Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 11. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 11.

Historia Ngumu Ya Pam Na Chanzo Cha Kukwepa Wanaume.

“Pam?” “Naomba tusizungumzie huko.” Akamsikia hata sauti imebadilika. “Mimi mumeo, Pam. Na huu ndio mwanzo wa kufahamiana.” “Mume tena!” Akawaza Pam. “Nitakufahamu vipi kama kuna mambo unanificha?” “Mambo mengine ni fedheha. Tuyaache tu.” “Kwangu si fedheha maana mimi ndio wewe, na wewe ndio mimi. Aibu yangu ni yako na yako ni yangu. Hatuwezi kukwepana tena. Au unataka mahusiano yetu yawe na vificho?” Akazidi kumuweka sawa akimbembeleza. “Hapana. Lakini naona…” Akasita.

“Labda niulize. Baba yeye yupo wapi?” “Wakati Eric yupo darasa la sita, mimi latatu, mama alishika ujauzito wa mapacha. Wakati huo tulikuwa tukiishi na baba huko Ruvuma. Kipindi hicho au sijui uwezo, mama hakuwa na uangalizi wa kitaalamu wa hospitalini. Watoto walifia tumboni, yeye hakujua. Siku za kujifungua zikafika na kupita ikabidi kuanzishiwa uchungu. Sasa inavyoonekana kwenye kujifungua ndiko kulitokea makosa. Walivuta wale watoto lakini mama akaathirika vibaya. Akapooza kuanzia kiuno kuja chini. Na penyewe ni kama aliponea kufa.” Akaendelea.

“Baba alipoona mama amekuwa mzigo. Mtu wa kuhitaji msaada wakati wote. Hawezi kutembea. Hajui haja inatoka wakati gani, ni mtu wa kujisaidai hapohapo akatuchukua mimi na Eric pamoja na mama yetu, na kuturudisha kwa bibi na babu. Inavyosemekana alisema angerudi, lakini mpaka hivi tunavyozungumza, hakuna anayejua alipo. Hatujui kama yupo hai au la.”

“Mjomba huyo ninayeishi naye sasahivi, au aliyetuchukua ukubwani kutusaidia mimi na Eric alisema alishakwenda kumtafuta huko Ruvuma tulipokuwa tukiishi mwanzo, inavyosemekana alihama, hakuna anayejua alipo. Ndio hivyo. Tukaishia kuishi kwa bibi na babu.”

“Eric alipomaliza kidato cha nne, akafaulu shule za bweni. Akafanya vizuri mpaka chuo cha uhasibu. Akawa akiishi kwa mjomba huku akisoma. Akamaliza na kupata kazi benki, ndipo akafahamiana na Sandra. Akamuomba anipe kazi. Wakati huo mimi nilikuwa kijijini. Nilimaliza kidato cha nne, nikafeli. Kwa hiyo nikawa nipo tu hapo, tukisaidiana na bibi kumsaidia mama, maisha yakawa yakiendelea.”

“Bibi yangu ana roho nzuri sana. Anaupendo sana na wanae. Alimuomba mjomba amsaidie kudadisi kama kuna chochote kinaweza fanyika kwa mama. Wakati mimi bado nipo kule kijijini nasoma, mjomba alikuja kumchukua mama. Akasema kuna madaktari wamefika nchini, wanatibu wakina mama wenye kistula. Unajua aina hiyo ya ugonjwa?” “Hapana. Labda jina ndio limenichanganya.”

“Wale kina mama wanapata tatizo la kujisaidia baada ya kujifungua. Basi akasema atampeleka waone watamsaidia vipi. Nakumbuka bibi alikuja naye huku mjini. Alikuwa hataki mtu mwingine amuhudumie asije mnyanyasa mwanae. Kufupisha habari, mama alifanyiwa. Ikasaidia kwa kiasi. Anaweza kujisikia haja. Ila hana uwezo wa kushikilia kwa muda mrefu. Sio mgonjwa. Akikaa hivi, unaweza usijue kama ni mlemavu. Mambo mengi anafanya akiwa amekaa. Na bibi naye anajitahidi naye sana kufanya awe msafi. Kwa hiyo ukimkuta amekaa, ni mpaka akwambie.”

“Kwa hiyo hiyo ndio historia yetu. Mimi, Eric na mama. Nahisi hata nikija kukutana na baba yangu naweza nisimkumbuke. Ni muda mrefu. Na nafikiri na yeye aliweka juhudi za makusudi tusiwe na mahusiano naye. Maana anapajua kwa kina mama, ila amechagua kutorudi.” “Pole sana Pam.” Akasikia kuumia.

“Huwezi amini, Mill. Eti inaniuma sana. Nimeshindwa kuelewa kabisa, mpaka leo! Najiuliza ni baba wa namna gani anayeweza telekeza mke na watoto wawili, tena baada ya mwenzie kupata matatizo ambayo na yeye alichangia! Hakika inaniuma sana kiasi ya kwamba imenijengea chuki kwa wanaume. Naona wote ni matapeli tu. Wanakutaka kwa kukutumia tu. Unakuwa kama bidhaa tu. Yakutumia, wakishamalizana na wewe, wanakutupa.” Ndipo Mill akamuelewa kukwepa kwake wanaume.

“Wamejaa utapeli na usaliti.” Akaongea kwa uchungu na hasira. “Si wote Pam.” “Basi mimi sijabahatika kukutana na hao wazuri. Maana wote hao wanaolala na kina Lona. Au hao wanao wahiwa na kina Lona na wenyewe kukubali, wote ni waume za watu. Wanawahonga mahela ya aibu mpaka uchungu.” Akaendelea kwa hasira.

“Poliny amezaa na mume wa mtu. Na alimshikia mimba makusudi kwa sababu anayo pesa. Sasahivi amenunuliwa gari na anatunzwa na huyo mtoto. Sasa jiulize, huo uaminifu uko wapi? Kama hawa wanaume wangetulia, hiyo pesa wanayotumia kwa hao wanawake wa nje, si wangewekeza kwa wake zao na kujenga familia zao? Najiambia pengine ndicho anachokifanya na baba yangu huko alipo. Kupata starehe ya wanawake tofauti tofauti kwa garama anayolipa mama yangu na mimi.” “Pole Pam. Pole sana mpenzi wangu.” Akamtuliza maana aliweza sikia hasira moyoni mwake.

Mill Naye Na Ya Familia Yake.

“Na mimi nina historia inayofanana na hiyo ila tofauti kidogo. Imenifanya niwe makini sana na maamuzi yangu juu ya mapenzi, nikihofia nisije rudia kosa la baba yangu.” Mill akaendelea.

“Ninachoshukuru yeye hakuwa akitelekeza watoto. Alikuwa akizaa na kututunza. Mimi nililelewa na mama, lakini kwa pesa ya mzee. Japo mama alikuja kuolewa kwengine, lakini swala la kunitunza halikuwa likisumbua, kwa kadiri ya uwezo wake. Nilipofika kidato cha nne, mama mzazi alifariki.” “Pole Mill.” “Asante.” “Pole sana.” “Nashukuru.”

“Akatuacha watatu sasa. Mimi na wadogo zangu. Baba wa kambo naye akaoa. Ndipo akanitaka niondoke.” “Hee!” Mill akacheka. “Ukifikiria, ni haki yake Pam! Undugu wetu ulikuwa kwa mama. Mama hayupo. Kinachonibakiza kwake ni nini?” “Na wadogo zako!?” “Wao hawakutaka kusoma. Waliacha shule mapema sana na kuingia mtaani kujitegemea wakiwa wadogo tu. Wote wawili ni wakiume. Kwa hiyo kubakia pale ndani na mke mpya, akaona shida.”

“Haya, nikamtafuta baba. Hakuwa na neno. Kuja kwenda kwake! Huku Dar sasa. Kumbe sikuwa peke yangu. Kuna watoto wengine nao wanatunzwa kwa huyo mwanamke, napo hapo hana ndoa. Ni mwanamke aliyezaa naye watoto wawili. Wakike na wakiume. Huyu mwanamke akaonekana amemuweza. Akambana na kufanikiwa kuishi naye hapo kwenye hiyo nyumba kubwa niliyowakuta wakiishi. Ndio sasa na yeye anakaribisha watoto wake hapo, kitu kilichokuwa kikimkera huyu mwanamke.”

“Kumbuka sikuwa peke yangu. Kila mtoto anatabia zake. Na yeye huyu mwanamke ni wale wanawake walio jiendeleza, anamsimamo wake jinsi ya kulea watoto wake. Sasa kuchanganyiwa na watoto waliolelewa na wakina mama tofauti tofauti! Wengine tumekutana hapo ukubwani, hawataki shule wala kazi. Wengine wazurulaji. Wengine walevi na bangi za ujanani. Ni fujo kwa yule mama, na yeye hawezi ondoka pale, maana tayari anao watoto wawili na mzee. Maendeleo mengi ya mzee aliyapata na yeye akiwepo. Anajiaminisha kama ndio mke halali.”

“Ila hakuwa na mapenzi hata kidogo na huyo mwanamke. Kila wakati anamwambia akichoka, au akiona watoto wake ni mzigo, aondoke amuachie watoto pale, atatafuta mwanamke mwingine atakayeweza ishi na vijana wake.” “Mill!” Pam akashangaa sana.

“Acha mama. Mazingira ya ujabu na udhalilishaji wa hali ya juu, mimi sikuwahi ona. Maana kule kwa mama yangu mzazi, kulikuwa na kuheshimiana, japo hapakuwa na uaminifu. Lakini mzee wa kule alikuwa akifanya mambo yake kwa wizi, mama asijue.” Mill akaendelea.

“Sasa kuja kuishi na baba mzazi! Na kwenye mazingira ya mama anayewalalamikia kila wakati! Kwanza mzee mwenyewe alikuwa hashindi nyumbani. Watoto wake wenyewe utajua kabisa hajasingiziwa. Ni wake. Umbile ni kama hivi unavyoniona mimi. Tulizaliwa wote wakubwa kama baba. Mbali na muonekano, wengine tabia ni kama za mzee. Walevi na wahuni kama mzee mwenyewe.” “Jamani!” Pam akazidi kushangazwa.

“Acha mama. Nakwambia nilitoka kwenye familia, nikahamishiwa kwenye aina hiyo ya fujo, halafu aliyenikaribisha mwenyewe hayupo hapo. Kumuona mara chache chache. Akirudi ni usiku, amelewa. Ukimtaka ni udamke naye kabla hajatoka kwenda kazini.”

“Mchana yupo kazini, na biashara zake, baada ya hapo, jioni anakuwa baa na wanawake wengine. Mimi nikakazana kusoma. Hakuwa na shida na si mchoyo na pesa yake, nafikiri ndio maana wasichana walikuwa wakimpenda. Alinisomesha bila shida. Na mpaka sasa ananisaidia japo naona anakaribia kushindwa.” “Sababu ya ugonjwa?” Pam akauliza.

“Ugonjwa umemnyong’onyesha. Halafu imekuwa zile mbio za sakafuni. Amefika ukingoni. Kwa asilimia fulani inabidi ajirudi sasa kwa huyu mama, ambaye amemuumiza kwa miaka yote. Anajirudi akiwa mgonjwa, anaanza kuoza! Huyu mwanamke kama binadamu hana furaha naye. Maana uzima wake alikula na wanawake wengine, sasahivi ndio anajirudi! Kwa asilimia kubwa utaona jinsi anavyo mnyanyapaa. Ndio maana nikisikia amezidiwa, narudi kumuuguza.” “Na ndugu zako wengine?” Akamsikia Mill akicheka kwa masikitiko.

“Wewe tuombee watoto wetu tu. Uzazi si kila kitu, mama. Yaani wale watoto wapo kunufaika tu. Na nina uhakika sasahivi mzee anamajuto, hawezi sema. Maana hata watoto wa huyu mama anayeishi naye sasahivi, walimuona jinsi mzee anavyoishi na mama yao, basi na wenyewe ni kama wamemzira mzee. Hakuna anayemjali sana, ndio maana inabidi mimi kuingilia kati. Nikiwepo mimi ndio angalau mambo yanaenda. Nikiondoka tu, kila mtu anampuuza. Na mwenyewe anajua ndio maana hataki kukaa tu nyumbani. Na kwa kuwa ni kazi ya serikali, basi anakwenda hivyohivyo.” “Pole Mill. Pole sana.”

“Asante. Kwa hiyo kwa kukua nikiona hizo fujo kotekote, kwenye familia ya baba na mama, kumeniongezea umakini sana. Maana nasikia na babu naye alikuwa hivyohivyo kama baba. Na vijana wa baba wapo hivyohivyo. Najionya kwa kujikumbusha kila wakati kuwa makini. Nikishajiingiza sehemu nikaona hakuna muelekeo, siwekezi muda wangu wala mapenzi. Najitoa mapema sana.” “Na huko nako kuna mapenzi ya kitapeli? Maana kwenye movie mnaonekana tofauti!” Alicheka Mill. Alicheka sana.

“Usicheke hivyo bwana! Inamaana wewe hujabahatika hata mzungu?” Alizidi kucheka Mill mpaka kupaliwa. “Bwana Mill!” “Mimi naona sina bahati. Sijapata mzungu.” “Mmmh! Kwa nini sasa? Hutaki watoto wakishombeshombe?” Alimfanya azidi kucheka. “Mimi nahisi wewe haupo serious.” “Huku michezo michezo ya kijinga utajikuta unanasa wewe mwenyewe.” Akawa hajaelewa.

“Kuna ambao wanaweza jitegesha makusudi, wapate mimba uanze kuwatunza. Zaidi weusi wa huku. Na mimi hilo nimekataa. Si nishakwambia nataka nirekebishe makosa ya kuanzia babu yangu?” “Nakumbuka.” “Basi mtindo wa kuonja onja visivyo vyangu, sina. Nikikwambia naiapisha nafsi, jua nafanya kwa makusudi kabisa. Sitaki kujiingiza matatizoni kwa tamaa za muda mfupi. Nipo makini huko na huku. Nikikwambia upo peke yako huko na huku wala si kwa kukupamba.” “Lakini hunifahamu Mill wewe! Kama na mimi tapeli je?” Akawa kama anamuonya.

“Usidhani nazungumza na wewe hapa nachoma muda wangu bure! Nishakuchunguza, nishajiridhisha. Labda tu uniambie kama hunitaki.” Kimya. “Pam?” Kimya. “Unanikana mama watoto wangu?” Akamsikia Pam anaanza kucheka. “Naona unataka kunikana mapema kweupee! Au maneno ya Lona yamekuingia?” “Hata kidogo. Ila wewe ndiye umemkasirisha. Ulikuwa unawanunulia vyakula, gafla unawaambia huna hela!” Alicheka Mill. Akacheka sana.

“Mwenzio alikuwa anajivunia kama nini! Kwamba amepata mmarekani ” “Lona si mwenzangu. Mwenzangu ni Pam. Na honga yote ile wala si kwa ajili yake. Nia yangu ilikuwa WEWE.” Alicheka Pam. Alicheka sana. “Acha masihara Mill!” “Mimi nimlishe Lona na wenzie kwa kipi mno!?” Akamfanya Pam azidi kucheka.

“Hakika mimi sikuwa na habari! Mwenzio mimi nabania pesa. Sikosei kuja kazini bila chakula. Shangazi analalamikaga, lakini sijali. Kikipikwa usiku, nakula nusu, nusu naweka cha mchana nile kazini. Na kitafunwa najitahidi pia kubeba. Si thubutu kumwaga pesa yangu mjini kwenye migahawa.” “Ndio maana kila nilipokuwa nikiuliza umeagiza nini, naambiwa hujaagiza. Lakini ndio hata maji ya kunywa ulikuwa hutaki Pam wangu au kunitesa tu!” Pam akazidi kucheka.

“Mimi nakunywa maji ya bure ya palepale kazini!” “Mmmh! Ulinifanyia kusudi tu bwana!” “Halafu sikutaka fujo na Lona. Ni muongeaji sana.” “Na ndiye anayeninyima raha. Maana najua akijua kama tunawasiliana, atakuingiza matatizoni.” Akatulia.

“Pam?” “Inabidi kuwa makini. Ila sijui mpaka lini!” “Muda utajibu. Usiwe na wasiwasi. Ninachotaka ni kukutoa barabarani usiku. Hilo sitaweza kufikiria mpaka nifanikiwe.” Akajua anazungumzia gari. “Usiwe na wasiwasi. Mimi nipo salama.” “Siwezi kutokuwa na wasiwasi, Pam. Hapana. Nipe tu muda mpenzi. Tutarekebisha kote. Kwa shangazi na usafiri. Tutaangalia kipi kianze.” Pam akatulia akimfikiria Mill. Alikuja na gia kubwa huyo! Mpaka akamfunga akili Pam. Simu ya kwanza tu, wanazungumza na kupanga kama wanandoa!

 “Naomba nikuombe jambo moja muhimu sana kwangu, Pam.” “Ni nini?” Pam akamuuliza taratibu akimfikiria huyo Mill anataka kuomba nini! “Naomba tukubaliane jambo. Ndio uwe msingi wa mahusiano yetu, ambao tutausimamia mpaka mwisho.” Pam akashangaa.

“Upo au nishakutisha.” “Nakusikiliza Mill.” “Nashukuru. Naomba tubakie wawili tu.” Pam akamuelewa. “Mimi si muhuni Mill!” “Hapana. Sijamaliza.” Ikabidi atulie. “Kuachana kwetu iwe ni mpaka tuzungumze kama hivi. Isitokee maneno ya kusikia yakakufanya ukaniacha, ni mpaka uhakikishe kutoka kwangu mimi mwenyewe. Tuzungumze, ndio tukubaliane. Na mimi hivyohivyo. Kama hujanisikia mimi mwenyewe kukwambia tuhitimishe, makubaliano yetu yanabakia ni mimi na wewe tu.” “Mill wewe!” Pam akashangaa sana.

“Wewe upo huko. Mimi nipo huku. Ukipata mwanamke huko, ukaamua kuachana na mimi?” “Bila mimi mwenyewe kukwambia, chochote utakachosikia ni batili. Nisubirie mimi mwenyewe nikwambie. Na nakuahidi sitakusaliti. Sitakutelekeza. Kilichotokea kwa baba yako, naomba usinifananishe na mimi.”

“Nakusudia kufanya tofauti na baba yangu. Na naomba uwe na mimi. Tujenge familia yetu. Tuwape watoto wetu kile sisi tumekosa. Au unaona ni ngumu sana?” Kimya. “Au unaona nimeharakisha sana? Kwamba ningevuta muda kwanza. Na maneno mengi ndipo baadaye nikwambie?” Kimya.

“Mwenzio najua ninachotaka. Na maadamu nimekupata wewe, sitaki kuvuta. Nakupenda Pam. Nakupenda sana. Ninapokwambia upo mawazoni mwangu, amini umefanikiwa kuingia moyoni mwangu siwezi kujisaidia. Ndio maana unaona nimejisalimisha kwako mapemaaa!” Kimya.

“Unanitisha Pam wangu! Ndio unanikataa?” “Hapana Mill! Ila sikuwa nimejiandaa. Nipo kama nimepatwa na mshituko.” “Pole. Nikuulize swali?” “Niulize tu.” “Nitangulie kuomba radhi pengine ndio lilitakiwa swali la kwanza. Upo kwenye mahusiano yeyote?” “Nisingeomba mawasiliano na wewe, Mill. Wala nisingekuwa na wewe kwenye simu muda wote huu.” “Nashukuru. Basi kama hakuna mtu, naomba mimi niwe kwenye kuchunguzwa. Ukiridhika na mimi, uniambie. Sawa?”

“Sawa. Na samahani Mill. Kwenye swala la mahusiano naomba niwe mkweli. Nimetishwa sana na wanaume. Na kwa kadiri ninavyoona wanaume wengine wanavyofanya hata pale ofisini kwetu na wanawake! Imezidi kunitia woga. Unajiuliza mwanaume huyuhuyu yupo na mke nyumbani, bado yupo na wanawake wengine nje! Anamwaga pesa nyingi kwa mwanamke wa nje, anabakisha nini kwa mkewe? Inawezekana alianza hivyohivyo kwa mkewe. Akihonga mapesa. Alipomuoa na kumuweka ndani ndio akageuka kama baba yangu! Inaniuma! Inaniuma sana na kunitisha.”

“Pole Pam.” “Hivi unavyoniona mimi, ni kama mama alijizaa. Inamaana thamani yake iliisha pale tu alipopatwa na matatizo! Kweli jamani?” “Nisikilize Pam na acha kulia. Mimi si baba yako. Na nimekusudia kuwa na wewe. Utakaposema ‘ndiyo’ kwangu, na ukatulia na mimi, jua mimi ndiye nitakuzika au wewe ndio utanizika. Katika shida na raha, jua hutanikwepa. Nitasimama na wewe bila kuchoka. Unanielewa? Na sina sababu ya kukudanganya. Kwanza kwa nini nikwambie yote haya? Si ningeishia salamu tu na maongezi ya kawaida kawaida tu?” “Lakini kweli!” Akawaza kwa sauti.

“Kulikuwa na faida gani au haraka gani ya kukwambia yote haya na nisha kupata kwenye simu? Si nisingeyaleta yote haya! Nayaleta kwa sababu mimi mwenzio nishaona mpaka uzee wetu. Pam aliye bibi si mrembo kama sasahivi.” Akamfanya Pam acheke.

“Kabisa.” “Basi Mill. Nimekuelewa. Mimi nitatulia na wewe.” “Na hakuna kuhitimisha hewani. Kama tulivyoanza kwa mazungumzo, tutahitimisha mimi na wewe kwa mazungumzo.” “Sawa.” “Kwa hiyo nijihakikishie Pam ni wangu?” Pam akacheka sana.

“Mill ulivyo na haraka!” “Sitaki michezo ya barabarani. Mwenzio najitunza Pam. Sitaki kuchezewa.” “Hutaki hata tufahamiane kwanza!?” “Nataka, lakini tukiwa sisi tu. Tusichanganye watu hapo katikati. Iwe mimi na wewe tu. Tujuane mapungufu yetu na lengo iwe kusaidiana ili tuendelee, sio tufahamiane halafu tukimbiane.” Mill alikuwa mtu wa kuzungumza vitu sahihi vya kumvutia Pam, mpaka akamuweka sawa. Yaani mpaka wanaagana, wawili hao wanazungumzia maisha ya pamoja si kutengana kama wanao anza, ila wanao endelea.

~~~~~~~~~~~~~~

 Pam akalala usingizi mzuri. Na alishavutiwa na Mill. Kwanza muonekano tu wenyewe analipa. Halafu mwanaume anayezungumzia uzee wake! Mkweli kwake! Hajaanza kama wengine kumtongoza kwa majigambo! Pam akajiaminisha amepata.

Asijue furaha aliyoweka kwa Mill. Huko alikuwa akishangilia mpaka Mike akajua usiku huohuo kama Mill safari hii amepata. Alijawa mipango mpaka Mike akamuhurumia na kumuomba atulie kwanza.

“Taratibu Mill! Tafadhali tulia, mchukulie taratibu sana, asije kuja kukufanya kichaa pindi akikusaliti. Tulia kaka.” “Hakika situlii mpaka mimi ndio niwe wa kwanza kumfikisha kanisani. Nikishamuoa. Nikafanikiwa kupata naye watoto. Hapo ndio nitatulia.” Akafikiria akajipinga. “Hapana. Kwa Pam sitatulia aisee! Labda kaburini.” Akaongea akiwa amejawa tabasamu. Akikumbuka sauti ya Pam na uzuri wake! Akatamani angekuwa karibu. Lakini ndio amerudi nchini. Akapoa. Akivuta subira.

Jumatatu.

Mahusiano yakaanza rasmi kati yao. Ila hata Mina alijua Andy anampenda. Alimchukulia taratibu, vile alivyo. Siku ya jumatatu alipotoka shule, akaenda ofisini kwa kaka yake. Akakaa nyuma ya meza yake kama kawaida. Chini kabisa, akaanza kufanya kazi zake.

“Kiongozi huna kazi zako unataka kufanyiwa mtandaoni?” Hatibu akamchokoza Andy alipoingia hapo ofisini kwao. Andy akawa hajaelewa. “Tuna kampuni yetu tumefungua mimi na Mina. Mimi meneja masoko. Natafuta wateja, halafu nampelekea bosi wangu Mina.” Andy akamsikia Mina anacheka nyuma ya meza. Watu wengine wakaanza kucheka.

“Bosi wako anafanya kazi kwenye mazingira magumu kweli!” Mwenzao akadakia. “Mwanzo mgumu. Au unasemaje bosi wangu?” Hatibu akadakia. Mina akaanza kulalamika. “Ron mnyanyasaji! Ananifukuza mezani kwake, anasema nitamuangushia vitu vyake, wakati mimi nimetulia.” “Wewe hutulii bwana! Unanifanya nashindwa kufikiria. Kaa tu hapohapo.” Ron akamjibu huku akiendelea na kazi.

Andy akaenda kumchungulia pale chini alipokaa. Akaanza kucheka. “Sasa hapo haumii?” “Nitafanyaje? Ron amenifukuza mezani.” Mina akalalamika. “Njoo ofisini kwangu.” Mina akaanza kucheka huku anaziba mdomo. Ron hata hakunyanyua kichwa kuwatizama, akaendelea na kazi zake.

“Twende.” Akazunguka kule nyuma alipokuwa amekaa Mina, akamkusanyia vitu vyake vyote. “Andy!” Mina akanong’ona kama anayesita. Andy akamshika mkono na kumnyanyua pale. Pakazuka ukimya kila mtu akiwa kama anashangaa, hawaelewi. Andy ni kiongozi wao, na wanajua yupo na Lora! Iweje leo Mina anakaribishwa ofisini kwake kwa staili ile! Utani wote ukaisha. Andy aliweza jua hali ya pale imebadilika gafla kwa alichofanya. Akaondoka na Mina, akamuingiza ofisini kwake.

Penzi Kikohozi!

Kisha akatoka. “Naombeni niweke jambo moja wazi. Kwa kuwa sina ninachoficha.” Kila mtu akamgeukia Andy. “Nilitaka kuliweka wazi hili ili mjue na kuelewa tu. Nipo kwenye mahusiano na Mina. Nimeona niliweke wazi kwenu kama wenzangu hapa kazini na kwa kuwa mlishakuwa mkimuona Lora akifika hapa. Lora ametambua uwepo wa Mina kwenye maisha yangu, na yeye Lora kama binti tuliyekuwa naye tokea watoto, ameelewa na ameheshimu hilo.”

“Na sisi tutaliheshimu hilo Kiongozi.” Akadakia mfanyakazi mwingine ambaye yupo hapo na kina Ron. “Nafikiri tunatakiwa kusema hongera.” Ukaanza utani kidogo, angalau ile hali ya wasiwasi ikatulia pale, Ron hakuchangia lolote akawa anaendelea na kazi. Andy akarudi ofisini alipokuwa amemuacha Mina.

Mina alifurahi sana. Akamkuta akicheka. “Unacheka nini?” “Nimefurahi. Nilikuwa naogopa!” Andy akacheka. “Nilikwambia sina kitu chakuficha.” “Sasa hivi nimeamini.” “Kwa hiyo ukiwa unakuja, unakuja kujisomea hapa.” Mina akafikiria kidogo.

~~~~~~~~~~~~~~

 “Nini?” “Tunatofautiana sana Andy.” “Kivipi?” Andy akauliza lakini alijua wazi ni kweli. “Upo na ustaarabu fulani hivi! Ambao mimi sina!” “Usiogope. Taratibu utajikuta tunaanza kufanana. Kikubwa ni mimi na wewe tuelewane. Mengine nitajifunza kutoka kwako na wewe utajifunza kutoka kwangu. Kile unachokiona kinatakiwa marekebisho, niambie ili tuzungumze.” Hapo Mina akaridhika.

“Basi naomba nifundishe kula kama wewe.” Andy akacheka. “Unapenda?” “Sio mbaya nikijua, ili tukifika kwenye migahawa kama ile uliyotupeleka jana, na mimi nijue jinsi ya kutumia vile vitu vyote.” Hilo likamfurahisha sana Andy.

 “Basi nitaandaa chakula kesho jioni, halafu nitakufundisha jinsi yakutumia vifaa vyakulia chakula, si ngumu.” Mina akafurahi na kubaki akitizamia siku ya kesho, ajifunze. Akakaa hapo na Andy mpaka jioni, wakatoka pamoja.

Jumanne.

          Siku inayofuata, jumanne, Mina alitoka shule, alipoingia tu ofisini kwa kina Ron, Lea akamuita kwa kumkonyeza. Mina akaanza kucheka. “Mtoto mbaya wewe!” “Nimefanyaje dada yangu?” Mina akauliza huku akicheka. “Umekaa hapa, unakataa dagaa kumbe unaye sato wako unambanika taratibu!” Mina alicheka mpaka akakaa.

“Hongera mwaya Mina mdogo wangu! Andy ametulia na anajiheshimu.” “Asante.” Mina akajibu kwa aibu. “Na utulie hivyo hivyo ili usimpoteze. Lakini nakuaminia mdogo wangu. Wewe umetulia.” Mina akacheka, akijua Lea hamfahamu hata nusu.

Mlango wa Andy ukafunguliwa. Akatoka. “Nilijua umepotea!” “Nilikuwa namsalimia dada Lea.” Mina akasimama na kumsogelea. “Vipi mtihani?” “Tumefanya kwenye kompyuta, tukapewa majibu yetu hapohapo. Nikisema, utafikiri najisifia. Heri ujionee mwenyewe.” Andy akacheka huku wakiingia ofisini kwake.

Baada ya muda wakatoka wawili hao. Andy akaaga kuwa wataonana kesho, wakaondoka. Ilikuwa saa 11 kasoro. Mina akampigia simu mama yake na kumwambia anakwenda nyumbani kwa Andy. Mama yake akajibu tu, ‘sawa’.

Nyumbani kwa Andy Tena Ila Kwa Sura mpya.

Walikwenda mpaka nyumbani kwa Andy. “Nilishatoa nyama yenye mfupa na kuilainisha. Nikupika tu kidogo kwa muda mfupi. Unataka kujifunza kuandaa meza?” “Hapo nitakuwa nimejifunza vitu viwili kwa wakati mmoja.” Andy akacheka. Akamvuta karibu. “Unanifurahisha Mina! Una moyo mnyenyekevu na kupenda kujifunza.” Mina akacheka taratibu.

“Asante.” Andy akamwangalia kama apate busu, akaona awe mpole. Akamwachia. “Naenda kubadili nguo, nakuja. Kama unataka kuzunguka kupaona humu ndani, karibu.” “Niambie nikuandalie nini jikoni.” “Hapana. Mapishi yenyewe ni rahisi sana. Sipiki kitu kigumu. Nakuja sasa hivi.” Akamuacha pale.

Akatoka na sweatpants ya kijivu na t-shirt nyeupee. “Andy wewe ni msafi!” “Nimeishi na mapadri. Hapakuwa na jinsi yakutokuwa msafi. Kila kitu kilitakiwa kiwe sehemu yake. Sasa hiyo ni kwa miaka yote nimekua nao tokea mtoto mpaka mtumzima! Sina jinsi nyingine ninayojua inatakiwa iwe, isipokuwa hivyo. Maana hapakuwa na uchaguzi. Hata kama hutaki ilikuwa lazima uwe kama wao.” Mina akamfuata nyuma.

Akaanza kumuelekeza jinsi ya kupanga meza na vijiko. Kipi kikae upande upi. Mpaka Mina akamaliza wakati Andy anaendelea kupika. Akamtolea vitambaa vya napkins. “Njoo navyo hapa jikoni nikufundishe vile wanavyovikunja kama hotelini kwa muundo tofauti tofauti.” Mina akaanza kujifunza taratibu.

Hatua kwa hatua, mpaka akaweza. “Unaakili sana, Mina!” Mina akacheka sana. “Kweli! Sidhani kama kuna kitu utataka kujifunza ukashindwa.” “Asante Andy. Na wewe ni mwalimu mzuri.”

Wakahamia mezani. Akaanza kumfundisha jinsi yakushika kisu na uma. Sehemu gani yakuweka napkin ili asijichafue na pia kutumia kujifutia wakati wakula. Mina akajitahidi kufuata maelekezo.

Kutumia uma na kisu kula nyama yenye mfupa, ikawa ngumu, akamuhurumia. “Basi nenda kanawe mikono uje ushike kwa mkono.” “Sasa nitajifunzaje? Acha nihangaike tu mpaka niweze.” Mara kadhaa nyama ilianguka nje ya sahani kabisa. Anaokota na kuirudisha kwenye sahani.

Akamuona ameanza kukata tamaa. “Niangalie Mina.” Akamwangalia. “Ili hiyo nyama isianguke, lazima uishikilie vizuri kwa uma. Kandamiza uma vizuri kwenye sehemu yenye mnofu. Ukishaona umeishikilia vizuri, ndio ukate sasa.” Akajaribu. Akamuona anacheka. Akajua anaanza kuelewa.

Kidogo ile hali ya wasiwasi ikapungua usoni. Japokuwa hakuweza kuacha mfupa mtupu bila nyama kama Andy kwa kutumia hizo nyenzo, lakini akafurahia kuona na yeye angalau ameweza kukata na kula kwa kisu na uma.

Walimaliza kula, wakaongea kidogo wakicheka. “Nifundishe na hivyo unavyoshika glasi.” Andy alicheka mpaka akapaliwa. “Mina!” “Kweli bwana! Nataka na mimi niwe wamaana.” “Wewe ni wamaana hata kama hutakula kwa kisu na uma. Bado wewe ni wa maana. Hii ni njia tu ya kula.” Mina akajisikia vizuri. Akasimama na kwenda kumbusu shavuni.

“Asante Andy.” Andy akacheka na kumvuta, akamuweka mapajani. Mina akawa amemkalia mapajani. Akamvuta mkono na kuubusu mara kadhaa huku akimtizama. “Nakupenda Mina. Nafurahia kuwa na wewe kila wakati.” Mina akacheka taratibu. “Asante Andy.”  Akambusu shavuni na kusimama.

“Mimi ndio nakuoshea vyombo. Umepika, naosha vyombo.” Andy akacheka tu. Wakasaidiana kutoa vyombo, wakipeleka jikoni. Mina akaanza kuosha wakati Andy anasafisha meza, alivyomaliza akamfuata jikoni.

Akabaki akimwangalia anavyoosha vyombo pale kwenye sinki. Mina akageuka. “Unawaza nini? Mbona kimya?” Mina akamuuliza na kuendelea na kuosha vyombo. Kimya.

“Andy?” Akamuita na kugeuka kabisa baada ya kumuona yupo mbali kimawazo. “Usiwe mbali bwana wakati mimi nipo hapa!” Mina akalalamika nakumfanya Andy acheke. “Sasa unawaza nini?”  “Nakufikiria wewe!” Mina akakausha mikono akamsogelea.

“Nini tena?” Mina akauliza kwa upole na kuongeza swali jingine. “Kuna kitu nimekuudhi au nimekosea?” Mina akauliza kwa wasiwasi. “Hapana. Lakini sidhani kama unajisikia ninachojisikia mimi, Mina!” Mina akashangaa kidogo. “Kivipi tena!?” “Ahhaaa! Sijui.” Andy akatoka nakurudi sebuleni, Mina akamfuata na kwenda kukaa pembeni yake.

“Kwa nini unasema hivyo Andy!?” Mina alikaa pembeni akisugua mikono yake kwa hofu, akajua ameshaharibu. “Unajua nilishakuwa na Lora nikiwa nimeshakuwa na wewe. Vile nilivyokuwa nikijisikia wakati nakushika wewe, ni tofauti nilivyokuwa nikimshika Lora. Ikaanza kuwa shida hata kumgusa! Na alikuwa akinigusa nilikuwa nikijitahidi kumkwepa kama hivi wewe unavyonikwepa mimi.” “Sikukwepi Andy!” Andy akabaki akimtizama.

“Kweli Andy!”  “Ila ni nini? Hivi unajua ni mara ngapi nimekuwa nikijaribu kukubusu na kukumbatia na wewe kunikwepa?” “Andy!” Mina akaishiwa nguvu. Akamsogelea na kumshika. “Sitaki ufanye kwa kuwa nimelalamika Mina.” “Hujui ni kiasi gani nafurahia ukinigusa Andy! Napenda unavyonishika na kila kitu, lakini...” Mina akasita.

“Nini?” “Nakosa ujasiri Andy!” “Kwa nini!?” Andy akashangaa. “Andy!” Mina akamshangaa kama vile asichoelewa ni nini! “Tafadhali niambie. Sielewi tatizo ni nini!”

~~~~~~~~~~~~~~

Love At first Sight.

Bado tofali zinapangwa. Kutoka kuona, kupenda, mpaka kuweza kuja kuishi pamoja, ni safari ndefu inayotakiwa kujuana, na kuvumiliana mbali na hisia.

Inaendelea…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment