Andy aliongea maneno machache lakini mazito kwa Mina.
Akarudi nyuma kabisa pale alipokuwa amekaa kama anayemkimbia Andy. Akabaki
akimtizama. Andy naye akanyamaza, wakabaki wakiangaliana. Akajifuta machozi
vizuri. Akasimama. “Unaenda wapi sasa?!” “Narudi nyumbani kwa mama Ron, Andy.”
“Hatujazungumza!” “Hapana. Uliniambia kuna kitu unataka kuniambia. Sasa
umeshaniambia, naona mimi niondoke. Naweza kutumia choo kabla sijaondoka?” Andy
akasimama kwenda kumuonyesha.
Mina akakaa chooni, akajiosha uso. Ndipo akatoka.
“Asante kwa chakula, Andy. Nashukuru.” “Naomba tuzungumze, Mina. Usiondoke
tafadhali.” “Naomba nikwambie ukweli Andy.” “Nakusikiliza. Lakini naomba
tukae.” “Hapana Andy.” Mina akakataa mpaka akatingisha kichwa.
“Mimi sipo hivyo kama unavyonifikiria nipo. Kama
umemuacha Lora kwa ajili yangu, nakuhakikishia umekosea kabisa. Na kama
mimi ndiye uliyekuwa ukizungumzia ‘Love at first sight’, ujue kuna mwenzio alijaribu kama wewe, haikuishia vizuri. Naomba
mimi niondoke Andy.” Andy akamsogelea.
Akamshika mikono yote miwili na
kumvutia sebuleni. “Nataka kujua iliishiaje?” “Akaanza kunipiga! Mpaka mama akaja kunitoa huko.” Andy hakuwa akielewa.
“Ulikuwa umeolewa?” Mina akanyamaza. “Mina?” Kimya. “Tafadhali naomba uwe na
imani na mimi! Hata hivyo huna chakupoteza. Hata nikijua, hunipendi,
pengine hatutaonana tena, na mimi nakuahidi sitamwambia mtu.” Mina akacheka.
“Kwa hiyo huna chakupoteza. Niambie tu.” “Sijasema
sikupendi bwana, ila naona kama tumekuwa na mahusiano au niseme mawasiliano
mazuri. Sitaki tupoteze. Mwenzio nafurahia.” “Nakuahidi hatuwezi
kupoteza. Ila kutusogeza karibu zaidi.” Andy akamsogeza karibu.
“Nataka kukufahamu Mina. Nilikupenda siku ya kwanza
unanifungulia mlango nyumbani kwenu.” Mina akacheka na kujifunika uso na
kuendelea kucheka. “Nilivyomchoza Ron?” Mina akauliza huku akicheka. “Kila
kitu. Nataka kukufahamu kwa kuwa nakupenda wewe. Hata Lora nimemwambia
kuwa siwezi kuendelea naye kwa kuwa hisia zangu zipo kwa mtu mwingine.”
“Usingefanya hivyo kwa haraka Andy! Angalau ungezungumza na mimi kwanza,
unifahamu kabla hujamuacha Lora, msichana mzuri!”
“Hapana. Wewe umenisaidia kutoingia kwenye ndoa ambayo
ingevunjika baada ya muda mfupi sana. Hisia zangu kwako na kuwa mkweli kwake
kumenisaidia kumjua Lora wa kweli ambaye alikuwa nyuma ya Lora yule
uliyekuwa ukimuona akinibusu mbele yenu. Akileta maua na chocolate. Ni watu
wawili tofauti.” Andy aliongea kwa kumfikiria Lora.
“Sijui ingekuaje kama tungeoana!” “Kwa hiyo Andy wewe
unatafuta mwanamke wa kuoa kabisa!” “Kwa sasa sitafuti tena. Na ndiyo! Nasubiri
nini tena?” Mina akacheka na kuinama kama anayefikiria. “Nikwambie ukweli
Mina?” Mina akamwangalia. “Jinsi ninavyojisikia nikiwa na wewe, au nikikushika
au ukinishika, sijawahi kujisikia hivyo kabla. Nafikiri ni zaidi ya mtazamo
wako wa nje. Huwa nakaa hapa nakumbuka jinsi ulivyonishika na jinsi
nilivyojisikia kwa wakati ule.” Andy akaendelea taratibu huku akivuta hisia.
“Ungenihurumia siku ile ya jumapili ambayo nilikuahidi
nitarudi kukuona! Kumbe hata Lora alinigundua! Nilikuwa sijatulia, natamani
waondoke nije.” “Kweli?” Mina akauliza huku akicheka taratibu. “Na kwa taarifa
yako nilikuwa nakuja kwa ajili yangu zaidi.” “Andy!” Akampiga kidogo. “Kwani
wewe hata ulijua kama nitakuja kukuona? Kwanza sidhani hata kama jina ulikuwa
ukilijua.” Mina akakubaliana na hilo huku akicheka.
“Sasa je! Mimi ndio nilitaka kuja kukuona Mina, ile
ahadi ilikuwa kwa ajili yangu. Nashangaa ni kwa nini wewe ndiye uliyeumia!” “Ni
jinsi ulivyoniahidi Andy. Ulinifanya nikusubirie siku nzima. Nilikuwa
nalia maumivu ya kichwa huku naangalia mlangoni nikijiambia labda utakuja.”
Andy akamsogelea karibu. Akaweka mkono pembeni ya shingo huku akimtizama Mina,
Mina akajilaza kwenye ule mkono kidogo. “Pole na samahani.” Mina akacheka. Wakati
Andy anataka kuinama kumbusu, Mina akakwepa.
“Hapana Andy. Naomba unisikilize kwanza, ndipo
uamue.” Mina akajisogeza pembeni kabisa. “Nisikilize kwanza Andy. Ili unijue
kwanza. Nimekuwa nikifanya makosa kama haya. Nimeishia kumuumiza mama na
Ron. Nimewaahidi kubadilika.” “Okay.” Andy akajirudisha nyuma.
Juu Ya Mina.
Mina akaanza. “Mwanaume wa mwisho niliyekuwa naye,
alisema ananipenda hivyo hivyo. Akataka niache kila kitu nikaishi naye.”
“Inamaana alikuoa?” Mina akanyamaza kidogo, kisha akaona ajibu tu. “Nilitoroka
naye, nikaenda kuishi naye Iringa.” “Kwa nini hukuaga?” “Kwa nani sasa? Mama au
rafiki yake?” Hapo Andy akawa ameshachanganywa. Ila akauliza.
“Kwa nini
umuage rafiki yake!” “Ndiye aliyekuwa mwanaume niliyekuwa naye kwa wakati huo,
baada ya kuachana na rafiki yao.” Andy akajikaza, na kutulia. Ila
akauliza akihisi pengine hajaelewa vizuri. “Kwa hiyo walikuwa marafiki watatu?”
Mina akarudi kukaa, Andy naye ikabidi arudi kukaa alipokuwa amekaa tokea
mwanzo.
“Nilianzana na Afidhi, nikiwa kidato cha pili.
Tukawa naye kwa muda, lakini kila mtu akasema haniongozi vizuri.” “Kivipi?”
Andy akauliza haraka kabla hajaendelea. “Alinitorosha wakati nipo kidato cha
pili. Akanifungia kwenye chumba chake kule
Magomeni Mapipa. Nikakaa hapo kama miezi miwili. Ndio rafiki yake,
Afidhi, yaani Mozee, akaniambia lazima nirudi nyumbani. Mama atakuwa na
wasiwasi.” “Muda wote huo wakati upo na Afidhi hukuwa ukiwasiliana na mama?”
Mina akainama na kupandisha mabega kukataa.
“Ehe?” “Sasa ndio Mozee akanilazimisha niondoke.
Kila siku Afidhi alipokuwa akienda kazini, yeye akawa anarudi nyuma ananiambia
lazima niondoke.” “Alikuwa akifanya kazi?” Andy akauliza taratibu. “Afidhi na
Mozee walikuwa wakifanya kazi kwenye magari ya baba yake Omar. Omar alikuwa
mwarabu aliyezaliwa hapa Dar, lakini mama yake na baba yake walikuja kurudi
Arabuni ndio Omar na kaka zake wakaachiwa mali zote. Lakini Omar ndiye
aliyekuwa karibu na kina Afidhi, kama mmiliki wa karibu anayewasimamia kwenye
kazi. Wakawa kama wameunga urafiki na Omar. Au nisema Omar aliweza kujishusha
akawa kama rafiki yao.” Mina akaendelea.
“Sasa kumbe walipokuwa wakikutana wao watatu, Afidhi
akawa anawasimulia mambo yetu.”
“Unamaanisha nini?” Andy akauliza taratibu. “Mambo ya mapenzi!” Mina akajibu
huku ameinama. “Ehe!” “Sasa ndio akasababisha tamaa kwa wenzake.
Alipokuwa akiondoka ananiacha nyumbani, Mozee akawa anakuja ananishawishi
nirudi nyumbani, akasema Afidhi haniongozi vizuri. Akaniambia hata hivyo ananidanganya,
ameoa.” “Ilikuwa kweli?” Andy akauliza.
“Mozee alikuwa muongo tu. Alikuwa anatafuta njia ya
mimi na Afidhi tuachane ili anichukue yeye. Siku hiyo akaja na taksii, akanichukua
na kunirudisha nyumbani. Hapo ikawa nilipotea kama miezi miwili hivi.”
Andy alikuwa akimtizama Mina kwa utulivu, Mina alikuwa anaongea ameinama.
“Si ndio nikaanzana na Mozee sasa! Hapo nikawa
namkwepa Afidhi, na yeye akaniambia Afidhi ananitafuta kama amechanganyikiwa!
Inabidi nimkwepe. Tukawa kwenye mahusiano na Mozee, mpaka nikaja kugundua na
yeye alinidanganya juu ya Afidhi. Nilipomuuliza, akaniambia alifanya hivyo kwa
kuwa ananipenda sana, anaona kama Afidhi hakuwa akinipenda kweli
kama eti yeye! Lakini sasa kuanzia hapo nikawa simwamini tena.
Nikaanza kumkwepa na yeye.”
“Akaanza kuwa kama amechanganyikiwa. Ananifuata
mpaka shule! Nikitoka namkuta ananisubiria nje. Mara aje mpaka nyumbani, ikawa
fujo tupu.” “Anataka nini sasa?” Andy akauliza. “Ananitaka mimi!” Mina
akasikika kitoto. “Akawa ananililia turudiane. Mimi nikamwambia siwezi kwa kuwa
yeye ni muongo! Akawa hasikii wala
haniachi. Ananivizia kila mahali.” “Ulimwambia mama?” Mina akatingisha kichwa
kukataa.
“Kwa nini sasa hukumwambia mama?” “Ningemwambia kipi
niache kipi Andy? Nilikuwa na majanga mengi, matatizo kila
mahali. Mama alikuwa akihangaika na kesi zangu mchana na usiku. Kipindi hicho
mimi nahangaika na Mozee, mama naye alikuwa akiomba kwa kusihi mpaka kulia kila
siku kwa uongozi wa shule nisifukuzwe shule.” “Kwa nini?” Mina akavuta pumzi
kwa nguvu, akanyamaza.
“Mina?” Akamuona anajifuta machozi akiwa ameinama
vilevile. “Niambie tu.” Akambembeleza. “Mwalimu mkuu alinifumania kwenye vyoo vyakiume. Wakataka
kunifukuza shule, kwa kuwa pia nilikuwa wakati mwingine siingii darasani.”
Mina akanyanyua uso na kumtizama Andy. Akakuta ametulia akimtizama. “Nilikwambia inatisha, Andy!” “Nini kilitokea
Mina?” Mina akarudisha uso chini. Na kujifuta machozi.
“Basi, ndio mama akawa ananifungia ndani.
Anatoka na mimi asubuhi kwenda shule, nakurudi naye jioni. Ukumbuke hizo fujo
zote hizo nipo kidato cha nne sasa. Ron alikuwa chuo tayari, huko Dodoma,
akarudi, akaniomba nitulie angalau nimalize kidato cha nne. Tukazungumza
nikamwambia mimi sipendi kukaa darasani.” “Kwa nini Mina?” “Nilikuwa
naona wanatufundisha vitu ambavyo hata sitakuja kuvitumia maishani!
Nikaona napoteza muda.” Andy akacheka.
“Kwa mfano nini?” “Mahesabu yale wanayochanganya namba na herufi!” Andy alicheka sana. “Usinicheke
bwana Andy! Kwani wewe pale kazini kwenu mnatumia hayo mahesabu?” “Algebra?”
“Ehe! Ona jina lenyewe jamani!” Andy akacheka tena na tena. “Kwa hiyo ndio
maana ulikuwa hutaki shule?” “Nilikuwa naona napoteza muda. Hata hivyo
acha tu niwe mkweli. Akili yangu haikuwa imetulia Andy. Mimi mwenyewe nikikaa
na kukumbuka mambo niliyofanya! Najishangaa.” Andy akampa tabasamu akiwa
amerudi kutulia tena.
“Ikawaje sasa?” “Kuhusu nini tena?” “Mozee na shule.”
Mina akacheka na kuinama. “Usiniache njia panda. Tafadhali nimalizie. Nataka
kujua.” Mina akamtizama kama ambaye anamshangaa kutaka kujua uchafu wote huo!
Alipomuona ametulia, akaamua kuendelea. “Kabla mama hajanifungia,
nilikwenda nikawafuata wote. Mozee na Afidhi. Hapo Omar alikuwepo. Nikawaambia siwataki
wote. Na akiendelea kunifuata kila mahali, mama amesema atawapeleka polisi.
Nikawadanganya kuwa nimempa mama picha zao. Waniache. Hapo nikawa
nimeenda na kijana mwingine hivi. Akawatisha akiwaambia yeye ndio Ron. Basi.
Wakaacha kunifuata. Sasa kumbe na Omar akawa ananitaka na yeye.” “Omar
bosi wao kina Afidhi!?” Mina akakubali macho chini.
“Ikawaje?” “Mimi sijui alipata wapi namba yangu ya
simu, na yeye akaanza kuwasiliana na mimi kwa simu. Akaanza kawaida tu. Ananihusia
nitulie niachane na watu wote, nijitahidi nimalize shule kama mama
alivyoniambia.”
“Akawa mwema kweli! Ushauri hauishi! Na simu
kila wakati. Lakini nilikuja kugundua ni wivu tu. Jamani Omar ana wivu,
ule wakupindukia. Hataki hata kuhisi kuna mtu ananiongelesha! Alikuwa akinikuta
naongea na mtu yeyote, hata mfanyakazi aliyemuweka yeye mwenyewe, ananipiga.”
Andy akakunja uso. “Umevuka mbele, umeniacha nyuma kabisa. Uliishia akikuhusia
umfuatilishe mama.” “Ule ulikuwa uongo wakunitenga na kila mtu, na kunifanya
nikae ndani. Nilipomaliza tu mitihani ya kidato cha nne, mama akajisahau
kidogo tu, na yeye akapata mwanya.” Mina akamwangalia Andy.
“Nakusikiliza Mina.” “Aliniambia ananipenda,
anataka anitunze. Niwe mpenzi wake yeye. Akanipanga na mipango mingii.
Akaniambia ana nyumba Iringa, niende nikaishi naye. Yeye hatakuwa kama kina
Afidhi. Atanitunza vizuri. Basi. Siku hiyo mama alipoondoka tu nyumbani,
nikamuandikia ujumbe kuwa nimeamua kuondoka, kwenda kuolewa. Asinitafute wala
kuchanganyikiwa kama mara ya kwanza nilipoondoka. Nikamuachia huo ujumbe, nikaondoka
na Omar. Lakini Andy, nilijuta.” “Kwa nini?” Andy akauliza taratibu tu.
“Alinitoa hapa, na kwenda kunifungia nyumbani kwake
Iringa mjini. Alikuwa na nyumba nzuri kweli. Akaniwekea wafanyakazi wawili.
Kila kitu alikuwa akinunua yeye, hataki nitoke nje. Alikuwa kama amepagawa!
Hana amani popote anapokwenda, wakati amenifungia ndani! Siruhusiwi kutoka hata
nje!”
“Kwanza
tulianza vizuri. Furaha na utulivu. Siku moja wakaja rafiki zake mle ndani, na
ndugu zake. Ni wale waarabu kabisa. Sasa mmoja wa rafiki zake akamtania tu.
Akamwambia akifa yeye, ataomba anirithi. Atanioa mke wa pili. Na
atahakikisha anachangamka kunizalisha kwa haraka ili nisije kumkimbia.
Wote tukacheka. Wakawa wanatania hivi na vile, kumbe Omar amekasirika
anakaribia kupasuka!”
“Walipoondoka wageni, alinipiga kama anayetaka
kuniua. Akaanza kuongea mambo mengi, ndipo nikajua hata sifa alizokuwa
akinisifia juu ya umbile na mengineyo ilikuwa ni tamaa tu. Kina Afidhi
walimfanya anitamani tu.” “Kivipi?” Andy akauliza tena. “Nikikwambia Mozee
alichanganyikiwa, ni alichanganyikiwa kweli kweli. Akawa kama mwehu,
anasema yeye hawezi kuishi bila
mimi. Akawa ananitafuta kama mwehu. Si ndio Afidhi akajua kuwa kumbe rafiki
yake alimzunguka! Wakaanza kugombana kazini na kupigana. Omar
akawa anawasikia na kuwaamulia wanavyogombana.” “Kukugombania?” Mina akanyamaza
na kuinama.
“Kwa hiyo na yeye ndio akakutamani?” Andy akauliza.
“Nilikuja kujua hilo nilipoanza kuishi naye. Bila kosa ananipiga. Mtu unayempenda kweli huwezi kumpiga vile.
Alikuwa akinipiga Andy, mpaka napoteza fahamu.” “Sasa kwa nini hukurudi
nyumbani?” Andy akauliza. “Alikuwa akinifungia Andy! Sikuwa nikiruhusiwa kutoka
wala kuzungumza na mtu. Mpaka wasichana wa kazi wa ndani hakutaka niwe nao
karibu. Wafanyakazi wanabadilishwa kila kukicha. Akiona tu nazungumza na
msichana wa kazi, ujue anampiga na kumfukuza. Walinzi nao wakawa wanaambiwa
walinde nje. Hawaruhusiwi hata kukaribia mlango wakuingia ndani. Ikawa fujo.
Akanijengea hofu, nilikuwa siwezi hata kutoka chumbani.” “Kwa nini!?”
“Aliniwekea kamera kila mahali! Akitoka hapo, ujue
macho yake yananiona kwenye simu. Halafu alikuwa na pesa nyingi za kuhonga
popote. Akawa ananitishia eti hata mama yangu mzazi hawezi kuja kunitoa
pale. Mimi ni wake mpaka kifo. Ikawa fujo, yeye mwenyewe hana amani,
mimi nikilio kila wakati. Kazi zinamshinda kwa kuwa hana anayemuamini na
mimi. Hawezi kusafiri tena kurudi huku kwenye biashara zao. Amebaki na mimi
kifungoni.”
“Basi
tukahangaishana wee, ndio kama baada ya mwaka na miezi hivi nikashika mimba.
Tena mtoto mwenyewe alikuwa akimtafuta, sina raha! Kila wakati
ananiuliza kama sijashika mimba. Sina raha, anataka mtoto, mimi nikawa sitaki
kuzaa naye.”
“Uzuri alikuwa hataki nipate shida. Ananinunulia kila
kitu, na hakutaka nifanye kazi. Lakini wivu ulikuwa ukimfanya hata
tusitulie. Lakini nilimuelewa ni kwa kuwa nilitembea na Mozee, baada ya Afidhi.
Na wote walikuwa marafiki sana.” “Halafu ukaja kumkubali na yeye.” Andy
akaongezea kugongelea msumari. Mina
akainama.
“Lakini nilimuhakikishia kuwa sitamsaliti.”
Akaongea kwa aibu bila hata kumtizama. “Ikawaje baada yakushika mimba.” “Jamani
Omar alifurahi! Sitasahau! Akawa ananipenda. Akajirudi na kuwa mpole.
Lakini akawa ananifungia vilevile.”
“Ila sasa mimi nikawa simtaki hata kumuona.
Alishakuwa amenipiga mara nyingi mno. Halafu alikuwa akishanipiga hivyo,
anaomba msamaha mpaka analia! Ataapa hapo kuwa hatarudia tena, lakini anakuja kurudia.
Kwa hiyo nilijua ni ngumu kuja kubadilika. Ni mtu mwenye mkono wakupiga tu.
Basi. Nikiwa na ujauzito wa miezi mitatu, siku hiyo tukawa tupo sebuleni. Yeye
ni msafi sana. Yaani ni wale wanaume wanaooga kwa kujisafisha kama wanawake.
Huwezi kumkuta na harufu popote, muda wowote. Msafi na harufu safi wakati wote.
Anaweza oga hata mara tatu kwa siku. Na hapo ni Iringa, na kuna baridi. Nyumba
imezungushiwa vigae, gari anaegesha nje ya mlango. Hachafuki, lakini lazima
aoge kila wakati.”
“Kipindi hicho tukawa hatuna msichana wa kazi. Alikuwa
na bibi anamleta pale atufanyie kazi. Naye akawa anakuwa mgonjwa mgonjwa. Kwa
hiyo Omar ndio akawa anafanya kazi za mle ndani kwa asilimia kubwa, ananiambia
mimi nikae tu. Basi. Tulipokuwa hapo sebuleni, akataka mapenzi baada yakumaliza
shuguli zake huko jikoni. Baadaye akaamua kwenda kuoga, mimi nikiwa nimejilaza
kwenye kochi. Alitaka sana nikaoge naye. Sasa mimi nikamwambia nimechoka,
nataka kupumzika. Lakini ukweli alikuwa ameshanikinahi, nasikia shida
akinishika. Nikajua nikienda naye bafuni, atanigusa tena. Nikamdanganya
kuwa nimepatwa vichomi, nataka nipumzike, ndio nikaoge.”
“Yeye akatangulia bafuni. Omar alikuwa hawezi kukaa na
jasho hata tone. Na ilikuwa akiingia kuoga, unaweza kumsahau. Atajisugua kama
ametoka shamba! Aliponiacha pale kwenye kochi, nikapitiwa na usingizi. Nafikiri
nililala kama dakika 15 hivi. Nikashituka, akawa bado hajarudi. Nikajiambia
niwashe tv kwa kuwa Omar aliizima wakati mimi nilikuwa nikiangalia mchezo.”
“Omar akiwa kwenye mapenzi hataki kelele ya kitu
chochote kile. Si redio, sio tv au simu. Alikuwa akiniambia anataka utulivu
kabisa. Anisikie mimi tu bila mwingiliano wa chochote. Yaani anisikie
mpaka pumzi yangu.” Andy akapandisha nyusi moja juu, Mina akainama.
“Alipotaka tufanye mapenzi, alinikuta mimi naangalia
mchezo, nikamwambia asubiri kwanza. Akasema mchezo ndio usubiri, akanizimia tv.
Basi nilipotoka usingizini wakati yupo bafuni, mimi nikapapasa nikaokota rimoti
aliitupa chini, kwenye kapeti. Ile nimeinyanyua tu, na yeye akawa anatoka
chumbani anarudi pale sebuleni.” Mina akanyamaza kidogo.
“Nini kilitokea?” Mina akaguna akiwa ameinama kisha
akamwangalia Andy. “Nilikwambia hakuwa akitaka niwasiliane na yeyote yule. Kwa
hiyo alikuwa akitembea na simu zake kila mahali. Sasa wakati yupo jikoni,
nafikiri kuna mtu alimpigia. Akazungumza naye na kuiacha hiyo simu huko huko
jikoni. Alipotoka na kuniona nimeshika kitu cheusi, yeye akajua ni simu yake.
Maana simu yake ilikuwa na cover jeusi.”
“Sitakaa
nikasahau ile siku. Jamani Omar alinivamia kwa kunirukia. Ile rimoti ikaruka
nakuingia chini ya makochi. Akaanza kunipiga kuwa nimetumia simu yake.
Nilikataa kwenda kuoga naye ili huku nyuma niibe simu. Nilikuwa siwezi
kuongea Andy, jinsi alivyokuwa akinipiga kama mwehu.”
“Yeye mwenyewe analia huku akinipiga, mimi nalia.”
“Sasa yeye analia nini?” “Analia anasema nataka kumkimbia. Yeye
amejitahidi kunipa kila kitu, lakini mimi siridhiki. Amejishusha amekuwa
kama mtumwa wangu, lakini bado siridhiki. Akanihesabia hapo. Analia kuwa
nimebadilika hata jinsi ninavyofanya naye mapenzi, sio kama mwanzo.
Namuonea kinyaa. Sitaki tena aniguse. Yaani ni shutuma nyingi akilia kama mwehu
huku akinipiga. Akasema eti napanga mipango nimkimbie na mtoto wake.”
“Uzuri nyumba yake ilikuwa na kapeti nyeupe. Akawa
amenitoa pale kwenye kochi, ananipiga chini. Si nikaanza kutokwa damu, ndio
akili zikamrudia sasa. Akajua ameshaua mtoto. Akanibeba na kunikimbiza
hospitalini. Mpaka kuja kuonana na daktari, nakufanyiwa vipimo, tukaambiwa
mimba imetoka. Jamani Omar alilia, karibu kuchanganyikiwa.
Akatolewa pale, akaambiwa inabidi mimi nilazwe. Akaitiwa taksi, ikamrudisha
nyumbani. Simu hana, akakumbuka iliingia chini ya makochi. Kufuata, akagundua
kama ilikuwa rimoti, simu aliiacha jikoni. Alilia Omar, akarudi hospitalini
usiku kama saa nane analia, anaomba msamaha.”
“Yaani Omar anakuwa kama anapagawa na pepo!
Anakasirika, likishuka, utamuonea huruma. Lakini nilikuwa nimeshachoka Andy.
Mwili ulishachoka na vipigo. Nikawa nimeshakata tamaa hata yakuja
kujiokoa tena mikononi mwake. Basi, nakumbuka manesi wakamfukuza na kumwambia
arudi nyumbani. Aniache nipumzike mpaka kesho yake asubuhi. Alipoondoka tu, nikamuomba nesi aliyekuwepo hapo anipe simu.” Mina
akajifuta machozi.
“Nikatamani kumpigia simu
mama ili nizungumze naye tu, lakini hofu yakurudi nyumbani ikawa
imeniingia. Naona aibu kurudi. Ule muda wote nilioishi na Omar
ukanifanya nikae chini nijifikirie, nikaona ni heri nife tu, mama yangu
apumzike. Na hapo ukumbuke mama alitulea mimi na Ron, tena yeye peke yake bila
msaada.” “Baba yuko wapi?” Akajifuta machozi.
“Alioa mwanamke mwingine wa dini yao baada ya mama
kukataa kubadilisha dini kuwa mwislamu. Tena hapo sisi tulishakuwa wakubwa tu
ndio anataka eti na mama abadili dini halafu yeye mwenyewe baba hakuwa hata
anajali mambo ya nyumbani! Alikuwa yupo kama hayupo tu. Nafikiri alioa wakati
mimi sijui nipo darasa la tano, nafikiri.” “Huwa anakuja kuwatembelea?” Mina
akafikiria.
“Mmmmh! Sikumbuki. Hata hatukuwa na mahusiano naye
mazuri. Kwanza hata hatujali mimi na Ron. Mama alitubadilisha majina mapema
sana. Alipoondoka tu, mama akabadilisha majina yetu kabisa. Mimi nilikuwa
naitwa Amina, ndio akaniita Aminata.
Ron alikuwa Ramadhani, jina la baba yake baba. Mama akaenda kutoa hilo jina.
Ndipo akampa jina la Ron. Akatoa kabisa ubini wa baba, akatupa wake. Nafikiri
hicho ndio kikamuudhi baba zaidi, akasema hatutaki tena.” “Pole Mina.”
“Asante, lakini
hata sijali. Ni mwislamu yule haswa. Ukimuona huwezi kujua hata alioa mkristo.
Amerudia dini yake, na anaishika kwelikweli. Ni yule wa swala 5 mpaka ana alama
hapa kwenye kipanda uso. Ana mke na watoto wake wale wakuvaa hijabu. Hawajiachi
wazi kama hivi mimi. Hana hata shida na sisi! Kwanza hatuendani kabisa. Tuache
hayo.”
“Basi, nikapewa simu, lakini nakumbuka nikashindwa
kabisa kumpigia mama. Nilikuwa nahamu nao! Ron na mama. Nilikuwa nina majuto,
nikajiambia ni heri nimuombe mama msamaha kabla sijafa pale au Omar akaja
kuniua. Nikamrikodia mama ujumbe kwa kutumia Whatsapp.
Nikamuomba msamaha. Nikamwambia nipo mahali ambapo sijui kama nitatoka, au kama
nitakuja kumuona tena. Nikamkumbusha mabaya yote niliyoyatenda. Nikamuomba
msamaha na kumshukuru kwa kutonikatia tamaa tokea nafikiri darasa la saba
nilikuwa namsumbua mama. Basi. Nikamtumia ule ujumbe. Haukufika,
nikasubiri baada ya muda, nikajaribu kufuta, nikaona inakubali kufuta kwenye
ile simu ya yule nesi tu, lakini sio kwa mama. Nikajua akija kuwasha simu hata
kama ni siku nyingine, atakutana na ujumbe wangu.”
“Ulimwambia
ulipo?” “Hapana Andy! Sikutaka aje anikute vile. Nipo nimepigwa! Halafu mpaka
mimba ikatolewa! Nilikuwa naogopa. Siju ni aibu! Sijui Omar
alishanitisha sana mpaka nikawa sina tumaini, sijui! Ila nilichotaka ilikuwa kuomba msamaha na kumshukuru,
basi.”
“Kesho yake asubuhi Omar akaja na kuanza fujo tena,
anataka waniruhusu nirudi naye nyumbani. Manesi wakamkatalia na kumwambia
wanamwitia polisi. Lazima nitibiwe nipone. Sasa mimi nikashangaa. Maana Omar
alikuwa anafahamika na kila mtu, na walikuwa wanamuogopa sana pale
mjini. Nikashangaa ni kwa nini siku hiyo wale manesi wanamkatalia, hawafanyi
kama anavyowaamuru! Basi, wakaja askari, wakamfukuza. Wakamuogopesha kuwa usiku
nilizidiwa karibu ya kufa, kwa hiyo akinitoa pale vilevile, nitamfia njiani.
Ndio akakubali kuondoka. Nikashinda pale, mchana akarudi, akawa ananiomba
msamaha.” Mina akacheka na kuguna.
“Omar akiomba msamaha, utamuhurumia! Nakwambia
alikuwa pale wodini amepiga magoti analia. Sasa kwa kuwa mimi namjua, nikawa
nipo kimya tu, watu wengine wakaanza kumbembelezea. Moyoni nikawa nasema ni
vile hawamfahamu. Hapo alikuwa analia msiba wa mtoto ambaye hata hakuwa
anacheza bado huko tumbonj! Akalia hapo wee, mimi nikapitiwa na usingizi.”
Akatulia kidogo, akamuona anafuta machozi akiwa ameinama.
“Nikaja kuamshwa na kilio cha mama.
Sikuamini Andy! Kumbe usiku ule kabla hapajapambazuka, ule ujumbe ulipoingia
kwa mama, ndio akampigia simu yule nesi na kumuulizia. Yule nesi akamwambia
kwamba pale ni hospitalini, nimelazwa. Na mume wangu ndiye aliyenileta akiwa
amenipiga mpaka akanitoa mimba. Ndio mama akamwambia mimi bado ni mdogo, na
Omar alinitorosha tu nyumbani. Akamuomba yule nesi asiniambie chochote,
mpaka atakapokuja yeye mwenyewe. Ndio yule nesi akamuhurumia mama, akawaambia
manesi wengine. Wakakubaliana wamdanganye Omar.”
“Mama alikuja na Ron, pamoja na polisi kutoka huku Dar
ambapo hakuna anayemfahamu Omar. Yule polisi alikuwa kama ndugu wa mama.
Akamtisha Omar, ndio Omar akamuomba mama msamaha, akasema atajirekebisha, yupo
tayari alipe mahari, anioe kihalali. Mama akakataa katakata. Akasema
mimi bado mdogo, hataki niolewe. Akamwambia akija kusikia hata
amenitafuta, safari hiyo watamfunga jela. Alilia Omar, lakini akakubali kuniachia.
Akataka kutoa gari iturudishe Dar, mama na Ron wakamkatalia. Wakamwambia
hawataki hata kumuona pale hospitalini karibu na mimi.”
“Basi. Mama na
Ron wakakaa na mimi pale hospitalini Iringa kama siku tatu hivi, nikaruhusiwa,
ndio nikarudi nyumbani. Lakini Andy, nilirudi nikiwa nimejifunza, sikuwa na
hamu. Sikuwa natoka, labda mama anitume dukani, narudi nyumbani haraka.”
“Kwanza aibu, hata kwa ndugu huwezi kwenda! Wenzangu
nilikuta wapo mbali kielimu. Mimi nikakuta majibu nimepata daraja la tatu
kwenda nne.” “Lakini bado ulijitahidi.” “Nilikuwa namasomo yangu hayo, nilikuwa
sifeli. Na ndio yaliniokoa.” Andy akacheka.
“Masomo gani?” “Kiswahili, English, nilichukua na
mapishi, na historia. Hayo nilikuwa nasoma na kuzingatia kidogo.” Wakacheka
kidogo, kisha wakatulia.
“Ehe!” “Ndio basi nimemaliza. Lakini mama na Ron wanawasiwasi
sana na mimi. Kila ninapotoka asubuhi, mama alikuwa akiniambia leo mpaka
analia, eti anakuwa na wasiwasi hajui kama nitarudi nyumbani. Vile ulivyokuwa
ukiniona nakuja kukaa pale ofisini kwenu, nilikuwa nikifanya makusudi ili kuwathibitishia
nimebadilika. Sitoroki tena na wala hakuna mambo ya wanaume. Ndio
maana nilikuwa nikitoka tu shule, nakimbilia pale kwa Ron.” “Kumbe!” Andy
akacheka kama anayefikiria. “Nini?” Mina akamuuliza. “Umejibu mambo mengi
sana.” Mina akainama. Pakazuka ukimya. Mina akajua ashakinahiwa na uchafu
wake, anatafuta jinsi ya kujitoa. Wote kimya.
~~~~~~~~~~~~~
Pale Penzi/hisia
Zinapokutana na uhalisia WENYEWE.
Ndipo Penzi
hupitishwa kwenye moto. Hapo ndipo hung’aa au huteketea kabisa.
Andy
ametambulishwa kwa Mina mwenyewe.
Uwamuzi
ni wake.
Kusuka au kunyoa!
Inaendelea…
0 Comments:
Post a Comment