Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 1. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 1.

Andy aligonga mlango akafunguliwa na msichana aliyemfanya abaki amedua. “Nikusaidie nini au sio wewe uliyegonga!?” Akamuuliza swali akimshangaa kwani Andy alibaki hapo nje ya mlango amekodoa macho. Akamwangalia na kutafuta kama kuna mtu mwingine nyuma yake na pembeni yake, kisha akarudisha macho kwake. Wakabaki wakitizamana kwa muda.

Ndipo akagutuka. “Nimemkuta Ron?”  Ikabidi aulize tu kwani Mina alifunga mikono kifuani na kubaki akimtizama na yeye. Alipomuulizia Ron, akamuona anacheka kisha akamwambia. “Shiiiiii!”  Akamshika mkono na kumvutia ndani huku yeye akinyata. Andy asielewe. Mina akaendelea kucheka kwa kujitahidi kupunguza sauti, halafu akawa kama aliyehamasika ghafla, huku amemshika Andy mkono akimuongoza njia mpaka karibu na sebuleni.

Kisha akamvuta ili ainame, akaelewa anataka ampe sikio. Andy akainama na kumpa sikio. “Usiongee chochote.” Akamnong’oneza sikioni akicheka taratibu. Kisha akamvuta tena kwa kumsogeza mpaka karibu na kochi. Akamuona Ron amelala huku anakoroma.

Mina akazidi kucheka huku ameshika mdomo wake. Akanyata mpaka sehemu ya kulia chakula akachukua jagi la maji, Andy akawa ameshaelewa ila akabaki akimtizama huku akitabasamu na kutaka kujua anachotaka kufanya.

Akarudi pale sebuleni alipokuwa amelala Ron kwa kunyata huku akimsihi Andy asiongee chochote kwa kuweka kidole chake kimoja juu ya midomo yake, akammwagia maji kichwani, Ron aliruka mpaka akaanguka sakafuni kutoka kochini. Andy akashangaa sana, hakutegemea!

“Hakika nitakuua Mina!” Ron aliongea akiwa chini sakafuni, ameloa. Ile kuamka tu, Mina akaanza kukimbia huku akipiga kelele. “Mama niokoe! Ron anataka kuniua mimi!” Andy akiwa ameduaa, akashangaa Ron ananyanyuka kwa kasi na kuanza kumkimbiza Mina. Alikimbia mpaka nje alipokuwa mama yake akaenda kusimama nyuma yake. “Leo lazima ulie Mina.” Ron aliongea huku akimfuata nyuma kwa hasira. “Utaniangusha bwana Mina, ni nini?” Andy akasikia sauti ya kimama ikiuliza.

“Leo mwanao lazima alie huyo. Ona alivyonilowesha nikiwa usingizini.” “Mimi nilikuwa namuamsha. Alikuwa anakoroma pale sebuleni, wakati mgeni wake amekuja, yeye hana habari! Ulitakiwa unishukuru sio kutaka kunipiga!” “Ona mama! Ona wewe mwenyewe. Mtoe hapo nyuma.” Akamsikia yule mama akicheka.

“Usicheke mama bwana! Atakuja kuniua usingizini kwa mshituko!” “Kwanza ulikuwa unanuka jasho. Hapo nimekusaidia kuoga. Unakwenda kujikausha tu na kujipaka mafuta.” Mina aliongea nyuma ya mama yake. Ron akataka kumvuta, Mina akapiga kelele kwa sauti. “Mwache bwana wee!” “Wewe unamuendekeza mama. Huyo nikimbamiza mara mbili tatu, akili yake itakaa sawa.”

Ron akataka tena kumshika. “Bwana weeee! Nenda kwa mgeni wako.” “Muongo huyo mama. Hakuna mgeni yeyote!” “Yupo, tena amekuona unavyokoroma.” Ron akarudi ndani huku akilalamika, Mina na mama yake wakicheka. “Wewe cheka tu, nikikukamata ndio utanijua.” “Utamkamata nani wewe! Unasaidiwa, badala ushukuru, unaleta ubabe! Na siku nyingine akija msichana wako namfungulia mlango akuone jinsi unavyokoromaga, uone kama hujaachwa.” Mama yake akaanza kucheka tena. “Akija kukukamata huyo!” “Kwani mimi sina miguu! Hawezi.”

Ron alirudi ndani, kweli akamkuta mgeni wake amesimama pembeni ya sebule, akaanza kucheka. “Karibu Mkuu hapo kwenye kochi kavu, nisubiri nikabadilishe. Huyu mtoto mjinga tu.” Ron akapitiliza ndani chumbani kwake.

Baada ya muda akatoka akiwa amebadilisha. “Ngoja nikutambulishe kwa mama kabla hatujatoka kwenda kwa kina Hatibu.” “Litakuwa jambo zuri.” Mara mama yake akaingia. “Mama, huyu anaitwa Andy, tupo naye kazini. Amehamishiwa kwenye tawi letu.” “Kwa hiyo mpo pamoja na Hatibu?” “Kwa kitengo chetu, ndiyo, au kwa kile tunachofanya, ila yeye ndio bosi wetu wa kitengo chetu.” “Acha hizo bwana Ron! Si umwambie tu mama kuwa tunafanya kazi pamoja!” Wakacheka, Andy akasimama na kumsalimia mama yake Ron kwa heshima tu. Wakazungumza kidogo, wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~

Walitoka pale bila yakumuaga Mina kwa kuwa hakuwepo, wakaelekea nyumbani kwa kina Hatibu kumchukua ili waende mpirani uwanja wa Taifa. Wote walijikuta wapo ofisi moja na wote watatu wakawa wapenzi wa timu inayofanana, halafu wafanyakazi wengine waliopo nao kitengo kimoja, wapinzani wao. Siku hiyo ya jumamosi timu yao walikuwa wakicheza mpira wa miguu na timu ya kutoka nchini Nigeria. Walikubaliana wakutane, kisha waongozane uwanja wa mpira.

~~~~~~~~~~~~~

Hatibu na Ron walianza kazi hapo kwenye hiyo kampuni wakati mmoja, wakajikuta mambo mengi wanaendana ndipo ukaribu ukaongezeka, wakaishia kuwa marafiki. Aliyekuwa kiongozi wao wa hicho kitengo alipata kazi kwenye kampuni nyingine kwa mshahara mkubwa zaidi, akaacha hapo kazi na kuacha nafasi hiyo wazi. Walifanya kazi kwa majuma kadhaa bila kiongozi, ndipo wakaletewa Andy kama kiongozi wao wa hicho kitengo.

Watatu hao hawakupishana sana kiumri, lakini  kwa muonekano tu, Andy alionekana analipwa vizuri zaidi yao. Au ana hali ya maisha nzuri zaidi yao. Alikuwa na gari nzuri sana. Na alikuwa akionekana nadhifu wakati wote. Hawakumsikia akilia shida kama wao kukopana pesa mara kwa mara pale ofisini.

~~~~~~~~~~~~~

Wakiwa ndani ya gari ya Andy  mazungumzo ya hapa na pale  yakaendelea mpaka walipofika uwanja wa Taifa, Andy akiwa ametulia sana. Mpira ukaendelea, wakishangilia na kukatishwa tamaa wakati timu yao ilipoanza kufungwa, Andy alikuwepo kama hayupo. Hatibu na Ron wakawa busy kushangilia wala wasijue kinachoendelea kwa Andy, kwanza hakuna aliyemjali mwenzake pale uwanjani. Kelele mpaka mpira ukaisha. Wote wakakutana hawanywi pombe. Wakaamua kurudi tu nyumbani. Walimshusha Hatibu kwanza na  ndipo  safari ya kurudi  Tegeta Mwisho kwa kina Ron ikaanza.

Foleni za barabarani na kuanzia muda waliotoka uwanjani na fujo, giza liliwakuta njiani.  Andy akatafuta jinsi ya kuuliza tokea walipokuwa peke yao, walipomshusha Hatibu, akashindwa, ndipo wazo likamjia. “Sikumkuta mzee nyumbani!” Akaanza Andy. “Tunaishi na mama tu. Mzee alikuja kuoa mwanamke mwingine.” “Kwa hiyo  mlizaliwa wawili tu?” Akatumia akili kwa haraka ili kumsogeza Mina kwenye mazungumzo. “Kwa mama, ndiyo. Ni mimi na Mina tu. Lakini huko mzee alipo anayo familia nyingine.” “Pole sana.” “Naona tumeshazoea hayo maisha. Hamna hata anaye lalamika tena.”  Akatafuta tena kuuliza, lakini ikabidi azunguke.

“Kwa hiyo ni mama ndiye aliyekuwa akiwasomesha?” “Kwa sehemu kubwa ni mama. Hata wakati mzee alipokuwepo, mama alikuwa akihangaika mwenyewe. Ndio maana hata nafikiri hatukuona tofauti kubwa sana mzee alipoondoka. Hata pale ni mama ndiye aliyejenga kwa mshahara wake huohuo wa ualimu. Alikuwa akijenga huku tunasoma.” “Na Mina naye alisomea Dodoma?” Akamsikia Ron akiguna.

“Vipi?” “Aaah! Mina na shule! Hataki  kabisa kusoma. Ameishia kidato cha nne, basi.” “Labda kuna kitu anapenda kufanya badala ya  shule.”  Kupika.  Hicho ndio kitu anapenda kufanya kuanzia asubuhi mpaka jioni na uchokozi. Basi.” Wakacheka.

“Amegoma kukua, na wala hana analowaza la msingi.  Vile unavyomuona ndio kamaliza. Hajui kukasirika na hata ukimkasirikia...” Ron akafikiria. “Kwanza huwezi kumkasirikia Mina kwa muda mrefu.  Sijui ameumbwaje yule mtoto!” Wakacheka.

Andy akatamani kuendelea kusikia habari za Mina, lakini akajikuta ameishiwa maswali ya mitego ili kumfahamu zaidi Mina. Walifika nyumbani kwa kina Ron, ni kweli ilikuwa Tegeta Mwisho haswa. Walipokuwa wakiishi ilikuwa mbali na barabarani. Na barabara ya kufika kwao ilikuwa ya udongo tena mbaya. Kama walionunua hicho kiwanja kwa bei ya chini haswa. Lakini nyumba ilionekana ilijengwa na kukamilika kwa bati safi tu.

Safari hii Andy hakuwa na sababu ya kushuka garini. Ron aliteremka kwenye gari na kumshukuru kwa lifti na kuwa pamoja siku hiyo ya jumamosi. Hata hakumkaribisha ndani, akafunga mlango kwa ahadi ya kuonana siku ya jumatatu kazini.

Huku Kwa Andy

Andy alirudi nyumbani kwake, akajiweka kochini, akajikuta anacheka. Akamkumbuka Mina na utundu wake, akacheka tena. Akachukua rimoti ya tv na kuwasha ili aangalie kinachoendelea ulimwenguni. Akajirudisha nyuma ya kochi.

Lakini akahisi sauti ya Mina masikioni kwake kama anayemnong’oneza kitu kama vile alivyofanya nyumbani kwao. Andy akajishika sikio. “Nachanganyikiwa nini!” Akajicheka na kuamua kubadili alichokuwa amekiweka kwenye luninga akiwa hata hajui ni nini kilikuwepo, akabadilisha kulia na kushoto, akakumbuka anatakiwa kanisani siku inayofuata asubuhi. Akaona akajipumzishe mapema, asiendelee kupoteza muda pale kochini.

Kwa Kina Ruhinda!

Siku za jumapili familia hiyo ya kina Andy huwa wanakutana nyumbani kwa wazazi wao Msasani, kwa chakula cha mchana wakiwa na familia zao. Dada yake Andy, Paulina, yaani mtoto wa pili kuzaliwa kwao, alikuwa ameolewa na wana watoto wawili. Wakike. Kaka yake mkubwa, Pius, naye alikuwa ameoa na watoto wawili, wakike. Mdogo wake wa kiume anayemfuata Andy, yaani waane kuzaliwa, ambaye ndio kitinda mimba, alikuwa daktari katika hospitali ya taifa Muhimbili. Yeye hakuwa ameoa.

Ilikuwa familia ya kisomi. Walio staarabika sana. Kila mtoto kwenye hiyo familia alisoma vizuri kama wazazi wao. Mzee Ruhinda alikuwa Mkurugenzi kwenye taasisi ya fedha. Mama Ruhinda alishastaafu, lakini alifanya kazi akiwa kiongozi wa ngazi ya juu tu katika bodi ya mambo ya ukaguzi/Auditing kisha akajiingiza kwenye NGO ambayo bado alikuwa kwenye ngazi ya juu tu akitumika huko.

Walikuwa na ndoa iliyoheshimika kwenye jamii. Wakalea watoto wao vizuri bila shida. Ni Andy na mdogo wake anayemfuata, Paul ndio hawakuwa wao wameanzisha familia.

Walikuwa ni wakristo wale wakwenda kanisani kila siku ya jumapili ya bila kukosa. Wakatoliki damu. Andy alihudumia kanisani, altareni tokea mdogo kabisa akiwa na mapadri akitumika katika kila misa, mpaka wakahisi atakuja kuwa padri. Alisoma vizuri katika shule za mapadri nchini Kenya, Nairobi, kuanzia darasa la tano mpaka sekondari. Ila chuo kikuu kwa shahada zote mbili alimalizia Kampala nchini Uganda, ndipo akarudi nchini Tanzania na kupata ajira bila shida. Akiwa ni mtoto ambaye hajakulia nyumbani kabisa. 

Kwa kuwa walikuwa wakimlipa vizuri na hakuwa na majukumu yeyote yale, alianza kuishi kwenye apartment za mtaa wa Zanaki. Katikati ya jiji, zikiwa zimekamilika kila kitu ndani, pakamfaa haswa. Kwani hakutaka hata kununua kitanda kwani bado alikuwa akijishauri kama anabaki nchini Tanzania, au arudi alikokulia, nchini Kenya ambako ndio kama nyumbani.

Maisha yakaendelea hapo akitumia vitu vya mle ndani ila akanunua gari nzuri sana ya garama ili imsaidie usafiri wakumzungusha jijini. Maisha nchini Tanzania yakaanza bila uhakika sana wakuwepo hapo nchini kwa muda mrefu, akisoma upepo, kama ambaye bado hakuwa na sababu ya kumbakiza sana nchini japo alikuwa na hiyo kazi nzuri ambayo alijua angeweza kuipata hata huko nchini Kenya, na familia yake ambayo bado alijiona kama mtu wa nje tu. Maana ndugu zake wote walisomea nchini wakiishi nyumbani kwao. Akawa kama aliye mguu mmoja ndani mwingine nje.

Maisha yakawa ni kazini na siku za jumapili kanisani kisha kuwepo nyumbani kwao Msasani akijaribu kujiunga na hiyo familia aliyokuwa akiiona wakati wa likizo tu. Sasa akawa amerudi akijaribu kuwa mmoja wao.

Shemeji yake, mume wa Paulina, alimwambia kuna viwanja vinauzwa Kigamboni, kujenga sio swala baya. Akaona hana chakupoteza. Pesa ipo. Ndipo akamsadia mchakato mzima wa kukimiliki hicho kiwanja, akaanza kujenga taratibu bila haraka wala shida kwani mshahara aliokuwa akilipwa, aliweza kulipia apartment hiyo nzuri na ya kisasa alipokuwa akiishi, kuendesha gari ya kifahari na kujenga bila kuhisi kupungukiwa. Pesa yake ni yake. Hana wakushiriki naye kipato chake. Kila anayemzunguka ana maisha mazuri na wanaingiza pesa nzuri tu.

Maisha yake yakaendelea yakiwa hayana makuu. Hanywi pombe, haongi mwanamke, hana familia inayomtegemea isipokuwa akijisikia kwa vitu vidogo vidogo kama zawadi kwa wazazi, watoto wa kaka yake na dada yake na hao ndugu, basi.

~~~~~~~~~~~~~

Wote walikuwa wakienda kusali kanisa moja. Familia nzima. Mpaka familia ya kaka yake na dada yake, walikuwa wakikutana kwenye misa ya kwanza kabisa ya kingereza ndipo wanarudi nyumbani kwa wazazi wao, wote, kama hakuna mwenye udhuru. Watapika na kula pamoja ndipo anayetaka kubaki au kuondoka, ruksa. Lakini ilifanyika kama desturi yao kuwa kila mlo wa mchana siku ya jumapili ni lazima wawe pamoja.

Jumapili Baada Ya Kumuona Mina.

Kutoka anapoishi Andy mpaka kanisa la St. Peter hapakuwa mbali sana haswa siku za jumapili mida hiyo ya asubuhi ambapo hakuna foleni. Dada yao wa pekee Paulina na familia yake waliishi Kinondoni, na familia ya kaka yao mkubwa aliyewahi kushika wadhifa ya msaidizi wa Gavana wa pesa, aliishi Mikocheni karibu na Kawe. Walikuwa na nyumba kubwa sana na ya kifahari. Akiwa kwenye wadhifa huo, alinunua nyumba mbili maeneo ya karibu kabisa na bahari, akabomoa na kujenga kwa muundo mzuri sana. Ukiingia hapo ndani ya uzio utajua Pius anayo pesa.

Kama kawaida ya familia hiyo ya kisomi, wote walijikuta wamefika kanisani dakika 15 kabla ya misa kuanza. Wakasalimiana wote wakiwa nje ya kanisa hilo. Zaidi watoto wao ambao walikuwa wanne, wote wakike. Wamekuzwa kwa malezi ya kigeni na kisomi.

Shule ni kila kitu kwao, na watoto wakaelewa hilo. Lugha ni moja tu, kingereza kwa familia nzima kwa muda mwingi wanapokuwa peke yao. Wakubwa kwa wadogo. Wakasifiana kupendeza kwa hili na lile, huku wakubwa wakipeana kwa ufupi habari za majukumu yao na maendeleo ya nchi huku wakisubiria muda wakuingia kanisani ufike.

Baada ya Misa kuisha, marafiki wa karibu sana wa familia hiyo ambayo waliendana kidini, maadili, uchumi pia, Machaki, ikawasogelea wakiwa na binti yao ambaye hakupishana sana na Paul kijana wa mwisho wa familia hiyo ya Ruhinda. Aliitwa Lora. Binti mzuri, nadhifu, msomi aliyekuzwa kwenye maadili kabisa yanayofanana na kina Paulina, kasoro yeye alisomea shahada yake ya pili nchini Uingereza. Vicheko vikaendelea mwishoe wakaagana.

Kaka yao mkubwa kina Andy, yaani Pius alishamshawishi Andy kumchangamkia Lora. Na hilo likawa jambo lililopo kwa wazazi pia. Zaidi mama Ruhinda, alimpenda sana Lora. Lakini kwa Andy aliweka uzito fulani hivi, ndugu wakawa hamuelewi, isipokuwa Paul mdogo wake. Yeye aliweza kuhisi ni kwa nini Andy anakuwa mzito kwa Lora.

Kama kawaida, walipofika nyumbani wanawake wote waliingia jikoni wakisaidiana na msichana wa kazi kuandaa chakula cha mchana. Misa ilikuwa ikiisha mapema tu. Kwa hiyo walikuwa na muda wa kutosha wakuongea wakati wakisubiria chakula. Jikoni alikuwepo mama yao, Mama Ruhinda, wifi yao, mke wa Pius, Raza, naye ni mama Ruhinda mdogo, Paulina na msichana wa kazi.

Sebuleni alikuwa Mzee Ruhinda, vijana wake hao watatu na mkwewe, mume wa Paulina. Watoto walikuwa sebule ndogo, maalumu kwa ajili ya wajukuu hao. Ilikuwa na kabati ndogo ya vitabu pembeni. Tv kubwa tu, na games pembeni. Meza nzuri tu ambazo huchezea na kuandika kama wangetaka. Kwa hiyo kila mtu alijua wapi pakukaa na nini chakufanya wanapofika kwenye nyumba hiyo.

Wapo wajukuu waliopenda kucheza games kila wakifika hapo. Wapo waliokimbilia kusoma vitabu vya hadithi ambavyo mama Ruhinda alijitahidi kuwabadilishia wajukuu zake mara kwa mara ili wakifika hapo, wanaopenda kusoma, wasichoke kusoma vitabu. Yupo aliyependa kuchora. Basi siku hiyo inakuwa siku ya furaha na mapumziko kwa wote. Na wajukuu hao walipenda siku hiyo ya kukutana hapo nyumbani kwa bibi na babu yao.

~~~~~~~~~~~~~

“Wewe vipi? Mbona kila saa unashika sikio?” Shemeji yake akamuuliza Andy. “Na mimi nimemuona tokea kanisani! Au lina infection nini?” Pius akaongeza, Andy akajishitukia. “Nipo sawa tu.” Akajibu na kujitahidi kutoshika. Wakamuona ametulia sana siku hiyo na tabasamu usoni wakati wote.

“Umemuona Lora leo? Amependeza kweli!” “Umeanza mama. Nimeshakwambia sina shida ya kuona.” Mama yake akakaa huku akicheka.

“Mbona swali dogo tu, lakini maelezo mengiii! Mama ameuliza kama umemuona Lora, basi?” “Na mimi nilikuwepo kanisani mkubwa! Wote tumemuona.” Andy akamjibu kaka yake, wote wakacheka. “Ndio uchangamke Andy! Vijana wa mjini watamuwahi!” Pius akaweka msisitizo.

“Kwanza ni binti anayeheshimika sana kwenye kampuni yao! Sifa zake zipo hata kwenye bodi ya wakurugenzi.” Akaongeza Mzee Ruhinda. “Hata kwenye jamii. Ni binti mzuri kwa kweli. Ametulia. Msomi. Halafu hatakuwa mzigo kwako. Inamaana mnasaidiana kwenye maisha. Halafu..” “Bila kukosea hizo sifa zitakuwa ni za Lora tu!”  Akaingia Paulina hapo sebuleni na glasi ya juisi.

“Ulijuaje!?”  Wote wakacheka. “Namjua mama kwa Lora. Huwa sifa zake haziishi. Akianza hapo, mpaka tunaondoka humu ndani. Mimi naona tuyamalize. Huyo Andy kama ni muoaji, basi ataoa. Kama si muoaji, utamnadi huyo Lora mpaka utachoka.” Dada mtu akaongeza. “Na mimi naona tubadili tu mazungumzo.” “Ulitaka tuzungumzie nini na wewe! Utaishia kuoa watu wa ajabu ajabu!” “Hakuna mtu wa ajabu mama. Kila kitu ni taratibu.” “Mpaka lini?” Mama yake akamuuliza Andy. “Njaa inauma mama yangu!” Andy akabadili mazungumzo, wote wakacheka. Mama yao akaguna.

“Maana Lora...” Akataka kuanza tena mama yao, wote wakaanza kucheka. “Mama Ruhinda! Jambo haliishi?” Paulina akauliza huku akicheka. “Wewe mwenyewe unampenda Lora!” Mama Ruhinda akamwambia Paulina. “Nampenda haswa. Natamani hata aolewe leo na huyo Andy. Maana ni binti mzuri, ametulia. Amesoma..” Andy akasimama. “Ngoja mimi nikacheze game na watoto. Naona hapa kwenye vikao vya harusi, sitapaweza.” Andy akaondoka hapo wote wakicheka.

Walikula huku wakitaniana kwa hili na lile. Mwishoe akaaga kaka mkubwa na familia yake, wakaondoka. Andy yeye hakuwa na haraka yakuondoka hapo kwao. Mara nyingi alikuwa anakuwa wa mwisho kutoka hapo. Akajikuta amebaki yeye na shemeji yake, Devi, kwenye baraza la nyuma ambapo na kwenyewe kulikuwa na sehemu nzuri tu ya kukaa. Mama Ruhinda aliweka viti vizuri ndani ya baraza hilo kubwa na kulizungushwa maua mazuri sana aliyokuwa akiweka mbolea ya maganda ya kila kitu anachotumia jikoni kwake. Basi maua hayo ya kwenye vyungu ambayo yalikuwa ndani na nje ya baraza hilo yalikuwa yakistawi sana. Huwezi kukosa maua nyumba hiyo.

Asilimia 7.

“Wewe leo una nini? Tabasamu halikuishi!”  Akacheka Andy kisha akamwangalia shemeji yake kama anayetaka kumuuliza jambo kisha akasita. “Ni nini?” Akacheka tena mwishoe akaamua amuulize tu. “Eti wewe unaamini kwenye ‘Love at first sight’? Yaani unamuona tu mtu kwa mara ya kwanza. Humjui hata jina lake, unajikuta unampenda kiasi chakumfikiria wakati wote! Unaamini hiyo inawezekana?” Shemeji yake akacheka kidogo huku akifikiria.

“Humfahamu kabisa?” Devi akamtega kutaka kujua kama ni yeye mwenyewe Andy ndio amependa au la! Andy akamgundua. “Acha hizo bwana! Wewe nijibu kama kuna kitu kama hicho?” “Sawa. Basi niulize hivi, inamaana huyo ‘aliyependwa’ hafahamiki kabisa?” Andy akacheka taratibu kama anavuta hisia, Devi alimuona maana aliweza kuzisoma hisia nzito usoni kwa Andy mpaka akashangaa.

Come on Andy! You are in Love Man!” “Shhhhh! Usitake mama Ruhinda atoke. Wewe nijibu. Kitu kama hicho kinawezekana?” “Hafahamiki kabisaaa!” “Labda niseme kwa asilimia 7 tu. Vile vitu vya msingi.” “Navyo vipoje? Vinaendana?” Andy akanyamaza kama anayefikiria.

“Kwa sababu Andy, zipo hisia na uhalisia wa maisha. Je katika hizo asilimia 7, ngapi zinaendana?”  Andy kimya. Hata katika zile 7, alizomfahamu Mina, hawakuendana hata kidogo. Akasita. “Lakini sijawahi kujisikia hivyo kwa mwanamke mwingine yeyote, Devi! Nakwambia ukweli ile ni ya kipekee.” Akajitetea Andy akisikika ameshindwa kujibu swali.

“Asilimia ngapi, Andy?” Shemeji yake akasisitiza swali lake. “Sijui.” “Come on Andy. You are smarter than that.” Akaongea akimjua fika shemeji yake, si mjinga. “Sidhani kama inajalisha.” “Niamini mimi kuwa huwa inakuja kujalisha baadaye. Sana tu. Sasa kabla hujavuka zaidi ya hizo asilimia 7 unazomfahamu, nashauri weka kikomo. Back off.” Shemeji yake akaweka msisitizo. Kimya.

“Unanielewa Andy? Mahusiano ambayo unafikiri yatakupelekea ndoa, ni zaidi ya hisia. Ndoa ina uhalisia wake ambao haupelekwi na hisia peke yake. Ndoa sio kufanya mapenzi tu. Baada ya hapo kuna kula, kulea watoto. Ikiwepo wavae vizuri, wasome shule nzuri na waishi kwenye mazingira mazuri, ambayo inahitajika pesa nzuri. Sio hisia peke yake. Hisia hailipi ada ya shule wala hainunui chakula. Sijui kama unanielewa?” “Nahisi nimeelewa. Na asante kwa ushauri. Nafikiri upo sahihi.” Andy akaafikiana na shemeji yake.

~~~~~~~~~~~~~

Alitoka pale angalau ule muhemko juu ya Mina ukachukua sura nyingine. Maneno ya shemeji yake yakaanza kumwingia. Mina hajasoma. Ameishia kidato cha 4 tu. Na kaka yake ameshamwambia Mina hataki kusoma. “Haonekaniki kama ni mtu mwenye uchu wa maendeleo. Angetafuta hata biashara akafanya!” Akawaza Andy akijitia moyo katika ushauri wa shemejie.

Hata hivyo katika familia ile ya kila mtu anayeimba usomi na maendeleo, Mina anaingiaje pale! Andy akaona ajitulize. Hata hivyo hadhi ya maisha yao ni ya chini mno, atamtambulisha vipi kwa wazazi! Akaona kweli asiongeze asilimia nyingine. Zibakie zilezile 7 alizomfahamu na aachane naye. Akajituliza.

Jumatatu!

Andy alifika kazini akaanza kazi kama kawaida. Waliingia kwenye kikao cha asubuhi ambapo kiongozi wao wote alikuwepo. Akatoa muongozo wa juma zima, Andy na watu waliokuwa chini yake wao wakarudi idarani kwao. Akagawa majukumu, kila mtu akaanza kazi. Alimtizama Ron kama amuulize kitu, lakini akasita na kujionya. Akakumbuka ushauri wa shemeji yake.

Akaondoka kabisa pale karibu na Ron na kuelekea kweye ofisi yake iliyokuwepo pembeni ya chumba hicho kikubwa tu ambacho wapo kina Ron, Hatibu na wafanyakazi wengine wanne ambao walipanga meza zao kuzunguka hicho chumba.

Lora Avunja Ukimya.

Ujumbe ukaingia. ‘Karibu kwa chakula cha mchana.’ Andy akasoma na kubaki akijishauri. ‘Ni lunch tu, acha woga Andy!’ Ujumbe mwingine ukaingia baada ya dakika 10. Andy akacheka. ‘Nilikuwa na kazi kidogo ndio mana nimechelewa kujibu. Samahani. Wapi na saa ngapi?’ Andy akarudisha ujumbe na kubaki akijishauri baada ya Lora kujibu. Hakika alisikia uzito, lakini akaona ni kweli Lora ni binti ambaye anafaa, ajaribu tu. Ulipofika muda wa chakula cha mchana, Andy akawaaga kuwa anatoka kwa chakula cha mchana. “Leo kiongozi unakwenda kula kwa wakuu nini?”  Akatania Hatibu. Andy akacheka tu na kuondoka.

Alikuta Lora alishafika. “Nimechelewa nini?” Akauliza Andy wakati akikaa. “Hapana, ila mimi sikutaka uje ndio unisubirie.” Wakacheka. “Vipi kazi lakini?” “Kama kawaida tu. Siwezi kulalamika. Vipi na wewe?” “Na mimi hivyo hivyo, siwezi kulalamika.” Akajibu Andy.

Muhudumu akaleta menu ya chakula na vinywaji. Wakaagiza. “Kwa hiyo umeridhika na ulipo?” Akauliza Lora na tabasamu usoni. Andy akacheka kidogo. “Niseme kwa sasa, ndiyo.” Lora akacheka. Jinsi alivyocheka Andy hakuelewa. Akakunja uso kidogo. “Kwa nini umecheka?” “Aah! Nimefurahi tu.” “Nini kimekufurahisha?” Andy akataka kujua zaidi maana kwa jinsi alivyolisoma lile cheko ni zaidi ya kuonyesha furaha. Maana Lora alicheka baada yakumjibu.

“Nimefurahi ulivyosema umeridhika. Ndio mtu wa kwanza kumsikia anasema ameridhika na alichonacho.” Akaanza Lora. Andy kimya akitaka kusikia mwisho wake.

“Haswa kwa msomi kama wewe. Sijui kama unanielewa? Mwingine angesema anatamani kazi ya bosi wake. Au anataka kuhama kampuni ili kutafuta nafasi ya juu zaidi.” Lora aliongea na tabasamu lakini ikamkera kidogo Andy. “Umejaliwa roho ya kuridhika. Ni kitu kizuri.” Akamalizia kwa kurekebisha kama kujirudi baada ya kumuona Andy hachangii ila kumsikiliza tu.

“Vipi mama Ruhinda lakini?” Akabadilisha mazungumzo. “Yupo.” Akajibu Andy na tabasamu. “Alinikaribisha siku ya jumapili, lakini bado hapajakuwa na utulivu. Nimemuahidi nitakuja.” “Karibu sana.” Akamalizia Andy. Chakula kikaletwa. “Unaonekana ni mpenzi wa samaki!”  Akachangia Lora na tabasamu kama kurekebisha ile hali ya uzito pale. “Sana! Kukiwa na uchaguzi, lazima samaki atashinda tu.” Akajibu Andy huku akitengeneza kitambaa kilichowekwa hapo mezani maalumu cha kujifutia au kujifunika usijichafue wakati wakula. Akakitoa pale kilipokuwa kimepambwa pembeni na kukitandika mapajani. Wakaanza kula kimya kimya. Visu na uma tu ndio vilisikika.

“Vipi lakini na wewe kazini? Umeridhika? Maana nimesahau kukuuliza na wewe.” Ikabidi Andy awe muungwana. Lora akacheka. Ni kweli alikuwa binti anayeoonekana anajielewa au anaelewa ni nini anazungumza. “Kwa kweli siwezi kulalamika. Nimeanza kwenye nafasi nzuri, na mshahara mzuri. Nikijilinganisha na wengi ambao nilisoma nao  darasa moja na nikawaacha hapa nchini wakiwa wameshaanza kazi hapa nchini kwenye makampuni mengine, kulalamika ni kukufuru.” Lora aliongea kiustarabu tu ila kwa kujigamba kidogo.

“Kwa maneno mengine umefikia ngazi ya juu kabisa!” Lora akacheka kidogo akitafuta jinsi ya kuzungumza kama asiharibu, kisha akasema. “Sio kwa kiburi, lakini ndiyo.” Wakacheka kidogo huku Andy akimwangalia.

“Si unajua kabla ya kwenda chuo kusoma shahada ya pili UK, nilifanya kazi inayofanana na hiyo?” Andy akabaki ametulia kidogo. “Kwa hiyo niliondoka pia nikiwa kwenye nafasi nzuri, nilichofanya ni kuongeza ujuzi tu. Halafu nikapata muda wa Internship, mafunzo, huko huko nchini Uingereza kama mwaka hivi. Ikanisaidia kuongeza ujuzi zaidi. Niliporudi hapa nchini, nikamkuta na mkurugenzi wetu naye anastaafu. Nikaomba mimi ile nafasi, na kwa kuwa nilishafanya naye kazi. Na tukawa tukielewana, halafu nimesoma, kwa hiyo alinipopeleka jina langu kwenye bodi ya wakurugenzi ambao ndio kina mzee Ruhinda.” Lora alicheka kidogo.

“Basi, nikafanyiwa usahili, na Mungu akawa upande wangu. Nikapata ile nafasi. Inanichukulia muda, lakini nafurahia sana.” “Hapo ni kweli umefika ngazi ya mwisho kabisa. Huna pakupanda tena.” Wakacheka kidogo na kuendelea kula.

~~~~~~~~~~~~~

Akamuona Andy anaangalia saa yake ya mkononi. “Vipi, muda umeisha nini?” “Umejuaje?” Andy akacheka kidogo huku akiuliza na kutizama saa yake ya mkononi tena. “Naona macho mkononi!” “Yeah! Ndio tumeanza juma, kuna mambo yakuweka sawa kabla halijaharibika jambo. Lakini nashukuru sana kwa chakula. Nimefurahia samaki.” Lora akacheka kiuungwana.

“Nimefurahi umekuja Andy. Naamini tutapata tena muda kama huu.” “Naamini hivyo.” Akajibu Andy na tabasamu huku akimwita muhudumu. “Mimi ndio nimekuita Andy. Naomba nilipe.” Andy akacheka. “Naomba kwa leo mimi ndio nilipie, wewe utalipa wakati mwingine.” Akaomba Andy kiuugwana.

“Sikio linawasha?” “Kwa nini?”  Akajishitukia Andy na kushusha mkono akiwa anamsubiria muhudumu aliyemwita afike hapo. “Naona unalishika kila wakati! Isijekuwa ni infection!” “Hapana. Lipo tu sawa.” Hata Andy hakujua kama anashika sikio kila wakati. Muhudumu akaleta bili, Andy akasoma. Akafungua walet yake, akatoa pesa na kumkabidhi. Akamshukuru muhudumu kwa huduma na kumgeukia Lora. “Asante.” “Karibu na kazi njema.” Andy akatoa tabasamu na kusimama. “Na wewe uwe na wakati mzuri.” “Asante.” Andy akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~

Aliingia kwenye gari yake akavuta pumzi kwa nguvu na kubaki kama ameduaa. Kama asiyejua chakufanya tena. Alikaa pale mpaka akashituliwa na Lora akiwa anagonga kioo cha dirisha lake la gari.

Akashusha. “Vipi, gari ina matatizo?” “Hapana. Vipi?” Wote waliwekeana tabasamu. “Nimeuliza tu. Maana nimekukuta umekaa tu ndani ya gari, nikajua umeshindwa kuondoka wakati uliaga ukiwa unawahi kazini!” Andy akajua amekamatwa. Akaona haitaji kujieleza kwa Lora. “Uwe na wakati mzuri Lora.” Akajibu hivyo Andy na tabasamu la kutotaka kuulizwa zaidi. Lora akarudi nyuma, Andy akaondoa gari.

~~~~~~~~~~~~~

Andy aliingia ofisini kwake na kutulia mezani. Akashangaa ni nini kibaya kilitokea kati yake na Lora! Lora hakuwa mgeni kwake. Alimfahamu kwa muda mrefu tu, lakini siku ile ikawa ngumu kweli kati yao. Labda kwa kuwa safari hii kulikuwa na agenda nyuma yake! Akajishangaa. Lora alikuwa msichana sahihi kwa mazingira yake na wazazi wake. Hakuhitaji marekebisho yeyote ili kuwa katika ulimwengu wake. Lakini!

“Ananiona mimi sina malengo ya mbeleni!”  Akawaza Andy. “Au ananiona mimi ni kama mtu ninayeridhika kirahisi tu!” Akaendelea kutafakari mazungumzo yao yaliyoendelea kwenye chakula cha mchana. “Au pengine hapakuwa na jambo baya! Mimi ndio nimeelewa vibaya1” Akajaribu kujituliza. “Labda tutoke tena.” Akajishauri Andy.

~~~~~~~~~~~~~

Ndio Kwanzaaa, tunaanza. Love at First sight! Ni kweli ipo?

Andy atafuata ushauri wa Shemeji au atafuata moyo?

Ni Mina asiyeendana na Familia, au Lora anayeendana na familia?

Inaendelea…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment