Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 12. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 12.

Bado Andy akawa hajamuelewa. Hofu ya kupatwa na kile kilichompata Omar ikamjia. Akikumbuka vile Mina alivyomsimulia alifika sehemu hataki hata amguse! “Ni nini Mina?” Akaendelea kusihi kwa wasiwasi, akidhania hamtaki au hajisikii kushikwa naye. “Maisha yangu niliyoishi nyuma yana...” Ikawa kama ameshamuelewa moja kwa moja.

“Yaani unataka kunipunja mimi sababu ya maisha yako ya nyuma!?” “Nakosa ujasiri!” “Hapana Mina. Sio na mimi. Mimi nimechukua hatua kubwa sana kwako. Nimejifunga kwako, na kila mtu anajua sasa hivi mimi ni wako. Ndiye niliyetakiwa nifaidi yote kuliko wote. Sasa tena mimi ndio napunjwa! Utakuwa hunitendei haki!” “Samahani Andy, basi nitajitahidi.”

“Unajitahidi vipi? Kwani hujisikii hata kunigusa?!” “Najisikia ila ukumbuke mara ya mwisho hali niliyokuwa nayo Andy. Niliingiwa na hofu. Kitu kilichokuwa hai, kikafa ndani yangu! Halafu ikabidi kitolewe na kusafishwa, tena bila ganzi! Iliuma Andy, hakuna jinsi nikakwambia ukaelewa. Mwili mzima unauma kila nikifikiria hivyo. Natetemeka.” Hapo Andy akaelewa vizuri.

“Samahani Mina. Hapo nimekuelewa sawasawa. Basi tuchukue taratibu. Nitakusubiri.” Mina akacheka na kumsogelea. “Wewe ni mtu mzuri Andy.” Andy akacheka.

“Nikumbatie tena.” “Una uhakika?” Mina akatingisha kichwa kukubali. Akamkumbatia vizuri. Mina akajipanga hapo kwenye kochi, Andy alikaribia kuvua suruali. Mina alimpa mabusu yakumchanganya, akabaki akitetemeka huku amemkumbatia kwa nguvu.

Maana alitulia hapo mwilini kwa Andy akiwa amemlalia. Andy akaona anajipunja, akamvuta zaidi, akanyoosha mguu mmoja kwenye kochi, Mina akawa katikati ya miguu, akajilaza kifuani huku akiendelea kunyonywa midomo yake kwa uchu. Mabusu hayo yakaendelea Mina akijizungusha katikati ya mapaja yake, akishikwa kwa uchu.

Alijaa kifuani, Andy akabaki aking’ang’ania hajui tena pakushika. Baada ya muda, Mina akajilaza kifuani na kumkumbatia kwa kupitisha mikono yote miwili pembeni ya kifua. Wakabaki wakivuta pumzi kwa nguvu.

Baada ya muda akanyanyua uso, akakuta Andy akimwangalia. “Nakupenda Andy, naomba hilo usilitilie shaka.” “Nimefurahi kukusikia na wewe ukiniambia Mina. Hukuwahi hata kuropoka!” “Ni hofu tu na aibu, Andy. Ila nakupenda.” “Basi nimefurahi kusikia hivyo. Inanipa ujasiri zaidi. Nilikuwa naona ni kama nalazimishia kila kitu!” Mina akacheka na kujirudisha kifuani. Wakatulia kwa muda.

“Acha nirudi nyumbani. Nisichelewe zaidi.” “Natamani tubaki wote!” Mina akacheka na kumbusu pale alipokuwa amemuegemea. “Urudi tena.” “Lini?” “Naomba tufanye jumamosi na jumapili ndio siku zetu zakuwa pamoja.” Mina akakaa.

“Lakini mimi naabudu kwengine na wewe unakwenda kanisani na wazazi wako. Itakuaje?” Hilo likawa swali la msingi na gumu. Andy ni mwaRC damu. Mina hajui kanisa jingine na la msingi la kung’ang’ania kama alivyomuona mama yake akifanya, kama Lutheran. Inakuaje?

“Cha kwanza nataka ujue wewe kwanza. Katika kila nilifanyalo nitakutanguliza wewe.” “Jamani Andy!” “Kweli Mina. Najenga familia yangu na wewe. Lazima nikuangalie wewe. Halafu juu ya baadaye itakuaje, naomba tulifikirie hilo. Mmoja wetu ni lazima alipe garama ili tuweze kuwa pamoja.” Mina akainama kama ambaye ashaona historia ya mama yake inataka kujirudia na kwake.

“Naomba tufikirie kabla hatujaweka au kuona ugumu wowote. Tumekubaliana kuwa tunapendana, si ndiyo?” “Nakupenda Andy.” “Basi hilo ndilo la msingi. Mengine naomba tujipe muda wakufikiria.” “Sawa.” Andy akamrudisha mpaka nyumbani. Akasalimia ndani, ndipo akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Maisha ya wapenzi hao yakaanza. Mina akitoka shule, anakwenda ofisini kwa Andy moja kwa moja. Anamsubiri mpaka akitoka, anamrudisha nyumbani. Ghafla Tegeta kukawa karibu sana kwa Andy. Andy akawa haonekaniki tena nyumbani kwao. Si jumamosi, si jumapili. Jumapili ya pili nayo ikaisha. Ikaja ya tatu pia akatoa udhuru.

Kila mtu nyumbani kwao akajua ni sababu ya kutoelewana jumapili ya mwisho kuwepo kwao kwa kutoendeleza mahusiano na Lora. Tokea aondoke hapo siku ile, Andy hakurudi tena. Alikuwa akituma ujumbe kila siku ya jumapili asubuhi akiwataarifu wazazi wake kuwa siku hiyo hatafika kanisani na nyumbani. Hivyo tu, basi. Hataonekana kwao wala kusikika tena mpaka jumapili nyingine tena akitoa udhuru.

Akazoea midomo ya Mina, akawa kama mwenye kiu naye kila wakati. Mikono yake wakati wote ilitaka kumpapasa. Jumamosi zikawa ni za Mina kuwekwa mikononi. Hata wakiwa na mipango siku hiyo, basi itatafutwa sababu ya Mina kuwepo hapo mikoni mwake. Akawa kama ameshachanganywa na Mina. Akili na mawazo ya Andy yakawa Tegeta kama hayupo hapo na Mina.

Jumamosi asubuhi anaanzia mazoezini, anarudi nyumbani kuoga. Saa nne asubuhi, anakuwa ameshafika nyumbani kwa kina Mina. Anatoka naye kwenda sokoni. Wananunua vitu vya nyumbani kwao, na nyumbani kwa Andy. Wanapeleka vitu kwa kina Mina, kisha wanarudi kwa Andy. Watakaa hapo kwa Andy wakishikana hapa na pale. Huku wakipika hiki na kile na kufundishana hili na lile mpaka usiku anamrudisha kwao.

~~~~~~~~~~~~~~

Na ili asimpoteze aje amuoe, Mina alikusudia aendelee hivyohivyo kumuonjesha mpaka atangaze ndoa, afunge watu midomo. Alimpenda sana Andy. Alitamani yeye ndio awe mwanaume wa mwisho kwake kwenye safari ya mapenzi. Lakini alijua fika, akishampa tu penzi, na hivi siku za jumamosi na jumapili wanakuwa wote, atakosa sababu ya kumuoa. Akakusudia ambane, awe anamuonjesha vya kupitiliza, lakini asimvulie nguo mpaka atangaze ndoa yeye mwenyewe. Akisha muweka ndani ndipo ampe yenyewe.

Basi akawa akimfanyia makusudi. Ulalaji wake hapo wakipeana kiss, ungemuhurumia Andy. Atajilegeza juu ya suruali ya mwenzie, huku matiti yote yapo kifuani, akimnyonya midomo mpaka masikio huku kucha zikipita shingoni. Basi Andy anakuwa kama bwege hapo kwenye kochi, hawezi hata kusogea! Hajui muda. Hajali yeyote ila huyo Mina tu. Atamng’ang’ania hapo abaki amemlalia mpaka aagwe.

~~~~~~~~~~~~~~ 

Jumapili, Andy mtoto huyo wa kikatoliki anaishia kanisani alipo Mina. Wakitoka hapo watakwenda kula kama familia. Mina akila na kisu na uma kama Andy. Vitajaa vicheko, wanawarudisha Ron na mama nyumbani, au Ron ataondoka na mama yake, Andy anarudi kwake na Mina amfanyie anayomfanyia mpaka usiku ndipo anamrudisha kwao.

~~~~~~~~~~~~~~

Mwezi na week vilipoisha, ikabidi mama yake ampigie simu Andy. “Nipo mama. Nakuwa na Mina.” “Sasa kwa nini usimkaribishe nyumbani?”  Andy akabaki kimya. “Itakuwa vizuri na sisi tumfahamu.” Mama Ruhinda akaongeza ushawishi. “Basi nitazungumza naye tuone.” “Inamaana ndio mmefika mbali hivyo!” Mama yake akashangaa. “Mama! Asante kwa mualiko, nitakujulisha kama tutakuja.” Andy akajibu na kuaga.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku ya jumamosi akiwa na Mina. Yakaanza mabusu. Safari hii akaongoza yeye mchezo. Akampapasa kwa kupitiliza kwa makusudi, mpaka akamuona ametulia kabisa kifuani na yeye amezidiwa. Akamwachia midomo taratibu huku mikono akiirudisha kiunoni mpaka Mina akaona aibu maana alifika juu haswa. Akajilaza kifuani akihema. Andy akambusu kichwani mara kadhaa akitulia.

Kisha akamchungulia pale alipokuwa amejilaza kifuani kwake amemkumbatia. “Naomba nikukaribishe na mimi kanisani kwetu.” Mina alishituka mpaka akakaa. “Andy!” “Utakuwa na mimi. Na baada ya hapo tutakwenda wote nyumbani kwa wazazi kwa ajili ya chakula cha mchana.” Mina akakosa raha kabisa mpaka Andy akamuona. Akajivuta pembeni kabisa.

“Kama haupo tayari ni sawa Mina. Nitasubiri.” Hilo likamfanya kumuhurumia, akaona ajirudi. “Natakiwa kuvaa aje?” “Kama kawaida unavyovaa kanisani kwenu. Kuwa kama wewe, usiogope.” Akabaki akifikiria. Akajua historia ya mama yake inataka kujirudia kwake. Maswala ya dini. Wakidhani ukristo na uislamu ni tatizo, sasa hivi ni madhehebu ndani ya ukristo.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake asubuhi alikwenda kumchukua Mina nyumbani kwao. “Umependeza Mina! Sana.” “Mwenzio nimemuamsha mama tokea saa 11 anisaidie kujiandaa.” Andy akacheka. “Alifanya nini sasa?” “Yeye tokea zamani anajua kuzichana hizi nywele zetu, tumetoa kutoka upande wa baba. Alikuwa akimchana na Ron, zinakaa vizuri sana. Sijui anafanyaje, lakini hata zangu anaweza kuzitoa nimenyooka vizuri zaidi! Sasa leo amenichana na kuzibana hivyo.” “Zimekupendeza sana. Unaonekana vizuri.” Mina akacheka.

“Umeona na hereni zangu lakini? Na Cheni!” Andy akacheka. “Umependa?” “Sana. Si umeona jinsi vilivyonipendeza? Nanukia vizuri. Asante Andy.” “Karibu.” Akataka kuinama na kumpa busu. “Utatoa mafuta ya mdomo Andy bwana!” “Yaani hayo mafuta ni muhimu kuliko mimi, Mina!? Hujaniona tokea jana!” “Basi Andy.” Akajinyanyua pale kitini, kabla Andy hajatoa gari pale nyumbani kwao.

Akaanza kumpa denda. Midomo hiyo ya Mina, huwa hatoshekagi. Kama ambaye hana haraka tena, Andy akaendelea kufurahia hiyo midomo ndipo akaondoa gari. “Umefurahi sasa?” “Kiasi.” Mina akacheka. “Tukitoka kwenu nitakukiss mpaka utosheke.” “Siwezi.” Mina akazidi kucheka.

“Leo utatosheka. Nakuja kivingine.” Andy alicheka. Akashindwa kunyamaza. Kila alipomwangalia Mina alicheka. “Can't wait! Itabidi tuharakishe kuondoka nyumbani.” “Hapo utafanya nikupe double dose.” Mina akaendelea kutoa ahadi za kupagawisha, Andy anacheka. Walifika kanisani wakiwa wanacheka kwa kujibishana maneno.

Andy alienda kumfungulia mlango wakaanza kutembea huku amemshika mkono kwa kupishanisha vidole vyao, akamvuta mkono mpaka kwapani, kwa hiyo akawa amemvuta Mina karibu wanatembea taratibu wakisogelea kanisani. Mina hakuwa akijua ndugu wa Andy kwa kuwaona japo aliona baadhi ya picha nyumbani kwake, lakini akili zilikuwa zimezama kwa Andy anaongea huku akimwangalia yeye na mbele ila wakicheka sana.

Mina Na Kina Ruhinda.

Akaona ameongea kitu cha kuchekesha hacheki! Akamwangalia usoni. “Andy?” Akaona anaangalia mbele na yeye akaangalia akaona watu mbele yao wamesimama kama kundi. Akarudi kumuangalia Andy, na yeye akamwangalia. Akajua ndio ndugu zake. Wakawasogelea.

“Shikamoo baba na mama. Huyu ndiye Mina.” “Deeng’iii!” Akasikika Paul huku akimtizama Mina kuanzia juu mpaka chini. “Shikamooni.” Akasalimia Mina akiangalia mmoja hadi mwingine taratibu. Kimya. Akarudi kumtizama Andy. Akamvuta kidogo kama anayemuita. Andy akainama, akamsogelea sikioni. “Nilitakiwa kufanya nini?” Akamnong’oneza sikioni huku amemshika sikio kama wengine wasisikie. Wote wakabaki wakiwatizama wao vile wanavyo nong’onezana. “Ni sawa.” Andy akamjibu. Mina akajisogeza karibu ya Andy na kunyamaza.

“Huyo mtoto umemtolea wapi, Andy!?” Akauliza mama yake kama aliyeshituka kutoka usingizini na kukutana na maajabu. Andy akabaki kimya akimwangalia mama yake. “Una miaka mingapi wewe mtoto? Umetimiza hata 18 kweli!?” Akamgeukia Mina. Mina akamwangalia Andy na kurudisha macho kwa mama Ruhinda. “Ninatimiza miaka 22-week ijayo.” Paul akaanza kucheka, wote wakamwangalia Andy kwa mshangao.

“Twende kanisani Mina.” Andy akawazunguka huku amemshika Mina mkono. “Wooo, Wooo!” Paul akaenda kusimama mbele yao. “Mbona hamna utambulisho Andy!?” Akamsogelea Mina. “Mimi naitwa Paul, mdogo wake Andy.” Mina akampa mkono. “Nimefurahi kukufahamu Paul. Mimi naitwa Mina.” Akajitambulisha huku akimwangalia Andy. “Karibu kanisani Mina. Ujisikie upo kwenye Misa takatifu.” “Asante.” Andy akaingia kanisani na Mina. Wakakaa upande uleule anaojua familia nzima wanakaa. Ndugu zake wakaingia na kujipanga pembeni yao, wazazi wao mbele na wajukuu. Misa ikaendelea, Mina akifuatisha hiki na kile, lakini kimya kimya mpaka Misa ilipoisha, wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

“Si tunaongozana nyumbani?”  Akauliza baba yake. Andy akabaki kama anayefikiria bila jibu. Mina yupo pembeni. Wote wanawaangalia. “Sijui baba!” “Mimi nafikiri mkaribie tu nyumbani kama hamna mipango mingine. Tule chakula pamoja ndipo tuachane. Msiishie tu hapa kanisani.” Tayari kukawa na kusita kwa Andy. Akabaki kimya bila yakutoa jibu. Mzee Ruhinda akamgeukia Mina. “Karibu mama nyumbani.” Akampa mkono. “Asante.” Mina akaitikia na goti. Ndipo wengine wakampa mkono. Lakini Mina akahisi kama kuna uzito tayari. Kama kawaida yake akanyamaza ili kuepusha shari.

Mina Nyumbani Kwa Kina Ruhinda.

Alifika hapo kwa kina Ruhinda, ndipo akawaelewa ni kwa nini wanamshangaa. Jumba lenyewe la huyo mzee Ruhinda, linatangaza ustaarabu na utajiri. Halafu kila mtu alijua nini chakufanya na wapi pakwenda, mpaka watoto! Akabaki ametoa macho. “Hatutakaa muda mrefu. Usiogope.” Andy akamnong’oneza. Wakakaa sebuleni, akaona yupo pale na wanaume tu.

Akaangalia kulia na kushoto, akagundua wanawake wapo jikoni. “Labda na mimi nikasaidie jikoni.” Akamnong’oneza Andy sikioni. Wakati tv imewashwa hapo sebuleni. “Sawa. Twende nikupeleke.” Wakanyanyuka.

Walifika jikoni wakakuta ukimya wa namna yake. “Mina anataka kusaidia chochote.” “Hamna kitu anachoweza kufanya humu ndani.” Akawahi mama Ruhinda kwa jazba. Andy akacheka na kumshika Mina mkono kama anayetaka kuondoka naye. “Labda aje anisaidie mimi kuandaa mboga za majani wakati natayarisha mchuzi.” Akawahi mke wa kaka yao, Raza.

“Paulina atapika hizo mboga.” Akajibu tena mama Ruhinda. “Kama Paulina anapika mboga, basi yeye aandae hata viungo ili asijikute amekaa tu.” Akaongeza Raza. “Hivi mmemuona huyo mtoto jamani au ni macho yangu tu!” Akaanza kwa ukali mama Ruhinda. Wote wakamgeukia.

Akiungua huku jikoni au akijikata! Hiyo kesi si itakuwa yangu mimi?” Andy akacheka na kutingisha kichwa. Akainama kwa kuchoka kabisa.

“Lakini mimi huwa napika kabisa! Naweza kupika kila kitu. Labda viwe vyakula vya kigeni.” Akaongea Mina kwa upole na unyenyekevu. “Na nitakuwa mwangalifu, sitajikata.” “Nyumbani kwenu. Lakini sio hapa kwangu. Hapa wewe ni mgeni, kakae sebuleni. Usubiri chakula.” Andy akamchukua Mina wake, wakarudi sebuleni kimya. Baba yake naye ni kama akajionya. Kimya. Mina akajisikia uchungu, akaona aende tu chooni akatulie.

~~~~~~~~~~~~~~

“Vipi lakini kazi?”  Pius akajaribu kubadili hali ya hewa pale akimuuliza Andy. “Nzuri tu. Tunaendelea.” Jinsi alivyojibu, hapakuwa na jinsi ya kuendeleza mpaka Mina akarudi na kukaa pembeni ya Andy. Akawasogelea mtoto wa Pius.

“Mina, kuna game za kwenye tv, unataka tukacheze?” Akauliza mtoto mdogo wa Pius. Mpaka mzee Ruhinda akacheka. “Mpaka watoto wanamuona ni mtoto mwenzao!” Akaongeza mama Ruhinda huko jikoni lakini kwa sauti ya juu ili kila mtu asikie.

“Mimi sijui kucheza hizo game. Labda unifundishe.” Mina akajibu vizuri tu. “Twende. Nirahisi sana.” Mina akamwangalia Andy. Alipomuona anacheka, akambusu shavuni bila hofu, palepale mbele ya ndugu zake na baba yake. Akasimama na kuondoka na mtoto wa Pius.

Kama alivyo Mina, akaanza kucheka kule chumba cha watoto anakocheza. Wakamsikia akicheka kwa sauti ya furaha kweli! Watoto wakawa wanacheza naye, Mina akawa ashasahau ya jikoni, anacheka, hana habari kama yuko ukweni! Kadiri alivyokuwa akicheka, wakamuona na Andy naye anacheka huku ameinama.

Alicheka vizuri Mina, ungejua hana hila moyoni mwake. Hata watoto waliokuwa wakisoma na kuchora wakahamia hapo kwenye game alipokuwa akicheza. Wakashindana kuendesha magari kwenye tv, watoto wanapiga kelele, na Mina naye anacheka kadiri anavyogongesha gari lake. “Mbona sasa mimi siwezi kama wewe?” Wakamsikia Mina anauliza huku akicheka. “Utazoea. Inabidi utulize mkono kabisa. Halafu uwe makini bila hofu.” Yule mtoto akawa anamuelekeza.

Mina alikuwa amekaa chini kabisa na mtoto mdogo wa Pius mwenye tabia kama mtoto wa kiume mpaka walisema alitakiwa awe wa kiume! Michezo yake mingi alipenda yakiume. Ndiye akawa sasa mwalimu wa Mina. Wakacheza hapo watoto wakifurahia. Hawakuwa wadogo. Vibinti vya miaka 10 kwenda juu.

 Huyo mdogo, Raza alimzaa akiwa amekata tamaa. Ndiye aliyekuwa na miaka 10. Wote wakajikusanya hapo kwa Mina. Hakuna hata aliyesoma au kufanya jingine ila kujisogeza hapo kwa Mina wakionekana kumfurahia. Wazazi wao wakahamisha masikio huko kwenye sebule ndogo ambayo wapo, wakawa wanawasikiliza wao.

Mama Mkwe!

Wakaja kuitwa na Raza kuwa chakula tayari. Mina na wale watoto wakatoka na kukuta kila mtu mezani. Mina akaenda kukaa pembeni ya Andy. “Nimeweza mwenzio.” Andy akacheka. “Nimesikia ulivyokuwa ukisababisha ajali!” Mina akaanza kucheka. “Dereva wewe lazima tuanze mafundisho ya nguvu.” “Lakini sasa hivi Mina amekuwa mtaalamu, anko! Ameshajua.” Mtoto mdogo wa Pius, aliyekuwa akimfundisha, akamtetea. “Kwa kuwa na wewe ni mwalimu mzuri ndio maana nimeelewa haraka.” Akaongea Mina na moyo wake washukurani. Ikawagusa wengi hapo mezani.

“Asante Mina. Utarudi tena tuje kucheza?” “Tutapanga na Andy. Halafu atazungumza na mama yako tuone.” “Yess!” Akasikika kufurahia mtoto wa Pius. “Kwa game huyu!” Baba yake akaguna.

“Wewe Mina umesema una miaka 22, umesomea mambo ya nini?” Mama Ruhinda akarusha hilo swali katikati ya hayo mazungumzo. Mina akatulia kidogo. Akajiweka sawa. “Ndio nasoma mambo ya kompyuta. Kudesign website, logo na mambo mengine.” “Hongera sana mama.” Akadakia mzee Ruhinda. “Asante.” “Unasomea wapi?” Akauliza Paulina. “TQ Tech.” Pakazuka ukimya, wakiangaliana kama wanashangaa.

“Ndio wapi!?”  Akauliza tena Paulina. “Ni chuo kidogo tu, kipo mtaa wa Samora.” Akajibu Mina taratibu tu bila hata wasiwasi. Andy akamsogezea chakula. Akapakua.

“Subiri kwanza Mina. Unasoma kompyuta kwa level gani?!” Akauliza mama mtu sasa. Mina akakunja uso akamgeukia Andy. Hakuwa hata ameelewa. “Anasomea certificate.” Akajibu Andy. Nakuzua ukimya mkubwa, mpaka Mina akashangaa. “Na mimi nataka kusomea kompyuta. Nilimwambia dad.” Mtoto mdogo wa Paulina akadakia.

“Kwa nini usomee certificate na sio degree?” Akauliza tena mama Ruhinda. Mina akamwangalia Andy. “Kwani hilo ni swali gumu huwezi kujibu mpaka Andy ndio akujibie?” Mama Ruhinda akauliza kwa ukali.Wengine kimya.

“Nimeanzia hapo, ndipo Ron aliponitafutia. Mwanzoni nilitaka kusomea sekretari. Ndio..” Wakamsikia Paul anaanza kucheka taratibu. Mina akamwangalia kama haelewi, kisha akaendelea.

“Lakini kwenye chuo hicho hicho kukawa na mambo ya kompyuta. Ndio nikamwambia Ron, nataka kusomea kompyuta. Ndio Ron akanilipia. Nikaanza kusoma kompyuta.” “Hiyo sio kusomea kompyuta. Unajifunza kutengeneza website kitu ambacho yeyote anaweza kufanya.” “Mama please!” Andy akalalamika.

“Nini Andy? Namueleza maana anaonekana hata haelewi ni nini anataka! Ameanza sekretari, amekuja kwenye kutengeneza website! Huhitaji kwenda shule kujifunza kutengeneza website. Ukiwa na kompyuta tu na Internet hata nyumbani kwako unajifunza.” “Kumbe!” Akashangaa Mina bila hila.

 “Kwanza shule ya form six ulimaliza wapi?” Akauliza tena mama Ruhinda. “Niliishia kidato cha nne.” Paul akashindwa kuvumilia, akacheka kwa sauti. Mina akashangaa. “Bwana jumapili ya leo nzuri sana. Karibu Mina kwenye familia.” “Asante.” Mina akamshukuru Paul aliyekuwa akicheka kishabiki, lakini alishukuru akiwa hajaelewa vizuri. Ila hakutaka matatizo kama kawaida yake, akajiambia atamuuliza Andy baadaye.  Lakini Paul akazidi kucheka na kuzidi kumchanganya Mina.

“Kwani nimekosea!?” Ikabidi Mina aulize sasa lakini akaonekana ameshaingiwa hofu mpaka uso ulionyesha wasiwasi. Akamwangalia Andy na wengine. “Mimi napenda nywele za Mina. Ndefuuuu! Halafuu nyingii. Zipo kama zimejiviringa hivi!” Mtoto wa Paulina ambaye ndio mrembo zaidi akaongeza. “Mimi nampenda mdomo wake. Yupo mzuri kila kitu.” Mtoto mkubwa wa Pius,  Poliny na yeye akaongeza akionyesha kumkubali sana Mina.

“Basi vile nilivyokwambia baba unipeleke wakaniwekee braces, mama akakataa ujue ningekuwa na meno yaliyojipanga vizuri kama hayo ya Mina!” Akalalamika mtoto huyohuyo mkubwa wa kwanza, mrembo  wa Paulina. “Mina wewe mzuri sana. Mama amesema nikinenepa kidogo tu, nisiwe kimbaumbau nitapendeza. Labda nitakuwa kama wewe.” Na mtoto wa Pius yule mdogo, mwalimu wake wa game, Mina, akaongeza. “Asanteni.” Paul akazidi kucheka mpaka alikuwa anatokwa machozi.

Mama Ruhinda alikuwa amebaki ametoa macho anamwangalia Andy, Andy anaendelea kula. “Kwa hiyo Mina wewe uliishia kidato cha nne tu?” Akauliza tena Paulina. “Ndiyo. Lakini sasa hivi nasoma. Nimeshachukua na fomu za IFM, Andy alinisindikiza. Nitaanza mwenzi wa 9 chuo kikianza.” Akajibu Mina taratibu. “Na mimi nataka kusoma IFM, mama, kama Mina.” Mtoto mdogo wa Pius akamwambia Raza mama yake nakumfanya Paul azidi kucheka.

“Ni mpaka uwe na cheti ndio wanakupokea. Kazana baby.” “Wala sidhani kama wana vigezo vigumu huko IFM. Mina si huyo ameishia kidato cha nne na yeye anaenda kusoma!” Akaongeza mama Ruhinda kwa dharau.

Mina akaanza kukosa raha. “Kula Mina.” Andy akaongea taratibu. “Kula.” Akaongeza Andy kwa kumbembeleza. “Sikutegemea Andy!” Akaanza tena mama Ruhinda. Andy akaweka kisu na uma chini na kumwangalia mama yake. “Mimi nashauri tumalize kula, mama.” Akasihi mzee Ruhinda taratibu.

“Kwa hiyo wewe unaona hivyo alivyokwenda kuokota hicho kitoto, kisicho na mbele wala nyuma ndio sawa?” Ugomvi akaununua mzee Ruhinda. Lakini kila mtu alijua hasira itamwishia yeye tu. Na yeye alifanya makusudi ili kumsitiri Mina pale mezani. Alishamuona amekosa raha.

“Ndiye tuliyeletewa mama! Mpe nafasi. Leo ndio siku ya kwanza kumuona. Mpe nafasi.” “Mtoto huyo anafanya naye nini? Ni project ambayo hatakaa akaimaliza! Amsafishe mpaka atakate. Haya, amsomeshe yeye na watoto atakao zaa! Atakuja kujenga kweli!” Mina aliumia sana.

“Kwa nini kwenda kujitwika mizigo mizito wakati wapo mabinti wazuri ambao hana hata haja yakuwahudumia? Anatafuta nini!?” Mina akamvuta Andy, Andy akampa sikio. Akaweka mkono, Mina akamnong’oneza. “Nyumbani kwenu wabaya Andy! Sio watu wazuri.” Akamwambia Andy masikioni huku akitokwa machozi.

“Samahani Mina.” Andy akanong’ona lakini sio sikioni, akimtizama usoni na kumfuta machozi. Mina akaweka kila kitu mezani. “Mimi naenda kula kwa mama Ron!” Akaongea Mina huku akisimama nakufuta machozi.

“Ungekula kwanza Mina. Kaa ule mama.” Akamsihi Mzee Ruhinda taratibu. “Mimi naenda kwa mama Ron! Mama Ron ukila hawezi kukwambia maneno mabaya. Hata kama umekosea, mama Ron anasubiri mpaka ule ndio anakwambia. Nyinyi kwenu ni wabaya.” Akaongea Mina akilia. Hapo anamjibu mzee Ruhinda.

Mnadharau watu.” Akaongeza Mina palepale mbele yao. “Kwetu hatudharau mtu yeyote yule. Mama na Ron walimkaribisha Andy, wakamuonyesha heshima na kumkarimu.” Mina akaongea kwa upole huku akilia. “Andy hajaniokota, amenikuta nasoma. Hata kama sio kitu cha maana ninachosomea, ila mama na Ron wameniambia najitahidi. Na ninapata zote 100! Mimi, mama yangu na Ron wananitunza vizuri tu. Wala sijawahi kumuomba mtu hela hata siku moja. Ron na mama ndio wananisomesha, wananinunulia kila kitu, wala sio Andy. Andy nampenda tu.” Mina akaendelea.

“Hata kama sisi hatufanani na nyinyi, lakini sisi hatuwaambii watu maneno mabaya! Na kila mtu akija kwetu tunampokea vile alivyo. Tunamkarimu na kumwambia maneno mazuri na ya heshima. Muulizeni Andy. Nyinyi ni wabaya, mnadharau watu. Na Mungu hapendi na amewasikia maneno yenu yote mabaya mliyosema juu yangu.” Kulikuwa kimya hapo wote ni kama hawakutegemea afanye hivyo. Kila mtu akimtizama Mina akiongea na kulia tena bila hofu mbele yao.

Andy akasimama na yeye. “Twende Mina.” Andy akamshika mkono na kumvuta pembeni. “Mimi naenda zangu kwa mama Ron! Wewe malizia kula na ndugu zako. Usiondoke kwenu, ila mimi naondoka. Kwenu ni wabaya, Andy. Hawapendi wageni na wanadharau watu. Ningejua kama hawafanani na wewe, mimi nisingekuja.” Mina akaendelea kuongea taratibu huku akilia, wote wakiwasikiliza.

“Twende nikusindikize nyumbani.” “Hapana Andy. Wewe baki tu. Nitachukua usafiri hapo nje. Nikifika kule karibu na nyumbani, nitamwambia Ron aje anichukue. Wewe malizia siku yako na ndugu zako. Ila mimi naondoka.” Wakasikia mlango unafunguliwa, ukafungwa. Kimya.

~~~~~~~~~~~~~~

Kishaumana Ukweni!

Wakiwa bado hawajaweka msingi wa kueleweka, matofali ya ndugu yameanza kuyumbisha penzi, hayajengeki!

Love At first Sight!

Inakuaje hapo?

Inaendelea…

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment