Andy alikaa hapo kwa muda akiwa ameduaa, asiamini
kilichomtokea. Akajuta kumuudhi Mina
kwa ajili ya Lora ambaye hana hata nidhamu!
Akajichukia kupuuza hisia za siku ya
kwanza tu pale Lora alipomcheka
baada yakumwambia anaridhika na kazi
yake. Akajuta na kuona anamkosa Mina
sababu ya Lora ambaye ni bure kabisa! Akachukia
kudhalilishwa na Lora ambaye ni kama mdogo wake tu! Akafikiria jinsi alivyosoma na kuheshimika na wengine, Lora
anamwambia SIO KITU! Akashangaa sana
nafsini mwake, akaona heri aende tu mazoezini. Maana ni kama kichwa kilikuwa
kinataka kupasuka.
Alikwenda gym. Alifanya mazoezi siku hiyo zaidi ya
siku zote alizokumbuka kukaa gym. Kila kiungo alikipatia zoezi zito, mpaka ile sauti ya Lora ikaanza kupungua masikioni
kwake. Akakimbia kama lisaa lizima kwenye mashine kitu kisicho kawaida yake. Akasikia kifua kimefunguka. Ndipo akarudi nyumbani.
Mapenzi Ni kama uyoga, huota popote.
Hakuchagua
kumpenda Mina. Alijikuta tu moyo umependa. Alioga na kwenda kujitupa
kwenye kochi, angalau akiwa ametulia lakini mawazo yakiwa kwa Mina. Ujumbe
ukaingia. ‘Nimepata barua. Asante Andy.’ Moyo wa
Andy ulijawa furaha, akacheka. ‘Ulielewa? Na je,
ujumbe ulileta maana?’ Akauliza
Andy. Akaona amesoma.
‘Kwanza nilifurahi kuona umechukua muda wako
kukaa chini na kuniandikia mimi!
Najua una majukumu mengi, Andy. Lakini kitendo
cha kuandika na kuniletea mpaka pale, nimeona umenithamini. Asante. Na samahani kama nilikuwa mkali sana kwako.
Sijui kwa nini niliumia sana! Samahani.’ Mina akamrudishia ule ujumbe.
‘Hapana. Mimi nilikukosea. Samahani na pole.’
Andy akarudia tena kuomba msamaha. ‘Yameisha. Uwe na usiku mwema.’ ‘Kuna sehemu niliomba kuanza
upya. Sijui ulisoma?’ Akarudisha
huo ujumbe kwa haraka.
Mina akacheka. ‘Niliona,
lakini sikuelewa Andy!’ ‘Ukinipa
nafasi, nitakueleza vizuri.’ Mina akabaki akitafakari. Muda kidogo
ukapita akisubiri. ‘Umeshalala?’ ‘Hapana. Nafikiria.’
‘Tunaweza kukutana?’ Akamuuliza. ‘Sidhani. Maana
nakuona upo na majukumu mengi Andy. Halafu una watu wanao kuhitaji. Sitaki tuwekeane tena ahadi ikashindikana tena.’ ‘Nipe nafasi ya pili, utaona
mabadiliko.’ Akarudisha hayo majibu kwa haraka.
‘Labda uniambie wewe ungependa tukutane
wapi! Mimi natoka darasani saa nane mchana. Jumatatu mpaka ijumaa. Jumamosi na
jumapili baada ya ibada, nakuwa tu nyumbani.’ Mina akarudisha huo ujumbe.
‘Basi naomba jumamosi hii, mida ya saa nne
asubuhi tukutane. Nakukaribisha nyumbani kwangu.’ ‘Nyumbani kwako!?’ Mina alishituka ndio maana akauliza hivyo. ‘Ndiyo. Sehemu ninayoishi.’ Mina akashindwa ajibu
nini.
‘Mina?’ ‘Naogopa Andy!’ ‘Kwa nini? Au huna
imani ya kuwa sisi peke yetu tu?’ ‘Hapana Andy. Wewe nakuamini. Lakini watu
wanaotuzunguka, hawawezi kutuelewa! Zaidi wewe unajulikana kuwa ni mpenzi wa Lora. Naamini hata yeye
hatafurahia kujua kama nipo kwako. Labda kama na yeye atakuwepo.’ Andy akausoma ule ujumbe. Akaishiwa nguvu kabisa.
‘Tunaweza kukutana sehemu ya nje tu, lakini
sidhani kama nyumbani kwako ni sehemu sahihi.
Naomba na wewe ufikirie Andy. Tafadhali. Nina maana nzuri tu kusema hivyo.’ Mina akaongeza ujumbe mwingine. ‘Nimeelewa Mina. Kuna sehemu nyingine ambayo wewe unafikiria
tunaweza kupata wakati mtulivu na kuzungumza?’ Andy akauliza akimpa
nafasi na yeye achague.
‘Kwa haraka sina sehemu ninayofikiria.
Lakini leo ni jumatano. Naomba tupate muda wakufikiria. Halafu tutajulishana.
Ni sawa?’ Kadiri alivyokuwa akisoma
majibu ya Mina, moyo wa Andy uliendelea kufurahia. ‘Wazo
zuri. Nashukuru Mina.’ ‘Asante Andy. Usiku mwema.’ ‘Na wewe.’ Angalau
majibizano hayo yakamtuliza kabisa Andy.
~~~~~~~~~~~~~~
Lakini yale mazungumzo yakaibua wasiwasi mwingine kwa Andy. Lora anajulikana na wengi kama mpenzi.
Tena kwa mabusu ya hadharani. Leo gafla anaonekana na Mina! Akakumbuka jinsi
Ron anavyomchunga dada yake! Akajua
Ron hatakaa akamuelewa.
Lea ambaye amekaa na Mina pale kazini na mara zote
aliwakuta wakizungumza na kucheka, je? Halafu Lea alishakuwa akipokea maua na chocolate
kutoka kwa Lora, akitaka amfikishie yeye Andy. Kwa muda mfupi sana tokea wawe
na Lora, Lora alishakuja pale kazini, wakatoka pamoja, tena Lora akiwa
amemshika mkono na kumuegemea kabisa, watu wote wakiona, na wakati mwingine Mina alikuwepo.
Muda mfupi Mina aliofanya kazi pale akielekezwa kazi na
Lea, na kwa kuwa alikuwa mdogo wake Ron, alishajulikana na kila mtu pale kazini
kwao. Na kwa utundu wa Mina, na vile anavyomchokoza
kaka yake kila mara, wafanyakazi wote pale kwenye ofisi ya hapo Samora,
walimfahamu Mina vizuri tu tena kwa kila wanapopita mapokezi na kumkuta amekaa
hapo na Lea. Kwa hiyo Mina na Lora wote walikuwa wakijulikana vizuri sana hapo kazini kwao. Akapoa
kidogo.
Na nyumbani kwao anawaambia nini? Kuwa Lora amemwambia
hafai! Hana akili za maendeleo! Kwamba yeye sio mwanaume wa ndoto zake! Akaona nikujidhalilisha. Kwa kuwa alifanya mazoezi mengi, mwili ulichoka,
akashindwa kufikiria matatizo. Akaenda kitandani. Akarudia tena jumbe za Mina.
Akalala.
~~~~~~~~~~~~~~
Alhamisi ikawa ndefu kwa Andy, zaidi ya siku zote
alizoishi duniani. Angalau Lora aliondoka kwenye picha, japo aliacha janga baya sana moyoni kwa Andy. Alimshusha hadhi kwa namna mbaya SANA. Ni kama alimtusi bila kumbakisha, akamdhalilisha na kumuacha. Alimvua uanaume wote na kumpunguzia ujasiri. Akabaki akijiuliza, na kujijibu huku akijitetea
yeye mwenyewe, kisha kujifariji.
Akavuta simu yake na kutizama jumbe za usiku uliopita.
Akatamani kumpigia Mina, akaona atulie. Akakumbuka ndiyo yaliyomponza.
Akamtumia ujumbe mfupi, ‘Naamini siku yako inaendelea
vizuri.’ Baada ya muda akarudishiwa ujumbe. ‘Nashukuru
kwa kunijulia hali. Nipo darasani. Mwalimu ametupa muda wa kujifunza. Nakutakia
siku njema.’ Ikawa kama ameaga tayari.
Andy akatamani kama wange chat kidogo. Lakini akaona
awe mstaarabu. ‘Asante na wewe. Nimefurahi umejibu.’
Mina akarudisha emoji ya mtu akicheka na ujumbe. ‘Hata
mimi nimefurahi.’ Andy akacheka na kubaki akiangalia zile jumbe. Ron
akaingia na Hatibu.
“Kiongozi naona leo mambo mazuri. Tabasamu mchana
huu!” Hatibu akamchokoza. Wakacheka. “Kiongozi anakula mema ya nchi! Kiti
kikubwa! Upepo mzito! Shida ipo wapi!” Ron akaongeza, wakacheka. Walifika hapo
kumtaarifu kuna sehemu wanakwenda ila watawahi kurudi.
~~~~~~~~~~~~~~
Usiku wakati analala, akiwa anajishauri kama atume
ujumbe wa usiku mwema kwa Mina au la. Kijana huyo mtu mzima ambaye hakuwahi
kupitia maisha hayo ya ujana ya mahusiano yakimapenzi kwa uzito huo, akawa
hajui anatakiwa afanye nini. Ujumbe ukaingia akiwa anaitizama simu yake.
‘Nilitaka kukutakia usiku mwema tu. Naamini
sijakosea.’ Andy akakaa kwa haraka. ‘Naona umeniwahi. Na mimi nilikuwa nimeshika simu ili
kukutakia usiku mwema.’ Akajibu Andy kwa haraka. ‘Asante.’ Akajibu Mina. ‘Umeshapata sehemu
ya kwenda jumamosi?’ ‘Bado.’ Mina akajibu kwa ufupi.
‘Au ulisahau? Mwenzio nasubiria kwa hamu!’ Akatuma huo ujumbe tena. Mina akacheka asimuelewe
Andy. Kimya. ‘Umeshalala?’ ‘Bado, namsubiria mama na
Ron.’ ‘Kwa hiyo naweza kupiga?’ ‘Ndiyo.’ Alipopata tu huo ujumbe, Andy
akapiga. Mina akapokea kwa haraka.
“Pole na kazi.” “Asante, na wewe pole na
shule.” Mina akacheka kidogo. “Asante. Sikutarajia kama naweza nikafurahia shule!” “Walimu
walikufanya nini huko shuleni?” Akauliza Andy kwa utani. “Wala sio walimu. Ni mimi tu mwenyewe.” “Itabidi unisimulie
zaidi siku ya jumamosi.” Mina akacheka.
“Vipi?” “Nina uhakika hutaki kujua historia
yangu, Andy. Unaweza ukakinahiwa, ukashindwa hata kunitizama usoni.
Ukaanza kunikimbia.” Andy akacheka. “Ndio mbaya
kiasi hicho?” “Zaidi ya hivyo unavyofikiria. Nakutakia usiku mwema.”
Akajua anamkimbia. “Usinikimbie bwana Mina! Hatujamaliza swala la wapi
tunakutana.” Mina akacheka taratibu bila yakujibu.
“Mina?” “Sijui Andy. Lakini..” Akasita. “Nini? Niambie tu.” “Labda
hiyo siku ya jumamosi tuzungumze kwenye simu tu. Itapunguza usumbufu.” “Sikujua
kama kwako unaona ni usumbufu! Samahani.” “Hata kidogo. Naomba usielewe vibaya,
ni kwa ajili yako. Najua una mambo mengi na watu wa muhimu wakuwafikiria. Sitaki niongezeke kwenye mambo
yatakayokusumbua, na yanayokufanya uyafikirie”
“Naomba hilo nije nilieleze kwa undani siku
tutakayo kutana. Ila wewe sio usumbufu
na ninaitamani hiyo jumamosi ingekuwa kesho.” “Kweli Andy!?” “Sina
sababu ya kukudanganya Mina. Natamani muda na wewe.” Akamsikia Mina akicheka taratibu.
“Na naomba uwe na imani na mimi.” “Nakuamini
Andy.” “Basi naomba ukaribie kwangu. Lakini nitataka kukuongezea imani yako
kwangu.” “Kwa
kufanyaje?” “Tuanzie hospitalini, nataka nipime UKWIMI nikiwa na wewe.” “Andy!
Mbona unaniogopesha?” “Kwa kuwa namaanisha kile ninachotaka kukwambia.”
Mina akanyamaza. “Ni sawa, Mina?” “Sawa, lakini nina
maswali mengi!” “Naomba uyatunze mpaka jumamosi. Unaweza kukuta yakajijibu.”
“Sawa.” Mina akajibu huku akivuta pumzi. “Sasa
hivi naweza kulala vizuri nikijua tuna uhakika wa kukutana jumamosi.”
Wote wakacheka. “Haya, usiku mwema Andy.” “Na wewe
Mina.” Wakakata.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku ya ijumaa kila mtu alijua Andy anafuraha. Aliimba
kwa miluzi mfululizo. Aliingia na kutoka
ofisini kwake kama ambaye asiyeweza kutulia sehemu moja. Mina naye hakuonekana
hapo ofisini kuanzia siku alipopata barua kutoka kwa Andy, hakurudi hapo tena.
Usiku tena akataka kupiga, Mina akamwambia yupo na
mama yake. ‘Tunakutana wapi?’ Andy akauliza. ‘Naweza kukukuta hospitalini.’ ‘Wazo zuri. Au ulitaka
nikufuate?’ ‘Hapana. Nitakuwa sawa tu. Asante kwa kujali lakini.’ ‘Karibu, ila
ukikwama, unijulishe.’ Wakaagana.
Hayawi, Yamekua.
Mina alijitahidi kupendeza. Mama yake alibaki
akimtizama. “Umesema unaenda wapi tena?” “Acha kunitega mama! Sijakwambia wapi
ninapokwenda.” Mama yake akacheka kwa wasiwasi kidogo. “Na ninaomba usiniulize
sana. Nimekuahidi kuto kukudanganya. Ila nakuahidi nikirudi nitakwambia
kila kitu.” “Basi niambie hata unapokwenda.” Mina akasimama kama anayefikiria. Akasita.
“Mama bwana!” “Usiniambie mengi. Niambie tu
unapokwenda Mina, mama. Niondoe wasiwasi.” “Nitarudi mama. Sitoroki
tena. Kwani nilipokuwa nikikutoroka nilikuwa nakuaga au ulikuwa ukiniona
nikiondoka?” Mama yake akanyamaza.
“Naomba niamini mama. Tafadhali. Nimekuahidi
nimebadilika, nimebadilika.” “Naomba ibakie hivyo Mina, mama yangu
mzazi. Tafadhali mama. Tumepumzika zaidi ya mwaka. Angalau akili zangu
zimetulia.” Mina akakaa, nakuanza kulia.
“Usinielewe vibaya Mina mwanangu. Na wala sina nia ya
kukutesa. Lakini wewe ni shahidi. Naingiwa na wasiwasi kila ninapokuona unatoka
hapa nyumbani. Nakuwa sijui kama nitakuja kukuona tena au la!” “Nimebadilika mama. Safari hii nimebadilika.
Nakwenda kuonana na mwanaume.” Mina akaongea akisihi. “Lakini huyu mwanaume sina maelezo naye mengi, ndio
nakwenda kumsikiliza.” Mina akajifuta machozi.
“Una muda gani tokea umfahamu?” Mama yake akamuuliza.
“Sio muda mrefu mama. Lakini ameniomba tukutane naye hospitalini kwanza ili
apime afya yake. Amesema baada ya hapo ndipo tutapata muda wa mazungumzo.
Anaonekana ni mtu mzuri. Sina uhakika na chochote ndio maana nilikuomba niende
kwanza nikamsikilize, ndipo niwe na cha kukwambia.” Mama yake akanyamaza.
“Mama?” “Sijui Mina, mama! Sijui!” “Ni nini mama jamani!?” Mina akaongea kwa
kulalamika. Ron akaingia. “Sikiliza Mina.” Akaanza Ron. “Umetupa muda mfupi
mzuri sana. Ukatuonyesha upande wako mwingine ambao hatukuuona kwa muda
mrefu sana labda tokea utoto wako. Umerudi shule. Ukasoma na mwalimu wako
anakusifia.” Akaendelea Ron.
“Mama alikuwa na tumaini kubwa sana. Sasa hili
unalotaka kulianzisha tena ndilo linalotutia mashaka.” Mina alilia sana.
“Nimebadilika Ron! Nimekuomba uniamini. Naomba niamini.
Nimebadilika kaka yangu. Najua umenigharimia. Najua namgharimu mama. Nimebadilika.
Nafikiria zaidi sasa hivi kuliko zamani. Ndio maana sikuondoka hivi hivi,
nimemuaga mama. Na nimeahidi nitarudi. Sitoroki tena.” Mina
aliongea huku akilia.
“Sina maelezo mengi na huyo mtu, ndio
maana nimemwambia mama anipe muda. Nimfahamu ili nijue ni nini chakuongea na
yeye juu yake. Lakini nataka kuwaambia kwa haraka ni mtu mzima. Ametulia.
Anamajukumu yake. Naamini atakuwa mtu mzuri ndio maana nimempa nafasi
yakumsikiliza. Sina maelezo naye mengi.”
Mina akajaribu kujieleza zaidi.
“Naomba uniamini mama. Nitarudi na sitachelewa kurudi. Na
nitakupigia baadaye ili tu ujue nipo na nitarudi nyumbani. Naomba uniamini mama
yangu. Najua nimekuwa nikikwambia hivi halafu naharibu, lakini safari
hii nimeamua mama yangu. Mwanaume nitakayemkubali, ujue atakuwa mume wangu. Na
nitamwambia cha kwanza, lazima aje kwenu, mumfahamu kwanza.”
“Kama ndio hivyo ni sawa.” Mama yake akakubali.
“Na wewe Ron?” Baada ya mama yake kukubali,
Mina akataka kumsikia kaka yake pia. “Naomba ukumbuke ahadi ya safari
hii Mina.” Mina akainama na kuendelea kulia. “Sisi tunakufikiria ndio maana
tunakwambia hivyo.” “Najua.” Mina akajibu.
“Basi naomba LEO urudi Mina. Iwe leo tafadhali. Uje
ulale hapa nyumbani isiwe vinginevyo.” “Nitarudi
Ron! Nakuahidi nitarudi.” “Sawa.” Ron akatoka. “Nitarudi mama.” “Sawa Mina mwanangu. Na hiyo simu
ya baadaye usisahau. Ujue naisubiria.” Mina akaumia sana. Akanyanyuka nakutoka
hapo chumbani, akitamani kama asiende. Lakini akajua Andy anamsubiria,
lazima aende. Alishamuamsha na ujumbe mzuri wa kumwambia ni kiasi gani
anamsubiria kwa hamu.
Mina&Andy.
Alifika hospitalini sehemu ya kuegeshea magari akiwa
anaonyesha wazi alikuwa akilia. Andy akamwangalia kwa makini. “Vipi? Nini
kimekuudhi?” Akatingisha kichwa kukataa na machozi yakaanza kumtoka tena. Andy
akamsogelea na kumvuta mkono aliokuwa akijifutia machozi, akaubusu. “Twende
tukapime afya. Baada ya hapo tutapata muda wa maongezi.” Akambusu tena,
akamshika mkono vizuri kwa upendo.
“Ungependa na mimi nipime au itakuwa gharama sana?”
Akauliza Mina wakati wanaingia ndani. Andy akasimama na kumshika mikono yake
yote miwili na kumtizama kwa karibu. “Juu ya gharama, hapana. Kuhusu
kupenda kwangu haijalishi. Upime, usipime, kwangu ni sawa. Upo huru
kufanya unachotaka. Ila mimi kupima inamaana kubwa sana, kwa kile ninachotaka
kukwambia baada ya hapa.” “Basi na mimi naomba kupima, japo nilishapima miezi
sita iliyopita.” “Sawa.” Andy akakubali bila shida.
Walitolewa damu, wakakaa nje wakisubiri. Andy akamvuta
mkono na kuanza kuuchezea mkono wake taratibu. Mina akamuona kama anayefurahia
japo mawazo yake yalikuwa mbali. Mara kadhaa alivishika vidole vyake na
kujaribu kuvipanga hivi na vile. Mina akawa akifurahia haswa. Akacheka
taratibu. “Una vidole vizuri!” Akamsifia. Mina akacheka huku akimwangalia kama
asiye muelewa lakini akasema. “Asante.” Mina akataka kama kumuegemea lakini
akajishitukia. Akacheka na kuinama akiwa amevuta mkono wake. Andy akambusu
kichwani na kucheka taratibu.
“Huu mkono ulikuwa kwangu Mina! Umeupokonya.” Akauvuta
tena uleule mkono wa Mina aliokuwa ameushikilia, Mina akacheka. Andy
akapishanisha vidole kama alivyomfanyia Lora na kuishia kumkera, lakini
kwa Mina akafurahia na kumtizama machoni. Mina akacheka tena na kuinama.
Wakaitwa ndani kwa mshauri nasaa. Wakapewa ushauri mrefu tu kwa muda mrefu ndipo
wakapewa majibu yao. Wote hawakukutwa na vijidudu vya UKIMWI. Andy hakushangaa,
kwa kuwa alijijua. Alifanya vile kwa ajili ya Mina. Mina naye tokea alipopima
akiwa na mama yake, hakukutana na mwanaume tena kwa hiyo na yeye alijua wazi
hakuwa na vijidudu vyovyote vile.
~~~~~~~~~~~~~
“Mbona hukuonyesha kushangaa matokeo, japo kufurahia
tu? Au ulijua nini?” Mina akacheka wakiwa wanaondoka hapo kuelekea nyumbani kwa
Andy. “Mama alishanipeleka kupimwa hospitalini zaidi ya mara tatu, kwa hiyo
nilijua kama sijaathirika.” Andy akamtizama. “Kwa nini mama alikupeleka
kupimwa mara zote hizo!?” “Kwa kuwa hakuwa akiamini kama sijaathirika.” Mina
akajibu. “Kwa nini hakuwa haamini?” Mina akanyamaza. “Mina?” “Kwa maisha
niliyoishi, Andy!” Mina akajibu kwa unyonge. Andy akamwangalia. “Ndio maisha
gani hayo?” Akauliza tena Andy. Taratibu tu.
“Naomba tuyaache Andy. Tafadhali.” “Kwa nini?” “Kwa
kuwa sitaki na wewe uongezeke kwenye idadi ya watu ambao wananitilia
mashaka! Naomba tuzungumzie kitu kingine. Tafadhali Andy.” Andy akamwangalia na
kurudisha macho barabarani. Wakanyamaza mpaka walipofika nyumbani kwa Andy.
“Naishi juu kabisa. Karibu.” “Asante.” Wakaongozana. Mina alifunguliwa mlango,
kuingia pananukia.
“Nani anapika?” Akauliza Mina huku akicheka. “Nilipika
ndio nikaondoka.” “Kumbe wewe ni mpishi mzuri!” Andy akacheka. “Vitu vichache
sana. Vingine nilinunua. Nilitaka ukija kusiwe na mwingiliano. Muda utakao kuwa
nao niutumie vizuri.” Mina akacheka na kumtizama vizuri kama ambaye anamchanganya.
“Njoo tule kwanza, ndipo tuzungumze.” “Asante. Ila
nyumbani kwako ni pazuri Andy. Pasafi!” “Nikwambie ukweli?” Mina akatingisha
kichwa huku akitabasamu. “Vingi unavyoviona hapa, nimevikuta humu humu ndani.
Na ndio moja ya kitu kinachonifanya niishi hapa.” “Sikujua! Lakini pia
hongera.” Andy akacheka na kuhamia sehemu ya kulia chakula. “Kaa hapa, nipashe
chakula moto, nikilete.” “Si nikusaidie?” “Mgeni siku ya kwanza.” Mina akacheka
na kukaa vizuri.
Andy akaandaa chakula na kukileta pale mezani, wakala
kimya kimya, akimuona vile anavyotumia kisu na uma vizuri. Akawa mpole.
“Unataka nikuongeze kitu chochote?” “Hapana. Nashukuru. Nimetosheka.” “Unaogopa
kunenepa?” Mina akacheka. “Hata wazo la unene na wembamba halipo kichwani
kwangu. Nakula mpaka nishibe. Hapa nimeshiba. Sijivungi.” “Kama hivyo sawa. Na
baadaye ukisikia njaa, uniambie.” Mina akacheka na kushukuru. Akamsaidia kutoa
vyombo na kuhamia sebuleni. Hapakuwa pakubwa sana. Unaona kila mahali.
“Nikuulize kitu Andy?” Andy akakaa kochi la pembeni
yake. “Chochote kile, karibu.” “Kwa nini nipo hapa? Na kwa nini umetaka mimi
nijue kama hujaathirika?” Andy akacheka kidogo kama anayefikiria. Kisha
akamuuliza. “Umeshasikia Love at first sight?” Mina akacheka kidogo. “Yaani unamuona tu mtu, unampenda?” “Ewaaa!
Bila kumfahamu hata kidogo.” Mina akacheka kidogo na yeye akawa kama anafikira,
akamuona anakunja uso.
“Hivi
inawezekana kweli au inakuwa kama zile tabia za wanaume wale wanao kuwa na
tamaa tu?” Andy akashituka kidogo. “Unamaanisha nini?” “Si unajua kuna wanaume
wanavutiwa labda na rangi fulani ya mwanamke. Au labda unakuta umbile au sauti?
Basi akiona hicho kitu tu kwa mwanamke, anamwambia unampenda. Na mbaya unakuta
wanaanza mahusiano.” Mina akaendelea.
“Wakianza mahusiano, anagundua labda umbile peke yake halitoshi
kwenye mahusiano. Anaanza kumnyanyasa mwenzake.
Tena hata kumpiga. Unakuta anampiga kila wakati, tena bila kosa!”
Akamuona Mina anatokwa na machozi.
“Halafu anaanza kumpiga hata kama hajamjibu
kitu kibaya! Anampiga tu hata akimkuta mwenzie amelala, anaanza kumpiga bila
sababu. Unakuta sasa huyo mwanaume anakuwa alianza mahusiano kwa kutamani tu.” Ikabidi Andy ahamie hapo. “Sizungumzii aina hiyo ya
kupenda Mina!” Akamgeuzia upande wake na kumfuta machozi kabisa. “Nazungumzia
kupenda kule ambako huwezi hata kupumua au kufikiria kwa ajili ya huyo mtu uliyemuona na kumpenda!
Unatamani awe wako kwa garama yeyote ile. Yaani unakuwa umeshajumlisha
madhaifu yote, ukajiambia nikimpata mimi huyo mtu, nitakuwa naye vile alivyo.”
Mina akacheka taratibu.
“Hayo mapenzi ya kwenye movie za kizungu
bwana!” Mina akaongea huku akijifuta
machozi. “Kwa hiyo huamini katika mapenzi ya kweli?” Mina akafikiria kidogo,
kikawa kama kitu kimepita kichwani. Akamwangalia Andy. “Kwani wewe unaamini!?”
Mina akauliza kwa upole. “Lakini ni swali la kijinga hilo. Nimewaona wewe na
Lora jinsi mnavyopendana. Lazima unaamini. Samahani.” Akajijibu Mina
mwenyewe na kuendelea.
“Lakini Andy, mimi nilifika sehemu nikaacha
kuamini kabisa. Inawezekana ipo, ila si kwangu. Naomba usichukulie jibu
langu maanani.” Mina akajirudi.
“Kwa nini?” “Aaha! Nahisi sikubahatika tu. Samahani.
Ulikuwa ukiongea wewe. Endelea.” Andy akajirudisha nyuma ya kochi akifikiria
aanzie wapi tena. Akakumbuka Mina huwa anakwepa hapo. “Lakini nitataka kujua
zaidi Mina!” “Hutakaa ukaniangalia jinsi unavyonitizama sasa hivi Andy. Hutakaa
ukatamani hata kunisikia.”
Mill Kwa Pam
Kazi ya kumuweka
kwenye mstari Pam, ikaanza. Mill akaanza kwa kwenda ofisini mida ya mchana.
Anatoa ofa ya vinywaji. Anamtuma mesenja wa ofisi, apite kote aulizie wanataka
vinywaji gani, kisha akanunue. Akafanya siku ya kwanza na ya pili. Anazunguka
kila meza anawaambia ofa ni kutoka kwa Mill, waagize wanachotaka.
Lona akazidi kupagawa na Mill akijua anayo pesa.
Piti anaporudisha jibu kwa Mill, anagundua Pam hajaagiza kinywaji chochote.
Ikawa hivyo mpaka mara ya tatu. Mill akashangaa maana wengine walikuwa
wakiagiza soda na maji pia. Kama kufuru
tu.
“Kwamba hata
maji hataki!?” “Dada Pam hana maneno mengi, kaka yangu. Ukimfikia na kumwambia
ni vya bure yeye anasema, ‘asante’, yupo sawa. Sina jinsi ya
kumlazimisha.” Akatoa pesa kwa walio agiza, akaondoka.
Siku inayofuata
akawahi asubuhi na mapema. Akamuomba tena Piti aulize kitafunwa. Maana hapo
ofisini walipata kahawa na chai ya bure. Piti akapita tena kila meza. Wengine
wakaagiza kupitiliza. “Pam ameagiza nini?” Likawa swali la kwanza mara Piti
aliporudi na kikaratasi kilichoandikwa oda za wafanyakazi wengine.
“Amenishukuru tu na kuniambia yeye ameleta kitafunwa chake.” Mill hakukata
tamaa.
Kesho yake
akafanya hivyohivyo. Matokeo yakawa yaleyale. Akafanya kwa juma zima. Kama
kuweka mazoea, ili Pam ajue kuna uhakika na vitafunwa vya bure asibebe, aje aagize pale, lakini ikawa hola.
~~~~~~~~~~~~~~
“Sasa hapa
utaishiwa Mill, ukose hata nauli yakurudi Marekani.” “Nitauza kile kiwanja.”
Jerry akawa anacheka, hana mbavu. “Nashauri uanze kuuza hiyo gari kwanza.”
“Nakusaidia wewe, kukuhakikishia ule
umbali nilio tayari kwenda kwa ajili yake.”
“Mike unamsikia?” “Nishamwambia akiishiwa nitamsaidia nauli ya kurudi. Ndio
maana unamuona hana neno kuliwa pesa yote.”
~~~~~~~~~~~~~~
Wakafikiri
anatania. Alichofanya ni kubadili gia. Akahamia kwa chakula cha mchana. Lona
akawa anazidi kufurahia akijua
anahongwa yeye. Maana alikuwa kila
akisikia Mill amefika, basi atapata sababu ya kumfuata hapo ofisini kwa Jerry,
maneno mengi hamalizi!
“Pam ameagiza
chakula gani?” “Amesema yeye huwa analeta chakula kutoka nyumbani.” “Basi ukiwa
unawapelekea wengine chakula, tangaza kuwa na kesho chakula kitakuwepo. Wote
wajiandae kwa chakula.” Piti si mbishi. Muungwana. Kazi yake kutumwa.
Akakubali. Akafanya hivyo na kufanya wote kumpongeza
Lona kwamba safari hii kapata mwanamme wa kuwafaa wote. Lona akajisifu kuwa ashaachana na wanaume wa bongo, kapata
mmarekani, anatema dola.
Kesho yake na
siku inayofuata ikawa hivyohivyo. Pam hakuagiza.
Akaendelea kuhangaika bila mafanikio. “Nifanyaje Jerry?” Jinsi alivyomuuliza,
haikuwa ya utani. Ikabidi Jerry awe rafiki. “Kama rafiki wa kweli na mtu
ninayemfahamu Pam, nakushauri uache. Unajimaliza bure. Ila kama
binadamu, nashauri pengine badili
njia. Hii ya kuhonga ushaona haifai. Na hivi Lona anavyojisifia, sijui
utafanyaje? Itamuina ngumu hata kwa Pam kukufikiria.
Atajua ni mchezaji tu.” Mill akaondoka akiwa ameumia ila hajakata tamaa.
Anamkwepaje Lona bila
kuleta matatizo kwa Pam? Na anampataje
Pam asiyehongeka? Yakabaki maswali
yasiyo na majibu. Akaangalia muda, ukawa hautoshei. Alikuwa amebakisha siku
chache aondoke nchini huku hakuna
dalili ya kumpata Pam.
~~~~~~~~~~~~~~
Akatulia kama
siku tatu bila kutokea hapo ofisini kwa kina Jerry. Siku ya nne wakapita mida
ya jioni akiwa na Mike. Hakutaka kuingia ndani, wakamuita Jerry nje. Wakawa
wakizungumza. Mike ndani ya gari, Jerry na Mill nje. Ila Mill akawa ameegemea
gari wanaongea na kucheka. Warembo wakatoka na pochi zao kwamba ndio wamemaliza
siku ya kazi. Moyo ukapasuka paa! Kama kumeanguka chuma sakafuni baada ya
kumuona Pam.
Kabla hajatupia
salamu, Lona akamuwahi wakiwa wanaelekea walipo upande wa kufuata daladala.
“Umepotea Mill! Nilijua umeondoka bila ya kuniaga.” “Nipo. Majukumu tu.” “Kama
mnaondoka sasahivi tunaomba lifti.” Akaongea tena Lona. Wawili kati ya hao
wasichana watatu akiwepo Pam wakachangamkia kuomba lifti. Pam hata hakuwatizama
mara mbili. Akaungana na kijana mwingine ambaye anafanya kazi hapo, wakawa
wanaendelea na safari yao.
“Pam, kuna
nafasi ya kuwatosha wote nyinyi watatu.” Mill akajikaza na kumwambia kwa sauti
ya kusikika kabisa. Akamgeukia. “Nashukuru, asante.” Hakujibu kwa jeuri, lakini
akawa anaondoka. “Tunaweza kukusogeza na wewe. Itakupunguzia usumbufu wa
daladala.” “Nashukuru. Lakini mimi nipo sawa. Asante. Muwe na jioni njema.”
Akaondoka kabisa hapo. Ila hata vile alivyojibiwa, nakutakiwa jioni njema, akaridhika.
“Leo nakupeleka
kwenye ile nyama choma, niliyokuahidi.
Safari hii mimi ndio nakupa ofa Mill.” Lona akahakikisha anamtoa macho na mawazo kwa Pam. “Nashukuru sana. Ila
naona itabidi tufanye wakati mwingine. Tupo na ratiba ngumu kidogo.” Jinsi
alivyomjibu, sura ya kazi na sauti kakamavu, Jerry akajua Pam keshamchanganya. Akaaga na kurudi
ndani. Wakaondoka na hao warembo.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku zikaisha za kubaki nchini. Alikuwa
akiondoka na ndege ya usiku, mida ya saa nne akaamua kwenda ofisini kwa Jerry, akitamani
kumuona Pam kwa mara ya mwisho kabla hajaondoka na azungumze naye japo hata
salamu tu. Akamkuta Jerry ofisini kwake na Sandra hivyohivyo. “Itakuwa sawa nikimfuata
ofisini kwao?” “Utamwambia nini?” Jerry akamuuliza. “Nimuage tu.” “Mill!?”
“Hakika siwezi ondoka bila ya
kuzungumza naye hata kidogo!” “Utamwambia nini na Lona yupo palepale?” Mill
akafikiria na kushindwa cha kujibu.
Mara mlango
ukagongwa, akaingia Pam. Jerry na
Mill wakaangaliana. “Naona niende sasahivi kabla hapajakuwa na foleni
nikachelewa.” “Naondoka usiku, Pam. Nimekuja kukuaga.” Mshangao wa Pam uliweza kuonekana mpaka usoni. Na vile
alivyozungumza Mill, Pam akabaki amekunja uso akimtizama kama ambaye hajamsikia sawasawa au hajamuelewa!
Mill naye akabaki akimwangalia.
Mara Lona
akaingia. “Harufu yako nimeipata tokea ofisini kwetu! Nikajua tu upo.” Hapohapo
Pam akatoka bila ya kusubiri. Mill alitamani alie. Lona alijaa hapo kwa hili na lile mpaka Mill akaondoka
nchini, hajapata nafasi na Pam.
~~~~~~~~~~~~~
Ni ipi hiyo
historia ya Mina ya kutisha kwa kiasi cha kuogopa
kusema au hata mama yake na Ron kushindwa kumuamini
tena?
Japokuwa Mill amejaribu kutupia neno, lakini imekua kama amegonga mwamba. Lona yupo katikati
ya Love At First Sight!
Endelea kufuatilia.
0 Comments:
Post a Comment