Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 15. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 15.

Jumatatu hiyo ya Mina kufuatwa na mama Ruhinda na kuondoka chuoni, kaka yake kwenda kumsaka, hakuchelewa kurudi ofisini. Baada ya kama dakika 45 akarudi. Akagonga. “Nimerudi Kiongozi. Baada ya muda mfupi tu nitakuwa nimekamilisha.” “Vipi Mina?”  Andy akauliza. Ron akaingia na kufunga mlango. “Atakuwa sawa. Tumeona kwa leo arudi tu nyumbani, akapumzike. Kesho ndio aje shule. Atakuwa sawa.” “Samahani sana Ron.” Andy akasimama.

“Nimeshazungumza na wazazi, wameelewa. Hakuna atakaye msumbua tena. Hata mimi ninaondoka kabisa hapa nchini.” Ron akashangaa sana. “Kwa nini!?” “Sitaki kumuharibia Mina. Amenieleza maisha yake, na jinsi mama alivyonieleza, naona ni heri nimuache tu. Mimi nimesoma Ron. Naweza kupata kazi popote kwa mshahara wowote. Nipo hapa nchini kwa ajili ya undugu tu. Tanzania sio nyumbani kama ilivyo Nairobi.” Andy akaegemea meza, Ron akiwa amesimama anamsikiliza.

“Nikirudi Nairobi nitaweza kupata kazi na kuishi vizuri tu.” “Sasa unaacha kazi hapa, umeshapata kazi kule?” Ron akauliza akisikika kujali. “Kule ni nyumbani Ron. Nina familia inayonielewa na inayoendana na mimi, sio kama hawa kina Ruhinda. Wale Mapadri ndio wamenilea mimi tokea mdogo sana. Katika uzima na maradhi, wamekuwa na mimi. Nina baba kule, zaidi ya huyu mzee Ruhinda. Ni baba kweli kweli kama alivyo mama Ron kwako.” Wakacheka.

“Kwa hiyo ninaposema ninarudi Nairobi, ujue narudi nyumbani kwa watu tunaozungumza lugha moja na kuelewana.”

“Nafikiria kukupendekeza wewe kwenye hii nafasi. Nafikiri utaweza Ron. Unafanya vizuri sana.” Ron akavuta kiti na kukaa. “Mimi huwa napatwa na kigugumizi linapofika swala la mapenzi.” Akaanza Ron. “Kidogo kama lina nichanganya vile! Sijui kwa kuwa nazungukwa na mifano ya ajabu ajabu ya watu wanaosema wanapenda au tulikuwa tukipenda!” Andy akarudi kukaa.

“Unajua niliishi na baba na mama. Wale watu sio kwa maneno. Hata kwa vitendo ungejua ni watu waliokuwa wakielewana. Walikuwa wakianza kucheka kwenye mazungumzo yao ambayo hayakuwa yakiisha, utajua ni watu wanao elewana. Stori za chuoni na kazini pia zilikuwa haziishi. Maana wote walikuwa wakifundisha shule moja kama mama alivyokwambia.”

“Hapakuwa na ugomvi, labda kule kupishana kwa kawaida tu. Sasa baba alivyoanza fujo zake za dini, hakika ungemuonea huruma, Andy. Yaani yeye mwenyewe dini ilionekana kama imekuwa mzigo kwake! Ile furaha ikamuisha kabisa. Ikawa fujo tu. Mara msikie ameoa huku. Haya, mkitulia mwezi hauishi, mnamuona amerudi nyumbani kama mgonjwa. Baada ya muda tena mnaona anakuja kufuatwa na dada yake. Anatolewa pale nyumbani, anakwenda kuozeshwa kwengine! Kama mjinga vile!”

“Nakumbuka kwenye kikao cha mwisho cha ndugu zake pamoja na mama. Mimi nilikuwepo. Mama alitaka Mina aende akasubirie kwa jirani. Wakati huo tulikuwa hatuishi pale Tegeta.” Ron akaendelea kama anayezungumza kwa kuvuta kumbukumbu.

“Nakumbuka kumwangalia baba na mama kwenye kile kikao. Wazi baba alionekana hakubaliani na ndugu zake kwa kile wanachomwambia mama. Lakini hakuongea sana zaidi yakusema watoto ni wa mama, aachiwe kuamua kufanya kile anachotaka na sisi. Basi. Wakamtisha mama, wakondoka na baba.”

“Siku baba anakuja kuomba talaka, nakumbuka baba kuzungumza maneno kama yale aliyozungumza mama. Juu ya sijui nyota yake na mwanamke aliyeoa. Lakini hakuwa hata na ujasiri na kile alichokuwa akikizungumza kwa mama! Na chakushangaza, alilala pale nyumbani siku hiyo. Alilala kama aliyekuwa amechoka haswa, alikuja kuamka saa nne asubuhi. Akasema hajalala usingizi wa namna hiyo kwa muda mrefu sana. Akaja kuondoka tena jioni yake. Hakurudi tena pale.”

“Sasa nakumbuka na wewe ulikuja pale nyumbani kwa staili hiyo hiyo. Ulizungumza na mimi. Ukajieleza kwa kina. Nikakuhoji maswali. Sijui kama unakumbuka siku ile uliponiita pale Surrender?” Andy kimya.

“Wasiwasi wangu juu yako na Mina ilikuwa ni sababu ya vile ninavyokufahamu Andy. Nikakuuliza kama kweli unamaanisha kwa Mina? Nikajaribu kukumbusha anapoishi Mina na watu tunao mzunguka. Maana nimeona hata ongea yako. Kula yako. Tabia zako. Jinsi unavyojibeba. Nilijua wazi mnatoka kwenye dunia mbili tofauti!”

“Ndio maana uliniona siku ile nikashangaa sana kuwa unawezaje kumuacha msichana kama Lora, kwa ajili ya mtu kama Mina! Tena nikakuonya kabisa, usimuache Lora kwa ajili ya Mina. Nikijua unafanya kosa. Lakini ukaeleza hoja zako kwa makini sana. Lakini lililokuwa kubwa ambalo mpaka sasa linasikika masikioni kwangu ni mapenzi.” “Kweli ni mapenzi.” Akaongeza Andy.

“Sasa hapo ndipo ninapochanganyikiwa Andy! Maana unaongea kama mama. Hivyo hivyo. Kuwa yeye na baba walipendana sana. Si na wewe ulimsikia?”  Andy kimya. “Changamoto alizokutana nazo baba, ni kama hazitofautiani sana na wewe! Yeye aliondoka akionekana kabisa hana furaha, ameenda kuoa. Ukimuona, huwezi kumlinganisha na sisi kabisa. Ni yule muislamu, ambaye huwezi kudhani hata alishawahi kumtongoza mkristo! Ana mke wake na watoto. Lakini nilikaa naye kwa muda mfupi tu, sikumuona yule baba niliyekuwa nikimfahamu mimi. Sijui kama unanielewa?”

“Kimaendeleo anaonekana amepiga hatua kubwa sana tofauti na vile alivyokuwa na sisi. Alikuja kuwa mwalimu mkuu wa shule ya sekondari. Nafikiri alirudi chuo au sijui, lakini akahamishwa akawa Afisa elimu hukohuko Mkuranga. Analo gari na ana nyumba yeye na mkewe. Wapo tu vizuri. Lakini ukimwangalia, ni kama hayupo pale kwenye yale mafanikio.” Ron akajisogeza tena.

“Hivi ni muda gani umepita tokea ufike pale nyumbani uzungumze juu ya upendo wako kwa Mina?”  Ron akamuuliza Andy bosi wake. Andy Kimya. “Sidhani hata kama miezi mitatu imefika. Kwa hakika hata hamjatimiza miwili. Au nimekosea?” Kimya. “Leo tumekaa mimi na wewe tena. Nashuhudia ukifanya kama kile alichokifanya baba yangu! Unakimbia kama yeye!”

“Kwa uhakika kabisa, utapata kazi nzuri. Mshahara mzuri. Unarudi nyumbani, huna tofauti na baba yangu! Alifanya kama wewe! Hatua kwa hatua, hivyo hivyo! Mpaka natilia mashaka hata ile waliyosema walimloga baba na Mina! Wewe unanifanya nitilie mashaka. Maana wewe huonekaniki kama wazazi wako na ndugu zako wamekuloga! Lakini unafanya kama baba yangu tu! Sasa najiuliza, hivi haya mapenzi watu wanayosemaga yapo, yanakuwepo kweli au nihisia tu za muda!” “Yapo Ron.” “Sasa huwa mnashindwa wapi!?” Akauliza Ron kwa kushangaa sana.

“Eti Andy? Huwa mnashindwa wapi? Maana kama nikimwangalia baba yangu, mpaka niliacha kwenda kumsalimia. Amezeeka kuliko mama na wakati nafikiri umri wanalingana na mama! Mama anaonekana anaaghueni ya maisha kuliko hata baba ambaye ni Afisa elimu! Mama anazidi kuwa kijana, na maisha yake yanaendelea, lakini yeye aliyekimbia, haonekaniki kufurahia hata!”

 “Nikikuonyesha baba yangu, utasema alitakiwa kustaafu. Amechoka, utamuhurumia. Ukifika tu, anataka kujua habari za mama, anavyo endelea! Kama anakula vizuri. Kama anafuraha. Maisha yake yakoje, hana hata habari na sisi ila kutaka habari za mama tu! Sasa mimi najiuliza, kama anampenda kiasi hicho, ni kwa nini hakupambana hata kidogo kutunza anachokipenda!”

“Dini yake yenyewe aliyokimbilia, haionekaniki hata kumpa furaha. Anaswali swala tano. Lakini huwezi ona ni wapi anafuraha. Akienda na kutoka kuswali yupo vilevile. Sasa unajiuliza, amekimbia nini na amepata nini! Watoto ambao amepata, ambao anawaongoza kwa njia anazopenda yeye na ndugu zake, ukiwaangalia, bora sisi.”

“Wakwanza kule kwa mke wake huyo wa dini yake, ni wakike. Anavaa kama vile walivyotaka Mina avae. Lakini hata kabla hajamaliza darasa la saba, alishazaa. Sidhani hata kama walitofautiana sana tabia na Mina wa zamani. Tabia zao nilikuwa nikizilinganisha tu. Na yeye umbile ni kama Mina. Wote wamefanana na huyo bibi wa Unguja, sema bibi amezeeka sana ndio maana ni rahisi kuwafananisha na shangazi.”

“Haya, huyo wapili ambaye ni wakiume, walimpeleka kwenye shule ile waliyotaka mimi nipelekwe, yule kijana alikataa shule mapema sana, sidhani hata kama alikwenda sekondari. Yupo tu nyumbani. Halafu ndio wana binti mwingine mdogo tu. Ukiangalia unajiuliza, hivi huyu baba mwenye familia hizi mbili, ameshindwa wapi? Huku hayupo na kule kwenyewe alipokimbilia pia aliyokimbilia hayatoi matunda ya maana!” Kimya.

“Sijui bwana! Ila nikushukuru kwa kunifikiria kwenye hii nafasi. Asante sana. Na ninakuahidi nitafanya vizuri. Sitakuangusha.” Ron akatoka, nakumuacha Andy amepoa kimya. Andy alirudi kukaa kwenye meza yake. Akafuta kabisa ile barua aliyokuwa ameandika kwenye kompyuta yake, yakuacha kazi. Akabaki akifikiria chakufanya.

Atafutaye Hachoki.

Ijumaa usiku wakiwa wamekaa tu nyumbani kwao, kama saa mbili na nusu hivi, wakashangaa hodi mlangoni. Ron akasimama kufungua mlango. Alikuwa Andy. Ron akashituka kidogo. “Karibu Kiongozi!” Mina na mama yake wakakaa sawa pale ndani. “Asante.” “Karibu baba. Naona wewe si mkulima.” Wakacheka. “Kwa nini mama? Au ndio mmemaliza kula nini?” “Muda si mrefu.” Andy akakaa. “Hamna hata masalio?” Akauliza Andy huku akicheka. “Pole. Tumekaa kihasara hapa, hakuna aliyepika. Na msomi wetu naye ametuambia amechoka, alikuwa na mitihani leo. Imebidi kumaliza kiporo cha jana.” Andy akamwangalia Mina.

“Pole na mitihani.” “Asante.” Mina akajibu. “Ulionaje?” “Sio mbaya, uzuri mwalimu alitutolea mambo yale yale aliyotufundisha. Kwa hiyo nimefanya.” “Mwambie juu ya ile website.” Mama yake akamwambia Mina. Mina akainama. “Ni nini Mina?” Andy akauliza kwa kumbembeleza. “Sio kitu. Mama naye!”  Mina akajibu huku akicheka kwa wasiwasi.

“Nataka kujua na mimi.” “Hata sio kitu cha maana Andy. Tulipewa kazi yakutengeneza website ya mtu. Sisi wote pale darasani. Mwalimu akasema atakayeitoa vizuri, itakuwa moja ya maksi za mtihani wa mwisho, na pia huyo mtu akilipa hiyo hela ya website yake, mwanafunzi atakayeshinda, atalipwa nusu ya hiyo pesa.” Mina akacheka kwa aibu.

“Kwa hiyo wewe umeshinda?” Andy akauliza, Mina akacheka huku akitingisha kichwa kukubali. “Safi sana. Hongera. Nikirudi kutoka safari nitakuletea zawadi.” Mina akakunja uso. “Unasafiri Andy?” “Naondoka na ndege ya kesho asubuhi. Mambo yote yakienda sawa, nitarudi jumanne au jumatano.” Mina akabadilika usoni. “Sasa mbona hujaniambia?” Akalalamika Mina, kama sio yeye aliyesema aachwe. “Ndio maana nipo hapa Mina. Nimekuja kukuaga. Safari imekuwa ya ghafla. Sijui kama nilikwambia mama.” Akamgeukia mama Ron.

“Nililelewa na mapadri, huko Nairobi. Sasa mmoja wa mlezi wangu. Ni kama baba yangu kabisa, anaishi huko. Miaka miwili iliyopita, alipata uaskofu. Ndiye nakwenda kumuona. Nilipanga kwenda na Mina weekend ile inayofuata. Ili akamuone. Alitamani sana kumuona Mina. Lakini ameitwa na uongozi huko Italy. Weekend hiyo niliyopanga kwenda na Mina, hatakuwepo. Sasa kwa kuwa anasafiri, na ni ghafla, nimeona niende tu nikazungumze naye kabla yakuondoka.” Mina akainama.

“Sitakaa sana, nitarudi.” Akaongeza Andy, Ron akajua ameamua kubaki. “Tunashukuru kwa kuja kutuaga Andy. Uwe na safari njema.” “Asante mama.” Andy akabaki akimwangalia Mina, Mina na yeye akamwangalia. “Kweli hujala?” Mina akauliza. “Sasa swali gani hilo? Wewe mwambie asubirie chakula ukapike mara moja kwenye gesi.” Mina akacheka. “Utasubiria?” Mina akauliza huku anacheka na kusimama. “Mara moja tu, utakula.” “Basi twende nikusaidie hata kukata nyanya.’’ “Ila ujue ni ugali tu na mchicha.” “Nitakula huo huo, twende.” Wakaongozana mpaka jiko la ndani.

~~~~~~~~~~~~~~

“Tokea lini kitu unachosoma umeanza kukiona sio chamaana?” Wakamsikia Andy akimuuliza. Mina hakujibu. “Au tokea ukutane na kina Ruhinda?” Mina hakujibu. “Niangalie mimi, Mina. Njoo kwanza.” Wakawa wanawasikia. “Najua familia ina nguvu, lakini si kwa Ruhinda kwangu au kwetu. Nina familia nyingine ambayo wamenilea mimi na wanaheshimu maamuzi yangu. Hiyo ndiyo nitakupeleka kukutambulisha. Najua watakupenda na kukuheshimu.” “Unajuaje Andy?” Wakamsikia Mina akiuliza.

“Kwa kuwa ndio wamenilea hivi. Mtazamo nilio nao mimi ndio wao. Hivi ninavyotazama mambo na watu ndivyo wao walivyonifundisha. Nimekuzwa hivi na wao. Huyo askofu ambaye ni kama baba yangu, nilimgusia tu juu yako, akataka nikupeleke. Kwa hiyo najua ni nini ninashozungumzia.” Mina akanyamaza.

“Halafu Mina, kuhusu hii familia ya hapa, naweza kuwa siku ile sikusema kitu lakini Mina, nakuhakikishia, haitakaa ikatokea tena. Nimeshazungumza nao na nimeweka mipaka juu yetu.” “Juu yetu!? Unamaanisha nini?” Mina akauliza taratibu.

“Nakuhakikishia hawatatuingilia tena. Kile tunachofanya na kuamini, ni mimi na wewe tu. Cha msingi ni mimi na wewe tupange na kuelewana. Hata ukiona lipo jambo ambalo hujalielewa na kulipenda, tafadhali niulize, sawa?” “Siku ile nilichukia Andy, walinidhalilisha na kunicheka waziwazi!” “Sio wewe tu! Kukudhalilisha wewe ndio mimi. Hawakufanya vizuri, naomba unisamehe mpenzi wangu.” “Nimefurahi umerudi Andy. Nilikuwa na hamu na wewe!” Andy akacheka.

“Mbona hukunitafuta sasa?” “Nilijua na wewe unanifikiria kama ndugu zako! Au utaanza kunidharau.” “Nakupenda Mina. Na mimi nilikwambia. Sipo kwenye maisha yako, kujaribu. Na ndio maana mimi nakutambulisha kila mahali. Sina chakujificha, najivunia vile ulivyo. Naamini mambo mengine kama wapi tunakwenda kuabudu siku ya jumapili, hayo ni mambo yamakubaliano tu. Lakini hayawezi kutufanya tushindwe kuwa pamoja.” “Wewe ni mtu mzuri Andy.” Mina akamwambia kwa upendo.

          Kila mtu akacheka. Mina akasikia. “Bwana mama! Sasa mnasikiliza nini?”  Andy akaendelea kucheka. “Sasa mimi sikuwa na njaa. Nilitaka tu kupata muda na wewe. Maadamu umenisamehe, acha nikajiandae na safari.” Mina akacheka. “Kwa hiyo sasa hivi utanipigia?” Mina akauliza kwa deko. “Nitakupigia kesho asubuhi kabla sijaondoka na...” “Ukifika. Ili nijue kama ulifika salama. Halafu jumatatu urudi.” Andy akacheka. “Ukitaka nirudi jumatatu nitajitahidi kurudi.” “Nataka.” Mina akaweka msisitizo.

“Basi nitarudi jumatatu. Mungu akipenda jioni nitakuja kukuchukua shule.” “Week ijayo ndio mwisho wa shule.” “Hongera sana.” “Asante. Sasa hivi tumeongea ndio nimeona nimefanya jambo la maana.” “Sana. Na usikubali mtu akwambie vinginevyo. Ingekuwa rahisi si kila mtu angejua unachofanya! Mimi mwenyewe sijui kutengeneza website japo nina shahada mbili! Hata ukinipa kompyuta na milioni tano ukaniambia nitengeneze, sitaweza kwa kuwa sio kitu nilichosomea. Na watu wanaishi kwa hiyo kazi tu. Ila sema kwa ajili ya ushindani au kujua zaidi, ndipo watu wanajiendeleza zaidi kwenye mambo hayohayo. Zipo mpaka shahada zake! Na nikwambie ukweli tu Mina, nchi nyingine kompyuta designing zinalipa sana. Na ndio ajira ambazo watu wanalipwa pesa nyingi kulinganisha na hata hiki ninachokifanya.”

“Kweli Andy?” “Kabisa. Mambo yanabadilika. Kila kitu ni kwenye kompyuta. Sio mahospitalini sio kwenye mabenki. Kila mahali ni kompyuta. Wewe utakuja kuona. Kazana tu kuongeza ujuzi. Ili uwepo kwenye nafasi ya juu, utaona. Tutakuja kuzungumza na kupanga zaidi. Si bado unapapenda IFM?” Mina akatingisha kichwa kukubali.

 “Basi tutapanga zaidi.” Wakatoka hapo jikoni kurudi Sebuleni. “Naomba niwaage.” “Naona umeongeleshwa, hata maji ya kunywa hujapewa!” “Mama! Andy hana njaa! Alikuja tu kuniona.” Mina aliongea na cheko, wakacheka.

“Haya baba. Uwe na safari njema.” “Asante. Ron!” Ron akamwangalia. “Niambie kiongozi.” “Tutaonana.” “Asante. Karibu sana.” Andy akatoka na Mina akiwa amemshika mkono.

Alichofanya nikufungua mlango wa dereva, Mina akapanda, yakaanza mabusu. Andy akiwa amesimama nje ya gari katikati ya mapaja ya Mina akiwa amekaa akiaangalia nje. Andy aliendelea kumkumbatia kwa nguvu huku akimvutia kwake.

“Naomba kuachana iwe kitu cha mwisho kabisa Mina. Iwe ni pale tutakapoona hakuna suluhi nyingine.” “Mimi mwenyewe sitaki tuachane Andy. Wewe nakupenda kiukweli.” Andy alifurahi huyo, nakushukuru Mungu kuzungumza na Ron. Angekimbia mapenzi matamu ya Mina. Akarudi haraka kwenye midomo yake.

“Nakupenda Andy. Nilikuwa na hamu na wewe!” “Hata mimi. Tutapata muda wakutosha nitakaporudi. Tulale pale kwenye kochi, nikukumbatie vizuri wakati nikinyonya hiyo midomo yako.” Mina akacheka na kufunika uso. Andy akajiweka uso kifuani kwa Mina. Katikati. Mina akamkumbatia kichwani nakujilaza, Andy akapitisha mikono nyuma yake akamkumbatia vizuri. Wakatulia kwa muda.

Alitulia Andy kapo katikati ya matiti hayo kama aliyelala, Mina akiwa amemlalia kichwani huku vidole vyake vikimpapasa nyuma ya shingo.

“Utanifanya nilale hapa kifuani kwako!” Mina akacheka. Akambusu mara kadhaa hapo katikati ya kifua. Akasimama akihema huku akimwangalia Mina. Akacheka na kuinama mbele ya Mina. “Acha mimi niondoke, kabla sijashindwa kuondoka kabisa.” Mina akacheka taratibu na kushuka garini.

“Jumatatu umeniahidi utakuja kunichukua shule.” “Mbona na kulala kifuani hukumbushii?” Mina akacheka sana. Akambusu tena. “Eti Mina?” “Utalala mpaka uchoke.” “Nisipochoka?” Mina akazidi kucheka.

“Kesho sitakuwepo. Hii ni pesa ya kununua vyakula vya hapa nyumbani na matumizi mpaka nikirudi.” “Huna haja yakufanya hivyo Andy. Sisi tupo sawa tu.” Andy akakunja uso. “Ni wewe unaongea au ni kina Ruhinda kupitia mdomo wako?” Mina akanyamaza.

“Eti Mina?” “Ni kwa sababu naona kuna kila kitu ndani!” “Nimetoka kuzungumza nini na wewe pale jikoni?” “Kwamba ni mimi na wewe ndio tutapanga mambo yetu.” “Na ndivyo tulivyokuwa mpaka nilipokupeleka kwa kina Ruhinda! Ndipo umeanza kutilia mashaka mapenzi yangu, na kunitilia mashaka mimi mwenyewe kwenye kila kitu kwako. Na sasa unaanza kubadili utaratibu wetu.” Mina akanyamaza.

“Jumamosi ilikuwa siku yetu yakununua vyakula vya nyumbani. Ni nini kimebadilika?” “Hamna Andy. Ila nimeona unasafiri. Utahitaji pesa zaidi.” “Siwezi nikawa na amani kule kama huku sijakuacha vizuri.” “Mimi nipo sawa Andy, usiwe na wasiwasi.” “Wewe unamtegemea Ron na mama. Unajuaje walivyo kwa sasa kipesa? Yaani unajulikana upo na mimi, halafu hata pesa ya vitu vidogo vidogo unataka umuombe mama! Sasa kuna kuwa na faida gani ya mimi kuwepo kwenye maisha yako? Kama ningekuwa sina kazi, hapo sawa. Lakini nina kazi na uwezo. Naomba wakati unaishi hapa nyumbani, mahitaji yako yawe juu yangu mpaka tutakapoanza kuishi wote. Ni sawa?” Mina akajisikia vizuri.

“Asante Andy.” “Tafadhali usianze kuzungumza lugha za watu wengine, na siku nyingine huna haja yakujieleza kwa yeyote yule jinsi ya sisi tunavyoishi. Zaidi wanapokuuliza juu yetu. Haimuhusu mtu, labda upende mwenyewe. Lakini si kama walivyokuwa wakikuhoji siku ile. Huwajibiki kwa yeyote isipokuwa mimi. Sawa?” “Sawa.” Mina akakubali na tabasamu la aibu usoni huku akipokea zile pesa. “Asante Andy.” “Karibu.” Andy akaondoka. Mina akarudi ndani na cheko.

