Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 13. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 13.

“Ila mama Pius, hukufanya vizuri mke wangu. Huyu binti yupo sahihi. Ameletwa hapa kama mgeni. Tungemkarimu, halafu ukapata muda wakuzungumza na Andy.” Akaongea mzee Ruhinda. “Kweli mama. Naona huyu binti ulimkataa hata kabla hujamuona.” “Na wewe Pius, unamuona huyu mtoto anafaa kuoa!?” Akauliza Paulina kwa mshangao. “Jibu hilo analo Andy. Mimi sina hilo jibu Lina. Hakuna kati yetu mwenye uwezo wakumfanya Andy aoe msichana tunayemtaka sisi!” Akaongeza Pius kaka mkubwa.

“Naomba nitoe angalizo.” Akaingilia Devi. “Sasa na wewe usianze.” “Hata! Naomba tu niseme jambo pengine mtaelewa. Maana msipoangalia, mtampoteza Andy, kabla hajarudi kwenye maisha yenu. Kumbukeni Andy hajakuwa kama nyinyi. Maisha ya Andy amekuwa akiwa mbali na nyinyi, tokea mtoto.” Hapo wote wakanyamaza.

“Andy hayajui haya maisha na nyinyi wote. Ni kama mtoto wa kambo kabisa.” Mama yake akashituka kidogo. “Naomba niwe wazi mama. Kwa heshima tu. Maana watoto wako wote umewakuza hapa nchini, ukiwaongoza na upo karibu nao. Ni Andy peke yake ndiye aliye watofauti.” Akaendelea Devi na kuwanyamazisha wote.

“Huyu Andy ni mtoto wenu, lakini amekuzwa mbali na tofauti na wengine wote. Sijui kama mnamfahamu msimamo wake juu ya watu wengine ukoje!? Eti jamani?” Kimya.

“Maana ni rahisi Paulina na Paul au hata Pius, kutizama mambo kwa jicho lako wewe mama, tofauti na Andy ambaye anatizama macho yake kama Padri.”  Devi akawatizama machoni. Ndio ni kama wanaanza kufunguka.

Mtazamo wake na wenu katika mambo au wetu sisi wote ni tofauti kabisa. Mimi najua ninachokiongelea, kwa kuwa nipo karibu sana na Andy, na nyinyi pia. Niwaambie ukweli kabisa. Jinsi anavyotizama mambo Andy, ni tofauti sana na nyinyi wote, na ndio maana akiwa na swali, hatampigia simu kaka yake Pius, atanipigia mimi.” Wote wakashangaa.

“Na alivyo na akili, atahakikisha anapiga muda anaojua sipo na dada yake. Atapiga kwenye simu ya mezani ya ofisini kwangu. Na atahakikisha anaweka wazi kabisa kuwa swali lake ni kwa sikio langu tu. Hatasema moja kwa moja, lakini utajua ndivyo anavyomaanisha.” Wakapoa.

“Chakuwahakikishia ni hivi, huyo mtoto, amemuingia Andy, kuliko atakavyosema. Ni Love at first sight. Anampenda Mina kuliko nitakavyowaambia, mkaelewa! Na mimi nilishajaribu kuzungumza naye mara ya kwanza tu alipomuona na kumfanya ashindwe kulala. Nikazungumza naye na kumuonya kwa muda mrefu sana, ndipo ikabidi amtafute Lora kwa mara ya kwanza kabisa, ili kumsahau Mina.” Wakashangaa sana.

“Kabisa! Lora alimtafuta ili asaidie kumtoa Mina kwenye mawazo. Lakini Andy alishindwa kabisa. Tulikuwa tukimuita asilimia 7.” “Nani?” Akauliza Paul. “Huyu Mina. Kwa vile alivyokuwa amechanganywa na huyu mtoto, akiwa hamjui, akawa anasema anamfahamu kwa asilimia 7 tu, lakini yupo tayari kuwa naye hata kama hizo 93 ni mbovu, atajifunza kuishi nazo.” Wakaangaliana.

“Kuna kipindi alisikia huyu mtoto anaumwa amelazwa, Lora akiwa kwenye picha, akanipigia kuniuliza chakufanya, nikamshauri aachane naye asimtafute kabisa ili asiendelee kuchanganywa. Atulize akili kwa Lora. Kweli akafuata ushauri wangu. Lakini hilo ni kosa ananilaumu nalo mpaka juzi nilipompigia simu kumjulia hali baada ya kupotea hapa. Na akakataa kabisa kumzungumzia Mina na mimi. Ni kama ananilaumu nilimshauri amtelekeze Mina akiwa mgonjwa tena amelazwa hospitalini.” Wote kimya.

“Ninachojaribu kukwambia mama yangu, na kukuomba. Najua unawapenda sana watoto wako na unawatakia mema, lakini nashauri labda kwa ajili ya kumpata Andy, angalau msizidi kumsukumia mbali na nyinyi, akaona mnamdharau au hamumuheshimu. Nyinyi woote, nashauri mjikaze tu, mjifunze, na mumuonyeshe mnaheshimu maamuzi yake.”

“Ila mkiendelea kutoa kasoro kila mwanamke anayemleta kwenu kwa heshima, kama yule Mganda sijui au Mkenya, mtampoteza Andy kabisa.” “Na kweli! Si mliona aliacha kuja hapa karibia mwezi sasa?” “Sawa sawa Pius. Na msifikiri kwa Andy inamsumbua. Hana anachokosa na kupoteza kwenu. Anaona nyinyi mpo timu moja, yeye yupo timu pinzani.” “Halafu yuko peke yake!” Akamalizia mzee Ruhinda.

Kumkosoa, kumcheka na kumbeza mbele ya msichana wake, sidhani kama ni sawa jamani!” Wote wakamgeukia Paul. “Mbona mimi nampenda tu Mina! Pale kanisani mbona mimi ndiye niliyemsalimia wakati nyinyi mlimchunia! Sema mimi nilikuwa nacheka ule utaratibu na vigezo vya hapa nyumbani na vile yule mtoto alivyo.” Paul akajitetea.

“Ni wewe Paulina ndio ulikazana kumuuliza maswali Mina kama mnataka kumuajiri!” Paul akamrushia mpira dada yake kujitoa lawamani. “Mimi nilitaka kumfahamu zaidi.” Na Paulina naye akajitetea. “Mmmh! Si kwa jinsi ile bwana! Tulisikia sana wakati mnamfukuza jikoni.” Akaongeza Paul akitoa lawama kwake zaidi. “Na mlimkatalia kwa kejeli mbele ya Andy mwenyewe! Tena baada ya yule mtoto kujinyenyekeza! Mngempa hata mchele aoshe jamani!” Devi aliendelea kulaumu.

Kama kitu kikamwingia mama Ruhinda. Alipoa kama sio yeye. Kila mtu akajisuta. “Ila wenyewe wanaonekana wanapatana na kuelewana. Si mmemsikia Mina?”  Kwa mara ya kwanza Raza akaongea kwenye mjadala wa Mina hapo mezani. “Anaonekana anamshauri vizuri, japo ni mdogo kwake. Hakutaka Andy aondoke hapa. Ingekuwa mtu mwingine angemshawishi Andy waondoke naye.” Akaongeza Raza.

“Na nafikiri hilo ndilo la msingi jamani! Ndoa ina mambo mengi sana mbali na uchumi.” Akaongeza mzee Ruhinda kwa tahadhari. Wakaendelea kula kimya kimya.

Kwa Andy & Mina.

Andy alimtoa hapo akataka apande kwenye gari yake, Mina akakataa. “Mimi nataka kwenda kwa mama yangu, Andy.” “Twende tukazungumze kwanza.” “Mimi sioni chakuzungumza.” Mina akaanza kulia tena. “Niangalie Andy. Mimi na nyinyi tuko tofauti kwa kila kitu! Hakuna popote tutakapoenda mimi na wewe. Siwezi kuishi maisha ya kujitetea, Andy. Sitaweza.” “Hutaishi na wao, utaishi na mimi.”

“Hata uniambie vipi, wale ni ndugu zako Andy, hawatakaa wakaondoka maishani kwako. Watakuwepo tu. Na mimi bado nitabakia kuwa mtu wa nje.” Andy akataka kumshika, Mina akarudi nyuma.

“Mimi naondoka Andy. Hata hivyo mimi na wewe tunatofautiana. Wewe una dini yako na mimi nina dini yangu. Kanisani kwenu mnafanya mambo mengi sana, mimi siwezi. Halafu wewe umezaliwa kwenye familia ya watu wanao dharau watu. Wanataka watu wanaofanana na nyinyi. Hiyo hatuwezi kubadilisha. Na kama hunifahamu bado, mimi watu kama ndugu zako siwezi kuishi nao Andy. Wanadharau watu wengine. Mimi nimezoea maisha kama ya pale kwetu. Tunakuwa na amani na tunaheshimu kila mtu. Siwezi Andy.” Andy alibaki kimya anamsikiliza.

“Wewe endelea na maisha yako. Tafadhali naomba uniache kabisa. Mimi ndio nimetulia, nataka kutulia nyumbani. Mambo kama haya sitaweza Andy. Wewe tafuta mwanamke anayefanana na watu wa kwenu. Mimi naondoka, naenda zangu kwa mama yangu na Ron.” Hapo hapo Mina akaondoka. Akakimbilia kituoni, akapata daladala, akaondoka. Na kumuacha Andy na hali mbaya na ahadi za yote atakayofanyiwa baada ya kutoka kwao. Alishaona siku yake ikiisha akiwa amejawa na penzi la Mina, sio KUACHANA.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina alipopanda tu kwenye daladala akampigia simu kaka yake kumuomba amfuate kituoni alijua watakuwa wameshatoka kanisani. “Kwema huko?” Akauliza mama Ron baada ya Ron kukata simu. “Sidhani. Kwa nini mimi nimfuate, asiletwe na Andy? Halafu kama analia!” “Basi huko atakuwa ameshawatoroka.” Wakacheka.

“Ngoja nimpigie, maana anaweza kuwa analia kweli. Mpaka aje afike hapa kichwa kitakuwa kinamuuma, kesho tena patakuwa hamna shule.” Mama yake akampigia. “Vipi mwanangu mzuri? Mambo yameenda vizuri huko?” Akaanza mama yake. “Mama, wale watu wabaya.” Mina akamuelezea mama yake kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Mama yake akaumia sana. “Pole. Njoo mama. Tena tulikuwa tupo tu hapa Mbezi kwa Mangi tunakula. Shukia hapo kituoni utatukuta hapa.” Akamtuliza, Mina akatulia.

~~~~~~~~~~~~~~

Hapohapo Andy akarudi nyumbani kwao, hata ndani hakuingia tena, akachukua gari yake akaondoka kuelekea nyumbani kwa kina Mina. Alikuwa na hali mbaya, kuachana na Mina haikuwa chaguzi. Kwamba haipo hata mezani. Alimtaka huyo Mina kwa hali na mali. Alishalemazwa na penzi la kuonjeshwa na Mina! Hapo alikuwa akisubiria kwa hamu siku atakuja mvua nguo amfaidi kwa undani. Leo wanampokonya tonge mdomoni! Hakukubali. Akakanyaga mafuta mpaka Tegeta, lakini akakuta nyumba imefungwa. Akataka kumpigia simu Ron, akaona awe muungwana. Asubiri tu.

Mungu Humpa Amtakaye.

Alikaa hapo mpaka ikafika saa 11 jioni ndipo akaona wanakuja, tena kwa kutembea tu. Wote watatu. Andy akashuka garini. Ron akasalimiana na Andy, Mina akaenda kufungua mlango, akapitiliza mpaka chumbani. Mama Ron akamkaribisha ndani. “Karibu baba.” “Asante.” Moja kwa moja kwenye makochi. Andy, mama Ron na Ron.

“Samahani mama yangu, najua Mina amekwambia.” “Wala huna haja yakuomba msamaha Andy mwanangu. Haya matabaka kwenye maisha ni Mungu mwenyewe ndiye ameyaweka. Hujalia watu kwa kadiri apendavyo yeye. Na ni ngumu sana matabaka haya kuendana, PENGINE kuwepo mkono wa Mungu mwenyewe, yaani Mungu aruhusu, lakini si vinginevyo.” Andy aliumia sana kusikia hivyo.

“Lakini Mina atakuwa na mimi, mama! Ataishi na mimi.” Akamuona mama yake anacheka taratibu kisha akaona aongee tu. “Mimi nitakuwa mkweli kwako Andy. Sitakuficha. Hayo ni maneno ya mwanzoni kabisa watu huyasema, kabla uhalisia wa ndoa haujaingia. Ni wachache sana wanaweza kusimamia hapo.” Mama Ron akaendelea.

“Huyu Ron huyu, ni mtoto wangu. Hata aoe mzungu au mswahili kama mimi mama yake, bado mimi ni mama yake tu. Ipo nguvu kubwa sana ya mama kwa mtoto. Wewe utakuwa shahidi yangu kwa lililotokea leo.” Mama Ron akaendelea. Taratibu tu.

“Mina aliponisimulia mkasa mzima. Jinsi mambo yote yalivyoenda. Mwishoni nilimuuliza swali moja tu. Katika yoote hayo, wewe ulisema nini? Sikusikia jibu lakueleweka kuwa katika yote hayo wewe ulisimamia upande gani au kwenye yale mahojiano, ulizungumza nini.” Andy akashituka kidogo.

“Niliambiwa karibu kila mtu alizungumza, kasoro wewe. Sikumwambia kitu Mina, lakini mimi mwenyewe nikafikiria. Kama leo ulikuja kumchukua hapa mwanangu, ukampeleka kwenu, mbele ya ndugu zako wanamsodoa, kesho akiwa mke wako mmeshazaa watoto wawili watatu, umeshamzoea, si watampiga, wewe ukiangalia na kumtoa tu kwenye ugomvi?” Andy akainama.

“Silaumu, lakini kwa haraka haraka, nasema inatokana na malezi na makuzi ya kwenu. Kile kilichoongelewa pale hakikuwa kosa. Kinaendana na nyinyi. Ndipo tunaporudi kwenye matabaka. Yapo Andy baba, na wala hatuwezi kuyaepuka. Mlipo nyinyi na sisi ni tofauti kabisa.” Akaendelea mama simba, akilinda mwanae. Ila kwa utaratibu tu bila ugomvi.

“Na sikwambii kwa hili lililotokea leo, hapana. Ni kwa uzoefu wangu wa haya mambo. Hawa watoto wawili, sikuzaa na muhuni wa mtaani. Alikuwa mume kabisa. Ila sababu ya utofauti wa DINI tulifunga ndoa ya serikalini. Tulikutana chuo cha ualimu, mapenzi yakawa mazito kuliko utofauti wetu wa dini. Wazazi pande zote walituonya na kutukatalia. Lakini wakati ule hapakuwa na jinsi tukaweza kuishi mbalimbali. Tukajikaza, sisi wenyewe, tukafunga ndoa. Maisha yakaanza.”

“Mwaka uleule akapatikana Ron. Wale ndugu waliosema wametususa sababu ya mimi kuolewa na mwislamu, na yeye kuoa mkristo, wakaanza kurudi kwenye picha taratibu. Na huwezi kumkataza mama yake asifike nyumbani au dada zake kuja kuona mtoto ambaye ni damu yao.”

“Kwao ni watu wa Pemba, Unguja kabisa. Wana uarabu, rangi kama hivyo Mina au huyu Ron, na nywele hawa watoto wamechukua kwao sema Mina amechanga kidogo na zangu ndio maana unaziona hivyo. Lakini ni kama hivi Ron akiacha kunyoa mpaka chini kabisa. Ni waislamu wa swala tano. Alfajiri swala ni ya msikitini. Mwanamke lazima kujisitiri. Ramadhani lazima kupikwe futari, ila na mwanamke wa dini yao. Mimi mkristo.”

“Wakwe wakija nyumbani, alfajiri wanaondoka na baba Ron kwenda msikitini, mimi nimelala ndani. Chakula ninachopika mimi hakiliwi kwa kuwa ni mkristo hawaamini nyama niliyopika kama imechinjwa na mwislamu na chakula ninachopika mimi hakiwezi kuliwa futari kwenye mwezi mtukufu!”

“Taratibu uhalisia wa mambo ukaanza kujidhihirisha. Mwenzangu akakazana kwa hili na lile ili tu kunusuru ndoa yetu ambayo pia haikuwa sawa kwa utaratibu wa kwao. Si ya msikitini. Tukakazana wee, LAKINI ukweli ukabaki pale pale. Mama ni mama. Ndugu zake ni ndugu zake.”

“Na uislamu wa mwenzangu au aliyekuwa mwenzangu, hakuukuta ukubwani. Ni yule wakuzaliwa nao. Hana ukweli wa Mungu mwingine isipokuwa aliofundishwa tokea mtoto. Na mimi hivyo hivyo. Fujo zikaanza. Ndugu wanamkumbusha hili na lile kwa makuzi ya kwao. Ikawa sasa mwezi wa ramadhani hakuna anayekuja kwetu, na yeye sasa inabidi kwenda kufuturu kwa dada yake, Mwananyamala! Ikawa fujo. Siku za sikukuu, mume yupo kwao, Unguja.”

“Haya, dada yake akaachika, na yeye akarudi kwao Unguja. Sasa kizazaa mwezi mtukufu. Baba yao hawa anakwenda kufuturu wapi kipindi hicho! Ikawa sasa fujo zaidi. Mara usikie kaoa mke wa daku, sijui wapi, mara usikie kamuacha. Ikawa sasa haonekaniki nyumbani. Hekaheka isiyoeleweka. Mimi na watoto wangu tukawa sasa makafiri. Hawatutaki tena.”

“Mwishoe nikaja kusikia amekwenda kupewa mke, huko kwao Unguja. Ndipo akaoa sasa, na ndio mwanamke ambaye akawa anatambulika nyumbani kwao na kuheshimika. Tulikuwa tukifanya kazi pamoja. Tukifundisha shule moja. Fujo zakuoa zilipoanza, nafikiri kwa heshima yangu, akaomba uhamisho. Akahamia Mkuranga.”

“Sikumuona yeye wala ndugu zake tena wakija hapa kwa la kheri wala la shari. Uzuri tulikuwa tumeshapanunua hapa, tumeanza msingi. Alipoanza hekaheka zakuoa, ndipo mambo yakaanza kuwa magumu sasa, ndipo nikaanza jukumu la wanangu mimi peke yangu bila msaada hata wa ndugu zangu, sababu walinikataza kuolewa naye, sababu ya dini, nikamngang’ania. Sasa kule kuachwa na watoto wawili, na yeye kuoa mwanamke mwingine wa dini yao nikageuka mimi kicheko kwa familia.”

“Hakuna anayetaka nimkaribie hata kwa kuomba chumvi. Wakanisusa mimi na hawa watoto wangu. Wakinicheka mimi na wanangu. Nikikwambia nipo mimi na wanangu, sio kwamba sina ndugu hapa mjini, lakini ni vile walivyotugeuza sisi kichekesho na kuonekana sisi ni watu tulioshindwa.”

“Na bahati yake ilivyokuwa nzuri, mwenzangu alivyoniacha tu nakuoa, huko Mkuranga akapandishwa na cheo, akawa mwalimu mkuu, wa shule ya sekondari Mkuranga. Ndugu zake wakazidi kufurahi na kumthibitishia mimi ndiye niliyekuwa na mkosi kwenye maisha yake. Namuwekea nuksi, mkewe mpya ndio nyota yake safi. Nyota zao sijui zinaendana, sasa hivi mambo yake yanaenda vizuri.”

“Hayo naambiwa na Kasimu mwenyewe, wala si ndugu zake. Yeye mwenyewe aliniambia mara ya mwisho alipokuja hapa kwangu, kunipa talaka yangu. Kwamba anataka huyo mke wake mpya, ndiye atambulike hata serikalini, anataka atoe jina langu.” “Watoto!?”  Akauliza Andy kwa mshangao.

“Hao watoto alishawatoa zamani sana kwenye maisha yake. Yaani hao alikuwa hata azungumzii tena baada yakumkatalia Ron asianze madrasa, na bibi yao alipokuja hapa, akataka Mina awe anavalishwa hijabu na mambo yao mengi. Nikakataa. Nikasema huyu mtoto mdogo hivi avaliswe hijabu na baibui, atachezaje! Wakasema maumbile yake hayafai kuachwa wazi, Mina ni mpana chini kama shangazi zake lazima asitiriwe kwa baibui na hijabu. Nikawaambia huyu mtoto hajachagua kuzaliwa hivyo, hawawezi kumnyima raha mwanangu, wamwache. Hapo Mina alikuwa darasa la 5 anakwenda la sita ndipo bibi yake alipokuja na hiyo hoja. Kuwa apelekwe shule ya kiislamu na mwili wake usitiriwe, ninavyomvalisha mimi si sawa.”

“Halikuwa jambo dogo hata kidogo! Na mimi kwa kuwa mtoto wao alishaanza kumanga manga huko nje. Hajali nyumbani, nikawa nina nguvu na watoto wangu. Kasimu akawa anaona hata aibu kulazimisha. Maana alikuwa anaonekana nyumbani mara chache. Na mara zote anazokuwa akirudi anakuwa kama aliyekimbia huko. Yaani anakuja kupumzika tu. Na haji na chochote.”

“Akila vizuri mfululizo labda wiki moja au mbili, akapata usingizi mzuri hapa, utasikia anaitwa tena kwao, Unguja. Kwa hiyo hata yeye alijua mimi ndio nahangaika na watoto. Hawezi kunilazimishia matakwa ya kwao. Basi nikawakatalia wazazi wake, nikakataa watoto wangu kuhama shule, na nikawaambia Mina havai hijabu wala baibui.”

Wakanitisha hapa wee, wakaniambi maneno yavitisho, na Kasimu, baba yao akisikia. Maana walikuja wazazi wake wote wawili, kaka zake na dada yake mkubwa. Mkorofi kweli kweli. Tena kafanana na Mina kuanzia kichwani mpaka unyayo utafikiri alimzaa yeye! Kasoro roho zao tu, naona hapo Mungu alinihurumia.”

Wakanitisha na wanangu. Wakaniambia kama Kasimu hatawapata hawa watoto, na mimi pia sitawapata. Wakasema mengi, Kasimu akabaki kimya hapa. Wakaondoka na mtoto wao, na mimi nikabaki na wangu, ndio mpaka leo sijawaona hata kupotea njia.”

“Lakini ukiniambia kama Kasimu hakuwa akinipenda, sikubali. Kasimu alinipenda sana, ila kulikuwa na pressure kubwa sana kutoka kwa ndugu zake na dini. Yeye kama binadamu alishindwa chakufanya.” “Pole mama.” Andy akasikika kama aliyeingiwa na huruma.

“Asante Andy mwanangu. Lakini ninachotaka kukwambia, huyu Mina unayemuona hapa, ni kwa maombi. Nimehangaika kwa kufunga na kuomba ili arudi na awe kwenye hali hiyo. Muulize Ron atakwambia.” Ron kimya.

“Tulikuwa tukipiga magoti hapa usiku kuchwa tukimsihi Mungu aturudishie Mina. Siku aliponitafuta kwa ujumbe akiwa Iringa amelazwa, sikupata ujumbe wake kwa wakati kwa kuwa nilikuwa kwenye mkesha wa maombi na huyu Ron. Akatuma ujumbe usiku, nikaja kuona ujumbe saa 12 alfajiri baada ya maombi. Ndipo nikapiga simu na kumpata nesi aliyemwazima simu. Hiyo ni baada ya kama miaka miwili ya kupotea kwake. Ninachotaka kukwambia mwanangu, huyu Mina ni muujiza wangu. Kwa wengine anaweza kuwa kituko au asiye na mbele wala nyuma. Lakini hapo alipo huyo, ni muujiza niliohangaika nao kwa mateso makali kwa miaka kama 8 hivi.”

“Natunza kama yai mpaka nione mwisho wake. Sitaki aje achanganywe hapo katikati kwa maneno yakumvunja moyo. Hajapita kama walipopita wengine. Hilo hata yeye anajua. Anachosoma kwa wengine si kitu, lakini kwangu au kwetu ni muujiza mkubwa mno. Ile tu kuona anakaa chini na kujifunza kitu, na kukizingatia!” “Na akarudi nyumbani.” Ron akaongeza. “Ewa! Kama alivyosema Ron. Ni muujiza ambao hakuna anayetuelewa. Hata Mina mwenyewe haelewi ila mimi na Ron tunajua ni nini Mungu ametutendea.”

“Kwa hiyo nikuombe kitu Andy mwanangu, naomba tumpe nafasi tu. Acha sisi tukokotane naye kidogo kidogo, hivyohivyo. Kama ni mpango wa Mungu akasogea na kufikia hivyo viwango vya juu, mkaja kukutana tena, basi. Ila kama sio bahati yake, Mungu akusaidie upate unayefanana naye. Lakini huyu Mina nakuomba atulie baba. Tafadhali sana. Mwache tu tuvutane hivyo hivyo kwa daraja letu sisi. Ila sidhani kwa sasa kama yupo tayari kukutana na watu wa madaraja yenu hayo. Mtamchanganya na kumfanya atilie mashaka hata kile anachokifanya sasa. Sijui kama umenielewa?”  Andy akanyamaza.

Akajua ndio amenyang’anywa mke. Ndio anafukuzwa ukweni. Andy akabaki kimya kwa muda akiwa ameinama. Wakamuona anasugua mikono. Kama anayetaka kuzungumza jambo, anashindwa. Akavuta pumzi kwa nguvu akiwa vile vile ameinama. Pakawa kimya kabisa.

Mwishoe akaona azungumze tu. “Naomba radhi mama, kwa kushindwa kusimama na Mina.” Akaanza Andy macho mekundu. “Naomba mnisamehe sana. Samahani.” Kimya. “Naomba niwaache mpumzike. Muwe na usiku mwema.” “Na wewe pia.” Akasimama Andy. Akasogea mpaka mlangoni akageuka.

Nampenda sana Mina. Sana. Sikuwa naye kwa majaribio. Nilitaka awe mke wangu. Nilimpeleka nyumbani nikifikiria na wao wataona kile nilichoona mimi kwa Mina, mbali na vigezo vingine. Lakini nasikitika imekuwa tofauti na imenigharimu kumkosa Mina. Usiku mwema.” Andy akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Mina ni kama akajionya hata hakutuma ujumbe wa bahati mbaya kwa Andy akiuliza kama alifika nyumbani salama au la. Andy naye akatulia kabisa. Hapakuwa na mawasiliano hata ya ujumbe kati yao. Jumapili hiyo ikaisha pakiwa kimya na ahadi zote za huba kuzikwa na kina Ruhinda na wenyewe kushindwa kuzitetea..

Mtafutaji Asiyechoka!

Wakati huku mahusiano ya Andy na Mina yameingia msukosuko wazazi nao wakiwa wameingilia kati, huku kwa Pam na Mill mahusiano yao yakaanza kwa kasi. Mill yupo na Pam kama mke kabisa. Anamuwazia kuanzia asubuhi mpaka usiku anakwenda kulala. Swala la kuhama na usafiri ikawa kero yake yeye Mill. Kila wakati anawaza hilo tu. Shida ikawa yake kuliko Pam mwenyewe. “Sitaki mtu amnyanyase Pam wangu.” Akakusudia moyoni.

Akamuomba aanze kutafuta pakuishi. “Nasita kutoka kwa shangazi Mill! Najiona kama najitenga na kujiweka peke yangu!” “Umekua Pam. Hata yeye mwenyewe atakupongeza.” “Tatizo likinipata huko?” “Pam mpenzi! Naomba tutembee kwa imani. Naweza nisiwe na majibu yote sasahivi, lakini naomba weka imani.” Kama kawaida yake. Mill alijaliwaga hekina ya maneno. Alijua kuzungumza kiasi cha kumuweka sawa Pam kila wakati.

Wakati akiendelea na juhudi ya kutafuta chumba sehemu karibu na Kinandoni zilipokuwepo ofisi za Sandra, karibu sana na Ubalozi wa Ufaransa, Pam akaanza kupokea mahela kutoka kwa Mill. Ya kodi na ya kununua gari. “Huna haja ya kuagiza. Tembelea kwenye yard. Nunua tu hapohapo nchini.” “Au ninunue kwa Sandra? Huwa anakuaga na magari anauza kwa wanaokopa na kushindwa kulipa. Yanakuwa na bei nzuri.” “Hapana Pam. Hayo magari yamebeba vilio vya watu. Yanauzwa si kwa hiari ya wa miliki. Iweje uje upokonywe kwa nguvu huko barabarani? Ni bora tugaramie, uwe salama.” Hilo nalo likakaa sawa.

Pam akafanikiwa kupata chumba Mkwajuni. Chumba kimoja na sebule. Hakuchukua muda, akakijaza vitu muhimu. Wakati akifanya yote hayo ni Mill peke yake aliyekuwa akijua mbali na mama yake mzazi ambaye ndio msiri wake. Walifanya mambo yao kimya kimya. Na yeye hakubadilisha maisha hata kuanza kujinunulia nguo mpya au kununua vyakula kazini. Pesa akawa anabania. Hata waliokuwa karibu naye hawakuona chochote cha tofauti.

Jerry hakujua kinachoendelea tena kwani wawili hao walibaki kuwasiliana wenyewe. Na yeye Pam kazini hakusema chochote. Simu za Mill anapokea na kuzungumza faragha. Hakuna aliyejua kinachoendelea kumbe Pam ndio ameishia kujazwa madola.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipokamilisha chumba chake ndipo akaaga sasa kwa shangazi yake na mjomba. Na akawapa na zawadi ya shukurani, akahama. Uhuru ukaongezeka. Ndipo akanunua gari sasa, tena hapohapo mjini. Akabahatika gari nzuri sana. Pam akawa wa usafiri binafsi sio wakudandia daladala. Ndipo minong’ono ikaanza sasa ofisini, ila hakuna mwenye jibu juu ya mabadiliko yake.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipoona amejiweka sawa, ndipo akamkaribisha mama yake amtembelee mjini. “Njoo mama yangu uoshe macho mjini.” Mama Eric akafurahi huyo! Uzazi mzuri. Na yeye ndio msiri wa bintiye. Yupo kijijini, lakini kila linaloendelea anamuhusisha mama yake kijijini.

Ikabidi amuombe mama yake, yaani bibi Shelukindo ambaye ni kama miguu yake, amsindikize mjini. Wawili hao wakatoka milimani, wakatua jijini kwa Pam. Wanawake watatu wa kisambaa ndani ya chumba kimoja. Vicheko wakati wote.

Mill akipiga simu basi atampa mama na bibi awasalimie pia. Akazoeleka huyo Mill hata kabla hajaonana nao. Penzi likanoga. Pam si malaya japo ni dawa ya maradhi ya wengi wenye gonjwa na maumbile ya kibantu. Akajaliwa juu mpaka chini. Akajaliwa na rangi ya mama yake, basi shida mjini. Lakini yeye kimya. Akili, moyo vyote kwa Mill wake.

Bibi Shelukindo vya mjini vikamchosha, akamkumbuka mumewe, wakamua kurudi na mwanae kijijini, ambaye ni mama Eric na Pam, lakini bado Pam akiwatunza kwa ukaribu tu.

Hatimaye Mill Arudi Jijini. Safari hii kwa ajili ya Pam.

Pam akatunza siku zake za likizo akimsubiria Mill. Mapenzi ya kwenye simu yakawanogea, Mill akazidiwa. Mwili unamtaka tu Pam. Shule zilipofungwa tu, kimya kimya akarudi jijini. Hata Jerry hakujua. Ila Mike na Kamila walijua kama anarudi mjini. Hakutaka mtu ampokee uwanja wa ndege ila Pam tu.

Pam akawahi uwanja wa ndege akimsubiria, peke yake. Alipendeza huyo Pam, kwa hakika alivutia. Ungejua matunzo anayopewa, anastahili. Hatimaye muda ukawadia. Ndege iliyokuwa imembeba Mill ikatua kwenye viwanja vya ndege vya Mwalimu Nyerere. Pam alikuwa miongoni mwa wengi waliokuwa wamesimama nje ya mlango kumsubiria Mill.

Wakaendelea kutoka abiria tofauti tofauti wa mataifa mbali mbali kutokea Doha, ambapo Mill aliunganisha ndege yake kutokea nchini Marekani. Yaani karibu na mwisho, akiwa anakaribia kukata tamaa, ndio anamuona Mill anatoka na masanduku mengi aliyokuwa ameyapanga kwenye kigari.

Moyo wa Pam ulijaa furaha ya ajabu kumuona Mill. Akashindwa kujizuia. Akamkimbilia na kumrukia, akajikuta machozi yakimtoka. Mwili wa Mill ni mkubwa, hakushindwa kumdaka, na kumkumbatia. Pam alikuwa haamini kama ameshikwa na Mill!  Mwanaume aliyefanikiwa kuuteka moyo wake vilivyo na kuyabadili maisha yake kwa hadhi ya namna yake.

Akambembeleza hapo, akaanza na busu la shingoni karibu na shavu. Ndevu zilizozunguka midomo ya Mill na kuungana na ndevu za chini ya kidevu, zikachongwa kwa umaridani mpaka kukutana na nywele za kichwa pembezoni mwa masikio zikamsisimua Pam vilivyo.

Ndipo akamkiss chavuni kidogo, akaja midomoni. Akanyonya midomo yake akiwa amemkumbatia. Kisha akahamia sikioni. “Na mimi nimefurahi kukuona Pam.” Akamnong’oneza sikioni na kumbusu na kukumsisimua zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~

Huyo Pam hakuwahi ona mwanamme wa kumpa mwili wake mpaka Mill. Hapo alikuwa tayari na penzi la Mill bila kuombwa, angempa. Alikuwa akimtamani huyo Mill asijue mwenzie alikuwa anamuandaa muda wote. Hakuacha kumwambia jinsi anavyompenda na kumuhitaji. Aliamsha hisia za Pam, hapo walikuwa wamejiandaa kujifungia kwenye kijinyumba anachoishi Mill na alisha mwambia Pam.

Hapo Pam ameenda kumpokea, lakini na yeye anasanduku la kuhamia hapo mpaka Mill aondoke nchini. Alijifungasha vitu vyake vya msingi alivyojua angehitaji anapokuwa na Mill, akafunga chumba chake na kwenda huko uwanja wa ndege kama anayesafiri.

~~~~~~~~~~~~~~

Atafutaye hachoki, akichoka keshapata!

Hangaika ya Mill hatimaye imezaa matunda. Pam mikononi mwake, na yupo tayari na fungate ya kabla ya ndoa.

Yapi yataendelea kwa wote?

 Mina&Andy je?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment