratibu. Nimeshakuletea aina nyingine ya sukari. Kwa nini hutumii?” “Anakula baa. Sukari zako zipo nyumbani. Atatumia saa ngapi?” Mama Kenny akajibu. Wakaanza kubishana yeye na mkewe hapo, Pam mgeni ametulia. Ila akagundua akizungumza Mill anamsikiliza.

“Kuna chakula Mill. Njoo ule na mgeni.” “Hicho chakula chako cha jumuiya mama Kenny, nakushukuru sana. Acha tukale mbele ya safari.” “Kweli unamleta mgeni hata maji asinywe!” “Atakunywa siku nyingine. Leo ilikuwa salamu tu. Tusikuharibie bajeti yako. Wewe kuwa na amani. Ikifika siku ya kula, tutakwambia. Leo tunapita tu. Sijamuona Sheila. Yupo?” “Amehamia chuo. Fujo za hapa amesema anashindwa kujisomea. Naona anataka kukuiga wewe.” Mill akacheka. “Bora achukue chake mapema.” Akasimama akijibu hivyo.

“Fuata masharti baba, tafadhali.” “Acha kumsikiliza mama Kenny! Ukirudi utanikuta.” “Nikukute mzima.” “Mill anapenda mambo ya wasiwasi! Maisha ni hayahaya, halafu bado unataka kuyaishi kwa kujifinyilia. Pam mama, karibu kwenye ukoo. Naona wewe hutaniharibia ukoo. Hatutaki mbegu za ajabuajabu sisi. Tunataka wazaliwe watoto wanao eleweka sio wakuwatetea kila wakati. Mara umtetee ni wa kike! Mara umtetee kafanana na bibi mzaa babu yake! Hatutaki fujo sisi! Mtoto kama ni wa kike, basi aonekanike ni wa kike na sura ya kike sio kama jambazi aliyeponea kuteketezwa kwa moto.” Pam akacheka akimtizama Mill.

“Nitakupigia kukuaga baba.”  “Hurudi tena?” “Kuna nini?” “Tutazungumza kesho. Lakini nataka tupate muda wa kuzungumza mimi na wewe kabla hujaondoka. Sio hapa.” “Na isiwe baa, tafadhali baba.” Akamuona anacheka. “Ndiko ulikotaka tukutanie?!” “Hapana wewe! Ni mazungumzo ya muhimu. Siwezi kuzungumzia baa. Vipi wewe?” “Basi tupange chakula cha mchana pamoja kesho.” Wakapanga na baba yake na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

“Mbona umekataa kula kwenu?” “Aaaah! Huwa namuhurumia sana mama Kenny. Yeye mwenyewe hana utulivu pale ndani. Fujo kama ile unayoiona pale. Kikipikwa chakula pale ni kama cha jumuia nzima. Sitaki kujiingiza kwenye mipango yake na kumtia shuguli zisizo na maana.” “Inamaana wote wale wanaishi pale?” “Wote kama unavyowaona vile. Na asilimia kubwa pale hawajasoma, au hawataki shule, wana kazi za kuwasaidia kuingiza pesa ya starehe, kuvaa vizuri kama vile ulivyowaona pale na kuendesha magari mazuri hapa mjini. Kula, kulala kwa mama Kenny.” Pam akanyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~

Mill aliondoka nchini kwa shida sana. Pam ni wale wasichana waliaji kwa kuagana na kumpokea mgeni. Alilia alipompokea Mill ikawa zaidi alipokuwa wakiagana. Ilibidi Mill kucheck in mizigo kwanza kisha kutoka nje kukaa naye mpaka mwisho. Yaani yeye alikuwa abiria wa mwisho kuingia kwenye ndege na mlango wa ndege kufungwa.

Mina&Andy

Kipindi hicho cha maandalizi ya harusi mama Ron akajitahidi kumficha Mina, kwa hiyo kuonana kwa wapenzi hao ikawa hadimu. Alipomaliza tu mitihani yake, akatulia ndani akiandaliwa mwezi mzima kwa harusi. Mama Ron hakutaka hata atoke nje. Mina akawa mwali haswa.

Siku mbili kabla ya harusi, Mina na ndugu baadhi walio chaguliwa na mama Ron, waliondoka jijini kuelekea nchini Kenya tayari kwa harusi. Walikuta wamechukuliwa upande mzima wa hoteli, nzuri tu. Wakapokea ukarimu kama waliotoa kwa wageni wa Andy nchini Tanzania.

“Nina hamu na Andy, mama! Acha nizungumze naye hata kidogo.” “Naomba tulia Mina. Una siku mbili tu! Utakabidhiwa huyo Andy mpaka kifo.” Mina akanyamaza lakini akiwa hajaridhika. Muda wote Ron ndiye aliyekuwa akiwasiliana na Andy kwa mipango na taratibu zote za hapo kabla na baada ya harusi watakapokuwa mapumzikoni. Mina aliandaliwa mwili kiswahili haswa! Kwa mwezi huo mmoja, ungependa kumtizama. Aliteleza na kuiva vizuri haswa.

~~~~~~~~~~~~~~

Usiku wa kuamkua siku ya harusi, Andy alimtumia ujumbe. ‘Ngumu kuamini kesho muda kama huu, utakuwa mikononi kwangu mpaka kifo chetu! Nakupenda Mina na nina kusubiri kwa hamu.’ Ilimgusa Mina, akabaki akirudia kusoma ule ujumbe akiwa amelala na mama yake. Akamuonyesha mama yake.

“Huyu kijana anakupenda Mina mwanangu. Naomba ukatulie mama. Tafadhali Mina.” “Nimebadilika mama. Nimetulia.” Mina akajibu na machozi. “Nimekuona. Ninachoongelea ni usije ukafika huko, ukazoelea huu upendo ukaanza kuhangaika.” Mina alipewa chumba cha peke yake na mama yake.

“Nimebadilika mama. Nitatulia.” Mina akasisitiza kwa kuumia akiona bado mama yake anawasiwasi naye. “Nakuombea iwe hivyo tu. Maana huwa mambo yanabadilika ukifika kwenye ndoa. Sasa usije ukafika huko, ukazoelea mambo ukamsahau huyu kijana. Hii yote ni pesa anamwaga kwa ajili yako tu. Naomba usije lisahau hilo.” Mina akanyamaza lakini akiumia moyoni akaona aondoke hapo, aende akatulie bafuni. Alikaa huko mpaka akajua akirudi atakuwa ameshalala. Na kweli alirudi akamkuta amelala, na yeye akapanda kitandani na kulala.

Siku Ya Harusi Ya Mina&Andy.

Mmoja wa ndugu aliyekuja naye Mina alikuwa ndiye anayempamba bibi harusi na wasimamizi. Waliamka mapema sana ili wasichelewe kanisani. Kufika saa nane mchana, kila mtu alikuwa tayari. Wakamuacha Mina na mama yake hapo chumbani wengine wakatoka kwenda kujimalizia huko vyumbani kwao tayari kwa kanisani.

Akaanza tena kwa Mina aliyekuwa ametulia kimya kwenye kochi akiogopa hata kumuongelesha tena mama yake asije akaanza tena na kumuharibia mudi ya siku hiyo.

 “Nia yangu ni nzuri Mina. Nataka ukawe makini huko. Zile tabia zako za kuchanganya wanaume walio marafiki, naomba ujichunge nazo Mina. Sio ufike huko akakutambulishe kwa marafiki zake halafu ukaanza kuwachanganya.” Mina alilia sana.

Ikawa kama siku huyo mama Ron amekumbuka mabaya yote ya Mina. Alihakikisha anamkumbusha uchafu wote huku akimuonya asije akarudia. Mina alishindwa hata kumjibu maana alionekana kama anajazba. Akanyanyuka kwenda chooni huku mama yake akiendelea kuongea. Akamtumia ujumbe Ron, nakuomba afike hapo.

Ron akafika hapo chumbani kwao kwa haraka. “Mina yuko wapi?” Akamuuliza mama yake aliyemfungulia mlango. “Ananidharau! Mimi namuhusia, ananiacha na kwenda kujifungia chooni, ananiacha nikiwa nazungumza!” “Kwani kuna nini tena?!” “Namwambia akatulie huko atakapoolewa. Ona hii pesa anayotumia Andy kwa ajili yake! Sasa sitaki akaanze ile michezo yake. Akaingia kwenye ndoa na kuanza kuchanganya hata na marafiki wa mwenzie. Akaanza kutuingiza tena aibu kwa ndugu wote waliojua leo anaolewa. Nikabaki kicheko tena.” Ron akaumia sana.

“Mama! Kwa nini imani yako inakosa matendo mama yangu?! Huyu Mina ametuonyesha kwa vitendo amebadilika. Ulitaka afanyaje?” “Mimi namuonya tu Ron.” “Usiendelee kuzungumza naye kama Mina wa nyuma! Mina uliyekuwa ukimuomba Mungu ambadilishe, Mungu ametujibu.”

“Amesema mwenyewe, hatakumbuka dhambi zake tena. Ameziweka mbali kama mashariki na magharibi ilivyo mbali! Amemuita Mina ni mbarikiwa. Sasa kwa nini unamzungumzia Mina wa zamani kwa Mina huyu ambaye hata Andy ametuhakikishia hata kwake amekuwa mgumu?”

“Kwa nini hutaki kutunza muujiza wako? Kwa nini unashindwa kuishi na Mina huyu aliyebadilika, na wewe ukakubali muujiza wako? Ulitaka nini kitokee ili uamini tena? Mina AMEBADILIKA mama. Na Andy ametuomba tuishi na Mina huyu si wa zamani! Kweli wewe unataka ukampotezee mtoto wako kwa Andy! Kwamba akiondoka, asirudi tena kwako?” Kimya.

“Nikuombe kitu mama yangu. Tafadhali mwache atulie ili ile garama uliyosema Andy amelipia kutufikisha hapa leo, ilete maana. Kama sisi tumeshindwa kuishi na Mina huyu, basi acha tumsaidie kumfikisha kanisani kwa Andy, akaishi naye. Tafadhali mama yangu. Naomba tuwaache wenyewe.”

“Mwache Mina atulie, afike kwa mwenzie akiwa ametulia. Tusiharibu siku ya leo.” Mama yake akatoka hapo chumbani kwa hasira. Wasiwasi ukabaki kwa Ron kama harusi bado ipo kwa Mina au amegairi.

~~~~~~~~~~~~~~

Nabii Hana heshima nyumbani kwao.

 Mama alishang’atwa na nyoka, ngumu kuamini kama majani yakitikisika ni upepo tu.

Walifanikiwa kuwakwepa kina Ruhinda, safari hii ni mama mzazi.

Harusi ipo?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment