Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 7. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 7.

 Kile kitu kikabaki moyoni kwa Pam, asielewe. “Kwamba amekuja kuniaga mimi!” Pam akahisi hakuwa amemsikia vizuri. Mill aliondoka nchini bila ya kupata muda mwingine tena na Pam. Alikaa miezi sita ndipo akarudi tena nchini. Baba yake alikuwa mgonjwa. Ndio alikuwa anaanza kuumwa. Alifika na kwenda hospitalini moja kwa moja. Akakaa na baba yake lakini akiwa na kina Mike, Kamila. Baadaye Jerry na mkewe Sandra nao pia wakawasili hapo hospitalini. Nia kumuona mgonjwa na huyo Mill mwenyewe.

Baada ya hapo ilikuwa jioni tu, wakaamua kwenda kula Mlimani City. Wakati wakila, Lona akampigia Sandra akimpa muendelezo wa mambo ya kazini, akagundua yupo hapo, na yeye hakuwa mbali, akaamua kumfuata kumkabidhi baadhi ya karatasi ya hicho walichokuwa wakizungumzia.

Akili ilimpaa alipofika na kumkuta na Mill naye yupo! Alifurahia Lona, mpaka akakaa kabisa bila hata ya kukaribishwa! Tena akavuta kiti karibu kabisa ya Mill. Akaanza kuzungumza yeye, akitaka kumsikia Mill. Habari za huko na mengine mengi ilimradi tu. Isitoshe akaomba na picha ya kumbukumbu siku hiyo. Wanao mjua Mill walijua wazi hafurahii ila kuwa muungwana tu kwa Lona. Alipoona hamalizi, amejaa hapo katikati yao, akichangia kila mazungumzo kama aliyepagawa, Mill akaomba arudishwe nyumbani, amechoka na safari.

~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake asubuhi ofisini ikawa nongwa. Habari ikabadilika. Ikawa Mill amerudi nchini, wametoka kwenda kula. Lona akajigamba kwa hili na lile juu ya Mill, mpaka akamchefua Pam aliyeanza hata kumfikiria Mill. “Ni wale wale tu.” Akajuta hata kumpitisha akilini mwake.

Alipotoka hospitalini kumuona baba yake mchana, moja kwa moja ofisini kwa Jerry. “Pam yupo?” “Acha nikutahadharishe, Mill. Ile picha aliyoomba jana Lona, akisema kama ukumbusho, imezagaa hapa ofisini, imekua gumzo.” Mill akashangaa sana. “Kwa nini tena!?” Akamueleza.

Haiwezekani Jerry!” “Nakwambia tena. Na hii ofisi ni ndogo na SHERIA yake kubwa na ya kwanza ambayo wamekubaliana mpaka hata kwa Sandra ni kama nilivyokwambia. Msichana ANAYEMUWAHI mwanaume hapa, MWIKO kwa mwanamke mwingine hata kumtizama kwa jicho la pili.” “Lakini Lona si mwanamke wangu!” “Maadamu amekuwahi, basi hapa inachukuliwa tayari wewe ni wake. Na katika hilo hata Sandra ilibidi kulisimamia ili kufanya hawa wanawake wanne, waweze kufanya kazi bila malumbano. Maana walishapigana hapa. Lona huyohuyo na mwenzie. Safari ile hukumkuta, alikuwa amejifungua. Sasahivi yupo. Ndio wakawekeana hiyo sheria mpaka kusainishana kwa Sandra.” Mill akatamani kurukwa na akili.

Haiwezekani Jerry!” “Nenda kamuulize Sandra hapo ofisini kwake atakwambia.” “Nampenda Pam, siwezi kukubali kirahisi! Japokuwa nimekuja kumuona baba, lakini nilikuwa nikikusanya pesa, ili nije kukaa kidogo, nijaribu tena kwa Pam. Lona hawezi akanifanya nikamkosa Pam.” “Nahisi katika hilo ushachelewa. Inamaana Pam ameshajua kila kitu. Amejua upo nchini kwa ajili ya Lona.” “Sio kweli!” Mill akapinga kwa uchungu kabisa.

“Lakini ndivyo wote hapa wanavyojua, tena kutoka kwa Lona mwenyewe na ushahidi juu. Picha. Utapinga vipi?” “Ninachojua ni lazima niwe na Pam.” Jerry akanyamaza. Asijue safari hii anamshauri vipi tena. Ukimya wa muda, akaamua kuondoka.

Wakati anatoka akakutana na Pam mapokezi. Mapigo ya moyo yakaanza kubadilika. “Mzima Pam?” Ikawa kama hajamsikia kabisa, akachukua kabrasha hapo juu ya kaunta, akaondoka kabisa kurudi ofisini kwao hata asimtizame wala kumjibu. Mill akajua Jerry alikuwa sahihi na kwa Pam ndio amejifungia milango yote. Akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Akapotea kabisa hata Jerry hakutaka kumtafuta kwa muda wakutosha ili tu Lona akose chakuzungumza. Baba yake alishatoka hospitalini, akawa yupo tu mtaani. Hana afanyalo, anajipanga jinsi ya kurudi kwa Pam. Mike akawa akimwangalia tu hana jinsi ya kumshauri. Kwa hakika alikuwa amenyongea. Gafla Mill aliyekuwa na utulivu wake tu, hana shida, mapenzi yakamnyong’onyesha.

Akiwa amebakisha siku chache aondoke bila jibu ya jinsi ya kumfikia Pam, akaamua kuyavulia maji nguo. Akatoka kama mwehu mpaka ofisini kwa kina Jerry. Bahati yake mbaya akawakuta wote mapokezi, wakiongea na kucheka na pochi zao begani, akajua ndio wanaagana. Muda wa kazi umeisha. Sandra na Jerry nao pia walikuwepo. Lona akaanza kumchangamkia, akamuona Pam anageukia mapokezi, akainamia simu yake. Mill akashindwa kujizuia.

Samahani Lona. Ni kwa heshima kubwa sana, lakini nimekuja hapa kwa ajili ya Pam.” Pakazuka ukimya. Pam alishituka na kugeuka. “Samahani sana. Lakini huo ndio ukweli na siwezi kuendelea kujificha. Na sio kwamba nimekuja tu hapa kutokea Tabata, hapana. Nimetoka mbali kwa ajili yake.” “Mimi nilishakuwahi. Pam hawezi kutuingilia.” Bila woga Lona akaongea mbele yao bila kupepesa macho.

“Najua mna sheria mmejiwekea. Lakini nilitaka Pam anisikie mimi mwenyewe. Nimevumilia, nimeshindwa na mimi naondoka nchini. Siwezi kuondoka nalo hili moyoni bila ya kumwambia Pam mwenyewe. Aliyenirudisha hapa nchini ni Pam, na mzee wangu ni mgonjwa. Ni hilo tu nataka Pam UNIELEWE.” Hapo akamwangalia Pam kabisa mpaka akainama kama aliyekuwa hajui chakuzungumza.

“Basi haitawezekana tena. Maana ndio sheria kubwa ya hapa, na hata Sandra mwenyewe anajua. Tulikubaliana tokea zamani. Huyo Pam kama angekuwa anakutaka, angekuwahi tokea mwanzo. Mimi nishakuwahi, hawezi hata kukusogelea tena.” Mill akamtizama akiwa anaweka huo msisitizo wake, alipomaliza tu, akageuza macho kwa Pam.

“Pam?” Akamuita, kimya akiwa ameinamia simu yake. “Lona alitukuta Mlimani City akiwa amemfuata bosi wenu. Hatukuwa na miahadi mimi na yeye. Na yeye ni shahidi yangu, huyu hapa. Namuheshimu kwa sababu ni dada mzuri tu na anajali. Lakini wewe ndio sababu ya kunirudisha hapa nchini. Sina uwezo wa kurudi huku kwa mwaka mara tatu au nne. Nimelipa garama kwa ajili yako.”

“Nimetoka mbali kwa ajili yako, wewe, Pam. Na ujue tu mimi si tajiri mwenye mapesa mengi ninayezunguka tu kwenye ndege!  Hapana. Sina hata vigezo vya kuweza kukopeshwa kwenye kampuni kama hii yenu, hata kama nikitaka kukopa nionekane na pesa kama wengine mliozoea kuwaona hapa, mimi siwezi. Na huu ni ukweli.” “Mmmh! Huo tena msala! Wote mnakuwa mnalia shida!” Akakejeli Lona na kucheka kwa sauti tu na kufanya wenzie wawili pia wacheka.

Lakini Mill akaendelea. “Kuniona hapa, jua ni juhudi tu. Nilikuwa nikifanya kazi kwa nguvu zote. Mchana na usiku ili tu nipate nauli ya kurudi huku, nikuone wewe, Pam.”

“Nasikitika muda umeniishia, nimeshindwa kuzungumza na wewe. Na kesho naondoka. Ni hilo tu nilitaka ulisikie kutoka kwangu mimi mwenyewe kabla sijaondoka.” Pam hata hakumjibu wala kumwangalia. Akabaki ameinamia simu yake. Kimya.

Mill akaondoka. Na Pam naye akaondoka hapo mapokezi kurudi ofisini kwao wakati walikuwa wameshafunga hata kompyuta. Inamaana siku ya kazi ilisha isha. Lona na yeye akatoka kwa haraka kama anayemuwahi Mill. Wengine wakaondoka kimyakimya.

Siku Aliyokuwa Akiondoka Nchini.

Siku aliyokuwa akiondoka Mill nchini alikuwa akiondoka na Mike pamoja na Kamila. Lakini kulikuwa na mvua karibia siku nzima. Kamila alishakuwa amemuandalia vyakula mbalimbali vya kubeba na kuondoka navyo nchini kama kawaida yake kumfungashia Mill vyakula vya nyumbani na wao wakawa wameshajifungasha vya kwao tayari kwa safari. Ndege ilikuwa ikiondoka saa nne na robo usiku. Kupitia uwanja wa ndege Doha kisha moja kwa moja mpaka JFK nchini Marekani. Kisha wangechukua gari ya kukodi hapo uwanja wa ndege JFK, mjini New York,  yakuwapeleka mjini Maryland ambapo anaishi Mill.

Mike alikuwa na Kamila kwenye nyumba yao kubwa. Walimpa Mill nyumba ndogo ya uwani. Kwa hiyo kila alipokuwa akifika nchini, anashukia hapo. Akawafuata nyumbani kwao kwenye hiyo nyumba kubwa. Akaanza moja kwa moja. “Kuna mvua sana. Nina wasiwasi na Pam.” Wawili hao wakabaki wakimwangalia. “Namaanisha jinsi atakavyorudi nyumbani.” Kimya. Mike na Kamila wakabaki wamemkodolea macho.

“Mbona mnaniangalia tu kama naongea kigiriki?!” “Sijui unataka nifanye nini Mill! Foleni sasahivi ni mbaya. Jiji limefunga, na yamebaki masaa machache tuondoke nchini. Hivi nilitaka kukupigia nikushauri tuwahi kuondoka, kupambana na foleni ili tusichelewe ndege.” “Namaanisha hivi, sitaondoka hapa nchini bila ya kujua kama Pam yupo salama na mvua hizi pamoja na radi.” Akaongea kwa msisitizo.

“Labda tumpigie simu Jerry, umuulizie wakati tukielekea uwanja wa ndege.” “Hapana. Nataka kwenda mimi mwenyewe.” Mike akabaki akimtizama.

“Basi au mimi nichukue usafiri mwingine, tukutane uwanjani.” “Kama umekusudia kwa kiasi hicho, basi tuondokeni sasahivi.” “Una uhakika? Maana sitaki kuwavurugia mipango yenu.” “Mpango tulionao na Kamila ni kuondoka na wewe. Na kwa asilimia kubwa yupo tayari. Naomba tumpe kama dakika 20 ajiweke sawa ndio tuondoke.” “Sawa.” Mike mtu wa watu. Anaweza kuchukuliana na yeyote. Mill alimjua. Sio rahisi kumkwaza Mike. Hata hapo yeye aliongea kwa amri, lakini Mike akiwa ametulia kabisa. Alipopata alichokitaka, akaondoka kurudi kwake, nyumba ndogo.

Baada ya nusu saa wakawa kwenye gari kuelekea ofisini kwa kina Jerry, wala si uwanja wa ndege. Barabarani akawa ametulia, anatamani Mike aliyekuwa akiendesha, apaishe gari kama anayewahi kuokoa kitu.

Wakafika mpaka ofisini kwa Jerry. Wakakuta karibia wote wanatoka. Mmoja wao alipanda kwenye gari lake ni kama akawapa lifti kina Lona na mwenzie. Wakatulia kidogo wamuona Sandra, Jerry, vijana wake wawili na Pam wanatoka. Wale vijana wawili wakapanda kwenye magari yao, Jerry akafunga milango ya ofisi, yeye na mkewe wakaondoka na kumuacha Pam amesimama pale nje. Wakamuona anatoa simu kama anayeangalia ujumbe. Kisha akabaki amesimama peke yake.

“Naomba usogeze gari pale ujaribu kumpa lifti.” “Unauhakika Mill! Maana hujui anapoishi! Hatujui itabidi tumpeleke umbali gani na sisi tuna safari! Tutachelewa ndege.” “Nina uhakika Mike. Hakika siwezi kuondoka hapa nchini na kumuacha amesimama pale. Sitaweza Mike. Sitaweza kufanya chochote huko niendapo. Kwanza sitaweza kuondoka.” Mike aliposikia hivyo na hapakuwa na mwanya uliowekwa wa kushauri akasogeza gari.

“Hujambo Pam?” Pam akawaangalia wote ndani ya gari. “Sijambo. Habari?” “Nzuri tu. Tunaweza kukusogeza kuliko ukae hapo peke yako.” Mike akawa muungwana yeye ndio akazungumza naye. Mill kimya pembeni yake. Kamila kiti cha nyuma amejituliza. “Mimi nipo sawa. Nashukuru.” “Mvua inanyesha na barabara zimefunga. Nina uhakika hata daladala zitakuwa hazitembei tena mida hii. Unarudije nyumbani?” Mike akashika kazi ya kumbembeleza ili watoke hapo.

“Mimi nipo sawa. Namsubiria kaka. Alisema atakuja kunichukua ndio maana nimebakia hapa nikimsubiria.” Mike akamgeukia Mill. “Hakika siwezi nikaondoka nikamuacha hapo nje na walinzi.” “Utafanyaje Mill, na mwenyewe amekataa? Anamsubiria kaka yake.” “Niache nisubirie naye. Nyinyi tangulieni na mizigo yangu. Nitachukua taksi kuwafuata.” “Mill!?” “Hakika siondoki bila kuhakikisha yupo salama.” “Kuna walinzi hapo. Kwa nini usiwaamini naye?” “Ingekuwa ni Kamila, ungemuacha hapo?” Mike akakwama.

“Nawaachia kila kitu changu. Check in mizigo yangu yote, niachie carry on yangu tu. Mimi nakuja nikikimbia.” Akashuka bila kutaka kumsikiliza tena Mike. Ikabidi kweli Mike na Kamila wawahi uwanja wa ndege na mizigo yake. Yeye wakamuacha.

Kwa Mara ya kwanza Mill&Pam peke yao.

Akamsogelea pale ukutani alipokuwa amesimama. Macho yakagongana, kwa haraka sana Pam akakwepesha ya kwake na kurudisha kwenye simu. “Pam!” Akamuita kwa upendo, akamwangalia. “Nataka kuhakikisha upo salama. Nitasimama hapa ili nisikukere. Ukija kuchukuliwa, na mimi nitaondoka.” “Mimi nitakuwa salama tu! Ungeondoka na wenzio uwahi ndege!” “Hakika siwezi. Sitaweza hata kufikiria nikijua nimekuacha hapa nje peke yako! Acha nikuache kwenye mikono salama ya huyo kaka yako, ndio niondoke kwa amani.” Pam akatulia.

Mill akajivuta pembeni kabisa. Lilikuwa baraza kubwa tu, juu limefunikwa na kumezungushiwa ukuta mzuri tu. Upo nusu wa hilo baraza kisha ngazi nne tu. Akawa amesimama kama mwisho, Pam mwanzo. Kimya akiangalia simu yake, yeye Mill ametulia tu.

Baada kama ya dakika 5, akamuona anamsogelea. Akaenda kusimama pembeni yake. “Asante kujali.” Akamsikia akiongea kwa sauti ya chini. “Karibu. Lakini naomba usiwe unafanya hivi, Pam! Wanadamu ni wazuri kukiwa na mwanga. Kukishakuwa na giza, wanageuka kuwa wanyama wa hatari waliojawa uchu wakupitiliza. Si sawa. Tafadhali ongeza umakini.” “Kaka aliniahidi tokea mchana kunipitia. Anafanya kazi benki.” Akamtajia. Hapakuwa mbali sana na hapo.

“Ni Teller. Nahisi pengine anafunga mahesabu ndio maana hata ameshindwa kunitafuta. Si unajua ni mpaka wao waweke sawa mahesabu ndio watoke?” “Umejaribu kumpigia?” “Simu yake siipati. Ila atanitafuta tu.” Mill akatulia. Pam anayezungumza naye hapo, amepoa na sura ya kike. Si jeuri kama alivyozoeleka.

“Unaendeleaje lakini?” “Vizuri.” Akamjibu kama anayepata shida kumtizama. “Vizuri hii ni ya jibu la wote, au kweli unaendelea vizuri?” “Mimi naendelea vizuri kabisa.” Akajibu vizuri kwa aibu zile za kike kabisa na kuzidi kumvutia Mill.

“Baba anaendeleaje?” Ikabidi na yeye kuwa muungwana, akamuuliza. Mill akamtizama kama ambaye hakutegemea. “Uliniambia ulirudi nchini kwa ajili yake pia!” Akajua jana alimsikiliza ila alishindwa kujibu mbele ya wafanyakazi wenzie. “Anaendelea vizuri. Alishatoka hospitalini. Asante kujali.” “Kwamba amepona kabisa?” “Ugonjwa alionao si wakupona kabisa. Ni kisukari. Na yeye ni mnywaji pombe asiyeweza acha. Ameathirika. Hivi wamemkata kidole gumba. Kilikuwa na kidonda. Kimeoza. Hawakutaka isambae. Lakini naona anaendelea vizuri.” “Afadhali.”

“Nilipokwambia sikuwa na miahadi na Lona. Yaani kile kilichoonekana kwenye picha aliyowasambazia si ilivyo, umeelewa?” “Ulisema jana.” “Nataka kujua kama umeniamini?” “Nimeamini. Lakini hakuna jinsi ya kufanya. Ile sheria ya kuwahi pale wanaisimamia mpaka Sandra mwenyewe amehakikisha wote ametusainisha na kutuapisha kwamba hatuta kiuka. Lona amekuwahi, Mill. Hakuna mtu pale anaweza badilisha hilo.” “Mimi sidhani kama mapenzi ya kweli yanazuiwa na sheria kama hiyo!” Pam akainama.

“Upendo una nguvu, Pam! Una nguvu ya ajabu SANA. Labda kusiwepo na penzi. Lakini penye penzi la kweli, hapatakosekana njia.” Akamuona amekunja uso akiwa bado ameinama. Mara simu yake ikaanza kuita.

~~~~~~~~~~~~~~

“Ni kaka!” “Afadhali tujue amefikia wapi.” Akapokea kama aliyepata ruhusa. “Kaka?” Akamsikia akimuita. Akasikiliza kwa muda, akamuona anapoa. “Poleni. Basi mimi nilikuwa nikikusubiria hapa nje kazini!” Akamuona anasikiliza kisha akasema. “Hamna neno. Nitatafuta njia ingine.” Akakata akiwa anaonekana ameumia.

~~~~~~~~~~~~~~

Akamuona amepoa. “Vipi?” “Anasema aliondoka huku mjini tokea mchana, mkewe alimpigia simu mtoto wao alipandisha homa.” “Poleni.” “Nashauri wewe uende tu, mimi nitatafuta jinsi yakufika nyumbani. Usichelewe ndege.” “Siwezi kukuacha hapa Pam. Hakika siwezi. Bora nikose ndege, lakini nihakikishe wewe upo salama. Acha nitembee kidogo niangalie taksii. Narudi sasahivi, sitachelewa.” Akaondoka kwa haraka.

Pam akamuona anaingia kwenye mvua bila kujali. “Sasa atasafirije akiwa amelowa hivi!?” Akajiuliza asiamini. Baada ya dakika kama 8 hivi, akamuona anarudi na magari mawili. Akashuka.

~~~~~~~~~~~~~

“Huyu nimezungumza naye, atakupeleka mpaka nyumbani. Kati ya madereva hawa wawili, huyu anaonekana ni mtu mzima na akili zake ni za mzazi. Hawezi kukugeuka njiani. Ila niahidi hutarudia kujiacha peke yako kwenye mazingira kama haya Pam. Ni bora umwambie Jerry akusub..” Akakumbuka kuna Sandra ambaye hawezi kuruhusu.

“Tafuta mapema kujua jinsi ya kurudi nyumbani salama. Taratibu tutatafuta gari yako.” “Nitaongeza umakini. Asante kujali. Uwe na safari njema.” “Na wewe ufike salama. Acha niwahi.” Pam akampa mkono. Akacheka.

Akaopokea na kumsogelea kisha kumbusu shingoni vizuri. Alimsisimua Pam na kushindwa kuelewa. “Pole. Nimekulowesha kidogo.” “Nakuhurumia wewe utasafiri umeloa.” “Usijali. Panda kwenye gari na mimi ndio niondoke.” Pam akaondoka na kupanda kwenye hiyo taksii aliyomtafutia. Akampungia mkono, akaondoka na ndio Mill akaanza kukimbilia uwanja wa ndege.

Mpenda Chongo, Kaona Kengeza.

“Nilisikia, lakini si kutoka kwa Lea mwenyewe. Ila kwa aliyeambiwa na Lea kuwa Gichiri alikuwa akikutaka.” Mina hakutegemea! “Mliishia wapi na Gichiri?” Andy akauliza taratibu tu. “Hakuniambia mimi moja kwa moja. Alimtuma Lea kwangu. Lea akaniambia. Lakini nikagundua Lea mwenyewe kumbe anamtaka Gichiri. Lakini Gichiri ni kama alikuwa akimuogopa Lea, akidhani ni mali ya bosi wenu. Ndio nikamwambia Lea, akamjibu Gichiri kuwa simtaki. Lea akauliza kutaka uhakika, akaniambia maana yeye anamtaka Gichiri, kama kweli mimi simtaki, yeye atazungumza naye. Basi, sikujua kilichoendelea. Ndio nikaacha ule mpango wakuwa sekretari, nikaanza kusomea mambo mengine, nikaacha kukaa pale mbele. Wakati mwingine nilikuwa nakwenda kukaa chini ya meza ya Ron, nafanya mambo yangu kwenye laptop aliyoninunulia. Makusudi tu, ili ajue ada anayonilipia naithamini na nimebadilika.”

“Kwa nini leo ulikuja ukilia?” Mina akainama. “Eti Mina?” “Tokea nirudi kutoka kwa Omar, sijawahi kutoka kama hivi. Kwa hiyo mama akawa anawasiwasi kuwa nimerudia tena. Kila nilivyokuwa nikimwambia kuwa ninakutana na mtu kwa mazungumzo tu, alikuwa akiniomba nirudi nyumbani, kama haamini tena! Iliniuma Andy. Niliharibu sana nyuma. Mama anahofu na mimi. Hivi hapa nilimuahidi nitampigia ili kumuhakikishia nipo sehemu salama. Nimesau tu. Naomba nimpigie nimtoe wasiwasi.” “Utafanya vizuri.” Andy akamruhusu.

~~~~~~~~~~~~~~

Akatoa simu na kumpigia mama yake. “Nipo salama mama. Tumeshatoka hospitalini. Nipo tunazungumza tu.” Akasikia kama mama yake anamuuliza swali. Mina akacheka. “Kila kitu kilienda salama.” Akamuona anacheka na kukata simu.

~~~~~~~~~~~~~~

“Angalau ameridhika.” Mina aliongea wakati anarudisha simu kwenye pochi yake. “Kwani wanajua upo na mimi?” “Hapana! Ndio maana mama aliingiwa na wasiwasi akitaka nimwambie nitakuwa na nani, nikashindwa.” “Kwa nini?” Mina akamwangalia kidogo akainama.

“Eti Mina?” “Kwa kuwa hata mimi nilikuwa sijui nakwenda wapi Andy! Halafu Ron alitusikia mimi na mama tukiongea. Akataka angalau niwaambie nitakapokuwa, lakini nilishindwa!”

“Fikiria mwenyewe, kwa kule nilikotoka, maisha niliyoishi, halafu eti leo Ron ajue nipo hapa na wewe, wakati wanajua unaye Lora, unafikiri angenielewa?” Andy akabaki amenyamaza. Mina naye akabaki kimya akimuacha atafakari. Alimwambia mazito ambayo yatamfanya abakiwe akimtafakari. Ukimya wa muda ukapita. Kila mmoja kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa jinsi alivyompenda huyo Mina, wakati huo alikuwa anashindwa kufikiria japo ameshamjua huyo Mina ndani na nje! Ingekuwa msichana mwingine, angeshamtafutia sababu aondoke hapo kwake. Ila kitendo chakushindwa kumfukuza mpaka hapo, akitamani aendelee KUWEPO naye tu hapo, akajiaminisha ni kweli anampenda huyo Mina.

Ila sasa atafanyaje na Mrembo huyo anayegombaniwa na wengi, katikati ya jiji hilo la wajanja! Anabeba kama ilivyo atajua mbele ya safari, AU ajiachie tu kuepusha dhoruba ya baadaye!

Akabaki akipiga hesabu, gafla zikageuka kama anazochukia Mina, zimejichanganya herufi na namba!

Algebra ya Mapenzi.

Andy atafanyaje?

Inaendelea…

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment