Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 4. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 4.

Akaosha uso na kubaki amesimama mbele ya kioo. Akasikia sauti ya kaka yake. Akafurahi sana. “Ron?”  Akatoka. “Twende wewe! Mama atakuwa na wasiwasi sana.” Mina akaanza kucheka huku anakimbilia alipo. “Kama usingenifuata leo, mwenzio ningelala hapahapa!” Ron akacheka. “Bado uwezekano upo. Barabara zimejaa maji na magari! Nimetembea zaidi ya nusu saa. Hakuna daladala. Twende tukajaribu wote.” Mina akasogea pale, Andy alikuwa amesimama.

“Kusanya vitu wakati mimi naenda ofisini kwetu kumpigia kwanza mama  simu kumtoa wasiwasi.” “Na mimi nilitamani kumpigia, lakini sina hela kwenye simu Ron! Jana ulisema leo ndio utaniwekea!” “Nilisahau.” Ron akajibu kirahisi tu huku akielekea ofinisi kwao.

Andy naye akarudi ofisini kwake. Mina akakusanya vitu vyake na kumfuata Ron. Akamsikia akizungumza na mama yake. “Nipo naye hapa. Yupo sawa tu.” Kisha akaongeza. “Basi acha tujaribishe tuone kama tutapata daladala. Usiwe na wasiwasi mama. Tutafika tu, japo sijui ni saa ngapi.” Wakaagana.

“Haya twende. Lakini usibebe simu wala huo mkoba. Vitaloa na kuharibika.” “Nitaacha wapi sasa?” “Lete nikuwekee hapa kwenye meza yangu mpaka kesho.” Wakati wanataka kutoka, Andy naye akatoka.

“Naweza kuwasaidia usafiri mpaka nyumbani.” Ron akageuka. “Kweli Kiongozi!? Maana najua kwako ni hapo mlango wa pili tu. Kwetu ni parefu mnoo!” “Hamna shida. Twendeni.” Ron akamshika mkono Mina. “Twende.” Akawa anatembea akimvuta kutoka nje, Andy akiwatizama kwa kujiiba bila kuongeza neno mpaka lilipokuwa gari la Andy ambapo wao viongozi hupata sehemu maalumu ya kuegesha magari yao nje ya ofisi tu, sio mbali.

Walipofika kwenye gari yake akawakaribisha. Ron akakaa kiti cha mbele, Mina akakaa nyuma. Kile kitendo cha kutoka tu ofisini kuingia garini ambako ni sehemu ya nje tu, wakaloa. Andy alikuwa na mwamvuli. Hakuwa ameloa. “Unasikia njaa? Maana nilisahau kukuachia hela, nilijua nitawahi.” Mina akajua kaka yake anamuuliza yeye. “Lea alininunulia chakula mchana. Halafu wananidai shule.” “Si ndio malipo ya mwisho?” “Bila hivyo sifanyi mtihani.” “Ulivyojitahidi hivyo!” Mina akacheka.

“Si nilikwambia nitamaliza? Na mpaka safari hii nifanye mtihani.” Ron akacheka. “Lazima utafanya tu. Nitalipa mwisho wa mwezi kabla ya muda wa mtihani kufika. Wewe kazana kusoma ili ufaulu vizuri.” Akamsikia anacheka.

Ron akageuka. “Nini?” “Nimenogewa mwenzio.” “Na nini?” Ron na mdogo wake waliendelea kuzungumza pale garini kama Andy hakuwepo. Na yeye Andy kimya akisikiliza huku akiendesha. “Ungekuwa na hela, au kama ungekuwa na wewe hurudi chuo, mimi ningeendelea, Ron.” Ron akashituka mpaka akageuka kabisa.

“Kwamba ungesoma tena baada ya hapa!?” “Pale pale chuoni wana masomo ya kompyuta ngazi ya juu kidogo, halafu yule mwalimu uliyesema nisimpigie.” Wote wakacheka.

“Na usimpigie.” “Basi yupo na yeye kwenye lile kundi letu. Kwa hiyo anayo namba yangu na wala hajanipigia na wala sijampigia.” Ron akacheka. “Ehe!” “Basi alisema pale pia wanafundisha mambo ya kompyuta kama yale, ila wanafundisha kwa ndani kidogo. Wanafundisha jinsi ya kutengeneza website mbalimbali. Kutengeneza logo za makampuni. Kalenda. Lebo. Vitu vingi.” “Kwa hiyo unataka na wewe ujifunze?” Ron akataka uhakika.

“Nimekwambia nimebadilika Ron! Nitasoma. Sasa hivi nimetulia. Kama ungekuwa na hela, ningesoma.” “Nitalipa Mina.” Mina hakutegemea. “Na wewe chuo?!” “Wewe usijali juu ya hela. Hata hivyo mama hajashindwa kukusomesha Mina. Kwanza atafurahi sana ukimwambia unataka kuendelea. Na hivi ulivyojitahidi mpaka sasa!”

“Na umwambie mama kuwa nimekaa hapo ofisini kwenu, sijavunja hata kikombe!” Ron akacheka. “Usicheke Ron! Mwambie mama ili aamini kuwa nimebadilika. Sasa hivi mimi ni mtu wakuaminika.” “Anajua Mina. Mama anakufuatilia au anatufuatilia kwa makini sana. Wewe kazana upande wako, mengine yatajijibu yenyewe.” “Asante Ron. Nimefurahi umeniamini. Na nakuahidi nitafanya vizuri mpaka utafurahi.” Ron akacheka taratibu na kugeukia mbele.

~~~~~~~~~~~~~

Maswali mengi yakaibuliwa ndani ya Andy aliyekuwa akiwasikiliza hapo wakati anaendesha. Wakatulia kwa muda. Ron alipogeuka nyuma, akamuona amelala kabisa. “Mina! Mina!” Ron akamuita lakini hakuamka. “Nataka alale kabisa kwenye kiti. Hapo ataumia shingo. Amekaa vibaya.” Andy akaona vile unavyomjali. “Unataka tusimame?” “Naona tutakuchelewesha tu. Ngoja nimvute.” “Hata hivyo magari hayaendi. Unaweza kufungua mkanda na kugeuka nyuma. Sitaondoa gari mpaka umalize.” Ron akaona ni wazo zuri.

Akaruka kabisa nyuma, akamtoa mkanda na kumvuta. “Bwana Ron!” “Nakuweka vizuri, acha ubishi.” “Nasikia baridi.” Akamsikia Mina akimlalamikia kaka yake. “Itabidi ujikaze tu. Hamna kitu chakujifunika. Mimi mwenyewe nimeloa. Sogea juu kidogo, shingo itakuuma.” Mina akasogea. Akamfunga tena mkanda akiwa amelala vilevile. “Usianze sasa kukoroma na kumwaga mate kwenye gari ya watu.” Akamsikia Mina akicheka taratibu. “Achana na mimi, Ron.” Ron akacheka na kurudi kukaa kiti cha mbele.

~~~~~~~~~~~~~

Mpaka anawafikisha nyumbani, ilishakuwa saa 4 usiku. Mama yao akatoka na mwamvuli mpaka pale garini. “Wote tumeloa mama. Huo mwamvuli jifunike tu wewe.” “Si atakohoa huyu! Mbona hata hujamfunika bwana!” “Sikuwa na kitu chakumfunika mama. Wote tumeloa, mizigo yote nimeacha ofisini.” Andy kimya.

“Mina! Mina mama!” “Mtingishe huyo mama. Hivyo unavyomuita hawezi kuamka. Au rudi ndani mimi nitamuamsha.” “Sasa sio kwa nguvu na wewe mpaka umuue kwa ugonjwa wa moyo!” Ron akacheka.

“Huu ndio muda wakumlipiza huyu.” Akamsikia mama yao anacheka. “Ujanja wote umemuisha. Muone. Mina!” Akamuita tena. “Na kweli mwanangu safari hii amejitahidi. Sijui ndio amekuwa kweli!” “Naona akili zimeanza kuongezeka. We Mina! Mina.” Ron akamtingisha, akakaa. “Tumefika nyumbani. Shuka ili mwenyewe Andy arudi kwake na yeye akapumzike.” Mina akabaki amekaa. “Mina!” Mama yake akaita. “Mama!” “Twende ukabadili nguo ulale.” Ron akamgeukia Andy na kumshukuru kwa kuwaleta nyumbani kisha akashuka.

“Asante baba. Mungu akubariki.” Akashukuru mama yao pia. “Amina mama.” Andy akajibu na kugeuka. Akamwangalia Mina. “Asante kwa lifti. Urudi salama.” Mina aliongea na sauti ya usingizi. “Karibu.” Andy akajibu na tabasamu. Mina akashuka.

~~~~~~~~~~~~~

Baada ya mama yake kumwambia atamsomesha, akabadilisha mawazo juu ya kuwa sekretari. Akakazana na mambo ya kompyuta. Akaacha kwenda kukaa pale mbele kwa Lea, sehemu ya mapokezi. Akitoka shule akawa anakwenda kukaa mezani kwa kaka yake. Anafanya kazi zake za shule au anasinzia hapo mpaka waondoke. Andy akamuwinda, mpaka akachoka. Wakawa wakiangaliana kwa mbali tu. Na Mina naye akajitahidi hata wasipishane koridoni hapo ofisini.

Alipomaliza mitihani ya awamu ya kwanza akaunganisha. Safari hii ikawa anaingia shule asubuhi kutoka mchana. Hakuwa na sababu yakumsubiri tena Ron, na wakati mwingine alitafuta sehemu yakujisomea. Anakaa hapo anasoma kidogo. Au anakwenda kwa Ron kumsalimia, ndipo anarudi nyumbani.

Akaweka bidii, Ron akampa zawadi ya laptop. Mina akaweka muda mwingi wa kufanya kazi kwenye hiyo kompyuta.

~~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo alitoka shule akaenda ofisini kwa Ron moja kwa moja kwenye meza yake. “Njaa inauma Ron!” Ron akanyanyua uso. “Kwa nini hujala?” “Sina hela!” Ron akamtizama kama asiyemwamini. “Mina!” “Mama alinipa, lakini kuna kitu nilinunua.” Akatoa walet yake akampa. “Hiyo na ya kesho. Sasa kesho nisiione sura yako hapa ukiomba hela.” Mina akacheka.

“Mina!” Hatibu akamuita. “Nataka unitengenezee website.” “Sitaki uchokozi wako Hatibu.” “Sasa wewe msomi gani hutaki kazi?” “Ndio nimeanza tu jamani!” “Kazana sasa. Mimi mteja wako wa kwanza.” “Kwa hiyo utanilipa?” “Pesa nyingi sana.” Mina akacheka. Wakati anageuka, akamuona Andy, kumbe alikuwepo hapo lakini upande wa mwisho kwenye meza ya mwenzao mwingine kina Ron.

Mina akataka kutoka, Ron akamuwahi. “We Mina? Unakwenda kula wapi sasa?” “Mgahawa wenye AC na pazuri, ili nisome kidogo.” “Nimekwambia hiyo pesa na ya kesho Mina! Usirudi tena hapa kesho na shida ya pesa yakula!” “Wewe usiwe na wasiwasi.” Mina akaondoka huku akicheka na wengine wakicheka.

Moyo Hauchagui Yupi Wakupenda.

Na kweli alikwenda kutafuta  mgahawa mzuri, akakaa hapo na kutoa laptop yake. Baada kama ya nusu saa tu, akashitukia Andy amekaa mbele yake. Akabaki ameduaa. “Naomba nikuagizie chakula.” Mina akabaki akimtizama bila ya kujibu. “Nilikuahidi siku ile hospitalini.” “Siku ile uliniahidi mengi na hukufanya Andy, kwa nini unataka iwe leo? Au kwa kuwa watu wako wa muhimu leo hawapo mimi ndio nakuja nyuma?” Mina akauliza taratibu tu.

“Nilikuomba msamaha Mina! Mbona unashindwa kunisamehe?” “Kwa kuwa halikuwa kosa Andy. Ulichofanya ni kugawa muda wako kwa mtu wako wa muhimu. Hukukosea. Ulikuwa radhi kuniacha mimi hospitalini, nikiwa nalia kichwa kinaniuma, ukabaki na mpenzi wako ukifurahia. Tafadhali usizungumzie uliyosema siku ile hospitalini, kwa kuwa unaniumiza bila sababu!” Mina akakusanya vitu vyake pale, akaondoka kabisa, nakurudi nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~

Siku inayofuata akiwa darasani, mwalimu akaingia na kuweka bahasha kwenye meza yake. “Iliachwa hapo ofisini kwangu.” Ilikuwa bahasha iliyofungwa, juu imeandikwa ‘Mina.’ Mina akafungua huku akihisi itakuwa imetoka tu kwa Andy. Ilikuwa imeandikwa kwa mkono. Akaanza kusoma palepale.

Mina!

Upo sahihi. Nilikosea sana. Hakuna namna rahisi yakueleza hili na ukanielewa kile nilichokuwa nikijisikia kila wakati nilipokuwa nikiangalia saa yangu nakujua muda wakukuona unazidi kuisha. Kile ulichosikia na kukihisi wakati nikikupa ahadi ya kurudi kuja kukuona, ilikuwa ni sahihi. Sikukudanganya. Nilimaanisha kwa ukweli, ila nilishindwa kutimiza ahadi yangu. Si kwa kutoona umuhimu wako, ila mazingira yalikataa.

Nakuandikia kukuahidi haitakaa ikatokea tena. Nimejifunza kutokana na hilo pia. Ukinipa nafasi nyingine, utakuja kuona mabadiliko. Tafadhali Mina. Naomba unisamehe na unipe nafasi nianze upya. Utagundua mimi sio tapeli. Tafadhali Mina. Hiyo ni namba yangu ya simu. Nasubiria majibu yangu.

Andy!

~~~~~~~~~~~~~

Andy aliiandika hiyo barua kwa mkono kusudi tu, kumuonyesha Mina amechukua muda wake, akamwandikia na kuipeleka yeye mwenyewe. Na ni kweli ilimgusa Mina. Akabaki darasani akimfikiria Andy lakini asimuelewe. Akawa na maswali mengi yasiyo na majibu. Andy naye akawa na wasiwasi kila wakati macho kwenye simu wakati wote. Mpaka anatoka saa 11 jioni, Mina akawa hajamwandikia chochote. Akajua bado amemkasirikia.

Tatizo ni kile anachojisikia Andy kwa Mina, alijua ni ngumu kwa mtu mwingine anayemfahamu yeye kibinafsi na familia aliyotoka, kumuelewa. Alimpenda kupita alivyowahi mpenda mwanadamu mwingine yeyote. Na hakujua ni kwa nini kwa Mina imekuwa hivyo!

Alimfanya mapigo ya moyo yaende kasi nakushindwa kujisaidia. Alimfikiria kuliko anavyojifikiria mwenyewe. Na Andy anajipenda haswa. Kwa kumtizama tu, utajua ni mtu anayejijali. Kuanzia mwili mpaka anachowaza, utajua ni mtu anayejielewa.

Lakini kila muda mdogo anaokuwa naye na kuzungumza naye hata jambo dogo tu, moyoni kwa Andy ni tukio la kukumbuka na kumfanya abaki akiwaza. Atabakia akifikiria midomo yake. Jinsi alivyozungumza. Alivyosimama na mengine mengi ilimradi alimpeleka kasi japo hawakuendana kabisa.

    Kisicho Riziki, Hakiliki.

Andy alijawa wasiwasi, asijue kingine chakufanya. Lakini ile hali ikamfanya athibitishe penzi lake kwa Mina. Alishakuwa na msichana, lakini hakuwahi kujisikia vile. Kila sekunde iliyokuwa ikienda, hajamsikia Mina, alizidi kuvurugwa. “Mungu wangu nisaidie!” Andy akajisalimisha kwa Mungu wake.

Kazi zilikuwa haziendi, macho kwenye simu muda wote. Akajiambia labda Mina atamjibu baada ya nusu saa, ikaja saa, mwishoe akajiambia labda anataka muda wakutosha. Kwa hiyo itakuwa baada ya kutoka darasani.

Ilipofika kwenye saa 10, akaamua kumtafuta Lora. ‘Tunaweza kuonana leo kwa juisi?’  Akamtajia na sehemu na muda. Lora akajibu, I would love that.’ Andy akashukuru vile alivyojibu kuwa angependelea.

Muda ulipokaribia, Andy ambaye hakuwa amefanya kazi karibia siku nzima, akaamua kusogea tu kwenye miahadi yake. Akafika hapo, akatafuta sehemu ya kukaa, akakaa hapo kama dakika kumi mbele ndipo Lora akatokea.

“Samahani, nilikuwa na majukumu, hivi hapa nimeacha ili tuje tuzungumze.” Andy alisimama wakati amefika. Akamvutia kiti, akakaa. “Asante.” Lora akashukuru wakati anajiweka sawa kitini.

Akamwangalia vizuri. Akampa tabasamu. “Mbona kama umejawa na wasiwasi hivyo?” Lora akamuuliza. Andy akacheka kidogo kama anayetafakari kitu. “Vipi?” Lora akauliza tena. “Hapana. Hii hali haihusiani moja kwa moja na hili ninalotaka kukwambia, japo inahusu.” Lora akajiweka sawa.

“Tuagize vinywaji kwanza?” “Ninahamu ya kujua unachotaka kuzungumzia zaidi kuliko hata hiyo juisi.” Andy akacheka kidogo na kufikiria tena kama anayetafuta pakuanzia. Muhudumu akaja, Andy akaomba waagize tu juisi maadamu wapo pale eneo la biashara, basi waagize hata hiyo juisi.

Yeye akaomba aletewe juisi ya embe, Lora akaagiza ya nanasi. Muhudumu alipoondoka tu, Lora akamgeukia Andy. “Niambie chochote unachofikiria Andy. Nakusikiliza” Andy akavuta pumzi kwa nguvu. Akamtizama Lora.

“Naomba niwe mkweli kwako Lora. Tafadhali usinielewe vibaya.” “Mbona unanitisha tena?” Lora akauliza na tabasamu usoni. “Yuko binti nampenda sana. Nimejitahidi kupuuzia hisia zangu, lakini nahisi nimeshindwa. Yeye sijamwambia. Lakini naona na nimejithibitishia kuwa nampenda na ninamuhitaji kwenye maisha yangu.”

“Sasa kadiri muda unavyozidi kwenda bila kumwambia, na hivi tunavyoendelea na wewe, naona ipo hatari yakumpoteza kabisa.” Andy akaendelea kwa tahadhari sana. Kama anayetoa plasta kwenye kidonda kibichi.

“Sasa nimeona nikwambie ukweli ili nisiwe kama tapeli kwako wakati sisi tumefahamiana kwa muda mrefu sana. Sitaki tuje tuwe maadui. Ninajua wewe ni muelewa, hata hili najua utalibeba vizuri na utaelewa tu.” Ile tabasamu alilokuja nalo Lora liliisha. Akabadilika kabisa usoni mpaka akamuogopesha Andy.

Lora Ambadilikia Andy Vibaya Sana.

“Nilijua tu Andy!” Akaanza Lora taratibu. “Mimi sio mtoto mdogo. Unakumbuka nilikushika mkono kanisani? Niliingiza mkono wangu katikati ya mkono wako. Baada ya muda mfupi sana ukauachia. Ilikuwa kama kule kusimama, ndiko kuliko kuokoa.” Andy akajisikia vibaya hakujua kama Lora alilijua hilo.

Nilihisi, lakini nikajiambia nilazima nihakikishe. Mara kadhaa nikataka nafasi ya kukushika, ukawa kama unanikwepa mpaka usiku tulipoondoka. Nilikuwa pale na familia yangu, lakini nilikuona wazi mawazo yako hayakuwepo pale. Mara zote uliweka macho kwenye saa.” Lora akaendelea.

Nilijua. Na nikakuona hata jinsi unavyoniangalia, ni kama unanikwepa. Ndio maana kuna kipindi nilikwambia, inabidi niwasubirie baba na mama kwa kuwa wamelewa. Sijui kama ulielewa?” Andy kimya.

“Ile kitu ikanifanya nilipofika nyumbani nifikirie zaidi. Nikaanza kuvuta taswira ya mabusu yote tuliyopata mimi na wewe. Nikaona ni kama mimi mara zote ndio naanza kukubusu. Na nikajiambia inakubidi kwa sababu ya busu la kwanza tulilopata nyumbani kwako!” Lora akaendelea ila kwa jazba kidogo.

“Ndio maana umeona ni kama na mimi niliamua kukuacha Andy. Niliona kuna uzito fulani kwako. Lakini na mimi naomba niwe mkweli tu, Andy. Unisamehe.” “Hamna shida.” Lora akapata jukwaa.

“Tuwe tu wawazi, ipo pressure pia ya wazazi nyuma yetu. Sijui wewe, lakini mimi nyumbani umekuwa ukiimbwa sana. Mama anatamani sana kuona tunaoana.” Andy akacheka kidogo. “Kweli Andy! Lakini ukweli mimi na wewe hatuendani kwa mambo ambayo sidhani kama wazazi hata tukiwaambia, wataelewa. Usinifikirie vibaya, lakini Andy, mimi napenda niolewe au niwe kwenye mahusiano na mtu ALIYENIPITA.” Andy akatoa tabasamu. Akamkumbusha mwanzoni kabisa.

Sitaki kujutia baadaye, ndio maana umenikuta bado nipo peke yangu. Nina wanaume wengi tu wanao nizunguka na kunigombania, lakini bado sijampata mtu sahihi kwangu.” Hapo akajisifia kwa waziwazi. Ila Lora analipa.

“Kwako nilijaribu sababu ya historia ya wazazi. Na nikajua pengine naweza kuja kukubadilisha mawazo na mtizamo.” Andy akakunja uso kidogo. “Nilikuomba usinielewe vibaya Andy! Na nikaomba ruhusa ya kuwa muwazi kwako.” “Ni sawa kabisa.” “Sasa mbona unakunja uso?” Lora akauliza kwa ukali kama mwalimu kwa mwanafunzi darasani. Akiwa amejitoa vazi la wema kabisa.

“Ni kwa kuwa bado sijakuelewa unamaanisha nini! Nilikuwa najaribu kutuliza mawazo, ila sina nia nyingine.” Andy akajaribu kumtuliza.

“Nakubali muonekano wewe ni mzuri tu. Ndio maana kila tunapokuwa mimi na wewe, watu wanatusifia kwa nje. Lakini maisha ni zaidi ya muonekano. Sijui kama unanielewa?” “Bado.” Andy akawa mkweli.

“Ndoa ni ya mpaka kifo kwa sisi wakatoliki. Haya, tunaingia kwenye ndoa, wewe ukiwa na haiba yako hiyo hiyo yakuridhika kwa ulichonacho wakati mimi naona bado unanafasi kubwa sana ya kukua katika maisha! Unaweza kupambana na ukasonga mbele au ukapata zaidi.” Andy alitulia akimwangalia Lora, asimmalize.

“Naomba unielewe na ukubaliane na mimi tu Andy. Umekuja nchini una zaidi ya miaka mitatu. Mpaka leo unaishi kwenye apartment za gharama sana. Huna majukumu, hutegemewi na watu. Kinachokushinda kujenga mpaka sasa ukaishi kwako ni nini kama si kuridhika na kuona ni sawa hiyo pesa unayotupa kwenye ile apartment ya gharama vile!” Lora akaendelea.

“Haya. Labda hilo tukalifumbia macho. Tukaoana. Unafikiri tukija kupata watoto, tutawaleaje? Tutawafundisha nini watoto kwa msimamo na mtizamo kama wako? Au kwa jinsi tunavyo tofautiana! Mimi nitawaambia kazaneni, wewe utakuwa ukiwaambia inatosha, mmefanya vizuri sana! Sasa tutakuwa tukijenga familia ya namna gani?” Lora aliongea kwa kujiamini bila hata kung’ata maneno. Kama anayehutubia kwenye vikao vya kazini kwake.

Mrembo huyo msomi alikuwa akizungumza kana kwamba anaongea na wafanyakazi waliopo chini yake. Andy alibaki kimya akimsikiliza. Muhudumu alishaleta juisi, lakini hakuna ambaye aligusa ya kwake.

“Ni kweli tusingefika mbali. Hata mimi nakuunga mkono. Kama kuna mtu umempata, yeye akaridhika na wewe hivyo ulivyo! Nashauri umchangamkie tu kabla hujapoteza hiyo bahati. Ila binafsi naona hapana.” Akaweka msisitizo Lora kana kwamba yeye ndiye aliyekuwa amemuita hapo Andy.

Andy akatoa tabasamu. “Hayo yote ulipanga kuja kuniambia lini? Maana ni jana usiku tu umetoka kunitumia ujumbe na kuniambia unanipenda sana.” Andy akauliza taratibu tu.

Hapo Lora akapaniki. “Unajua ni kama vile wewe ulivyokuwa ukipokea busu langu. Unajiambia moyoni pengine kuna kitu cha tofauti utakuja kujisikia baadaye! Ndivyo hivyo hivyo na mimi. Nilikuwa najiambia labda baadaye utakuja kupata ile hali ya muamko wa maendeleo. KUTAMANI zaidi. Hutabaki kuridhika na vidogo.” Andy akacheka taratibu huku akimtizama akiwa ametulia tu.

“Kweli Andy! Hata mama nilimwambia. Natamani kuolewa na mtu ambaye ananipita kimasomo, mshahara na cheo. Yaani mwanaume ambaye ukisema ni KICHWA ndani ya nyumba, anakuwa kichwa katika kila eneo. Sio kwenye neno la Mungu tu, halafu kwengine anapelea! Yaani inabidi mama ndio awe anapambana! HAPANA kwakweli.” Lora akawa kama amemvua nguo Andy. Alijitahidi kumdhalilisha kisomi. Ilimradi tu kuachwa kule kusimuache yeye ameshindwa.

“Halafu hata hivyo sasa hivi nipo kwenye kipindi ambacho nahitajika sana kazini. Sina muda wa ‘drama’. Hata hapa nimekuja ili kujua una shida gani! Nikahisi ni kama ulitaka kuja kuniomba kunioa, nilipanga kukwambia HAPANA kwakweli!” Andy akacheka na kuinama kama anayefikiria.

“Kama huna la nyongeza, naomba niwahi kwenye majukumu yangu ya msingi.” “Ni hilo tu. Hakuna lanyongeza.” Lora akasimama akafungua pochi yake, akatoa pesa. Akaiweka hapo mezani. “Naamini itatosha kwa vinywaji vyote na tip ya muhudumu.” Akaongeza Lora na kuondoka kwa kujiamini. Andy alibaki ameduaa.

Mill&Pam.

          Wakati Mike amejitosa kwenye kampuni kubwa ya urithi akifanya kazi kwa bidii na kuingizia kampuni hiyo faida bila wizi, akiishi na Kamila, yeye Mill alikusudia maisha yawe nchini Marekani. Kupambana kufa na kupona mpaka afanikiwa huko. Na Jerry mmoja wa rafiki yao wa muda mrefu tokea sekondari, yeye alioa mapema tu. Sandra alihakikisha hachezewi. Alimbana Jerry mpaka akamuoa.

Na Sandra mwenyewe alikuwa akilipa. Alijaliwa uzuri wa kike. Na ni wale ambao huwa wanasifa ya, ‘beuty with the brain.’ Alikuwa mzuri wa sura na umbile, lakini pia alijaliwa akili nzuri ya kufikiria pamoja na utendaji.

Pesa ya wizi waliyopata yeye na wenzie waliokuwa wakifanya kazi pamoja yeye hakuichezea, akaizalisha na kumfanya afanikiwe mapema sana.

          Alitokea kwenye familia yenye uwezo na inayofahamika. Alipomaliza tu chuo cha uhasibu IFM, akatafutiwa kazi kwenye benki kwenye kitengo cha mikopo, wanalipwa kwa commision, yaani malipo kwa vile walivyokopesha wateja na mshahara kidogo.

Sasa kwa kuwa malipo makubwa ya kipato chao ilikuwa ikitegemeana na ukopeshaji aliungana na vijana wengine watatu hapo, wakatafuta njia ingine mbadala ya kujinufaisha.

          Wanne hao wakawa wakitoka kwenda kwenye maofisi ya watu, mashuleni na sehemu zenye mkusanyiko wa wafanyakazi wengi, basi wanauza mikopo ya benki yao lakini haikujalisha. Wakope au wasikope, maadamu waliandikisha majina ya wahudhuriaji, basi wakirudi ofisini kwa majina yaleyale, wanayatengenezea taarifa ya kutosha, kisha wanawapa mkopo hewa. Ile pesa inaingia mifukoni mwao.

          Kazi ikaendelea kwa wanne hao. Kupiga pesa ya kampuni kwenda mbele. Ila Sandra akili kichwani. Pesa akawa anaiweka kwa jina la Jerry ili wasimkamate. Lengo ni kuja kufungua kituo chake/chao cha kukopesha.

Basi Jerry akaanza mchakato wa kujenga kampuni yao, Sandra ameajiriwa, anaendelea kuiba kwa akili. Mafanikio ya haraka. Hakubweteka kama wenzie. Pesa ya kuanzisha tu cha kwao ilipotimia na Jerry kukamilisha utaratibu wote, hakufanya kama wenzie. Starehe za kupitiliza, wakitapanya, akajitoa mapema hata kabla hawajakamatwa maana dalili zote, walikokuwa wakielekea ni kukamatwa, wenzie walizidisha tamaa na starehe za ujana.

          Yeye na Jerry wakakazana kwenye lao kwa juhudi zote. Na hivi Sandra alishakuwa na uzoefu, haikuchukua muda kufanya vizuri, akitumia madhaifu ya kule alikokuwa ameajiriwa na kuiba hiyo pesa, kubana wafanyakazi wake na kujinufaisha zaidi.

Hakutaka kuajiri waliosoma sana ili asilipe mshahara mkubwa na pia awaendeshe vile atakavyo. Aliajiri warembo wa nguvu kwenye kampuni yake. “Huhitaji wasomi kukopesha watu. Tutatumia udhaifu wao, kufanya biashara yetu.” Ikawa ndio falisafa ya Sandra.

Akaajiri warembo na vijana wawili tu. Yeye na Jerry ndio wakawa wanashikilia pesa yote. Hakuna mwanya wakuiba. Walibana kila kona, huwezi muibia mwizi. Sandra akaweka juhudi, maisha yakaendelea na Mungu akawajalia watoto wawili. Sandra akahakikisha hakuna kosa la mimba ya bahati mbaya. Watoto wawili tu. Wote wakiume. Basi.

~~~~~~~~~~~~~~

          Sasa Mike mtu wa watu, japokuwa Sandra alikuwa akimbana sana Jerry mpaka kukera, lakini hakumpoteza kama rafiki. Na Jerry naye akawa Mike ndio mtu wake wa kutolea dukuduku lake la ndoa. Yakimzidia kwenye ndoa yake basi Mike akawa ndio jalala lake. Atamtupia kila kitu. Na Mike naye alijaliwa hekima ya ajabu. Alijua kumshauri na kumtuliza mpaka akabakia kwenye hiyo ndoa yake na Sandra japokuwa yeye mwenyewe Mike hakuwa na ndoa takatifu ila alikuwa akiishi tu na Kamila kama mke mpaka ikazoeleka kama ni mkewe kihalali.

          Mill yeye hakuwa akiwepo nchini mara kwa mara, kwa hiyo ukaribu ulikuwa zaidi kwa Mike lakini alikuwa akirudi basi kukutana ni mara chache sana, tena sehemu za kula. Na mara nyingi Sandra alikuwepo kama mlinzi. Hawakujali hilo. Ukaribu na kwa Sandra ikabidi pia kuongezeka. Maana ilikuwa ukimtaka Jerry ni lazima upitie kwa Sandra.

~~~~~~~~~~~~~

          Kuna kitu Jerry alimuagiza Mill amletee kutoka nchini Marekani. Kwa hiyo alipofika nchini siku inayofuata ilikuwa ya kazi, ikabidi wamfuate ofisini kwake. Mike alimsindikiza. Walipofika mapokezi Jerry naye akatoka wakawa wanazungumza hapo mapokezi kama ambao hawataki kukaa sana hapo. Wakabidhiane, waondoke kisha kuja kukutana jioni kwenye nyama choma.

Wakati wakizungumza hapo wakiwa wamesimama tu, na Pam naye akiwa na mwenzie wakawa wanatoka kuelekea benki. Kwa hakika Mill alichanganywa. Alipatwa hali ambayo haijawahi mpata kwa mwanamke. Mwenzie Pam akamchangamkia haswa kama aliyeona alumasi mchangani.

“Bosi, huyo mteja mpya nimemuwahi mimi. Nitamuhudumia mimi mwenyewe.” “Lona kwa kuwahi! Huyu sio mteja, ni rafiki yangu.” “Sasa uwaambie bosi wangu. Nishawahi mimi.” Bado Mike na Mill walikuwa hawajaelewa ule MSISITIZO. Mill yeye hakuwa hata akimtilia maanani huyo Lona, mawazo yalikuwa nje alikotoka Pam.

Lona akaendelea kung’ang’ania. “Sio tena na mwingine…” “Lona, huyu ni rafiki yangu.” “Nimekusikia lakini…” “Haishi hapa nchini.” Ikabidi Jerry amkatishe maana alizidi kung’ang’ania.

“Hivi unavyomuona, anapita tu. Anaondoka. Ni mkazi wa Marekani.” “Kwani Marekani mbinguni Jerry bosi wangu! Au kutaka kunibania tu?” “Basi mama.” “Maana naona unamsemea!” Lona akaendelea kulalamika. Jerry akanyanyua mikono juu akicheka. “Basi Lona. Najiweka pembeni.” “Na wengine uwaambie. Uwe shahidi yangu. Sio kuja kunikana baadaye wakati umenisikia kabisa, NIMEWAHI.” “Sawa mama. Mill huyo!” Mill ndio akarudisha akili pale.

“Kwema?” Akawa anawauliza akiwaangalia sasa, Jerry na Lona. “Nakukaribisha mjini. Na baada ya kazi mimi nipo free, naweza kukuzungusha mjini.” “Unafikiri basi mimi mgeni? Najua kila kona. Nilikuwa machinga kabla sijaondoka.” “Machinga uwe wewe!” “Muonekano unaweza kukudanganya. Ila asante. Sasa Jerry?” Akawa kama anamtoa kwake. Akataka aendelee na Jerry.

“Sasa hapa kuna viwanja vipya. Sehemu mbalimbali za kula. Najua huko mnalishwa mavyakula yakizungu. Hapa nitakupeleka kwenye kuku wa kienyeji. Kuku wa kweli. Halafu ofa yangu. Wala usijali.” “Basi hilo nitalikumbuka.” “Na…” “Lona! Unachelewa benki na utagombana na Sandra.” Ikabidi Jerry kuingilia maana alizidi kumbana Mill. Ndio akili ikamrudia, akaondoka huku akiomba Jerry ampe Mill namba yake.

Jerry akacheka akitingisha kichwa. “Nikupe namba yake?” “Nataka ya yule mwenzie. Anaitwa nani tena?” “Pam.” “Ewaah!” “Sasa kama unataka mwanamke, ni afadhali ujichukulie Lona. Pam hutamuweza.” “Kwa nini?!” “Nakwambia humuwezi Pam. Kwanza si umemuona jinsi alivyotupita hapa? Hata salamu hajawapa. ndivyo alivyo Pam. Wewe kama unahamu na waswahili, Lona huyo!” “Wewe vipi Jerry! Mbona unaning’ang’anizia nisikotaka? Nimekwambia namtaka Pam.” “Usifikiri haja hiyo unayo wewe peke yako! Ni msururu. Wanakuja kukopa hapa, hata wasio na shida na pesa, ilimradi tu kumpata Pam na bado wanagonga mwamba. Achana naye. Vipi Mike?” Akawa anamkwepa Mill kwa kurudisha mawazo kwa Mike, Mike akacheka.

“Naona upo kimya!” “Mimi yangu macho kaka.” “Naomba namba ya Pam.” “Mill!” “Hakika namtaka yule mtoto.” “Humpati. Nakuhakikishia humpati. Mimi nawajua wote hawa wasichana. Achana na Pam. Nikupe ya Lona?” “Wewe vipi Jerry?! Mwanamke wako nini?” Jerry akashituka sana.

“Naona unanibania!” “Sasa kama unafikiri mimi nakubania, jioni tukikutana, mwambie Sandra unataka namba ya Pam. Nakuhakikishia mimi sitamwambia chochote Sandra. Halafu utamsikia atakachokwambia juu ya Pam. Mimi nitanyamaza kimya.” “Sawa.” Wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~

Jioni wakakutana. Mike na Kamila, Jerry na Sandra, na huyo Mill. Katikati ya vicheko Mill akachomekea mpaka akamshangaza Jerry. “Mzee! Bado unalo tu!?” “Kwani wewe ni Sandra!?” “Kwa Pam wala usijichoshe. Jiachie tu. Kuna warembo pale kibao.” “Mimi namtaka Pam.” “Humpati. Kama ni shida ya mwanamke, wewe endelea na Lona. Kwanza nasikia ameshakuwahi.” “Mbona nina uhakika nazungumza kiswahili lakini ni kama hamnielewi! Ninayemtaka mimi, Mill, ni Pam. Na si kwamba nina shida na mwanamke, nina shida na Pam.”

“Wala haupo peke yako. Kuna msururu pale! Tuna kazi ya kujiangalizia na kujipatia pesa.” “Sikukwambia mimi?” Jerry akamuuliza. “Wanakuja kukopa pale hata wasio na shida na pesa! Ilimradi tu wakutane na Pam. Na nikikwambia msururu, basi jua ni mrefu. Walio nazo na wasio nazo, wote wapo wamejipanga, wakiamini siku moja watapata ‘ndiyo’ ya Pam.” Sandra akaongeza kumuweka sawa, aelewe. Lakini wapi! “Na mimi najiunga.” Mill akafanya wacheke wasiamini.

“Hakika ninamtaka Pam. Mimi sijapata mwanamke mwenye vigezo vyangu vyote. Ndio kwa mara ya kwanza nakutana naye. Pam! Hakika nitapambana.” “Sasa wewe unajuaje kama anavyo vigezo vyako vyote?” Mike akamuuliza.

“Ya ndani ndio nitataka msaada. Lakini mpaka sasa, kwa tabia yake, kwa jinsi nilivyowasikiliza hawa wanae fanya nae kazi, ambao wanamjua, nisharidhishwa naye. Si malaya. Kwamba hata nikimuacha hapa nchini, nitakuwa na amani kuwa hatanisaliti. Na ndicho kilichokuwa kikinisumbua, hata Mike nilimwambia. Natamani kuoa nyumbani, lakini wengi niliokutana nao, mambo mengi, hawajatulia. Ndio nimekutana na Pam. Sasa nikipata nafasi ya kumfahamu zaidi, naoa!” “Acha masihara Mill! Kwamba unataka wa kufunga pingu kabisa!” “Sasa upate mtoto kama Pam, halafu unamuachia nani kama si ukichaa huo? Wewe vipi Jerry!?”

“Kwanza wala usiende mbali, hiyo ya kumfahamu Pam kwa kupitia mwenyewe, sahau. Pam ananyodo, wote pale wanamjua. Kupata salamu yake mwenyewe shida!” “Yeye mwenyewe shahidi. Alitupita pale bila hata kutuangalia! Na si kwa bahati mbaya! Ndio mtindo wake. Hasimami kusalimia mtu.” “Basi huyo ndio namtaka mimi.” Mike akabaki akimwangalia tu.

“Kaka mbona hutii neno?” “Acha mimi niwe mtizamani tu.” Mike akajibu akicheka. “Naombeni namba yake ya simu.” “Huo ndio mwiko wake. Na pale nishawaonya. Atakayemtoa Pam pale, ajue anamfuata. Namfukuza kazi mchana kweupe. Maana alisema mtu asigawe namba yake hata akija kaka yake yeye mwenyewe Pam, akauliza namba yake, asipewe. Lasivyo tutaonana wabaya.” “Na anavyokwambia hivyo Sadra, hataki mtu ambugudhi Pam. Na wote wanamjua, Pam kipenzi cha Sandra. si mwizi.” Jerry akaongeza.

“Na kwambia hivi, hata umpe milioni 10 apeleke benki. Kule akaambiwa katika hiyo milioni 10, kumezidi elfu kumi, Pam atarudisha. Na ni yeye peke yake ndio mwaminifu pale. Nikiwa na dili zangu za maana, kama mimi na Jerry hatupo, basi namuachia Pam, japo yeye peke yake ndio hajasoma pale. Hana elemu kubwa, lakini ni bora pesa yangu aishike yeye, ndio napata amani popote pale nilipo lakini si wale wengine. Kwa hiyo kama unataka namba ya Pam, uipate kwa Pam mwenyewe.” Mill akatulia akifikiria.

“Upo kaka?” “Mpaka hapa mnachofanya ni kunipa sababu ya kupambana mpaka nimpate. Naona sifa zake zinazidi tu. Hakika mimi ndiye nitamuoa Pam.” Akaapa Mill wengine wanao mfahamu Pam wakicheka. “Walioapa kama wewe ni wengi Mill! Wengi sana.” “Wanaapa kwa mke wa mtu! Pam mke wangu mimi na Mungu alikuwa akinitunzia mimi.”

“Wewe kijukuu cha mtume?” “Wala si kijukuu cha mtume, mimi mwana wa Mungu, na nilishaomba kwa Mungu mwanamke kama Pam. Ni muda tu. Atakuja kukutana na mumewe.” Wakaendelea kumtania kwa hili na lile, wakazungumza mengi Mill akijipanga na kuomba ushirikiano wao. Zaidi kutoka kwa Jerry na Sandra. “Wala usiwe na wasiwasi na sisi. Sisi tupo kama alivyosema Mike, watizamaji. Ilimradi tu, usimkere kiasi chakushindwa kufanya kazi. Hapo tutagombana.” Sandra akaweka msisitizo.

~~~~~~~~~~~~~~

Je, Andy amekosa bara na pwani? Lora amemuacha kwa fedheha kubwa sana, huku akiwa hana tumaini na Mina ambaye hata hajafahamu lengo lake ila kujua mahusiano kati yake na Lora. Kile anajisikia kwa Mina, tokea siku ya kwanza anamuona, hawezi jisaidia japo vigezo vingi hawaendani. Ila moyo umependa tokea siku ya kwanza anamtia machoni. Love at First sight.

Mill ameapa kumpata Pam mwenye vigezo vyake vyote alivyoona siku ya kwanza kumtia machoni. Love at first sight. Amekubali kuunga msafara kama wengine.

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment