Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 43. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 43.

Haikuchukua muda Ezra akawa ameshafika. Akampigia.
“Nipo hapa nje getini, nishafika.” “Nakuja sasahivi.” Akaweka chupa ya uji kwenye kikapu na bakuli pamoja na kijiko. Akatoka. “Kumbe unayaweza!” Mode akamchokoza. “Unafikiri wangekuwa wanarudi burebure!” Akajibu akielekea nje. Hawana mbavu.

    “Jelini, umevaa kitu ndani wewe mtoto?” “Nimevaa mama jamani! Siendi kumtega! Mwenyewe namgeuza geuza samaki wangu mpaka jumamosi. Nikimuanzia leo, hataondoka hapa.” Mode alicheka, hana mbavu. “Dozi yake?” Akaendelea kumchokoza. “Ileile kama ya makurubembe ya mjini! Hapunguziwi mtu kitu.” Na yeye akaendelea kujibu akitoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~

    Akatoka nje ya geti, akamkuta anamsubiria nje ya gari. Akamdaka na kumkumbatia kwa nguvu zote. “Pole Ezra, na samahani mpenzi.” Akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu akiwa bado amemkumbatia.

    “Niambie kama umenisamehe.”  Akajivuta pembeni kidogo na kapu lake dogo mkononi, akibembeleza kama siye yeye! Ulimi laini, wa kuyeyusha hasira. “Yameisha Jelini. Yameisha mpenzi. Niahidi kama tutabaki salama.” “Tutakuwa salama Ezra. Tena mimi na wewe tu. Njoo ndani ya gari unywe uji, upunguze njaa.” Kama kawaida, wakakaa kwenye uwanja wao wanapofanya mengi. Kiti cha nyuma.

    Akashusha cup holder/kitu cha kuegemea au kuwekea chupa au vikombe au glass, cha katikati ya kiti cha nyuma, akamminia uji na kuanza kumpoozeshea kama mtoto, Ezra akimwangalia asiamini kama huo usiku unaishia hivyo, maana alijua ndio basi tena.

    “Huu utafaa.” Akabaki amejiegemeza. “Ezra? Unasinzia?” “Hapana. Nahisi nimechoka tu. Sijapumzika, sijala, sijanywa, nilikuwa na hofu! Sijawahi ogopa hivi Jelini! Sijawahi. Halafu nikawa sijui jinsi ya kutengeneza.” Jelini akamuhurumia na kuzudi kuhukumiwa.

    “Pole Ezra. Na samahani sana. Nikikuahidi sitarudia tena nilichofanya itasaidia?” “Naweza kukosea tena Jelini!” “Sasahivi najua unanihitaji na unanipenda Ezra. Mwanzoni uliponiambia sijachelewa, ukweli ulinitisha. Nikajua hunihitaji mimi kama Jelini. Lakini sasahivi nina uhakika wa mapenzi yako ya dhati kwangu. Mengine najua ni mapungufu ambayo tutajifunza kuishi nayo kwa kadiri itakavyokuwa ikitokea.”

    “Nakuahidi chochote kitakachotokea kuanzia sasa nitajua ni hasira tu lakini si kwamba hunitaki. Nitajifunza kuishi na wewe, sitaondoka tena. Tafadhali naomba yaishe. Nakuahidi haitatokea tena.” Akajibembelezesha kwa mengi akimtuliza. Na hivi Ezra mwenyewe alishakuwa akitaka yaishe na kujiapia ataishi naye hivyohivyo akijua anayependwa ni Colins, hakutaka mengi.

    “Yameisha Jelini. Na nimefurahi bado mipango yetu itaendelea. Au unasemaje?” “Na mimi nataka iendelee. Najua unaweza ukachoka au ukazoea, lakini mwenzio nakupenda na nakutaka wewe Ezra. Ninakusubiria wewe.” Akataka kumkiss.

    “Utaungua na uji. Kula kwanza. Mimi mwenyewe nina hamu na wewe.” “Naomba uweke hapo mbele angalau nikushike kidogo. Pengine nitatulia. Nilikuwa na hali mbaya! Kidogo tu.” Uji ukahamishwa kiti cha mbele. Akarudisha ule mkono wa katikati ya kiti cha nyuma, akajisogeza mpaka kifuani, akajiweka kama wanavyopendaga wengi walio bahatika kumkumbatia kimwana huyo.

    Zile pumzi nzuri shingoni kwa Ezra, na harufu murua, akainama kupata kiss. Jelini akamdaka midomo, mikono laini na kucha vikaanza kubarizi shingoni, masikioni mpaka kwenye nywele. Ezra alipewa romance hiyo, mpaka akalemewa akitamani amalize kila kitu.

    “Natamani jumamosi ndio ingekuwa leo.” “Unakumbuka mafundisho ya mchungaji?” Ezra akacheka na kumuachia. “Naona bora basi ninywe tu uji.” Jelini akampa bakuli la uji wakicheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~

    Maana waliambiwa kadiri siku zinapokaribia za kufunga ndoa, ndio hatari inapoongezeka. Kujimilikisha siku chache kabla ya ndoa na tamaa kuzidi. Aliawaambia kama hawatakuwa makini wanaweza kujikuta wanakula ng’ombe mzima na kubakisha mkia.

~~~~~~~~~~~~~~~~

    Wakati anakunywa uji akamuona Jelini anatoa simu kama anayetaka kuitumia. “Nakuhitaji tuwe wote hapa garini Jelini! Nani tena huyo!?” “Junior. Nilikuta jumbe zake, sijasoma wala sijamjibu, nikakupigia wewe kwanza. Acha nizungumze naye kwa ufupi tu wakati unakula. Nimtulize. Anawasiwasi sana.” Hapo akakubali akijua na yeye atapata majibu mengi ya wasiwasi wake maana alimjua Junior, kuna upande yeye alimuwezea Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akampigia hapohapo akapokea. “Jelini?” “Samahani Junior. Nilirudi nyumbani, nikalala kabisa. Jema ndiye aliyeniamsha. Isingekuwa yeye, pengine mpaka sasahivi ningekuwa nimelala.” “Hamna shida. Nilitaka kukujualia hali.” “Nashukuru kujali Junior. Ila…” Akasita na kumwangalia Ezra aliyekuwa akisikiliza ila macho kwenye uji aliopikiwa. Ulikuwa ukinukia karanga. Mzuri.

“Ni nini tena?!” “Mimi nampenda Ezra. Na si kwamba nipo naye nusu nusu. Kwamba nipo naye lakini akili zipo kwa Colins.” Junior kimya akisikiliza. “Unanisikiliza?” “Nakusikiliza Jelini.” “Nampenda mpenzi wangu na nina muheshimu. Najua kile kilichotokea juzi kinaweza onekana vibaya, lakini sio kwamba kuna kitu kinaendelea kati yangu na Colins.” Akaendelea.

“Ila naomba unielewe Junior. Huyu Colins alikuwa kwenye maisha yangu, tena ya karibu sana. Tukapita naye kwingi. Tukapanga mpaka idadi ya watoto. Kulikuwa na mahusiano ya ndani sana. Lakini tulishakubali kama hatutaweza kuwa pamoja. Na mimi sio muhuni.” “Nazidi kukuelewa Jelini.” “Basi jua mimi sio msaliti.” Akaendelea wakimsikiliza kwa makini sana kutaja kujua moyo wake zaidi.

“Ninachotaka kusema, si kwa kujitetea, najua nawajibika kutoa maelezo kwenu na kuomba msamaha. Ni kama nimemdhalilisha Ezra wangu. Lakini sikukusudia. Ni jambo lilitokea kama vile kazi ya macho ya kawaida. Huwazi wala kupanga wakati gani unafunga na kufungua. Ilinitokea kwa kunishitukiza. Na mimi nilijisikia vibaya, ndio maana niliondoka pale. Nilijua nimeharibu.”

“Sasa Ezra alipokuja na kuzungumza na mimi vile, nikajua hanitaki tena! Ananioa kama msichana mwingine tu. Sio mimi kama Jelini. Na mimi nia yangu nataka kuolewa na mtu ambaye ananipenda na nimeleta maana kwake.” “Ezra anakupenda sana Jelini. Sana, mpaka namuhurumia!” “Ndio nimejua kama ile ilikuwa ni hasira tu, kwa sababu nilimuumiza. Lakini na mimi nampenda mpenzi wangu. Sipo naye kwa bahati mbaya.”

“Nimeamua kuwa na Ezra, kwa sababu najua ni majibu ya maombi yangu. Hata Colins mwenyewe amekiri hivyo. Na nakuahidi nitajifunza kuishi na majibu ya maombi yangu. Hapa nilipompitisha Ezra siku mbili hizi, sitarudia tena, nikijua ananipenda.” Anaendelea kuzungumza, asijue alivyo washitua. Wao walibakia kwa Colins! Mpaka Ezra akashindwa kunywa huo uji.

“Unasema Colins amekiri nini?” Jelini aliropoka. Akajua amekamatwa tena. Akatulia. “Jelini?” “Nipo.” “Tunazungumza tu. Nataka kujua yeye Colins alisema nini?” “Sio muhimu na sisemi hivyo kwa sababu yeye amesema. Mimi mwenyewe nampenda Ezra. Na sitamsaliti hata na Colins.” “Hilo umethibitisha. Na nakushukuru kwa uaminifu wako. Ila nilitaka kujua kwa upande wa Colins.” Kimya.

“Tafadhali Jelini. Najua nyinyi wawili mnahistoria nzito. Na nasikia sifa ya Colins, hakubali kushindwa, zaidi linapofika swala lako.” “Safari hii amekubali kushindwa na Ezra. Anamsifia sana!” Wakashangaa wasiamini.

“Kwamba anamfahamu Ezra?!” “Na wewe. Anawafahamu vizuri sana, tena kwa undani. Alikuwa anatamani kama angemkuta Ezra na mapungufu ili ampatie sababu. Lakini anamfahamu Ezra kwa undani, naona kuzidi ninavyo mfahamu mimi! Kwa kweli amemsifia. Na nina uhakika amemtega Ezra na mwanamke, akagundua Ezra si malaya.” Walishituka wawili hao, mpaka Ezra akapaliwa na uji. Ikabidi Jelini ampigepige mgongoni na kumpa maji. “Pole.” Jelini akaendelea kumtuliza akimpapasa mgongoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Hawakutegemea wala hakuwa akikumbuka kama kuna tukio lolote la tofauti la mwanamke kumtongoza. Ni kama alishazoea hayo. Wanawake wa jiji hilo! Wakutane na mwanaume mwenye pesa kama za Ezra! Halafu anausafiri kama wake! Mjumba wa nguvu vile! Sura inalipa! Hao wawili walishazoea kutongozwa mpaka kwa hila.

~~~~~~~~~~~~~~~~

“Daah! Nahisi Ezra yupo kama mimi. Sijategemea!” Junior akasikika upande wa pili, akitaka Jelini arudi kwenye simu. “Colins anamuheshimu Ezra. Sana. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi juu ya Colins. Na yeye anataka nifanikiwe. Hatatusumbua na Ezra. Usiwe na wasiwasi.” “Nashukuru kusikia hivyo mama. Kwa hiyo harusi bado ipo?” “Mimi bado nataka kuolewa na Ezra.” “Yesss!” Junior akasikika. Jelini akacheka taratibu.

“Tunakupenda Jelini. Na hili sitachoka kukwambia. Tunakupenda na kukuhitaji sana. Wewe ni kiungo muhimu kwetu sisi wanne. Bila wewe, ujue kila kitu kina simama. Mipango yetu yote tuliyopanga kufanya weekend hii sisi wanne kabla ya harusi, jua ilisimama kwa sababu wewe haukuwepo.” “Samahani Junior.”

“Ndio ujue ulivyo wa muhimu kwetu. Ezra hajala tokea tulipofungua ile ijumaa. Hata maji ameshindwa kuweka mdomoni. Ndio ujue hatukudharau. Maana tungekuwa tunakudharau, au wewe ni kama mwanamke tu mwingine, maisha yetu yasingesimama wewe unapoondoka. Ndio uelewe umuhimu wako, hata kama tusipo kwambia.”

“Na mimi nawahitaji Junior, ndio maana niliumia nilipodhani mnanichukulia poa. Na nakuahidi sitarudia tena. Sasahivi nakuahidi mabadiliko. Sisemi hapatakuwa na matatizo, lakini si kwa namna hii. Nitakabiliana nayo nikijua Ezra ananipenda na ananihitaji.” “Nashukuru Jelini.”

“Kwa hiyo na wewe umenisamehe kwa kumdhalilisha Ezra?” “Yameisha mama. Sisi tunataka amani kati yetu. Tutabebana hivyohivyo katika madhaifu yetu. Usikimbie tu. Ila nina ombi.” “Ombi gani?”

“Naomba uwe unatufichia aibu yetu.” Jelini akaelewa na kuumia sana mpaka akajikuta machozi yakimtoka. “Tafadhali, nakusihi. Ikitokea tunakukosea, kama ni Ezra, zungumza na mimi. Nakuahidi sitamtetea. Na kama ni mimi au Emelda, zungumza na Ezra. Tubebe tafadhali. Itatusaidia kuwa imara kuliko umoja wetu uongozwe na watu wa nje.” “Nimekosa Junior.”

“Hapana. Si kwa kukutuhumu. Ninaomba huu ndio uwe msingi wetu kuanzia sasa. Najua bado hujatuamini kama mama, Jema pengine na Colins. Lakini nakuhakikishia na sisi tunahitaji kuwa katika moja ya watu unao waamini unapokuwa umeumia. Na sisi tuwe kimbilio lako. Binafsi nakuahidi kuwa na wewe pale hisia zako zinapokuwa zimeumia au upo na shida. Na sina tabia ya kumchoka mtu au kumuhesabia mtu. Hilo ndilo ombi langu kwako. Tubebe, tusitiri maana najua sisi sio wakamilifu.” Akapoa huyo Jelini, akashindwa cha kujibu.

“Umenielewa?” “Nimeelewa Junior. Na sitarudia tena. Nakuhidi nilichofanya juzi, kusambaza mambo ya ndani, huko nje, hakitarudia tena. Utaona kwa vitendo. Nampenda Ezra. Sitaki kumdhalilisha.” “Nakushukuru. Basi nikuache upumzike. Nilitamani tutoke sisi wanne kesho, lakini mama amekataa. Anasema alishatuambia mwisho ni jumamosi. Kuanzia leo mnatakiwa mpumzike ndani.”

“Hata hivyo kuanzia kesho kuna ratiba zinaendelea pale nyumbani kwa mchungaji. Wakina mama wanakuja kuanzia saa nne, kuzungumza na mimi pamoja na Emelda. Mama mchungaji ameweka hiyo ratiba mpaka siku ya kitchen party. Na amemsisitiza na mama pia. Hapatakuwa na mwanya. Tuvumilie tu. Kuanzia jumapili ijayo tutakuwa huru.” “Hayo ndio nilitaka kukusikia ukisema. Asante Jelini. Usiku mwema.” “Na wewe Junior. Nitakuona jumamosi.” “Daah! Asante mama.” Wakacheka na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~~

Inaendelea…



CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment