![]() |
Ijumaa jioni akaamua kumtumia ujumbe Lora akiwa hana
uhakika kama atajibiwa baada ya kuachana kwa staili ile siku ya jumatatu. Lora
hakuwa binti wa hovyo. Mwanaume yeyote angefurahia kumpata. Kwa uzuri
alijaliwa. Binti wa kisasa na hata kwakumwangalia tu, alionekana ana mipango.
‘Week yako inaishaje?’ Akatuma huo ujumbe. Akasubiria karibu masaa mawili,
hajajibiwa. Andy alijua anajifanya aghali tu, lakini alijua na yeye
analipa. “Atapata wapi mwanaume kama
mimi!” Akajisifia Andy kwa kiburi kidogo. Baada ya masaa mawili na nusu,
Lora akajibu. ‘Nani mwenzangu?’ Andy akacheka sana. ‘Samahani
nilikosea namba.’ Na yeye Andy akaweka nguvu, akatuma huo ujumbe na
kusogeza simu mbali kwa hasira.
Jioni wakati anakaribia kutoka ofisini, akaona simu ya
Lora ikiingia. Akaiangalia na kuamua kuipuuza. Alishamkera. Akarudisha simu mfukoni, akaenda kuwaaga kina Ron.
“Tutaonana jumatatu jamani.” “Mapumziko mema Kiongozi.” Akajibu Hatibu na
wengine kasoro Ron aliyekuwa ameinamia kompyuta yake kama amezama kwenye
anachofanya.
Ikabidi Andy ajisogeze. “Sasa vipi kesho?” Akauliza Andy akitaka uitikiwaji kutoka kwa
Ron zaidi. “Mimi nipo tu, Mkuu.” Akawahi Hatibu. “Tupe muongozo. Au unasemaje
Ron?” Ron akanyanyua kichwa na kumtizama Hatibu akiwa amekunja uso kidogo kama
ambaye hakuwa akijua ni nini Hatibu anazungumza.
“Vipi kesho
yako? Kiongozi anauliza.” Hatibu akamuweka sawa. “Kwani kesho kuna mpira
tena!?” Ron akauliza kwa mshangao kidogo. “Kwani lazima mpira tu, wewe vipi
bwana?” “Hapana. Nilijua nimepitwa na ratiba ya soka.” “Kwa hiyo?” Hatibu
akauliza huku Andy akiwaangalia. “Tunaweza kukutana kwangu tukaangalia ligi ya
Uingereza kesho jioni. Au mnasemaje?” Akaongeza Andy, lakini nia yake zaidi ni
Ron. Ukweli Andy hakuwa na marafiki wengi mjini. Tokea mtoto alikuwa akiishi
Nairobi shule za bweni.
“Mimi nitatokea Kiongozi. Mpira wa wengi unanoga.”
Akaongezeka na mwingine na mwingine, wakajikuta wamefika wanne, lakini Ron
akawa hajatoa jibu la moja kwa moja. Simu ya Lora ikaingia tena. Akataka
kuipuuza, akaona aipokee maana kila mtu alitulia kwa muda wakimtizama yeye na
simu aliyokuwa ameitoa mfukoni, akabaki akiitizama ikiita. “Basi nitawaona
kesho jioni.” Akaaga Andy huku akipokea simu.
“Hellow!” “Andy?” Akauliza Lora. “Ulikuwa
ukimpigia nani?” Andy akauliza taratibu tu. “Samahani.
Tokea asubuhi nilikuwa na vikao vya hapa na pale, mambo yalikuwa mengi.
Nilisoma ujumbe bila kusoma jina.” Andy akajua anadanganywa. “Okay.” Akajibu Andy. “Kwa
hiyo ndio sikuwa nimejua kama ndio wewe, nikakuuliza ni nani!” “Utakuwa
hukusoma ujumbe uliofuata. Niliomba msamaha kuwa nilikosea namba.”
Akamsikia Lora anacheka.
“Nani huyo mwenye bahati yakuuliziwa week
yake inaishaje?” “Mwenye namba yangu sahihi.” Akajibu Andy huku akitoka hapo ofisini. “Haya
bwana! Na mimi nataka kujua week yako iliendaje?” “Acha kuiga sasa!”
“Siigi! Kweli nataka kujua.” Lora akaongea huku akicheka. “Ilikuwa nzuri.” “Nimefurahi kusikia hivyo.” “Yaani umefurahi kusikia week yangu imeenda vizuri!?”
Andy akauliza kama hasadiki. “Kabisa.” “Sawa.”
Wakatulia kidogo.
“Kesho tunaweza kukutana kwa kifungua
kinywa?” Akauliza Lora. “Ila mimi huwa siku za jumamosi natumia muda mwingi
mazoezini, gym.” “Naweza kuja huko nikaungana na wewe?” “Unamaanisha uje ufanye
mazoezi!?” Akauliza Andy kama ambaye hajamuelewa vizuri
wakati amemsikia vizuri tu. “Ndiyo. Au hamruhusiwi
wageni? Maana mimi huwa nakimbia kila siku asubuhi. Sasa naweza kuja kukimbia
huko na wewe.” Andy akatulia kidogo, akaona atoe nafasi nyingine.
“Sawa. Hiyo itakuwa nzuri tu. Sikujua kama
unapenda mazoezi!” “Ni kukimbia tu. Huwa siwezi kuanza siku bila kukimbia.
Labda niwe mgonjwa.” Hilo nalo
likamfurahisha Andy. Angalau akaanza kucheka na kuendeleza mazungumzo baada
yakuona na hilo wanaendana. Waliendelea kuongelea mambo mengi juu ya
umuhimu wa mazoezi huku wakicheka. Waliambiana hili na lile, safari hii na yeye
Lora akawa kama amejionya. Akajiwinda maneno.
Andy & Lora.
Siku ya
jumamosi saa moja kasoro asubuhi wote wakajikuta wanaegesha magari yao sehemu
moja. Wakacheka. “Mimi nilikuwa nakuwahi wewe ili nisikucheleweshe.” “Na mimi
nilikuwa nakuwahi, sikutaka unisubirie kama siku ile.” Andy akaongeza wakati
anamsogelea. Akataka kumpa mkono, Lora akajidai kama hajauona, akamsogelea na
kumbusu shavuni na kurudi kumwangalia machoni na tabasamu zuri usoni. Andy
akacheka kidogo.
Wote walikuwa wamevaa nguo za mazoezi. Lora alipendeza
na mwili wake, ungependa kumtizama. Wakaingia ndani moja kwa moja wote
wakaelekea kwenye traid mill, mashine ya kukimbilia au kutembea. Wakaanza
kukimbia. Kweli Lora alionekana ni mkimbiaji. Alikimbia mpaka Andy mwenyewe
akasalimu amri. “Mimi naona nihamie kwenye kunyanyua vyuma.” Lora akacheka huku
akiendelea kukimbia. “Nitakufuata. Acha mimi nimalizie hizi dakika tano.”
“Sawa.” Andy akaondoka na kumuacha akikimbia.
Wakati anaendelea na mazoezi ya kifua, Lora akawa
anakuja akiwa anatokwa jasho, anajikausha na taulo dogo. “Ndio unafanya nini?” Akauliza.
“Pumzika kidogo, nikuonyeshe.” Akasimama pembeni huku akimwangalia akiendelea.
Baadaye akajiunga naye. Akawa anamwelekeza na kufanya pamoja. Kukawa na kucheka
na mazungumzo kidogo juu ya kile wanachokifanya.
Wakawasogelea warembo wawili. “Rafiki yangu amependa couple
yenu!” Mmoja wa wale warembo wakawaambia Lora na Andy. Wakacheka. “Asante.”
Akajibu Lora huku akimwangalia Andy. Wale warembo wakaondoka. Wakabaki
wakicheka tu bila kuzungumzia hilo tena. Andy alikuwa amevaa na yeye kata
mikono nyeupe na pensi nyeusi na mistari mweupe pembeni. Raba nzuri ya Nike, na
soksi hizo hizo za Nike nyeupe. Safi.
~~~~~~~~~~~~~
Andy alimwambia baada ya mazoezi waende nyumbani kwake
atamtengenezea kifungua kinywa kizuri. Mrembo Lora akahamasika kujaliwa na pia akakubali akitaka pia akapaone nyumbani
kwake kujua jinsi alivyojijenga kama ni mume wa kuoa au la! Maana hata yeye
Lora alikuwa na mume wa ndoto zake.
Hakutaka mwanaume aliyechini yake kiuwezo na kimawazo. Angalau walingane na awe
na akili za maendeleo sio mzubavu.
Kwa umri wake na urembo wake hakuwa amekosa wanaume au mume wa kumuoa, ila alichagua sana. Hakupata mwenye vigezo
vyake vyote. Kila mwanaume alikuwa na kasoro alizoshindwa kuzifumbia macho na kukubali ndoa.
Kwa Andy.
Wakaongozana mpaka kwa Andy akamkaribisha sebuleni.
Akawa muungwana akajituliza kochini akisubiria mwenyeji wake afanye mambo yake
kama alivyoahidi. Andy aliingia jikoni akaanza kwa kutengeneza smothie
nzuri yenye virutubisho muhimu kwa mwili. Lora akaipenda. Wakati wakinywa hiyo smothie,
akarudi tena jikoni kutengeneza omlet nzuri sana aliyochanganya na
uyoga. Ikaleta ladha zuri kwa zile mboga mboga alizochanganyia kwa kiasi na
viungo kwenye yai. Hapo napo Lora akasifia. Wakakaa na kula na maongezi ya hapa
na pale wakijaribu kufahamiana.
Hapakuwa na ubishi kuwa wawili hao waliendana. Muda
mwingi walijikuta wakicheka mpaka mapungufu mengi aliyoyaona kwa Andy akakubali
kuyafungia macho. Angalau Andy akapitishwa japo hakuwa asilimia 100 kwake.
Akajiambia akitangaza ndoa, wakishaoana, kwa kuwa amesoma na ana kazi tayari atamrekebisha tu. Kwa wakati huo afunike
kombe, mwanaharamu apite.
“Sasa kabla muda wa chakula cha mchana haujanikuta
hapa, acha mimi niende. Nikaoge, niende salon.” Andy akacheka na kusimama ili
atoe vyombo. “Nashukuru kwa kuja. Uwe na siku njema.” Akaelekea jikoni.
Wakati anageuka akiwa jikoni, Lora alikuwa nyuma yake.
Andy alijua anachotaka. Akajisogeza
karibu zaidi. “Nimefurahia kila kitu.” Lora aliongea kwa sauti tulivu na ya chini. “Hata mimi nimekuwa
na wakati mzuri. Naamini tutapata wakati..” Lora akawahi midomo ya Andy.
Akambusu mara mbili mfululizo. Andy akamshika kiunoni na kumvutia kwake na
mkono mwingine akamshika shingoni ili kupata busu zuri zaidi.
Wakabadilishana ndimi, Lora akitoa pumzi nzuri
za kimahaba. Mwishoe Andy
akamwachia na kumwangalia, Lora akacheka
akilamba midomo ya nje taratibu kama aliyefurahia walichokuwa wamefanya, huku
Andy akiwa bado amemkumbatia. Akambusu kichwani. Lora akamwangalia.
“Nitakuona wakati mwingine. Asante.” Lora akajitoa
mikononi huku akicheka taratibu. Akaondoka wote wakihema maana walifikia sehemu
ambayo ni vile Lora alikumbuka amelowa jasho kwa mazoezi na atakuwa akinuka
huko chini zaidi. Asingethubutu kujitoa kwake kwa mara ya kwanza akiwa na
harufu ya jasho, lasivyo angechangamkia penzi. Lakini alifurahia sana.
Ilipofika jioni kina Hatibu na wafanyakazi wengine
wakaanza kuingia mmoja baada ya mwingine. Andy akajua Ron alishindwa kufika,
akatulia tu. Alishapata busu zito asubuhi kutoka kwa Lora, nafsi ikatulia.
Akawahudumia vinywaji wageni wake huku maongezi na vicheko vikiendelea lakini upande mwingine wa nafsi ya Andy ulitaka kujua ni kwa nini Ron hajafika. Akapingana na
hilo wazo lakini akashindwa.
Hatibu alipokuwa anafuata maji jikoni, Andy naye
akamfuata akijidai anataka kumsaidia. “Naona Ron ameshindwa kufika!” Akatupia
hilo neno wakiwa jikoni akimpa maji mgeni wake. “Nilikuwa naye hospitalini
karibia jioni nzima hii. Tulikuwa tukisubiria dada yake apewe kitanda.” Moyo wa
Andy ukashituka sana.
“Hospitali tena!?” “Yeah. Nilimpigia mchana
kumwangalia, na kumuuliza kama ataweza kuungana nasi, ndio akaniambia wapo pale
tokea asubuhi, amemsindikiza mama yake,
dada yake alikuwa akipandisha homa tokea jana asubuhi. Asubuhi hii
akaanza kutapika ndio ikabidi wampeleke hospitalini.” Hatibu akawa amemaliza.
“Sasa walimkuta na nini?” Andy akauliza tena.
“Wamempima vitu vingi, lakini si unajua mambo ya hospitali kama zile! Ugonjwa
ni mmoja tu. Malaria. Wamemuanzishia
dripu. Naona watamlaza hapo kwa siku chache. Ameshindwa kumeza dawa, anatapika
sana. Ila mpaka mimi naondoka, alikuwa amelala.” “Kwa hiyo wamemuacha na mama
yake?” “Hapana. Pale hakuna nafasi ya kulala na muuguzaji! Wodi yenyewe ilikuwa
imejaa. Ilibidi kusubiria kweli. Wamekaa pale tokea asubuhi!” Andy akajisikia kuumia sana mpaka akajishangaa!
“Umesema ni hospitali ya wapi?” Hatibu akamuelekeza
mpaka wodi. “Lakini si unajua pale mida yake? Labda kumpigia tu Ron nakuulizia
hali yake. Ila nafikiri Ron atakuwa kazini jumatatu. Hawezi kuacha kuja kazini
sababu ya hilo.” Hatibu akaongea hivyo asijue
tatizo wala sio kazi. Zile habari zikamuumiza
sana Andy na kumpokonya raha nzima
ya mpira. Na bahati mbaya na timu yake ikawa imefungwa. Usiku huo ukawa mbaya zaidi kwake hata asikumbuke tena
busu la Lora.
Jumapili. Mina!
Alishindwa kujizuia kabisa. Asubuhi na mapema Andy
alielekea hospitalini kumuona Mina
kana kwamba anamfahamu. Akaulizia ilipo wodi aliyoambiwa na Hatibu,
akaonyeshwa. Alimkuta Mina amelala. Akamgusa. “Mina!” Akamgusa tena kidogo.
Akaamka. Mina akamwangalia akacheka. “Rafiki yake Ron?” Akauliza na tabasamu la
usingizi. “Ulikuja nyumbani.” Akaongeza Mina kama anayejaribu kumkumbuka na
cheko la kichovu. Andy akacheka huku akitingisha kichwa kukubali.
“Wewe mbaya!” Akalalamika Mina taratibu. “Kwa nini
unasema hivyo, Mina?” “Uliondoka bila kuniaga wakati mimi ndiye
niliyekufungulia mlango, wakati rafiki yako akiwa anakoroma!” Wakacheka
taratibu, Mina akafunga macho. “Samahani.” Andy akamfanya Mina afungue macho.
Akacheka taratibu. “Nakuchokoza tu. Hata hivyo sikuwepo nyumbani. Mama
alinituma, kurudi nikaambiwa mlishaondoka.” “Afadhali sina kosa.” Wakacheka
tena kidogo.
“Unajisikiaje?” Akamuuliza. “Nimeacha kutapika. Ila
kichwa bado kinauma sana.” Machozi yakatoka
pembeni ya macho ya Mina, akataka kujifuta. Andy akayawahi. Mina akacheka
taratibu. “Asante. Lakini mama amesema labda dripu
ya tatu itakuwa nafuu.” “Labda. Pole sana.” Akamfuta tena machozi. “Ila
bado kichwa kina moto!” Andy akampapasa kichwani kwa upendo, taratibu.
“Walinipa dawa ya kushusha homa. Sidhani kama masaa nane yamepita. Wanakuja
kuichoma hapa.” Akamuonyeshea pale palipounganishwa dripu.
“Unajua hata wanakupa dawa gani?” “Walimwandikia Ron,
jana. Akaenda kununua. Ni nyingi, ila najua ipo yakuzuia kutapika na kushusha
homa.” “Pole sana. Basi ni kweli kuzipa hizo dawa muda, utapona tu.” “Naamini
hivyo.” Mina akajibu taratibu. Wakatulia kidogo.
Kisha Mina akamwangalia. “Umependeza na unanukia
vizuri.” Andy akacheka. “Nikitoka hapa, nakwenda kanisani.” “Basi uniombee nipone.” “Nitakuombea.” Wakacheka tena
taratibu. “Sijakuletea kitu. Unatamani kula nini?” “Hamna shida. Nashukuru hata
kwa kuja kuniona.” Mina akanyoosha mkono wake wa kushoto kule alipokuwa
amesimama Andy, Andy akaupokea na kuuminya kidogo. Mina akacheka taratibu kama
aliyeridhika.
“Nitakuona baadaye.” “Kwani utarudi tena?” Mina
akauliza. “Ndio maana nimeuliza una hamu ya kula nini!” Mina akacheka na
kung’ata midomo. “Niambie chochote kile.” Akamwambia kwa kumbembeleza. “Natamani
bahati hiyo ningeipata wakati mwingine.” Wakacheka.
“Wakati mwingine unakuja, niambie leo.” “Tokea juzi
sina hamu kabisa ya kula. Ila mama alisema ataleta uji wa limao, nijaribu
kunywa leo kwa kuwa sijala kama siku tatu hivi, natapika tu!” “Pole sana.”
“Asante. Kwa hiyo usilete kitu chochote kile.” Bado Andy alikuwa amemshika
mkono.
Mwisho akajishitukia na kumwachia. “Sawa. Basi
nitakuona baadaye.” “Haya. Asante.” Mina akafunga macho, Andy akimtizama.
Akamfunika vizuri. Akabaki akimtizama. Mina akafungua macho, akamkuta bado
amesimama akimwangalia.
Akatoa tabasamu. “Nilifikiri umeshaondoka! Nafunga
macho kupunguza maumivu ya kichwa. Eti naona kama huu mwanga wa taa
unanizidishia maumivu ya kichwa!” Andy akamgusa tena kwenye kipanda uso
taratibu. “Pole. Wewe pumzika tu, mimi nitaondoka.” Hapo hapo Mina akafunga
tena macho. Akatamani kama ainame na kumbusu, akaona aondoke tu kabla hajafanya
jambo lakuja kumfanya ajute baadaye.
Akamtengenezea shuka tena. “Asante.” Mina akashukuru
akiwa amefunga macho. Andy alitamani kama asiondoke, lakini pia hakuwa na
majibu yakutosheleza kwa Ron endapo
atamkuta hapo, na kwa familia yake
endapo atakosa kufika kanisani kama ilivyo ada kwao. “Nitakuona baadaye Mina.”
Kama aliyekuwa akiahidi. Mina
akafungua macho na kutingisha kichwa kukubali. Andy alimtizama kidogo,
akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~
Alifika kanisani akiwa amewahi kidogo. Akabaki
akifikiria garini. Akapotea kabisa mpaka akasikia kioo cha gari kikigongwa tena
taratibu. “Lora!” Akashusha kioo. “Nimeshajua kwenye gari ndio maeneo yako
yakupata muda wakutafakari mambo yako.” Wakacheka, Lora akajisogeza na kumbusu
midomoni. Lakini safari hii Andy hakurudisha busu. Lora akashangaa nafsini
kwake. Akashuka. “Umependeza sana Lora!” “Asante. Hata wewe.” “Asante.” “Naona
muda umefika.” “Kina mama Ruhinda wapo kule mbele, naona wote wamefika, nilikuja
kukuangalia wewe.” “Oooh! Niliwahi kidogo, nikaamua kutulia hapa. Vipi lakini?”
Andy akauliza huku wakitembea kuelekea jengo la kanisa.
“Safi.
Jana nililala vizuri.” Wakacheka, Andy akijua anachomaanisha. “Siku nyingine
huwa hulali vizuri?” Andy akauliza na kumtizama na tabasamu. “Jana zaidi.”
Wakacheka, ukimya ukazuka. Andy akapotelea mawazoni huku wakitembea.
Waliwakuta wazazi wao hapo nje wakiongea na kucheka
pamoja na ndugu zao. Andy akasalimia wote. “Leo umechelewa wapi?” Akauliza mama
yake. “Imekuwa kinyume. Niliwahi zaidi nikaamua kubaki kwenye gari.” Maongezi
yakaendelea kidogo, wakaingia kanisani. Wakajikuta wamekaa pamoja. Lora na
Andy. Andy akatoa tabasamu.
“Leo naona ndio siku ya kutimiza ahadi yangu kwa mama
Ruhinda.” Lora akanong’ona. “Oooh! Leo ratiba imeruhusu?” Andy akauliza na
tabasamu, Lora akacheka na kutingisha kichwa kukubali. “Karibu sana.” “Asante.”
Walikuwa wakinong’ona. Misa ilipoanza tu, wakanyamaza.
Kwa Mina.
Wakati amelala, akamsikia mama yake anaongea na Ron.
Akafungua macho. “Vipi?” Ron akamuuliza. “Kichwa
bado kinauma sana.” “Usilie sasa. Wamekupa dawa?” "Hata sijui!” “Pole
mama yangu mzazi. Utapona.” Mina akafunga macho. “Hakipoi
mama! Kinauma sana.” Mina akalalamika huku akilia. “Naenda kumuuliza
yule nesi pale kama wamempa dawa ya kupunguza maumivu. Kichwa gani hakitulii
jamani!” Mama yao akaondoka pale.
“Halafu rafiki yako alikuja.” Mina akamwambia Ron huku akifuta machozi. “Hatibu?”
Akauliza Ron kwa uhakika. “Hapana bwana na wewe!
Yule aliyekuja nyumbani akakukuta unakoroma.” Ron akacheka. “Yule sio
rafiki yangu wewe, bosi wetu!
Alikuja muda gani?” “Asubuhi hii.” Mina
akajibu. “Labda Hatibu atakuwa alimwambia jana alipoona sijakwenda nyumbani
kwake na Hatibu. Alitukaribisha kwake jana jioni tukaangalie mpira.” Mina
akanyamaza kama anayefikiria.
Mara wakamsikia mama yao akijibiwa vibaya sana mpaka wagonjwa wengine
wakamgeukia. Yule nesi alikuwa ana mjibu lakini kama anayemgombesha! Na alionekana mdogo hata kwa mama yao.
Ron aliumia sana. “Samahani mama. Nimeuliza tu. Sikuwa
na nia mbaya.” Wakamsikia mama yao akiongea kwa unyenyekevu. “Hapana bwana!
Maana nyinyi mmeshazoea kusema manesi wa hapa hatufanyi kazi yetu vizuri,
tunaiba dawa za wagonjwa wenu, tunawauzia wengine. Kwa hiyo kila tunalowafanyia
mnaona halifai!” Mama Ron akaona aondoke tu arudi alipokuwa amewaacha wanae.
Kwa Andy.
Misa iliendelea, akili
na mawazo ya Andy vilikuwa
hospitalini, kwa Mina. Akasugua
mikono taratibu huku akikumbuka kuminya mikono ya Mina, nakuona tabasamu usoni
mwake. Akavuta pumzi kwa nguvu, akatamani kama angeendelea kubaki naye pale
akimfariji wakati mgonjwa. “Huu ndio
wakati ambao pengine angenihitaji zaidi!” Akajutia Andy kutokuwepo pale na
Mina. “Lakini hata hivyo walisema huwezi
kukaa pale muda mrefu.” Akajifariji huku misa ikiendelea.
Kijana
huyo aliyetumikia altareni hakuhitaji kuwepo pale kimawazo ili kujua ni wakati
gani wakupiga magoti, wakusimama na kukaa. Alifuatisha kila kitu bila kukosea,
japo mawazo hayakuwepo pale kabisa.
Akashitukia mkono wa Lora katikati ya mikono yake.
Akashituka kidogo na kumtizama. Akapokelewa na tabasamu zito kutoka kwa Lora.
Naye akarudisha. “God! Natamani Lora
ndiye angekuwa Mina.” Akawaza Andy huku akitamani atoe ule mkono wa Lora
pale katikati ya viganja vyake. Lakini isingekuwa rahisi. Lora alishapenyeza
kabisa na vidole vyake katikati ya vidole vya Andy. Akafungamanisha kabisa. Hakupata
kile alichokipata wakati alipomshika Mina na kushindwa
kumwachia. Andy akashangaa.
Akahisi labda
hakuwa amemshika vizuri Lora. Akaminya kidogo kama alivyomfanya Mina, Lora
akacheka kwa sauti ya chini kwa furaha, akajiegemeza kidogo begani, lakini haikuwa kama kwa Mina. Akaangalia ile
mikono yao pale ilivyokuwa. Akaona hakuna
jinsi nyingine angeushika ule mkono wa Lora, akajisikia alichojisikia kwa Mina ambaye hata hawakupishanisha vidole!
Akasogeza kulia na kushoto. Haikuwa kama Mina, akatulia. Mungu akasaidia
ikafika muda wakusimama. Ikabidi kuachiana mikono. Hilo likamfurahisha Andy.
Misa iliisha, wakakusanyika nje. Kila mtu akatafuta
sababu ya kucheka, lakini walijua hatimaye Andy amemfurahisha mama Ruhinda,
maana alikuwa na furaha yakupita kiasi. Alichangamka akajikuta anaalika nyumbani
kwake familia yakina Lora, wote.
Wazazi na ndugu zake. Paulina na Raza, wakakonyezana. Andy akawaona na yeye
akacheka taratibu. Baada ya mazungumzo, wakakubaliana familia zote waelekee
nyumbani kwa Ruhinda kwa ajili ya chakula na ilikuwa siku ya mchezo. Game
day.
~~~~~~~~~~~~~
Kama ilivyo desturi yao wanawake walielekea jikoni ila
wakamwambia mama yake Lora na Lora, wao wakae tu sebuleni. Wakiwa jikoni Lora
naye akaingia humo ndani. Zikaanza stori huku kila mmoja akiandaa chakwake
kwani waligawana. Baada ya muda na yeye mama Lora akaingia humo jikoni. Vicheko
vilitawala kwenye hiyo nyumba ungejua wazi ni watu ambao wanaelewana katika
kila eneo. Chakula kiliwekwa mezani, kikasindikizwa na mazungumzo mazuri na
vicheko vingi tu, wasijue kile kinachoendelea
ndani ya cheko la Andy. Alitamani
familia hiyo ya kina Lora waage ili na yeye atoke. Lakini haikuwa hivyo. Ni kama hawakuwa na haraka kabisa! Baada
ya chakula wao wakaunga kwenye game. Mashindano na vicheko vikakolea.
Muda wa mchana wa kuona
wagonjwa ukafika na kupita. Bado ugeni upo. “Hata hivyo sasa hivi ni kwa wanao peleka
chakula tu.” Akajifariji Andy wakati akiangalia saa yake. Lakini haikuwa
hivyo. Wakaendelea kuwepo tu mpaka jioni.
Ilipofika saa
12 na nusu jioni ndio watu wakaanza kutawanyika. Alianza kuondoka dada yao na
watoto. Walisema wanawahi kurudi nyumbani kesho watoto wao wanamitihani shuleni
wanataka siku hiyo wawahi kulala. Maana waliunganisha na mpira, ligi hiyo hiyo
ya Uingereza. Zikaletwa bia hapo. Jumapili ikazidi kupendeza ndipo Paulina na
Devi wakaona waage. Vilijaa vicheko vya kilevi huku wakishangilia mpira. Wakati
wote Lora alikuwa karibu na Andy kitu kilichozidi kumfurahisha mama yake.
Saa moja kamili, ndipo Lora akaondoka na wazazi wake. Maana
wadogo zake wawili walishaondoka mapema na gari yao. Walikuja pale wakiwa
wanaendesha magari mawili tofauti. Walipowaacha hapo, ikabidi Lora ndiye awe
dereva kwani wazazi wake walikuwa wamekunywa.
Andy aliangalia muda na kuumia sana
moyoni.
Akabaki akisaidia kusafisha pale, kwani alianza
kuondoka dada yake, akaacha bado watu wakinywa na kula kidogo kidogo. Paul naye
aliga baada ya muda mfupi tu, akasema ameitwa kazini. Akaja wifi yake na kaka
yake, sababu ikawa kama ya dada yao. Kurudisha watoto nyumbani sababu ya shule
kesho yake. Akajikuta amebaki na wazazi wake wakiwa wamekunywa na wao, hakuna
jinsi mama yake angeweza kumsaidia msichana wa kazi. Andy akasaidia kusafisha
pale ndipo akarudi kwake, ilishakuwa saa tatu na nusu usiku. Akajichukia kupita
maelezo. Kutoa ahadi mara mbili mbili na kushindwa kutimiza! Hilo likamuumiza
mwenyewe hata kabla hajalaumiwa na mtu.
Jumatatu.
Jumatatu siku ya kazi, foleni. Hakuna jinsi angeenda
hospitalini asubuhi hiyo na kuwahi kazini kwenye kikao cha asubuhi. Akaazimia
kuanza ofisini kwanza, ndipo mchana anunue chochote aende akamuone Mina
hospitalini. Alifika kazini, akapata ujumbe kutoka kwa Ron akimuomba au
kumtaarifu kuwa atachelewa kidogo. ‘Bila shaka.’ Akamjibu
kwa haraka, akielewa kabisa kuwa nilazima anapitia kwanza hospitalini kumuona
dada yake.
Ilipofika kama kwenye saa tatu hivi, Ron akawa
anaingia kazini. Moja kwa moja akaelekea ofisini kwa Andy. “Samahani sana
nimechelewa.” “Hamna neno. Vipi hali yake lakini?” “Imebidi nimuhamishe asubuhi
hii. Bado analalamika kichwa. Tumefika asubuhi ya leo, tumemkuta analia,
anaonekana hajalala, nikaona...” Mara mlango ukagongwa mara moja. Wote
wakageukia mlangoni. Ron alikuwa amekaa mbele ya meza ya Andy.
Akaingia Lora natabasamu zuri. “Leo siku nzima
nitakuwa hapo kwenye hiyo hoteli jirani yenu. Tuna kikao hapo.” Akamsogelea
Andy na kumbusu midomoni. Alikuwa ameshikilia kimfuko, wazi kilionekana
kimebeba vitafunwa. “Nimekuletea sambusa za chai.” Akaongeza Lora. “Mimi naomba
niwaache Kiongozi.” Akasimama Ron.
“Hapana, mimi sikai, nimepita tu kumletea kitafunwa. Nyinyi endeleeni tu na
kazi.” “Hamna neno. Sisi tupo tu, tutazungumza hata baadaye. Hapakuwa na
mazungumzo ya maana.” Akaaga Ron, nakutoka.
Lora alijawa tabasamu zuri, akapendeza. Ungependa kumtizama binti huyo ambaye hakuonyesha
hata na hila usoni mwake isijue kinachoendelea moyoni kwa Andy. Na kweli
hakukaa muda mrefu. Akaacha zile sambusa, na kumwambia anarudi kwenye kikao,
walikuwa na mapumziko mafupi, wakapewa hizo sambusa, akamwambia alipozipenda
yeye, akaona amletee na yeye. Lora alifanya jambo zuri sana lakini lilimnyima raha Andy, alishindwa hata kusimama na
kumsindikiza. Miguu ilimwisha nguvu, akabaki ameduaa.
Anarudije tena kuuliza kwa kaka yake Mina
aliyeshuhudia akidakwa
midomo asubuhi hiyo na mrembo aliyeacha kikao na kuleta sambusa, habari za Mina
aliyemuahidi jana angerudi kumuona halafu asiende,
huku nyuma akazidiwa mpaka kuhamishwa hospitali! Anaulizaje tena! Anaanzia
wapi! Heri ingekuwa Hatibu, lakini ni Ron ndiye aliyeshuhudia! Andy akabaki
ameduaa pale mezani.
Akajua maji yameshavuka magoti. Yanapanda juu.
Akamuhurumia Mina, asijue chakufanya. “Heri
ningefuata ushauri wa Devi.” Akajilaumu Andy kujipeleka yeye mwenyewe
hospitalini na kutoa ahadi ambazo
hata hakuulizwa.
Akakumbuka jinsi alivyolia Mina akimwambia kichwa
kinamuuma na kushindwa kumsaidia kwa chochote, na wala hakurudi! “Heri kaka yake amemuhamisha hospitali
nyingine.” Akajifariji lakini bado moyo ulimuuma, dhamira ikazidi kumsumbua
kwa msichana mgeni kabisa kwake!
Akakumbuka vile Mina alivyomshukuru kwa dhati kwa
kumfuta tu machozi na kumshukuru kwa kwenda! Akakumbuka jinsi alivyomshika
mkono. Akavuta pumzi kwa nguvu, Andy akabaki hajui chakufanya. “Daah!” Tayari
Andy akajikuta yupo kwenye wakati mgumu, tena njia panda.
Kwa Shemeji.
Andy akanyanyua simu na kumpigia simu shemeji yake. “Kwema?” Akauliza Devi. “Kwa
mfano ile asilimia 7 ipo matatizoni, unafanyaje?” Moja kwa moja akatupa
swali bila hata salamu. “Nilikwambia Andy, BACK OFF!”
“Nilifuata ushauri wako.” Akajitetea kitoto. “Sasa
umejuaje kama yupo matatizoni?” Andy akanyamaza. “Unajiingiza pabaya Andy! Toka mapema kabla hujaingia nakushindwa kujitoa
kabisa.” “Nitajuaje sasa kama nimeshaingia
kabisa?” “Kwani unashindwa kujitoa?” Akauliza. Kimya. Hakupata jibu.
“Andy?” “Nafikiri naweza.” Akaongea kama asiye na uhakika, Devi akajua. “Andy!” “Naweza.” Akamuhakikishia. “Hapana Andy. Tunazungumza hivi ni kwa kuwa umeshajua huwezi kujitoa tena. Lakini mimi nakuhakikishia UNAWEZA Andy. Hesabu hasara na faida. Andika hata chini hapohapo ulipokaa. Ona wapi kunalemea. Kisha chukua hatua
tafadhali.” Devi akashauri. Kimya.
“Nikwambie ukweli mwingine, Andy?” Akauliza kwa tahadhari. “Nakusikiliza.”
“Nahisi ukiendelea kutafuta asilimia
nyingine zaidi, unavingi vyakupoteza kuliko faida. Niliwaona jana na Lora. Nyinyi watu kwa kuwaangalia tu,
mnaonekana mlikusudiwa kuwa pamoja. Mama hajakosea.
Hata Paulina alisema wakati tunarudi nyumbani. Nashauri
rudisha macho yako sehemu sahihi. Utapunguza migongano na misuguano
isiyo na sababu.” Kimya.
“Unanisikia Andy?” “Nipo.” Shemeji yake akacheka kwa kusikitika. “Najua upo, lakini nataka kujua kama unanisikia!”
“Nimesikia.” “Kweli Andy? Maana kile nilichokiona jana kati yenu, si chakukiachia.” “Wakati mwingine
muonekana wa nje huwa unaficha uhalisia
wa ndani.” Ule usemi ukamfanya shemeji yake atulie kabisa. Akajua
lipo zito linaloendelea kwa Andy.
“Labda niulize tena. Ni kwa asilimia ngapi,
umempenda Asilimia 7?” “Kwa
asilimia 120.” Akajibu Andy kwa haraka
bila hata kuchelewa. Shemeji yake akabaki kimya kwa muda akajua mambo
yamebadilika.
“Kwa asilimia ngapi unajisikia kumpenda
Lora?” “Naam!” Andy akauliza kwa mshituko
kidogo akajidai kama hajasikia swali. “Andy!?”
Devi akamuita kwa kumshangaa. “Umesema nini? Naomba
urudie swali.” “No. Never mind.” Devi akajua anapoteza muda tu.
Hakutaka kurudia tena swali.
Kuanzia mwanzo mpaka mwisho Andy alikuwa akisikia neno
hadi neno. Ghafla hajasikia swali la msingi hivyo! Akaona amwache tu. “Basi tutaongea baadaye.” Andy akaaga kwa haraka kama
ambaye aliyeshukuru kutoulizwa tena hilo swali. Bila kusubiri jibu, akakata
simu.
~~~~~~~~~~~~~
Kwa Asilimia 7, zimeshazidi asilimia 120, wakati Lora, kipenzi cha familia, ameshindwa kujibu na kusema wakati
mwingine muonekano hudanganya! Kipi kitaendelea kwenye hizo asilimia 120 wakati
hata hospitalini alishindwa kutokea!
Inaendelea….
0 Comments:
Post a Comment