~~~~~~~~~~~~~~

“Muone! Si ulisema humtaki tena wewe!” Mama yake akamtania. “Namtaka Andy lakini sio wale ndugu zake.” Wakacheka. “Na maneno yote yale niliyompa siku ile, sikutegemea kama atakuja kurudi huyu kijana! Anaonekana anakupenda.” “Mimi mwenyewe nampenda.” Wakacheka, Ron kimya.

 Andy.

Andy akiwa anaelekea uwanja wa ndege alimpigia simu asubuhi kama alivyoahidi, wakazungumza wakikumbushana wanavyo pendana. “Urudi Andy, ujue nakusubiri.” Andy akalifurahia sana hilo. Kutoka kujisikia familia yake haimuhitaji, leo mrembo Mina, toto zuri anamwambia anamuhitaji! Ikamuongezea faraja ya ajabu. Kuwa na yeye anahitajiaka!

“Nitarudi kwa ajili yako Mina.” Akamsikia Mina akicheka kwa furaha. “Nakupenda Mina. Nakupenda sana.” “Ukirudi nitakuonyesha jinsi ninavyokupenda na kukuhitaji Andy.” Wakazungumza mpaka Andy akafika uwanja wa ndege, akamsubiria mpaka akapanda ndege ndipo wakaagana.

Na alipotua tu uwanja wa ndege wa Nairobi akampigia tena simu kumtaarifu kuwa amefika salama na amepokelewa. “Uwe na wakati mzuri, Andy.” “Asante na wewe Mina, wangu.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~

Jumamosi usiku Ron akapata simu kutoka kwa Andy. “Najua itakuwa nimewataarifu muda mfupi, lakini alitaka kuja kuwaona kabla hajasafiri.” “Sidhani kama kutakuwa na tatizo. Nitazungumza na mama, kisha nitakutaarifu. Lini?” “Kesho ingekuwa nzuri, lakini ana misa mpaka jioni. Naomba iwe jumatatu tafadhali.” “Basi nitazungumza na mama, kisha nitakujulisha.” Ron akaonekana kutoa ushirikiano.

“Nashukuru sana Ron, asante kwa kila kitu.” “Karibu. Mnategemea kuwa wangapi?” Andy akakadiria. “Lakini Ron, tafadhali msihangaike sana. Lengo kubwa ni kutaka kukutana na nyinyi na mfahamiane.” “Sawa.” Wakapanga, wakaishia kukubaliana wao wawili, wakahitimisha kila kitu.

Ukisema Cha nini!

Mama Ron alijawa furaha hata hakujali udhia wa muda. Aliomba rafiki zake wakaribu wafike hapo nyumbani siku ya jumatatu, wakamsaidia kupika na kuandaa hapo tayari kwa wageni. Ilipofika saa 11 jioni Andy akawa anawasili na wageni wake wanne. Macho yaliwatoka na kuongeza utisho wa namna yake pale walipoona ni mapadri wenye sare za kipadri na askofu mwenye kofia ile ndogo siyo ya misa pamoja na joho lake.

Heshima ikaongezeka zaidi. Na hata mama Ron akajisikia vizuri mbele ya wenzie. Ni Mina. Mtoto aliyesumba jamii. Anajulikana kama mtoto aliyeshindikana. Leo ameleta watu wa heshima wa kiasi hicho! Angalau mama Ron akaanza kufutwa machozi kwa namna yake.

Walikaribishwa ndani, yakaanza mazungumzo. Hali ya hofu ikaanza kupungua kwani wakaanza kusikika ni watu wa kawaida, waliojaa unyenyekevu wa kiutumishi. Walikarimiwa vizuri na kwa heshima. Wote wakaonekana kumfahamu vizuri Andy.

“Andy ni mtoto niliyemlea mimi mwenyewe tokea mdogo kabisa.” Akaanza huyo askofu. “Anao udhaifu ambao inabidi Mina uufahamu ili uweze kumuelewa na kumchukulia.” Wote wakatulia kumsikiliza. “Akikasirika au akiingiwa hofu, huwa hawezi kabisa kuongea.” Hapo hata wale mapdri walianza kucheka na Andy mwenyewe kwa kuwa hawakuwa wakijua ni nini askofu wao anataka kuzungumza.

“Wakati ni mdogo tu. Waliletwa kwangu kuwa wamevunja kioo cha mlango wa kanisa dogo la mapadri. Nikawachapa wote na kuwapa adhabu. Hiyo ikaisha. Siku nyingine kabisa alipokuwa akisafisha ofisini kwangu kwenye mazungumzo yakawaida tu, ndipo akaniambia hakuwepo katika kundi la wale watoto waliokuwa wakicheza na kuvunja kioo.”

“Nilishangaa lakini sikumwambia. Ndipo ikabidi sasa kufuatilia kwa yule aliyekuwa amewaleta kwangu. Akaniambia yeye aliwakusanya tu wote waliokuwa karibu na tukio siku ile, na kuwaleta kwangu. Ndipo ikabidi sasa kuwa naye karibu na kumchunguza zaidi. Ndipo nilipo gundua huo udhaifu kwake.”

“Unaweza kumchapa mpaka ukachoka, akiona umetulia kabisa. Siku nyingine, ndipo anaweza hata kuzungumza na wewe akajieleza na ukamuelewa. Kwa hiyo ni kitu nilitaka na nyinyi mkifahamu juu ya Andy.” Wakapata jibu la kwa nini siku alipompeleka Mina kwa kina Ruhinda hakuzungumza. Ikawa kama anamjibia Andy.

Akaendelea huyo aliyekuwa baba wa Andy. Askofu. “Kitu kingine ambacho Mina awe na uhakika nacho, Andy anapoamua kufanya jambo. Au anapokwambia ‘Ndiyo’ kwa jambo fulani, ujue atalisimamia na kulilinda kwa gharama yeyote ile labda hilo jambo limfie, kwamba haliwezekaniki tena na yeyote.” Akaendelea.

“Mimi ni mpenzi sana wa maua. Sasa nilipokuwa nikisafiri, mtu niliyekuwa nikimwachia maua yangu ya ofisini. Ndani na nje, alikuwa Andy. Kwa kuwa nilikuwa ninauhakika nitayakuta salama. Mtu hupimwa kwa vitu vidogo. Katika hilo tu, nikajua nikisafiri nani nimuache katika lipi, lakini Andy katika yale mambo yaliyohitaji umakinifu na uendelevu bila kukosa.”

“Padri Antoni ni pacha wa nje wa Andy. Walijiita hivyo tokea wapo wadogo, wamekua pamoja tokea siku ya kwanza wazazi wao wanawaacha pale shuleni. Isipokuwa mwenzake aliamua kuingia kwenye upadri. Anamfahamu Andy ndani na nje, na ndio maana na yeye alitamani kuja kuona familia ya Mina. Tunashukuru sana kutupokea na kutukarimu.” Yule askofu akashukuru kwa heshima wakapeana mikono.

“Sasa Andy ameniambia anataka kuoa karibuni ila Mina anasoma.” Mina akacheka na kuinama. “Kwa heshima yako mama, tunaomba tu baraka zako ili tulikamilishe hili na ninakuahidi Mina ataendelea kusoma tu hata akisha kuolewa na Andy. Ukikubali hili, basi tutarudi kutoa mahari baada yakujua taratibu zote.” Mama Ron hakutegemea swala la ndoa kwa Mina tena kwa haraka vile! Asijue mwenzie huwa anaonjeshwa asali, ndio anataka kujenga mzinga kabisa! Ndio haraka zote hizo. Akababaika kidogo maana wote walikuwa wakisubiria jibu, lakini mwalimu akachangamka. “Nashukuru kwa hiyo heshima, basi Ron atamjulisha Andy.” Hilo likawa lipo sawa.

“Ombi la mwisho.” Askofu akaendelea, wakacheka. “Hilo hata magoti nitapiga mama.” “Hamna sababu. Karibu tu.” “Asante.” Akatulia kidogo yule askofu. Mapadri wengine wakimsikiliza kwa makini sana bila kuingilia zaidi yakutingisha kichwa kuafiki kila anachokizungumza askofu wao.

“Huyu Andy ni mtoto niliyelea mwenyewe kama nilivyowaambia. Nakuomba mama, na Mina mwanangu, nifungishe hiyo ndoa mimi mwenyewe kama nilivyofanya kwa mwenzie kumpa upadrisho. Hata Andy mwenyewe sikuwa nimemwaambia hilo. Lakini ni ombi langu binafsi kwenu.” Mama Ron akacheka na kuinama kama anayefikiria. Pakazuka ukimya.

“Inamaana hiyo harusi ikafungwe Roman?” Akauliza mama Ron. “Tafadhali mama.” Akasihi askofu na kuendelea. “Lakini wapi wataabudu baada ya hapo, ni juu yao wenyewe. Ila ile siku ya harusi, tafadhali naomba hiyo niisimamie mimi mwenyewe.” “Naomba hilo nimuachie Mina mwenyewe. Ila binafsi, kwa heshima mliyotuonyesha, hakika imenigusa. Sidhani kama Mina atakuja kupata heshima kama hii!” Wakamuona yule mama anafuta machozi.

“Mungu awabariki. Binafsi ni wapi wanaenda kuabudu baada ya hapo au sasa hivi, sijali. Maadamu dini ni moja, hilo halina shida kabisa kwangu. Sitataka madhehebu yawazuie Andy na Mina. Naamini watafikia tu mwafaka.” Mina hakutegemea.

Maana alijua swala la dini ndilo liliharibu ndoa ya wazazi wake, kusikia hivyo! Hata Andy akasimama. “Asante mama. Nashukuru.” Akampa mkono kabisa. Vikaanza vicheko hapo, mwishoe wakaagana. Askofu na mapadri walikuwa wakienda kulala kwenye nyumba za mapadri Kurasini. Andy akawarudisha.

~~~~~~~~~~~~~~

Ndani ya mwezi, Mina akalipiwa mahari na mapadri hao. Mama Ron siku hiyo alialika ndugu karibu wote walioweza kufika, majirani na wafanyakazi waliokuwa wakifanya kazi na mama huyo na kumfahamu Mina kama mtoto asiyewezekanika. Muhuni na hashikiki. Watu walikula na kunywa, wakisherehekea mahari ya Mina BILA kina Ruhinda wala upande wa baba yao Mina na Ron ambao waliwasusa.

~~~~~~~~~~~~~~

Andy hakurudi tena nyumbani kwao na wala hawakumuona kanisani. Ila siku hiyo ya jumapili familia hiyo wakiwa kanisani wakasikia tangazo la kwanza la ndoa kati ya Andrew Ruhinda na Aminata. Baba yake akashituka na kumgeukia mkewe, wakabaki wameduaa.

Tangazo lilisema ndoa hiyo itafungwa jijini Nairobi nchini Kenya katika kanisa kubwa la Cathedral Basilica of the Holy Family. Jambo zuri kwa kijana wao, likageuka fedheha kwa familia nzima ya Ruhinda. Vile wanavyofahamika na kuheshimika kwenye jamii. Halafu Andy anaoa bila wao kuambiwa au hata  kukaribishwa! Ikawa aibu kubwa kwa familia ya Ruhinda haswa kwa watu wa karibu yao, wanao wafahamu familia hiyo. Kila walipoulizwa juu ya harusi hiyo, hawakuwa na majibu yakutosheleza.

~~~~~~~~~~~~~~

Andy amesimama kiume mpaka amefanikiwa hatua ngumu na ya msingi. Anabaraka zote za baba mlezi na mama Ron. Bado siku takatifu atakapokabidhiwa Mina kama mke.

Mill naye huko kwa baba yake?

Inaendelea….

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment